Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Ali Salim Khamis (14 total)

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii kuweza kutoa mchango wangu. Kwanza nitangulie kwa kusema kwamba kutenda inatoka moyoni na haitoki mdomoni. Sasa nijikite katika huu Mpango na nimsaidie Kaka yangu hapa Waziri wa Fedha pengine inaweza ikasaidia ili kulivusha Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilivyoangalia katika kulinyanyua Shirika la Ndege la Air Tanzania, Waheshimiwa Wabunge Shirika la Air Tanzania ni Shirika la mwanzo Afrika Mashariki na nchi zote za Afrika Mashariki zinalitegemea shirika hili. Hatujui kilichosibu ni nini mpaka leo tumekuwa wa mwisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Shirika hili kufa, sijui hawa ambao walishiriki kulisababishia shirika hili kufa walichukuliwa hatua gani na mpaka leo hii inaonekana kwamba upo umuhimu wa kulihuisha shirika hili tena jambo ambalo mimi siamini kama tuna uwezo kwa sasa hivi kulihuisha Shirika la Ndege la Air Tanzania eti tu kwa sababu tutanunua ndege tatu siyo kweli. Ikiwa hakuna hatua ambazo tumezichukua wakati shirika limekufa, leo hii tuchukue hatua ya kulifufua shirika hili siamini mpaka sasa hivi na sijui kama Mheshimiwa Waziri wa Fedha wataalam wako wamekushauri sahihi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano, ukiangalia leo Ethiopian Airline hawakukurupuka tu kuanzisha Shirika la Ndege, walitafuta wataalam ambao ni wazoefu wa kuanzisha Mashirika ya Ndege. Ukiangalia Emirates Air hawakuanzisha tu shirika kwa sababu walikuwa na pesa, lakini walitafuta wataalam ambao wana fani ya kuanzisha mashirika ya ndege, ndiyo maana leo wamefanikiwa. Leo tunakwenda katika ushindani wa kujenga shirika la ndege, majirani zetu Ethiopia ambao tumewasaidia siku nyingi mpaka mwaka jana wana ndege 76 na wame-order ndege mpya 46 ili kulihuisha shirika zikiwemo ndege za Air Bus.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sijui manufaa ya hizi ndege ambazo zitanunuliwa na Serikali zije ziwanufaishe wananchi, imani yangu kukuomba Mheshimiwa Waziri ungerudi tena ukafanya utafiti kabla ya fedha hizi za umma hazijapotea.
Leo ukiangalia shirika hili lina madeni chungu nzima, na ikumbukwe kwamba shirika hili ni Shirika la Tanzania, ikiwemo na Zanzibar, Zanzibar imechangia asilimia kubwa ya shirika hili na ukiangalia katika takwimu ndege ambazo zilikuwa zikimiliki shirika la Air Tanzania nyingi zimenunuliwa na Serikali ya Zanzibar, lakini matokeo yake fedha hizi zote zimepotea na hakuna hatua ambazo zimechukuliwa, sasa tusitegemee kwamba shirika hili litahuika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba fedha za wananchi zisitumike kununua ndege, watu wakafanya haraka kununua ndege, watafutwe wataalam ambao wanaweza kushauri ili kuanzisha shirika litakalokuwa na tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona hapa shirika la Precision Air, tulitegemea kwamba lile shirika litakuwa ni Shirika la Tanzania japo kuwa la wazalendo, lakini matokeo yake lilipoanza kufanya kazi vizuri Kenya Airways wameanza kulimiliki hili shirika, asilimia 51 sasa hivi iko Kenya Airways badala ya Precision Air, matokeo yake ni nini? Hili shirika maana yake tena sasa haliendi kuwa Shirika la Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo namwomba Mheshimiwa Waziri ungetafuta watu ambao wana fani hii ya kuanzisha mashirika ya ndege ili zikitumika fedha za umma, zitumike kwa mantiki ambayo imekusudiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili niongelee katika masuala ya utalii. Mheshimiwa Waziri umetuletea kitabu chako hiki cha Mpango. Ukija kwenye ukurasa huu wa 14, unaelezea suala zima la utalii. Kutoka mwaka 2010 mpaka 2014, kumekuwa na ongezeko la watalii kutoka 784,709 na mpaka mwaka 2014 tumepata watalii 1,142,217, maana yake ni ongezeko la watalii 357,508 kwa muda wa miaka minne. Kwa hiyo, ukigawa hii kwa ratio ya miaka minne maana yake Tanzania tunapata watalii 89,000 kwa wastani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tujiulize vivutio vya utalii tulivyonavyo, hivyo kweli sisi tulileta watalii 89,000 kwa mwaka mzima? Hii Wizara inafanya shughuli gani, Bodi ya Utalii inafanya kazi gani. Ikiwa leo hii inaonesha pato la nchi hapa lilivyoongezeka kupitia hawa watalii, 357,000 kutoka dola milioni 1,254,600 mpaka kufikia dola 2,006,000, ni tofauti ya dola 1,880,599, hili ni ongezeko la pesa za kigeni kwa watalii 357,000. Je, Mheshimiwa Waziri hukuliona hili, kwamba hili ni eneo ambalo lingeweza kusaidia nchi yetu kuweza kupata mapato zaidi na kuweza kwenda huko tunakotaka kujitegemea katika huo uchumi wa viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia suala la bandari, Mheshimiwa Waziri bandari ndiyo uchumi nchi, Dubai, Hongkong wanafanya jeuri ya fedha kwa sababu ya bandari. Leo bandari zetu ukienda katika hii bandari ambayo unaambiwa inaimarishwa ya Dar es Salaam bado, bandari ambayo inaweka msongamano wa mizigo mpaka inakuwa watu kuchukua mizigo yao badala ya kwenda kufanya biashara wapate faida, sasa wanakula hasara kwa sababu ya mizigo inayorundikana katika bandari moja ya Dar es Salaam na kuchelewa kutoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukiangalia hiyo Reli ya Kati, imeanzia katika Bandari ya Tanga lakini Bandari ya Tanga haishughulikiwi imeachwa hivi tu na wala haimo katika Mpango. Bandari ndiyo shingo na roho ya uchumi wa nchi, leo inaachwa Bandari ya Tanga inakufa na Bandari ya Mtwara tunaenda kujenga Bandari ya Bagamoyo. Hivi tutegemee kweli huu uchumi wa viwanda utakua na wakati bandari ya Tanga ina miundombinu ya reli kutoka bandarini kwenda sehemu nyingine, leo tumeua kila kitu!
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sijui, napata mashaka kwamba kweli tunaweza kufanikiwa kwenda katika uchumi wa kati kupitia viwanda ambavyo tunategemea kwamba viwe mkombozi wa nchi hii. Nina imani kama kweli unajenga ile dhana ya kiuchumi, basi naomba ufahamu kwamba bandari ndiyo uti wa mgongo wa nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la uvuvi, miaka iliyopita michache tu, Mheshimiwa Rais wa sasa alikuwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, alikamata meli hapa, meli ile ilikamatwa ina samaki wa bahari watupu, baada ya kuwakamata hao watu na meli kukamatwa kupelekwa Mahakamani haikuonekana kwamba kuna umuhimu, kwa kuwa bahari yetu ina samaki wa kutosha, sasa tuwekeze katika uvuvi ili pato la nchi yetu liongezeke. Ndiyo maana nimetangulia kusema kwanza kwamba kutenda inatoka moyoni siyo kwa mdomo, sasa ikiwa hali hii tutakwenda nayo hivi, tutazungumza haya leo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nimesafiri nimepitia uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam kulikuwa na mvua, uwanja wa International Airport unavuja, sijui kama Waziri mhusika kama ameenda kutembelea pale, nenda ushuke pale eneo la abiria mtu anashuka kwenye ndege ya Emirates au Etihad, ama Qatar eneo la kushukia abiria hakuna feni, hakuna air condition, watu wanatoka majasho sasa ni impression gani ambayo unampa mgeni anaingia ndani ya nchi yako, anakuona wewe ni mtu wa aina gani? Hii ndiyo taswira ambayo tunawapa watu wanaoingia hapa kwamba hawa watu wenyewe ni wa hovyo hovyo tu, kila kitu chao wameweka hovyo hovyo tu, lazima wewe atakudharau mwanzo tu anapofika akiona hali kama ile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo International Airport inavuja, wageni wanafika pale airport, maana yake ingekuwa angalau kuna mafuriko, uwanja umejaa maji sawa, Lakini leo mvua ya kawaida tu uwanja unavuja! Sijui kama Waziri amewahi kwenda kwenye eneo la abiria wanaposhuka kwenye uwanja wa ndege, kutoka katika safari zao nchi za nje ili aende akashuhudie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia na kunipa afya njema na niwatakie Waislam wote duniani Ramadhan Kareem. Pia niwape pole wale wote ambao wamepatwa na maafa, ajali iliyotokea kule Karatu Arusha na wale wote waliopata majanga ya mafuriko hasa Visiwa vya Zanzibar ambapo pia kulitokea upepo mkali ulioezua majumba zaidi ya 70 na mvua ambazo zilisababisha maafa makubwa na majumba mengi kuharibika kutokana na mafuriko hayo ya mvua. Kwa hiyo, nawapa pole wote ambao wamefikwa na maafa haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuomba utumie busara yako ya kiti kama vile ambavyo tuliwafariji hawa ambao walipatwa na tetemeko kule Bukoba na watoto wetu kule Karatu tukajitolea Wabunge ile posho yetu ya siku moja basi ningeomba busara yako itumike ili siku hii ya leo basi ichangie maafa ambayo yametokea kule Zanzibar, ukilinganisha sasa hivi kuna maradhi ya mlipuko ya kipindupindu, ningeomba busara yako ya Kiti itumike ili kuweza kudumisha muungano wetu Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza hayo, leo nataka nijikite katika jambo moja tu ambalo linahusiana na hii Tume ya Pamoja ya Jamhuri ya Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza kwanza Tume hii ya Pamoja, ipo kikatiba, tokea mwaka 1977 jambo hili liliridhiwa katika Katiba yetu lakini kwa masikitiko makubwa tokea 1977 jambo hili lilipopitishwa katika Katiba yetu limekuja kutungiwa sheria mwaka 1996, miaka 19 baadaye. Kama hiyo haitoshi, jambo hili baada ya kupitishiwa sheria kuundwa kwa Tume yenyewe imekuja kuundwa mwaka 2003 miaka saba baadaye, baada ya kupitishwa sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli ni jambo la masikitiko na ni jambo la aibu kwamba leo tumeunganisha nchi zetu hizi kwa ajili ya mustakabali wa vizazi vyetu na jamii zetu kutokana na nchi zetu hizi ambazo zimeungana. Ukija katika masuala ya Muungano, yameelezwa katika Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano na naomba leo niyasome ili kuweka Hansard vizuri, inaonekana pengine baadhi ya watu hatuna uelewa wa haya mambo ya Muungano, lakini ukiisoma Katiba hii ya Jamhuri ya Muungano mambo haya 22 inaonesha wazi kwamba mambo yote katika nchi hii ni ya Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mambo haya ya muungano, ni Katiba ya Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Muungano, pili ni mambo ya nchi za nje, ulinzi na usalama, Polisi, mamlaka ya mambo yanayohusiana na hali ya hatari, uraia, uhamiaji, mikopo na biashara ya nchi za nje, utumishi katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano, kodi ya mapato inayolipwa na watu binafsi na mashirika, ushuru wa forodha na ushuru wa bidhaa zinazotengenezwa nchini Tanzania unaosimamiwa na idara ya forodha, bandari, mambo yanayohusiana na usafirishaji wa anga, posta na simu, mambo yote yanayohusiana na sarafu na fedha, leseni ya viwanda na takwimu, elimu ya juu, maliasili ya mafuta pamoja na mafuta yasiyochujwa na motokaa na mafuta ya aina ya petrol, Baraza la Taifa la Mitihani ya Tanzania, usafiri na usafirishaji wa anga, utafiti, utabiri wa hali ya hewa, takwimu, Mahakama ya Rufaa, uandikishaji wa vyama vya siasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiyataja maeneo haya yote ukizungumzia ukusanyaji wa kodi ni jambo la Muungano, kwa hiyo kodi zote zinazokusanywa hapa ndani ya nchi hii ni mambo ya muungano. Leo kuna tozo mbalimbali zinazotozwa ambazo hizi si za kodi zimeainishwa pia katika taasisi mbalimbali. Kwa mfano, Ofisi ya Rais ni ya Muungano lakini yenyewe inakusanya tozo ambazo hizi zinatakiwa zije katika Mfuko wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sababu hii ni sehemu ya ofisi ya Muungano, lakini Msajili wa Vyama vya Siasa, Mahakama ya Rufaa kama ilivyotajwa huku lakini kuna mashirika mbalimbali, mashirika ya ndege na kadhalika, mpaka leo hii mwongozo umetoka kwamba iwekwe akaunti ya pamoja kati ya nchi hizi mbili ili kutunza haya mapato ya Jamhuri ya Muungano na kuzinufaisha hizi nchi mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi leo miaka 40 umri wa mtu mzima, zimeundwa Tume chungu nzima. Ukiangalia utafiti huu ambao umefanywa na Tume ya Katiba kuna tume zimeundwa zaidi ya 11 humu ndani ya book hili ambalo limetolewa kuna Tume ya Mark Bomani, na Tume ya Shellukindo na wengine ambao imeelezea jinsi ya kuifanya Tanzania iondokane na hizi kero za Muungano. Hata hivyo, mpaka leo hii cha ajabu na cha kusikitisha suala hili halijapatiwa ufumbuzi miaka 40, halafu tunaambiwa kwamba Serikali hii ni Serikali sikivu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Serikali hii kumbe yale ambayo yametokea kwa nchi hii kwa ajili ya mchanga wa madini kwamba, nchi hii imedhulumiwa na wawekezaji hakuna tofauti na dhuluma ambayo Zanzibar imefanyiwa muda wote huu wa makusanyo ya Muungano hayakuwekwa katika sehemu ya Muungano ili kunufaisha hizi nchi mbili, hakuna tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukiangalia kwa ratio ya asilimia 21 katika mgao katika mambo ya muungano, ukiangalia hii trilioni 1.4 ambayo ameitaja Rais, siku ile Tume ilivyowasilisha taarifa yake, Zanzibar tulitakiwa tupate karibu bilioni 66. Sasa ina maana sio ninyi tu mnaoathirika pia Zanzibar nayo inaathirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana tulivyokwenda kwenye uchaguzi mwaka 2015 tulisema kwamba, Zanzibar hii itajitegemea kwa uchumi wa huduma na hii Tanganyika ina rasilimali, madini, kilimo na kadhalika. Leo ukiangalia nchi kama Malaysia imestawi katika uchumi kwa sababu ya Singapore. Singapore haina resource ya aina yoyote lakini imewekeza katika huduma, leo Malaysia inanufaika kupitia Singapore. Sasa sisi tunakwenda wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu liangalieni hili, ikiwa jambo hili halitapatiwa ufumbuzi wa haraka basi inaonesha wazi kwamba wenzetu wa Tanganyika hamko tayari kulipatia ufumbuzi jambo hili na inabidi sasa tukazungumze lugha nyingine kule kwetu kwa ajili ya kuwaambia Wazanzibari Muungano huu imetosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya njema nami kupata fursa hii kuchangia katika bajeti hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita katika mambo manne ambayo zaidi ya haya yatakuwa yanahusiana na mambo yale ya Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 133 inaeleza kwamba kunatakiwa kuwe na Kamati ya Pamoja ya Fedha ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia katika Ibara ya 134 ikaeleza majukumu ya Kamati hiyo, lakini pia kulitakiwa kuwe na Akaunti ya Pamoja ya Fedha baina ya Zanzibar na Tanganyika ili kuweza kuthibitisha mapato ya Muungano katika Akaunti hiyo ya Pamoja ya Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukichukua Katiba hii mwaka 1977, mpaka leo hii ni miaka 40 sasa hivi na hii imepelekea Zanzibar kukosa fursa zote za kufanya maendeleo ya visiwa vya Zanzibar kwa sababu ya tatizo hili la kutokupatikana account ya pamoja, kuweza kuyajua mapato halisi ya Muungano na mgao halisi kwa nchi mbili hizi. Sasa namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atuambie kwamba sasa ni lini Akaunti hii itafunguliwa kwa ajili ya kuweka mapato yote ya Muungano ili upatikane mgao sahihi kwa ajili ya nchi hizi mbili? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kuchangia hapa katika Wizara ya Fedha kusema kwamba ukiangalia Katiba hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaonesha mambo yote ni ya Muungano. Leo ukimwangalia Mheshimiwa Waziri wa Ardhi na Nyumba, anaitwa ni Waziri Waziri wa Ardhi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; lakini ukija huku ndani tunawatafsiria watu tunasema kwamba ardhi siyo mambo ya Muungano, jambo ambalo Katiba hii ya Jamhuri ya Muungano inakataa inasema kwamba yule ni Waziri wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, ina maana mapato na ukiangalia kwamba kodi ya Mashirika, watu binafsi, ushuru wa forodha; haya yote ni mambo ya Muungano. Kwa hiyo, ukitazama kwamba kodi hizi zinapokusanywa kabla hazijaanza kutumiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano inakua ni mapato ya Jamhuri ya Muungano baina ya Tanganyika na Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa muda wote huu, imepelekea kulifanya Taifa la Zanzibar kuwa Taifa dhoofu, kuwa Taifa ambalo halijui mustakabali wake katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa leo atuambie sasa ni lini Akaunti hii inafunguliwa kwa ajili ya kudumisha mustakabali wa nchi hizi mbili?

TAARIFA . . .

MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nafikiri Mheshimiwa hajaisoma Katiba vizuri. Katika Muungano huu mwanzo kulikuwa hakuna kitu kinaitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kulikuwa na nchi ikiitwa Zanzibar ambayo mpaka leo inaitwa Zanzibar na nchi ambayo inaitwa Tanganyika. Tanganyika na Zanzibar ndiyo zimefanya kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Sasa leo akitoa taarifa hiyo nitamshangaa sana. Kwa hiyo, naomba niendelee na mchango wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa, atueleleze hii akaunti ambayo imesemwa kwamba lazima kuwe na akaunti itakayothibitisha mapato ya Jamhuri ya Muungano. Kwa hiyo, tuambiwe ni lini akaunti hii itaanzishwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wa Visiwa ni tofauti na uchumi wa nchi ya Bara kama Tanganyika. Uchumi wa Visiwa siku zote ni uchumi wa huduma. Leo naomba nitoe mfano. Tuchukulie mfano wa nchi ya Singapore; Singapore ni Kisiwa kidogo, yaani kisiwa cha Unguja ni karibu mara mbili ya Singapore. Kisiwa hiki hakina resources za aina yoyote, isipokuwa wao wanatumia bandari na huduma ambazo wanatoa kwa Taasisi mbalimbali za kibiashara na kifedha duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo imekuwa kwamba Singapore, unapotaka huduma ya aina yoyote ya kifedha ama ya kibiashara unaipata Singapore. Ukiangalia leo Singapore wamewekeza katika bandari tu ya Singapore peke yake kwa siku inapokea makontena 91,000 ambayo ni sawa sawa na meli 60 zinazofunga kwa siku Singapore; na Kijiji chenyewe ni kidogo. Kama hiyo haitoshi, Singapore leo ndio wenye destination kubwa ya utalii. Meli zote za Kitalii ambazo zinakwenda katika sehemu mbalimbali duniani zinaanza safari zake kutoka Singapore.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu wa 2017 Singapore imefanya location ya meli za kitalii kwenda sehemu mbalimbali duniani 63. Crew Ship ambapo katika meli hizi watalii wanatoka Australia, Marekani, Ulaya na sehemu nyingine duniani wanakwenda Singapore. Wakifika Singapore wanapanda meli wanakwenda kwenye utalii wao, wakirudi wanarudi Singapore wanachukua ndege wanarudi makwao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa leo cha ajabu, nashangaa, Mheshimiwa Waziri wa Utalii hapa kwetu, anashindwaje kuitumia fursa ya Zanzibar pamoja na Mbuga ama vivutio vya kiutalii vilivyopo Tanzania kuweza kuihuisha nchi hii kiuchumi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukiangalia Tanzania imekuwa maskini kwa sababu imeinyima fursa tu Zanzibar. Wakati aliyekuwa Waziri Mkuu wa Malaysia Dkt. Abdallah Mahadhir naye pia alikuwa na nia kama ambayo aliifanya Baba wa Taifa, kuifanya Singapore na Malaysia iwe ni nchi mmoja. Singapore wakakataa wakasema sisi tunataka tujiendeshe wenyewe na matokeo yake leo Singapore kwa kujiendesha wenyewe na kujitegemea imechochea maendeleo katika nchi ya Malaysia kwa haraka sana. Leo Malaysia ni miongoni mwa nchi ambazo zinakuwa kiuchumi kwa…

TAARIFA . . .

HE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unilindie muda wangu tafadhali. Inaonekana Mheshimiwa Keissy alikuwa hajasikia nazungumza nini, kwa sababu mwanzo nilinukuu hii Katiba. Hii Katiba ya Jamhuri ya Muungano, inasema kwamba Waziri wa Utalii ni Waziri wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Sasa sijui yeye anavyosema anafuata Katiba ipi? Kwa hiyo, inaonekana hata yeye mwenyewe hafahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Singapore imechochea ukuaji wa kiuchumi wa nchi ya Malaysia na leo kila mtu anafananisha kwa kusema kwamba Malaysia inaendelea kiuchumi kwa haraka zaidi. Hii ni kutokana na Kisiwa cha Singapore kuweka uchumi wa huduma na kuiacha Malaysia iweze kujiendesha katika uchumi wa mazao na kibishara kupitia Singapore.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunampongeza Mheshimiwa Rais kwamba amefanya kazi nzuri ya kusimamia rasilimali za nchi hii ili watu ambao walikuwa wanazipora, sasa nchi hii iweze kunufaika. Nachukua fursa hii kumwomba Mheshimiwa Rais kwamba kama ambavyo amechukua juhudi kwa ajili ya kuzuia makinikia, sasa umefika wakati sasa wa kupata suluhisho katika Muungano wetu. Mwisho hapa Mheshimiwa Waziri wa Fedha alitujibu kwenye bajeti yake kwamba jambo hili bado lipo kwenye mazungumzo baina ya nchi mbili hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ikiwa leo tumeungana na sisi tunasema ni ndugu, miaka 40 hatujapata maelewano ya nchi hii kupata Akaunti ya Fedha ya Pamoja ya Jamhuri ya Muungano? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona sasa ifike mahali, kama ambavyo mmekubali kwamba mlifanya makosa katika mikataba ya madini, basi na hapa mkubali kwamba mliwakosea Wazanzibari na sasa tunaelekea katika mwanzo mpya kwa ajili ya kutafuta mustakabali wa Muungano wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ilikuja mifano mbalimbali. Mheshimiwa Rais Mstaafu alipendekeza, aliunda Kamati ya kutengeneza Katiba mpya; na tuliamini kwamba alikuwa na nia njema na Kamati hii ikafanya kazi ya Jaji Warioba, matokeo yake ilipokuja hapa Bungeni kwa sababu ile nia na dhamira ilikuwa bado, Katiba ile imekataliwa na matokeo yake watu wakatayarisha Katiba nyingine pendekezwa ambapo yale maoni ya wananchi yakakataliwa na yakatupwa pembeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, alivyotokea Mheshimiwa Warioba, kutaka kutoa maelezo ya mambo yalivyokwenda, kilichofanyika, alitumiwa watu wa kwenda kumvamia na asitoe ule uhalisia wa mambo. Leo hii watu wale wale wameonekana ni watukufu, wametukuzwa kwa ajili ya kuonekana ni watu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii ya kuchangia. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema na leo hii kuweza kupata fursa ya kuweza kuchangia katika Bajeti hii ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nilikuwa na maswali zaidi kwa Mheshimiwa Waziri ili atakapokuja hapa aweze kutupa ufafanuzi. Kwanza ukiangalia kitabu cha Waziri cha mwaka 2017/2018 kinasema kwamba Waziri aliomba bilioni 500 kwa ajili ya ununuzi wa ndege tatu za Bombardier; Q400, tatu; pamoja na CS300, mbili; na ndege kubwa ya 787.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika Mpango ambao tumewasilishiwa Machi mwaka huu na Waziri wa Fedha pia anasema kwamba amelipa bilioni 7.8 kwa ajili ya kutekeleza mkataba wa ununuzi wa ndege, lakini pia ameomba bilioni 495.6 kwa ajili ya kukamilisha malipo ya ndege mbili za CS300 kwa malipo ya asilimia 30 na ndege kubwa ya 787 kwa malipo ya asilimia 52.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mwaka jana amesema Waziri kwamba ameomba hizi fedha kwa ajili ya kufanya malipo ya ndege hizi, lakini mwaka huu huu tena ameomba tena karibu bilioni zile zile 500 anaenda kulipia tena ndege hizi hizi ambazo ziliombewa fedha wakati ule. Sasa namwomba Waziri atakapokuja hapa atufafanulie ni ndege zipi nyingine ambazo zinazoenda kulipiwa na kule mwanzo katika kitabu cha mwaka 2017/2018 hakueleza kwamba analipia asilimia 30 ya hizi ndege mbili CS300. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadaye Waziri wa Fedha amesema kwamba ameomba fedha kwa ajili ya kulipia tena ndege ya Bombardier Q400, sasa naomba Waziri kujua haya maelezo ambayo ameyatoa Waziri wa Fedha je, kuna Q400 nyingine ya nne ama ni zile zile tatu za nyuma ambazo zilinunuliwa hapo kabla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kusisitiza mwaka juzi na mwaka jana tulitoa ushauri hapa kwa Waziri kwamba hakuna anayekataa shirika la ndege kuanzishwa ili lilete tija katika Taifa letu, lakini tulisema kwamba biashara ya ndege ni biashara ya ushindani na tunahitaji wataalam wa biashara za ndege wapewe shirika hili ili waweze kulianzisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kwa haraka haraka limeanzishwa shirika lakini hadi hivi leo Kamati hapa imesema kwamba shirika hili limeshindwa kuungwa katika hii Taasisi ya Mashirika ya Ndege ya IATA ili kuweza kujiendesha shirika hili na badala yake tunatafuta kampuni nyingine ili ifanye kazi hii kwa niaba yetu ambayo ina uwezo wa kufanya kazi na IATA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii inaonesha wazi kwamba yale tuliyokuwa tunayasema ndiyo ambayo yanayojitokeza sasa hivi. Ukiangalia ripoti hii ya CAG. CAG anasema kwamba ununuzi wa ndege umekiuka taratibu za manunuzi. Hatusemi hivi kwamba tunaipinga Serikali, sio kwa sababu ya kuipinga Serikali lakini tunaisaidia Serikali ifanye kazi zake na iwe ni tija kwa wananchi; lakini leo shirika hili linakwenda kuwa mzigo kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikupe mfano mmoja, kabla shirika hili halijarejeshwa hapa kuwa marehemu na South African Airways yalijitokeza mashirika matatu kulifufua hili shirika. Shirika la kwanza ni British Airways pamoja na Emirates na la tatu ni hili South Africa. British Airways walikuwa na lengo la kuifanya Air Tanzania iwe ndiyo kama career yao kwa East Africa pamoja na Africa kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Emirate walitoa offer kwa Air Tanzania kwamba wakipewa hili shirika wakilitumia kwa ajili ya East Africa hii liweze kufanya kazi kupitia Emirate kwa pamoja, pamoja na shirika la Emirate wangefanya matengenezo ya viwanja vyote vya ndege ambavyo leo tunavipigia kelele hapa ndani ya nchi yetu. Hata hivyo, kwa bahati mbaya sana kutokana na kwamba hatuna viongozi ambao wanauzalendo na nchi hii wakatanguliza maslahi yao binafsi na British Airways na Emirates wakajiondoa na shirika likachukuliwa na South African Airways likarudi hapa shirika likawa marehemu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Emirates kukosana na Air Tanzania walikwenda kuingia makubaliano na shirika la Srilanka na wakafanya nao kazi kwa muda mrefu na wakawajengea kiwanja cha ndege cha kimataifa chenye shape kama ile ambayo imetengenezwa Dubai International Airport. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa leo tunapozungumza utaratibu kwa sababu jambo lolote bila ya sera na utaratibu maalum Serikali haiwezi kufanya biashara ya ndege. Leo tuangalie Shirika la Air Rwanda, Serikali hiyo ilijitwika kifua kulichukua shirika wakawa wanaliendesha. Sasa hivi wanatafuta wawekezaji waliendeshe kwa sababu Serikali imeshaona kwamba ina mzigo mkubwa wa kulihudumia shirika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimwombe Mheshimiwa Waziri tunayasema haya kwa maslahi ya Taifa la Tanzania. Tuliposema kwamba waje wataalam, mtaalam unapompa kazi anaangalia mpaka liability ya taasisi husika.

Kwani kulikuwa na ulazima lazima tuseme hii inaitwa ATCL. Leo hapa tukiangalia Emirates kuna mashirika matatu sasa hivi, kuna Emirates yenyewe, kuna Fly Dubai kuna Etihad.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yote yanafanya kazi na mashirika yote matatu haya yanakuja hapa Tanzania, yanafanya kazi zake yote matatu kila siku na yanafanya kazi kwa mafanikio makubwa. Sasa na sisi ilikuwa lazima tukae tutafakari ili kumsaidia Rais wa nchi hii aweze kufikia yale malengo ambayo anayakusudia, lakini naona sasa kwamba upande wa Mawaziri wanamwangusha Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu ikiwa Rais alikuwa na nia ambayo ya kuonesha kabisa kunyanyua uchumi kupitia shirika la ndege lakini leo badala ya kufuata zile taratibu za kuonyesha kwamba shirika hili lingeweza kuleta tija na maslahi kwa Watanzania matokeo yake linakwenda kuwa mzigo. Hapa leo ukiangalia kwenye kitabu hiki hapa cha Waziri ambacho amekitoa tulisema hapa kwamba unapochukua career tofauti za ndege lazima na base ya matengenezo zinakuwa tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana leo Waziri kakubali maneno yangu na ndiyo maana kaingia mkataba na Ethiopian Airline kuzifanyia service ndege hizi za Air Tanzania. Tuliyasema haya katika Bajeti ambayo ilipita kuonesha kwamba lazima kutakuwa na cost za kuendesha shirika, sasa leo kwa sababu hatuwezi kujiendesha wenyewe ilibidi tutafute sasa shirika lingine liweze kutusaidia katika kufanyia maintenance ndege hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimwombe Waziri hii nchi ni yetu sote, tukiharibikiwa tumeharibikiwa sote. Sasa wasianze kulitoboa jahazi halafu tuzame sote. Ikiwa kuna uwezekano wa kuweka kalavati, tuweke hilo kalavati ili tusizame tufike safari yetu; lakini haiwezekani kwenda katika namna hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ukija katika suala la reli ya kati. Mheshimiwa Rais alimwomba aliyekuwa Rais wa South Africa, Jacob Zuma kwamba atusaidie kujenga reli ya kati, lakini haikuwezekana. Hata hivyo, tukapata bahati nyingine akaja Rais wa Uturuki na Rais akamweleza nia ya kujenga reli ya kati kwa standard gauge na Rais wa Uturuki alikubali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa tunapata mkanganyiko, tunasema Rais alivyomaliza kuzungumza na Rais wa Uturuki anasema tumefanikiwa tumezungumza na Serikali ya Uturuki, tumeweza kupata reli ya kati ya standard gauge, lakini huku tunaambiwa kwamba fedha ambazo zinatumika kujenga hii reli ni fedha za ndani. Sasa part yao hao Waturuki ni ipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba akija hapa Waziri atueleze inakuwaje kwa sababu inawezekana pengine watu wakawa hawana uelewa wa kutosha halafu taarifa zikatoka vingine. Hebu leo waje watueleze hapa… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka ajibu maswali.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia kuwa katika hali ya afya njema. Na mimi naomba nitumie fursa hii kuchangia katika Wizara hii ya Mawasiliano na Uchukuzi. Kwanza ningependa ninukuu Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano katika nyongeza ya kwanza katika masuala ya Muungano.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Katiba yetu kwenye mambo ya Muungano mojawapo ni bandari. Sasa, bandari ni uchumi wa nchi, na mpaka leo hii toka Muungano huu tulipoungana miaka 53 bado suala hili liko katika masuala ya Muungano ambayo Zanzibar wameonesha wazi kuwa wanao uwezo wa kuisimamia bandari na kuweza kujitegemea kupitia bandari yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hadi leo hii bado suala hili limewekwa katika masuala ya Muungano na inapelekea kuizua Zanzibar kuwa na ile free port kujenga port kubwa pale ambayo iweze kusaidia kupokea mizigo inayotoka Kusini kufika Zanzibar na ile ya Kaskazini kufika Zanzibar wakagawana mizigo ile badala ya kusafiri umbali mrefu katika kusambaza mizigo katika hili eneo la Afrika Mashariki. Sasa nimuombe Waziri, iko haja sasa wakatafakari kutumia ile Ibara ya 98(b) kuletwa mswada hapa ili suala la bandari hili lisiwe tena la Muungano na liachiwe Zanzibar iweze kujitegemea ili kuendesha bandari yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni suala la Posta na Simu, hili pia ni jambo la Muungano. Tangu ilipovunjika Jumuiya ya Afrika Mashariki mwaka 1979 lilianzishwa hili shirika, lakini mpaka sasa hivi Zanzibar hatujaona faida yake ni ipi. Kwa hiyo, namuomba Waziri atakapokuja hapa kuhitimisha hoja hii basi atuambie, at least hii miaka kumi ya Rais aliyestaafu Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete kuambiwa TTCL imetengeneza kiasi gani na mgao wa Zanzibar ni kiasi gani, wametupa kiasi gani na bado kiasi gani tunawadai ili tujue, kwa sababu hii ni kama mali ambayo tumempa mtu anatukamatia, lakini hatujui hesabu, hatujui kitu chochote. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atupe ufafanuzi wa jambo hili la Posta na Simu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu ni suala la anga. Taasisi hii inakusanya makusanyo mbalimbali kwa ajili ya nchi yetu. Lakini bado mpaka sasa hivi masuala hayo hayapo wazi, namuomba Waziri atakapokuja hapa atuambie miaka hii kumi ya Rais Mstaafu, Idara hii imekusanya kiasi gani na imetoa mgao wake kwa Zanzibar kiasi gani, na kiasi gani tunawadai kwa sasa ambacho hawajalipa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la nne ni suala la ndege. Mwaka wa jana hapa nilitoa ushauri katika Wizara hii, kwamba ni kweli tunahitaji Shirika la Ndege na hili wala hakuna mtu analipinga, lakini nikatoa ushauri kwamba tutafute mtaalamu wa masuala ya ndege, biashara za ndege ili huyu atuongoze kuonesha tuanzishe shirika kwa namna gani. Mfano, leo Shirika la ATCL tulipotoa ushauri Serikali imekimbilia kwenda kununua ndege haraka haraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, matokeo yake tumenunua ndege ya Bombardier ambayo hii ni Kampuni ya Canada, lazima wa Canada walete base yao hapa kwa ajili ya kuzifanyia mantainance hizi ndege. Lakini miezi saba baadaye tumeingia mkataba na Boeing ambao nao inabidi walete base yao kwa ajili ya kuifanyia mantainance ndege hizi za Boeing ambazo zitakuwepo hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, shirika kubwa kama hili Ethiopian Airline kwa miaka sabini zimekuwa zikifanya kazi ya biashara ya ndege kwa kutumia kampuni moja tu ya Boeing, kuanzia sasa hivi sasa baada ya kuona kwamba wameshakuwa sustain ndipo wameanza kuingia mkataba na kampuni ya Air Bus kwa ajili ya kuongeza huduma zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hapa lengo la kuanzisha Air Tanzania ni biashara, lakini mpaka leo biashara hii ipo Serikalini haiwezi kuendelea. Biashara ukiichanganya kwenye Serikali haiwezi kuendelea. Lazima Shirika la Ndege la Air Tanzania liwe independent ndipo liweze kuendeshwa kwa faida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano; leo kuna Shirika hapa la TPDC. TPDC inafanya kazi sasa hivi lakini hili Shirika linaendeshwa kwa hasara, kwa sababu ina fedha na kodi ambazo Serikali imeziweka inalipwa na TPDC ambazo ukiuliza hizi pesa zinalipwa kwa sababu zipi haijulikani. Mwisho wa siku ikija kuombwa bajeti zao hapa ile bajeti ambayo wameomba wao kufanya kazi zao za kawaida tu hawapati, lakini wao wameshazalisha fedha na fedha zimepelekwa Serikalini, halafu Serikali inawarudia TPDC wanaambiwa kwamba waweze kujiendesha wao wenyewe. Hatuwezi kuendesha biashara namna hii.

Mhsimiwa Naibu Spika, sasa inaonekana kwamba wataalam wetu ambao wanatushauri, wanatushauri ambavyo visivyo. Sasa Mheshimiwa, Shirika hili la Air Tanzania toka lilivyoanzishwa, amesema hapa Mheshimiwa Silinde kwamba Mwalimu Nyerere alituachia ndege 11 lakini leo inaonekana ndege hizi sita imekuwa jambo la ajabu. Ndege 11 zilikuwa zinafanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa shirika hili toka lilipoanzishwa linatua katika viwanja vyetu kule Zanzibar, lakini halilipi kodi hili shirika, sasa kwa nini lisilipe kodi mpaka leo hii, hapa mwaka wa jana nilimuuliza Mheshimiwa Waziri hapa akajibu swali langu akasema kwamba kuna deni la milioni 230 linahakikiwa na CAG halafu tutalipa. Juzi ninamuuliza hapa anasema hata hajui kama zimelipwa. Sasa sijui huyo CAG mpaka leo hajamaliza wakati CAG ameshawasilisha ripoti zake mara mbili hapa Bungeni hakuna hili jambo. Sasa tuambiwe kwamba ni lini Air Tanzania (ATCL) italipa deni lake la landing fees kwa Mamlaka ya Viwanda vya Ndege ya Zanzibar na tupewe deni lile halisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jana alisema Bhagwanji hapa sisi sote ni ndugu moja, sasa kwa nini mnatuzamisha sisi tusipate kuendelea na hili jambo mmelifanya kama liwe la Muungano? Sisi hatujakataa kwamba liwe la Muungano lakini sasa hivi imeonyesha kamba mashirika haya kwamba sisi tunachangia lakini hatufaidiki nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwamba Wizara ya Muungano ilivyokuja hapa imetoa ratio ya asilimia 21 kwa
79. Nimuombe Mheshimiwa Waziri sasa, shirika limeanza kufanya kazi naomba sasa kila baada ya muda patolewe takwimu kuhusu Shirika hili kama tumepata faida au tumekula hasara ili tujue Zanzibar mgao wao ukoje. Kama mgao wetu ni hasara tushaijua hasara, lakini kama kuna faida basi tushee faida kupitia Shirika la Ndege la ATCL.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo biashara ya Ndege imekuwa ni ya ushindani mkubwa. Shirika letu hili tulilibinafsisha kwa Shirika la Ndege la South African Airways. Na tulipowapa South Africa tumewapa na zile route zetu ambazo sisi tulikuwa tunakwenda. Leo tumeshanunua ndege ya 787 Dreamliner kwa ajili ya kwenda nchi za mbali. Lakini namuomba Waziri atuambie hizi route ambao itakwenda hii ndege atakapokuja hapa atuambie kwamba ndege yetu tuliyonunua mpya kubwa itakwenda kwenye route hizi huko Ulaya na Marekani anaposema. Kwa sababu ninavyofahamu kupata route kwenda Ulaya na Marekani si jambo rahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano tu Kenya Airways leo wana route mbili kutoka Nairobi kwenda London, lakini kwa sasa hivi kwa Shirika lao limetetereka kidogo katika maswala ya kiuendeshaji na Oman Air wao wana route moja kutoka Muscat kwenda London, matokeo yake sasa Oman Air wametafuta hii route kwa muda mrefu ili wawe na route mbili kutoka Muscat kwenda Heathrow lakini wamekosa, wamerudi kwa Kenya Airways wamekwenda kununua ile route.

Mheshimiwa Naibu Spika, route hii wamenunua kwa 20 million USD, tena kwa masharti ambayo Kenya Airways imewambia kwamba tunakupeni hii route tunakuuzieni lakini pia ndege yetu moja kubwa lazima muitumie kwa ajili ya kufanya kazi, yaani waikodi Oman Air; na wamekubali kulipa 20 million USD kwa sababu ya route moja tu kutua Heathrow. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nimuombe Mheshimiwa Waziri atuambie kwamba ni route zipi ambazo ndege hii itakwenda ambazo zipo available, kwa sababu tayari route tulishamuuzia South African Airline akaua Shirika letu yeye wakaendelea na shirika lao na sasa hivi wanapata maendeleo makubwa kupitia ATCL ambayo ilikuwepo?

Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli wa mambo ni kwamba kama Serikali haitotafakari basi tunaweza tukajikuta kwamba lengo la kuanzisha hii ndege kwamba itupe faida matokeo yake ikawa ni mzigo kwa Taifa letu.
Mheshimiwa Naibu Spika, zamani British Airways ilikuwa inakuja hapa Tanzania, Dar es Salaam lakini imesitisha safari za kuja Dar es Salaam, kwa nini, kwa sababu ya ushindani wa kibiashara na kwamba leo Emirates ana ndege nne ambazo zinakwenda Uingereza kila siku, kwa hiyo route ile ndiyo ambayo abiria wanaitumia na British Airways imejikuta kwamba imekosa abiria wa kutosha kuweza kuitoa ndege Londan kuleta hapa. Kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Waziri aliangalie hili sana kwa sababu hapa lengo na madhumuni ni kwa ajili ya kujiendesha kiuchumi ili Taifa letu liweze kufunguka na kutoka kwenye umaskini.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru Mheshimiwa Naibu Spika.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar ni visiwa; uchumi wake ni wa huduma kwa ajili ya kusaidia Tanganyika ili iweze kuendelea. Mfano mzuri ni Singapore na Malaysia. Leo Malaysia inakua kiuchumi kwa haraka sana. Gruiz au Meli za kitalii, leo zinaondokea Singapore. Kwa hiyo, watalii wote wanataka kusafiri na meli za kitalii wanakwenda Singapore ndiyo waanze safari yao. Singapore ndiyo nchi ya kwanza iliyorusha Air Bus 380 kutoka Singapore kwenda Australia kwa mafanikio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kisiwa cha Penang kinachangia Malaysia kiuchumi kwa asilimia 60. Sasa wakati umefika wa kuiachia Zanzibar itekeleze uchumi wa huduma na baadaye kuisaidia Tanganyika kujitegemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Account ya Pamoja ni lazima ifunguliwe na ianze kazi na mgawo wa mapato ya Muungano yawekwe wazi kila nchi ipate haki yake. Kuendelea kulipuuza jambo hili litaleta madhara makubwa katika Muungano.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu kunijalia leo hii kusimama hapa kwa ajili ya kuchangia bajeti hii. Leo mimi nitakuwa zaidi na maswali na nina mambo matatu tu ya kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimuulize Waziri wa Fedha, makusanyo yote ambayo yamekusanywa ndani ya nchi ni shilingi trilioni 21, matumizi yake ni shilingi trilioni 21, wapi imewahi kutokea makusanyo yaliyokusanywa na matumizi yakaenda sawasawa? Yaani hata shilingi haibaki, 21 trillion mmekusanya, 21 trillion mmetumia. Hebu mtuambie ninyi wachumi na watu wa bajeti hii imekaaje? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili ni kwamba ukiacha hayo hizi shilingi trilioni 21 zimekwenda kwenye matumizi ya kawaida tu, deni, mishahara, hizi fedha za maendeleo hapa ziko wapi?

T A A R I F A . . .

MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba niendelee kwa sababu jana yeye mwenyewe alikiri kwamba siyo mchumi, wapo wachumi hapa watasema kwamba unapokusanya unatumia 100% hakuna hata senti ambayo inabakia unatumia kama ilivyo, watatuambia hapa wachumi wapo, tuna madaktari wawili hapa watatueleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuonyesha kwamba hizi taarifa ni za kutengeneza tuje katika pato la Taifa. Pato la Taifa Mheshimiwa Waziri wa Fedha amesema kwenye kitabu chake kwamba ni shilingi trilioni 50. Sasa hivi Tanzania current population ni watu milioni 59, sasa milioni 59 ukigawa kwa shilingi trilioni 50 unapataje 2,275,000 kuwa pato la mtu wa kawaida kwa kila Mtanzania?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba wakija hapa watusaidie hizi hesabu zimekaaje kwa sababu ukifanya hesabu hapa, kama ukifanya kwa hiyo milioni 50 maana yake pato la kila Mtanzania ni wastani wa 1,063,000. Sasa hapa Waziri wa Fedha anatuambia kwamba pato la Mtanzania limeongezeka na ni 2,275,000 kwa mwaka wakati yeye mwenyewe amekiri hapa pato la Taifa ni shilingi trilioni 50. Kawaida katika kujua pato la mwananchi unagawa pato la Taifa kwa idadi ya watu ambao unao. Sasa Mheshimiwa Waziri akija hapa atuambie hii hesabu imekaaje. Nasema haya kuonyesha kwamba haya ni mambo ya kutengeneza. Sasa tukisema hii ni bajeti hewa tunakosea? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikitoka hapo tuje kwenye masuala ya uwekezaji. Serikali ya Awamu ya Tano ilisema kwamba inafufua Shirika la Ndege kwa ajili ya kukuza uchumi wa nchi hii. Ukichukua taarifa hii ya CAG anasema wazi kwamba taratibu za manunuzi ya umma hazikufanyika na Serikali imekiuka Kanuni ya 10(4), Kanuni ya Manunuzi ya Umma katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyopitishwa mwaka 2013. Sasa ikiwa leo utaratibu tu tunaukosea, tunakwendaje kuwekeza na mradi huu uweze kuwa na tija kwa wananchi wa Tanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa zinakinzana, ukiangalia kitabu cha Mheshimiwa Dkt. Mpango anasema kwamba mwanzo waliomba shilingi bilioni 500 kununua ndege na mwaka 2017/2018 wakaomba tena shilingi bilioni 500 kumalizia kulipia ndege na sasa wameshaomba tena pesa nyingine kwa ajili ya kukamilisha malipo kwa baadhi ya ndege na utaratibu wa kufanya operesheni lakini inatofautiana na kitabu cha Waziri wa Uchukuzi. Waziri wa Uchukuzi anasema mwaka jana wameomba kwenda kukamilisha malipo ya ndege sita lakini leo humu Waziri Mheshimiwa Dkt. Mpango kwenye kitabu chake anasema wametenga shilingi bilioni 495.6 na kuwa wamekamilisha malipo ya asilimia 30 ya ndege mbili za CS3100 wakati huku walisema wanakamilisha malipo, sasa hii biashara mnaifanyaje?

Mheshimia Naibu Spika, nimuombe Waziri akija hapa atupe sera ya ufufuaji wa hili Shirika la Ndege, atuambie hapa sera ni hii kwa sababu ikiwa sera ya shirika imekosekana unatengenezaje business plan? Unalifanyaje Shirika lijiendeshe kwa faida? Ukiangalia kuna mashirika kadhaa ambayo yana hali mbaya kwa sababu hapa tatizo siyo kununua ndege, tatizo ni utaratibu wa kuendesha shirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Shirika la Alitalia, wanazo ndege lakini sasa hivi linatafutiwa wabia ili waweze kuliendesha shirika. Kuna Shirika la British Airways sasa hivi Qatar ndiyo wanakwenda kulihuisha lina-suffer. Kuna Shirika la Air Rwanda limeshafilisika tayari. Kuna Shirika la South Africa sasa hivi linaomba watu wakalisaidie ili lifufuke. Sasa sisi tukisema hapa hatusemi kwa sababu tunaichukia Serikali, tunataka hili shirika liendeshwe kwa faida. Kama tunaendesha shirika kwa kupitia safari zetu za ndani basi tungeanzia hapa halafu baadaye tukaenda sehemu nyingine lakini huku tunakoelekea na ndege ambazo mmenunua inaonekana wazi ndege hizi mnakwenda kuzikodisha kwa mashirika mengine kwa sababu mtakuwa hamuwezi kuzihudumia na wala hamtaweza kufanya ushindani wa kibiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapoyasema haya tunayasema kwa sababu nchi hii ni yetu sote. Ikiwa hamtaki ushauri huu ambao tunawapa matokeo yake mtakuja kuona. Kwa sababu Serikali ya Awamu ya Tano mnakataa kujibu maswali ya Serikali ya Awamu ya Nne, mnasema Serikali ya Awamu ya Tano imejipambanua, imeamua, inafanya, sasa hii yenu nyie mkimaliza anakuja kujibu nani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimalizie kwa kusema kwamba tatizo kubwa linaloonekana ni kwamba Rais amewaamini watu wake lakini wanapomrejeshea taarifa hawamrejeshei taarifa sahihi. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na mimi kunipa fursa ya kuchangia machache katika mapendekezo ya mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza hii ni mara ya tatu mimi nachangia mapendekezo ya huu mpango. Lakini kwa bahati mbaya, Waziri wa Mipango anapokuja hapa yale yote ambayo tunazungumza naye anakuwa hayazingatii kabisa.

Kwanza nataka niende katika masuala ya miradi ya kiuchumi ambayo jambo la kufurahisha jana yupo Mbunge mmoja alichangia hapa. Tulisema kwamba tokea awali baada ya dhamira ya kuanzisha miradi hii mikubwa kwa mfano, Air Tanzania ni kwa ajili ya uchumi wa nchi na tukasema kwamba tunakubalina kabisa kwamba tunahitaji Shirika la Ndege ili kuweza kunyanyua uchumi wa nchi yetu. Lakini ilikuwa lazima tufanye utafiti wa kutosha, tutafute wataalam watusaidie ili tukianzisha Shirika liweze kuwa la mafanikio. Lakini haraka haraka shirika likaanzishwa, hakuna tatizo, lakini nimwambie Mheshimiwa Waziri Mpango bado hujachelewa, biashara ya ndege ni biashara moja ngumu sana katika dunia, sio Tanzania tu katika dunia biashara ya ndege ni ngumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitaka kujua matatizo ambayo tunayakabili kwa sasa bado shirika letu halijaanza kazi, ni kwamba tulianza na Bombardier lakini baadae tukaja kwenye Boeing, lakini leo Kampuni ya Bombardier kwa zile ndege za JET imenunuliwa na Air Bus, angalia sasa kwamba ndege hizi ambazo zinakuja sasa hivi E220, wanaozuhudumia sio Bombardier tena ni Air Bus kwa sababu hiki kiwanda kwa ndege za JET hiki kimenunuliwa na Air Bus. Lakini pia tuna hiyo Boeing ambayo tuna ndege moja tayari na nyingine inakuja mwaka 2020 na Bombardier tunazo hizi ndege zao za Q400 ambazo Bombardier bado wenyewe wanazihudumia.

Sasa bado hatujachelewa, ndege zimeshanunuliwa sasa ni wakati wa kutafuta watalaam waweze kulisimamia hili shirika ili liweze kuendeshwa kwa faida, vinginevyo shirika hili litakufa. Kwa sababu leo vitabu vyako viwili vinatofautiana hivi, mapendekezo ya mpango ukurasa wa 14 na kitabu chako hiki ambacho cha hotuba yako uliyoisoma ukurasa wa 27 vinatofautiana.

Kwanza kwenye mapendekezo ya mpango umeelezea hapa kwamba ndege jinsi mlivyozinunua na nini, lakini baada ya kununua hizi ndege ndio sasa mnaenda kutafuta soko la hizi ndege. Hichi ni kitabu chako umeandika wewe mwenyewe vyote vitabu hivi viwili umeandika wewe mwenyewe. Kwa maana baada ya kuliimarisha shirika la ndege lakini pia ndio mnaenda kutafuta masoko sasa ya kuweza kufanya hii biashara ya ndege. Lakini huku unasema kwamba kwenye kitabu hiki cha mapendekezo ya mpango ambacho tulipewa kabla inasema kwamba ndege hizi zitaanza kwenda katika miji hii ambayo imetajwa hapa Bombay, Bujumbura, Guangzhou na Entebe. Lakini kitabu hiki ambacho wewe ulichotusomea hapa Bungeni, kinasema kwamba miji ambayo ndege yetu itakwenda ni Mumbay, Bujumbura, Guangzhou na Entebe. Sasa sijui kipi ni sahihi kati ya hivi viwili, kwa hiyo, naomba uangalie zaidi ili uone tujue wapi pana usahihi na wapi hapana usahihi. (Makofi)

Kwa hiyo, hilo ni jambo moja ambalo ninakushauri kwa sababu hili shirika mmetumia fedha nyingi sana kwa ajili ya kuliimarisha, kwa hiyo, kama mnataka lifanye faida na linyanyue uchumi basi inabidi sasa patafutwe watu ambao ni wataalam, tuwape kazi hii ili watufanyie reform ya shirika letu. Lakini pia utakapokuja hapa utuambie hili shirika baada ya kununua hizi ndege, ni baada ya muda gani litaweza ku- break even ili tujue kwamba tunakokwenda ni wapi. Kwa hiyo, naomba kwamba utakapokuja kuhitimisha hoja yako ile business plan ambayo mnayo mtuambie baada ya miaka mingapi shirika litakuwa limerejesha ule mtaji na lianze kutengeneza faida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ni kwamba katika mpango huu ambao ameuleta Mheshimiwa Waziri, hakuna kipengele hata kimoja kinachoonesha Zanzibar kimo katika mpango huu ili kuiendeleza Zanzibar na mara nyingi tumesema toka tumetaka kuanza bajeti ya mwaka 2015/2016 tumesema kwa nini haitafutwi japo mradi mmoja au miwili au mitatu ambayo inakuja katika mapendekezo ya mpango kwa ajili ya Zanzibar? Kwa nini kuna tatizo gani? Tatizo gani ambalo linatusababishia mpaka leo kila siku tuzungumzie Zanzibar kwenye mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba huu mpango kwa sababu ni mapendekezo ya mpango utakapoleta mpango halisi basi tuone kwamba Zanzibar, kuna mradi gani wa kiuchumi ambao utaweza kuisaidia Zanzibar. Halafu ukiangalia sisi Zanzibar tuna bahari kubwa tu na sasa hivi mwezi huu nafikiria mwishoni mwa mwezi kuna fanyika mkutano wanaita blue economy ambao unafanyika Kenya, ambao unahusisha mazao ya bahari unakwenda kufanyika, sasa kwa nini basi kusifanyike utafiti wataalmu wako, wasifanye utafiti wakaona kwamba kuna eneo hili mahususi la Zanziba likaweza kukuza uchumi wa Zanzibar kwa nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia la mwisho niseme kwamba Mheshimiwa Mpango katika Bunge lililopita baada ya kutoa maelezo ya mwelekeo kuhusu deni la Zanzibar katika masuala ya TANESCO iliposemwa hapa ulitoa maelezo mazuri sana na Mheshimiwa Spika akakubali, na tukakubaliana kwamba Bunge hili likija hii VAT kwenye deni la umeme, iondolewe lakini kwenye miswada hii imekuja hapa halikuondolewa hili suala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikwambie Mheshimiwa Mpango najua masuala yote yanapitishwa kwenye cabinet, lakini suala hili ujachukua juhudi za makusudi kuhakikisha ili jambo lina malizika, wewe mwenyewe personally hujachukua juhudi za makusudi kwa sababu sisi tunazungumza na viongozi ambao wa Zanzibar ambao unafanya nao mawasiliano, lakini ujachukua ile juhudi ya makusudi ya kuonesha jambo hili lina malizika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mtuambie kwamba sisi Zanzibar siyo ndugu zenu, ndugu zenu ni watu wa Rwanda, Kenya huko na Zambia hao ndiyo jamaa zenu sisi hatumo miongoni mwa Taifa hili ili tujuwe haiwezekani kwamba priority anapewa kutoka Rwanda au kutoka Kenya lakini Zanzibar, anaonekana kama ni mtumwa tu analitumikia hili Taifa. Huu ukoloni utaisha lini? Sisi tumeungana hapa kwa nia njema kabisa, lakini leo sasa hivi, mnaanza kutubadilishia maneno mnatufanya kama sisi watumwa wenu tu, wala hamjali tukipiga makelele.

Mimi nawashauri Wazanzibari wenzangu kwamba sasa ni afadhali tutafute njia ya kutafuta umeme sisi wenyewe badala ya kuja kumpigia magoti.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na mimi kunipa fursa ya kuchangia machache katika mapendekezo ya mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza hii ni mara ya tatu mimi nachangia mapendekezo ya huu mpango. Lakini kwa bahati mbaya, Waziri wa Mipango anapokuja hapa yale yote ambayo tunazungumza naye anakuwa hayazingatii kabisa.

Kwanza nataka niende katika masuala ya miradi ya kiuchumi ambayo jambo la kufurahisha jana yupo Mbunge mmoja alichangia hapa. Tulisema kwamba tokea awali baada ya dhamira ya kuanzisha miradi hii mikubwa kwa mfano, Air Tanzania ni kwa ajili ya uchumi wa nchi na tukasema kwamba tunakubalina kabisa kwamba tunahitaji Shirika la Ndege ili kuweza kunyanyua uchumi wa nchi yetu. Lakini ilikuwa lazima tufanye utafiti wa kutosha, tutafute wataalam watusaidie ili tukianzisha Shirika liweze kuwa la mafanikio. Lakini haraka haraka shirika likaanzishwa, hakuna tatizo, lakini nimwambie Mheshimiwa Waziri Mpango bado hujachelewa, biashara ya ndege ni biashara moja ngumu sana katika dunia, sio Tanzania tu katika dunia biashara ya ndege ni ngumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitaka kujua matatizo ambayo tunayakabili kwa sasa bado shirika letu halijaanza kazi, ni kwamba tulianza na Bombardier lakini baadae tukaja kwenye Boeing, lakini leo Kampuni ya Bombardier kwa zile ndege za JET imenunuliwa na Air Bus, angalia sasa kwamba ndege hizi ambazo zinakuja sasa hivi E220, wanaozuhudumia sio Bombardier tena ni Air Bus kwa sababu hiki kiwanda kwa ndege za JET hiki kimenunuliwa na Air Bus. Lakini pia tuna hiyo Boeing ambayo tuna ndege moja tayari na nyingine inakuja mwaka 2020 na Bombardier tunazo hizi ndege zao za Q400 ambazo Bombardier bado wenyewe wanazihudumia.

Sasa bado hatujachelewa, ndege zimeshanunuliwa sasa ni wakati wa kutafuta watalaam waweze kulisimamia hili shirika ili liweze kuendeshwa kwa faida, vinginevyo shirika hili litakufa. Kwa sababu leo vitabu vyako viwili vinatofautiana hivi, mapendekezo ya mpango ukurasa wa 14 na kitabu chako hiki ambacho cha hotuba yako uliyoisoma ukurasa wa 27 vinatofautiana.

Kwanza kwenye mapendekezo ya mpango umeelezea hapa kwamba ndege jinsi mlivyozinunua na nini, lakini baada ya kununua hizi ndege ndio sasa mnaenda kutafuta soko la hizi ndege. Hichi ni kitabu chako umeandika wewe mwenyewe vyote vitabu hivi viwili umeandika wewe mwenyewe. Kwa maana baada ya kuliimarisha shirika la ndege lakini pia ndio mnaenda kutafuta masoko sasa ya kuweza kufanya hii biashara ya ndege. Lakini huku unasema kwamba kwenye kitabu hiki cha mapendekezo ya mpango ambacho tulipewa kabla inasema kwamba ndege hizi zitaanza kwenda katika miji hii ambayo imetajwa hapa Bombay, Bujumbura, Guangzhou na Entebe. Lakini kitabu hiki ambacho wewe ulichotusomea hapa Bungeni, kinasema kwamba miji ambayo ndege yetu itakwenda ni Mumbay, Bujumbura, Guangzhou na Entebe. Sasa sijui kipi ni sahihi kati ya hivi viwili, kwa hiyo, naomba uangalie zaidi ili uone tujue wapi pana usahihi na wapi hapana usahihi. (Makofi)

Kwa hiyo, hilo ni jambo moja ambalo ninakushauri kwa sababu hili shirika mmetumia fedha nyingi sana kwa ajili ya kuliimarisha, kwa hiyo, kama mnataka lifanye faida na linyanyue uchumi basi inabidi sasa patafutwe watu ambao ni wataalam, tuwape kazi hii ili watufanyie reform ya shirika letu. Lakini pia utakapokuja hapa utuambie hili shirika baada ya kununua hizi ndege, ni baada ya muda gani litaweza ku- break even ili tujue kwamba tunakokwenda ni wapi. Kwa hiyo, naomba kwamba utakapokuja kuhitimisha hoja yako ile business plan ambayo mnayo mtuambie baada ya miaka mingapi shirika litakuwa limerejesha ule mtaji na lianze kutengeneza faida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ni kwamba katika mpango huu ambao ameuleta Mheshimiwa Waziri, hakuna kipengele hata kimoja kinachoonesha Zanzibar kimo katika mpango huu ili kuiendeleza Zanzibar na mara nyingi tumesema toka tumetaka kuanza bajeti ya mwaka 2015/2016 tumesema kwa nini haitafutwi japo mradi mmoja au miwili au mitatu ambayo inakuja katika mapendekezo ya mpango kwa ajili ya Zanzibar? Kwa nini kuna tatizo gani? Tatizo gani ambalo linatusababishia mpaka leo kila siku tuzungumzie Zanzibar kwenye mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba huu mpango kwa sababu ni mapendekezo ya mpango utakapoleta mpango halisi basi tuone kwamba Zanzibar, kuna mradi gani wa kiuchumi ambao utaweza kuisaidia Zanzibar. Halafu ukiangalia sisi Zanzibar tuna bahari kubwa tu na sasa hivi mwezi huu nafikiria mwishoni mwa mwezi kuna fanyika mkutano wanaita blue economy ambao unafanyika Kenya, ambao unahusisha mazao ya bahari unakwenda kufanyika, sasa kwa nini basi kusifanyike utafiti wataalmu wako, wasifanye utafiti wakaona kwamba kuna eneo hili mahususi la Zanziba likaweza kukuza uchumi wa Zanzibar kwa nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia la mwisho niseme kwamba Mheshimiwa Mpango katika Bunge lililopita baada ya kutoa maelezo ya mwelekeo kuhusu deni la Zanzibar katika masuala ya TANESCO iliposemwa hapa ulitoa maelezo mazuri sana na Mheshimiwa Spika akakubali, na tukakubaliana kwamba Bunge hili likija hii VAT kwenye deni la umeme, iondolewe lakini kwenye miswada hii imekuja hapa halikuondolewa hili suala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikwambie Mheshimiwa Mpango najua masuala yote yanapitishwa kwenye cabinet, lakini suala hili ujachukua juhudi za makusudi kuhakikisha ili jambo lina malizika, wewe mwenyewe personally hujachukua juhudi za makusudi kwa sababu sisi tunazungumza na viongozi ambao wa Zanzibar ambao unafanya nao mawasiliano, lakini ujachukua ile juhudi ya makusudi ya kuonesha jambo hili lina malizika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mtuambie kwamba sisi Zanzibar siyo ndugu zenu, ndugu zenu ni watu wa Rwanda, Kenya huko na Zambia hao ndiyo jamaa zenu sisi hatumo miongoni mwa Taifa hili ili tujuwe haiwezekani kwamba priority anapewa kutoka Rwanda au kutoka Kenya lakini Zanzibar, anaonekana kama ni mtumwa tu analitumikia hili Taifa. Huu ukoloni utaisha lini? Sisi tumeungana hapa kwa nia njema kabisa, lakini leo sasa hivi, mnaanza kutubadilishia maneno mnatufanya kama sisi watumwa wenu tu, wala hamjali tukipiga makelele.

Mimi nawashauri Wazanzibari wenzangu kwamba sasa ni afadhali tutafute njia ya kutafuta umeme sisi wenyewe badala ya kuja kumpigia magoti.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Usimamizi wa Matumizi ya Fedha za Umma katika Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2017
MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu siku hii ya leo kuweza kutujalia hapa tukiwa wazima na nikushukuru wewe kunipatia hii fursa kwa ajili ya na mimi kutoa maoni yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ripoti imeeleza wazi na query zote ambazo zilitokea ni kwa sababu ya Hazina. Hazina ndio ambao wamesababisha query hizi na Mkaguzi ikabidi atoe hoja zake na ninafikiri sote tunakubaliana kwamba na mwisho yametolewa mapendekezo huku kwamba, mfumo wa mahesabu wa Hazina ni shida, kwamba ikiwa leo Halmashauri zinatumia mfumo wa hesabu wa EPICOR lakini Hazina inatumia mfumo wa excel. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli taarifa zimeletwa kutoka Serikalini, lakini bado Mkaguzi aliweka hoja kwa sababu hazikupita katika mfumo rasmi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kibaya ni kwamba fedha ambazo zimetoka kwenye Hazina, tuchukue mfano leo Serikali, Serikali ndio inapanga bajeti, wanakaa wanapanga bajeti yao wanakutana na CAG, CAG anafanya approval akishafanya approval inaletwa Bungeni hapa sisi tunapitisha. Sasa ikishapitishwa hapa na Sheria ya Matumizi ikishapitishwa matokeo yake Hazina wanakwenda kubadilisha matumizi ya bajeti ambayo imepitishwa na Bunge pasipo na kumtaarifu CAG. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuna exchequer chungu mzima hapa zimeonesha kwamba, kuna fedha zimefanyiwa matumizi ambayo hayakupitishwa na Bunge na wala hakutaarifiwa CAG, jambo ambalo lilikuwa rahisi tu. Serikali walikuwa na uwezo wa kwenda kwa CAG kutokana na bajeti tunayoipeleka hapa kumetokea dharura hii tufanyie marekebisho hapa tupate approval halafu baadaye inaletwa Bungeni kuja kupitishwa pia hili limeshindikana, lakini Hazina wanafanya halafu baadae ndio Mkaguzi anakuja kuona. (Makofi)

MHE. MARIAM N. KISANGI: Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ali kuna Taarifa. Mheshimiwa Mariam Kisangi.

T A A R I F A

MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mimi kwanza sina shida na adjustment, adjustment ni mambo ya ndani ya utawala, sina shida nayo na wala sijazungumzia habari ya adjustment, mimi nimezungumzia reallocation. Kuna reallocation mbalimbali ambazo zimefanyika na ndiyo maana CAG ali-raise query kwa sababu hazikufata utaratibu kwa mfano... (Makofi)

MHE. KHADIJA NASSIR ALI : Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba unitunzie muda wangu kwa hisani yako.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ali Salim unaipokea taarifa hiyo?

MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Soika, siipokei kwa sababu siyo utaratibu huo. Kama ikitokea hivyo Serikali inayo mamlaka ya kufanya reallocation, hilo halina mjadala, lakini kwa sababu bajeti hii ilishapitishwa Bungeni na Serikali inafanya reallocation imtaarifu CAG approve hiyo reallocation yao. Hilo ndilo tatizo, si kwa sababu…

NAIBU WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ali Salim unaipokea taarifa hiyo?

MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, siipokei hiyo taarifa kwa sababu kwanza mimi nataka nimfahamishe Mheshimiwa Naibu Waziri. Yeye alileta taarifa hapa Bungeni, na taarifa hii amesema kwamba bilioni 203 zilikuwa transfered to Zanzibar, lakini Mheshimiwa Kiula amesema fedha zile zilikusanywa Zanzibar na hazikuondoshwa Zanzibar zilitumika pale pale Zanzibar, sasa hapa dakika kumi zilizopita hapa taarifa zinatofautiana. Ndiyo maana nasema kuna shida ya mfumo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ninaposema tusikilizane tunasema haya kwa maslahi ya nchi yetu, mimi nimezungumzia kuhusu mfumo…

MHE. KABWE Z. R. ZITTO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ali Salim kuna taarifa nyingine.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ali Salim unaipokea taarifa hiyo?

MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa hiyo naipokea na kwa kuongezea tu baada ya query hii ya CAG ya shilingi bilioni 976 Hazina ilipeleka document za clear dola bilioni 1.25 lakini bilioni 975.1 hazijapatiwa majibu mpaka sasa. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii na mimi kutoa mchango wangu wa maandishi kama ifuatavyo:-

Kwanza nianze na maradhi ya Corona. Ili kudhbiti ugonjwa huu mambo yafuatayo yazingatiwe:-

Mosi, kama Serikali imeamua shughuli za kijamii waendelee kama masoko, maeneo ya usafiri wa umma na kadhalika, wakati umefika sasa nikuzuia watu kutoka nje ya nchi, pia maeneo yaliyopatikana maambukizi yazuiliwe watu kutoka na pia kuingia.

Jambo la pili ni muhimu kuangalia upatikanaji wa vifaa vya uchunguzi pamoja na vifaa kwa ajili ya wauguzi na madaktari kuweza kujikinga na maambukizi wakati wa kutoa huduma kwa wagonjwa.

Tatu, katika Ofisi ya Waziri Mkuu iko haja ya kutenga bajeti ya dharura ili kukabiliana na janga hili kwani dharura inaweza kutokea wakati wowote.

Mheshimiwa Spika, nnem mwaka 2017 tulipitisha sheria ya mgawanyo wa wafanyakazi katika taasisi za Muungano asilimia 72 kwa 28 likiwemo Bunge la Jamhuri ya Muungano hadi sasa marekebisho ya wafanyakazi bado, naomba lifanyiwe kazi ili uwiano upatikane.

Tano, kutokana na janga la Corona Serikali iangalie ni namna gani kuangalia kuondoa kodi kwa biashara zote zilizoathirika kutokana na janga hili walau kwa miezi mitatu.

Mheshimiwa Spika, ni matumaini yangu kuwa ushauri wangu utafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa nami ya kuweza kuchangia mawili/ matatu. Nataka nijielekeze zaidi katika masuala haya ya mafuta na gesi. Ripoti ya Kamati imeelezea wazi juu ya matatizo ya kisheria ambayo yanalikabili Taifa katika masuala ya miradi hii ya gesi ya SONGAS. Pia tatizo hilo hilo lipo katika suala baina ya Zanzibar na Bara kuna tatizo kama hilo ambalo liko katika mikataba hiyo ya SONGAS.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano, nyongeza ya kwanza, suala la mafuta na gesi ni suala la Muungano na kwenye Ibara ya 34 inaeleza wazi na Ibara ya 64 pia nayo inaeleza jinsi ya masuala ya mafuta na gesi ambayo ni mambo ya Muungano. Kama hiyo haitoshi mwaka 2015, Bunge hili lilipitisha Sheria ya Mafuta kuonesha kwamba nani hasa anastahiki kusimamia mafuta na gesi katika Tanzania. Sasa kilichojitokeza kwanza mwaka 2009 Baraza la Wawakilishi liliazimia kwamba suala la mafuta litolewe katika mambo ya Muungano, kwa sababu suala hili liliingizwa katika masuala ya Muungano mwaka 1968 katika Katiba ya muda ambayo kimsingi liliingizwa bila ridhaa ya Wazanzibari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukiendelea Zanzibar sasa hivi imetunga sheria yake, Sheria Na.6 ambayo inasema kwamba mafuta ni mali ya Zanzibar na Zanzibar wao ndio wenye mamlaka ya kuchimba mafuta na Katiba ya Zanzibar iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2010 imeeleza wazi mipaka ya Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ukiangalia katika sheria hii ya mwaka 2015 Kifungu cha 47, kimeleta marekebisho kumpa mamlaka Waziri wa Nishati wa Bara kwamba ndiye ambaye atatoa maelekezo jinsi masuala yote mazima ya mafuta. Pia Zanzibar nao katika sheria mpya ambayo imetungwa ya mwaka 2016, Sheria Na. 6 nayo vile vile imempa mamlaka Waziri wa Nishati wa Zanzibar kusimamia masuala ya mafuta. Sasa niombe kutokana na mkanganyiko huu wa kisheria na kikatiba nafikiri sasa ni wakati muafaka kuleta mjadala wa katiba ili suala hili la mafuta Zanzibar washughulike na masuala yao ya mafuta na Bara na wao washughulike na masuala yao ya mafuta.

Mheshimiwa Naibu Spika,Leo ukiangalia masuala haya mafuta huko mbeleni yataleta mgogora sana. Matatizo haya haya ndio matatizo ambayo yanaikabili miradi hii mikubwa ya gesi sasa hivi, ukiangalia Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haipati kitu katika suala zima la masuala ya gesi. Ndio maana leo kila mtu analizungumzia hapa kwamba mikataba ina shida, kwa hiyo sasa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Bunge hili imetengeneza sheria kama zile ambazo wametengenezewa wao na SONGAS…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele imeshagonga.

MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, nimeandika kwa maandishi pia mchango wangu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia siku hi ya leo kuwa na afya njema na kusaidia kutoa michango yetu kwa ajili ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli ulio wazi kwamba suala la biashara limeingia katika matatizo makubwa na mimi nina mambo kama matatu tu hivi ambayo nitayazungumzia leo. La kwanza; kuonesha kwamba biashara ina utata ni kwamba nchi imetengeneza dheria hata bidhaa zake zinazotoka ndani ya nchi nazo zinalipiwa ushuru kama bidhaa ambazo zinatoka nchi za nje, kwa kweli hili ni jambo la ajabu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kule Zanzibar tuna Kiwanda cha Maziwa kikubwa tu ambacho kinazalisha maziwa ya kutosha, lakini leo maziwa yale yakitoka Zanzibar kuja bara yanatakiwa yalipe ushuru kama maziwa ambayo yametoka nchi za nje, hili ni jambo la aibu sana na la ajabu sana. Kibaya zaidi, TRA inaonekana kwamba kuna jambo maalum hapa linaendelea kuhusu Zanzibar kwa sababu baada ya Wazanzibari kulalamikia huu ushuru, TRA imempa fursa mwekezaji Said Salim Bakhresa kumwondolea VAT ya asilimia 87 ili kiwanda kile kihame kutoka Zanzibar na kije kijengwe bara ili aweze kufanya biashara zake. Hili kwa kweli ni jambo la aibu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atuambie shida hapa hasa ni nini. Maana yake ikiwa leo anajiwekea vikwazo yeye mwenyewe ndani ya nchi, atashindanaje na Rwanda, Kenya na Burundi, atashindana nao vipi, ikiwa ndani ya nchi yake mwenyewe amejiwekea vikwazo yaani biashara zisiende, hawa walioko nje ya nchi hii anashindana nao vipi? Kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri akija hapa atuambie kuhusu jambo hili linakaakaaje na matatizo haya yanaondoka.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, Mheshimiwa Waziri ni shahidi; mimi na Mheshimiwa Waziri Kakunda tulikwenda kwenye semina moja na semina hiyo inahusiana na masuala ya wajasiriamali pamoja na wafanyabiashara. Mwenyewe alikiri katika semina ile kwamba wafanyabiashara kwa mfano walioko mpakani baina ya Tanzania na Uganda wamehama wale wenye biashara zao kutoka Tanzania wote wamehamia Uganda, kwa sababu Uganda akishakata leseni yake ya kufanyia biashara hana bughudha nyingine anafanya biashara zake kwa utulivu, bila shida yoyote. Sasa leo ikiwa imefika mahali Watanzania wanaacha nchi yao wanakwenda kufanya biashara sehemu nyingine kutokana tu na vikwazo vya biashara ndani ya nchi hii, kwa kweli hili ni jambo la kusikitisha sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano mmoja; leo ukitaka kwenda kuwekeza UAE, UAE sharti lao kubwa ambalo wanalo lazima upate raia wa ile nchi akudhamini ndiyo uweze kufungua kampuni au kuanzisha biashara. Ukishafanya hivyo, basi wewe process zake hata wiki haifiki, umesajili ampuni yako, unafanya biashara zako na inakupa citizenship ya watu watatu ambao umetokanao ulikotoka ili wasimamie shughuli zako kufanya kazi zao katika nchi ya UAE. Leo ndani ya nchi yetu hii tumeporomoka mpaka tumefika watu wa 147 katika nchi 190. Hivi sasa Mheshimiwa Waziri nimwambie tu kwamba sasa hivi baadhi ya wawekezaji wanaangalia fursa kufanya biashara zao ama uwekezaji wao katika nchi ya Burundi, nchi ambayo inaonekana kwamba haiko tulivu katika masuala ya kisiasa, leo wawekezaji wanafikiria wakawekeze huko Burundi kulikoni kuja kuwekeza Tanzania hapa! Kwa kweli hili ni jambo la aibu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri akija hapa atuambie shida hasa ni nini? Tumsaidie kitu gani ili haya matatizo yatatuke?

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu, kule Kilwa Masoko waliambiwa wananchi wa kule kwamba watayarishe eneo ili waweze kujenga Kiwanda cha Mbolea. Eneo tayari limetayarishwa lakini mpaka leo hii hakuna jambo lolote ambalo limefanyika na watu wameondolewa katika maeneo yao kusubiri ili kiwanda cha mbolea kijengwe ili kuimarisha uchumi huo wa viwanda kupitia wakulima wetu ambao wanalima kule katika eneo la Kusini, sasa shida ni nini? Mheshimiwa Waziri akija hapa atuambie tatizo ni nini hasa ambalo mpaka leo linakwaza mambo haya? Kila kona ya nchi hii kuna shida ya suala la biashara na viwanda. Hebu akija hapa Mheshimiwa Waziri atuambie jambo ambalo linamkwaza ambalo mpaka hivi leo linamfanya asifanye kazi zake vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, kwa nini Mheshimiwa Waziri mpaka toka alipoteuliwa kuwa Waziri hajawaita wafanyabiashara akakaa nao akawasikiliza, shida iko wapi ili akaona kwamba ni taasisi gani ambayo inakwamisha au kuna ugumu mahali gani halafu tukatafuta njia ya kutokea hapa, lakini leo anakuja analeta bajeti hii ili ikishapitishwa hapa ndiyo imetoka matatizo ya nchi yanabaki kama yalivyo. Sasa Mheshimiwa Waziri akija hapa naomba atupatie ufumbuzi wa masuala haya ili Bunge lione ni namna gani bora kusadia nchi hii iweze kutoka katika masuala haya yenye mkwamo huu wa biashara pamoja na viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli sasa hivi ukija kwenye suala la biashara, hii dhana ya biashara kule Zanzibar yaani kama kuna njama za makusudi hivi kuiua biashara Zanzibar isifanyike. Sasa tunaomba Mheshimiwa Waziri ndiyo maana hapa kunaingia masuala mengi ya kuona kuna matatizo gani katika masuala ya Muungano ili yaweze kutatuliwa haya biashara zifanyike kwa uhuru…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019
MHE. ALI SALIM KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kutujalia leo kuweza kuwasilisha ripoti zetu mbili hizi, lakini pia nikushukuru wewe Mheshimiwa Naibu Spika kunipa fursa hii na nitangulie kuwapongeza Wenyeviti wa Kamati kwa kazi nzuri ambayo wamefanya na leo wameweza kuwasilisha taarifa hizi hapa kwa ajili ya utekelezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nina mambo mawili tu ya kuchangia kwenye Kamati zetu mbili hizi na la kwanza ni suala la bandari. Suala la bandari tukichukua kumbukumbu nyingi ambazo zimepita huko nyuma ni jambo la kwanza ambalo Mheshimiwa Rais alitilia mkazo na nguvu nyingi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba bandari inafanya kazi zake kwa weledi. Pia Mheshimiwa Waziri Mkuu na yeye alichukua jitihada hizo ili pia kuhakikisha kwamba bandari inafanya kazi zake vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, bandari ni uchumi wa nchi katika Taifa letu ama Taifa lingine lolote lile duniani. Leo ukiangalia Dubai ukiacha masuala ya mafuta jambo kubwa ambalo wanalitegemea katika kuendesha nchi yao ni bandari na wanapokea mizigo mingi kutoka sehemu mbalimbali na kusafirisha mizigo mingi na kuongezea pato lao la Taifa kwa nchi yao. Kwa hiyo ni muhimu na sisi sasa kuona kwamba bandari ni sehemu ya kuweza kukuza uchumi wa nchi yetu na kuonekana kwamba ni mahali pazuri pa kuweza kukusanya mapato ili kuleta ufanisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nayasema haya kwa sababu kwa mujibu wa taarifa yetu ambao tumewasilisha hapa toka mwaka 2010 mpaka mwaka 2019 bandari inahangaika kuweka mifumo ya kieletroniki kwa ajili ya kukusanya mapato na kupatikana uhalisia ni mapato kiasi gani ambayo yanapatikana. Gharama kubwa ambayo imetumika zaidi ni kwamba zaidi ya bilioni 57 zimeshatumika kwa ajili ya kuweka hiyo mifumo lakini bila mafanikio. Sasa tuombe kwamba Serikali kama nilivyotangulia kusema Mheshimiwa Rais alifanya juhudi kubwa, lakini katika eneo hili la bandari mpaka leo kwenye masuala haya ambayo ni muhimu ya ukusanyaji wa mapato hayajakamilika ili kupata ufumbuzi wa mfumo sahihi wa kuweza kutoa takwimu sahihi na mapato sahihi ambayo yanakusanywa kwenye bandari.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kama ambavyo Kamati imeshauri naona sasa ifike mahali kwamba bandari iweze kufikia mwisho kwa ajili ya kuweza kuokoa fedha za walipa kodi ili kuweza kuweka mifumo sahihi na ambayo itaweza kutoa takwimu sahihi za mapato yanayopatikana katika bandari yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ambalo nimekusudia kuchangia leo na nilimwona Mheshimiwa Waziri wa Fedha hapa muda si mrefu na nina imani yupo na Naibu Waziri yupo. Kuna jambo ambalo ni muhimu kulielekeza kwake Mheshimiwa Waziri wa Fedha na jambo hili linahusiana na Shirika letu la Ndege ambalo mara ya mwisho katika ukaguzi wa mwisho ambao umefanyika 2018/2019, Mkaguzi ameonesha tahadhari ya Shirika letu la Ndege kwenda kwenye hatari ya kufilisika kama madeni ambayo yapo hayatalipwa. Sasa Serikali imechukua jukumu la kwamba watalipa hayo madeni ili kuhakikisha kwamba Shirika linafanya kazi zake upya na kutengeneza faida.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha ambaye yupo hapa kwamba hii commitment ambayo Serikali imekubali kuchukua juu ya Shirika la Ndege basi itekelezwe kwa wakati ili shirika lisije likapata matatizo kama yale ambayo yametokea huko awali na ukizingatia sasa hivi uwekezaji ambao umeshafanyika ni zaidi ya trilioni moja na nusu kwa ajili ya kulirudisha shirika hili ili liweze kufanya kazi kwa mafanikio.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, mwaka 2016/2017 na 2017/2018 nilitoa ushauri hapa kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha ambaye alileta hoja mezani na nikasema kwamba kuanzishwa shirika ni jambo jema na tukakubali kwamba shirika hili litasaidia nchi, lakini tukatoa mawazo kwamba tunahitaji uweledi kwenye hili shirika. Najua kwamba wapo wataalam kwenye hili Shirika la Ndege Tanzania wanafanya kazi vizuri lakini utaalam wao una kikomo yaani unafika mahali lazima upate usaidizi kutoka kwa wataalam ambao wamebobea katika biashara hizi za ndege ili kulinyanyua shirika liweze kufanya kazi zake vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano, leo ukiangalia shirika letu la ndege la Air Tanzania limeshindwa hata kuanzisha safari za kutoka aidha, Dar es Salaam- Nairobi au Dar es Salaam – Zanzibar – Nairobi mpaka huu muda ambao tunazungumza. Leo Jomo Kenyata Airport ni hub katika Afrika Mashariki katika masuala ya kibiashara iwe ya ndege na mambo mengine, lakini hadi leo shirika letu halijaweza kwenda Nairobi, lakini ukiangalia Kenya Airways wanakuja mara saba kwa siku Dar es Salaam pamoja na Zanzibar.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii inaonesha kwamba sasa tunahitaji wataalam waliobobea zaidi katika masuala haya ili kulifanya shirika liweze kufanya kazi zake kibiashara zaidi na kuweza kuleta faida katika shirika hilo na hasa ukizingatia kwamba mwaka 2017/2018 shirika limepata hasara ya bilioni 10 baada ya tax, lakini 2018/2019 limepata hasara ya bilioni 16. Kwa hiyo badala ya hii hasara kupungua inaongezeka sasa na nature ya biashara hii maana yake leo ukipata hasara bilioni 10, mwakani ipungue ili mwisho wa siku iweze ku-recover ile loss na iweze kutengeneza faida.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa namwomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa sababu yeye ndio ambaye alileta hoja ya kulisimamia shirika hili na nina imani kwamba commitment ya Serikali kwamba wamekubali kulisimamia na ili shirika liweze kuendelea vizuri basi, sasa wakati umefika kwa Serikali kufikiria kutafuta mtaalam mbobezi katika masuala haya ya biashara ya ndege ili aweze kulisaidia Shirika la Air Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikupe mfano wa pili mdogo tu, Air Tanzania imeanza kuja Dodoma na inakuja mara mbili kwa siku, lakini baada ya kuanzishwa hii route ya kuja Dodoma kwa sababu ya potentially ya biashara ya ndege utakuwa leo Precision Air anakuja mara tatu kwa siku wakati mwingine mara nne Dodoma na ndege zinajaa. Sasa wapi tunafeli tuna matatizo wapi ili tuone kwamba shirika tunalisaidia liweze kujiendesha kibiashara zaidi na liweze kwenda kwenye ushindani wa biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa badala ya kwamba sisi tulianzisha shirika ili tuweze kupata faida matokeo yake tunatengenezea watu njia kuwafanya watajirike zaidi katika hii biashara na sisi tunabaki kuwa tunawafuata wao nyuma. Kwa hiyo haya ni mambo ambayo yanaonesha kwamba pamoja na kazi nzuri ambayo wanafanya wataalam wetu lakini wanahitaji utaalam wa ubobezi ili kuwatoa hapa waliko kwenda kwenye stage nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nikushukuru kwa kunipa fursa. (Makofi)