Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Dr. Augustine Philip Mahiga (24 total)

MHE. HAFIDH ALI TAHIR aliuliza:-
Baadhi ya Watanzania wanajitafutia maisha katika nchi mbalimbali duniani na wamepata maendeleo katika sekta mbalimbali:-
(a) Je, ni Watanzania wangapi wanajulikana rasmi kuwa wako ughaibuni, wanachangiaje maendeleo ya nchi yao na kwa kiasi gani?
(b) Je, ni Watanzania wangapi wakiwemo kutoka Tanzania Zanzibar ambao hawakufuata taratibu walipoondoka lakini Balozi zetu zina taarifa ya uwepo wao kwenye nchi hizo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE, USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI, KIKANDA NA KIMATAIFA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hafidh Ali Tahir, Mbunge wa Dimani, lenye vipengele (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania waishio nje ya nchi wanakadiriwa kuwa zaidi ya milioni moja kote duniani. Makadirio hayo yanatokana na takwimu tunazokusanya kupitia Balozi zetu ambazo zinashirikiana kwa karibu na Jumuiya za Watanzania katika maeneo yao ya uwakilishi. Hata hivyo, idadi hiyo inaweza kuwa ndogo kwa kuwa bado hatujaweza kukamilisha uwezo wa kuwafikia Watanzania wote ughaibuni kwa ajili ya kuwatambua na kuwahesabu. Mipango ya kutekeleza azma hiyo inaendelea na hivyo tunatarajia siku za usoni tutaweza kuwa na takwimu bora kabisa za wenzetu walioko ughaibuni.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inaendelea na juhudi za kuhamasisha Watanzania waishio ughaibuni kuona umuhimu wa kuchangia maendeleo ya nchi yao. Tumeweza kupata mafanikio kadhaa yanayopatikana kutoka kwenye mwitikio wa baadhi ya Watanzania hao. Taasisi zetu za fedha hazijaweza kukusanya takwimu zote za fedha zinazotoka ughaibuni kwa Watanzania kama kama remittance, kwasababu ya changamoto mbalimbali ikiwemo gharama kubwa za utumaji wa fedha nyumbani. Changamoto hizo zinawalazimisha kutumia njia mbadala kama hawala. Hata hivyo, imeweza kuthibitika kuwa kaya nyingi zinapata misaada ya fedha kutoka kwa ndugu zao na jamaa zao waishio ughaibuni. Mathalani, asilimia 12 ya kaya za Zanzibar zinaishi kwa kusaidiwa na ndugu zao hao.
Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania hao wameendelea kuratibu na kuleta misaada hapa nchini hususan katika sekta ya afya na elimu. Mifano michache, mwezi Februari, 2015 Watanzania waishio Marekani walifanikisha upatikanaji wa mashine ya kupimia saratani ya matiti yenye thamani ya dola za Marekani 200,000 iliyotolewa katika Hospitali Kuu ya Jeshi ya Lugalo.
Aidha, mwezi Julai 2015 Watanzania wengine kutoka huko huko Marekani, waliratibu ziara ya kitabibu ya Madaktari wa Marekani kuja kutoa huduma za tiba bure za magonjwa kama ya moyo, meno na saratani ya kizazi na matiti katika hospitali ya Mwananyamala, Dar es Salaam pamoja na Hospitali ya Mnazi Mmoja kule Zanzibar. Vilevile walitoa msaada wa vifaa tiba vyenye thamani ya dola za Marekani 300,000 katika hospitali hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, siyo rahisi kubaini idadi ya Watanzania walioondoka bila taratibu zilizopo hapa nchini. Watu wanaondoka kwa sababu tofauti na wakifika huko siyo rahisi kufahamu yanayotokea. Hata hivyo wale wanaojiandikisha katika Balozi zetu, mara nyingi taarifa za muhimu zaidi ni kuthibitisha Utanzania wao. Madhumuni yetu ni kuwatambua kama Watanzania wenzetu, kuwapa huduma wanapohitaji na kuwahamasisha kusaidia ndugu zao walikotoka na kuchangia maendeleo ya nchi.
Aidha, kupitia Balozi zetu, tumekuwa tukiwasisitiza Watanzania waishio ughaibuni kuheshimu sheria na taratibu za nchi wenyeji ili kuendelea kulinda heshima na sifa nzuri ya nchi yetu.
MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza:-
Sudan Kusini imekubaliwa kujiunga na Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Je, ni lini Serikali itafungua Ubalozi katika nchi hiyo ili kutengeneza mazingira ya kunufaika na fursa zilizoko katika nchi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI (K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Taifa la Sudan Kusini lilianzishwa mwezi Julai, 2011 baada ya kura za maoni za wananchi wa nchi hiyo kuamua kujitenga kutoka nchi ya Sudan na kuunda Taifa jipya ya Sudan Kusini. Aidha, mwezi Aprili, 2016 nchi ya Sudan Kusini ilijiunga na Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kwa sasa Tanzania haina Ofisi za Ubalozi nchini Sudan Kusini. Katika kipindi hiki ambacho Serikali haijafungua Ubalozi nchini Sudan Kusini, shughuli za Kibalozi kwa nchi hiyo zinafanywa na Ubalozi wetu, Nairobi nchini Kenya.
Malengo ya Wizara kwa mwaka 2016/2017 ni pamoja na kuongeza uwakilishi wetu nje ya nchi kwa kufungua Balozi mpya na Ofisi za Kikonseli hususan katika nchi ambazo Taifa linanufaika zaidi na fursa za kiuchumi kama vile soko la bidhaa zetu, biashara, uwekezaji, ajira pamoja na utalii.
Aidha, naomba ieleweke kuwa licha ya kuwepo kwa fursa hizo, maamuzi ya kufungua Ofisi za Ubalozi nchini Sudan Kusini pamoja na uendeshaji wa shughuli za Ofisi za Ubalozi zitakazofunguliwa zitategemea na Serikali itakapokuwa tayari Kibajeti.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA aliuliza:-
Ofisi nyingi za Balozi zetu katika nchi mbalimbali zimekodishwa. Aidha, ofisi nyingine ujenzi haujakamilika au hazijafanyiwa ukarabati kwa muda mrefu sasa na ofisi nyingine zina madeni makubwa.
(a) Je, ni lini ujenzi wa baadhi ya ofisi za Ubalozi zitakamilika ikiwemo ya Msumbiji?
(b) Je, Serikali ina mkakati gani wa kukarabati ofisi chache za Ubalozi zilizopo pamoja na kununua samani mpya?
(c) Je, kwa nini Serikali isilipe madeni ya Balozi zetu kwa wakati ili kuepusha aibu kwa Taifa?
NAIBU WAZIRI KILIMO, MIFUGO NA UVUVI (K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, Mbunge, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa ofisi na makazi ya Balozi zetu umekuwa ukitekelezwa kwa awamu kwa kuzingatia upatikanaji wa fedha za bajeti ya maendeleo. Mwaka wa fedha 2016/2017, Wizara ilipanga kutekeleza miradi ya ujenzi katika Balozi zake ikiwemo Maputo, Nairobi na Stockholm na uboreshaji wa mifumo ya mawasiliano kati ya Balozi na Makao Makuu wa Wizara. Mradi wa Maputo umepangiwa shilingi 1,316,435,000. Tunategemea utekelezaji wa mradi huu ufanyike pale Wizara itakapopokea fedha kutoka Hazina.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua kuwa fedha za bajeti ya maendeleo hazikidhi mahitaji, Wizara inaendelea kushirikisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kama vile Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na Taasisi ya Miradi ya Maendeleo ya Miundombinu katika ujenzi wa majengo ya ofisi na vitega uchumi katika Balozi zetu. Wizara inaamini uamuzi wa kuishirikisha mifuko hiyo itaongeza kasi ya ujenzi wa majengo ya ofisi katika Balozi zetu.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati wa Wizara uliopo hizi sasa katika kukarabati majengo ya ofisi yaliyopo kwenye Balozi zetu ni kuendelea kuiomba Serikali kutenga fedha za bajeti ya maendeleo; pili, kuelekeza Balozi zetu kutumia utaratibu wa karadha (mortgage finance) ili kuwezesha Balozi kupata fedha za ukarabati, kununua na kujenga majengo ya ofisi na vitega uchumi; na tatu, kuishirikisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii iliyopo nchini kutekeleza miradi ya Wizara Balozini kwa Wizara kuingia makubaliano na vyombo hivyo. Aidha, Wizara itaendelea na utaratibu wa kununua kwa awamu samani mpya za ofisi kwa kuzingatia upatikanaji wa fedha.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika nyakati tofauti imekuwa ikitoa fedha kwa ajili ya kulipa madeni ya Balozi zake nje. Serikali ilitoa kiasi cha shilingi 7,315,720,301.84 kulipa madeni ya Wizara yaliyohakikiwa na Wakaguzi wa Hesabu. Hadi kufikia tarehe 30 Juni, 2016 deni lililobaki ni shilingi 15,540,603,526. Madeni haya yameanza kukaguliwa na Hazina, hivyo ni matarajio yetu kuwa baada ya kukamilika kwa ukaguzi huo, Hazina itatoa fedha za kulipa madeni hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, katika mwaka wa fedha 2016/2017 Hazina imetoa mwongozo unaoelekeza kuandaa mpango wa bajeti ambao unaelekeza madeni yote ya Wizara, Wakala na Taasisi za Serikali kulipwa moja kwa moja na Hazina.
MHE. HAMAD SALIM MAALIM aliuliza:-
Kwa kuwa Mabadiliko ya Kumi (10) ya Katiba ya Zanzibar yanaitambua Zanzibar kuwa ni nchi.
Je, ni lini Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itairuhusu Zanzibar kuwa na uwakilishi rasmi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki?
WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ruhusa yako, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hamad Salim Maalim, Mbunge wa Kojani kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Ibara ya 2(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 pamoja na mabadiliko yake imebainisha kuwa eneo la Jamhuri ya Muungano ni eneo lote la Tanzania Bara na eneo lote la Tanzania Zanzibar na ni pamoja na sehemu yake ya bahari ambayo Tanzania inapakana nayo. Aidha, Jedwali la Kwanza kwenye Katiba hiyo limebainisha kuwa masuala ya mambo ya nje ni masula ya Muungano.
Kwa muktadha huo, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ndiyo mwanachama katika Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa maslahi yote ya Zanzibar katika Jumuiya ya Afrika Mashariki yanazingatiwa ipasavyo. Kabla ya kushiriki katika Mikutano ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kumekuwa na vikao vya maandalizi ambavyo hushirikisha pande zote mbili za Muungano ili kuandaa msimamo wa pamoja wenye kuzingatia maslahi ya pande zote mbili.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hushiriki katika ngazi zote za Mikutano ya Wakuu wa Nchi Wanachama, Baraza la Mawaziri la Jumuiya na Mabaraza ya Mawaziri ya Kisekta yafuatayo:-
(a) Baraza la Mawaziri la Kisekta la Uwekezaji, Fedha, Viwanda na Biashara;
(b) Baraza la Mawaziri la Kisekta la Afya;
(c) Baraza la Mawaziri wa Kisekta la Uchumi, Mawasiliano na Hali ya Hewa;
(d) Baraza la Mawaziri la Kisekta la Elimu, Sayansi na Teknolojia, Utamaduni na Michezo;
(e) Baraza la Mawaziri la Kisekta la Jinsia, Vijana, Watoto na Maendeleo ya Jamii;
(f) Baraza la Mawaziri la Kisekta la Nishati;
(g) Baraza la Mawaziri la Kisekta la Kilimo na Usalama wa Chakula; na
(h) Baraza la Mawaziri la Kisekta la Amani na Usalama.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mikutano hiyo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hushiriki katika ngazi za wataalam, Makatibu Wakuu na Mawaziri. Aidha, kati ya Wabunge tisa wa Bunge la Afrika Mashariki, Wabunge watatu wanatokea Zanzibar. Ahsante.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA (K.n.y. MHE. ALLY SALEH ALLY) aliuliza:-
Utaratibu wa kutunga Sheria wa Jumuiya ya Afrika Mashariki unahusisha maslahi ya nchi zote tano wanachama wa EAC kuelekea fungamano la kiuchumi na siasa.
(i) Je, hadi sasa ni sheria ngapi zimeshatungwa na kwa mgao wa maeneo yapi?
(ii) Je, hatua gani huchukuliwa unapotokea mgongano baina ya sheria ya ndani na ile ya Jumuiya?
(iii) Je, kuna utaratibu gani wa kutoa elimu ya umma kuhusu Sheria za Jumuiya?
WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ruhusa yako napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Saleh Ally, Mbunge wa Malindi, lenye vipengele (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu kuanzishwa kwa Bunge la Afrika Mashariki mwezi Novemba, 2001 hadi hivi sasa jumla ya sheria 78 zimeshatungwa. Kati ya hizo, sheria 20 zimesharidhiwa na Wakuu wa Nchi na Wanachama na nyingine zipo katika hatua mbalimbali za kusainiwa na kuridhiwa. Sheria zilizotungwa zimelenga katika kuimarisha biashara, kukuza uchumi baina ya nchi wanachama na Jumuiya ya Afrika Mashariki na kuwezesha taasisi na vyombo vya jumuiya kutekeleza majukumu yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya sheria hizi ni Sheria ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Usimamizi wa Forodha ya mwaka 2004, Sheria ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Kusimamia Uondoaji wa Vikwazo Visivyo vya Kiushuru ya mwaka 2017, Sheria ya Udhibiti wa Uzito wa Magari ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya mwaka 2013 na Sheria ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Uanzishwaji wa Vituo vya Utoaji Huduma kwa Pamoja Mipakani ya mwaka 2013.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Ibara ya 8(4) ya Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Sheria za Jumuiya zina nguvu kuliko za nchi wanachama. Hivyo basi, ikitokea mkingano baina ya Sheria za Jumuiya na zile za nchi wanachama, nchi wanachama hazina budi kuzifanyia marekebisho sheria hizo ili ziendane na Sheria za Jumuiya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Tanzania sheria mbalimbali za kodi zilifanyiwa marekebisho, ili ziendane na utekelezaji wa Sheria ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Usimamizi wa Forodha ya mwaka 2004 ambayo ndiyo sheria inayotumika kwa nchi zote wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, ili kuendana na makubaliano yaliyofikiwa katika Itifaki ya Soko la Pamoja la Jumuiya ya Afrika Mashariki, Serikali ya Tanzania imefanya marekebisho katika Sheria ya Masoko na Mitaji na Dhamana, Sura ya 79; Sheria ya Kubadilisha Fedha za Kigeni Sura ya 271; pamoja na Kutunga Sheria ya Kuratibu Ajira za Wageni Nchini Na. 1 ya mwaka 2015. Vilevile Serikali inaendelea na mapitio ya sheria mbalimbali ili kuainisha na zile za Jumuiya ya Afrika Mashariki.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara imekuwa na utaratibu wa kutoa elimu kwa umma lengo likiwa ni kuwawezesha wananchi kunufaika na fursa zinazotokana na mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, ikiwa ni pamoja na kuwapatia uelewa wa sheria zilizopitishwa na Bunge la Afrika ya Mashariki. Elimu hii hutolewa kupitia vyombo vya habari, tovuti ya Wizara, makongamano, vikao vya wadau, warsha, blog za kijamii na mitandao ya kijamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mathalani mwezi Julai Wizara iliratibu kampeni ya kuhamasisha vijana wa Kitanzania kutumia fursa za biashara zitokanazo na mtangamano wa Afrika Mashariki iliyojulikana kama Chungulia Fursa, iliyolenga kuwahamasisha vijana kufanya biashara za kuvuka mipaka ya Tanzania iliyofanyika katika mikoa ya Dodoma, Mwanza, Manyara na Arusha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Wizara ilitoa elimu ya faida na fursa za mtangamano kwa wanafunzi wa Vyuo vya Elimu ya Juu na Wajumbe wa Baraza la Vijana wa Zanzibar. Mafunzo hayo yalifanyika mwezi Machi, 2018 na yaliongozwa na kaulimbiu iliyosema Vijana na Jumuiya ya Afrika Mashariki. Ahsante. (Makofi)
MHE. JUMA S. NKAMIA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya ya Chemba?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juma Selemani Nkamia, Mbunge wa Chemba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Wilaya ya Chemba ni moja ya wilaya zinazokabiliwa na ukosefu wa huduma za mahakama ya wilaya. Kwa nyakati tofauti, nimekuwa nikilieleza Bunge lako Tukufu kwamba Mahakama ya Tanzania inakabiliwa na changamoto kubwa ya miundombinu ya kutolea huduma za kimahakama katika ngazi zote. Kati ya Wilaya 139 zilizopo nchini, ni Wilaya 34 tu zenye majengo ya mahakama.

Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Mahakama ya Tanzania imekuwa ama ikiazima majengo kwenye Ofisi za Halmashauri, Mkuu wa Wilaya au kupanga pale yanapokosekana kabisa majengo hayo, ili kuendelea kutoa huduma za kimahakama. Katika maeneo ambayo Mahakama ya Tanzania haina kabisa majengo huduma hiyo imekuwa ikiendelea kutolewa na mahakama ya wilaya nyingine iliyopo jirani kwa utaratibu wa kuitembelea kwa ratiba walizojipangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na uhaba wa miundombinu takribani wilaya mpya 29, ikiwemo ya Chemba mkoani Dodoma ambayo imetokana na Wilaya ya Kondoa bado haina Mahakama ya Wilaya. Hivyo, Wilaya hiyo kwa sasa inaendelea kuhudumiwa na Mahakama ya Wilaya ya Kondoa. Hata hivyo, katika mwaka wa fedha 2019/2020, mpango wa Mahakama ya Tanzania ni kuhakikisha kuwa jengo la Mahakama ya Wilaya ya Chemba linajengwa kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa lengo la Serikali ni kusogeza huduma za mahakama karibu na wananchi, naomba kumthibitishia Mbunge kwamba tutafanya kila jitihada ya kuendeleza ujenzi wa mahakama kila wilaya hapa nchini inapokuwa inawezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI aliuliza:-

Ibara ya 13(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema kwamba “Watu wote ni sawa mbele ya sheria na wanayo haki bila ya ubaguzi wowote, kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria”; lakini kumekuwa na kiwango cha juu cha matukio na kesi zinazohusu kuvunjwa kwa haki za kiraia kwa kufanywa na vyombo vya dola:-

(a) Je, kwa kipindi cha mwaka 2010 – 2015 ni kesi ngapi zimefunguliwa Mahakamani kuhusu madhara yanayofanywa na vyombo vya dola dhidi ya raia, na huchukua muda gani hadi kutolewa hukumu?

(b) Je, kesi hizo zimekuwa zikigharamiwa kwa kiasi gani kutoka Mfuko wa Fedha za Umma tangu mwaka 2010 – 2015?

(c) Je, Serikali inafanya jitihada gani kuhakikisha wananchi wake pamoja na vyombo vya usalama wanapata elimu ya uraia?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Immaculate Sware Semesi, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi cha mwaka 2010 – 2015 Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora haijafungua kesi yoyote Mahakamani kuhusu madhara yanayofanywa na vyombo vya dola dhidi ya raia. Tume imekuwa ikipokea malalamiko ya uvunjwaji wa haki za binadamu dhidi ya vyombo vya dola na kuyashughulikia kwa kufanya uchunguzi wa kawaida, usikilizwaji hadharani na kufanya usuluhishi na upatanishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbinu hizi zimeonekana kuwa na mafanikio makubwa katika kuwapatia wananchi haki yao wanayostahili, hivyo kutokuwa na umuhimu wa kufungua mashauri Mahakamani. Ikumbukwe kuwa ufunguaji wa mashauri Mahakamani ni hatua ya mwisho iwapo njia nyingine zote zimeshindikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimeeleza, kwa kuwa Tume haijawahi kufungua kesi yoyote ya haki za binadamu katika Mahakama zetu kwa kipindi cha mwaka 2010 – 2015, hivyo basi, hakuna gharama zozote za ufunguaji wa mashauri Mahakamani zinazohusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi cha mwaka 2010 – 2015, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imefanya jitihada mbalimbali ili kuhakikisha wananchi pamoja na vyombo vya usalama wanapata elimu ya uraia. Jitihada hizo ni pamoja na kuelimisha Umma kupitia vyombo mbalimbali vya habari, mikutano, maadhimisho, machapisho na warsha mbalimbali katika kipindi cha 2010 hadi 2015.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya vipeperushi na vijitabu 40,638, makala 18,300 za Mpango Kazi wa Kitaifa wa Haki za Binadamu, majarida yaliyowekwa kwenye tovuti ya Tume ni matano, vipindi vya redio na televisheni ni 115 na kufanya mikutano na wananchi kuhusu haki za binadamu na hasa katika kumiliki ardhi kwenye mikoa 21 ya Tanzania Bara na Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata katika kipindi cha kuanzia 2015 hadi sasa, jitihada hizi zimeendelea kufanywa na Wizara yangu Waheshimiwa Wabunge na Bunge hili kwa ujumla kwamba haki zitakuwa zinatendeka na kwamba tunaendelea kubuni mbinu na mikakati mbalimbali itakayowezesha kuendelea kuwafikia wananchi wengi iwezekanavyo.
MHE. HASSAN E. MASALA aliuliza:-

Je, nini mpango wa Serikali juu ya kuboresha jengo la Mahakama Wilayani Nachingwea?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Elias Masala, Mbunge wa Nachingwea, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mahakama ya Tanzania haipo katika mpango wa maboresho ya majengo ya Mahakama nchini, ambapo pamoja na mambo mengine imekusudia kusogeza haduma ya Mahakama karibu na wananchi. Ili kufikia lengo hilo, Mahakama imeendelea kutatua changamoto kubwa ya uhaba na uchakavu wa majengo kwa kuendelea na kukarabati majengo nchi nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mahakama ya Tanzania inafahamu tatizo la uchakavu wa majengo mengi ya Mahakama nchini, ikiwemo jengo la Mahakama ya Wilaya Nachingwea. Katika kukabiliana na changamoto hii, Mahakama imeweka kipaumbele katika kuboresha na kujenga majengo ya Mahakama nchini kulingana na mpango mkakati wa miaka mitano ambao umeendelea kutekelezwa kwa awamu kutegemea na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumfahamisha Mheshimiwa Mbunge wa Nachingwea kuwa kutokana na uhitaji mkubwa wa rasilimali na rasilimali chache zilizopo, katika mpango mkakati wa miaka mitano, Mahakama iliamua kujipanga upya na kuweka vipaumbele ili kuhakikisha tunaondokana na changamoto hii. Aidha, tayari tathmini ya jengo la Mahakama Nachingwea imeshafanyika. Kimsingi jengo hili linahitaji kujengwa upya na siyo kufanyiwa maboresho. Aidha, baada ya tathmini hiyo kufanyika ujenzi wa jengo hilo umewekwa kwenye mpango wetu wa ujenzi wa Mahakama wa mwaka 2020/2021kutegemeana na upatikanaji wa fedha.
MHE. DKT. SULEIMAN ALLY YUSSUF aliuliza:-

Ibara ya 130 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano inataja kazi za Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, moja ya kazi zake ni kufanya uchunguzi juu ya mambo yanayohusu uvunjaji wa Haki za za Binadamu na ukiukwaji wa msingi ya utwala bora.

(a) Je, kwa nini ripoti za tume hiyo haziwekwi wazi kwa Umma?

(b) Je, Serikali haioni kuwa umefika wakati wa kujenga utamaduni wa ripoti hizo kujadiliwa Bungeni?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA (K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Suleiman Ally Yussuf Mbunge wa Mgogoni lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijalijibu Mheshimiwa Ally Yussuf, amesema wadhurumiwa wote kwa hiyo inawezekana hata yeye kuna ambao amewadhurumu lakini naomba nijibu swali kama alivyouliza maana hakuuliza hivyo huko nyuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kweli kwamba Ibara ya 130 ya katiba ya Jamhuri ya Muugano ikiosomwa kwa pamoja na sheria ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora Na. 7 ya 2001) inaipa Tume mamlaka ya kufanya uchunguzi wa mambo yote yanayohusu uvunjwaji wa haki za binadamu, kifungu cha 28(1)(a) mpaka (f) cha sheria hiyo (Na. 7 ya 2001) kinafafanua kuwa, tume baada ya kufanya uchunguzi na kuthibitisha kuwepo kwa uvunjifu wa haki za binadamu itawaslisha taarifa na mapendekezo yake kwenye mamlaka kusika kwa ajili ya utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha 33 (1) (a) –(c) cha Sheria Na. 7 ya 2001 kinaitaka Tume kuwasilisha taarifa yake ya mwaka katika Bunge la Jamhuri ya Muungano na Baraza la Mawaziri kupitia wanaoshughulikia masuala ya haki za binadamu kwa Tanzania Bara na Zanzabar, hata hivyo, Tume imekuwa ikitimiza jukuu hilo kwa mujibu wa sheria. Aidha, hakuna sheria yoyote inayokataza taarifa za Tume kujadiliwa Bungeni endapo Mbunge ataona kama kuna jambo la kuibua kutoka kwenye taarifa iliyowasilishwa.
MHE. ALLY SALEH ALLY (K.n.y. MHE. DKT. SULEIMANI ALLY YUSSUF) aliuliza:-

Kutokana na maendeleo ya kiuchumi na kijamii kumekuwa na ongezeko kubwa la makosa katika jamii jambo ambalo linasababisha mfumo wa utoaji haki pamoja na Mahakama kuelemewa.

(a) Je, kila Jaji au Hakimu anapangiwa kesi ngapi kwa mwaka ili kupunguza mlundikano wa kesi?

(b) Je, ni mambo gani kimsingi yanayosababisha mashauri kuchukua muda mrefu?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Suleimani Ally Yussuf, Mbunge wa Mgogoni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mahakama ya Tanzania imejiwekea utaratibu ili kuhakikisha mashauri yote yanayofunguliwa Mahakamani yanamalizika kwa wakati. Utaratibu huu ni pamoja na kujiwekea malengo ya idadi ya mashauri yatakayoamuliwa na Jaji na Hakimu kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, malengo ni kuhakikisha tunapunguza mlundikano wa mashauri Mahakamani ambapo kwa mwaka kila Jaji anatakiwa kumaliza mashauri 220; Mahakimu katika Mahakama za Hakimu Mkazi wa Wilaya kumaliza mashauri 250 na katika Mahakama za Mwanzo 260.

Mheshimiwa Spika, pia Mahakama imejiwekea ukomo wa muda wa mashauri kukaa Mahakamani. Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu ni miaka mwili; Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya mwaka mmoja na Mahakama za Mwanzo ni miezi sita. Mikakati hii imesaidia kupunguza mlundikano wa mashauri kwa kiasi kikubwa hususan kwa Mahakama za Mwanzo ambapo kwa sasa mlundikano wa mashauri ni asilimia sifuri.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada hizo bado Mahakama zetu zimekuwa zinakabiliwa na changamoto za mlundikano wa mashauri na baadhi ya mashauri kuchukua muda mrefu zaidi. Changamoto hizi zimetokana na idadi ndogo ya Majaji na Mahakimu ikilinganishwa na idadi ya mashauri yanayofunguliwa katika Mahakama zote nchini. Vilevile upelelezi katika Mahakama na mashauri kuchukua muda mrefu na mashahidi kutotoa ushahidi wao kwa wakati katika baadhi ya mashauri yanayofunguliwa katika Mahakama zetu nchini ni miongonzi mwa sababu na baadhi ya mashauri kuchukua muda mrefu Mahakamani. Hata hivyo ninamshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli kwa kuteuwa Majaji 11 wa Mahakama ya Rufaa na Majaji 39 wa Mahakama Kuu katika Awamu ya Tano, ahsante.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA aliuliza:-

Kwa mujibu wa GN. No. 222 na 223 ya mwaka 1972 pamoja na marekebisho yake ya mwaka 2002, Wazee wa Mabaraza ya Mahakama wanateuliwa na vikao vya Chama cha Mapinduzi (CCM) na Kamati za Maadili za Mahakimu zipo chini ya Uenyekiti wa Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya:-

Je, ni lini Mahakama itaacha kuingiliwa na siasa?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, Mahakama ya Tanzania ni moja ya mihimili mitatu ya dola ambayo kwa mujibu wa Ibara ya 4 na 107(B) ya Katiba, Mahakama ni Mhimili huru na hauingiliwi na chombo chochote katika utekelezaji wa majukumu yake ya utoaji haki.

Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji wa majukumu yake, Mahakama imekuwa ikiwatumia Wazee wa Baraza katika ngazi ya Mahakama za Mwanzo na Mahakama Kuu ambao hupatikana kwa mujibu wa Kanuni za Wazee wa Baraza katika Mahakama za Mwanzo
G.N. No. 222/223 za Mwaka 1972, ambao huteuliwa kulingana na sifa za umri na uzoefu walionao katika masuala mbalimbali hasa ya kijamii katika eneo husika.

Aidha, Wazee wa Baraza huwa na jukumu moja la kuishauri Mahakama na ushauri wao hauifungi Mahakama katika kutoa uamuzi inaouona unafaa. Hata hivyo, Wizara yangu imeanza mchakato wa kuboresha sekta ndogo ya mfumo wa haki, jinsia nchini ambao pamoja na mambo mengine inapitia Sheria za Kamati zote ambazo zimetungwa miaka mingi iliyopita ili ziendane na wakati.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Kamati za Maadili za Mikoa na Wilaya, Sheria ya Usimamizi wa Mahakama ya Mwaka 2011, imebainisha majukumu ya Kamati hizi kwa mujibu wa vifungu vya 50 na 51. Lengo la Kamati hii ni kushughulikia malalamiko ya ukiukwaji wa maadili ya utendaji wa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo na Mahakimu Wakazi katika kutimiza shabaha na kulingana na kusawazishana (checks and balances) katika utendaji wa Mihimili ya dola. Kamati hizi haziingilii uhuru wa Mahakama ambayo inatekeleza majukumu yake ya utoaji haki ambao unatajwa kwa mujibu wa Ibara ya 107 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, ninapenda kulifahamisha Bunge lako Tukufu kuwa, nchi yetu itaendelea kuheshimu misingi ya mgao wa madaraka baina ya mihimili ya Dola na kamwe Mahakama haiwezi na haiingiliwi na chombo kingine cha Dola katika utekelezaji wa majukumu yake.
MHE. OMARI M. KIGUA aliuliza:-

Serikali imekuwa na utaratibu wa kutenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa Mahakama za Mwanzo:-

Je, ni lini Serikali itafanya ukarabati wa Mahakama za Kata za Kimbe, Kwekivu na Kata ya Mswaki ambazo zimechakaa sana?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Omari Mohamed Kigua, Mbunge wa Kilindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, miongoni mwa changamoto zinazoikabili Mahakama ya Tanzania ni uhaba na uchakavu wa miundombinu. Kwa sasa, kuna jumla ya Mahakama za mwanzo 960 katika mikoa yote nchini. Idadi kubwa ya majengo ya Mahakama hizi ni chakavu na ni finyu kuweza kutoa huduma kwa mahitaji ya sasa hususan kukidhi ongezeko la mashauri. Hivyo, majengo mengi yanayohitaji kujengwa upya, ngazi ya Mahakama ya Mwanzo ni muhimu sana kwa kuwa inabeba takriban asilimia 70 ya mashauri yote yanayopelekwa Mahakamani.

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na changamoto hii, Mahakama imejiwekea mpango wake wa ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya Mahakama kwa awamu.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kilindi ina Mahakama za Mwanzo tatu zinazofanya kazi ambazo ni Songe, Mswaki na Kwediboma. Majengo ya Mahakama zote hizi ni ya zamani kiasi cha kuhitajika kujengwa upya, siyo kukarabatiwa. Aidha, Mahakama tatu za Kimbe, Kwekivu na Mswaki alizouliza Mheshimiwa Mbunge, majengo yake hayafanyi kazi kabisa, yamefungwa kutokana na uchakavu.

Mheshimiwa Spika, wananchi waliokuwa wanapata huduma katika Mahakama za Mwanzo za Kwekivu na Kimbe wanalazimika kufuata huduma Mahakama ya Mwanzo Songe ambako ni mbali. Mahakama ya Mwanzo Mswaki inatumia jengo la Kijiji kwa shughuli za Mahakama. Kutokana na hali hiyo, Mpango wa Serikali ni kujenga upya kabisa Mahakama hizi na siyo kufanya ukarabati.

Mheshimiwa Spika, pamoja na ukweli kwamba Mahakama zote zilizotajwa na Mheshimiwa Mbunge ni chakavu sana, lakini bado mahitaji ya Mahakama kwa nchi nzima ni makubwa na hivyo, tutaendelea na kazi ya ujenzi na ukarabati wa Mahakama za Mwanzo na Mahakama za ngazi nyingine kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, kupitia Mpango huo, napenda kumthibitishia Mheshimiwa Mbunge kuwa Mahakama ya Mwanzo Kwekivu na Kimbe zitajengwa katika mwaka wa fedha 2020/2021.

Mheshimiwa Spika, mwisho, ninawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa kuendelea kushirikiana na Serikali na Mahakama na kuona umuhimu wa kuidhinisha fedha zinazohitajika kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa Mahakama zetu nchini. Ninaomba tuendelee kuona umuhimu wa mhimili huu katika utoaji wa haki nchini. Ahsante. (Makofi)
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-

Tarafa ya Wampembe ina Kata za Kala, Wampe mbe, Kizumbi na Ninde na ambazo zote ziko umbali wa zaidi ya km 80-150 kutoka Makao Makuu au mahali ambapo huduma za Mahakama zinaweza kupatikana:-

Je, ni lini Serikali itajenga walau Mahakama ya Mwanzo katika moja ya Kata hizo hususani Kata ya Wampembe ili kusogeza huduma hiyo kwa Wananchi?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Napenda kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata Nkasi Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha kuwa na huduma za haki zinazozingatia karibu na wananchi Mahakama ya Tanzania imeazimia kuwa na Mahakama Kuu na Mahakama ya Mahakimu Mkazi kwa kila Mkoa, Mahakama ya Wilaya kwa Wilaya na katika ngazi za tarafa kuwa na walau Mahakama moja ya mwanzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tarafa ya Wampembe aliyouliza Mheshimiwa Mbunge tayari Mahakama ya Mwanzo ipo na inatumia jengo la Ofisi ya Tarafa. Ni kweli kwa muda mrefu wananchi wa Tarafa hii wamekuwa wamekuwa wakifuata huduma za Mahakama umbali mrefu. Lakini kuanzia tarehe 23 Aprili, 2018 Mahakama ya Mwanzo ya Wampembe ilifunguliwa na mpaka sasa inaendelea kutoa huduma kwa wananchi kwa eneo hilo na maeneo ya jirani. Pamoja na jitihada hizo Mahakama inaendelea na kuratibu na kupata eneo katika Tarafa hiyo ili uweze kujenga jengo la Mahakama ya Mwanzo Wampembe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka huu wa fedha Wizara yangu, kwa kushirikiana na Mahakama tumepanga kujenga jengo la Mahakama ya Wilaya ya Nkasi, ambalo pia litatumika na Mahakama ya Mwanzo ya Yanamanyere. Ujenzi huu unatarajiwa kuanza mwezi Mei mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kutoa shukurani za dhati kwa Mheshimiwa Mbunge wa Halmashauri ya Wilaya kwa kujitahidi na kuuliza swali hilo na jitihada zote zinazofanyika kuwezesha upatikanaji wa jengo la kuendesha Mahakama ya Mwanzo Wampembe ambalo linatuwezesha kutoa huduma kwa wananchi wa eneo hilo na maeneo jirani wakati tukiendelea na taratibu za kupata jengo la Mahakama ahsante.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA aliuliza:-

Je, Serikali haioni ni wakati muafaka wakuleta Bungeni marekebisho ya Sheria ili kupunguza kiwango cha ushahidi kwenye kesi za ubakaji na hasa ubakaji wa Watoto?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ushahidi katika kesi za daawa ya jinai hususan kwa watoto wenye umri chini ya miaka 18 yanaadhibiwa kwa mujibu wa Kifungu cha 130(1) na 13(2)(e) cha Kanuni za Adhabu, Sura ya 20. Makosa haya kwa mujibu wa Sheria ya Ushahidi yanahitaji kuthibitishwa pasipo kuacha shaka yoyote ili mtuhumiwa atiwe hatiani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kiwango cha kuthibitisha mashauri ya jinai pasipo kuacha shaka yoyote, kiwango cha ushahidi kitategemea mazingira ya kosa husika na namna yalivyotendeka na mashahidi walioshuhudia kutokea kwa tukio hilo. Sheria haijatoa masharti ya idadi ya mashahidi wanaotakiwa kutoa ushahidi. Hivyo, kila kesi huangaliwa kwa kuzingatia mazingira yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo na kwa lengo la kumlinda mtoto aliyeathirika na tukio la ubakaji, mwaka 2016 Bunge lako Tukufu lilifanya marekebisho katika Kifungu cha 127 cha Sheria ya Ushahidi kwa kuondoa masharti ya kumhoji mtoto ili kupima ufahamu wake na badala yake kuweka masharti ya Mahakama kujiridhisha kuwa mtoto ana uwezo wa kusema ukweli pekee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa Serikali inaendelea na itaendelea kufanya maboresho ya Mfumo wa Haki Jinai ili kuondoa vikwazo vyote vinavyokwamisha usikilizwaji, siyo tu wa mashauri ya namna hii, bali mashauri yote yanayohusu makundi ya watu katika jamii yetu ili kulinda utu wao ikiwemo watoto, wanawake, wazee na watu wenye ulemavu wanaoathirika na vitendo vya ukatili ikiwa ni pamoja na ubakaji. Ahsante.
MHE. FATMA H. TOUFIQ aliuliza: -

Serikali imeanza kampeni ya kusajili watoto chini ya miaka mitano ili kupata vyeti vya kuzaliwa, lakini bado Watanzania wenye umri zaidi ya miaka mitano na kuendelea hawana vyeti vya kuzaliwa:-

Je, Serikali imejipangaje kutoa vyeti vya kuzaliwa kwa Watanzania wenye umri zaidi ya miaka mitano na kuendelea?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) imekuwa ikitekeleza Mkakati wa Usajili wa Matukio Muhimu ya Binadamu na Takwimu ili kuboresha hali ya usajili nchini. Mkakati huo una mipango mbalimbali ambayo imekuwa ikitekelezwa na Serikali ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa Watanzania wote wenye umri wa zaidi ya miaka mitano wanasajiliwa na kupatiwa vyeti vya kuzaliwa.

Mheshimiwa Spika, mojawapo ya mipango hiyo ni kusajili na kutoa vyeti vya kuzaliwa kwa watoto wote waliopo kwenye mfumo rasmi wa elimu na kufanya kampeni za uhamasishaji kwa kuwafuata wananchi katika maeneo yao ya makazi.

Mheshimiwa Spika, mkakati huu wa kusajili watoto waliopo katika mfumo rasmi wa elimu umefanikiwa kusajili jumla ya watoto 325,583 wenye umri wa miaka mitano hadi 17 katika jumla ya wilaya kumi na tisa ambazo ni Njombe, Ludewa, Makete, Wanging’ombe, Ilala, Kinondoni, Kigamboni, Temeke, Iringa, Kilindi, Musoma, Bariadi, Tarime, Singida, Songea, Bunda, Maswa, Kahama na Manyoni. Wakala utaendelea na utaratibu huu ili kuhakikisha wilaya zote nchini kulingana na mpango uliopo.

Vilevile wakala umeendelea kuwafikia wananchi wasio katika mfumo rasmi wa elimu kupitia kampeni za maadhimisho mbalimbali ya kitaifa na hasa kama vile maonesho ya Saba Saba na Nane Nane yanayofanyika nchini kwa kutoa elimu ya muhimu wa usajili wa matukio muhimu ya binadamu.

Mheshimiwa Spika, Wakala wa Usajilli, Ufilisi na Udhamini (RITA) unatarajia kuanzisha huduma ya usajili kwa njia ya mtandao ili kuwafikia wananchi wengi kwa urahisi ambapo wananchi wataweza kufanya maombi yao katika mfumo wa mtandao na baadaye kufika ofisi ya RITA iliyo karibu na hasa katika maeneo ambapo Serikali za Mitaa zipo.

Mheshimiwa Spika, Wakala wa Usajilli, Ufilisi na Udhamini (RITA) umejiwekea malengo ya kusajili na kutoa vyeti vya kuzaliwa kwa wananchi wapatao 15,917,602 ifikiapo mwaka 2025. Idadi hii itafanya wananchi wasio na vyeti vya kuzaliwa kupungua hadi kufika 21,508,277 ambao ni chini ya asilimia 50 ya wananchi wote ambao wamefikisha umri wa zaidi ya miaka mitano.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa wito kwa wananchi wote ambao hawana vyeti vya kuzaliwa kufika kwenye Ofisi za Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) kwa ajili ya kusajiliwa na kupewa vyeti vya kuzaliwa ikiwa ni haki yao muhimu ya kutambuliwa. Kadhalika, nawaomba Waheshimiwa Wabunge wote kuendelea kushirikiana na Serikali kwa kuwaelimisha wananchi katika majimbo yenu juu ya umuhimu wa kusajili matukio muhimu ya binadamu ikiwa ni pamoja na kujisajili na kupatiwa vyeti vya kuzaliwa. Ahsante.
MHE. ANATHROPIA L. THEONEST (K.n.y. MHE. GIMBI D. MASABA) Aliuliza:

Wilaya mpya ya Itilima haina Mahakama ya Wilaya, jambo linalosababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi kwenda Wilaya jirani ya Bariadi kupata huduma hiyo:-

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya Itilima?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masamba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Wilaya ya Itilima kwa sasa haina Mahakama ya Wilaya na wananchi wanalazimika kusafiri umbali mrefu takriban kilometa 37 kufuata huduma katika Wilaya ya Bariadi. Aidha, changamoto hii ipo kwenye Wilaya 27 nchini, ambazo zinapata huduma katika wilaya za jirani. Hii inatokana na ukweli kwamba Mahakama ya Tanzania bado inakabiliwa na uhaba wa majengo katika maeneo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimekuwa nikieleza katika Bunge lako, Mahakama imejiwekea mkakati wa kutatua changamoto hii hatua kwa hatua kupitia mpango wake wa miaka mitano na kujenga na kukarabati majengo ya Mahakama kwa ngazi zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama ya Wilaya ya Itilima ipo kwenye mpango wa kujengwa kwa mwaka 2019/ 2020 pamoja na Mahakama nyingine za Wilaya za Busega, Kyerwa, Misenyi, Gairo, Mbogwe, Songwe, Rufiji, Kibiti, Nyang’hwale, Mvomero, Uyui, Kaliua, Uvinza, Buhigwe, Kakonko, Chamwino, Chemba, Ikungi, Mkalama, Butiama, Rorya, Ubungo, Malinyi, Tanganyika, Mkinga, Kilosa, Kilombero, Hanang na Nkasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Itilima kwa kutupatia kiwanja cha kujenga Mahakama ya Wilaya yenye ukubwa wa mita za mraba 5,028. Aidha, nitoe pia shukrani zangu za dhati kwa Halmashauri za Wilaya zote nilizozitaja kwa kutupatia viwanja kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya Mahakama. Ahsante.
MHE. ALLY SALEH ALLY aliuliza:-

Katika masuala ya Haki za binadamu Tanzania ina wajibu wa ndani na nje na kila wajibu unahitaji kuonekana wazi ili kujenga imani kwamba haki za Binadamu zinatekelezwa katika viwango vya Kisheria, Kikatiba na Kimataifa?

(a) Je, Serikali itatimiza vipi matakwa haya ya ndani na nje?

(b) Je, ni kiasi gani Serikali imekuwa ikijenga misingi ya usimamizi, ufuatiliaji na utekelezaji wa Haki za Binadamu ndani ya nchi?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Saleh Ally (Malindi) lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, Sheria zetu za nchi, Mikataba ya Kimataifa na Kikanda, Serikali ina wajibu wa kuheshimu na kulinda haki za binadamu nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutimiza wajibu huo, ndani ya nchi, Serikali imeweka mfumo wa Kisheria na Kitaasisi ili kuhakikisha kuwa masuala ya haki ya za binadamu nchini yanalindwa, yanatekelezwa na kuheshimiwa ipasavyo. Kwa kufanya hivyo, Serikali ilianzisha Chombo mahsusi, kitakachosimamia masuala ya haki za binadamu nchini ambacho ni Tume ya haki za binadamu na Utawala Bora iliyoanzishwa kwa mujibu wa Katiba na imewekwa ikifuatilia utekelezaji wa misingi ya haki za binadamu na Utawala bora na kuishauri Serikali namna bora ya kuboresha utekelezaji wa wajibu wake ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania kama ilivyo kwa nchi nyingine duniani, ambazo zimeridhia Mikataba mbalimbali ya Kimataifa na Kikanda, inayohusu haki za binadamu imekuwa ikijenga misingi ya usimamizi, ufuatiliaji na utekelezaji wa haki za binadamu ndani ya nchi kwa kutunga Sheria mbalimbali na kuanzisha Taasisi na mfumo inayosaidia utekelezaji wa misingi iliyowekwa kwa mkataba ya Kimataifa na Kikanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania, imekuwa ikiwasilisha taarifa zake kuhusu utekelezaji wa haki za binadamu nchini katika vyombo mbalimbali vya Kimataifa na Kikanda. Taarifa hizo hujadiliwa na mapendekezo ya kuboresha haki za binadamu nchini hupokelewa na kutekelezwa kwa kuzingatia Sheria za nchi, mila na desturi za Watanzania pia.
MHE. JANET Z. MBENE aliuliza:-

Serikali iliingia Mikataba na Uwekezaji na Wadau mbalimbali kwenye Sekta tofauti ambayo kwa sababu mbalimbali imesitishwa na Serikali?

(a) Je, ni Mikataba mingapi imesitishwa na ni sekta zipi zinaongoza?

(b) Je, Serikali imeingia gharama kiasi gani, katika kesi zilizofunguliwa Mahakamani na kusitishwa kwa Mikataba hiyo?

(c) Je, Serikali imepata faida au hasara gani kwa kusitisha Mikataba hiyo?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Janet Zebedayo Mbene Mbunge wa Ileje, lenye sehemu (a) (b) na (c) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Ni kweli Serikali imekuwa ikisitisha Mikataba ya Uwekezaji kutokana na sababu mbalimbali, moja ikiwa ni kwa upande mmoja mwingine ni Mkataba wa kushindwa kutimiza masharti kwa mujibu wa Mkataba au makubaliano ama inapobainika kuwa kulikuwa na udanganyifu ambao haukuweka wazi taarifa za msingi wakati wa kuingiwa katika Mikataba hiyo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Serikali bado inaendelea na mapitio ya Mikataba yote, iliyoingiwa na Serikali ili kutambua kama vigezo na masharti kama ya Mikataba hiyo vinatimizwa ipasavyo. Mara zoezi hili, likikamilika Serikali itakuwa na takwimu sahihi ya Mikataba yote, iliyosainiwa sambasamba na kuifanya tathmini ya gharama zake zilizotumika kwa kesi zilizofunguliwa kutokana na usitishwaji wa Mikataba husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Hati Idhini ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, iliyochapishwa katika gazeti la Serikali kwa Tangazo namba 48 la mwaka 2018 na Sheria ya marekebisho mbalimbali ya Sheria ambayo pamoja na mambo mengine imerekebisha majukumu ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambapo utekelezaji wa majukumu ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imeboreshwa zaidi, kwa kuanzishwa kwa Idara itakayoishughulikia utekelezaji wa Mikataba yote baada ya kufanyiwa mapitio yaani vetting. Jukumu hili litawezesha kutambua na kupata takwimu sahihi za Mikataba yote iliyositishwa, inayotakiwa kusitishwa na inayotakiwa kufanyiwa marekebisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, Pia, mabadiliko ya Sheria hiyo yameanzisha Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ambayo kwa sasa inasimamia mashauri yote ambayo Serikali inashtaki au kushtakiwa. Kwa sasa Ofisi hii inaendelea na kazi ya utambuzi wa mashauri yote dhidi ya Serikali kutoka katika Wizara na Taasisi zote za Serikali. Jitihada zote hizi, zina malengo ya kusaidia upatikanaji wa takwimu sahihi na mashauri yaliyofunguliwa kutokana na usitishwaji wa Mikataba na kutambua faida na hasara zake.
MHE. SILAFU J. MAUFI aliuliza:-

Mgane anapobaki na watoto hundi zinazolipwa kama kuna malipo huandikwa kwa jina lake, lakini kwa wajane huwa ni tofauti, anapewa masharti ya kulipiwa mahakamani na awe na muhtasari wa kikao cha upande wa mwanaume na ndipo malipo yafanyike kwa mgao maalum.

(a) Je, kwa nini mjane asiandikwe jina lake kwenye hundi na asimame na watoto wake kwa kupewa haki hiyo?

(b) Je, Serikali haioni kama inamnyanyasa mjane?

(c) Kama ni sheria; je, Serikali haioni kwamba ni wakati wa kuiangalia upya sheria hiyo?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Silafu Jumbe Maufi, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, masuala ya mirathi yanasimamiwa na Sheria ya Mirathi, Sura ya 352. Sheria hii inatoa utaratibu mzima unaohusu masuala yote ya mirathi, wosia, kufungua mashauri ya mirathi, usimamizi, pingamizi la msimamizi au msimamizi anapofariki au asipotendewa haki.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, sheria za nchi zinatambua kuwa mirathi na usimamizi wake unaweza kuongozwa na Sheria ya Kiislam au Sheria ya India ya mwaka 1885 kwa wasiokuwa waislamu. Matumizi ya sheria hizi yanaangalia maisha ya marehemu, dini na namna marehemu alivyozikwa. Pia sheria hizi zinaeleza namna mali itakavyopaswa kugaiwa kwa wanufaika huku ikiainisha kila mnufaika kwa kiwango anachopata.

Mheshimiwa Spika, nchi yetu inajali na kutambua kuwa binadamu wote ni sawa na hii imeelezwa katika Ibara ya 12(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977. Ibara ya 13(2) ya Katiba inatoa marufuku kwa sheria yoyote kuweka shauri lolote lile la kibaguzi katika matumizi yake.

Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo hakuna sheria yoyote inayompa mgane haki zaidi mjane au kwa namna yoyote kuonesha ubaguzi. Hata hivyo, utaratibu unaofanyika unatamka msimamizi wa mirathi kuwasilisha mchanganuo wa malipo na hundi huandikwa kwa wanufaika wote pasipo kujali jinsia zao.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuwa na sheria nzuri, kumekuwa na uelewa mdogo miongoni mwa baadhi ya wananchi kuhusu sheria, kanuni na taratibu zinazohusu masuala ya mirathi. Wizara yangu kupitia RITA na wadau mbalimbali imekuwa ikitoa elimu kwa makundi mbalimbali kuhusu mirathi na maendeleo na kubuni mbinu zitakazosaidia ili elimu ya mirathi iwafikie wananchi wengi zaidi.

Mheshimiwa Spika, kupitia Bunge lako tukufu, ninaomba Waheshimiwa Wabunge wote tushirikiane katika kuchangia jitihada za Serikali katika kufikisha elimu ya mirathi kwa wananchi wetu katika maeneo yetu yanayotuhusu, ahsante.
MHE. SAED A. KUBENEA aliuliza:-

Serikali ilitangaza kuwa wanasheria wote walioko kwenye mashirika ya umma watafanya kazi chini ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ili kupunguza gharama za uendeshaji wa kesi na kuwapa ufanisi kwenye ufuatiliaji wa kesi zinazofunguliwa dhidi ya Serikali.

(a) Je, utekelezaji wa agizo la Serikali kuhusu mawakili binafsi kutosimamia kesi za Serikali limefikia wapo?

(b) Je, ni kiasi gani cha fedha kilichookolewa tangu mashirika ya Serikali yaache kutumia mawakili wa nje?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Saed Ahmed Kubenea, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kutokana na mabadiliko ya Sheria ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali yaliyofanywa kupitia Sheria ya Marekebisho ya Sheria mbalimbali Na. 2 ya mwaka 2018 yaliyopitishwa na Bunge lako tukufu, yaliwezesha kufanya wanasheria wote katika utumishi wa umma kuwa chini ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Mabadiliko hayo yalitokana na Tangazo la Serikali Na. 50/2010 lililotambua kuwepo kwa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ambayo amepewa jukumu la kusimamia, kuratibu na kuendesha mashauri yote ya madai ambayo Serikali inashtaki au inashtakiwa.

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu kupitia Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali tayari imeshatoa maelekezo kwa Wizara na Taasisi zote za Serikali kuwasilisha mashauri yote ya madai dhidi ya Serikali katika Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kwa ajili ya uratibu, usimamizi na uendeshaji.

Mheshimiwa Spika, kutokana na uwezeshaji wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kwa sasa mashauri yote ya madai dhidi ya Serikali yanasimamiwa na ofisi hii isipokuwa kama itaonekana kuwepo kwa ulazima wa kuhusisha mawakili binafsi. Hii hutokea iwapo mashauri husika yamefunguliwa katika mahakama za nchi za nje zisizokuwa za Kimataifa ambazo kwa baadhi ya nchi sheria zake za ndani na taaluma ya uwakili haziruhusu mawakili wa nchi nyingine kufanya shughuli za uwakili hasa uwakilishi mahakamani ndani ya nchi husika.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, inapotokea hitaji la kutumia mawakili binafsi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali hulazimika kutoa kibali cha Serikali cha kuajiri Wakili kutoka ndani ya nchi hiyo itakayoshirikiana na Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali katika kusimamia uendeshaji wa shauri husika.

Mheshimiwa Spika, kuwepo kwa ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kumesaidia kupunguza gharama zilizokuwa zinalipwa na wakili binafsi ambazo kwa tathmini ilifanyika uendeshaji wa kila shauri moja hapa nchini zilikuwa hazipungui shilingi 5,000,000 na kwa upandea mashauri yaliyofunguliwa nje ya nchi gharama za kumlipa wakili kwa kila shauri ilikuwa hazipungui dola za Marekani 300,000 mpaka 2,500,000 kwa kila shauri.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza katika hotuba yangu ya bajeti 2019/2020 kwa mwaka 2018/2019 Serikali iliokoa kiasi cha shilingi 9,018,957,011 ambazo zingelipwa kwa mawakili binafsi. Ninapenda kulithibitishia Bunge kuwa Serikali itaendelea kuokoa fedha nyingi zaidi ambazo zitasaidia kuleta maendeleo katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, tunaendelea na kazi ya ukusanyaji wa mashauri yote ya madai kutoka kwa Wizara na Taasisi zote za umma/Serikali. Zoezi hili litakapokamilika litasaidia kufanya tathmini ya kina na kupata thamani halisi ya fedha zilizookolewa na Serikali kupitia maboresho haya mapya. Ahsante.
MHE. DKT. SULEIMAN ALLY YUSSUF aliuliza:-

Mfumo wa Mahakama umejiwekea utaratibu wa kuanza na kuamaliza mashauri ambapo kwa Mahakama ya Rufaa na Mahakama Kuu ni miaka miwili, Mahakama za Mahakimu Wakazi ni mwaka mmoja na Mahakama za Mwanzo ni mie zi sita. Utaratibu huu ni mzuri ambao unaendana na msemo usemao: “Haki iliyocheleweshwa ni sawa haki iliyonyimwa.”

Je, ni kwa nini utaratibu huu haufuatwi na badala yake kesi nyingi zinachukua muda mrefu?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshi miwa Spika, n apenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Suleiman Ally Yussuf, Mbunge wa Magogoni, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli Mahakama ya Tanzania imejiwekea utaratibu wa kuhakikisha mashauri yote ambayo yanafunguliwa Mahakamani yanakuwa na muda maalum wa kukamilika katika ngazi husika za Mahakama kama yalivyo maelezo kwenye Swali la Msingi la Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Spika, utaratibu huu kwa kiasi kikubwa umesaidia kupunguza changamoto ya mlundikano na mashauri kuchukua muda mrefu kusikilizwa. Pamoja na mfumo huu mzuri, bado kwa baadhi ya Mahakama utaratibu huu umekuwa haufuatwi kutokana na sababu mbalimbali kama idadi ndogo ya Majaji na Mahakimu ikilinganishwa na mashauri yanayofunguliwa Mahakamani, upepelezi kwa baadhi ya mashauri y a jinai kuchukua mud a mrefu, maahirisho ya mara kwa mara kutoka kwa Wadaawa wenyewe na sababu nyingine nyingi ambazo zinawagusa wadau wakubwa wa Mahakama katika uendeshaji wa mashauri.

Mheshi miwa Spika, itakumbukwa, w akati w a maadhimisho ya kilele cha Wiki ya Sheria nchini Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ali ke mea ucheleweshwaji wa upelelezi katika mashauri mbalimbali na kutaka taasisi zinazohusika kufanya kazi hiyo kwa haraka ili haki za watuhumiwa zipatikane kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni Jaji Kiongozi aliwataka Mahakimu wa Mahakama za Wilaya na Mahakama za Hakimu Mkazi nchini kutopokea kesi za jinai ambazo upelelezi au ushahidi wake haujakamilika (Tangazo la Serikali Na. 296 la mwaka 2012). Utekelezwaji wa mwongozo huu utasaidia sana usikilizwaji wa mashauri haraka na hivyo haki kupatikana kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, vilevile ninamshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli katika Awamu ya Tano kwa kuteua idadi kubwa ya Majaji wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani.

Mheshimiwa Spika, napenda kulithibitishia Bunge lako kuwa, Serikali kwa kushirikiana na Mahakama, tutaendelea kuhakikisha changamoto hizi zinapungua kwa kiasi kikubwa ikiwa ni pamoja na kuongeza idadi ya Majaji na Mahakimu katika Mahakama zetu.
MHE. ALMASI A. MAIGE aliuliza:-

Wilaya ya Uyui haina Mahakama ya Wilaya na ina Mahakama moja tu ya Mwanzo inayotumia chumba kidogo katika jengo la Mkuu wa Wilaya ya Uyui baada ya kutelekeza Mahakama ya Mwanzo ya Upuge:-

(a) Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya ya Uyui?

(b) Je, ni kwa nini Serikali ilitelekeza Mahakama ya Mwanzo ya Upuge pamoja na majengo yake katika Kijiji cha Upuge?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Almasi Athuman Maige, Mbunge wa Tabora Kaskazini lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, uhaba wa majengo ni moja ya changamoto kubwa inayoikabili Mahakama ya Tanzania, Mahitaji ya majengo ya kuendeshea shughuli za mahakama hapa nchini ni makubwa, Kwa msingi huo, mahakama imejiwekea utaratibu wa kujenga majengo haya kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya Uyui ni miongoni mwa majengo ya Mahakama za Wilaya 33 yaliyopangwa kuanza kujengwa mwezi June, 2020 kwa ufadhili wa Benki ya Dunia, kwa sasa mahakama ipo katika hatua za mwisho kukamilisha mchakato wa awali ili ujenzi wa majengo hayo uanze kwa muda kama ilivyo katika mpango wa mahakama.

Mheshimiwa Spika, Serikali haikulitelekeza jengo la Mahakama ya Mwanzo Upuge, sababu kubwa ilikuwa ni uchakavu wa jengo lenyewe ambalo halikuwa rafiki kuendelea kutumika kuendeshea shughuli za mahakama. Hata hivyo, tunatoa shukrani zetu za dhati kwa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Uyui kwa kutuwezesha kupata ofisi kwa ajili ya kuendelea kutoa huduma za Mahakama ya Mwanzo Upuge wakati tukiendelea na taratibu za ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya ambayo pia itakuwa na Mahakama ya Mwanzo katika jengo moja.
MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:-

Wananchi wa Hydom wameandaa eneo kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama kwa sababu Polisi wakikamata watuhumiwa huwapeleka Mbulu Mjini kilomita 86 ilipo Mahakama ya Wilaya:-

(a) Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Hydom?

(b) Je, Serikali haioni kuwa inapata hasara sana kupeleka Mahabusu Mbulu Mjini umbali wa kilomita 86 kutoka Hydom?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, uhaba wa majengo ni moja ya changamoto kubwa inayoikabili Mahakama ya Tanzania, mahitaji ya majengo ya kuendeshea shughuli za mahakama hapa nchini ni makubwa, kwa msingi huo, Mahakama imejiwekea utaratibu wa kujenga majengo haya kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wa Manyara, Wilaya za Mbulu, Hanang, Kiteto na Simanjiro hazina majengo ya Mahakama za Wilaya. Aidha, Wilaya ya Mbulu ina Mahakama za Mwanzo tatu tu zinazofanya kazi, ambazo ni Daudi, Endagkot na Dongobesh, licha ya ukubwa wa Wilaya yenye Tarafa tano. Hivyo, Tarafa mbili za Hydom na Nambisi hazina Mahakama za Mwanzo changamoto inayowafanya wananchi wa Hydom kutembea umbali mrefu kufuata huduma za mahakama katika Mahakama ya Mwanzo Endgkot ama Dongobesh.

Mheshimiwa Spika, vigezo vinavyotumika kuainisha maeneo ya kipaumbele ni pamoja na umbali, idadi ya watu, wingi wa mashauri na shughuli za kiuchumi ambazo mara nyingi ni kiashiria cha kuongezeka kwa idadi ya mashauri. Kwa kuzingatia vigezo hivyo na mpango wetu wa ujenzi, nipende kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa Mahakama ya Mwanzo Hydom imepangwa kujengwa mwaka 2020/2021.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE aliuliza:-

Wananchi wa Wilaya ya Mbogwe wanapata changamoto kubwa katika kupata huduma za kimahakama kwa kuzifuata Wilaya za jirani:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Mahakama ya Wilaya Mbogwe?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Augustino Manyanda Masele, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, uhaba wa majengo ni moja ya changamoto inayoikabili Mahakama ya Tanzania. Mahitaji ya Majengo ya kuendeshea shughuli za Mahakama hapa nchini ni makubwa. Kwa msingi huo, Mahakama imejiwekea utaratibu wa kujenga majengo haya kwa awamu kulingana na mpango wa ujenzi na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya Mbogwe ni miongoni mwa Majengo ya Mahakama za Wilaya 33 yaliyopangwa kuanza kujengwa mwezi Juni na kukamilika mwezi Disemba, 2020 kwa ufadhili wa Benki ya Dunia. Kwa sasa Mahakama ipo katika hatua za mwisho kukamilisha taratibu za awali ili ujenzi wa majengo hayo uanze kwa muda kama ilivyo katika mpango wa Mahakama. Tayari Mshauri Elekezi amefanya mapitio ya michoro na ujenzi unatarajiwa kuanza kama ilivyopangwa.