Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Nassor Suleiman Omar (3 total)

MHE. NASSOR SULEIMAN OMARY aliuliza:-
Uhakiki wa vyeti feki umeathiri wafanyakazi wengi na wengine wamepoteza ajira zao:-
Je, ni wafanyakazi wangapi wamepoteza ajira zao sekta ya elimu pekee?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nassor Suleiman Omar, Mbunge wa Ziwani, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2016/2017 na 2017/2018, Serikali ilifanya uhakiki wa vyeti vya watumishi wa umma ili kubaini waliokuwa na vyeti halali na waliokuwa na vyeti vya kughushi. Katika uhakiki huo, jumla ya Walimu 3,655 walibainika kuwa na vyeti vya kughushi, hivyo walipoteza sifa za kuendelea kuwa watumishi wa umma.
MHE. NASSOR SULEIMAN OMAR aliuliza:-

Kilimo cha mazao ya viungo vya chakula ni biashara yenye tija kubwa duniani kwa sasa:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhamasisha kilimo hicho hapa nchini?
NAIBU WAZIRI KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nassor Suleiman Omar, Mbunge wa Jimbo la Ziwani, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa mazao ya viungo kutokana na mchango wake katika kipato cha mkulima mmoja mmoja na pia katika kuliingizia Taifa fedha za kigeni. Kutokana na umuhimu huo, Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi imeandaa mkakati wa kuendeleza mazao ya viungo (Spice Sub Sector Strategy twenty fourteen) ambao unalenga kuongeza uzalishaji na tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo mahususi katika mkakati huo ni utoaj mafunzo ya kuongeza ujuzi katika uzalishaji kwa wataalam na wakulima, uanzishwaji wa vituo vya kukusanyia mazao na kupanga madaraja na kuunda masoko ya pamoja ya wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo mengine mahsusi yanayofanyiwa kazi ni kuhamasisha na kusimamia uanzishwaji wa vitalu vya kuzalisha miche na mashamba ya miti mama kwa ajili ya kuzalisha miche bora ya aina za mazao hayo. Mkakati huo unatekelezwa kwa pamoja na wadau mbalimbali zikiwemo Taasisi zisizo za Kiserikali na Vyama vya Wakulima ambazo ni pamoja na Sustainable Agriculture Tanzania, Chama cha Wakulima wa Viungo, Amani (CHAWAVIA) na Jumuiya ya Wakulima wa Viungo Wilaya ya Muheza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali pia imeandaa mwongozo wa uzalishaji wa mazao ambao umeainisha maeneo yanayofaa kwa uzalishaji wa mazao mbalimbali yakiwemo mazao ya viungo. Mwongozo huo unalenga kuonesha fursa za uzalishaji wa mazao mbalimbali yakiwemo mazao ya viungo. Wizara ndani ya miezi sita ijayo itakamilisha zoezi la usajili wa wakulima wa mazao mbalimbali nchini ikiwemo mazao ya viungo kwa kubaini idadi yao, ukubwa wa mashamba na mahali alipo ili kuwahudumia kwa ufanisi zaidi na kuongeza tija.
MHE. NASSOR SULEIMAN OMAR aliuliza:-

Utamaduni katika kila nchi ni utambulisho wa Taifa; na kwa kuwa kuna upotevu mkubwa wa utamaduni wa asili kwenye makabila yetu nchini:-

Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kufufua utamaduni wa asili wa makabila yetu?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nassor Suleiman Omar Mbunge wa Ziwani kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba Serikali ni msimamizi na mratibu wa shughuli zote za utamaduni ikiwepo sera ya utamaduni na sheria zinazohusu utamaduni jamii ndio mmiliki wa utamaduni. Hivyo, nitumie fursa hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge akiwemo muuliza swali, taasisi, asasi na mashirika ya jamii nzima ya watanzania kuwa mstari wa mbele katika kulinda utamaduni wetu na kufufua pale unapofifia. Wizara yangu inatambua na kupongeza mwamko mpya katika jamii wa kuhimiza na kuendeleza utamaduni wetu maeneo kadhaa nchini kwa mfano: Tamasha la ngoma ya utamaduni la Dkt. Tulia Traditional dance ambalo linafanyika katika Mkoa wa Mbeya. Tamasha la majimaji Serebuka Songea, Tamasha la Bulambo ambalo linafanyika Mwanza, Tamasha la Chamwino Dodoma, Tamasha la Nyasa na Matamasha ya makabila mbalimbali yanayoendelea katika Kijiji cha Makumbusho Jijini Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Serikali wizara yangu mbali na kuhimiza matumizi ya lugha ya Kiswahili ndani na nje ya nchi inaendelea na tafiti za kiutamaduni za makabila mbalimbali nchini lengo likiwa ni kuhifadhi. Mkazo zaidi umewekwa kwenye tamaduni za makabila au jamii zenye wazungumzaji wachache ambao zipo katika hatari ya kutoweka. Aidha, wizara inashirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii katika kuendesha tamasha jipya la urithi wa utamaduni inasimamia kila mwaka tamasha la kimataifa ya sanaa na utamaduni Bagamoyo ambao ni kivutio kikubwa kwa wanasanaa, wadau wa sanaa na wapenzi wa sanaa kutoka ndani na nje ya nchi na kwa sasa wizara inaratibu tamasha la utamaduni wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (JAMAFEST) litarajiwa kufanyika Jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 21 hadi 28 mwezi mwaka na mwaka huu na kuwavutia wanasanaa na wadau takribani laki moja kutoka ndani na nje ya Jumuiya.