Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Halima Abdallah Bulembo (7 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Kwa majina naitwa Halima Abdallah Bulembo, ni Mbunge wa Viti Maalum kundi la vijana au Mbunge mdogo kuliko wote. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba kumpongeza Mheshimiwa Rais, katika kipindi alipokuwa akitafuta kura aliahidi kutowaangusha vijana na ukiangalia Baraza lake Mawaziri wengi ni vijana, ukimuangalia kaka yangu Wakili msomi Mavunde ni kijana, kuna Injinia Masauni ni kijana, kuna Dkt. Kigwangalla na kuna Dkt. Possi, tunamuahidi na sisi vijana hatutomuangusha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo, naomba pia kusema kidogo. Nina masikitiko katika suala zima linaloendelea Bungeni, Wabunge wenzetu wa Upinzani kuwa wanatoka. Ningeshauri kale kautaratibu ka posho tungekuwa tunasaini saa 12 jioni tuone pia kama wangekuwa wakitoka? (Makofi).
Baada ya hayo machache, naomba kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa hotuba yake nzuri, ni hotuba yenye kufufua matumaini, ni hotuba yenye kujali wananchi hasa wanyonge, ni hotuba yenye kujali na kuleta nuru na matarajio mapya kwa wananchi na kiukweli Tanzania mpya inaonekana chini ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mimi ni kijana, nitaanza na tatizo sugu la vijana ambalo ni ajira na kaka yangu Mheshimiwa Mavunde naoma unisikilize. Katika hotuba ya Rais, alizungumzia tatizo la ajira kwa vijana. Wote tunafahamu kwamba ajira ni tatizo sugu si kwa Tanzania tu lakini ni kwa dunia nzima. Tatizo hili linahitaji msukumo zaidi wa Kiserikali, Taasisi mbalimbali lakini vilevile linahitaji sisi wenyewe Wabunge tukipata fursa za ajira tuzipeleke kwa vijana, tusisubirie Serikali tu, tukiendelea kusubiria Serikali ifanye kila kitu tutaishia kubaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika suala zima la ajira naomba kuwaambia Watanzania kwamba vijana wengi wanajiajiri na vijana ambao wanakuwa na uwezo wa kujiajiri ni kuanzia umri wa miaka 18 mpaka 35 ambayo ni asilimia 32 ya Watanzania, kwa hiyo vijana ni kundi kubwa. Safari hii kuna utaratibu vijana wengi wamekuwa wakienda Jeshini, ushauri wangu kwa Serikali, nilikuwa naomba katika kila Kambi ya JKT, kuwe na Chuo au Vyuo vya VETA, vijana wanapotoka hapo wapewe mikopo na nyenzo za kazi. Kwa hivi tunaweza tukasaidia kwa namna moja ama nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapo hapo naomba kuzungumzia suala la mikopo, niko na vijana bado. Masharti ya mikopo yamekuwa makubwa! Kijana leo anamaliza Chuo Kikuu anataka kujiajiri, anaambiwa ukitaka mkopo leta kiwanja, leta nyumba! Jamani, ndiyo nimemaliza chuo, nyumba naipata wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ningeomba Serikali iongee na taasisi za fedha zilegeze masharti kwa vijana wanaokuwa wamemaliza Chuo, ili waweze kujiajiri. Tunaona nchi inaendeshwa kwa watu wengi ambao wamejiajiri, tuwasaidie vijana wafike kule wanakotaka kufika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ninalotaka kuzungumzia ni suala la ushuru. Mheshimiwa Rais aliahidi na aliongea kwa msisitizo mkubwa kwamba, atapunguza na kuondoa ushuru kwa wafanyabiashara wadogo wadogo. Alisema pia, ataondoa harassment zinazofanyika na mgambo wa Manispaa na Majiji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kinachofanyika wote tunakijua, wafanyabiashara wadogo bado wananyanyasika, inatia uchungu. Unamkuta mama lishe kajipangia pale anauza chakula, mgambo anakuja anamwambia kama hutaki nikufukuze nipe 1,000/=! Tangu asubuhi hiyo 1,000/= ndiyo anayoitafuta! Kwa hiyo, kaka yangu Mheshimiwa Simbachawene watu wako hawa uongee nao vizuri, bado wanaendelea kunyanyasa watu wetu na tukumbuke katika nchi yoyote kuna wafanyabiashara wakubwa kama akina Bakhresa, kuna wafanyabiashara wa kati kama akina Shabiby, lakini kuna wafanyabiashara wadogo wadogo! Sasa kwa nini wale wakubwa hawaonewi mnawaonea wadogo, si haki! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais alisema kabla ya kuwafukuza wale au kuwaondoa, mwambie mama hapa hustahili kukaa, lakini eneo lako husika ni hili. Unamwambia hapa hufai kukaa, eneo la kukaa halifahamiki, hujampangia! Ni wakati wa Halmashauri za Manispaa na Wilaya ziitikie kwa vitendo hotuba ya Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Naibu Spika, kila Halmshauri ioneshe ni wapi imetenga maeneo kwa hawa watu. Wafanyabiashara wanaishi kwa mashaka, hawana matumaini, wanatapakaa mitaani! Kwa kufanya hivyo tunazidi kumtia aibu Mheshimiwa Rais kuonekana alichokuwa anakizungumza na kuwaahidi wafanyabiashara wadogo wadogo si sahihi. Kwa hiyo, mimi naomba sana Serikali itie mkazo katika masuala haya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la mwisho kabisa nataka nimalizie na suala zima la elimu. Naomba kumpongeza Mheshimiwa Rais kwamba ameweza kulitimiza kwa asilimia kubwa, elimu imekuwa bure kuanzia elimu ya msingi mpaka kidato cha nne.
Lakini pia nataka kuzungumzia kuhusu vijana wanaomaliza Chuo Kikuu kwamba kunakuwa na fursa vijana wengi huomba kwenda kusoma nje ya nchi. Lakini fursa hizi kwa uzoefu na kwa utafiti wangu Tanzania ya leo ina Vyuo Vikuu vingi, lakini vijana wengi wanaomaliza Chuo Kikuu huomba zile fursa za kutaka kusoma nje, lakini ambao hupata fursa siku zote wanachukuliwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Mzumbe! Kwa maana bado sitaki kuamini kama ile dhana ambayo ilikuwa inasema mtu akisoma Mzumbe na UDSM ndiyo anakuwa hatari kabisa. Siku hizi kuna wanafunzi ambao wana uwezo mkubwa wapo UDOM, wapo Tumaini, wapo katika kila chuo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa naomba vigezo mnavyovitumia kuwachukua hawa vijana kuwapa nafasi za kusoma nje ya nchi, zifike katika kila chuo, zisiende UDSM na Mzumbe peke yake, tuwape vijana wote haki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema machache hayo naomba kushukuru sana, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa juhudi zake kubwa anazozifanya za kuhakikisha wananchi wa Tanzania wanapata maendeleo. Vilevile naomba kuwapongeza ndugu zangu Wazanzibar kwa kumaliza uchaguzi salama, kwa kurudi na amani, sasa ni kazi tu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijajielekeza kwenye hoja yangu, naomba sana kumshukuru Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo kwa suala zima alilosimamia kuhusu kuonekana kwa Bunge live. Napata shida sana pale watu wanapong’ang’ania kuonekana kwenye tv at least ningekuwa nasimama mimi Mbunge mpya, mdogo niseme nionekane lakini kuna watu wana majina, nina mdogo wangu ana miaka sita anamjua Mbowe ni Kiongozi wa Kambi ya Upinzani, sasa anang’ang’ania kuonekana kwenye tv ili iweje? Tukiachilia mbali hilo, tumeona sasa hivi Wabunge wa Upinzani wakisema hoja zao zikisikika. Kwa hiyo, naomba sana kumpongeza Mheshimiwa Nape.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo, naomba kuzungumzia bajeti ya Waziri Mkuu na naomba nijielekeze kuzungumzia mustakabali wa vijana katika nchi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Waziri Mkuu inasema utafiti wa mwaka jana vijana ni asilimia 59 hii inaonesha vijana ni kundi kubwa. Vijana hawa wanatakiwa kuwekewa mazingira mazuri, mazingira bora kwa sababu ndiyo nguvu kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vijana ambao wamegawanyika katika makundi matatu, kuna kundi la vijana ambao wanamaliza elimu ya msingi wanashindwa kuendelea na elimu, hawapewi vitu vya kufanya na mbaya zaidi Wabunge wengi au watu wengi ndiyo wanaowachukua kuwafanya wafanyakazi wa ndani, hii inaumiza. Unajua suala la ajira inabidi tuliongelee kutoka moyoni, wewe unamuona ni binti ana miaka 13 anakuja kukuomba kazi za ndani unamwajiri na umesimama hapa Mbunge unasema ajira kwa vijana huu ni unyanyasaji. Tunapozungumzia ajira inabidi sisi wenyewe tuonekane kwamba suala hili sisi wenyewe halitufurahishi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kuna suala linaniudhi sana, vijana wengi sasa hivi wanamaliza chuo kikuu mashallah unamkuta mtu amemaliza degree yake ya kwanza anaenda kusoma masters anafika hadi Ph.D, linapokuja suala la kupata ajira anaambiwa awe na experience, experience inatoka wapi. Usiponipa ajira ili nifanye kazi experience nitaitoa wapi? Suala hili linaumiza na naomba Wizara husika ilitilie maanani. Tunamwona Mheshimiwa Rais kawateua Wabunge ambao hawakuwepo katika mrengo wa kisiasa, wameteuliwa kuwa Wabunge wamekuwa Mawaziri na wanafanya kazi nzuri kwa nini hawa vijana tusiwape nafasi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Kamati yangu nilikuwa nazunguka sana naona wanakuja mainjinia, mimi ninamdadisi tu, baba shikamoo, hivi una muda gani hapa, mwanangu niko muda mrefu nina miaka 40 wakati kuna watu wamemaliza chuo, wanaweza, ni vijana wadogo hawapewi nafasi, wanawaacha tu walewale wa siku zote wanang’ang’ania zile nafasi. Si jambo zuri tuwape vijana nafasi waonyeshe uwezo wao.
Naomba Wizara iseme kama kila mwaka tunaajiri watu labda 500 katika hao asilimia 20 wawe ni vijana waliotoka vyuoni ili na wao waweze kupata nafasi, bila kuwapa nafasi hatuwezi kuona nguvu kazi zao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine ambacho nataka kuzungumzia ni vijana wajasiriamali wapewe mikopo. Juzi nimeuliza swali Mheshimiwa Waziri kanijibu, lakini hawa vijana wajasiriamali ndiyo wengi wamejiajiri lakini mitaji yao ni midogo. Naomba bajeti ya Wizara ione inaweza kuwasaidia vipi vijana wajasiriamali. Kama nilivyotangulia kusema awali niliomba hifadhi za jamii ziweze kujengewa uwezo ili vijana waweze kwenda kukopa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine Mheshimiwa Rais aliagiza vijana wanaocheza pool table wachukuliwe na watafutiwe sehemu ya kupelekwa, hii imekuwa ni shida. Mheshimiwa Rais hakusema wale vijana wachukuliwe wapelekwe Polisi au watishiwe maisha maana sasa imekuwa tafrani. Lengo la Mheshimiwa Rais lilikuwa zuri kwani alisema vijana wale wachukuliwe watafutiwe kazi za kufanya kwenye mashamba makubwa ambayo watu wanayahodhi. Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya watumie zile fursa wakimkuta kijana anacheza pool table wamchukue wamwambie heka yako moja hii hapa lima nyanya, naamini kijana umemfundisha analima, amepata faida shilingi milioni mbili hawezi kurudi kucheza pool table. Kinachoshangaza Maaskari wanawachukua wanawafunga na kwa kuwa ni agizo la Mheshimiwa Rais anamwambia nipe hela nikuachie, wamefanya kama ni mtaji, kwa hiyo hili suala Wakuu wa Wilaya na Mikoa walisikilize. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna hili suala linaitwa betting maarufu kama mkeka sijui mnalijua suala hili, siyo vijana tu hata watu wazima wanaenda kucheza lakini hii ni kamari na hili ni bomu linalokuja kulipuka, likija kulipuka tutakuwa tumechelewa. Kijana kama mimi saa mbili asubuhi anaenda kucheza betting. Hao watu wa betting wanaenda kuomba leseni Halmashauri na wanapewa wanasema ni biashara, si biashara inaua nguvu kazi za vijana. Naomba wahusika walifuatilie kwani siyo suala zuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni kwamba kila Halmashauri huwa zinatenga asilimia tano kwa ajili ya vijana. Halmashauri nyingi hazitengi asilimia hiyo. Nilikuwa nashauri Serikali iwape hati chafu kila Halmashauri ambayo haitatekeleza jambo hili ili kuwalazimisha kufanya kile kinachotakiwa kupeleka asilimia tano kwa vijana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuomba Wizara katika bajeti hii Mfuko wa Maendeleo ya Vijana uongezewe uwezo. Kwa kufanya hivyo itarahisa pesa kufika kwa vijana kiurahisi zaidi na kuwawezesha kupata maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho kabisa naomba kuzungumzia hili agizo tena la Mheshimiwa Rais kwa Serikali za Mitaa kutenga maeneo maalum yaani hili suala mimi linanikera.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimewashuhudia Mapolisi wanawakuta vijana wengine wamekaa tu mtaani wanakamatwa, Mheshimiwa Rais kaagiza watu hawatakiwi kuonekana, Mheshimiwa Rais tusimchonganishe na wananchi, tusimchonganishe na vijana. Wakuu wa Mikoa na viongozi wengine yale mashamba wanayohodhi wao kama wao watumie fursa zile kuwapa vijana ili waweze kupata mafanikio.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili na mimi niweze kuchangia na ninaomba nijielekeze moja kwa moja katika mchango wangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunajadili bajeti muhimu kuliko bajeti yoyote nchini. Leo tunajadili bajeti inayohudumia Watanzania wengi kuliko bajeti yoyote nchini na leo tunajadili Bajeti ya Taifa la sasa na hasa hasa Taifa la baadaye. Nitawaonyesha takwimu kuthibitisha maelezo yangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa Watanzania tunakadiriwa kuwa takribani milioni 50, nusu ya Watanzania wana umri wa miaka 17 kwa maana nyingine nusu ya Watanzania ni watoto. Kwa mujibu wa takwimu ya Taifa ndiyo inasema hivyo, kati ya watoto takribani milioni 25, watoto wetu milioni 12 wako katika shule zetu za awali, shule za msingi na shule za sekondari. Nizungumzie shule za awali. Kwa utafiti wa hali ya uchumi mwaka 2014, inaoneshsa idadi ya wanafunzi wa awali iliongezeka kwa asilimia 1.9 kutoka wanafunzi 1,026,466 mwaka 2013 hadi kufikia wanafunzi 1,046,369. Utafiti huo huo unaendelea kuonyesha idadi ya wanafunzi wanaojiunga na elimu ya msingi inazidi kupungua kutoka wanafunzi 8,202,892 mpaka wanafunzi 8,231,913 sawa na upungufu wa asilimia 0.4.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti huo huo unaendelea kuonesha wanafunzi wa kidato cha kwanza mpaka cha sita, idadi yao imeendelea kupungua kutoka wanafunzi 1,800,056 mpaka wanafunzi 1,704,130 sawa sawa na upungufu wa asilimia 5.5.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Basic Education Statistics yaani BEST, watoto wa Kitanzania milioni nne wako katika elimu ya msingi na watoto wa Kitanzania milioni nne wako katika elimu za sekondari. Kwa maana hiyo hapa tunazungumzia robo ya Watanzania wako mashuleni, robo ya Watanzania wako madarasani na wengine wamekaa chini kwa kukosa madawati, na wengine matumbo yao hayana kitu kwa kutoka familia fukara na shule hazina chakula na wengine wanagombea kitabu kimoja kwa kuwa hatuna vitabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri robo ya Watanzania inafundishwa na walimu wasiokuwa na hamasa na hamasa hii inakosekana kutokana na walimu kutokuwa na mishahara mizuri, kutokupandishwa madaraja katika kazi zao, kutokuwa na makazi yanayoeleweka na wengine kuwa walevi wa kutupa kutokana na stress za maisha. Tunajua kila mtu akiwa na stress zake anaamua pa kwenda wapi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kunauwezekano mamilioni ya watoto wetu wanafundishwa na walimu walevi, lakini leo hii nani ana mamlaka ya kuwawajibisha hawa walimu walevi ilihali elimu haina ukaguzi mzuri, nani ana mamlaka ya kuwaadhibisha walimu hawa kwakuwa hatuwezi kutatua kero zao, nani ana mamlaka? Hakuna. Robo ya Taifa tunaiweka mashakani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, robo ya wananchi wanapata robo ya bajeti. Bajeti ya Wizara ya Elimu ni shilingi trilioni 1.3 kwa pesa za Kitanzania. Tunaambiwa bajeti nyingine ipo TAMISEMI.
Mimi ningeshauri au ningeomba Wizara na Serikali yangu ingeipa bajeti ya Wizara ya Elimu peke yake na bajeti hii ingewekwa kwa uwazi ili tuweze kukokotoa, tujue asilimia 25 ya wananchi wanapata asilimia 25 kweli ya bajeti yao? Tukijumlisha na bajeti inayopelekwa TAMISEMI ambayo tunaambiwa iko TAMISEMI bado bajeti ya Wizara ya Elimu iko chini ya asilimia 10. Tunawakosesha watoto wetu haki ya kuwa na elimu bora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka miwili ya chekechea na miaka mitatu ya elimu ya msingi ni muhimu sana na wote tunajua kwamba elimu ya awali ni muhimu kwa vijana wetu. Lakini vile vile kama Watanzania tunajua Watoto wetu hawa wana matatizo, hawana msaada wa Kiserikali, hawana msaada wa kisera na wala hawana msaada wa kisheria kutoka hizi elimu za mwanzoni. Hali hii inabidi ibadilike kama tunataka kweli kujenga Taifa lililoelimika kwa mujibu wa Dira ya Taifa 2025.
Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo au takwimu za utafiti ya UWEZO inaonesha katika wanafunzi 10 wa darasa la tatu, ni wanafunzi watatu pekee wanaoweza kusoma sentensi ya darasa la kwanza na ni wanafunzi watatu wanaoweza kukokotoa hesabu za darasa la kwanza. Hii inaonesha kwamba Watoto wetu hawapati fursa nzuri ya kusoma huku tangu awali kwenye hizi elimu zao za mwanzoni. Tukitaka kubadili hali hii inabidi tuwekeze. Tuwekeze katika kupata kizazi cha wanafunzi wanaopenda kujisomea, wanafunzi ambao watakuwa na uwezo mkubwa wa elimu, wadadisi na hata wabunifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 50 ya vijana wanaomaliza elimu ya msingi hawaendi shule za sekondari na asilimia 75 ya wanafunzi wanaomaliza kidato cha nne hawaendi kidato cha tano na cha sita. Na sera yetu ya elimu sasa hivi inaunganisha elimu ya msingi ya sasa na elimu ya sekondari ya sasa kuwa elimu ya msingi kwa miaka 10. Hawa ambao hawapati fursa za kuendelea wanakwenda wapi? Rasilimali hii ya Taifa inaenda wapi? Na hapa ndiyo tunapokuja kuhitaji ufundi stadi na ufundi mchundo.
Naomba kuipongeza Serikali yangu kwa kuamua kuunganisha Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi na VETA lakini hapo hapo Serikali ya chama changu, Serikali ya Chama cha Mapinduzi iliahidi kujenga Vyuo vya VETA katika kila Halmashauri ya Wilaya tangu mwaka 2005. Mheshimiwa Waziri, mimi ninaimani kubwa na wewe, naomba usimamie suala hili litekelezwe. Zijengwe hizo VETA katika kila Halmashauri ya Wilaya ili tuwape vijana wetu stadi za maisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba kutoa ushauri katika suala hili kwamba tuamue kugeuza Jeshi la Kujenga Taifa yaani JKT liwe VETA kwa maana ya kwamba kila kwenye Jeshi la JKT tusajili VETA. Vijana wetu wanapoenda kusoma miaka miwili, mwaka mmoja waweze kupewa skills maalum za maisha na baada ya hapo waweze kupewa mikopo ya vifaa, hii itawajengea wenyewe uwezo wao wa kufanya kazi na tutajenga Taifa la watu ambao wanapenda kufanya kazi wao kwa wao, kujiajiri au kuajiriwa na Mheshimiwa Waziri, ningeomba suala hili la VETA liwe mpango maalum na lisimamiwe na Jeshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa naomba kuzungumzia walimu. Naomba kuzungumzia walimu wa kada maalum, walimu wa awali kwa maana ya chekechea mpaka darasa la kwanza, kuanzia darasa la kwanza mpaka la tatu. Walimu hawa wawe na mafunzo maalum, wapewe motisha maalum na Vyuo Vikuu vitoe shahada maalum kwa walimu hawa ili tuweze kuwajengea uwezo watoto wetu wanaokua kuanzia chekechea mpaka darasa la kwanza, la pili na la tatu. Na hii tukifanya hivyo tutawapata watu wengi, watoto wetu watakuwa na mwanzo mzuri, wataweza kufanya kazi vizuri kwa bidii lakini pia walimu hawa wa kada maalum wawe walimu maalum na wawe na mishahara maalum siyo wanapewa mishahara ambayo haieleweki Mheshimiwa Waziri. Kwa kufanya hivyo, tutaibadilisha Tanzania yetu katika kizazi kimoja tu kwa kuwekeza kwa walimu, kwa watoto na let us .....
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunajadili bajeti muhimu zaidi kuliko zote nchini. Tunajadili bajeti yenye kuhudumia watu wengi zaidi kuliko bajeti yoyote nchini; tunajadili bajeti ya Taifa la sasa na hasahasa Taifa la baadaye, nawaonesha takwimu kuthibitisha maelezo yangu haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania inakadiriwa kuwa na watu milioni 50 hivi sasa, asilimia 50% ya Watanzania hawa wapo chini ya miaka 17. Maana yake nusu ya Watanzania ni watoto, hii ni kwa mujibu wa takwimu ya Taifa. Katika watoto hawa takribani milioni 25, watoto milioni 12 wapo kwenye shule za awali, msingi na sekondari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, shule za awali. Utafiti wa hali ya uchumi wa Taifa mwaka 2014 inaonesha idadi ya wanafunzi katika elimu ya awali imeongezeka kwa 1.9% kutoka wanafunzi 1,026,466 mwaka 2013 hadi kufikia wanafunzi 1,046,369.
Mheshimiwa Mwenyekiti, shule za msingi. Utafiti huo huo unaonesha 2014, idadi ya wanafunzi katika elimu ya msingi ilipungua wanafunzi 8,202,892 kutoka wanafunzi 8,231,913 sawa na upungufu wa 0.4%.
Mheshimiwa Mwenyekiti, shule za sekondari. Utafiti huo pia unaonesha mwaka 2014, idadi ya wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha sita ilipungua hadi wanafunzi 1,704,130 kutoka wanafunzi 1,804,056 sawa na upungufu wa 5.5%.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Basic Education Statistics (BEST) watoto wa Kitanzania milioni nane wapo kwenye shule zetu za msingi, milioni nne wapo kwenye shule zetu za sekondari; kwa maana hiyo hapa tunazungumzia robo ya Watanzania wapo madarasani, mashuleni, wengine wamekaa chini kwa kukosa madawati, wengine matumbo hayana kitu kwa kutoka familia fukara na shule hazina chakula na wengine wanagombania kitabu maana hakuna vitabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri robo hii ya Watanzania inafundishwa na Walimu wasio na hamasa kutokana na mishahara midogo, kukosa makazi, kutopandishwa madaraja na hata wengine kuwa walevi wa kutupwa kutokana na stress za maisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia na mamilioni ya watoto wetu wanaweza kuwa wanafundishwa na Walimu walevi, nani atawawajibisha ilhali ukaguzi wa elimu hautiliwi maanani? Nani atathubutu kuwawajibisha ilhali hatuhangaiki kutatua kero zao? Naomba kuwaambia robo ya Taifa letu tumeliweka mashakani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, robo ya wananchi wanapata bajeti robo, Wizara ya Elimu ina bajeti ya sh. trilioni 1.3 hivi; tunaambiwa nyingine ipo TAMISEMI, ni vema Serikali ikaweka bajeti nzima ya Wizara ya Elimu pamoja na wazi ili tuweze kujua kwa uhakika kama 25% ya wananchi wanapata 25% ya bajeti yetu ya Taifa, lakini hata tukiweka zilizokwenda TAMISEMI bado bajeti yetu ya elimu ni chini ya 10% ya bajeti nzima. Tunawanyima watoto wetu haki yao ya kupata elimu bora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka miwili ya chekechea na miaka mitatu ya shule ya msingi ni muhimu sana, lakini sisi sote tunajua hali ya watoto wa Kitanzania ni mbaya sana, hakuna msaada wowote wa Kiserikali, Kisera au Kisheria kuhusu siku za mwanzo za mtoto. Hali hii inabidi ibadilike kama tunataka kujenga Taifa lililoelimika kwa mujibu wa Dira ya Taifa 2025.
Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo ya utafiti ya uwezo yanaonesha kuwa katika kila watoto 10 wa darasa la tatu ni watoto watatu tu wenye kuweza kusoma sentensi ya darasa la kwanza na kukokotoa hesabu za darasa la kwanza, hii inaonesha watoto wetu hawapati fursa ya kusoma vizuri katika miaka yao ya mwanzoni shuleni. Jamani tuwekeze kubadilisha hali hii na tukiweza kuwekeza tutapata kizazi cha watoto wenye uwezo mkubwa wa elimu wenye kupenda kusoma, wadadisi na wabunifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, 50% ya vijana wanaomaliza darasa la saba hawaendelei na elimu ya sekondari, pia 75% ya vijana wanaomaliza kidato cha nne hawaendi kidato cha sita. Hivi sasa Sera yetu ya Elimu inaunganisha elimu ya sasa ya msingi na elimu ya sasa ya sekondari na yote kwa pamoja kuwa elimu ya msingi kwa miaka 10, vijana hawa wanaomaliza hawaendelei, wanakwenda wapi? Rasilimali hii inapotelea wapi? Hapo ndipo tunapohitaji elimu ya ufundi stadi na ufundi mchundo.
Naipongeza Serikali kwa kuamua kuviunganisha Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi na VETA. Ilani ya uchaguzi ya chama chetu iliahidi kujenga VETA kila Halmashauri ya Wilaya toka mwaka 2005. Namwomba Mheshimiwa Waziri tutekeleze ahadi hii ili kuwapa stadi za maisha vijana wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuamue kugeuza Jeshi la Kujenga Taifa kuwa VETA, kila Kambi ya Jeshi isajiliwe kuwa VETA ili wale wanaokwenda Jeshini kwa miaka miwili, mwaka mmoja uwe wa kupata skills maalum za maisha, apewe mkopo wa vifaa, tutoke kwenye maneno twende kwenye vitendo. Tutumie rasilimali za nchi kujenga vyuo, kufundisha Walimu wa vyuo hivi na kujenga Taifa la watu wanaofanya kazi ama kuajiriwa au kujiajiri, suala la VETA liwe ni mpango malum na utekelezwe na jeshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, ni kuhusu Walimu. Nashauri Kada Maalum ya Elimu ya Awali (Chekechea mpaka Darasa la Tatu) kada hii iwe na mafunzo maalum na motisha maalum, vyuo vikuu vitoe shahada maalum za kada hii na tuwe na mradi maalum wa utafiti wa namna watoto wanajifunza kutokana na kada hii na hawa wasiwe Walimu wa kawaida. Walimu wa watoto wetu wadogo wawe Walimu maalum na mishahara yao iwe malum.
Kama tunataka kujenga Taifa la watu wanaojifunza tuanze sasa kuwekeza kwa Walimu na watoto wetu katika hatua za mwanzo kabisa. Tubadilishe Tanzania ndani ya kizazi kimoja tu kwa kuwekeza kwa Walimu wa watoto wetu kuanzia ngazi za chini; let us derisk the Nation, let us build the foundation, education at early age is the foundation.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja ya Waziri wa Elimu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili nami niweze kuchangia. Kwanza kabisa naomba kumpongeza Mheshimiwa Waziri, dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu na Naibu Waziri wake, Mheshimiwa Kigwangalla kwa hotuba yao nzuri na kwa kazi nzuri ambazo wanakuwa wakiwafanyia Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujielekeza moja kwa moja katika mchango wangu. Kwanza kabisa naomba kuzungumzia Bima ya Afya, nazungumzia Bima ya Afya kwa vijana wajasiriamali. Vijana ambao wanafanya kazi kwenye maofisi huwa wanawekewa ulazima wa kukatwa asilimia fulani katika mishahara yao ambayo inawapelekea kupata Bima ya Afya; lakini kwa vijana wajasiriamali hakuna kitu kama hiki, ni baadhi ambao wanakuwa na uelewa au wanakuwa na mwamko wa kujua nini faida ya Bima ya Afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia nguvu kazi ya Tanzania ni vijana na wanaofanya kazi ni takriban milioni 23 ya Watanzania. Wajasiriamali ninaowazungumzia hapa ni wale madereva wa bodaboda, mama lishe, fundi ujenzi, mafundi vyerehani, ndiyo ninaowazungumzia hapa. Wengi hawajajiunga na Mifuko au Bima za Afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kuzungumzia ni kwamba, naiomba Wizara iiombe Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ishuke chini kwa hawa vijana wajasiriamali, itoe elimu kubwa kuhusiana na Bima ya Afya, iwaambie faida ya Bima ya Afya ni nini? Leo dereva wa boda boda ukimwambia achange sh. 50,000/= kila mwezi anaona pesa yake inapotea, haelewi umuhimu ni nini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii Mifuko yetu ya hifadhi ikishuka chini kwa hawa vijana wajasiriamali ikawaelezea umuhimu, ikawaambia kwamba unapojiunga na Mfuko wa Hifadhi, automatically unapata Bima ya Afya, NHIF.
Hii itakuwa ni rahisi zaidi kwa wao kuelewa tofauti na kumwambia yeye achange kila mwezi sh. 50,000/= au sh. 100,000/= na kadhalika, inakuwa ni ngumu. (Makofi)
Ndugu zangu, tuelewe tu, tuwawezeshe wajasiriamali waelewe kwa sababu kijana wa leo mjasiriamali anapoumwa anapokwenda hospitali ndipo mtaji wake unapomalizika. Dereva boda boda anapata ajali, anavunjika mguu, anaambiwa kutibiwa kwake ni shilingi milioni tatu, nne mpaka tano, huo ndiyo mtaji wake aliutafuta kwa miezi kadhaa. Anapokuwa na Bima ya Afya inamsaidia yeye kupata matibabu bila kuumiza ule mtaji ambao alikuwa ameuweka kwa muda mrefu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ninalotaka kuzungumzia ni mimba za utotoni. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri kataja baadhi ya mikoa kama sita, kataja Mkoa wa Mara, Shinyanga, Geita, Singida na Dodoma kwamba ndiyo imeathirika kwa kiasi kikubwa na mimba ya utotoni. Naomba kumwambia dada yangu na kaka yangu, mimba za utotoni zimeathiri karibu Tanzania nzima. Suala hili lipo katika kila mkoa, linawagusa watu wengi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna adhabu zimekuwa zikitolewa kwamba ukimpa mimba mtoto wa kuanzia mwaka mmoja mpaka miaka nane, unafungwa maisha.
(Hapa baadhi ya Waheshimiwa Wabunge walinong’ona)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuanzia tisa mpaka kuendelea chini ya miaka 18, wengine wanaichukulia kama ubakaji wanasema au mapenzi. Unamkuta baba mwenye umri wa miaka 35, 40, 43 au 50 anakuja kumshawishi binti mdogo mwenye umri wa miaka 15, anampatia ujauzito. Kwa maisha yetu ya kawaida binti mwenye miaka 15 anakuwa bado ni mwanafunzi, kwa hiyo, anamwachisha shule kwa ajili ya ule ujauzito. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba adhabu kali itumike kukabiliana na hawa akinabab. Mara nyingi unamkuta mtu mwenye miaka 45, ni mfanyakazi TRA, ni Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, lakini anamharibia maisha huyu binti mwenye miaka kumi na tano. Tunajuaje huyu binti leo angekuwa Waziri kama dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu? Baadaye huko, tunajuaje labda leo angekuwa Makamu wa Rais kama Mheshimiwa Samia Suluhu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi naomba sana Wizara ya Afya ifikirie ni adhabu gani au mkakati gani itakuja nao kuweza kuwadhibiti hawa akina baba wanaotuharibia watoto wetu wadogo ambao hawajamaliza masomo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine na suala langu la mwisho, nataka kuzungumzia madawa ya kulevya. Tanzania yetu nikizungumzia Mkoa wa Dar es Salaam; kituo kinachotoa dawa kwa ambao wameathirika na madawa ya kulevya, ni Mwananyamala pekee. Hakuna kituo kingine! Ukienda pale Mwananyamala utalia, utasikitika, utawaonea huruma. Kama Mkoa wa Dar es Salaam ndiyo mkoa mkubwa ambao unaathirika; ndiyo kuna waathirika wakubwa wa madawa ya kulevya. Kuna kituo kimoja ambacho ndiyo cha Mwananyamala, foleni ni ya kufa mtu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba Wizara ione itafanyaje kuunda mfumo katika kila Kanda kuweka hivi vituo vya kutoa huduma za hawa walioathirika na madawa ya kulevya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hiyo tu, naomba Wizara ije na mfumo wa Rehabilitation Centers kwa hawa ambao wameathirika na madawa ya kulevya. Siyo madawa ya kulevya tu, kuna wagonjwa wa akili, wavutaji sigara ambao ni walevi kupitiliza. Mtu mwenye madawa ya kulevya leo, anaenda Mwananyamala, anapewa pesa, anarudi Mtaani. Atarudi kila siku Mwananyamala kuomba pesa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutafute hizi rehabilitation ambazo mtu anakuwa anahudumiwa, akitoka pale anapelekwa kule anakaa kwa kipindi fulani, akija kutoka tayari ameshaachana na kile kitu ambacho kilikuwa kikimsumbua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile naomba Wizara itoe mwamko kwa hizi rehabilitation centers za watu binafsi. Kuna moja ipo Bagamoyo ambako amepelekwa Chid Benz, kuna moja ambayo ipo Kigamboni; basi tuwashike mkono, tuwatie moyo, tuweze kuwaongezea ili wawasaidie vijana wetu. Kama sisi wenyewe tumeshindwa kuanzisha, wamepatikana watu kama hao, wana moyo wa kusaidia vijana, tuwashike mkono, tuwape msaada waweze kuwasaidia vijana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri suala la madawa ya kulevya analifahamu, linaumiza sana vijana, linaumiza nguvu kazi ya Taifa na wote tunatambua kwamba vijana ni nguvu kazi ya Taifa. Naomba litiliwe sana mkazo, atakapokuja kutoa hitimisho lake na useme nia yenu ama mfumo wenu ni upi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo machache, nakushukuru na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye mchango wangu. Leo nilivyokuwa nikijiandaa kuchangia niliona ni vyema kupitia Ilani za Uchaguzi za vyama vitatu vilivyoweka wagombea wa Urais mwaka 2015 ili kuona sintofahamu ambayo imekuwa ikitokea mara kadhaa hasa hasa humu Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu ambacho nimekiona ni jambo moja kubwa tu kwamba hatupaswi kushambuliana kwa sababu Mheshimiwa Rais anafanya mambo ambayo hata wapinzani walipaswa kumpongeza. Leo nitatoa mifano kadhaa kudhibitisha hili, naomba mnisikilize kwa makini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano wa kwanza Shirika la Ndege la Kitaifa; katika Ilani ya Uchaguzi wa CCM aya ya 41 tuliahidi naomba kunukuu

“Katika kipindi cha miaka mitano ijayo Chama cha Mapinduzi kitaielekeza Serikali kufanya mambo yafuatayo; kuimarisha huduma za Shirika la Ndege la Taifa.” mwisho wa kunukuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Ilani ya Chama cha UKAWA, ukurasa wa 40 eneo la miundombinu walisema naomba kunukuu:

“Kujenga Shirika la Ndege la Taifa linalojiendesha kwa misingi ya faida.” mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Ilani ya Uchaguzi ya ACT Wazalendo, aya ya 5.23, ukurasa wa 20 waliahidi naomba kunukuu:

“Kuunda upya Shirika la Ndege la Taifa ili iwe chachu ya kuongeza mapato ya fedha za kigeni nchini”. Mwisho wa kunukuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais amehakikisha anafufua Shirika la ATCL kwa kununua ndege sita ili kuongeza njia, kukuza biashara, kupata faida na mapato ya fedha za kigeni. Rais ametekeleza Ilani ya CCM, UKAWA na ACT Wazalendo kwa mpigo, haunganishi nchi huyu? Anaunganisha jamani. (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimwa Mwenyekiti, mfano wa pili ni reli, Ilani ya Uchaguzi wa CCM ukurasa wa 56 tuliahidi naomba kunukuu:

“Kuanza ujenzi wa reli zifuatazo kwa kiwango cha Kimataifa (standard gauge) kama ifuatavyo:- Dar es Salaam, Tabora, Kigoma, Mwanza, Uvinza, Msogati, Burundi na Isaka mpaka Kigali Rwanda, Mtwara, Songea, Mbambabay na matawi ya kwenda Mchuchuma na Liganga, Tanga, Arusha, Musoma, Kaliuwa, Mpanda, Kalema”.

Ilani ya uchaguzi ya CHADEMA, ukurasa wa 40 waliahidi, nanukuu:

“Kujenga reli mpya kukarabati zilizopo kwa viwango vya kisasa.” Mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais amehakikisha ujenzi wa reli ya kisasa ya kimataifa umeanza. Rais ametekeleza matakwa ya CCM na ya UKAWA, Rais anaunganisha nchi, huu sio muda muafaka wa kumpinga Rais, huu ni muda muafaka wa kumuunga mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa ushauri kwa ndugu zangu wapinzani waibue masuala mapya yale waliyokuwa wakisema kila mwaka tumepata Rais ambaye anayatekeleza. Haitakuwa mbaya wao wakiona wameishiwa hoja wafunge milango, wahamie kwetu, haitakuwa mara ya kwanza wala hakuna atakayewacheka. (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema miaka ya 1960 kuna chama kinaitwa United Tanganyika Party, waliokuwa enzi hizo watakijua, kilifunga ofisi kikahamia TANU kwa kuonekana hawana hoja za msingi. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1963 kulikuwa kuna Chama kinaitwa ANC cha Zuberi Mtemvu mtakuwa mnakijua miaka hiyo kilifunga ofisi na kuhamia TANU kwa kuwa hakikuwa na hoja. Kwa hiyo na wao kama hawana hoja mpya, tunawakaribisha CCM, tujenge nchi na tutawapokea vizuri kwenye Ukumbi wa JK, barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wetu anafanya kazi kwa bidii, anajitahidi huu sio muda muafaka wa wao kumbeza, kumdharau, kumdhoofisha badala yake ni kumuunga mkono kwa bidii na Rais anatekeleza matakwa ya Watanzania wote inapokuja suala zima la maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia bajeti ya makadirio ya Serikali ya mwaka wa fedha mwaka 2019/2020

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii ya nne ya Serikali ya Awamu ya Tano, imeonesha msimamo madhubuti wa Serikali ya Chama cha Mapinduzi chini ya Mwenyekiti wetu Rais John Pombe Magufuli kwa kuendeleza miundombinu ya msingi ili kuwezesha uchumi imara.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana wakati nachangia Bajeti Kuu ya Serikali nilizungumzia umuhimu wa kutengeneza mazingira mazuri kwa ajili ya vijana kujiajiri. Nimefurahishwa sana na uamuzi wa Serikali wa kuamua kufuta kodi kwa muda wa miezi sita; suala hili litapelekea vijana kupata chachu kubwa ya kuweza kujiajiri. Natoa wito kwa vijana wote nchini kuchukua fursa hii; Serikali ina mifuko mbalimbali inayosaidia vijana kutoa mitaji. Mpaka sasa Serikali kupitia vikundi vinavyoendeleza vijana vikundi 775 vimeshapewa mitaji jumla ya bilioni 4.2, kwa hiyo naipongeza sana Serikali yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili Mheshimiwa Waziri wa Fedha nakuomba kwa unyenyekevu mkubwa; nimesema mara kadhaa hapa Bungeni kwamba Mkoa wa Kagera ndio mkoa pekee unaopakana na nchi nyingi Afrika Mashariki. Mkoa wa Kagera unapakana nan chi za Uganda, Rwanda pamoja na Burundi. Vilevile kupitia Ziwa Victoria Mkoa wa Kagera unaifikia Kenya. Nilikuwa naiomba Serikali yangu sikivu ije na mkakati wa makusudi wa kuufanya Mkoa wa Kagera kuwa kituo kikubwa cha biashara. Najua sasa hivi Serikali inatekeleza miradi mikubwa kama barabara, reli na umeme, lakini pia hili la biashara ni kubwa kwa sababu itapelekea nchi yetu kunufaika zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa juhudi anazozifanya kutokana na kupinga suala zima la rushwa. Hapo zamani tulipata kusikia kwamba kuna kipindi bajeti ya Serikali asilimia 30 ilipotea kupitia manunuzi. Kwa sasahivi hadithi hii haipo fedha zikipangwa kwenda kwenye shughuli za umma zinafika kwenye shughuli za umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumalizia kwa hadithi moja, hii hadithi inasikika sana TBC, nadhani wengi wetu tunaijua. Kwamba kulikuwa kuna binti mfalme yupo kilimani kunahitajika mchumba kwenda kumuoa, na sharti lilikuwa, utakapokuwa unakwenda chochote utakachokisikia usigeuke nyuma, pembeni wala nyuma. Kwa hiyo watu wakawa wanapita wakifika katikati wanasikia woowoowoo akigeuka kushoto, kulia anageuka jiwe, kushoto kulia anageuka jiwe. Sasa kuna kijana mmoja ambaye alikuwa jasiri yeye hakugeuka nyuma alitembea moja kwa moja mpaka kule kilimani akamfikia huyo binti mfalme.

Waheshimiwa Wabunge nataka niwaambie kiongozi bora ni yule anayesimamia anachokiamini. Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli huu ni mwaka wa nne sasa amesimamia kwenye miradi mikubwa anayoitengeneza. Hajatikiswa na kelele za ndani wala za nje, yeye amesimama imara anaelekea kule kukamilisha miradi yake mikubwa, anaenda kumfata binti mfalme, binti mfalme huyo ndiye Tanzania ya viwanda; kwamba atakapokamilisha miradi hii Tanzania ya viwanda itakuwepo. Kwa hiyo naomba sana kumpongeza Mheshimiwa Rais na aendelee na msimamo wake huo na nina wapongeza Mawaziri wote wanaomuwezesha yeye kufikisha lengo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru.