Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Juma Kombo Hamad (14 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema mchana huu na kupata fursa hii ya kuchangia kwenye bajeti hii ya Wizara muhimu, Wizara ya ELimu.
Pili kwa sababu ni mara ya mwanzo kabisa nichukue fursa hii pia kuwashukuru wapigakura wangu wa Jimbo la Wingwi kwa kunipatia ushindi mkubwa wa asilimia 90 dhidi ya mgombea mwenzangu. Pia nikishukuru chama changu, Chama cha Wananchi (CUF) kwa kuniamini kabisa na kunipa fursa hii, nakiahidi kwamba sitakiangusha, nitakitumikia kwa nguvu zangu zote kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nianze kwa kusema kwamba ili tufanikiwe na ili tuendelee tunahitaji tuwekeze kwenye suala zima la elimu. Kinachoonekana hapa bado kama vile hatujakuwa tayari kuwekeza katika suala zima la elimu. Kinachoonekana hapa ni kama vile tunakuja kutaniana, kwa sababu kile ambacho kimezungumzwa mwaka wa jana, kile ambacho kimezungumzwa mwaka wa juzi ndicho kile kile kinachopigiwa kelele, hakiongezeki wala hakipungui.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ambayo ili zungumzwa mwaka wa jana tulipaswa leo tuje tuione angalau imetatuliwa kiasi fulani ili tuondoke pale tulipokuwa mwaka wa jana na sasa tuzungumzie kitu kingine. Lakini hadi sasa wenzangu wengi wamezungumza hapa, tunapiga kelele kwa matundu ya vyoo, tunapiga kelele ukosefu wa madawati na vitu vingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninamuomba Mheshimiwa Waziri, kwa nia njema kabisa, hebu fuatilia zile hotuba mbili, hotuba ya Kambi ya Upinzani pamoja na hotuba ya Kamati. Kama utazifuata vizuri basi zimetoa mwanga mzuri wa kukuongoza kufikia kule Watanzania tunakokuhitaji. Na wala sioni sababu ya kwamba usifuate mawazo yale ya vitabu vile viwili, ni vitabu ambavyo vimezungumza vizuri, vimetoa mapendekezo mazuri, vimetoa maelekezo mazuri ambayo yatatutoa hapa tulipo na kuelekea pale tunapopahitaji.
Ninakuomba sana mama yangu, kwamba kwa hili bora tu ulifuate ili maelekezo yale ukichanganya na uliyo nayo wewe mwenyewe basi utapata kitu cha kushika na mwakani utatueleza kitu kipya kabisa hapa kwenye Bunge lako hili Tukufu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika uwekezaji huu yamezungumzwa mengi, lakini lazima tukubali kugharamia, lazima tukubali kuchagua vijana tuwapeleke wakasomee taaluma mbalimbali ili waje waisaidie Tanzania; nchi nyingi zimefanya hivyo. Hata China pale ilipo leo kwanza ilianza zaidi miaka kumi kula hasara kwenda kuwasomesha vijana nje ya nchi kusoma kwa ajili ya taaluma fulani ili kwenda kuisaidia nchi yao. Sasa na sisi si aibu wala si fedheha.
Leo kuna mtu alitoa mfano hapa, mpaka leo tunategemea marubani, tunagemea ma-captain wa meli zile ambazo ziko hapa ndani ya nchi yetu ukienda pale unawakuta wote ni wageni. Kwa nini tusiende tukasomeshe wakwetu? Hivi kuna ugumu gani kuwa rubani? Hivi kuna ugumu gani kuwa captain wa meli? Hivi kuna ugumu gani kuwa meneja wa kiwanda fulani au mtandao fulani ambaye huyu atakuwa ni mzalendo wa nchi yetu? Naomba kumshauri Mheshimiwa Waziri afuate yale mawazo, naamini atatukwamua katika hatua hii na tutakwenda katika hatua nyingine nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo ninaomba kulizungumzia hapa ni suala la mikopo. Suala la mikopo limekuwa na malalamiko makubwa na ya muda mrefu hasa kwa upande wa Zanzibar. Mimi nikuombe kitu kimoja katika hili, nikuombe wakati utakapokuja, au ujiandae kuanzia sasa, kama utakuwa hujajiandaa basi ujiandae vizuri ili kuwe na utaratibu maalum wa utoaji wa mikopo. Suala la elimu ya juu, suala la Bodi ya Mikopo ni suala la Muungano, Wazanzibari wanahusika katika suala hili, hawapaswi kama vile kuchotewa, kama vile ni waalikwa. Zanzibar si mualikwa katika ile Bodi ya Mikopo, Zanzibar ni mshirika kwa sababu suala la elimu ya juu Kikatiba, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni suala la Muungano.
Sasa mimi nikuombe tu kwamba uandae utaratibu mzuri, wakati unakwenda kufanya udahili unatuletea hapa bajeti, unaisoma bajeti. Ukionesha kwamba fungu hili ndilo la mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu utuambie basi katika fungu hili kiasi hiki ndicho kinachokwenda kwa wanafunzi watakaodahiliwa watokao Zanzibar. Sioni kama kuna dhambi, sioni kama kuna tatizo hapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba sana Mheshimiwa Waziri sana kwamba hili ulifanye ili kuondoa haya malalamiko ya muda mrefu. Utakapotuambia, pengine fungu la mikopo lina milioni 40, lakini hizi Shilingi 200,000 zitakwenda kwa wanafunzi wa Zanzibar, wewe utakuwa umejiondoa kwenye malalamiko, na umeitoa wizara kwenye malalamiko. Tutajua tuna wanafunzi wangapi kutoka Zanzibar ambao watapata mikopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Tanzania.Nitakuomba sana hili ulichukue, ulifikirie na ulipatie maamuzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la tatu ambalo ninaomba kulizungumzia hapa ni suala la uwekezaji hasa katika vyuo vikuu. Kumekuwa na malalamiko ya muda mrefu, na Serikali hapa ilifanya jambo kubwa na lenye nia njema kabisa. Suala la uanzishwaji wa sekondari katika kila kata lilikuwa ni suala muhimu, limetekelezwa na Serikali kwa kiasi fulani, hivyo hivyo, lakini lipo na limetekelezwa. Sasa, kuna ukanda huu wa Kusini, baada ya kuanzishwa sekondari hizi za kata imepelekea wanafunzi wengi kujiunga na sekondari za O-Level na A-Level. Udahili wa wanafunzi kwenda vyuo vikuu umeongezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini miaka mingi mmekuwa mkisema Chuo cha Ualimu kilichoko Mtwara mtakigeuza kiwe Chuo Kishiriki cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mpaka leo suala hili halijachukuliwa hatua yoyote. Tunakuomba Mheshimiwa Waziri, kwa heshima zote mama yangu Ndalichako ukija hapa utueleze, kile chuo ni lini kitachukuliwa hatua ya kugeuzwa sasa kuwa Chuo cha Ualimu na sasa kiende kwenye kuwa chuo kishiriki kisaidie ule ukanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mikoa mitatu, Lindi, Mtwara na Ruvuma, huu ni ukanda mmoja, mikoa hii imefuatana kabisa, lakini hakuna hata chuo kikuu kimoja cha Serikali. Tunakuomba sana suala hili lichukuliwe hatua na ni vyema utakapokuja hapa sasa utuambie ni lini suala hili litachukuliwa hatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa kusema kwamba hakuna elimu bora bila huduma bora za walimu. Muda umefika sasa kuwaonea huruma walimu, wamehangaika muda mrefu sana. Imefika muda sasa kuboresha maslahi ya walimu katika nyanja zote, ukae pamoja na TAMISEMI uboreshe, uone kwa namna gani mtashirikiana kuikwamua kada hii ya walimu katika sekta au katika maslahi ya walimu. Walimu hawa ni wetu, ni Watanzania wenzetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wengi wamekuwa wakisema, hata wewe leo usingekuwa Waziri wa Elimu kama hujapitia kwa walimu. Ulianza darasa la kwanza mpaka ulipofika, waliokuwezesha hapo ni walimu. Hebu wahurumie walimu, waonee huruma walimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninaomba mchango wangu kwa leo uwe huo, ninaamini kwamba mawazo yangu haya yatasaidia kwa namna moja ama nyingine kufikia pale tunapopahitaji, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Spika, nashukuru kuwa miongoni mwa wachangiaji wa Wizara hii kubwa, Wizara ya Fedha na Mipango.

Mheshimiwa Spika, kabisa niungane na waliopita kuzungumza japo kwa ufupi au hata kuitaja barabara ile inayokwenda Kigoma kutoka Nyakanazi kwamba ni barabara muhimu na ni barabara ambayo nilipata fursa na mimi kwenda kwenye msiba ule wa kumsitiri Mwalimu wetu, Mbunge mwenzetu Mwalimu Bilago, nikaona mazingira yalivyo, nikaona barabara ilivyo kwa kweli inahuzunisha na inatia huruma sana.

Mheshimiwa Spika, naamini kwamba ni miongoni mwa barabara zile ambazo siku za mvua magari yanazama kwenye mito ikisubiri siku mbili au tatu wananchi wapate kupita kwa ajili ya kufika Kigoma na maeneo mengine ya kule. Kwa hiyo, ni vyema Wizara ya Fedha barabara ile waingalie kwa jicho la huruma sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, ukiangalia kitabu cha Kamati ukurasa wa 26 kumezungumzwa hizi milioni 50 kila kijiji, lakini ikiwa Serikali ya Awamu ya Tano hii inakwenda ukingoni tena tunakwenda kwenye mwaka wa tatu sasa, Waziri wa Fedha anakuja hapa kutuaminisha kwamba sasa kumetengwa jumla ya bilioni 60 ambazo zinakwenda kufanya utafiti yaani pilot studies kwa ajili ya kuona kwamba vipi tutafanikisha mpango huu wa milioni 50 kila kijiji.

Mheshimiwa Spika, hii maana yake ni kwamba, kwa miaka mitatu sasa bado tunakwenda kwenye pilot studies, kwenye kufanya research kuona vipi tutafanikisha utoaji wa fedha hizi, lakini tukumbuke kwamba milioni 50 kila kijiji ni ahadi ya Rais na imo ndani ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Hii inamaanisha kwamba wananchi Watanzania tuliwadanganya. Tuliwadanganya kwa sababu kama hadi leo miaka mitatu fedha hii haijatoka ina maana hakuna dalili na bado tunakwenda kufanya study, bado hakuna dalili ya Watanzania kupata fedha hii na ni wazi kwamba huu ulikuwa ni usanii wa kisiasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la tatu ni kuhusu mfumo wa kodi ambao mara nyingi tumekuwa tukiuliza na umekuwa ni wenye utata kwa kiasi kikubwa sana. Naomba nitoe maelezo kwamba mifumo ya kodi kwenye bandari hizi za Afrika Mashariki inatofautiana sana kutokana na interest za nchi na tozo ambazo zimo katika kila nchi ambayo inahusika na Bandari hizo husika. Kwa mfano, container ambalo lina futi 20, ina uzito sawa, thamani sawa, bandari ya Dar es Salaam wanatoza dola 240 wakati bandari ya Mombasa wanatoza dola 70 tu, hii ni tofauti kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kontena ambayo urefu wa futi 40, bandari ya Dar es Salaam wanatoza dola 420, wakati bandari ya Mombasa wanatoza dola 105, hii ni tofauti. Gari ambayo ina thamani ya dola 10,000 bandari ya Dar es Salaam wanatoza 1.6% wakati Bandari ya Mombasa inatoa 0.8% hii ni tofauti kubwa. Kuonesha kwamba utofauti huu haupo tu baina ya Bandari ya Zanzibar ambayo kila siku inakandamizwa, inaonewa kwa sababu tu ya mfumo huo wa kodi lakini suala hili haligusi bandari nyingine za Mombasa na bandari nyingine ambayo ziko ndani ya Afrika Mashariki na Kati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka kusema nini, nitakachokizungumza hapa, tumekuwa tukiuliza mara nyingi kwamba, vipi mifumo hii ya kodi ambayo inaenda kuua uchumi wa Zanzibar, inaenda kuua bandari ya Zanzibar, lini itapatiwa ufumbuzi na lini Wanzanzibari wataachwa waendeleze masuala yao ya biashara bila kulazimishwa kwamba eti wafuate mfumo wa TANCIS,kwa sababu tofauti hii zipo kila mahali.

Mheshimiwa Spika, tumekuwa tukilalamikia suala hili sana, nataka nioneshe sisi kama Wabunge kutoka Zanzibar kwa sababu sisi Wabunge kutoka Zanzibar Jimbo letu ni kama Zanzibar. Kwa sababu kama Mbunge siwezi kuzungumzia suala la maji Jimboni kwangu, siwezi kuzungumzia suala la kilimo jimboni kwangu, kwa hiyo, jimbo langu ni Zanzibar sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumezungumzia masuala hapa, hata leo tumezungumzia masuala ya kodi ya umeme. Sisi tumeuziwa umeme na TANESCO lakini tumeuziwa kwa bei ambayo si sahihi. Tumekuwa tukilalamikia, Serikali kupitia Wizara ya Fedha inatuambia tunazungumza. Tumekuwa tukizungumzia tozo za bandari haziko katika mazingira sahihi kwa bandari ya Zanzibar. Kodi zile zinaua bandari ya Zanzibar, tumeambiwa suala hili tunazungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumezungumza masuala ya vyombo ya moto, tumelalamika sana, leo ni vitu vya ajabu sana, leo mtu kutoka Burundi, mtu kutoka Kongo, mtu kutoka Zambia anaingia Tanzania na gari lake, anatumia miezi miwili kwa kujaza tu fomu pale mpakani, halafu anaweza kuongeza tena miezi miwili lakini mtu kutoka Zanzibar huu ni uonevu, udugu uko wapi? Mtu kutoka Zanzibar hana uwezo wa kuleta gari Tanzania Bara akaweza kutumia. Huo udugu wa damu uko wapi?

Mheshimiwa Spika, kila siku tunasema udugu wa damu, tunadumisha, tunadumisha ndio ni sahihi, hakuna anayekataa umoja lakini umoja uwe na nia njema. Tukizungumza haya tunaambiwa tunazungumza, tutazungumza mpaka lini? Miaka 54 ya Muungano, kero hizi zimeanza muda mrefu zipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kila siku akija Waziri wa Fedha tutazungumza, akija Waziri mwingine yoyote, tunazungumza, tunazungumza mpaka lini? Juzi hapa tumelalamikia masuala ya Akaunti ya Pamoja ya Fedha. Leo tumeona kwenye kitabu kwa ajili ya Tume ya Pamoja ya Fedha inafanya kazi gani? Mheshimiwa Mpango kwenye hotuba yake amesema kabisa kwamba, tayari tume ile imekamilisha kufanya utafiti. Sasa hii fedha iliyotengwa hapa ya nini? Maana amesema mshahara ni zero points.

Mheshimiwa Spika, sasa kama kuna mshahara zero points sasa ile bilioni ngapi uliyoitenga imo kwenye kitabu ni ya kazi gani kama watu wamekamilisha utafiti na hii akaunti itaanzishwa lini ili tuone sasa kuna equality kwenye masuala ya mgawanyo wa fedha za muungano. Kuna equality katika makusanyo ya fedha za muungano, tujue nani anahusika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yote haya tunaambiwa tunazumgumza. Huu unaoendelea unaitwa ulaghai wa kisiasa ambao hakika kila siku unaendelea kudumaza na kuua maendeleo ya upande mmoja wa Muungano. Kwa sababu hizi zote ambazo nimezizungumza hapa hizi ndizo channel za maendeleo katika Taifa, katika nchi. Zanzibar ni nchi ya visiwa inajitegemea kimaendeleo ina Serikali yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuendelee kuangalia, Mheshimiwa Mpango aje atujibu sasa haya masuala ya kodi bandari na tozo. Leo Zanzibar pale unasafirisha hata vitenge 10, kanga 10 au tano, TV moja ya kuja kuangalia mwenyewe ukija pale unapigwa difference. Leo wafanyabiashara wote soko lote, tulilokuwa pengine lingekuwa soko linaloenda kuchukua bidhaa Zanzibar kuleta maeneo ya Tazania Bara mikoa tofauti leo wamehamia Uganda.

Mheshimiwa Spika, tukitoka hapo nje tu hapo wajasiliamali wapo wanasema hili shati linatoka Uganda hili, shati hili linatoka Kongo, kitenge hiki kinatoka wapi, wale wote walikuwa wanakuja Zanzibar wanachukua bidhaa na kuleta Tanzania Bara kuuza, leo soko lile wafanyabiashara wa Zanzibar limekufa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho niseme mwisho leo tunaambiwa hapa bidhaa zinazotoka na inasikitisha sana maji, kama kuna maji Zanzibar yanayozalishwa na kiwanda kilichopo Zanzibar hayaruhusiwi kuuzwa Tanzania bara. Inaashiria nini? Tulipiga marufuku sukari wakasema Zanzibar haitoshi. Hivi vifaa vyote, bidhaa zote zinazouzwa Tanzania Bara, zinazozalishwa Tanzania Bara ndio zikavushwa Zanzibar?

Mheshimiwa Spika, sio kweli huu ni usanii wa kisiasa ambao kimsingi haukubaliki, lakini tukisema tunazungumza hivi tunazungumza na nani? Tunazungumza na mtu ambaye hana mamlaka, mtu ambaye hana uwezo wa kusema, mtu ambaye wanaenda kuzungumza naye asubuhi jioni wanamwona mpuuzi wanasema achana naye yule. Sisi tunaendelea na mambo yetu, hili haliwezekani.

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumze hayo kwa masikitiko makubwa nikijua kwamba Wizara ya Fedha na Mipango itakuja na majibu ya haya sasa kuona kwamba vipi tunaenda kutatua hizi changamoto ambazo tumezizungumza hapa, kwa nia njema kabisa na kwa nia njema kwa nchi hizi. Hizi story za kwamba tunazungumza, tunazungumza at least zifikie mwisho sasa tuone kwamba maendeleo haya yanakuwa kwa Tanzania nzima na sio upande mmoja wa Muungano.

Mheshimiwa Spika, Zanzibar haina pa kwenda, Zanzibar hatulimi mahindi, Zanzibar hatulimi nyanya, Zanzibar hatulimi, yote tunatumia kutoka Tanzania Bara na yanaingia vizuri tu, lakini leo kinachozalishwa Zanzibar unaambiwa lazima tukifikie kiwango hiki, lazima tutoe hiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi nichangie mawili, matatu kuhusiana na hotuba ya Waziri Mkuu. Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchangia hotuba hii ya Waziri Mkuu kwa kuanza kuchangia katika sehemu
ambayo mara nyingi tumekuwa tukiisemea au imekuwa ikizungumzwa humu kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wazanzibari mara nyingi wamekuwa wakijiuliza hatma ya Mashekhe hususan kupitia Wizara ya Katiba na Sheria, lakini leo nimeamua kulizungumza hili kwenye hotuba hii ya Waziri Mkuu tukiwa na matumaini kwamba kilio hiki sasa kinaweza kikasikika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni juzi tu kupitia Mahakama Kuu ya Zanzibar, Jaji wa Mahakama Kuu ya Zanzibar alinukuliwa kupitia vyombo vya habari akisema kwamba Mashekhe wale wameletwa huku kwa makosa na sasa wanatakiwa warejeshwe Zanzibar kwa namna yoyote itakavyokuwa. Kwa bahati mbaya sana hatukuona hata dalili ya namna ambavyo kuna ushughulikiwaji wa suala lile kuona kwamba Mashekhe wale sasa watarejeshwa Zanzibar na kama ni kuhukumiwa basi watahukumiwa Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni miaka minne sasa Mashekhe wale wako ndani, haijulikani tatizo ni nini isipokuwa kinachoonekana pale ni mihemko au hisia tu za kisiasa ambazo zimewafanya Mashekhe wale wanaendelea kusota ndani. Miaka minne imetosha, kama masuala ya upelelezi hayajakamilika kwa nini basi wasipewe dhamana wakaendelea kufuatiliwa wakiwa pamoja na familia zao na huku kesi ile inaendelea? Miaka minne ni mingi sana, naamini kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu ni kubwa, Waziri Mkuu ni mtu mkubwa katika Serikali hii, ndiyo msimamizi mkuu wa shughuli za Serikali anaweza akasikia vilio hivi vya Wazanzibari kuona kwamba Mashekhe wale ni sehemu ya Watanzania wanasikilizwa na wanaachiwa na wanaendelea kuwa huru pamoja na familia zao, hilo ni moja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, katika mambo ambayo tutayapitisha kupitia Bajeti ya Waziri Mkuu hii ambayo tunaijadili sasa ni pamoja na kujadili Fungu Namba 27 ambalo linagusa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa. Ni jambo ambalo halikujificha, liko wazi kwamba Msajili wa
Vyama vya Siasa sasa ameamua kwa makusudi kabisa kuingilia na kupandikiza migogoro ndani ya vyama vya siasa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema haya kwa sababu ofisi hii majukumu yake yamezungumzwa ndani ya sheria inayoongoza vyama vya siasa ya mwaka 1992. Moja, kusimamia kumbukumbu za vyama vya siasa; pili, kusajili vyama vya siasa ambavyo vimekidhi matakwa ya sheria hiyo;
tatu, ni kufuta chama cha siasa ambacho kimekwenda kinyume na taratibu hizo ambazo zimezungumzwa ndani ya sheria pamoja na majukumu mengine lakini haya matatu ndiyo majukumu makuu ya Ofisi hii ya Msajili wa Vyama vya Siasa. Kwa bahati mbaya sana Msajili wa Vyama vya Siasa leo amejipa majukumu mengine, sijui kayatoa wapi, madaraka haya sijui ameyatoa wapi ya kuona kwamba sasa ana mamlaka ya kuchagua chama cha siasa kiongozwe na nani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania wote wanafahamu, Watanzania wote wana akili timamu na wanafahamu kwamba Profesa Lipumba alijiuzulu Agosti, 2015 kwa kuandika barua ya kujiuzulu kabisa. Baada ya miezi kumi Profesa Lipumba anasema anarudi katika nafasi yake ya
Uenyekiti. Katika Katiba hii ya Chama cha CUF hakuna sehemu yoyote ambayo inatoa mamlaka kwamba mtu anapojiuzulu baada ya muda anaandika barua kwamba narudi kwenye nafasi yangu, hakuna. Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa ilipokea barua na minutes zote za vikao
kwamba sasa wanaokaimu nafasi ya Mwenyekiti ni hawa. Chama cha CUF kupitia Baraza Kuu la Uongozi kikaunda Kamati ya Uongozi ya Chama na kupeleka kila kilichotakiwa kwa Msajili wa Vyama vya Siasa kutambulisha kwamba sasa wanaoongoza majukumu ya Mwenyekiti ni hawa kwa muda wa miezi kumi. Baada ya miezi kumi Profesa Lipumba anaandika barua ya kurudi kwenye nafasi yake ya Uenyekiti, very shameful. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Jaji akaamua kwa makusudi kabisa kwa sababu eti anataka kuivuruga CUF kutambua kurudi kwa Profesa Lipumba bila kufuata sheria, kanuni, Katiba ya nchi, kwa matakwa yake akaamua sasa kupandikiza mgogoro ndani ya Chama cha CUF. Chama cha CUF hakina mgogoro.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niweke sawa, mama yangu mmoja pale alifananisha mgogoro wa Chama cha CUF na ndoa ya mtu na mke wake, akasema kwamba mambo ya mtu na mkewe yanamalizwa chumbani. CUF haikuwa na mgogoro, mgogoro huo ulimalizika mapema Profesa kajiuzulu, Mkutano Mkuu wa Chama ukaitishwa, quorum ikaridhika kwamba Profesa kajiuzulu kama Katiba inavyozungumza, ya nini leo Msajili kufanya haya? Tena angalia sasa cha kushangaza, Msajili wa Vyama vya Siasa anatambua vikao vile na mkutano ule ulikuwa halali lakini anasema maamuzi yake ni haramu. Maana yake ni sawa na kusema nguruwe haramu, lakini mchuzi wake halali, hii haiingii akilini, kwa makusudi akaamua kufanya alivyofanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, juzi cha ajabu zaidi Msajili huyo wa Vyama vya Siasa alikuja kwenye Kamati, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria, kama Mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria tulimuuliza sheria hizi umezitoa wapi? Nashukuru Kamati yangu imeandika kama miongoni mwa maazimio, ukurasa wa 30, Kamati pia inaagiza Ofisi ya vya siasa, si jukumu lake. Migogoro ya vyama vya siasa viachiwe vyama vya siasa, Msajili asiwe ni sehemu ya mgogoro wa chama cha siasa. Chama kina taratibu, sheria, Katiba na kanuni zake, leo iweje yeye apange? Ni ajabu! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, juzi anatushangaza hapa sasa, anakuja kwenye Kamati anajitetea siku ya pili anasema anamtangaza kwamba sasa Sakaya ni Kaimu Katibu Mkuu. Sakaya alishasimamishwa uanachama, Sakaya alishasimamishwa uongozi, leo kwa sababu tu una mambo
yako unayatafuta unakuja …
Mheshimiwa Sakaya, Mbunge wa Kaliua, anamtambua kwamba eti ni Kaimu Katibu Mkuu wa Chama, aibu! Katibu Mkuu wa Chama yupo anafanya shughuli zake za kisiasa kama kawaida unashawishiwa, wewe umepanda shetani gani? Aliyekushawishi ni nani? Kakupandikiza nini? Kama kuna mtu anakusukuma au anakushawishi, wewe ni Jaji unapaswa uwe na heshima. Tunasema kama ana ndoto ya kufikiria kwamba Chama cha CUF kinakwenda kufa mikononi mwake, Chama cha CUF hakifi, kitaendelea kuweko imara na kitaimarika zaidi. Kama anahisi kwamba Chama cha CUF kinakwenda kufa basi hilo alisahau kabisa (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kidogo suala la utekaji. Nchi hii haiko salama tuseme kweli. Asubuhi watu wameomba miongozo umewakatalia ni suala la hatari. Kama unakumbuka kila siku zikienda mbele hali hii inazidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ulinisimamisha kidogo naomba dakika yangu moja ambayo ulinisimamisha…
NAIBU SPIKA: Zilikuwa ni sekunde 10 ambazo zimeshaisha.
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, tulishuhudia Salma Said, Mwandishi wa DW alitekwa uwanja wa ndege...
NAIBU SPIKA: Haya ahsante sana Mheshimiwa.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Usimamizi wa Matumizi ya Fedha za Umma katika Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2017
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi, nichukue fursa ya kuwapongeza Wenyeviti wote wawili wa Kamati ya LAAC na PAC kwa kuwasilisha ripoti kwa ufasaha na ufanisi mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nirudi kwa kaka yangu pale Mheshimiwa Allan Kiula kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilitoa maelezo juu ya fedha ulizodai kwamba zilipelekwa Zanzibar na Serikali ilijibu kwamba, hakuna fedha waliyopokea kwa, ile fedha ambayo ilitajwa na CAG. Hii fedha… (Makofi)

MHE. ALLAN J. KIULA: Taarifa.

MHE. JUMA KOMBO HAMAD:… hii fedha hakuna, otherwise utupatie document ambazo zinathibitisha kwamba fedha ile ili…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Juma Kombo kuna Taarifa. Mheshimiwa Kiula.

T A A R IF A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Juma Kombo unaipokea Taarifa hiyo?

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, tuache unafiki na uwongo. Hii fedha Waziri wa Fedha alikuja hapa akatuambia kwamba fedha hii ilikwenda Zanzibar na, baada ya kushindwa kuthibitisha ndio mara nyingine akaja tena hapa akatuambia kwamba, fedha hii imekusanywa Zanzibar.

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, tusilishane uongo kwa jambo ambalo halipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye hoja...

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Kombo naomba ukae kidogo.

Waheshimiwa Wabunge, twende sawasawa, kwanza tusikilize kwa sababu tunajibizana kwa michango na kwa taarifa iliyoko hapa mbele, tuwe tunasikilizana vizuri ili tusikatishane pale ambapo hakuna sababu. Tusikilizane vizuri, mtu anayechangia kwanza umsikilize vizuri ili unapojibu usizungumze kile ambacho hajasema tunafikia hapo.

Nafikiri hilo limeeleweka, tusikilizane vizuri ili tuweze kwenda sawasawa, tusikilizane kwa makini. Kama unataka kumjibu mwenzio msikilize kwa makini. Mheshimiwa Juma Kombo.

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, kuna falsafa ya uongo ambapo muongo anatakiwa awe na kumbukumbu, ili asisahau kile ambacho kwamba anakizusha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye hoja na nianze na ku-declare ni Mjumbe wa Kamati ya LAAC. Na nianze na upungufu ambao tuliuona wakati wa kukagua hizi Halmashauri kwamba pungufu moja ambalo tumeliona ni suala la upungufu wa watendaji katika Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika changamoto kubwa ambayo tunaenda nayo kama Tanzania ni suala la ajira, lakini kila halmashauri ambayo ilikuwa inakuja mbele ya kamati basi unakuta kama kuna kila kitengo kina upungufu wa watumishi au wafanyakazi. Niombe kwa Serikali na TAMISEMI kwamba, suala hili ni vyema walishughulikie kwa sababu, Watanzania wengi hawana ajira na kama hawana ajira kila Halmashauri inayokuja pengine ina upungufu wa asilimia zaidi ya 50 ya watendaji katika Halmashauri, hiki ni kitendo cha aibu kwa Tanzania kwamba, vijana wako wamemaliza chuo, wamemaliza kusoma, lakini nafasi za ajira Tanzania kwenye Halmashauri zetu zipo, lakini kila siku wanapiga kelele ajira hakuna, ajira hakuna, lakini nafasi za vijana kuwaajiri zipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali kupitia TAMISEMI ambao ndio responsible kwa Halmashauri zetu walitizame hili kwa kina na kwa sababu vijana wapo ambao hawana ajira, hawana kazi, basi wawaajiri ili waende wakatumikie wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu nyingine ambayo naomba niizungumze ni suala la udhibiti wa mfumo wa wa fedha, Kitengo cha Udhibiti wa Fedha za Ndani. Na hapa pia, kuna changamoto hiyo hiyo kwamba, katika kila Halmashauri, takribani Halmashauri 50 ambazo sisi tumejaribu kuzihoji, basi unakuta kitengo kinahitaji watu wanne, lakini ama kuna mtu mmoja, ama kuna wawili.

Mheshimiwa Naibu Spika, huu ni udhaifu mkubwa ambao unajitokeza, lakini pia, kitengo hiki hakina facility yoyote. Kina upungufu wa watendaji, kina upungufu wa fedha, kina upungufu wa vifaa kama vile gari, kamera na vitu vingine. Kwa kweli ni jambo ambalo na ukizingatia Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani ni kitengo muhimu na ndio jicho la halmashauri, ndio jicho la Mkurugenzi wa Halmashauri. Sasa kama hawezeshi na bahati mbaya sana ya Halmashauri nyingi utakuta mkurugenzi anamfanya kama yule Mkaguzi wa Ndani kama ni adui, kwa maana ya kwamba hataki kumpa taarifa za kina, kwa hiyo, hawezi kumuwezesha kwenye kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo na kwenye vitabu vya fedha wakati mwingine anamwekea vikwazo mbalimbali na kwa sababu yuko chini yake inakuwa Mkaguzi wa Ndani hana nguvu za kuweza kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni vyema Serikali ikaanza kufikiria kwamba wale watu Wahasibu, Wakaguzi wa Ndani kama ikiwezekana na inayowezekana basi wawe nje ya mfumo wa uajiri wa Halmashauri ili waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi, waweze kuwakabili Wakurugenzi na kuwahoji juu ya masuala ya matumizi ya fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni kutokutekelezwa kwa maagizo ya Kamati. Utakuta kila Halmashauri kama imepewa maagizo kumi, basi ikija imetekeleza maagizo mawili na hii ni aibu sana kwamba Kamati ya Bunge ambayo ipo kwa niaba ya Bunge imetoa maagizo kwenye Halmashauri, maagizo kumi, lakini Halmashauri inakuja mara nyingine au mwaka mwingine imetekeleza maagizo mawili au matatu. Kwa kweli hii ni dharau kubwa na Halmashauri lazima TAMISEMI isimamie vizuri suala hili, Ofisi ya CAG isimamie vizuri suala hili, lakini na Bunge litoe maagizo makali na maazimio makali juu ya suala hili la utekelezwaji wa maagizo ya Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ya Bunge ni Bunge, kwa sababu, Kamati ya Bunge ipo kwa niaba ya Bunge haipo kwa niaba kwamba labda ni Mheshimiwa Vedasto au ni Mheshimiwa Mama Kaboyoka, hapana, ni Bunge. Kwa hiyo, maagizo yanayotolewa pale yanatolewa na Bunge. Sasa halmashauri kwenda kukaa kitako wakajishughulisha nyingine bila kutekeleza maagizo yale hii kwa kweli si jambo jema na ni jambo la aibu ambalo mwisho wa siku linakuwa halileti ufanisi mzuri kwa maendeleo ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo naomba kulizungumza… eeh! Vipi sasa? Hata tano bado!

Mheshimiwa Naibu Spika, ni suala la Mfuko wa Wanawake, suala hili lina changamoto nyingi, juzi hapa/ mwaka jana tumepitisha sheria na uko mfumo wa 4:4:2 kwamba asilimia 4 iende kwa waawake, asilimia nne kwa vijana na asilimia mbili kwa watu wenye ulemavu kwa kweli, ilikuwa ni jambo zuri na jambo jema. Lakini halmashauri zote ambazo tumezikagua zimebakia na madeni makubwa katika kipindi hiki kabla ya sheria hii kuipitisha. Ni vyema Serikali itafakari upya kama ikiona kwamba ni jambo la busara basi madeni yale ya nyuma, sio mikopo maana kuna vitu viwili tofauti, kuna mikopo ambayo wamekopa, lakini kuna na madeni ambayo yamebebwa na Halmashauri ambayo kimsingi hayalipwi wala hayatalipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iangalie utaratibu mzuri hapa wa kuweka jambo hili, ikiwezekana na ikionekana ni jambo la busara, basi Halmashauri, Taasisi za Serikali zisamehewe madeni yale ya nyuma na sasa tuanze upya na mfumo huu wa 4:4:2 ambao upo kisheria. Na mfumo huu ukisimamiwa vizuri basi tutaweza kuleta ufanisi kwa makundi haya ya akinamama, vijana pamoja na watu wenye ulemavu kuliko kuhangaika sasa na madeni yale ya nyuma ambayo kimsingi hayalipwi na yanatumiwa kama ni muamvuli au ni kichaka cha kujificha kwa hii 4:4:2 ambayo ipo sasa hivi kisheria. Naomba Serikali iliangalie hili vizuri na ikiwezekana walifanyie utaratibu, ili liweze kwisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende na sakata hili la Halmashauri ya Kaliuwa. Kaliua kuna kashfa kubwa na fedheha kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika watumishi 66 ambao walibainika na ripoti ya CAG kwamba wamehusika na ubadhirifu wa shilingi bilioni 3.3 ni watumishi wawili tu ambao hadi sasa wamechukuliwa hatua, bahati mbaya sana na hapa nakuwa najiuliza inawezekana wengine wasiridhike, lakini huu ndio ukweli. Nakuwa najiuliza huo utakatifu wa Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli uko wapi? Kwa sababu ni lazima tujiulize hata ikiwa kuna watu litawananihii, lakini huo utakatifu unaozungumzwa humu tena na Wabunge wa Serikali hii uko wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, tuishauri Serikali ili iwachukulie hatua watu ambao waepiga fedha za Serikali. Kama shilingi bilioni 3.3 zimepigwa halafu mtumishi/ Mkurugenzi ambaye yuko pale kipindi hiki fedha hizi zinapigwa, alikuwa Mtendaji baadae akawa Mkurugenzi leo ni Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halafu tunakuja hapa tunajisifu kwamba sisi ni watakatifu, Rais anatumbua. Hebu tumuone basi, leo kwa ripoti hii ambayo imemtoa Mkurugenzi huyu kwa Tume ya Uchaguzi ambaye anaitwa Athumani Kihamia, tumuone Rais Dkt. John Pombe Magufuli katoka na kauli na leo kamtumbua. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia mawili, matatu katika Wizara hii muhimu, Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana wakati tuko katika Bunge la Bajeti, Mheshimiwa Waziri aliyekuwa na dhamana muda huo au mwaka jana aliwaambia Wabunge wa Bunge hili Tukufu na Watanzania kwa ujumla kwamba jembe la mkono litakuwa historia, lakini jembe la mkono litaonekana au litatumika katika maeneo matatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo ambalo jembe la mkono litatumika kwa mujibu wa Mheshimiwa Waziri wa kipindi hicho alisema jembe la mkono litaonekana kwenye majumba ya kumbukumbu (makumbusho), alisema jembe la mkono litatumika kwa ajili ya kuchimbia makaburi lakini alisema jembe la mkono litaonekana kwenye Nembo ya Chama cha Mapinduzi na kwamba jembe la mkono halitatumika tena kwa shughuli za kilimo na alisema haya kwa sababu sasa Tanzania inaelekea kwenye uchumi wa kati na uchumi wa viwanda. Kwa hiyo, kama tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda lazima tuboreshe kilimo na lazima tuwe na zana bora kwa ajili ya kuendeleza kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufanya winding-up ya hotuba yake atueleze hadi sasa shughuli hii au azma/dhamira hii tumefika katika eneo gani. Tumevuka pale ambapo tulikuwa tunahitaji kuvuka au bado Watanzania wanaendelea kuhenyeka na kuumia kwa kutumia jembe la mkono. Nadhani ni wakati sasa wa kupata angalau maelezo ya Serikali kupitia Wizara hii kuwaeleza Watanzania tumefikia katika hatua gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nataka kuchangia ni la uvuvi. Tanzania tumebarikiwa kuwa na eneo kubwa la bahari lakini Tanzania ni pamoja na Zanzibar. Zanzibar ni visiwa ambavyo vimezungukwa na eneo lote la bahari, bahari kubwa ni bahari ya Hindi. Kiuhalisia ni kwamba hatujaitumia bahari ipasavyo katika masuala ya uvuvi wa samaki lakini katika kutumia resource zilizomo ndani ya bahari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimtaarifu Waziri kama atakuwa hajui, lakini nina imani anajua kwa sababu naamini ni mlaji wa samaki. Hivi Waziri anajua kwamba hapa Dodoma tunakula vibua kutoka China?
Hivi Waziri anatambua kwamba tunakula vibua kutoka South Africa? Namwomba Mheshimiwa Waziri atambue hili, hivi sisi Watanzania tuna sababu gani kwa eneo kubwa la bahari ambalo limejaa resource ya samaki kwa nini hadi leo tunakula vibua vya South Africa. Mheshimiwa Waziri tunaomba na eneo hili atufafanulie kidogo tuone uhalisia na ukweli hasa wa matumizi ya bahari yetu ambayo tunayo katika Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao la korosho. Wachangiaji wengi wamezungumza hapa kwamba zao la korosho linastawi zaidi na sana pembezoni mwa Ukanda wa Bahari au Ukanda wa Pwani. Natambua kwamba Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi si miongoni mwa Wizara za Muungano lakini kila siku hapa tunajivunia kwamba Wizara zilizoko katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Wizara ambazo zinafanya kazi kwa niaba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zinafanya kazi kwa pamoja. Hebu tueleze hivi mmekaa lini kusaidiana na Wizara ambayo iko kwenye Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika masuala ya utafiti na kuangalia labda kwa kiasi gani zao la Korosho tunaweza kuliimarisha kwa upande wa Zanzibar na likawa ni sehemu na mbadala wa zao la karafuu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikupe pole na nimwombe Mwenyezi Mungu akujalie uendelee kuwa na afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la demokrasia na utawala bora na haki za binadamu nchini mwetu linapotea kila siku. Leo Tanzania, wananchi wanatekwa na kuuawa, wanasiasa na wanaharakati pia wanahujumiwa na Tanzania hata waandishi wa habari na vyombo vya habari hawako salama. Hali hii haileti afya kwa Taifa. Tunaiomba sana Serikali na Wizara ya Mambo ya Ndani, usalama kwa wananchi ni jambo muhimu kwa mustakabali wa amani ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza kuna vijana sita Pemba wametekwa na wa watatu kati yao hadi sasa hawajulikani walipo. Vijana hawa wametekwa Pemba Jimbo la Mtambwe na hadi sasa vijana watatu hawajaonekana nao ni Thuwein Nasor Hemed (30), Khamis Abdallah Mattar (25), Khadid Khamis Hassan (30). Tunaomba Serikali itupe jibu, je vijana hawa wapo wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la sukari ya Zanzibar kuzuiwa kuuzwa Tanzania Bara sio haki na ni uonevu mkubwa Zanzibar na maendeleo ya Wanzanzibari, jambo hili halileti afya kwa Muungano wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kodi hasa katika Bandari ya Dar es Salaam ni tatizo na ni kero kubwa, mustakabali wa biashara kwa wafanyabiashara wa Zanzibar. Tunaiomba sana Serikali kulifanyia kazi suala hili ili kuleta nafuu kwa wafanyabiashara wa Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, msamiati wa kero za Muungano sasa imekuwa hadithi zisizo na tija kwani kila siku kero hizi zinaongezeka na kuzidi kudumaza maendeleo ya Zanzibar. Kama suala hili halikupatiwa ufumbuzi linaweza kutikisa Muungano hatimaye kuvunjika kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kuwaweka watu mahabusu kwa muda mrefu bila kuwafikisha Mahakamani sio jambo jema. Suala la Mashekhe wa Uamsho na dhuluma wanayofanyiwa sasa imekuwa haivumiliki tena. Ni lazima Serikali kutoa jibu juu ya Mashekhe hawa. Sasa ni miaka mitano wapo ndani bila kufikishwa Mahakamani, hii sio haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni uonevu uliovuka mipaka na uvumilivu unafika mwisho. Ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na nimshukuru Mwenyezi Mungu nami kunipa fursa hii ya kupata kuchangia angalau mawili matatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha atakapokuja kufanya majumuisho, atujibu masuala au mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ni mambo ambayo yamekuwa yakileta mkanganyiko na utata katika taarifa mbalimbali ambazo zinatoka hususan kwenye vyombo vya habari na kwenye mitandao ya kijamii. Sasa ili tujiridhishe, naye kwa sababu ndiye msemaji wa Wizara ya Fedha, basi atakapokuja ana wajibu wa kutuweka wazi ili tujue kipi ni kipi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni mgao wa Zanzibar kwenye mapato ya Muungano, kwa sababu kila siku tunapiga kelele hapa kwamba kuanzishwe account ya pamoja ya fedha ili suala hili lisiwe na utata. Ikianzishwa account ya pamoja ya fedha ina maana ni kusema kwamba mgao utakuja kwenye bajeti na itaonekana kwamba haya ndiyo makusanyo ya Muungano na huu ndiyo mgao kwamba Tanzania Bara ilipata hiki na Zanzibar ilipata hiki, kwa hiyo hilo ni suala la kwanza ambalo namuomba sana Waziri wa Fedha atakapokuja aje atujibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, ni hilo la mgao lakini sasa kupitia mikopo ya nje, kwamba suala la mikopo ya nje ni suala la Muungano sasa aje atuambie Tanzania, Mwaka 2018/2019 na 2019/2020 inategemea kukopa nini na ilikopa nini na Zanzibar ilipeleka nini. Ninachomuomba sana aje awe mkweli kwa sababu ilitokea mwaka jana kusema katika ile 1.5 trillion kuna bilioni kadhaa zilikwenda Zanzibar, baada ya kutamka hivyo Waziri wa Fedha wa kule akasema kwamba huku hakuna shilingi tano ambayo imekuja sasa utakapokuja Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Mpango uje utuambie uhalisia na ukweli ulivyo kwenye mikopo ya nje inayohusu Muungano, umekopa kiasi gani na Je, katika mkopo uliokopa ile 4.5 umeipeleka? Uje utuambie na utuambie ukweli kabisa katika jambo hilo.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, jana Zanzibar kuliwasilishwa bajeti na katika bajeti iliyowasilishwa Zanzibar kukatajwa miradi mitatu na bajeti ile ikasema wazi kwamba katika miradi hii mitatu imekwamishwa na upande wa pili wa Muungano kwamba haijatekelezwa kwa sababu mkwamo huu umetokana na upande wa pili wa Muungano:

Mheshimiwa Naibu Spika, moja; suala la barabara ya Wete-Chake ambayo ina mradi wa BADEA. Hii barabara ina udhamini na ufadhili wa BADEA na bahari mbaya sana tunapofuatilia tunakuta kwamba miradi ya BADEA kwa upande wa Bara hata ukienda Mkoa wa Kagera kuna miradi kadhaa ambayo imefadhiliwa na BADEA lakini barabara hii moja kutoka Wete-Chake ambayo ni kilometa hazizidi 40 mradi huu Mheshimiwa Mpango umeletewa barua ukakumbushwa unatakiwa uweke sign tu kwa ajili ya utekelezaji wake lakini umeshindwa kuweka sign. Umeshindwa kwa sababu hauna interest na hii barabara, lakini wewe ujue Mheshimiwa Mpango wewe ni Waziri wa Fedha inawezekana Wizara ya Fedha siyo ya Muungano lakini unasimamia fedha ambazo ni za Muungano, unasimamia Benki Kuu ambayo ni ya Muungano, unasimamia Hazina ambayo inadhibiti fedha ambayo ni jambo la Muungano. Waziri unapojivua ukasema kwamba mimi ni Waziri wa upande mmoja wa Tanzania Bara na ukajaribu kujikita zaidi kwenye mambo yanayohusiana na Tanzania Bara hapa utakuwa unapotea Kaka yangu na siyo sahihi kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati unasimamia jambo linalohusu pande mbili za Muungano lazima ulisimamie kama vile ni Waziri unayehusiana na pande zote mbili. Unapokuja mradi upo Zanzibar na unataka sign yako kwa nini unapata kigumumuzi? Mheshimiwa Waziri suala moja ni hilo uje utujibu sasa kwamba barabara hii pamoja na kukumbushwa siyo mara moja, wala mbili, wala tatu, ufadhili upo unataka sign yako kwa nini unakwama uje utujibu.(Makofi)

Mbili; suala jingine ni Airport ya Zanzibar Terminal II, kwa kweli tunasikitika sana na tunasikitika sana Mheshimiwa Mpango kuwa ni sehemu ya mtu ambae unakwambisha maendeleo ya Zanzibar. Airport hii inataka kupatiwa mkopo kwa ajili ya kufanyiwa finishing. Imeshajengwa, takribani imeshakamilika inataka kufanyiwa finishing inahitaji fedha kidogo tu, inahitaji mkopo lakini bado Wazanzibar na kupitia bajeti ya jana Baraza la Wawakilishi imesema wazi kwamba wewe ndiyo umekwamisha mradi huu. Kwa maana tunaposema ni wewe tunasema ni Serikali ya Jamhuri ya Muungano imekwamisha kwa sababu Serikali ya Jamhuri ya Muungano inakopa kwa niaba ya pande mbili za Muungano, suala la mikopo ni suala la Muungano sasa wewe unapokopa kwa uoande mmoja ukasahau upande mwingine lawama zinakuja kwako, hilo ulijue.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo suala hili nalo ukija uje utujibu mkwamo uko wapi, maana yake kuna taarifa kwamba hawa watu walikula hela, wataje! Kama mlipeleka hela zikaliwa watajwe mbona humu Bungeni wanatajwa waliokula hela? Watajwe ili tujue nini cha kufanya lakini usijibebeshe wewe msalaba ambao haukuhusu, kama haukuhusu, kama unakuhusu basi hapa tutakusulubu wewe.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la tatu na muhimu sana ni suala la Bandari ya Mpigaduri. tatizo la Zanzibar ni uchumi, tatizo hasa la Wazanzibar ni uchumi na tatizo la Zanzibar ni umaskini, kinachotukwaza sisi ni umaskini sasa umaskini huu wa Zanzibar unanasibishwa kwamba umesababishwa na upande mwingine wa Muungano. Kwamba upande mmoja wa Muungano unaweka vipaumbele vyake, unaweka miradi yake, unaweka taratibu zake zinakwenda lkini upande wa pili kule unakwamba. Kwa mfano, Bandari ya Mpigaduri ipo ni mwaka zaidi ya 10 na wafadhili wapo, wahisani wapo, wawekezaji wapo ambao wako tayari kuwekeza katika Bandari ya Mpigaduri hata Wachina karibuni miaka miwili, mitatu walikuja pale kufanya survey kutaka kuwekeza Bandari ya Mpigaduri lakini ukija ukiombwa sasa na bahari nzuri sana deni la Zanzibar ni bilioni tano, Zanzibar nzima inadaiwa bilioni tano. Bilioni mbili ni mikopo ya ndani, bilioni tatu tu ni mikopo ya nje hata tukichanga wenyewe tuna uwezo wa kulipa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mpango unadaiwa trilioni 50 na bado unakopa tunadaiwa bilioni 300, tukikuambia huu hapa mkataba sasa unataka kujazwa mara umeandikwa kwa kiarabu, ulisema ufadhili huu wa Serikali ya Oman, Bandari ya Zanzibar kwa asilimia 80 ilikuwa idhaminiwe na Serikali ya Oman ukataba ukaingiwa, uliandikwa kwa kiarabu, ulipoletewa ukasema umeandikwa kwa kiarabu ukatafsiriwa kwa Kiingereza umeletwa huna jibu hivi tufanye nini? tatizo hasa nini? Miradi imekuja imeikuta miradi kama hii lakini imetekelezwa upande mmoja wa Muungano upande ule kule visingizio haviishi, hivi ninyi hamna watu wa tafsiri wa Kiarabu katika Serikali nzima ya Jamhuri ya Muungano siyo kweli hilo nalo linahitaji jibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bandari kwa upande wa Zanzibar ni uchumi, Bandari kwa upande wa Zanzibar ni suluhisho na ni ajira. Bandari ambayo ilikuwa ijengwe na Serikali ya Oman ilikuwa na uwezo wa kuweza kuchukua meli 16 kwa mara moja. Meli kubwa, meli za kisasa ambazo wanaziita wenyewe ni 4G meli ambayo inaweza kubeba makontena 400 mpaka 800 lakini kisingizio chako na Wizara yako na wataalam wako na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha hili analizungumza wazi wazi kwamba eti ikijengwa Bandari ya Zanzibar itaua Bandari ya Tanganyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mpango, Mheshimiwa Waziri wa Fedha anasema kwamba kujenga Bandari ya Zanzibar itaua Bandari ya Tanzania Bara lakini kuimarisha Bandari ya Tanzania Bara haitaua Bandari ya Zanzibar ambayo ndiyo uchumi wa Zanzibar, hivi ninyi Watanzania Bara mna mangapi ambayo mnaimarisha? Mna madini, mna ardhi kubwa, mna kilimo, mna ufugaji, mna uvuvi, hivi kujenga Bandari Zanzibar ni kosa kwamba kuimarisha uchumi wetu leo ni kosa? Huo umuhimu wa kuwa ndugu, umuhimu wa kuimarisha Muungano uko wapi? Hivi mnatueleza nini, mnajenga taswira gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, nasikitika sana na hili niseme wazi kwamba ndani ya Bunge hili kuna Wabunge wanatokea Zanzibar na walikuwa ni viongozi wakubwa kule inafika mahali mtu ni Mtendaji Mkuu wa Serikali anasimama Bungeni humu anatumia dakika 10 anaona aibu na anaona haya kuitaja Zanzibar halafu kesho na keshokutwa mwaka 2020 eti anajinasibu anagombea Urais! Wazanzibar siyo mapoyoyo kiasi hicho watakuhukumu. Unaona haya kwa sababu unategemea Urais!

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Juma Kombo Hamad kila Mbunge ana haki ya kuchangia aonacho ni bora, huwezi ukaanza kusema mtu anaona haya unajuaje aliona haya? Kwa sababu bajeti hii ni Bajeti Kuu na Wabunge wengi tu wanazungumza habari za Majimbo yao hamna mtu anawakataza lakini wakati wa kuzungumzia Majimbo ulishapita, ni kwenye ajeti za kisekta ndiyo tunazungumzia Majimbo, sasa hivi unazungumza Bajeti Kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Mbunge, wewe ukiamua kutaja Zanzibar ni sawa lakini kiongozi mwingine akiamua kutokutaja usitake wewe kumuwekea maneno kana kwamba yeye amekosea sana mchango wake kwa sababu wewe mawazo yako ndiyo bora, siyo sawasawa. Mheshimu kama yeye anavyokushimu wewe, heshimu mawazo yake na mchango kuhusu Mbunge huyo mwingine aliyechangia unaondoka kwenye Taarifa Rasmi za Bunge. (Makofi)

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba Mheshimiwa Waziri wa Fedha, suala la bandari ambalo kwa mujibu wa takwimu itazalisha ajira karibu 80,000 kwa Zanzibar ni jambo kubwa sana, bandari ambayo itajengwa Zanzibar ile dhana kama kuna dhana, kama kuna tongo za masikio watu zinawatoka wanasema itaua bandari ya Tanzania Bara siyo kweli. Bandari ambayo inaenda kujengwa Zanzibar ni kisaidizi cha bandari ya Tanzania Bara au ni partner wa bandari ya Tanzania Bara. Nchi hii si ni moja? Si tunashirikiana kwenye masuala ya biashara? Si tunashirikiana kwenye masuala ya uchumi? Tunategemeana kwa masuala ya uchumi? Hivi kwa nini huku ni sawa huku siyo sawa?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mpango kwa dhana hiyo ya umoja na juzi tumepitisha sheria hapa kwamba mtukopee, sheria ile ikapitishwa humu kwenye Bunge walioipitisha ni sawa, walioikataa ni sawa, sasa leo kama kutukopea hamtaki mnachokihitaji ni nini? Baraza la Wawakilishi sasa hivi kule Zanzibar lina Wajumbe wa CCM watupu lakini inafika mahali Mheshimiwa Dkt. Mpango unaambiwa bajeti ya Zanzibar ndiyo umekwamisha miradi hii, hivi tukueleweje? Maana kama ni mpinzani ni sawa, lakini bajeti ya nchi, bajeti ya Zanzibar inaenda kukusulubu wewe kwamba hawa ndiyo waliokwamisha miradi, hivi hamna haya? maana yake lazima tufike mahali tuambiane ukweli siyo sisi ni bajeti ambayo ilisema kuwa miradi hii minne imekwamishwa na hawa. Bandari ya Mpigaduri, barabara ya Wete-Chake na vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kudumisha umoja wetu, kwa kudumisha Muungano wetu haya mambo lazima yaondoke, lazima yashughulikiwe ipasavyo. Mheshimiwa Dkt. Mpango huna budi ushughulike kama Waziri unayehusika na pande zote mbili hata kama Wizara ya Fedha siyo ya Muungano.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo inashangaza umetuletea bajeti, juzi nchi za Afrika Mashariki zimewasilisha bajeti zote zimewasilisha bajeti, nikashangaa nilikuwa najiuliza, humu haujataja Zanzibar umetaja mara mbili wakati unampongeza Dkt. Shein na umekuja kuitaja tena Zanzibar wakati unazungumzia VAT ya umeme, nadhani uliitaja ili ionekane tu umeitaja, lakini haujazungumzia chochote kingine! Sasa mimi nikajiuliza, Zanzibar haiwasilishi bajeti kwa sababu siyo nchi miongoni mwa nchi za Afrika Mashariki ni sawa, lakini basi tunawasilisha bajeti ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania basi hata kutaja angalau hicho ambacho kinapatikana kule Zanzibar, kwa nini kisiwemo ndani ya hii bajeti? Kwa hiyo Mheshimiwa Mpango mimi nakuomba sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la utalii na hili niseme kwamba suala la utalii siyo suala la Muungano kiukweli, lakini nimestuka wakati tunalalamikia masuala ya biashara tulilalamika kwamba biashara Zanzibar…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii ya kuchangia angalau kwa uchache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza niwashukuru viongozi wangu wa Kambi ya Upinzani kwa kutupa maelekezo mazuri na kutuongoza na kufikia kwenye ufanisi hadi leo tumo na tunaendelea kujadili katika Bunge hili la bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote humu tunakumbuka kwamba katika dunia hii nchi yoyote hata zile ambazo zimeendelea, tukielekea kwenye uchaguzi kitu cha mwanzo wagombea Urais wanachokijadili ni suala la kuongeza ajira kwa wananchi wao hususani kwa vijana. Pili wanajadili mkakati imara na madhubuti wa kuondoa umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na msemaji aliyepita hivi punde, Mheshimiwa Silinde kwamba bado Mheshimiwa Mpango katika hotuba hii hajatuonyesha mkakati imara wa Serikali namna gani na kwa njia zipi ataondoa tatizo la ajira kwamba ni kwa namna gani atawaajiri vijana wa Kitanzania. Pia ni mkakati gani atakaoutumia katika kuhakikisha umaskini uliokithiri wa Watanzania unapungua kwa kiwango fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili nina imani, suala hili mara nyingi linajitokeza hapa Bungeni, dada yangu pale Mheshimiwa Angellah Kairuki ana jawabu lake moja mara zote huwa analizungumza kwamba tunafanya uhakiki na baada ya kumaliza uhakiki tutaajiri vijana wa Kitanzania kwa kiasi fulani. Hebu wakati wa kufanya majumuisho, Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mheshimiwa Kairuki mje basi mtueleze ni lini sasa mtawaajiri vijana wa Kitanzania. Tunaenda kwenye mwaka wa pili sasa wa Rais John Pombe Magufuli bila vijana wa Kitanzania kupewa ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo napenda kulizungumza ni mfumo wa kodi ambao tunauendeleza Tanzania. Miongoni mwa mambo ya Muungano suala la Wizara ya Fedha siyo suala la Muungano lakini kodi ni suala la Muungano, kwa maana ya TRA. TRA ipo na inakusanya kodi kwa maslahi ya nchi nzima ya Tanzania kwa maana ya Zanzibar na Tanzania Bara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa ni sahihi kabisa kwamba Zanzibar haifuati mfumo wa kodi wa kilimwengu kwa maana ya mfumo wa kuthaminisha bidhaa kwa ajili ya kodi, ni sahihi kwamba Zanzibar mfumo huu imeukataa na haiufuati. Haiufuati kwa sababu ya uchumi wake mdogo na population ya Wazanzibar ni ndogo, uchumi wa Zanzibar hauwezi kuulinganisha na uchumi wa Tanzania Bara. Tanzania Bara ina mchango mkubwa katika kufanya uchumi wa Zanzibar hauendi mbele kwa sababu ya mfumo mbovu wa kodi tunaouendeleza Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema kwamba suala la Mtanzania yeyote kutoka Zanzibar na kitu pengine cha shilingi milioni moja, kwa mfano tv akalipishwa kodi pengine laki moja na nusu Zanzibar, anakuja kutumia katika matumizi yake ya kawaida lakini anafika Tanzania Bara bandarini anaambiwa alipe difference, hii sio sahihi. Mheshimiwa Waziri wa Fedha ipo haja sasa ya kutafuta namna bora ya mfumo wa kodi ili kuhakikisha kwamba wajasiriamali wadogo wadogo wa Zanzibar wana-enjoy soko la Tanzania Bara. Leo anatoka mjasiriamali na mzigo wake mdogo wa shilingi pengine milioni moja au moja na nusu anakuja kutafuta riziki Tanzania Bara, lakini mzigo ule Zanzibar kalipia kodi pengine shilingi laki mbili, lakini akifika Tanzania Bara anaambiwa lipia tena laki mbili tukiwa na dhana eti ni difference, hii siyo sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tena mdogo wangu mmoja alizungumza kule kwamba hata zile bidhaa zinazotoka ndani ya nchi, zinazozalishwa Tanzania Bara au Zanzibar lakini zikivuka kutoka Tanzania Bara kuja Zanzibar au kutoka Zanzibar kwenda Tanzania Bara pia zinalipishwa kodi. Hata Afrika Mashariki tumeandaa utaratibu wa kusameheana kodi kwa bidhaa ambazo zinazalishwa ndani ya Afrika Mashariki, leo iweje ndani ya Tanzania moja tuna mifumo ya ajabu ya kulipishana kodi? Mheshimiwa Waziri wa Fedha hii siyo sahihi.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitoe ushauri tungekuwa na mfumo kwamba basi kama tuna difference tungekuwa na baadhi tu ya bidhaa au aina fulani ya bidhaa au thamani fulani ikifikia ndiyo suala la difference hapa mnalizingatia. Siyo sahihi kwamba mjasiriamali ana mzigo wake mdogo anakuja kutafuta riziki Tanzania Bara au mjasiriamali anaondoka hapa na mzigo wake mdogo kwenda Zanzibar tuwe na mfumo wa ajabu wa kodi ambao unadumaza upande mmoja wa Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Tume ya Pamoja ya Fedha, ni sahihi kwamba Zanzibar stahiki yake kwa mujibu wa sheria ni asilimia 4.5. La ajabu la kwanza, Mheshimiwa Mpango, ipo haja sasa kuufanyia review ya mfumo huu wa asilimia 4.5 na kuuangalia upya kwa sababu ulipitishwa miaka 40 nyuma. Uchumi wa nchi hizi unabadilika, lakini uchumi wa Tanzania Bara siyo uchumi wa Zanzibar, uchumi wa Zanzibar ni uchumi wa bidhaa, uchumi wa Tanzania Bara umejitawanya katika mambo tofauti tofauti. Sisi kule Zanzibar hatulimi korosho, ufuta wala pamba, uchumi wetu unategemea bandari na bidhaa kutoka nje. Inapofika mahali kwamba suala la mfumo wa Tume ya Pamoja ya Fedha kutokuwepo…

TAARIFA

Mheshimiwa Mwenyekiti, jawabu limetoka, tena limetoka kwa watu wa CCM kule nyuma kwamba Makunduchi wanalima korosho, lakini mbili/ tatu za kula wenyewe, sisi tunazungumzia zao la biashara.(Makofi)

Mheshimiwa Mattar ni rafiki yangu, umerogwa na nani? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la Tume ya Pamoja ya Fedha, nikuombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha utakapokuja kuhitimisha ulitolee majibu suala hili kwa sababu limechukua muda mrefu na hili ndiyo mwarobaini wa kukuweka wewe salama. Mheshimiwa Mpango nataka nikuhakikishie kwamba Wazanzibari hawatokuelewa bila suala hili kupata ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mpango na tuna ushahidi kwamba hata hiyo asilimia 4.5 kwanza haifiki kikamilifu, ikifika ni asilimia 2.5 au 3.5 lakini pia hata huo mrejesho wenyewe hauendi. Mheshimiwa Mpango hadi sasa hivi Zanzibar inakudai mrejesho tena karibuni wa shilingi bilioni 30, Mheshimiwa Mpango umerogwa na nani? Yaani wewe huna haya wala aibu? Yaani Zanzibar leo inaikopa huna aibu? Kwa uchumi ule mdogo unakuja kuikopa Zanzibar? Hili Mheshimiwa Mpango inabidi uje utujibu ni lini fedha hii utairejesha Zanzibar? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, naomba nizungumzie suala la madini. Hili suala limezungumzwa kwa mapana yake. Mimi nataka kuzungumza kitu kimoja kwamba ili Watanzania wawaelewe CCM na wafute ile dhana inayosambaa kwenye mitandao kwamba CCM ni ukoo wa panya, baba mwizi, mama mwizi na mtoto mwizi ni kwa waliohusika kupelekwa mahakamani. Hii ni kwa sababu viongozi walioshutumiwa wote walikuwa viongozi waandamizi wa CCM, majanga haya yanafanywa viongozi hao ni viongozi wakuu wa CCM, ni Mawaziri, Makatibu Wakuu na kadhalika, tuone sasa viongozi wale wanapelekwa mahakamani, wamechunguzwa na wamechukuliwa hatua stahiki kwa sababu tayari ripoti mnayoita ya kisayansi imethibitisha kwamba viongozi hawa wamehusika kwa namna moja au nyingine. Hapo ndiyo msemo huo tutau- delete sasa kwenye mitandao kama CCM ni ukoo wa panya kwamba baba mwizi, mama mwizi na viongozi wengine wezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mungano na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipatia hizi dakika tano niseme machache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muda mrefu tulikuwa tunazungumzia juu ya suala la Muungano na hizi zinazoitwa kero za Muungano, lakini sasa ni dhahiri kwamba imenoga. Imenoga kwa sababu pande zote hususan za Wabunge kutoka Zanzibar sasa wameungana na wamekutana kwenye angle moja ya kusemea namna kero hizi za Muungano zinavyoathiri maendeleo na uchumi wa Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wa Zanzibar ni uchumi wa visiwa, uchumi wa visiwa siku zote unategemea zaidi biashara, biashara za fedha, benki na biashara nyingine. Leo biashara hizi zote kwa kutumia kivuli cha Muungano zimekufa na uchumi wa Zanzibar tayari ni kusema kwamba tayari ni sawa na kusema umekufa kwa sababu umesimama na biashara Zanzibar haziendi kwa sababu ya mfumo mbovu wa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisikitike sana, leo wafanyabiashara kutoka Tanzania Bara wameona bora kwenda kuchukua bidhaa Mombasa, Uganda na Kongo kuliko kusafiri kwenda Zanzibar kuchukua bidhaa kama ilivyokuwa zamani kwa sababu tu ya mifumo mibovu ya kodi, kuna nini hapa? Ni kutokana na ukiritimba na mfumo mbovu wa kodi na mfumo mzima wa mzunguko wa biashara hasa katika Tanzania yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze suala la pili, Zanzibar ilikuwa na system ya kusajili meli, miezi miwili mitatu nyuma mfumo huu wa usajili meli umezuiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nikwambie Zanzibar kwa mwezi ilikuwa inakusanya jumla ya dola 79, jumla ya shilingi milioni 333 kwa mwezi. Nikwambie sasa ninavyozungumza Zanzibar mpaka inazuiwa ilikuwa imesajili meli 457. Leo kwa sababu Zanzibar imezuiwa na vikwazo vile vimewekwa leo zimebakia meli 350 tu, watu mmoja mmoja waliosajili meli zao wanaondoka kwa sababu ya vikwazo ambavyo vimewekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme usajili wa meli, Zanzibar toka miaka kumi iliyopita, Zanzibar zimekamatwa meli mbili kwa hizo sababu zilizotajwa kwamba ni sababu ya unga, lakini kuna nchi mwezi mmoja zinakamatwa meli zisizopungua 27, Zanzibar miaka 10 zimekamatwa meli mbili? hivi kuna sababu ipi kwamba Zanzibar zimekamatwa meli ipi na iwekewe vikwazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa zilizopo sasa ni wazi na ni dhahiri kwamba Zanzibar inanyang’anywa usajili wa meli na usajili wa meli sasa unawekwa kwa jina la Tanzania. Huu ni uonevu na ni uonevu ambao haukubaliki, Muungano huu ambao tunauhubiri kila dakika na kila wakati kwa kweli umekuwa ni tatizo kwa uchumi wa Zanzibar na kwa kweli umekuwa ni kilio kikubwa kwa uchumi wa Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukisikitikia mifumo hii ya kodi ambayo tumekuwa tukizungumza, kila Mzanzibar anaenyanyuka analilia mfumo wa kodi. Mimi binafsi nimewahi kumfuata Waziri wa Fedha tukazungumza kirafiki kabisa, nimemfuata Naibu Waziri wa Fedha nikamfuata nikazungumza naye, lakini kwa masikitiko majibu ninayoyapata ni ya aibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unafika Waziri wa Fedha au Naibu wake anakujibu na anakwambia hasa kwamba wewe nia yako Bandari ya Tanzania Bara ife, sasa ndio maana nikamuuliza tu ina maana wewe umeridhika baada ya kuua Bandari ya Zanzibar, kwa sababu Bandari ya Zanzibar ni kama vile imekufa, biashara hakuna lakini yeye ameridhika kwamba Bandari ya Zanzibar ife, lakini amefurahi kuinyanyua Bandari ya Tanganyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali hii haikubaliki, lazima tuwe na mkakati na msimamo imara wa kuhakikisha kwamba bandari zote mbili zinatumika na tunaziimarisha kwa maslahi ya uchumi wa pande zote mbili, Tanzania Bara na Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuwa na Waziri wa Fedha au Waziri wa aina yoyote ambaye ana-favor upande mmoja na kuukandamiza upande mwingine, hii haikubaliki na haitokubalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme wazi kama kuna watu ambao watavunja Muungano ni watu wanaowadanganya wananchi kwamba tunatatua kero za Muungano, lakini tukitizama kero za Muungano kila uchwao zinazidi, uchumi wa upande mmoja kila uchwao unanyanyuka na uchumi wa upande mwingine kila uchwao unakufa. Sababu hii kizazi kinachokuja hakitokubali na nina kuhakikishia Muungano huu utaenda kuvunjika bila ridhaa na mitazamo ya watu. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipatia dakika tano hizi na naomba niseme machache. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia kupata muda huu wa dakika chache na nianze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Katiba na Sheria kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 133 na Ibara ya 134, inazungumzia uwepo wa Tume ya Fedha ya Pamoja na Akaunti ya Pamoja ya Fedha ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tume hii ilianzishwa mwaka 1996 na ilizinduliwa rasmi mwaka 2003.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja atuambie je, Tume hii ipo na kama ipo inafanya kazi gani? Naomba hili suala liwekwe sawa, kwa sababu uwepo wa Kamati ya Pamoja ya Fedha na Tume ya Pamoja ya Fedha au Akaunti ya Pamoja ya Fedha bila shaka ingetufanya sisi Watanzania tukawa na mgawanyo sahihi wa mapato ya Muungano na Tume hii ingetusaidia sisi kuondoa na ikawa ndiyo kimbilio la kuondoa changamoto zote zinazogusa maslahi ya pande mbili za Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa sababu Tume hii haipo ingawa imezungumzwa kwenye Katiba, ni suala la Kikatiba, lakini kwa sababu haipo na haijaundwa tunaamini kwamba kero za Muungano ambazo tokea juzi zimekuwa zikitawala kwenye Wizara hizi mbili za Katiba na Sheria na Wizara inayoshughulikia mambo ya Muungano zitaendelea kuwepo na haziwezi kutatuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatujui ni sababu zipi ambazo au kuna changamoto zipi ambazo zimepelekea Tume hii ya Pamoja ya Fedha mpaka leo iwe haipo na haijaanzishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo naomba nilizungumze ni Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya nne (4) ambayo imezungumzia mamlaka mbili za Serikali ikiwemo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Katiba imezungumzia Mamlaka mbili za Mahakama; Mahakama ya Tanzania Bara au Mahakama ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lakini imezungumzia Mahakama ya Zanzibar ambazo Taasisi hizi mbili zote zina mamlaka sawa ya kiutendaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mamlaka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano inatekeleza matakwa na masuala yanayohusu Muungano na Mamlaka ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatakiwa isimamie masuala yanayohusu Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Kumekua na mwingiliano mkubwa wa utekelezaji wa majukumu haya.

Mhesimiwa Mwenyekiti, ambacho nataka kukisema hapa kwamba tumekuwa tukizungumzia malalamiko mengi na masuala mengi yanayohusu utekelezwaji wa Mamlaka hizi mbili kwamba kumekuwa na mwingiliano na kumekuwa na kutokuaminiana katika utekelezaji wa majukumu. Tunachokizungumza hapa ni kwamba, Wizara ituweke wazi na akija Mheshimiwa Waziri atuweke wazi juu ya Mamlaka hizi mbili zinatendaje majukumu yake.

Mheshimiwa Mwneyekiti, kubwa, Zanzibar imekuwa ikipigania mara nyingi kujiunga na Taasisi ambazo ingeruhusiwa kujiunga, lakini Mamlaka moja imekuwa ikichukua fursa ya kuiamuru Mamlaka nyingine kwamba hamna haki ya kujiunga na Taasisi hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukishirikiana katika masuala pengine ya Zanzibar kujiunga na FIFA, Zanzibar kujiunga na CAF, lakini tumeambiwa au tunaelezwa kwamba tunashirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili Zanzibar ijiunge na vyombo .

Mheshimiwa Mwenyekiti, masikitiko makubwa ni pale Zanzibar ilipokuja kuruhusiwa kujiunga na OIC kwa nini iliambiwa ijitoe? Halafu leo tunajikomba tunakuja kusema kwamba tunaisaidia Zanzibar ili ijiunge na FIFA, ili ijiunge na CAF huu si uongo kweli?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunapigania kujiunga na vyombo hivi kwa nini leo tusiiruhusu Zanzibar kwa sababu ina uwezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo naomba nizungumze, nalielekeza kwa Mkurugenzi wa Mashtaka. Kila siku tumekuwa tukilalamika kuna kesi zimechukua muda mwingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale Masheikh wa Uamsho na wale Masheikh waliokamatwa katika Mji wa Arusha, tunaomba kama Ofisi hii ya Mkurugenzi wa Mashtaka imeshindwa kupeleka ushahidi wale ni Watanzania, wale ni Wazanzibari tunaumia na lazima tuwasemee kwa sababu hawana mtu wa kuwasemea, lazima tutasimama Bungeni, tutaendelea kusema, tutaendelea kupiga kelele. Kama Serikali kupitia Ofisi hii imeshindwa kuthibitisha kwamba wale watu wana hatia basi waachiwe huru waende kwenye familia zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie na Tume ya Haki za Binadamu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo naomba nilizungumze ni suala la ujenzi wa viwanda. Hakuna Mtanzania yeyote ambaye anakataa dhamira ya ujenzi wa uchumi wa viwanda, lakini uchumi wetu wa viwanda ulenge pia kwa wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na maneno na yana ukweli kwa kiasi kikubwa sana kwamba, viwanda vinavyojengwa haviwalengi wananchi, viwanda vinavyojengwa havilengi kwenye Halmashauri na Wilaya ambazo zimejengwa. Leo hata kiwanda chenye thamani ndogo tu kikijengwa Serikali inaenda inachukua maeneo yote ya viwanda, inachukua tozo zote katika viwanda, hivyo nitoe ushauri tu kwamba, viwanda vinavyojengwa baadhi ya tozo katika viwanda hivyo, baadhi ya mapato katika viwanda hivyo ziendelee kubaki au tozo hizo au fedha hizo ziendelee kubaki kwenye Halmashauri husika.

Mheshimiwa Spika, vile viwanda vingekuwa na mgawanyiko, kukawa na viwanda vyenye viwango fulani ambavyo pengine ni viwanda vikubwa vikaenda moja kwa moja Serikalini, lakini viwanda vidogovidogo na viwanda vya kati pengine tungefikiria pato lake tukaliacha kwenye Halmashauri husika, ili wananchi wa maeneo hayo waendelee kufaidika na viwanda ambavyo vinajengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye kitabu cha Mheshimiwa Dkt. Mpango, nafikiri kama sikosei ni ukurasa wa 16 amezungumza kwamba, Tanzania kwa mwaka inatoa wahitimu karibu laki nane, lakini akazungumza kwamba ajira Serikalini zinazowezekana tunatarajia kuajiri watu 40,000. Sasa angalia kwamba, leo tuna wahitimu laki nane, lakini Serikali ina uwezo wa kutoa ajira elfu arobaini tu, wapi na wapi? Watu elfu arobaini ni asilimia tano tu. Mheshimiwa Waziri wa Fedha hivi hajioni kwamba, ana-fail? Kama Watanzania wanaohitimu ni laki nane, hawa wengine waende wapi au wafanye nini?

Mheshimiwa Spika, ipo haja ya sasa Wizara ya Fedha na Serikali kwa jumla kukaa kutafakari hili. Mheshimiwa Mpango amekuja hapa na bajeti yake hii kwa mbwembwe sana, amekuja na mbwembwe nyingi, ving’ora na vitu vingine vingi. Katika bajeti ile Mheshimiwa Dkt. Mpango amekuja na maandiko mengi ya Biblia.

Mheshimiwa Spika, labda Mheshimiwa Waziri anajiandaa na yeye kuwa msaidizi wa kuongoza. Mimi naamini kwa maandiko aliyokuja nayo tunapata matumaini kimsingi kwa sababu, yupo mmoja katika viongozi wakubwa tu alisema anajiandaa kuwa msaidizi wa kuongoza malaika mbinguni.

Mheshimiwa Spika, sasa labda Mheshimiwa Dkt. Mpango na yeye anajiandaa sasa kuwa msaidizi wake. Sasa tuone basi kama ni hivyo, kama unataka kwenda mbinguni na una ndoto ya kuwa msaidizi wa kuongoza malaika mbinguni, basi hayo aliyoyaandika yatekeleze, Yesu hakuwa bahili. Toa fedha kwenye taasisi zinazogusa watu, toa fedha kwenye taasisi ambazo, Wizara ambazo zinagusa maisha ya watu, asitoe fedha kwa sababu ya kutaka kuonekana kajenga reli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, reli ni nzuri inagusa maslahi ya watu, lakini inagusa maslahi ya watu wachache, kuna sekta hapa zinagusa maslahi ya watu wengi, toa fedha. Naamini akija ku-wind up utakuja na maneno mazuri zaidi kuliko yale ambayo…

T A A R I F A . . .

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Spika, tumuombe Mheshimiwa Waziri kwamba, haya aliyoyaandika basi ayatekeleze na ayatekekele kwa vitendo bila upendeleo, bila hiyana na bila ubahili wa kutoa fedha, hususan fedha katika taasisi ambazo zinagusa watu kama vile kilimo, maji, ili bajeti inayokuja aje hapa azungumze vizuri zaidi kuliko vile ambavyo amekuja hapa.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni suala la Katiba Mpya. Tanzania katika Serikali ya Awamu ya Nne ilileta mchakato wa Katiba. Katiba ambayo tulikuwa na matumaini ingekuwa ni suluhisho la matatizo ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, ninalo lingine, ujumbe umefika kwamba bado Watanzania wana kiu ya kuona Tanzania inapata Katiba mpya. Kwa hiyo hili litambulike wazi kwamba bado hatujasahau kwamba fedha za Watanzania zilitumika nyingi na mchakato huu uli- cost muda wa watu wengi na muda wa taasisi nyingi, lakini baadaye ukawekwa pembeni. Kwa hiyo haja bado ipo.

Mheshimiwa Spika, nije kwenye suala la Deni la Taifa. Kila Mtanzania amekuwa akipiga kelele kwamba deni la taifa linakua kwa kiasi kikubwa sana. Serikali zetu hizi zinakuwa na matatizo, kwamba mpaka jambo litokee ndipo waone kwamba hili suala hili ni la kweli. Watanzania wamekuwa wakipiga kelele wengi wachambuzi wa bajeti hii hata wamekuwa wakisema sana wataalam wamekuwa wakisema sana, kwamba ukuaji wa deni la Taifa ambao unaloendelea sasa hauko salama kwa Watanzania na ni wazi kwamba hautaiacha salama Tanzania.

Mheshimiwa Spika, ningemwomba tu Mheshimiwa Waziri Mpango awe na tahadhari na hili ili hatimaye mzigo huu asije akaubeba pekee yake kwa sababu mwishowe; Waswahili kule kwetu wanasema vyako vyako vyako na wenzio vikikupata ni vyako pekeo. Mheshimiwa Mpango mzigo huu iko siku utakuja kuelemewa peke yako. Kuna standard gauge inataka kujengwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru na siungi mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nami nafasi hii ya kuchangia mawili, matatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote tumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametupa afya, bado tupo na tunaendelea na pia nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na msemo wa Kiswahili, watu wa Pwani tunakuwa na msemo tunasema kwamba, “ukipenda boga, basi upende na mti wake.” Siyo sahihi kwamba unapenda boga, lakini mti wake unautia moto. Hii itakuwa siyo sahihi na wala haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia udugu siku zote ni kufaana na siyo kufanana. Kama kufanana, miaka 50 tumefanana vya kutosha, lakini sasa tunatakiwa tuwe na mwelekeo mpya kabisa wa kufaana hususan katika masuala mazima ya kiuchumi. Kama tutajaribu kuimba na kusifu tu masuala ya Muungano lakini bila kusaidiana kiuchumi, bila kupeana fursa zaidi za kiuchumi, kwa kweli Muungano huu utakuwa hauna mwendo mwema na hauna afya kwa Watanzania hususan wale walioko Zanzibar kwa maana ya Wazanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba kimsingi ni ukweli usiopingika kwamba Muungano kama Muungano ni muhimu na hakuna anayekataa hata mmoja. Siyo kweli kwamba kuna Wazanzibar fulani hawataki Muungano, siyo kweli kabisa. Wazanzibar wanataka Muungano. Kama alivyosema Kaka yangu Mheshimiwa Jaku tunahitaji Muungano ambao utakuwa na maslahi kwa pande zote mbili. Hatuhitaji Muungano ambao umejikita maslahi ya upande mmoja hii itakuwa siyo muungano. Naomba Mawaziri watakapokuja ku-wind up kwanza waje wanijibu masuala mawili ambayo tumekuwa tukiyazungumza mara kwa mara pale tunapopata fursa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni kuhusiana na vyombo vya moto. Kwa kweli tumekuwa tukipata taabu sana Wazanzibar, hasa sisi Wabunge, tumekuwa tukibughudhiwa sana na TRA na Polisi kwa sababu tu tuna magari yamesajiliwa kwa namba za Zanzibar. Hii siyo halali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi kwenye mchezo ule wa Simba na Mazembe ya Congo, tuliwakuta Wakongo wanahojiwa kwenye vyombo vya habari. Walikuja hapa na magari yao na wakafanya shughuli zao Dar es Salaam, Tanzania hii hii na halafu wakaondoka na magari yao. Leo hakuna Mzanzibar anayethubutu kuja Tanzania Bara na gari yake akatumia, hii siyo haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi binafsi na-declare kwamba ipo siku nilifukuzwa na TRA na Polisi usiku Dar es Salaam. Nasimama, wananiambia tuna wasiwasi na gari yako. Kwa nini? Unatumia namba za kigeni. Aah, nikashangaa, nikamwuliza wewe nani? Mimi Afisa wa TRA. Hii namba ya wapi? Namba ya Zanzibar. Hivi Zanzibar leo ni nchi ya kigeni na Dar es Salaam? Ananiambia kwani Zanzibar ni Tanzania Bara. Nikataka kujua kumbe hivi kuna nchi inaitwa Tanzania Bara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi ni vitu ambavyo vinahitaji majibu. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja anipe jibu sahihi juu ya suala hili kwamba ni lini sasa bughudha hii na adhabu hii itaondoka kwa Wazanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo nataka Mheshimiwa Waziri aje anijibu kwa kina ni suala la uwepo wa Account ya Pamoja ya Fedha ambayo imetajwa wenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 133. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, mwaka juzi 2017 tulizungumza suala hili akaahidi kwamba linakwenda kutatuliwa; mwaka jana 2018, tulizungumza suala hili akaahidi kwamba linakwenda kutatuliwa. Leo tunataka commitment ya Serikali kwamba ni lini sasa suala hili linakwenda kumalizwa na tuone Account ya Pamoja ya Fedha ambayo itashughulika na mgawanyo sahihi wa mapato ya Muungano baina ya Zanzibar na Tanzania Bara au Tanganyika unakwenda sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yote haya yanakuja kwa sababu moja; hakuna siku Serikali ya Chama cha Mapinduzi imekuwa na nia njema na Muungano huu. Hiyo ndiyo kauli simple kabisa, ndiyo kauli rahisi. Siku Muungano huu unaundwa uliundwa kwa siku mbili baina ya Mwalimu Nyerere na Karume, lakini tunazungumzia kero ya Muungano tena ambayo iko ndani ya Katiba inachukua miaka 50, nia njema iko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuimba tu kwamba tuna nia njema, tunataka kutatua kero za Muungano, sijui tunafanyeje, wakati nia njema hakuna. Vijana wetu hao, wote vijana; Mheshimiwa Makamba na Mheshimiwa Mussa, wote wana utashi wa kuona kero za Muungano zinatatuliwa. Tena hata ukizungumza nao unahisi kwamba wanaumia na wako tayari kuona kero za Muungano zinatatuliwa. Ushirikiano wanaopata bila shaka ni tatizo, Serikali haiko tayari kuona kero hizi zinatatuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Muungano limekuwa na shida na ndiyo maana zipo taarifa zinasema na ni sahihi kabisa, hata mgogoro uliokuwepo katika miaka ya 1970 baina ya Mwalimu Nyerere na Karume sababu ilikuwa ni Muungano. Hata mgogoro uliomwondoa Jumbe kwenye madaraka kama Rais wa Zanzibar akafukuzwa Urais, akafukuzwa nafasi zote sababu ilikuwa ni Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata Mashehe ambao leo wako jela kwa mwaka wa sita sasa; siyo ugaidi, wala siyo suala la uanaharakati, wala siyo suala lolote, ni kwa sababu walisimama na Wazanzibar kudai maslahi zaidi…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: …ya kiuchumi kwa ajili…

MWENYEKITI: Taarifa. Mheshimiwa Kombo kaa chini kwanza.

T A A R I F A

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mzungumzaji, anaposema kwamba Chama cha Mapinduzi hawana nia njema na Muungano huu na Chama cha Mapinduzi sasa hivi kina umri wa zaidi ya miaka 51 na Chama cha Wananchi CUF walipojaribu kuja na Muungano wa Shirikisho, Chama cha Mapinduzi ndiyo kilisimama imara kupinga Muungano ule wa shirikisho. Kwa hiyo, suala la kusema Chama cha Mapinduzi hakina nia njema na Muungano huu, siyo sawa sawa. (Makofi)

MWENYEMITI: Ahsante. Mheshimiwa Kombo, taarifa hiyo.

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuchauka ndugu yangu wewe umekwenda juzi CCM…

MWENYEKITI: Jibu taarifa yake. Mengine yaache.

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: …hayo mapenzi yako na CCM yamekuja lini? Au kwa sababu Mbunge! Subiri kesho kutwa CCM wakuangushe halafu uanze kuimba imba huko. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba nia njema ndiyo itakayodumisha Muungano. Naomba niseme moja na katika hili naomba Mheshimiwa Jenista anisikilize vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fursa ya mazungumzo ambayo ipo sasa kwenda kutatua changamoto hizi za Muungano, baada ya muda hazitakuwepo tena na tutakuja kushuhudia mambo mengine ambayo hayastahili. Kwa sababu unapobana fursa za kiuchumi za Zanzibar, vizazi vinavyokuja havitakubali kuona kwamba wao hawa-enjoy fursa za kiuchumi kama zile ambazo wenzao Watanzania Bara wanazipata ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hili hawatalikubali. Kwa hiyo, ushauri wangu ni kwamba tutumie fursa ambayo ipo, tutumie nafasi ambayo sasa hivi tunayo ili kutatua changamoto hizi tukiwa na nia njema ya kwenda kwenye Muungano ambao utadumu na utadumisha usawa na haki kwa pande hizi mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie mchango wangu kwa kusema kwamba, suala la mazingira Wizara hii bahati mbaya sana hakuna fedha ya ndani ambayo imetengwa katika kuendeleza suala la mazingira ndani ya nchi yetu ya Tanzania. Fedha yote inayotegemewa ni ya misaada kutoka nje. Hii inadhihirisha au inaonyesha kwamba ni kiasi gani Serikali haiko serious na kuendeleza suala la mazingira katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana wakati wa kupitisha bajeti na Waheshimiwa Mawaziri pamoja na Cabinet iwe serious na suala la mazingira kwa sababu ni muhimu na ni suala ambalo linagusa binadamu na viumbe vyote vilivyomo ndani ya Tanzania yetu. Bila mazingira sahihi na bila kudumisha mazingira, Taifa hili litatupotea na tutakuja kujutia nafasi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.4) wa Mwaka 2016
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii nikiwa mtu wa mwanzo kuchangia muswada huu, nikushukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuchangia kile ambacho nilitaka kukisema hapa, nimpongeze Mnadhimu na Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani kwa kile ambacho amekiwasilisha kwa ufasaha mkubwa sana. Lakini pia niunge mkono hotuba ya Kamati ya Katiba na Sheria na mimi nikiwa miongoni mwa Wajumbe wa Kamti hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie muswada huu nijielekeze kwenye Ibara ya 13 ya muswada huu inayohusiana na masuala ya mikopo ya Serikali pamoja na misaada na dhamana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jambo la aibu kubwa kuona kwamba miaka 50 ya uwepo wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lakini hadi leo tunakuja kupitisha sheria ambayo inaifanya sasa Zanzibar, maana tunaweka masharti ya kukopa Zanzibar kama vile Serikali ya Mtaa, tunaipa mamlaka kama Serikali ya Mtaa, masharti ambayo inawekewa kukopa Serikali ya Mtaa ndiyo masharti ambayo leo tunaiwekea Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Hili ni jambo la aibu na ni jambo la masikitiko makubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tupo katika mjadala, si mara moja wala mbili, kwenye Kamati ya Katiba na Sheria, tumelizungumza suala hili lakini bado Serikali ya Jamhuri ya Muungano kupitia Mwanasheria Mkuu kaendelea kubakia na msimamo wake, kaendelea kifungu kile kile kukibakisha na masharti yale yale, alichokibadilisha ni matumizi ya lugha tu. Lakini masharti yako palepale kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili ipate mkopo wa aina yoyote, kwa matumizi yoyote ni lazima ikakopewe au Serikali ya Jamhuri ya Muungano ikakope halafu Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ianze sasa procedure ya kuomba mkopo ndani ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hii ni aibu na ni aibu ya mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hilo ambalo limezungumzwa hapa kwa kina na Mnadhimu na Msemaji wa Kambi ya Upinzani limezungumzwa kwa ufasaha. Ni miaka mingi suala hili limekuwa ni kero kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ni kero kwa Wazanzibari, kwamba leo, miaka 50 mtoto kakua tayari, kwa nini Serikali ya Jamhuri ya Muungano isianze kufikiria sasa kuipa angalau mamlaka Zanzibar ya kuanza kutembea kwa miguu yake? Kuna tatizo gani? Kuna ubaya gani sasa Zanzibar kuanza kuiachia kidogo kidogo ikatembea kwa miguu yake? Mpaka leo tunaendelea, maana mnaandaa sheria ya kuendelea tu, maana kile kinachozungumzwa kwamba kilichopo hapa ni…
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiifafanua kwa kina Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya sasa inatambua mamlaka tatu. Tujiulize, hivi mamlaka ya Tanganyika ambayo imo ndani ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hivi inakopewa na nani? Inaenda kumsujudia nani ikakopewe, maana yake ni mamlaka ambayo imejivisha koti la Muungano, huoni sehemu yoyote, huoni sheria yoyote kwamba sasa yale mambo ambayo yanagusa Tanganyika, si mambo ya Muungano, ni ya Tanganyika, yanaomba ruhusa kwa nani kwenda kujitafutia mkopo, msaada na kitu kingine chochote nje ya Tanzania au ndani ya Tanzania. Mamlaka hii ya Tanganyika inaomba ruhusa kwa nani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini mamlaka ya Zanzibar ambayo kuna Serikali kamili, kuna Rais, kuna Baraza la Wawakilishi, kuna kila kitu. Kwa nini kila siku iombe ruhusa? Kwa nini kila siku ije ipige magoti kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuomba ruhusa eti ikakopewe? Huo msingi wa kukopa, kwamba sio ikakopewe tu lakini Serikali ya Jamhuri ya Muungano ikakope halafu waje waanze sasa kuiwekea masharti Zanzibar kwamba baada ya Serikali ya Muungano kukopa ikapewa masharti haya, huko ambako imeenda kukopa, na hiyo ikija sasa inapanga masharti mapya kuipangia Zanzibar kama vile ambavyo Serikali ya mtaa fulani imewekewa masharti, hivi mnatuelekeza wapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nadhani muda umefika sasa, miaka 50 si kidogo, muda umefika sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba Pendekezwa ukisoma Ibara ya 254(1), (2) na ya (3) imezungumzia vizuri suala hili na tayari ilikuwa imeshaipa Zanzibar kutaka kutembea kwa miguu yake, na wanazungumza kwamba kuna matatizo ya Kikatiba. Matatizo ya Kikatiba ya nchi hii hayakuanza leo, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mpaka leo inatambua uwepo wa Waziri Kiongozi kwenye Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, hivi Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haijavunja Katiba ya Muungano? Kimsingi tayari imevunja Katiba ya Muungano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia ndani ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano kuna mambo yameorodheshwa kama mambo ya Muungano, utekelezaji wake hautekelezwi kama mambo ya Muungano, Zanzibar inatekeleza kivyake na Tanzania Bara inatekeleza kivyake. Kwa nini leo tuambiwe kwamba kurekebisha kifungu hiki, kutoa mamlaka kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwenda kukopa, kwenda kuomba misaada nje ya nchi, nje ya Tanzania inavunja Katiba ya Muungano, kwa hili tu? Kwa nini tusiseme kukusanya kodi sasa, kwa sababu ni suala la Muungano ile ZRB kule Zanzibar ifutwe, kwa nini tusiseme?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tusiseme masuala ya hali ya hewa sasa Zanzibar isiwe na kitengo kinachotabiri masuala ya hali ya hewa? Kwa nini tusiseme kwamba hapa tunavunja Katiba tuje tuseme tunavunja Katiba eti kwa sababu tunaomba sasa Zanzibar ipewe mamlaka ikakope nje ya nchi. Kwa nini tunasema tunavunja Katiba eti kwa sababu tumesema Zanzibar sasa iende ikaombe misaada nje ya nchi, hapo tunavunja Katiba. Tulijiunga na OIC kwenda kuomba misaada tukaambiwa tunavunja Katiba tujitoe, kwa nini kila sehemu ambapo kuna maslahi ya Zanzibar tunaambiwa tunavunja Katiba? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwe wawazi na tuwe wakweli, muda umefika sasa kuiachia Zanzibar ianze angalau kutambaa kama si kutembea. Zanzibar nayo ina mahitaji, leo inafika mahali Serikali ya Jamhuri ya Muungano inataka kwenda kukopa eti halafu waje waikopeshe Serikali ya Zanzibar, pia tunawekewa masharti kwamba tunakwenda kuwakopea lakini mtumie kwa matumizi haya na haya, hee! jamani, hata huyo mke time nyingine unampa nafuu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, huyo mke uliyemuoa ukamtolea mahari wakati mwingine akikwambia nipe laki moja wala humhoji unaenda kutumia nini. Mambo mengine ni yake yeye, wewe si utakuja kuyaona tu? Huwezi kumwambia kwamba nakupa laki moja lakini katumie kwa hiki na hiki na hiki. Hii ndoa au ujeshi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nimalizie kwa nia njema kabisa. AG akubali kwamba kile kifungu ambacho kiliwekwa ndani ya Katiba Pendekezwa ambalo bado halijamaliza mchakato wake basi kinyofolewe kiwekwe katika maeneo haya, na kilizungumza wazi kwamba Zanzibar sasa ina mamlaka ya kwenda kukopa nje na ndani ya nchi, halafu haya masharti mengine yatafuata baadaye. Si lazima na wala si wajibu na kama Katiba hii, hii Katiba ni yetu sisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba hii haijatufunga kwamba sasa Zanzibar lazima tuikabe koo hata pa kusema, hata pa kufurukuta haina. Lazima tujipangie mikakati kama ni kweli tuna nia njema ambayo haipo ya kuendeleza na kuudumisha Muungano huu. Hiyo nia haipo na ndiyo maana vifungu hivi vya Katiba ndiyo kwanza vinaandaliwa ili kuendelea kuibana Zanzibar ili Zanzibar iendelee kuja kusujudia Bara kwa maslahi ya watu fulani. Ahsante sana, nashukuru sana kwa nafasi hii.
Muswada wa Sheria ya Kulitangaza Jiji la Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi wa Mwaka 2018
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, name nakushukuru kwa kupata fursa hii ya kuchangia. Kwanza, nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye ametujaalia kuja tena katika Bunge hili la Kumi na Mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na mchango wangu wa hoja ambayo iko mezani kwa kunukuu Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ukienda kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 4(1) naomba kwa ruhusa yako niisome.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasema ifuatavyo: “shughuli zote za mamlaka ya nchi katika Jamhuri ya Muungano zitatekelezwa na kudhibitiwa na vyombo viwili vyenye mamlaka ya kiutendaji, kwa maana ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, inaendelea kwa kusema: “vyombo viwili vyenye mamlaka ya kutekeleza utoaji haki” kwa maana ya Mahakama Kuu ya Zanzibar na Makama Kuu ya Tanzania Bara au Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara hiyo ya 4(1) inaendelea “na pia vyombo viwili vyenye mamlaka ya kutunga sheria na kusimamia utekelezaji wa shughuli za Umma kwa maana ya Bunge na Baraza la Wawakilishi.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inazungumzia vyombo viwili vyenye
mamlaka ya kutunga sheria, lakini leo chombo kimoja kikajipa mamlaka kila siku kutunga sheria kwa niaba ya chombo kingine. Hii siyo haki. Kama kuna kitu ambacho kinafanywa isivyo halali. Kama kuna kitu kinafanywa kibabe na kinyume na sheria na Katiba ya Tanzania na Zanzibar ambazo zote mbili ninazo, basi ni kitendo cha kutunga sheria bila kuishirikisha Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukilalamikia mambo mengi kwamba Zanzibar tunaonewa, hatushirikishwi, hatupewi haki sawa na mdau mwingine wa Muungano huu. Tumekuwa tukisema vitu vingi, lakini bado dharau hizi na ubabe huu unaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, donda hili linaloendelea dhidi ya muungano wetu, I am sure litaendelea, lakini ipo siku litaathiri Muungano huu. Tutakuja kutaka kuurejesha sasa, lakini kazi ya kuurejesha itakuwa kubwa na haitawezekana tena kwa sababu tu ya kutotii sheria na Katiba za nchi tulizonazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hizi wakati zinaungana, zilikuwa na mamlaka sawa. Nia njema ya Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere na nia njema ya Abeid Amani Karume, ilipaswa ibebwe na ifanyiwe kazi na hata viongozi wa leo. Siyo tu kwamba tumerithi, tunaendeleza, lakini hatujali wala hatuthamini juhudi ya upande mmoja kwa sababu tu uwezo wa kusema, uwezo wa kutenda tumenyang’anywa na hatunao. Hii siyo halali na tutaendelea tu kusema kwa sababu hatuna namna nyingine ya kufanya. Tutaendelea kusema na kulalamika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taarifa tu, mwaka 1973 wakati Mwalimu Nyerere anatangaza nia ya kuhamishia Makao Makuu Dodoma, Rais wa Zanzibar alikuwa Aboud Jumbe Mwinyi. Aboud Jumbe Mwinyi wakati anatunga kitabu chake cha The Partnership, kitabu hiki kimeandikwa na Aboud Jumbe Mwinyi; The Partnership, Muungano wa Tanganyika na Zanzibar miaka 30 ya Dhoruba. Muungano huu ukiwa na miaka 30, Jumbe aliuita kwamba ni Muungano wa dhoruba kwa sababu tu ya kutokuthaminiwa upande mmoja wa Muungano; kwa sababu tu ya kuonekana Zanzibar siyo chochote siyo lolote; kwa sababu tu ya kuonekana Zanzibar haina hadhi wala haina nguvu wala haina la kufanya ndani ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania au ndani ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Jumbe alilalamikia kitendo cha Nyerere kutangaza nia ya kuhamishia Makao Makuu Dodoma, leo mwaka 2018 tunapitisha Sheria ya Kuhamishia Makao Makuu Dodoma bila kuishirikisha Zanzibar. Huu ni msiba mkubwa na ni dharau iliyovuka mipaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni dharau iliyovuka mipaka kwamba hatujali, tunafanya tunavyotaka, basi fanyeni. Endeleeni kufanya, lakini Wazanzibari tupo, tutaendelea kusema, tutaendelea kutetea, Wazanzibari wanatusikia, wanatuelewa na wanafahamu kinachoendelea na wanaifahamu dhuluma ambayo inaendelea na wanafahamu dhuluma ambayo wanafanyiwa kwamba leo inapitishwa sheria. Ibara ya (2) imezungumza kwamba sheria hii itatumika Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar. Zanzibar haikushirikishwa, ni dhuluma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhuluma siyo lazima unyang’anywe mali au unyang’anywe nyumba, hii ni sheria. Hili ni jambo kubwa linalotuhusu pande zote mbili, siyo kutetea tu kila kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunifahamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali ipo Dar es Salaam, masafa ya kuondoka Dar es Salaam na Unguja ambapo ndiyo kwenye Makao Makuu ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa ndege ni dakika 15, kwa boti ni saa moja na nusu umeshafika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dada yangu pale alisema, leo kumtoa Afisa wa Serikali Zanzibar kuja Dodoma ni siku tano. Anachukua siku tano, asafiri kutoka Unguja alale Dar es Salaam, Dar es Salaam achukue basi afike Dodoma, pengine siku ya tatu yake ndiyo kuna kikao, halafu aondoke Dodoma siku nyingine yake afike Dar es Salaam, alale Dar es Salaam siku ya pili achukue boti, siku tano. Tumekuwa tukilalamikia vitu vingi bila kupatiwa majibu. Vikao tunavyoambiwa vinakaa havina athari yoyote, havina impact yoyote, havina tija yoyote.