Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Makame Mashaka Foum (2 total)

MHE. MASHIMBA M. NDAKI (K.n.y. MASHAKA MAKAME FOUM) aliuliza:-
(a) Je, tangu Serikali ilipoanza kutoa mikopo ya Elimu ya Juu, ni kiasi gani cha fedha kimetolewa mpaka bajeti ya mwaka 2015/2016?
(b) Je ni kiasi gani kimerejeshwa ndani ya kipindi hicho?
(c) Je, Chuo gani kinaongoza kwa wanafunzi wake kupata fedha nyingi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Makame Mashaka Foum, Mbunge wa Kijini, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, tangu Serikali ilipoanza kutoa mikopo ya Elimu ya Juu mwaka 1994/1995 hadi mwezi Machi, 2016, kiasi cha shilingi trilioni 2.44 kimetolewa kwa wanafunzi 378,504 kwa kusudi hilo.
(b) Mheshimiwa Spika, urejeshwaji wa mikopo kutoka kwa wanufaika ulianza mwaka 2006/2007 na hadi kufikia tarehe 31 Machi, 2016 kiasi cha shilingi bilioni 93.9 kilikuwa kimerejeshwa kati ya shilingi bilioni 256.2 ambazo zilikuwa zimeiva kwa kurejeshwa.
(c) Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2014/2015, Chuo kilichoongoza kwa wanafunzi wake kupata fedha nyingi za mikopo ni Chuo Kikuu cha Dodoma.
MHE. MASHIMBA M. NDAKI (K.n.y. MHE. MAKAME MASHAKA FOUM) aliuliza:-

Sheria Na.9 ya mwaka 2010 ya Watu wenye Ulemavu imeainisha haki za msingi za Watu wenye Ulemavu ikiwa ni pamoja na haki ya ukalimani katika maeneo ya utoaji huduma kama vile hospitali, taarifa ya habari, shuleni nk:-

Je, Serikali inachukua hatua gani ili kuharakisha utekelezaji wa sheria hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, WATU WENYE WALEMAVU (MHE. STELLA IKUPA ALEX) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Makame Mashaka Foum, Mbunge wa Kijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Watu wenye Ulemavu Na.9 ya mwaka 2010, imeweka misingi ya upatikanaji wa haki kwa watu wenye ulemavu ikiwepo haki ya upatikanaji wa habari kwa kundi la viziwi kupitia wakalimani katika sehemu mbalimbali ikiwemo hospitali, shuleni pamoja na vyombo vya habari yaani luninga.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na jitihada za kuweka mikakati ya kuwa na wakalimani wa kutosha wa lugha ya alama kwa kuanzisha programu ya mafunzo ya lugha ya alama katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kupitia Mradi wa LAT (Lugha ya Alama Tanzania). Chuo kimeandaa mwongozo wa mwaka 2019 wa majaribio ya kufundishia na kujifunza Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) kwa kutumia Lugha ya Alama ya Tanzania kwa darasa la awali, la kwanza na la pili. Aidha, imeandaliwa kamusi ya lugha ya alama na machapisho mbalimbali yanayotoa mwongozo wa namna ya kujifunza lugha hiyo kwa lengo la kuongeza wakalimani.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuendeleza kundi kubwa la wakalimani na watumiaji wa lugha ya alama, Serikali imechukua hatua ya kutumia lugha ya alama kama lugha ya kufundishia na kujifunzia shuleni. Aidha, kufundisha lugha ya alama kama somo mojawapo katika shule na vyuo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu katika kilele cha Wiki ya Viziwi iliyofanyika katika Manispaa ya Iringa alitoa maagizo kwa vyuo vya elimu ya juu na kati kuweka mtaala ambao utawezesha wahitimu kusoma lugha ya alama kama somo la lazima katika masomo yao (compulsory subject). Aidha, Mheshimiwa Waziri Mkuu aliagiza vyombo vyote vya habari kuwa na wakalimani wa lugha ya alama katika vipindi vya luninga zao.