Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Lazaro Samuel Nyalandu (1 total)

MHE. LAZARO S. NYALANDU aliuliza:-
Vijiji vyote vya Tarafa ya Ilongero, Mtinko na Mgori bado vinahitaji mfumo wa usambazaji maji kutoka visima virefu vilivyopo kwenye baadhi ya vijiji na tarafa hizo tatu zinahitaji kuongezewa visima virefu na mabwawa ya kuhifadhia maji ya mvua.
Je, Serikali ina mpango gani wa kufanikisha mradi huo ili kuwaondolea adha wananchi wa Jimbo la Singida Kaskazini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lazaro Samuel Nyalandu, Mbunge wa Jimbo la Singida Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Singida inaendelea kushirikiana na washirika mbalimbali wa maendeleo katika kuhakikisha huduma ya maji inapatikana. Hadi sasa wananchi wanaopata huduma ya maji kwa Halmashauri ni asilimia 53 sawa na wakazi 130,908.
Mheshimiwa Spika, katika Tarafa ya Ilongero kuna miradi 24, Tarafa ya Mtinko kuna miradi 14 na Tarafa ya Mgori kuna miradi kumi iliyokamilika na inatoa huduma ya maji. Miradi mingi kati ya hii inatumia nguvu ya nishati ya jua kuendesha mitambo ambayo imeunganishwa moja kwa moja kwenye chanzo au kisima na kujengewa kituo kimoja cha kuchotea maji.
Mheshimiwa Spika, Halmashauri imeanza kufanya upanuzi wa miundombinu ya maji katika kijiji cha Pohama, Tarafa ya Mgori, ambao umefikia asilimia 90 ya utekelezaji. Halmashauri inaendelea kufanya usanifu wa miradi ya maji kwa ajili ya ujenzi wa mitandao ya mabomba kutoka kwenye visima katika vijiji vya Mtinko na Ghalunyangu, Tarafa ya Mtinko na Ngamu, Tarafa ya Ilongero. Aidha, ujenzi wa miradi hiyo unatarajiwa kukamilika katika mwaka wa fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji, Halmashauri imepanga kuchimba visima virefu na kujenga mitandao ya mabomba katika vijiji 11 na vijiji hivyo ni pamoja na Merya, Mughamo, Mughunga, Msange, Itaja, Mudida, Ughandi, Kijota, Mwasauya, Mtinko na Mwakiti. Pia kufanya ukarabati na upanuzi wa miradi katika Vijiji vya Msange, Ghalunyangu, Ngimu, Mdilu, Mwasauya, Pohama, Nkwae, Msisi na Sagara.