Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Ally Mohamed Keissy (47 total)

MHE. ALLY M. KEISSY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mwambao wa Ziwa Tanganyika wavuvi wengi wanatoka DRC-Congo. Cha ajabu wanakata leseni kwa bei kama mvuvi mwenyeji wa Ziwa Tanganyika. Je, ni lini Serikali itachukua hatua ili wavuvi kutoka nchi za jirani walipie leseni kama inavyotakiwa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Keissy kwa sababu amekuwa akifuatilia kwa karibu sana changamoto mbalimbali za uvuvi na hasa katika maeneo ya Jimbo lake. Tumepata taarifa kwamba kuna wavuvi wanaotoka nchi za jirani wanavua katika maziwa yetu. Kwa vyovyote vile, hii ni kinyume na sheria. Tunaomba Waheshimiwa Wabunge taarifa kama hizi tuendelee kuzipata. Tukitoka hapa mimi mwenyewe nitachukua hatua za makusudi za kufuatilia ili tuweze kujua nani amehusika, tuwajue Maafisa wa Halmashauri wanaotoa leseni kwa watu hao ili kuweza kuchukua hatua stahiki.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimwia Spika, kwa kuwa Mkoa wa Kigoma pamoja na Wilaya zake zinaingiza gharama kubwa sana katika Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa kutumia majenereta, zaidi ya bilioni 160 kwa mwezi, kwa nini Serikali pamoja na Wizara ya Nishati na Madini isifanye haraka mradi huu ili kuokoa pesa kwa Mkoa wa Kigoma?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa shughuli za ugawaji wa umeme katika Mji wa Kigoma ni gharama kubwa na gharama alizozitaja Mheshimiwa Keissy kwa kweli ni kidogo siyo shilingi milioni 160 isipokuwa ni shilingi milioni 600 kila siku za mafuta tunatumia.
Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia uzito huo huo, ndiyo maana Serikali imesema itaanza ujenzi wa mradi huo wa Malagarasi ndani ya miezi sita kuanzia sasa, kuanzia mwezi Februari mwakani shughuli za ujenzi kwa ajili ya kuwapatia umeme wa uhakika wananchi wa Kigoma zitaanza. Kama nilivyosema shughuli hizi zitachukua miaka mitatu hivyo mwaka 2020 shughuli za ugawaji wa umeme katika Mji wa Kigoma zitakamilika na umeme utakuwa ni wa uhakika ambao haukatiki.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na jiografia ya Wilaya ya Nkansi, naomba hilo swali labda angesaidia kujibu Mheshimiwa Stella Manyanya, Naibu Waziri wa Elimu, Teknolojia na Elimu ya Juu. Inaonekana hilo swali halikujibiwa jinsi inavyotakiwa na aliyeandika hilo jibu, hajui Wilaya ya Nkasi ilivyo; Kipili iko wapi, Namanyere iko wapi, Kala iko wapi, Itindi iko wapi, Kabwe iko wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na majambazi katika mwambao wa Ziwa Tanganyika, hilo gari haliwezi kuhudumia vijiji vya mwambao wa Ziwa Tanganyika. Kwa hiyo, lini Serikali, itawapatia mgawo wa mafuta wa kutosha Wilaya ya Nkasi?
Mheshimiwa Naibu Spika, gari lenyewe liko Wilaya ya Nkasi, hata mafuta halina! Lini itaongeza mgao wa mafuta katika Wilaya ya Nkasi? Lini itawapatia pikipiki vijana wa Marine Kipili, ili kuondoa tatizo la usafiri ambako unatokea ujambazi katika vijiji vilivyopo jirani jirani na mwambao wa Ziwa Tanganyika ili kupunguza uharamia katika mwambao wa Ziwa Tanganyika?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ni kweli kwamba Wilaya ya Nkasi kijiografia imekaa na changamoto nyingi sana hasa ikizingatiwa kwamba baadhi ya vijiji vyake kama Kipili, Kala, Wampembe na vijiji vingine kama Samazi, vimekaa mbali kidogo, vinahitaji mwendo mrefu kuvifuata. Kwa hiyo, vinahitaji mafuta ya ziada. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Serikali imefanya jitihada kubwa sana katika Mkoa wa Rukwa na Nkasi kwa ujumla. Kwanza kuna maboti ya kutosha ambayo yalipelekwa kwa ajili ya Jeshi la Wananchi ambao wamekuwa wakishirikiana kwa karibu sana na Jeshi la Polisi.
Vilevile kuna vituo ambavyo vimeanzishwa katika maeneo hayo na hivyo, kuwezesha kuwa na urahisi wa kuwafikia wananchi wanapokuwa na tatizo, hususan katika kijiji cha Kipili. Kwa hali hiyo, naamini kwamba pamoja na jitihada ambazo zimekuwa zikiendelea kufanyika hali ya Nkasi kwa sasa ni bora kuliko ilivyokuwa hapo awali. Ahsante sana.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Kituo cha afya cha Kirando kilianzishwa miaka 42 iliyopita wakati Kirando ikiwa ni Kijiji, leo kina wakazi mara 50 zaidi kutoka miaka 42, aliyekuwa Waziri wa Afya Mheshimiwa Dkt. Seif Rashid alifika pale Kirando na akaniahidi kwamba hiki kituo kweli kimezidiwa na ninafanya mpango wa kuwa hospitali kamili.
Lini Serikali yako itaipa hadhi kituo cha afya Kirando kuwa hospitali kamili kwa kuwa kimezidiwa na wagonjwa?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli inawezekana kabisa kwamba katika huduma za vituo mbalimbali vya afya kumekuwa na kuzidiwa kwa sababu ya umbali kutokana na maeneo yetu kati ya kituo kimoja hadi kingine. Lakini kwa
suala la kituo cha afya ya Kirando ambacho Mheshimiwa Mbunge anasema kwamba kimezidiwa na je ni lini au kuna mikakati gani ya kuimarisha ili kiweze kutoa huduma hiyo au kubadilishwa kuwa hospitali.
Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani kikubwa hapa ni ushirikiano kati ya mamlaka ya Serikali za Mitaa ambapo Waheshimwia Wabunge ni Madiwani kule katika kupanga vipaumbele vyetu, ni vizuri mkawa mnaturahisishia kazi ya kupanga halafu mnajua kabisa kwamba hatua zile huwa ikitoka pale mnaenda kwenye Mkoa ambapo mnashauriana, katika Sekretarieti ya Mkoa kwenye kikao cha ushauri cha Mkoa pale ndipo ambao mnaweza mkaja na mapendekezo halafu Serikali Kuu tukaona tuanze na lipi katika eneo lenu.
Mheshimiwa Ally Keissy, nikuombe tu kwamba kama mtasema tukiimarishe hiki na kuwa hospitali, basi jambo hili lije kwa utaratibu wa kisheria kama ulivyoelezwa katika Sera ya Afya.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Wilaya ya Nkasi, kuna Ranchi ya Kalambo ambayo iligawiwa kwa wafugaji block kama kumi, kila block heka 3000 mpaka 2500 kila mfugaji, block kumi. Lakini hizo block kumi hakuna ng‟ombe zilizopelekwa baadhi ya blocks na baadhi ya waliochukua hizo block ni wajanja hawana mfugo hata mmoja wanakaa wanakodishia wafugaji.
Je, Serikali iko tayari kupitia upya Ranchi ya Kalambo ili kugawa upya kwa wafugaji ili kuondoa matatizo ya wafugaji na wakulima nchini?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa kwamba kuna changamoto kubwa sana katika ranch ya Kalambo na ranch nyingine ambazo zinamilikiwa na NAFCO, hasa zile ambazo zimegawiwa kwa Wawekezaji.
Nimfahamishe tu Mheshimiwa Mbunge kuwa kwa sasa Wizara inafanya tathmini ya kuangalia namna uwekezaji ule ulivyofanywa ili ikigundulika kwamba kuna wawekezaji walipewa ranchi za NAFCO lakini hawatumii ipasavyo wanyang‟anywe na kupewa kwa wafugaji na wawekezaji wengine ambao watatumia inavyotakiwa.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Nkasi leo ina miaka 40 tangu ilipoanzishwa, lakini haina hospitali ya Wilaya, wala Serikali haina mpango wa kujenga hospitali ya Wilaya. Ni lini Serikali yetu itakuwa na azimio la kujenga hospitali ya Wilaya hasa katika Makao Makuu ya Wilaya katika Mji wetu wa Namanyere?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninamfahamu Mheshimiwa Keissy kuhusu suala la tatizo la afya. Miongoni mwa mambo ambayo ninayakumbuka Mheshimiwa Keissy alipendekeza kituo kimoja kile cha afya kukipandisha grade kuwa hospitali ya Wilaya kama sikosei. Alizungumza hapa Bungeni kwamba kituo kile cha afya licha ya kuwahudumia wananchi wa Jimbo lake, wengine wanatoka katika nchi mpaka ya Congo. Hili nilisema siku ile kwamba Mheshimiwa Keissy jambo hili tumelichukua, katika mpango wa pili wa afya kila Halmashauri kuwa na hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Keissy naomba niseme tu kwamba tutaungana pamoja katika mipango kwa sababu tunajua Wilaya yako ipo pembezoni na ina changamoto nyingi. Tutajitahidi kwanza kuhakikisha kile kituo cha afya tunakiangalia na mimi nimekiri wazi kwamba nikija kwako lazima nikitembelee kituo cha afya, tutashawishi wenzetu wa Wizara ya Afya wakiangalie kama kimefikia vigezo kipandishwe kuwa hospitali ya Wilaya, tutakuunga mkono ili wananchi wa eneo lako lazima wapate afya. Jambo hili umelipigia kelele sana toka Waziri Mkuu wa mwanzo Mheshimiwa Peter Pinda nilikusikia ukilizungumza, nasema kwamba tupo pamoja katika hili.
MHE. ALLY M. KEISSY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Waziri ametembelea mpaka Wilayani kwangu Nkasi kule na kujionea mwenyewe jinsi matatizo ya mawasiliano ya Redio TBC hayafiki kule kwetu. Ni lini sasa bataweka mkazo ili watu wanaokaa mwambao mwa Ziwa Tanganyika waache kutegemea matangazo kutoka DRC Congo?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI,SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba katika Mikoa michache ambayo nimeitembelea ni pamoja na Mkoa wa Rukwa na Jimboni kwake Nkasi na nimpongeze kwa juhudi walizozifanya Halmashauri ya Wilaya Nkasi kwa kuanzisha redio yao na inafanya vizuri sana. Ni kweli pia kwamba usikivu wa Shirika la Utangazaji la Taifa kwa Wilaya ya Nkasi ni mbovu na baadhi ya maeneo yakiwemo ya Kabwe na maeneo mengine kwa kwa kweli wanasikiliza matangazo kutoka nchi jirani ya Congo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema tumeweka mkazo mkubwa kuhakikisha mikoa hii ya pembezoni tunaimarisha usikivu wa Shirika letu la Utangazaji la Taifa ili wananchi wetu waache kusikiliza redio za nchi jirani ikiwezekana watu wa nchi jirani wasikilize redio yetu na Shirika letu la Utangazaji wa Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie katika maeneo yote niliyotembelea kwa bahati nzuri, baada ya ziara yangu Mkurugenzi wa TBC Dkt. Rioba amekwenda huko nilikopita, na kuhakikisha kwamba yale niliyoyaagiza yanatekelezwa; na nichukue nafasi hii kumpongeza Mkurugenzi wa TBC kwa kazi nzuri anayofanya, ya kulibadilisha Shirika letu la Utangazaji na mimi naamini kwamba kwa kasi yake mambo yatakwenda vizuri.
MHE. ALLY M. KEISSY: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Mheshimiwa Naibu Waziri katika swali lake la kwanza alisema kwamba ana ziara ya Iringa, Mbeya na Songwe. Je, yuko tayari sasa katika hiyo ziara kuunganisha mpaka Wilaya ya Nkasi akajionee mwenyewe matatizo ya Afya, Elimu na Barabara katika Wilaya yetu ya Nkasi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ziara yangu inaanzia Mkoa wa Iringa, nitakwenda Mkoa wa Njombe, Mbeya, Rukwa, nikitoka hapo nitakwenda Mkoa wa Kigoma halafu namalizia Mkoa wa Tabora, hiyo ni phase namba moja. Baadaye nitakwenda Mkoa wa Mara, Geita, Mwanza, Kagera, halafu nitarudia katika Kanda ya Mashariki. Kwa hiyo, Mheshimiwa Keissy mpo katika awamu ya kwanza ya ziara yetu kubaini changamoto ili kuona jinsi gani Ofisi ya Rais TAMISEMI, tutafanya kuwahudumia wananchi wa Tanzania.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kijiji cha Kipili, Wilaya ya Nkasi, Mkoa wa Rukwa, tulikuwa na Chuo cha Uvuvi, na kulikuwa na generator na cold room, lakini bahati mbaya awamu zilizokuja ikageuzwa ikawa secondary school na uvuvi ukaisha, na sisi watu wa mwambao tunategemea sana uvuvi, hasa mwambao wa Ziwa Tanganyika, na hakuna Chuo:-
Je, ni lini Serikali itakirudisha Chuo cha Uvuvi cha Kipili ili kusaidia wavuvi wetu wa mwambao wa Ziwa Tanganyika?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, suala alilolisema Mheshimiwa Keissy, Serikali ilikuwa na nia njema kufuatana na mahitaji la kupanua elimu, ikafanya mabadiliko hayo, lakini kwa kuzingatia kwamba Jimbo la Mheshimiwa Keissy wananchi wake wanategemea uchumi wa uvuvi, sisi pamoja na TAMISEMI tutashirikiana kuangalia utaratibu mpya wa kuweza kurejesha utaratibu wa kuwa na chuo ambacho kitasaidia vijana wetu kuweza kujifunza na kuweza kumudu kazi hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili litaendana pia na mpango wa Wizara ya Elimu na Ufundi, ambao unahusisha vyuo vya VETA katika kila Wilaya ili tuweze kupata wanafunzi wengi ambao watafanya kazi kwa utalaam zaidi. Hili jambo linaenda sambamba na Mheshimiwa Jumaa Hamidu Aweso wa Jimbo la Pangani ambaye alishaongelea kwamba wananchi wake pia wanahitaji sana kufufuliwa kwa chuo ambacho uchumi mkubwa wa Pangani wa vijana unategemea uvuvi.
MHE. ALLY M. KEISSY: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Katika Ziwa Tanganyika tuna Halmashauri tano na kila Halmashauri ina licence yake na mvuvi anakata licence, lakini anapotaka kuhama kwenda Halmashauri nyingine hata kama licence yake haijakwisha muda lazima alipie licence upya kwenye Halmashauri anayokwenda. Je, ni lini Serikali itaondoa kero hii kwa wavuvi?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama nilivyosema hapo awali kwamba ziko tozo ambazo zimekuwa ni chanzo cha mapato ya Halmashauri mbalimbali na moja ya vyanzo hivi vya mapato kwa Halmashauri zetu ni leseni. Bahati mbaya sana kwa kanuni tulizonazo na Sheria ya Uvuvi iliyopo leseni hizi za Halmashauri zimekuwa za maeneo ya Halmashauri husika yaani hazihamishiki na ndiyo maana kumekuwa na huu usumbufu kwa wavuvi kwamba leseni zinazotolewa na Halmashauri ya Sikonge haiwezi kwenda kutumika katika Halmashauri ya Urambo, hili ndilo limekuwa changamoto. Nimpe tu faraja Mheshimiwa Mbunge kwamba hili nalo liko katika mambo ambayo yanaangaliwa na hiyo Tume ya Taifa ya Makatibu Wakuu inayopitia upya hizi kodi ambazo zimekuwa kero kwa wananchi.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, Asante sana. Pamoja
na jibu zuri la Naibu Waziri. Sasa lini Serikali itatoa kero kwa hizi kodi ndogo
ndogo za akina mama hasa wakinamama wauza vitumbua, wauza mchicha,
wauza dagaa, wauza nyanya ili kutoa kero kwa wananchi wetu wasiendelee
kudhulumiwa na kuteswa na hawa wakusanya kodi na hawa Wanamgambo,
imekuwa kero na Serikali kila mara ilitangaza hapa kwamba kodi ndogondogo
hizi ni kero lini Serikali itatangaza Halmashauri zote ziache mara moja kutoza
akina mama kwenye masoko madogo madogo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, tukifanya rejea wakati wa kampeni ya uchaguzi ya mwaka 2015. Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akijinadi kwa wananchi ni suala zima la mchakato wa kuondoa hizi kero ndogo ndogo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Mheshimiwa Keissy, nimefanya ziara katika maeneo mbalimbali hata pale maeneo ya Ilala pale katika soko letu la Ilala, soko la Feri, Sokola Pugu Kajungeni na maeneo mbalimbali, soko la Mwanjelwa kule Mbeya. Hizi ni miongoni kwa concern lakini siyo hivyo utakuta mtu wa kawaida analipishwa risiti isiyokuwa sawasawa ndio maana tumezielekeza Halmashauri zote. Sambamba na hilo tukaona sasa lazima tubainishe ipi ni kero ambayo itaweza sasa ikashughulikiwa vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, ndio maana sasa kwa mujibu wa utaratibu wetu tumeandaa sheria sasa inakuja hapa Bungeni, ambayo sheria ile itaainisha sasa sheria ambayo marekebisho ya Sheria ya Mambo ya Tozo na Ushuru Sura ya namba 290 itakuja hapa na sisi Wabunge wote tutashiriki, na nina imani kwamba Mungu akijalia huenda Mkutano ujao wa Bunge inawezekana sheria hiyo itaweza kufika mara baada ya wadau wakishashiriki vya kutosha.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaziagiza Halmashauri zote kwamba yale mambo ambayo unaona kwamba hili ni kero, kwa sababu hili suala Mameya wote, Wenyeviti wa Halmashauri wanajua kwamba sehemu hizo wamepewa kura na wananchi wao. Jambo ambalo naona kwamba jambo hili halina tija kwa wananchi wetu wa kawaida, naomba tulifanyie kazi, lakini jambo ambalo mmeona mmeliweka kwa mujibu wa sheria basi mlisamize kwa utaratibu bora, siyo kwenda kutoa kapu la mama anauza vitunguu barabarani au anauza nyanya barabarani hilo jambo litakuwa siyo sawasawa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nazielekeza Halmashauri zote hasa Mameya na Wenyeviti wa Halmashauri waweze kukaa pamoja na Kamati zao za Fedha, wabainishe ipi ni kero kwa sasa kabla sheria hii haijakuja hapa Bungeni ili mradi kuweza kuondoa kero kuwafurahisha wananchi waishi katika maisha ya utaratibu wa kujenga uchumi wa nchi yao.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri. Swali; je, wale Wakandarasi au Halmashauri zilizolipa pesa kwa Wakandarasi hewa, mtachukua hatua gani? Kuna miradi kadhaa katika Wilaya ya Nkasi ambayo pesa zililipwa lakini hakuna kilichofanyika.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA Mheshimiwa Naibu Spika, kama Mkandarasi amelipwa lakini kazi hajafanya, maana yake huo ni wizi; jambo la kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwaambie na hili tumelisema katika vipindi mbalimbali, Wakandarasi wowote ambao kwa njia moja au nyingine wamechukua fedha na kazi wametelekeza, tutahakikisha, nami nitawaomba Wakurugenzi wote waweze kuwabainisha; hasa wale Wakandarasi wa maji waliotekeleza miradi katika maeneo yao. Kwa sababu tukirejea katika Bunge lililopita, Waziri wa Maji hapa alisema wazi kwamba Wakandarasi ambao watashindwa kutekeleza wajibu wao watafutiwa hata suala la kupata tenda katika nchi yetu. (Makofi)
Kwa hiyo, Mheshimiwa Keissy, naomba tukitoka hapa unipe rejea ya hao Wakandarasi ili mradi tuweze kuwafanyia kazi. Lengo kubwa ni kwamba, wananchi wetu waweze kupata huduma ya maji.

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, TAMISEMI, hoja ya Mheshimiwa Keissy ndiyo tumeshaanza kuifanyia kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maji na Umwagiliaji tumeamua kuchukua hatua kwamba hatuwezi kupeleka hela kwenye Halmashauri mpaka walete certificate. Tumefikia hili kwa sababu hela zilikuwa zinapelekwa, halafu zinatumika, lakini ukienda kule hakuna kilichofanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyozungumza huko nyuma katika Bunge hili, ni kwamba tunakwenda kuunda Kamati ya Wataalam. Utaleta certificate yako kabla hatujailipa, tutatuma wataalam kwenye eneo twende tukaangalie kama hiyo kazi imefanyika ili tuweze kupambana na hili suala ambalo lilitaka kutupeleka pabaya.
MHE. ALLY M. KEISSY: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kama Serikali ipo tayari kupeleke pesa hizo, lakini nataka kujua ni shilingi ngapi zitapelekwa kwa ajili ya kumalizia huo mradi wa Skimu ya Lwafi? Nataka kujua kiasi cha pesa.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, fedha itakayopelekwa kule ni shilingi milioni 550 na fedha hii inatolewa na Serikali ya Japan na tayari taratibu za kuipeleka hiyo fedha zimeshafanyika ila kumekuwa na matatizo kidogo kupanua ile item ya kulipia kwa upande wa Halmashauri, ndiyo Serikali inaendelea kupanua. Fedha hiyo ipo tayari na wakati wowote itaingia.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Vituo vya Kirando na Kabwe ni majengo ambayo Wizara ya Mambo ya Ndani ilinunua kwa wananchi wa kawaida. Ni majengo yaliyojengwa kwa tofali mbichi na hata leo akienda kuyaona hayana milango, saruji na yanabomoka na baadhi ya nyumba za uani wanazolala polisi hazina milango kabisa. Je, katika hizo nyumba 4,136 vituo vya Kirando ni miongoni mwa vituo vitakavyokarabatiwa?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kufanya ziara katika Wilaya ya Nkasi kuvitembelea Vituo vya Polisi Kirando na Kabwe na vituo vya Uhamiaji vya Mwambao wa Ziwa Tanganyika ambavyo viko katika hali mbaya sana, havistahili Polisi kuishi wala kufanyia kazi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa nyumba 4,136 hausiani na ukarabati wa vituo vya Kabwe na Kirando. Hata hivyo, kama nilivyozungumza katika jibu langu la msingi ni kwamba tuna program vilevile ya ujenzi wa vituo vya polisi nchi nzima. Ingawa kutokana na udharura wa vituo vya Kabwe na Kirando kwa kuwa ujenzi wa vituo na uimarishaji wa usalama katika nchi yetu unakwenda sambamba na maendeleo ya nchi hii, basi ikiwa Mheshimiwa Mbunge ataona inafaa si vibaya katika Mfuko wa Jimbo akaangalia uwezekano wa kukarabati vituo hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusiana na ziara, tutaangalia uwezekano huo. Kama ambavyo nimekuwa nikizungumza kila siku, wajibu wetu ni kuweza kufanya ziara nchi nzima katika maeneo yote kuangalia changamoto zinazokabili vyombo hivi ambavyo viko chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani na Nkasi ni moja ya sehemu hizo.
MHE. ALLY M. KEISSY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa mara ya kwanza Serikali kutoa jibu zuri la kuridhisha kwa wananchi wa Nkasi.
Kwa kuwa aliyekuwa Waziri wa Ujenzi, Mheshimiwa John Pombe Magufuli aliniahidi mimi humu Bungeni kwamba mara baada ya kukamilika ile barabara yuko tayari kutoa yale majengo kwa Chuo cha Ufundi VETA. Na sasa barabara yetu inakwenda speed ya ajabu, imebaki kilometa 10 au 12 na wakandarasi wameniahidi Januari au Disemba kipande cha barabara hiyo kitakamilika.
Je, lini sasa mazungumzo kati ya Wizara ya Elimu na Wizara ya Ujenzi yataanza haraka iwezekanavyo wananchi wapate kile chuo?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wake tumeupokea, na mara baada ya kumaliza Bunge hili, tutawasiliana na wenzetu Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ili tuweze kuona suala hili kabla hata barabara hazijaisha.
MHE. ALLY M. KEISSY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Jiji la Dar es Salaam linashangaza kwani wamechukua kampuni ya kutoka Kenya ili kukusanya fedha za maegesho ya magari Dar es Salaam. Vilevile hawatumii mashine za EFD kukusanya pesa na kupandisha kutoka Sh.300 kwenda Sh.500. Hivi kweli nchi nzima ya watu milioni 50 wamekosa kampuni yoyote katika nchi yetu mpaka kuchukua Kampuni ya Kenya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue concern hii ya Mheshimiwa Keissy lakini ninavyojua katika suala la ukusanyaji Manispaa za Ubungo, Ilala na Kinondoni zinakusanya zenyewe lakini kwa ukubwa wake Manispaa ya Temeke na Kigamboni, Halmashauri ya Jiji yenyewe inasimamia jambo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala la kampuni kutoka Kenya kukusanya nadhani huo ni mchakato wao lakini ninavyojua ni kwamba kuna utaratibu maalum kwa Jiji la Dar es Salaam, kila Manispaa kwa maana ya Ilala, Kinondoni na Ubungo zina utaratibu wake wa kukusanya ila Manispaa ya Temeke na Kigamboni Jiji lenyewe linasimamia kwa taarifa nilizokuwa nazo, wanasimamia kama Wakala wa Jiji la Dar es Salaam. Kwa hiyo, Mheshimiwa Keissy kuhusu hii kampuni kutoka Kenya kukusanya fedha hizi ngoja tuzi-cross check zaidi lakini inawezekana ni taarifa za kimagazeti zaidi kuliko uhalisia wake.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Katika kijiji cha Kirando mwambao wa Ziwa Tanganyika, TPA wameweka mtu wao kutoza ushuru mzigo wowote unaotoka pale katika kijiji cha Kirando wakati TPA hawajaweka huduma yoyote. Hamna kibanda, hamna hata
choo, hamna chochote walichoweka lakini kila mwananchi anayesafirisha mzigo kwenda Kabwe, kwenda Mwandakerenge, kwenda Mvuna anatozwa ushuru na watu wa TPA.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA
MAWASILIANO: Mheshimiwa Spika, kuna huduma nyingi za bandari na mojawapo ni kuwa na vyoo, sehemu ya kupumzikia lakini kuna huduma zile za kutoa mzigo kutoka kwenye maji na kuupeleka kwenye nchi kavu. Ile huduma ina gharama, inahitaji kulipiwa. Kwa hiyo, wale ambao wanapata hiyo huduma hata kama hizi huduma zingine hazijakamilika kwa vyovyote vile watatakiwa walipie ili kurecover zile gharama wanazotumia watu wa bandari.
Mheshimiwa Spika, labda tu hoja yake ni kwamba
tuboreshe hii bandari ya Kirando ili huduma zote za bandari ikiwa ni pamoja na uwepo wa vyoo na huduma zingine eneo la kupumzikia abiria tuzijenge. Hilo nimelipokea, tutalifanyia kazi.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kuna Halmashauri nyingi zilianzishwa kwa misingi ya kisiasa na kuacha Halmashauri ambazo zina hadhi kabisa ya Halmashauri. Vipi Serikali inaonaje kuzifuta mara
moja Halmashauri ambazo zilianzishwa hazina vigezo na kuzipa Halmashauri zenye vigezo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya Mheshimiwa Keissy ndio hoja ile ile ya Mheshimiwa Juma Nkamia. Ndio maana nimesema tukisema kuanzia leo hakuna kugawanya Halmashauri zingine, kuna Halmashauri zingine zina mzigo mkubwa kutokana na jiografia yake ilivyo kubwa kwelikweli. Kwa hiyo, tukisema kuanzia leo ni marufuku nadhani kuna baadhi ya Halmashauri hatutazitendea haki. Hata hivyo, ni kweli kuna Halmashauri zingine sasa hivi ukiziangalia kweli kama inawezekana tuzifute kwa sababu jiografia yake na hata population ya watu bado ni ndogo zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, haya yote ni
mawazo ya Waheshimiwa Wabunge lakini jambo kubwa ni kuijenga vizuri Serikali yetu. Nadhani mawazo yao ngoja tuyachukue na tuone kwa pamoja way forward ni nini, lengo likiwa hapo baadaye Serikali yetu iweze kuendeshwa vizuri.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, nakushuku sana. Kwanza naishukuru Serikali kusema kweli kutenga pesa za daraja kiungo muhimu sana kuhusu barabara. Hii barabara ni muhimu inaunganisha mikoa mitatu; Katavi, Rukwa na Songwe, ni muhimu kwa ajili ya wakulima wetu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka jibu sahihi, ni lini Serikali itakuwa tayari kujenga barabara ya lami katika mwambao wa Ziwa la Rukwa ili wananchi wafaidike? Atoe tarehe maalum, ni lini na mwaka gani? Maana hili daraja litajengwa, barabara inaweza ikaendelea hivyo hivyo kuwa tope wananchi wakateseka. Mwambao kule wanalima sana mazao muhimu sana. Kwa kuwa hii nchi ina njaa kila sehemu, tutakuwa tunakomboa sana wananchi wengine kutokana na mwambao wa Ziwa Rukwa kuwa na ardhi nzuri sana…
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, hii
barabara inaanzia Mkoa wa Katavi, Kibaoni inakwenda mpaka Songwe kupitia Mwambao wa Ziwa Rukwa.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Ally Keissy ameuliza kwa sauti nzuri. Nikupongeze sana kwa hilo kwa sababu imenitia moyo.
Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Ally Keissy kwamba kama ambavyo nimejibu katika jibu la swali la msingi barabara hizi zote tunazitafutia fedha. Nimhakikishie kwamba procurement ya kupata mjenzi wa daraja la Kamsamba ambalo ndilo tunaanza nalo ni katika muda wa wiki mbili, tatu zijazo tutakuwa tumeshakamilisha. Ile hela ambayo ilitengwa mwaka huu itatumika na hatimaye mwaka unaofuata kwa hela hizi ambazo tumezitenga ambazo nilieleza toka mwanzo nazo tutakuwa tumekamilisha hii kazi itakuwa imekwisha.
Mheshimiwa Spika, baada ya hapo, sasa tunaenda kwenye barabara hizo.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mwaka jana Mwenge ulizimwa Simiyu, Mtukufu Rais John Pombe Magufuli alizuia misafara ya Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya na baadhi ya Wakurugenzi na kuokoa kiasi cha pesa sijui zaidi ya shilingi bilioni sita.
Nataka kujua kwa mwaka mzima kukimbiza Mwenge wa Uhuru kunagharimu Taifa hili shilingi ngapi? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Keissy.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nimpongeze Mheshimwa Keissy kwa kutambua namna ambavyo Mwenge huu wa Uhuru kwa maagizo ya Mheshimiwa Rais uliweza kuokoa fedha nyingi sana ambazo zilikuwa zikitumiwa na Wakuu wa Mikoa na viongozi wengine kuhudhuria katika mbio hizo za Mwenge. Tumekubaliana kwamba ni lazima tuendelee kuthamini namna nzuri ya matumizi ya fedha katika kukimbiza Mwenge wa Uhuru. Kwa hiyo, hilo halina shaka Mheshimiwa Keissy na sisi tunalisimamia vizuri kwa maagizo ya Mheshimiwa Rais wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya Mwenge wa Uhuru ambayo Mheshimiwa Keissy anataka kujua ni kiasi gani zimekuwa zikiandaliwa kutoka Halmashauri moja kwenda nyingine. Hivyo kama anataka kujua ni kiasi gani bajeti zinatumika katika kila Halmashauri moja kwenda nyingine nitamuomba aonane na mimi na tutawasiliana na hizo Halmashauri.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwanza Mbunge aliyeuliza swali kwamba Wabunge wanatumia zile pesa, namshukuru sana Naibu Waziri alivyoeleza kuhusu zile pesa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pesa Wabunge hawashiki, pesa zinakwenda kwa Mkurugenzi, Mwenyekiti yeye ni Mwenyekiti tu. Kuna Afisa Mipango, kuna Madiwani wawili, kuna watendaji wawili ndipo utagawa zile pesa, hatugusi hata senti tano moja sisi kuweka kwenye mafuta.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, huu Mfuko wa Jimbo nimezungumza tangu mara ya kwanza una matatizo. Kuna majimbo mengine na tujimbo twingine.
Huu mfuko hauwezi kufutwa kwa sababu kuna Wabunge wengine kama Viti Maalum, mzee wangu anasema Majimbo, Majimbo mengine yana watu 30, watu 40, mengine kata 10 Jimbo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza kama nilivyosema mara ya kwanza usimamishwe, wafanye tathmini upya, wagawe upya kutokana na idadi ya watu na ukubwa wa majimbo. Haiwezekani kuna majimbo mengine ni madogo wanapewa sawa na Jimbo kubwa haiwezekani. Ifanywe tathmini upya ili hela ziende kwa usawa bila ubaguzi wowote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majimbo ambayo hayana vigezo, hayastahili kuapata mfuko wa Jimbo mkubwa, haiwezekani. Jimbo lako la Ilala kubwa lipate sawa na Jimbo...
Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuende na takwimu sahihi, haiwezekani.
Swali, Wabunge Viti Maalum hawaruhusiwi kupata Mfuko wa Jimbo na wasitegemee kuzipata, kwa sababu Mbunge wa Jimbo ndiyo anastahili kupata ule Mfuko wa Jimbo na ikiwezekana Wabunge wale wengine wachunguzwe walikotoka. Haiwezekani wewe uliyekuja kuzungumza hapa wakati ulikotoka wewe hauna hata wa...(Kicheko)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Keissy ameuliza maswali ya nyongeza pia ametoa maelezo ya nyongeza. Hata hivyo katika maelezo yake kuna vitu vya msingi amevisema.
Kwanza ambacho ndicho nitakachokijibu vingine nitaviacha kwa sababu kwa mujibu wa Kanuni natakiwa kujibu swali moja. Ni kweli kwamba kuna vigezo vinavyotumika katika kugawa fedha hizi, vigezo hivi vimesemwa katika jibu la msingi. Kigezo cha kwanza ni idadi ya watu ambayo ni asilimia 45. Mgao sawa kwa kila Jimbo asilimia 25, kiwango cha umaskini asilimia 20, ukubwa wa eneo asilimia 10. Fedha yoyote itakayotengwa kwenye bajeti hapa itaingizwa katika hii formula.
Kwa hiyo, bahati mbaya sana kwa mwaka huu wa fedha, fedha iliyotengwa ilikua kidogo kwa sababu Hazina hawakutambua majimbo haya mapya, hatukuwa na mawasiliano mazuri. Nataka niwahakikishie kwamba kigezo hiki sasa kwa mwaka huu wa fedha tumesahihisha hayo makosa yote na sasa majimbo yote yanahesabika, yaliyoongezeka na kosa hilo halitafanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba kuna baadhi ya Majimbo yanapewa fedha kidogo kwa mujibu wa formula hii, hilo haliwezekani isipokuwa fedha zimeshuka tu kwa sababu zilikuwa kidogo na tulilazimika kuziingiza kwenye formula hii kama zilivyo, ndiyo maana ni tofauti na iliyotolewa nyuma na iliyotolewa sasa.
MHE. ALLY K. MOHAMED:Ahsante sana Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi bima za afya baadhi ya maduka na hospitali zinatumika vibaya, kuzidisha double allocation mtu anaenda kutibiwa anaweza akaandikwa double akaiga saini ya mteja au na zingine zinazidisha bei mara mbili, je, nani anazikagua bima ya afya kabla ya malipo, kwa kuwa zinaendesha wizi wa hali ya juu.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti ni kweli kwa kipindi kirefu sasa hata ukija kuangalia wakati mwingine kuna takwimu na kuna fraud inafanyika katika hizi document hasa za bima ya afya na ndio maana sasa hivi utaratibu wa bima ya afya imeweka sasa hivi document ambayo haijakaa vizuri hawawezi kuilipa, lakini hili sasa naomba niwa sisitize hasa katika wenzetu wa bima ya afya wahakikishe wanaweka mechanisim nzuri ya kuweza kuangalia tuna monitor hizi fomu zinajazwa vizuri, lakini sio kujazwa tu, iangalie ili mradi compliance kwamba fomu iliyojazwa ndio kweli iliyotoa matibabu.
Kwa hiyo Mheshimiwa Keissy naomba tuichukue hoja hii kwa sababu ni hoja ya msingi tunaenda kulinda fedha za wananchi, fedha za serikali tutaenda kulisimamia vizuri kwa kadri iwezekanavyo.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, naishukuru Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Rais, Mheshimiwa John Pombe Magufuli, kwa mara ya kwanza wananchi wa Kazovu, Isaba, Chongo na Katete wataona hata bajaji na gari. Nilipoingia Bungeni mwaka 2010 kilio changu cha kwanza ilikuwa ni barabara lakini awamu ya sasa ni awamu ya chapakazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali dogo, Mheshimiwa Naibu Waziri juzi umetuma wakandarasi wako kuangalia kipande kilichosalia cha kutoka Kazovu kwenda Korongwe, lini sasa Serikali yako itasaidia kipande hicho kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi haina fedha?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Keissy kwa kazi kubwa anayoifanya ya kutafuta barabara hii ijengwe na hatimaye sasa amepata majibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa na mimi napokea salamu hizo za pongezi kwa niaba ya Serikali kwamba tumedhamiria barabara hii ikamilike. Ndiyo maana nimepeleka wataalam wangu kwenda kuiangalia kazi hiyo ili hatimaye tuangalie namna gani tunafanya na kama tulivyojibu katika swali la msingi kwamba sasa tunatafuta fedha kwa ajili ya kuishughulikia barabara hii tukianzia na feasibility study and detail design.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, kumekuwa na malalamiko mengi sana, hii inaitwa road licence kama anavyosema, gari yangu mfano imekaa jikoni, uani, garage miaka mitatu, sina pesa za kutengeneza lakini nikadaiwa hiyo road licence na faini juu. Kwa nini Serikali isione kwa sasa kwamba kwa nini wasiingize kwenye mafuta ili gari yangu ikitembea mimi nilipie kodi moja kwa moja kuliko kumtesa mtu gari yake imekaa jikoni miaka mitatu aendelee kulipa kodi wakati hana uwezo hata kununua spare. Gari yake kama anavyosema imepata ajali, lakini gari inaweza kukaa miaka mitatu, asiyekuwa na uwezo wa kutafuta pesa, lakini itaendelea kudaiwa road licence na inapigwa na faini juu, hii ni halali kweli? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa nini msichukue kigezo cha kuweka kwenye mafuta, pesa kwenye mafuta, ili ninapotembeza ile gari yangu nalipia moja kwa moja road licence?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, najua ni jambo muhimu sana hili kwa Taifa letu na kwa wananchi wetu. Kama Serikali tumesikia na tunalifanyia kazi kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya mwanzo, lakini naendelea kusisitiza na kumwambia ndugu yangu Ally Keissy hii tunalipia umiliki na sio matumizi ya gari yako barabarani.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na jibu zuri la kuridhisha la Serikali nina swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Mto Lukuga kupoteza maji katika Ziwa Tanganyika, je, Serikali iko tayari kuwahamasisha wananchi wanaokata miti katika milima yote inayozunguka Ziwa Tanganyika, ili wakati wa masika maporomoko yote yanayoleta tope, mchanga, kupunguza kina cha maji ya Ziwa Tanganyika, kuacha shughuli hizo?
Mheshimiwa Naibu Spika, pia, je, Serikali iko tayari kuwaelimisha wananchi waache kukata miti hovyo na kuwachukulia hatua wote wanaofanya kandokando ya Ziwa Tanganyika kufanya shughuli ambazo Serikali hairidhishwi, kama kujenga karibu na ziwa na kuharibu vyanzo vya maji vinavyoporomosha maji katika Ziwa Tanganyika?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niseme kwamba, nilipata fursa ya kwenda Kinshasa kwa ajili kukutana na Mawaziri wenzangu wa Mazingira kuhusu suala la kupungua kwa kina cha maji cha Ziwa Tanganyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikutana na Waziri wa Burundi, Zambia na Congo; na mpaka sasa hivi, nimpe tu taarifa njema Mheshimiwa Keissy, kwamba tumefika mahali pazuri kati ya Serikali hizi na Benki ya Dunia kuhusu upatikanaji wa zile fedha za kujenga banio ili kuzuia maji kutoka kwa kasi kwenye Ziwa Tanganyika kwa upande wa Congo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu hili suala la pili, ni kweli changamoto ipo kubwa. Nilipata bahati ya kutembea mikoa yote iliyo katika Mwambao wa Ziwa Tanganyika na kuna tatizo kubwa sana la shughuli za kibinadamu zinazosababisha ziwa kujaa tope na hata Bandari ya Kigoma pamoja na Kasanga na miji yote iliyoko kando ya mwambao kupata changamoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumetoa maelekezo kwa Wakuu wa Wilaya na viongozi wa halmashauri katika maeneo yote kuhakikisha kwamba, Sheria ya Mazingira inazingatiwa na shughuli za kibinadamu katika mita 60 kutoka kwenye mwambao wa Ziwa zinasitishwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu changamoto iliyopo kwa sababu watu wengi wanategemea uvuvi na shughuli nyingine na maji yaliyopo pale kufanya hiyo. Kwa hiyo, tunategemea ushirikiano wa Mheshimiwa Mbunge ambaye yeye ni mwanamazingira mzuri sana, Mheshimiwa Keissy, pamoja na viongozi wote tuweze kufanikiwa katika hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, wito wangu ni kwamba, Wakuu wa Mikoa ya mwambao wa Ziwa Tanganyika wanaweza kufanya mkutano na forum pamoja na Wabunge, ili kujadili ustawi wa Ziwa Tanganyika kwa ujumla na sisi Ofisi ya Makamu wa Rais tutakuwa tayari kuunga mkono huo mkutano (forum) wa wadau wote wa Ziwa Tanganyika, ili kuangalia suala hilo na masuala mengine yanayohusiana na ustawi wa ziwa hilo.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Ingawa Serikali ina mpango sana wa kufungua mabenki ya wakulima, je, Serikali haioni kama tatizo hiyo benki inafilisika kwa kuwa wakati wa msimu mkulima analazimishwa asiuze mazao bei anayotaka? Kwa mfano, mahindi kule kwetu yanashuka bei, mengi hakuna mahali pa kupeleka.
Je, Serikali haioni kwamba iweke sheria mtumishi abanwe mshahara wake ili asiutumie hovyo ili wakati wa matatizo awasaidie majirani zake kama vile wakulima wanavyofanywa ili wasiuze mazao wasaidie sehemu zenye njaa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Spika, nashukuru unaelekea kunilinda tusifungue suala hilo kwa sababu ni jambo zito lakini naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kwa sasa tunatambua changamoto ambayo imeletwa na zuio la kuuza mahindi nje kitu ambacho kimefanyika na Serikali kwa nia njema. Kwa sasa Serikali inajitahidi kuongea na WFP ya Serikali ya DRC Congo vilevile Sudan ya Kusini ili kuangalia namna ya wakulima wetu kuweza kuuza mahindi nje.
Mheshimiwa Spika, naomba tu niendelee kusema kwamba zuio hilo halina nia mbaya lakini tunajitahidi kuhakikisha kwamba nchi yetu inakuwa na usalama wa chakula. Vilevile tunajaribu kuangalia kama tutapata fedha ili NFRA iweze kununua mahindi mengi zaidi lakini Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko nayo imekaribia kupata mkopo wa kununua zaidi ya tani 10,000. Kwa hiyo, tunaamini pamoja na changamoto iliyopo tutahakikisha kwamba baadhi ya mahindi ya wakulima yataweza kununuliwa.
Mheshimiwa Spika, kubwa zaidi tunaendelea kutoa rai kwa wafanyabiashara wanunue mahindi maeneo ambayo yanapatikana kwa wingi ambayo bei yake bado ni nzuri na wapeleke maeneo ambayo hayajapata mavuno vizuri, kwa mfano mwaka huu tuna uhaba wa chakula Mwanza, Simiyu, Shinyanga huko kote kunahitajika chakula. Kwa hiyo, wafanyabiashara wetu watumie kama fursa kwa sababu mara nyingine tunaposema tutoe fursa ili wakulima wetu wauze mahindi nje, ukweli wa mambo wanaouza mahindi nje siyo wakulima ni walanguzi. Mara nyingi mkulima bei anayoipata bado ni ndogo ile ile wala haifanani na ikikaa kidogo na akauza baadaye ndani.
Mheshimiwa Spika, vilevile lengo letu la kuongeza uwezo wetu wa kuhifadhi chakula ni ili wakulima wetu waweze kuhifadhi ili ikiwezekana wauze kwa utaratibu wa stakabadhi ghalani ambayo wanaweza wakapopeshwa fedha na mabenki kwa kutumia akiba yao ambayo itakuwepo kwenye maghala.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachukulia mfano wa mabasi, kuna utingo, kuna dereva, kuna konda, mwenye licence ya kuendesha chombo pale ni mmoja tu ambaye ni dereva, utingo hana licence wala konda. Cha ajabu katika Ziwa Tanganyika mwenye chombo anakuwa na wavuvi wake kama kumi au kumi na tano na wote wanalazimika kuwa na leseni. Je, Serikali haioni kama ni kero?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, haya ndiyo mabadiliko tunayokwenda kuyafanya katika Kanuni za Uvuvi, kuboresha ili kuweza kumuinua mvuvi wa Tanzania. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Keissy kanuni yetu ya Uvuvi tunayokwenda kuibadilisha itazingatia matakwa haya ya Waheshimiwa Wabunge.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Hii Awamu ya Tano, kila siku namsikia Mheshimiwa Rais anazungumza haya mambo, kwamba ukinunua kitu dukani omba risiti; ukienda hotelini, omba risiti, je, Serikali imejipangaje kuhusu hawa wauza mitumba na wanaotembeza mali (machinga) na mama ntilie kwa ajili ya kutoa risiti ili tupate kodi ya Serikali yetu? Serikali imejipangaje hapo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Keissy, kwa nyakati tofauti amekuwa akihimiza sana suala la ulipaji kodi. Naomba tukiri kwamba hii nchi haitaweza kwenda bila watu kulipa kodi. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais, 2015 ametudokeza sehemu moja, mfanyabiashara mmoja anaingiza karibu shilingi milioni saba kila dakika. Kwa hiyo, kuna watu wakubwa wanakwepa kodi na wadogo wakati mwingine kodi hazikusanywi vizuri.
Mheshimiwa Keissy naomba nikuhakikishie, Ofisi ambayo inaongozwa na kaka yangu, Mheshimiwa Dkt. Mpango imejipanga vizuri kuhakikisha kwamba inafanya utaratibu mzuri, kila mtu atalipa kodi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nisisitize tena; na sababu ni kwamba katika kada zote, kila mtu atawekewa utaratibu mzuri ilimradi kodi tupate shilingi trilioni 29.54 kutimiza matakwa ya bajeti yetu. Naomba tushirikane na Serikali kwamba wale wenye sheli za mafuta waweke mashine za mafuta na kila mtu atumie mashine za EFD katika Halmashauri zote, tutumie elektroniki na kila utaratibu, kwamba Mheshimiwa Dkt. Mpango ametuwekea utaratibu kuona jinsi gani tutafanya tukusanye kodi kila mtu alipe kodi bila kukwepa kodi.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante leo ni karibu siku tatu BBC inatangaza kuhusu Ziwa Tanganyika kuathiriwa na kukata miti, na kutoweka samaki. Je, Serikali ina mpango gani kuzuia na kusaidia kuzungumza na nchi ya DRC Kongo, Burundi na Zambia ili kujenga kibanio katika mto Luguga ili maji yasiishe katika Ziwa Tanganyika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tutakachofanya tutafanya tadhimini ili tuone hasa ambacho kinasababisha upungufu wa samaki pamoja na uharibifu wa mazingira unaofanyaika katika Ziwa Tanganyika ili tuweze kujua hasa hatua stahiki tunazotakiwa kuchukua ili kuweza kurejesha hali hii, na katika kufanya hivyo ushauri alioutoa Mheshimiwa Keissy tutauzingatia baada ya kuwa tumefanya uhakiki na kubaini yawezekana zipo factors nyingine ambazo hazifahamiki kwa sasa. Kwa hiyo, zitafahamika tu pale ambapo tutafanya tadhimini na kujiridhisha.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria inasema mwambao wa Ziwa Tanganyika ni mita 60, lakini kuna upendeleo wa hali ya juu hasa kwenye Kijiji cha Kilando, wanavunjiwa watu na baadhi hawavunjiwi ambao wako chini ya hiyo kiwango cha mita 60. Je, Mheshimiwa Waziri anatoa tamko gani kuhusu wananchi wanaokaa mwambao mwa Ziwa Tanganyika kuacha upendeleo, kuvunjiwa baadhi ya watu na wengine kuachwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hii sheria au utaratibu huu kwanza lengo lake kubwa ni kuhakisha tunalinda vyanzo vyetu vya maji. Leo hii katika nchi yetu maeneo mbalimbali, maeneo chepechepe, maeneo oevu, yote yanatoweka kwa sababu kuna uvamizi mkubwa sana na ndio maana tunakumbwa na janga kubwa na ukosefu wa maji katika maeneo yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, imani yangu kwamba, sheria itafuatwa hasa na Watendaji wetu wa chini, tusifanye double standard katika maeneo mbalimbali. Lazima kama tunafuata sheria utekelezaji wa sheria kwa sababu tunasema sheria ni msumeno, lazima ufuate hakuna kusema kumwonea mtu huyu na unamuacha mtu huyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Keissy kwamba wataalam wetu tutawaelekeza kwamba wanapokwenda kutekeleza sheria, lazima waache utaratibu wa double standard ili sheria itekelezwe kwa haki katika nchi yetu.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Hivi vyanzo vya maji kuvihakiki ni kwingine, Ziwa Tanganyika hakuna kazi inayofanyika, watu wanajenga majumba mpaka yanagusa Ziwa Tanganyika, lakini hakuna operation iliyofanyika, hakuna chochote. Hivi vyanzo vya maji ni kwingine tu, Ziwa Tanganyika mbona hakuna chochote kinachofanyika katika nchi hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye swali letu la msingi, ni kwamba katika maziwa yote, mito yote pamoja na bahari ni kweli kabisa kwamba Sheria yetu Na. 20 ya 2004 ya Usimamizi wa Mazingira inakataza shughuli za binadamu kufanyika ndani ya mita 60.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto iliyoko Ziwa Tanganyika ni sawa na changamoto ambazo ziko kwenye maeneo mengine. Ndiyo maana tumesema tunataka tubaini ili tujue ukubwa wa tatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo wale wanaofanya shughuli za binadamu kwenye mita 60 katika Ziwa Tanganyika. Inawezekana wanafanya kwa mujibu wa kifungu cha 57(2) lakini tutatuma timu ya wataalam chini ya Mkurugenzi wa Mazingira kwenda kuona kama hao aliowasema Mheshimiwa Keissy wanaruhusiwa kwa mujibu wa kifungu cha 57(2) au la ili tuweze kuchukua hatua stahiki. (Makofi)
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, asante sana. Kwanza nampa pole ndugu Jaku jana kwa kutolewa nje ya Baraza la Wawakilishi na Naibu Spika.
Mheshimiwa Spika, lini sasa utafanyika utafiti maalum wa uagizaji sukari upande wa Zanzibar ili kulinda Kiwanda cha Mahonda?
Mheshimiwa Spika, lini sasa Zanzibar itajiunga na Mfumo wa Kodi wa TANSIS? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, kimsingi Wizara yetu imekuwa ikifanya kazi kwa karibu sana na Mheshimiwa Waziri upande wa Zanzibar, kwa hiyo, katika suala hili la kufanyia utafiti juu ya sukari Zanzibar ni suala muhimu sana ili kuona kwamba kunakuwa na sukari ambayo itawezesha hata kukifanya hata Kiwanda cha Mahonda kifanye kazi yake vizuri zaidi na kuwe na ile bei ambayo ni shindani. (Makofi)
MHE. ALLY M. KEISSY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Ziwa Tanganyika linamilikiwa na nchi nne: Burundi; Zambia; DRC Congo; na Tanzania. Hivi karibuni Ziwa Tanganyika upande wa Uvira DRC Congo ghafla limebadilika rangi na kuwa rangi ya kijani ingawa maji hayana rangi. Je, Wizara ya Muungano na Mazingira inayo taarifa hii?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba ziwa hili linamilikiwa na nchi tatu na kuna Mamlaka ya Ziwa Tanganyika (Lake Tanganyika Authority) na juzi tulikuwa na mkutano hapa na viongozi wa Mamlaka hiyo kuzungumzia uhifadhi mzima wa Ziwa Tanganyika ikiwemo hili suala lakini pia suala kubwa zaidi la kukatika kwa ukingo kwenye Mto Lukuga ambao unatoa maji mengi kwenye Ziwa Tanganyika na kuyapeleka Mto Congo. Kwa hiyo, haya masuala mawili tunayafuatilia na tutampa mrejesho Mheshimiwa Mbunge kuhusu matokeo yake.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi wa Ruafi Katongoro umegharimu zaidi ya shilingi bilioni 1.8 ili kusaidia wakulima zaidi ya 4,000 katika vijiji vya Kata ya Itete, Kirando na Kipili. Lakini mpaka sasa huo mradi haunufaishi wakulima na umejengwa chini ya kiwango.
Je, Waziri yuko tayari kutuma wataalam kwenda kukagua kama huo mradi kweli hizo pesa zimetumika za JICA Japan bilioni 1. 8 ni halali na scheme yenyewe haifanyi kazi yoyote?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge Keissy kwamba niko tayari wakati wowote baada ya Bunge Mheshimiwa Mbunge tuambatane na wewe twende tukaangalie hiyo scheme. (Makofi)
MHE. ALLY M. KEISSY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Lini mradi wa maji ambao ulipatikana kwa njia ya ufisadi katika Kijiji cha Kamwanda, Kirando utaanza? Maana yake wananchi mpaka sasa wanasubiri, siyo kosa lao, wanateseka siyo kosa lao, wananyanyaswa siyo kosa lao. Lini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na nia njema ya Serikali katika kuhakikisha inatatua tatizo la maji na imekuwa ikipeleka fedha nyingi maeneo mbalimbali, lakini kumekuwa na ubabaishaji na wakati mwingine hata baadhi ya wakandarasi kufisadi fedha za Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilifanya ziara katika Jimbo la Mheshimiwa Keissy tukagundua ufujaji fedha zile, tukahakikisha kwamba TAKUKURU wanachukua hatua. Sasa hivi kuna hatua mbalimbali ambazo zinachukuliwa na vyombo hivi vya dola. Namwomba nimweleze Mheshimiwa Keissy, katika kipindi hiki sisi kama Wizara ya Maji tutahakikisha wananchi hawa wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza wakati Serikali ikiendelea na suala zima la kuwashikilia wale watu ambao wanawatuhumu.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa naibu Spika, ahsante sana. Kuhusu Hoteli ya Kitalii ya Mikumi: Je, Mheshimiwa Naibu Waziri anafahamu kwamba mwekezaji wa kwanza alifanya hujuma makusudi baada ya kuchukua shilingi bilioni nne na mpaka leo akaichoma hoteli ile?
Je, Serikali imechukua hatua gani kwa yule mwekezaji wa kwanza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli kama Serikali hatuna taarifa kama kweli ile ilichomwa kama hujuma, lakini tunachojua ni kwamba ilipata janga la moto mwaka 2009 na ikaungua yote. Yule aliyekuwa amekabidhiwa baada ya hapo, alishindwa kuendeleza. Baada ya kuona ameshindwa kuendeleza, ndiyo maana Serikali tukaamua tena kuchukua hatua kuhakikisha kwamba tunamtafuta mwekezaji mwingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwekezaji huyu sasa liyepatikana amekuja na michoro mizuri sana na design nzuri sana ambazo ninazo hata baaadaye Mheshimiwa Keissy naweza nikamwonyesha hapa jinsi ilivyo ambapo tunategemea itakapofika mwaka 2019 hoteli yenyewe itakuwaje? Kwa hiyo hilo tunalo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hilo la kusema kwamba alifanya hujuma, hizo taarifa hatunazo kama Serikali.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Msimu uliopita mbolea na mbegu Mkoa wa Rukwa hazikufika kwa wakati na hazikuwa na impact yoyote. Je, msimu unaokuja atatuhakikishia kwamba mbolea na mbegu zitafika kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye jibu langu la msingi la Mheshimiwa Dkt. Nagu, nilijibu kabisa kwamba Serikali imeshajipanga kuhakikisha kwenye msimu ujao mbolea inafika kwa wakati.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, Zanzibar sukari haitoshi kwanza.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Spika, naomba niwaeleze hili suala sio rahisi namna hiyo mnavyofikiria, ndiyo siyo suala rahisi, I am very good in talking a can talk, simple rahisi, Mheshimiwa Turky ulipopewa kibali na Serikali kuagiza sukari kwa nini wewe ukuuza bei rahisi? (Kicheko)
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsnate sana. Tangu alipouziwa hilo shamba, leo ni miaka 12, lakini mpaka leo hajaendeleza hata ekari moja, imekuwa ni shamba pori na kusababisha vijiji vilivyozunguka hilo shamba vya Sikaungu, Songambele na Msanda Muungano kukosa sehemu ya kulima. Mkoa wa Rukwa, wananchi wote wanategemea kilimo, sasa kwa nini wanasitasita wasimpelekee Mtukufu Rais kulifyekelea mbali hili shamba, kulifuta kama alivyofuta mashamba mengine?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Hilo shamba linamilikiwa na Halmashauri ya Sumbawanga DC na Manispaa. Cha ajabu, vigezo gani vilitumika, mkataba uliingia peke yake na Manispaa ya Sumbawanga kuuza hilo shamba bila Manispaa ya Sumbawanga DC kushirikishwa?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Ally Keissy kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la ufutaji mashamba halianzii kwenye Wizara ya Ardhi, suala la ufutaji mashamba kama halijaendelezwa wahusika wa kwanza ni zile mamlaka zenyewe za upangaji miji katika maeneo yao. Kwa hiyo, kama wao waliona kwamba hili shamba pengine halijakidhi vigezo, linatakiwa kufutwa, walitakiwa wao walete mapendekezo hayo kwa Waziri na Waziri angemshauri Mheshimiwa Rais kulifuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hiyo haitoshi, walikuwa pia na mgogoro naye na walipelekana Mahakamani. Halmashauri yenyewe husika ikatoa shauri Mahakamani na wakakubali ku-settle nje ya court. Kwa hiyo, sisi kama Wizara hatuwezi kuingilia makubaliano yao. Kwa hiyo, kama bado wanaona hajaendeleza, basi warudi tena wao wachukue maamuzi kama waliyokuwa wamechukua mwanzoni ya kuchukua hatua. Wakileta, sisi tutashughulikia vinginevyo itakuwa kidogo ni tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili anaongelea kwamba shamba lile linaingia katika Halmashauri mbili; nadhani katika ziara yangu niliyofanya mwaka 2017 suala hili nililipata na nililitolea maelekezo. Nilisema kama pale ambapo unakuta shamba la mwekezaji limeingia katika Halmashauri mbili tofauti, ni jukumu la Halmashauri husika kuzungumza naye kuweza kuona ni namna gani Halmashauri zote mbili zitafaidika na mwekezaji huyo kama ameingia katika maeneo yao. Sasa sisi kama Wizara hatuwezi kuwapangia namna ya kukubaliana, kwa sababu ni mazungumzo kati ya mwenye eneo na mwenye mamlaka ya upangaji miji na yule mwekezaji aliyeko katika eneo lao. Kama itashindikana, wanahitaji ushauri kutoka Wizarani, tuko tayari kuwasaiia kwa suala hili.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri yanaridhisha lakini ahakikishe kweli, maana yake vijiji hivi vimekaa porini sana, havina mawasiliano, tena kwenye mbuga za wanyama mtu akijeruhiwa inakuwa taabu hata mawasiliano ya gari kuja kuwachukua.

Mheshimiwa Spika, swali la pili la nyongeza; katika Kijiji cha Kizi ambapo kuna mkongo wa mawasiliano umejengwa na Serikali lakini kijiji hakina mawasiliano, je, Mheshimiwa Waziri, nimemfuata ofisini kwake zaidi ya mara kumi kuhusu Kijiji cha Kizi, vipi anaoneje hilo swali langu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ally Keissy kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza ametaka nimhakikishie kwamba eneo hilo ambalo limetajwa nitafikisha mawasiliano. Kama nilivyomhakikishia ni kwamba vifaa viko bandarini, sasa hivi tulikuwa tunafanya clearance kwa ajili ya kuvipeleka sehemu husika. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutapeleka hayo mawasiliano kabla ya mwisho wa mwezi wa Sita kama nilivyoahidi.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusu Kijiji cha Kizi; tayari nimekwishatembelea kijiji hicho na tulikuwa na Mheshimiwa Mbunge. Kwanza nimpongeze kwa jinsi anavyofuatilia masuala ya mawasiliano, katika majimbo mengi sana hapa nchini, jimbo lake lina asilimia 93 ya kupatikana kwa mawasiliano, nimhakikishie tu kwamba hicho kijiji chake kilichobakia tutakwenda tutashughulikia na tutakiingiza kwenye Mpango wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri tuliambatana naye mpaka Kipiri Port. Sasa namuuliza lini usanifu wa barabara ya Namanyere – Kipiri Port utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Keissy, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli nimetembelea eneo la Kipili, Mheshimiwa Mbunge anafahamu yapo mambo mengi, nimpongeze tu kwa kweli kwa ufuatiliaji wake kwa sababu hata hii Bandari ya Kipili kule iko vizuri, tumeona maendeleo mazuri lakini uko umuhimu sasa wa kuunganisha kwamba tunakuwa na bandari nzuri lakini tunahitaji pia tuwe na barabara nzuri ya kuwapeleka wananchi katika maeneo hayo. Tumeona pia kuna uchumi mzuri, kuna samaki wanavuliwa maeneo yale wananchi hawa wanahitaji hii barabara.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie tu Mheshimiwa Keissy, kama tulivyojipanga katika mwaka huu wa fedha tuliitengea fedha kwa ajili ya usanifu, harakati za awali zinaendelea, lakini katika mwaka unaokuja pia tutaweka mapendekezo ya fedha,ili tukamilishe usanifu na tuweze kuanza kujenga kipande hiki cha barabara kilometa kama 72 hivi kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika. Mradi wa Ruafi Katongoro Irrigation skimu serikali imetumia zaidi ya bilioni 1.8; Lakini hauna faida yoyote kwa wakulima zaidi ya 2000 wa Kata za Kilando, Kipili pamoja na Itete.

Je, ni lini Wizara kilimo na umwagiliaji itaenda kuimarisha mradi wa skim ya katongoro na ruafi ili wakulima wanufaike na kilimo cha mpunga?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali moja la Mheshimiwa Ally Keissy kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyokuwa najibu swali la msingi, kwamba kuna miradi mingi ambayo imejengwa chini ya kiwango pamoja na Serikali kupeleka kiasi kikubwa sana cha fedha kwa ajili ya mahitaji ya wakati huo. Kwa sasa hivi serikali tutatuma timu ya wataalam kwenda kuangalia mapungufu yaliyofanyika katika mradi huo; na haraka iwezekanavyo baada tathimini hiyo tutaanza kupanga fedha kwa mujibu wa bajeti kwenda kuwahudumia watu hawa zaidi ya 2000 kwenye kilimo cha kisasa.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, High School ya Kirando tumejenga maabara leo miaka minne, na mlileta vifaa vya maabara vinakaa chini vinaliwa na mchwa. Lini Serikali itapeleka pesa kumaliza majengo matatu ambayo yako tayari yameshapigwa bati lakini yamekaa kama vichaka vya kuchezea panya ndani?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Keissy na DC wake wa Wilaya ya Nkasi, ndugu yangu Saidi Mtanda, katika wilaya ambazo zinafanya kazi kubwa sana ya ujenzi wa miundombinu ni Wilaya ya Nkasi.

Mheshimiwa Spika, na niseme juhudi iliyofanywa na wananchi katika eneo hilo, hasa ujenzi wa hiyo maabara, juzijuzi kama nilivyosema tulipeleka fedha ili wabainishe yale maboma, nadhani hilo ni miongoni mwa maboma. Nimuagize Mkurugenzi katika vile vipaumbele ambavyo tumepeleka fedha hizi za maboma hilo liwe sehemu mojawapo, sasa sijui kama watakuwa hawajaingiza. Lakini tutafuatilia, kuhakikisha ofisi yetu maabara hiyo inakamilika, maabara iweze kufanya kazi, Mheshimiwa Keissy usiwe na hofu.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nchi yetu kwa sasa ina miundombinu mizuri kuliko enzi za ukoloni au enzi zilizopita. Je, Serikali inaonaje kwa muda huu kupunguza idadi ya wilaya, idadi ya majimbo ya mikoa ili Serikali ipate pesa, i-save pesa kwa ajili ya kupunguza idadi ya mikoa, idadi ya majimbo na idadi ya wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, tumemsikia Mheshimiwa Ally Keissy kwa maoni yake na mtazamo wake lakini maeneo haya kiutawala yakiwepo majimbo ya uchaguzi ya Waheshimiwa Wabunge hawa wapendwa, wilaya, mikoa na maeneo mengine ya kata na vijiji yanaanzishwa kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa utakapofika wakati wa kuona kwamba kwa hilo wazo la Mheshimiwa Keissy ni muhimu kufanyiwa kazi tutalifanyia kazi. Kwa sasa msimamo ni kwamba tutaendelea kuimarisha maeneo yaliyopo kujenga miundombinu, kupeleka huduma mbalimbali za kijamii ili watu wote waweze kupata maisha ambayo ni bora zaidi.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Vifo vingine vya akina mama vinatokana na akina mama wenyewe. Juzi tu Kirando katika Jimbo langu la Nkasi Kaskazini, mama mmoja, tena zao lake la nane, kachelewa mwenyewe makusudi, Kirando kuna kituo kizuri cha afya kikubwa na kizuri kinafanya na operesheni, ni kizuri sana. Kajifanyia operesheni mwenyewe kwa kutumia nyembe na katoa mtoto. Hivi sasa yuko hospitali katika Kituo cha Afya cha Kirando, hali yake siyo nzuri, ila hali ya mtoto ni nzuri. Vifo vingine vinasababishwa na akina mama wenyewe kuchelewa kwenda kwenye Vituo vya Afya. (Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA MADINI (K.n.y. WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO):
Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Afya, naomba nijibu hoja ya Mheshimiwa Keissy kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kama nilivyozungumza katika majibu ya nyongeza ni kwamba akina mama wote nchini unapokuwa mjamzito, pale anapojitambua tu kwamba sasa hivi amekuwa mjamzito ni vyema ukaenda kliniki kwa ajili ya kwanza unaenda kupimwa, wanaangalia development ya mtoto, lakini vilevile wanaangalia afya yako wewe mama kama inakwenda vizuri na kama kuna tatizo watakwambia na nini ufanye.

Mheshimiwa Spika, vilevile ni kwamba kwa kipindi hicho wanakupa elimu ya uzazi salama. Kwa hiyo, ni vizuri wakina mama wote wakati wa kujifungua hili suala usichukulie kama zamani, tulikuwa na ma-tradition healers wale wanaitwa Wakunga wa Jadi, wasiende tena kule. Wengine pengine alivyosema Mheshimiwa Keissy, huyu mama ana uzao mwingi, kwa hiyo, ameshakuwa na experience, anaona kwamba kuzaa ni kitu rahisi, lakini kumbe kila kizazi ni special. Ni vizuri ukaenda kwenye Kituo cha aAya ukapewa huduma na Manesi ambao ni professional.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, kuna mradi wa maji Kirando Mheshimiwa Naibu Waziri anaujua, Waziri anaujua. Je, lini sasa mtampa mkandarasi kazi aanze kupeleka maji katika Kijiji cha Kirando wakati tumeokoa huo mradi shilingi bilioni tatu ilikuwa shilingi bilioni 7.5 tukawabana majizi na wengine waka fukuzwa kazi kwenda usanifu wa pili mradi umefika shilingi bilioni 4.6 lakini mpaka leo hajapewa mtu mwenye uwezo kwenda kumalizia ule Mradi wa Maji Kirando?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kiukweli amefanya kazi kubwa sana na sisi kama viongozi wa Wizara tumefika katika eneo lile la Kirando kiukweli moja ya miradi ambayo imekuwa ikichezewa ilikuwa miradi ya maji vijijini na tunalishukuru Bunge lako tukufu na Mheshimiwa Rais itakapofika tarehe 1 Julai miradi yote ambayo imekuwa ikisimamiwa na Halmashauri inarudi kwetu katika Wizara yetu ya Maji.

Mheshimiwa Spika, nataka nikuhakikishie makandarasi kwa maana ya Kampuni pamoja na Wahandisi wa Maji ambao wametutia hatiani sisi Wizara ya Maji hawana nafasi ya kazi katika Wizara yetu ya Maji. Lakini makampuni yale mengine yote tutayafutia na katika kuhakikisha kwamba hayatofanya kazi yoyote katika Wizara yetu ya Maji, na nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge baada ya kutatua changamoto ile na kuokoa fedha tunamuagiza mkandarasi kwa maana ya utangazaji wa kazi ili ianze mara moja ili wananchi wake wa Kirando waweze kupata huduma ya maji safi na salama. Ahsante sana.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kuna baadhi ya Wenyeviti katika vijiji vyetu baada kuteuliwa tu baada ya miezi mitatu/minne wanajiuzulu wengine wanafariki, lakini hakuna chaguzi zinafanyika na mfano hasa kwenye Wilaya yangu kunakaa wazi, wanateuliwa tu mtu anakaimu anakuwa pale, sasa demokrasia inasemaje kuhusu watu wanaojiuzulu na wanaofariki kwa nini uchaguzi haufanyiki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, inawezekana kweli, nimesikia sikia naomba nitoe maelekezo, kwanza, hakuna mtu anaitwa Kaimu Mwenyekiti wa Kijiji, Kitongoji au Mtaa kwa mujibu wa Sheria za Serikali za Mitaa, haipo hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachofanyika ni kwamba Wajumbe na kuna watu wengine mtu akijiuzulu anakaimu kwa muda mrefu na anatembea na muhuri kwamba ni Mwenyekiti, hilo zoezi kama lipo kuanzia sasa na leo muda huu, likome halipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachofanyika mtu akijiuzulu Wajumbe wa Serikali ya Mtaa wanapokutana kwenye kikao, miongoni mwao anakuwa Mwenyekiti wa kikao hicho na uenyekiti wake unakoma mara tu baada ya kikao kuisha wakati ule, anayepaswa kufanya kazi ya kiutendaji ni Mtendaji wa Kijiji au Mtendaji wa Mtaa mpaka uchaguzi ufanyike, lakini uchaguzi wa Serikali za Mitaa, wakati wowote ikitokea gap tunategemea kupata taarifa kutoka ngazi ya Kijiji au Mtaa inakuja TAMISEMI, tunaruhusu wafanye uchaguzi kwa sababu kwanza unasimamiwa na eneo husika pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mtu akijiuzulu, kwa mfano mwaka mmoja kabla ya Uchaguzi Mkuu kama sasa, hatukuruhusu kwa sababu sheria inazuia huu muda hauruhusiwi, lakini muda wowote wa nyuma Mheshimiwa Ally Keissy kama ilitokea ni bahati mbaya sana na tunaisimamia tupate taarifa baada ya uchaguzi huu, kama inatokea mtu amejiuzulu baada ya muda siyo mrefu sana inabidi achaguliwe ili wananchi wahudumiwe na mtu ambaye wamempigia kura, waweze kumwajibisha kwa ile imani waliyompa. Ukikaimisha mtu ambaye hawakumchagua wao watashindwa kumwajibisha na ukienda kumuhoji anasema mimi siyo Mwenyekiti nilikuwa nakaimu na anakimbia majukumu yake. Ahsante. (Makofi)