Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Andrew John Chenge (20 total)

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii niweze kuchangia kidogo tu katika hoja hizi mbili zilizo mbele ya Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa taarifa zake nzuri alizoziwasilisha siku ya Jumatano, tarehe 8 Juni humu Bungeni, kwa maana ya kwamba ile taarifa ya uchumi (the state of the economy) pamoja na taarifa kuhusu utekelezaji wa Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2015/2016 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka ujao wa fedha. Aliziwasilisha kwa ufasaha, na nimshukuru sana na timu yake, sio kazi rahisi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, hii ni bajeti ya kwanza kwa uongozi wa awamu ya tano ya nchi yetu. Lakini kama ilivyo bajeti yoyote, lazima uangalie kwa mwaka uliopita, kwa maana hiyo ni mwendelezo wa hayo mazuri ambayo yamefanyika huko nyuma, na tunaendelea kuyaboresha zaidi. Na unaiona sura ya bajeti hii, imebeba mambo mengi mazuri, ukianzia kwenye mpango, na bahati nzuri mwaka huu tunaanza kutekeleza mpango huu wa pili wa maendeleo, na mwaka wa kwanza katika Mpango huo wa Pili wa Maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, na kwenye taarifa ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 30, ameeleza maeneo ya vipaumbele katika mwaka ujao wa fedha; yapo katika makundi manne, kwa sababu ya muda sitaweza kuyasema, lakini ndiyo naona mwelekeo mzuri wa kule ambako Serikali inataka kuipeleka nchi yetu, lakini hasa katika kukuza uchumi na hivyo kuleta ustawi mzuri wa wananchi wetu, mimi naipongeza sana Serikali kwa hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili, niwapongeze sana, unafahamu ukiangalia mapato, ongezeko la makusanyo ya mapato, Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Naibu Spika, lazima tuipongeze Serikali, tuipongeze TRA na wote hao walioifanikisha kwa sababu kwa mara ya kwanza tumeweza kwenda zaidi ya shilingi trilioni moja kwa mwezi, sio kitu kidogo, ukilinganisha na mwaka jana ambapo tuliweza kwenda mpaka shilingi bilioni 900 na kitu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tuna changamoto kubwa ambayo Waziri wa Fedha ameielezea kwenye hotuba hii, kwamba tukiweza kuyasimamia maeneo ambayo tunajua ni oevu kwa mapato ya Serikali, tutaweza kufanya vizuri zaidi. Ameelezea matumizi ya mfumo wa zile mashine elektroniki. Tupende tusipende Waheshimiwa, najua bado utamaduni wetu wa kutodai risiti na kutotaka kufanya nini, bado, lakini huu ni mwanzo mzuri. Tukiweza kuyasimamia hayo sasa hii dhana nzima mimi naiona ya kuingiza mapato yasiyo ya kodi kwamba TRA iyakusanye, mimi naamini tutafanya vizuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili la misitu na mazao yanayotokana na misitu, mimi naelewa there is a lot to be collected na ninarudia msemo wa Kiingereza; taxes are never paid, taxes are collected. Na tukiangalia maeneo ambayo tunajua yapo mapato halali ya Serikali tutayakusanya, na hilo nimpongeze sana Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa kuanza na kasi hiyo ya kuziba mianya ambayo ilikuwa inapoteza mapato ya Serikali. Kwa hiyo natoa pongezi hizo kwa nia njema kabisa na kuwataka wote tukaze buti, twende mbele kwa faida ya Taifa hili. (Makofi)
Kwa Watanzania, na sisi kama viongozi, mimi nasema kama tunataka Tanzania uchumi ukue, lazima tukubali wote sasa leo tutoe jasho kidogo kwa faida ya kesho. Unaumia leo, lakini unajua unajenga msingi imara wa uchumi wa nchi yako kwa faida ya watoto wako, kwa faida ya wajukuu zako, kwa faida ya Tanzania hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna eneo moja, wataalam wa uchumi watasema, lakini mimi niliyefundishwa, unaiona kabisa bajeti ya Serikali, nia ni nzuri kabisa lakini nakisi ya bajeti tuliyonayo ni shilingi trilioni 7.48. Sasa imepanda kidogo ukilinganisha na huu mwaka tunaomaliza na ukiipima dhidi ya Pato la Taifa unaona imepanda kutoka asilimia 4.2 kwenda asilimia 4.5, sasa hii ina implications nyingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nasema wataalam wetu waliangalie hili, kwa sababu standard norm ni asilimia tatu, sasa tukiruhusu iende kwa speed hiyo, hii nakisi ya bajeti itatusumbua. Ukiangalia kwa sasa Waziri anapendekeza shilingi trilioni 5.37 zipatikane kutoka ndani, maana yake ni nini kwa benki zetu? Kwa benki zetu hizi, shilingi trilioni 5.37 ni pesa nyingi, na maana yake uwezo wa sekta binafsi kwenda kufika tena kwenye benki hizi tunaanza kuiminya; tulione hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mimi nasema lazima tukope na nilisema juzi, tunakopa pesa hizi kwa masharti yapi na tunazielekeza wapi? Naona haziendi kwenye matumizi ya kawaida, hongereni sana Serikali kwa hilo, zinakwenda kwenye maendeleo, zinakwenda kulipa hati fungani na dhamana za Serikali ambazo zimeiva, huo ni utaratibu wa kawaida. Lakini sehemu kubwa inakwenda kwenye maendeleo na ndiko tunakotaka tuone. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilisema juzi wakati tunajadili Fungu 50 (Vote 50), basi Serikali itueleze zoezi la nchi yetu kupata sovereign rating limeishia wapi? Kwa sababu tukiweza kupata sovereign rating na inakuwa inahuishwa kila wakati tutaweza ku-access mikopo hii kwa gharama nafuu lakini pia na Private Sector itaweza na yenyewe hivyohivyo ikapata access kwenye masoko ya Kimataifa kupata fedha ambazo tunazihitaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niunganishe hapo hapo miradi ya maendeleo kwa upande wa PPP. Kweli twende mbali zaidi, maana sasa hivi kila siku unaambiwa ni mradi wa Dar es Salaam, mabasi ya kasi yale; sawa ni PPP ile au kutengeneza dawa inasemwa inakuja, sawa, barabara ya Chalinze - Dar es Salaam, sawa, Kinyerezi umeme sawa. Lakini yapo maeneo mengi, kwa nini Serikali inakuwa nzito sana katika eneo hilo la ubia kati ya sekta binafsi? Kwa sababu hiyo ndiyo itaiwezesha Serikali kuachana, maeneo fulani yaende kwa sekta binafsi kwa ubia na Serikali, tufanye hivyo kwa haraka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwisho, unaona ukurasa wa sita wa taarifa ya uchumi, kilimo...
Ohoooo! Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, naunga mkono hoja hizi mbili.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii niweze kuchangia kidogo kuhusiana na mapendekezo ya mpango wa maendeleo ya Taifa kwa mwaka 2020/2021 ambao ndio utakuwa umefika ukomo wa kipindi cha miaka mitano kwa huu mpango wa pili ambao tumeanza kuutekeleza tangu 2016/2017.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na timu yake kwa kutuletea mapendekezo haya na wewe umesema sasa hivi vizuri sana huu ni mwendelezo katika utekelezaji wa mpango wa pili wa maendeleo ya Taifa ambao tumeingia sasa huu mwaka wa nne. Ni kweli lazima tu-take stock na ndio maana Serikali inakuja hapa na mapendekezo haya. Sisi kama wadau kama sehemu ya uongozi wa Taifa hili ambao tumeaminiwa na watanzania wema katika nyumba yao hii tuweze kuona namna ya kuboresha, kuishauri Serikali ndio kazi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge waliotangulia katika kuchangia tuisaidie Serikali maana nikilalamika nikishamaliza kulalamika kwani itakuwa imesaidia? Saidia kuonyesha njia, mimi nadhani tukienda hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa haya makubwa inayoyafanya sasa unaweza usione muunganiko wa moja kwa moja kwa maendeleo ya mwananchi mmoja mmoja kwa Bwawa la Nyerere la kufua umeme. SGR inayojengwa hata ndege hizi zinazonunuliwa lakini nawaambieni miradi hii itakapokamilika suala tunalosema la tija, ufanisi kwenye viwanda vyetu, umeme ndio kichocheo kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia reli hii ambayo nitaisemea sasa hivi reli ya kati ndio kiini ni injini ya ukuaji wa uchumi wa mataifa yote na ndege hizi utalii watanzania Mwenyezi Mungu ametujalia kitu ambacho lazima tuendelee kukinufaika, tunufaike nacho sasa na kesho na kesho kutwa. Pesa hiyo ndio inayoenda kusaidia kuboresha huduma za jamii kama afya, maji yote haya ambayo tunayaongelea kwa faida ya watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitaki kuchukua muda mwingi kwa hilo lakini sisi kazi yetu tuishauri Serikali katika maeneo ambayo tunadhani tunaweza tukafanya vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na hili la kilimo, limesemwa vizuri sana kwenye taarifa ya waziri aliyowasilisha; niseme pia ni Mjumbe wa Kamati ya Bajeti tumeyasema sana lakini nashukuru taarifa ya Kamati ya Bajeti. Waheshimiwa Wabunge isomeni lakini tumeongea sana na Serikali kwenye kamati kusaidia haya mawazo na sisi tunabaliana na wengi mnaosema kwenye kilimo, kwenye uvuvi, kwenye mifugo huko tukiweza kuboresha hayo maana ndio sekta ambazo ukinyanyua hizo ndio zinaunganisha na zinachochea ukuaji wa sekta nyingine ifanywe vizuri kwenye kilimo nasema kilimo cha Tanzania kama tutafanikiwa kikuwe kwa kasi asilimia sita na tukawa persisted kwa kipindi kirefu miaka 10, 20 utaona mchango wake kwa Pato la Taifa tulikuwa kubwa sana na ndio itabeba wananchi wengi kuwaondoa katika lindi la umasikini, mipango ndio hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimia naomba sana katika vipaumbele vya mwaka kesho tuweke intervention kubwa tupeleke kwenye kilimo pia kwenye mifugo, kwenye uvuvi ionekane kwenye bajeti yetu kwenye sekta hizo kupitia mpango huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naelewa Serikali maana tunamaliza mpango huu wa pili mwakani ndio tutakuwa Bunge litakuwa karibu linakaribia kuvunjwa lakini Tanania ipo itaendelea kuwepo wananchi wa Tanzania watakuwepo na Serikali itaendelea kuwepo na Bunge la Tanzania litaendelea kuwepo, kwa hiyo watakaorejea tunataka tuje tuone angalau ifanyike tathimini ya kipindi tuone mpango wa pili wa miaka mitano ambao tulikuwa tumemaliza kuutekeleza kipindi hicho tunapoenda kwenye mpango wa tatu wa maendeleo ya Taifa letu tuone ni nini ambacho tumefanikiwa sana, nini maeneo gani hatukufanikiwa sana, nini kifanyike ili tunapoenda kwenye mpango huo wa tatu na wa mwisho tuwe kweli confidence.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali hata katika hatua hii kwa sababu kupanga mwalimu alikuwa anatukumbusha kupanga ni kuchagua tungekuwa na rasilimali nyingi ambayo unaweza kutekeleza yote haya kwa wakati mmoja tungeweza kufanya hivyo lakini hatuna lazima kile kidogo ambacho tumekubaliana kukifanya tukifanye kwa ufanisi na ndio maana mimi nasema naelewa baadhi yetu tungependa tuone mambo tunasema haya ni mengi mno tuliyoyabeba, lakini utafanyaje Tanzania hii nchi ni kubwa tuna wananchi milioni karibu 53,000,000 lazima uende hivyo unaumia hapa kidogo lakini huko mbele wengine panaenda vizri, ukifanya stock nzima unasema Tanzania inasonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa reli concern yangu iko kwenye taarifa ya bajeti kama ripoti ya taarifa ya bajeti Kamati ya Bajeti tunafanya vizuri tumetumia pesa ya ndani jasho la Watanzania kutoka Dar es Salaam mpaka Morogoro heshima kubwa kwa nchi hii heshima ehee! Tujivunie wananchi pesa ya ndani tumekopa kutoka Morogoro kuja Makutupora ndio lakini ni mkopo wetu wa Watanzania. Na tunajiandaa sasa tutafute pesa nyingine kutoka Makutupora kwenda Tabora, kwenda Isaka, kwenda Mwanza na baadae kwenda Tabora, kwenda Kigoma, Uvinza Msongati tutatoka Kaliuwa, Mpanda tuende mpaka Kalema, ndio mipango yetu hii kalema kwenye Lake Tanganyika tuna mipango tunaiona Tanzania na majirani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nini concern yetu na ndio imo kwenye taarifa ni kwamba tunachukua mikopo hii bahati mbaya ni ya muda mfupi, masharti yake ingependeza kama tungeshambulia reli hii, ujenzi wa reli hii kwa wakati mmoja kwa sababu tunajua pesa hizi kwa kupata mkopo wa muda mrefu itakuwa ni ngumu sana lakini tukiweza vipande hivi tukavishambulia kwa wakati mmoja tutakuwa tumekamilisha ujenzi wa reli hii na matawi yake muhimu haraka sana na ndio tutaona faida, ndio ushauri wetu huo kwa Serikali. Naelewa misaada imepungua sana, mikopo ya masharti nafuu imepungua sana, eneo ambalo tunaweza tukapiga hodi na nadhani tumekaa vizuri ni kwenye export credits iwe ni ya Waingereza ya Wafaransa ya Wajerumani angalau ukipata mkopo ule mpaka miaka 21 window hiyo ipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri naiomba Serikali tuangalie option hizo tutafanya vizuri na kwenye reli nasema reli hii tuikamilishe naomba sana Serikali reli hii ya Kati tuikamilishe na ningependa sana ndoto aliyonayo Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli aikamilishe reli hii wakati wa uongozi wake heshima kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho tuna miradi mikubwa kwanza nipongeze kazi nzuri ya Dar es Salaam Bandari Port Gati moja mpaka namba 7 ile kazi inaenda vizuri, tunapanua lango pale kuingilia kazi nzuri. Mtwara inaenda vizuri sana is the natural Port Mtwara is the deep sea Port ehee nashukuru sana Magati yale yanaongezeka. Tanga ya sasa na sawa tunawekeza kwenda toka mita depth ya mita
4 kwenda 15 lakini Mwambani ndio yenyewe Tanga Mwambani ndio kwenyewe eehe tuangalie huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini narudia kama kwa Bagamoyo tumeona muwekezaji huyo hafai haimaanishi kwamba mradi wa Bandari ya Bagamoyo haufai hapana, tutafute muwekezaji mwingine ambaye ataendana na matakwa yetu ili bandari ya Bagamoyo ijengwe ndio matumaini ya Taifa hili Dar es Salaam pamoja na maboresho yanayoendelea hatutaweza kupata meli zile kubwa za tani kuanzia 50,600 yale yanaitwa ports kwanama yale hayawezi kuingia kwenye lango la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba Liganga na Mchuchuma tukamilishe mazungumzo kama imeshindikana na muwekezaji huyo tutafute mwingine lakini hii taarifa hii kila mwaka tunarudi nayo mpaka tunataka kumaliza miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua muda wangu ndio huo lakini mimi naipongeza sana Serikali Mheshimiwa Waziri wa Fedha na timu yako hongereni sana tuwaunge mkono najua changamoto ni mapato tuwasaidie ni maeneo yapi tunadhani tunaweza tukaongeza to argument mapato ya Serikali ya ndani hasa mapato ya ndani ya kodi ya siyo ya kodi mnaona tangu tuanze matumizi ya ufanisi wa electroniki, mapato yanaongezeka ya kodi lakini pia na yasiyo ya kodi. Nadhani likisimamiwa vizuri tutaweza kupanda kutoka kwenye trilioni 1.2 ambao tumegota kidogo sasa na tukaweza kuongeza mapato yetu. Tuangalie maeneo mengine ameyasema vizuri Mheshimiwa Masoud eeh! Bahari ya Hindi tutumie, blue economy ya Tanzania hiyo hiyo tuichukue vizuri tufanye mambo makubwa, inawezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umenipa heshima umenivumilia mchango wangu ni huo tuhimize tufanye maamuzi ya haraka katika maeneo ya vipaumbele ambayo tumejiwekea sisi wenyewe nakushukuru sana ubarikiwe sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.4) wa Mwaka 2016
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii jioni ya leo. Nianze kwa kusema naunga mkono hoja hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kabla sijaanza kuchangia, napenda nichukue nafasi hii na mimi kuwapongeza Wabunge wenzetu hawa wanne; Mbunge wa Jimbo la Dimani Mheshimiwa Juma Ali Juma, na walioteuliwa na Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, rafiki yangu Profesa Palamagamba Kabudi na rafiki yangu Abdallah Bulembo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, na niseme tu mimi na ninaamini kwa Wabunge wote tunawahakikishia ushirikiano wa karibu na niwatakie kila lililo jema katika shughuli zenu za Ubunge, karibuni sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili niishukuru sana Serikali kupitia Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa muswada huu, amewasilisha vizuri shabaha ya muswada huu, marekebisho yote ambayo yamebebwa na muswada huu katika sehemu mbalimbali. Ni muswada mzuri na huwa nasema mimi mara nyingi humu Bungeni, uzuri wa sheria yeyote ni pale unapoanza kuitumia ndipo utaona. Mojawapo kazi kubwa ya Bunge hili ni kutunga sheria, hatuwezi kuogopa kutunga sheria kwa kusema kwamba kitu hiki kimeletwa haraka sana, lakini tunapaswa sasa tuwe watulivu na tujenge hoja ambazo zinaweza zikaboresha muswada. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi namheshimu sana rafiki, msomi mwenzangu Tundu Lissu, kayasema mazuri tu mengine. Lakini mimi ningesaidia kama angeenda step further kutusaidia hapa kifanyike nini? Ame-fall shot ya hiyo, because hata mimi hapa naweza nikalalamika tu hapa, lakini nikishamaliza kulalamika hatujalisaidia Bunge, hatujasaidia nchi, lakini bado tuna muda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, muswada huu mimi nitajielekeza kwenye eneo moja tu hili la mikopo, dhamana na misaada ya Serikali. Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mikopo ya nje na dhamana inayotolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mikopo hiyo, suala la Muungano, hasa utatungaje au utaletaje sheria ambayo inakinzana na matakwa ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maana inayoweza kwenda kukopa nje, ni ile sovereign inayotambulika Kimataifa, ambayo ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Sasa kupitia muswada huu inapendekezwa angalau tufanye utaratibu ambao utawezesha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwenda kupata mikopo hii, lakini kupitia mgongo wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hakuna njia nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha 12 kilichoandikwa, tena kimeandikwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yaweza (may), mahali ambapo yule mkopeshaji anataka aone kwamba kuna mkataba wa kuhamisha zile pesa kwenda kwenye Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni matakwa ya lender yule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hali halisi uendeshaji wa Serikali na kutafuta mikopo duniani hauendi katika hili mnalotuambia hapa. Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaweza ikaenda mahali pa source ambayo haihitaji kupitia mlango wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano kama lender yule hahitaji masharti hayo, hakuna tatizo kabisa! Hakuna tatizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tusiwadanganye Watanzania kwamba eti mlango umefungwa, ni pale tu ambapo mkopeshaji yule anasema, hapana mimi nadhani wewe unapaswa upitie mlango wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ni masharti ya mkopaji kwa sababu yeye anasema wewe nataka uje na kofia ya sovereign state. Sasa mimi hata tungeliongea mpaka asubuhi misingi ya sheria za kimataifa ndiyo hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unapo on-lend (kufaulisha) lazima yale masharti ya mkopo, ule mkopo mama, lazima uyazingatie unaweza ukayapeleka yakawa juu zaidi, tumefanya kwa mashirika mengi ya umma hapa. Kile ambacho Serikali ya Jamhuri ya Muungano inakopa kutoka Benki ya Dunia, Benki ya Afrika au kokote kule, kwa sababu kuna gharama ya kutoa ule mkopo kwenda kwa yule. Lakini pia kama una uwezo unaweza ukatoa kwa masharti nafuu, maana yule wa nje yeye hajali, mkopo unapoiva lazima ulipwe in full.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha 27 cha Sheria ya Mikopo, Dhamana na Misaada kiko wazi. Lender yeyote wala hahitaji kujua kama ukopaji wenu umezingatia matakwa ya sheria ya Tanzania, na ndio uzuri wa sheria hii kwamba inawalinda wale waiamini Tanzania kwamba ukiikopesha Tanzania hata yule aliyetoa zile pesa uka-on-lend aki-default lakini bado unaikamata Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, huo ndio utaratibu. Kwahiyo, nadhani Mheshimiwa Tundu Lissu unanielewa ninachokisema iki-default ni nini anaye-default katika hali hiyo ime-default Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yetu ya ndani tuyaache ya ndani, katika hali hiyo inakuwaje, itakuwa ni mara ya kwanza hii? Mbona tunadaiana tu Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilikuwa inatudai nafahamu mimi na Serikali ya Jamhuri ya Muungano inaidai Zanzabar na mashirika mengine, wanadaiana ni masuala ya biashara mengine mengi hayo. Sasa ukiongelea TANESCO tunadaiana, TANESCO wanaidai bilioni 60 lakini yote haya Tanzania itaendelea kuwepo tu leo na kesho na kesho kutwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la msingi ni kuweka utaratibu ambao mhusika ataambiwa kwamba tulikubaliana haya na haya, wataketi kitako. Suala la misaada nakubaliana na Mheshimiwa Lissu lilikuwa na maneno neno sawa, lakini mimi siamini kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haina wasemaji wake. Msemaji wake mkuu ni Rais wa Zanzibar na washauri wake. Lakini mimi ushauri wangu kama mnasumbuka kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imewekwa kwenye sehemu ya parastal local government unaweza ukaiondoa tu ukaipatia kifungu cha peke yake. Lakini lengo likawa ni ku-on lend, misingi ni ile ile, tatizo liko wapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nisaidie kwenye maeneo machache ya kiuandishi. Ili tuende pamoja na Waheshimiwa Wabunge nitumie muswada kama ilivyokuwa published na Serikali tarehe 21 Oktoba, 2016. La kwanza nimemsikia AG wakitoa definition mpya ya mikopo inayotoka nje ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wametoa definition ambayo katika schedule of amendment mnaiona resident sources lakini nonresident sources haipewi definition. Pamoja na kwamba hii ni definition ya IMF lakini mimi napata shida kidogo kwa sababu mikopo, tunayoiongelea ni mikopo ya sovereign state, sovereigh borrowing. Sasa unaposema non-residents tutakapoenda kwenye ukurasa unaofuata maana yake ni nini? Mnatuchanganya kweli kweli. Mimi ningelipenda ile non-residents source na yenyewe ipewe definition, ili tukae vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafanya marekebisho kwa sheria iliyopo, na lazima tutumie terminology ambazo zimo na zimepewa definition au zimetumika throughout kwenye sheria ya sasa, sheria mama. Ukichukua schedule of amendment primary loan wanasema means any loan secured by the government.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa secured hatujawahi kulitumia katika sheria hii, tunatumia neno raise, you raise a loan. Nimeona maneno mengine utayaona contracted haya maneno hatujawahi kuyatumia katika sheria hii. Ni vyema tukawa na mtiririko ulio sahihi katika maeneo haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine, nimemsikiliza sana Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu alipokuwa anasoma hotuba yake nzuri, anasema neno stock or stocks vifutwe lakini maelezo sikuyapata vizuri, labda naweza nikasaidiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa wanasheria na wafanyabiashara, kwa ngazi za kimataifa, na kule tulikotoa sheria hii neno bonds ukienda kwa Waingereza traditionally maana yake ni stocks na ndiyo maana sheria hii ilikuwa inatumia yote na kwa vile sasa tunataka kwenda kukopa kwenye Soko la Fedha la Kimataifa mimi ninaomba sheria hii ichukue sura pia za nchi nyingine ambao tutaenda kwenye masoko yao ya fedha, nashauri tusiiondoe definition ya stock or stocks. Lakini kama mnaiondoa, sasa msiiondoe kwa utaratibu mliotumia wa short hand maana tutapata matatizo, ningependa wanasheria wa ofisi yako wakusaidie AG.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ukienda ukurasa wa 7, 8 na 15 unapokuta maneno hayo yalivyotumika ukifuta tu neno stock yanayobaki hayana maana. Kwa hiyo, kama mnataka kwenda kwa namna hiyo lazima muifuatilie sheria kila kifungu muone ilivyokaa na muionyooshe ikae vizuri, ndio ushauri wangu katika eneo hilo. Lakini ningekuwa mimi ningeomba sana tusi-disturb environment ya mikopo na hasa tu kule tunakoelekea sasa hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja ukurasa wa tano wa muswada. Nimeyaeleza yaliyoko kwenye tano pale, kama tungependa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar isionekane, or tuandike ka-paragraph kanakosimama peke yake; lakini inaongeza nini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashuka kidogo ya stocks nimeiongelea, nashuka tena kidogo foreign loan means any loan contracted; nimesema tutumie maneno raised throughout ambayo ndio maneno ambayo yako kwenye sheria ya mikopo. Tunashuka kidogo, kwenye 6(b), mimi hapa nakubaliana sana na Serikali kwa sababu concession loan zimepungua sana, mikopo ya masharti nafuu, na Mheshimiwa Waziri wa Fedha huwa anatukumbusha mara nyingi hapa Bungeni.
Sasa hivi dunia hii inaenda kwenye mikopo ya kibiashara zaidi, lazima tuyakubali haya; mimi nayakubali hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unaposhuka chini kwenye kile kifungu kipya cha 2 kinachopendekezwa hapo ndio sasa nimepata shida sana, pamoja na marekebisho ya Serikali yaliyoletwa. Kinasema foreign loan ambapo walipashwa waanze a foreign loan may be raised.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nina matatizo na hapo hayajakaa vizuri yatatuchanganya. Maana tunapaswa tuseme, moja, a foreign loan by direct borrowing, pili, non-resident, sasa na hapo nimeshtuka kidogo, non-residents tuna maana gani hapa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini unasema futa neno issue or issue ingiza maneno ambayo mnayaona katika ile schedule of amendments, inapoteza meaning mpaka uje tena uhangaike kuingiza issuance of bonds halafu ndipo uendelee. Ndiyo maana ikiandikwa vizuri inaweza ikatusaidia labda AG atatusaidia anapo-windup kumalizia kuhitimisha hoja yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, umeni-warn kuhusu muda wangu. Nimalizie la mwisho ni la msingi sana, ukurasa wa 6 clause ya 8(b) kwenye provisory wanasema uingize neno not naombeni sana mkisome kifungu hicho, is mirror image ya kifungu cha 3 cha sheria hii. Ukisoma vizuri ule mtiririko ningekuwa na muda wote mngeona, lakini AG na team yako mimi naona mtaliona hilo hakuna haja ya kuongeza neno not yanajitosheleza yalivyo sasa hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipatia nafasi. Nimalizie kwa kusema naunga mkono hoja hii mia kwa mia, lakini ninawaomba sana Waheshimiwa Wabunge, kazi yetu mojawapo ya kufanya ni kutunga sheria za nchi yetu, tuziboreshe pale tunapoona panahitaji maboresho na tunafanya vizuri, lakini tusiwe tunaendelea kulalamika katika Bunge lako haitasaidia Watanzania na Bunge lenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi niungane na Waheshimiwa Wabunge katika kuchangia hoja iliyo mbele yetu. Nianze kwa kusema naiunga mkono hoja hii asilimia mia moja lakini mniwie radhi kwa sauti yangu kidogo leo haijakaa vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili na mimi niseme, haya yanayoendelea pamoja na kwamba ni michezo ya kisiasa lakini isitukwaze. Sisi kwa mujibu wa Katiba, Sheria na Kanuni za Bunge, akidi ya maamuzi tunayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kama kuna kitu Mbunge amekereka kanuni zina utaratibu. Mimi nawasihi wenzangu hawa tutumie Kanuni zetu, huo ndiyo utaratibu wa Kibunge na siyo kwenda kufanya vikao kantini na maeneo mengine. Mimi siko nyuma yako, bali niko bega kwa bega na wewe. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, Deni la Taifa, nimesikiasikia hata kwenye hotuba ya wenzetu wanalisemea hili, ndiyo linakua lakini Tanzania ya leo siyo ile ya mwaka 1960, 1970, 1980. Taifa hili linakua na mahitaji yake yanazidi kuwa makubwa na lazima Serikali kupitia bajeti yake iweze kuwahudumia wananchi katika sura hii. Hoja siyo deni la nchi hii kukua, hoja ni kwamba tunapochukua mikopo hii iwe ni mkopo wa muda wa kati au muda mrefu tunazielekeza wapi?
Mheshimiwa Naibu Spika,tukizielekeza kwenye consumption ndiyo inakuwa tatizo, lakini tukizielekeza katika maeneo ya uzalishaji yanayotujengea uwezo ya uchumi wetu kukua kwa haraka deni letu litaendelea kuwa himilivu. Tulielewe hilo lakini kusema kwamba tunagawanya deni hilo kwa population haiendi hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa mkakati wetu wa kusimamia Deni la Taifa na Sheria yetu ya Mikopo, Dhamana na Misaada labda Waziri angeweza kutusaidia tu tukajua huwa tunafanya tathmini ya Deni la Taifa baada ya muda gani maana ni vizuri tukajua deni la kipindi cha muda wa kati au muda mrefu. Pia vile viashiria ambavyo vinatumika, maana ukichukua kwa mfano thamani ya sasa ya deni la Taifa uwiano wake na Pato la Taifa ni asilimia ngapi. Maana nadhani haya ndiyo yanapaswa sisi kama Wabunge Serikali iwe wazi ili kupunguza haya maneno. Unapolinganisha ukomo, ule ukomo ukisema ni asilimia 50 msingi wake ni nini au unaposema deni letu la Taifa kwa sasa thamani ni hii lakini ukilipima kwa mauzo yetu ya nje ya bidhaa zetu na huduma ni asilimia ngapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, haya ndiyo masuala ya msingi. Nadhani Waziri wa Fedha anapokuja kuhitimisha atusaidie katika kuyasema haya ili nchi na Wabunge tuweze kulipata hili suala vizuri. Naamini deni hili linahimilika na tutaendelea kuwa nalo na tutaendelea kukopa lakini tukope kwa misingi ambayo inajenga Taifa letu.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili amelisema kwa sura tofauti Mheshimiwa Janet Mbene, nataka niulize tu tumekuwa na hili zoezi la nchi yetu kufanyiwa tathmini ili iweze kukopesheka nje, ile sovereign rating imesemwa sana humu. Mara ya mwisho nakumbuka katika bajeti ya Serikali ya mwaka 2013/2014 Serikali ilisema wako advanced sana lakini sasa hivi hatusikii tena.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna faida zake kwenda route hiyo kwa sababu ndiyo unapata access kwa mikopo from masoko ya kimataifa ya masharti nafuu lakini pia na makampuni ya Kitanzania yanaweza pia na yenyewe kupata mitaji kutoka kwenye masoko ya Kimataifa. Sasa tungependa tuelezwe ni nini kimetukwamisha tena tunarudi nyuma.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ni hili la Public Private Partnership. Kusema kweli visingizio vimekuwa vingi. Naiomba Serikali ile miradi 125, maana mwanzoni tuliambiwa sheria haijakaa vizuri, ni kweli maana mtu anakuja hapa na pesa zake umuambie afuate Sheria ya Manunuzi kulikuwa na mgongano, tukasema tuunyooshe na Bunge likafanya kazi yake. Wakasema kuna centers nyingi sana za maamuzi na kadhalika tukanyoosha sheria. Wakasema sasa imeleta miradi 125 inafanyiwa uchambuzi ili kuona kama inakidhi kuingia katika mfumo huo mpaka leo hatuoni kinachoendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo huu unachochea uwekezaji lakini pia unapunguza mzigo wa Serikali kwenye bajeti ili tuelekeze nguvu katika maeneo ya afya na maji lakini barabara, miundombinu ya reli, bandari na kadhalika tunashirikiana na private sector kwa misingi tuliyojiwekea na hili mimi nasema linawezekana na linafanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la nne limesemwa ni Benki ya Kilimo, inatia huruma sana kwa ahadi ya Serikali ya muda mrefu kutotekelezeka na mimi nasema there is more than one way of skinning a cat. Benki ya Rasilimali ya Tanzania Serikali ilipoianzisha miaka 1970 na ile iliyokuwa Tanzania Rural Development Bank kabla ya kuwa CRDB, Serikali ilichukua line of credit kutoka AIDA, European Investment Bank na Nordic Investment Bank kuweza ku-capitalize hizi benki.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuwe wabunifu tukienda na lugha hii, kwanza Benki ya Maendeleo kwa Sheria ya Mabenki na Financial Institution unahitaji upate leseni minimum fifty billion, ten billion ndiyo fedha za kwenda kukopesha halafu tunasema ikopeshe kwa masharti nafuu maana yake ifanye hasara tangu day one haiwezekani.
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali kweli kwa hili tu-capitalize the bank na tuone namna ya kufanya. Hizi hati fungani za mtaji zinawezekana zikatumika kwa sababu ukinitolea ni kama I owe you money, interest utakuwa unanilipa ndani ya miezi sita na principal mwisho wa mwezi, angalau una-clean up balance sheet yangu na wengine wanaoniangalia kama benki niweze kukopesheka, ndiyo tunaiomba Serikali ilione kwa mtazamo huo.
I owe you money, interest utakuwa unanilipa ndani ya miezi sita na principle mwisho wa mwezi ili kama benki niweze kukopesheka, ndiyo maana tunaiomba Serikali ilione kwa namna hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho. Hii Mifuko ya Hifadhi kwa principle hiyo hiyo, najua Serikali ime-underwrite Mifuko hii hasa PSPF; lakini kwa vile tumechukua pesa na tumezitumia kwa maendeleo yetu, nadhani tuwe wakweli tu, tunapowasema tutatoa a non cash bond kweli tuitoe. Tukisema tutatoa bilioni 80 mwaka huu kwenye bajeti zionekane kuliko kuzidi kuididimiza Mifuko hii halafu wafanyakazi waliostaafu kama mimi unakuta hawalipwi kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama mimi nilikaa kwa kipindi cha miezi saba silipwi pensheni na, ni kweli eeh, lakini ndiyo haya mambo tunayosema, Serikali wasikasirike maana tumezitumia pesa hizi kwa nia njema, lakini tuje sasa na utaratibu utakaotusaidia kuyajibu hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kabisa, Waheshimiwa Wabunge Kanuni za Bunge zinawaruhusu wala tusionekane kuwa ni wanyonge; hii Sheria ya Manunuzi kama Serikali hawataileta sisi wenyewe; hata mimi mmoja wao kwa sababu najua kuandika hizi sheria, tutaleta amendment ya sheria humu! Eee! Hilo tusiogope maana fursa hizi zipo tunaweza kuyafanya haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, amelisema vizuri sana Mheshimiwa Ritha, kwenye Sheria ya Micro-finance. Mimi nilikuwa consulted kufanya kazi hiyo na tulifanya kazi kubwa na akina Dunstan Kitandula. Sasa kwa kuiheshimu Serikali tukasema kwa sababu wanalifanya tukasema hebu waanze tutakuja ku-takeover baadaye, lakini naona sasa again halisemwi tena. Sasa tutayafanya hayo Waheshimiwa Wabunge tukitaka na ndio moja ya kazi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja hii mia kwa mia.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. ANDREW J. CHENGE – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA SHERIA NDOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia fursa hii niweze kuhitimisha hoja yangu, hoja ya Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo. Niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yenu. Niwashukuru sana waliochangia kwa kuongea humu Bungeni, Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete, Mheshimiwa Mlinga na Mheshimiwa Aida Khenani. Pia kuna Waheshimiwa Wabunge wamechangia hoja hii kwa maandishi ambao ni Mheshimiwa Lucia Mlowe, Mheshimiwa Zuberi Kuchauka na Mheshimiwa Juma Othman Hija. Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongea kwa kifupi sana. Ukimuona nyani mzee porini ufahamu kwamba amekwepa mishale mingi sana. Kwa hiyo, ndugu zangu hii ndiyo hali ya maisha. (Makofi/Kicheko) Mheshimiwa Mwenyekiti, tumewasilisha hoja hii, Waheshimiwa Wabunge mtakapopata fursa isomeni, hoja ya msingi hapa ni kwamba Sheria Ndogo ni sheria halali za nchi hii na zinawagusa wananchi wetu katika maisha yao ya siku hadi siku. Mimi nashukuru sana uamuzi wa Mheshimiwa Spika kwamba Kamati hii iwe inapewa fursa ya kuwasilisha taarifa yake mapema kabla ya taarifa zote. Kwa sababu tusipofanya hivyo kama mnavyoona sasa hivi wananchi wataendelea kuumizwa tu kwa sheria ambazo zina dosari na ambazo zingeweza kurekebishwa. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wetu amesema ziko kodi, ada na tozo nyingi sana kwenye mazao hasa ya biashara, hilo ni agizo, tunategemea kwamba Wizara zenye sekta hizo watafanya haraka ndani ya uwezo wao kuzipitia zile sheria na kanuni, kama msingi wake uko kwenye sheria mama basi wafanye marekebisho kupitia sheria mama kuleta Muswada wa Marekebisho hapa Bungeni. Kama ni kwenye Sheria Ndogo ndiyo unachukua nafasi ya Kamati hii kuyaleta mapema ili tuweze kuyapitia tuyanyooshe twende mbele. Hivyohivyo kwa maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, maelekezo mazuri sana ameyatoa alipokuwa katika ziara Mikoa ya Kusini. Maana tukiacha hizi zitaendelea kutumika, ni sheria. Kwa hiyo, nimeona hilo niliseme kwa sababu linatuhusu sote. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Hija ameshauri tu kwamba labda Kamati ya Sheria Ndogo itusaidie hii migogoro ya wafugaji na wakulima, mtoe mchango wenu kwa hilo. Napenda sana hiyo lakini hali halisi sio hivyo. Kamati hii inafanya uchambuzi wa Sheria Ndogo ambazo zimewasilishwa hapa Bungeni na Serikali. Ombi langu kwenu kama viongozi, kwa sababu tatizo hili ni kubwa, tukianzia chini kwenye maeneo yetu katika kutunga au kupendekeza maoni yetu ya kutunga Sheria Ndogo ambazo zitasimamia matumizi bora ya ardhi, Sheria Ndogo hizo ndiyo zitaweza sasa kufanikisha hilo ambalo Mheshimiwa Juma Othman Hija anapendekeza lakini sisi hatuwezi kwenda tukafanya kazi ambayo siyo sehemu ya majukumu ya Kamati hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la elimu, kuwawezesha wanasheria, kwanza wanasheria kwenye Serikali za Mitaa au Halmashauri zetu tumelisema kwenye taarifa, hiyo ndiyo inachangia dosari nyingi ambazo zinaonekana katika Sheria Ndogo hizi. Hata hivyo, mimi najua uandishi wa sheria ni taaluma ya kipekee na ndiyo maana hata kwenye Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ni wachache na wale wazuri, hii siyo feature ya Tanzania tu, nenda kokote ndani ya Nchi za Jumuiya ya Madola tatizo hili lipo, kwa sababu hawa is a special breed, wanafunzwa namna ya kuandika. Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili uweze kufika ile grade tunayoitaka lazima uwe una uzoefu mpana sana wa sheria lakini pia na masuala ya kijamii sasa kuwapata hao itatuchukua muda. Hata hivyo, tukasema tunapendekeza angalau kwa wanasheria waliopo katika Halmashauri zetu wakinolewa kila baada ya muda kama walivyofanya juzi hapa Dodoma, wamefanya semina ya wanasheria wote hawa waliletwa hapa, ya siku tatu, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu imetoa inputs zake, wanasheria wa TAMISEMI wametoa inputs, ndivyo inavyotakiwa, labda itatusaidia sana katika kuimarisha uandishi wa sheria. Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema vizuri, jamani Ofisi ya Mpigachapa Mkuu wa Serikali, ofisi kwanza yenyewe ni hatari. Serikali imetoa ahadi na sisi tunaamini kabisa kwamba ahadi ni deni tunategemea tuone ndani ya muda mfupi ofisi hiyo inaboreshwa kiutendaji lakini kwa vifaa vya kisasa. Maana haya tunayoyasema ya kuwasilisha Sheria Ndogo kwa mujibu wa Kanuni ya 37(2) na kwa mujibu wa kifungu cha 38 cha Sheria ya Tafsiri yanategemea ofisi ya Mpigachapa Mkuu wa Serikali. Kama hajafanya utakuwa unaonea Serikali kwamba kwa nini hamjaleta mawasilisho yenu Bungeni, lakini acha tuone. Kuna mchango mzuri tu wa Mheshimiwa Kuchauka, yeye anasema hawa wananchi wanaokaa karibu na hifadhi ndiyo wanasaidia kutunza hifadhi hizi lakini tunapata mapato kiduchu asilimia 25. Sasa yeye anapendekeza waongezewe, hayo ni ya kwenu huko, sisi tunasimamia Sheria Ndogo kama itakuja na mapendekezo hayo na yamekubalika kule itakuwa ni uamuzi wenu. Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme moja, Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, Sura ya 290, kupitia Bunge la bajeti mwaka wa fedha 2011/2012 wote mliokuwa Bungeni mnakumbuka, yaliletwa marekebisho ya kuongeza cess ya mazao ili watoze kwa kuangalia hali halisi ya Halmashauri yako, kati ya asilimia tatu mpaka asilimia tano. Hata hivyo, ukweli wa mambo, hakuna Halmashauri nchini ambayo imetoza chini ya asilimia tano, zote zimepiga ile ceiling. Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wa Kamati, ingawa siyo la kwetu lakini tunayaona, tumemwambia na Waziri wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwamba kama malalamiko ni haya hebu tujitahidi basi tukaweka ifahamike. Maana sasa hivi mmewapa ile leeway wanapiga mpaka kwenye ceiling, ni afadhali ikafahamika kama ni asilimia tano iwe asilimia tano, kama ni mbili au tatu iwe tatu, tutakuwa tumeiweka sheria katika msingi mzuri. Mheshimiwa Mwenyekiti, nisingependa nipigiwe kengele ya pili, kazi hii tumeianza, tunaomba Kamati hii iendelee kuungwa mkono kwa kuwezeshwa. Hawa wajumbe wa Kamati hii kazi yao ni kusoma documents. Wenyewe pia ili waweze kuifanya kazi hii vizuri lazima wawezeshwe vizuri. Tofauti na baadhi ya wajumbe ambao ni wanasheria kama akina Mheshimiwa Ridhiwani, Mheshimiwa Ngeleja na wanasheria wengine lakini wengine hawa siyo wanasheria na siyo lazima uwe mwanasheria kuweza kuzifanya kazi hizi lakini ukisaidiwa ukawasikia wale ambao wamebobea katika masuala haya mtakuwa mmeisaidia sana Kamati hii. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, nisichukue muda wako mwingi, tuna mambo mengi sana leo, lakini niwashukuru Waheshimiwa Wabunge waliotuunga mkono. Nami nimalizie kwa kusema maoni na mapendekezo yote ambayo yamo kwenye taarifa ya Kamati sasa Bunge lako iyakubali kama Maazimio yaliyopitishwa na Bunge. Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii asubuhi hii ya leo ili nichangie hoja iliyoko mbele ya Bunge lako Tukufu. Nianze kwa kusema naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Profesa Mbarawa, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa wasilisho lake zuri. Naelewa nyuma ya wasilisho hilo ni kazi nzuri iliyofanywa na viongozi wa Wizara hiyo pamoja na taasisi ambazo zipo chini ya Wizara hiyo. Hongereni sana kwa kazi nzuri, tunawashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda, niungane tu na Waheshimiwa Wabunge waliotangulia kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa uamuzi wa hekima na busara lakini wa kijasiri sana kuhusiana na reli ya Kati. Uamuzi huu ni wa msingi sana katika kufungua fursa mbalimbali za maendeleo ya nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika,Naendelea kuiomba Serikali iendelee kuweka kipaumbele cha juu katika upatikanaji wa fedha za ujenzi wa reli hii kwa sababu wenzetu wa Northern Corridor wako mbali sana na shughuli hii. Kwa hiyo, nami naiomba sana Serikali twende nalo lakini naipongeza sana Serikali kwa hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze kwenye mambo ya nyumbani, politics is always local. Nianze kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tarehe 11- 12 Januari, alitembelea Mkoa wa Simiyu hususan Bariadi Makao Makuu ya Mkoa na Maswa. Akiwa Bariadi alifanya mambo makubwa sana na ndiyo maana wananchi wa Mkoa wa Simiyu tunaendelea kumshukuru sana. Moja, Mheshimiwa Rais alizindua barabara iliyokamilika ya kutoka Lamadi mpaka Bariadi yenye kilometa 71.8.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, akiwa pale pale alitoa tamko kuhusiana na ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Simiyu. Tatu, alimaliza ngebe kuhusiana na mradi mkubwa wa maji kutoka Ziwa Viktoria, matenki makubwa yakae wapi. Nne, alitoa maelekezo kuhusu gharama za ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa kwamba waziangalie kwa lengo za kuzipunguza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kwenda Maswa Mheshimiwa Rais alitoa maelekezo kwamba ujenzi wa barabara ya kutoka Bariadi kwenda Maswa kilometa 49.7 utangazwe; na kweli naona kwenye Bajeti hii Wizara imezingatia hilo. Tukiwa Maswa aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa barabara inayoendelea sasa hivi kutoka Mwigumbi kuja Maswa. Haya ni mambo makubwa sana katika kufungua Ukanda huu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Simiyu ni Mkoa mpya, Makao Makuu yake yako Bariadi. Tunahitaji tuunganishwe sisi na Mikoa jirani ya Singida na Arusha. Ndiyo maana Ilani ya Uchaguzi ya CCM inatamka, tufanye Upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara ya kutoka Bariadi kwenda Kisesa - Mwandoya - Mwanhuzi mpaka Sibiti. Njia tunayoona sisi ni kupitia Mkalama kuja Iguguno. Kwa hiyo, tungependa sana hili lionekane. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, mimi nimekuwa Mwanasheria Mkuu nikiwa Mbunge. Hii barabara ya kutoka Odeani - Mang’ola - Matala, Sibiti kwenda Mwanhuzi – Lalago – Mhunze – Kolandoto, imekuwa inaongelewa story, story, story. Kwa mwaka huu nakubaliana na Serikali kwa hayo waliyosema kwamba wamekamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Mwaka kesho kama ikiendelea hivi mimi nitasema, maneno waache sasa waweke muziki. Hii barabara tunataka ijengwe. Kusema kweli ukishakamilisha usanifu huo, inakuwa sehemu ya kutoka Bariadi mpaka Mwanhuzi kwa sababu sehemu nyingine umeshamaliza. Kwa hiyo, waache maneno, waweke muziki. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukishafungua ukanda huo na kwa mapendekezo mengine ambayo tumeweka, barabara za kufunguliwa Ukanda wa Mkoa wa Simiyu, tutafungua maeneo hayo kiuchumi na kijamii. Sasa nilihangaikia sana hii Sheria ya Barabara kuweka vigezo vya namna ya kupandisha madaraja barabara hizi, basi tupate angalau maamuzi kwa nchi mzima. Vigezo vipo kwenye sheria hiyo. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri waliangalie hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema ya nyumbani hayo, lakini nami kama Kiongozi wa Kitaifa niseme. Nchi hii ya Tanzania inafunguka kwa barabara. Angalia hizi barabara za kikanda, maeneo yote kuunganisha Tanzania na nchi jirani tumefanya vizuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi jirani sehemu ambayo naiona ni muhimu kwetu sana na nimeiona kwa mbali kwenye hotuba hii ni Kasulu – Kibondo – Manyovu na Burundi. Pia naiona kwa mbali Sumbawanga – Matai – Kisesya – Sanga Port ni muhimu sana. Naiona kwa mbali pia, Bagamoyo – Saadani – Tanga – Horohoro – Lungalunga – Mombasa – Nairobi – Isiyolo – Moyale – South Ethiopia. Haya ndiyo mawazo tumekuwa nayo, maana upande wa Uganda - Sudan ya Kusini Arua - kuja mpaka Kyaka tayari tunaendelea. Tukikamilisha kazi inayoendelea ya kutoka Nyakanazi – Kakonko – Kasulu mpaka Kigoma na tukashuka sasa kutoka Uvinza tukaelekea Mpanda - Stalike twende mpaka Kithi – Sumbawanga – Laela – Kikana – Tunduma unaiona nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nimesafiri, namwelewa rafiki yangu Mheshimiwa Zuberi aliyoyasema, lakini nimeona humu, kutoka Masasi tukijenga barabara Masasi pale Nachingwea unaenda Nanganga, halafu Nanganga unaweza kushuka hivi kwenda Ruangwa. Haya ndiyo tunataka kuyaona humu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesafiri juzi pia, sikuamini, nimetoka Masasi nikaelekea Mtambaswala, Mangaka kule nikatoka pale nikarudi kutoka Mangaka nikaelekea Tunduru, barabara safi. Tukatoka pale tumekwenda mpaka Tunduru mpaka Namtumbo, Songea. Safi! Songea unakwenda mpaka Mbinga, sasa tunabaki sehemu ya Mbinga kwenda Mbamba Bay. Jamani, mambo yanafanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ambayo naitaka sana na nimeona kwa mbali, tukifungua Ukanda wa Kusini kwa chakula, angalieni ukitoka Kidatu uje Ifakara, piga hilo Lupilo uende mpaka Malinyi - Londo unakuja Lumecha, Songea, unafungua yote. Ni ukanda tajiri sana. Tukiyafanya hayo tutakuwa tumeisaidia sana nchi hii. Naiona Tanzania ikifunguka. Kwa sababu ya muda, siwezi kuyasemea yanayoendelea Ukanda wa juu wa kwetu kule, lakini yamo kwenye taarifa hii. Naishukuru sana Serikali kwa kazi hii wanayoifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa reli ya kati, kwa sababu tunatafuta mzigo utakaoweza kulipa reli hii, nadhani tuje tuiangalie kutoka Isaka kwenda Keza – Kigali - Msongoti. Pia Kaliua – Mpanda – Karema, maana mzigo wa DRC kwa Ziwa Tanganyika tungependa sana tuubebe huo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sipendi kupigiwa kengele, Mheshimiwa Waziri akinisaidia; aah, nimalizie, sehemu moja ambayo nataka tuangalie pia, kutoka Mpemba pale kwenda Isongole upande wa Malawi tutakuwa tumekamilisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa hayo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii nami niweze kuchangia kwenye hoja hii. Nitamke naunga mkono hoja hii mia kwa mia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Naibu wake na timu yake kwa kuandaa hotuba nzuri, ina taarifa nyingi za manufaa kwa maendeleo ya nchi yetu. Mnyonge mnyongeni lakini haki tuwape. Hii Wizara inajitahidi sana Waheshimiwa, kwa nchi nzima tunaona sura hiyo lakini ni kwa saabu ya rasilimali fedha ambalo ndilo linalotusumbua wengi hapa, lakini tunawapongeza wanafanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Mkoa wa Simiyu, naendelea kuishukuru Serikali kupitia hotuba hii kwa mradi mkubwa ambao ni wa kihistoria kwa Mkoa wa Simiyu kutoka Ziwa Victoria ambao utahusisha Wilaya zote tano za mkoa huo. Lakini nitakuwa mchoyo sana wa fadhila nisipotambua kazi kubwa iliyofanywa na Rais mstaafu Mheshimiwa Dkt. Jakaya Kikwete, maana yeye tangu mwaka 2005 alipoingia madarakani ndio amehangaika sana na mradi huu kwa kutambua hali halisi ya ukame katika Mkoa wa Simiyu. Mimi naamini mbele ya safari mradi huu utakapokamilika hata katika awamu ya kwanza wamkumbuke angalau awepo katika uzinduzi wa mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nirudie tena kumshukuru sana Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli, juzi alipokuwa Bariadi aliusemea mradi huu kwa nguvu na akamaliza kabisa akakata mzizi wa fitna kuhusiana na mradi huu ambao ulikuwa umeanza kuoneshwa kuhusu wapi matenki ya maji yakae na alisema bila kumung’unya maneno mradi huu utatekelezwa na matenki ya maji yatakaa palepale kwenye Mlima wa Ngasamo, tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utekelezaji, mimi ningependa tu Waziri labda kesho anapohitimisha anithibitishie, kwa sababu mradi huu umesanifiwa kwa kutambua hali halisi ya mkoa huo, kwamba yatakuwepo mabomba makubwa mawili, bomba moja la maji ambayo hayakutiwa dawa (raw water) na bomba lingine ndiyo la maji safi ambayo ndiyo yatatumika kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lile la maji ambayo hayakusafishwa, hayakutiwa dawa ni kusaidia kurejesha hali ya uoto wa asili katika maeneo hayo lakini pia kwa mifugo; na ndiyo maana hoja kubwa ya mradi huu ilikuwa ni kuangalia hali nzima ya mkoa huo ili mifugo hii isiende maeneo mengine kwenda kuharibu mazingira. Kwa hiyo ningependa hiyo confirmation tuipate, kwamba bado dhana ni ile ile katika usanifu wa mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali, nimeona pesa ambazo zimetengwa kwa Mji wa Bariadi ambao ni makao makuu ya Mkoa wa Simiyu. Mahitaji ya maji ni makubwa, idadi ya watu inazidi kuongezeka Bariadi na viunga vyake, tunahitaji hizo pampu tano kwa sababu visima vile vitano vimechimbwa mwaka juzi na viko pale. Sasa tungependa tupate umeme, ziunganishwe, tuongeze uzalishaji wa maji na tusambaze kwa matumizi ya wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye Jedwali Namba 5A, pesa ambayo imetengwa kwa kutekeleza miradi ya maji vijijini. Nina vijiji vitatu ambavyo tumepata maji tangu mwaka 2012; vijiji hivyo ni Igegu, Masewa na Sengerema katika kata ya Dutwa, kata ya Sapiwi na kata ya Masewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wananchi hawa wanajua kuna maji, wanafahamu, waliyaona wakati wanachimba visima hivi, ningependa sasa zile pesa ambazo nimeziona angalau zikatumika katika kusambaza mabomba ili maji yatoke chini yawafikie wananchi hawa kwa matumizi ya maendeleo yao. Naendelea kushukuru Serikali, nimepata maji ya msaada wa Serikali ya Misri, kisima kirefu pale Kololo lakini nazidi kuomba tena kwa Ngulyati, Mhango na Kasoli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu skimu ya umwagiliaji, nimeona ya Mwasubuya, lakini tuna eneo kubwa ambalo tunaamini Kasoli tukiweza kujenga bwawa kubwa tukafanya shughuli ya umwagiliaji sehemu kubwa ya eneo la Simiyu tutaweza kujitosheleza kabisa kwa mahitaji yetu ya chakula, kwa hiyo, naiomba Serikali ione hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije sasa mwisho, kwamba niliposema mnyonge mnyongeni. Waheshimiwa Wabunge na mimi nakubaliana na walionitangulia kwa kusema kwamba tutafute njia nzuri ya kuishauri Serikali ituongezee pesa katika Wizara hii na njia nzuri ni hii ambayo kesho Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha hoja hii, tujaribu kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, naona nia njema ya Serikali, lakini tukifuata Kanuni zetu suala hili likarejeshwa kwenye Kamati ya Bajeti tuweze kufanya uchambuzi wa kina, njia ambayo naiona ya haraka ambayo hata kwenye ukurasa wa 13 wa hotuba hii mnaona, iliyonyanyua bajeti hii ni tozo ya shilingi 50. Asilimia 52.7 ya pesa ambazo zimefika zimetokana na tozo hii. Sasa hivi kwa wastani tunaingiza lita bilioni 1.8 za dizeli na lita bilioni 1.2 za petroli. Tukiangalia kwa suara hiyo uwezekano wa kupata fedha tukaongeza kwa asilimia 100 tena yaani shilingi 50 na tukipiga mahesabu tunaweza tukaongeza shilingi 100. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unafahamu maendeleo lazima tuyatolee jasho na ninawaomba sana Waheshimiwa Wabunge safari hii hii lugha ya kusema kwamba tutaongeza mfumuko wa bei, tulikatae kwa sababu sio hoja ya msingi. Hii inawezekana tukayafanya haya, mahitaji ya maji kwa watu wetu ni makubwa na tunaona, sasa tukiendelea namna hii hatutafika kokote, mimi ndiyo ushauri wangu na inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii. Nianze kwa kumpongeza sana mtoa hoja Mheshimiwa Profesa Mbarawa kwa hoja yake nzuri ambayo inatoa matumaini kwa Watanzania katika sekta zote tatu muhimu ambazo anaziongoza. Niwapongeze pia Naibu Mawaziri na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi kubwa wanayoifanya. Tanzania inafunguka na inaunganishwa, sote tunaona, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitasema kwa kifupi katika maeneo ambayo nadhani ni muhimu. Moja ambalo nadhani tusaidiane Waheshimiwa Wabunge ni hili la TANROADS na TARURA kwa upande wa financing. Nimesikia mawazo mazuri tu ya Waheshimiwa Wabunge kuhusiana na kuongeza nguvu ya financing lakini kwa kupendekeza kwamba asilimia 70 ambayo ndiyo inakwenda TANROADS na 30 inakwenda TARURA tufanye uwiano mzuri, ni wazo zuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kusema, ukiangalia mtandao wa barabara zetu hizi za lami ambazo tunajenga kwa gharama kubwa, barabara kuu na za mikoa, sehemu kubwa ni kama asilimia tunayoweza kugharamia kwa matengenezo/matunzo ya kila mwaka haifiki asilimia
60. Sehemu kubwa ya barabara hizi hazitunzwi, sasa ukipunguza tena ukasema upeleke TARURA ujue network kubwa ya nchi hii ambayo tumeijenga kwa gharama kubwa itaharibika haraka sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tuendelee kuishauri vizuri Serikali, tutafute vyanzo vipya vya mapato badala ya kwenda na approach hii. Najua zoezi hili limekuwa linafanyika, tufike mahali basi tuone hii road users’ fee or charges, mapendekezo yaliyokuwa yanafanyiwa kazi tumefika nayo wapi? Mimi naliona hilo ni bora kuliko hii ya kusema tukagawane mbao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanzia mimi nachokoza tena, hii source ya shilingi ya mafuta nasema kwa sasa tujaribu kuiangalia tena. Maana yake nasema tuangalie kuongeza katika bajeti ya Serikali mwaka huu ili tukatunishe TARURA kwa kuanzia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza juhudi za Serikali kwa kazi inayofanyika Simiyu sasa hivi. Barabara ya Lamadi – Bariadi imekamilika, Mwigumbi – Maswa imekamilika, sehemu ya Bariadi – Maswa mkandarasi yuko site na bajeti tunaiona, shilingi bilioni kumi hizo zimetengwa na Serikali kwa mwaka ujao wa fedha. Matarajio yangu ni kwamba hata hicho kidogo kitapatikana ili mkandarasi afanye kazi na tuone kazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Mto Sibiti, daraja hilo linalotuunganisha sisi kwenye barabara ya kutoka Bariadi - Singida - Arusha linaendelea vizuri, tunaipongeza Serikali. Tunataka tuone barabara unganishi kwa pande zote mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe radhi sana Mheshimiwa Waziri, jana wakati na-chair Kikao nilisoma kwa harakaharaka nikamwandikia ki-note kwa sababu nilikuwa sijaisoma vizuri hotuba yake, ilikuwa ni barabara ya zaidi ya miaka 30. Tunaongelea barabara ya kutoka Kolandoto – Lalago – Mwanhuzi – Matala – Mang’ola – Oldeani Junction, kila Waziri aliyepita pale Wizarani barabara hii ipo. Najua pesa ndiyo hivyo, ombi langu kwa sababu imo kwenye mpangokazi wa TANROADS, tufike basi mahali vipande ambavyo vimekamilika tuanze kuvitengeneza kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye ukurasa wa 32, baada ya kumwomba samahani Mheshimiwa Waziri kwa mkanganyiko wangu wa jana, barabara ya Karatu – Mbulu – Haydom - Mto Sibiti - Lalago – Maswa, mimi sina problem kwa sababu nataka tufungue nchi hii lakini unapoiangalia pale sehemu kubwa ya barabara hiyo kuanzia Kolandoto – Munze – Lalago – Mwanhuzi - Sibiti - Mang’ola - Oldeani Junction tumeshafanya upembuzi yakinifu na detailed design, sasa wanapoichanganya hivi wanatuchanganya, si kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama KfW wanatoa hizi pesa tunawapongeza na tunawashukuru, lakini sehemu kubwa imeshafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Waheshimiwa napenda waje wanisaidie kwa maelezo yanayotosheleza kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda tusaidiane kuelewa. Hii barabara inayopendekezwa ya kutoka Karatu – Endebash, ninavyoifahamu ni kansa, unashuka nayo unakuja mpaka Kilimapunda pale, unashuka nayo Mbulu unakwenda Dongobesh unakwenda Haydom. Sasa napenda tusaidiane, ikitoka Haydom inaelekea wapi, inaenda Matala au Kidarafa? Napenda tuelewane maana hatuwezi kuwa tunafichana njia hii inapita wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na wazo la Serikali kwamba ikitoka pale tunarudi sasa Sibiti tunapandisha kwenda Mwanhuzi anayetaka kwenda Shinyanga anakata mpaka Lalago lakini ukifika pale Lalago unapandisha kwenda Maswa. Ndiyo utamu wa mapendekezo haya. Nadhani ma-engineer wote hebu waliangalie hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadaye tungependa tuone barabara inayounganisha upande wa Singida, barabara ya kutoka Sibiti maana chemchemi unaiona pale, unashuka kuja Mkalama, si ndiyo hivyo, halafu unakuja Gamanga, Ilemo huku au unaweza ukaja moja kwa moja mpaka Iguguno, tusaidiwe kuelewa barabara unganishi ni ipi? Nataka tu wanisaidie lakini nataka maendeleo ya haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hizi tunazijenga kwa gharama kubwa. Nisingependa tugombanie fito, lakini angalau kama hii ya Kolandoto nairudia sana, tuwe na muono wa pamoja hasa katika maeneo ambayo hayana connectivity nzuri kama Mkoa mpya wa Simiyu. Nadhani Mheshimiwa Profesa Mbarawa atanielewa kwa nini nalisema kwa uchungu namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, napongeza sana upande wa reli, napongeza sana reli ya kisasa kiwango cha kimataifa. Ombi langu kwa Serikali na nalisema kwa kujivuna, twendeni tukakope tushambulie maeneo yote kwa pamoja tusiende kwa spidi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, natoa hongera for a good and comprehensive speech. Nina issue mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mara ya kwanza katika historia ya Wizara hii, barabara ya Kolandoto – Lalago – Mwanhuzi – Mataka - Mang’ola - Old Junction haikutajwa katika body ya hotuba ya Mheshimiwa Waziri, imefichwa kwenye kiambatisho Na. 3. Nilitegemea vipande vya barabara hiyo ambavyo FS/DD ulikamilika zamani (Kolandoto hadi Mwanhuzi na Sibiti) vingeanza kutengewa fedha kwa ajili ya ujenzi. Ikumbukwe kuwa barabara hii imekuwepo kwenye mipango ya Serikali tangu mwanzoni mwa miaka ya 1990.

Mheshimiwa Naibu Spika, Makao Makuu ya Mkoa wa Simiyu - Bariadi haujaunganishwa kwa barabara ya lami kati yake na Mkoa wa Singida na Arusha. Sehemu ya kutoka Kolandoto – Mwanhuzi - Sibiti) FS/DD umekamilika. Ni vema sasa FS/DD ikaanza katika ya Ng’oboka –Mwandoya – Kisesa - Bariadi. Sehemu ya kipande hiki kipo katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2015 - 2020. Naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, Naibu Waziri wake Mheshimiwa Dkt. Mwanjelwa na timu ya Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe unafahamu kama tuna Wizara ambayo ina idadi kubwa ya wasomi ni Wizara ya Kilimo. Waheshimiwa Wabunge huo ndiyo ukweli, hizi changamoto naziona na mmezisema vizuri sana, upande wa bajeti mmeisema vizuri sana, sasa sisi ni Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nadhani badala ya kwenda kwa anachopendekeza Mheshimiwa Bashe, tuangalie kanuni zetu. Kanuni ya 105 inatoa fursa zile siku za mwisho baada ya mjadala wa Wizara zote Serikali na Kamati ya Bajeti wafanye majadiliano eneo hili la kilimo liwe miongoni mwa maeneo ambayo tunadhani yaangaliwe. Nadhani tukienda hivyo, tutakuwa tunaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, mmesema vizuri maana tunaiona development budget ya Wizara hii inaenda chini lakini hotuba ya Waziri ina maeneo mengi mazuri sana, sina muda wa kuyasema lakini eneo la umwagiliaji, nchi hii kwenye mabonde lakini tukienda kwa sera yetu na mikakati yetu angalau tuelekee katika kupata hekta milioni moja ambazo tumejiwekea, sasa hii imekuwa ni ngonjera tu. There is a big disconect kati ya Wizara ya Fedha, Wizara ya Umwagiliaji na Wizara ya Kilimo katika mikakati yetu lakini tukienda kwa pamoja tutafanya vizuri. Kuna maeneo mengi ya nchi hii ambayo ni kukinga maji tu ya mvua haya Mwenyezi Mungu anatupa, kuyakinga na kuyatumia kwa shughuli za umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda niongelee kuhusu pamba. Mimi nimekulia kwenye zao hili la pamba na Victoria Federation ilikuwa inafahamika, Afrika nzima walikuwa wanakuja kujifunza Tanzania. Sitaki kurudi kwenye historia, tulivuruga sisi wenyewe lakini nasema hivi mimi kama kiongozi wa Bariadi sitakubali utaratibu unaopendekezwa na Serikali wa kulazimisha ushirika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamba kwetu ni siasa kali, pamba ni uchumi, pamba ni hali yetu ya maisha. Ushirika ni kitu kizuri sana ndiyo nimeanza nalo, tulikuwanao, tulipambana na Wahindi na Waganda ndiyo tukaanzisha shughuli zetu, lakini haikuwa suala tu la kulima na kuuza pamba, uchambuzi wa pamba, zile ginneries zote zilikuwa za wakulima. Sasa huwezi ukanidanganya mimi pamba nikuletee eti kutoka kwenye AMCOS halafu iende kwa mtu private, ulishasikia ni ushirika huo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja lakini siyo kwa hoja hiyo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Naibu wake, Katibu Mkuu, Naibu Makatibu Wakuu na Watendaji wote wa Wizara hii pamoja na wataalam wa taasisi ambazo ziko chini ya Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba hii ni pana, ni nzuri na inatoa mwelekeo. Sote tumekubaliana kwamba Wizara hii ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji ni mojawapo ya sekta za kipaumbele katika Mpango wetu wa Maendeleo katika kuipeleka nchi yetu kufikia uchumi wa kati na nguzo kubwa ni viwanda. Tunaliona hili, wamelisemea vizuri, changamoto zilizopo na jinsi wanavyokabiliana nazo, nawapongeza sana, endeleeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado nasumbuliwa sana na suala zima la gharama za uwekezaji nchini, bado ziko juu sana. Hili limesemwa vizuri tu kwenye hotuba unaona hali ya upatikanaji wa umeme, maji na miundombinu mingine yote ya kiuchumi ambayo inaendana na kufanikisha uwekezaji gharama gharama ziko juu. Sasa, kuanzia leo mniite Bwana Reli, kwa sababu nitakuwa naizungumzia katika kila Wizara hata kama haihusiki nayo. Nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa uamuzi wake huo na tutakapokamilisha reli hii tutaona uchumi wa Tanzania utaibuka kama uyoga, ikumbukeni tarehe ya leo, Bwana Reli anasema. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Serikali, narudia kama nilivyosema juzi wakati nachangia kwenye Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Pamoja na jitihada nzuri za sasa, napenda Serikali iendelee kutafuta mikopo ya masharti nafuu ili tuweze kushambulia ujenzi wa reli hii tuikamilishe. Hii ni kwa maana ya reli ya kati pamoja na matawi yake yote ya msingi, tufanye kazi hiyo na tutaona uchumi wa nchi utakavyokua kwa kasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishuke kwenye upande wa mradi huu wa siku nyingi sana wa Liganga kwa chuma na Mchuchuma kwa upande wa makaa ya mawe. Kusema ukweli kwa nchi hii kama mpaka leo tunaendelea kuongea kwa lugha hiyo ni tatizo. Hata kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri nadhani ukurasa wa 13, hiyo Kamati ya wataalam, kinachosemwa pale ni kwamba timu hiyo imekamilisha taarifa ya awali wala hatuambiwi ni nini. Maana Waheshimiwa Wabunge, hizi sheria mbili tulizopitisha mwaka jana, mimi nasema Bunge lipo, kama kuna vifungu ambavyo tunaamini kwamba vinakwamisha kwenda mbele, Serikali ndiyo ileile iliyoleta Miswada hiyo Bungeni sasa Serikali hiyohiyo haiwezi ikaogopa kurejea Bungeni na kueleza kwa nini hatuendi mbele. Bunge lipo ndiyo kazi hiyo, watajenga hoja, tutawasikiliza na tutafanya marekebisho twende mbele. Haiwezekani tunaenda mbele tunarudi. Tangu mwaka 2011 Septemba waliposaini mkataba, NDC pamoja na ile kampuni ya China, what is wrong with us Tanzanians? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani tuna vivutio lakini hatuendi mble, jenga hoja, unamwambia mwekezaji bwana, haya hatuyakubali, mwambie ili afunge virago aende lakini hatuwezi kila mwaka tunaenda mbele na kurudi nyuma. Mimi nasema tuufikishe mradi huu mwisho. Mheshimiwa Waziri, tueleze exactly changamoto ni nini kwa sababu navyokumbuka mimi mkataba ule unatoa 20% ya free carried interest kwa Serikali bila kulipa kwa sababu madini hayo ni National patrimony yetu. Pia inaiwezesha Serikali kupitia NDC kupata an additional 49%. Tuliweka wazi kabisa kwamba mikopo yote ya uwekezaji itakayochukuliwa ambayo wana-estimate kuwa three billion US dollars, ni lazima ikubalike na pande zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi huwa nasema tufike mahali mradi huu utekelezwe. Tulikuwa tumepanga by now, mwaka huu wa fedha, kwa upande wa umeme tungekuwa tumefikia hizo megawatt 600 na chuma kingekuwa kimeanza kuzalishwa mwaka 2015. Kwa hiyo, reli hii tungekuwa tunaanza kutumia vyuma vyetu lakini what is wrong with us? Tusimuangushe Rais Magufuli kwa nia yake njema ya kuleta maendeleo ya haraka kwa nchi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma ukurasa wa 69 wa hotuba kuhusu hili suala la tozo na ada zenye kero zinazojirudiarudia, tumelisema, bado tunaelezwa ooh, tunakaribia kumaliza. Mheshimiwa Waziri nadhani unapohitimisha, hebu mtueleze exactly, najua kuna vested interest za Mawaziri, wanataka kuendelea taasisi ambazo ziko chini ya Wizara zao, wanategemea sana mapato yanayotokana na tozo na ada hizi lakini sisi tunataka kujenga mazingira mazuri ya kuwekeza na kufanyia biashara Tanzania. Kama tozo basi ziwe na mtiririko mmoja, tunasema One Stop Centre. Tumeona Benjamin Mkapa wameweka wote pale, tungependa hata Export Processing Zones za maeneo ya mikoani utaratibu huohuo utumike maana humkwazi mwekezaji. Nadhani tuyafanyie kazi haraka haya maana tumeyasema sana mpaka unafika mahali unachoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa jambo la jumla tu. Kusema kweli tunafanya kazi nzuri, amelisema vizuri sana Mheshimiwa Dkt. Mary Nagu na nilimsikiliza Mheshimiwa Rais kwenye National Business Council siku ile lakini hayo ambayo yameamuliwa pale napenda visiwe vikao hivi ambavyo havina record, havina yatokanayo ili kikao kinachokuja haya mengi haya yawe yameshatanzuliwa, siyo tena wanakumbushana kulikuwa na kikwazo gani, tumalize tunaenda mbele. Mheshimiwa Waziri, wewe ndiyo sekta yako hii, hayo ambayo unadhani yanakukwamisha lazima uwe mwepesi kuyasema na ndiyo maana taasisi ambazo ziko chini ya Wizara hiyo zina wataalam wengi tu. Angalia hayo ambayo wameyafanya, nadhani tukifanya kwa haraka tutayafanikisha lakini sio ya watu wazima tunaongea kila mwaka yale yale hatuendi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, nimeona project za kielelezo ni hii reli yetu ya kutoka Tanga – Arusha - Engaruka. Sasa najiuliza, nimesoma speech ya Waziri wa Ujenzi juzi, ninyi mnachotuambia ni nini hapa maana inaonekana hamuongei pamoja. Mnachosema kwenda kutekeleza, mtatekeleza nini maana kule kwenye ujenzi hatukuona chochote ambacho kinaongelewa kuhusu ujenzi wa reli mpya ya kutoka Arusha - Lake Natron na mwaka kesho mtakuja na lugha hizi hizi, kwa hiyo tunabaki hapo hapo. Let’s walk the talk tumalize, yale ambayo hatuwezi kuyafanya tuseme haya hatuwezi kuyafanya sekta binafsi itakuja tu kama tutaijengea mazingira wezeshi na rafiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, nikupongeze sana Waziri na timu yako, endeleeni. Mazingira ndiyo hayo lakini tusibebe mambo mengi kwa wakati mmoja. Tuchukue vipaumbele vichache tuweze kuvisimamia ili twende mbele. Ahsanteni sana, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Kumi na Kumi na Moja wa Bunge
MHE. ANDREW J. CHENGE – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA SHERIA NDOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi niweze kuhitimisha hoja yangu iliyo mbele ya Bunge lako. Nitajitahidi niongee kwa kifupi sana kwa sababu ya muda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kumi waliopata nafasi ya kuchangia kwa kuongea humu Bungeni na Waheshimiwa Wabunge wawili waliochangia kwa maandishi, niwashukuru sana. Mmeielewa hoja na mmeeleza vizuri changamoto ambazo zipo katika shughuli za sheria ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na moja la jumla, Waheshimiwa Wabunge ndiyo maana Serikali inapoleta miswada tujitahidi sana tunapoiunga mkono Serikali, maana shughuli za Serikali lazima ziende, lakini tuwe makini sana wanapowaambia kwamba masuala haya tutakwenda kuyaweka kwenye regulations.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli muswada hauwezi ukafafanua kila aspect lakini ile misingi na mipaka ya utekelezaji wake unataka uione, iwe katika sheria mama na mkifanya hivyo usimamizi wenu kama Bunge, oversight, control, supervision ya sheria ndogo utakuwa na maana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona zipo kanuni, sheria ndogo ukiziona unajiuliza hivi…, lakini kwa sababu ni sheria za nchi zinatumika, lakini tukianza vizuri kuwa makini na kile ambacho tunakikasimu then tutakuwa on a good footage. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, limesemewa vizuri sana, kwa nini hizi sheria ndogo zisianze kutumika mpaka hapo utaratibu fulani unapofanyika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu hivi, katika nchi za Madola, tuna mifumo ya aina mbili ya kusimamia madaraka ambayo Bunge limekasimu kwa vyombo vingine. Mfumo wa kwanza unaitwa affirmative resolution procedure yaani unaleta hizo rasimu zako za sheria ndogo unaziweka mezani kabla hazijaanza kutumika na Wabunge ndiyo wanapata nafasi ya kuona kinacholetwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hatua hiyo wanaweza wakasema no, kanuni hizi na hizi au kanuni hii hapana, kwa hiyo, wanakwenda kuirekebisha huko halafu ndiyo inakwenda kuchapishwa kwenye Gazeti la Serikali ianze kutumika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna utaratibu wa pili ambao unaitwa negative resolution procedure ambao sisi Tanzania ndiyo tunaangukia humo, kwamba ukiisoma Sheria yetu ya Tafsiri ya Sheria, na ndiyo maana taarifa ya Kamati inasema udhibiti wa Bunge siyo wa moja kwa moja, unasubiri kwanza ichapishwe kwenye Gazeti la Serikali ili iwe sheria ndogo halafu iwasilishwe Bungeni. Lakini ikishachapishwa imeshaanza kutumika, ndiyo tofauti ile ya affirmative na hii ya negative. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mmelisema vizuri Waheshimiwa Wabunge Mheshimiwa Rashid Abdallah, Mheshimiwa Hawa Ghasia, Mheshimiwa Zainab na wengine Mheshimiwa Kingu na Mheshimiwa Aida, kila mmoja karibu amegusia Mheshimiwa Ridhiwani wameyagusia, mimi nasema yote haya jamani yanazungumzika, hizi ni sheria zilitungwa na Bunge hili. Tukiona kwamba utaratibu wa negative resolution procedure haujakaa vizuri tunajenga hoja, tunashauriana na Serikali tukielewana tunafanya marekebisho, tu-adopt the negative ni nanii affirmative relation procedure. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naelewa Mheshimiwa Mdee amelisema vizuri sana Bunge letu halikai kila siku. Lakini unaweza kwa sababu tunajua lini mikutano yetu ya Bunge inapaswa kufanyika. Mnaweza mkajipanga na sheria ikasema wazi except kwa aina fulani ya sheria ndogo za dharura zile maana dharura ni dharura hauwezi ukasema isubiri sijui nini. Unaweka utaratibu ambao unawezesha Bunge kupitia Kamati husika kuweza kuyaangalia haya, mimi nadhani tutakapokuja kuelewana kwa hivyo tutaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana mlioiona maana hizi ni sheria wala usiseme Sheria Ndogo kwa sababu ni subsidiary, lakini zitatumika na wanachi na zingine is very hash ikikosewa tu kidogo unamuumiza mtu; na hapa nichukue nafasi kumshukuru sana Mheshimiwa kwa kuona busara aliyoiona kwamba turejeshe utaratibu huu na Taarifa za Kamati ziwe zinawasilishwa mara mbili kwa mwaka maana ni sheria zinatumika, tusiruhusu wananchi wanaendelea na vyombo vingine wanaendelea kuumia kwa sababu tu sheria hazijapitiwa na Bunge kupitia Kamati husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge kundi la sheria ndogo limetajwa kwenye Sheria ya Tafsiri subsidiary legislation means any order, proclamation, rule of court, regulation, notice, by law or instrument made, narudia made under any act or other lawful authority. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, huo ndiyo msingi ni vema tunapoyaangalia haya tuzingatie, sheria ndogo haiwezi ikavika ukuu ambayo haina katika sheria mama. Hiyo misngi ya kutunga sheria na tafsiri haiwezi ikajibika ukuu ambao haina katika sheria mama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa vile Serikali ipo najua nilivyosema kwenye taarifa tunafanya kazi karibu sana na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Mheshimiwa Jenista Mhagama kama coordinator wa shughuli za Serikali na Chief Whip wa Serikali Bungeni katika shughuli hizi na hili la BASATA niseme namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Dkt. Mwakyembe kwa sababu alipofika kwenye Kamati aliliona na akasema kiungwana tu jamani nipeni muda na mtu muungwana akimwambia hivyo lazima na wewe uoneshe uungwana, ndio maana tukasema sisi tutasema tu kwamba ilipaswa ije lakini kwa sababu haijakaa vizuri tumekubaliana itakuja katika Mkutano mwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kwa sababu lazima sasa baadae Bunge litaamua nisome sasa maazimio haya ili Bunge litakapohojiwa lijue linaamua nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya kwanza inahusu dosari ya uandishi wa majedwali ikilinganishwa na vifungu vya sheria.

KWA KUWA katika uchambuzi wa Kamati imebainika kuwa baadhi ya sheria ndogo zinadosari mbalimbali katika majedwari kuhusu vifungu vinavyoanzisha majedwali husika.

NA KWA KUWA kwa mujibu wa kifungu cha 25(2) cha Sheria ya Tafsiri ya Sheria kinabainisha kwamba majedwali ni sehemu ya sheria;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba Wizara ambazo sheria ndogo zake zimebainika kuwa na dosari katika majedwali zifanyanyiwe marekebisho ili kuondoa dosari hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, azimio la pili linahusu kukinzana na masharti ya sheria mama au sheria nyingine za nchi.

KWA KUWA baadhi ya sheria ndogo zilizofanyiwa uchambuzi na Kamati zimebainika kuwa na vifungu vinavyokinzana na masharti ya sheria mama au sheria nyingine za nchi.

NA KWA KUWA kukinzana huko ni kwenda kinyume na masharti ya kifungu cha 36 cha Sheria ya Tafsiri ya Sheria kinachotoa sharti kuwa sheria ndogo kutokwenda kinyume na masharti ya sheria mama.

NA KWA KUWA kukinzana huko kuna ifanya kanuni husika kuwa ni batili kwa kiwango kilichokinzana.

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba Wizara zinazohusika kufanya marekebisho katika sheria ndogo hizo ili kuondoa vifungu vinavyokwenda kinyume na masharti ya sheria mama au sheria nyingine za nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii. Nianze kwa kusema naunga mkono hoja zote mbili. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na timu yake kwa kazi nzuri ambayo wameendelea kuifanya. Tunaelewa changamoto mlizonazo na kwa hali yetu hii tunaelewa lakini nasema hongereni sana kwa haya ambayo mnayafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia huko tulikotoka miaka 20 iliyopita maboresho ambayo yamefanywa consistently na Serikali hasa kuanzia Awamu ya Tatu, Awamu ya Nne na yanayoendelea sasa ndiyo yamewezesha kuona mafanikio tunayoyaona sasa hivi. Jitihada za Serikali za kuhakikisha kwamba tunakuwa na uchumi wa jumla ulio tulivu, tunajenga mazingira mazuri ya uwekezaji na kufanya biashara, tunaendelea kuwekeza kwenye miundombinu ya barabara, umeme, maji, yote haya ndiyo yanawezesha mafanikio haya tunayoyaona. Mheshimiwa Waziri na timu yenu naendelea kuwapongeza sana pamoja na changamoto za rasilimali fedha ambazo tunazo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi hii mikubwa ambayo Mheshimiwa Rais wetu ameanza kuitekeleza, pamoja na maneno mengi, hii ndiyo itakayochochea zaidi maendeleo yetu. Ujenzi wa reli ya kati kwa standard gauge na matawi yake muhimu, maboresho yanayoendelea sasa hivi katika bandari ya Dar es Salaam, niongeze hapo, siyo maboresho tu na upanuzi wa bandari ya Dar es Salaam lakini napenda tuanze ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo kwa sababu tunafahamu Bandari ya Dar es Salaam tayari imekuwa chocked. Tujenge bandari mpya ya Bagamoyo ambayo itakuwa ni kwa faida kubwa ya Taifa hili kwa miaka 100 inayokuja ili tuweze kushindana na tujenge mazingira ambayo yatatuwezesha kutumia nafasi yetu ya kijiografia kama vizuri kama nchi, tunaweza, tunaweza. Ndiyo maana Mwalimu alikuwa anatukumbusha wakati wenzetu wanatembea sisi tukimbie. Ndiyo maana ya kufanya uwekezaji mkubwa kama huu, ndio una gharama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, narudia, ni vema tukachukua uamuzi haraka, tukapata a financing instrument itakayotuwezesha ku-fund reli ya kati na matawi yake tumalize mapema kuliko hii ya kwenda vipande vipande na tutaona jinsi uchumi utakavyokua kwa haraka. Hili linawezekana, ni ombi langu sana kwa Serikali, twende haraka na baadaye mtaona faida kwa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha tulilisema miaka minne iliyopita mamlaka ya nchi haiwezi ikajiondolea sovereignty yake. Nashukuru mmerejesha mamlaka ya Waziri wa Fedha ya kuweza kusamehe pale inapobidi miradi mikubwa kwa faida ya maendelao yetu, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu, kwa miradi ambayo tayari iko kwenye pipeline maamuzi yafanyike haraka, twende mbele. Baada ya Bunge kama litakubali marekebisho haya tufanye maamuzi ya haraka. Matamanio yangu ni kuona Mradi wa Liganga na Mchuchuma unaanza kutekelezwa katika mwaka ujao wa fedha na ndiyo tutaona faida. Tukianza utekelezaji wa Mradi huo wa Liganga na Mchuchuma mtaona wawekezaji kwa upande wa PPP kwa eneo hilo maana mzigo upo. Ndiyo rai yangu kwa Serikali twende haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee suala la Electronic Tax Stamp. Ripoti ya Kamati ya Bajeti ni nzuri sana mapendekezo yako wazi. Sasa hivi tunatumia stamp za kodi za karatasi na wanalipia nadhani kama dola moja. Kinachogomba hapa nilivyowasikia Waheshimiwa Wabunge wengi ambao wamechangia kwenye eneo hili wanasema malipo ambayo atachukua mwekezaji hayawiani vizuri na kiwango cha uwekezaji wake na lingine ni ule muda wa miaka mitano. Bidhaa ambazo tulianza nazo na stamp hizi za kodi za karatasi, tunajua ni pombe kali, mvinyo, filamu za wasanii wetu hawa, pamoja na sigara. Pamoja na maeneo ambayo wameanza kutumia mfumo huu ambao una tija sana hawajabeba bidhaa zote kwa wakati mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri tuanze na bidhaa chache na hasa hizi ambazo tayari zilikuwa zinatumia mfumo huu. Pendekezo langu la pili ni kwamba viwango vya sasa vinavyotumika vya dola moja kwa stamp ya karatasi ndiyo viendelee kutumika katika mfumo huu. Tunaweza kuongeza hata bia lakini tusiingize bidhaa zingine kama maji, soda na juice, hapana, tusifike huko kwa sasa kwa maoni yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani tukienda hivyo tutakuwa tumeliweka vizuri suala hili. Tunataka tujiridhishe na uzalishaji wa ndani wa viwanda hivi na baada ya pale tutaona, Serikali itakuja Bungeni itaonesha, pale ambapo mapato yatakuwa yameongezeka tutakuwa na hoja ya msingi ya kusema sasa twende mbele kwenye bidhaa nyingine, tukienda hivyo tutafanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda mfumo huu mpya tufanikiwe kwa sababu haiwezekani leo Tanzania makusanyo yetu ya ndani yawe around 15 au 14.5 chini ya viwango tunavyovifahamu katika region hii vya kati ya 17 na wengine wameenda mpaka 20. Naomba sana tuunge mkono jitihada hizi za Serikali lakini tuanze na bidhaa chache ambazo tutazisimamia lakini pia viwango vinavyotozwa sasa ndivyo vitumike, tusiongeze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kutoongeza Ushuru wa Bidhaa na hili tumekuwa tukilisema na baada ya mwaka mmoja tutaona numbers. Napenda eneo hili Waheshimiwa Wabunge Serikali ituelewe, tusiwe tunaenda mbele halafu tunarudi, tuwe very consistent tulee manufacturing industry ya Tanzania bado contribution yake kwenye pato la Taifa ni ndogo sana ya asilimia 5 tunapenda ipande kwa haraka kwa asilimia 10 mpaka 15 na mtaona faida ya uchangiaji wake katika uchumi. Tukienda na hatua hizi za kwenda mbele na kurudi hatutaona tutakuwa tunarudi pale pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho naomba tuwekeze katika sekta ya kilimo kwa upana wake. Land bank ambayo tumeizungumzia kupitia TIC tufike mwisho, maeneo hayo yapatikane na tukaribishe wawekezaji wakubwa. Wawekezaji wadogo hawa wakulima wetu wametusaidia mpaka sasa lakini ili kwenda kwa kasi kubwa kwenye kilimo lazima tukaribishe wawekezaji wakubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, ubarikiwe sana kwa kunipatia nafasi hii, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii. Nianze kwa kusema naunga mkono hoja zote mbili. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na timu yake kwa kazi nzuri ambayo wameendelea kuifanya. Tunaelewa changamoto mlizonazo na kwa hali yetu hii tunaelewa lakini nasema hongereni sana kwa haya ambayo mnayafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia huko tulikotoka miaka 20 iliyopita maboresho ambayo yamefanywa consistently na Serikali hasa kuanzia Awamu ya Tatu, Awamu ya Nne na yanayoendelea sasa ndiyo yamewezesha kuona mafanikio tunayoyaona sasa hivi. Jitihada za Serikali za kuhakikisha kwamba tunakuwa na uchumi wa jumla ulio tulivu, tunajenga mazingira mazuri ya uwekezaji na kufanya biashara, tunaendelea kuwekeza kwenye miundombinu ya barabara, umeme, maji, yote haya ndiyo yanawezesha mafanikio haya tunayoyaona. Mheshimiwa Waziri na timu yenu naendelea kuwapongeza sana pamoja na changamoto za rasilimali fedha ambazo tunazo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi hii mikubwa ambayo Mheshimiwa Rais wetu ameanza kuitekeleza, pamoja na maneno mengi, hii ndiyo itakayochochea zaidi maendeleo yetu. Ujenzi wa reli ya kati kwa standard gauge na matawi yake muhimu, maboresho yanayoendelea sasa hivi katika bandari ya Dar es Salaam, niongeze hapo, siyo maboresho tu na upanuzi wa bandari ya Dar es Salaam lakini napenda tuanze ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo kwa sababu tunafahamu Bandari ya Dar es Salaam tayari imekuwa chocked. Tujenge bandari mpya ya Bagamoyo ambayo itakuwa ni kwa faida kubwa ya Taifa hili kwa miaka 100 inayokuja ili tuweze kushindana na tujenge mazingira ambayo yatatuwezesha kutumia nafasi yetu ya kijiografia kama vizuri kama nchi, tunaweza, tunaweza. Ndiyo maana Mwalimu alikuwa anatukumbusha wakati wenzetu wanatembea sisi tukimbie. Ndiyo maana ya kufanya uwekezaji mkubwa kama huu, ndio una gharama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, narudia, ni vema tukachukua uamuzi haraka, tukapata a financing instrument itakayotuwezesha ku-fund reli ya kati na matawi yake tumalize mapema kuliko hii ya kwenda vipande vipande na tutaona jinsi uchumi utakavyokua kwa haraka. Hili linawezekana, ni ombi langu sana kwa Serikali, twende haraka na baadaye mtaona faida kwa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha tulilisema miaka minne iliyopita mamlaka ya nchi haiwezi ikajiondolea sovereignty yake. Nashukuru mmerejesha mamlaka ya Waziri wa Fedha ya kuweza kusamehe pale inapobidi miradi mikubwa kwa faida ya maendelao yetu, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu, kwa miradi ambayo tayari iko kwenye pipeline maamuzi yafanyike haraka, twende mbele. Baada ya Bunge kama litakubali marekebisho haya tufanye maamuzi ya haraka. Matamanio yangu ni kuona Mradi wa Liganga na Mchuchuma unaanza kutekelezwa katika mwaka ujao wa fedha na ndiyo tutaona faida. Tukianza utekelezaji wa Mradi huo wa Liganga na Mchuchuma mtaona wawekezaji kwa upande wa PPP kwa eneo hilo maana mzigo upo. Ndiyo rai yangu kwa Serikali twende haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee suala la Electronic Tax Stamp. Ripoti ya Kamati ya Bajeti ni nzuri sana mapendekezo yako wazi. Sasa hivi tunatumia stamp za kodi za karatasi na wanalipia nadhani kama dola moja. Kinachogomba hapa nilivyowasikia Waheshimiwa Wabunge wengi ambao wamechangia kwenye eneo hili wanasema malipo ambayo atachukua mwekezaji hayawiani vizuri na kiwango cha uwekezaji wake na lingine ni ule muda wa miaka mitano. Bidhaa ambazo tulianza nazo na stamp hizi za kodi za karatasi, tunajua ni pombe kali, mvinyo, filamu za wasanii wetu hawa, pamoja na sigara. Pamoja na maeneo ambayo wameanza kutumia mfumo huu ambao una tija sana hawajabeba bidhaa zote kwa wakati mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri tuanze na bidhaa chache na hasa hizi ambazo tayari zilikuwa zinatumia mfumo huu. Pendekezo langu la pili ni kwamba viwango vya sasa vinavyotumika vya dola moja kwa stamp ya karatasi ndiyo viendelee kutumika katika mfumo huu. Tunaweza kuongeza hata bia lakini tusiingize bidhaa zingine kama maji, soda na juice, hapana, tusifike huko kwa sasa kwa maoni yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani tukienda hivyo tutakuwa tumeliweka vizuri suala hili. Tunataka tujiridhishe na uzalishaji wa ndani wa viwanda hivi na baada ya pale tutaona, Serikali itakuja Bungeni itaonesha, pale ambapo mapato yatakuwa yameongezeka tutakuwa na hoja ya msingi ya kusema sasa twende mbele kwenye bidhaa nyingine, tukienda hivyo tutafanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda mfumo huu mpya tufanikiwe kwa sababu haiwezekani leo Tanzania makusanyo yetu ya ndani yawe around 15 au 14.5 chini ya viwango tunavyovifahamu katika region hii vya kati ya 17 na wengine wameenda mpaka 20. Naomba sana tuunge mkono jitihada hizi za Serikali lakini tuanze na bidhaa chache ambazo tutazisimamia lakini pia viwango vinavyotozwa sasa ndivyo vitumike, tusiongeze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kutoongeza Ushuru wa Bidhaa na hili tumekuwa tukilisema na baada ya mwaka mmoja tutaona numbers. Napenda eneo hili Waheshimiwa Wabunge Serikali ituelewe, tusiwe tunaenda mbele halafu tunarudi, tuwe very consistent tulee manufacturing industry ya Tanzania bado contribution yake kwenye pato la Taifa ni ndogo sana ya asilimia 5 tunapenda ipande kwa haraka kwa asilimia 10 mpaka 15 na mtaona faida ya uchangiaji wake katika uchumi. Tukienda na hatua hizi za kwenda mbele na kurudi hatutaona tutakuwa tunarudi pale pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho naomba tuwekeze katika sekta ya kilimo kwa upana wake. Land bank ambayo tumeizungumzia kupitia TIC tufike mwisho, maeneo hayo yapatikane na tukaribishe wawekezaji wakubwa. Wawekezaji wadogo hawa wakulima wetu wametusaidia mpaka sasa lakini ili kwenda kwa kasi kubwa kwenye kilimo lazima tukaribishe wawekezaji wakubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, ubarikiwe sana kwa kunipatia nafasi hii, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi ya asubuhi hii niseme kwa kufupi. Nampogeza sana Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mheshimiwa Engineer Isack Kamwelwe na Naibu wake Mheshimwa Aweso.

Mheshimiwa Spika, vile vile nampongeza Katibu Mkuu wa Wizara hii Profesa Kitila Mkumbo, Naibu Katibu Mkuu Engineer Kalobelo, watendaji wote na Watumishi wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri ambayo wanaendelea kufanya. (Makofi)

Mheshiwa Spika, hotuba ya Mheshimiwa Waziri ni nzuri, imebeba matumaini kwa Watanzania kwenye sekta hii muhimu. Waswahili wanasema mnyonge mnyongeni, lakini haki mpeni. Naamini Wizara hii ingeweza kufanya mambo makubwa, lakini limitation ya rasilimali fedha, hiyo ndiyo tunaiona sote. Tunawapongeza kwa haya, hata kwa ile pesa kidogo ambayo wameweza kupewa, mnaona matokeo kwa kazi waliyofanya kwa mwaka huu tunaomaliza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naipongeza sana Serikali, maana ukilinganisha bajeti ya mwaka 2017/2018 ambao tunaumaliza, kwa upande wa fedha za maendeleo mwaka huu Serikali tofauti na mwaka 2017/2018 ambapo sehemu kubwa ya bajeti ya maendeleo ilikuwa ya kutoka nje, safari hii bajeti ya maendeleo ni fedha zetu za ndani. Naipongeza sana Serikali kwa hilo na tuendelee hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ila tu kwenye Fungu Na. 05 kwa upande wa umwagiliaji, bado sehemu kubwa ya fedha za kutoka nje. Nadhani kama tunataka tufikie malengo letu ambayo mpaka sasa tuko nyuma sana, maana tulikuwa tumepanga ifikapo mwaka 2015 tuwe tumekuwa na ekari milioni moja za umwagiliaji wala hatujafika huko.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, unaiona hali hii, lakini hata kwako hapo, mimi huwa napita na Waheshimiwa Wabunge wote tunapita sehemu ya Itanana pale au Kibaigwa hapo, kipindi cha masika hayo maji tungeweza kuyavuna tukafanya mambo makubwa. Siyo mbali, hapo kwenye Jimbo lako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo niseme mambo ya Bariadi. Naishukuru sana Serikali, naona mradi wa kutoka Ziwa Victoria kupeleka Mkoa wa Simiyu, mradi mkubwa wa kitaifa unatoa matumaini. Nimeaangalia kitabu cha Volume IV siuoni mradi huo, ila kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kwenye schedule ukurasa 198 naona zipo shilingi bilioni 15. Sasa napenda Mheshimiwa Waziri anapokuja ku-wind-up hoja yake hili suala tulielewe sote vizuri, kwa sababu haiwezekani tukapitisha mradi huo lakini kwenye eneo la pesa za maendeleo hazionekani. Yawezekana labda zimewekwa kwenye fungu lingine, sitaki kuwasemea lakini watanisaidia kulielewa hili.

Mheshimiwa Spika, tuwape wananchi wa Simiyu matumaini ya kupata maji salama ya uhakika. Sisi tuna shida sana ya maji, lakini kwa mradi huu naona tunaenda vizuri. Wananchi wa Busega, wananchi wa Bariadi, wananchi wa Itilima, wananchi wa Meatu na wananchi wa Maswa, mradi huu utatuleta manufaa makubwa sana kwa maendeleo yetu. Tuombe tu kwamba utekelezwe kwa haraka, usanifu huu ukamilike mwezi huu na kweli tuanze kazi ya kuandaa zabuni ya kufanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Spika, la pili, Mfuko wa Taifa wa Maendeleo ya Maji tulianzisha zaidi ya miaka saba iliyopita, lakini napenda sasa Serikali iende na wakati. Tulianza na Wajumbe wanne; Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Mjumbe mmoja anatoka Wizara ya Maji na Umwagiliaji, Wizara ya Fedha na Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Jamani tunataka Mfuko huu uwe ndiyo engine ya maendeleo katika kusukuma miradi ya maji. Naomba basi tupanue sura ya uwakilishi kwenye bodi hiyo, isiendelee kukaa kama kitengo cha Wizara. Tunataka isimame iwe na CO wake, Sekretarieti yake, Meneja wa Mfuko, wasimamie shughuli hii. Naomba sana Serikali walione hilo kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, lingine ni la skimu za umwagiliaji. Mwaka 2016 Serikali ilitaja kwenye bajeti yake, kulikuwa na mabwawa kama kumi na bwawa moja lilikuwa katika Jimbo langu la Bariadi, Bwawa la Kasoli. Sasa hapa katikati silioni tena. Mheshimiwa Waziri silioni Bwawa la Kasori, nimeangalia humu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona Skimu ya Umwagiliaji ya Mwasibuya inaenda vizuri. Naishukuru Serikali kwa mipango hiyo na pesa ambayo nimeiona humo. Napenda kama siyo mwaka kesho tuweke Bwawa la Kasoli lakini pia na eneo la Ikungulyambesha, mbona Wajapani walikuja wakaangalia eneo hilo, lakini kwa sababu ya tatizo la usanifu haikuwa imekaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira (BARUWASA) Bariadi. Sijui tumekosea nini, hii ni class. Daraja la Tatu, Mamlaka hii ya BARUWASA ni class three. Kwa mujibu wa kanuni zetu, unapokuwa kwenye ngazi hiyo wewe unastahili kupewa na Serikali kupitia Wizara, ruzuku ya kulipia umeme wa TANESCO wa kuendesha hizi pump za kuzalisha maji. Sisi hatupewi, tumekosea nini nauliza?

Mheshimiwa Spika, napenda sana Mheshimiwa Waziri hili utusaidie utupatie majibu ambayo yatawapatia wananchi wa Bariadi matumaini. Tuna shida ya maji, kama yalivyo maeneo mengi ya nchi hii. Siwezi kuwa mchoyo, lakini kile ambacho tunakipata tunataka rasilimali fedha hiyo itumike vizuri. Naelewa maeneo yetu mengi tuna tatizo la absorption capacity. Naiomba sana Serikali tuangalie watalaam wetu, tuwagawe katika njia ambao itawezesha Halmashauri zetu nyingi kunufaika na rasilimali fedha hizi ambazo zinatolewa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, nisingelipenda kupigiwa kengele ya pili; naipongeza Serikali kwa kazi nzuri wanayofanya. Tuendelee kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja hii. Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. ANDREW J. CHENGE – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA SHERIA NDOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi niweze kuhitimisha hoja yangu. Niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamepata nafasi ya kuchangia hoja ya Kamati hii lakini baadhi yao hasa wale Wajumbe wa Kamati yenyewe; Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete, Mheshimiwa Salome Makamba na wameelezea vizuri. Yupo Mheshimiwa Mnzava sikujua ni mwanasheria huyu, alielezea vizuri sana, namshukuru sana. Mheshimiwa Dkt. Kolimba na Mheshimiwa Mukasa, nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nifanye sahihisho moja, limetumika neno Kamati ya Sheria Ndogo Ndogo, hii siyo Kamati ya Sheria Ndogo Ndogo ni Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo. Tuelewane, hizi ni sheria za nchi wala siyo sheria ndogo ndogo, ni sheria kabisa zinazotokana na mamlaka ya Kikatiba ambapo Bunge linapoona inafaa kukasimu, linakasimu madaraka yake. Kupitia Kamati hii ndiyo linachungulia kudhibiti yale ambayo limekasimu kuona kama yamekaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi tumesema sheria hizi zinapotungwa na mamlaka inayokasimiwa zinaanza kutumika kabla ya kuwasilishwa humu Bungeni. Ndiyo maana busara ya Spika kwamba tuwahishe Kamati hii iwe inatoa taarifa zake mapema ili kusaidia kutoonea wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko tunakoelekea bado nashauri ni vyema tukaangalia utaratibu huu wa Sheria Ndogo kuanza kutumika zinapochapishwa kwenye Gazeti la Serikali, hiyo ndiyo hoja na inazungumzika. Ndani ya nchi za Jumuiya ya Madola baadhi ya nchi zimebadilisha utaratibu ambao Tanzania tunautumia lakini nasema kwa sasa huo ndiyo utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisingependa nichukue muda mrefu, matokeo ya uchambuzi wa kazi tuliyofanya kwa mwaka mzima mnayaona kwenye taarifa pamoja na lile jedwali. Tumeelezea changamoto ambazo zipo, ni kama tano, tunaiachia Serikali ione namna gani tunavyoweza kuzipunguza. Zipo zile za wazi kabisa, hii ya ku-copy tu Sheria Ndogo za Halmashauri fulani bila hata kuzamia, nadhani hapa ni suala la kutokuwa makini tu kwa wahusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme moja, Ofisi ya Waziri Mkuu hasa kupitia Ofisi ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Jenista Mhagama amekuwa mtu wa karibu sana katika kuunganisha shughuli za Kamati na Serikali, yeye kama daraja na wanayaona mapema na hasa zile ambazo zinahusu Ofisi ya TAMISEMI wanawapelekea haraka sana ili wafanye masahihisho na hatimaye kuzichapisha tena na kuletwa humu Bungeni. Tunamshukuru sana kwa kazi hiyo na tutaendelea kushirikiana naye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo hii changamoto kubwa ya uandishi wa sheria, uchache wa wataalam hawa, hili sio la Tanzania tu. Nimekulia kwenye Ofisi ya Mwanasheria Mkuu naelewa kazi nzito walizonazo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu kwa upande wa Idara ya Uandishi. Kazi hii siyo ya kila mwanasheria, kazi hii unahitaji wanasheria wanaoipenda ile kazi, wenye weledi, wanaoifahamu sheria katika mapana yake sio katika eneo dogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunapowapata wanasheria kama hawa, changamoto kubwa ipo namna ya kuwatunza wabaki Serikalini au kwenye taasisi za Serikali. Ni utaalam wa kipekee huu, tunao wachache lakini naishauri Serikali iendelee kuwekeza kwenye eneo hili, bado hatujafanya vizuri. Tulifanya vizuri mpaka miaka ya 1980 sasa tumeanza kuwapoteza hawa ambao tulikuwa nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri zetu, TAMISEMI wajitahidi kwa kadri inavyoweza kuwanoa wanasheria walionao. Mimi najua baadhi yao wanaweza wakapata mafunzo wakaongeza weledi wao wa namna ya kuzichambua na kuziandaa hizi sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge hili ndilo linakasimu mamlaka yake kwa mamlaka mbalimbali, nawaombeni sana Waheshimiwa Wabunge shughuli ya kukasimu itaendelea tu kwa sababu Bunge haliwezi likafanya kazi zote na kutunga sheria aspect zote zikawa kwenye sheria. Tunapokubali kama Bunge kukasimu nawaombeni sana tuwe makini kwamba ile misingi ambayo tunakasimu ikatungiwe kanuni lazima tuiweke katika lugha ambayo siyo pana sana na hii ndiyo kazi ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana Ofisi ya Bunge, Katibu wa Bunge katika kuwajengea uwezo Wabunge wa kuchambua Miswada, naomba hili liendelee. Serikali nayo ione uwezekano huu wa kuwajengea uwezo Wabunge wa kuchambua Miswada, tusiachie wageni kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii Kamati inachambua makaratasi na yanashuka kama mvua. Siyo kazi nyepesi na inafanywa na watu ambao siyo wanasheria, mimi nawapongeza sana lakini nazidi kuiomba Ofisi ya Katibu wa Bunge waangalieni kwa jicho la huruma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu lipokee na kukubali taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Sheria Ndogo kuhusu shughuli zilizotekelezwa kwa kipindi cha kuanzia Januari, 2018 hadi Januari, 2019 pamoja na maoni na mapendekezo yaliyomo katika taarifa hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii nami niweze kusema machache kuhusiana na hoja iliyo mbele yetu. Nianze kwa kusema, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Profesa Mheshimiwa Mbarawa, Naibu wake Mheshimiwa Aweso, timu nzima ya Wizara ya Wataalam ikiongozwa na Profesa Mkumbo na msaidizi wake Engineer Kalobelo, viongozi wote, watendaji na wataalam. Ni miongoni mwa Wizara ambazo kusema kweli zinafanya kazi nzuri, ni kwa sababu tu ya rasilimali fedha zinakuwa zinatuangusha. Tuwatie moyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitaanza na ya nyumbani kidogo, maana mcheza kwao hutunzwa. Nina miradi ya siku nyingi sana ambayo haijapata fedha. Nikianza na Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi, kuna visima vilichimbwa tangu mwaka wa fedha 2012/2013, mpaka leo maji yapo lakini wananchi hawajanufaika na jitihada za kodi zao kupitia miradi hii. Miradi hii ipo Masewa, Igaganulwa, Sengerema, Nkololo na Igegu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Nkololo ni kichekesho kusema kweli, kwa sababu tumepata msaada kutoka Serikali ya Misri na Waziri wa Ujenzi sasa hivi Mheshimiwa Engineer Kamwele alipokuwa Naibu Waziri wa Maji alienda akatembelea mradi huu. Ni mradi ambao umetoa maji mengi sana, tunataka tuwasambazie wananchi wa center hiyo kubwa ya Nkololo. Amemaliza kuwa Naibu Waziri, akawa Waziri (full minister) wa Maji, maji hayajasambazwa. Mheshimiwa Prof. Mbarawa, rafiki yangu, naomba mtusaidie kwa upande wa miradi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi ambao ndiyo Makao Makuu ya Mkoa wa Simiyu, tuna miradi ambayo tumeleta Wizarani, imesimama miezi sita sasa. Mradi wa Sanungu, Mahina, Nyangokolwa; nilimsikia Mheshimiwa Gimbi asubuhi akiuliza swali la nyongeza, lakini ndiyo hali halisi.

Mheshimiwa Spika, pia Nyakabindi, Bupandagila, kunahitaji kuunganishiwa na kusambaziwa maji kwa ajili ya wananchi hawa na sekondari yetu kongwe ya Bupandagila, wananchi hawapati maji. Kuna Giriku, Kidali Mandam na Mbiti. Kote huko maji yapo, tunataka tu tupate fedha tuwapatie huduma wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Izunya hivyo hivyo. Kisima hiki kina maji mengi sana, tunaweza tukatoa kwa Mitaa yote ya karibu pale Nyamhimbi, Ntuzu na Chenge Sekondari. Yote haya ni mambo ambayo tungependa tuyaone. Ni ombi langu kwa Serikali tuwaone wananchi wa Bariadi kwa jicho la huruma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri wakati anajibu swali hili asubuhi alipoulizwa na Mheshimiwa Gimbi Masaba, naipongeza Serikali yetu kwa hatua ya msingi ya kuanza kutekeleza mradi wa kutoa maji haya Ziwa Victoria na kuyafikisha katika Miji ya Nyashimo, Bariadi, Lakangabilili, Itilima Pale, Maswa na hatimaye Meatu, Kisesa na Mwanhuzi. Huu ndiyo ukombozi kwetu. Hii ndiyo huwa naita kwa ukanda wetu kama Simiyu. Kwetu hii ndiyo royalty, ndiyo mrahaba kwetu wananchi wa Tanzania. Ahsante sana Serikali ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Magufuli. Sasa tunapata matumaini kwamba mradi huu utaanza kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona kwenye nyongeza ya saba, zipo pesa shilingi bilioni 19.5 zimetengwa kwa shughuli hiyo. Naamini tutaanza vizuri. Najua muda wangu siyo rafiki, hayo ambayo yamo humu ndani ya hotuba ya Mheshimiwa Waziri ambayo wanatarajia kuyatekeleza katika mwaka ujao wa fedha iwapo pesa itapatikana kwa wakati yatatekelezwa. Ni imani yangu kwa Serikali kwamba fedha ikipatikana yatatekelezwa na ninaomba iwe hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili nami niseme tu kwa upande wa shida ya maji nawe unajua, ni kubwa. Lazima tufanye kila linalowezekana kuunga mkono jitihada za kuwapatia huduma ya maji wananchi wetu. Wazo la kuondoa kodi kwenye mitambo ya kuchimba maji ni moja njia ya kusaidia. Tulianza vizuri huko nyuma.

Mheshimiwa Spika, miaka ya nyuma tulikuwa tumeondoa kodi kwenye mitambo. Hapa katikati tukajichanganya tena kwa sababu ya ombi letu, misamaha ya kodi imekuwa mingi sana na kadhalika, ndiyo ikatufikisha hapa. Naiomba Serikali tualiangalie tena suala hili. Wenzetu hapa katika East Africa, wote wameshaondoa kodi kwenye mitambo ya maji, ni sisi tu hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naiomba Wizara ya Fedha, Wizara ya Maji na Serikali kwa ujumla, tumalize biashara hii na private sector isaidie katika kutoa huduma hizi. Tutaona viwango vitashuka sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije kwa hili la hoja ya Kamati. Mimi kama Mbunge, wewe kama Kiongozi wetu, naomba sana, Waheshimiwa Wabunge mnisikilize, naomba sana…

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, hebu tusikilizane. Kuna lots of talking, please.

MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Spika, nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge, sisi tusimamie maamuzi yetu. Tuna Azimio la Bunge ambalo lilitaka tuongeze shilingi 50 kwa mafuta. Huu ni mwaka wa tatu mfululizo Kamati inasema; sio mimi, Kamati na ni Azimio la Bunge. Sasa sisi Bunge tusipoheshimu maamuzi yetu, nani atayaheshimu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba maamuzi yetu tuyalinde kwa wivu wa hali ya juu sana. Mojawapo ni hili. Napenda sana, maana tunajenga nyumba moja, tusigombanie fito na Serikali. Sisi tumetoa pendekezo hili la kuongeza shilingi 50/= kwa kila lita ya mafuta ya petrol na diesel na tunaona figures tunazozitaka. Tunataka tufikie kiwango cha kupata shilingi bilioni 300 karibu na 20 na kitu kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama Serikali itakuja na alternative ambayo inatupeleka huko, sisi tutakuwa tayari baadaye kuja kuondoa Azimio letu kwa utaratibu wa Kibunge. Kwa sasa hivi inakuwa ni very awkward kwamba sisi wenyewe Wabunge tulipitisha Azimio hapa na Serikali ilikuwepo, haikufanya mabadiliko kwenye Azimio hilo na lipo. Sasa tunataka twende kwenye force nyingine, haiwezekani.

Mheshimiwa Spika, nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge, sisi tung’ang’anie kwenye shilingi 50/= kwa lita. Halafu tutaisilikiza Serikali kama ina alternative ambayo ni sustainable, endelevu ya kutufanya tuhangaike na suala zima la maji. Hizi ndiyo kura za uhakika. Unaona, ingekuwa siyo Mfuko huu wa Maji, tungekuwa mahali pabaya sana.

Mheshimiwa Spika, naomba sana Waheshimiwa Wabunge tuiunge mkono Serikali, lakini na Serikali ituelewe sisi kama wawakilishi wa wananchi kwamba tuna hoja ya kujenga na siyo ya kubomoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Spika, nikishukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ili nami nichangie kwa ufupi tu.

Mheshimiwa Spika nipongeze kazi nzuri inayofanywa na Wizara hii kwenye maeneo muhimu ya ujenzi wa barabara, mawasiliano na uchukuzi. Hongereni sana, naelewa rasilimali fedha ndiyo zinatusumbua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jana nimetoka Bariadi kuja Dodoma nimeona kazi nzuri inayofanywa kati ya Bariadi na Maswa, mkandarasi anaendelea na pesa imetengwa tena. Tungependa tukamilishe barabara hii ikiwezekana mapema mwaka huu au mwaka kesho tuweze kutoka moja kwa moja Dar es Salaam – Dodoma – Shinyanga – Mwigumbi –Bariadi – Lamadi – Musoma – Sirari - Nairobi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Bariadi imekaa katikati kwa ukanda wa Kaskazini Mashariki mwa Tanzania na ndiyo maana tunasema sana barabara, tulitegemea katika Mwaka huu ujao wa fedha angalau kipande cha Bariadi kuja Moboko-Mwanuzi mpaka Sibiti kingeliweza kufanyiwa feasibility study yaani upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Lakini naona siioni kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri hata kwenye majedwali yale ya kipande hiki hakipo, tunaendelea kuiomba Serikali kwamba tuunganishwe na mikoa jirani ya Singida na Arusha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine mkisoma hotuba za Wizara hii kwa miaka mitatu iliyopita barabara ya Kolandoto, Munze, Lalago mpaka Thibiti ilikuwa inaenda mpaka Matala - Mang’ola na Odiang Junction. Sasa hivi tunaongelea kasehemu kadogo tu, tumeanzisha mradi mzuri tu huu wa kutoka Karatu, Mbulu, Haydom, Sibiti, Lalago Maswa. Ningependa Serikali ituambie kwa kazi iliyofanyika kwa kipande cha kutoka Sibiti, Matala, Mang’ola na Odiang Junction ile sehemu tunaiacha au tunaendelea nayo? Ningependa nipewe majibu na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije kwenye upande wa barabara, mimi kuna barabara nasema kwa sababu tunajua hali ya Tanzania iliyvyo kuna maeneo mengine ni ukame, mengine yana hali nzuri ya barabara, naendelea nashukuru Serikali nimeona upande wa barabara ya Kidatu – Ifakara - Tupilo kuelekea Malinyi - Londo mpaka Lumecha Songea nashukuru sana kwa sababu tukiweza kukamilisha barabara hii tunafungua njia ambayo eneo lenye utajiri mkubwa sana wa chakula na hali nzuri ya hewa. Lakini ningependa tuangalie pia uwezekano wa kutoka Ifakara twende Kihansi, twende Mlimba, twende Taweta, twende mpaka Madeke, twende mpaka Lupembe maana tukiyabeba haya yote unaifungua sehemu hiyo yenye utajiri na kuweza kupeleka chakula kwa haraka katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho naomba tunafanya kazi nzuri katika kupanua Bandari ya Dar es Salaam, napongeza Serikali lakini nasema mwaka jana nilishauri reli yetu ya kati hii tunayoijenga sasa hivi ni afadhali tukachukua mkopo wa muda mrefu kuliko hii ya mikopo ya masharti ya muda mfupi ambayo yatakuja kutuumiza, maana hata kabla hatujaanza kuitumia reli hii tutaanza kulipa madeni haya. Lakini tukichukua madeni ya muda mrefu na kwa masharti nafuu tunajenga reli hii tukamilisha yote kwa wakati mmoja ili tuweze kupata faida ya uamuzi mzuri huu unaofanywa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa bandari ya Dar es Salaam itatusaidia kwa muda mfupi tu. Duban na Bellair na sasa Nakala lakini upande wa Lam na Mombasa wenzetu hawa wanaangalia mbali sana, tungependa na sisi Bandari hizi Mungu ametupa nafasi nzuri sana, Bandari ya Mtwara, Bandari ya Dar es Salaam, Bandari ya Bagamoyo Mbegani narudia kuishauri Serikali na Mwambani hizi kwa upande wetu wa Tanzania zikiweza hizi zikajengwa, hii ndio future ya Tanzania kuunganisha na nchi za Maziwa Makuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningependa sana Bunge lako tuendelee kuishauri Serikali waone faida ya haya. Najua muda wangu ndio huo lakini nikushukuru sana kwa nafasi uliyonipa, naishukuru Serikali kwa haya wanayoyafanya, niungane na Mheshimiwa Serukamba kwamba tuangalie kwa haraka na sio kupoteza muda, sekta binafsi ishirikiane na sekta ya Umma kwa PPP katika kuyafanya mengi haya na tusiogope. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Kumi na Nne na Mkutano wa Kumi na Tano wa Bunge
MHE. ANDREW J. CHENGE - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA SHERIA NDOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipatia fursa hii ili niweze kuhitimisha hoja yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru sana Makamu wa Mwenyekiti wa Kamati hii, Mheshimiwa William Mganga Ngeleja, Mbunge wa Sengerema kwa jinsi alivyowasilisha na umahiri aliouonesha katika kuwasilisha taarifa ya kamati. Amewasilisha vizuri, mtiririko wa hotuba yake na maelezo ya taarifa ya kamati yametiririka vizuri. Pia nimshukuru kwa maneno mazuri aliyosema kuhusiana na mimi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapokuwa kiongozi, na baadhi yetu kama mimi huwa napenda sana kile kidogo nilichovuna niweze kumega kwa wenzangu, ndiyo maana yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hii ujumbe wangu kwa viongozi wengine katika Bunge hili, tuna-talents nyingi sana katika nyumba hii, tusiwe wachoyo kwa kuwashirikisha wenzetu katika kile ulichonacho, na ndiyo tutajenga Institution ya Bunge kwa leo na kesho. Leo sisi tupo kesho hatupo lakini tunataka tuendelee kuliboresha Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge waliosimama na kuongea kuiunga mkono hoja hii. Niwatambue Mheshimiwa Taska Mbogo, Mheshimiwa Saed Kubenea, Mheshimiwa Goodluck Mlinga, Mheshimiwa William Ngeleja mwenyewe, Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote wameongea vizuri sana katika kazi nzuri inayofanywa na Kamati kwa lengo la kujenga. Hata hivyo niseme neno moja, jana wakati tuna ile hoja ya Kamati ya Sheria Ndogo kuhusiana na ule Muswada wa Marekebisho ya Sheria Mbalimbali uliohitimishwa jana Bungeni. Napenda sana nimpongeze Mheshimiwa Mariam Kisangi, na jana alisema maneno mazuri tu. Yeye amekuja kwenye Kamati hiyo kujifunza, na katika kipindi kifupi aliweza kutoa mchango mzuri sana kwenye Kamati na jana mlimsikia humu. Hata hivyo linalonifanya niyaseme ya jana yawezekana wengine mmeyapatia tafsiri tofauti. Alisema katika kipindi cha wiki moja chini ya uongozi wa Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mheshimiwa Chenge amefundishwa mambo mengi, sasa nasema hivi, niliyomfundisha ni mambo ya sheria. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eeh, eeh!Ya sheria tu, lakini ni mwanafunzi mzuri, Waheshimiwa Wabunge!

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwanasheria Mkuu amesema maneno mazuri sana, ya mafunzo kwa wanasheria wetu, lakini mimi ningependa niende mbele zaidi, continuing education kwa wanasheria wa Serikali ni kitu kizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa faida ya Taifa hili mimi napenda kuiona Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ule upande wa uandishi wa sheria, ile Idara ya Uandishi wa Sheria ambayo ndiyo roho ya Serikali, mimi nashauri na niiombe Serikali kwa moyo wa dhati kabisa, tuendelee kuwekeza, tuendelee kuwekeza katika uandishi wa sheria. Kada hii ya wanasheria duniani kote ina waandishi wa sheria walio wazuri wachache sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tumeanza kuwa na crop nzuri ndio wanafika kustaafu, wengine wameondoka wakaenda kutafuta greener pastures, lakini zoezi la kuilinda na kuiendeleza Ofisi ya Uandishi wa Sheria katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu mimi naomba liwe ni ajenda ya kudumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, kwa sura ya pili kwa upande wa Ofisi ya Bunge, tunataka Ofisi ya Mwanasheria wa Bunge iwe na waandishi pia ambao wataweza kuwasaidia Wabunge katika hoja mbalimbali ambazo wanazileta humu Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, amelisema pia Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, unaona kuna element ya improvement katika uandaaji wa sheria ndogo zinazowasilishwa Bungeni ukilinganisha na kule tulivyoanza; tungependa hii trend iwe nzuri; ninaamini kwa assurance ambayo Mheshimiwa Waziri wa Nchi ameyasema nadhani litaenda likaboreshwe hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Wizara na Idara za Serikali watashirikishwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, Idara ya Uandishi wa Sheria mapema tutaweza kupunguza sana kasoro zilizokuwa zinajitokeza, hasa katika ukiukwaji wa sheria mama ambayo ndiyo msingi unaoruhusu sheria ndogo husika kutungwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo kwa sababu hoja hii imeungwa mkono na wajumbe wote waliochangia, mimi ningependa nihitimishe kwa kuliomba Bunge lako Tukufu kwamba Maazimio ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo, yaliyowasilishwa Bungeni kupitia taarifa ya kamati ambayo yapo kwenye Ibara ya 8(1), 8(2), 8(3) na 8(4) ya taarifa ya kamati, sasa yakubaliwe na Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa wa Mwaka 2018
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii. Nami niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu waliotangulia kusema hukusu hoja hii. Mtaniwia radhi Waheshimiwa Wabunge kwa sauti yangu kwa sababu wiki mbili zote hizi zimekuwa na mahangaiko kwangu kutokana na Muswada huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze na moja la kusema naunga mkono Muswada huu. Ni Muswada mzuri, umekuja kwa wakati na kwa shabaha na lengo zuri tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sheria hii imetungwa mwaka 1992, baadhi yetu tulikuwa humu Bungeni. Sheria hii tumeifanyia marekebisho hapa katikati lakini hayakuwa marekebisho makubwa sana mpaka miaka 10 iliyopita 2009 tulipoleta marekebisho mengi kidogo. Lengo kubwa la kipindi hicho na mtakaokumbuka ilikuwa ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na Sheria ya Vyama vya Siasa ambayo inakubalika na hao wanasiasa ambao ndiyo viongozi wa vyama hivi au wanachama wake lakini pia miongoni mwao au miongoni mwa vyama hivyo vinapata bahati ya kuongoza nchi. Ndiyo maana katika sheria hiyo utakuta yale makatazo kama walivyosema wengine yanaanza kwenye Ibara ya 20(2) ya Katiba. Ndiyo maana masuala ya ubaguzi wa dini, maeneo unakotoka, kuhakikisha tunaulinda Muungano wetu, yote hayo yapo ndani ya Katiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishukuru sana Serikali kupitia Muswda huu imekubali kufanya marekebisho ambayo Bunge lilifanya lakini likakosea. Bunge lina mamlaka ya kutunga sheria kwa jambo lolote la Muungano na kwa masuala mengine ambayo ni ya Tanzania Bara lakini Bunge halina mamlaka ya kutunga sheria ambayo inakwenda kinyume na Katiba. Hilo liko wazi kabisa na concern ya Waheshimiwa Wabunge naielewa, nawaheshimu sana wanaposema hivyo, wanatukumbusha vizuri tu. Mwaka 2009 tuliingiza kifungu miongoni mwa sababu za kufuta chama cha siasa, nia ilikuwa ni nzuri lakini hatukufika katika kukiweka kwenye Katiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ukikisoma kifungu hicho hata chenyewe maana kina makatazo kwamba chama kwenye Katiba yake kisiruhusu wanachama wake kutukana. Sasa kuna Katiba ya chama ambayo tutakuta imendikwa Katiba yangu itaruhusu wanachama wake kutukana?

Mheshimiwa Spika, sasa na chenyewe ilikuwa ni kituko lakini kwa bahati nzuri sasa tumepata nafasi nzuri ya kuyasahihisha hayo. Mimi nashukuru sana Serikali imeliona hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana mtoa hoja, Mheshimiwa Jenista na timu yake, Msajili wa Vyama vya Siasa, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu na Kamati ya Katiba na Sheria. Mimi uliniruhusu nikakae nisikilize, nilikuwa mwakilishi wako msikivu, nilikaa kuanzia siku ya public hearing ya kwanza, ya pili, ya tatu, ya nne, wiki nzima tukahamia kwenye Kamati lakini na kule nilikuwa naweza kusimama tu pale Mwenyekiti anaponiomba nisaidie. Kwa hiyo, nashukuru sana Wajumbe wa Kamati hiyo kwa kazi nzuri waliyoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, marekebisho yaliyofanyika kwenye Schedule of Amendments ya Serikali sote tunaona ni kazi kubwa na siyo nyepesi. Mimi nasema tujipongeze lakini tuipongeze Serikali inapokubali hoja nzuri zinazoletwa na Waheshimiwa Wabunge. Hapo ndiyo tunaposema Serikali yetu ni sikivu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vyama vya siasa ni uwanja wa kulea viongozi wetu. Kupitia marekebisho haya tunaanza kuona matumaini mapya kwa nchi hii kupitia vyama vya siasa. Mimi sipendi kurudia yaliyosemwa lakini tukiweza kuyasimamia haya kwenye vyama vyetu, uwanja wa siasa Tanzania utaanza kuwa tambarare. Tunapoongelea utawala bora na demokrasia, lazima uanzie kwenye vyama vyenyewe vya siasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kifungu cha 6C(5) kinatamka wazi kabisa kwamba mwanachama kama sheria hii itapita hataweza kufukuzwa tu kama kiongozi anavyotaka. Lazima taratibu za Katiba zizingatiwe. Sasa unapolikataa na hilo sielewi lakini mimi naona ni mambo mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme mawili ya mwisho, la kwanza ni kuhusu vyama kuungana (merging) tumehangaika nalo sana na siyo suala rahisi. Niishukuru Serikali kwa kuliona hilo kwa sababu hatuwezi kuandika sheria yenye macho. Sheria inapaswa isiwe na macho itende haki kote kote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana Serikali imeliona hilo na hiyo ni kwa sababu Katiba ya Jamhuri ya Mungano wa Tanzania hairuhusu mwanachama kiongozi aliyepatikana kwa kupendekezwa na chama chake hapa katikati akaondoka kwenda chama kingine, lazima apoteze nafasi aliyonayo. Tulifanya yale makosa mwaka 2009, ndiyo kilikuwepo kifungu hicho, wengi walisema tulikikosea, ni kweli tulikikosea lakini sasa tumepata nafasi ya kukisahihisha, tukiondoe. Kikiendelea kukaa kitaweza kuleta mtikisiko wa Kidola maana haiwezekani nchi hii ikawa na vacuum katika uongozi wa nchi yetu. Rais wa Jamhuri ya Muungano akishapatikana isipokuwa kama atajiuzulu mwenyewe, atakuwa impeached, au atafariki dunia atasubiri mpaka uchaguzi mwingine kama yeye ni mgombea ataendelea, kama siyo yeye amsubiri amkabidhi Rais mteule, ndiyo Katiba hiyo. Kwa utaratibu wa merging unazaa chama kipya, viongozi wapya wa vyama na wanachama wapya na ndiyo maana matokeo yake hayo yanafikisha kuleta constitutional crisis. Tumeliacha hilo ili Serikali iendelee kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, dunia ya leo siyo ya merge ya miaka ya TANU na Afro-Shiraz. Dunia ya leo ni ya mashirikiano ya coalition na ndiyo maana Ibara ya 51(2) cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu nafasi ya Waziri Mkuu mtaona concept ile ni ya coalition. Iwapo chama cha Rais hakikupata Wabunge wengi humu, Waziri Mkuu hatapatikana kutokana na chama cha Rais, lazima Wabunge walio wengi kutoka vyama vingine washirikiane.

Mheshimiwa Spika, muda wangu ni huo lakini mimi naipongeza Serikali kwa kutuletea Muswada huu na kwa kukubali marekebisho mengi ya Waheshimiwa Wabunge. Yale ya Katiba tumejitahidi sana kuhakikisha kwamba hatukiuki Katiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipo kifungu kidogo tu cha kiongozi anayetaka kuanzisha chama. Tunaweza tukaki- justify kama kilivyo kwa kwenda kusema kwamba kwa sababu hakuna haki au uhuru usio na mipaka, Ibara ya 30 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano lakini mimi najaribu kuomba tuliangalie, tungeweza tu kusema huyu awe ni Mtanzania wa kuzaliwa basi. Ukiisoma Sheria ya Uraia wewe kama ni Mtanzania wa kuzaliwa maana yake moja ya wazazi wako ni wa kuzaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nadhani sisi ni Wabunge, tunatunga sheria lakini lazima tutunge sheria from an informed position kwa kuheshimu sheria zilizopo. Nisingependa tupate nafasi ya watu kwenda kusema kifungu hiki kinaleta ubaguzi wa aina fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hivyo, nakushukuru sana. (Makofi/Vigelegele)