Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Ruth Hiyob Mollel (12 total)

MHE. RUTH H. MOLLEL aliuliza:-
Kwa muda mrefu Serikali imekuwa ikipeleka viongozi na wananchi wengine nje ya nchi kwa matibabu yanayohitaji utaalam wa hali ya juu:-
(a) Je, Serikali imetumia kiasi gani cha fedha kwa matibabu nje ya nchi kuanzia mwaka 2011 – 2015?
(b) Je, Serikali imetumia kiasi gani cha fedha kununua vifaa tiba vya kisasa kwa ajili ya Hospitali za Mikoa ambazo kwa sasa zimepandishwa hadhi na kuwa za rufaa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Hiyob Mollel, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, takwimu sahihi zilizopo za fedha iliyotumika kwa matibabu ya nje ya nchi kuanzia mwaka 2012 ni Sh.32,856,890,858.90. Takwimu za miaka ya nyuma ya hapo zilizopo hazina usahihi wa kutosha na zinaendelea kufanyiwa kazi na pindi zitakapokaa sawa tutamkabidhi Mheshimiwa Mbunge kwa ajili ya rejea yake.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kiasi cha fedha zilizotumika kununua vifaa vya kisasa kwa ajili ya Hospitali za Rufaa za Mikoa zilizopandishwa hadhi ni sh. 4,128,262,150/=. Mchanganuo wa fedha hii ni kama ifuatavyo:-
(i) Mgao wa kawaida wa fedha za kununulia vifaa ulikuwa ni sh. 2,292,187,500.
(ii) Mkopo wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kwa ajili ya kununulia vifaa uliotolewa kwa Hospitali za Rufaa ngazi ya Mkoa ni sh.1,836,074,650.
MHE. RASHID A. SHANGAZI (K.n.y. MHE. RUTH H. MOLLEL) aliuliza:-
Mheshimiwa Rais amepunguza idadi ya Wizara kutoka 23 hadi 18 ili kupunguza gharama za uendeshaji:-
Je, ni kiasi gani cha fedha za walipa kodi zilizookolewa kwa kuwa na idadi ndogo ya Wizara.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Hiyob Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ya Mheshimiwa Rais ya kupunguza Wizara kutoka Wizara 28 hadi 18 ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi yake, ya kupunguza gharama za uendeshaji na ukubwa wa Serikali aliyoitoa wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 na katika Hotuba yake wakati akizindua Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Lengo likiwa ni kuboresha huduma kwa wananchi wetu kwa kuelekeza matumizi makubwa ya Serikali katika huduma za kijamii, kama vile afya, elimu, maji, miundombinu na mawasiliano pamoja na miradi ya maendeleo.
Uundwaji wa Serikali ya Awamu ya Tano bado unaendelea, kwa sasa Serikali inafanya uchambuzi wa kina wa majukumu ya kila Wizara, na taasisi zake ili kuainisha majukumu ambayo ni muhimu kuendelea kutekelezwa na Serikali na taasisi zake au la na kuchukua hatua stahiki. Uchambuzi huu utaiwezesha Serikali kubaini majukumu yanayofanana ndani ya taasisi, lakini yanatekelezwa na kitengo au Idara zaidi ya moja, au majukumu yanayofanana, lakini yanatekelezwa na taasisi zaidi ya moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi hili pia litawezesha kubaini, kama idara au vitengo ndani ya Wizara na taasisi zake, vina majukumu ya kutosha ya kuhalalisha uwepo wake. Kukamilika kwa uchambuzi huu, ndio itakuwa msingi kwa Serikali kuuhisha miundo ya mgawanyo wa majukumu wa Wizara na taasisi zake na hivyo kujua gharama halisi, zitakazotokana na kupunguzwa kwa Wizara kutoka 28 hadi kufikia 18.
MHE. RUTH H. MOLLEL aliuliza:-

Mashirika ya Hifadhi ya Jamii yamewekeza katika miradi mbalimbali kwa kutumia michango ya wanachama:-
Je, wanachama wamepata gawio kiasi gani na faida ya uwekezaji?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Hiyob Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mifuko ya hifadhi ya jamii imegawanyika katika makundi makuu mawili. Mifuko inayoendeshwa kwa mfumo wa pensheni yaani defined benefits schemes na mifuko inayoendeshwa kwa mfumo wa akiba yaani defined contribution schemes. Mfumo unaotumika Tanzania ni mfumo bayana wa pensheni (defined benefits schemes).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa mfumo huu, malipo ya mafao ni ahadi ambayo mfuko huahidi kumlipa mwanachama pindi anapojiunga na mfuko kupitia vikokotoo maalum vya mafao vilivyowekwa kisheria. Hivyo, katika mfumo huu hakuna utaratibu wa kumlipa mwanachama gawio badala yake ukokotoaji wa mafao ya mwanachama huzingatia mshahara wa mwanachama na muda wa uchangiaji. Kwa mwanachama aliyechangia kwa kipindi kinachostahili (vesting period) na ambaye mshahara wake ulikuwa ukiongezeka katika kipindi cha ajira yake kiasi cha mafao anacholipwa wakati wa kustaafu ni kikubwa zaidi kuliko kiasi alichochangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kiasi cha pensheni wanacholipwa wastaafu nchini ni asilimia 72 ya mishahara yao ya mwisho. Kiasi hiki hulipwa kila mwezi kwa muda wote wa uhai wa mwanachama. Hivyo, uwekezaji na faida yote inayopatikana katika uwekezaji unaofanywa na mifuko ya hifadhi ya jamii husaidia mfuko husika kuweza kulipa mafao kama ulivyoahidi pamoja na mafao mengine ya muda mfupi kama vile mafao ya uzazi, matibabu na mazishi.
MHE. MCH.PETER S. MSIGWA (K.n.y. MHE. RUTH H. MOLLEL) Aliuliza:-
Nchi yetu inaendeshwa kwa kuzingatia Katiba, Sheria na Kanuni katika kuajiri na kuwasimamisha kazi watumishi wa umma. Kuna baadhi ya watumishi wa umma wamesimamishwa kazi na Mheshimiwa Rais, RC na hata DC bila kuzingatia Sheria ya Utumishi wa Umma na Kanuni zake.
Je, Serikali inasemaje kuhusu hili?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA Alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua za nidhamu katika utumishi wa umma hutekelezwa kwa kuzingatia Katiba, Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo mbalimbali. Kwa mujibu wa Ibara ya 36 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, Rais ndiye mwenye mamlaka ya mwisho kuhusu usimamizi na
uendeshaji wa utumishi wa umma, ikiwemo kuanzisha, kufuta Ofisi na kuchukua hatua za nidhamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara hiyo ya 36(2) imempa Rais uwezo wa kukasimu madaraka yake kwa mamlaka mbalimbali ndani ya utumishi wa umma. Hata hivyo kukasimu madaraka hakuwezi kutafsiriwa kwamba Rais hana mamlaka hayo tena kama ilivyofafanuliwa katika Ibara ya 36(4) ya Katiba na Kifungu cha 21(4) cha Sheria ya Utumishi wa Umma Sura ya 298.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale maelekezo ya kuchukua hatua za kinidhamu dhidi ya watumishi wa umma yanapotolewa na Viongozi wa Serikali, Mamlaka za Nidhamu za watumishi husika ndizo zenye dhamana ya kuchukua hatua kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Utumishi wa Umma.
RUTH H. MOLLEL aliuliza:-
Maboresho ya utendaji wa Serikali za Mitaa yalilenga kuimarisha na kujenga uwezo wa Serikali za Mitaa kujiendesha kwa kuwapatia rasilimali watu na fedha za kutosha kutekeleza Sera ya Ugatuaji wa Madaraka.
Je, Serikali ina lengo gani kuimarisha Serikali za Mitaa ziweze kujiendesha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Hiyob Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Ibara za 145 na 146 za Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mamlaka za Serikali za Mitaa ni mamlaka shirikishi za kisheria na kidemokrasia zilizoanzishwa kwa kwa lengo la kuwashirikisha wananchi katika shughuli zote za maendeleo, huduma za jamii, utawala bora, utekelezaji wa sheria, ulinzi na usalama kwa kuzingatia kanuni za uwazi na uwajibikaji.
Mheshimiwa Spika, tangu mwaka 1999 Serikali imetekeleza programu mbalimbali za kuboresha utendaji katika ngazi ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa. Miongoni mwa programu hizo ni Programu ya Maboresho ya Serikali za Mitaa iliyolenga kuimarisha miundo na mifumo ya Mamlaka za Serikali za Mitaa ili zijiendeshe na kuwahudumia wananchi kwa ufanisi. Aidha, Programu ya Maboresho ya Usimamizi wa Fedha imeimarisha na kuinua uwezo wa Halmashauri katika kukusanya mapato na kudhibiti matumizi.
Mheshimiwa Spika, katika kuziimarisha zaidi Mamlaka za Serikali za Mitaa, bajeti ya ruzuku ya maendeleo kwa Halmashauri imeongezeka kutoka shilingi bilioni 49 mwaka 2008 hadi shilingi bilioni 249 mwaka 2017. Aidha, kuanzia mwaka 2015, Mamlaka za Serikali za Mitaa zimeruhusiwa kwa mujibu wa sheria kuajiri watumishi wake wa kada 22 za ngazi za chini ikiwemo Watendaji wa Vijiji baada ya kupata kibali cha kuajiri. Ahsante.
MHE. RUTH H. MOLLEL aliuliza:-
Serikali yoyote duniani inaendeshwa na rasilimali watu wenye weledi, ari na uzalendo. Ili Watumishi hawa wafanye kazi kwa moyo wanahitaji kuthaminiwa, kutambuliwa mchango wao na kupewa stahili zao bila bughudha:-
Je, Serikali imebuni mkakati gani wa kuwapa motisha na ari Watumishi wa Umma ili wafanye kazi kwa kujituma badala ya vitisho?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Hiyob Mollel, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, napenda kutoa maelezo kwamba utekelezaji wa shughuli za Serikali huendeshwa kwa mujibu wa Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo mbalimbali inayosimamia Utumishi wa Umma ambapo kila mtumishi hupaswa kuzingatia wakati wa kutekeleza majukumu yake. Hivyo, Serikali haitumii vitisho wala bughudha katika kusimamia watumishi wake, bali husimamia sheria, kanuni na taratibu hizo.
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kuwa Watumishi wa Umma ni rasilimali ya msingi katika kufanikisha utekelezaji wa majukumu na malengo yake kwani nguvu na mafanikio ya Taifa lolote inategemea aina ya Watumishi lililonao na ni kwa msingi huo, Watumishi hawana budi kuendelezwa na kupewa motisha ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo. Kwa kutambua umuhimu wa motisha kwa Watumishi wa Umma, Serikali inayo mikakati mbalimbali inayolenga kuongeza ari kwa Watumishi wa Umma na hivyo kuwawezesha kufanya kazi kwa weledi na kwa kujituma. Mikakati hii ni pamoja na:-
(a) Kupunguza kiwango cha kodi ya mapato kwenye mshahara au Pay As You Earn kutoka asilimia 14 mwaka 2010/2011 hadi asilimia tisa mwaka 2016/17. Hatua hii imesaidia kuongezeka kwa kiwango cha mshahara anachobakinacho mtumishi baada ya kukatwa kodi.
(b) Kuongeza kima cha chini cha mshahara kutoka Sh.100,000/= mwaka 2010/2011 hadi Sh.300,000/= mwaka 2015/2016 sawa na ongezeko la asilimia 200.
(c) Kupitia Waraka Na. 3 wa mwaka 2011 unaohusu utaratibu wa kuwakopesha watumishi vyombo vya usafiri, Serikali imekuwa ikiwakopesha Watumishi vyombo vya usafiri ili kuwapunguzia adha ya usafiri wakati wa kwenda kazini na kurudi majumbani.
(d) Kutoa dhamana kwa watumishi wakati wanapokopa fedha katika Benki na Taasisi mbalimbali za kifedha.
(e) Kuanzisha Watumishi Housing Company Limited kwa ajili ya kujenga nyumba za gharama nafuu na kuwauzia au kuwakopesha Watumishi ili waishi kwenye makazi yenye staha.
(f) Kupitia sera ya mafunzo katika Utumishi wa Umma ya mwaka 2013, Serikali imekuwa ikitumia rasilimali fedha kwa ajili ya kugharamia mafunzo ya Watumishi wa Umma ili wawe na weledi wa kutosha.
(g) Serikali imekuwa ikiratibu nafasi za mafunzo ya muda mrefu na mfupi kwa Watumishi wa Umma kutoka kwa nchi na wadau wa maendeleo kama vile Ubelgiji, Uholanzi, Australia, Jamhuri ya Korea, Ujerumani, China, Japan, India, Malaysia, Indonesia, Singapore, Sweden na Jumuiya ya Madola na nchi zinginezo.
(h) Pamoja na Serikali kufanya zoezi la tathmini ya kazi kwa lengo la kubaini uzito wa majukumu ya Kada mbalimbali za Watumishi na hivyo kuwa msingi wa kupanga ngazi za mishahara. Zoezi hili linatarajiwa kukamilika katika mwaka 2017/2018.
MHE. RUTH H. MOLLEL aliuliza:-
Utumishi wa umma ndiyo injini ya maendeleo katika nchi. Watumishi wa umma hawatakiwi kuwa na mrengo wowote wa itikadi ya kisiasa ili kutumikia wananchi kwa muda wote hata yanapotokea mabadiliko ya vyama tawala baada ya uchaguzi.
i. Je, Serikali ya Awamu ya Tano ina mkakati gani wa kuhakikisha utumishi wa umma ni thabiti na wa kuaminika wakati wote?
ii. Je, ni watumishi wangapi wa umma ambao wamegombea vyeo katika chama tawala wakati wapo katika ajira ya utumishi wa umma?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA Alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Hiyob Mollel, Katibu Mkuu Mstaafu, senior citizen mwenzangu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Kanuni ya 65(1), Jedwali la Tatu, Sehemu ya IX ya Kanuni za Utumishi wa Umma za mwaka 2003 ikisomwa kwa pamoja na aya ya 50 ya Taratibu za Uendeshaji Utumishi wa Umma za mwaka 2003, watumishi wa umma wanatakiwa kutokuwa na mrengo wowote wa itikadi ya siasa ili kuwatumikia wananchi kwa muda wote bila ubaguzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kulihakikishia Bunge lako tukufu kuwa kanuni hizi zimeendelea kuwepo pia katika Serikali ya Awamu ya Tano na hivyo kuendelea kuimarisha utumishi wa umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa waraka wa Mkuu wa Utumishi wa Umma Na.1 wa mwaka 2015 unaosimamia ushiriki wa watumishi wa umma katika uongozi wa kisiasa watumishi wote wa umma waliogombea na kupata nafasi za uongozi wa kisiasa walistaafu na hawapo tena katika utumishi wa umma.
MHE. . JOSEPH R.SELASINI - (K.n.y MHE. RUTH H. MOLLEL) aliuliza:-
Serikali ya Awamu ya Tano inajinasibu kuzingati Utawala wa Sheria, Kanuni na taratibu katika Utumishi wa Umma. Hata hivyo, kuna ushahidi kuwa baadhi ya viongozi wanakiuka maadili na taratibu lakini wameachwa pasipo kuchukuliwa hatua zozote za kinidhamu:-
(a) Je, tunaweza kujenga uchumi imara bila Watumishi wa Umma kuzingatia Kanuni na Sheria za Utumishi wa Umma?
(b) Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha Taifa linadumisha umoja ulioasisiwa na Baba wa Taifa?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UTUMISHI NA UTAWALA BORA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Hiyob Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, napenda kusisitiza kuwa nchi yetu inaongozwa kwa mujibu wa Sheria, Kanuni na Taratibu zinazojumuisha zile zinazosimamia Utumishi wa Umma. Endapo wapo watu wanaokiuka sheria, hao wanafanya hivyo kutokana na upungufu wao na kamwe haiwezi kutafsiriwa kuwa ni Sera ya Serikali ya Awamu ya Tano kwenda kinyume cha sheria.
Mheshimiwa Spika, hatua hizi za kinidhamu huchukuliwa pale inapothibitika pasipo shaka yoyote kuwa kosa limetendeka kwa makusudi. Pale ilipogundulika kuwa utendaji usiozingatia sheria unatokana na kutoelewa misingi ya Sheria, Serikali imelazimika kutoa mafunzo maalum ili kuwajengea uwezo watendaji wake ili watekeleze majukumu yao kwa ufanisi.
(b) Mheshimiwa Spika, napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kuwa Umoja wa Tanzania ulioasisiwa na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Shekhe Abeid Aman Karume unaendelezwa kwa njia mbalimbali, ikiwemo kuadhimisha siku maalum za viongozi hawa, ambapo maoni yao huakisiwa kupitia mikutano ya hadhara na makongamano mbalimbali kwa lengo la kuenzi malengo yao.
MHE. RUTH H. MOLLEL aliuliza:-

Ardhi ni rasilimali ya msingi katika nchi yoyote duniani na tamaa ya kupora ardhi imesababisha migogoro na vita:-

(a) Je, Serikali ilitenga bajeti kiasi gani kuanzia mwaka 2010 – 2015 kwa ajili ya kupima matumizi ya ardhi?

(b) Je, kati ya kilometa za mrada 945,000 za Tanzania ni eneo kiasi gani limepimwa hadi Disemba 2015?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda nijibu swali la Mheshimiwa Ruth Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa nabu Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi Namba 6 ya Mwaka 2007, uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi ni jukumu la mamlaka za upangaji ambazo ni Tume ya Taifa ya Upangaji wa Matumizi ya Ardhi kwa ngazi ya Taifa, Halmashauri za Wilaya pamoja na Halmashauri za Vijiji. Serikali imekuwa ikitenga fedha za kuwezesha uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi kila mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuanzia mwaka wa Fedha 2010 na 2011 hadi 2014/2015, Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi ilitenga na kutumia kiasi cha shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya kuandaa na kutekeleza mipango ya matumizi ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini. Aidha, wadau wa maendeleo wamekuwa wakiziwezesha mamlaka za uandaaji kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti ya kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi imekuwa ikiboreshwa mwaka hadi mwaka. Kati ya mwaka 2015 hadi 2018 Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi ilitenga jumla ya shilingi bilioni 6.3 kwa ajili ya kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi nchini. Kati ya fedha hizi kiasi cha shilingi bilioni 1.3 kimetumika kati ya mwaka 2015/2016 na 2017/2018 na kiasi cha bilioni tano kimetengwa kwa bajeti ya Tume kwa Mwaka 2018/2019.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, ardhi ya Tanzania imegawanyika, katika aina tatu ambazo ni ardhi ya kawaida, ardhi ya hifadhi na ardhi ya vijiji. Hadi sasa kuna takribani vipande vya ardhi 2,000 vilivyopimwa ambavyo vinakadiriwa kuwa na ukubwa wa eneo la kilometa za mraba 141,750 sawa na asilimia 15 ya eneo la nchi. Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi inaendelea na uboreshaji wa kumbukumbu za ardhi ikiwemo takwimu za upimaji ardhi kupitia mfumo unganishi wa kutunza kumbukumbu za ardhi, yaani ILMIS.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha kuwa eneo la ardhi ya nchi lililopimwa linaongezeka. Mojawapo ya mikakati hiyo ni mkakati wa kupanga, kupima na kumilikisha kila kipande cha ardhi nchini ulioanza kutekelezwa mwaka 2016 kupitia programu mbalimbali ikiwemo Programu ya Kuwezesha Umilikishaji wa Ardhi, yaani Land Tenure Support Progamme, katika Wilaya ya Kilombero, Ulanga na Malinyi Mkoani Morogoro. Ni matarajio ya Wizara kuwa, kupitia mkakati huu idadi ya vipande vya ardhi vilivyopimwa itaongezeka na hivyo kupunguza eneo la nchi ambalo halijapimwa.
MHE. RUTH H. MOLLEL aliuliza:-

Mtambo wa kuchoma takataka za hospitali na dawa zilizokwisha muda wake upo katika Kijiji cha Dundani Wilayani Mkuranga. Uchomaji unapofanyika moshi mzito huingia kwenye nyumba na maeneo ya wananchi wanaoishi karibu na mtambo huo na kuhatarisha afya zao:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kunusuru afya na maisha ya wananchi wanaoishi karibu na mtambo huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Hiyob Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba upo mtambo wa kuchomea taka na dawa zilizokwisha muda wake uliojengwa na mwekezaji katika Kijiji cha Dundani, Wilaya ya Mkuranga. Hapo awali mtambo huo ulikuwa na kasoro za ujenzi ambapo Serikali ilimwagiza mwekezaji kuzirekebisha kwa ilani ya tarehe 18, Oktoba, 2017 yenye kumbu. Na. NEMC/HQ/EA/05/0702/VOL1/7 sambamba na kusimamisha shughuli za mtambo mpaka kasoro zitakapokuwa zimerekebishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, marekebisho hayo yamefanyika na baada ya mamlaka zote, ikiwemo Serikali ya Kijiji cha Dundani kujiridhisha kwamba hakuna tena moshi unaoathiri mazingira, mtambo huo umeruhusiwa kuendelea na kazi na mpaka sasa hakuna taarifa yoyote iliyofika katika Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji, Wilaya ya Mkuranga kulalamikia shughuli za mtambo huo.
MHE. RUTH H. MOLLEL aliuliza:-

Shule ya Msingi Vikindu katika Wilaya ya Mkuranga ina mikondo miwili (A na B) darasa la kwanza hadi la saba na mwaka 2019 darasa la kwanza na la pili yalikuwa na wanafunzi 300 kila darasa.

(a) Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha uwiano wa mwalimu na mwanafunzi wa 1:45 unazingatiwa kwa mujibu wa Sera ya Elimu ya Msingi?

(b) Je, kwa msongamano huo tunaweza kupata wanafunzi walioelimika na kukidhi malengo ya Tanzania ya viwanda?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Hiyob Mollel, Mbunge wa Viti maalum kama ifuatavyo swali lake ambalo lina sehemu (a) na (b):-

(a) Mheshimiwa Spika, ongezeko la uandikishaji wa wanafunzi katika Halmashauri ya Mkuranga limetokana na juhudi za Serikali za kuhamasisha wananchi kuandikisha wanafunzi shuleni kupitia mpango wa elimu msingi bila malipo. Ili kukabiliana na msongamano wa wanafunzi katika Shule za Msingi Vikindu, Serikali imechukua hatua mbalimbali ikiwemo kujenga Kituo Shikizi cha Juhudi, Kitwangi, Mitawa na Muungano. Kituo Shikizi cha Muungano kilichopo katika Kijiji cha Vikindu kinatarajiwa kukamilika mwezi Februari, 2020 na kitakuwa na uwezo wa kupokea wanafunzi 300. Mkakati mwingine ni wanafunzi kusoma kwa kupokezana yaani double section ambapo kuna madarasa ya asubuhi na ya mchana.

(b) Mheshimiwa Spika, kama ilivyoelezwa kwenye sehemu (a) hatua mbalimbali zimechukuliwa na zinaendelea kuchukuliwa na Serikali ili kuhakikisha msongamano wa wanafunzi madarasani unapungua na kuwezesha kupata elimu bora. Ahsante.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI (K.n.y. MHE. RUTH H. MOLLEL) aliuliza:-

Migogoro ya wakulima na wafugaji imekuwa tatizo sugu katika maeneo mengi nchini pamoja na kazi kubwa ambayo imefanywa na Serikali:-

(a) Je, Serikali imetenga kiasi gani cha bajeti kwa ajili ya kupanga matumizi ya ardhi nchi nzima?

(b) Kijiji cha Matenzi Kata ya Beta Wilayani Mkuranga kina wafugaji takribani 10,000: Je, Serikali ina mkakati gani wa kupima eneo hilo kabla migogoro haijaanza?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi kwa mujibu wa Sheria ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi Na. 6 ya mwaka 2007, ni jukumu la mamlaka ya upangaji ambazo ni Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi kwa ngazi ya Taifa na Halmashauri za Wilaya na Vijiji kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikitenga fedha za kuwezesha uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi kila mwaka. Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2017/2018 hadi 2019/2020 Serikali imetenga shilingi bilioni saba za matumizi ya kawaida na maendeleo kwa ajili ya kupanga matumizi ya ardhi na kutatua migogoro ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2018/2019 Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi, iliendelea kuwezesha upangaji wa matumizi ya ardhi katika vijiji vyote vinavyozungukwa na hifadhi za misitu na hifadhi za Taifa. Kazi hii itaendelea katika mwaka wa fedha 2019/ 2020 ikijumuisha upangaji wa matumizi ya ardhi katika vijiji vyote vinavyopitiwa na Mradi wa Bomba la Mafuta pamoja na wilaya zote mpakani mwa nchi jirani. Aidha, wadau mbalimbali wa maendeleo wamekuwa wakiwezesha mamlaka za upangaji kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Uandaaji wa Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi Na. 6 ya mwaka 2007, kifungu cha 33(1) kinatoa mamlaka kwa Halmashauri za vijiji kujiandalia mipango ya matumizi ya ardhi. Vilevile, vifungu vya 9(1) na 21(2)(b) vya Sheria ya Ardhi ya Vijiji Na. 5 ya mwaka 1999 na miongozo ya kuandaa mipango ya vijiji wa mwaka 2013 vinatoa mamlaka kwa Halamshauri za Wilaya kujengea vijiji vyake uwezo na kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi pamoja na kuratibu kazi hizo.

Mheshimiwa Spika, Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi imeshajengea uwezo na kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi ya vijiji katika Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga. Hivyo, ni jukumu la Halmashauri hiyo kuendeleza kazi ya kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi ya vijiji vyake kwa kutoa kipaumbele kwenye vijiji vyenye migogoro ya matumizi ya ardhi na tishio kwa hifadhi ya ardhi na mazingira, hususan hicho Kijiji ambacho Mheshimiwa amekitaja cha Beta ambacho anasema kina mifugo zaidi ya 10,000.