Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Elias John Kwandikwa (132 total)

MHE. MARWA R. CHACHA aliuliza:-
Katika bajeti ya 2016/2017 kipande cha barabara (Mugumu – Nata), ni barabara pekee inayounganisha Mkoa wa Mara na Arusha, kilitengewa fedha shilingi bilioni 12; tangazo la zabuni ya barabara lilitoka mara tatu na mwishoni mkandarasi wa kujenga barabara hiyo akapatikana, lakini Serikali ilikataa kusaini mkataba kwa maelezo kwamba Serikali haina fedha wakati fedha zilitengwa kwenye bajeti.
(b) Je, ni kwa nini Serikali haioni umuhimu wa barabara hii ambayo iko kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM?
(c) Je, Serikali inawaambia nini wananchi wa Mkoa wa Mara kuhusu ujenzi wa barabara hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hii ni mara yangu ya kwanza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu, naomba uniruhusu nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa rehema zake, na nimshukuru kipekee Mheshimiwa Rais kwa kuniteua ili niweze kutumika kama Naibu Waziri wa Ujenzi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Marwa Ryoba Chacha, Mbunge wa Serengeti, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara hii tayari imeshaiweka kwenye mpango wa ujenzi kwa kiwango cha lami barabara hii ya Mugumu – Nata yenye urefu wa kilimotea 41.725 na barabara ya kuunganisha Mji wa Mugumu zenye urefu wa kilometa 1.575 kwa kukamilisha usanifu wa kina na nyaraka za zabuni.
Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya uhakiki wa fidia ya mali za wananchi zitakazoathiriwa na ujenzi wa barabara ya Mugumu – Nata na tathmini hiyo imeshapelekwa kwa Mthamini Mkuu wa Serikali kwa mapitio na kuidhinishwa ili hatimaye malipo ya fidia kwa wananchi yafanyike.
Mheshimiwa Spika, Serikali ilishaanza taratibu za ununuzi kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo, hivyo, baada ya malipo ya fidia kufanyika, taratibu za kumpata mkandarasi zitakamilishwa ili ujenzi kwa kiwango cha lami uanze. Aidha, kwa sasa Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) inaendelea kuifanyia matengenezo barabara ya Mugumu – Nata ili iweze kupitika majira yote ya mwaka.
MHE. DEO K. SANGA aliuliza:-
Bomba la mafuta la kwenda Zambia limepita katikati ya Mji wa Makambako na barabara ambayo ipo juu ya bomba hilo hairuhusiwi kutengenezwa hivyo kuwa na mashimo mengi na kuhatarisha maisha ya watu wanaoitumia barabara hiyo.
(i) Je, ni lini Serikali italihamisha bomba hilo?
(ii) Je, kwa nini barabara hiyo isitengenezwe, ili wananchi waendelee kupita kwa urahisi wakati Serikali inajipanga kulihamisha bomba la mafuta?
NAIBU WAZIRI UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga, Mbunge wa Makambako, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua usumbufu wanaopata wananchi wa Makambako kutokana na bomba la mafuta kwenda Zambia (TAZAMA) linalopita katika Mji wa Makambako. Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) inawasiliana na Kampuni ya Tanzania na Zambia ya kusafirisha mafuta kutoka Tanzania kwenda Zambia (TAZAMA Pipeline Limited) kuainisha hatua stahiki zitakazochukuliwa kuondoa tatizo hilo. Wakati mawasiliano yanafanyika pamoja na kuainisha hatua za gharama zitakazotumika, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania itatengeneza maeneo yaliyoharibika, ili wananchi waweze kutumia barabara hiyo bila matatizo.
MHE. MARTHA J. UMBULLA aliuliza:-
Barabara ya kutoka Kibaya, Wilayani Kiteto kwenda Ranchi ya NARCO iliyoko Kongwa inaharibiwa na magari makubwa yanayobeba mahindi kutoka Kiteto kwenda soko maarufu la Kibaigwa, Kongwa na Serikali ilishaahidi kuijenga kwa kiwango cha lami. Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hiyo?
NAIBU WAZIRI UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Martha Jachi Umbulla, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Arusha – Kibaya – Kongwa ina urefu wa kilometa 430. Barabara hii inaunganisha Mikoa ya Arusha, Manyara na Dodoma, na lengo la Serikali ni kuijenga kwa kiwango cha lami. Barabara hii itakapokamilika itarahisisha usafirishaji wa mazao na mifugo katika Mikoa ya Arusha, Manyara na Dodoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2016/2017 na 2017/2018 Serikali imetenga jumla ya shilingi 1,350,000,000 kwa ajili ya kufanya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara hii. Aidha, mnamo tarehe 21 Aprili, 2017 Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) imesaini mkataba na Mhandisi Mshauri Kampuni ya Cheil Engineering Company Limited kutoka Korea ya Kusini ikishirikiana na Kampuni ya Inter-consult ya Tanzania kufanya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na kuikamilisha katika kipindi cha miezi 21.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya usanifu itakapokamilika na kujua gharama halisi za mradi Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami. Aidha, Serikali kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) inaendelea kuifanyia matengenezo ya aina mbalimbali barabara hii, ili iendelee kupitika kwa urahisi wakati tunaendelea na maandalizi ya kuijenga kwa kiwango cha lami.
MHE. ALBERT O. NTABALIBA aliuliza:-
Soko la Kimataifa la Mnanila – Buhigwe lilikuwa kwenye mpango wa kujengwa mwaka 2012/2013, lakini hadi sasa soko hilo halijajengwa. Je, ni lini soko hilo litajengwa?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, naomba nitangulie kumjibu Mheshimiwa Albert Obama na nichukue fursa hii kutambua na kumpongeza Mheshimiwa Mbunge huyo kwa juhudi zake za kufuatilia maendeleo ya ujenzi wa Soko la Mnanila– Buhigwe. Mheshimiwa Obama pia aliwahi kuuliza swali kama hili ambalo lilijibiwa Juni, 2015.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyokuwa nimeeleza katika jibu langu la awali, Serikali kupitia Mradi wa Uwekezaji wa Sekta ya Kilimo Wilayani (District Agriculture Sector Investments Project - DASIP) ilipanga kujenga masoko saba ya mpakani katika maeneo ya Mnanila - Buhigwe, Mutukula - Misenyi, Kabanga - Ngara, Nkwenda - Kyerwa na Muronga - Kyerwa, Remagwe - Tarime na Busoka - Kahama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo ujenzi wa masoko mawili ya Mnanila na Mutukula haukuingia katika mpango wa ujenzi wa masoko hayo kutokana na kucheleweshwa kwa taratibu za malipo ya fidia kwa wananchi. Mradi wa DASIP ulihitimishwa mwaka 2013/2014 na masoko matano yaliyokuwa yanajengwa yalikamilika kwa kiwango cha kati ya asilimia 40 mpaka 60. Wizara ya Kilimo ambayo ndio ilikuwa inasimamia mradi wa DASIP inaendelea na juhudi za kukamilisha ujenzi wa masoko hayo kwa kutumia vyanzo vya ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na Mradi wa DASIP kufikia ukomo Serikali inaishauri Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe kuingiza ujenzi wa soko hilo katika Mpango wa Maendeleo na Bajeti ya Halmashauri ili kufanikisha ujenzi wa soko hilo na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji itaendelea kutafuta wahisani wa maendeleo, ili kujenga soko la mpakani eneo la Mnanila.
MHE. MBARAKA K. DAU aliuliza:-
Serikali imekamilisha ujenzi wa barabara ya kuruka ndege katika Uwanja wa Ndege Mafia kwa awamu ya kwanza kwa ufadhili wa Mfuko wa Millenium Challenge Account (MCA).
Je, ni lini Serikali itajenga jengo la abiria na kuweka taa za kurukia kwenye uwanja huo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbaraka Kitwana Dau, Mbunge wa Mafia kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, mradi wa ukarabati na upanuzi wa kiwanja cha ndege cha Mafia uliofadhiliwa na Shirika la Changamoto za Milenia la Serikali ya Marekani na kutekelezwa kupitia Mfuko wa Changamoto za Milenia Tanzania (Millennium Challenge Account – Tanzania) ulikamilika mwaka 2013. Mradi huo haukuhusisha ujenzi wa jengo jipya la abiria, barabara ya kuingia kiwanjani, maegesho mapya ya magari, maegesho mapya ya ndege (apron), barabara za viungio (taxiways) pamoja na usimikaji wa taa na mitambo ya kuongeza ndege wakati wa kutua.
Mheshimiwa Spika, kazi zilizosalia ambazo usanifu wa kina ulifanyika katika mradi wa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina uliohusisha viwanja saba kwa fedha za Benki ya Dunia na kukamilika mwaka 2009 hazijaanza kutekelezwa. Serikali inaendelea na jitihada za kutafuta fedha kutoka vyanzo mbalimbali, zikiwemo fedha za ndani na washirika wa maendeleo, kwa ajili ya kukamilisha kazi zilizosalia.
Mheshimiwa Spika, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa Serikali inatambua umuhimu wa Kiwanja cha Ndege cha Mafia kwa Wilaya ya Mafia kwa kuwa kutokana na jiografia yake kisiwa hiki kinategemea zaidi kiwanja hiki katika kuchochea shughuli za uchumi zikiwemo utalii. Hivyo, Serikali itaendelea kutafuta fedha ili kuweza kukamilisha ujenzi wa kiwanja hiki.
MHE. JOHN J. MNYIKA aliuliza:-
Eneo la hifadhi ya barabara ya Morogoro katika Jimbo la Kibamba ni pana kuliko barabara kuu nyingine nchini na inaingia katika makazi ya asili ya wananchi.
(a) Je, ni lini Serikali itawalipa wananchi fidia kwa ardhi ya asili ya tangu kabla ya uhuru ambao walihamia wakati wa vijiji vya ujamaa?
(b) Je, ni lini Serikali itawasilisha Muswada wa Marekebisho ya Sheria husika ili eneo la hifadhi ya barabara iwiane na barabara kuu nyingine nchini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa John John Mnyika, Mbunge wa Jimbo la Kibamba, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Barabara ya mwaka 1932 (The Highway Ordinance Cap.167) kifungu namba 52 eneo la hifadhi ya barabara ya Morogoro kuanzia maili 10.02 yaani kilometa 16 kutoka Posta ya Zamani mpaka maili 23.12 yaani kilometa 37 ni futi 400 ambazo ni sawa na takribani mita 120 kila upande kutoka katikati ya barabara. Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kupitia TANROADS imeweka nguzo za kuonesha mipaka ya eneo la hifadhi ya barabara katika eneo tajwa na maeneo mengine nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya barabara ya Morogorio kati ya kilometa 16 na kilometa 37 iko ndani ya Jimbo la Kibamba ambapo hifadhi ya barabara ni mita 120 kila upande kutoka katikati ya barabara. Hivyo Serikali haitalipa fidia kwa mwananchi yoyote wa Jimbo la Kibamba aliyejenga au aliyefanya maendelezo yoyote ndani ya eneo la hifadhi ya barabara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haina mpango wa kuwasilisha Muswada wa Marekebisho ya Sheria ili kufanya eneo la hifadhi ya barabara Morogoro liwiane na barabara kuu nyingine nchini kwa kuwa eneo la hifadhi ya barabara ya Morogoro lililotengwa linahitajika kwa ajili ya upanuzi wa barabara ili kuwaiana na mahitaji ya sasa na ya miaka ijayo.
MHE. FELISTER A. BURA aliuliza:-
Wakati wa Kampeni za Uchaguzi Mkuu mwaka 2015 aliyekuwa mgombea Urais kupitia tiketi ya CCM Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliwaahidi wananchi wa Kongwa na Mpwapwa kujenga barabara ya Mbande – Kongwa - Mpwapwa kwa kiwango cha lami. Je, ni lini barabara hiyo itaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Felister Aloyce Bura, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Mbande – Kongwa – Mpwapwa yenye urefu wa kilometa 49.19 ilifanyiwa usanifu wa kina kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami na usanifu ulikamilika mwaka 2013. Baada ya kukamilika kwa usanifu Serikali imeanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami kwa awamu ambapo mwezi Julai, 2017 sehemu ya barabara yenye urefu wa kilometa 11.7 kutoka Mbande kuelekea Kongwa ilianza kujengwa. Hadi mwishoni wa mwezi Oktoba, 2017 kiasi cha kilometa tano za sehemu ya barabara ya Mbande - Kongwa zimekamilika kujenga hadi tabaka la juu (basic course). Mkandarasi anaendelea na kazi ya ujenzi kwa kiwango cha lami.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA aliuliza:-
Serikali ilipanga kujenga na kupanua Uwanja wa Ndege wa Sumbawanga Mjini:-
Je, ni lini ujenzi huo utakamilika pamoja na kuwalipa fidia wananchi wanaozunguka uwanja huo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa ukarabati wa uwanja wa ndege wa Sumbawanga upo kwenye hatua ya manunuzi. Mkataba wa usimamizi wa kazi ya ujenzi ulitiwa saini baina ya Serikali na kampuni ya SMEC kutoka Australia mwezi Oktoba, 2016.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Mwezi Juni, 2017 Serikali ilitiliana saini mkataba wa ujenzi wa ukarabati wa uwanja huo na Kampuni ya Sino-Shine Overseas Construction and Investment East Africa Limited kutoka Nchini China. Utekelezaji wa mradi huo utakapoanza unategemewa kukamilika ndani ya miezi 18. Kazi ya ujenzi wa uwanja huo zitaanza mara baada ya Serikali kukamilisha taratibu za malipo ya fidia kwa wananchi wanaostahili kulipwa ili waondoke kupisha ujenzi wa uwanja.
Mheshimiwa Naibu Spika, maandalizi ya ulipaji wa fidia kwa wananchi watakaoathirika na mradi huo yapo katika hatua ya uhakiki wa mwisho kabla ya ulipaji wa fidia kuanza.
MHE. KEMIREMBE J. LWOTA aliuliza:-
Je, ni lini ujenzi wa Daraja la Kigongo Busisi utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kemirembe Julius Lwota, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mradi wa ujenzi wa Daraja la Kigongo – Busisi pamoja na barabara unganishi unatekelezwa katika hatua mbili. Hatua ya kwanza, ambayo tayari upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na uandaaji wa nyaraka za zabuni. Upembuzi yakinifu ulikamilika tarehe 11 Julai, 2017. Aidha, kwa sasa Mhandisi Mshauri ambaye ni Kampuni ya Cheil Engineering Ltd kutoka Korea Kusini akishirikiana na AFRISA Consultant pamoja na Apex za Tanzania anaendelea na kazi ya usanifu wa kina na kuandaa nyaraka za zabuni. Kazi ya usanifu wa kina zimepangwa kukamilika mwezi Julai, 2018 kwa gharama ya shilingi bilioni 2.8.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kukamilika kwa kazi ya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na uandaaji wa nyaraka za zabuni gharama halisi za ujenzi wa daraja zitafahamika. Baada ya gharama kufahamika, Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa daraja hilo.
MHE. JESCA D. KISHOA aliuliza:-
Mkoa wa Singida kwa sasa ni mkoa wa kimkakati, hasa kufuatia kazi ya kuleta Makao Makuu Dodoma.
Je, ni lini Serikali itahakikisha mkoa huo unapata uwanja wa ndege hasa kutokana na umuhimu wake?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jesca David Kishoa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuboresha uwanja wa ndege wa Singida. Kutokana na umuhimu huo, Serikali ya Awamu ya Tano tayari imechukua hatua za kuwezesha kuimarisha uwanja wa ndege wa Singida ambapo hadi kufikia mwezi Mei, 2017 imekamilisha upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na kuandaa makabrasha ya zabuni kwa ajili ya kufanya ukarabati na upanuzi wa uwanja huo kwa kiwango cha lami. Uwanja wa ndege wa Singida ni miongoni mwa viwanja 11 vya ndege vilivyopata ufadhili wa Benki ya Dunia katika hatua ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa mradi wa uboreshaji wa viwanja hivyo. Viwanja vingine ni Lake Manyara, Musoma, Iringa, Tanga, Songea, Kilwa Masoko, Lindi, Moshi, Njombe na Simiyu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kukamilika kwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina niliourejea hapo juu, Serikali imeanza kutafuta fedha kutoka katika vyanzo mbalimbali kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa viwanja hivyo ukiwemo uwanja wa ndege wa Singida. Mradi huo ukikamilika utawezesha kuruka na kutua ndege kubwa zenye uwezo wa kubeba takribani abiria 70. Aidha, kazi ya ukarabati na upanuzi zitahusisha ujenzi wa jengo la abiria, jengo la mawasiliano na kuongozea ndege, kituo cha hali ya hewa pamoja na miundombinu mingine. Utekelezaji wa mradi huu utaanza mara tu fedha za mradi huu zitakapopatikana.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY aliuliza:-
Wilaya ya Mbulu haina barabara ya lami kutokana na kuzungukwa na Bonde la Ufa kuanzia Karatu, Mto wa Mbu, Babati – Hanang hivyo, kufanya magari makubwa kutoka Uganda, Kenya na Dar es Salaam kuzunguka umbali mkubwa ili kufika Mbulu Mjini.
Je, Serikali ina mpngo gani wa kutekeleza ahadi yake ya kuweka lami katika barabara ya Karatu – Mbulu – Hydom - Mkalama – Lalago Shinyanga ili kurahisisha usafiri katika njia hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia Paul Issaay, Mbunge wa Mbulu Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Karatu – Mbulu - Hydom – Mkalama – Lalago – Kolandoto, yenye urefu wa kilometa 389 ni kiungo muhimu kwa Mikoa ya Arusha, Manyara, Mara, Shinyanga na Singida kwa kupitia Kusini mwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kuwa barabara hii ina umuhimu mkubwa wa kiuchumi na kijamii na ni kiungo muhimu kati ya Mikoa ya Arusha, Manyara, Mara, Shinyanga na Singida. Maandalizi ya ujenzi kiwango cha lami ya barabara hii yameanza kwa hatua za awali, ambapo Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) imeingia mkataba na Mhandisi Mshauri aitwaye HP Gauff Ingenieure GmbH & Co. KG – JBG ya Ujerumani ili kufanya kazi ya upembuzi yakinifu ambayo inaendelea hadi sasa. Kazi hii inagharamiwa na Serikali ya Ujerumani kupitia Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW).
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, baada ya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kukamilika, Serikali itatafuta fedha na kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami.
MHE. ANDREW J. CHENGE aliuliza:-
Sera ya Serikali ni kuunganisha Makao Makuu ya Mikoa kwa barabara za kiwango cha lami. Mkoa wa Simiyu haujaunganishwa na mikoa jirani ya Singida na Arusha.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina barabara ya Bariadi – Kisesa – Mwanhuzi hadi Daraja la Mto Sibiti na hatimaye ijengwe kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Andrew Chenge, Mbunge wa Bariadi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeshaanza juhudi za kuunganisha Mkoa wa Simiyu na Mikoa jirani ya Singida na Arusha kwa kufanya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa mchepuo wa kusini wa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti (Serengeti Southern Bypass). Upembuzi yakinifu unajumuisha barabara ya Karatu – Sibiti kupitia Mbulu na Karatu kupitia Ziwa Eyasi hadi Sibiti – Mwanhuzi – Lalago hadi Maswa. Matokeo ya mapendekezo ya njia ipi ya kupita yatapatikana kazi hii itakapokamilika katika mwaka wa 2018. Kazi hii inafadhiliwa na Serikali ya Ujerumani kupitia Benki yake ya Maendeleo (KfW).
Aidha, upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa barabara ya Kolandoto Junction – Lalago – Mwanhuzi – Sibiti
– Oldean Junction (kilometa 328) umekamilika ikiwemo sehemu ya barabara kuu ya Ng’oboko – Mwanhuzi hadi daraja la Sibiti. Kazi hii imegharamiwa na Serikali ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Bariadi – Kisesa Mwanhuzi hadi daraja la Sibiti imegawanyika katika sehemu mbili kama ifuatavyo: sehemu ya kwanza ni barabara ya Mkoa wa Baliadi - Kisesa – Mwandoya hadi Ng’oboko yenye urefu wa kilometa 100.71 inavyoungana na barabara kuu ya Kolandoto – Lalago – Mwanhuzi hadi Daraja la Sibiti. Sehemu ya pili ni sehemu ya barabara kuu kuanzia Ng’oboko – Mwanhuzi hadi daraja la Sibiti yenye urefu wa kilometa 79.1.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi sasa ujenzi wa daraja la mto Sibiti lenye urefu wa mita 82 pamoja na barabara unganishi (kilometa 25) unaendelea na unatarajiwa kukamilika katika mwaka wa fedha 2018/2019.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Bariadi – Kisesa - Mwandoya – Ng’oboko (kilometa 105) pamoja na Sibiti – Mkalama – Nduguti – Iguguno hadi Singida (kilometa 103.54) ziko kwenye mpango mkakati wa miaka mitano kwa ajili ya kufanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi hizo tajwa za usanifu zikikamilika, Serikali itatafuta fedha za kujenga barabara zote kwa kiwango cha lami kwa awamu na kulingana na upatikanaji wa fedha. Hivyo, Makao Makuu ya Mikoa ya Simiyu, Arusha na Singida yatakuwa yameunganishwa.
MHE. AJALI R. AKBAR aliuliza:-
Wilaya ya Newala ni Wilaya kongwe ambayo hata utawala wa Wajerumani ulizingatia mpango bora wa matumizi ya ardhi ambao Wilaya hiyo imepangwa tangu enzi lakini hivi karibuni TANROADS wamefanya upanuzi wa barabara ulioelekea hadi Chitandi – Masasi.
Je, kwa nini Serikali kupitia TANROADS Mtwara isifanye tathmini ya nyumba za wakazi hao na kuwalipa fidia?
MHE. AJALI R. AKBAR aliuliza:-
Wilaya ya Newala ni Wilaya kongwe ambayo hata utawala wa Wajerumani ulizingatia mpango bora wa matumizi ya ardhi ambao Wilaya hiyo imepangwa tangu enzi lakini hivi karibuni TANROADS wamefanya upanuzi wa barabara ulioelekea hadi Chitandi – Masasi.
Je, kwa nini Serikali kupitia TANROADS Mtwara isifanye tathmini ya nyumba za wakazi hao na kuwalipa fidia?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ajali Rashid Akbar, Mbunge wa Newala Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Mbuyuni – Makong’onda – Newala sehemu ya Chitandi – Masasi yenye urefu wa kilometa 41.55 ni barabara ya mkoa inayoungana na barabara ya Mkoa ya Mtwara – Newala – Masasi yenye urefu wa kilometa 221. Barabara hii ina upana wa eneo la Hifadhi ya Barabara ya mita 60. Kabla ya marekebisho kupitia Sheria ya Barabara ya mwaka 2007 upana wa eneo la hifadhi ulikuwa mita 45, yaani mita 22.5 kutoka katikati ya kila upande wa barabara. Sehemu ya barabara hii inapita katika milima mikali ya Makong’onda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, katika bajeti ya mwaka 2016/2017 ilitenga shilingi milioni 581.586 na mwaka 2017/2018 ilitenga shilingi milioni 396.437 kwa ajili ya kuboresha ahadi ya barabara kufikia kiwango cha lami katika milima ya Makong’onda na kupunguza ajali kwenye sehemu ya miteremko mikali. Jumla ya kilometa mbili za barabara katika milima Makong’onda zimejengwa kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na utekelezaji wa upanuzi wa barabara unaoendelea, Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) ilitoa notisi kwa wananchi wanaomiliki mali ndani ya mita 22.5 za eneo la hifadhi ya barabara ili waondoe mali zao na kuacha wazi eneo hilo kwa kuzingatia matakwa ya Sheria ya Barabara Namba 13 ya Mwaka 2007 na kanuni za mwaka 2009.
Aidha, kwa walio ndani ya mita 7.5 ambazo ni kutoka zinapoishia mita 22.5 za eneo la hifadhi ya barabara na mita 30 zilizoainishwa katika Sheria ya Barabara Namba 13 ya mwaka 2007, tathmini ya mali zao itafanyika pindi Serikali itakapohitaji maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutolewa notisi hizo, baadhi ya wananchi walipeleka malalamiko yao katika Mahakama ya Ardhi ya Kanda ya Mtwara kupinga kuondoa mali hizo ambapo hadi sasa shauri hilo bado liko Mahakamani. Taratibu za Kimahakama zitakapokamilika, Serikali itachukua hatua stahiki kwa kuzingatia uamuzi wa Mahakama.
MHE. SELEMANI J. ZEDI aliuliza:-
Barabara ya kuanzia Tabora - Mabali – Bukene – Itobo hadi Kahama ni muhmu sana kwa shughuli za kiuchumi kwa wananchi wa Jimbo la Bukene na barabara hii ipo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM.
Je, ni lini barabara hii yenye urefu wa kilometa 149 itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Selemani Jumanne Zedi, Mbunge wa Bukene, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Tabora – Mambali - Itobo yenye urefu wa kilometa 115 ni sehemu ya mradi wa barabara ya Tabora – Mambali - Itobo hadi Kagongwa Wilayani Kahama yenye urefu wa kilometa 180, inayounganisha Wilaya ya Tabora, Nzega na Kahama. Kwa sasa barabara hii inafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa ajili ya kujengwa kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkataba wa kazi hiyo ulisainiwa tarehe 14 Septemba, 2017 na ni wa miezi 15. Kazi hii inafanywa na Mhandisi Mshauri M/s Nimeta Consult kwa gharama ya shilingi milioni 789.205. Hadi sasa jumla ya shilingi milioni 608 zimeshatolewa kwa ajili ya kazi hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara hii utaanza baada ya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kukamilika kulingana na upatikanaji wa fedha. (Makofi)
MHE. DKT. STEPHEN L. KIRUSWA (K.n.y. MHE. CATHERINE MAGIGE) aliuliza:-
Serikali ilishatoa ahadi ya kujenga barabara ya Mto wa Mbu hadi Loliondo kwa kiwango cha lami.
Je, mchakato wa mradi huo umefikia hatua gani na ujenzi wake utaanza lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J.KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Catherine Valentine Magige, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Stephen kwa kuchaguliwa kuwa Mbunge na ninamtakia kila la heri katika kuwatumikia wananchi wa Longido. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa ujenzi wa barabara ya Mto wa Mbu – Longido kwa kiwango cha lami na imeshaanza kutekeleza ujenzi wa barabara hiyo kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Mkataba wa awamu ya kwanza ya ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara hii unaohusisha kilometa 49 kutoka Loliondo (Waso) hadi Njiapanda ya Sale tayari umesainiwa na utekelezaji ulianza tarehe 18, Oktoba, 2017. Ujenzi wa sehemu hii ya barabara unaotekelezwa na mhandisi aitwaye Ms China Wu Yi Co. Ltd. kwa gharama ya shilingi 87,126,445,712.35 unasimamiwa na TECU (TANROADS Engineering Consulting Unit). Mradi huu unaogharamiwa na Serikali ya Tanzania kwa asilimia 100 unatarajiwa kukamilika baada ya miezi 24.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kulihakikishia Bunge lako tukufu kuwa Wizara yangu itaendelea kutekeleza ahadi ya Serikali na miradi iliyowekwa katika Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015 ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. RITTA E. KABATI aliuliza:-
Kiwanja cha Ndege cha Nduli kipo katika mpango wa Serikali wa Ujenzi wa viwanja 11:-
(a) Je, ni lini kiwanja hicho kitajengwa?
(b) Mpaka sasa hakuna kituo cha kujaza mafuta katika kiwanja hicho; je, ni utaratibu gani unaotumika ili kiwepo kituo cha mafuta katika kiwanja hicho?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS JOHN KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:
(a) Kiwanja cha Ndege cha Nduli kililichopo Mkoani Iringa ni miongoni mwa viwanja 11 vya ndege vilivyofanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina uliomalizika mwezi Mei mwaka 2017. Katika mwaka wa fedha wa 2017/2018, Serikali ilitenga fedha za ndani kwa ajili ya maandalizi ya ujenzi wa kiwanja hicho ikiwa ni pamoja na kutangaza zabuni.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kutokana na Benki ya Dunia kuonesha nia ya kufadhili ujenzi wa uwanja huu, Serikali ilisitisha taratibu za ndani za manunuzi ili kusubiri manunuzi kufanyika kwa kuzingatia taratibu za Benki ya Dunia. Hivyo, uwanja huo utaanza kujengwa mara moja baada ya taratibu hizo kukamilika.
(b) Kwa sasa kiwanja hiki hakina ndege za kutosha zinazoweza kuvutia uwekezaji wa kituo cha mafuta. Ni vema ieleweke wazi kwamba sera ya uwekezaji katika viwanja vya ndege inatoa fursa ya kuuza mafuta ya ndege kwa makampuni binafsi yenye leseni ya Mamlaka ya Usafiri wa Anga TCAA.
Mheshimiwa Naibu Spika, Makampuni yenye leseni hizo na yaliyoingia mikataba ya biashara ya mafuta ya ndege na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania TAA ni Puma, Oilcom, Total na Prime fuels. Kwa hiyo, ni utashi wa makampuni ya mafuta na nguvu ya soko inayosukuma uwekezaji wa biashara ya mafuta katika viwanja vya ndege. Ni matumaini yangu kwamba kiwanja hiki kitakapokamilika kujengwa kitawavutia wawekezaji na hatimaye kumaliza tatizo hili.
MHE. HAROON M. PIRMOHAMED aliuliza:-
Barabara ya Rujewa – Madibira ni tegemeo na ni kiungo muhimu kati ya Rujewa – Madibira na Madibira – Mafinga na Serikali imekuwa ikitoa ahadi kwa muda mrefu kwamba itajengwa kwa kiwango cha lami. Je, ni lini sasa barabara hiyo itaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Haroon Mulla Pirmohamed, Mbunge wa Mbarali, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Rujewa – Madibira – Mafinga yenye urefu wa kilometa 152.1 ni barabara ya mkoa inayohudumiwa na Wakala wa Barabara nchini (TANROADS). Kazi ya usanifu wa kina na kuandaa nyaraka za zabuni kwa ajili ya kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami ilikamilika Agosti, 2012.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa sasa inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 kiasi cha shilingi bilioni 2.57 kilitengwa kwa ajili ya kuanza maandalizi ya ujenzi wa barabara hii. Aidha, kwa sasa Serikali itaendelea kuifanyia matengenezo ya aina mbalimbali barabara hii ili ipitike kirahisi kwa wakati wote wakati inatafuta fedha za kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI aliuliza:-
Uwepo wa mawasiliano ya uhakika kati ya Visiwa vya Ukerewe na Mkoa wa Mara ni muhimu kwa uchumi wa wananchi wa Ukerewe na hatua kadhaa zimeshachukuliwa kuhakikisha daraja kati ya Lugezi na Kisorya linajengwa. Je, ni hatua ipi inachukuliwa na Serikali kuhakikisha daraja hilo linajengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kabla sijajibu swali, naomba uniruhusu nami niungane na Waheshimiwa Wabunge wote kumshukuru Mungu kwa kukurejesha na afya njema. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Michael Mkundi, Mbunge wa Ukerewe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa kuimarisha mawasiliano kati ya visiwa vya Ukerewe na mikoa mingine, imefanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa barabara yote ya Nyamuswa – Bunda – Kisorya – Nansio (Ukerewe) yenye urefu wa kilometa 118.
Aidha, usanifu umejumuisha madaraja mawili ya Lugezi yenye urefu wa mita 600 na mita 450 yanayounganisha Kisorya na Nansio pamoja na maandalizi ya nyaraka za zabuni. Kazi ya usanifu imekamilika na ujenzi kwa kiwango cha lami kati ya Bulamba hadi Kisorya katika barabara hii unaendelea.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa barabara hiyo, pamoja na madaraja mawili kati ya Kisorya na Nansio ili kuunganisha Kisiwa cha Ukerewe na Mikoa ya Mara, Simiyu na Mwanza.
MHE. CECIL D. MWAMBE (K.n.y. MHE. JOHN J. MNYIKA) aliuliza:-
Ujenzi wa barabara za mzunguko/mchepuko kwa kiwango cha lami ni muhimu katika kupunguza msongamano kwenye barabara kuu ya Morogoro.
(a) Je, ni lini barabara ya Tangibovu – Kibaoni – Goba – Mbezi – Malamba Mawili – Kinyerezi utakamilika?
(b) Je, ni lini ujenzi kwa kiwango cha lami kwa barabara nyingine za mzunguko/mchepuko katika Jimbo la Kibamba utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John John Mnyika, Mbunge wa Kibamba, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua tatizo la msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam na kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano mnamo mwaka 2010 ilianza kutekeleza ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara za pete (ring roads) na zile za mchepuo.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara zinazojumuishwa kwenye mpango huo ambazo ziko katika Jimbo la Kibamba ni barabara za Bunju ‘B’ – Mipiji Magohe – Victoria – Kifuru hadi Pugu Kilitex yenye urefu wa kilometa 33.7 na barabara ya mchepuo ya Tangibovu – Goba – Mbezi Mwisho – Msigani
– Malambamawili – Kifuru – Kinyerezi hadi Banana, yenye urefu wa kilometa 26.
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa barabara ya mchepuo kuanzia Tangibovu – Goba – Mbezi Mwisho – Msigani – Malambamawili – Kifuru – Kinyerezi umetekelezwa kama ifuatavyo:-
(i) Ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara yenye urefu wa kilometa 16 kuanzia Tangibovu – Goba – Mbezi Mwisho umekamilika mwaka 2016;
(ii) Ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara yenye urefu wa kilometa nane kuanzia Msigani – Kifuru – Kinyerezi umekamilika mwaka 2017; na
(iii) Ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara yenye urefu wa kilometa mbili kutoka Mbezi Mwisho hadi Msigani pamoja na barabara ya kuingia na kutoka kwenye Kituo cha Mabasi Mbezi unaendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa barabara ya Bunju ‘B’ – Mpiji Magohe – Victoria – Kifuru hadi Pugu Kilitex yenye urefu wa kilometa 33.7 ambayo inapita kwenye Jimbo la Kibamba utaanza mara baada ya usanifu kukamilika na fedha za ujenzi kupatikana.
MHE. IGNAS A. MALOCHA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatoa fedha za kujenga barabara ya Ntendo – Muze (kilometa 37.04) kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ignas Aloyce Malocha, Mbunge wa Kwela, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Barabara ya Ntendo – Muze yenye urefu wa kilometa 37.04 ina umuhimu wa kipekee kiuchumi kwa Bonde la Ziwa Rukwa, kwani ndiyo inayotumika kusafirisha mazao kutoka Bonde la Ziwa Rukwa kwenda kwenye masoko. Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara ya Ntendo – Muze imeendelea kutenga bajeti kila mwaka kwa ajili ya matengenezo mbalimbali ya barabara hii ili ipitike bila matatizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii itaendelea kufanyiwa matengenezo mbalimbali kwa kiwango cha changarawe na zege hususan sehemu korofi na miteremko mikali ili iendelee kupitika majira yote ya mwaka. Kwa sasa Serikali itaendelea kukamilisha ujenzi kwa kiwango cha lami barabara zinazounganisha Makao Makuu ya Mikoa na nchi jirani na hatimaye barabara za Mikoa.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018 jumla ya shilingi milioni 170 zimetengwa kwa ajili ya ukarabati wa kiwango cha zege sehemu zenye miinuko na miteremko mikali maeneo ya Mlima Kizungu. Aidha, Serikali itaendelea kutenga fedha katika bajeti ya mwaka wa fedha 2018/2019 ili barabara hii iendelee kupata matengenezo yatakayoiwezesha kupitika majira yote ya mwaka. (Makofi)
MHE. HASSAN E. MASALA (K.n.y. MHE. HASSAN S. KAUNJE) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itaanza kujenga kwa kiwango cha lami barabara ya Ngongo - Ng’apa - Milola ambayo ipo chini ya TANROADS?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Seleman Kaunje, Mbunge wa Jimbo la Lindi Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ya Ngongo - Ng’apa- Milola yenye urefu wa kilometa 42 ni barabara ya Mkoa inayohudumiwa na Wakala wa Barabara (TANROADS) Mkoa wa Lindi. Barabara hii ni sehemu ya barabara ya Ngongo - Ruangwa na Nanganga yenye urefu wa kilometa 162.
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara hii imeendelea kutenga bajeti kila mwaka kwa ajili ya kuifanyia matengenezo ya aina mbalimbali ili iendelee kupitika kiurahisi ambapo katika mwaka wa fedha 2017/2018, jumla ya shilingi bilioni 1.149 zimetengwa naa jumla ya kilometa 30 zimefanyiwa matengenezo ya muda maalum.
Mheshimiwa Spika, kuhusu ujenzi kwa kiwango cha lami sehemu ya barabara ya Ngongo - Ng’apa - Milola kilometa 42 kwa sasa kipaumbele ni kukamilisha kwanza barabara za kuunganisha Makao Makuu ya Mikoa pamoja na nchi jirani ndipo barabara za kuunganisha Wilaya zitafuata. Hivyo, barabara hii itaendelea kufanyiwa matengenezo ya aina mbambali kwa kiwango cha changarawe ili iendelee kupitika majira yote ya mwaka wakati Serikali ikitafuta fedha za kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kama sehemu ya maandalizi ya ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami. (Makofi)
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA aliuliza:-
Mwezi Septemba 2015 Serikali ya Tanzania, China na Oman kwa pamoja zilisaini mkataba wa ujenzi wa Bandari mpya ya Bagamoyo:-
Je, ni lini ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo utaanza rasmi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Shukuru Jumanne Kawambwa, Mbunge wa Bagamoyo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo utaanza rasmi mara tu Timu ya Wataalam wa Serikali (Government Negotiation Team) kukamilisha majadiliano na wawekezaji ambao ni Kampuni ya China merchants port holdings company limited ya China na Oman State General Reserve Fund na Serikali kuridhia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 7 Desemba, 2016 Serikali ilifanya uamuzi kwamba mradi wa ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo utekelezwe kwa ubia na sekta binafsi ili kuharakisha utekelezaji wa mradi huo. Kufuatia uamuzi huo tarehe 31 Machi, 2017 Serikali ya Tanzania ilipokea andiko la mapendekezo ya uwekezaji lililowasilishwa kwa pamoja kati ya Kampuni ya China Merchants Port Holding Company Limited ya China na Oman State General Reserve Fund.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inatarajiwa kuwa timu ya majadiliano ya Tanzania itakamilisha majadiliano hivi karibuni na ujenzi kuanza mara tu baada ya mkataba wa uwekezaji wa mradi kusainiwa kati ya Serikali na wawekezaji.
MHE. ALMAS A. MAIGE aliuliza:-
Barabara ya Tabora – Mambali – Bukumbi – Shitage - Tulole mpaka Kahama ipo katika mpango wa Serikali wa kujenga barabara za lami nchini:-
(a) Je, ni lini ujenzi wa barabara hiyo utaanza?
(b) Kumekuwa na mvutano wa wapi barabara hiyo ingepita baada ya kufika Mambali, mapendekezo ya Bodi ya Barabara ya Mkoa ni kuwa barabara hiyo ipite Bukumbi, Shitage, Tulole na kuunga Kahama; Je, Serikali inatoa msimamo gani baada ya mapendekezo hayo ya Bodi ya Mkoa wa Tabora?
(c) Je, ni lini kipande cha barabara hiyo kitachukuliwa na TANROADS?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Almas Athuman Maige, Mbunge wa Tabora Kaskazini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ambayo ipo katika mpango wa kujengwa kwa kiwango cha lami ni ya Tabora – Mambali – Itobo - Kagongwa - Kahama yenye urefu wa kilometa 180. Barabara hii ipo katika hatua za mwisho za upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ambapo kazi ya usanifu inafanywa na Mhandisi Mshauri NIMETA Consult na inatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Julai mwaka 2018. Baada ya kazi ya usanifu kukamilika Serikali itatafuta fedha ili kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara hii.
Mheshimiwa Spika, kuhusu kupandishwa hadhi kwa barabara ya Mambali – Bukumbi - Shitage na Tulole tayari sehemu ya barabara ya Mambali hadi Bukumbi yenye urefu wa kilometa 28.5 ni barabara ya mkoa inayohudumiwa na TANROADS na sehemu ya Bukumbi - Mhulidede kilometa 24.7 imekasimiwa kufanyiwa matengenezo na TANROADS kuanzia mwaka wa fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Spika, sehemu ya Mhulidede – Tulole kilometa 21 imeanza kuhudumiwa na TANROADS kuanzia mwaka huu wa fedha 2017/2018 na kufanya barabara yote ya Mambali – Bukumbi – Mulidede - Tulole - Kahama kuhudumiwa na TANROADS. (Makofi)
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA aliuliza:-
Upanuzi wa barabara kutoka mita 22.5 hadi 30 kutoka katikati ya barabara umesababisha baadhi ya wananchi katika Kitongoji cha Sanzale, Kata ya Magomeni kufuatwa na barabara na nyumba zao kuwekwa X:- Je, ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi hao?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Shukuru Jumanne Kawambwa, Mbunge wa Bagamoyo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Sheria ya Barabara ya mwaka 1932 ilifanyiwa mabadiliko mwaka 2007, ambapo eneo la hifadhi ya barabara lilibadilika kutoka mita 22.5 kutoka katikati ya barabara kila upande wa barabara kuu na barabara za Mikoa kuwa mita 30 na hivyo kufanya eneo la hifadhi ya barabara kuwa mita 60 badala ya mita 45 za awali.
Mheshimiwa Spika, kutokana na mabadiliko hayo, Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) ilifanya zoezi la kuainisha maeneo yote yaliyoathirika na Sheria mpya ya Barabara ya mwaka 2007 kwa nchi nzima. Aidha, wananchi wote wenye mali zao katika eneo la kuanzia mita
• hadi 30 kutoka katikati ya barabara kila upande ambao wamewekewa alama ya “X” ya kijani watalipwa fidia kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa pindi maeneo yatakapohitajika kwa ajili ya ujenzi au upanuzi wa barabara na hivyo mali zao kuathirika.
MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:-
Barabara Kuu ya kwenda nchi jirani ya Zambia imepita katikati ya makazi ya watu na sehemu za biashara hasa katika Mji Mdogo wa Mbalizi na barabara hiyo inatumiwa na magari ya mizigo ambayo mara nyingi huwa ni chanzo cha ajali.
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga barabara mpya ili kuhakikisha ajali zinapungua?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Tanzam highway inayoelekea nchi jirani ya Zambia ni barabara inayopita katika maeneo yenye makazi ya watu. Aidha, kutokana na tabia ya watu kupenda kufanya biashara ndogondogo kandokando ya barabara, kumekuwepo na msongamano mkubwa wa watu katika sehemu zinazopitiwa na barabara hii. Hali hii imejitokeza hasa katika maeneo ya Mbeya Mjini, Mbalizi, Uyole, Mlowo, Vwawa, Tunduma, Igawa, Chimala na Igurusi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ipo kwenye mpango wa kuikarabati barabara kuu ya Tanzam kuanzia Igawa hadi Tunduma ambapo katika mradi huo maeneo yenye matukio mengi ya ajali, ikiwemo eneo la mteremko wa Mbalizi, yataboreshwa ili kupunguza ajali. Mradi huu utajumuisha ujenzi wa barabara ya mchepuo kuanzia Uyole hadi Songwe na kazi hii ipo kwenye hatua ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina.
MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y. MHE. GODBLESS J. LEMA) aliuliza:-
Barabara ya Mzunguko wa Afrika Mashariki (by pass) inayojengwa katika Jiji la Arusha na viunga vyake inaonekana kusuasua ingawa fedha za ujenzi zimeshapatikana.
Je, ni lini Serikali italipa fidia kwa wananchi walioacha maeneo yao kwa ajili ya mradi huo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Godbless Jonathan Lema, Mbunge wa Arusha Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa mradi wa barabara ya mzunguko inayojengwa katika Jiji la Arusha na viunga vyake ni sehemu ya mradi wa Arusha – Holili yaani Taveta hadi Voi, ambayo ni mradi wa kikanda chini ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Tanzania Mradi wa Barabara ya Arusha – Holili unatekelezwa kwa awamu. Awamu ya kwanza inahusisha upanuzi wa Barabara ya Arusha kutoka Sakina hadi Tengeru yenye urefu wa kilometa 14.1 kutoka njia mbili za sasa hadi njia nne ambayo ujenzi wake umekamilika mnamo Julai, 2017 na sasa upo katika kipindi cha uangalizi (Defects Liability Period).
Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu ya pili inahusisha ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara ya mchepuo (Arusha by pass) yenye urefu wa kilometa 42.4 ambayo ujenzi wake ulianza tangu Februari, 2017 na unategemea kumalizika Juni, 2018. Mradi huu unagharamiwa na Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB).
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wa Serikali katika kutekeleza mradi huu ni pamoja na kulipa fidia kwa wananchi watakaoathirika na ujenzi wa barabara hii. Jumla ya shilingi bilioni 21.195 zimetumika kulipa fidia kwa wananchi walioathirika na barabara hiyo ya mchepuo. Zoezi la kulipa fidia lilianza tarehe 22 Machi, 2016 na hadi sasa jumla ya wananchi 742 walioathirika na mradi huo wamepokea malipo yao ya jumla ya shilingi bilioni 21.195 na hakuna mwananchi anayedai fidia tena kwenye mradi huu.
MHE. EZEKIEL M. MAIGE aliuliza:-
Wakati akihutubia mkutano wa kampeni Kharumwa Mheshimiwa Rais aliwaahidi wananchi wa Nyang’hwale kwamba barabara ya Kahama – Busangi – Kharumwa – Buyagu – Busisi itajengwa kwa kiwango cha lami; na Ilani ya CCM ya mwaka 2015 - 2020 imesema barabara ya Kahama - Bulige – Solwa – Mwanangwa itafanyiwa upembuzi yakinifu kwa ajili ya kujengwa kwa kiwango cha lami.
Je, kuna maandalizi gani yanayoendelea ya kutekeleza ahadi hiyo ya Rais na ile ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako naomba kwanza nianze kwa kuwatakia ndugu zangu waislam wote nchini mfungo mwema katika mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Ezekiel Magolyo Maige, Mbunge wa Msalala kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ya Kahama – Busangi – Kharumwa – Buyagu hadi Busisi yenye urefu kilometa 156.68 ni barabara ya mkoa inayounganisha mikoa mitatu ya Shinyanga, Geita na Mwanza. Aidha, barabara ya Kahama - Bulige – Solwa – Mwanangwa yenye urefu wa kilometa 150 ni barabara ya mkoa inayounganisha mikoa ya Shinyanga na Mwanza. Barabara hizi ni miongoni mwa barabara ambazo Serikali imepanga kuzijenga kwa kiwango cha lami. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, napenda kumthibitishia Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako tukufu kuwa Wizara yangu itaendelea kutekeleza ahadi za viongozi wakuu kwa awamu kutegemeana na upatikanaji wa fedha. Kwa hiyo, barabara ya Kahama – Busangi – Kharumwa – Buyagu – Busisi itatekelezwa kama Mheshimiwa Rais alivyoahidi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara ya Kahama – Bulige – Solwa – Mwanangwa (kilometa 150) ni kweli ipo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015. Napenda kumjulisha Mheshimiwa Mbunge kuwa tayari upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara hii umekamilika, kama ilani inavyoelekeza. Kwa sasa Serikali inaendelea kutafuta fedha za kugharamia ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami.
MHE. SAED A. KUBENEA aliuliza:-
Serikali katika Bunge la Kumi iliwasilisha Muswada wa Sheria ya Makosa ya Mtandao ambayo ilidhihirika kuwa na upungufu na baadhi ya wadau waliona kuwa kama sheria ikipita inaweza kuifanya nchi kuwa adui wa matumizi ya mtandao wa teknolojia ya habari na mawasiliano na sheria hiyo sasa inawaathiri watumiaji wa mitandao, kompyuta, simu za mikononi, saa, televisheni na vifaa vingine vinavyofanana na hivyo:-
Je, ni lini Serikali italeta Bungeni Muswada wa kuifanyia Marekebisho Sheria hiyo inayobana uhuru wa mwananchi wa kupata habari?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano pamoja na marekebisho madogo kwenye jibu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saed Ahmed Kubenea, Mbunge wa Ubungo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Makosa ya Mtandao Na. 14 ya Mwaka 2015 ni sheria adhibu kwa maana ya penal law ambayo inaainisha makosa na adhabu dhidi ya uhalifu unaotendeka mtandaoni. Sheria hii imeanisha makosa yanayotokana na matumizi mabaya ya mitandao na adhabu zake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uwepo wa sheria hii una manufaa makubwa kwani imesababisha kupungua kwa makosa ya mtandao, upatikanaji wa haki pale mtu anapotenda kosa, kwani kabla ya hapo kulikuwa na changamoto katika uainishaji wa makosa na adhabu hali iliyopelekea haki kutopatikana. Pia uwepo wa sheria hii umewezesha kuimarika kwa matumizi salama ya mtandao kama vile, Serikali Mtandao, Elimu Mtandao, Biashara Mtandao na hivyo kuleta maendeleo kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii ni muhimu sana katika nchi yetu na badala ya kuwaathiri watumiaji au wananchi, imesaidia kupunguza uhalifu wa mitandao, kwani wananchi wameanza kujua na kuelewa faida na hasara ya kutumia mitandao. Mfano, wahalifu wanaoiba fedha kwa njia ya mtandao wanashughulikiwa na sheria hii na haki kupatikana tofauti na ilivyokuwa hapo awali, kwani wananchi wengi walikuwa wakipoteza haki zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu za hali ya uhalifu kuanzia Januari hadi Desemba, 2017 iliyotolewa na Jeshi la Polisi inaonesha kuwa uhalifu kwa kipindi hicho ni matukio 4,824 yaliyoripotiwa, ukilinganisha na matukio 9,441 yaliyoripotiwa katika kipindi kama hicho mwaka 2016 ambapo ni sawa na upungufu wa asilimia 48.9. Hivyo kwa sasa Serikali haina mpango wa kuleta Muswada wa Marekebisho ya Sheria hii hadi hapo kutakapokuwa na uhitaji wa kufanya hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua fursa hii kuwahimiza wananchi kutumia fursa chanya zinazotokana na matumizi sahihi ya mtandao kuliko kutumia mitandao kwa ajili ya kufanya mambo ambayo ni kinyume na sheria za nchi na tamaduni za Kitanzania.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA aliuliza:-
Wakati ujenzi wa barabara muhimu ya Ipinda – Matema ukiendelea.
Je, ni lini wananchi, taasisi kama makanisa na ofisi za vijiji katika vijiji vya Matema, Katusyo, Mababu, Ngyekye, Katela na Ngeleka ambao hawajabomoa majengo yao kwa sababu hawajafidiwa fidia zao ambayo kimsingi ni haki yao na kupisha ujenzi unaoendelea wa barabara hii muhimu sana katika maendeleo na uchumi wa Wilaya ya Kyela Mkoani Mbeya zitalipwa fidia hizo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Hebron Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Barabara ya Kikusya – Ipinda – Matema yenye urefu wa kilometa 39.2 ni barabara ya mkoa inayohudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) ambapo ujenzi kwa kiwango cha lami unatekelezwa kwa sehemu ya Tenende hadi Matema (kilometa 34.7).
Mheshimiwa Spika, wakati wa utekelezaji wa mradi huu na kwa kuzingatia Sheria ya Barabara ya mwaka 2007 na Kanuni zake za mwaka 2009, uthamini wa mali za wananchi na taasisi zilizoathiriwa na ujenzi wa barabara hii ulifanywa.
Mheshimiwa Spika, baada ya kukamilika kwa uthamini huo ambao ulifanywa na Mthamini kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Kyela, malipo yalifanyika kwa waliostahili tarehe 17 Septemba, 2017 katika vijiji vya Masebe, Mpunguti, Mpanga, Ipinda, Ngamanga, Bwato, Mpegele, Ngeleka, Katela, Mababu, Kilombero, Kisyosyo na Matema. Hata hivyo, baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Ipinda walifungua mashtaka Mahakamani dhidi ya Serikali na hadi sasa hawajaondoa mali zao zilizo ndani ya eneo la hifadhi ya barabara.
MHE. JUMA S. NKAMIA aliuliza:-
Je, ni lini barabara ya lami kutoka Handeni – Chemba - Kwamtoro hadi Puma Singida itaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juma Selemani Nkamia, Mbunge wa Chemba kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ya Handeni – Kiberashi - Kwamtoro – Singida yenye urefu wa kilometa 461 inayopita katika Mikoa ya Tanga, Manyara, Dodoma na Singida inaunganisha Ukanda wa Mashariki, Ukanda wa Kati na Ukanda wa Kaskazini Magharibi. Barabara hii inaunganisha mikoa ambayo mradi wa bomba la mafuta kutoka Hoima Uganda hadi Tanga unakopita. Mradi huu ni muhimu sana kwani utaweza kuinua uchumi wa nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kutumia fedha za ndani tayari imekamilisha upembuzi yakinifu wa kina wa barabara hii. Ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara hii utaanza katika mwaka wa fedha 2018/2019 ambapo shilingi bilioni moja zimetengwa kwa ajili ya kuanza maandalizi ya kazi ya ujenzi.
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na juhudi za kutafuta fedha za kutosha kukamilisha ujenzi wa barabara hii muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu.
MHE. JULIUS K. LAIZER (K.n.y. MHE. JOHN J. MNYIKA) aliuliza:-
Barabara za pete (ring roads) na barabara za mchepuo (feeder roads) ni muhimu katika kupunguza msongamano na matatizo ya miundombinu kwa wananchi:-
(a) Je, Serikali itakamilisha lini ujenzi wa barabara hizo zilizoanza kujengwa katika Jimbo la Kibamba?
(b) Je, Serikali itaanza lini ujenzi wa barabara ambazo zimetajwa katika mipango ya Serikali lakini hazijaanza kujengwa mpaka sasa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa John John Mnyika, Mbunge wa Kibamba, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kama mkakati wa kupunguza msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam, Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano mnamo mwaka 2010 ilianza kutekeleza ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara za pete (ring roads) na barabara za mchepuo (bypass).
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara zilizoingizwa kwenye mpango huo ambazo ziko kwenye Jimbo la Kibamba na hatua za utekelezaji wake uko katika hatua mbalimbali ni kama ifuatavyo:-
Barabara ya Bunju B – Mpiji Magohe – Victoria – Kifuru hadi Pugu yenye urefu wa kilometa 33.7 (outer ring road); barabara ya Mbezi –Msigani –Malambamawili – Kifuru – Kinyerezi – Banana (sehemu ya Kinyerezi – Mbezi – Malambamawili – Kifuru) yenye urefu wa kilometa 10; na barabara ya Tegeta – Kibaoni – Wazo Hill -Goba – Mbezi/ Morogoro Road yenye urefu wa kilometa 20.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ambazo ujenzi kwa kiwango cha lami umekamilika ni sehemu ya barabara ya Mbezi – Msigani – Malambamawili – Kifuru – Kinyerezi – Banana kuanzia Msigani – Kifuru yenye urefu wa kilometa nane na barabara ya Tegeta Kibaoni – Wazo Hill – Goba Mbezi/ Morogoro road sehemu ya Goba Mbezi/Morogoro Road yenye urefu wa kilometa saba.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ambazo ujenzi wa kiwango cha lami unaendelea ni barabara inayoanzia Msigani mpaka Mbezi yenye urefu wa kilometa mbili zikiwemo barabara za kutoka na kuingia kwenye kituo cha mabasi ya Mbezi na barabara nyingine ni Goba – Madale yenye urefu wa kilometa tano. Barabara ambayo usanifu wake bado unaendelea ni barabara ya pete (outer ring road) ya Bunju B – Mpiji Magohe – Victoria – Kifuru hadi Pugu yenye urefu wa kilometa 33.7.
MHE. INNOCENT L. BUSHUNGWA aliuliza:-
Wananchi wa Bushagaro wamekuwa wakitengwa na maeneo mengine wakati wa vipindi vya mvua kwa sababu ya ubovu wa barabara ya Nyakahanga-Chamchuzi, na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano wakati wa kampeni za uchaguzi za mwaka 2015 aliahidi ujenzi wa barabara hiyo kwa lami na kuweka kivuko eneo la Chamchuzi:-
(a) Je, ni lini barabara hiyo itatengenezwa na kuwekwa kivuko?
(b) Je, ni lini ahadi ya kujengwa kwa lami kilomita 5 ya kianzio kwa ajili ya kutengeneza eneo korofi la Kajuna Nketo itaanza kama Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano alivyoahidi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Lugha Bashungwa, Mbunge wa Karagwe, lenye sehemu (a) na (b), kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Nyakahanga – Chamchuzi (km 97) inahusisha barabara ya Kajura – Nkeito (km 5) na barabara ya Nyakahanga – Nyabionza – Nyakakika (km 92), ambazo ni barabara za Wilaya zinazohudumiwa na Wakala wa Barabara Vijijini (TARURA). Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali ilitenga shilingi milioni 150 kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) ili kufanya matengenezo sehemu korofi na kujenga makaravati. Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali imetenga shilingi milioni 150 ili kuendelea kuifanyia ukarabati barabara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutekeleza ahadi zake pamoja na ahadi za Viongozi Wakuu wa Taifa zilizotolewa katika nyakati mbalimbali. Utekelezaji wa ahadi hizo unazingatia sera na vipaumbele vilivyowekwa na Serikali ambavyo ni pamoja na kukamilisha kuunganisha Makao Makuu ya Mikoa, kuunganisha Tanzania na nchi jirani kwa barabara za lami na ujenzi wa barabara nyingine muhimu, ikiwemo barabara ya Nyakahanga – Chamchuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uwekaji wa kivuko eneo la Chamchuzi, Serikali kupitia Wizara yangu itapeleka wataalam eneo la Chamchuzi ili kutafiti katika eneo hilo kuona uwezekano wa kuweka kivuko. Utafiti huo pamoja na mambo mengine, utahusisha kutambua kina cha maji ya mto iwapo kinatosha kuweka kivuko ambacho kitaelea kipindi chote cha mwaka. Mahitaji ya miundombinu yote katika eneo hilo kama vile barabara unganishi na maegesho ya kivuko (ramps) katika pande zote mbili za mto. Uamuzi wa kuweka kivuko katika eneo hilo utategemea matokeo ya utafiti huo.
MHE. HAMIDU H. BOBALI aliuliza:-
Wakati wa kampeni za Urais mwaka 2015 Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli alifika Kijijini Nangaru katika Jimbo la Mchinga na kuahidi kupandisha hadhi Barabara ya Mtange – Chikonji – Nangaru kutoka hadhi ya Halmashauri kuwa barabara ya Mkoa:-
a) Je, ni lini barabara hiyo itapandishwa hadhi?
b) Je, ni kwa nini Serikali huchukua muda mrefu kutekeleza ahadi mbalimbali zilizotolewa na Mheshimiwa Rais wakati wa Uchaguzi Mkuu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mwasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hamidu Hassan Bobali, Mbunge wa Mchinga, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, utakumbuka kuwa, mwezi Julai, 2017, Serikali ilianzisha rasmi Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kwa ajili ya kusimamia na kuendeleza mtandao wa barabara za Wilaya. TARURA imeanzishwa kwa Sheria ya Wakala wa Serikali (The Executive Agency Act), Sura 245 kupitia Gazeti la Serikali, GN No. 211, la tereha 12 Mei, 2017. Lengo la uanzishwaji wa wakala huu ni kuhakikisha kuwa barabara za Wilaya zinapata msukumo wa usimamizi wa kutosha kuliko ilivyokuwa hapo awali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Serikali imesitisha zoezi la upandishaji hadhi wa barabara za Wilaya kuwa za Mkoa kwa vile kuna Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) ulioanzishwa mahsusi na kupewa jukumu la kusimamia na kuendeleza barabara za Wilaya nchini. Ni matumaini yangu kuwa mtaipa ushirikiano TARURA, ili iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kukidhi matarajio ya wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utekelezaji wa ahadi ya Viongozi Wakuu, ahadi hizi zinajulikana na zitaendelea kutekelezwa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. DKT. DAMAS D. NDUMBARO (K.n.y. MHE. PROSPER J. MBENA) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya kutoka Bigwa – Mvuha – Kisaki katika Wilaya ya Morogoro Vijijini kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Prosper Joseph Mbena, Mbunge wa Morogoro Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ya Bigwa – Mvuha – Kisaki (km 133.28) ni barabara ya Mkoa inayohudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Morogoro. Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) tayari imeanza maandalizi ya ujenzi wa kiwango cha lami kwa barabara hii ambapo kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa sehemu ya Bigwa – Mvuha (km 78) inayofanywa na Kampuni ya Mhandisi Mshauri M/S Unitech Civil Consultants Limited ya Dar es Salaam imekamilika. Serikali ipo kwenye hatua ya kutafuta fedha za ujenzi.
Mheshimiwa Spika, ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Bigwa – Mvuha – Kisaki (km 133.28) utatekelezwa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Aidha, Serikali inaendelea kutenga fedha kwa ajili ya matengenezo ya aina mbalimbali kwa barabara hii ili iweze kupitika majira yote ya mwaka ambapo katika mwaka wa fedha wa 2018/ 2019 jumla ya shilingi milioni 1,822.550 zimetengwa kwa ajili ya matengenezo.
Mheshimiwa Spika, vilevile Serikali inaendelea na ukarabati kwa kiwango cha changarawe katika sehemu ya Mvuha – Kisaki (km 65.29). Sehemu hiyo ni kipande cha barabara ya Ubena Zomozi – Ngerengere – Mvuha – Kisaki Stiegler’s Gorge inayoelekea katika Mradi wa Kufua Umeme wa Mto Rufiji (Rufiji Hydropower Project). Kazi za ukarabati wa barabara hiyo unaendelea na utekelezaji wake umefikia asilimia 50.
MHE. HAWA A. GHASIA aliuliza:-
Je, ni lini Kivuko cha MV Mafanikio kitalala upande wa Msangamkuu ili kuwezesha dharura zinazojitokeza za wagonjwa hasa akinamama wajawazito kuhudumiwa wakati wa usiku?
NAIBU WAZIRI UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Abdulrahaman Ghasia, Mbunge wa Mtwara Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kivuko cha MV Mafanikio ambacho hutoa huduma ya kuvusha magari na abiria kati ya Msangamkuu na Mtwara Mjini eneo la Msemo, wakati wa usiku kinaegeshwa kwenye boya lililopo upande wa Mtwara Mjini. Kivuko hiki huegeshwa upande wa Mtwara Mjini kutokana na eneo hilo kuwa na kina kirefu cha maji hivyo kufanya kivuko kuwa salama wakati wa kupwa kwa maji ya bahari (low tide).
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2017, Serikali kupitia Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) imenunua boti ndogo iitwayo MV Kuchele yenye uwezo wa kubeba abiria nane ambayo inatumika kutoa huduma ya dharura kati ya Msangamkuu na Mtwara Mjini nyakati za usiku, ikiwemo huduma ya kuvusha akinamama wajawazito.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Boti hiyo kwa sasa huegeshwa upande wa Mtwara Mjini kwa sababu za kiusalama na endapo huduma ya dharura itahitajika upande wa Msangamkuu, mawasiliano hufanywa kwa njia ya simu ili boti hii iweze kutoa huduma hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mikakati wa Serikali ni kuweka miundombinu itakayowezesha boti hiyo kuegeshwa upande wa Msangamkuu wakati wa usiku ikiwemo nyumba ya kulala kwa ajili ya Nahodha wa boti hiyo.
MHE. MARTIN A. M. MSUHA aliuliza:-
Je, ujenzi wa barabara ya Mbinga hadi Mbambabay kwa kiwango cha lami unatarajiwa kukamilika lini?
NAIBU WAZIRI UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO – (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alexander Msuha Mbunge wa Mbinga Vijijini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara ya Mbinga Mbambabay yenye urefu wa kilometa 66 umeanza ambapo tarehe 3, Aprili, 2018 Wizara yangu kupitia Wakala wa barabara Tanzania TANROADS ilisaini mkataba wa ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara hii na kampuni ya China Henan International Corporation group company limited (CHICO) ya nchini China kwa gharama ya Sh,129,361,352,517.84 na muda wa ujenzi wa miezi 33 hadi tarehe 2 Januari, 2021.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya ujenzi inasimamiwa na mwandishi mshauri SMES International Limited wa nchini Australia kwa gharama ya Dola za Kimarekani 1,818,649.42 na fedha za kitanzania Sh.7,179,356,000.
MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE aliuliza:-
Ni Sera ya Serikali kuhakikisha mawasiliano baina ya watu wake katika maeneo ya nchi yanawezeshwa na kujengwa kikamilifu:-
Je, Serikali imejipangaje kuhusu utekelezaji wa ahadi ya ujenzi wa Daraja la Wami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Kikwete, Mbunge wa Chalinze, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua kuwa Daraja la sasa la Wami lenye urefu wa mita 88.75 lililopo Mkoa wa Pwani ambalo ni jembamba ni kiungo muhimu katika Barabara Kuu ya Chalinze – Segera. Kwa kutambua umuhimu huo, Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) imeanza maandalizi ya ujenzi wa daraja jipya litakalojulikana kwa jina la Daraja Jipya la Wami (New Wami Bridge) ambapo mnamo tarehe 28 Juni, 2018, ilisaini mkataba wa ujenzi na Kampuni ya Power Construction Corporation ya Nchini China kwa gharama ya Sh. 67,779,453,717 na muda wa ujenzi ni miezi 24. Daraja Jipya la Wami litakuwa na urefu wa mita 513.5 na upana wa mita 11.85 na litajengwa umbali wa mita 670 pembeni ya daraja la zamani kwa upande wa chini yaani Mashariki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu na wananchi kuwa ujenzi wa daraja hili jipya utagharamiwa na Serikali kwa asilimia 100 na utajumuisha ujenzi wa barabara unganishi za daraja kwa pande zote mbili zenye jumla ya kilometa 3.82 ili kuweza kuunganisha daraja jipya na Barabara Kuu ya Chalinze – Segera.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa mkandarasi yuko kwenye hatua ya maandalizi ya ujenzi, yaani ujenzi wa ofisi na nyumba za wafanyakazi pamoja na kuleta vifaa, mitambo na wataalam ili kazi ya ujenzi wa daraja ianze.
MHE. DANIEL E. MTUKA aliuliza:-
Kampuni ya Simu ya Viettel (Halotel) imepewa zabuni ya kusimika minara ya mtandao wa simu katika Jimbo la Manyoni Mashariki. Kasi ya usimikaji wa minara hiyo ni ndogo; mfano Vijiji vya Hika – Sanza hakina mawasiliano ya simu kabisa:-
Je, Serikali ina mkakati gani thabiti wa kuibana kampuni hiyo ili kutekeleza mkataba wake kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Edward Mtuka, Mbunge wa Manyoni Mashariki, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, upo mkataba kati ya Serikali na Kampuni ya Mtandao ya Viettel kuhusu utekelezaji wa mpango wa mawasiliano. Mkataba huo ulisainiwa tarehe 16 Julai, 2014 ukiwa na mpango wa kukamilisha utekelezaji wake ndani ya miaka mitatu hadi kufikia tarehe 30 Novemba, 2017. Katika mkataba huo makubaliano ya kufikisha mtandao wa mawasiliano ya simu kwenye vijiji 4,000 yalitakiwa kufanyika katika awamu tatu. Awamu ya kwanza ni kufikisha mtandao wa mawasiliano ya simu kwenye vijiji 1,800 ifikapo Novemba, 2015; awamu ya pili ni kufikisha mtandao wa mawasiliano ya simu kwenye vijiji 1,200 kwa kipindi cha Novemba, 2015 hadi Novemba, 2016 na awamu ya tatu kufikisha mtandao wa mawasiliano ya simu kwenye vijiji 1,000 kwa kipindi cha Novemba, 2016 hadi Novemba 2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia tarehe 30 Julai, 2018, jumla ya vijiji 3,712 vilikuwa vimefikiwa na mtandao wa mawasiliano ya simu. Aidha, ucheleweshwaji na utekelezaji wa mradi huu umechangiwa na changamoto mbalimbali zikiwemo upatikanaji wa vibali vya ujenzi wa minara hususani kwenye maeneo ya hifadhi za Serikali, mbuga za wanyama na kadhalika ambapo vibali vimekuwa havipatikani kwa wakati. Vilevile taratibu za masuala ya mazingira zinazoratibiwa na Baraza la Taifa la Hifadhi ya Usimamizi wa Mazingira (NEMC) zinachukua muda mrefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Serikali kupitia ukaguzi wa mradi na vikao mbalimbali inaendelea kusimamia utekelezaji wa mkataba wa Kampuni ya Simu ya Viettel ili kuhakikisha kwamba makubaliano yaliyowekwa yanakamilishwa. Aidha, usimikaji wa minara kwa ajili ya mtandao wa simu katika Vijiji vya Hika, Igwamadete, Isimbanguru, Mangoli na Mafulungu unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa Septemba, 2018. Hivyo, baada ya kukamilika kwa minara itakayosimikwa katika maeneo hayo kipande cha barabara ya Manyoni – Hika – Sanza kitakuwa na mawasiliano ya simu.
MHE. ENG. RAMO M. MAKANI aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Reli ya Kusini (Southern Circuit) ya Mtwara - Mbambabay - Mchuchuma - Liganga?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajibu swali napenda kufanya rekebisho dogo ni kwamba isomeke ni Mbunge wa Tunduru Kaskazini, siyo Tunduma. Kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mhandisi Ramo Matala Makani, Mbunge wa Tunduru Kaskazini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imedhamiria kujenga reli ya Kusini kutoka Mtwara hadi Mbambabay na matawi yake ya Mchuchuma na Liganga baada ya upembuzi yakinifu uliofanywa mwaka 2016 na Kampuni ya KORAIL ya Korea kuonesha kuwa mradi huu unaweza kurejesha gharama za uwekezaji za sekta binafsi kutokana na fursa lizizopo katika Ukanda wa Maendeleo wa Mtwara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa umbembuzi yakinifu huo Mhandisi Mshauri alipendekeza mradi huu utekelezwe kwa utaratibu wa kushirikisha sekta binafsi na umma yaani PPP.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali kupitia Shirika la Reli Tanzania (TRC) imetenga kiasi cha shilingi bilioni tatu kwa ajili ya kumpata mshauri wa uwekezaji yaani Transaction Advisor wa kuandaa andiko la kunadi mradi huu na kutafuta wawezekaji kwa utaratibu wa kushirikisha sekta binafsi na sekta ya umma (PPP), tathimini ya kumpata Transaction Advisor mahili inaendelea baada ya kujitokeza washauri 12 wanaoshindanishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kukamilika kwa andiko Shirika la Reli Tanzania (TRC) litatangaza zabuni katika vyombo mbalimbali vya habari kwa lengo la kumpata mwekezaji mahiri na mwenye masharti yanayovutia. Aidha, naomba ushirikiano wa Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge ili tuweze kupata wawekezaji mahili katika endelezaji wa reli hii muhimu.
MHE. MARY D. MURO aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya TAMCO Kibaha kupitia Vikawe kuunganisha na barabara ya Bagamoyo ili kupunguza msongamano wa magari yanayoenda Mbezi Boko na Bagamoyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Mary Deo Muro, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ya TAMCO kupitia Vikawe hadi Mapinga yenye urefu wa kilometa 23 ni barabara ya Mkoa inayohudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) ambapo kilometa 22 zimejengwa kwa kiwango cha changarawe na kilometa moja imejengwa kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Spika, kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina pamoja na tathmini ya fidia katika barabara hii ilikamilika katika mwaka wa fedha 2012/2013. Utekelezaji wa ujenzi wa kiwango cha lami umeanza kwa awamu ambapo kilometa moja imekamilika kujengwa. Vilevile taratibu za ununuzi kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami wa kipande cha kilometa 2.5 zimekamilika ambapo Mkandarasi Skol Building Contractors amepatikana na anategemewa kusaini mkataba mwishoni mwa mwezi huu wa Septemba, 2018.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2018/2019 kiasi cha shilingi bilioni 1.5 kimetengwa kutoka Mfuko Mkuu wa Serikali kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami. Aidha, taratibu za ununuzi wa mkandarasi wa ujenzi kwa kiwango cha lami kwa kipande kingine cha kilometa 1.5 zimeanza. Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Pwani anaendelea kufanya matengenezo mbalimbali barabara hii ili iweze kupitika majira yote ya mwaka ambapo shilingi bilioni 1.789 zimetengwa katika mwaka huu wa fedha kutoka Mfuko wa Barabara.
MHE. ALEX R. GASHAZA aliuliza:-
Barabara ya Nyakahuwa – Rulenge – Murugarama yenye urefu wa Km 85 imeahidiwa kutengenezwa kwa kiwango cha lami sambamba na barabara ya Nyakahuwa – Murusagamba tangu kipindi cha kwanza cha uongozi wa Awamu wa Nne lakini mpaka sasa barabara hizo hazijatengenezwa:-
Je, ni lini barabara hizi ambazo ni kichocheo cha maendeleo kwa Tarafa za Murusagamba, Rulenge, Kabanga na Jimbo la Ngara kwa ujumla zitaanza kutengenezwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba nijibu swali la Mhehimiwa Alex Raphael Gashaza, Mbunge wa Ngara, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, nia ya Serikali kuzijenga barabara za Nyakahuwa-Kumubuga – Murusagamba (km 34) na Kumuguba – Rulenge – Murugarama (km 75) kwa kiwango cha lami ipo pale pale. Tayari Serikali imeanza mazungumzo na Benki ya Maendeleo ya Afrika ili kupata fedha za kujenga barabara hizo kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa taratibu za kumpata Mhandisi Mshauri atakayefanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara hizi utakaogharamiwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika zipo katika hatua ya mwisho za ununuzi. Mradi huo utahusisha pia ujenzi kwa kiwango cha lami barabara ya Rulenge – Kabanga Nickel (Km 32)
Mheshimiwa Spika, wakati maandalizi hayo yakiwa yanaendelea, Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) itaendelea kuzifanyia matengenezo ya aina mbalimbali barabara hizi ili ziweze kupitika majira yote mwaka. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali imetenga jumla ya shilingi milioni 454.74 kwa ajili ya matengenezo ya barabara ya Nyakahuwa- Kumubuga – Murusagamba na shilingi million 457.3 kwa ajili ya maengenezo ya barabara ya Kumubuga – Rulenge – Murugarama.
MHE. PASCAL Y. HAONGA aliuliza:-
Barabara ya kutoka Mji wa Mlowo kuelekea Rukwa kupitia Kamsamba imekuwa muhimu katika kukuza uchumi wa Mkoa wa Songwe, Rukwa na Taifa kwa ujumla:-
Je, Serikali haioni kwamba ni wakati muafaka wa kuitengeneza kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Pascal Yohana Haonga, Mbunge wa Mbozi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ya Mlowo – Kamsamba yenye urefu wa kilometa 130 ni barabara ya Mkoa inayohusumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mkoa wa Songwe. Wizara yangu kupitia TANROADS imeanza kutekeleza ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami, ambapo TANROADS Mkoa wa Songwe imeshatangaza zabuni ili kumpata Mhandisi Mshauri atakayefanya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Baada ya kukamilisha hatua hiyo, ujenzi kwa kiwango cha lami utaanza.
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara hii kiuchumi na kijamii, imekuwa ikitenga fedha kila mwaka za kufanyia matengenezo mbalimbali, ambapo kwa mwaka wa fedha 2017/18 imetenga shilingi bilioni 1.439 na kwa mwaka wa fedha 2018/2019 zimetengwa shilingi bilioni 1.089 kwa ajili ya matengenezo ya barabara hii ili iweze kupitika majira yote ya mwaka. Vilevile, Wizara inaendelea na ujenzi wa daraja la Momba katika Kijiji cha Kamsamba na kazi inatarajiwa kukamilika Agosti, 2018.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya Mpemba hadi Ileje kwa kiwango cha lami ili kuunganisha na kuboresha mpaka wa Malawi na Tanzania katika eneo la Isongole?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ya Mpemba – Isongole ambayo ni barabara kuu yenye urefu wa kilometa 50.3 inaunganisha nchi yetu na nchi jirani ya Malawi inahudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mkoa wa Songwe. Barabara hiyo inaanzia katika Barabara Kuu ya TANZAM, eneo la Mpemba, katika Mamlaka ya Mji wa Tunduma, Wilaya ya Momba. Barabara hii ni kiungo cha kufika katika Mji wa Itumba ambao ni Makao Makuu ya Wilaya ya Ileje na maeneo ya jirani ya nchi ya Malawi.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, Serikali inatambua umuhimu wa barabara hii kiuchumi na kijamii na kwa kuwa, ndiyo barabara inayounganisha wananchi wa sehemu mbalimbali wa Wilaya ya Ileje na nchi jirani ya Malawi na Zambia, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) inaendelea kujenga Barabara ya Mpemba – Isongole kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa utekelezaji wa mradi upo kwenye hatua za awali, zikiwemo ujenzi wa Kambi ya Mhandisi mshauri ambayo imefikia 80%, kusafisha eneo la ujenzi wa barabara kilometa 10, ujenzi wa makalvati manne na uwekaji wa tabaka la chini la barabara.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2017/2018 Serikali imetenga shilingi bilioni 4.455 kwa ajili ya ujenzi wa kiwango cha lami na katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imetenga shilingi bilioni 10 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa barabara hii, ili mradi huu uweze kukamilika kama ulivyopangwa.
MHE. AMINA S. MOLLEL (K.n.y. MHE. CATHERINE V. MAGIGE) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi 55 wa Kata za Oldonyosambu na Mateves Wilayani Arumeru Mkoani Arusha waliopisha ongezeko la barabara ya Arusha- Namanga toka mwaka 2013.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Catherine Valentine Magige, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, tathmini ya mali za wananchi 55 wa Kata ya Oldonyosambu walioathiriwa na ujenzi wa barabara ya Arusha - Namanga ilifanyika mwaka 2013 na kiasi cha shilingi milioni 281.501 kilihitajajika kwa ajili ya kuwalipa fidia. Uhakiki wa tathmini hiyo ulifanyika na umekamilika, tayari Serikali imeshatoa Shilingi milioni 66.821 katika mwaka wa fedha 2017/2018 kwa ajili ya kulipa sehemu ya fidia hiyo.
Mheshimiwa Spika, malipo ya fidia yatafanyika kwa pamoja kwa wananchi wote mara baada ya Wizara yangu kupokea fedha zote zinazohitajika kwa ajili ya kulipa fidia hiyo.
Mheshimiwa Spika, napenda kumfahamisha Mheshimiwa Mbunge kuwa wananchi wote wanne (4) kwa Kata ya Mateves wameshalipwa fidia yenye jumla ya shilingi bilioni 2.225, hivyo hakuna mwananchi wa Kata ya Mateves anayeidai Serikali fidia.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya Geita – Bukoli – Kahama kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lolesia Jeremia Bukwimba, Mbunge wa Busanda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Geita – Bukoli - Kahama yenye urefu wa kilometa 120 ni barabara ya mkoa inayohudumiwa na Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS). Mpango wa kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami umeanza ambapo kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina imekamilika tangu mwaka wa fedha 2014/2015.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu kupitia TANROADS imepanga kutekeleza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami katika sehemu kuu mbili. Sehemu ya kwanza (Lot.1) ni Geita – Nyarugusu – Bulyanhulu Junction (km 58.3) na sehemu ya pili (Lot.2) ni Bulyanhulu Junction – Kahama (Km 61.7). Utekelezaji wa ujenzi utaanza mara fedha zitakapopatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati Serikali inaendelea kutafuta fedha, TANROADS itaendelea kuimarisha barabara hii kwa kuifanyia matengenezo ya aina mbalimbali ili iweze kupitika majira yote ya mwaka. (Makofi)
MHE.DKT. HADJI HUSSEIN MPONDA aliuliza:-
Serikali imekuwa akiahidi kufungua barabara ya Miku1mi – Ifakara –Lupiro - Kilosa kwa Mpepo – Londo – Namtumbo (T16) yenye urefu wa kilomita 396 inayounganisha Mikoa ya Morogoro na Ruvuma:-
(i) Je, ni lini barabara hii itafunguliwa ili ianze kutumika kwa kuwaunganisha wakazi wa mikoa hii miwili?
(ii) Je, ni lini kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara hii ya T16 utakamilika na kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Hadji Hussein Mponda, Mbunge wa Malinyi, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa Serikali imepanga kuunganisha mikoa yote nchini kwa barabara za lami ikiwa ni pamoja na barabara ya kuunganisha Mikoa ya Morogoro na Ruvuma, kwa kupitia Barabara Kuu ya Mikumi – Kidatu- Ifakara – Mahenge/Lupiro – Londo hadi Lumecha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa barabara hii imekwishafunguliwa na inapitika wakati wa kiangazi tu kutokana na baadhi ya maeneo kutopitika wakati wa masika. Kazi ya kuimarisha sehemu zisizopitika inaendelea kadri Serikali inavyopata fedha. Serikali imeanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami kwa awamu na itaendelea kulingana na upatikanaji wa fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Awamu ya Kwanza, Serikali ilijenga sehemu ya barabara kutoka Mikumi hadi Kidatu (kilomita 35.2); Awamu ya Pili, Serikali imekamilisha ujenzi wa Daraja la Kilombero lenye urefu wa mita mia tatu na themanini na nne pamoja na barabara unganishi yenye urefu wa (kilomita 9.142) inayoishia kwenye Kijiji cha Kivukoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeanza utekelezaji wa awamu ya tatu inayojumuisha ujenzi kwa kiwango cha Lami sehemu ya barabara kutoka Kidatu hadi Ifakara yenye urefu wa kilomita 66.9 ambapo Mkandarasi Reynolds Construction amekabidhiwa site ya kazi na kazi hii imepangwa kukamilika ifikapo tarehe 4 April, 2020.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu barabara ya Ifakara Mjini – Mahenge/Lupiro-Kilosa kwa Mpepo – Londo – Lumecha (kilomita 426,) usanifu wa kina ulikamilika mwezi Juni, 2017. Serikali inaendelea kutafuta fedha za ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara hii.
MHE. JASSON S. RWEIKIZA aliuliza:-
Barabara ya kuanzia Kanazi, Kata ya Kemondo kupitia Ibwera kwenda Katoro, Rubale na Izimbya ipo chini ya TANROADS, na ni muhimu kwa wakazi wa Bukoba na kwa uchumi wa Taifa:-
Je, ni lini barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jasson Samson Rweikiza, Mbunge wa Bukoba Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara tajwa inaitwa Kyetema – Kanazi – Kyaka 2 yenye urefu wa kilometa 42.37 na inapita katika vijiji vya Ibwera na Katoro. Barabara nyingine ni Rutenge – Rubale – Kishoju yenye urefu wa kilometa 74 ambayo inapita katika Vijiji vya Izimbya na Rubale. Barabara zote hizo ni barabara za Mkoa na zinahudumiwa na Wakala wa Barabara (TANROADS). Barabara hizi ni kiunganishi muhimu cha barabara kuu za lami ambazo ni barabara ya Mutukula – Bukoba – Kagoma – Lusahunga na barabara ya Kyaka – Bugene.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua umuhimu wa baraba hizi, Serikali imekuwa ikitenga fedha kila mwaka kwa ajili ya kuzifanyia matengenezo ya aina mbalimbali ili ziweze kupitika wakati wote wa mwaka. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, barabara ya Kyetema – Kanazi – Kyaka 2 imetengewa shilingi milioni 598.13 na barabara ya Rutenge – Rubale – Kishoju imetengewa shilingi milioni 333.20. Aidha, Serikali imejenga kwa kiwango cha lami maeneo korofi yenye urefu wa kilometa 4.8 sehemu ya Kyetema hadi hadi Kanazi kwenye barabara ya Kyetema – Kanazi – Kyaka 2.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa kipaumbele cha Serikali ni ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara za kuunganisha makao makuu ya mikoa, pamoja na barabara za kuunganisha Tanzania na nchi jirani. Hivyo, ujenzi kwa kiwango cha lami kwa barabara za mikoa zikiwemo barabara za Kyetema – Kanazi – Kyaka 2 na Rutenge – Rubale – Kishoju utaendelea kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. LATHIFAH H. CHANDE aliuliza:-
Serikali ilitenga jumla ya shilingi bilioni 6.4 kwa mwaka 2012 mpaka mwaka 2015 kwa ajili ya ukarabati wa kawaida wa barabara ya Nangurukuru – Liwale yenye urefu wa kilometa 230 na barabara hii inawaunganisha watu wa Liwale na Wilaya za Lindi na Mkoa wa Pwani na Dar es Salaam:-
Je, Serikali iko tayari kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lathifah Chande, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi ni kuhakikisha kuwa kwanza makao makuu ya mikoa yote inaunganishwa kwa barabara za lami ambapo kwa sasa karibu mikoa yote nchini imeunganishwa kwa barabara za lami. Pili, kuunganisha nchi yetu na nchi za jirani kwa barabara za lami ambapo karibu 64% ya barabara kuu zimejengwa kwa kiwango cha lami. Tatu, ni kuhakikisha kuwa, barabara zote za mikoa ambazo nyingi zinaunganisha makao makuu ya Wilaya zinapitika majira yote ya mwaka. Kwa sasa barabara nyingi za wilaya zimejengwa kwa kiwango cha changarawe na zinapitika majira yote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo, napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Lathifah Chande, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Nangurukuru – Liwale ni barabara ya mkoa inahudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Lindi. Hivyo, Wizara yangu kupitia TANROADS inaendelea kuifanyia matengenezo mbalimbali yatakayoiwezesha barabara hii kupitika majira yote ya mwaka. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, jumla ya shilingi bilioni 1.086 zimetengwa kwa ajili ya ukarabati na matengenezo ya muda maalum na katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali imetenga shilingi bilioni 1.76 kwa ajili ya kuendelea na ukarabati na matengenezo ya muda maalum kwa barabara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, Serikali ya Chama cha Mapinduzi kupitia Ilani yake ya Uchaguzi ya mwaka 2015 imepanga kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami. Kwa sasa inatafuta fedha kwa ajili ya kuanza kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina.
MHE. JESCA D. KISHOA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itajenga barabara inayounganisha Mkoa wa Singida na Bandari ya Tanga inayoanzia Kijiji cha Unyankhanya kupitia Makyungu Misughaa – Chemba hadi Tanga ili kuchochea maendeleo ya Mkoa wa Singida?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jesca David Kishoa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Makyungu – Chemba hadi Tanga inayoanzia Kijiji cha Unyankhanya ni sehemu ya mradi wa ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Handeni – Kiberashi – Kijungu – Chemba – Kwamtoro hadi Singida yenye urefu wa kilometa 460 ambapo kazi ya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina pamoja na uandaaji wa nyaraka za zabuni iliyofanywa na Mhandisi Mshauri aitwaye Inter-Consult Limited ya Dar es Salaam ikishirikiana na Mhandisi Mshauri aitwaye Consult Aurecon kutoka Afrika Kusini ilikamilika mwaka 2016.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami. Kwa kutambua umuhimu wa barabara hii kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi ikiwa ni pamoja na kuhudumia mradi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga eneo la Chongoleani, Serikali itahakikisha barabara hii inajengwa kwa kiwango cha lami.
MHE. OMARY T. MGUMBA aliuliza:-
Barabara ya Bigwa – Kisaki ni muhimu kiutawala na kiuchumi kwa kuwa inaunganisha Mbuga ya Selous, Mkoa wa Pwani, Lindi na Mtwara:-
• Je, ni lini barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami?
• Nyumba za wakazi zilizopo pembezoni mwa barabara hiyo zimewekwa alama ya X kwa muda mrefu lakini wananchi hawajalipwa fidia. Je, ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi hao?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Omary Tebweta Mgumba, Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, lenye sehemu (a) na (b), kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) inaendelea na kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami barabara ya Bigwa – Kisaki kwa kuanza na kipande cha barabara ya kuanzia Bigwa - Mvuha chenye urefu wa kilometa 78. Mhandisi Mshauri alitoa Ripoti ya Awali (Draft Final Report) tangu tarehe 2 Julai, 2017. Kazi hii imefanywa na Kampuni ya Unitec Civil Consultants Limited ya Dar-es- Salaam ikishirikiana na Kampuni ya Mult-Tech Consultant Limited kutoka Gabone, nchini Botswana. Kwa sasa Mhandisi Mshauri anaendelea kufanya marekebisho mbalimbali yaliyoelekezwa na Wakala wa Barabara (TANROADS) ili kukamilisha kazi hiyo ya usanifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mara baada ya usanifu wa barabara hii kukamilika na gharama kujulikana, Serikali itatafuta fedha ili ujenzi uanze kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Aidha, Serikali italipa fidia kwa wananchi ambao nyumba zao zitaathirika na ujenzi wa barabara ya Bigwa – Mvuha – Kisaki zilizowekwa alama ya X kwa mujibu wa Sheria ya Barabara ya mwaka 2007 na Kanuni zake za mwaka 2009.
MHE. CECIL D. MWAMBE (K.n.y. MHE. SAED A. KUBENEA) aliuliza:-
Serikali ya Awamu ya Nne chini ya Mheshimiwa Dkt. Jakaya Kikwete iliahidi kujenga kwa lami barabara ya kutoka Kimara Mwisho kupitia Mavulunza – Bonyokwa Segerea hadi kuungana na barabara ya Nyerere yenye urefu wa Kilomita 4.7 na ambayo imekasimiwa kwa TANROADS:-
(a) Je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara hiyo kwa lami kama ambavyo iliahidiwa miaka mitano iliyopita?
(b) Je, Serikali haioni umuhimu wa kujenga barabara hiyo ili kupunguza tatizo la foleni?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saed Ahmed Kubenea, Mbunge wa Ubungo, lenye kipengele (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa ujenzi wa barabara ya Kimara Mwisho kupitia Mavulunza - Bonyokwa hadi Segerea hadi kuungana na barabara ya Nyerere yenye urefu wa kilomita nane (8) unategemea kuanza mara baada ya kukamilisha utekelezaji wa mpango wa sasa wa ujenzi wa barabara za kupunguza msongamano unaoendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa barabara za kupunguza msongamano Jijini Dar es Salaam unaendelea vizuri. Mpaka kufikia mwezi Aprili, 2018, ujenzi wa barabara ya Banana - Kinyerezi – Kifuru – Marambamawili - Msigani hadi Mbezi Mwisho yenye urefu wa kilomita17, ambayo inaunganisha barabara ya Nyerere na Morogoro umefikia asilimia 90. Kwa sasa ujenzi unaendelea ili kukamilisha sehemu ya barabara iliyobaki yenye urefu wa kilomita mbili (2) kuanzia Msigani mpaka Mbezi Mwisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kukamilika kwa barabara hii kutaunganisha barabara ya Nyerere, Morogoro na Bagamoyo kupitia barabara ya Mbezi Mwisho, Goba, Tangi Bovu ambayo ujenzi umekamilika.hata hivyo, Serikali inaendelea kutenga fedha za matengenezo ya barabara ya kutoka Kimara Mwisho – Bonyokwa - Segerea ili kuhakikisha inapitika vizuri wakati wote.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-
Bandari katika mwambao wa Ziwa Nyasa kutoka moja kwenda nyingine zipo kwa umbali mrefu sana hususan upande wa Wilaya ya Ludewa; hii imekuwa ni kero kubwa kwa sababu hakuna miundombinu ya barabara ambayo ingerahisisha huduma ya usafiri:-
(a) Je, ni lini Serikali itatupatia bandari katika Vijiji vya Nkanda, Nsele, Kyaghomi, Makonde na Yigha?
(b) Je, ni lini huduma za usafiri wa meli zitaanza tena ili kupunguza kero ya usafiri kwa wananchi waishio kandokando ya Ziwa Nyasa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) ina mkakati wa kuboresha na kujenga miundombinu ya bandari na gati mbalimbali katika Ziwa Nyasa. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali kupitia TPA ilitenga fedha kwa ajili ya kuendeleza Bandari za Mbambabay, Itungi, Kiwira, Ndumbi, Manda, Matema, Liuli na Lupingu Wilayani Ludewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mipango hiyo, bado kuna timu toka Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania inafanya usanifu wa awali katika vijiji alivyotaja Mheshimiwa Mbunge vya Nkanda, Nsele, Kyaghomi, Makonde, Yigha na maeneo jirani. Baada ya usanifu wa awali, Serikali itatambua maeneo gani yanafaa kuweka vituo vya kushusha na kupakia abiria na mizigo ili kuwaondolea adha abiria katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali bado inaendelea kumalizia ujenzi wa meli ya abiria itakayotoa huduma katika eneo la Ziwa Nyasa, hivyo tunatumaini wananchi watapata huduma ya usafiri wa meli kabla ya mwaka huu 2018 kwisha.
MHE. ANNE K. MALECELA aliuliza:-
Mfuko wa Pensheni wa Serikali za Mitaa (LAPF) umemuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuamua kukiboresha Kiwanda cha Tangawizi cha Mamba Miamba kilichoko Wilaya ya Same katika Jimbo la Same Mashariki.
Je, Serikali haioni kuwa kuna umuhimu sasa kuboresha barabara zinazoelekea Mamba Miamba Kiwandani?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, Mbunge wa Kuteuliwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ya Mwembe – Miamba – Ndugu yenye urefu wa kilometa 90.19 inayopita eneo la Mamba Miamba Kiwandani ni barabara ya Mkoa inayohudumiwa na TANROADS Mkoa wa Kilimanjaro. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, barabara hii imetengewa jumla ya shilingi bilioni 1.487 kwa ajili ya kuifanyia matengenezo ya muda maalum kwenye eneo lenye urefu wa kilometa 22.5 katika Vijiji vya Mtunguja, Mhezi, Kwizu, Marindi, Mshewa, Mwembe, Mbaga, Gohe, Kambeni na Manka pamoja na matengenezo ya kawaida yanayofanyika katika Vijiji vya Dindimo, Kanza na Miamba. Vilevile kufanyika matengenezo ya madaraja yatakayohusisha ujenzi wa madaraja (drifts) mapya mawili katika Kijiji cha Mbaga na ukarabati mkubwa wa Daraja la Mwerera lililopo katika Kijiji cha Mwerera.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2018/2019 barabara hii pia imetengewa jumla ya shilingi bilioni 1.250 kwa ajili ya kuifanyia matengenezo mbalimbali yakiwemo ya ukarabati na matengenezo ya kawaida na muda maalum.
Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuifanyia matengenezo muhimu barabara hii ili iendelee kupitika bila matatizo muda wote.
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA aliuliza:-
Je, kwa nini Serikali haitaki kukarabati Uwanja wa Ndege Mtwara?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maftah Abdallah Nachuma, Mbunge wa Mtwara Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali iko katika hatua za mwisho za kukamilisha taratibu za manunuzi kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa Kiwanja cha Ndege cha Mtwara. Hadi sasa mkandarasi kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa kiwanja hiki amepatikana ambaye ni Beijing Construction Engineer Group Co. Ltd. ya China kwa gharama ya shilingi bilioni 50.366. Hatua iliyobaki ni mkandarasi kukamilisha taratibu za kupata udhamini (bank guarantee) ili aweze kulipwa malipo ya awali (advance payment) na kukabidhiwa eneo la mradi. Hivyo, mradi huu utaanza kutekelezwa mara tu baada ya taratibu za manunuzi kukamilika.
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kumsimamia mkandarasi akamilishe jukumu lake ili kazi ya ukarabati wa uwanja uweze kuanza mara moja.
MHE. SILVESTRY F. KOKA aliuliza:-
Barabara ya TAMCO – Mapinga kupitia Kata ya Pangani ilichukuliwa na TANROADS takribani miaka nane (8) iliyopita:-
Je, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya kujenga barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Silvestry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) imekamilisha maandalizi ya kuijenga kwa kiwango cha lami barabara ya TAMCO – Mapinga yenye urefu wa kilometa 23 kwa kufanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, pamoja na uthamini wa mali ambao ulikamilika Febrauri, 2014. Baada ya usanifu wa kina kukamilika, Serikali imeanza kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2013/2014 kilomita moja ilijengwa kwa kiwango cha lami na katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 4.234 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali kupitia TANROADS imekamilisha taratibu za ununuzi wa kumpata Mkandarasi na inaendelea na maandalizi ya kusaini mkataba. Vilevile katika mwaka wa fedha 2018/2019 jumla ya shilingi bilioni 1.5 zimetengwa kwa ajili ya kuendelea na mradi huu.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza:-

Katika Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015 wananchi wa Korogwe waliahidiwa ujenzi wa barabara ya lami kutoka Korogwe - Dindira – Bumbuli.

Je, ni lini ujenzi huo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara ya Korogwe - Dindira hadi Bumbuli inayopita kwenye maeneo yenye uzalishaji mkubwa wa mazao ya biashara na matunda imeanza kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa lengo la kujenga kwa kiwango cha lami barabara yote ya Soni – Bumbuli – Dindira - Korogwe yenye urefu wa kilomita 77 ikiwemo sehemu ya Bumbuli - Dindira - Korogwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina sehemu ya Soni - Bumbuli yenye urefu wa kilomita 21.7 imekamilika mwezi Juni mwaka 2018. Hivi sasa Serikali ipo katika hatua ya ununuzi wa kumpata mtaalam mshauri wa kufanya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa sehemu iliyobaki ya Bumbuli-Dindira-Korogwe yenye urefu wa kilomita 5.3. Kiasi cha shilingi milioni 130 zimetengwa katika bajeti ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa mwaka wa fedha 2018/2019 kwa ajili ya kuanza kazi hiyo. Usanifu utakapokamilika na gharama za ujenzi kujulikana, fedha za ujenzi zitafutwa ili ujenzi wa kiwango cha lami uanze kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA (K.n.y. MHE. ISSA A. MANGUNGU) aliuliza:-

(a) Je, barabara ya Kilwa imeshakabidhiwa kwa Serikali kutoka kwa mkandarasi aliyejenga barabara hiyo (KAJIMA)?

(b) Je, barabara hiyo ipo katika kiwango kinachotakiwa?

(c) Je, ni nani anagharamia ukarabati usiokwisha wa barabara hiyo kati ya Serikali na mkandarasi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ally Mangungu, Mbunge wa Mbagala, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na taratibu za mikataba ya ujenzi wa barabara, kabla ya mradi haujapokelewa na Serikali panakuwepo kipindi cha matazamio ambacho mkandarasi hutakiwa kurekebisha kasoro zozote zitakazojitokeza katika kipindi hicho kwa gharama zake mwenyewe. Utaratibu huu ndiyo unaotumika katika mradi wa ujenzi wa barabara ya Kilwa ambapo mkandarasi alifanya marekebisho ya mapungufu yaliyojitokeza katika kipindi cha matazamio cha miaka miwili kuanzia tarehe 15 Mei, 2012 hadi tarehe 31 Desemba, 2014 kwa gharama zake mwenyewe.

Mheshimiwa Mwenyeiiti, mara baada ya mkandarasi kufanya marekebisho ya sehemu zilizokuwa na mapungufu, wataalam wa Wizara walifanya ukaguzi na kujiridhisha kuwa barabara hiyo ina viwango vya ubora vinavyokubalika kulingana na matakwa ya mkataba na kukabidhiwa rasmi Serikalini tarehe 31 Desemba, 2014. Hivyo, majukumu ya mkandarasi (KAJIMA) yamekamilika katika barabara hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikifanya matengenezo ya kawaida ya barabara hii kama ilivyo kwa barabara zingine ili iweze kudumu kwa muda mrefu.
MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:-

Wilaya ya Mbeya, Mkoa wa Mbeya na Wilaya za Ileje na Songwe Mkoa wa Songwe zinaunganishwa kwa barabara za vumbi kuanzia Mbalizi kuelekea Ilembo, Iwinji hadi Ileje na Mbalizi kuelekea Mshewe.

(a) Je, ni lini Serikali itaunganisha barabara hizo kwa lami?

(b) Je, ni lini Serikali italipa fidia wananchi waliopisha upanuzi wa barabara za Mbalizi, Mshewe, Mjele hadi Mkwajuni Songwe?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara alizotaja Mheshimiwa Mbunge ni barabara za Mbalizi - Shigamba - Isongole zenye urefu wa kilometa 96.8 na barabara ya Mbalizi – Chang’ombe – Mkwajuni – Patamela – Makongolosi yenye urefu wa kilometa 117. Barabara hizo ni za Mkoa na zinahudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Mbeya na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Songwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sera ya Serikali kwa sasa ni kuunganisha Makao Makuu ya Mikoa na nchi jirani kwa barabara za kiwango cha lami, ambapo tayari Makao Makuu ya Mkoa wa Mbeya na Mkoa wa Songwe yameunganishwa kwa barabara ya lami ya Mbeya hadi Tunduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, kwa kuzingatia umuhimu wa barabara hizo, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) imefanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ili kuijenga kwa kiwango cha lami kwa barabara ya Mbalizi – Chang’ombe – Mkwajuni – Patamela – Makongolosi kilometa 117, sehemu ya Mbalizi hadi Galula kilometa 56. Aidha, Serikali imekuwa ikizifanyia matengenezo mbalimbali ya barabara hizi za Mbalizi – Shigamba – Isongole kilometa 96.8 na barabara ya Mbalizi – Chang’ombe – Mkwajuni – Patamela – Makongolosi kilometa 117 kila mwaka ili ziweze kupitika na majira yote ya mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu wananchi watakaopisha ujenzi wa barabara ya Mbalizi – Mshewe – Mjele – Galula. Serikali itawalipa fidia kutokana na sheria na taratibu kabla ya kuanza ujenzi.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA aliuliza:-

Mkandarasi aliyepewa tenda ya kujenga barabara ya lami kutoka Urambo kwenda Kaliua kilometa 28 ameonyesha udhaifu mkubwa katika kutekeleza kazi hiyo tangu awali:-

Je, kwa nini Serikali isisitishe mkataba wa mkandarasi huyo haraka kwa kumpata mkandarasi mwenye uwezo na uzoefu ili kukamilisha ujenzi wa barabara hiyo muhimu kwa wakati na ubora?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Magdalena Hamis Sakaya, Mbunge wa Kaliua, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mradi wa Ujenzi wa kwa kiwango cha lami wa barabara ya Urambo-Kaliua kilomita 28 ni moja kati ya miradi iliyotengwa mahsusi na Serikali kwa ajili ya wakandarasi wa ndani ili kuwajengea uwezo na kupata miradi mikubwa ya barabara. Mchakato wa kumpata mzabuni ulifanyika kwa malengo hayo.

Mheshimiwa Spika, aidha, muungano wa Wakandarasi watatu wazalendo, Salum Motor Transport Limited, Annam Road Works Company Limited na Jossam Company Limited walikidhi vigezo na hivyo kushinda zabuni hiyo. Utekelezaji wa mradi huu ambao unagharamiwa na Serikali ya Tanzania kwa asilimia 100 ulianza rasmi tarehe 30 Agosti, 2017 na muda wa utekelezaji ni miezi 26. Hadi sasa wakandarasi hawa wameendelea na kazi japo kwa kasi ndogo lakini kwa kiwango cha kuridhisha ambapo utekelezaji umefikia asilimia 35.

Mheshimiwa Spika, kasi ndogo ya utekelezaji ilichangiwa na mabadiliko ya hali ya hewa ambapo mvua nyingi ziliathiri utekelezaji ambapo mkandarasi ameomba kuongezewa muda. Hatua nyingine zinazochukuliwa na Serikali ni pamoja na kuhakikisha kuwa Mhandishi Mshauri wa mradi anaendelea kuwafundisha wakandarasi hawa kuhusu usimamizi wa miradi ili lengo lililopangwa liweze kufikiwa.

Mheshimiwa Spika, naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa kutokana na hatua mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa na Seikali, mradi huu utakamilika kwa ubora na viwango vilivyopangwa kimkataba. Hivyo, kusitisha mkataba kwa hatua iliyofikiwa haitakuwa na tija kwa Serikali kwani tuna imani kuwa kutokana na mafunzo wanayoyapata wakandarasi hawa wazawa watakamilisha mradi huu kwa viwango vinavyotakiwa.
MHE. ZAYNABU M. VULU (K.n.y. MHE. MBARAKA K. DAU) aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaongeza urefu wa njia ya kurukia (run way) katika Uwanja wa Ndege wa Mafia?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbaraka Kitwana Dau, Mbunge wa Mafia, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Sera ya Taifa ya Usafiri wa Anga inataka kila mkoa kuwa na Kiwanja cha Ndege cha Daraja la 3C chenye uwezo wa kuhudumia ndege za kubeba abiria kati ya 50 na 100. Aidha, kwa mikoa inayowakilisha kanda, Viwanja vya Ndege vinavyopendekezwa ni kuanzia Daraja la 4C kwa ajili ya kuhudumia ndege za kubeba abiria kati ya 100 na 200 zinazoweza kufanya safari za kikanda na kimataifa. Kiwanja cha Ndege cha Mafia ni miongoni mwa viwanja vvya Daraja la 3C.

Mheshimiwa Spika, katika kuboresha Viwanja vya Ndege nchini, Serikali kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege ilikamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa viwanja saba ikiwemo Kiwanja cha Ndege cha Mafia mnamo mwaka 2009. Kazi hii ilifuatiwa na ukarabati na upanuzi wa Kiwanja cha Ndege kwa kiwango cha lami katika ya mwaka 2011 na 2013. Kazi zilizofanyika ni pamoja na ukarabati wa barabara ya kuruka na kutua ndege kufikia urefu wa mita 1,620 na upana wa mita 30, ukarabati wa kiungio na maegesho ya ndege kwa ikiwango cha lami, ujenzi wa mfumo wa maji ya mvua kiwanjani na ujenzi wa uzio wa usalama.

Mheshimiwa Spika, kazi hizi zilifanyika kwa ufadhili wa Shirika la Changamoto za Milenia (MCC) la Serikali ya Marekani. Baada ya maboresho haya, kiwanja kipo kwenye kiwango cha Daraja la 2C ambapo kina uwezo wa kupokea na kuhudimia ndege zenye ukubwa wa aina ya ATR42, DASH 8 na Fokker 50 ambazo zina uwezo wa kubeba abiria kati ya 30 na 50.

Mheshimiwa Spika, katika mipango yake ya muda wa kati na mrefu, Serikali itaendelea kukamilisha kazi zilizobaki ambazo ni pamoja na ujenzi wa jengo la abiria na miundombinu yake yaani barabara ya kuingia na kutoka kiwanjani, maegesho ya magari, barabara ya kiungo na maegesho ya ndege pamoja na usimikaji wa taa na mitambo ya kuongozea ndege. Pamoja na kuwa kwa sasa kiwanja hiki kipo Daraja la 2C, eneo la ziada limeshatengwa ili kukidhi mahitaji ya upanuzi wa kiwanja kwa siku za baadaye na kukamilishwa kwa kiwanja kuwa Daraja ya 3C.
MHE. CECILIA D. PARESSO (K.n.y. MHE. ESTHER A. BULAYA) aliuliza:-

Wananchi wa Vijiji vya Manyamanyama, Nyasura, Bunda Mjini na Balili, mwezi Julai, 2003 walivunjiwa nyumba zao kupisha hifadhi ya barabara baada ya TANROADS kuongeza umiliki wa hifadhi toka mita 16 hadi mita 22.5:-

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwalipa wananchi hao fidia na ni lini itafanya hivyo?

(b) Je, ni tathmini ipi itatumika kuwalipa kwani kumekuwepo na mserereko mkubwa wa thamani ya shilingi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Amos Bulaya, Mbunge wa Bunda Mjini, lenye Sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Jedwali la Kwanza la Sheria ya Barabara ya Mwaka 1932 pamoja na Marekebisho yake, yaani The Highways Ordinance ya Mwaka 1932 Barabara ya Mwanza – Bunda – Tarime – Kenya Border, yaani Sirari, imeainishwa kama barabara kuu yaani Territorial Main Road. Kwa mujibu wa kanuni zilizotungwa chini ya sheria hiyo upana wa hifadhi ya barabara kuu ikiwemo sehemu ya Balili – Bunda – Manyamanyama yenye urefu wa kilometa 9.8 zilikuwa futi 75 kila upande kutoka katikati ya barabara ambayo ni sawa na mita 22.5.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu mwaka 1932 barabara hii ilipoainishwa kuwa barabara kuu imeendelea kuwa na hadhi hiyo hadi mwaka 2007. Upana wa hifadhi ya barabara hiyo ulibadilika kutoka mita 22.5 kuwa mita 30 kila upande kwa mujibu wa Sheria ya Barabara Namba 13 ya Mwaka 2007 na sio mita 16 kwenda mita 30, kama alivyodai Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na maelezo hayo, Serikali itawalipa fidia wananchi waliokuwa nje ya hifadhi ya barabara ya mita 22.5 wakati eneo hilo litakapohitajika kutokana na mabadiliko ya Sheria Namba 13 ya Barabara ya Mwaka 2007 kwa vile wamefuatwa na barabara. Aidha, ulipaji wa fidia utazingatia Sheria ya Ardhi Namba 4 ya Mwaka 2001 na Sheria ya Ardhi ya Vijiji Namba 5 ya Mwaka 2001 na Kanuni zake.
MHE. ENG. RAMO M. MAKANI aliuliza:-

Je, Serikali ina mipango ipi ya muda mfupi, wa kati na mrefu ya kushughulikia changamoto zinazojitokeza katika matengenezo ya miundombinu nchini baada ya ujenzi wake kukamilika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ramo Matala Makani, Mbunge wa Tunduru Kaskazini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukabiliana na changamoto ya matengenezo ya miundombinu ya barabara na madaraja, Serikali ilianzisha Bodi ya Mfuko wa Barabara mwezi Julai, 2000 kwa lengo la kufanya matengenezo mbalimbali ya barabara ya kawaida, matengenezo ya muda maalum, matengenezo ya maeneo korofi na matengenezo ya madaraja. Ili kukabiliana na changamoto za matengenezo ya miundombinu ya barabara baada ya kukamilika kwa ujenzi, Serikali imekuwa ikiongeza bajeti ya matengenezo kila mwaka kupitia Mfuko wa Barabara kwa ajili ya kufanya matengenezo mbalimbali ya barabara nchini. Bajeti ya matengenezo ambayo imekuwa ikiongezeka kila mwaka inatumika kufanya matengenezo ya kawaida, matangenezo ya muda maalum, matengenezo ya maeneo korofi na matengenezo ya madaraja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu ilivyoanzishwa Bodi ya Mfuko wa Barabara bajeti ya matengenezo imekuwa ikiongezeka kila mwaka. Kwa mfano, katika bajeti ya mwaka 2000/2001 zilitengwa Sh.44,436,708,674 na Mwaka wa Fedha 2010/2011 zilitengwa Sh.286,907,000,000 na Mwaka wa Fedha 2018/2019 zimetengwa jumla ya Sh.908,808,000,000. Mfuko huu unaimarishwa kila mwaka ili miundombinu ya barabara na madaraja iweze kutengenezwa na kupitika majira yote ya mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia inaendelea kudhibiti uzito wa magari kwa kujenga mizani na kupima uzito wa magari kwenye barabara zote za lami zilizokamilika na zinazopendelea kujengwa nchi nzima ili kuzinusuru barabara hizo kutokana na uharibifu mkubwa unaosababishwa na magari yanayozidisha uzito. Mizani inajumuisha mizani ya kudumu, mizani inayohamishika na mizani inayopima magari yakiwa kwenye mwendo, yaani Weigh in Motion.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) unaendelea kufanya tafiti mbalimbali kupitia Maabara Kuu ya Vifaa vya Ujenzi kwa kushirikiana na Taasisi ya Utafiti ya Afrika Kusini, lengo ni kubaini sababu za baadhi ya barabara hapa nchini kuharibika katika kipindi kifupi mara baada ya kukamilika. Wizara kupitia TANROADS tayari imekwishatoa mwongozo wa usanifu wa uchanganyaji wa lami, yaani Guideline for Asphalt Mix Design, unaozingatia mabadiliko ya mifumo ya miundo na vyombo vya usafiri, hali ya hewa na viwango sahihi vya vifaa vya ujenzi wa barabara. Mwongozo huu ulianza kutumika Mwezi Novemba mwaka 2018.
MHE. PAULINE P. GEKUL aliuliza:-

(a) Je, ni lini wananchi wanaodai fidia kutokana na barabara ya mchepuo kutoka Arusha – Singida na Arusha – Dodoma katika Mji wa Babati watalipwa fidia?

(b) Je, ni lini ujenzi wa barabara hizo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Pauline Philip Gekul, Mbunge wa Babati Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa mchepuo kutoka barabara za Arusha – Singida na Arusha – Dodoma kwa Babati Mjini (Babati Baypass) unatekelezwa kwa pamoja na mradi wa barabara ya mchepuo wa Bwawa la Mtera (Mtera Baypass) katika barabara ya Iringa – Dodoma chini ya ufadhili wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB). Aidha, taratibu za ununuzi wa kumpata Mhandisi Mshauri atakayefanya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina upo katika hatua za mwisho ambapo kazi ya upembuzi yakini na usanifu wa kina itakayotekelezwa na Mhandisi Mshauri itahusisha pia usanifu wa mwelekeo ulio bora na sahihi wa barabara ya mchepuo kwa kuzingatia vigezo vya kitaalam kama vile gharama za ujenzi, uhifadhi wa mazingira pamoja na usalama wa watumiaji wa barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na hadidu za rejea alizopewa Mhandisi Mshauri ni pamoja na kutambua watu na mali zao watakaoathiriwa na mradi. Baada ya Mhandisi Mshauri kukamilisha jukumu la kitaalam; tathmini ya mali za wananchi zitakazoathiriwa na mradi itafanyika kwa kufuata sheria na taratibu na hatimaye fidia kulipwa kwa walengwa kwa kuzingatia sheria zilizopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kukamilisha kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina pamoja na maandalizi ya nyaraka za zabuni, kazi hii itatangazwa ili kumpata mkandarasi wa kujenga barabara hiyo.
MHE. PETER A. LIJUALIKALI aliuliza:-
(a) Je, ujenzi wa barabara ya Kidatu – Ifakara umefikia hatua gani?
(b) Je, barabara hii inatarajiwa kukamilika lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA), alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Peter Ambrose Lijualikali, Mbunge wa Kilombero lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ya Kidatu-Ifakara yenye urefu wa kilometa 66.9 ni sehemu ya barabara ya Mikumi – Ifakara – Mahenge/Lupiro – Kilosa kwa Mpepo – Londo Lumecha yenye urefu wa Kilometa 534.4 inayounganisha Mkoa wa Morogoro na Ruvuma katika Mto Londo.
Mheshimiwa Spika, mkataba wa ujenzi wa barabara hii seuemu ya Kidatu – Ifakara (kilomita 66.9) na daraja la Ruaha Mkuu (mita 130) ulisainiwa tarehe 24 Julai, 2017 kati ya Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango na mkandarasi aitwaye Reynolds Construction Company kutoka nchini Nigeria kwa gharama ya Euro 40,441,890.81 bila VAT na inasimamiwa na Mhandisi Mshauri aitwaye Nicholas O,Dwyer Company Limited kutoka Ireland kwa gharama ya Euro 1,648,310.00 ambapo ujenzi wake unatarajiwa kukamilika tarehe 2 Aprili, 2020.
Mheshimiwa Spika, hadi sasa mkandarasi ameleta mitambo eneo la kazi kwa asilimia 90 na amekamilisha ujenzi wa kambi na maabara ya vifaa vya ujenzi kwa asilimia 100. Aidha, mkandarasi anaendelea na upimaji wa barabara, uhamishaji wa nguzo za umeme, simu na mabomba ya maji na kusafisha eneo la barabara pamoja na kujenga njia za mchepuo. Maandalizi ya eneo la kusaga kokoto na kufanya matengenezo ya kawaida ya barabara ya kutoka Kidatu hadi Ifakara ili iendelee kupitika majira yote ya mwaka.
MHE. HASSAN S. KAUNJE aliuliza:-
TANROADS ilifanya upanuzi wa Road Reserve tangu mwaka 2011 ambayo ilihusisha tathmini ya mali zilizopo kwenye maeneo husika:-
Je, ni lini wananchi wa Lindi watalipwa stahili zao?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Kaunje, Mbunge wa Lindi Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa Sheria ya Barabara ya Mwaka 2007 na Kanuni za Menejimenti ya Barabara za Mwaka 2009 iliongeza eneo la hifadhi ya barabara kutoka mita 22.5 mpaka mita 30 kwa barabara kuu na barabara za mikoa kutoka katikati ya barabara kila upande wa barabara. Kwa kuzingatia sheria ya zamani ya barabara (highway Ordinance Cap. 167) wananchi waliojenga ndani ya mita 22.5 kutoka katikati ya barabara wamevunja sheria hivyo Wizara kupitia TANROADS imekuwa ikichukua hatua ya kuweka alama za X nyekundu na wananchi hao wanatakiwa waondoke eneo hilo na hawatalipiwa fidia yoyote kwa mujibu wa sheria.
Mheshimiwa Spika Wizara kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) imechukua hatua ya kuweka kumbukumbu ya mali zote zilizopo ndani ya mita 7.5 zilizoongezeka kutoka eneo la hifadhi ya barabara la mita 22.5 hadi mita 30 kila upande wa barabara kwa kuziwekea alama ya X ya kijani kwa ajili ya uthamini na malipo ya fidia endapo eneo hilo litahitajika hapo baadaye kwa ajili ya ujenzi na upanuzi wa barabara.
MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-

Uwanja wa Ndege wa Njombe umekuwa kero kwa wananchi, kwani upo katikati ya Mji na haujakarabatiwa kwa muda mrefu matokeo yake uwanja huo umejaa barabara hizo. Aidha, watu wanaopita katika barabara hizo zisizo rasmi hukamatwa na kutozwa faini:-

Je, ni lini mkakati wa Serikali juu ya uwanja huo ili kupunguza kero kwa wananchi hao?
NAIBU WAZIRI, UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanja cha ndege cha Njombe kilijengwa na Wakoloni, yaani kabla ya uhuru miaka ya 1940 na kuanza kutumika rasmi 1945. Miaka hiyo Mji wa Njombe ulikuwa mdogo sana na hivyo kiwanja kilikuwa mbali na makazi ya watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria za Kitamaifa za Usalama wa Anga hairuhusiwi watu, wanyama, magari na kadhalika kukatiza kwenye viwanja vyovyote vya ndege. Kwa mantiki hiyo, vitendo vya baadhi ya wananchi wa maeneo hayo kukatiza katika kiwanja hicho ni vya uvunjivu wa sheria na ndiyo maana wananchi hao hukamatwa na kutozwa faini au kuadhibiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika juhudi za kukarabati kiwanja cha ndege cha Njombe, Serikali imepanga kufanya upembuzi yanikifu na usanifu wa kina kwa kutumia fedha za mkopo kutoka Benki ya Dunia uliohusisha pia viwanja vya ndege vya Iringa, Songea, Lindi, Kilwa Masoko, Tanga, Moshi, Lake Manyara, Singida, Musoma na kiwanja kipya cha Mkoa wa Simiyu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina imekamilika kwa viwanja hivyo ambapo taarifa ya mwisho iliwasilishwa tarehe 28 Machi, 2017. Hatua iliyopo kwa sasa ni utafutaji wa fedha kutoka vyanzo mbalimbali kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa kiwanja hicho. Upanuzi huo utahusisha ujenzi wa uzio kuzunguka eneo lote la kiwanja ili kudhibiti wananchi wanaokatisha kiwanja hicho kinyume cha taratibu.
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE aliuliza-:-

Je, Serikali itakamilisha lini ujenzi wa barabara ya kutoka Kibaoni kupitia Majimoto mpaka Inyonga kwa kiwango cha lami ukizingatia kuwa daraja la Kavuu limekwishakamilika ili barabara hiyo ianze kutumika?
NAIBU WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:--

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Pudenciana Wilfred Kikwembe, Mbunge wa Kavuu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kibaoni-Majimoto- Inyonga ni barabara ya mkoa yenye urefu wa kilometa 152 inayohudumiwa na Wakala wa Barabara (TANROADS) Mkoa wa Katavi. Barabara hii ni ya changarawe na inapitika majira yote ya mwaka.

Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa barabara hii, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) imetangaza zabuni kwa ajili ya kumpata Mhandisi Mshauri wa kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ikiwa ni pamoja na kuandaa nyaraka za zabuni kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami. Zabuni kwa ajili ya kazi hiyo zinatarajiwa kufunguliwa taehe 11 Februari, 2019.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hatua hizo, Serikali imeanza kujenga sehemu ya barabara hii kwa awamu kwa kiwango cha lami kuanzia Mji wa Inyonga ambapo katika mwaka wa fedha 2017/2018, jumla ya kilometa 1.7 zilijengwa. Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019 mkandarasi wa kujenga kilometa 2.5 amepatikana na yupo katika hatua za maandalizi ya kuleta vifaa na wataalam katika eneo la mradi ili kuanza kazi.
MHE. DEO K. SANGA aliuza:-

Serikali ilichukua eneo la Idofu kwa ajili ya kujenga One Stop Center lakini hadi leo wananchi hawajalipwa fidia:-

(a) Je, ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi hao?

(b) Je, ni lini Serikali itaanza kujenga One Stop Center kama ilivyokudia?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga, Mbunge wa Makambako, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilifanya uthamini wa eneo kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Ukaguzi wa Pamoja (One Stop Inspection Station – OSIS) cha Makamboko katika eneo la Idofu Makambako. Tayari kazi ya uthamini wa mali na mazao yatakayoathiriwa na mradi huo imekamika. Wananchi ambapo mali zao zimeathirika na maradi watalipwa fidia kwa kuzingatia Sheria Na.4 ya Ardhi ya mwaka 2001 kabla ya ujenzi wa kituo cha ukaguzi wa kuanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tayari imeanza hatua za maandalizi ya awali wa ujenzi wa Kituo cha Ukaguzi wa pamoja kwa kusaini mkataba na Mhandisi Mshauri UWP Consulting (T) Limited akishirikiana na UWP Consulting ya Afrika kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na uandaaji wa nyaraka za zabuni kwa vituo vya Ukaguzi wa Pamoja vya Mikumi, Makambako na Mpemba. Mhandisi Mshauri amekamilisha kazi ya awamu ya kwanza ya upembuzi yakinifu na usanifu wa awali mwezi Juni, 2018. Kazi ya usanifu wa kina itakamilika mwishoni mwa mwezi Februari, 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi hizi zinatekelezwa kwa fedha za mkopo kutoka Benki ya Dunia. Malipo ya fidia yakikamilika na Serikali kupata fedha ndipo ujenzi kwa Kituo cha Ukaguzi wa Pamoja cha Makambako utaanza.
MHE. IGNAS A. MALOCHA (K.n. y. MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI) aliuliza:-

Tunaishukuru Serikali kwa kutujengea barabara ya lami kutoka Mpanda –Sumbawanga:-

Je, ni lini Serikali itamaliza kipande cha kilomita 86 eneo la Hifadhi ya Katavi kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sebastian Simon Kapufi, Mbunge wa Mpanda Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Sumbawanga hadi Mpanda yenye urefu wa km 245 ilifanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina mwaka 2009. Serikali kwa kutumia fedha za ndani imekamilisha ujenzi wa kilometa 188.5 kwa kiwango cha lami sehemu za Sumbawanga - Kanazi, (kilometa 75), Kanazi - Kizi - Kibaoni (kilometa 76.6) na Sitalike – Mpanda (kiolometa 36.9).

Mheshimiwa Spika, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa Serikali inatambua umuhimu wa kuunganisha Mkoa wa Rukwa na Katavi kwa barabara ya lami, hivyo ujenzi wa sehemu iliyobaki kati ya Kizi - Lyamba Lya Mfipa - Stalike (kilometa 86) utaanza mara moja kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. SUSAN L. KIWANGA aliuliza:-

Barabara kutoka Ifakara hadi Mlimba mpakani mwa Mkoa wa Njombe (Madeke) ni kero kubwa kwa wananchi wa Jimbo la Mlimba:-

Je, ni lini Serikali itajenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Susan Limbweni Kiwanga, Mbunge wa Mlimba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Ifakara – Mlimba – Taweta - Madeke yenye urefu wa kilometa 220.22 inaunganisha Mkoa wa Morogoro na Njombe katika Kijiji cha Madeke. Barabara hii ni ya changarawe na udongo ambapo sehemu kubwa inapitika vizuri isipokuwa maeneo yanayohitaji kuimarishwa ili nayo yapitike wakati wote wa mwaka.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, Serikali imeshakamilisha kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa sehemu ya barabara kutoka Ifakara Kihansi (km 126) ikiwa ni hatua ya awali ya kuanza mipango ya ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami. Hatua hiyo itawezesha kuunganisha sehemu ya barabara hiyo na kipande cha barabara ya lami yenye urefu wa kilometa 24 kilichojengwa hapo awali kati ya Kihansi na Mlimba. Kufuatia kukamilika kwa hatua hiyo, Serikali imeanza kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, aidha, katika mwaka wa fedha wa 2019/2020 kipande kilichobaki kati ya Mlimba hadi Taweta kimewekwa kwenye mpango ili kufanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Serikali itaendelea kutenga fedha za matengenezo ili barabara hii iweze kupitika wakati wote wa mwaka wakati fedha za ujenzi kwa kiwango cha lami zinatafutwa.
MHE. RICHARD M. NDASSA aliuliza:-

Usanifu wa kina wa barabara ya Isandula (Magu) – Bukwimba Station – Ngudu hadi Hungumalwa ambayo ni kilometa 74 umeshakamilika:-

Je, ni lini barabara hiyo itaingizwa kwenye bajeti ili ijengwe kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Richard Mganga Ndassa, Mbunge wa Sumve, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Isandula hadi Hungumalwa yenye urefu wa kilometa 71 ni Barabara ya Mkoa inayohudumiwa na Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS). Barabara hii inapita katika Mji wa Bukwimba, Nyambiti na Ngudu na ni barabara muhimu katika kukuza uchumi wa Wilaya za Magu, Sumve na Ngudu. Barabara hii pia ni kiungo kati ya barabara kuu ya Mwanza – Sirari na Mwanza – Shinyanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua umuhimu huo, Wizara yangu inaifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina barabara hiyo kwa lengo la kuijenga kwa kiwango cha lami. Kazi ya usanifu wa kina inatarajiwa kukamilika mwezi Mei, 2019. Baada ya usanifu huo kukamilika na gharama kujulikana, barabara hiyo itaingizwa kwenye mpango wa ujenzi kwa kiwango cha lami kutegemeana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati ujenzi huo wa kiwango cha lami ukisubiriwa, Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS) itaendelea kuifanyia matengenezo barabara hiyo kuhakikisha kuwa inapitika majira yote.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA aliuliza:-

Barabara ya Kyaka – Kasulu hadi Benako Ngara imeishia Bugene:-

Je, ni lini barabara hiyo ya lami itajengwa hadi Benako?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oliver Daniel Semguruka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Kyaka – Bugene – Kasulo (Buneko) yenye urefu wa kilometa 178 ni barabara kuu na inahudumiwa na Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS) Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara hii kiuchumi na kijamii iliamua kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Awamu ya kwanza ilihusisha sehemu ya barabara toka Kyaka hadi Bugene (Nyakahanga) yenye urefu wa kilometa 59.1. Sehemu hiyo tayari imekamilika kujengwa kwa kiwango la lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, awamu ya pili inahusisha sehemu ya barabara kutoka Bugene hadi Kasulo (Benako) yenye urefu wa kilometa 118.9. Sehemu hii kwa sasa inafanyiwa upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na uandaaji wa nyaraka za zabuni kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami. Kazi hii ipo katika hatua za mwisho chini ya Mhandisi Mshauri LEA International Ltd ya Canada ikishirikiana na LEA International Ltd ya Asia Kusini. Kazi hii inagharamiwa na Jumuiya ya Nchi za Afrika Mashariki na itajengwa kupitia mradi huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati sehemu hiyo ikisubiriwa kujengwa kwa kiwango cha lami, Wizara itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kufanyia matengenezo mbalimbali ili kuhakikisha kuwa barabara hii inapitika vizuri majira yote. Katika mwaka wa fedha 2018/2019 jumla ya shilingi milioni 650.371 zimetengwa kwa ajili ya matengenezo mbalimbali ya barabara hiyo.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA aliuliza:-

Serikali inajitahidi kujenga barabara ili kupunguza foleni pamoja na kurahisisha usarifi na usafirishaji, lakini barabara zinawekwa matuta ambayo siyo rafiki kwa vyombo vya usafiri jambo linalosababisha baadhi ya watumiaji wa barabara hizo kuzikimbia, kwa mfano, matuta yaliyowekwa katika barabara ya Msata – Bagamoyo:-

Je, matuta ni sehemu ya alama za barabarani?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Ally Mtolea, Mbunge wa Temeke, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, alama za barabarani hutumika kutoa ujumbe wa matumizi sahihi ya barabara katika eneo husika. Alama hizo huwekwa kwenye milingoti pembezo mwa barabara au huchorwa katika uso wa barabara kutoa tafsiri sahihi ya matumizi ya barabara. Hata hivyo, kutokana na baadhi ya madereva kutozingatia alama za barabarani hususan, alama za ukomo wa mwendo (speed limit), Serikali hulazimika kujenga matuta katika maeneo ambayo ni hatarishi ili kuwalazimisha madereva kupunguza mwendo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua kuwa baadhi ya matuta ya barabarani siyo rafiki kwa vyombo vya usafiri, Serikali iliandaa mwongozo wa usanifu wa barabara wa mwaka 2011 Road Geometric Design Manual, 2011 ambapo pamoja na mambo mengine, imeweka viwango bora vya ujenzi wa matuta barabarani. Kwa kuzingatia mwongozo huo, Wizara yangu kupitia TANROADS imepitia upya matuta yote yaliyojengwa katika barabara kuu hapa nchini na kubaini kuwa matuta 323 siyo rafiki kwa vyombo vya usafiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya uboreshaji wa matuta hayo inaendelea ambapo hadi sasa matuta 281 yemerekebishwa. Baadhi ya barabara ambazo matuta yamerekebishwa ni Kibaha - Mlandizi (6), Morogoro – Iringa (12), Mara – Simiyu (matuta 12), Igawa – Songwe (matuta matatu), Uyole – Kasumulu (matuta mawili) Mwanza – Simiyu (matuta tisa), Shelui – Nzega (matuta matano), Singida – Manyara (matuta 23), Mtukula – Bukoba (matuta saba) pamoja na maeneo mengine kwa ujumla (matuta 202).

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge na wananchi kwa ujumla kuwa matuta yote ambayo hayastahili kuwepo barabarani yataondolewa na yale ambayo hayakidhi kiwango yatajengwa upya. Aidha, natoa wito kwa madereva wote nchini kuzingatia alama za barabarani ikiwemo alama za ukomo wa mwendo (Speed limit).
MHE. ALHAJ ABDALLAH M. BULEMBO aliuliza:-

Mheshimiwa Rais alipofungua Uwanja wa Ndege wa Bukoba alisema kuwa Uwanja wa Kanjunguti hautajengwa tena, badala yake shilingi bilioni tano zilizokusudiwa kutumika huko Omukajunguti ziende kwenye upanuzi wa kiwanja cha Bukoba:-

(a) Je, ni lini Serikali itatekeleza agizo la Mheshimiwa Rais?

(b) Je, Serikali haioni ni tatizo kwa utuaji wa ndege kutokana na hali ya hewa ya eneo hilo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Alhaj Abdallah Majurah Bulembo, Mbunge wa Kuteuliwa, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa uzinduzi wa kiwanja cha ndege cha Bukoba tarehe 6 Novemba, 2017, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, aliagiza ufanyike uchambuzi wa kina, kama kuna haja ya kujenga kiwanja kipya cha ndege katika eneo la Omukajunguti au kupanua kiwanja cha ndege kilichopo Bukoba, yaani kutoka Daraja la II C hadi Daraja la II C.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na agizo hilo la Mheshimiwa Rais, Serikali iliunda timu ya wataalam ili wafanye uchambuzi wa kina na hatimaye waweze kuishauri Serikali ipasavyo. Baada ya uchambuzi, timu hii ya wataalam ilibaini mambo yafuatayo:-

(1) Kupanua kiwanja cha ndege cha Bukoga kutoka Daraja la II C hadi la III C, kutahitaji utoaji wa ardhi isiyopungua hekari 75 ambayo tayari imeendelezwa. Ardhi hii inayohitajika itagusa nyumba za makazi zipatazo 200, Kituo cha Afya Zamzam, Makanisa mawili (WinnerS Chapel na Pentekoste Assembly of God), Msikiti, Shule za Msingi mbili, Zamzam na Bilele, barabara za Kashozi na Kashai pamoja na kuziba njia ya Mto Kanoni.

(2) Kupanua kiwanda hiki, kutasababisha jengo la abiria kuhamishwa ili kukidhi matakwa ya kiusalama ya usafiri wa anga. Pia kutakuwa na ugumu wa kupata eneo la kusimika taa za kumsaidi rubani kutua.

(3) Kutakuwa na ugumu wa kukiendeleza kiwanja hiki kufikia madaraja ya juu zaidi huko mbeleni.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kubaini mambo hayo, wataalam walitoa ushauri ufuatao kwa Serikali:-

(1) Kwa sasa Kiwanja cha Ndege cha Bukoba hakina eneo la kutosha kwa Daraja la II C, tunakipandisha kwenda daraja la juu, ardhi zaidi itahitajika.

(2) Kwa sasa Kiwanja cha Ndege cha Bukoba kinafaa kusimikwa sehemu ya taa (AGL System) za kukiwezesha kufanya kazi usiku na mchana.

(3) Uongozi wa Mkoa wa Kagera ufanye utafiti wa kina (detail survey) kujua gharama na athari za utoaji wa ardhi inayotakiwa kwa ajili ya upanuzi wa kiwanja ndege cha Bukoba.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati Serikali ikiendelea kushughulikia mapendekezo haya ya wataalam, sehemu ya fedha iliyokuwa itumike kulipa fidia kwenye eneo la Omukajunguti, zitatumika kusimika taa katika Kiwanja cha Ndege cha Bukoba ili zisaidie marubani wakati wa uwepo wa hali mbaya ya hewa, pia kukiwezesha kiwanja kutoa huduma usiku na mchana.
MHE. HASSAN E. MASALA aliuliza:-

Je, ni lini ujenzi wa barabara ya Masasi – Nachingwea – Ruangwa - Nanganga utaanza kufanyika kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Elias Masala, Mbunge wa Nachingwea, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Masasi – Nachingwea - Ruangwa hadi Nanganga yenye urefu wa kilometa 145 ni barabara ya Mkoa inayohudumiwa na Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS).

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na umuhimu wa barabara hii kiuchumi na kijamii, Serikali iliamua kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwe lengo la kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami, kazi ambayo ilikamilika mwaka 2018. Hivi sasa Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati Serikali inatafuta fedha za ujenzi wa barabara hii, itaendelea kutengewa fedha za matengenezo mbalimbali ili iendelee kupitika wakati wote ambapo katika mwaka wa fedha 2018/2019 jumla ya shilingi milioni 547.4 zimetengwa kwa ajili ya kuifanyia matengenezo barabara hiyo.
MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-

Barabara za Makete Njombe na Itone - Ludewa zipo katika ujenzi lakini ujenzi huo unakwenda pole pole sana:-

Je, ni lini ujenzi wa barabara hizo utakamilika?
NAIBU WAZIRI, UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Njombe - Makete kilometa 107.4 umejengwa katika sehemu mbili za Njombe - Moronga kilometa 53.9 na Moronga - Makete kilometa 53.5 ili kuharakisha utekelezaji wake. Hatua ya utekelezaji inayofikiwa hadi Machi, 2019 ni asilimia 25.2 ambapo kazi zinatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Januari, 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa ujenzi kwa kiwango cha zege wa barabara ya Itoni – Ludewa – Manda sehemu ya Rusitu - Mawengi kilometa 50 umefikia asilimia 20.14. Mradi huu unatarajiwa kukamilika mwezi Oktoba, 2020. Napenda nimkahakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa Wizara kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) itaendelea kuwasimamia Wakandarasi wa miradi hii ili waweze kukamilisha ujenzi wa barabara hiyo kwa wakati uliopangwa.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI aliuliza:-

Barabara ya Likuyufusi – Mkenda yenye urefu wa kilometa 123 inayounganisha nchi mbili za Tanzania na Msumbiji, bado haijaanza kujengwa kwa kiwango cha lami:-

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Likuyufusi – Mkenda yenye urefu wa kilometa 123 ni barabara kuu inayounganisha nchi mbili za Tanzania na Msumbiji na inahudumiwa na Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS).

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara hii iliamua kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa lengo la kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami, kazi ambayo ilikamilika mwaka 2013. Katika Mwaka wa Fedha 2018/2019 shilingi bilioni 5.86 zimetengwa kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwepo kwa uchimbaji na usafirishaji wa makaa ya mawe katika Kijiji cha Muhukuru kilicho kilometa 74 kutokea Songea katika barabara hiyo, kumesababisha kuongezeka kwa magari mengi na mazito yanayobeba makaa ya mawe. Kufuatia hali hiyo, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS) imeamua kufanya mapitio ya usanifu wa kina (Design Review) ili kukidhi mahitaji halisi yaliyojitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kazi hiyo kukamilika, Serikali itaendelea kutafuta fedha zaidi kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami.
MHE. FREDY A. MWAKIBETE aliuliza:-

Wananchi wa Busokelo katika Kata ya Luteba walianza kutengeneza barabara inayounganisha Mikoa ya Mbeya na Njombe kupitia Mlima ya safu za Livingstone:-

Je, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo kuunga mkono juhudi za wananchi hao?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fredy Atupele Mwakibete, Mbunge wa Busokelo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua Barabara ya Njombe-Makete-Isyonje Mbeya (kilometa 203.6) kama barabara rasmi inayounganisha Mikoa ya Njombe na Mbeya. Barabara anayoitaja Mheshimiwa Mbunge inayounganisha Wilaya ya Makete, Mkoa wa Njombe na Rungwe, Mkoa wa Mbeya ambayo ni barabara ya Mkoa. Aidha, kutoka Luteba hadi Ipelele katika Wilaya ya Makete kilometa 7.5, hakuna barabara inayoonekana wazi ni eneo la Milima mikali ya Livingstone.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara ya Njombe-Makate kilometa 107.4 ambayo ni sehemu ya barabara ya Njombe-Makate- Isyonje-Mbeya inayounganisha Mkoa wa Njombe na Mkoa wa Mbeya. Sehemu hii ya barabara hadi sasa ujenzi wake umefikia asilimia 26.

Mheshimiwa Spika, barabara inayopita katika safu ya Milima ya Livingstone inahitaji upembuzi yakinifu ambao ndiyo itakuwa msingi wa kufanya maamuzi. Kuhusu sehemu inayotengenezwa na wananchi katika safu ya Mlima Livingstone, Serikali itaangalia namna ya kusaidiana na wananchi waliojitolea kutengeneza sehemu hiyo ya barabara pamoja na upatikanaji wa fedha.
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA aliuliza:-

Ujenzi wa Barabara ya Makofia-Mlandizi-Vikumburu kwa lami ni ahadi ya Ilani ya CCM tangu mwaka 2010, na kwa sababu upembuzi yakinifu na usanifu wa barabara hiyo umekamilika:-

Je, ni lini ujenzi wa barabara hiyo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Shukuru Jumanne Kawambwa, Mbunge wa Bagamoyo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Makofia-Mlandizi- Vikumburu ni barabara ya mkoa inayohudumiwa na Wizara yangu kupitia TANROADS Mkoa wa Pwani inayounganisha Wilaya za Bagamoyo, Kibaha na Kisarawe. Serikali imeanza mpango wa kuijenga barabara ya Makofia-Mlandizi- Vikumburu kwa kuanza na hatua ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina pamoja na kuandaa nyaraka za zabuni na uthamini wa mali zitakazoathiriwa na ujenzi.

Mheshimiwa Spika, kazi ya usanifu ilikamilika Agosti, 2017 kwa kipande cha Makofia-Mlandizi na kipande cha Malandizi-Maneromango usanifu ulikamilika Novemba, 2018. Baada ya usanifu wa sehemu iliyobaki ya Maneromango- Vikumburu kukamilika na gharama ya barabara nzima kujulikana, ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara hii utaanza kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, wakati Serikali ikiedelea kutafuta fedha za ujenzi, barabara hii itaendelea kufanyiwa matengenezo mbalimbali ili kuendelea kupitika kipindi chote cha mwaka. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, jumla ya Sh.753,381,515 zimetengwa kwa ajili ya kuifanyia matengenezo mbalimbali barabara hii.
MHE. OMARI A. KIGODA aliuliza:-

Je, ni lini hatma ya kipande cha barabara ya Handeni- Mziha ambacho Serikali iliahidi kwamba Mkandarasi akishalipwa ujenzi utaanza, hasa ikizingatiwa kuwa barabara hiyo inaunganisha mikoa miwili?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Omari Abdallah Kigoda, Mbunge wa Handeni Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Handeni- Mziha yenye urefu wa kilometa 70.1 ni sehemu ya barabara ya Handeni- Mziha-Turiani-Dumila yenye urefu wa kilometa 154.7. Sehemu ya Handeni –Mziha (kilomita 70.1) iko katika Mkoa wa Tanga na inahudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Tanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Handeni – Mziha-Turiani umekamilika. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali imetenga jumla ya shilingi bilioni mbili kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara ya Handeni- Mziha- Turiani kilometa 104 kwa kiwango cha lami. Aidha, katika mwaka wa Fedha 2019/2020 tumepanga kuitengea barabara hii fedha za ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako kuwa nia ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kuijenga kwa kiwango cha lami barabara ya Handeni –Mziha-Turiani ili kuiunganisha Mikoa ya Tanga na Morogoro kwa lengo la kuchochea na kuinua uchumi wa maeneo husika.
MHE. MAHMOUD H. MGIMWA aliuliza:-

Barabara ya kutoka Kinyanambo A – Isalavamu – Igombavanu – Sadani hadi Madibira ilikuwepo kwenye Ilani ya CCM ya mwaka 2005 – 2010 na 2010 – 2015 lakini hadi sasa haijajengwa kwa kiwango cha lami:-

(a) Je, ni sababu zipi zilizofanya Serikali kutoanza ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami, hasa ikizingatiwa kuwa barabara hiyo ni muhimu kwa uchumi wa Wilaya za Mbarali na Mufindi?

(b) Je, ni lini sasa ujenzi wa barabara hiyo utaanza?

(c) Je, ni lini Serikali itaanza uthamini kwa ajili ya kuwalipa fidia wananchi wanaopisha ujenzi wa barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mahmoud Hassan Mgimwa, Mbunge wa Mufindi Kaskazini, lenye Sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kinyanambo (Mafinga) – Madibira ni barabara ya Mkoa inayosimamiwa na Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na inajulikana kama Barabara ya Rujewa – Madibira – Kinyanambo yenye urefu wa kilometa 152. Barabara hii ambayo kwa sasa ipo katika kiwango cha changarawe, ikiunganisha Mkoa wa Iringa, sehemu ya Kinyanambo na Mkoa wa Mbeya sehemu ya Madibira, imepita maeneo muhimu yenye kilimo cha mahindi na mpunga.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) tayari imefanya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na kuandaa nyaraka za zabuni kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami. Kazi hii ilikamilika mwaka 2009 ikiwa ni pamoja na kufanya uthamini kwa ajili ya kuwalipa fidia wananchi watakaopisha ujenzi wa barabara hiyo.

Mheshimiwa Spika, Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara hiyo kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Hata hivyo, wakati Serikali inatafuta fedha za ujenzi barabara hiyo, itaendelea kufanyiwa matengenezo mbalimbali kila mwaka ili iweze kupitika majira yote ya mwaka.
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itavunja Bodi za Wahandisi kutokana na kauli ya Mheshimiwa Rais?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maftaha Abdallah Nachuma, Mbunge wa Mtwara Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Usajili wa Wahandisi ilianzishwa chini ya Sheria ya Usajili wa Wahandisi Na. 15 ya mwaka 1997. Bodi hii inalo jukumu la kusajili wahandisi na makampuni ya kihandisi pamoja na kusimamia shughuli za uhandisi na mwenendo wa wahandisi na makampuni ya ushauri wa kihandisi hapa nchini. Kwa kuzingatia majukumu iliyopewa, Bodi ya Usajili wa Wahandisi tangu kuanzishwa kwake imekuwa ikitekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa na kwa mujibu wa sheria iliyoanzisha bodi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa, moja ya Bodi zinazofanya kazi vizuri na kwa weledi wa kutosha ni Bodi ya Usajili wa Wahandisi na baadhi ya mafanikio yaliyopatikana kutokana na kuanzishwa kwa Bodi hiyo ni kusajili jumla ya wahandisi 25,263 katika madaraja tofauti hadi kufikia Machi, 2019. Sambamba na hilo, makampuni ya ushauri ya kihandisi yapatayo 338 yameweza kusajiliwa katika kipindi hicho zikiwemo maabara za upimaji vifaa vya ujenzi 32.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano haina kumbukumbu zozote zinazoonyesha kuwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliwahi kutoa kauli ya kuivunja Bodi ya Usajili wa Wahandisi.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA aliuliza:-

Je, ni lini ujenzi wa barabara ya mchepuo ya Mlima Nyoka - Songwe yenye urefu wa kilometa 48.9 utaanza baada ya ya usanifu na upembuzi yakinifu kukamilika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Hebron Mwakagenda, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa ujenzi wa barababa ya mchepuo inayoanzia Uyole yaani Mlima Nyoka hadi Songwe kilomita 48.9 ni mahsusi kwa ajili ya kupunguza msongamano wa magari katika barabara kuu ya TANZAM katika Jiji la Mbeya.

Mheshimiwa Spika, upembuzi na usanifu wa kina wa barabara hii ulikamilika chini ya usimamizi wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Hata hivyo, ilionekana kuwa ipo haja ya kufanya mapitio ya usanifu huo ambao katika mwaka wa fedha 2018/ 2019 kiasi cha shilingi milioni 2.6 kimetengwakwa ajili kupitia na kukamilisha usanifu huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi huu umeingizwa kwenye mradi wa ukarabati wa barabara kuu ya TANZAM kuanzia Igawa hadi Tunduma unaofandhiliwa na Benki ya Dunia kwa kushirikiana na Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, mkataba ulisainiwa tarehe 18 Disemba, 2018 kati ya Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na Mhandisi Mshauri Studio International ya Tunisia ikishirikiana na Global Professional Engineering Service ya Tanzania kwa ajili ya kazi ya mapitio ya usanifu wa kina wa barabara hii. Kazi hii inatarajiwa kukamilika tarehe 18 Februari, 2020. Hadi sasa Mhandisi Mshauri yupo eneo la mradi anaendelea na kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara hii itakapokamilika na Serikali kupata fedha, ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami utaanza.
MHE. SEIF K. GULAMALI aliuliza:-

Wakati wa Kampeni za Uchaguzi Mheshimiwa Rais aliahidi kujenga barabara za Ziba - Puge na Ziba - Choma kwa kiwango cha lami:-

Je, ni lini Serikali itetenga fedha za usanifu wa barabara hizo na hatimaye kuanza ujenzi ili kutimiza ahadi ya Mheshimiwa Rais?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Seif Khamis Gulamali, Mbunge wa Manonga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Ziba - Puge yenye urefu wa kilometa 83.06 na barabara ya Ziba - Choma yenye urefu wa kilometa 26.6 ni barabara za Mkoa zinazohudumiwa na Wakala wa Barabara TANROADS, Mkoa wa Tabora.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Puge - Ziba na barabara ya Ziba - Choma zitakuwa miongoni mwa barabara zitakazopewa kipaumbele katika kutengewa fedha kwa ajili ya kuzifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa lengo la kujenga barabara hizo kwa kiwango cha lami. Aidha, Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara hizo imekuwa ikizitengea fedha kila mwaka kwa ajili ya matengenezo mbalimbali ili ziendelee kupitika majira yote ya mwaka. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, kiasi cha shilingi milioni 712.922 kimetengwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara ya Puge - Ziba na kiasi cha shilingi milioni 170.3 kimetengwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara ya Ziba - Choma.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE aliuliza:-

Daraja la Godegode limesombwa na maji wakati wa mvua za masika na daraja hilo ni kiungo kikubwa kati ya Jimbo la Kibakwe na Jimbo la Mpwapwa ambalo ndiyo Makao Makuu ya Wilaya Mpwapwa.

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga daraja hilo ili kurudisha mawasiliano kati ya Wananchi na Kata za Godegode, Pwaga, Lumuma, Mbuga na Galigali?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa George Malima Lubeleje, Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli daraja la Godegode lilisombwa na maji wakati wa mvua kubwa iliyonyesha kipindi ha masika mwaka 2018. Kwa kuzingatia umuhimu wa daraja hilo, Serikali ina mpango wa kurudisha mawasiliano kati ya Mpwapwa na Kata ya Godegode, Pwaga, Lumuma, Mbuga na Galigali kwa kujenga Daraja jipya. Ujenzi wa Daraja hilo utaanza kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2019/20 ambapo jumla ya shilingi milioni 325 imetengwa kwa ajili ya kazi hiyo.
MHE. HUSSEIN N. AMAR aliuliza:-

Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, katika ziara yake Wilayani Nyang’hwale tarehe 11 Novemba, 2013 akiongozana na aliyekuwa Waziri wa ujenzi Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Mheshimiwa Kassim Majaliwa Najaliwa alitoa ahadi kwa wananchi ya kujenga barabara ya kutoka Busisi – Busolwa – Nyijundu – Kharumwa, Bukwimba hadi Nyang’holongo kuelekea Kahama Mjini kwa kiwango cha lami pamoja na kuondoa tatizo la mawasiliano ya simu:-

(a) Je, ni lini ahadi hiyo ya viongozi wakuu wa nchi itatekelezwa?

(b) Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi hizo kwa kujenga minara ya mawasiliano ya simu ili maeneo ya Nyamtukuza, Kanegere, Nyugwa na maeneo mengine yaweze kusikika na kuchochea maendeleo ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa, Hussein Nassor Amar, Mbunge wa Nyang’hwale, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Busisi – Busolwa – Nyijundu – Kalumwa – Bukwimba – Nyang’hongo hadi Kahama yenye urefu wa kilometa 204.68 ni barabara ya mkoa inayohudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) iliyoko katika Mikoa ya Mwanza kilometa 41, Mkoa wa Geita kilometa 68.68 na Mkoa wa Shinyanga kilometa 95.

Mheshimiwa Spika, ahadi ya viongozi wa nchi ikiwemo ahadi ya ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara tajwa itatekelezwa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Wakati Serikali ikiendelea kutafuta fedha, barabara hii itaendelea kufanyiwa matengenezo mbalimbali ili iendelee kupitika majira yote ya mwaka.

(b) Mheshimiwa Spika, kufuatia ahadi iliyotolewa na Rais Awamu ya Nne na utekelezaji wa Sera ya Serikali, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote iliainisha uhitaji wa mawasiliano katika Wilaya ya Nyang’hwale yakiwemo ya maeneo ya yaliyoahidiwa ili kutambua maeneo yote yenye uhitaji wa mawasiliano kwa ajili ya ufikishaji wa huduma hiyo.

Mheshimiwa Spika, kabla ya tathmini hiyo, Serikali ilikuwa imejenga mnara wa mawasiliano katika Kata ya Shabaka mwaka 2013 yenye wakazi takribani 12,072 katika mradi uliotekelezwa na Kampuni ya Vodacom.

Mheshimiwa Spika, baada ya uainishaji kukamilika na ukubwa wa uhitaji kubainika, Januari 2014, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote ilitangaza zabuni ya kufikia huduma za mawasiliano katika Kata za Busolwa, Kafita, Kakora, Nyijundu, Mwingiro, Nyabulanda na Nyugwa. Utekelezaji ulianza Aprili, 2015 ambapo wakazi zaidi ya 68,544 ikiwemo Kata ya Nyugwa wamefikishiwa huduma ya mawasiliano.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali itaendelea kutekeleza ahadi iliyotolewa kwa maeneo yaliyobaki ya Nyamtukuza, Kanegere na maeneo mengine ili yaweze kusikika na kuchochea maendeleo katika maeneo husika kadri ya upatikanaji wa fedha, hususan katika mwaka wa fedha 2019/2020.
MHE. AHMED A. SALUM aliuliza:-

Usanifu na upembuzi yakinifu wa barabara ya kutoka Mwanza – Solwa – Bulige kwa kiwango cha lami umekamilika:-

Je, ni lini mradi huu utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ahmed Ally Salum, Mbunge wa Solwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Mwanangwa – Misasi – Salawe – Solwa – Kahama yenye urefu wa kilometa 150 ni barabara ya mkoa inayohudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kupitia Mikoa ya Mwanza na Shinyanga. Kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa ajili ya kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami ilikamilika Desemba, 2017 kwa gharama ya shilingi milioni 798.8.

Mheshimiwa Spika, kipaumbele cha Serikali sasa ni kuunganisha Makao Makuu ya Mkoa na nchi jirani kwa barabara za lami zilizoainishwa kwenye Shoroba za Maendeleo (Development Corridor). Barabara nyingine ikiwemo ya Mwanangwa – Misasi – Salawe – Solwa – Kahama itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, Serikali imeendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuifanyia matengenezo barabara hii ili ipitike majira yote ya mwaka. Katika mwaka wa fedha 2019/2020 kiasi cha shilingi bilioni 1.6 zimetengwa.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa barabara ya Lushoto – Mlalo kilomita 45 kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Lushoto – Mlalo yenye urefu wa kilometa 41.93 ni sehemu ya barabara ya Mkoa ya Lushoto – Mlalo – Umba Junction yenye urefu wa kilometa 66.23 inayohudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS).

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, ilianza kuijenga kwa kiwango cha lami kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Hadi kufikia Mwaka wa Fedha 2018/2019, jumla ya kilometa 8.6 zimeshakamilika kwa gharama ya Sh.5,263,802,375. Aidha, katika Mwaka wa Fedha 2019/2020, Serikali imeendelea kuitengea fedha barabara hii kwa ajili ya kuendelea na ujenzi. Sehemu iliyobaki yenye urefu wa kilometa 33 itaendelea kujengwa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA aliuliza:-

Ujenzi wa Barabara ya Mtwara – Newala – Masasi (kilometa 210) umeanza kwa kiwango cha lami kutoka Mtwara hadi Mnivata (kilometa 50).

Je, Serikali ina mpango gani kwa kilometa 160 zilizobaki?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota, Mbunge wa Nanyamba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa barabara yote ya Mtwara – Nanyamba – Tandahimba – Newala – Masasi, kilometa 210, pamoja na Daraja la Mwiti ulikamilika mwaka 2015. Mpango wa Serikali ni kujenga barabara yote kwa kiwango cha lami kwa awamu. Awamu ya kwanza inahusisha sehemu ya Mtwara – Mnivata, kilomita 50, ambayo utekelezaji wake hadi kufikia Desemba, 2019 ulikuwa asilimia 76. Jumla ya shilingi bilioni 3.4 zimetengwa katika mwaka wa fedha 2019/2020 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi.

Mheshimiwa Spika, ujenzi kwa kiwango cha lami kwa kilometa 160 zilizobaki pamoja na Daraja la Mwiti utaanza katika mwaka wa fedha 2020/2021.
MHE. ALLAN J. KIULA aliuliza:-

Barabara itokayo Iguguno –Nduguti –Sibiti hadi Meatu ni kiungo muhimu cha Mikoa ya Singida na Simiyu:-

Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara hiyo hasa ikizingatiwa kuwa kazi kubwa ya ujenzi wa Daraja la Sibiti imekamilika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Allan Joseph Kiula, Mbunge wa Iramba Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Bariadi – Kisesa – Mwandoya – Ngoboko – Mwanhuzi – Sibiti – Mkalama hadi Iguguno Shamba yenye urefu wa kilometa 289 ni barabara ya Mkoa inayohudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS). Sehemu kubwa ya barabara hii ni ya changarawe na inapitika wakati wote wa mwaka.

Aidha, ujenzi wa Daraja la Sibiti na barabara unganishi kwa kiwango cha changarawe zenye urefu wa kilometa 25 umekamilika. Hata hivyo, taratibu za manunuzi ziko katika hatua ya mwisho kwa ajili ya kuzijenga kwa kiwango cha lami barabara hizo unganishi zenye jumla ya urefu wa kilometa 25.

Mheshimiwa Spika, pamoja na juhudi nilizotaja, mkakati wa Serikali kwa sasa ni kukamilisha kuunganisha makao makuu ya mikoa kwa barabara za lami na kujenga barabara kuu zote zinazounganisha Tanzania na nchi jirani kwa kiwango cha lami kama ilivyoainishwa kwenye Shoroba za Maendeleo (Development Corridors). Baada ya hapo, barabara nyingine ikiwempo ya Iguguno – Mkalama – Sibiti – Mwanhuzi – Ngoboko – Bariadi zitafuata kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. AUG USTINE V. HOLLE aliuliza:-

Je, ni lini ujenzi wa barabara ya Kasulu Mjini hadi Kibondo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Augustine Vuma Holle, Mbunge wa Kasulu Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kasulu Mjini - Kibondo kilometa 149 ni sehemu ya barabara ya Nyakanazi - Kasulu kilometa 236 kuelekea hadi Kigoma na pia kutokea Kasulu kuelekea Manyovu/mpakani mwa Tanzania na Burundi kilometa 68.25.

Mheshimiwa Spika, Serikali tayari imechukua hatua kadhaa za kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami ambapo kwa kupitia Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) zimepatikana fedha kwa ajili ya ujenzi wa kiwango cha lami kwa sehemu ya Kabingo – Kasulu – Manyovu kilometa 260.6.

Mheshimiwa Spika, kwa hivi sasa maandalizi ya kusaini mikataba ya ujenzi yanaendelea na kazi za ujenzi zinatarajiwa kuanza mwezi Machi, 2020.
MHE. JOYCE B. SOKOMBI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itawalipa fedha zao wananchi wa Musoma ambao maeneo yao yapo pembezoni mwa Uwanja wa Musoma na wameshafanyiwa tathmini ili kupisha upanuzi wa ujenzi wa uwanja huo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Mawasiliano ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Joyce Bitta Sokombi, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeanza utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Musoma ambao uko katika hatua za awali za manunuzi ili kumpata Mkandarasi. Mchakato wa manunuzi unakwenda sambamba na ulipaji wa fidia kwa wananchi watakaoathirika na mradi huu wa ujenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Musoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itahakikisha kwamba, wananchi wanaostahili kulipwa fidia wanalipwa kabla ya kuanza utekelezaji wa mradi huu wa upanuzi wa ujenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Musoma.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI aliuliza:-

Barabara ya Likuyufusi – Mkenda yenye urefu wa kilometa 124 inayounganisha Tanzania na Mozambique mpaka sasa bado haijajengwa kwa kiwango cha lami.

Je, ni lini Serikali itapeleka pesa na kuanza ujenzi huo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Likuyufusi – Mkenda yenye urefu wa kilometa 124 ni barabara muhimu kutokana na ukweli kwamba inaunganisha nchi mbili za Tanzania na Msumbiji na pia inahudumia wananchi wengine wa vijiji vya Mkenda/Mitomoni hadi Likuyufusi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), ilifanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara hii kwa kumtumia Mkandarasi Mshauri M/s Crown Tech. Consult (T) Ltd. wa Dar es Salaam ambaye alikamilisha kazi hiyo mwaka 2012. Baada ya kukamilika kwa usanifu huo, kulijitokeza ongezeko kubwa la matumizi katika barabara hiyo kutokana na kugundulika na kuanza kuchimbwa kwa makaa ya mawe katika eneo la Muhukuru pamoja na matarajio ya uwekezaji wa shamba la miwa na kiwanda cha sukari eneo la Nakawale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na mabadiliko hayo, Wizara yangu kupitia TANROADS inapitia upya usanifu wa awali ili kuzingatia mahitaji ya sasa. Kazi hiyo imeshaanza na inatarajiwa kukamilika mwezi Juni 2020. Baada ya kukamilika kwa kazi hiyo, Serikali itajua gharama halisi za ujenzi na kuanza kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami.
MHE. ESTER A. MAHAWE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi wa Sinai, Hangoni, Kwere na Mruki waliopitiwa na barabara ya “By Pass” ya magari makubwa yatokayo Dodoma na kutokea stendi mpya ya Babati Mjini?
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ester Alexander Mahawe Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa barabara ya mchepuo Babati Bypass katika barabara ya Dodoma Babati, Arusha na Singida Babati unatekelezwa kwa pamoja na mradi wa Mtera Bypass katika barabara ya Iringa Dodoma chini ya ufadhili wa Benki ya Maendeleo ya Afrika na uko katika hatua ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na maandalizi ya makablasha ya zabuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya majukumu ya Mhandisi Mshauri ni kutambua sehemu ambamo barabara ya mchepuo itapita yaani alignment. Mara baada ya maeneo itakamopita barabara ya mchepuo kujulikana na kukubaliwa na Serikali kazi itakayofuata ni ya usanifu wa kina ambapo mali zitakazokuwa katika maeneo inamopita barabara ya mchepuo zitatambuliwa na kufanyiwa tathimini kwa ajili ya fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua iliyofikiwa sasa ni kwamba kazi ya upembuzi yakinifu inaendelea lakini bado maeneo na mali zitakazoathiriwa na mradi itakamopita barabara hayajajulikana, hivyo mali na kutathiminiwa na kufidiwa hazijajulikana Serikali italipa fidia kwa mujibu wa sheria.
MHE. ANNE K. MALECELA (K.n.y. MHE. DAVID M. DAVID) aliuliza:-

Je, ni lini Serikali kwa kushirikiana na Mashirika ya Simu itawapelekea huduma ya simu wananchi wa Kata za Msindo Mshewa, Mhezi, Vumari, Vudee, Tae, Suji, Gavao, Saweni na Ruvu Jiungeni?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. David Mathayo David, Mbunge wa Same Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano Kwa wote imetoa ruzuku kwa ajili ya ujenzi wa minara ya mawasiliano katika Wilaya ya Same ambapo wakazi zaidi ya 13,531 wamefikiwa na huduma za mawasiliano katika Kata za Bombo, Maore, Mshewa, na Ruvu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa wote imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya kufikisha huduma za mawasiliano nchi nzima. Kwa upande wa Same Magharibi, Serikali iliviainisha Vijiji vya Kata za Vumari, Suji na Ruvu Jiungeni ili kuangalia mahitaji halisi ya mawasiliano na hatimaye vimeingizwa katika orodha ya vijiji vya zabuni ya Awamu ya Nne. Zabuni hiyo ilitangazwa tarehe 18 Julai, 2019 ambapo mwisho wa kurudisha vitabu vya zabuni hiyo ni tarehe 3 Oktoba, 2019, ikifuatiwa na tathmini ya zabuni husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Mshewa imefikishiwa huduma za mawasiliano ambapo minara miwili (2) ya tigo imejengwa na kuihudumia kata hii. Pamoja na jitihada hizi na uwepo wa minara hii baadhi ya maeneo ya kata hii yanaonekana kuwa na changamoto za mawasiliano. Kata hii itafanyiwa tathmini zaidi ili kubaini maeneo mahususi ambayo bado yana changamoto ya mawasiliano ili yafanyiwe kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasialiano kwa wote (UCSAF) imevipokea vijiji vya kata za Msindo, Mhezi, Vudee Tae, Gavao na Saweni na itavifanyia tathmini kuangalia mahitaji halisi ya mawasialiano na kasha kuviingiza katika orodha ya vijiji vya zabuni zitatazotekelezwa kulingana na upatikanaji wa fedha hususani katika mwaka wa fedha 2019/2020.
MHE. EMMANUEL P. JOHN aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya NARCO (Hogoro) Kibaya – Olkesimeti – Oljoro - Arusha kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Emmanuel Papian John Mbunge wa Kiteto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa ujenzi wa barabara ya NARCO (Hogoro) hadi Kibaya – Olkesumeti - Oljoro hadi Arusha yenye urefu wa kilomita 450 uko katika hatua ya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na maandalizi ya nyaraka za zabuni. Kazi hiyo inafanywa na Mtaalam Mshauri M/S Cheil Engineering Co. Limited wa Korea Kusini akishirikiana na Inter-Consultant Ltd wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtaalam Mshauri tayari amewasilisha taarifa ya awali (Draft Final Report) mwezi Julai mwaka 2019 kwa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na kupatiwa maoni kuhusu mapungufu ambayo tayari ameagizwa kuyafanyia kazi. Taarifa ya Mwisho ya Usanifu (Final Design Report) inatarajiwa kukamilika ifikapo mwishoni mwa Septemba, 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya usanifu kukamilika na gharama kujulikana, Serikali itaanza ujenzi wa barabara hii kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI aliuliza:-

Barabara ya Mlalo kupitia Ngwelo – Mlalo –Makanya- Mlingano mpaka Mashewa ni ya muda mrefu sana ipo chini ya halmashauri licha ya kwamba barabara hiyo ni kichocheo muhimu cha uchumi katika majimbo manne ya Lushoto, Mlalo, Bumbuli na Korogwe Vijiji.

Je, ni lini Serikali itaipandisha hadhi barabara hiyo na kuwa chini ya TANROADS kutokana na umuhimu wake kiuchumi kwa wananchi wa majimbo hayo?
NAIBU WAZIRI UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajibu swali ninaomba kwenye jibu langu nifanye marekebisho kidogo Mheshimiwa Mbunge kuna kosa la kiuchapaji ni Mbunge wa Lushoto siyo Mbunge wa Bumbuli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Shaabani Omari Shekilindi Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara iliyotajwa na Mheshimiwa Mbunge kwa sasa ni barabara ya wilaya inayohudumiwa na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA).

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Serikali kuanzisha Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), imesitisha utaratibu wa kupandisha hadi barabara za Wilaya kuwa barabara za Mikoa (kwa kigezo cha kutohudumiwa ipasavyo) kwa vile TARURA imeanzishwa mahsusi kwa jukumu la kuendeleza barabara za wilaya nchini kikiwemo barabara ya Mlalo kupitia Ngwelo – Mlalo- Makanya – Mlingano mpaka Mashewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale inapobidi barabara kupandishwa hadhi, upandishaji wake utafanyika kwa kuzingatia vigeo vya kitaalam kwa mujibu wa Sheria ya Barabara Na. 13 ya Mwaka 2007 na kanuni zake za Mwaka 2009. Hivyo, Mheshimiwa Mbunge anashauriwa kufuata taratibu zilizoweka katika Sheria tajwa ili barabara hiyo ipandishwe hadhi.
MHE. ISSA A. MANGUNGU (K.n.y. MHE. ABDALLAH A. MTOLEA) aliuliza:-

Eneo la kipande cha barabara ya Kilwa – Rangi Tatu – Kongowe limeharibika vibaya na kusababisha foleni na ajali nyingi.

(a) Je, ni lini Serikali itajenga barabara hiyo kikamilifu kwa kiwango cha lami ili kuondoa kero hizo?

(b) Je, ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kujenga kipande hicho kwa njia nne mpaka Kongowe itaanza lini?

(c) Daraja la Mto Mzinga katika kipande hicho lipo katika hali mbaya na hatarishi: Je, ni lini Serikali itajenga daraja jipya kama alivyoahidi Mheshimiwa Rais wakati akiwa Waziri wa Ujenzi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ali Mangungu, Mbunge wa Mbagala, lenye sehemu (a),( b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya ujenzi wa barabara katika Jiji la Dar es Salaam kwa lengo la kushughulikia tatizo la msongamano wa magari katika Jiji hilo. Miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa barabara ya mabasi yaendayo haraka kwa awamu ya pili, (BRT Phase II) ambao unahusisha barabara ya Kilwa kuanzia Gerezani hadi Mbagala Rangi Tatu. Kazi za ujenzi wa barabara na vituo vya mabasi ulianza mwezi Mei, 2019 na umepangwa kukamilika mwaka 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), ipo katika hatua za mwisho za kukamilisha usanifu kwa ajili ya upanuzi wa barabara ya Kilwa kuanzia sehemu ya Mbagala Rangi Tatu hadi Kongowe yenye urefu wa kilometa 3.8 kutoka njia mbili kuwa njia nne. Usanifu huo unahusisha Daraja la Mzinga. Baada ya kukamilika kwa usanifu huo, Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya ujenzi.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA aliuliza:-

Kivuko kilichopo Bukoba Vijijini Kyanyabasa hakikidhi viwango kabis:- Je, ni lini Serikali itaweka kivuko au daraja litakalokidhi viwango?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oliver Daniel Semuguruka, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kivuko cha MV Kyanyabasa kinachotoa huduma kati ya Buganguzi na Kasharu eneo la Kyanyabasa katika Mto Ngono kilinunuliwa mwaka 2005 na kina uwezo wa kubeba abiria 50 na magari madogo mawili kwa pamoja. Kivuko hiki kilifanyiwa ukarabati mkubwa mwaka 2016 na kinaendelea kutoa huduma kwa wananchi wa Bukoba bila matatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuendelea kutoa huduma nzuri na zenye viwango, Serikali katika mwaka wa fedha 2020/2021, imejipanga kukifanyia maboresho makubwa ikiwa ni pamoja na kuweka viti na paa kwa ajili ya abiria kujikinga na mvua na jua; kuweka taa kwa ajili ya kutumika kuvusha abiria kwa dharura nyakati za usiku na ukarabati utakaohusisha kubadilisha milango pamoja na kupaka rangi.

Mhehimiwa Naibu Spika, kivuko kilichopo kwa sasa kinatosheleza kutoa huduma inayohitajika kwa wananchi wa eneo hilo. Hivyo, hakuna haja ya kujenga daraja kwa sasa. Serikali itaangalia uwezekano wa kujenga daraja siku za usoni pale itakapohitajika.
MHE. HASSAN E. MASALA aliuliza:-

Je, ni lini Barabara ya Masasi – Nachingwea – Nanganga itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Elias Masala, Mbunge wa Nachingwea, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Masasi – Nachingwea – Nanganga yenye urefu wa kilometa 106 ni barabara ya mkoa na inasimamiwa na Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Lindi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, Wizara yangu kupitia TANROADS iliifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ambao ulikamilika mwaka 2018. Baada ya kukamilika kwa usanifu huo, Serikali sasa inatafuta fedha kwa ajili ya kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. SILVESTRY F. KOKA aliuliza:-

Serikali inajenga njia ya barabara nane kutoka Ubungo hadi Kibaha:-

Je, barabara hiyo inaishia eneo gani la Mji wa Kibaha?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Silvestry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ipo katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya ujenzi wa barabara na madaraja nchini ikiwemo mradi wa upanuzi wa barabara kuu ya Morogoro sehemu ya Jiji la Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani. Mradi huu unahusisha upanuzi wa barabara kutoka njia mbili za zamani mpaka njia nane hadi njia 12 katika baadhi ya maeneo pamoja na ujenzi wa madaraja ya Kibamba, Kiluvya, Mpiji na Mlonganzila Overpass.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Serikali ipo katika utekelezaji wa awamu ya kwanza ya mradi huu kuanzia Kimara na kuishia Kibaha Maili Moja mbele ya mizani ya zamani takribani mita 150 kutoka mizani ilipo. Barabara hii inayopanuliwa ina jumla ya kilometa 19.2. Lengo la mradi huu ni kupunguza msongamano mkubwa wa magari yanayopita katika barabara hiyo ambayo yanazidi magari 50,000 kwa siku ikizingatiwa kuwa Jiji la Dar es Salaam ni kitovu cha biashara hapa nchini na kuna bandari inayotumiwa na nchi jirani za Malawi, Zambia, Burundi, Rwanda, Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Mradi huu unatekelezwa na Mkandarasi Estim Construction Co. Ltd wa hapa nchini kwa gharama ya Shilingi bilioni 140.45 na kusimamiwa na Kitengo cha Usimamizi wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS Engineering Consulting Unit – TECU). Utekelezaji wa mradi huu unagharamiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa asilimia 100. Hadi sasa utekelezaji umefikia asilimia 48 na mradi umepangwa kukamilika mwezi Januari, 2021.
MHE. MARTHA J. UMBULLA aliuliza:-

Uwanja wa Ndege wa Arusha ni muhimu sana kutokana na ukweli kuwa ni lango la kurahisisha watalii kuelekea kwenye Mbuga zetu za Wanyama na Hifadhi ya Taifa.

(a) Je, ni lini Serikali itapanua na kuboresha uwanja huo ili kuwezesha Watalii wengine kutumia ndege zetu na nyingine kutua Arusha kwa urahisi?

(b) Je, Serikali haioni kuwa Uwanja wa Ndege wa Arusha ungetumika kimkakati kukuza Sekta ya Utalii nchini na kuongeza pato la Taifa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Wziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Martha Jachi Umbulla, Mbunge Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA) na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) imeendelea kukikarabati Kiwanja cha Ndege cha Arusha ambapo mwaka huu wa fedha 2019/2020 kazi ya kuboresha maegesho ya magari, kukarabati barabara za viungo zimeshaanza na ziko katika hatua mbalimbali za utekelezaji. Taratibu za kumpata Mkandarasi kwa kazi ya kurefusha barabara ya kuruka na kutua ndege kutoka mita 1640 za sasa hadi mita 1840 sambamba na ujenzi wa eneo la kugeuzia ndege yaani (Turning pads) zinaendelea. Ujenzi huu utawezesha ndege kubwa aina ya Bombardier Q 400 za ATCL kutumia kiwanja hiki.

Aidha, mipango ya kuweka taa za kuongezea ndege kwenye uwanja huo utawekwa kwenye mwaka wa fedha 2020/2021.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO (K.n.y. MHE. LAMECK O. AIRO) aliuliza:-

Mheshimiwa Rais akiwa kwenye ziara ya kujinadi wakati wa kampeni Wilayani Rorya aliwaahidi wananchi wa Rorya kujenga barabara ya lami kutoka Mika-Utegi hadi Shirati;lakini hadi sasa ahadi hiyo haijatekelezwa:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutekeleza ahadi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lameck Okambo Airo, Mbunge wa Rorya, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Mika – Utegi – Shirati hadi Ruari Port ni barabara ya mkoa inayosimamiwa na Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Mara. Barabara hii ina urefu wa kilometa 48.73. Kati ya hizo, kilometa 40.13 zimejengwa kwa kiwango cha changarawe na kilometa 8.6 zimejengwa kwa awamu kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeanza maandalizi ya kuijenga barabara hii (km 48.73) kwa kiwango cha lami kwa kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Kazi hiyo inafanywa na Makampuni ya Cordial Solution Ltd. na Atkins Tanzania Ltd yote ya Tanzania. Wakati makampuni hayo yakiendelea na kazi, yaliongezewa kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara ya usalama na ulinzi kutoka Shirati – Masonga hadi mpakani mwa Tanzania na Kenya (km 16.4). Gharama ya kazi zote ni shilingi milioni 679.621 na inatarajiwa kukamilika mwezi Juni mwaka 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami utaanza baada ya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kukamilika na fedha za ujenzi kupatikana. Aidha, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii Serikali itaendelea kuifanyia matengenezo mbalimbali. Kwa mfano, katika mwaka wa fedha 2019/2020, barabara hii ya Mika – Utegi – Shirati imetengewa shilingi milioni 630.148 kwa ajili ya matengenezo mbalimbali.
MHE. GODFREY W. MGIMWA aliuliza:-

Barabara ya Kalenga kuelekea Ruaha National Park ni ya muhimu sana kwa uchumi wa Jimbo la Kalenga, Iringa na Tanzania kwa ujumla:-

Je, Serikali ina mpango gani juu ya kuitengeneza barabara hiyo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Kalenga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Kalenga kuelekea Ruaha National Park ambayo inajulikana kama barabara ya Iringa – Msembe ni barabara ya mkoa inayosimamiwa na Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Iringa. Barabara hii ina urefu wa kilometa 104, kati ya hizo, kilometa 18.4 zimejengwa kwa kiwango cha lami na kilometa 85.6 zimejengwa kwa kiwango cha changarawe.

Mheshimiwa Spika, barabara hii inaunganisha Makao Makuu ya Mkoa wa Iringa na Mbuga ya Wanyama ya Ruaha na inapita katika maeneo muhimu ya Makumbusho ya Mkwawa na maeneo mengine yenye kilimo cha mpunga na mahindi.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), imekamilisha kazi ya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na kuandaa makabrasha ya zabuni kwa ajili ya kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami na kazi hii imefanywa na Kampuni ya ENV Consult (T) Ltd ya hapa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2019/ 2020, jumla ya shilingi billioni 4.221 zimetengwa kwa ajili ya maandalizi ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara hii kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. OMARY A. KIGODA aliuliza:-

Barabara ya Handeni – Mziha ni barabara ya mkakati na ipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Je, ni lini Serikali itamalizia kipande kilichobaki kutoka Handeni mpaka Mziha?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Omary Abdallah Kigoda, Mbunge wa Handeni Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Handeni – Mziha yenye urefu wa kilomita 70 ni sehemu ya barabara ya Handeni – Mziha – Turiani – Dumila yenye urefu wa kilomita 154.6 ambayo inasimamiwa na Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mikoa ya Tanga na Morogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mkoa wa Tanga imekamilisha kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara hiyo sehemu ya Handeni – Mziha (kilomita 70) kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 1,160 kwa ajili ya maandalizi ya kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami.
MHE. RITTA E. KABATI Aliuliza:-

Wananchi waliopisha ujenzi wa barabara ya mchepuo ya Tumaini kuchepusha magari makubwa kupita katikati ya Mji wa Iringa walilipwa fidia zao baada ya muda mrefu sana kufanyiwa tathmini.

(a) Je, sheria inasemaje?

(b) Je, Serikali ipo tayari kuwapatia nyongeza ya fidia zao?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa mwongozo wa uthamini wa fidia wa mwaka 2016 na Kanuni ya Sheria ya Ardhi ya Mwaka 2001, malipo ya fidia yanapaswa kufanyika kwa wakati ndani ya muda wa miezi sita. Endapo hayatafanyika ndani ya muda huo, malipo hayo yanapaswa kulipwa pamoja na riba. Serikali inatambua kuwa waathirika 188 wa Kata ya Igumbilo na Kihesa na makaburi 43 yalihamishwa ili kupisha ujenzi wa barabara ya mchepuo ya Tumaini – Iringa. Jumla ya shilingi 4,623,369,257.11 zimetumika kulipa fidia waathirika wa mradi huo. Aidha, shilingi 14,550,500 zimetumika kuhamisha makaburi kutoka katika eneo la mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itawalipa wananchi riba kwa mujibu wa sheria mara fedha itakapotolewa na Hazina.
MHE. JEROME D. BWANAUSI Aliuliza:-

Serikali iliahidi kujenga minara ya mawasiliano ya simu katika Kata za Sindano, Lupaso, Lipumburu, Mchauru na Mapili (Chikolopola) ambazo zipo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji.

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Jerome Dismas Bwanausi, Mbunge wa Lulindi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote iliviainisha vijiji vya Kata ya Sindano, Lipumburu, Namtona, Mchauru na Chikolopola (Mapili) na kuviiingiza vijiji vya Kata za Mchauru katika mradi uonatekelezwa na Kampuni ya Simu ya MIC (Tigo) ambapo vibali vya ujenzi kutoka NEMC vimekwisha patikana. Kata za Sindano na Lipumburu ziliingizwa katika mradi wa awamu ya tatu ambayo ilitiwa saini tarehe 15 Desemba, 2018 ambapo utekelezaji wake unategemewa kukamilika mnamo mwezi Desemba, 2019 ambapo Kata ya Sindano inafikishiwa huduma na Kampuni ya Vodacom wakati Lipumburu itafikishiwa huduma na TTCL.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, vijiji vya Kata za Lupaso na Chikolopola vimeingizwa katika orodha ya miradi ya zabuni iliyotengwa mwezi Julai, 2019. Utekelezaji wa mradi unategemea kuanza mwezi Oktoba, 2019.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST Aliuliza:-

Je, Serikali imefikia wapi katika mchakato wa kulipa fidia kwa wananchi wa Kipunguni waliotakiwa kusitisha kuendeleza maeneo yao ili kupisha upanuzi wa kiwanja cha ndege?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (ELIAS J. KWANDIKWA) Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonist, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uwepo wa wananchi 1,182 eneo la Kipunguni yaani wananchi 381 Kipunguni Mashariki na wananchi 801 Kipunguni A ambao maeneo yao yalifanyiwa uthamini kwa ajili ya kulipwa fidia baada ya maeneo hayo kuwekwa kwenye mpango wa kutwaliwa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) kufuatia mradi wa maboresho ya miundombinu na usalama wa Kiwanda cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere, Dar es Salaam yanayoendelea kufanywa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi ambao maeneo yao yapo kwenye eneo la mradi kuwa Serikali itawalipa fidia pale itakapotenga fedha kwa ajili ya mradi husika.
MHE. PASCAL Y. HAONGA (K.n.y. MHE. DAVID E. SILINDE) Aliuliza:-

Je, ni lini barabara ya Mlowo – Kamsamba – Kiliyamatundu – Kibaoni itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa David Ernest Silinde, Mbunge wa Momba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Mlowo – Kamsamba – Kiliyamatundu – Kibaoni yenye urefu wa kilometa 369 ni barabara ya Mkoa na inahudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mikoa ya Songwe, Rukwa na Katavi. Aidha, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) imekamilisha ujenzi wa Daraja la Momba lenye urefu wa mita 84 na barabara unganishi zenye urefu wa kilometa 1.2.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina inaendelea kwa barabara kuanzia Kamsamba hadi Mlowo, kilometa 130.14 na barabara ya mchepuo kwa kuingia Makao Makuu ya Wilaya ya Momba, kilometa 15, kwa gharama ya shilingi milioni 765.46. Kazi hii imefikia asilimia 75.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali imetenga jumla ya shilingi milioni 180 kwa ajili ya kufanya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa barabara na kuijenga kwa kiwango cha lami sehemu ya barabara hii kuanzia Kiliyamatundu hadi Kasansa (sehemu ya Kilyamatundu – Muze (km 142) na Ntendo – Muze (km 37.04), taratibu za kumpata Mshauri Elekezi wa kufanya kazi hiyo zinaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu sehemu ya barabara kutoka Kasansa hadi Kibaoni (km 60), sehemu ya kuanzia Kibaoni hadi Majimoto (km 34) ipo kwenye hatua za manunuzi ya kumpata mshauri elekezi kwa ajili ya kufanya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara ya Kibaoni – Majimoto – Inyonga (km 162). Aidha, sehemu iliyobaki kuanzia Muze – Mamba – Majimoto (km 55) Serikali inatafuta fedha ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii kwa ajili ya usafiri wa wananchi na usafirishaji wa mazao ya chakula na biashara yanayozalishwa na wananchi wa maeneo ya Kata za Igamba, Hulungu, Itaka, Nambinzo hadi Kamsamba pamoja na maeneo ya Kiliyamatundu, Muze, Kasansa, Majimoto hadi Kibaoni, Serikali inaendelea kutenga fedha kila mwaka kwa ajili ya kuifanyia matengenezo mbalimbali ili iendelee kupitika majira yote ya mwaka na mara tu usanifu wa kina utakapokamilika, ujenzi kwa kiwango cha lami kwa barabara hii utafanyika kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. ALLAN J. KIULA aliuliza:-

Sera ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kuunganisha kwa barabara za lami:-

Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya lami inayounganisha Mikoa ya Simiyu na Singida kupitia Daraja la Sibiti lililopo Wilaya ya Mkalama?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Allan Joseph Kiula, Mbunge wa Jimbo la Iramba Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mikoa ya Simiyu na Singida inaunganishwa na barabara yakutokea Bariadi kupitia Maswa – Lalago-Ng’hoboko- Mwanhuzi- Sibiti – Mkalama- Gumanga – Nduguti - Iguguno Shamba hadi Singida Mjini yenye urefu wa kilomita 341 na inaunganishwa pia na barabara ya kutoka Bariadi kupitia – Mwandoya – Ng’hoboko – Mwanhuzi – Sibiti – Mkalama – Gumanga – Nduguti – Iguguno Shamba – Singida Mjini yenye urefu wa kilomita 338 na barabara hizi zinahudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mikoa ya Singida na Simiyu.

Mheshimiwa Spika, Ujenzi wa Daraja la Mto Sibiti lenye urefu wa mita 82 umekamika na ujenzi wa barabara unganishi zenye jumla ya urefu wa kilomita 25 umekamilika kwa kiwango cha changarawe na ambapo taratibu za manunuzi za kuzijenga kwa kiwango cha lami zinaendelea. Barabara ya Sibiti – Mkalama – Gumanga – Nduguti hadi Iguguno kilomita 106 ipo upande wa Mkoa wa Singida na sehemu ya barabara hii kuanzia Sibiti hadi Mkalama kilomita 27 inaendelea kufanyiwa usanifu wa awali kupitia Mradi wa Serengeti Southern Bypass sehemu iliyobaki ya barabara hii ni barabara ya kiwango cha changarawe na hupitika majira yote ya mwaka.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Mkoa wa Simiyu barabara ya kuaznia Sibiti- Mwanhuzi-Ng’hoboko kupitia Lalago- Maswa hadi Bariadi, sehemu ya kuanzia Bariadi - Maswa kilomita 49.5 inaendelea kujengwa kwa kiwango cha lami na sehemu ya kuanzia Maswa – Lalago – Ng’hoboko – Mwanhuzi – Sibiti kilomita 146.83 inaendelea kufanyiwa usanifu wa awali kupitia mradi wa Serengeti Southern Bypass Kisesa hadi Bariadi ni bararaba ya changarawe na inapitika vizuri majira yote ya mwaka.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara hii inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kufanya usanifu wa kina kwa sehemu zilizobaki ziweze kujengwa kwa kiwango cha lami.
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza:-

Jimbo la Tunduru Kusini limepakana na Msumbiji kupitia Mto Ruvuma kuanzia mpaka wa Wilaya ya Nanyumbu na Wilaya ya Namtumbo:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kufufua barabara ya ulinzi inayounganisha mikoa yote ya Kusini yaani Mtwara na Ruvuma?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate Mbunge wa Tunduru Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara anazozungumzia Mheshimiwa Mbunge ni barabara ya Mahangamba, Madimba, Tangazo, Kitaya, Mnongodi, Mapili, Mitemaupinde yenye urefu wa km 351 na barabara ya Mtwara pachani Lusewa, Tunduru yenye urefu wa km 300 zinazohudumiwa na Wakala wa barabara Tanzania TANROADS Mkoa wa Mtwara na Mkoa wa Ruvuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa kutambua umuhimu wa barabara hizi, hasa kwenye ulinzi wa mipaka ya nchi yetu Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Mtwara tayari imefungua sehemu ya barabara kuanzia Mahangamba, Madimba, Tangazo, Kitaya na Mnongodi – Mapili yenye urefu km 216 kwa kiwango cha changarawe. Katika mwaka wa fedha 2019/ 2020 jumla ya shilingi bilioni mbili na milioni mia nane sabini na nane zimetengwa kwa ajili ya kuendelea kufungua km 90.4 za barabara hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Ruvuma inaendelea kufanya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na uandaaji wa nyaraka zabuni kwa sehemu ya barabara ya Mtwara - Pachani, Lusewa – Tunduru ambapo kazi hiyo imefikia asilimia 65.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Pamoja na Serikali kuendelea kufungua barabara hizo Serikali inaendelea kuzifanyia matengenezo mbalimbali sehemu ya barabara iliyofunguliwa ili iendelee kupitika majira yote ya mwaka.
MHE. PASCAL Y. HAONGA aliuliza:-

Wilaya ya Mbozi ambayo ni Makao Makuu ya Mkoa wa Songwe inapakana na Wilaya ya Songwe; Wilaya hizi mbili hazijaunganishwa kwa barabara hivyo Wananchi wanaotoka Wilaya ya Songwe kwenda Makao Makuu ya Mkoa hulazimika kupitia Mkoa wa Mbeya?

(a) Je, ni lini Serikali itatengeneza barabara ya changarawe kutoka Kata ya Magamba ambayo ipo Wilaya ya Songwe kupitia Kata ya Magamba ambayo ipo Mbozi?

(b) Kata za Magamba, Itumpi, Bara, Itaka na Halungu hazina vivuko na madaraja hali inayosababisha usumbufu kwa Wananchi; Je, ni lini Serikali itajenga vivuko katika Kata hizo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kabla ya kujibu swali naomba kufanya marekebisho ya kiuchapaji kidogo katika ile sehemu ya swali sehemu ya (b) sehemu ya Kata ya Iyempi isomeke Itumpi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Pascal Yohana Haonga Mbunge wa Mbozi lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara anayozungumzia Mheshimiwa Mbunge ni barabara inayoanzia Kijiji cha Mlowo na kupitia Vijiji vya Zelezeta, Isansa, Nafco, Magamba, Itindi hadi Galula. Sehemu ya barabara inayoanzia Kijiji cha Mlowo, Zelezeta, Isansa, Nafco hadi Magamba yenye urefu wa km 34 ni barabara ya Mkoa inahudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Songwe. Aidha, sehemu hii inayoanzia Magamba, Itumpi hadi Galula yenye urefu wa km 32 inahudumiwa na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mjini (TARURA) Mkoa wa Songwe na inapitika vizuri majira yote ya mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa kutambua umuhimu wa barabara hii kwenye Sekta ya Kilimo, biashara na madini ya makaa ya mawe Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) imekuwa ikiifanyia matengenezo mbalimbali barabara hii ili iweze kupitika majira yote ya mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu nyingine za barabara alizouliza Mheshimiwa Mbunge zinasimamiwa na Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) Mkoa wa Songwe iliyopo chini ya Ofisi ya Rais TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutenga fedha za kutosha kuiwezesha TANROADS na TARURA kuihudumia barabara hii pamoja na kuimarisha madaraja aliyoyataja Mheshimiwa Mbunge.
MHE. TUNZA I. MALAPO (K.n.y. MHE. SUSANNE P. MASELLE) aliuliza:-

Kutokana na umuhimu wa kimkakati katika nyanja mbalimbali za maendeleo kwa Mikoa ya Kanda ya Ziwa na nchi yetu kwa ujmla:-

Je, ni lini Jiji la Mwanza litakuwa na uwanja wa ndege unaoendana na hadhi na ukuaji wa kasi wa jiji hilo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, katika juhudi za Serikali za kuboresha miundombinu ya viwanja vya ndege, Serikali iliingia mkataba wa ukarabati mkubwa wa Kiwanja cha Ndege cha Mwanza Oktoba, 2012 na Kampuni ya Beijing Construction Engineering Group Co. Ltd (BCEG) wenye thamani ya shilingi 89,291,995,422. Mchanganuo wa fedha hizi ni kuwa Serikali ya Tanzania inachangia asilimia 82.5 na wabia wa maendeleo asilimia 17.5.

Mheshimiwa Spika, kazi kubwa zinazofanyika katika uboreshaji huu ni pamoja na kurefusha barabara ya kuruka na kutua ndege (runway) kutoka mita 3,300 kwa upana wa mita 45 hadi mita 3,800 kwa upana wa mita 45; kujenga majengo ya kuongozea ndege (control tower); kituo cha hali ya hewa; jengo la kupokea na kuhifadhi mizigo; kuboresha na kupanua maegesho ya ndege (aprons); kujenga barabara za viungio (taxways) na kituo cha umeme (power station).

Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Machi, 2019, ujenzi wa kazi hizi za mradi umefikia asilimia 87 na mkandarasi anaendelea vizuri na kazi ya ujenzi na anatarajia kumaliza kazi zote ifikapo Juni, 2019.

Mheshimiwa Spika, Serikali pia ipo kwenye mazungumzo na wabia wa maendeleo ambapo wameonyesha nia ya kufadhili jengo kubwa na la kisasa la abiria litakaloendana na maboresho haya makubwa ya kiwanja pamoja na hadhi ya Jiji la Mwanza. Tunategemea kufikia Mwezi Oktoba, 2019, kazi za ujenzi wa jengo hili zitakuwa zimeanza.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-

Kumekuwa na kero kubwa sana kwa abiria wanaotumia bandari kwenda Zanzibar kwa boti ambapo hulipishwa ushuru wa bandari kwa mizigo hata boksi la kilo kumi tu au mchele kilo 20 kwa malipo ya shilingi 9,750.

Je, ni mizigo gani ambayo abiria anapaswa kulipia ushiri huo wa bandari (Wharfage)?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kufuatana na mwongozo wa tozo (tariff book) kifungu kifungu 29 wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA), tozo ya wharfage inatozwa inatozwa kwa mizigo ya biashara yenye uzito zaidi ya kilo 21 na yenye zaidi ya mita moja ya ujazo inayopita kwenye gati, jeti na maboya yaliyo chini ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA).

Mheshimiwa Spika, TPA haikusanyi tozo yoyote kwa abiria ambao wana vifurushi binafsi (personal effects) vyenye uzito au ujazo mdogo chini ya kilo 21 au mita moja ya ujazo wanaotumia bandari kwenda Zanzibar kwa boti kwenye eneo la baggage room. Aidha, abiria wanaotumia bandari kwenda Zanzibar kwa boti ambao hutozwa ushuru wa bandari katika eneo la baggage room ni wale tu wanaokuwa na mizigo mikubwa tena kwa madhumuni ya kibiashara.

Mheshimiwa Spika, TPA inapenda kuwasisitiza wateja/ abiria wote wenye mizigo ya kibiashara kwenda au kutoka Zanzibar kutumia eneo la Azam Sea Link lililotengwa kwa ajili ya shughuli za kibiashara ili kuondokana na usumbufu kwenye eneo la baggage room ambalo limetengwa mahsusi kwa ajili ya abiria wenye mizigo yao binafsi (personal effects).

Mheshimiwa Spika, tunapenda kutoa wito kwa wateja wetu wote wanaotumia bandari kwenda Zanzibar kwa boti wahakikishe kuwa mizigo yao inapimwa kabla ya kupakiwa ili wajue kama uzito wake unastahiki kutozwa ushuru wa bandari au la, kuepuka usumbufu unaoweza kujitokeza.
MHE. MAHMOUD H. MGIMWA aliuliza:-

Barabara ya Mtiri - Ifwagi - Mdaburo - Ihamu - Mpangatazara hadi Mlimba inaunganisha Wilaya ya Mufindi na Kilombero, na ni muhimu sana kiuchumi na kijamii kwa mikoa hiyo miwili. Aidha, Mheshimiwa Rais aliahidi kuipandisha hadhi barabara hii kuwa chini ya TANROADS.

(a) Je, ni lini Serikali itapandisha hadhi barabara hiyo ili kuwa chini ya TANROADS?

(b) Je, kuna mkakati gani wa dharura kuhakikisha barabara hiyo inapitika kwa wakati wote?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mahmoud Hassan Mgimwa, Mbunge wa Mufindi Kaskazini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Mtiri – Ifwagi - Mdaburo – Ihamu – Mpangatazara hadi Mlimba ni barabara ya Wilaya inayohudumiwa na Ofisi ya Rais, TAMISEMI kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Wilaya ya Mufindi. Kufuatia kuundwa kwa TARURA mwaka 2017 maombi ya kupandishwa hadhi barabara za Wilaya kuwa za Mkoa au kusimamiwa na TANROADS kwa kigezo cha kukosa fedha limesimamishwa kwa muda ili kuipatia TARURA fursa ya kutekeleza majukumu mahsusi ya kuundwa kwake.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara hii inayopita kwenye maeneo yenye uzalishaji mkubwa wa mazao ya biashara na chakula pamoja na kuendelea kuifanyia matengenezo mbalimbali, barabara hii imewekwa kwenye mpango wa kukarabatiwa kupitia ufadhili wa Benki ya Dunia kupitia mradi ujulikanao kama Road Inclusion and Social Economic Opportunities (RISE). Ahsante sana.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA aliuliza:-

Je, ni lini madaraja ya barabara ya Gairo – Chakwale – Idilo – Kilindi yatajengwa au kukarabatiwa ili barabara hiyo iweze kupitika wakati wote wa masika na kiangazi bila matatizo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christine Gabriel Ishengoma, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Gairo – Chakwale – Idilo – Kilindi ni barabara ya mkoa inayounganisha Wilaya ya Gairo iliyopo Mkoa wa Morogoro na Wilaya ya Kilindi iliyopo Mkoani Tanga. Sehemu ya barabara hii kwa upande wa Mkoa wa Morogoro inaitwa Iyogwe – Chakwale – Ngilori (kilometa 42) na sehemu iliyobaki ya kutoka Iyogwe – Kilindi iko Mkoa wa Tanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia umuhimu wa barabara hii kiuchumi na kijamii hususan katika wakati wa kusafirisha mazao ya kilimo na chakula kwa Wilaya ya Gairo na Kilindi, katika mwaka wa fedha 2019/2020 Serikali kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) imetenga kiasi cha shilingi milioni 100 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa vented drift moja na box culverts mbili kwenye mito mikubwa ya Chakwale, Nguyani na Matale iliyoko katika barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Mkoa wa Morogoro na Mkoa wa Tanga itaendelea kuifanyia matengenezo mbalimbali barabara hii ili iweze kupitika majira yote ya mwaka.
MHE. YOSEPHER F. KOMBA aliuliza:-

Nyumba za makazi pembezoni mwa reli Wilayani Muheza zimewekewa alama ya ‘X’ zikisubiri kubomolewa kwa kigezo cha kujenga kwenye eneo la reli wakati walipewa maeneo hayo kIhalali na Serikali.

Je, ni nini hatma ya wananchi hao ambao wanaishi kwa mashaka?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Yosepher Ferdinand Komba, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo;-

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa Serikali ni kuendelea na ujenzi wa mtandao wa reli nchi nzima. Hata hivyo, umejitokeza uvamizi mkubwa wa maeneo ya reli katika maeneo mbalimbali yanayopitiwa na reli.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali kupitia Shirika la Reli Tanzania (TRC) iliendesha zoezi la kutambua maeneo ya reli nchi nzima na kubaini uvamizi huo na hivyo kuchukua hatua ya kuweka alama ‘X’ na kutoa notisi ya kuwataka wananchi hao kupisha katika maeneo hayo. Kufuatia zoezi hilo TRC imekuwa ikipokea malalamiko kutoka kwa wananchi mbalimbali wakiwemo wananchi wa Muheza. Shirika la Reli Tanzania (TRC) limeanza kukutana na viongozi wa mikoa mbalimbali husika ili kufahamu sababu za madai hayo katika maeneo ambayo ni hifadhi ya reli.

Mheshimiwa Naibu Spika, ifahamike kuwa maeneo yote yaliyowekwa alama ‘X’ ni hifadhi halali ya reli na mipaka yake iiwekwa tangu mwaka 1967 kupitia ramani ya mipaka ya reli.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo nimuombe Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Muheza kuwa na utaratibu wa kupata taarifa za kina za matumizi ya maeneo husika kabla ya kuyatwaa na kuanza kuyaendeleza kwani husababisha usumbufu kwa Serikali na hasara kwa mali zilizoendelezwa katika maeneo hayo.
MHE. HAWA A. GHASIA (K.n.y. MHE. RASHID A. AJALI) aliuliza:-

(a) Je, kipimo halisi cha barabara kwa barabara kuu ya lami ni kipi?

(b) Je, upana kwenye miji ipitayo barabara unafanana na eneo ambalo halina makazi?

(c) Kama upana haufanani kwenye miji na eneo ambalo halina makazi, je, nini kipimo halisi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Akbar Ajali, Mbunge wa Newala Vijijini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa kifungu namba 12 cha Sheria ya Barabara (The Roads Act) namba 13 ya mwaka 2007 na Kanuni zake za mwaka 2009, barabara kuu ni barabara ambazo huunganisha makao makuu ya mkoa mmoja na mkoa mwingine au makao makuu ya mkoa na mji mwingine mkubwa au bandari au uwanja wa ndege au nchi jirani. Kwa mujibu wa kanuni namba 29(1)(a) ya Kanuni za Usimamizi wa Barabara (The Roads Management Regulations) ya mwaka 2009, upana wa eneo la hifadhi ya barabara kuu ni mita 60 yaani mita 30 kutoka katikati kila upande wa barabara. Aidha, kifungu namba 27(1)(a) kimeweka upana wa njia (lane) kwenye barabara kuu kuwa mita 3.25.

Mheshimiwa Naibu Spika, upana wa eneo la hifadhi ya barabara kuu hufanana kwenye miji na kwenye eneo ambalo halina makazi bali upana wa njia hutofautiana kati ya maeneo ya miji na maeneo yasiyo na makazi. Kufuatana na kifungu namba 50(1)(d) cha Kanuni ya mwaka 2009 upana wa njia huongezeka kwa mita 1.5 hadi 2.5 kwa kila upande wa barabara kwenye maeneo ya makazi yenye watumiaji wengi wa barbara kwa ajili ya usalama wa waenda kwa miguu na waendesha baiskeli.
MHE. MARY P. CHATANDA (K.n.y. MHE. AGNESS M. MARWA) aliuliza:-

Tangu ujenzi wa barabara ya Makutano, Sanzate hadi Natta uanze umepita muda mrefu bila mkandarasi huyo kukamiisha kazi.

Je, ni lini ujenzi huu wa barabara utakamilika ili kuwaondolea adha wananchi wanaotumia barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Agness Mathew Marwa, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Makutano Juu – Sanzate – Natta ni sehemu ya barabara ya Makutano Juu – Natta – Mugumu – Loliondo – Mto wa Mbu – Makuyuni yenye urefu wa kilometa 437.

Mheshimiwa Spika, sehemu ya barabara hii kuanza Makutano Juu-Sanzate kilometa 50 inaendelea kujengwa kwa kiwango cha lami na ubia wa Wakandarasi wazawa waitwao M/s Mbutu Bridge JV kwa gharama shilingi bilioni 50.4 na kusimamiwa na Kampuni ya Mshauri Elekezi M/s UWP Consulting (T) Ltd. ya Tanzania kwa kushirikiana na Kampuni ya Mshauri Elekezi M/s Consulting Ltd. kutoka Afrika Kusini.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa barabara hii ulianza tarehe 5 Aprili, 2013 na ilipaswa kukamilika tarehe 16 Mei, 2015 na aliongezewa muda hadi tarehe 28 Februari, 2019.

Hata hivyo kutokana na changamoto mbalimbali zikiwemo mabadiliko ya usanifu wa tabaka la msingi wa barabara kutoka usanifu wa awali wa G45 kwenda usanifu tabaka la saruji (CM) kucheleweshwa kwa malipo ya fidia pamoja na mvua nyingi zilizonyesha wakati wa ujenzi huo zilisababisha maradi huu kusimama kwa muda mrefu. Kutokana na changamoto zilizijitokezo wakati wa ujenzi wa barabara hiyo, mkandarasi ameomba muda wa nyongeza utakomwezesha kumaliza ujenzi wa barabara hii mwezi Januari, 2020 ambapo maombi hayo yanafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa ujenzi wa barabara hii unaendelea vizuri ambapo maendeleo ya kazi kwa ujumla yamefikia asilimia 70.8. Aidha, ujenzi wa daraja kubwa la Kyaramo na madaraja madogo saba katika mradi kusika yamekamilika kwa asilimia 100, hivyo endapo Serikali itaridhia maombi ya mkandarasi kuongezwa muda, inatarajiwa kwamba ujenzi wa barabara hii utakamilika mwezi Januari, 2020.
MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:-

Ujenzi wa barabara ya Makutano-Nyamuswa- Sanzate.

(a) Je, ni lini barabara ya Makutano Juu - Sanzate itakamilika?

(b) Je, Serikali kupitia wataalam wake imeridhika na kiwango cha uwekaji lami katika barabara hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa ujenzi wa barabara ya Makutano Juu - Sanzate-Mgumu - Loliondo - Mto wa Mbu (kilometa 452) ulianza tarehe 5 Aprili, 2013 chini ya Mkandarsi M/S Mbutu Bridge JV akisimamiwa na Mhandisi Mshauri UWP Consulting Tanzania Limited ya Dar es Salaam kwa kushirikiana na UWP Consulting Limited kutoka Afrika Kusini na hadi hivi sasa ujenzi umefikia asilimia 70.77 na mkandarasi ameomba nyongeza ya muda hadi mwezi Januari, 2020 ili kukamilisha mradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, ninapenda kumtaarifu Mheshimiwa Mbunge kuwa barabara ya Makutano Juu - Sanzate itakamilika ifikapo Januari, 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia wataalam wake, hususan Mhandisi Mshauri aliyeko eneo la mradi na wataalam wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) ngazi ya Mkoa na Makao Makuu kuhakikisha kuwa kazi ya ujenzi inakuwa na ubora hivyo materials zote za ujenzi hupimwa ili kuhakikisha ubora wa viwango vinavyotakiwa katika mradi husika. Kwa kuzingatia utaratibu huu, ujenzi unatekelezwa kwa mujibu wa mkataba.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapandisha hadhi barabara ya Katoro – Busanda – Nyakamwaga – Nyubululo – Kamena - Nyamalimbe – Mwingiro kuwa barabara ya Mkoa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lolensia Jeremiah Bukwimba, Mbunge wa Busanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kufuatia kuanzishwa kwa Wakala wa Barabara, Vijijini na Mijini (TARURA) barabara ya wilaya ikiwemo barabara ya Katoro Busanda – Nyakamwanga – Nyabululo – Kamena – Nyanalimbe – Mwingiro kilometa 68 zinahudumiwa na TARURA iliyoanzishwa mahususi kwa ajili hiyo. Hivyo zoezi la upandishwaji hadhi barabara kutoka barabara za Wilaya kuwa barabara za Mikoa ikiwemo kukasimu (designation) limesimamishwa kwa muda na Serikali kwa nchi nzima ili kuipatia TARURA fursa ya kutekeleza jukumu hilo mahususi la kuanzishwa kwake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia maelekezo hayo, namshauri Mheshimiwa Mbunge ashirikiane na Ofisi ya Rais TAMISEMI na TARURA katika kusimamia mipango yao kuhusu barabara hii. Hata hivyo, taratibu za kuomba kupandishwa hadhi barabara imeainishwa kwenye Kanuni Na. 43 na 44 za mwaka 2009 za Sheria ya Barabara Na. 13 ya Mwaka 2007 ambapo Bodi ya Mkoa ya Barabara (Regional Roads Board) huwasilisha maombi kwa Waziri anayehusika na barabara iwapo barabara tajwa itakuwa imekidhi vigezo vya kupandishwa hadhi.
MHE. MARY P. CHATANDA (K.n.y. MHE. ISSA A. MANGUNGU) aliuliza:-

Barabara ya Kilwa eneo la Rangi Tatu – Kongowe – Mikwambe inaharibika na ni finyu sana:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuijenga barabara hiyo kwa njia nne?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ali Mangungu, Mbunge wa Mbagala, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ipo katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya ujenzi wa barabara ikiwemo Barabara Kuu ya Kilwa kuanzia eneo la Rangi Tatu – Kongowe – (kilomita 3.8) na barabara ya Mkoa kuanzia Kongowe – Mikwambe – Kibada – Mji Mwema hadi Kivukoni (kilomita 17.55). Lengo ni kupunguza tatizo sugu la msongamano wa magari na ajali barabarani.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kilwa kuanzia Mbagala Rangi Tatu hadi Kongowe yenye urefu wa kilometa 3.8 inatarajiwa kupanuliwa toka njia mbili na kuwa njia nne kazi ambayo inahusisha pia upanuzi wa daraja la Mzinga. Kazi ya usanifu wa kina inaendelea na inatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Julai, 2019.

Mheshimiwa Spika, kazi ya upanuzi na matengenezo maalum kwa sehemu korofi ya barabara ya Kongowe – Mikwambe – Kibada – Mji Mwema hadi Kivukoni ilitekelezwa awamu kwa awamu kadri fedha zilivyopatikana. Kazi ya upanuzi awamu ya mwisho kwa barabara hii imekamilika mwezi Desemba, 2018 ilifanyika kati ya Mikadi na Kivukoni.
MHE. MARWA R. CHACHA aliuliza:-

Barabara inayojengwa kuunganisha Mkoa wa Mara na Arusha inasuasua sana, kwani tangu ilipoanza kujengwa 2013 mpaka leo hata kilomita 50 zimeshindwa kukamilika.

(a) Je, Serikali ina mkakati gani dhidi ya ukamilishaji wa barabara hii?

(b) Je, ni lini wananchi waliofanyiwa tathmini watalipwa fidia zao?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Marwa Ryoba Chacha, Mbunge wa Serengeti, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara inayounganisha Mikoa ya Mara na Arusha yenye urefu wa kilomita 452 kutoka Makutano Juu (Musoma) – Natta – Mugumu – Loliondo hadi Mto wa Mbu ilifanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na kukamilika mwaka 2013. Aidha, baada ya kukamilika kwa usanifu ujenzi wa barabara hiyo umeanza kwa awamu ambapo kilomita 50 kutoka Makutano Juu hadi Sanzate na kilomita 49 kutoka Wasso hadi Sale Junction unaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli mkandarasi amechelewa kukamilisha kazi kwa wakati kutokana na changamoto mbalimbali. Hata hivyo, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kupitia TANROADS imeshachukua hatua mbalimbali ili kuhakikisha kuwa mkandarasi anamaliza kazi iliyobaki kwenye barabara ya Makutano – Sanzate inayotarajiwa kukamilika mwezi Septemba mwaka huu. Sehemu ya pili ya Sanzete – Natta yenye urefu wa kilomita 40 ipo katika hatua ya manunuzi kwa ajili ya kumpata mkandarasi. Aidha, kwa upande wa Mkoa wa Arusha, kilomita 49 kutoka Wasso hadi Sale ujenzi kwa kiwango cha lami unaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wote waliofanyiwa uthamini wanaendelea kulipwa fidia zao kabla ya kazi ya ujenzi kuanza. Aidha, mpaka sasa waathirika nane (8) wamefidiwa kiasi cha shilingi 12.871 kwa Mradi wa Wasso – Sale kilomita 49. Katika Mradi wa Makutano – Sanzate kilometa 50 wananchi waliolipwa fidia ni watu 433 kwa jumla ya shilingi milioni 2.608. Ahsante sana.
MHE. JOYCE B. SOKOMBI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga barabara itokayo Bunda kwenda Musoma Vijijini ili kuwapunguzia wananchi wa Saragana, Bugoji, Mabui Merafuru, Melaturu, Kangetutya na Kanderema aidha ya kuzunguka kupitia Musoma Mjini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joyce Bitta Sokombi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo; ingawaje marekebisho aliyoyafanya sikuyapata sawasawa kwa hiyo kama nitakosea haya majina magumu naomba aniwie radhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipande cha barabara kuu kutoka Bunda hadi Manyamanyama chenye urefu wa kilomita 5.79 kinahudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Mara. Aidha, ukarabati wa kipande hiki ulikamilika mwaka 2016 na kwa sasa kipo katika hali nzuri hivyo kupitika kwa urahisi wakati wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Mkoa kutoka Manyamanya kupitia Vijiji vya Bugoji – Saragana hadi Nyambui kilomita 37.45 inahudumiwa na Wakala wa Barabara (TANROADS) Mkoa wa Mara na kwa sasa barabara hii inapitika vizuri. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali ilitenga jumla ya shilingi milioni 351.976 kwa ajili ya matengenezo mbalimbali ya barabara hii. Aidha, kwa mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali imetenga jumla ya shilingi milioni 130.855 kwa ajili ya kuendelea kuifanyia matengenezo mbalimbali barabara hii ili ipitike majira yote ya mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara inayoanzia Saragana hadi Kanderema kupitia Vijiji vya Mabui Merafuru na Kangetutya ni barabara ya wilaya ambayo ipo chini ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini (TARURA). Hivyo namshauri Mheshimiwa Mbunge awasiliane na TAMISEMI kuhusu mipango waliyonayo kwa sehemu hiyo ya barabara.
MHE. VUMA A. HOLLE Aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutatua mgogoro wa ardhi kati ya Kijiji cha Mgombe na Kambi ya Jeshi Mtabila?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijajibu swali, kwa ruhusa yako naomba nimshukuru Mungu kwa kunijalia afya njema na kuniwezesha kusimama hapa mbele ya Bunge lako. Vile vile namshukuru sana Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na Amirijeshi Mkuu wa Majeshi yetu kwa kuniamini na kuniteua kuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nawashukuru sana wananchi wa Jimbo la Ushetu, wapiga kura wangu kwa kuniamini na kunipitisha bila kupingwa na kwa kura nyingi ambazo walizitoa kwa Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakupongeza wewe pamoja na Spika kwa ushindi mkubwa na kuaminiwa na Bunge hili. Vile vile nawapongeza Wabunge wote kwa kuchaguliwa na wananchi kuwa Wabunge wa Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa napenda kujibu swali la Mheshimiwa August Vuma Holle, Mbunge wa Kasulu Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kambi ya Jeshi ya Mtabila – 825/KJ ipo Wilayani Kasulu, Mkoani Kigoma. Eneo husika lina ukubwa wa ekari 12,206.05 ambalo awali lilitumiwa kama Kambi ya wakimbizi. Aidha, mwaka 2012 eneo hili lilikabidhiwa kwa Jeshi na kuwa Kiteule na mwaka 2014 kiliundwa Kikosi cha Jeshi Mtabila.

Mheshimiwa Naibu Spika, mgogoro wa ardhi ulianza baada ya wananchi wa Vijiji vya Mgombe na Katonga kuvamia eneo hilo kwa shughuli za kilimo na hatimaye kuweka makazi. Kwa sasa wananchi waliokuwa wamevamia eneo hilo wameondolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imeanza kuutatua mgogoro uliopo kwa kufanya vikao na uongozi wa Wilaya. Tarehe 11 na 12 Januari, 2021 Viongozi wa Kikosi cha Jeshi Mtabila walikutana na Uongozi wa Wilaya ya Kasulu na kuamua kuihamisha barabara inayokuwa inapita katikati ya kambi kuelekea Kijiji cha Shunga hadi Nchi ya Burundi ipite mpakani mwa eneo la Kambi. Pia, TANROADS wameweka alama za barabara tarehe 13 Januari, 2021 ikiwa ni hatua ya kuitambua barabara hiyo na kuiendeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu itatuma timu ya wataalam kukutana na uongozi wa Mkoa, Wilaya na Vijiji husika kwa lengo la kutatua mgogoro huo. Nawaomba wananchi wawe na subira wakati Serikali inalifanyia kazi suala hili na kulipatia ufumbuzi. Aidha, Wizara inawasihi Viongozi wa ngazi zote kuwaelimisha na kuwasisitiza wananchi katika maeneo yao kutovamia maeneo ya Jeshi. (Makofi)
MHE. OMAR ISSA KOMBO Aliuliza:-

Je, ni kwa nini Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) limewarudisha nyumbani Vijana ambao walishafika Kambini kwa ajili ya kuanza mafunzo?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Omar Issa Kombo, Mbunge wa Wingwi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, JKT ilisitisha mafunzo ya vijana wa kujitolea kwa mwaka wa fedha 2020/2021 kutokana na sababu zifuatazo:-

(1) Kutoa nafasi kwa JKT kutathmini mafunzo yaliyofanyika na kuandaa utaratibu wa kuwa na mitaala bora ya mafunzo ya vijana itakayowawezesha vijana hao kujitegemea wanapomaliza mafunzo badala ya kutegemea kuajiriwa.

(2) JKT kwa kushirikiana na Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kufanya mawasiliano na taasisi zingine kama, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Tume ya Vyuo Vikuu na Baraza la Mitihani (NECTA) kuandaa utaratibu wa kuongeza muda wa mafunzo ya vijana wa mujibu wa sheria kuwa mwaka mmoja badala ya miezi mitatu ya sasa na kuchukua vijana wengi zaidi wanaomaliza kidato cha sita huku idadi ya vijana wa kujitolea ikipunguzwa.

(3) Kutoa fursa kwa JKT kukamilisha mpango wa kuwawezesha vijana kupata mitaji wanapohitimu mafunzo kwa kushirikisha taasisi nyingine ambazo ni Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Fedha na Mipango, Wizara ya Kazi na Vijana na TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa mkakati huu utasimamiwa na Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, JKT itaendelea kutoa elimu kwa umma na kwa vijana wanaojiunga na JKT kujitolea kuelewa kwamba, lengo la mafunzo ni kuwawezesha waweze kujitegemea baada ya mafunzo hayo badala ya kutegemea ajira.
MHE. MOHAMMED MAULID ALI Aliuliza:-

(a) Je, Serikali inatambua mgogoro wa ardhi baina ya wananchi na Kambi ya Jeshi la Wananchi iliyopo Chukwani Zanzibar?

(b) Je, Waziri yupo tayari kufuatana na Mbunge ili kukutana na wananchi na kufahamu hali halisi ya mgogoro huo uliodumu kwa muda mrefu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maulid Ali Mohammed, Mbunge wa Jimbo la Kiembe Samaki lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-


(a) Mheshimiwa Spika, Kambi ya Chukwani imepimwa na inatambuliwa kama Kiwanja Namba 787 na ramani yake imepata usajili Namba S.40/07. Eneo hili limepewa Hati Miliki Namba Z.20.2007. Hata hivyo, kuna wananchi wachache wanafanya shughuli za kibinadamu ndani ya eneo la kambi. Wananchi hawa sio wavamizi, wanatakiwa kulipwa fidia kwani ni maeneo yao ya siku nyingi kabla ya Jeshi kutwaa na kupima eneo hilo, pia ilikubalika waondoke baada ya kufanyiwa uthamini na kulipwa fidia.

Mheshimiwa Spika, Wizara inatambua mgogoro huo na hivi sasa ipo katika mpango wa miaka mitatu wa kuondoa migogoro yote iliyopo katika maeneo yake ikiwemo Kambi ya Jeshi ya Chukwani iliyopo Zanzibar. Mpango huo utajumuisha na kupatiwa Hati Miliki za maeneo yake yote.

(b) Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa alikuwa anauliza kwamba tupo tayari kwenda kuonana na wananchi. Nimwambie tu kwamba tupo tayari kwenda kuonana na wananchi ili tuweze kukaa nao, tujue sasa asili na chanzo cha mgogoro huo na tuwaeleze hatua ambayo tumefikia kama Serikali. Nakushukuru.
MHE. FLORENT L. KYOMBO Aliuliza:-

(a) Je, ni kwa nini Jeshi la Wananchi wa Tanzania lisifuate utaratibu, ili kumiliki eneo la wananchi wa Kitongoji cha Byawamala, Kijiji cha Bulifani, katika Kata ya Kyaka, badala ya kuhamia eneo hilo kwa nguvu na hivyo kuibua mgogoro kuhusu eneo hilo?

(b) Je, ni kwa nini eneo hilo lisigawanywe kwa Jeshi na Wananchi kwa kuwa eneo hilo ni kubwa na limekuwa pori kwa sasa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI K.n.y. WIZARA YA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Florent Laurent Kyombo, Mbunge wa Nkenge, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, eneo la jeshi linalotambulika kama Kiteule cha 21- KJ lipo Bulifani, Kyaka, Wilaya ya Misenyi. Eneo hili lilitumika wakati wa Vita vya Uganda kwa kujikinga na kuyashambulia majeshi ya Nduli Idd Amin Dada. Mpaka sasa eneo hilo bado lina mahandaki yaliyotumika wakati wa vita. Hivi sasa eneo hili linakaliwa na askari wetu na limekuwa Kiteule cha 21-KJ Kaboya.

Mheshimiwa Spika, mwezi Julai, 2021 timu ya wataalamu wa ardhi kutoka Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa walikwenda kutembelea eneo hilo na kufanya tathmini ya uthamini na upimaji. Eneo hili litaingizwa kwenye mpango wa miaka mitatu ya kuondoa migogoro iliyopo katika maeneo yote ya jeshi, mpango ambao umeanza Aprili, 2021. Naomba wananchi wawe na subira katika kipindi hiki kifupi kilichobakia.

Mheshimiwa Spika, eneo hili halitaweza kugawanywa kwa wananchi kwa kuwa, lipo kwa matumizi ya jeshi na eneo hili limekaa kimkakati zaidi. Nakushukuru.
MHE. MICHAEL M. KEMBAKI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaupatia ufumbuzi mgogoro wa ardhi kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania na wa kazi wa Mtaa wa Kinyambi na Bugosi katika Halmashauri ya Mji wa Tarime?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, kabla sijajibu swali na kwa ruhusa yako naomba nimshukuru Mungu kwa afya na kuniwezesha kusimama hapa. Kwa vile ni mara yangu ya kwanza kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Rais mama yetu mama Samia Suluhu Hassan kwa kuniacha niendelee kutumika kwenye Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kama Waziri. Baada ya shukrani hizo naomba sasa kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Kambaki Michael Mbunge wa Tarime Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wananchi waliokuwepo kabla ya eneo kuchukuliwa na Jeshi hawajalipwa fidia. Uthamini uliofanywa na Halmashauri ya Tarime ulikamilika na ambapo kiasi cha shilingi 1,651,984,692.76 zilihitajika. Jedwali lilipelekwa kwa Mthamini Mkuu wa Serikali mwezi Machi 2020 kupata idhini na lilirejeshwa Tarime kwa marekebisho.

Mheshimiwa Spika, mwezi Machi, 2021 Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa iliwasiliana na Halmashauri ya Wilaya ya Tarime na majibu yaliyotoka ni kwamba, uthamini huo utarejewa kwa kuwa ulifanywa kwa muda mrefu na pia baadhi ya nyaraka zilikosekana kuhalalisha fidia hiyo.

Mheshimiwa Spika, Wananchi wa Mtaa wa Kinyambi na Bugosi wanaombwa wawe na Subira katika kipindi hiki ambacho Halmashauri inafanya taratibu za kurejea uthamini huo. Utaratibu wa uthamini utakapokamilika Serikali italipa fidia kwa wananchi hao kwa mujibu wa Sheria, Kanuni na Taratibu za nchi.
MHE. AHMED YAHYA ABULWAKIL aliuza:-

Je, ni lini Serikali itawaunga mkono wananchi wa Chukwani waliojitolea kujenga Kituo cha Polisi cha ghorofa moja kwa kumalizia ujenzi wa kituo hicho?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-

Mheshimwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ahmed Yahya Abdulwakil Mbunge wa Kwahani, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa Kituo cha Polisi Chukwani ulianza mwaka 2015 na unatekelezwa kwa mchango wa nguvu za wananchi na wadau werevu wa Ulinzi na Usalama huku Jeshi la Polisi likitoa wataalam wa ushauri na usimamizi kwa mafundi wake. Gharama ya ujenzi inatarajia kufikia kiasi cha shilingi 98,000,000/= hadi kukamilika kwake. Kwa sasa ujenzi umefikia hatua ya kumalizia (finishing) na gharama za kumalizia zinahitajika shilingi 40,000,000/=.

Mheshimiwa Spika, Serikali inafanya utaratibu wa kutumia fedha za mfuko wa Tuzo na Tozo ili kumalizia ujenzi wa vituo mbalimbali vilivyosimama katika ujenzi kutokana na kukosa fedha kikiwemo Kituo cha Polisi Chukwani. Hata hivyo, kwa kushirikiana na wananchi na wadau werevu, Kituo hiki kitaendelea kukamilishwa ili kianze kazi ya kuwahudumia wananchi wa eneo hili na maeneo jirani. (Makofi)
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA aliuliza:-

Je, ni gharama kiasi gani na taratibu gani hutumika ili kupata huduma za ulinzi za SUMA JKT?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, huduma ya Ulinzi toka SUMA JKT Guard inapatikana kupitia njia kuu nne, ikiwemo:-

(1) Idara ya masoko kutembelea wadau wa huduma ili kutangaza shughuli za kampuni;

(2) Mteja mwenyewe kuwasilisha barua za maombi ya kupatiwa huduma ya ulinzi;

(3) Kampuni imesajiliwa katika mfumo wa manunuzi ya Serikali ya TANEPS ambapo wadau, hasa Taasisi za Serikali hutumia kutangaza zabuni.

(4) Ushiriki katika mchakato wa zabuni shindanishi zinazotangazwa kupitia magazeti na vyombo vya habari.

Mheshimiwa Spika, naomba nifafanue zaidi kuwa gharama ya kupata huduma za ulinzi za SUMA JKT Guard kwa mlinzi mmoja bila silaha ni shilingi 590,000 kwa mwezi ikijumuisha VAT, lakini silaha moja ni shilingi 129,800 hivyo mlinzi akiwa na silaha, gharama yake ni shilingi 719,800 kwa mwezi. Huduma ya mlinzi mmoja kwa maeneo ya migodini ni shilingi 944,000/= ikiwa ni pamoja na VAT kwa mwezi.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA aliuliza: -

Je, ni lini wananchi wa Kata ya Mwakijembe ambao mashamba yao yalitwaliwa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) watalipwa fidia?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dunstan Luka Kitandula, Mbunge wa Mkinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania lilianzisha Kituo cha Ulinzi mwaka 2017, eneo la Kata ya Mwakijembe. Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Mkinga Mkoani Tanga iliona umuhimu wa kutenga eneo hilo kwa matumizi ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania ili kuimarisha ulinzi kwenye maeneo ya mpakani. Aidha, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama ilitembelea eneo husika mwaka 2017 kujionea hali halisi. Eneo husika awali lilikuwa ni la mradi wa Serikali wa umwagiliaji maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kata ya Mwakijembe wanaombwa wawe na subira pindi taratibu za kisheria za utwaaji wa eneo zikikamilika. Serikali italipa fidia kwa wananchi kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia sababu zilizotolewa hadi Jeshi kukabidhiwa eneo hilo, Jeshi litaendelea kutumia eneo hilo wakati taratibu za ulipwaji wa fidia zinaendelea.