Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. CAN.RTD Ali Khamis Masoud (2 total)

MHE. KANALI (MST) MASOUD ALI KHAMIS aliuliza:-
Kwa muda mrefu sasa Serikali imekuwa ikitoa ahadi za kutatua tatizo la usafiri kwa Jeshi la Polisi bila mafanikio. Kwa mfano, Kituo cha Polisi Mfenesini, Zanzibar hakina gari la uhakika kwa takribani miaka 10 sasa:-
(a) Je, ni lini Serikali itapeleka gari Kituo cha Polisi Mfenesini?
(b) Je, ni lini magari ambayo yamekuwa yakizungumzwa kwa muda mrefu yatawasili nchini ili kuondoa adha ya usafiri?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kanali (Mst) Masoud Ali Khamis, Mbunge wa Mfenesini, lenye sehemu
(a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Polisi Mfenesini kipo Mkoa wa Kaskazini Unguja katika Wilaya ya Kipolisi Mjini Magharibi A. Mkoa wa Kaskazini Unguja una jumla ya magari 13 ambayo yanatoa huduma za doria na kazi nyingine za Polisi katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Mjini Magharibi ikiwemo Kituo cha Polisi Mfenesini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kituo cha Polisi Mfenesini kitapatiwa gari mara baada ya taratibu za upatikanaji wa magari utakapokamilika. Hata hivyo, gari la Mkuu wa Polisi wa Wilaya hutoa huduma pale inapotokea dharura ikiwa ni pamoja na kuwachukua mahabusu waliopo katika kituo hicho.
Mheshimiwa Naibu Spika, magari haya yamekuwa yakiwasili nchini awamu nchini awamu kwa awamu ambapo hadi sasa jumla ya magari 231 yamekwishawasili kati ya magari 777 yaliyokuwa yameagizwa.
MHE. KANALI (MST.) MASOUD ALI KHAMIS aliuliza:-

Serikali imekuwa ikijitahidi kujenga nyumba kwa ajili ya wapiganaji wake ili waishi kambini kama taratibu za Jeshi zinavyoelekeza:-

(a) Je, kwa nini sasa nyumba nyingi katika Kambi za Jeshi wanapewa wafanyakazi ‘Raia Jeshini’ kwa ajili ya kuishi?

(b) Je, wafanyakazi raia wana haki ya kupewa nyumba za kuishi za Askari?

(c) Je, kwa nini Askari wanaruhusiwa kuzihama nyumba zilizojengwa kwa ajili yao na kuhamia katika nyumba binafsi?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENA TAIFA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kanal (Mstaafu) Masoud Ali Khamis Mbunge wa Mfenesini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, raia wanaofanya kazi Jeshini hupewa nyumba za kuishi kwa mujibu wa Kanuni za Majeshi ya Ulinzi ya Wananchi wa Tanzania. Aidha, ugawaji wa nyumba hizo unategemea na uwezo uliopo.

(b) Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni za Majeshi ya Ulinzi ya Wananchi wa Tanzania Juzuu ya kwanza (Utawala), Ibara ya 21.30 Makazi ya waliooa kutumia Raia, Kifungu Kidogo cha Kwanza (1) kinasema, bila kuathiri maagizo yoyote yaliyotolewa na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, wakati makazi yanayofaa ya kiraia hayapatikani, Kamanda wa Kituo, Kikosi au sehemu nyingine anaweza kumgawia makazi ya waliooa raia ambaye ni Mtumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye anajaza nafasi katika Muundo wa Jeshi na ambaye si kibarua.

Hali kadhalika, Juzuu ya Kwanza (Utawala) Ibara Ndogo ya Pili inaeleza kuwa, kwa idhini ya Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Kamanda Kituo Kikosi au sehemu nyingine anaweza kumgawia makazi ya waliooa raia, mbali na yule aliyetajwa katika sehemu ya kwanza ya aya hii, wakati kazi zake ni zile ambazo zinachangia ufanisi au maslahi ya kituo, kikosi au sehemu nyingine, endapo makazi yanayofaa ya kiraia hayapatikani anaweza kupewa nyumba kuwa makazi.

(c) Mheshimiwa Spika, Maafisa au Askari wanaruhusiwa kutoka kambini au vikosini na kuhamia katika nyumba zao binafsi. Aidha, hulazimika kubaki kambini au vikosini kutokana na sababu maalum za kimajukumu.