Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Eng. Joel Makanyaga Mwaka (15 total)

MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-
Barabara ya kutoka Makao Makuu ya Wilaya ya Chamwino kuelekea Kaskazini ni vumbi na ina madaraja mawili makorofi yaliyoko kati ya Chilonwa na Uzali na lingine kati ya Dabalo A na Dabalo B. Daraja lililopo kati ya Chilonwa na Nzali limewahi kuua watu mwaka 2014 na mifugo mingi pia imekufa kwenye daraja hilo:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuyajenga madaraja hayo mawili ambayo ni muhimu sana kwa uchumi wa Wilaya ya Chilonwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, madaraja aliyotaja Mheshimiwa Mbunge yote yapo katika barabara ya Chamwino Ikulu Junction, kuelekea Chamwino Ikulu - Dabalo hadi Itiso yenye urefu wa kilometa 80.43 ambayo ni barabara ya mkoa inayohudumiwa na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS), Mkoa wa Dodoma.
Mheshimiwa Spika, kati ya Chilonwa na Nzali kuna daraja la mfuto (vented drift) lililojengwa mwaka wa fedha 2013/2014 ambalo linatumika ingawa linakabiliwa na changamoto ya kuziba yaani siltation. Aidha, kati ya Dabalo A na Dabalo B pia kuna daraja la mfuto ni solid drift lililojengwa mwaka wa fedha 2014/2015 ili sehemu hiyo iweze kupitika.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) itaendelea kuyafanyia matengenezo madaraja hayo mawili yaliyopo ili yaweze kupitisha maji na barabara hiyo iweze kupitika majira yote ya mwaka. Aidha, Wakala wa Barabara utaendelea kuifanyia matengenezo ya aina mbalimbali barabara hii ili kuhakikisha inatumika kwa usalama wa watumiaji na kuwaletea maendeleo ya kiuchumi na kijamii wananchi wa Chilonwa.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-
Barabara inayounganisha vijiji vya Msanga na Kawawa ni muhimu sana kiuchumi kwa kata ya Msanga na Wilaya ya Chamwino na pia kuna mazao mengi ya uhakika kutoka Kawawa na vitongoji vyake, lakini barabara hiyo ni korofi sana kwa sababu ya mbuga iliyoko kati ya vijiji hivyo viwili na zaidi, daraja kubwa lililopo limevunjika kabisa kiasi kwamba halipitiki kabisa wakati wa mvua na wakati wa kiangazi hupitika kwa taabu sana.
Je, Serikali ina mpango gani wa kurekebisha barabara hiyo na kulijenga daraja husika ili kuboresha mawasiliano ya vijiji hivi viwili na masuala ya usafirishaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Jimbo la Chilonwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na umuhimu wa barabara hii, Serikali katika mwaka wa fedha 2015/2016 imetenga shilingi milioni 46.3 kwa ajili ya kujenga kivuko (box culvert), kuichonga barabara kwa urefu wa kilometa tano na kuiwekea changarawe sehemu korofi yenye urefu wa kilometa nne. Aidha, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017, barabara hii imeombewa shilingi milioni 130 kwa ajili ya ukarabati ili kuifanya ipitike wakati wote.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-
Serikali ilikuja na mpango mzuri wa umeme Vijijini na kupitia mradi wa REA kukawa na REA I, REA II na sasa REA III na Serikali iliahidi kwamba miradi yote ya REA II ambayo haijakamilika hadi kuanzishwa kwa REA III itatekelezwa sambamba na REA III:-
(a) Je, ni lini Serikali itatekeleza miradi yote ya REA II Jimbo la Chilonwa katika Vijiji vinne vya Kata ya Msamalo(Myunga, Msamelo, Mnase na Mlebe) Vijiji viwili vya Kata ya Zajilwa (Zajilwa na Mayungu) na Kijiji cha Kata ya Manchali?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuviingiza vijiji ambavyo havikuwepo kwenye mpango wa REA II katika mpango wa REA III?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi za kupeleka umeme katika Vijiji vya Kata za Manchali, Msamalo na Zajilwa kupitia mradi wa REA Awamu ya II zitakamilika mwezi Novemba mwaka huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Vijiji vyote vya Jimbo la Chilonwa ambavyo havikupata umeme kupitia REA awamu ya II vitapatiwa sasa umeme kupitia REA Awamu ya III. Kazi ya kupeleka umeme kwenye vijiji hivyo itahusisha ujenzi wa umeme msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 68, ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 301, pia ufungaji wa transformer 45. Mradi huu pia utapeleka umeme kwa wateja wa awali 11,276. Kazi zitaanza mwezi Desemba mwaka huu na kukamilika mwaka wa fedha 2019. Gharama ya mradi huu ni shilingi bilioni 12.09
MHE. JOEL M. MAKANYAGA Aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia maji wananchi wa vijiji vya Jimbo la Chilonwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA Alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mpango wa Maendeleo ya Sekta ya Maji nchini, kuanzia mwaka 2012/2013 hadi mwaka 2014/2015 imetekeleza miradi ya maji kwa vijiji vya Itiso na Membe kwa jumla ya shilingi milioni 758.7 vikiwa na jumla ya vituo vya kuchotea maji 23 ambavyo vinahudumia wakazi wapatao 7,475.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka wa fedha 2016/2017 Halmashauri inakamilisha mradi wa maji katika kijiji cha Wilunze ambao utahudumia jumla ya watu 2,867 kwa maeneo ya Makaravati, Mbelezungu, Majengo na Chalinze Nyama kwa jumla ya shilingi milioni 347.9 katika Jimbo la Chilonwa.
Aidha, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Halmashauri imepanga kutumia shilingi bilioni 1.053 kwa ajili ya kujenga miradi ya maji ikiwa ni pamoja na vijiji vya Magungu na Segala katika Jimbo la Chilonwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kuboresha huduma ya maji katika Jimbo la Chilonwa na maeneo mengine nchini kwa kadri rasilimali fedha itakavyopatikana.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-
Wananchi wa Chilonwa wanaishukuru Serikali kwa kuendelea kukarabati daraja lililoko kati ya kijiji cha Mahampha na Nzali kwa kiwango cha mkeka, korongo hili hupitisha maji mengi sana wakati wa masika toka Bwawa la Hombolo kiasi cha kukosa mawasiliano kabisa kati ya Kaskazini na Kusini mwa Jimbo la Wilaya ya Chamwino kwa ujumla wake.
Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kulijenga daraja hili kwa kiwango cha daraja la kupitika juu na sio ya mkeka ili kuondoa kero hii ya kukatika kwa mawasiliano kabisa wakati wa masika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikilifanyia ukarabati daraja la Mfuto yaani drift liitwalo Chilonwa lililopo kati ya kijiji cha Mahampha na Nzali ili kuhakikisha kuwa daraja hilo pamoja na barabara ya Chamwino Ikulu - Dabalo junction hadi Itiso yenye urefu wa kilometa 75 inapitika majira yote ya mwaka. Kwa kawaida daraja la mfuto (drift) hujengwa katika eneo lenye kina kifupi ambalo maji hukatisha barabara yaani shallow water crossing. Hali hii ndio iliyosababisha daraja la mfuto kujengwa kati ya kijiji cha Mahampha na Nzali. Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) inaendelea kufanya uangalizi wa karibu wa eneo hili ikiwa ni pamoja na kuangalia mapungufu yaliyopo na kupendekeza aina ya daraja ambalo litakuwa suluhisho la kudumu katika eneo hilo.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-
Barabara inayounganisha Vijiji vya Msanga na Kawawa ni muhimu sana kiuchumi kwa Kata ya Msanga na Wilaya ya Chamwino na pia mazao mengi ya uhakika kutoka Kawawa na Vitongoji vyake lakini barabara hiyo ni korofi sana kwa sababu ya mbuga iliyopo kati ya vijiji hivyo viwili na daraja kubwa lililopo limevunjika kabisa kiasi kwamba halipitiki kabisa wakati wa mvua na wakati wa kiangazi hupitika kwa taabu sana.
Je, Serikali ina mpango gani wa kurekebisha barabara hiyo na kulijenga daraja husika ili kuboresha mawasiliano ya vijiji hivyo viwili na masuala ya usafirishaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa barabara hii, Serikali katika mwaka wa fedha 2015/2016 ilitoa shilingi milioni 40 ambazo zimejenga kivuko (box culver) na kufungua mifereji ya kuitisha maji ya mvua (river draining). Aidha, mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali imetumia shilingi milioni 100 kuifungua barabara hiyo urefu wa kilomita 8, kujenga madaraja mbonyeo (solid drifts) matano likiwemo la mita 50 katika mto unaopitisha maji kutoka Hombolo na kuweka changarawe sehemu korofi kwa urefu wa kilomita 1. Serikali itaendelea kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino ili kuhakikisha daraja hilo linatengewa fedha na kujengwa katika mwaka wa fedha 2018/2019 kupitia TARURA.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-
Serikali imefanya kazi kubwa kujenga mtandao wa barabara za kiwango cha lami nchini, kipindi cha nyuma
barabara kuu zilikuwa zinawekwa matuta ili kudhibiti ajali, lakini hivi karibuni Serikali imefuta utaratibu wa kuweka matuta kwenye barabara hizo na hivyo kuwa chanzo kikubwa cha ajali zinazosababisha majeruhi, ulemavu na vifo. Kwa mfano, eneo la Buigiri, Wilaya Chamwino lina ajali nyingi kutokana na barabara kukosa matuta.
(a) Je, Serikali haioni kuwa kuna umuhimu wa kurejesha utaratibu wa kuweka matuta kwenye barabara?
(b) Kama utaratibu wa matuta hauwezekani, je, Serikali haioni kuwa kuna haja ya kuyaondoa matuta yote kwenye barabara kuu ili kuondoa malalamiko ya wananchi kwa viongozi wao kwenye maeneo ambayo hayana matuta?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Mwakanyaga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijatoa majibu ya swali namba 61 la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga Mbunge wa Chilonwa, lenye sehemu (a) na (b) napenda kutoa maelezo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kuboresha usalama barabara na kurekebisha sehemu hatarishi kwenye barabara kuu na barabara za mikoa nchi nzima ikiwemo barabara ya Morogoro - Dodoma eneo la Buigiri ili kupunguza ajali za barabarani. Hatua zilizochukuliwa na Serikali kupunguza ajali za barabarani ni pamoja na kuweka au kurudisha alama zote muhimu za barabarani ikiwemo za kudhibiti mwendo, kuweka michoro ya barabarani na kurekebisha kingo za madaraja zilizoharibika, uwekaji wa matuta na kadhalika kama ilivyokuwa ikifanya kipindi kilichopita.
Katika mwaka wa fedha 2017/2018 TANROADS itaendelea kuweka vivuko vya watembea kwa miguu (zebra crossing) na alama zote muhimu nchini pale tutakapohitaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kutoa maelezo ya awali napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga Mbunge wa Chilonwa, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli ajali za barabarani zina sababisha majeruhi, ulemavu na vifo kwa watu wetu ikiwa ni pamoja na kusababisha hasara kubwa kiuchumi kwa Taifa letu. Moja ya njia ambayo Serikali imekuwa ikitumia kupunguza ajali kwenye baadhi ya sehemu ni kuweka matuta ya barabarani. Hata hivyo, napenda kulieleza Bunge lako Tukufu kuwa, kiutaalam hairuhusiwi kuweka matuta kwenye barabara kuu. Aidha, matuta yaliyowekwa katika barabara kuu yaliwekwa kwa lengo la kupunguza ajali za barabarani kama njia ya mpito. Wizara inafanya utafiti kupata njia mbadala ya kupunguza ajali kabla ya uondoshaji wa matuta hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa mpito, Serikali inaendelea kurekebisha matuta ambayo yalijengwa bila kuzingatia viwango vilivyomo kwenye Mwongozo wa Wizara wa Usanifu wa Barabara (Road Geomentric Manual ya 2011) kulingana na upatikanaji wa fedha.
Aidha, inapobainika kuwa kuna haja ya kuweka matuta kwenye barabara, matuta hayo yatawekwa kulingana na viwango vilivyoainishwa kwenye mwongozo huu.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuzifungua Zahanati za Solowu na Makoja ambazo zimekamilika ili kuwapunguzia adha ya kufuata huduma ya afya vijiji vya mbali akina mama, watoto, wazee na wananchi wa vijiji hivyo kwa ujumla?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Zahanati za Solowu na Makoja zimejengwa na Halmashauri kwa kushirikisha nguvu za wananchi. Ujenzi wa Zahanati ya Solowu imegharimu shilingi milioni 79.605 ambapo wananchi wamechangia shilingi milioni 10.6 na Halmashauri imechangia shilingi milioni 69; na ujenzi wa Zahanati ya Makoja imegharimu shilingi milioni ambapo wananchi wamechangia shilingi 640,000.00 na Halmashauri imechangia milioni 136.8.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari Zahanati za Solowu na Makoja zimetengewa fedha MSD kiasi cha shilingi 640,800.00 kila moja kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa katika robo ya tatu ya mwaka huu wa fedha, na tayari Halmashauri imepeleka order kwa ajili kupatiwa dawa kwa matumizi ya zahanati hizo. Dawa na vifaa hivi vitachukuliwa kutoka Bohari ya Dawa ya Serikali Dodoma mara taratibu zitakapokuwa zimekamilika. Aidha, baadhi ya vifaa na vifaa tiba mbalimbali kwa ajili ya zahanati hizi vilishanunuliwa na vimehifadhiwa katika Kituo cha Afya cha Chamwino na vitapelekwa kwenye zahanati hizo kabla ya mwisho wa mwezi huu Aprili, 2018. Vifaa na vifaatiba hivyo ni pamoja na vitanda vya kuzalishia, vifaa vya kutakasia, magodoro, seti za kuzalishia, vitanda vya hospitali, mizani ya kupimia uzito kwa watoto na watu wazima, vifaa tiba, vitanda vya kupimia wagonjwa, mashine za kupimia shinikizo la damu, samani kwa maana ya meza, viti na makabati pamoja na ma-shelves ya kuhifadhia dawa. Wakati huo hu halmashauri imepanga watumishi wawili wa kada ya uuguzi kwa kila zahanati ambao wataanza kutoa huduma ndani ya mwezi ujao wa mwezi Mei, 2018.
MHE. ENG. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwaunga mkono wananchi wa Kata ya Haneti kwa kumalizia ujenzi wa chumba cha upasuaji ambacho kilianzishwa kwa nguvu za wananchi na Mfuko wa Jimbo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatoa pongezi kwa wananchi wa Kata ya Haneti pamoja na Mbunge wao Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga kwa juhudi kubwa za kuibua na kuanza ujenzi wa chumba cha upasuaji kwa ajili ya kuokoa maisha ya wananchi hususani akina mama na watoto. Ujenzi huo umefikia hatua ya kufunika jamvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia maelekezo ya Serikali kuboresha miradi kupitia fedha za miradi ya maendeleo na kuchagua miradi michache itakayotoa matokeo ya haraka, Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino katika mwaka wa fedha 2017/2018 ilitengewa shilingi milioni 350 kwa ajili ya ujenzi wa chumba cha upasuaji katika Kituo cha Afya cha Haneti na shilingi 350 kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Mlowa Barabarani. Ujenzi huo utakamilishwa baada ya fedha hizo kupokelewa kutoka Hazina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa majengo haya ya upasuaji yatakapokamilika kwa kiasi kikubwa yatawezesha kuboreshwa kwa huduma za akinamama wajawazito pamoja na kupunguza kwa kiasi kikubwa vifo vitokanavyo na uzazi.
MHE. ENG. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-
Barabara inayounganisha Kata ya Haneti na Kata ya Segala kupitia Kata ya Zajilwa ni muhimu sana kwa kufungua mawasiliano katika kata hizo tatu:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa barabara hiyo, inatengenezwa kwa kiwango cha kupitika muda wote kwa mwaka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha, 2017/2018 Serikali ilitenga na ilitoa fedha zote shilingi milioni 132.1 ambazo zimetumika kufanya matengenezo, si tu kwenye barabara aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge bali barabara ndefu zaidi ya kutoka Segala – Zajilwa – Haneti – hadi Umoja yenye urefu wa kilometa 80. Barabara hiyo, imekamilika na sasa inapitika muda wote wa mwaka.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati Bwawa la Ikowa linalohudumia Skimu ya Umwagiliaji ya Chalinze iliyopo Kata ya Manchali na Bwawa la Buigiri iliyopo Kata ya Buigiri?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA): Mheshimiwa Spika, nashukuru, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Bwawa la Ikowa lililopo Wilayani Chamwino, Kata ya Manchali lilijengwa mwaka 1959 kwa ajili ya kupata maji ya mifugo na kumwagilia, jumla ya hekta 300 katika Skimu ya Chalinze. Kutokana na mabadiliko ya tabia nchi na shughuli za kibinadamu katika maeneo hayo, bwawa lilijaa mchanga, magogo ya miti pamoja na tope kutoka katika korongo la Mjenjeule na hivyo kusababisha kupungua kwa kina cha maji katika bwawa hilo.

Mheshimiwa Spika, kufuatia hali hiyo Serikali ilifanya ukarabati mkubwa wa bwawa hilo mwaka 2009 kwa kunyanyua kingo na tuta za bwawa na hivyo kuliwezesha kumwagilia eneo la hekta 50 tu kati ya hekta 300 zilizokuwa zinatumika katika kipindi hicho. Aidha, tathmini iliyofanyika mwaka 2012 ilibaini kuwa zinahitajika shilingi bilioni 1.2 kwa ajili ya ukarabati wa bwawa na kunyanyua tuta ili kuongeza kina cha hilo bwawa ili kuwezesha kumwagiliwa hekta 300 katika Skimu ya Chalinze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bwawa la Buigiri ambalo liko katika Kata ya Buigiri lilijengwa 1960 ikiwa na uwezo wa kumwagiliwa hekta 40 na kunyeshea mifugo. Kufuatiwa bwawa kuvuna maji ya mvua ya mafuriko, lilijaa mchanga na kupungua kina cha maji. Pamoja na Serikali kurikarabati bwawa hilo, katika kipindi cha mwaka 2005 na mwaka 2009 bado bwawa hilo liliendelea kujaa mchanga na tope kutokana na shughuli za kibinadamu zinazosababisha uharibifu wa mazingira katika vyanzo vya maji. Aidha, tathmini iliyofanyika mwaka 2012 ilionesha kuwa bwawa hilo linahitaji ukarabati wa sehemu ya kutoroshea maji (slipway) na kunyanyua tuta ili kuongeza kina kwa gharama ya shilingi milioni 475.

Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa bwawa hilo kwa wananchi wa Wilaya ya Chamwino, Wizara ya Kilimo kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, itatenga fedha katika bajeti ya mwaka 2019/2020 kwa ajili ya kuyafanyia tathmini ya kina na usanifu kuandaa nyaraka za zabuni kwa ajili ya kutangaza na ukarabati. Aidha, Serikali inashauri wananchi wanaoishi kwenye maeneo ya vyanzo vya maji na kufanya shughuli za kibinadamu kushiriki katika kuboresha mazingira yao ili changamoto za kujaa mchanga na tope, iweze kupata ufumbuzi wa kudumu.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha ujenzi wa Zahanati ya Kijiji cha Chilonwa iliyoanzishwa kwa nguvu za wananchi ambayo kwa sasa imefikia kwenye linta?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Chilonwa ni miongoni mwa Kata 36 za Wilaya ya Chamwino, ina vijiji viwili vya Nzali na Mahama, Kata ina huduma za Zahanati moja iliyopo katika Kijiji cha Nzali. Wananchi wa kijiji cha Mahama walianzisha ujenzi wa Zahanati ya Kijiji ambayo kwa sasa jengo limefikia hatua ya lInta. Katika kuunga mkono juhudi za wananchi, Halmashauri ya Chamwino katika mwaka wa fedha 2019/2020 kupitia mapato yake ya ndani imetenga shilingi milioni 30 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa zahanati hiyo katika Kijiji cha Mahama. Ahsante.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-

Je, Serikali inatoa kauli gani juu ya mabwawa ya zamani yanayotumika katika kilimo cha umwagiliaji ambayo yamepungua kina na kushindwa kuwasaidia wananchi hususan Mabwawa ya Kijiji cha Buigiri, Kijiji cha Chalinze na Kijiji cha Izava?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Jimbo la Chilonwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Bwawa la Buigiri ambalo lipo katika Kata ya Buigiri lilijengwa mwaka 1960 likiwa na uwezo wa kumwagilia hekta 40 na kunyweshea mifugo. Bwawa hilo limekuwa likijaa mchanga na tope kutokana na mafuriko na hivyo kupungua kwa kina cha maji. Pamoja na Serikali kukarabati bwawa hilo katika kipindi cha mwaka 2005 na mwaka 2009 kwa kuongeza kina kwa mita moja bado bwawa hilo liliendelea kujaa mchanga na tope kutokana na shughuli za kibinadamu zinazofanyika juu ya bwawa na kusababisha mchanga na tope kujaa bwawani. Tathmini iliyofanyika mwaka 2012 ilionesha kuwa bwawa hilo linahitaji ukarabati wa sehemu ya kutoroshea maji na kunyanyua tuta ili kuongeza kina kwa gharama ya Shilingi milioni 475.

Mheshimiwa Spika, bwawa la pili Bwawa la Ikowa lililopo katika Kijiji cha Chalinze na Ikowa lilijengwa mwaka 1959 kwa ajili ya kupata maji ya mifugo na kumwagilia jumla ya hekta 96 kati ya hekta 220 katika Skimu ya Chalinze. Kutokana na mabadiliko ya tabianchi na shughuli za kibinadamu katika maeneo hayo, bwawa hilo limekuwa likijaa mchanga na tope kila msimu wa mvua na hivyo kusababisha athari katika tuta na kupungua kwa kina cha maji katika bwawa hilo. Tathmini iliyofanyika mwaka 2012 ilibaini kuwa zinahitajika shilingi bilioni 1.2 kwa ajili ya ukarabati wa bwawa na kunyanyua tuta ili kuongeza kina cha bwawa na hivyo kuwezesha kumwagilia hekta 220 katika Skimu ya Chalinze.

Mheshimiwa Spika, bwawa la tatu ni Bwawa la Izava lilijengwa miaka ya 1972/1973 kwa ajili ya mifugo na kilimo cha umwagiliaji. Pamoja na changamoto ya kujaa mchanga na matope bwawa hilo limeendelea kutoa huduma kwa wananchi hadi mwaka 2015 ambapo kupitia Mradi wa TASAF ililikarabati pamoja na kushirikiana na wananchi kupitia utaratibu wa kufanya kazi za kujitolea na kutumia kiasi cha Sh.7,418,000 kuwalipa wananchi hao. Mwaka 2017/2018, wakati wa mvua za msimu, kingo za bwawa hilo zilibomoka na hivyo kushindwa kutunza maji kwa ajili ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, Serikali itatuma timu ya wataalam kwa ajili ya kufanya usanifu wa kina ili kubaini mahitaji halisi ya ujenzi wa mabwawa hayo kwa wakati huu. Aidha, Serikali inashauri wananchi wanaoishi kwenye maeneo ya vyanzo vya maji na na upande wa juu wa bwawa kuacha kufanya shughuli za kibinadamu ili kuboresha mazingira yao na kutatua changamoto za kujaa mchanga na tope ziweze kupata ufumbuzi wa kudumu.
MHE. JOEL M. MWAKANYAGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuitengeza barabara inayounganisha kijiji cha Bwawani kilichopo Kata ya Manchali na Kijiji cha Ikowa kilichopo Kata ya Ikowa ili iweze kupitika katika kipindi chote cha mwaka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshmiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa, kama ifuatavyo:-

Mheshmiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Wilaya ya Chamwino imekuwa ikifanya matengenezo ya mara kwa mara ili kuwezesha barabara hiyo kupitika nyakati zote. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali ilifanyia matengezo barabra ya Chinangali II – Ikowa yenye urefu wa kilomita tatu kwa gharama ya shilingi milioni 14.15.

Mheshimiwa Spika, ili kuifikia barabara ya Chinangali II – Ikowa ni lazima kutengeneza kwanza barabara ya Mwegamile – Makoja - Ikowa na katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 114 kwa ajili ya kufanyia matengezo barabara ya Mwegamile –Makoja – Ikowa. Aidha, tathmini iliyofanywa na Wakala wa Barabra za Vijiji na Mijini (TARURA) imebainisha kuwa jumla ya shilingi milioni 668.2 zinahitajika kufanya matengenezo makubwa ambayo ndiyo itakuwa suluhisho la kudumu kwenye barabara ya Ikowa - Kiegea kwa maana ya Bwawani yenye urefu wa kilomita 12.3.

Mheshimwia Spika, katika mwaka wa fedha 2018/ 2019, Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino imetengewa bajeti ya shilingi bilioni 1.4 kwa ajili ya matengenezo ya barabara na ilipokea kiasi cha shilingi bilioni 1.2 ikiwa ni asilimia 82 ya bajeti. Baadhi ya barabara zilizotengenezwa ni barabara ya lami ya Chamwino Mjini, Haneti – Kwahemu- Gwandi na Zajilwa. Chinangali II – Chilowa na barabara ya Dabalo – Segela. Aidha, kwa mwaka fedha 2019/2020 Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino imetengewa kiasi cha shilingi bilioni 1.366 kwa jili ya matengenezo ya barabara.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na jitihada za kutafuta fedha kuiwezesha TARURA kuimarisha mtandao wa barabara wa Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino ikiwa ni pamoja na barabara inayounganisha Kijiji cha Bwawani – Ikowa.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuitengeneza kwa kiwango cha kupitika muda wote wa mwaka barabara inayounganisha Kijiji cha Mbelezungu na Kijiji cha Majeleko vyote vikiwa ndani ya Kata ya Majeleko?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Mbelezungu – Majeleko yenye urefu wa kilometa 10 imeingizwa kwenye mtandao wa barabara zinazohudumiwa na Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA) na hivyo kukidhi vigezo vya kufanyiwa matengenezo kupitia fedha za Mfuko wa Barabara. Aidha, tathmini ya barabara hiyo imefanyika na kubaini zinahitajika shilingi milioni 288.9.

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuifanyia matengenezo barabara hiyo kulingana na upatikanaji wa rasilimali fedha.