Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Bahati Ali Abeid (1 total)

MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR (K.n.y. MHE. BAHATI ALI ABEID) aliuliza:-
Simu fake zimezimwa kwa sababu ya madhara ya kiafya kwa Watanzania.
(a) Je, wananchi wanaoendelea kuzitumia kwa matumizi mengine hazitawaletea madhara ya kiafya?
(a) Kama zina madhara, je, Serikali haioni kuwa sasa ni wakati muafaka wa kutoa elimu kwa umma?
WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bahati Ali Abeid, Mbunge wa Mahonda, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kuwepo kwa Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta (EPOCA) ya mwaka 2010 na Kanuni za EPOCA za mwaka 2011 zimewezesha kutekelezwa kwa mfumo rajisi wa namba za utambulisho wa vifaa vya mawasiliano vya mkononi ambayo ilipelekea kuzimwa kwa simu zenye namba tambulishi bandia ilipofika tarehe 17 Juni, 2016.
Mheshimiwa Spika, mfumo huu wa kielektroniki ulizinduliwa rasmi tarehe 17 Disemba, 2015 na unahifadhi kumbukumbi za namba tambulishi za vifaa vya mawasiliano ya mkononi kwa lengo la kufuatilia namba tambulishi za vifaa vinavyoibiwa, kuharibika, kupotea au ambavyo havikidhi viwango (bandia) vya matumizi katika soko la mawasiliano. Namba tambulishi za vifaa vyote vya mawasiliano vya mkononi ambavyo vimeibiwa, vimeharibika, kupotea au visivyokidhi viwango vya matumizi katika soko la mawasiliano haviruhusiwi kuunganishwa kwenye mtandao wa watoa huduma tangu tarehe 16 Juni, 2016.
Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo ya utangulizi, naomba kujibu swali hili kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, wananchi wanaoendelea kutumia simu fake ama zisizokidhi viwango vya kulinda afya ya watumiaji ama zenye namba tambulishi bandia wanaweza kudhurika na matumizi yake kwani hazikutengenezwa kwa kupitia mfumo unaodhibiti simu hizo kutokuwa na kemikali hatari zinazoweza kudhuru binadamu na mazingira kwa mfano zebaki na kemikali nyinginezo.
(b) Mheshimiwa Spika, kabla na baada ya kuzima simu fake, Serikali imekuwa ikielimisha umma kuhusu tahadhari ya kutotumia simu hizo ili kuepuka madhara ambayo yanaweza kutokea kutokana na kutumia simu hizo zisizokidhi matakwa ya kulinda afya ya watumiaji. Aidha, Serikali inaendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu wananchi kujiepusha na matumizi ikiwa ni pamoja na kuzikusanya simu hizo na kuziteketeza kwa mujibu wa utaratibu uliopo.