Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Kasuku Samson Bilago (8 total)

MHE. KASUKU S. BILAGO aliuliza:-
Kifungu cha 3 cha Kanuni za Utumishi wa Umma za mwaka 2003, na Kifungu cha 1(26) cha Kanuni za Kudumu za mwaka 2009 vinatoa tafsiri ya neno mwajiri kuwa ni mtu au taasisi ambayo mtumishi wa umma anaingia naye mkataba wa ajira na kumlipa mshahara.
Je, kwa kuzingatia tafsiri hiyo, mwalimu ambaye ni mtumishi wa umma, mwajiri wake ni nani?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UTUMISHI NA UTAWALA BORA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua fursa hii kujibu swali la Mheshimiwa Mwalimu Kasuku Samson Bilago Mbunge wa Jimbo la Buyungu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mwajiri wa watumishi wote wa umma wakiwemo walimu ni Serikali ambayo ndiyo inakusanya mapato na kulipa mishahara ya watumishi wake. Hata hivyo, Serikali imekasimu madaraka kwa mamlaka mbali mbali kama ilivyoainishwa kwenye kifungu cha 6(1) cha sheria ya Utumishi wa Umma Sura ya 298.
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kutungwa kwa sheria ya Tume ya Utumishi wa Walimu, sheria namba 25 ya mwaka 2015, Idara ya Utumishi wa Walimu ndiyo ilikuwa Mamlaka ya Ajira na nidhamu kwa walimu wote walio kwenye Utumishi wa Umma. Baada ya kutungwa kwa sheria hiyo ya Tume ya Utumishi wa Walimu namba 25 ya mwaka 2015, iliyoanzisha Tume ya Utumishi wa Walimu.
Tume hii sasa ya Watumishi wa Walimu pamoja na majukumu mengine itakuwa Mamlaka ya Ajira na Nidhamu kwa Walimu wa shule za msingi na sekondari walioajiriwa na Serikali.
WAZIRI WA NCHI OFISI YA RAIS (UTUMISHI NA UTAWALA BORA): Mheshimiwa Naibu Spika samahani.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutekeleza jukumu la kuwa mwajiri, Serikali huingia Mikataba ya Ajira na kulipa mishahara ya Walimu kupitia mamlaka za Serikali za Mitaa wanakofanyia kazi.
MHE. KASUKU S. BILAGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Kabla sijaruhusu swali langu kujibiwa naomba marekebisho madogo kwenye majina yangu yaliyo kwenye majibu ya Waziri. Jina langu Samson halina (iiI kule mwisho na jina langu Bilago halina N katikati halisomeki Bilango linasomeka Bilago.
MHE. KASUKU S. BILAGO aliuliza:-
Kumekuwa na malalamiko kwa baadhi ya wastaafu kutolipwa mafao yao baada ya kustaafu:-
(a) Je, kuanzia Januari hadi Disemba, 2015 ni watumishi wangapi wa umma wamestaafu utumishi?
(b) Je, kati ya hao ni wangapi wamelipwa mafao yao?
(c) Kama kuna ambao hawajalipwa, je, ni kwa sababu gani?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kasuku Samson Bilago, Mbunge wa Buyungu, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Idadi ya watumishi wa umma waliostaafu, kati ya Januari, 2015 na Disemba, 2015 ni 7,055
(b) Kati ya watumishi 7,055 waliostaafu, watumishi 5,057 wamelipwa mafao yao.
(c) Jumla ya watumishi waliostaafu 1,998 hawajalipwa mafao yao kutokana na sababu zifuatazo:-
(i) Upungufu wa baadhi ya nyaraka muhimu katika majadala ya wastaafu.
(ii) Waajiri kuchelewa kuwasilisha nyaraka muhimu zinazotakiwa kuthibitisha uhalali wa utumishi wa wahusika kabla ya mfuko kuanzishwa Julai, 1999.
MHE. COSATO D. CHUMI (K.n.y. MHE. KASUKU S. BILAGO) aliuliza:-
(a) Je, Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014 itaanza kutekelezwa lini katika kipengele cha Elimu ya Msingi (Chekechea - Kidato cha Nne)?
(b) Je, ni Walimu wangapi wa Sekondari wanahitajika ili kutekeleza Sera hiyo?
(c) Je, hali ya miundombinu katika shule zetu ikoje katika kutekeleza Sera hiyo.
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kasuku Samson Bilago, Mbunge wa Buyungu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa kipengele cha Elimu Msingi ambapo watoto watasoma kwa miaka kumi mfululizo utaanza mara baada ya kupitishwa kwa mabadiliko ya Sheria ya Elimu, Sura ya 353 ya mwaka 1978 na Sheria nyingine zitakazoleta ufanisi katika utekelezaji wa kipengele hicho. Aidha, uwepo wa miundombinu ya kutosheleza na Walimu wa kutosha, vitazingatiwa kabla ya utekelezaji kuanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa takwimu zilizopo idadi ya Walimu wa sekondari ni 88,999 na kati yao 18,545 ni Walimu wa masomo ya sayansi na hisabati. Walimu 70,454 ni Walimu wa masomo ya lugha, sanaa na biashara. Hata hivyo, kuna upungufu wa Walimu 22,460 wa masomo ya sayansi na hisabati katika Shule za Sekondari na kuna ziada ya Walimu 7,988 wa masomo ya Sanaa, Lugha na Biashara. Uchambuzi wa mahitaji halisi ya miundombinu na Walimu wanaohitajika kwa ajili ya utekelezaji wa Elimu Msingi unaendelea kufanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kupitia Halmashauri za Wilaya, Jiji na Manispaa, Serikali imeendelea kutenga fedha katika bajeti katika kila mwaka kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu katika shule za Msingi na Sekondari. Lengo ni kupunguza changamoto ya utoshelevu wa miundombinu kama vile vyumba vya madarasa na nyumba za Walimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2015/2016, Serikali ilitenga kiasi cha shilingi bilioni 67.83 kwa ajili ya kuimarisha miundombinu, ambazo tayari zimeshapokelewa kwenye halmashauri na zinatumika kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa nyumba za madarasa, ujenzi wa vyoo vya Walimu na wanafunzi na ujenzi wa nyumba za Walimu. Shule ambazo zinanufaika na hicho kiasi cha bilioni 67 jumla yake ni 528 nchini kote. Aidha, katika mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 48.3 kwa ajili ya kuimarisha miundombinu ya shule za msingi na sekondari.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na uimarishaji wa miundombinu, katika mwaka wa fedha 2015/2016, Serikali inatarajiwa kuajiri Walimu 35,411 katika shule za msingi na sekondari, ili kuongeza idadi ya Walimu kwa lengo la kuongeza tija katika sekta ya elimu hapa nchini.
MHE. KASUKU S. BILAGO aliuliza:-
Kwa muda wa miaka tisa sasa baadhi ya wananchi wa Wilaya ya Kakonko nyumba zao zimewekwa ‘X’ kwa lengo la kuvunjwa ili kupisha ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami:-
(a) Je, ni wananchi wangapi kati ya hao wenye alama ya ‘X’ kwenye nyumba zao wanakidhi vigezo vya kulipwa na sababu ni zipi kwa wasiolipwa?
(b) Je, ni kiasi gani cha fedha kitatumika kulipa fidia nyumba hizo?
(c) Je, fidia hiyo itazingatia gharama ya nyumba kwa sasa au gharama ya zamani ya nyumba zilizowekwa ‘X’ na ni lini watalipwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kasuku Samson Bilago, Mbunge wa Buyungu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, eneo la Kakonko ni mojawapo ya maeneo yanayopitiwa na barabara kuu inayopitia Tunduma – Sumbawanga – Mpanda – Kanyani – Kasulu – Kibondo – Kakonko hadi Nyakanazi. Alama za ‘X’ ziliwekwa ili kubainisha wananchi waliojenga ndani ya hifadhi ya barabara ambayo ina upana wa mita 30 kutoka katikati ya barabara kila upande.
Mheshimiwa Spika, hakuna mwananchi anayekidhi vigezo vya kulipwa nyumba iliyowekwa ‘X’ kwani nyumba hizo ziko ndani ya hifadhi ya barabara yaani ndani ya mita 22.5 kutoka katikati ya barabara kwa mujibu wa Sheria ya Barabara ya mwaka 1967 na nyongeza ya hifadhi ya
barabara ya mita 15 yaani mita 7.5 kila upande kwa mujibu wa Sheria ya Barabara ya mwaka 2007.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hakuna nyumba iliyofuatwa na barabara, hakuna fedha ya fidia kwa ajili ya nyumba hizo. Aidha, kuna mashamba 99 ambayo yamo ndani ya hifadhi ya barabara iliyoongezwa ya mita 7.5 ambayo yatalipwa fidia kulingana na sheria zilizopo.
MHE. KASUKU S. BILAGO aliuliza:-
Jimbo la Buyungu Wilayani Kakonko linapakana na nchi ya Burundi, hivyo raia wa nchi hizi mbili wanafanya baadhi ya shughuli za kibiashara na kijamii kwa kushirikiana kwa muda mrefu hata kabla ya Burundi kujiunga na Jumuiya ya Afrika Mashariki.
(a) Je, ni lini Serikali itafungua Ofisi ya Uhamiaji katika kijiji cha Muhange iliyofungwa bila sababu za msingi?
(b) Je, kwa nini Warundi wakija kufanya biashara kwenye masoko ya ujirani mwema au kulima mashamba hukamatwa na kufungwa jela?
(c) Je, kwa nini Warundi 254 waliofungwa kwa makosa kama hayo wasirudishwe kwao ili kupunguza msongamano magerezani?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kasuku Samson Bilago, Mbunge wa Buyungu, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Uhamiaji katika Kijiji cha Muhange ilifungwa kutokana na sababu za kiusalama baada ya nchi jirani ya Burundi kuingia katika machafuko miaka ya 1990. Hata hivyo Serikali itaangalia endapo mazingira ya sasa yanaruhusu kujenga Ofisi hiyo.
(b) Mheshimiwa Spika, Idara ya Uhamiaji inatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria na taratibu zinazoruhusu wageni kuingia nchini, kuishi na kufanya kazi. Hivyo, wageni wote waingiapo nchini wakiwemo raia wa Burundi wanapaswa kuafuata sheria na taratibu zilizopo.
(c) Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna msongamamno wa wafungwa katika Magereza yetu nchini kutokana na sababu mbalimbali ambapo kwa sasa kuna jumla ya wafungwa 725, raia wa Burundi katika Mkoa wa Kigoma ambao wamefungwa kwa makosa mbalimbali.
Hata hivyo, ipo sheria inayoruhusu kumrudisha mfungwa kwao kwa yule ambaye sio Mtanzania. Sheria hiyo inaitwa The Transfer of Prisoners Act (No. 10) of 2004 na Kanuni zake (The Transfer of Prisoners Regulations of 2004).
Mheshimiwa Spika, sheria hii inatumika pale tu mfungwa wa nchi nyingine anapoomba kumalizia sehemu kifungo chake kwenye nchi yake ya asili.
MHE. KASUKU S. BILAGO aliuliza:-
Maeneo mengi ya Wilaya ya Kakonko yanaonyesha kuwepo kwa madini yenye thamani kama dhahabu na almasi.
(a) Je, kuna tafiti zozote zilizofanyika kuhusu upatikanaji wa madini Wilaya ya Kakonko?
(b) Kama zipo, je, ni madini gani yanapatikana na ni katika maeneo yapi?
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kasuku Samson Bilago, Mbunge wa Buyungu, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuanzia miaka ya 1970 Serikali kupitia Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) imekuwa ikifanya tafiti mbalimbali za kubaini uwepo na upatikanaji wa madini katika Wilaya ya Kakonko. Baadhi ya tafiti zilizofanyika ni pamoja na upimaji na uchoraji wa ramani za kijiolojia katika eneo la Kakonko. Maeneo mengine yaliyofanyiwa kazi hiyo ni Kalenge na sehemu ya Kibondo. Aidha, kati ya mwaka 1980 na 1985, Serikali kwa kushirikiana na Shirika la UNDP walifanya utafiti mwingine wa madini ya chokaa katika eneo la Bumuli Wilayani Kakonko.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti hizo zilibaini uwepo wa madini ya dhahabu katika maeneo ya Mwironge, Mwiruzi na Nyakayenze; chokaa katika eneo la Bumuli na katika eneo ya Keza, Kibingo, Nkuba pamoja na maeneo ya Kasanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti za kina zinahitajika ili kujua kina cha madini yaliyogunduliwa. Serikali inaendelea kuhamasisha makampuni mbalimbali binafsi ili kufanya utafiti wa kina na kuendeleza uchimbaji katika Jimbo la Kakonko.
MHE. KASUKU S. BILAGO aliuliza:-
Walimu wa Elimu Maalum wanapohitimu kwenye Vyuo vya Patandi na SEKOMU hawapelekwi kwenye shule za vitengo vya elimu maalum:-
(a) Je, Serikali haioni kama inapoteza rasilimali fedha na watu kwa kutoa elimu isiyo na tija kwa Walimu hao?
(b) Je, ni lini Serikali itawapanga walimu wenye elimu maalum kwenye shule na vitengo vyenye mahitaji hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo alilosema Mheshimiwa Bilago halihusiani kabisa na swali lake. Hata hivyo, nataka kumwambia kwamba kukatika kwa mkanda si kuvuliwa kwa mkanda. Ahsante sana. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kasuku Samson Bilago, Mbunge wa Buyungu lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutoa mafunzo kwa Walimu ni miongoni mwa mikakati ya kuongeza tija ya kazi na ubora wa elimu inayotolewa, si kupoteza rasilimali fedha na rasilimaliwatu. Kwa muktadha huo, Chuo wa Walimu wa Elimu Maalum Patandi hudahili Walimu kutoka kazini ambao huhitimu kwa viwango vya astashahada na stashahada. Chuo Kikuu cha Elimu Maalum SEKOMU hudahili walimu kutoka kazini na pia Walimu wapya kwa kiwango cha shahada.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vyuo vyote viwili, wahitimu waliodahiliwa kutoka kazini hurudi kwenye vituo vyao vya kazi wakisubiri uhamisho kwenda kwenye shule za vitengo vya elimu maalum; na wahitimu ambao hudahiliwa kabla ya ajira huajiriwa na Serikali na kupangiwa shule zenye vitengo vya elimu maalum na wengine huajiriwa na Sekta Binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya mwaka 2012 na 2015 Serikali iliajiri Walimu wapya 614 wa elimu maalum ambao walipangiwa kufundisha kwenye shule zenye vitengo vya elimu maalum. Hadi Desemba 2016 wapo Walimu 3,957 wa elimu maalum nchini sawa na asilimia 74.3 ya Walimu 5,324 wanaohitajika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha Walimu wote wenye taaluma za elimu maalum wanatumika vizuri, nazielekeza Halmashauri zote ziwahamishie Walimu wa elimu maalum kwenye shule zenye vitengo vya elimu maalum ifikapo Desemba 31, 2018. (Makofi)
MHE. KASUKU S. BILAGO aliuliza:-
Kaya zinazonufaika na Mfuko wa TASAF kwa vigezo vya umaskini baada ya kukidhi vigezo zimeanza kupata wakati mgumu na usumbufu mkubwa ikiwa mmoja wa wanakaya ni kiongozi wa Serikali ya Kijiji. Mfano baba wa kaya ndiye anakidhi vigezo vya kunufaika na mafao ya TASAF huku mama akiwa Mjumbe wa Serikali ya Kijiji, matokeo yake anaondolewa kuwa mnufaika na kuamuliwa kurudisha fedha yote aliyokwishanufaika nayo.
(a) Je, kuwa Mjumbe wa Kijiji kunaondoa umaskini wa kaya?
(b) Je, kaya maskini inapataje uwezo wa kurudisha fedha walizotumia?
(c) Je, ni kwa nini Serikali isiangalie upya vigezo vya wanufaika wa TASAF kwa kushirikisha wadau wengi?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, leo mimi nimeamka vizuri, nimefurahi sana, ndiyo maana niliwahi kuja. Nataka nichukue nafasi hii kuwapongeza vijana wangu wa Yanga… (Makofi/ Kicheko)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Tuliowatuma wakatuwakilishe kule Ethiopia, wamevuka, wanasonga mbele, ndiyo timu peke yake ya wakubwa nchi hii inayoshiriki mashindano ya kimataifa. (Makofi/Kicheko)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, tunazidi kuwaombea wasonge mbele wapate mafanikio, wabebe vizuri bendera ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya utangulizi huo mzuri tu, naomba sasa kuchukua nafasi hii kujibu swali la Mheshimiwa Kasuku Samson Bilago, Mbunge wa Buyungu, kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, mpango wa kunusuru kaya maskini una kanuni na taratibu zake za uendeshaji. Taratibu za uendeshaji wa mpango huu ziko bayana kwamba katika utambuzi wa kaya maskini, viongozi wa vijiji, mitaa, shehia hawaruhusiwi kutambuliwa kama walengwa. Hii iliwekwa hivyo ili kuondoa ukinzani wa kimaslahi kwani wao ndiyo wasimamizi wa shughuli zote za mpango katika maeneo yao. Ni kweli kwamba kuwa Mjumbe wa Serikali ya Kijiji hakuondoi umaskini wa kaya yake, hata hivyo, kanuni za mpango zinaruhusu iwapo kaya ya mjumbe inakidhi vigezo vingine vyote vya umaskini lakini anayo hiyari ya kuacha uongozi na kuchagua kuwa mlengwa.
(b) Mheshimiwa Spika, kaya ambazo zilitakiwa kurejesha fedha zilizopokelewa ni zile za wafanyabiashara, watumishi, viongozi na watu wenye uwezo ambao hawakustahili kupokea fedha hizi. Nakiri kwamba katika kuziondoa kaya hizo zilikuwepo zilizoondolewa kwa makosa kwa sababu tu zilikuwa zimeanza kuonyesha mafanikio na kujiimarisha kiuchumi chini ya mpango huu nazo zikatakiwa kurejesha fedha. Hali hii imeleta usumbufu mkubwa kwa kaya hizo.
Naomba kutoa wito kwa watendaji katika halmashauri na vijiji kuacha kuzidai fedha kaya ambazo zilinufaika kwa kutambuliwa kuwa ni kaya maskini na zikatolewa kwa makosa. (Makofi)
(c) Mheshimiwa Spika, yapo mambo mengi mazuri tuliyojifunza katika kipindi cha kwanza cha awamu ya tatu ya TASAF. Aidha, tumekutana pia na changamoto ambazo zitazingatiwa katika kipindi hiki ambapo tupo katika mchakato wa maandalizi ya kipindi cha pili cha awamu ya tatu ya TASAF. Ushauri wa Mheshimiwa Mbunge kuhusu kuwashirikisha wadau wengi zaidi ili kupata maoni yao katika kubainisha vigezo vya kuwapata wanufaika wa TASAF utazingatiwa.