Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Saumu Heri Sakala (4 total)

MHE. SAUMU H. SAKALA aliuliza:-
Baadhi ya Waajiri ikiwemo Mashirika binafsi wamekuwa wakiwanyima haki ya msingi wafanyakazi wao kujiunga katika vyama mbalimbali vya wafanyakazi nchini kwa kutishia au kuwatafutia sababu ya kuwafukuza kazi pindi wanapojiunga na vyama hivyo:-
a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka Sheria itakayowabana waajiri wenye tabia ya kuwatishia au kuwafukuza kazi pale wanapojiunga na Vyama vya Wafanyakazi nchini?
b) Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa elimu kwa waajiri na kuwalazimisha kubandika Sheria hii ofisini kwa wafanyakazi ili wajue haki zao?
NAIBU WAZIRI WA SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WALEMAVU (MHE. ANTHONY P. MAVUNDE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saumu Heri Sakala, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, tayari ipo Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini Na. 6 ya Mwaka 2004 ambayo kupitia Kifungu cha 9 (1), kinaeleza wazi kuwa wafanyakazi wanayo haki ya kuanzisha au kujiunga na Vyama vya Wafanyakazi pamoja na kushiriki kwenye shughuli halali za Vyama vya Wafanyakazi. Aidha, Kifungu cha 9 (3) cha Sheria hiyo, kinaeleza kuwa ni marufuku kwa mtu yoyote kumbagua mfanyakazi kwa sababu tu mfanyakazi huyo ni mwanachama wa chama cha wafanyakazi au anashiriki katika shughuli halali za chama.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi yangu itaendelea kuimarisha huduma za ukaguzi na usimamizi wa sheria za kazi, pamoja na kutoa elimu kuhusu sheria za kazi ili kuongeza uelewa wa waajiri, wafanyakazi na umma kwa ujumla ili kuhakikisha kuwa wafanyakazi wanatumia haki na uhuru huo ipasavyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria hailazimishi mwajiri kubandika Sheria ofisini ili wafanyakazi wasome haki zao. Hata hivyo, Kifungu namba 16 cha Sheria hii kinawataka waajiri kubandika haki za wafanyakazi sehemu za wazi ili wazijue haki zao.
MHE. SAUMU H. SAKALA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itaanza kutekeleza ahadi yake ya kuanza kuwalipa wazee pensheni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saumu Heri Sakala, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaanza kutekeleza ahadi yake ya kuwalipa pensheni wazee mara baada ya maandalizi ya utekelezaji wake kukamilika. Maandalizi hayo ni pamoja na kuunda vyombo vya usimamizi wa mpango huo katika ngazi zote, kuweka mfumo na miundombinu muhimu kwa ajili ya kutekeleza mpango huo, kufanya utambuzi na usajili wa walengwa, kutoa elimu kwa umma na kujenga uwezo wa watendaji wa mpango. Vilevile maandalizi haya yatahusu maandalizi ya ziada kama vile rasilimali fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu mkubwa wa mpango huu ndiyo maana inalishughulikia suala hili kwa umakini mkubwa ili tu mara utekelezaji wake utakapoanza uwe endelevu na wenye manufaa kwa wazee nchini.
MHE. SAUMU H. SAKALA aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kutengeneza magari yaliyopo kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Pangani kwa haraka kutokana na uhaba wa magari unaosababishwa na ubovu wa magari?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi
ya Rais (TAMISEMI), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saumu Heri Sakala, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Pangani
ina jumla ya magari 15 ambapo kati ya hayo magari 11 yanafanya kazi. Matengenezo ya magari ya Halmashauri yanafanyika kupitia fedha za matumizi mengineyo zinazotengwa kila mwaka.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2016/2017 Halmashauri hiyo iliidhinishiwa shilingi 52,500,000 kwa ajili ya matengenezo ya magari na katika mwaka wa fedha 2017/2018 Halmashauri hiyo imetengewa shilingi milioni 73. Hivyo, Halmashauri inashauriwa kuweka kipaumbele na kuhakikisha fedha zinazotengwa zinatumika kutengeneza magari ili kuimarisha usimamizi wa Halmashauri.
MHE. SAUMU H. SAKALA aliuliza:-
Kando kando mwa Bahari ya Hindi Mkoani Tanga, pameibuka bandari bubu ambazo nyingine zinakuwa kubwa na kuhudumia watu wengi zaidi na askari wasio waaminifu hufanya bandari bubu hizo kuwa vyanzo vyao vya mapato kwa kuchukua rushwa kwa watu wanaopitisha mizigo yao katika bandari hizo.
Je, ni lini Serikali itazirasimisha bandari hizo na kuzifanya zitambulike ili wafanyabiashara wanaozitumia wawe huru?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saumu Heri Sakala, Mbunge wa Viti Maalum, swali lake kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina taarifa ya uwepo wa bandari bubu katika mwambao wa Pwani ikiwa ni pamoja na maeneo ya Tanga. Aidha, kuibuka kwa bandari hizi bubu kumeleta changamoto za kiusalama, kiulinzi na kiuchumi. Hivyo, ili kudhibiti matumizi ya maeneo haya mamkala zinazohusika za pande zote mbili za Serikali ya Muungano zinashirikiana na kudhibiti hali hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na mikakati ya pamoja na vikao vya kiutendaji ambavyo vimekuwa vikifanyika kwa kuwahusisha Wakuu wa Mikoa yote ya mwambao na visiwani, Wizara zinazohusika kutoka Bara na Visiwani, Mamlaka ya Usafiri Baharini ya Zanzibar (ZMA) Mamlaka ya Usafiri Nchi Kavu na Majini (SUMATRA), Shirika la Bandari la Zanzibar (ZPC), Mamkala ya Usimamizi wa Bahari Tanzania (TPA), Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Uhamiaji, Halmashauri na vyombo vyote vya ulinzi na usalama nchini. Mikakati ya pamoja iliyowekwa ni pamoja na:-
(a) Kutambua bandari zenye umuhimu kwa wananchi kiuchumi na kijamii ili kuzirasimisha kwa kuziweka chini ya uangalizi wa vijiji vilivyo kwenye maeneo husika;
(b) Kuimarisha ushirikiano na Serikali za Mitaa kwa kutumia Kamati za Ulinzi na Usalama ili zihusike katika kudhibiti matumizi mabaya ya bandari bubu katika maeneo ambayo mamlaka husika hazina uwakilishi wa moja kwa moja;
(c) Kuwa na kaguzi za mapoja kwa lengo la kuongeza ufanisi katika matumizi ya vifaa kama vile boti za ukaguzi na kadhalika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na umuhimu wa suala hili, Serikali kupitia mamlaka nilizokwishazitaja, inasimamia kuhakikisha mikakati hii iliyowekwa inatekelezwa kwa wakati ili bandari bubu hizi zikiwemo za mwambao wa Mkoa wa Tanga zirasimishwe na kuwekwa chini ya uangalizi wa mamlaka husika.