Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Eng. Joel Makanyaga Mwaka (26 total)

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Natambua umuhimu wa Mpango kwamba, ndiyo dira ya maendeleo ya nchi kwa maana ya kujua tunatoka wapi, tuko wapi na tunataka kwenda wapi, tunakwendaje na kwa sababu gani?
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Waziri kwa Mpango huu. Naomba nichangie kwa kuzingatia kwamba mimi ni Mbunge wa Jimbo la Chilonwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, miundombinu; barabara zinazounganisha Wilaya, (maeneo mbalimbali na Makao Makuu ya Wilaya), ni mbaya sana na hazipitiki vizuri. Hii inafanya uchumi wa Wilaya inayotegemea sana ushuru wa mazao inakuwa mbaya sana. Kwa kuwa wanunuzi wengi wanafika kwa tabu na hivyo wananunua mazao kwa bei ya chini sana jambo linalodidimiza pia uchumi wa wakulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kuangalia kwa makini na kuzisaidia Halmashauri na hasa Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino kwa kujenga madaraja muhimu strategic kama haya yafuatayo:-
(a) Daraja linalounganisha Kijiji cha Msanga na Kijiji cha Kawawa.
(b) Daraja linalounganisha Kijiji cha Chilonwa na Kijiji cha Nzali.
(c) Daraja linalounganisha Kijiji cha Dabalo na Kijiji cha Igamba (Dabalo B)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, viwanda; Wilaya ya Chamwino na Jimbo la Chilonwa kwa jumla hakuna kiwanda chochote. Tunahitaji Agro-Based Industry/Factory na hasa cha ku-process zabibu. Jambo hili litainua uchumi wa mtu mmoja mmoja, lakini pia kukuza uchumi wa Wilaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha na kuunga mkono mpango mzima na kuomba hayo niliyoyaainisha hapo juu yafanyiwe kazi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono mikakati mbalimbali inayochukuliwa na Wizara hii. Natambua changamoto nyingi zilizo mbele katika kutekeleza mikakati hii. Naunga mkono hoja kwa kusisitiza yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo ndiyo uti wa mgongo na unahitaji kupewa kipaumbele kwa kuhakikisha upatikanaji wa pembejeo zote zinazohitajika kwa wakati; lakini vile vile tunapozungumzia viwanda hapa nchini ni lazima tujue kwamba viwanda vinategemea mazao yatokayo shambani (kilimo).
Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu kwa maana ya barabara ni muhimu sana kwani mazao hayo kutoka mashambani, ili yafike kiwandani kwa gharama nafuu, ni lazima yapite kwenye barabara zinazopitika kirahisi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia viwanda ni muhimu ili mazao yetu yapate soko la uhakika. Ndani ya Jimbo la Chilonwa tunalima sana zao la zabibu, lakini soko lake ni baya sana kwa kuwa, hakuna kiwanda cha uhakika cha kuweza ku-process zabibu. Naomba Wizara hii isaidie kuweka msukumo kwa Wizara za TAMISEMI na Viwanda kuweza kuharakisha ujenzi wa kiwanda cha uhakika cha ku-process zabibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, maendeleo ya uhakika yatakayotupeleka kwenye nchi ya uchumi wa kati yatapatikana kwa kuwa na viwanda, tena viwanda vinavyotumia mazao yetu kama malighafi yake. Kufikia uchumi wa kati ni kuinua uchumi wa mtu mmoja mmoja ambao kwa ujumla wake ndio utakaopandisha uchumi wa nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza na kuunga mkono hoja ya Wizara kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijielekeza Mkoani kwangu Dodoma, Wilayani kwangu Chamwino na Jimboni kwangu Chilonwa, naomba kuomba yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iweke mazingira rahisi kwa wananchi wa Jimbo la Chilonwa kuweza kukipa na kuanzisha viwanda vidogo vidogo vinavyochakata/process mazao yanayozalishwa jimboni kama vile mashine za kukamua alizeti, ufuta pia, mashine za ku-process mahindi na kuuza sembe mijini badala ya kuyauza mahindi (value addition).
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kipekee zao la zabibu ambalo kwa hakika ndio mkombozi wa uchumi wa wananchi wa Dodoma ambao bado unasinzia. Kwa zabibu naiomba Wizara ifanye kufuatilia Halmashauri ya Chamwino ili kuisaidia kufanikisha ujenzi wa kiwanda cha zabibu cha kisasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda cha kisasa ni kile kitakachowezesha uzalishaji wa juice, mvinyo na concentrate ya mvinyo. Hiki ni kiwanda tofauti na vile vidogo vidogo na vichache vilivyopo vinavyozalisha mvinyo tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchangia Wizara hii kama ifuatavyo:-
Nampongeza Mheshimiwa Waziri, Profesa Muhongo kwa hotuba yake nzuri iliyosheheni mambo muhimu kuhusiana na nishati na madini.
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza kwa kupewa/kutengewa bajeti kubwa kwa lengo la kuboresha mambo ya nishati ambayo ni muhimu sana katika kuipeleka nchi yetu kwenye uchumi wa kati. Naomba nimwombe Mheshimiwa Waziri kwamba, wajitahidi kuhakikisha mipango inakwenda kama ilivyopangwa kwa faida ya wananchi wote wa Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nimwombe Mheshimiwa Waziri yafuatayo katika Jimbo langu la Chilonwa:-
Umeme wa REA Phase II ulikuwa ufike hadi Kata ya Zajilwa, Kijiji cha Zajilwa, lakini haujafika, naomba sasa ufike.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba umeme katika REA Phase III uende pia, maeneo yafuatayo:-
Vijiji vya Gwandi Bwawani na Magungu vilivyo Kata ya Zajilwa; Vijiji vya Izava, Umoja, Segala, vilivyo Kata ya Segala; Vijiji vya Ikombo, Solou na Itiso vilivyo Kata ya Itiso; Vijiji vya Manyemba, Chiwondo, Igamba, Nayu, vilivyo Kata ya Dabalo; Vijiji vya Chitabuli, Mlimwa, vilivyo Kata ya Membe; Vijiji vya Bwawani na Chalinze B vilivyo Kata ya Manchali; Vijiji vya Mlebe, Msamalo, vilivyo Kata ya Msamalo; Vijiji vya Makoja, Butiama, Ikowa, vilivyo Kata ya Ikowa; Kijiji cha Humekwa, kilicho Kata ya Haneti na Kijiji cha Kawawa kilicho Kata ya Msanga.
Mheshimiwa Spika, nawasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, naomba nichukue fursa hii kukushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitamke kwamba kwa vile leo ni mara yangu ya kwanza kusimama na kuchangia katika Bunge hili, nachukua nafasi hii kumpongeza sana Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa Dkt. Magufuli kwa kuchaguliwa kwake kwa kishindo mwaka 2015, lakini nimpongeze vilevile kwa kutufanyia kazi kubwa ya kutupatia Baraza la Mawaziri zuri sana. Tunaona kazi wanayoifanya na kila mtu anaiamini. Na mimi naomba nichukue fursa hii kuwaambia Mawaziri wachape kazi, tuko nyuma yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo nitamke vile vile kwamba kwa vile ni mara yangu ya kwanza kusimama na kuchangia, niwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Chilonwa, ambao waliona waniamini na mimi niwawakilishe katika mjengo huu katika kuleta matatizo yao na kushirikiana kutatua matatizo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mwigulu kwa hotuba yake nzuri ambayo ametupa asubuhi hii kupitia kitabu hiki ambapo amejikita vizuri katika masuala ya kilimo na nyanja zake zote. Amegusia kila eneo na namna gani Wizara yake inajipanga, kufanya kwa ajili ya Watanzania; lakini pia katika nyanja za mifugo, pamoja na sekta zote. Ameeleza kwa umakini kabisa, ni nini Serikali inataka kutufanyia sisi Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vivyo hivyo amekwenda kwenye suala la uvuvi na sekta zake zote, masuala ya kupanga siku zote yana changamoto, na sisi tuko hapa leo kuijadili hii hotuba yake kwa lengo la kuonesha changamoto zilizopo tukitegemea kabisa kwamba watazichukua na kuzifanyia kazi na kuboresha yale ambayo wanakusudia kuyafanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii sasa nijielekeze kwenye Jimbo langu la Chilonwa. Jimbo la Chilonwa tunalima sana, lakini huwa tuna matatizo ya hapa na pale ya mvua. Jimbo la Chilonwa tunafuga kwa kiasi chake, tatizo hatuna uvuvi kwetu. Nikizungumzia suala la kilimo, naomba sana kwa upande wa pembejeo ambapo imeonesha dhahiri kwamba safari hii pembejeo zitapatikana kwa wakati na pembejeo zinazostahili. Isiwe kwamba tunaletewa mbegu ambazo unapanda hazioti tena, isiwe kwamba tunaletewa mbegu wakati wa kupanda umepita. Tunaamini haya yaliyozungumzwa hapa ndani ndiyo yatakavyotekelezwa na sisi tunaomba iwe hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba kilimo ni biashara. Pale inapokuwa mwananchi analima halafu anakosa sehemu ya kupeleka mazao yake, au analima inakuwa ngumu sana kwake kusafirisha mazao yake kuyapekeka kunakostahili, linakuwa tatizo kubwa sana. Tatizo la miundombinu kuingia vijijini hebu lifanyiwe kazi. Najua Serikali inajipanga, lakini naomba nisisitize kabisa, lifanyiwe kazi na hasa katika Jimbo langu la Chilonwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wanalima sana mahindi na kwa taarifa yako, najua Wabunge wengi tunajua humu, mahindi ya Dodoma yana soko kubwa sana duniani. Mahindi ya Dodoma hayatumii kemikali. Dodoma hatutumii mbolea za chumvi chumvi hata siku moja! Dodoma tunahitaji mvua tu! Tatizo letu ni mvua, ndiyo inayotusumbua. Kwa hayo, mazao kidogo tunayopata, yana soko kubwa sana. (Makofi)
Kwa hiyo, naiomba sana Serikali itusaidie kutuwezesha mazao yetu yafike sehemu yanapotakiwa kwenda kiurahisi. Inapokuwa ngumu kuyafikisha mazao sokoni, wanunuzi, walanguzi au wafanyabiashara, wanakuwa na sababu ya kununua mahindi kwa bei ya chini sana. Kama atasafiri kwenda vijijini kwa shida sana, njia haipitiki, anachukua siku tatu kufika sehemu ambayo angetumia masaa mawili, matatu, kwa vyovyote vile atataka kwamba atakapokuja kwenye soko, mahindi yake yawe competitive. Kwa hiyo, atataka anunue mahindi kwa bei ya chini na kwa kufanya hivi, mwananchi anaathirika sana kiuchumi. Kwa hiyo, naomba sana suala la miundombinu, barabara za kuelekea vijijini liangaliwe kwa macho mawili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili mtu aweze kulima lazima kuwe na amani. Nasema wazi, katika Jimbo langu la Chilonwa, vilevile kuna tatizo la migogoro ya ardhi ambayo naweza kuisema vile ni migogoro ya mipaka. Ardhi kwa maana ya wakulima na wafugaji wanavutana. Mipaka inafika wakati fulani Wilaya moja na nyingine kama alivyozungumza ndugu yangu hapa Mheshimiwa Nkamia, tunavutana sana mipaka ya kulima na hasa unapofika wakati wa kulima na Wilaya tunazopakana nazo, ingawa tatizo kubwa kwa kweli ni wafugaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili naomba sana Serikali iangalie uwezekano wa kuwapatia wafugaji maeneo maalum kwa ajili ya malisho, lakini katika maeneo hayo njia rahisi ya kuwafanya waende kwenye maeneo hayo ya malisho ni kuhakikisha kwamba maeneo hayo yanakuwa na majosho na maji ya kutosha kuwapatia mifugo yao ili waweze kwenda na kufuga huko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye mazao ya biashara. Bahati mbaya Dodoma mazao ya biashara siyo mengi, lakini tuna alizeti na vilevile tuna zabibu. Namuombe sana ndugu yangu Mheshimiwa Mwigulu, zao la zabibu ambalo umetuheshimu, limeonekana katika kitabu chako, huku nyuma naona zao la zabibu, hili zao ni mkombozi mkubwa sana wa mwananchi wa Dodoma, lakini tunahangaika nalo kupita kiasi kwa sababu ya soko. Watu wanakuja wananunua kwa bei wanazotaka, wanakwenda kuuza bei kubwa. Mtu akija shambani atanunua kilo moja shilingi 500.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taarifa yako, kilo moja inaweza kuwa na mikungu hata mitano ya zabibu. Ukija mjini hapa mkungu mmoja wewe unanunua shilingi 1,000, yeye ananunua shilingi 500 anakuja kuuza hapa mjini shilingi 5,000. Huyu mwananchi atainuka lini? Dawa peke yake ni kuhakikisha tunamwekea kiwanda cha uhakika cha zabibu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ombi langu kwa Serikali, iangalie namna ya kuisukuma Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino, ina mpango wa kuweka kiwanda, lakini inasuasua sana. Naombe kabisa, ndugu yangu Mheshimiwa Waziri chukua fursa hii, wasiliana na Halmashauri ile ujue shida yao ni nini? Tumefika mara nyingi, tunaambiwa kiwanda kinafuata muda siyo mrefu, lakini kila siku, sasa tuna zaidi ya miaka miwili, kiwanda hakionekani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo machache, naomba nichukue nafasi hii kutamka kwamba naiunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwnyekiti, kwanza kabisa, nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuwa mmoja kati ya wachangiaji wa hotuba ya Waziri wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hilo niendelee kumpongeza sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania kwa kazi yake kubwa anayoifanya. Hapa tunapiga kelele ya vitu vingi lakini wenye kusikia wamesikia. Leo akiwa safarini kwenda Arusha amezungumza mambo mazito juu ya watu wanaoleta fujo na biashara yetu ya sukari. Ni jambo ambalo linawagusa wananchi na yeye mwenyewe linamgusa sana ndiyo maana analikemea kila anapokwenda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza kwa dhati kabisa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa hotuba yake nzuri aliyoiwasilisha kwa umakini kabisa. Wakati akianza nilikuwa naangalia kitabu chake kilivyo kikubwa nikasema hii itakuwa kazi hapa lakini ikawa kazi kweli. Amei-summarize kwa uzuri kabisa, hakuna kitu alichoacha ambacho mtu hakuelewa. Utapitia na utapata details za yale aliyokuwa ameya-summarize, nampongeza sana. Amezungumzia kwa undani kuhusu viwanda kwamba Serikali yetu ya Awamu ya Tano inajipanga kufanya nini kwenye viwanda, akizungumzia viwanda vidogo sana, viwanda vidogo na viwanda vikubwa. Amezungumzia biashara na uwekezaji wake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba namuunga mkono na naunga mkono hoja hiyo. Naiunga mkono kwa dhati kabisa nikitambua kwamba safari tuliyonayo ambayo tumejiwekea ya kuingia kwenye uchumi wa kati hatujakosea njia. Njia sahihi ni hii ya kupitia viwanda, kwa nini? Tunapozungumzia kuelekea kwenye uchumi wa kati maana yake tunazungumzia kipato cha mtu mmoja mmoja ambapo mwisho tunazungumzia kipato cha Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tuna shida ya ajira, kama mtu hufanyi kazi hakuna jinsi utajiongezea kipato lakini unapokwenda kuwainua wananchi kwa viwanda maana yake unakwenda kunyanyua vipato vyao. Unaponyanua vipato vyao maana yake unapandisha kipato cha Taifa na hii ndiyo njia sahihi ya kutupeleka kwenye uchumi wa kati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia kilimo, ili kilimo kiweze kuboreshwa lazima soko la uhakika liwepo. Kilimo kipo lakini soko halina uhakika, kwa hiyo kilimo kiko katika levels za chini. Tutakapoweka viwanda vitakavyofanya processing ya mazao yetu ya viwandani maana yake nini? Maana yake watu wengi zaidi wataji-engage kwenye kilimo ambacho soko lake lipo. Tunapozungumzia ufugaji vilevile, tunataka watu wafuge wakiwa na uhakika wa masoko yao. Tunapozungumzia uvuvi tunataka watu wavue wakiwa na uhakika wa masoko ya mazao wanayoyapata. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia viwanda maana yake tunazungumzia value addition ya products zetu tunazozipata. Hili ndilo tatizo kubwa ambalo tumekuwa nalo Watanzania, tatizo hili pia nchi za Afrika tumekuwa nalo sana, kazi yetu ni kuzalisha malighafi na kuwapelekea Wazungu na nchi za nje, wao wanaenda ku-add value, wanatengeneza faida kubwa na kuturudishia sisi tena.
Kwa hiyo, tunapokwenda kwenye hatua hii ya kuzalisha wenyewe, tunapata ajira. Tunapoweka viwanda maana yake kuna watu wanapata ajira viwandani kwa ajili ya ku-process yale mazao lakini mazao yanapotoka pale lazima yafanyiwe biashara, tayari watu wanapata biashara pale pale. Kwa hiyo, ukiangalia chain nzima, hii ndiyo njia sahihi ya kumuongezea kipato Mtanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda sasa nijikite kwangu kwenye Mkoa wa Dodoma, Wilaya ya Chamwino na hasa Jimboni kwangu Jimbo la Chilonwa. Jimboni kwangu ni wakulima na ni wafugaji. Tunalima kiasi cha kutosha pamoja na shida ya mvua iliyopo lakini Mungu anatujalia tunapata kiasi cha kutosha lakini tatizo kubwa ni soko. Nilizungumza juzi kwamba kama tukipata soko la uhakika watu watalima kwa wingi na viwanda vitapata malighafi za kutosha. Tunalima alizeti, ufuta na mahindi lakini soko lake ni duni. Kwa sababu hakuna soko la kuaminika wafanyabiashara wanakuja wananunua kwa bei wanazotaka. Kama tukiwa na uhakika wa viwanda kwamba nalima alizeti najua naipeleka kiwanda gani akinifuata mfanyabiashara nitamuuzia bei ambayo najua hii inanilipa mimi, inalipa muda wangu niliokuwa shambani, inalipa pembejeo zangu nilizotumia shambani na kupata faida kidogo lakini kwa sasa tunauza maadam tuuze. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika upande wa viwanda na mazao yetu, kuna mazao yanahitaji viwanda vidogo vidogo, vidogo sana lakini kuna mazao yanahitaji viwanda vikubwa na vya kati kwa upande wa alizeti, ufuta na mahindi. Ninachokiomba kwa Serikali na kupitia kwako wewe Waziri hebu tuangalie namna ya kuwawezesha wananchi wapate mikopo ya kuweza kuanzisha hivi viwanda vidogo vidogo vya ku-process mazao yao kama alizeti, ufuta na mahindi. Sisi kwetu Chilonwa tuna biashara ya uhakika ya zabibu yenye shida ya soko.
Naomba nikuombe wewe sasa Waziri kupitia kwako Mwenyekiti tunahitaji tupewe kiwanda cha uhakika cha kutengeneza mvinyo. Tukipata kiwanda cha uhakika cha kutengeneza mvinyo maana yake watu kwa wingi sana watajitokeza kulima zao la zabibu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda hili niliweke sawa kidogo. Kuna mchangiaji mwenzangu mmoja alisema kuna viwanda vya aina mbalimbali, naomba nishauri katika hili tusikimbilie viwanda tu, tunapofikiria viwanda basi tuweke viwanda vyenye teknolojia ya kisasa. Kwa mfano, unapozungumzia Kiwanda cha Mvinyo ambavyo ndiyo vingi viko hapa Dodoma vidogo vidogo, kazi yao ni kukamua ile zabibu na kutengeneza mvinyo, basi! Hayo siyo mazao peke yake unayoweza kuyapata kutokana na zabibu. Viwanda vya wenzetu vina-process unapata juice lakini unaweza ukai-ferment ukapata mvinyo (wine) lakini vilevile unaweza ukai-concentrate ukapata kitu kinaitwa concentrates hizi ambazo tunapigia kelele hapa kwamba wafanyabiashara wengi wa viwanda vya mvinyo wengi wana-import concentrates wanakuja kutengenezea mvinyo hapa wakisema kwamba wametumia zabibu za hapa nchini, sio kweli! Basi na sisi tuanzishe kiwanda cha namna hiyo tuweze kutengeneza juice, mvinyo na concentrates. Tukifanya hivyo tutakuwa tumefanya value addition kubwa sana na kuipatia nchi hii hata fedha za kigeni hasa tukizungumzia concentrates ambazo zina soko la uhakika huko nje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nitamke kwamba naunga mkono hoja na ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kwanza kabisa nikushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wamechangia wachangiaji wengi na mimi niko ndani yao yaliyozungumzwa kwa hakika ni yale ambayo na mimi ningependa niyazungumze kwa undani. Lakini nataka nijiweke kimsingi katika kukubaliana nao kwamba elimu ndiyo kila kitu, ndiyo msingi wa maendeleo bila kuwa na elimu bora Taifa halitapiga hatua yoyote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kuwa na elimu bora safari yetu ya kuelekea Tanzania ya uchumi wa kati itakuwa ni ndoto kwa sababu huko tunazungumzia kuwa na viwanda pamoja na kwamba tunapuzungumzia Tanzania ya viwanda maana yake tunazungumzia industrialization. Tukienda katika historia wenzetu wamepita huko miaka ya 1800 wakati sisi tuko kwenye primitive, lakini leo sisi tunazungumzia industrialization basi tuifanye iwe kweli kwa maana ya kwamba iwe elimu bora ndiyo maana wachangiaji wote wanapiga kelele elimu iwe bora tuweze kwenda jinsi tunavyotaka sisi Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme machache, kwanza nimevutiwa sana na hotuba ya Mheshimiwa Waziri, hotuba imesheheni kila kitu ambacho kinahitajika kutufanya sisi tuweze kusonga mbele katika nyanja ya elimu na kwa hiyo kuweza kutubeba sisi kutupeleka katika Tanzania ya uchumi wa kati. Lakini tatizo liko wapi, tunapopiga kelele na elimu kuwa siyo bora, elimu duni tatizo liko wapi, mipango mizuri tunayo, mikakati mizuri tunaiweka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme tu ili tuweze kufika tunakotaka, tunahitaji kuwa na elimu bora inayozingatia usawa kwa wanafunzi wote. Tunapozungumzia elimu bora tunazungumzia elimu yenye mitaala iliyosimama na syllabus zilizosimama, zisizobadilika badilika, hii ni sera hatuwezi kuwa na sera ya kutufikisha popote inayobadilika badilika kila wakati. (Makofi)
Kwa hiyo, mimi naona sehemu moja ambayo inaleta shida kwetu ni hapo kwamba sera zetu mitaala yetu syllabus zetu zinabadilika na zinabadilika na watu. Leo yuko Mama Ndalichako anakuja kivyake, kesho anakuja Mwaka anakuja kivyake, keshokutwa anakuja Mheshimiwa Zungu anakuja kivyake hatuwezi kusonga mbele hata siku moja, tunatakiwa tuwe na sera iliyosimama, haijalishi leo yuko nani, kesho yuko nani ili tuweze kuwa na elimu bora.
Pili, tunahitaji kuwa na walimu bora, walimu bora utawapata wapi? Lazima uwapate vyuoni je wanadahiliwa vipi kuingia vyuoni. Tumesikia hapa tatizo la udahili wa vyuoni. Tumesikia hatua zilizochukuliwa na Mheshimiwa Waziri kwa wale waliotufikisha pabaya pamoja na kwamba tunalia hawa wanafunzi waliofutiwa masomo kwa kweli tunaomba Serikali iwafikirie mara mbili mbili, kuwapoteze muda mwingi na sasa waende wakaanze upya na hawajui waanzie wapi kwa kweli siyo sahihi. Tunaiomba Serikali iwafikirie kwa sababu halikuwa tatizo lao tunajua kuna namna yoyote inaweza ikafanyika ili nao waweze kujikwamua kimaisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini udahili vyuo vya walimu viko vipi huko wanakosoma walimu kukoje vyuo viko sawasawa au wanakwenda kupitisha muda tu miaka miwili, mitatu wanatoka wanakuja kufundisha? Hayo ni mambo ya msingi katika kuhakikisha kwamba tunakuwa na elimu bora. Mazingira ya kufundishia yako vipi? Madarasa yako vipi, madarasa yasiyokuwa na sakafu, madarasa ambayo darasa moja linaingia wanafunzi mia moja naa mpaka mwalimu anakosa pa kusimama, hilo ni darasa ambalo mwalimu anaweza akafundisha kweli? Tunajua mwalimu anapofundisha ana standard awe na wanafunzi wangapi darasani, aweze kuwapitia hata wale walio slow learners kuwavuta waende na wenzao. Sasa mwalimu anapokuwa na darasa limejaa hata pa kupita haoni atawasaidia vipi hao wengine slow learners na hata hao first learners hawawezi ku-learn chochote katika darasa ambalo limesheheni wanafunzi kiasi hicho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia vifaa vya kufundishia, viko mashuleni kweli? Maana yake sisi ndiyo tunaotoka huko vijijini, ndiyo tunaotoka huko kwenye majimbo yetu, shule zina vifaa vya kufundishia? Serikali ina mpango gani katika hili?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia maslahi bora ya walimu. Ukishakuwa na mwalimu bora lazima awe na maslahi bora maslahi bora ya mwalimu ni pamoja na mshahara wake uwe mzuri, tunazungumzia kwamba ukitaka kuwa Mbunge lazima utapita kwa mwalimu, ukitaka kuwa Rais lazima upite kwa mwalimu, ukitaka kuwa daktari lazima upite kwa mwalimu, lakini huyu mwalimu ukishapita umemuacha hapo nyuma, leo kuna mwalimu aliyenifundisha mimi pengine nikianza kumgeukia nyuma ninachokipata mimi kama mshahara wangu ukilinganisha na cha mwalimu hakuna heshima hata dakika moja. Wanavunjika moyo, wanaona kwamba kazi hiyo ni kazi ya kudharaulika sana, hebu tuifanye kazi ya walimu kuwa kazi ya heshima kwa kuwaangalia kwenye maslahi yao kwa upande wa mishahara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na mishahara hiyo waliyonayo stahili zao wanazostahili wanazipata inavyostahili? Mwalimu anahamishwa, hapati hela ya uhamisho. Mwalimu anatakiwa kwenda kwenye semina au walimu wanatusaidia kwenye kusahihisha mitihani pesa za kusahihisha mitihani hawazipati kwa wakati unaostahili. Hivi tunawaangalie kweli walimu kwa karibu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la nyumba za walimu. Walimu huko vijijini mkienda utawaonea huruma, wanakaa kwenye vibanda ambavyo huwezi kuamini, sasa tunaanza kuwaambia walimu wakipangiwa shule wakienda wakiripoti wanaondoka, hata mimi ningeondoka, anakwenda kuingia kwenye kibanda ambacho huwezi kuamini, kweli mwalimu ametoka chuoni anakuja kuwafundisha wanafunzi anaingia kwenye kibanda hamna taa okay mambo ya taa siyo tatizo watanunua siku hizi kuna mambo ya solar kuna nini, lakini kibanda kimejibana kidogo kidogo tu, kitanda hakuna nafasi ya kuweka kitanda cha sita kwa sita hakiingi kweli jamani? Hii siyo sawasawa hebu tuwaangalie kwa karibu.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho na muhimu katika ubora wa elimu ni hili la kuzikagua shule. Shule hazikaguliwi kabisa, ukienda shuleni ulianza mara mwisho wamekaguliwa lini utacheka, hazikaguliwi na hiki ndicho chanzo kikubwa cha elimu kushuka pamoja na walimu kuwa wamekataa tamaa lakini kama wanajua kuna mtu anawafuatilia nyuma basi hata kawoga kidogo kanakuwepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu naomba haya masuala Mheshimiwa Waziri ayachukue pamoja na mengine mengi waliyozungumza wenzangu ayachukue na Serikali iyafanyie kazi kama kweli inataka kufanya Tanzania tuwe na elimu bora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili usawa kwa wanafunzi. Tuna wanafunzi wengine wenye mahitaji maalum, mahitaji maalum…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante,
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya Ardhi. Kwanza kabisa nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uhai sisi sote tuliomo humu ndani, tumekutana leo tuweze kuifanya kazi hii muhimu kwa Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kututunzia Rais wetu Mheshimiwa Rais. Dkt. John Pombe Magufuli tukitambua na kazi yake kubwa aliyonayo. Tunaomba aendelee kumtunza aifanye kazi kwa uaminifu kadri atakavyomjalia. Mwisho, nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Wizara ya Ardhi, kwa kuleta hotuba nzuri hapa, ambayo tumeisikia ina mantiki na changamoto nyingi ambazo tunazijadili sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nianze tu kwa kusema kwamba, nionavyo mimi ardhi ni eneo muhimu sana katika safari yetu hii tuliyoianza ya kuelekea kwenye Tanzania ya uchumi wa kati. Kama tulivyokwishaona katika mijadala yetu mbalimbali tuliyofanya ya Wizara ambazo tungezifanya kama viwanda, kilimo na mifugo, ujenzi na kadhalika. Wizara zote hizi tumezijadii zikizingatia mpango wa maendeleo wa miaka mitano ambayo ndani yake sasa tunajadili mpango wa maendeleo wa mwaka mmoja mwaka 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nianze sasa kwa kumpongeza kwa dhati Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri iliyoenea na kusheheni kila kile tunachokitegemea Watanzania nini kipo, nini tunakitegemea. Hata hivyo, niseme kwamba, nitoe mfano ambao tunaujua wote kwamba, nini kilianza kuku au yai, kila mtu ana majibu yake humu ndani, lakini nikikuuliza Wizara ipi muhimu katika Wizara zetu nyingi tulizonazo kila mtu atakuwa na majibu yake vilevile lakini nitakwambia Wizara ya Ardhi iko mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, iko mbele na wachangiaji wote waliopita wamekwisha yasema haya, Wizara ya Viwanda haitakuwepo kama hakuna ardhi utavijenga wapi hivyo viwanda, Wizara ya Kilimo na Mifugo utalima wapi, utafuga wapi kama ardhi haipo, ujenzi yawe wa barabara au nini utatengeneza wapi barabara kama hakuna ardhi, lakini kikubwa ni wapi unalima, wapi unajenga na wapi unafuga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ndio kazi kubwa ambayo Wizara ya Ardhi inayo na ndiyo haya ambayo Mheshimiwa Waziri amejitahidi sana kuelezea mikakati na mipango aliyonayo angalau kwa mwaka huu wa 2016/2017, nini wanatarajia kama Wizara kukifanya. Niseme kama kuna tatizo kubwa katika Wizara hii ni migogoro ya ardhi, imekithiri na imedumu muda mrefu shida ni nini? Shida iko wapi? Kwa nini hatuitatui, kwa nini haifiki mwisho? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia kwako nichukue mfano wa kwangu Wilaya ya Chamwino na hasa Jimbo la kwangu la Chilonwa, Mheshimiwa Waziri Lukuvi, alishawahi kuwa Mkuu wa Mkoa hapa Dodoma, analifahamu sana Jimbo langu la Chilonwa, anafahamu sana matatizo ya ardhi yaliyopo Jimbo la Chilonwa, maeneo ya Kata ya Segala kule Izava, kule Walii ambako tumepakana na Wilaya ya Kongwa anafahamu sana tatizo la migogoro lililopo kule Dabalo katika Vijiji vya Chiwondo ambavyo pia vimepakana na Kongwa, kule hakuna usalama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa, wafugaji wanaleta fujo sana. Ninavyozungumza hapa nilipo wanaingiza mifugo kwenye mashamba ya wakulima, huku wakiwa wamejiandaa na mikuki na mishale, mkulima atokee wampige mishale, hakuna amani. Nimuulize tu Mheshimiwa Waziri, kuna mpango gani wa kutatua haya matatizo ambayo yameshakuwa ya muda mrefu, shida ni nini? Ukiangalia maeneo niliyoyataja maeneo ya Izava, Walii na Chiwondo yanapata huduma zote za kijamii toka Wilaya ya Chamwino, kuanzia maji, shule, ikija wakati wa sensa, kujiandikisha kupiga kura, hata mimi mwenyewe nimepigiwa kura na hawa, lakini ikifika wakati wa kilimo tayari utaona migogoro imeanza wanakuja wafugaji wanaotoka maeneo ya Kongwa wakidai kwamba yale maeneo ni ya Kongwa. Inaonekana labda kweli ni maeneo ya Kongwa, Serikali iko wapi wakati siyo wa kilimo kuingilia na kutatua yale matatizo once and for all. Shida ni nini? Kwa kweli niseme tu, sitaki kuingia kwenye historia lakini niseme kama hakutakuwa na maelezo mazuri wakati Mheshimiwa Waziri una-wind up…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nashukuru sana kunipa nafasi hii ya kuchangia katika Wizara hii ya Afya, na mimi nianze kwa kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara ya Afya kwa kazi nzuri na kubwa wanayoifanya, tumeona hata katika uwasilishaji wa bajeti yao hotuba yao ilivyosheheni mambo yaliyo ya muhimu sana kwa wananchi wa Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijikite kwanza kabisa kusema Watanzania tunayo kazi kubwa sana mbele yetu, kazi hii tumedhamiria kwamba tuondoke hapa tulipo kwenye ulimwengu wa tatu, nchi maskini, tuingie angalau kwenye nchi yenye uchumi wa kati. Ili tuweze kufanikiwa katika hili kama afya zetu zitakuwa mgogoro hatutaweza kufika huko salama, tutakuwa tunasuasua sana na itatuchukua miaka mingi kufika kwenye nchi ya uchumi wa kati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili nichukue nafsi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Ummy Mwalimu katika maadhimisho ya siku ya usafi wa mazingira na ujenzi wa vyoo bora kimkoa Dodoma yalifanyika katika Kata ya Aneti kijiji cha Umekwa katika Jimbo langu la Chilonwa. Namshukuru sana kwamba alishiriki pamoja na kushiriki aliweza kutoa ahadi mbalimbali kwamba atasaidia kumalizia ujenzi wa chumba cha upasuaji pale kwenye Kituo cha Afya cha Aneti nakushukuru sana Mheshimiwa Ummy kwa kazi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile aliahidi kutupatia madaktari katika Zahanati za Aneti, Chinene pamoja Umekwa katika Kata hiyo ya Aneti. Kama vile haitoshi kwa sababu ya speed kali tunayokwenda nayo hadi sasa tunavyoongea katika kijiji cha Aneti tayari tumeshapewa daktari mmoja, tunakushukuru sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia uliahidi kuipatia shule ya msingi Umekwa shilingi 400,000 kwa ajili ujenzi wa vyoo bora pale shuleni, nashukuru sana kwa haya mambo mazito unayotufanyia. Nisimalize bila kukushukuru sana wewe pamoja na Wizara yako kwa kutuangalia Chamwino kwa jicho la huruma sana kwamba ulitupatia fedha kwa ya ajili ya kuboresha pale kituo cha afya cha Chamwino shilingi milioni 500, lakini pia ukatupatia fedha kwa ajili ya kuboresha zahanati ya Mpunguzi shilingi milioni 700 na juzi pia umetupatia tena fedha kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya Wilaya ya Chamwino shilingi bilioni 1.5, tunakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa nimalize kwa kukuomba Mheshimiwa Waziri tuna mahitaji mengi sana ya afya katika Jimbo la Chilonwa, nakuomba sana uliangalie kwa huruma sana kijiji cha Kwahemu ambapo wananchi wameanza ujenzi wa zahanati, lakini wamefika njiani tukisaidiana wote pamoja na Mbunge, Diwani na nani tunasuasua, tunaomba sana utuangalie pale kama unaweza kutusaidia angalau tuweze kumalizia ile zahanati, kijiji hicho kiko ndani sana, kiasi kwamba kusafiri toka pale kwenda Aneti inakuwa shida sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo machache nashukuru sana, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwanza kabisa nichukue nafasi hii nikushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika bajeti yetu hii, ya mwaka 2016/2017 nikitambua wazi kwamba ni bajeti ya kwanza kabisa ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa, na ndugu yetu, kamanda wetu, Rais John Pombe Magufuli, Hapa Kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii pia nikupe pole kwa haya unayoyapita sasa, lakini ndiyo maisha yenyewe, tatizo huwa ni uelewa na ufahamu ilivyo kila sehemu kunapokuwa na jamii fulani lazima kuwe na sheria na kanuni zinazowaongoza. Bila kuwa na sheria na kanuni inakuwa vurugu mechi. Sisi kama Wabunge tunapaswa kwa hakika kuonesha dhahiri kwamba Wananchi hawakukosea kutuchagua kutuleta hapa tuoneshe kwamba tunatakiwa kwenda kwa sheria na kanuni mbalimbali za maeneo tunayokuwepo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napata shida ninapoona humu ndani tunakuwa viongozi wa kutokufuata hizo sheria na kanuni. Lakini ni jambo nalo lisilokwepeka kunapokuwa na jamii tuko wa aina mbalimbali tuwasamehe tu, lakini naamini sisi humu ndani tunaifanya kazi ya watu waliotutuma hata kwa niaba yao kuhakikisha kwamba nchi hii inasimama na Serikali ya Awamu ya Tano inakwenda kutekeleza bajeti yake ambayo imelala sana katika kuwatetea wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii pia nimshukuru sana Waziri wa Fedha na Mipango, Naibu Waziri na timu yake yote, kwa hotuba yao nzuri waliyotuletea hapa ambayo sasa tunaijadili inayohusiana na bajeti ya Serikali ya mwaka 2016/2017. Nawapongeza kwa sababu ninatambua nchi yoyote itajiendesha kwa wananchi wake kulipa kodi, na hata misaada mbalimbali ambayo Serikali yetu inapata kutoka nchi za wenzetu ni kodi za wenzetu, kwa hiyo na sisi tunapaswa tulipe kodi tuendeshe nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimefurahishwa zaidi na bajeti hii pale nilipoona imeweka asilimia 40, imelenga kumsaidia Mtanzania. Nasema kumsaidia Mtanzania kwa sababu imepelekwa kwenye maendeleo. Tatizo letu limekuwa kubwa, wananchi wetu wanapiga kelele sana na hata wenzetu upande wa pili wamekuwa wakilibeba sana. Hawaoni maendeleo ya haraka kwa sababu fungu hili lilikuwa linatengwa dogo sana. Kwa sasa kwa kuweka asilimia 40 nina amini tutakwenda na tutaona mabadiliko makubwa au maendeleo ya haraka kwa maendeleo ya wananchi kutokana na fungu hili kuongezwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, wengi wamechangia na wamechangia kwa umahiri wao, naomba nizungumze suala hili tu kidogo kwa mfano ulipaji wa kodi na maendeleo ya nchi kwa ujumla. Naamini tunapozungumzia kulipa kodi, kuna kodi mbalimbali, kuna kodi za mazao ya shamba, mazao ya viwanda, za biashara na kadhalika. Katika mzunguko huu wa hizi kodi ndipo tunapotengeneza maendeleo ya nchi na tunapoona ushiriki wa kila mmoja wetu katika kuleta maendeleo ya nchi yetu. Nichukue mfano wa mkulima wa pamba; analima pamba kama yeye anaipeleka kiwandani, kiwandani itatengenezwa nyuzi, itapelekwa kwenye kiwanda itatengenezwa nguo, itapelekwa dukani itauziwa watu mbalimbali na kadhalika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nichukue mfano huu nijikite kwenda kutetea hoja moja ya kwamba TRA sasa ikusanye mapato ya property tax badala ya Halmashauri. Majengo tunayoyaona mijini sehemu kubwa ni ya biashara, ni viwanda na ofisi. Wanahudumia akina nani? Wanahudumiwa wananchi wa Tanzania, wako wapi? Asilimia 70 ya Watanzania wako vijijini, ina maana gani? Ina maana kwamba hayo majengo, hizo biashara za mjini na ofisi za mjini zinaendeshwa pia na watu wa vijijini kwa kiasi kikubwa, kama ni vyakula vikitengenezwa vitakwenda mpaka kijijini kwenye asilimia 70, kama ni nguo zitakwenda mpaka vijiji kwenye asilimia 70 ya wananchi.
Tukiangalia Halmashauri za vijijini mapato yao ni kidogo, kwa sababu maendeleo makubwa yako mijini, Halmashauri za mijini zina mapato makubwa kwa sababu zinabebwa na Halmashauri za vijijini. Kwa hiyo, unapoacha wa mjini anafaidi wakijijini hafaidi, kwa kiasi fulani tunakuwa hatuwatendei haki, lakini naamini sasa kwa kusema TRA ikusanye itaweka ratios ambazo zitaisaidia kwamba hata Halmashauri za vijijini zipewe fungu na makusanyo hayo. Sawa mjini watapata fungu lao kubwa, lakini vijijini na wao hawataachwa watapewa fungu ili kwa pamoja tuweze kuangalia namna gani tunasukuma maendelo.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo machache nichukue nafasi hii niseme tu kwamba naunga mkono hoja kwa asilimia 100 asante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JOEL M. MAKANYANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Mawaziri wote wawili kwa kazi nzuri sana mnayoifanya. Nawapongeza sana pia kwa bajeti yenu nzuri iliyowasilishwa Bungeni tarehe 23 Aprili, 2018.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakiri sana kwamba mipango yote mliyoianisha ni mipango mizuri sana na kwamba kama ikifanikiwa kutekelezeka basi nchi hii tutashuhudia maendeleo kwa kasi kubwa. Kwa maana hii naiomba Serikali ijitahidi kupeleka fedha kwenye miradi iliyotengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe shukurani zangu nyingi sana kwa kazi nzuri iliyofanyika katika kazi zifuatavyo:-

(i) Daraja kati ya Kijiji cha Chilonwa na Kijiji cha Nzali lilifukuliwa upande mmoja na sasa mwaka huu pamoja na mvua kuwa kubwa, lakini maji yalipita juu ya daraja kwa kimo cha futi moja tu badala ya mita moja karibia na futi tatu. Hongereni sana.

(ii) Kwa ujenzi wa madaraja mawili, moja dogo na moja kubwa pale kwenye Kijiji cha Membe, ahsante sana.

(iii) Ukarabati wa barabara yote kutoka Buigiri kwenda Chamwino Ikulu, kwenda Chilonwa, kwenda Membe, kwenda Dabalo, kwenda Itiso hadi Segala, Izava umeendelea kufanyika kwa ubora mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi mahsusi:-

(i) Daraja lililopo kati ya Kijiji cha Chilonwa na Kijiji cha Nzali ifukuliwe na upande wa pembeni ambapo lipo daraja lingine (madaraja haya yanafanya kazi sambamba). Hii itasaidia kuhakikisha maji hayapiti juu ya daraja kabisa.

(ii) Lipo daraja linaingia Dabalo linahitaji kutengenezwa/kujengwa ili eneo hilo liweze kupitika bila hofu wakati wa mvua.

(iii) Lipo daraja linalopokea maji kutoka daraja la hapo juu (namba 2) linalounganisha Kijiji cha Dabalo A na Dabalo B (Igamba) nalo naomba lipewe kipaumbele (daraja hili sasa lipo chini ya TARURA).

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba uyapokee maombi yangu kwa niaba ya wananchi wa Jimbo langu la Chilonwa.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. JOEL J. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja katika mjadala huu wa bajeti ya Serikali mwaka 2017/2018. Nianze kabisa kwa kumpongeza Waziri wa Fedha na Mipango, Naibu wake pamoja na timu yao nzima kwa uandaaji wa bajeti nzuri kabisa waliyoiandaa hapa na walivyoiwasilisha kwa umahiri kabisa hapa ndani. Nianze kwa kuiunga mkono bajeti hii kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuudhihirishia umma kwamba bajeti hii imedhihirisha nia thabiti ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kuipeleka Tanzania kwenye uchumi wa kati kupitia viwanda kwa maana ya Tanzania ya viwanda. Bajeti hii inatilia mkazo ujenzi wa Reli ya Kati kwa kiwango cha standard gauge. Reli hii itakapojengwa kwa kiwango cha standard gauge itasaidia mambo kama yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa itasaidia kutupatia pesa za ziada kwa maana ya kusafirisha mizigo ya nchi jirani. Pili, itatusaidia kupunguza gharama ya uzalishaji ya viwanda vyetu tulivyonavyo na viwanda tunavyovitegemea katika kuingiza nchi yetu katika uchumi wa kati. Mwisho, itatusaidia sana kutuondoa na tatizo kubwa la utumiaji mkubwa wa pesa katika kufanya matengenezo ya mara kwa mara kwenye barabara zetu kwa sababu ya kupitisha mizigo mizito ambayo inapitishwa sasa kutokana na ukosefu wa reli madhubuti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti hii vilevile imejikita kumwangalia Mtanzania wa chini kabisa kwa maana ya ile asilimia kubwa kati ya asilimia 65 hadi 70 ya Watanzania ambao ni wakulima. Tunaiona bajeti hii imeamua kumwondolea mzigo wa kodi kero mbalimbali mwananchi, imepunguza kodi za mazao ya chakula na kupunguza kodi za mazao ya biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile bajeti hii imeonesha wazi kabisa kumjali Mtanzania wa kawaida na wa chini kwa kuhakikisha kwamba anapata umeme kule aliko kijijini kupitia mpango wa REA awamu ya tatu. Katika hili, kupitia uchangiaji wa bajeti hii niombe kabisa wahusika wahakikishe kwamba ukamilishaji wa REA awamu ya tatu unafanyika ili wananchi waweze kufaidika na mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia bajeti hii inajikita katika kuwasaidia Watanzania kuingia kwenye viwanda. Kwa mfano, inajikita kuanzisha mashamba ya miwa ili kuanzisha viwanda vingine vya sukari vitakavyowasaidia wananchi kupata uchumi kwa maana ya kulima miwa. Katika hili niombe kabisa juzi nilipata fursa ya kuongea na Waziri wa Ardhi kwamba katika Jimbo langu la Chilonwa, Kata ya Dabalo Serikali imeweza kuongea na wananchi pamoja na wawekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, amepatikana mwekezaji ambaye yuko tayari kuanzisha kiwanda pale, mazungumzo yalishafanyika na wananchi walishalima miwa, miwa imefika kiwango cha kuvunwa sasa lakini mwekezaji huyo bado kuna tatizo dogo la kupatiwa hati ya kiwanda ili aweze kujenga kiwanda na zoezi la wananchi kuanza kujipatia fedha kwa ajili ya biashara ya miwa ianze kuwafaidisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti hii ni nzuri sana kwetu na tunaposema bajeti ni nzuri tunakuwa na vigezo. Kitu kizuri au kibaya unapokilinganisha na kingine lakini kama ndio kwanza unakipata hakiwezi kuwa kizuri au kibaya ni kwamba umeanza. Tunaposema bajeti hii ni nzuri tunailinganisha na bajeti za miaka kadhaa iliyopita, tunaona na tunashuhudia wenyewe jinsi bajeti ilivyosimama katika kumsaidia Mtanzania wa kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo wenzetu ambao wanajaribu kuibeza hii bajeti, waone kwamba bajeti hii tunakwenda mbele hatua moja baada ya nyingine, ni sawasawa na mtu katika maisha yako ya kawaida. Leo unapokuwa mtu wa kawaida huna hata baiskeli unatamani sana uwe na baiskeli, huwezi kutamani uwe na ndege hata siku moja, lakini ukipata baiskeli kesho utatamani uwe na pikipiki, huwezi kutamani kuwa na gari wakati huna pikipiki, ukipata pikipiki kesho utatamani uwe na gari. Kila jambo linakwenda kwa hatua, hapa tulipofikia ni hatua muhimu sana na tuna uhakika tuko kwenye njia sahihi ya kutufikisha kwenye Tanzania ya uchumi wa kati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii sasa kwa umakini kabisa, niiombe Serikali itusaidie wananchi wetu vijijini waweze kusaidiwa katika matatizo ya maji waliyonayo. Tumesema kutakuwa na michango ya Sh.40/= katika kila lita kwa maana ya replacement ya road license, lakini tunajua kabisa kwamba pesa hiyo inapokusanywa kutoka kwenye chanzo chochote cha Serikali inakwenda kutumika katika sekta mbalimbali ambazo zinakwenda kuwasaidia Watanzania. Vilevile katika suala la ahadi za viongozi, niombe sana Serikali izingatie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wetu wanajisikia kama viongozi wanatoa ahadi na ahadi zile zinatekelezeka. Kwa kweli naishukuru Serikali hii sikivu, juzi nilikuwa na swali kuhusu ujenzi, nikamchukua Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano tukaenda naye kwenye daraja ambalo Mama Samia alitoa ahadi wakati wa kampeni na nashukuru kwamba Serikali imetenga fungu kwa ajili ya kuanza kulishughulikia safari hii. Vilevile niseme, isiishie hapo tu, kuna daraja linalounganisha Kijiji cha Msanga na Kijiji cha Kawawa, vilevile ni kati ya ahadi zilizoahidiwa na Serikali wakati ule, naomba zote zitiliwe maanani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mchango huo mfupi, naomba kuunga mkono hoja tena. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hotuba mbili za Mawaziri wa Wizara ya TAMISEMI pamoja na Utawala Bora ambazo zimewasilishwa hapa jana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa ninampongeza Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, kwa utendaji wake mzuri. Tunashuhudia sasa tuna miaka miwili na nusu tangu ameingia madarakani na tuliona mwanzo kabisa alipoanza watu tulifika mahali tukafikiri kwamba hii ni nguvu ya soda, lakini tunadhihirisha muda unavyokwenda nguvu hii inazidi kuwa kubwa zaidi. Kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili nichukue fursa hii kuwapongeza Mawaziri husika wa Wizara ya TAMISEMI pamoja na Utawala Bora, Mheshimiwa Jafo pamoja na Naibu Mawaziri wako, pia kwa Mheshimiwa Kepteni Mkuchika, mmedhihirisha kwamba ninyi ni hodari na kwamba Mheshimiwa Rais hakukosea kuwateua katika nafasi hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia kwanza kabisa suala la utawala bora, wachangiaji walio wengi wamejaribu kuchangia, nami nataka niguse sehemu ambayo naona kama haijapewa uzito unaostahili. Katika suala la utawala bora vipo vigezo vingi vinavyotumika kusema hapa kuna utawala bora wengi wamevizungumza hivyo, lakini mimi nizungumzie suala la kuwa msikivu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kuwa kiongozi bora kama wewe siyo msikivu, lazima uwasikilize wenzako, lazima uwasikilize walio chini yako wanasema nini ili utoke hapo ujue namna gani ya kuifanya kazi yako iende vizuri. Katika hili niwe wa kushuhudia katika hili pamoja na Wabunge mliomo ndani humu, kwamba Serikali hii ya Awamu ya Tano ni sikivu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nipo kwenye Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa, tulikuwa watu wa kwanza wakati tumeanza kujadili hizi bajeti kwenye Kamati zetu, tarehe 19 Machi ndipo tulianza kujadili hizi bajeti na siku hiyo tulikuwa tunajadili bajeti ya Utawala Bora. Wajumbe wa Kamati walilizungumzia kwa kina sana na kwa uchungu sana suala la watumishi walioachishwa kazi kutokana na kigezo cha kutokuwa na elimu ya kidato cha nne na tunashukuru Mheshimiwa Waziri alilichukua na akasema atalifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama vile haitoshi, tarehe 4 Aprili tulianza vikao vya Bajeti hapa ndani na Wabunge humu ndani wamechangia kwa nguvu sana, kwa uchungu sana, suala hili la watumishi walioachishwa kazi kwa kutokuwa na elimu ya kidato cha nne. Tarehe 9 Aprili nataka muone jinsi gani Serikali yetu ni sikivu Mheshimiwa Waziri, Kepteni Mkuchika, amesimama hapo mbele na kutoa tamko ambalo tunalijua sisi sote. Tuseme nini sasa kama siyo usikivu wa Serikali. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa msemaji anayeendelea kuongea sasa hivi kwamba hata hao watu ambao walifukuzwa kwenye kazi walifukuzwa na Serikali ile ile ambayo imewarudisha. Kwa hiyo, hakuna usikivu wowote kwa sababu wangetaka kusikia wasingewafukuza toka mwanzo, siyo wanasubiri waondoke halafu wawarudishe tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Sina haja ya kusikiliza ushauri huo kwa sababu unaposema mtu msikivu ni baada ya kupewa ushauri. Bunge tunafanya kazi gani humu ndani, kazi yetu ni kuishauri Serikali. Baada ya kuwa yametendeka mambo ambayo hayako vizuri tumefanya kazi yetu ya kuishauri Serikali na Serikali imesikia, imetekeleza, tuseme nini sasa? (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa yake lakini kwa angalizo, naipokea. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee upande wa TAMISEMI, katika kuzichambua bajeti za Wizara hizi mbili, jambo lililojitokeza la wazi ni kwamba upelekaji wa fedha za maendeleo kwenye Halmashauri zetu ni mdogo sana unasuasua, jambo hili linafanya miradi yetu ya maendeleo kwenye Halmashauri haiendi katika kasi tunayoitarajia. Sambamba na hilo, ilijidhihirisha pia suala zima la ukusanyaji wa mapato ya ndani kwenye Halmashauri zetu pia linasuasua, haya mambo yote yanachangia kufanya miradi yetu ya maendeleo kusuasua katika Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili naomba nizungumze suala moja, ninaiomba sana TAMISEMI, pale Halmashauri zinapokuja zinahitaji ushauri basi maamuzi yawe yanatoka mapema ili kama kunahitajika kuchukua plan B Halmashauri ziweze kuchukua na kusonga mbele na masuala ya maendeleo. Katika hili nitoe mfano mmoja kwa Mheshimiwa Jafo, Waziri wa TAMISEMI, Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino imekuwa na matatizo ya ulipaji fidia kwa viwanja vilivyopimwa katika maeneo ya Buigiri na maeneo ya Aneti, pesa imekosekana ya kulipa fidia, Halmashauri imekuwa ikijaribu kupata hela kutoka sehemu mbalimbali bila mafanikio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara ya mwisho tumeandika barua kama Halmashauri, imekuja ofisini TAMISEMI kwa maana ya kwamba watusaidie tupate mkopo ili tuweze kulipa fidia kwa wananchi na viwanja vile viweze kugaiwa. Viwanja hivi vikigaiwa ni chanzo cha kuleta maendeleo, watu watajenga na kodi zitakusanywa, mapato ya ndani yataongezeka na miradi ya maendeleo itatekelezeka. Ninaomba sana katika hili Mheshimiwa Waziri uliangalie kwa karibu kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ninapenda nizungumizie ni suala zima la elimu. Tunalia sana na masuala ya elimu na hasa tunalia ukosefu wa walimu, sehemu kubwa tunalia walimu wa sayansi mashuleni. Jambo hili pia liko mezani kwako Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI. Kuna walimu wa sayansi ambao walikuwa form six, lakini wamesoma wamemaliza wamepata degrees zao mpaka sasa wana miaka mitatu wanafanya kazi hawajarekebishiwa mishahara yao, wanateseka sana lakini pia wanavunjwa mioyo katika utekelezaji wao wa kazi. Tunaomba haya mambo yafanyike kwa haraka ile watu waweze kufanya kazi kwa moyo mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuishukuru sana TAMISEMI, walitupatia kama Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino shilingi milioni 500 kwa ajili ya kukarabati kituo cha afya pale Chamwino, pia walitupatia shilingi milioni 400 zilienda kwa Ndugu yangu Mheshimiwa Livingstone Joseph Lusinde kule Jimbo la Mtera kukarabati zahanati. Kama vile hiyo haitoshi pia wametupatia shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Chamwino, tunasema ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo machache, naomba kuunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JOEL M. MWAKANYAGA: Mheshimiwa Spika, naomba kushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika hotuba ya bajeti kuu ya Serikali iliyowasilishwa na Waziri Mheshimiwa Dkt. Mpango tarehe 14 mwezi huu.

Mheshimiwa Spika, pili, nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, nitaendelea kumpongeza kila nikisimama kwa sababu kazi yake anayoifanya tunaiona ni nzuri na moja kati ya vigezo kwamba kazi inayoyofanywa ni nzuri tunaona, bajeti hii imetolewa katika kipindi chake akiwa Rais. kwa hiyo, hii ni bajeti ambayo ina mwongozo moja kwa moja toka kwa Mheshimiwa Rais na ni bajeti nzuri kama tunavyoiona, nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatu nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango yeye pamoja na Naibu wake, lakini pamoja na Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa Wizara ile kwa kazi kubwa waliyoifanya katika kuiandaa hotuba hii na bajeti hii ambayo sasa tunaijadili hapa Bungeni. Mwisho, nimpongeze yeye binafsi kwa uwasilishaji mzuri sana wa bajeti alioutoa siku ile ya tarehe 14 hapa Bungeni.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kusema kwamba mpango ni mpango na mipango tunayo sisi sote, majumbani mwetu tuna mipango mingi na hakuna mtu anayepanga na mipango yake ikatimilika asilimia 100, si kawaida. Utapanga kufanya vitano, utatekeleza vitatu au vinne mpango ni dira, dira inapokuwa nzuri una hakika kwamba wewe unapiga hatua nzuri; mipango yetu ni mizuri na ndiyo maana tunasema bajeti hii ni nzuri sana. Bajeti hii ni nzuri kwa sababu imelenga kwa wananchi wa kawaida, wananchi wa chini kabisa. Kwa nini nasema hivyo, tukienda kwenye kitabu cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa kuanzia 42 kuendelea hadi 46 yako mambo mengi yaliyozungumzwa pale.

Mheshimiwa Spika, nijikite kwenye misamaha na mfumo wa kodi ambao baadhi umejionesha pale. Serikali imesamehe kodi ya ongezeko la thamani kwa baadhi ya malighafi muhimu zinazokuja kutumika viwandani kuzalisha bidhaa zinazotumika kwa Watanzania. Pia Serikali hiyo hiyo imeongeza ushuru wa bidhaa za kutoka nje kwa bidhaa ambazo pia zinazalishwa hapa nchini, lakini pia tumeona Serikali safari hii haijagusa kabisa kuongeza kodi kwenye bidhaa zote za mafuta ikiwemo diesel pamoja na petrol.

Mheshimiwa Spika, hatua hizi ni muhimu sana, hatua hizi zitasaidia sana kupunguza mfumuko wa bei za bidhaa mbalimbali zinazozalishwa hapa nchini. Tunapopunguza gharama za uzalishaji maana yake bei za bidhaa zetu ama zitabakia constant, ama zitashuka chini kidogo. Kwa hiyo basi, kama tulivyoona kwenye punguzo na ongezeko ya kodi mbalimbali ambazo tumezitaja hapo nyuma kwa mfano, madawa ya binadamu, vyakula vya binadamu, vyakula vya mifugo, hivi ni vitu ambavyo moja kwa moja vinamgusa Mtanzania wa kawaida.

Mheshimiwa Spika, vilevile hatua hizi zinalenga kulinda viwanda vya ndani jambo ambalo ndilo kipaumbele kikubwa cha Serikali yetu ya Awamu ya Tano ya Tanzania ya viwanda. Tunapolinda viwanda vya ndani maana yake tunakuza ajira kwa Watanzania. Suala la uchumi wa Tanzania limejitokeza wazi kabisa kwamba linakua kwa kasi kubwa sana, lakini ukiangalia upande wa pili wa mwananchi wa kawaida, uchumi wa mwananchi wa kawaida hauonekani kukua kwa kasi sambamba na kasi ya uchumi wa Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, hili ndilo kipaumbele cha nchi yetu cha Serikali ya Awamu ya Tano kwamba Tanzania ya viwanda inalenga kuwe na viwanda vingi, viwanda vinavyotegemea sana mazao ya kilimo. Kwenye kilimo ndiko kunaajiri zaidi ya asilimia 75 ya Watanzania, sasa ukiwezesha kuwa na Tanzania ya viwanda maana yake unatengeneza soko kwa ajili ya mazao yetu yanayozalishwa hapa Tanzania, maana yake unawawezesha Watanzania wa kawaida kupata kipato kitakachowasaidia kukuza uchumi wao. Katika kilimo utakuta Watanzania wote tupo, wapo Watanzania wa kawaida lakini wako vijana sehemu kubwa, wako akinamama na hata walemavu wako humohumo ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ili mipango hii iweze kuwa na tija, Serikali inatakiwa ijizatiti. Ijizatiti kweli katika kukusanya mapato yake, ihakikishe kwamba taratibu zote za ukusanyaji wa mapato, tumesikia baadhi ya Wajumbe wakichangia hapa wasiwasi unaokuwepo juu ya nani anasimamia nini katika ukusanyaji wa mapato haya. Ni vizuri tukajihakikishia kwamba tuko kwenye mikono salama, pesa yetu isichopoke chopoke huku na huko ili moja kwa moja itumike katika kuitekeleza hii Bajeti ya mwaka wa bajeti 2018/2019.

Mheshimiwa Spika, niombe sana, pesa hii inapopatikana ielekezwe kule kunakohusika. Wizara mbalimbali zimeleta bajeti zao na ndiyo hii sasa imeletwa kwa ujumla, imeletwa kama Bajeti Kuu ya Serikali. Kama Wizara hazitapewa bajeti zao walivyoomba basi suala zima la Bajeti hii kutokuwa na manufaa sana kwa wananchi litakuwa limeleta shida.

Mheshimiwa Spika, nije kwa upande wa ardhi, bajeti hii inahitaji wananchi wafanye kazi. Wananchi wanatakiwa kuwa na peace of mind katika kuzifanya kazi zao. Kama wananchi watakuwa na hali ya migogoro ya hapa na pale ya ardhi maana yake ni nini? Zoezi zima la uzalishaji kwao litakuwa siyo la ufanisi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimwombe sana ndugu yangu Waziri wa Ardhi, kuna migogoro mingi ambayo unaishughulikia, naomba uishughulikie kwa kasi kubwa. Nakuamini sana Mheshimiwa Lukuvi kazi unayoifanya, lakini nikuelekeze pia, hata hapa Dodoma kuna migogoro ya ardhi, hata kule Chamwino kuna migogoro ya ardhi na bahati nzuri wewe ulishawahi kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma unafahamu nini ninachokizungumza, unayafahamu maeneo ya Wali kule kuna mgogoro wa ardhi kati ya Wilaya ya Chamwino na Wilaya ya Kongwa. Inafika mahali wananchi wanakimbia maeneo yao, kipindi cha kulima wanakimbia maeneo yao wanashindwa kufanya kazi inavyostahili. (Makofi)

Mheshimiwa pika, ahsante sana, labda nimalizie moja tu kwa upande wa viwanja kwako, Mheshimiwa Lukuvi viwanja pale Buigiri vimepimwa siku nyingi lakini zoezi zima la kuvigawa vile viwanja limekuwa tatizo. Mheshimiwa Waziri alikuja pale Wilayani akaotoa maelekezo lakini maelekezo hayo yajafuatwa. Naomba sana alitekeleze hili ili wananchi wafanye kazi kwa amani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo machache, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nashukuru sana kupata nafasi hii leo kuwa mmoja kati ya wachangiaji katika hotuba ya Waziri wa Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa John Joseph Pombe Magufuli pamoja na Serikali yake yote, kwa namna wanavyofanya kazi kwa umakini mkubwa sana unaotuletea Taifa manufaa makubwa sana ambayo sote tunayaona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia nafasi hii kumpongeza sana Waziri wa Wizara hii pamoja na Naibu Mawaziri wake wote wawili kwa kazi kubwa wanayoifanya ambayo sote tunaiona. Kipekee kabisa nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa namna alivyoiwasilisha hotuba hii hapa leo asubuhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii sasa niseme kwamba toka Serikali ya Awamu ya Tano imeingia madarakani tumeona hatua kadha wa kadha zinazochukuliwa ambazo zinalenga kuboresha maslahi ya nchi hii. Tumeona hatua madhubuti zilizokwisha kuchukuliwa mpaka sasa zinazoihusu Wizara hii ya Madini, mojawapo ikiwa ni suala la makinikia, kazi kubwa imefanyika, sisi sote tuna masikio tulisikia, tuna macho tuliona, tunaona jinsi gani mambo yanavyokwenda sasa ukilinganisha na hapo awali kuhusiana na suala zima la makinikia na mapato ya Serikali kupitia jambo hili la makinikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona pia hatua ya ujenzi wa ukuta kuzunguka machimbo ya tanzanite kule Mererani. Kwa hakika mambo haya pamoja na mengine mengi yameongeza kwa kiasi kikubwa sana mapato ya Wizara hii katika uchumi na ujenzi wa Taifa hili la Tanzania. Tunawashukuru sana na kuwapongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Dodoma kama inavyooneshwa kwenye kitabu hiki tulichogawiwa cha Wakala wa Jiolojia Tanzania kuhusiana na madini yanayopatikana Tanzania, Dodoma pia ipo kwenye orodha na ina madini mengi sana. Dodoma hakuna wilaya ambayo haina madini, kila wilaya ina madini yasiyopungua mawili, matatu ambayo yanapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile sasa Wizara zote ziko Dodoma ikiwepo na yake, naomba waangalie ni namna gani madini haya ikiwemo madini nikel, dhahabu na chrysoprase ambayo yanachimbwa kwa wingi sana katika Wilaya ya Chamwino na hasa katika Jimbo langu la Chilonwa yataweza kunufaisha wananchi wetu. Halmashauri hatuna tunachopata kwa maana ya service levy na corporate responsibilities hatuzioni katika maeneo yetu ambako madini haya yanachimbwa. Kwa hiyo, kwa wao kuwa hapa Dodoma hebu wasaidie Halmashauri zetu ziweze kuwa miongoni mwa Halmashauri zinazofaidi machimbo haya yaliyopo hapa Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuangalia hiki kitabu niseme tu sijaelewa sana ni kwa nini, kuna madini yanaitwa dhahabu nyeusi (black gold) na najua anafahamu, haya ni mawe. Mawe haya kulingana na wachimbaji kwa jinsi tulivyokaa na kuongea nao wanachimba kule Kibaha pia lakini wakilinganisha na hapa Dodoma madini hayo wanayachimba kule Itiso, madini ya hapa yana ubora wa hali juu sana, siyaoni kwenye hiki kitabu. Tulivyokwenda kutembelea kule madini haya ya black gold yanatumika kwa sehemu kubwa sana kutengeneza marumaru yenye ubora wa hali ya juu sana na zote zinauzwa nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Serikali kuhamia Dodoma kwamba sasa ujenzi mwingi unafanyika hapa Dodoma, hebu nilete rai kwa Waziri, waangalie namna gani wanavyoweza kuhakikisha marumaru zinazopatikana Itiso zinakuwa sehemu kubwa ya ujenzi ya majengo yanayojengwa hapa Dodoma kwa kipindi hiki ili angalau kama Serikali tuweze kuwa na sehemu ya kufanya mchakato wa yale mawe na kupata final product tu-generate ajira kwa ajili ya vijana wetu pia na kipato kwa ajili ya wananchi wetu. Naomba sana Mheshimiwa Waziri akiona inafaa pamoja na Naibu Mawaziri, mmojawapo baada ya bajeti hii hebu tukatembee huko mkajionee wenyewe kwa macho ni nini kinachoendelea kule na ni namna gani kwa ukaribu zaidi mnaweza mkasaidia kuhakikisha kwamba Halmashauri zetu zinaweza kunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, niseme kwamba naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Rais Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Serikali nzima ya Awamu ya Tano na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa kazi kubwa inayoendelea kwenye WIzara hii. Naipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa kutoa pesa za kutosha kwa Wizara hii kulingana na bajeti ya 2018/2019 (page 10 and 11). Matumizi ya kawaida fedha iliyotoka ni asilimia 72.66 Vs asilimia 75. Miradi ya maendeleo fedha iliyotoka ni asilimia 60.98 Vs asilimia 75.

Mheshimiwa Spika, naipongeza sana miradi mikubwa ya Kitaifa kama ilivyoorodheshwa kitabuni ukurasa 53, 61, 117, 192 na kadhalika. Vile vile naipongeza sana Serikali kwa miradi mikubwa hapa Jijini na Mikoani Dodoma. Miradi hiyo ni Dodoma outer ring roads pages 47,176 and 271. Ujenzi wa Ikulu ya Chamwino zikiwemo na barabara za kwenye Mji wa Chamwino. Ujenzi wa Miji ya Kiserikali pale Mtumba. Lami barabara ya Kongwa Junction – Mpwapwa – Gulwe – Kibakwe.

Mheshimiwa Spika, nina ombi mahsusi; daraja kati ya Chilonwa na Nzali ambayo ni ahadi ya Mheshimiwa Makamu wa Rais, mama Samia Suluhu Hassan. Barabara ya Chalinze Nyama – Chilonwa – Dabalo – Itiso – Chenene. Mawasiliano ya simu za mkononi katika Kata zifuatazo: Zajilwa (ina vijiji vitatu) Segola (ina vijiji vitano) Haneti (ina vijiji vinne) Itiso (ina vijiji vinne) Dabalo (ina vijiji vitano) pia kwa sasa kuna Dabalo ni Mji mdogo na Membe (ina vijiji vitatu). Kata hizi tano zina mawasiliano hafifu tena kwa wakati fulani.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika hoja hii ya Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wengi wamezungumza masuala muhimu kwa kuipongeza kazi kubwa iliyofanywa na Mheshimiwa Waziri pamoja na Wizara yake yote ya Fedha na Mipango. Nami sitabaki nyuma, naomba nichukue nafasi kuipongeza sana Wizara hii na Waziri mwenyewe kwa kazi kubwa kwa mpango huu waliotuletea hapa mbele. Ni mpango unaoonekana kabisa unaenda kutuvusha maana tuna lengo la kuivusha Tanzania toka hapa tulipo kuipeleka kuwa Tanzania ya viwanda ili tuingie katika uchumi wa kati mwaka 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba nijikite katika masuala matatu hivi katika kitabu hiki tulichopewa cha Mapendekezo ya Mpango, kwanza nizungumzie suala la elimu. Suala la elimu kama ilivyoorodheshwa katika kipengele namba 4.5.1.1(b), kuboresha mazingira ya utoaji elimu katika ngazi za shule za awali, shule za msingi, shule za sekondari ikijumlisha ujenzi wa madarasa, mabweni na maabara, hili ni jambo zuri sana. Tunapozungumza kutaka kulivusha Taifa kutoka hapa kuingia katika uchumi wa kati elimu ni kitu cha msingi sana. Elimu yetu ni lazima ianzie huko chini awali, msingi, sekondari baadaye ndiyo tunakuja kupata elimu za ujuzi na stadi mbalimbali pamoja na elimu ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima kubwa wananchi wa Tanzania wamekuwa wakijitolea sana kufanya shughuli za maendeleo kuunga mkono Serikali yao katika sekta hii ya elimu. Wamezungumza baadhi ya wasemaji waliopita kwamba wananchi wamejitolea wamejenga shule yamebaki maboma, wamejenga zahanati yamebaki maboma, wamefanya kazi nyingi sana lakini yamebaki maboma, Serikali ina mpango gani juu ya hili? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili napenda kabisa niungane na wazungumzaji waliopita nikim-cite ndugu yangu Mheshimiwa Kanyasu kwamba Serikali ina haja ya kufikiria sasa inafanya nini na maboma haya yanayobaki kila wakati. Halmashauri zetu hazina uwezo, haziwezi hata dakika moja, maboma ni mengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama hilo halitoshi kuna suala zima la watu kujikusuru, wamejenga madarasa mawili kwa uchache ili tusiendelee kuweka maboma mengi, unajenga madarasa mawili mnaezeka mnayaweka sawa. Mkitaka kuanzisha shule, tumesikia shule zina wanafunzi wengi sana wa kuzidi kabisa haifai shule kuwa na wanafunzi 7,000 lakini wananchi wetu wanajitolea wamejenga madarasa mawili wanataka kuisajili shule haiwezekani, sasa tunafanya nini? Siyo tunawavunja nguvu kweli, tunawavunja moyo badala ya kuwatia moyo kwa kuzisajili hizi shule labda na kuwaambia tunaomba kila baada ya mwaka basi muongeze madarasa mawili mengine mzisajili shule ziweze kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna shule nyingi ambazo zimekamilika lakini madarasa mawili haijasajiliwa. Kwa hili kwa kweli ningeshauri Serikali hebu iliangalie kwa kina shule zote ambazo zimekamilika zikiwa na madarasa hayajafika hayo sita zisajiliwe ili wanafunzi waanze kusoma. Tuambizane tu kwamba kila mwaka tujitahidi tuweze kuongeza madarasa mengine pamoja na nyumba za walimu ili tuweze kusonga mbele. Hilo ni kwa upande wa shule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la pili la maji na afya. Maji ni muhimu sana ili wananchi wetu wawe na afya bora. Wananchi wetu wakiwa na afya bora wataweza kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo na katika kuisukuma nchi kuivusha kutoka hali hii ya uchumi tuliyonayo hadi uchumi wa kati lakini maji safi na salama ni shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikishangaa ukiangalia kwa kiasi kikubwa sana vyanzo vya maji na salama ama vinatokana na mito ama vinatokana na mabwawa yaliyojengwa kama hivi tunaona kuna mabwawa ya Farkwa yanatakiwa kujengwa huo lakini wewe ni shahidi Kanda yetu ya Kati, Dodoma maji chini ya ardhi ni mengi sana. Mji wa Dodoma kwa wasiojua unapata maji siyo ya bwawa, siyo ya mto, maji yanatoka kwenye visima kule Mzakwe kwa Mji wote wa Dodoma. Hii ni kudhihirisha kwamba chini ya ardhi Dodoma kuna maji mengi. Sasa inashangaza, nenda vijijini kwetu watu wana shida ya maji kwa nini Serikali isiweke nguvu ya makusudi kuchimba visima vya uhakika kila kijiji ili watu wapate maji safi, wawe na afya bora na washiriki katika kuleta maendeleo ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la maji na kilimo. Tunazungumzia kuivusha nchi hii kwenda kwenye uchumi wa kati kupitia viwanda vinavyotegemea kilimo. Kama kilimo chetu tutategemea mvua nadhani hapo tumepotea njia. Kilimo chetu lazima kiwe kilimo cha uhakika. Kilimo cha uhakika ni kilimo cha umwagiliaji ama utatumia mabwawa lakini kwa Dodoma kama tunavyoendelea kusema Dodoma maji chini ni mengi Serikali ifanye juhudi ya makusudi maeneo fulani fulani ichimbe visima kwa ajili ya vijana kufanya shughuli za umwagiliaji na uzalishaji ambao utalisha viwanda vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niongelee suala zima la umeme. Tunapozungumzia Tanzania ya viwanda maana yake tunazungumzia umeme lakini umeme bado ni tatizo sehemu kubwa sana vijijini yaani tunataka kusema kwamba maendeleo yaje mjini vijijini hapana. Naipongeza sana Serikali kwa mpango mzima wa REA ambao unakwenda kwa kasi vijijini naomba kasi yake iongezwe ili hivi viwanda ambavyo vimeshamiri mijini pia vikapatikane huko vijijini na mambo mengine ya uzalishaji yapatikane vijini badala ya kila jambo kuja mjini. Mazao yazalishwe vijijini yaje mjini kuchakatwa, kwa nini yasichakatwe huko huko, mjini zije ama semi-finished product au finished products kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, mchango wangu ni huo, maoni yangu ni hayo Mheshimiwa Waziri kama akiyachukua akiyafanyia kazi nitashukuru sana. Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, nashukuru kupata nafasi nami niweze kuchangia katika hoja hii iliyo mezani inayohusu Kamati Tatu za Kudumu za Bunge. Kwa sababu ya muda naomba niende haraka haraka tu.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli napongeza Kamati zote tatu, viongozi wao pamoja na Wanakamati wote kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wameifanya, tumezisikia ripoti zao, zimekaa vizuri, wala hakuna shaka yoyote juu ya hiyo. Tunachokifanya hapa ni kujaribu kuongeza nyama kidogo, lakini kuweka msisitizo kwa baadhi ya mambo ambayo wameyazungumza wenzetu kwenye ripoti zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa haraka haraka niseme kwamba sasa Serikali yetu ya Awamu ya Tano iliyoko madarakani imemaliza miaka mitatu. Ni kazi kubwa ambayo imeshafanyika sasa hivi, kila mtu anaiona. Kazi hii ndiyo ilikuwa chanzo cha Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa John Pombe Joseph Magufuli kusema kwamba katika awamu hii yeye anasema Hapa Kazi Tu. Katika Serikali ya Awamu ya Tano bila kuwa na Hapa Kazi Tu, mambo makubwa yanayotendeka yasingeweza kutendeka kufikia hapa tulipofika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba Serikali iliamua kwa dhati, kwa kauli moja kwamba tuijenge Tanzania ya Viwanda ambayo itaisaidia nchi hii kuvuka toka katika uchumi wa chini kwenda uchumi wa kati. Hizi ndizo kazi kubwa zinazofanywa na Wizara mbalimbali. Kati ya Wizara hizo, ziko Wizara ambazo zinasimamiwa na Kamati hizi tatu ambazo tunajidiIi hapa leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikizungumzia kwa uchache kabisa, Kamati ya TAMISEMI, tunazungumzia masuala ya elimu. Katika elimu, Awamu ya Tano walisema Elimu Bila Malipo. Elimu Bila Malipo bila kumung’unya maneno, imekuwa na matokeo chanya sana kwa Taifa letu, tunawapongeza sana. Tulikuwa na kampeni ya kuhakikisha watoto wetu wote wanaingia darasani na wanakaa kwenye madawati, tulifanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kupitia kauli hii ya Elimu Bila Malipo, sasa hivi tatizo la madawati limerudi pale pale, kwa sababu watoto walioandikishwa kuingia Darasa la Kwanza wamekuwa wengi kuliko vile ilivyotegemewa. Kazi kubwa bado tunayo mbele, tunatakiwa tuifanye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, kuna maboma mengi ya madarasa na nyumba za Walimu ambayo yanahitaji kumaliziwa. Tunafahamu Serikali inatoa rai kwa Halmashauri zetu kuhakikisha kwamba maboma yote yanakamilishwa ili yaweze kutumika inavyostahili.

Mheshimiwa Spika, naomba kupitia hadhara hii leo kwamba siyo Halmashauri zote ambazo zina uwezo wa kukamilisha maboma hayo kwa muda mfupi. Kwa hiyo, naiomba Serikali zile Halmashauri ambazo kwa sababu moja au nyingine zinapata shida kuyakamilisha maboma, kwa Serikali iwaunge mkono ili maboma haya yaishe, watoto waingie madarasani waweze kusoma.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo kwa haraka haraka kabisa, tunaipongeza Serikali sana kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali za Wilaya 67, ujenzi wa Vituo vya Afya 350 katika Wilaya mbalimbali na Kata mbalimbali. Hata hivyo, huko nako kuna tatizo kubwa la maboma. Naendelea kuiomba Serikali ijaribu kuzisaidia Halmashauri ambazo haziko vizuri kuhakikisha kwamba nao wanaweza kukamilisha maboma hayo na wananchi waweze kupata huduma inayostahili kama tulivyokuwa tumekusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kuzungumza suala zito na muhimu kabisa la majisafi na salama. Bado tatizo la majisafi na salama ni kubwa sana katika vijiji vyetu, pamoja na vijiji ambavyo kwa kweli…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Joel.

MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, naunga mkono hoja Kamati zote tatu. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. JOEL M. MWAKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika hoja ya Bajeti ya Wizara ya Kilimo. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya, niipongeze Wizara kwa maana ya Waziri, Naibu Waziri pamoja na timu nzima ya Wizara kwa bajeti yao nzuri waliyotuletea safari hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naomba kwa sababu ya muda, niende tu moja kwa moja kwenye jambo mahsusi ambalo ningependa kuongea leo. Kilimo kwa Kanda ya Kati, sehemu kubwa tutegemee kilimo cha kumwagilia. Suala la mvua hapa Dodoma ni tatizo kubwa sana, Dodoma ina register mvua nyingi sana lakini zinazokuja bila mpangilio unaoweza kuwezesha mazao kukua na kutoa mazao yanayotegemewa. Kwa hiyo njia peke yake ni kulala kwenye kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikizungumza suala la kilimo cha umwagiliaji, maana yake tunahitaji mabwawa. Tunayo mabwawa ya zamani ambayo yapo tayari lakini bado kuna mipango ya kuweka mabwawa mapya; hivi ndiyo vitu vya Serikali kuweza kuvishughulikia kwa ukaribu kabisa katika eneo letu hili la kati.

Mheshimiwa Spika, mabwawa ya zamani, nimebahatika mara mbili hivi kwenda na Mawaziri kwenye maeneo ya mabwawa kwenye Jimbo langu la Chilonwa. Nimekwenda kwenye Bwawa la Bwigiri, Bwawa la Ikoa na Waziri, wakati Maji na Umwagiliaji, Mheshimiwa Kamwele, lakini na juzi nimekwenda na Naibu Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Omary Mgumba. Hoja ya wananchi kwamba mabwawa yanafukulika ilichukuliwa na Serikali na kusema kwamba wanayafanyia kazi hatuoni mrejesho wowote juu ya mabwawa haya.

Mheshimiwa Spika, ninaiomba Serikali, iwasaidie wananchi wa eneo hili ili waondokane na tatizo hili wanalolizungumza Waheshimiwa Wabunge wengine waliopita, la kila wakati kulia njaa ilhali Dodoma ina ardhi nzuri inayokubali mazao yote, Dodoma unalima kila aina ya zao.

Mheshimiwa Spika, nimeshangaa, sasa hivi Jimboni kwangu wanavuna pamba, sikuamini wakati tunaambiwa tupande pamba lakini sasa hivi wanavuna pamba, maeneo ya Segala kule, nimekwenda nimeshangaa na macho yangu. Kwa hiyo kila zao linakubali ila shida ni maji. kwa hiyo, tunaomba sana masuala ya mabwawa haya, hebu yapate mrejesho unaoeleweka ili wananchi wawe na uhakika wa kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda, niende pia kwenye suala la mafunzo kwa wakulima hawa. Wakulima wanahitaji kupewa mafunzo ya nini cha kufanya kwenye maeneo yao mbalimbali. Si kila ardhi inakubali kila zao, basi wapewe elimu ya eneo hili hapa wajue afya ya udongo wa eneo walilopo inakubali mazao gani ili waweze kupanda hayo mazao. Vilevile, hata ikibidi watumie mbolea basi watumie mbolea gani katika udongo ule badala ya kutumia kila mbolea kwa kila zao kila sehemu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda basi nichukue nafasi hii kwa heshima na taadhima niunge mkono hoja kwa asilimia 100, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba kushukuru kupata nafasi hii ya kuweza kuchangia katika hotuba zilizotolewa na Mawaziri wa Wizara hizi mbili ambazo zipo chini ya Ofisi ya Rais. Pili, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya. Sisi wote tunaona na tunashuhudia yale yanayoendelea katika Awamu hii ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze sana Mawaziri wetu wawili, Mheshimiwa Jafo pamoja na Naibu wake lakini pia Mheshimiwa Mkuchika pamoja na Naibu wake katika Wizara zetu hizi mbili kwa taarifa zao walizoziwasilisha hapa jana ambazo zimezihidhirisha kabisa nia na kusudi zima la Serikali ya Awamu ya Tano katika kuhakikisha kwamba Tanzania hii inavuka kutoka hapa ilipo kuingia katika Tanzania ya uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025. Nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo nianze kwa kuunga mkono hoja za Wizara zote hizi mbili kwa asilimia mia. Kwanza kabisa, niseme kwamba kupanga ni kuchagua, Serikali yetu ya Awamu ya Tano ilipanga na ikachagua kwamba tunataka kufika mwaka 2025 nchi yetu iwe imeingia kwenye uchumi wa kati na njia tutakayoichukua ni hii ambayo tunaiona sasa, tunaziona bajeti zetu zilivyo makini kabisa kuhakikisha kwamba tunafika huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo mipango mikubwa, midogo na ya kati ambayo lazima yote iende kwa pamoja katika kuhakikisha kwamba tunaweza kuvuka na kufika kule tunapotaka. Tuna mipango mikubwa ambayo tunaiona, mipango ya Stiegler’s Gorge, SGR na kununua ndege ni mipango mikubwa. Mipango hii wakati mwingine watu wanashindwa kuoanisha, tunahitaji macho haya ya usoni, ya kwenye ubongo na ya rohoni tuweze kuona kwa ujumla wake tukajumlisha kwamba kweli mipango hii inawalenga Watanzania wote na hasa wa kipato cha chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango hii ndiyo inaweza kutuwezesha sisi kutekeleza mipango mingine midogomidogo iliyo muhimu kwa ajili ya wananchi wa kati. Ukizungumzia elimu, ili tuweze kuingia katika Tanzania ya uchumi wa kati, tunahitaji wananchi wetu wawe na elimu bora. Tunaiona mipango ya Serikali ya elimu bila malipo lakini tunaiona mipango ya Serikali hii, tumekuwa tukilia walimu lakini sasa ajira zimetoka kwa walimu elfu nne na mia saba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi ukatekeleza matakwa yako yote kwa wakati mmoja hata siku moja. Kila jambo ni mchakato, utaangalia kwenye elimu, afya na kadhalika, kwa hiyo, lazima twende kidogo kidogo. Walimu hawa wachache ambao Serikali imetoa ni mpango kamili na mwaka kesho na mwaka kesho kutwa lakini mwisho wa siku tutakuwa na uwanja mzuri wa kutoa elimu iliyo bora kwa vijana wetu. Mbagala Zachiem

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji ni muhimu pia, tunahitaji wananchi wetu wawe na afya bora. Afya bora siyo suala la kwenda zahanati au kwenye kituo cha afya tu bali unaishi vipi nyumbani, mazingira yako yakoje? Bila maji mazingira majumbani yanakuwa ni shida tupu na tunaweza kuhatarisha afya zetu kutoka nyumbani moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imejitahidi sana kuhakikisha kwamba wananchi wanapata maji na sisi Wabunge wenyewe kupitia Mifuko yetu ya Majimbo tumejitahidi sana. Mimi jimboni kwangu toka nimeingia 2015 hadi leo nimekwishachimba visima kumi na mbili, lakini juzi Serikali imenisaidia nimepewa visima nane. Kama watu hawayaoni haya hawataona kitu. Nachoiomba Serikali ni kuongeza kasi, visima hivi vikichimbwa basi viweze kuwekewa miundombinu ili watu waweze kuyafaidi maji hayo na yaweze kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia vituo vya afya 352 katika Halmashauri zetu, katika hivyo viwili vinatoka Halmashauri ya Chamwino; kimoja Jimbo la Chilonwa na kingine Jimbo la Mtera. Tunaishukuru sana Serikali kwa kazi kubwa wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hospitali za wilaya 67, katika hizo moja ipo Halmashauri ya Chamwino, tunaipongeza sana Serikali. Kama hiyo haitoshi, nakushukuru sana Mheshimiwa Jafo na namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutuletea Hospitali ya Uhuru katika Wilaya yetu ya Chamwino. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili mambo yote haya yaweze kwenda lazima kuwe na mawasiliano mazuri baina ya maeneo yetu mbalimbali. Barabara na madaraja yanaendelea kujengwa awamu kwa awamu, kama nilivyosema hatuwezi kufanya mambo yote kwa wakati mmoja. Jimboni kwangu tumetengeneza madaraja mengi, Daraja la Manyemba, daraja la kutoka Mlebe kuja Chinangali II na sasa tunashughulikia daraja la kutoka Makoja kuja Mwengamile, ni kazi kubwa inayofanywa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la TARURA na TANROADS, watu wanazungumzia kujaribu ku-balance, ni jambo jema lakini n kuangalia wapi kuna jukumu gani la kufanya na wapi kuna jukumu gani la kufanya. Mimi naiomba Serikali angalau basi kutoka asilimia 30 TARURA iende kwenye asilimia 40 hata tusipofika 50 ili nayo iweze kuboresha kazi zake nzuri ambazo inaendelea kuzifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, MKURABITA ni jambo jem,a tunataka wananchi hawa wajiletee maendeleo yao wenyewe, wanyanyuke kiuchimi. Mtu mmoja mmoja ili aweze kunyanyuka kiuchumi anahitaji kuwezeshwa na Serikali na Serikali imeleta MKURABITA ili watu waweze kurasimisha maeneo yao, wakapata hati miliki za kimila, hati hizi zikatambuliwa na mabenki ili waweze kukopa na kujiletea maendeleo. Ninachokiomba Serikali isimamie kwa dhati mabenki kuhakikisha kwamba wanazitambua hizo hati na wananchi wanapata mikopo kadri inavyostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, TASAF sasa tunaingia awamu ya tatu. Naiomba sana Serikali maeneo yale ambayo yalikuwa haijafika sasa ikafike maana ndiyo mpango kamili wa TASAF III. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalize kwa ombi mahsusi la maboma ya shule, nyumba za walimu, zahanati na maabara ambapo wananchi wetu wameweka nguvu zao nyingi sana, wamejitolea kujenga na wamefika mahali wamekwamba. Sawa Serikali imeweka nguvu lakini naiomba iongeze nguvu zaidi ili maboma haya yaweze kumalizika na wananchi waweze kuyafaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia kwa kuunga mkono hoja hii asilimia mia, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hoja hii ya bajeti ya Wizara ya maji, Wizara ambayo ni muhimu sana kwa maisha ya binadamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi kubwa anazoendelea kuzifanya ambazo zinatudhihirishia na zinatupa matumaini makubwa sana kwamba mpango wetu wa kuiingiza nchi katika uchumi wa kati mwaka 2025 tutaufikia bila wasiwasi wowote kwa kuchapa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji kwa kazi zao kubwa wanazozifanya pamoja na timu yao nzima Wizarani pale. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa namna alivyowasilisha taarifa yake hapa jana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kabisa kwa kuunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. Maji ni kila kitu, maji ni uhai kwa binadamu, kwa wanyama na kwa mimea, maji ni uhai kwa kila kitu chenye uhai hapa duniani. Maji safi na salama ni afya. Maji safi na salama ni afya kwa binadamu. Kwa mpango wetu tulinao wa kuivusha nchi yetu kuipeleka kwenye uchumi wa kati tunahitaji watu wenye afya njema. Bila maji safi na salama itakuwa ngumu kufika huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nichukue nafasi hii niipongeze mipango mizuri sana ya Wizara ambayo imesomwa na Mheshimiwa Waziri jana ambayo iko kwenye kitabu hiki imejieleza kwa uzuri sana. Tumeona kuna mipango inazungumzia ujenzi wa mabwawa ya mikakati. Mabwawa ya mikakati yametajwa hapa, moja kati ya mabwawa hayo liko bwawa la Farkwa lililoko Chemba hapa Dodoma. Bwawa hili linakusudiwa pamoja na mambo mengine liweze kuwa chanzo kikubwa cha matumizi ya maji hapa Jijini Dodoma na viunga vyake vyote, Wilaya ya Bahi, Chamwino na Wilaya ya Chemba yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia jinsi watu wanavyo-flow Dodoma sasa hivi, ukizingatia sasa ofisi zote za Wizara zote, Serikali nzima sasa iko Dodoma, sasa wako Mtumba, hata wale wachache waliokuwa wanazembea zembea, wanategea tegea kuja Dodoma sasa hawana namna inabidi waje. Mji huu utafurika watu sana muda sio mrefu. Maji yako wapi? Maji ya Mzakwe, sawa! Hadi wakati huu bado yanajitosheleza, lakini kwa flock ya watu itakayokuja muda sio mrefu tutaanza kulia tatizo la maji. Kwa hiyo niombe sana Wizara waangalie sana suala zima la kukamilisha miradi mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la ukarabati wa mabwawa ya zamani. Yako mabwawa ya zamani na yametajwa kwenye kitabu hiki ukurasa wa 56, kati ya mabwawa hayo, yako mabwawa ya Dodoma, liko bwawa la Ikowa ambalo liko Wilaya ya Chamwino na liko bwawa la Buigiri ambalo pia liko Wilaya ya Chamwino. Mabwawa haya awali kama ilivyo leo kwenye kitabu yalijengwa kwa maana ya kudhibiti mafuriko lakini tulivyoendelea hivi kuja kilimo chetu kimekuwa shida mabwawa haya yamekuwa yakitumika sasa kama ni chanzo kikubwa sana cha kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabwawa hayo sasa yameingia shida. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Wizara nzima kwa ujumla lakini Waziri aliyepita Engineer Kamwelwe alipata nafasi akatembelea mabwawa ya Buigiri na mabwawa ya Ikowa akayatolea kauli kwamba mabwawa haya yatashughulikiwa ili watu waendelee kufaidi na kunufaika na mabwawa yale kwa kufanya kilimo cha umwagiliaji. Hata hivyo, mpaka sasa kimya! Tatizo tunaweza kuwa tunalijua, ndiyo hapo tunaposema, tusione shida wakati mwingine, ni kweli kunaweza kuwa na ufisadi wa watu kuhujumu fedha za umma kwenye miradi ya maji, lakini sio kila sehemu na ukiangalia sehemu kubwa sana ni ukosefu wa fedha kufika kwenye maeneo husika. Fedha za maendeleo hazifiki jinsi zinavyopangwa, shurti zingefika hata hizo kidogo, basi tusingekuwa hapa tulipo leo. Suala hili tunaomba Wizara ihakikishe inakamilisha miradi yake mapema inavyowezekana ili watu waweze kufaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la utafiti na uchimbaji wa visima mbalimbali ni jambo zuri sana. Hii ni mikakati mizuri ambayo tunasema Wizara yetu imekuja nayo na tunaomba mikakati hii basi itekelezeke kweli kweli. Katika mikakati hii, katika utafiti na uchimbaji wa visima hivi bahati nzuri na wilayani kwangu, Wilaya ya Chamwino, tumepata visima 14. Katika visima 14, visima nane viko kwenye Jimbo langu la Chilonwa. Pamoja na visima hivi nane vilivyochimbwa juzi, leo hivi nazungumza nina visima 20 katika Jimbo la Chilonwa peke yake ambavyo vimechimbwa, sawa, maji yamepelekwa maabara yameonekana yako safi na salama kwa matumizi ya binadamu lakini maji bado yapo chini, hakuna pump, hakuna chochote, tunamaliza miaka miwili. Sasa watu wanafika mahali fulani, kama sisi wa CCM tunasema utekelezaji wa Ilani, Ilani ya CCM ndiyo inavyotuambia sasa wameNtuchimbia maji wanasema maji yako chini, yako wapi? Tunayataka maji tuyatumie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii niombe sana suala zima la kuiomba Wizara ihakikishe kwamba miradi yote iliyowekwa hapa itimie, ikamilike ili wananchi waweze kufaidi matunda ya kazi ambazo zinafanywa sasa. Nichukue nafasi hii mimi niunge mkono wale ambao wana hoja ya kusema maamuzi yetu tuliyoyafanya vikao vya nyuma kwamba tupate Sh.50 toka kwenye mafuta ili iweze kusaidia Mfuko wa Maji wa Taifa naliunga mkono kwa kweli, kwa sababu naamini hilo linaweza kusaidia upatikanaji wa fedha ili kuweza kutatua matatizo haya ya miradi isiyokamilika kwenye maeneo yetu mbalim bali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya haya machache, kwa nafasi hii tena niseme naiunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, lakini naomba sana ukamilishaji wa miradi hii ufanyike mapema. Ahsante.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika Mpango huu wa Maendeleo Mwaka 2020/ 2021. Awali ya yote nichukue nafasi hii kuipongeza sana Serikali yetu ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Rais wetu, mpendwa wetu Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya kulifanyia Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, yeye pamoja na Naibu wake, Katibu Mkuu na timu nzima ya pale Wizarani kwa kazi kubwa wanayoifanya, kazi kubwa waliyoifanya katika kutuandalia mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango huu ni muendelezo wa Mpango wa Miaka Mitano wa Maendeleo ulioanza mwaka 2016/2017 unakuja kuishia katika mpango huu tunaojadili leo 2020/2021. Mpango huu unatekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi, chama ambacho ndio chama tawala; ilani ya uchaguzi imeeleza inataka kuwafanyia nini Watanzania, kubwa inalotaka kuwafanyia Watanzania ni kuwavusha Watanzania kutoka kwenye hatua tuliyonayo sasa na kutupeleka kwenye nchi ya uchumi wa kati, inataka kutuvusha kupitia viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi hii imepangiliwa vizuri sana na Wizara husika, kwamba, ili tuweze kufika huko, ili viwanda vyetu viweze kusaidia kuivusha nchi hii kutoka hapa kwenda kwenye uchumi wa kati ni lazima mambo fulani fulani yawekwe sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango huu uko vizuri kabisa, umejipanga vizuri kabisa kwamba tunahitaji tuwe na umeme wa kutosha, tuwe na umeme wa bei rahisi ili tuweze kuzalisha bidhaa zenye bei ambazo zina ushindani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hali tuliyonayo sasa, tunazalisha mazao mengi; tunazalisha pamba na tunasafirisha pamba ghafi, lakini tunaweza tukasafirisha pamba ambayo imekuwa semi processed kwa kiasi fulani. Shida kubwa inakuwa wapi? Gharama ya uzalishaji inakuwa juu. Unakuta mtu anaona akinunua pamba ghafi akaenda kui-process mwenyewe, gharama ya ku-process kwake inakuwa ni ndogo. Kwa hiyo, anaona bora anunue pamba ghafi. Tukisema tui-process kidogo kuiongeza thamani, gharama inakwenda juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali imeliona hili ikasema hapana, lazima tuwe na mkakati wa kuzalisha umeme wa kutosha na wa bei rahisi. Ndiyo ikaja na mpango mzima wa Stiegler’s Gorge. Uzalishaji wa umeme wa megawat 2,115 ni umeme mwingi sana utakaosaidia kushusha gharama ya umeme na kuhakikisha viwanda vinapata umeme na kufanya kazi ya uzalishaji kuwa rahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili linaenda sambamba na mpango wa Serikali vilevile kuhakikisha kwamba wananchi wanapata umeme kote nchini. Mpango wa mwaka 2021 nchi nzima, vijiji vyote, vitongoji vyote wananchi wote wawe wamepata umeme ni mpango unaoenda sambamba na ujenzi wa Stieglers Gorge ili umeme uwepo wa kutosha tusije tukajikuta tumesambaza umeme kwa maana ya nguzo na waya kufika kila sehemu lakini tunafika mahali fulani, umeme wa kuwapa wananchi unakuwa haupo. Kwa hiyo, naupongeza sana mpango huu, ni mpango uliokaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala zima la usafirishaji, kusafirisha malighafi kutoka sehemu moja hadi nyingine, kusafirisha end products, yaani mazao tunayozalisha katika viwanda vyetu kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine pia ni kitu cha muhimu sana ambacho Serikali yetu imeliona na imelifanyia kazi nzuri sana. Tunaona barabara zetu nyingi sana zimewekwa lami sasa. Nchi yetu sasa hivi imeunganishwa kwa sehemu kubwa sana, jambo ambalo linafanya usafiri unakuwa rahisi, mtu anatoka hapa asubuhi anajikuta jioni yuko Mwanza. Ni jambo lilikuwa siyo rahisi sana, unafikiria kwenda siku mbili tatu ukiwa barabarani, lakini mtu anatoka hapa kwenda Songea, kwenda Njombe, kwenda Mbamba Bay huko kwa muda mfupi sana. Tunaipongeza sana Serikali kwa jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu, katika suala la usafirishaji wa bidhaa, usafirishaji wa mizigo mbalimbali tukaona kwamba reli ya kati ifanyiwe uboreshaji. Tukaja na wazo la SGR ambapo sasa tunaipongeza Serikali. Kipande cha kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro kimeshafika asilimia 63, ni jambo la kuipongeza sana. Kipande cha kutoka Morogoro hadi Makutupora hapa Dodoma, nacho kimefikia asilimia 16. Tunaipongeza sana Serikali kwa hilo. Mipango yote hii inaonyesha jinsi gani Serikali imejipanga kuhakikisha kwamba inakwenda na ratiba yake iliyojiwekea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la afya. Tukienda kwenye kitabu cha mwongozo wa Mpango ukurasa wa 17 kipengele cha 58, imeongelewa kwa uzuri kabisa na kwa kina, lakini mimi niseme kitu kimoja; afya ndiyo kila kitu. Tunahitaji wananchi wetu wafanye kazi ili waweze kuzalisha mashambani. Tunahitaji watu wetu wawe na afya bora ili waweze kufanya kazi viwandani. Kwa hiyo, suala la afya ni suala la muhimu sana, naipongeza Serikali. Hadi sasa tunazungumzia Vituo vya Afya zaidi ya 352. Hadi sasa tunazungumzia Hospitali za Wilaya 67 tumekwenda hatua kubwa sana. Naipongeza sana Serikali kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la maboma. Wananchi wetu wamejitoa, wamefanya kazi kubwa sana huko vijijini. Wamejenga majengo ambayo wameshindwa kuyamalizia. Wanaweza kutoa nguvu zao wakasaidia kujenga, lakini inafika mahali fulani wanashindwa kumalizia. Naiomba sana Serikali, hebu iangalie, hakuna Halmashauri ambayo haipendi kukamilisha haya maboma, lakini Halmashauri hazifanani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Dkt. Mpango, hebu aliangalie hili kwa kina, Halmashauri ambazo hali yake siyo nzuri sana kimapato, zipewe support ya kumalizia haya maboma. Tunawavunja nguvu sana wananchi katika kazi ya kujitolea na kujenga maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la elimu liko hivyo hivyo, nalo lina maboma ambayo ningependa kabisa nayo yafanyiwe kazi katika mpango huo niliosema hivi sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la maji haliko mbali na hivyo nilivyosema. Suala la maji kwa ujumla wake limetekelezwa kwa asilimia 82.6. Naipongeza sana Serikali. Pamoja na kwamba bado maeneo mengine, suala la maji safi na salama ni tatizo, lakini Serikali imefanya kazi kubwa sana, naipongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa kilimo, ukienda kwenye kitabu cha Mwongozo kile ukurasa wa sita jedwali 1.2 linaonyesha uuzaji wetu nchi za nje ulishuka kwa asilimia 4.2, lakini ununuzi wetu wa bidhaa kutoka nje ulipanda kwa asilimia 8.9. Hii maana yake ni kwamba tumeshindwa kusafirisha bidhaa kwenda nje. Nami mtazamo wangu ni kilimo. Kilimo kisiposimamiwa vizuri kikatuletea bidhaa za kutosha kusafirisha nje, basi hali hii itaendelea kujitokeza mwaka hadi mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu, kuna suala zima la mabwawa ya umwagiliaji sehemu mbalimbali, hebu Serikali ije na majibu yanayoeleweka. Kuna mabwawa ya zamani, tumeshazungumza sana humu Bungeni suala la ukarabati wa mabwawa ya zamani. Serikali imekuja na mipango mingi sana kwamba watayaangalia waone ni namna gani wa kuyaboresha haya masuala. Basi iwe na kauli ya kusema ili huko kwa wananchi tujue nini cha kufanya. Mabwawa hayatengenezwi, maji hayapatikani, umwagiliaji umeshuka chini na suala zima la uzalishaji wa kilimo unashuka chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwanza kabisa kwa kuunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. Pili nichukue nafasi hii kwa niaba ya wananchi wote wa mkoa wa Dodoma kumkaribisha Mheshimiwa Rais kwa mikono miwili hapa Dodoma. Juzi alikuja kujiandikisha pale Chamwino kwamba sasa yeye ni mkazi wa Chamwino rasmi. Katika…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Makanyaga kwa mchango wako mzuri na ushauri.

MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii awali ya yote nikushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuwa mmoja kati ya wachangiaji wanaochangia katika Taarifa za Kamati zetu tatu ambazo zimewasilisha Taarifa zao leo; Kamati ya TAMISEMI, Kamati ya Katiba na Sheria na Kamati ya Sheria Ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote niwapongeze sana waliowasilisha Taarifa hizi, wameziwasilisha kwa makini na zimeandaliwa kwa ubora, zimeeleweka na tunawaunga mkono na tunawapongeza kwa kazi kubwa wanazozifanya kwenye Kamati zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi ili iweze kuendelea inahitaji kuwa na amani, nchi ili iwe na amani inahitaji kuwe na Utawala Bora, ili kuwe na Utawala Bora tunahitaji sana kuwa na Sheria nzuri. Sheria nzuri zitagemea na wakati, kuna Sheria zilikuwa nzuri miaka ya nyuma lakini kadri tunavyokwenda mbele inabidi zibadilike ziende na wakati. Kuna Sheria ambazo sasa tunazo zinatusaidia ni nzuri sana lakini huko mbele tunakokwenda zitatakiwa zibadilike ili ziende na wakati na ndiyo maana tuna hizi Kamati kuzipitia Sheria zetu kwa wakati tofauti tofauti ili kuja na Sheria muafaka kwa wakati muafaka tulionao. Kamati zetu za Katiba na Sheria pamoja na Sheria Ndogo wanaifanya hiyo kazi kwa vizuri sana, nawapongeza sana. (Makofi)

Mhesheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala zima la Uraia pacha; uraia pacha kwa wakati tulionao, ninaiomba sana Serikali iuangalie kwa karibu. Naziomba Kamati zetu hizi husika hasa Kamati ya Katiba na Sheria iangalie kuingiza na kuifanya nchi yetu iwe na Uraia Pacha. Tunapozungumzia maendeleo, maendeleo lazima yawe shirikishi, tunaposema maendeleo shirikishi maana yake tunashirikiana sote wananchi tulio ndani ya Nchi na walio nje ya nchi. Kwahiyo, tunapoondoa hii Sheria inakua haipo kwetu, tunaacha kuwashirikisha kwa karibu kabisa Ndugu zetu ambao wanaishi nje ya Nchi. Kwa hiyo, naomba sana Kamati husika ziliangalie jambo la uraia pacha iwe ni Sheria inayokubalika hapa Tanzania pia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwashukuru sana Mheshimiwa Waziri Jafo na Manaibu wake wote wawili na Wizara nzima kwa ujumla, nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuchika, Makamu wake pamoja na Wizara nzima kwa ushirikiano mkubwa ambao wametuonyesha sisi Wajumbe wa Kamati ya TAMISEMI. Tumeshirikiana nao vizuri katika kuwashauri, katika kuwaeleza na tunashukuru kwa kweli wamekuwa wasikivu sana. Serikali hii ni sikivu kupitia kwa Mawaziri wetu hao katika kuyatekeleza yale ambayo Kamati inawashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la MKURABITA; amelizungumza mwenzangu hapa jirani lkwa kipfupi. MKURABITA wakati unaanzishwa kwa maana ya kurasimisha rasilimali na biashara za wanyonge ili ziweze kuwasiaidia katika maisha yao. Amezungumza kwa uzuri kabisa kwamba watu wengi na sisi tumepata nafasi kama Kamati, tumetembelea sehemu nyingi, tumeona watu wakikabidhiwa Hati za Kimila katika mpango mzima wa MKURABITA ili ziweze kuwasaidia wao kujinyanyua kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme bado kuna Mabenki yanasumbua kuzitambua Hati hizi za Kimila katika kuwasaidia wananchi kujiletea maendeleo. Niombe sana Mheshimiwa Mkuchika na Wizara yako hebu mliangalie hili kwa karibu sana. Mabenki ambayo bado yanasumbua yapewe maelekezo ili wananchi waweze kufaidika na mali zao walizonazo. Maeneo fulani tumejenga mpaka vituo vya biashara lakini vinaonekana havifanyikazi kwa sababu watu wa kwenda pale na kufanya hizo biashara hawapo kwa sababu hawana fedha kwahiyo naomba sana mliangalie hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili; ameongea Makamu wangu Mwenyekiti hapa madeni ya Madiwani. Halmashauri nyingi Madiwani wanazidai halmashauri hawajalipwa fedha. Hivi tunavyoelekea mwisho Madiwani hawajui nini cha kufanya lakini tumshukuru sana Mheshimiwa Jafo ulizungumza kwa umakini na kwa ukali sana wakati tupo kwenye kikao cha Kamati, umetoa maelekezo. Naomba maelekezo hayo uyakazie ili kwa kweli tufikapo mwezi wa sita tusingumzie tena madeni ya Madiwani kwenye halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nizungumzie kwa uchache kuhusu barabara; kweli barabara zipo, mvua zimenyesha na barabara zinaharibika tena kwa sabbau ya mvua. Niombe sana TARURA wajitahidi sana, waweze kuzirudisha barabara zetu katika hali ya kupitika ili mawasiliano yaendelee kuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa machache hayo, naomba niunge mkono hoja kwa asilimia 100 Kamati zote hizi tatu, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. JOEL M. MWAKA: Mheshimiwa Spika, naomba niongelee kilimo cha umwagiliaji pamoja na wakulima wenyewe. kilimo cha umwagiliaji kwa Mkoa wa Dodoma na Kanda ya Kati kwa ujumla kinategemea mabwawa. Mabwawa ya zamani sasa yanaelekea kutoweka kutokana na kujaa tope. Nimepata bahati mara mbili kuwapeleka Mawaziri kuyaona na kuzungumza na wananchi wanaolima. Kwanza nilikwenda na Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji wakati huo, Mheshimiwa Engineer Kamwelwe; pili, nilikwenda na Naibu Waziri wa Kilimo na Umwagiliaji sasa, Mheshimiwa Omary Mgumba. Ahadi zilizotolewa za kuyarekebisha Mabwawa ya Buigiri na Ikowa bado hazina mrejesho kwa wananchi, naomba mrejesho. Mabwawa mapya; ujenzi wa Mabwawa ya Membe na Kwahemu bado hakuna maendeleo mazuri, naomba mrejesho au taarifa.

Mheshimiwa Spika, mafunzo kwa wakulima; ili wananchi walime kwa tija kunahitajika elimu; elimu ya kilimo chenyewe, elimu juu ya afya ya udongo, ili waweze kulima mazao yanayostahili na ikibidi kutumia mbolea basi waweke mbolea inayostahili na elimu ya kilimo hai (organic agriculture). Naomba kuwe na vituo vya mafunzo ya kilimo kwa wakulima angalau kila kata au hata kila kijiji ambapo wanalima kilimo cha umwagiliaji kila baada ya miezi mitatu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. DKT. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika hoja hii ya bajeti kuu ya Serikali ya mwaka huu 2019/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kasi kubwa ambayo sote tunaishuhudia, tunaiona ya ukuaji wa uchumi wa taifa letu la Tanzania; nampongeza sana. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, yeye pamoja na Naibu wake; na nipongeze timu nzima ya wafanyakazi wa Wizara kwa kazi kubwa wanayoifanya pale. Tumeona safari hii wametujia na bajeti ya trilioni 33.11 ikiwa ni ongezeko la takriban asilimia 1.9 kutoka kwa bajeti ya mwaka jana ya trilioni 32.48; nawapongeza sana kwa kazi kubwa hiyo mliyofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo mimi nianze kabisa kwa kuunga mkono hoja hii ya Wizara ya Mipango ambayo imeletwa mbele yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuzijadili kwa kina Bajeti za Wizara mbalimbali na tukazipitisha, leo tunajadili Bajeti Kuu. Bajeti Kuu ambayo ndiyo muunganiko wa bajeti zote za Wizara zote ambazo tulizipitisha hapa siku za hapa karibuni.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulisomewa taarifa na Waziri wa Mipango kwamba wanajipanga vipi kukusanya hizi trilioni 33.11 zitakazokwenda kukidhi haja ya bajeti ya Wizara zote kwa mwaka huu 2019/2020. Mimi kwa upande wangu naunga mkono hatua zote na njia zote ambazo zimependekezwa. Tumeshuhudia kuna maeneo kodi zimetolewa, tumeshuhudia kuna maeneo tozo zimetolewa lakini kuna maeneo pia zimeongezwa kiutaalam na kukidhi haja, ya kwamba bajeti hii ikawe kweli ni bajeti ya mfanyakazi wa chini hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipongeze sana miradi mikubwa ya Serikali ambayo imewekwa kama kipaumbele. Mradi wa SGR, SGR ni ujenzi wa reli ya kisasa, mwendo wa kasi, yenye uwezo wa kufanya kazi kubwa ya kubeba mizigo ambayo itapungua matumizi ya barabara zetu ambazo zimekuwa zikiharibika kwa kubeba mizigo mikubwa sana. Napongeza sana kwa sababu usafiri ni kitu muhimu sana katika kuleta maendeleo ya nchi yoyote ile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napongeza sana mradi wa Stiegler’s Gorge, kwa maana ya kupata umeme. Tunapozungumzia kutaka kuivusha nchi yetu kutoka katika uchumi wa chini hadi uchumi wa kati hakuna namna na namna ambayo sisi tumeichagua ni kupitia viwanda. Viwanda bila umeme tutakuwa tunatwanga maji kwenye kinu. Tunahitaji umeme mwingi na nafuu ili viwanda vyetu viweze kuzalisha bidhaa ambazo zina bei inayoweza kuchukulika na mfanyakazi wa kiwango cha chini hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba tunazihitaji fedha kwa ujumla wake ili tuweze kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo hapa nchini. Tunahitaji fedha ili tuweze kutekeleza miradi ya REA. Wamezungumza wengi humu ndani kwamba REA imeonesha dhahiri kwamba ni eneo ambalo limemnufaisha Mtanzania wa kawaida. Umeme umefika vijijini maeneo mengi ya nchi yetu hadi kufikia sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika kwamba ya REA si nzuri, inasuasua kwa kiasi kikubwa sana. Tunahitaji tupate pesa ili Serikali ielekeze pesa hizi kwenye maeneo ambayo bado REA haijafika ikafike ili angalau kulingana na mpango wetu kufika 2021 vijiji vyote na vitongoji vyote nchi hii viwe vimeshapata umeme. Naogopa kwa kasi hii tuliyonayo sasa huenda hilo lisitimie, lakini naomba sana; nawaamini sana, Dkt. Mpango kwa mipango yako mikubwa unayoiweka hapa basi suala la REA liangalie kwa macho ya karibu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili nizungumzie barabara. Barabara kwa maana ya TARURA kwa maana ya TANROADS, mgao wa fedha kati ya TANROADS na TARURA wengi wameunzungumza hapa; na mimi niwe mmoja wapo wa kuzungumza. Nakuomba tuangalie namna ya kuweza kuwaongezea angalau kidogo TARURA kutoka asilimia 30 wanazozipata sasa angalau wapate asilimia 40 ili nao waweze kufanya kazi inayotegemewa kwa ajili ya kuwaletea maendeleo wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, TARURA wanabeba eneo kubwa sana la barabara hapa Tanzania, tena barabara ambazo ni za udongo, barabara ambazo kila mvua ikinyesha zinaharibika, barabara ambazo kila mwaka lazima zifanyiwe matengenezo; tofauti hata na TANROADS, TANROADS wanashughulikia barabara kubwa ambazo kwa kiasi kikubwa zimeshatengenezwa kwa umakini mkubwa, zina lami haziharibiki mara kwa mara.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Wizara iliangalie hilo kwa manufaa ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji fedha ili tuweze kutekeleza miradi ya kilimo. Wengi wamezungumza hapa ndani kwamba ili tuweze kuivusha nchi na jinsi tulivyojipangia sisi wenyewe, kwamba tunataka kuivusha nchi toka uchumi wa chini hadi uchumi wa kati kupitia viwanda vinavyotegemea kilimo. Tutegemee kilimo, tukizungumzia kilimo cha kutegemea mvua hapa tutakuwa tunajidanganya. Tunahitaji kuzungumzia kilimo cha umwagiliaji, chenye uhakika hivyo tunahitaji mabwawa ya uhakika.

Mheshimiwa Naibu Spika, wamezungumza baadhi ya watu waliopita kwamba maeneo mengi ya Tanzania hasa haya ya kati mvua si za uhakika sana, lakini ardhi yetu ni bora, nzuri na ina rutiba ya kutosha, shida ni maji; lakini maeneo haya haya tunayoyazungumza maji yapo karibu; tunaweza kutengeneza mabwawa na kuchimba visima. Kwa hiyo niombe sana fedha zipatikane ili suala zima la kilimo cha umwagiliaji lipewe umuhimu wake kama tunavyolizungumza hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji; tunahitaji fedha tupeleke kwenye miradi ya maji; maji safi na salama. Watanzania tunahitaji tumtue ndoo mwanamke, mambo ya kutembea kilometa na kilometa; na kwenye vijiji vyetu kuna maeneo; mimi kuna kijiji cha Nzali wananchi wa Kitongoji cha Mapinduzi akina mama kazi yao ni kuondoka alfajiri kurudi saa 9 hadi saa 10; hii sio. Pamoja na kwamba kuna mambo mengine yanachengesha; tumekwenda mara mbili tunawachimbia visima pale hatupati maji; sasa wenyewe wanasema kwamba kuna wazee hawataki maji yapatikane. Sasa hilo nalo ni jambo lingine lakini kwa hakika tunahitaji kumtua ndoo mwanamke. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo nizungumzie kuhusu miradi ya elimu. Tunahitaji watoto wetu waende shule ili taifa letu liweze kwenda huko kwenye uchumi wa kati, tunahitaj liende kwenye uchumi wa kati likiwa na wananchi wenye kuelimika. Watoto wetu waende shule, madarasa yapatikane, maabara zipatikane na nyumba za walimu zipatikane; zote hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji miradi ya afya pia iweze kutekelezeka. Tupate zahanati kila kijiji, vituo vya afya kila kata na hospitali za wilaya ili wananchi tuweze kuwa na afya njema ili tuweze kuifanya kazi ya kuweza kuvusha nchi kutoka hapa tulipo kwenda uchumi wa kati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo machache, naunga mkono tena hoja kwa asilimia 100. Ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Kulitangaza Jiji la Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi wa Mwaka 2018
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi leo niweze kuwa mmoja kati ya wachangiaji watakaoingia kwenye historia ya Wabunge waliochangia Muswada huu wa kuitangaza Dodoma kuwa Makao Makuu ya nchi.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote, nimpongeza sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, kwa uamuzi wake wa dhati wa kuamua kuyatekeleza kwa vitendo maamuzi yaliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Kwanza chini ya uongozi wa Rais, Baba wa Taifa, Marehemu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere mwaka 1973. Leo tukiwa tunayazungumzia ni miaka 45 tangu hayo yametendeka na sasa tunaona yanakwenda kutekelezeka kwa ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, si kwamba siku za nyuma hayakuwa yanatekelezeka. Tunachokifanya hapa sasa ni kuweka sheria itakayofanya jambo la kuchezea Dodoma kuwa Makao Makuu lisiwepo tena. Maana tumeona siku za nyuma wakijaribu kwenye awamu mbalimbali zilizopita, kila Rais aliyekuja; Awamu ya Pili, ya Tatu, ya Nne, hakuna ambaye alilipinga jambo hili, lakini kila kulipokuwa kunatokea move ya kuja Dodoma ulikuwa unaona inakwenda kwa muda mfupi na baadaye watu wanarudi Dar es Salaam. Kwa umakini kabisa Rais huyu ameona kwamba tatizo lililopo hakuna sheria na sisi tunampongeza sana kwa hili. Sasa tunatunga sheria ifanye iwe vigumu kabisa kwa mtu yeyote kuja kujaribu kusema Makao Makuu ya nchi yahamie sehemu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya yanayozungumzwa na Waheshimiwa Wabunge humu ndani ni kweli, kwamba ni gharama kuhamishia Makao Makuu sehemu nyingine. Sasa kama alivyosema msemaji aliyepita Makao Makuu ya nchi yako Dodoma, tukubali tusikubali yako Dodoma hapa leo; Waziri Mkuu yuko Dodoma, Mawaziri wote wako Dodoma, ofisi zote kubwa za Serikali ziko Dodoma, aliyebakia ni Rais peke yake. Kwa hiyo, tukiliacha hili akaja mwingine kusipokuwa na sheria akasema tunahamishia Makao Makuu Mwanza, itakwenda, akipata consensus ya Wabunge wengi humu ndani, two-third ya Wabunge lakini gharama hii itaendelea kumuumiza Mtanzania. Sasa sisi tunaona ni vyema kwamba gharama hii iishie hapa kuja Dodoma, ndiyo maana tunampongeza sana Rais kwa kuhamia Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme tu haya aliyozungumza mwenzangu, Dodoma ni katikati ya nchi, Dodoma ndipo zinakutana njia nne zote kutoka Kusini hadi Kaskazini kwa maana ya kutoka Johannesburg hadi Cairo Misri. Ukitoka Mashariki unatoboza baharini huko hadi Magharibi, hapa ni katikati. Ni kweli ufikaji wa hapa Dodoma kutoka Mwanza ni rahisi, ufikaji wa hapa Dodoma ukitoka Kaskazini huko Kilimanjaro ni rahisi, ufikaji wa Dodoma toka kona zote ni rahisi kwa sababu ya ukatikati wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kusema teknolojia imekuwa lakini bado viko vitu vinahitaji presence ya watu, si kila kitu makaratasi. Rais akitaka kukutana na viongozi mbalimbali wa nchi hii hawatatuma vikaratasi, watasafiri physical waje hapa, gharama hizi ambazo tunaziona ndogo ndogo ndani ya muda mrefu ni gharama kubwa. Ndiyo gharama ambazo zinaweza kusaidia katika kuleta maendeleo ya nchi hii kwenye sekta nyingine hizo kama afya, elimu na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa heshima kubwa na taadhima, mimi nitamke kuunga mkono asilimia 100 Muswada huu wa Sheria Kuifanya Dodoma itamkwe kuwa Makao Makuu ya Nchi. Naomba kuwasilisha.