Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Tundu Antiphas Mughwai Lissu (9 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. TUNDU A. M. LISSU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa sababu muda nitazungumzia masuala mawili tu na yote yanahusu mahakama.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kwanza linahusu masuala ya kinidhamu ya Majaji. Tarehe 30 Novemba, 2014, Bunge hili lilipitisha Azimio kwamba Rais aunde Tume ya Uchunguzi ya Kijaji kuchunguza Majaji wa ESCROW. Majaji wawili ambao kwa ripoti maalum ya uchunguzi ya Kamati ya Kudumu ya Bunge hili iliwakuta wamechukua mamilioni ya fedha kutoka kwa yule bwana wa ESCROW James Rugemalira.
Mheshimiwa Naibu Spika, Majaji wawili Aloysius Mujulizi na Profesa Eudes Ruhangisa. Bunge lilipitisha Azimio, baadae Mheshimiwa Rais Kikwete alipozungumza na wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam, tarehe12 Disemba mwaka huo alisema kwamba, suala la nidhamu ya uchunguzi wa Majaji hao linapelekwa kwa Tume ya Utumishi wa Mahakama lianzie huko, halafu baadaye ndiyo liletwe kwa Rais kwa ajili ya hatua zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mapema mwaka jana na baadaye mwishoni mwa mwaka jana Mheshimiwa Jaji Mkuu aliviambia vyombo vya habari kwamba uchunguzi wa Majaji hawa wawili ulikuwa umeisha kamilika! Leo ni mwaka mmoja na nusu, tangu Azimio la Bunge, kuhusu Majaji wa ESCROW pamoja na wengine litolewe, taarifa iko wapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, tafadhali Mheshimiwa Waziri utakapokuja kujumuisha, utuambie Majaji waliochukua shilingi milioni mia nne, mia nne kutoka kwa Rugemalira na Bunge hili likapitisha Azimio kwamba washughulikiwe kwa mujibu wa Katiba, kitu gani kinatokea na huu ukimya ni wa nini?(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hili suala la nidhamu ya Majaji ni suala muhimu sana, mahakama zetu zimechafuka, tunapenda kulalamika Mahakimu, Mahakimu, Mahakama zetu katika ngazi zote zimechafuka! Kitu cha ajabu kabisa ni kwamba tumekuwa tunachukua hatua dhidi ya Mahakimu wa Mahakama ya Mwanzo once in a long while, Majaji hawaguswi! Hatuna malaika wala watakatifu katika Mahakama Kuu, hatuna malaika wala watakatifu katika Mahakama ya Rufani ya Tanzania, kitu cha ajabu ni kwamba mara ya mwisho na hii ni muhimu, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania amechukuliwa hatua ilikuwa mwaka 1991, Mheshimiwa Jaji Mwakibete alipoundiwa Tume ya Uchunguzi akaondolewa madarakani. Miaka zaidi ya 25 Mahakama ni rushwa tupu na kila mtu analalamika hapa! Lakini ikifika kuchukua hatua, kila mtu anaogopa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa hili ambalo liko wazi kabisa la waliokutwa wamechukua mamilioni ushahidi wa nyaraka upo, tuambiwe imekuwaje? Tusinyamaziwe tafadhali, mahakama zetu kama tunakubali kwamba kutumbua majipu ya muda mrefu ni kitu muhimu, haya ya wazi haya, tusiyaache hilo la kwanza.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kitu cha pili ambacho kinasemwa sana ni hiki kinachoitwa kuanzishwa kwa Mahakama ya Mafisadi. Mara nyingi ninapoona watu ambao wanaonekana onekana kama wana akili hivi, kama wamesoma hivi, kama wanajua sheria hivi, halafu wanazungumza vitu vya ajabu kabisa, nakuwa nafedheheka sana.
Waheshimiwa Wabunge, tumekuwa na Mahakama ya Mafisadi tangu mwaka 1984; kwa miaka 32 leo tuna Mahakama ya Mafisadi. Sasa haiitwi jina hilo inaitwa kwa kiswahili maarufu inaitwa Mahakama ya Wahujumu Uchumi. Ilianzishwa wakati wa crackdown ya Sokoine wa wahujumu uchumi na walanguzi. Mahakama Kuu inaposikiliza kesi zote za rushwa, Mahakama Kuu inaposikiliza kesi zote za kutakatisha fedha haramu, Mahakama Kuu inaposikiliza kesi zote za hujuma ya uchumi, makosa kwa mfano yanayohusiana na Sheria za Wanyamapori, Sheria za Dawa za Kulevya and so on and so forth, inakaa kama Mahakama ya Mafisadi, imeanzishwa kwa mujibu wa sheria. Sasa unashangaa watu wanaoonekana kama wanafahamu wanazungumza, tunampongeza Mheshimiwa Rais sana, ameamua kutuanzishia Mahakama ya Mafisadi nonsense!
Mheshimiwa Naibu Spika, nani aliyewaambia hakuna Mahakama ya Mafisadi? Kama mnataka kuibatiza tu semeni, halafu ukiuliza eehe! huo Muswada uko wapi? Aah tutaianzisha tu kama Division ya Mahakama Kuu, nonsense! Division ya Mahakama Kuu inahitaji Sheria, kuna Division ya Mahakama Kuu ya Ardhi, imeundwa kwa sheria. Division ya Mahakama Kuu ya Ajira Kazi, imeundwa kwa Sheria, Division ya Mahakama Kuu ya Biashara, imeundwa kwa sheria, hii Division ya Mahakama Kuu ya Mafisadi, sheria yake iko wapi? Hii ambayo mnasema mtaianzisha sijui mwezi Julai!
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mambo haya, ambayo tunaambiwa tuna wataalam wa sheria wanaofahamu fahamu, why are they allowing these nonsense to go on. Kwa nini watu wenye utaalam wa sheria, madaktari hapa na wengine maprofesa, kwa nini wanaacha ujinga huu unaendelea kusambaa? Nafahamu na kwa sababu nimeshughulikia haya masuala kwa miaka mitano Bunge lililopita, kwamba kuna matatizo makubwa kuhusiana na uendeshaji wa kesi za ufisadi, nayafahamu, lakini kusema kwamba hakuna mahakama ya kuyashughulikia ni kuthibitisha ujinga tu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunataka kupigana sawa sawa na tatizo la ufisadi, tuzungumze kuna tatizo gani katika Mahakama ya Economic and Organized Crimes Court iliyoanzishwa na Marehemu Sokoine mwaka 1984. Tusijifanye tunatengeneza mambo, hakuna kitu kipya hapa, Mahakama hii ipo for the past 32 years, ina matatizo yes, tuyazungumze hayo matatizo. Lakini tusizungumze as if hakuna kitu, tunaanzishiwa kitu kipya na Rais John Pombe Magufuli. Akizungumza Rais, namsamehe siyo mwanasheria, akizungumza Daktari wa Sheria nafedheheka sana kwa sababu anajua kama hajui anapaswa kujua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kwa vile muda hakuna, hivi umri wa kustaafu wa Jaji Mkuu ni miaka mingapi? Hivi huyu Jaji Mkuu wa kwetu hajafikisha huo umri wa kustaafu? Wenzake wote aliokuwa nao darasa moja, Jaji Msofe, Jaji Masati, Dkt. Steven Bwana, walishastaafu miaka mingi, Jaji Mkuu wetu umri wake wa kustaafu ni lini? (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. TUNDU A. M. LISSU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naomba nianze kwa kuzungumzia moja ya vitu ambavyo ni omission sijui ni nini kwa kiswahili, lakini kuna vitu ambavyo vinashangaza kwa jinsi ambavyo tumejisahau.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma Katiba ya Kenya ya sasa hivi, vile vifungu vya mwanzo kabisa vimezungumzia nembo za taifa la Kenya; wimbo wa Taifa na maneno yake; court of arms na nembo nyingine za Taifa la Kenya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Tanzania huu utakuwa ni mwaka wa 66 tangu tupate uhuru. Mheshimiwa Waziri utakapokuja kuzungumza hapa hebu waeleze Wabunge hawa kama kwa sheria za Tanzania (sizungumzii Katiba), kama Wimbo wetu wa Taifa unatambuliwa kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu miaka kumi baada ya kupata uhuru mwaka 1971 Bunge hili lilitunga sheria inayoitwa Sheria ya Nembo za Taifa na sheria ile inazungumzia Bendera ya Taifa na ile Bibi na Bwana (court of arms). Wimbo wa Taifa (Mungu Ibariki Afrika) siyo nembo ya Taifa kwa mujibu wa sheria za Tanzania. Mheshimiwa Waziri, atakapokuja kuzungumza hebu aje atuelezee usahaulifu huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, miaka 48 iliyopita kuanzia mwaka 1969 mpaka 1971 kilikuwa kipindi ambacho nchi yetu iliua uhuru wa vyombo vya habari kwa kutaifisha vyombo vya habari vya binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili gazeti la Daily News lilitokana na kutaifishwa kwa The Standard. Magazeti mengi yalikuwa nationalized. Tukaingia kwenye utawala wa kiimla kwa maneno ya Mheshimiwa Waziri hapa, kwenye vitabu vyao, nimekuja na copy hapa. Tukaingia kwenye dola la kiimla ambalo halikuwa linatambua uhuru wa habari na tumeenda na uimla huo mpaka 1984 tulipopata Bill of Rights kwenye Katiba yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bill of Rights hii ni muhimu sana kwenye masuala ya uhuru wa vyombo vya habari. Tofauti na haki nyingine, haki ya kupata habari imeondolewa kile kitu kinaitwa clawback clauses, haina clawback clauses. Uhuru wa kupata na kusambaza habari, hautegemei sheria kwa mujibu wa Katiba hii. Ukienda kwenye nyingine inasema kwa mujibu wa sheria, kwa kufuatana na sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Article 18 ya Katiba imeondoa clawback clauses, lakini unashangaa Mheshimiwa Rais anawaambia watu hadharani kwamba msifikiri mna uhuru wa habari wa aina hiyo. Not to that extent.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba yetu imeondoa mipaka ya uhuru wa habari. Kwenye haki ya habari there are no clawback clauses. Mheshimiwa Waziri atakapokuja hebu tunaomba atusaidie, haya maneno anakuwa ameshauriwa au anakuwa anajisemea tu. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii katika awamu hii, kama kuna kipindi ambacho uhuru wa habari unakabiliwa na tishio kuliko kipindi kingine chochote ni tangu mwaka 2015. Silaha za choice, kuna Sheria inaitwa Electronic and Postal Communications Act, imetumika kukamata watu wengi sana kwa sababu ya ku-execise uhuru wao wa habari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Makosa ya Mtandao na Sheria ya Huduma ya Vyombo vya Habari; hizo sheria tatu ndiyo zinazotengeneza utatu haramu kwenye masuala ya uhuru wa vyombo vya habari. They constitute the biggest threat on press freedom in this country. Ndiyo maana polisi wanatembea all over kwenye cyber space.

Ukiisema Serikali vibaya, ndani! Ukimkosoa Rais au Waziri, ndani! Nani aliyewaambia katika nchi hii kwamba the President is above the law? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nani aliyesema kwa mujibu wa sheria gani kwamba Rais hawezi akasemwa vibaya? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Mheshimiwa mmoja aliwahi kuwa Jaji Mkuu wa nchi hii, alisema hiyo dhana kwamba Rais yupo juu ya sheria yenyewe ina-undermine Katiba. Mheshimiwa Jaji Mkuu Samata!

Sasa Bunge hili lina wajibu, msifikirie hii ni kelele ya wapinzani, Bunge hili lina wajibu wa kulinda uhuru wa habari. Mkinyamaza kimya ninyi mlio wengi, leo ni sisi, kesho ni Mheshimiwa Nape na keshokutwa ni wewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilizungumza wakati tunapitisha Sheria ya Vyombo vya Habari, nilinukuu maneno ya baba wa Rais wa sasa wa Ghana wakati Nkurumah anapitisha sheria ya kuweka watu kizuizini, anamtumia Waziri wa Mambo ya Ndani anaitwa Tawia Adamafio. Wakamwambia Tawia Adamafio, angalia unatengeneza mtego wa panya, utakukamata wewe. Kweli Tawia Adamafio alikuwa mtu wa kwanza katika historia ya Ghana kuwekwa kizuizini kwa sheria aliyoipitisha mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafadhalini Waheshimiwa Wabunge, hizi sheria; haya mambo mabaya ambayo yanafanyika nchi hii halafu mnayalinda yasisemwe, mnatuziba sisi mdomo mnafikiria mtashughulikia sisi; mnashughulikia Bunge hili na mkishalishughulikia hili Bunge, mtashughulikiwa ninyi wenyewe na hakutakuwa na mtu wa kuwapigieni kelele; hakutakuwa na mtu wa kuwasemea kwa sababu wengine wote tutakuwa tumenyamazishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni kuhusu wasanii wetu! Kuna kitu kinaitwa artistic freedom. Wasanii wanapotunga nyimbo, wana-exercise their freedom of speech as well. Ukiwakamata, ukawateka nyara na kuwatesa, una-violate their artistic freedom, una-violate their freedom of speech. Sasa hatujawahi kuona katika vipindi vingine vyote katika uhuru wa nchi hii wasanii wakitekwa nyara kwa sababu ya nyimbo zao, tumeiona kwa … (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. TUNDU A. M. LISSU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kunipa fursa ya kuchangia. Naomba nianze kwa kushauri Wizara, Mheshimiwa Waziri na timu yake kwamba kuna haja kubwa sana sasa ya ku-diversify vyanzo vya utalii wetu na mapato ya utalii.

Waheshimiwa Wabunge wamezungumza mengi tangu Mheshimiwa Ally Saleh asubuhi na wengine wamegusia. Nchi nyingi duniani zinapata mapato makubwa kutokana na utalii wa historia tu, museums! Ukienda Vietnam War Museum in Washington DC, Lincoln Memorial, Washington Memorial, nenda kwenye museum za Ujerumani, nenda kwenye museum inaitwa Robben Island, it is a national park in South Africa. Mamia ya maelfu ya watalii wanakwenda sio kwa sababu kuna wanyamapori; wanakwenda kwa sababu kuna historia. Sasa sisi asilimia 90 ya mapato yetu ya utalii ni wanyamapori na tunajipongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fikiria siku hawapo au mnafikiri wataendelea kuwepo milele. Fikiria hivi kuna siku hawapo, unafanya nini, fikiria! Kwa hiyo, hoja kubwa Mheshimiwa Waziri, think of diversification, weka mayai yako kwenye makapu mengi, kapu moja likianguka yatakayovunjika ni machache, hilo niliachie hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, haya masuala ya uhifadhi na mahusiano ya wananchi wanaoishi katika maeneo ya karibu na hifadhi zetu. Leo hii zaidi ya asilimia 30 ya total land mass ya Tanzania imehifadhiwa na maana yake nikwamba, wananchi kwa mamilioni wameondolewa kwenye maeneo hayo, wafugaji na wakulima hawapo. Namna pekee ambayo tumeitumia kwa miaka zaidi ya 50 ya kulinda maeneo haya ni kuyafanya kuwa maeneo ya kijeshi. Ndiyo maana katika sehemu kubwa yenye uvunjifu mkubwa wa haki za binadamu kwenye Tanzania ya leo ukiachia vituo vya polisi ni kwenye maeneo ya hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhifadhi wa aina hii unaotegemea kutesa na kunyang’ana watu maeneo yao hauna future. Kuna siku hawa watu wataamka, watajibu halafu tutaenda wapi.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba nisaidie tu, kuna sababu gani ya kisayansi leo ya kuwakataza wafugaji wa Kimasai ambao hawawindi kuchunga kwenye hifadhi walikofukuzwa mwaka 1959. Kama unataka kujua sayansi inasemaje soma Allan Rodgers na Kay Homewood 1995 – The Maasailand Ecology, wamesema maeneo haya ya uhifadhi yana wanyamapori kwasababu wafugaji wa Kimasai hawana shida na wanyamapori, sio wawindaji. Mmewafukuza mnawaharibia uchumi wao wa kiufugaji, siku wanyama wao wakiisha watakuwa wawindaji, wakipata bunduki kama Karamoja muone mtakwenda wapi na wanyamapori wenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namna ya kuokoa long term, maslahi ya uhifadhi, namna ya kuwaokoa wanyamapori hawa na maeneo haya ni kuhakikisha kwamba zile shughuli za matumizi ya ardhi ambazo kihistoria hazina athari kwenye uhifadhi (pastoralism) zinakuwa integrated. Ngorongoro is a failure kwa sababu imekuwa undermined, the idea was good lakini imetekelezwa vibaya. Wamasai wa Ngorongoro leo ni maskini kuliko Wamasai wengine wote, sio kwa sababu Mungu amesema wawe maskini, ni kwa sababu yahii militarism katika conservation. Tunahitaji a new thinking, Mheshimiwa Mbunge wa Ngorongoro yuko hapa na sijamuona akizungumza, Wamasai wake…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Lissu ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. TUNDU A. M. LISSU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Mimi nimepinga sera za uwekezaji za Chama cha Mapinduzi kabla sijawa CHADEMA, kabla sijaja Bungeni toka mwaka 1999. Yaliyofanyika na Mheshimiwa Rais Magufuli juzi ni ya hovyo, nitayapinga kama ambavyo nimepinga sera zote ambazo zimetufikisha leo hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwa kifupi. Hoja iko hivi, kwa haya ambayo yametendeka, sahauni kabisa diplomasia ya kiuchumi. Suala siyo Acacia watafanya nini? Suala ni kwamba watu wote tunaohusiana nao kiuchumi, Wachina ambao ndio the biggest investors in the world today na ndiyo biggest proponents wa free trade na globalization today. Fikiria Wachina watafanya nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, fikiria EU watafanya nini? United States, ile North America Economic Group itafanya nini? Japan, all the major economic blocks of this world fikiria zitafanya nini kwa sababu ya kitendo kimoja tu cha kunyang’anya michanga ya dhahabu kwa hoja ambazo, kwa wanaojua; sizungumzii wasiojua, washangiliaji hawa, kwa wanaojua, ni hoja za kijinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni kwamba leo hii kiuchumi dunia hii ni multipolar, mwanadiplomasia wetu ataelewa nikisema multipolar wengine wote hawa ni wapiga debe tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kitu kinaitwa Silk Road Economic Belt, kuna kitu kinaitwa The 21st Century Maritime Silk Road, these are the biggest economic initiatives in today’s world economy. We are not a member! Kenya ni member wa 21st Century Maritime Silk Road yaani Kenya ya leo ndiyo marafiki wakubwa wa kiuchumi wa China kuliko sisi ambao tumekuwa marafiki wa China wa miaka yote, kwa sababu tunazungumza economic diplomacy, we don’t know nothing about the economic diplomacy. Ndiyo maana tunafanya haya tunayoyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje, ni mwanadiplomasia, anafahamu haya, asikubali hizi kelele, nchi yetu sasa hivi ina hali mbaya kidiplomasia kwa sababu tumefanya kitu ambacho kisheria ni makosa kwa mujibu wa sheria zetu, kwa mujibu wa mikataba ni makosa, kwa mujibu wa Sheria za Kimataifa ni makosa na gharama tutakayolipa ninyi Wabunge mnaopiga kelele, gharama tutakayolipa ni kubwa kuliko huo mchanga wa Acacia. We will become an economic busket case kama Zimbabwe. Tusishabikie maamuzi ya kijinga kwa sababu tu yamefanywa na Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje, kazi za Mawaziri ni kumshauri Rais. Our economic diplomacy and our economic development is on the brink kwa sababu tumeharibu mahusiano. Kwa hili tu, tumeharibu mahusiano ya kiuchumi kila mahali. Siyo na Acacia. Suala siyo kupelekwa mahakamani tu, suala ni kwamba mwekezaji gani atakayetaka kubakisha hela zake hapa? Mwekezaji gani atakayetaka kuleta hela zake hapa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema siyo Wamarekani na Wazungu tu, fikiria na Wachina ambao ndiyo wawekezaji wakubwa wa dunia hii.
Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Kamisheni ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Malawi pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Amani na Usalama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
MHE. TUNDU A. M. LISSU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia. Naomba niseme kwamba nitachangia hoja ya Kuridhia Mkataba wa Kuanzisha Tume ya Pamoja ya Bonde la Mto Songwe, kati ya Tanzania na Malawi. Kwa sababu ya muda naomba nijielekeze kwenye suala moja tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkataba kati ya Tanzania na Malawi juu ya Bonde la Mto Songwe ni Mkataba wa Kimataifa, it is an International Treaty, tuanzie hapo. Ni mkataba wa Kimataifa kati ya nchi mbili. Pili, kwa vile ni mkataba wa Kimataifa, mkataba wa Kimataifa huu kama kuna sheria nyingine yoyote ya Tanzania inayokwenda kinyume na matakwa ya mkataba huu wa Kimataifa, mkataba wa Kimataifa unasimama sheria ya nchi inatanguka, basic International Law 101. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, kitu ambacho ni muhimu sana na ambacho tunahitaji majibu ya Serikali kuhusiana na mkataba huu wa Kimataifa ni ule unaohusu utaratibu wa utatuaji wa migogoro chini ya mkataba huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Ibara ya 13(3) ya mkataba huu, The Songwe River Basin Convention, endapo kutakuwa na mgogoro kati ya Tanzania na Malawi ambao ndiyo wahusika wa mkataba huu, endapo kutakuwa na mgogoro kuhusiana na masuala mbalimbali yanayohusiana na mkataba huu wa Kimataifa, Ibara ya 13(3) inasema mgogoro huo utapelekwa kwenye Mahakama ya SADC; the parties shall refer the matter to the SADC Tribunal or shall appoint an adhoc arbitrator through mutual agreement which shall be in writing. The arbitrator’s decision shall be final and binding on the parties.

Mheshimiwa Naibu Spika, ikipelekwa kwenye Mahakama ya SADC au ikapelekwa kwa msuluhishi wa Kimataifa, uamuzi wa Mahakama ya SADC au uamuzi wa huyu msuluhishi wa Kimataifa utakuwa ni wa mwisho na utatufunga sisi pamoja na Malawi, sasa shida iko hapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkataba wa Bonde la Mto Songwe unahusu rasilimali ya maji, unahusu acquatic resources, unahusu water resources, unahusu lakes, unahusu rivers. Haya yote niliyoyataja yanajulikana katika sheria, ile sheria ilipitishwa kwa shamrashamra sana humu ndani, ile sheria ya kutangaza mamlaka ya kudumu ya utajiri wa nchi; The Natural Wealth and Resources Permanent Sovereignty Act iliyopitishwa hapa mwezi Julai. Sheria ile imesema, hizo nilizozisema, rasilimali za maji, vile vitu vilivyoko kwenye maji, samaki and so on and so fourth, lakes, rivers, everything, kifungu cha 11 cha sheria ile kimesema kwamba ni marufuku kwa rasilimali hizi zilizotajwa kuamuliwa nje ya Mahakama za Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba na Waheshimiwa Wajumbe wajiridhishe wakaangalie kifungu cha tatu cha sheria ile, waangalie na kifungu cha 11(1), (2) na (3) cha sheria ile ili wajiridhishe juu ya hiki ninachokisema.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo letu la miaka yote na tatizo letu hasa la Bunge hili ni ushabiki usiokuwa na maana yoyote. Tumeruhusu Bunge linapitisha sheria za mambo makubwa bila kuzitafakari, matokeo yake ndiyo haya. Sasa tuna mkataba wa Kimataifa unaosema rasilimali zetu za maji, maziwa, mito, kuhusiana na Bonde la Mto Songwe zitaamuliwa kama kutakuwa na mgogoro katika Mahakama ya SADC. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wale walioenda ku- negotiate huu mkataba na umesainiwa tarehe 18 ya Mei, hakukuwa na watu wa Attorney General’s Office, hakukuwa na watu wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali? Hakukuwa na watu wa Wizara ya Katiba na Sheria na tuna maprofesa pale! Niliposema proffesorial rubbish, this is what I meant, hawakuwepo? Hawa ambao walileta baadaye hii Sheria ya Natural Wealth and Resources (Permanent Sovereignty) hawakujua kwamba kuna mkataba umekuwa negotiated, ume… (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. TUNDU A. M. LISSU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Maneno ya Mheshimiwa Mbene wala hayahitaji heshima ya kujibiwa, naomba niendelee.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni hivi, nimeuliza swali la msingi hapa, huu mkataba umesainiwa tarehe 18, Mei 2017. Je, Mheshimiwa Waziri wa Maji Gerson Lwenge alienda peke yake? Yeye Engineer mambo ya sheria anaweza asiyafahamu, alikuwa peke yake? Hakupata ushauri wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali? Hakupata ushauri wa Waziri wa Sheria? Wale walioleta Sheria hii ya Permanent Sovereignty over Natural Wealth hawakujua matakwa ya mkataba huu?(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, matokeo yake nimezungumza na nitaendelea kuzungumza tena, matokeo yake ni aibu hizi! Mmetunga sheria miezi miwili iliyopita, leo mnaleta mkataba mnatunga sheria nyingine ya kuitengua na mtaitengua. Waheshimiwa Wabunge, nawaomba sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo hili la mgongano kati ya sheria inayosema maliasili na utajiri wa nchi yetu ushughulikiwe na Mahakama zetu uko vilevile kwenye Mkataba ambao unakuja kesho wa Bomba la Mafuta, kaangalieni. Mkataba wa Bomba la Mafuta unasema tukigombana Uganda na Tanzania kwa sababu ya bomba la mafuta mgogoro ule unaenda kuamuliwa London na hawa ambao wanajifanya ndio watetezi wa rasilimali za nchi hii, hatuoni! (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, nawaombeni, mimi nina maneno makali sana, lakini nani aniambie kama haya ambayo tumeyapitisha yako sahihi. Aniambie haya ninayoyasema ni ya uwongo, kwamba hatujaleta mkanganyiko wa kisheria hapa, kama tumeleta mkanganyiko wa kisheria tunatunga mkataba wa Kimataifa, tunapindua kile tulichokipitisha hapa kwa majidai mengi. Tunakitengua miezi miwili baadaye, sisi ni watu wa aina gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, hasa Waheshimiwa Wabunge mlio wengi, narudia tena wito wangu, haraka haraka haina baraka, maangamizi ya Taifa hili na maanguko ya Bunge hili ni hicho kinacholetwa kila leo kwa hati ya dharura. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. TUNDU A. M. LISSU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba nianze kwa kusema kwamba, mimi sio mtaalam wa maandiko matakatifu lakini kuna

mahali katika Biblia kunasema watu wangu wanaangamia kwa kukosa maarifa, na nchi yetu inaangamia kwa sababu ya kukosa maarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, asubuhi umesema kwamba haya masuala ya madini yanahitaji semina. Hilo ni jambo muhimu sana, kwa sababu hoja hii inahitaji maarifa sana haiwezi ikajadiliwa sawasawa kwa hizi dakika tano au kumi.

Mheshimiwa Spika, nataka nijikite katika masuala ya madini kwa sababu ambazo ziko wazi kabisa. Kamati ya Rais ya Profesa Osoro ya jana na Kamati ya Profesa Mruma ya mwezi uliopita, siyo ripoti za kwanza kuzungumzia, kuchunguza matatizo ya kwenye sekta ya madini katika nchi hii, siyo za kwanza na Rais Magufuli siyo wa kwanza.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2002, Rais Mkapa aliunda Kamati iliyoongozwa na Jenerali Mboma inaitwa Kamati ya Mboma kuchunguza matatizo ya sekta ya madini, hasa madini ya vito vya thamani 2002. Mwaka 2004 Waziri Mkuu Fredrick Sumaye, Serikali ya Mkapa iliunda Kamati ya Dkt. Jonas Kipokola, kuchunguza matatizo ya sekta ya madini, taarifa yake ni ya Agosti, 2004.

Mheshimiwa Spika, mwaka uliofuata 2005 Rais Mkapa na Serikali yake waliunda Kamati ya Bukuku alikuwa Katibu Mkuu Wizara ya Fedha kuchunguza matatizo ya sekta ya madini. Mwaka 2006 miezi michache baada ya Rais Kikwete kutawazwa kuwa Rais akaunda Kamati ya Lawrence Masha bahati nzuri nimekuja na taarifa yake hii hapa. Kamati ya Lawrence Masha kuchunguza Sheria za Madini, Sheria za Kodi, Sheria za Fedha, mikataba ya madini, kila kitu cha madini, taarifa hii hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 2008 baada ya mgogoro wa Buzwagi hapa Bungeni, Rais Kikwete aliunda Kamati ya Jaji Mark Bomani hii hapa, Kamati ya Jaji Mark Bomani taarifa yake ni ya Aprili, 2008. Kamati ya Osoro na Kamati ya Profesa Mruma ni Kamati ya sita kuundwa kushughulikia masuala ya madini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimekuja na muhtasari wa Kamati ya Profesa Osoro ya jana hii hapa na kwa sababu nafahamu taarifa zote hizi za Kamati zingine, naweza nikawaambia Waheshimiwa Wabunge, hadidu za rejea za Kamati ya Mruma na Osoro ni zilezile zilizokuwa hadidu za rejea za Kipokola, za Bukuku, za Lawrance Masha na za Kamati ya Bomani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, matokeo yake, findings na recommendations ziko hapa kwa kiasi kikubwa ni findings na recommendations zilezile zilizokuwa kwa Bukuku, zilizokuwa kwa Kipokola, zilizokuwa kwa Masha, zilizokuwa kwa Bomani, hazijawahi kutekelezwa kwa sababu mnayoifahamu.

Mheshimiwa Spika, watu ambao wameuza madini ya nchi hii walipitisha sheria kwenye Bunge hili na ndio maana inashindikana na hii ya Dkt. Magufuli, nazungumza Mungu anasikia na watu wasikie, mtaniambia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika taarifa hii ya jana, wamependekeza watu fulani fulani washughulikiwe, Mawaziri, Makamishna, Mwanasheria Mkuu Bwana Chenge, akina Ngeleja, akina nani, naombeni niwaambieni kitu Waheshimiwa Wabunge ili muwe na maarifa. Mtu wa kwanza kusaini mikataba ya madini na leseni za madini tarehe 5 Agosti, 1994, Meja Jakaya Mrisho Kikwete, leseni ya Bulyanhulu hii inayopigiwa kelele leo, Leseni ya Bulyanghulu ya tarehe 5 Agosti, 1994 ilisainiwa na Jakaya Kikwete akiwa Waziri wa Maji, Nishati na Madini, hakuwa na kinga ya Urais wakati ule, hana kinga ya Urais leo kuhusiana na masuala aliyoyafanya wakati hajawa Rais. Hana! Alisaini leseni siyo ya Bulyanhulu peke yake, pia ya Nzega na ya Geita. Golden Pride - Nzega na Geita Gold Mine zina sahihi ya Kikwete, anaponaje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mapendekezo haya anaponaje? Kama mnataka kweli kushughulikia watu walioshiriki mambo haya, mbona mnachagua chagua? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hizi leseni na hizi sheria tatizo kubwa tangu mwaka 1999 wenye kujua tumesema, tatizo kubwa ni sheria za Tanzania. Sisi ni wanachama wa Mkataba wa Kimataifa wa kulinda uwekezaji (The MIGA Convention). Tumesaini mikataba na nchi moja moja zenye wawekezaji Tanzania, nchi 26, mikataba ya kulinda Wawekezaji hawa. Tumetunga Sheria ya Madini yenyewe, Sheria za Kodi za mwaka 1997, Sheria ya Uwekezaji ya Mwaka 1997. Hizi za 1997 zilipitishwa siku moja tarehe 26 Machi, under Certificate of Urgency. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama kuna mchango utakaoutoa kama Spika na utakumbukwa, upige marufuku hii habari ya Certificate of Urgency kwenye utungaji sheria, inatuletea mabomu. Sheria za Gesi Asilia na mafuta mlizotufukuza hapa mkazipitisha ni mabomu matupu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesoma hizo takwimu mlizoambiwa na Profesa Mruma na Profesa Osoro za madini ambayo yameondoka. Mimi sitasema sana, nawaombeni kama mnaweza, mlinganishe takwimu za utajiri wa madini zinavyozungumzwa kwenye Kamati ya Bomani na mlinganishe na utajiri unaozungumzwa kwenye Kamati ya Profesa Osoro, halafu mniambie nani ni mwongo kati ya hizo mbili.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, nashukuru.
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dokta John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua anazochukua kukabiliana na Upotevu wa Mapato ya Serikali katika Sekta ya Madini
MHE. TUNDU A. M. LISSU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Wajibu wa Kikatiba wa Bunge hili ni kuisimamia na kuishauri Serikali, wajibu wa Bunge siyo kuishangilia au kuimba mapambio kwa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema wajibu wa Kikatiba wa Bunge ni kuisimamia na kuishauri Serikali siyo kuisifia na kuiimbia mapambio. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili Azimio siyo Azimio la Bunge ni Azimio la wana CCM kumpongeza Mwenyekiti wao wa CCM. Kama sisi siyo wanafiki, kama Wabunge wa Bunge hili siyo wanafiki, basi kwa vile mnataka tumsifu Magufuli kwa kuunda Kamati, tuanze na Rais Benjamin Mkapa aliyeunda Kamati ya Jenerali Mboma, aliyeunda Kamati ya Dkt. Kipokola, aliyeunda Kamati ya Dkt. Bukuku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama sisi siyo wanafiki, twende kwa Kikwete aliyeunda Kamati ya Lau Masha, akaunda Kamati ya Mark Bomani, kama sisi sio wanafiki lakini kwa sababu ni wanafiki hatuko tayari hata kusema kwamba…

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza, huyo tunayeambiwa amethubutu, mikataba yote ya madini anayoita ya wizi bado ipo, hakuna uliobadilishwa hata mmoja. Hivi tunavyozungumza, sheria zote ambazo zimetungwa miaka yote hii ambazo zimetuleta hapa tulipo, hakuna iliyoguswa hata moja. Hivi tunavyozungumza asilimia 100 ya madini ya dhahabu yanayochimbwa Geita yanasafirishwa kutokea Geita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza asilimia 100 ya dhahabu inayochimbwa North Mara Tarime inasafirishwa nje kupitia Kiwanja cha Ndege cha Kewanja Tarime. Asilimia 95 ya dhahabu ya Bulyanhulu inasafirishwa nje kutokea kiwanja cha Bulyanhulu. Asilimia 95 ya dhahabu ya Buzwagi inasafirishwa kutoka Buzwagi…

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Taarifa mbili zilizotolewa na Profesa Mruma na Profesa Osoro hazina utaalam wowote, haziwezi zikasimama mahali popote.
Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari za Mwaka 2016
MHE. TUNDU A.M. LISSU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa fursa ya kuchangia Muswada huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuchangia, naomba majedwali ya marekebisho ambayo tumeyapeleka Ofisi ya Katibu asubuhi hii yaingizwe kwenye mjadala huu kwa sababu Kanuni ya 86(11) ipo wazi. Kama tunataka kutunga sheria basi tufuate Kanuni za utungaji wa sheria, majedwali yetu yote tuliyoyapeleka yaingizwe ili sheria hii tuijadili na tuipitishe kama inavyotakiwa na Kanuni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kufafanua mambo kadhaa ambayo yamezungumzwa utafikiri ni mambo mapya lakini siyo mambo mapya hata kidogo. Naomba sana Mwalimu wangu Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe anisaidie kama nitakuwa nakosea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, inazungumzwa hapa kwamba suala la accreditation ya waandishi wa habari ni jambo jipya kwamba hatuwezi tukaachia holela tasnia hii, ni kitu kipya, ni kitu muhimu na kadhalika. Siku ambayo Sheria ya Magazeti ilitungwa mwaka 1976 siku hiyo hiyo ilitungwa Sheria ya Shirika la Habari la Tanzania (SHIHATA) na sheria ile pamoja na mambo mengine iliipa SHIHATA mamlaka ya kuandikisha waandishi wa habari na kuwapa vitambulisho. Kwa hiyo, kwa muda wa miaka 24 ambayo Shirika la Habari Tanzania lilikuwepo kwa mujibu wa sheria, moja ya majukumu yake ilikuwa accreditation ya waandishi wa habari. Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe kama nakosea naomba aniambie Mwalimu wangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, mwaka 2000 ilipopitishwa Sheria ya Kufuta Shirika la Habari Tanzania, sheria ile ilikasimu mamlaka yaliyokuwa ya SHIHATA kwa Idara ya Habari Maelezo isipokuwa mamlaka ya ku-accredit waandishi wa habari yaliondolewa. Mamlaka ya kusajili waandishi wa habari yaliondolewa kwa mujibu wa kifungu cha 4(2) cha Sheria ya Kufuta SHIHATA. Kama nakosea Mwalimu wangu nisahihishe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kitu muhimu ni kwa nini mamlaka ya accreditation yaliondolewa mwaka 2000 na Sheria ya Kufuta SHIHATA. Sababu ipo kwenye taarifa ya Tume ya Rais ya mfumo wa Chama Kimoja au Mfumo wa Vyama Vingi maarufu kama Tume ya Nyalali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1991 Tume ya Nyalali ilipotoa taarifa yake pamoja na mapendekezo mengi mengine ilisema kwamba Sheria ya Magazeti, Sheria ya SHIHATA iliyokuwa inaweka utaratibu wa waandishi wa habari kuandikishwa, asipoandikishwa hafanyi kazi, sheria hiyo inakwenda kinyume na matakwa ya Katiba ya uhuru wa habari na uhuru kwa vyombo vya habari. Ndiyo maana accreditation ya waandishi wa habari iliondolewa kwa sheria iliyofuta SHIHATA. Kama nakosea Mwalimu wangu naomba unisahihishe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuulizane kama accreditation ya waandishi wa habari iliondolewa kwa sababu inapingana na Katiba kwa sababu inazuia uhuru wa habari kwa nini inarudishwa sasa hivi? Tukijibu hilo swali tutakwenda mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee, masharti haya ambayo yako kwenye Muswada huu, masharti ya udhibiti wa magazeti yaliingizwa kwa mara ya kwanza katika sheria inayoitwa Sheria ya Magazeti ya mwaka 1928 (Newspapers Ordinance 1928). Ndiyo iliweka utaratibu huu ambao umepigiwa kelele tangu mwaka 76 ilipotungwa hii Sheria ya Magazeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa kudhibiti magazeti kwa kutumia mamlaka ya usajili …
Umeelezewa vizuri sana na mwandishi wa kitabu hiki, The Media History of Tanzania.
Lengo la sheria ya kikoloni, lengo la Sheria ya Magazeti ya mwaka 1928 ilikuwa kuhakikisha kwamba an indigenous press haikui.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mamlaka ya usajili wa magazeti ya mwaka 1928 yaliingizwa kama yalivyo na Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976. Sasa kwa wasiofahamu, naomba mkaangalie mjadala wa Bunge wa mwaka 76, Edgar Maokola Majogo alizungumza kitu gani. Edgar Maokola Majogo alisema sheria hii tunayopitisha ina harufu nyingi ya kasumba za kikoloni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii masharti ya Sheria ya Magazeti ya mwaka 1928 yaliyoingizwa kwenye Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976, miaka 40 baadaye yameingizwa kama ilivyo katika Muswada huu. Maana yake ni kwamba tangu mwaka 1928 utaratibu wetu wa udhibiti wa magazeti, wa udhibiti wa habari falsafa haijabadilika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, vifungu vyote vya uchochezi vilivyopo katika Muswada huu vimeingizwa kama vilivyo kutoka kwenye Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976. Sasa hapa ni muhimu tujue vilitoka wapi kwenye Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1952 miaka miwili kabla TANU haijaanzishwa wakoloni wa Kiingereza walileta sheria, iliingizwa katika Kanuni yetu ya Adhabu kwenye Penal Code sheria ambayo iliingiza makosa yote ya uchochezi kama yalivyo katika Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976 na kama yalivyo katika Muswada huu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mjadala wa Baraza la Kutunga Sheria LEGCO la mwaka 1952, wakati vifungu hivi vinaingizwa walikuwa wanasema kuna haja ya kudhibiti wanaopinga Serikali, kuna haja ya kudhibiti wachochezi. Ndiyo maana, Mwalimu wangu naomba anisaidie, watu wa kwanza kupatikana na hatia ya uchochezi kwa mujibu wa sheria hii walikuwa watatu. Wa kwanza alikuwa Mheshimiwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, wa pili alikuwa Robert Makange, Mhariri wa Gazeti la ...
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.4) wa Mwaka 2016
MHE. TUNDU A. LISSU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya mimi kuchangia vile vile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitachangia kwa kiasi kikubwa katika Sheria ya Mikopo, Misaada na Dhamana za Serikali na kama bado muda utatosha nitazungumza kidogo kuhusu marekebisho ya Sheria ya Wanyamapori.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna msemo wa kiingereza unasema unaosema the road to hell is paved with good intentions (njia ya kwenda jehanamu imepambwa kwa nia njema). Sasa nia njema peke yake haiwezi ikatosha tunapotunga sheria. Lazima tuangalie potential consequences za hiyo sheria tunayoitunga. Kwa hiyo, kutuambia kwamba lengo la muswada ni zuri kwa hiyo tupitishe ni kutuelekeza jehanamu kwa kutegemea tu nia njema. Hatuwezi tukafanya hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, muswada huu unapendekeza hivi; Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iwe mdeni wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano. Serikali ya Jamhuri ya Muungano inakopa pesa say kutoka Benki ya Dunia au kutoka Mabenki ya Kibiashara ya Kimataifa au nchi za kigeni, masharti ya mkopo huo yanadai kwamba ulipwe kwa muda fulani, kwa riba fulani, kwa fedha za kigeni. Halafu kwa Muswada huu, Serikali ya Zanzibar tunaikopesha sisi, Serikali ya Jamhuri ya Muungano inaikopesha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa masharti yale yale ambayo tumepewa sisi na Benki ya Dunia au Mabenki ya Biashara au Taasisi zingine za kigeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba tuulizane tu. Tusitegemee tu nia njema, what if they do not pay? What if they are unable to pay, for whatever reasons. Itakuwaje Serikali ya Zanzibar ikishindwa kulipa huo mkopo kwa masharti yale yale ambayo sisi tumekopa nje (Serikali ya Jamhuri ya Muungano) itakuwaje? Tutakamata mali zao? Tutawashtaki? Tutafanyaje? Wakishindwa kulipa itakuwaje? Hilo la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, muswada unapendekeza vilevile kwamba Serikali inakopa pesa nje kwa masharti hayo, masharti ya mikopo ya kimataifa sio marahisi sana, inakopa nje halafu linakuja Shirika la Umma kwa mfano UDA au Shirika la Elimu Kibaha au National Insurance Corporation au Air Tanzania, Serikali inaikopesha kwa masharti yale yale ambayo imekopa nje ilipe kwa dola, ilipe riba, ilipe kwa muda fulani; ndiyo masharti yanayozungumzwa kwenye muswada huu. Tusizungumzie nia njema, nia njema itatupeleka kuzimu.
Mheshikmiwa Mwenyekiti, itakuwaje Air Tanzania wakishindwa kurudisha hiyo hela Serikalini? Itakuwaje Shirika la Elimu Kibaha wakishindwa? Itakuwaje Halmsahauri ya Wilaya ya Ikungi, imekopa pesa Serikalini kwa utaratibu huu ikishindwa kulipa? Kwa sababu Halmashauri za nchi hii karibu zote zinaitegemea Serikali kwa karibu asilimia 90, zimenyang‘anywa vyanzo vya mapato, hazitozi kodi za majengo na mapato mengi zimenyang‘amywa, zikishindwa kulipa itakuwaje? Kwa hiyo, haitoshi tu kuwaambia watu nia njema, nia njema, tunaunga mkono nia njema ya Serikali, tutaenda kuzimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nirudi kwenye suala la utaratibu huu kwa Serikali ya Zanzibar kwa sababu watu hawaelewi matatizo makubwa ambayo yanakabili Muungano wetu kwa sababu ya matatizo kama haya. Kumekuwa na mgogoro kwa wasiofahamu (mwalimu wangu anafahamu vizuri sana) kumekuwa na mgogoro nchi hii kwa zaidi ya miaka 40 juu ya mapato ya Muungano, zaidi ya miaka 40. Jumbe aling‘olewa madarakani mojawapo kwa sababu ya hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar wamekuwa wanadai kwamba pesa zinazokuja kwa jina la Jamhuri ya Muungano hawazipati. Tukatengeneza utaratibu unaosema wapate asilimia 4.5 ya fedha zinazokuja kama misaada ya kibajeti. Kwa misaada ya bajeti wapate asilimia 4.5; hawajawahi kupata hata hiyo, haijawahi kutokea. Kwenye misaada ile ambayo sio ya kibajeti, hela za basket fund na hizo tunawapa kwenye budget support na budget support wazungu wameiondoa, hiyo general budget support imeondoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Zanzibar miaka yote wanasema hatupati mgao wetu halali na ndiyo maana iliundwa Tume ya Pamoja ya Fedha mwaka 1984 wakati Jumbe anaondolewa madarakani. Ndiyo maana Katiba iliingizwa maneno kwamba kutakuwa na A Joint Account (Akaunti ya Pamoja) ya Serikali ya Muungano na Serikali ya Zanzibar ili kutatua hili tatizo la Zanzibar kutopata mgao wake miaka yote, tangu mwaka 1984 halijashughulikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume ya Pamoja ya Fedha ilipendekeza tangu mwaka 2006 ikarudia tena mwaka 2010, tutatue matatizo ya mgawanyo wa mapato ya Muungano, haijatokea. Na kama kuna sababu kubwa ya resentment juu ya Muungano ya Wanzanzibari ni hii. Sasa badala ya kutibu magonjwa hayo, badala ya kutibu matatizo hayo, tunapendekeza hivi, wawe wadeni wetu wa kudumu. Wakitaka hela za maendeleo waje tuwakopeshe. Tuwakopeshe sawa na UDA, tuwakopeshe sawa na ATCL, tuwakopeshe sawa na Halmashauri ya Wilaya ya Newala.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatengeneza utaratibu ambao utazaa matatizo makubwa zaidi ya Muungano na hatuwezi tukafanya hivi tukiwa; we can only do this if we are blind. Tunaweza tukafanya hivi kama ni vipofu, na kama hatujui lakini kama tunafahamu matatizo ya mgawanyo wa mapato ya Muungano this is not the way to go. Tafadhali sana tusitegemee nia njema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna chombo cha Kikatiba kimeundwa tangu mwaka 2003 lakini kilitungiwa sheria mwaka 1996, miaka 20 iliyopita. Tume ya Pamoja ya Fedha, chombo cha Kikatiba, hiki ndicho kinatakiwa kifanye maamuzi juu ya masuala haya; mikopo, misaada na dhamana za Serikali ya Muungano kwa fedha za Muungano kwa ajili ya mambo ya Muungano; haijawahi kufanya kazi, badala yake tunaletewa vitu kama hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali mimi sijui nisemeje, lakini naomba niwaambieni Waheshimiwa Wabunge tunatengeneza bomu, na tunalitengeneza tukiwa na macho meupe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho la mapendekezo ya Sheria ya Wanyamapori. Ni hivi, muswada huu unapendekeza kwamba mtu akituhumiwa kwa nyara ya Serikali, amekamatwa na nyamapori, kabla hajapelekwa mahakamani, kabla hajashtakiwa, hakimu atoe kibali, hiyo nyamapori iuzwe au ipikwe iliwe au iwe otherwise disposed. Halafu hakimu akishaamua kumbuka kesi haijafunguliwa, kibali cha hakimu tayari ni ushahidi kamili wa jambo litakalobishaniwa, endapo hiyo kesi itafunguliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sijawahi kuona ni mwanasheria kidogo, wanasheria waliomo humu ndani hebu nisaidieni hiyo ni ya wapi ambapo ushahidi unakubaliwa kabla kesi haijafunguliwa? Ni ya wapi hiyo? Mwanasheria Mkuu wa Serikali seriously unatuletea hii, nani atakayepona? Maana utafungwa tayari hakimu ameshakubali ushahidi, kabla mwenyewe hujashtakiwa, nani atakayepona? Kuna safeguard zipi dhidi ya watu watakaosingiziwa? Nchi hii kama hamfahamu magereza yamejaa, yamefurika kwa watu wanaosingiziwa kesi za ajabu ajabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunahalalisha mambo hayo Waheshimiwa kwa kuleta mapendekezo kama haya. Nyamapori, hakimu anasema eeh nimeshaona hii ni ushahidi tayari, kabla kesi haijafunguliwa umekwenda na maji.
Waheshimiwa Wabunge, hili si tatizo la CHADEMA, sio tatizo la UKAWA, tunawatengenezea Watanzania mazingira ambayo watakandamizwa sana, tusikubali. Tusikubali kuambiwa nia njema itawaumiza watu wetu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.