Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Khatib Said Haji (33 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nianze kutoa shukrani kwa Mwenyezi Mungu kunijalia leo kusimama hapa nikiwa na afya njema. Pili, niwashukuru kwa dhati sana wananchi wa Jimbo la Konde kwa kunirejesha tena hapa ili niweze kuwawakilisha.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu, kwa umuhimu mkubwa sana natoa pongezi kwa wananchi wa Zanzibar kwa maamuzi mema na ya dhati ya kumchagua Maalim Seif Sharif Hamad kuwa Rais wa Zanzibar. Suala la Jecha kasema nini, Mwenyezi Mungu ataisimamisha haki hapa duniani na watu wote wataona. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo ilikuwa ni bashrafu, sasa nataka nianze kuchangia. Ukurasa wa nane wa hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyeitoa hapa alisema, naomba ninukuu:- “Eneo lingine linalolalamikiwa ni Polisi. Kuna malalamiko mengi ya wananchi
kubambikiwa kesi, upendeleo, madai ya Askari kutotimizwa, ukosefu wa nyumba za Maaskari na kadhalika”.
Mheshimiwa Naibu Spika, malalamiko ya raia wa nchi hii juu ya Polisi ni mengi sana. Wakati mwingine tunaweza kuwalaumu Polisi wakati amri hizi wanazozitekeleza Polisi zinatoka kwa viongozi wa CCM. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya uchaguzi mkuu ilitoka amri ya Kiongozi Mkuu wa Serikali, Waziri Mkuu akiwaambia ni marufuku vyama vya siasa kufanya mikutano ya hadhara hasa kwa wale waliokuwa hawakushinda. Kiujumla tangazo lile lilihusu kutubana sisi vyama vya
upinzani kuonana na wananchi wetu kuwaeleza ukweli juu ya yaliyotokea katika uchaguzi mkuu, hii siyo sawa! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vyama vya siasa vipo kwa mujibu wa Katiba. Tunapoapa hapa kabla ya kuanza kazi hizi tunaapa kuilinda, kuitetea na kuiheshimu Katiba hii. Leo unapokurupuka na amri zako zilizo kinyume na Katiba hii, wewe ndiyo unayesababisha fujo, tukubaliane! Kuna mambo tunayoinishiwa kama vyama vya siasa kwa mujibu wa Katiba tuna haja ya kuyatenda. Hatulazimiki kuomba vibali kwa Polisi tunapotaka kufanya mikutano yetu ya hadhara, tunalazimika kutoa taarifa, leo imepotea hii na badala yake twende tupige magoti
kwao wao ni nani? Hilo ni moja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukurasa wa kumi wa hotuba ya Mheshimiwa Rais alizungumzia suala la Zanzibar kwa kifupi sana kana kwamba si jambo muhimu sana. Naomba ninukuu sehemu tu:-
“Mheshimiwa Spika, aidha, kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na wadau wa siasa hususan vyama vya CUF na CCM, tutahakikisha majaribu ya kisiasa yanayoikabili Zanzibar yanamalizika kwa usalama kabisa”.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya neno hili alilolisema Rais mpaka leo hii Mheshimiwa Magufuli hajasema tena neno lingine lolote linalohusiana na Zanzibar, hajasema! Ameishia kuwaalika Ikulu baadhi ya viongozi na pale alipokuwa akitoka hakuna lolote alilolizungumza
kuweka njia ya kuonyesha kwamba analichukulia uzito suala la Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka nieleze sisi ni wawakilishi wa wananchi. Mimi kabla ya kuja hapa Bungeni nilikutana na wananchi wangu wa Jimbo la Konde na kimoja walichotaka niseme nitakisema hapa bila kujali kwamba litawapendeza au litawakasirisha.
Sikuja hapa kwa mapenzi ya yeyote, nimekuja hapa kwa mapenzi ya Mungu kwa uwakala wa watu wa Konde. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mnaposimama mkasema kwamba uchaguzi wa Zanzibar, wengine wamesema hapa, utarudiwa tarehe 20…
MHE. KHATIB SAID HAJI: Tulieni mgangwe maradhi si kitu. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza tujiulize hao waliosimamia hilo waliapa kutii Katiba wanarudia uchaguzi, Tume ya Uchaguzi, Jecha alipofuta uchaguzi ule alifuta kwa aya ya ngapi ya kanuni na sheria za nchi hii?
MHE. KHATIB SAID HAJI: Akamuulize, nitawauliza ninyi mliomuweka. (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, alivunja sheria za nchi, mtu anayestahiki kuweko gerezani, Magufuli anakwenda Zanzibar kwenye sherehe za Mapinduzi anakaa ubavuni kwake, anatujojea Wazanzibari. Tunasema haki itasimama kuwa haki hata mfanye nini hamtaipinga.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, anayepigwa, anayedungwa sindano kila mmoja anahisi maumivu anayopata mdungwa sindano lakini tako linalodungwa sindano ndiyo linaloathirika zaidi na maumivu ya sindano hiyo.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Spika, mambo ya Zanzibar yanachukuliwa kiutani, mnalifanyia jambo hili utani ndugu zangu. Ni wajibu tujue kwa mfano Jimbo langu la Konde uchaguzi uliopita CCM mlipata kura 700 mwaka huu mmepata kura 500.
Kwa mujibu wa sensa Jimbo lenye wananchi 50,000, CCM wako mia tano. Leo mnapofanya masihara ya kusema kwamba uchaguzi unarudiwa, kwa wana CCM 500 walioko kwenye Jimbo la Konde mnatutakia amani kweli ninyi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuliangalia jambo hili kwa ujumla wake. CCM katika Kisiwa cha Pemba hakuna, vurugu ikianza wale watu hata tukisema nyumba kumi zizunguke nyumba moja, haiwezekani hawatafika popote. Msiweke mazingira ya kuitia nchi ile kwenye joto la uhasama na uuwaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mwalimu Nyerere aliwahi kunukuliwa katika miaka ya sitini akiwa Marekani au Uingereza, akisema kwamba: “Laiti angekuwa na uwezo angevihamisha visiwa vile vya Zanzibar vikawa mbali na Bahari ya Hindi kwa sababu anahisi vitakuja kutuletea
shida hapo baadaye”. Mwisho wa kunukuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hilo halikuwezekana. Nawauliza CCM mliobakia, nia yenu sasa ni kutuua Wazanzibar wote ili lengo lile mlilolikusudia Wazanzibar wasiwepo duniani mlitimize?
Kama lengo si hilo, kwanza kabisa nachukua nafasi hii nikiwa mwakilishi wa wananchi wa Konde na Mbunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuziomba Jumuiya za Kimataifa, walioshuhudia ukweli na uhalali wa kazi waliyoifanya Wazanzibar ya kuchagua Rais
wanayemtaka walisimamie hili kwa nguvu zao wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo Watanzania wanahukumiwa kwa kukosa msaada wa mabilioni ya shilingi kwa kuwalinda wahuni wa Zanzibar wasiozidi kumi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Bunge lililopita, kuna Mheshimiwa Mbunge mmoja, alitamka yafuatayo naomba kunukuu, alisema na akamuomba Rais Kikwete, nia yake ya kuiona Zanzibar inabaki na ustawi ni wakati wa utawala wake tu. La pili..
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. KHATIB SAID HAJI: Ole wenu…
SPIKA: Mheshimiwa muda wako umekwisha, naomba ukae.
Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ninamshukuru Mungu kunijalia na mimi leo kuwa mchangiaji katika hoja hii muhimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu tumekuwa tukipanga mipango kadhaa, waswahili wanasema mpango siyo matumizi, tumekuwa tukipanga lakini hatutumii, ni vema tujiulize tunapokosea ni wapi katika mipango hii, bila shaka kuna makosa tunayoyafanya ambayo yanatupelekea tunapanga vizuri lakini hakuna matokeo mazuri ya mipango yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii katika Mpango kuna jambo zito kubwa sana ambalo linajielekeza kuifanya Tanzania iwe ni nchi ya uchumi wa viwanda. Kusema tumesema sana juu ya hili na siyo mwanzo leo kusema kwamba nchi hii haiwezi kuendelea bila kuwa na mpango madhubuti wa kuendeleza viwanda vyetu. Leo hii yalaiti mimi nataka niseme wazi CCM mmemsaliti Mwalimu Nyerere, mimi siko radhi na Watanzania hawako radhi, mmemsaliti Mwalimu Nyerere kwa nini, kwa sababu Mwalimu Nyerere nchi hii alijitahidi kuwaonesha mfano, kwamba viwanda ndiyo vitakavyotutoa hapa tulipo na kwenda mbele. Matokeo yake mmekuja na sera zenu za ajabu, mmeua viwanda vyote, sasa mnafufua viwanda kwa maneno matupu, neno tupu hakuna utekelezaji unaofanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba ya Msemaji wa Kambi ya Upinzani, ndugu yangu Mheshimiwa Silinde, alizungumzia habari ya kusema lengo la Wachina kujenga pale Kurasini Logistic, ni kuifanya nchi hii kuendelea kuwa madalali, dampo ni kweli! Lakini imekosolewa vikali, hata mimi nataka niseme kwamba Mheshimiwa ndugu yangu Silinde mzoea udalali hawezi kazi ya duka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tukubaliane nao hivyo hivyo, kwa sababu tukisema tunakataa Wachina kujenga pale, uwezo wa kujenga viwanda kushnei, hakuna! Tutasema tumekaa humu, tutapita, watakuja na watakaopita, kwa Itikadi hii na utendaji huu wa Sera za Chama cha Mapinduzi, hebu ndugu zangu igeni yale mazuri yetu, ambayo tunawapa mawazo ninyi muyafuate, nchi hii ni yetu wote, nchi hii hakuna kitabu chochote kitakatifu kilichotaja CCM wala CUF wala CHADEMA, vitabu vyote vimewataja waja wa Mwenyezi Mungu atakao waweka sehemu moja aliyopenda yeye, tumejichagulia majina tumejiita Watanzania, wa Afrika katika dunia hii, lakini hakuna hilo andiko liko wapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaposhauri tuna malengo mazuri, nataka kusema kwamba ndugu zangu, tufuateni yale mawazo bila kujali anayeyatoa ni nani. Lile zuri na wewe Mheshimiwa Naibu Spika nimesikia huko, Bwana Mkubwa kamtumbua Wilson Kabwe, jamani tulisema hapa, Ezekiel Wenje alisema mpaka povu likamtoka, ninyi wenzetu huko mlifanyaje, sisi tulikuwa wabaya, leo mnatulaumu eti vyama vyetu hivi vya UKAWA vilimsimamisha Mheshimiwa Edward Lowasa kuwa mgombea wa Urais, Mheshimiwa Edward Lowasa akiwa CCM akitembea mnampokea kama malaika ninyi?
Mheshimiwa Naibu Spika, ninyi alienda Tanga nilikuwepo Katibu Mwenezi wa CCM alimpiga mtu kutaka kumuua kwa sababu kamkaripia Lowassa, kweli uongo? Mliimba nyimbo nzuri za kumpamba, mpaka mkatusadikisha kweli yaweza kuwa yale maneno yetu hatuko sawa, hebu tumuangalie. Leo tumefanya kosa kubwa, miaka yote mliokuwa naye alikuwa mzuri, mbaya kwetu, kwenu kizuri, tutakuwa naye na tutakufa naye Lowassa na Mungu akimuweka 2020 ndiye huyo huyo, mkipenda msipende dozi ni hiyo hiyo, mkinywa mkitema shauri yenu! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumzie jambo moja lililonigusa sana. Mheshimiwa Zungu siyo mara ya kwanza, siyo mara ya pili, siyo mara ya tatu amekuwa akishauri toka Bunge lililopita. Makampuni ya simu yanaiibia nchi, hii nataka niwaulize yeye yule siyo mpinzani, Mheshimiwa Zungu ni Mbunge wa CCM. Mheshimiwa Zungu alichokisema ni kwa maslahi ya nchi hii, mlifanya yapi, mmetekeleza lipi, hamna! Tutawasifu wafanyao mazuri na tutawakosoa wanafanya mabaya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, waliopewa jukumu la kusimamia suala hili hawajaitendea haki nchi hii, kama mu-watumbuaji wazuri wa majipu angalieni hili siyo jipu ni busha! Lazima tuangalie kile kinachokosesha mapato nchi hii, tukiangalia bila kuoneana haya, kuna tatizo gani kuandaa wataalam wetu makini, wakaona ni kwa kiasi gani Tanzania inapoteza mapato kutokana na makampuni ya simu. Yupo nani nyuma ya makampuni ya simu tuambieni, yuko nani? Siyo bure iko sababu. Siyo bure kwa sababu tafadhalini tunayoyasema hapa siyo kwa ajili ya ushabiki ni kwa ajili ya kuisaidia nchi hii, itoke ilipo iende mbele. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia juu ya maamuzi ya kukurupuka yanayochukuliwa na watendaji wa nchi hii. Nchi hii mmeingia mkataba wa himaya moja ya forodha kufanya mizigo ya Congo sasa hivi iwe inalipiwa kwao kabla ya kutoka katika Bandari ya Dar es salaam, jambo ambalo limechangia kushuka kwa makontena katika Bandari ya Dar es Salaam kufikia asilimia 50. Hebu niwaulize tumefanya yale kwa faida ipi?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu nchi ya Congo, mimi niliwahi kuwa mjasiriamali nilikaa pale Congo katika Mji wa Lubumbashi, nchi ile haijasimama utawala wake sawa sawa, pale unaweza kupeleka containers akaja Kanali tu wa Jeshi akatoa amri pitisha hizo kontena tano na zinapita. Sasa wafanyabiashara wale wa Congo mnapoweka vile vikwazo ambavyo haviisaidii nchi hii, wametafuta bandari ya Beira, wametafuta bandari za nchi nyingine wameiacha Dar es Salaam imedoda, mnapata faida gani? Mambo ya Wacongo yanawahusu nini ndugu zangu, msiba wa Kichina Mmasai anaingiaje? Waacheni wenyewe sisi tukusanyeni kodi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo nimesoma gazeti moja, nimeona taarifa Serikali inasema kwamba imeliona hili na mnalifanyia kazi, nawaomba sana ndugu zangu shitukeni mapema, kule Beira wakizoea utamu wa kule hakuna atakayerudi hapa, anzeni sasa kuchukua hatua msisubiri kesho na kesho kutwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumzie suala la utawala bora. Suala la utawala bora lina mtazamo mpana sana. Mojawapo ikiwa ni wananchi wenyewe wafaidike na utawala bora wenyewe. Nasikitika kwa kituko ambacho kimefanywa na Serikali yenu ya kuzuia matangazo haya wananchi wa Tanzania wasione wawakilishi wao wanasema nini, amesema mwenzangu hapa mmoja kwamba ule umaarufu Dkt. Chegeni mliokuwa mkiupata kwenye TV sasa hamtoupata tena. Kila Mbunge aliyeingia hapa mpaka ukiitwa Mbunge tayari wewe ni maarufu tu, ukaonekana kwenye TV usionekane kwenye TV wewe tayari ni maarufu tu. Wengine tuna umaarufu wa ziada.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi mwenyewe ni maarufu kwa sababu ni baba watoto nina familia na watoto wasiopungua 12, nina mke wangu ambaye naweza kumfanya Waziri Mkuu, mimi Rais wa familia na watoto wangu Baraza la Mawaziri, siyo umaarufu mdogo huo? Kila umaarufu una ngazi yake, leo umaarufu wangu siwezi kuufananisha na Mheshimiwa Magufuli lakini hata umaarufu wa Mheshimiwa Magufuli hauwezi kuwa zaidi ya Mheshimiwa Barrack Obama, hauwezi kuwa sawa! Kwa hivyo, humu hamna uwezo wa kutupunguzia umaarufu tulionao, mimi ni maarufu, mimi ni Rais kwenye familia yangu, watoto 12 ninao ni Baraza tosha kabisa la Mawaziri na mama watoto Waziri Mkuu wangu, ninataka umaarufu gani tena. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tafadhalini sana fikirieni tena kwa makini, hatutafuti umaarufu tunataka Watanzania wajue wawakilishi wao waliowachagua wanasimamia vipi yale wanayoelekeza wawakilishe kwa Serikali yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapo katika utawala bora kwa masikitiko tu ni kwamba leo hii nchi inayoitwa Zanzibar, nilisema kabla ya Bunge hili, kabla ya uchaguzi haramu uliofanyika mara ya pili Zanzibar, nilisema kwamba jamani tufikirieni maneno ya nchi wahisani wanayosema juu ya kuikatia misaada nchi yetu. Hili jambo misaada hii tusikae tukisema tutakula mihogo, mihogo ipo siku zote mbona hatukushiba? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo jamani Watanzania wenzangu, Wabunge wenzangu, niwaambie wazi watu wasiozidi kumi Zanzibar wanaifanya nchi hii iingie katika historia nyingine ya kuonekana nchi isiyo na demokrasia, wakati tunajidai ni nchi ya demokrasia. Kisiwa cha Zanzibar ambacho Mheshimiwa Ally Keissy alisema ukiwaita kwa filimbi wanakusanyika tunapatikana, wanainyima mamilioni ya Watanzania misaada katika nchi hii, siyo haki na tusijidai. Tumekuwa na matatizo, madeni yameongezeka, muda wote wakati ambapo tulikuwa tukipewa misaada, kuondoka kwa misaada hii ni tatizo, fikirieni tena.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Bunge hili, napenda kuwaambia wananchi wangu wa Jimbo la Konde, kwa sababu kule kwetu Zanzibar hata kufanya mikutano hatufanyi, ile nchi imekaa ndivyo sivyo, kile kisiwa kimekaa ndivyo sivyo, utawala bora haujulikani. Kwa mfano, leo akitokea CCM mmoja katika Jimbo akienda ku-report tu wale wana-CUF wameniangalia kwa jicho baya, kijiji kizima wanapelekwa askari wanakwenda kukisomba wanakiweka ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, siropoki! Tarehe 17 siku tatu kabla ya uchaguzi, mwana CCM mmoja katika Jimbo langu, alizua kwamba amechomewa nyumba hakikuungua hata kibakuli kimoja, walikuja kuchukuliwa wazee wa kijiji 30 wakaswekwa ndani kwa sababu tu ya amri ya kisiasa ya Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba. Utawala bora gani mnaoujadili nyinyi hapa Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba alitoa tangazo la kupiga marufuku wananchi wa Mkoa ule wasitembee usiku, ana mamlaka gani kisheria na Kikatiba kutangaza hali ya hatari katika Mkoa? Nchi hii ina Majemedari Wakuu wa Majeshi, Amiri Jeshi Wakuu wangapi? Hebu niambieni maajabu hayo kuna Amiri Jeshi wangapi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nasema na ninawaambia wananchi wa Jimbo la Konde kwamba dini zote zinakataza mtu kushirikiana na dhalimu, dini zote zinakataza kabisa mtu kushirikiana na mtu aliye dhalimu kwa njia yoyote.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, nawaomba wananchi wangu kuanzia mimi mwenyewe wasishirikiane na madhalimu muda wote wa uhai wa maisha yao, wasishirikiane nao. Kama wanauza watii masharti ya leseni kwa sababu inataka lazima kuuza, lakini kununua ni hiyari yao na hakuna atakaethubutu kuwaingilia, waendelee kufanya wanaloweza kuhakikisha madhalimu hawakamatani nao, hawashirikiani nao katika lolote na hilo nawaunga mkono mia kwa mia.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwape mfano tu mimi mwenyewe nimeanza, Mwakilishi wa CCM haramu aliyechaguliwa tarehe 20 alinipigia simu nikamwambia ukome kama ulivyokoma kuzaliwa mara ya pili kwenye tumbo la mama yako, na nilimwambia asinisogelee na akinisogelea hamtaniona tena hapa Bungeni, tutamalizana huko huko, hamtaniona. Haiwezekani, unakaaje na watu wanaodhulumu haki za watu?
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi hii imejijengea historia sasa ya kuifanya ile Zanzibar ni kichaka, leo ninyi mnatafuta watalii wakija wakiwinda vitalu na kupiga wanyama badala yake ninyi mnachukua Jeshi lenu mnalipeleka Zanzibar kuwalinda mama zetu na baba zetu, haki iko wapi? Wameleta magari yote ya Tanzania Bara kuja katika Kisiwa cha Pemba; mnawawinda nini, mnawatakia nini mama zetu, ndugu zetu, watoto wetu, tuna lipi baya, kukataa tu kuiunga mkono CCM ndiyo kosa letu? Kama hilo ndiyo kosa niwahakikishieni hata dunia iundwe mara ya pili CCM hatutaikubali na hatuitaki!
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami kabla ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kuweza kusimama hapa na pia napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwajalia Wabunge wenzangu wote ambao tuko hapa, tupo katika hali ya afya njema na salama kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kwanza kabla ya kutoa mchango wangu wa mpango huu kuitakia heri Kamati ya Uongozi ya Chama cha CUF chini ya Jenerali Julius Mtatiro. Pili nimtakie kheri kipenzi cha Wazanzibari, Maalim Seif Sharrif Hamad nikimwambia zidisha uzi huo huo na kwa niaba ya Wabunge wa Chama cha Upinzani cha CUF, wote wako pamoja na wewe na Kamati ya Uongozi wa CUF na hawatayumba na hawatayumbishwa, wale wote wenye dhana kwamba CUF itakufa, watakufa wao kabla CUF haijafa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mbunge mwenzangu Mheshimiwa Stanslaus Nyongo aliongelea suala la mdororo wa mizigo katika bandari yetu. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Viwanda na Biashara, Mheshimiwa Nyongo ni Mjumbe mwenzangu tuko katika Kamati moja inayoongozwa na Mwenyekiti shupavu Mheshimiwa Dkt. Dalaly Peter Kafumu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango kama huu mwaka uliopita mimi ni miongoni mwa waliosimama hapa kwa mdomo huu huu, kiti hiki hiki, kipaza sauti hiki hiki nikatahadharisha juu ya mpango wa Serikali kuingia kwenye mfumo mmoja wa himaya hii ambao utawafanya Wakongo walipie mizigo yao kabla ya kuondoka katika bandari ya Dar-es-Salaam.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitahadharisha kwa kujua kwamba, athari zake wafanyabiashara wa Congo wana mbinu zao ambazo hazihusishi nchi yetu na nikatahadharisha sana kwamba, tutahadhari na mpango ule tusijiingize katika jambo lile ambalo limekuwa ni source moja kubwa ya mdororo wa mizigo katika bandari ya Dar-es-Salaam.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati nzuri sana tulipopata bahati ya kwenda katika Bandari ya Dar-es-Salaam Kamati yetu kutembelea na kuona uhalisia wa mambo ulivyo na taarifa tulizopewa na Watendaji wa Bandari, tuliporudi na kuiambia Serikali ukweli wa tulichokiona, zilikuja tafsiri tofauti tofauti ambazo tulionekana sisi ni waongo na hatuna ukweli katika tunayoyaeleza, au tumetumwa au tunatumiwa!
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Bunge yenye mchanganyiko wa Vyama vyote inakwenda kufanya kazi kwa ajili ya maslahi ya kuisaidia nchi hii, leo tunapoeleza ukweli, tunapokuwa tofauti na Watendaji wa Serikali ambao wanaogopa kumwambia Rais ukweli, huu ni ukweli! Wanaogopa kumwambia Mheshimiwa Magufuli ukweli uko hivi, wakadharau na wakasema waliyoyasema, lakini namshukuru Mwenyezi Mungu kitu cha ukweli kitaonekana tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi Waziri wa Biashara na Viwanda, Mheshimiwa Charles Mwijage, akikutana na Taasisi ya Wafanyabiashara Wasafirishaji (TATOA), kauli aliyosema ni ushahidi Watanzania nyote mmeisikia. Amekaa na wenye ma-truck anawaambia kwa muda waliofikia mizigo katika bandari yetu imepungua na sasa kinachofuata ni malori yenu mtafute parking myaweke na ikiwezekana wekeni vilainishi (grease), ili msubiri, hatujui ni mwaka huu au mwaka ujao. Nani mkweli na nani mwongo? Kamati kweli au Waziri mwongo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu mhukumuni kwa matendo yake, msimhukumu kwa dhana hafifu. Tuliyasema yale, leo Waziri amekuja kumthibitishia Rais kwa mlango wa nyuma kama ni kweli Kamati iliyoyasema, mdororo wa mizigo Bandari ya Dar-es-Salaam umekithiri na umeathiri sekta nyingi sana. Umeathiri uuzaji wa mafuta katika ma-truck, umeathiri huduma za mahoteli, umeathiri hata wale madereva, dereva yule wa truck kutoka Tanzania hadi Congo ana vituo chungu nzima, humo si ajabu wengine wameshazaa na watoto! Watu wale leo hawapiti, mashaka yameongezeka, uchumi umedorora, mahoteli yamefungwa! Sisi tunasema ukweli, ule mpango haufai na tunaiomba Serikali izingatie hili na iuondoe mara moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kodi katika huduma za mizigo ya transit ni kigezo cha pili ambacho kimesababisha wafanyabiashara wa Congo wakimbie! Naomba Mheshimiwa Waziri, jambo hili pia walizingatie kwa makini ili bandari yetu irudi katika hali yake, wafanyabiashara warudi na sekta za uchumi za nchi hii ziweze kupanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi nyingi duniani ndani ya siku 100 za utawala wao huwa wanatoa taswira ya hali za uchumi za nchi zao zinavyoendelea, leo tuna mwaka mmoja wa utawala huu wa Chama kizee bado hatujajua hasa Watanzania wanaelekea wapi katika mfumo wa uchumi wa nchi hii. Hili ni jambo la kusikitisha sana! Sasa tunapowaambia hapa siyo kwamba, tunawaambia tunawachukia, tunawaambia ili mjue kama ni wajibu wetu kuwawakilisha wananchi na kuwaambia yale yaliyo ya kweli na hakuna budi myafuate, kwa sababu, sisi pamoja na kwamba ni washauri, lakini mshauri anayemalizia na kuwa na azimio huyo ni mshauri tofauti na washauri wa ngoma za mtaani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie Kituo cha Uwekezaji ambacho kimeandikwa katika taarifa ya Kamati, Kituo cha Uwekezaji cha Biashara cha Kurasini; mradi huu mkubwa wa Kituo cha Uwekezaji cha Kurasini ni jambo lililoanza mwaka 2010 na Bunge lililopita kwa mara ya mwanzo walitakiwa kulipa bilioni 45 Tanzania shillings ili kuuwezesha mradi ule mkubwa wa uwekezaji uwepo ndani ya nchi yetu. Matokeo yake mradi ule ulisuasua kutoka shilingi 45 bilioni ukaenda mpaka shilingi bilioni 60 ni mwaka wa pili, ukaenda mpaka shilingi bilioni 90 mwaka wa tatu, ukaenda mpaka shilingi bilioni 120, ndiyo matokeo yake umemaliza kulipwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kusikitisha leo katika taarifa hii nimeona wanasema kama wale wafadhili ambao walikusudia kuendeleza mradi ule kuutekeleza wameondoka na haijulikani hatima yake. Tukumbuke kwamba, pesa za Watanzania zilizotumika, Watanzania walioondolewa maeneo yale kupisha mradi ule ni gharama kubwa ambayo imepatikana na maslahi hayaonekani yako wapi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tatizo ni nini? Tatizo ni kuchelewa kwetu kufanya maamuzi katika mambo ya msingi ya nchi hii. Tunachelewa, ni hodari sana wa kuandika kwenye karatasi, lakini ni wazito sana wa kutekeleza yale ambayo tunadhani yanaleta tija kwa nchi hii. Leo mradi ule ambao ulikuwa unagombaniwa na nchi zote za Kiafrika, Tanzania ikapata bahati ikachaguliwa na China kuletewa mradi ule mkubwa tumekaa hapa tumebabaika-babaika mpaka tayari mradi ule, leo nimeona kwenye taarifa umeondolewa wakati Tanzania ikiwa imeshalipa mabilioni ya shilingi kupata lile eneo na Watanzania waliokuwa wakiendesha maisha yao pale wametupwa hata hatujui wametupwa wapi! Leo matokeo yake tunakuja kuona hapa kwenye taarifa kama wafadhili wale wamejiondoa. Hiyo ni hasara nyingine kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huku kusuasua kwa kutekeleza miradi ambayo ni fursa kwa nchi inatueletea shida sana. Leo ni mwaka karibu wa 10 tunazungumza ndani ya nchi hii kuna chuma pale Liganga na Mchuchuma na kwenye mpango huu, kila mpango unaokuja tunaambiwa, tunasadikishwa kwamba, mradi wa chuma Liganga na Mchuchuma utafanyika, lakini matokeo yake tunaishia kusoma vitabu! Laiti mradi ule ungekuwa uko Kenya au Uganda au Burundi, leo tayari nchi zile zingekuwa zinazalisha chuma kile kwa wingi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika sana Mwenyezi Mungu akishawapa anawapa, lakini kwa ugoigoi ambao tuko nao hata kama ingekuwa Mwenyezi Mungu anafikiria kuuondoa, bora angeuondolea mbali kwa sababu anatupa riziki tuzitumie kwa niaba ya watu wetu, lakini hatuwezi kutumia zile fursa, badala yake tunaandika kwenye makaratasi tu hatuwezi kufanya chochote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango huu tena leo nimeona nia ya Serikali juu ya kufufua viwanda. Imezungumzwa hapa General Tyre ya Arusha na viwanda vingine, TEMDO na kadhalika. Mheshimiwa nyimbo hizi hebu sasa Waheshimiwa Mawaziri, Serikali, wawe tayari kile wanachotusadikisha kinaweza kufanyika waweze kukifanya kwa muda unaowezekana. Leo hakuna asiyejua kwamba nchi ina demand kubwa ya matairi ya magari, biashara ya matairi ya magari ni biashara kubwa sana duniani, leo fursa ipo, mipira ndani ya nchi hii inazalishwa, lakini bado tunaimba wimbo tunafufua General Tyre kwenye vitabu, kwenye utekelezaji hakuna kinachotekelezeka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao Maprofesa wengi wabobezi wa uchumi, wabobezi wa uchumi chungu nzima kwenye nchi wa kuisaidia Serikali kuandaa mipango mizuri ya uchumi, leo badala yake kupata wachumi wakatoa ushauri wao na kukaa na Serikali, leo wachumi mnawapeleka kuzoa taka mkiwapiga picha na wheelbarrow Mheshimiwa Mwenyekiti, Wachumi wa kuisaidia nchi hii mnawapiga picha wakizoa taka na ma-wheel barrow! What? Tutakwenda wapi? Wachumi wetu tunawageuza vituko tukitegemea nchi itakwenda mbele! Hasara yao. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie lile Shirika la TEMDO. TEMDO ile taasisi imeanzishwa kwa ajili ya kusaidia uvumbuzi wa viwanda vidogovidogo na mashine ambazo zinaweza kuwasaidia Watanzania kuanzia wa viwango vya chini kabisa, lakini cha kusikitisha Mheshimiwa Serikali imeanzisha taasisi ile kwa kujua umuhimu na faida zake, lakini taasisi ile imetupwa kama yatima. Wamekuwa wakilazimisha waonekane wapo kwa kutenda mambo ambayo hata Serikali haiwasaidii hata senti tano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunafanyaje? tunaanzisha kitu kwa nia ya kusaidia Taifa, lakini leo mnakitelekeza mnakifanya yatima! Matatizo ni yapi, hakuna kinachofanyika pale wakati wana uwezo mkubwa wa kusaidia kama vile viwanda amesema mwenzangu, viwanda vidogo-vidogo vya soksi, viwanda vya juice, viwanda vya kuteketeza taka kwenye mahospitali, ni watu ambao wana ujuzi mkubwa na wamesomeshwa na Taifa hili, lakini badala yake wametelekezwa. Naomba Mheshimiwa Waziri waiangalie hii taasisi, hakuna nchi zilizoendelea bila kuwa na taasisi za uvumbuzi kama hizi, taasisi za utafiti kama hizi ambazo zinaweza kusaidia nchi zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii itakuwa ni nchi ya ajabu sana kwamba, leo tunapozungumzia suala la uimarishaji wa viwanda, lakini wawekezaji wanapotoka nje ya nchi kuja hapa kutaka kuwezeshwa kuwekeza katika maeneo wanapata usumbufu sana kuanzia kwenye ardhi na watu wa NEMC wanakuwa ni vikwazo vikubwa vya uwekezaji katika nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uko ushahidi wamekuja wawekezaji hapa, Mwekezaji anatumia mpaka mwaka mmoja kuhangaikia vibali vya kuweza kuwekeza miradi ambayo italeta tija kwa nchi hii, italeta ajira kwa nchi hii. Wako wawekezaji wamekuja na wamehangaika mwisho wameondoka kwa kuona kwamba sisi ni Taifa ambalo hatuko tayari. Hawakufanya kosa Rais Museveni na mwenzie Rais Kagame siku zile walipoamua wakasema katika East Africa kuna nchi zilizo tayari kimaendeleo na kuna nchi kama Tanzania tuziache kwa sababu wao hawako tayari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri, kwanza tuwe tayari kusikiliza ushauri unaotolewa na Waheshimiwa Wabunge. Pili, tuwe tayari kumshauri na kumwambia ukweli Mtukufu Rais kwamba, hali halisi ilivyo ni hii. Yule tunatakiwa ni Rais wetu tumheshimu na nawaahidi watu wa CCM tunamheshimu Rais Magufuli, lakini niwaambie hatutamwogopa katika kumwambia ukweli utakaosaidia kulijenga Taifa hili. Tutamheshimu ni Rais wa Tanzania, ni Rais wetu, lakini muwe tayari kumweleza ukweli, mnapoendelea kumfichaficha hamumsaidii! Mficha maradhi kifo humuumbua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wa Tanzania ukikua kwa kumshauri na kumwambia ukweli Rais, sifa na maendeleo ya nchi yetu ndio itakayotufanya sisi tujione ni Wabunge bora ni Mawaziri bora ni Serikali bora, lakini kuendelea kuona kila mmoja aah! Bwana mkubwa hafikiki! Itatuletea dhara na sisi tunawaambia haya, kama sisi tungekuwa na nia mbaya sana na Chama cha Mapinduzi tusingeyasema haya, tungekaa tu kwa sababu tunajua mnaharibikiwa. Watanzania sasa hivi wote wanalia hali ilivyo! Watanzania walikuwa hawajawahi kulia kwa ukosefu wa dawa katika nchi hii, mara hii mnasikia kilio!
Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto wetu wanalia na mabegi barabarani wanarudishwa makwao hawana pesa katika mikopo! Leo huduma nyingine zote zimedorora, lakini akishuka hapa Mheshimiwa Waziri wa Fedha atasema uchumi wetu umekua! Uchumi umekua mabenki yanaeleza kabisa, draft imetolewa mabenki yote yame-collapse! Hasara tupu ambayo ipo katika nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tuwe pamoja katika hili, tumshauri Mheshimiwa Rais Magufuli. Mtukufu Rais sio Mungu ni mwanadamu akiambiwa atasikia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuwa mchangiaji wa mwanzo jioni hii. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kunijalia kusimama hapa yote hii ni rehema zake na wala sio lingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze mchango wangu kwanza kwa kusema ninashukuru kwa bajeti tuliyoletewa hapa na kwa sababu kuna mengi ya kuzungumza nataka kutoa na mimi mawazo yangu kama yataonekana ya maana naomba Mheshimiwa Waziri uyazingatie. Katika bajeti hii limezungumzwa sana na katika Bunge hili na awamu hii na Serikali yetu tumezungumza sana habari ya viwanda. Mimi nataka nikupe maeneo matatu ambayo binafsi nahisi kwamba tukienda sawa tunaweza kupiga hatua kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu tumekuwa tukizungumza habari ya kiwanda cha General Tyre, Arusha. Lakini cha kusikitisha ni kwamba tunaishia kwenye kuzungumza. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Viwanda na Biashara. Binafsi tumefanya ziara kule siyo chini ya mara tatu kwa kuona umuhimu wa kiwanda kile kufufuliwa. Sote tumefika hapa kwa kutumia gari na ili gari lizunguke au litembee lazima litumie tairi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda kile kingefufuliwa yale matairi, magari ya Serikali na mashirika ya umma tu wakawa yanatumia matairi yanayozalishwa na General Tyre ingekuwa tayari ni soko moja kubwa. Lakini kwa bahati mbaya sana imekuwa ni hadithi, hakuna utekelezaji katika jambo hili. Naomba sana leo hii ukichukulia idadi ya tairi za piki piki zinavyotumika nchi hii, tena tairi kutoka China sizizo na viwango, ajali sizizo na msingi zinatokea, magari yanapata ajali kwa matairi ambayo yanaingizwa, kwa hiyo, soko la matairi ndani ya nchi hii, wacha kiwanda cha General Tyre hata vikizaliwa vitatu bado Tanzania tuna demand kubwa ya matairi, hebu fikirieni hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nataka nizungumzie kuhusu Kiwanda cha Tanga Fresh. Kiwanda cha Tanga Fresh kimekuwa kikiandamwa na majanga mara kwa mara nilimsikia Mheshimiwa Kitandula akizungumzia kuhusu vikwanzo ambavyo wanavipata, Waheshimiwa wale wa Kiwanda cha Tanga wameshindwa hata kupata mikopo ya benki kwa sababu eti kuna waliowauzia majengo yale kwamba TRA wanawadai wale wahusika. Anayedaiwa siyo wanunuzi, wanaodaiwa ni waliouza. Leo iweje kiwanda kile kinakuwa kila siku kiko ndani ya taabu. Mkumbuke kiwanda cha Tanga ni tegemeo kubwa sana kwa watu wa Tanga, wafugaji wa Tanga wanakitegemea kiwanda kile kwa kiasi kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba kimetoka kwenye mdomo wa FCC wakikishutumu kwa muda mrefu sana kuhusu kukiuka kwa baadhi ya mambo kikawa kiko ndani ya matatizo, wamekuja sijui ni TBS sasa hivi wamekuja TRA.

Mheshimiwa Waziri unajua kwenye meza yako iko barua ya kiwanda kile kutaka kusaidiwa kufanya kazi zake kwa uzuri, tuvilee viwanda vyetu. Naelewa kwamba kuna viwanda vya Kenya, Brooklyne ambao hawapendi kuona Tanga Fresh ni washindani wao wakubwa. Leo Tanzania tuna kiwanda cha Tanga Fresh na Asas ndiyo viwanda vikubwa vya maziwa. Lazima tuvilee, uzalendo uanzia hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie A - Z na mnaelewa kuna tatizo gani. Kuhusu rate yao ile ambayo wamewekewa. Nawaomba sana Malaria ni janga la kitaifa na lazima tulikuwa kwenye semina pamoja na Naibu Waziri alisikia malalamiko ya kiwanda kile ambayo ina hatarisha kwenda kufungwa na kupunguza idadi kubwa ya wafanyakazi katika kiwanda kile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani michango hiyo mitatu kwenye kusaidia bajeti yetu inatosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie kauli ambazo zimekuwa zikitawala sana kuhusu makanikia. Kiongozi mwenza wa UKAWA Mheshimiwa Francis Mbatia aliongea kwamba katika sisi hakuna anayepinga jitihada za kunusuru mali za Taifa hili. Kama limesemwa hilo na Mwenyekiti wetu na hakuna aliyempinga maana yake ni kwamba hayo ndiyo mawazo yetu. Wasijitokeze wengine wakatulisha maneno kuonekana kwa Watanzania kana kwamba tunapinga juhudi za kulinda mali zetu. Hiyo ndiyo ajenda yetu siku zote na tumekuwa tukiwaambia hivyo. Lakini kwa sababu yalitoka upande huu mliyaona siyo. Sasa mme-prove ndiyo twendeni mbele, tusiangalie nyuma tena, tuko pamoja katika hili la kulinda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jamani kila mtu ana-style yake ya kulipokea jambo. Wenzetu mnakimbilia sana sherehe celebrate festivals. Sisi kwanza tunapima upepo kuona mambo yanaendaje.

Waheshimiwa Wabunge niwape mfano, Bunge la Katiba mlisherehekea sana. Wengine wakakata viuno humu ndani lakini Katiba iko wapi mpaka leo. Hamkutosheka mkaenda jamhuri mkacheza na mkaimba, Katiba iko wapi mpaka leo. Kwa hiyo, si hoja awali, ni heri hatima. Hayo sisi wengine tunaota ndoto kubwa kwa pesa zile zilizotajwa tunatamani yatokee na Tanzania inufaike na yale yaliyozungumzwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme tunapozungumza haya wengine mnatupa majina mabaya. Yuko Mbunge mmoja kule alinyanyuka akatuita sisi UNITA akamfananisha Kiongozi wetu na Savimbi. Lakini nawaonya wanasiasa wenzangu, majina mabaya tusiitane kiasi hicho, kwa sababu leo upo huko inaweza ika-change ring ukaja huku. Wako viongozi wakubwa walikuweko huko leo tunao huku na wako wengine tulikuwa nao huku leo wako huko. Haya ni mambo ya mbadilishano tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mtu anatuita sisi UNITA, lakini mimi nakumbuka Bunge la Katiba alikuwemo Mheshimiwa mmoja anaitwa Ibrahimu Lipumba aliwaita ninyi Intarahamwe. Leo Intarahamwe katafute Intarahamwe mwenzio wamekwenda kukaa nao. Ni suala la muda la muda tu kwa sababu anakamilisha kazi aliyopewa ni rasmi tu atakuwa Mkuu wa Mkoa, atakuwa Mkuu Msaidizi wa Gavana tunayaelewa hayo. Tunamwombea safari njema. Akamilishe kazi yake aliyotumwa arudi akaye na Intarahamwe wenziwe. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie kuhusu misaada ya wahisani. Hili nisingetaka kulizungumza kwa sababu ninapozungumza wahisani nitaigusa Zanzibar na nikigusa Zanzibar nitagusa uchaguzi wa Zanzibar na najua kuna watu hawataki nizungumze uchanguzi wa Zanzibar, lakini hili haliepukiki. Mwanzo nilisema Uchaguzi wa Zanzibar ni chozi la mbwa mmelikosea kulinywa moto, halitaweza kunyweka tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme hivi, kwenye bajeti yako hii asilimia 12.5 umetegemea fedha za wahisani. Fedha za wahisani kwenye bajeti iliyopita unatuambia haikutoka na ndiyo ukweli. Leo umerudi umeandika tena humu kwamba unategemea asilimia 12.5 ni fedha za wahisani. Wahisani wamegoma kutoa pesa na sababu mnaijua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchaguzi uliofanyika Zanzibar na Sheria ya Mtandao yanainyima nchi hii fursa ya kupata fedha zile za kuisaidia bajeti. Nisingeshughulika sana kama ingekuwa ni pesa ambayo haimo kwenye bajeti ningeacha kusema hilo. Hasa mimi nawashauri Wahisani wanaozuia kutoa pesa zile wazungumza na ninyi lakini ninyi mnashindwa kufika point. Mnashindwa kufikia makubaliano nawaomba sana, fursa hii wa sababu ya kumlinda Daktari Mohamed Ali Shein.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limeshafutika hilo halipo. Ahsante sana nawaambia Waziri wa Mambo ya Nje anajua masuala anayokumbana nayo
msaidieni. Kubalini na eleweni nini kimetokea. Uchaguzi ulifanyika tarehe 25 Oktoba, ndiyo huu uliomuweka Rais John Magufuli madarakani tunamtambua, wala hatupingi kwa hilo, lakini uchaguzi mwingine ule, uchaguzi wa Zanzibar umefanyika matokeo ndiyo yametuweka sisi Wabunge humu. Eti chakula kimepikwa jungu moja wa chini umeiva wa juu haukuiva mmeyaona wapi. Haya ni maajabu ya dunia, uchaguzi uliisha na matokeo wahisani yote wanayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dunia ilikuwa inaangazia uchaguzi wetu na waliona, leo Mheshimiwa Jecha maana afadhali ingekuwa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ilifuta uchaguzi ule, lakini Tume ya Uchaguzi haikufuta, Jecha alitoka pale akaenda akakaa kwake sijui siku hiyo aliwekewa kikuba gani na mkewe akakinusa akaenda chafya, akafuta uchaguzi wa Zanzibar. Huu ni upumbavu ambao unatutesa ndani ya nchi. Unatutesa kwa sababu sisi tunaumia sana. Nchi hii inayo bajeti yetu ni high jump, hatukufikia asilimia 29 tumeweka 30 na leo mchezo wa high jump mrukaji anaanzia chini kwenda juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya mara hii ya Mheshimiwa Mpango sasa pale alipokuwa hakufika kapandisha ule mti juu zaidi ili aruke, sasa sijui maajabu ambayo yatatumika. Sielewi maajabu gani yatatumika, mimi nakuombea dua sana. Lakini nakuomba kaaeni mtafakati suala la Zanzibar dunia inatuangalia. Suala la mitandao dunia inawangalia, tumalizeni tufaidike, za makanikia bado zina muda. Mimi yalaiti ingekuwa zile za makilikia zinatoka katika kipindi hiki ningesema tuwaache Wazanzibar waendelee wanavyokwenda, maamuzi yao yadharauliwe. Lakini kwa sababu ya tunategemea wahisani lazima muukubali ukweli hata kama ni mchungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yuko mwanafalsafa mmoja alisema usiyempenda akisema maneno mazuri yakubali, na unayempenda anaposema mabaya uyachukie.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie katika hoja iliyoko mbele yetu inayohusu Muungano na mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda nami kwanza kumwomba Mwenyezi Mungu atujaalie Wabunge na Viongozi wetu afya njema na wale ambao afya zao zimetetereka miongoni mwao hata mimi, tujiombee Mungu atupe uzima ili tuweze kulijenga Taifa hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti namwombea kwa dhati tu Mheshimiwa Magufuli kama anavyopenda kusema tumwombee na mimi namwombea. Pia, namwombea kipenzi cha Wazanzibari, Mheshimiwa Seif Sharrif Hamad
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mungu ampe afya njema na nawaombea hao wengine walioko huko pia Mungu awajaalie afya njema ili tutakapochukua madaraka halali Zanzibar waone namna tunavyoendesha nchi Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye maombi yangu niweke upande wa pili. Pamoja na kwamba tumejiombea dua tupate uzima, lakini ikiwa Mwenyezi Mungu mwenyewe aliowajaalia maradhi ni kwa ajili ya dua zetu tulizoomba wale tuliodhulumiwa, Mwenyezi Mungu awaongezee maradufu maradhi hayo, ili wajue kama Mwenyezi Mungu yuko na Mwenyezi Mungu ndiye mwenye uwezo wa kutenda kila jambo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nianze kuchangia kwa kushukuru kuniweka mtu wa tatu na kulishukuru Bunge lako leo kutupanga wa upande huu tuwe wa mwanzo kuchangia, hii ina maana kubwa, hata Rais anapolihutubia Bunge hupewa yeye nafasi kwanza halafu sisi tukaja mwisho kuchangia. Kwa hivyo, leo wale mliowaweka badala yangu wote, najua hawana la kusema watalisema baada ya nitakayoyasema mimi, kaeni wanafunzi mjifunze. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema juzi Mwanasheria Mkuu wa Serikali wakati anatoa mchango wake hapa alijinasibu sana na akasema mengi sana kuhusu uhalali wa kilichofanyika 20/3/2016 Zanzibar. Wanasema wajuzi wa mambo uongo unapoendelea kusemwa na usipokanushwa unaonekana ukweli. Bahati mbaya sana hayupo nilitaka niyaseme haya akiwepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar, Kifungu cha 71 na Kifungu cha 72 ambacho kwa kuokoa muda nitasoma Kifungu cha 72. Kinasema hivi: “Mahakama Kuu ya Zanzibar ndiyo pekee yenye mamlaka na uwezo wa kusikiliza na kuamua mashauri yote yanayohusiana na uchaguzi wa Zanzibar.” Hicho ni kifungu.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiona wanawashwa ujue sindano inawapata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanaosema hata sisi hatukwenda Mahakamani, lakini Tume ya Uchaguzi ilitakiwa izingatie Kifungu hiki. Kwa hivyo, tunachosema hapa ni kwamba, uchaguzi wa Zanzibar uliofanyika mara ya pili ulikuwa ni uchaguzi wa haramu na umewapa madaraka ambao haukustahiki kuwepo, maana yetu ni Katiba hii. Sasa kama Katiba hii hamuikubali na Katiba hii ndiyo alioapia Rais wa Zanzibar na ndiye muapaji wa kwanza kushika Katiba hii, maana yake ni kwamba Katiba hii ni haramu hata kuishika. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yamesemwa na tutaendelea kusema kwamba mnadhani limekwisha lakini ninalowaambia halijakwisha, la Zanzibar halijapita! Lipo na litaendelea kuwepo. Mambo ya Zanzibar ni wale wanaosema ni sawa na mchuzi wa mbwa, ukiukosa kuunywa wa moto ukipoa haunyweki tena! Utakuwa ni uvundo na subirini soon uvundo wa mambo ya Zanzibar mtaanza kuuona. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru katika Mkutano wa 15, Bunge la mwaka 2010, Bunge lililopita, nilinyanyuka hapa nikasema kwamba hakuna haja kusheherekea na kutumia mabilioni ya Tanzania kwa ajili ya sherehe za Muungano, nilisema hapa ndani, mwenye kukariri Hansard iko aende akatafute najua nilisema mimi. Nilisema tunapoteza pesa nyingi kusheherekea kitu kisicho na maana yoyote. Muungano wa Tanganyika na Zanzibar Mheshimiwa Waziri uliouremba na kuupaka kila aina ya poda, lipstick, manukato au udi, hakuna kitu!
Muungano wa Zanzibar na Tanganyika tuliungana kwa madhumuni makubwa ya kusaidiana kiuchumi, kudumisha amani na kuleta maendeleo ya nchi zetu hizi. Leo kama nchi hizi zimekuwa ni katika mstari wa mwisho kwa umaskini duniani mnajivunia nini na Muungano huu? Kipi cha kujivunia? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naona aibu sana kwamba Muungano huu umekuwa ni silaha tu ya kukidhi matakwa ya watawala kuendelea kuitawala Zanzibar kimabavu, hili ndilo lililoko! Nataka nikuhakikishie, Wazanzibari wamefikia mahali pamoja na unyonge wao, lakini siku ya hukumu tunaiandaa kwa ajili ya wote wanaodhulumu haki za Wazanzibari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ilikuwa ni nchi ya mstari wa mbele katika ukombozi wa nchi za Kusini mwa Afrika, lakini Tanzania hiyo leo imekuwa ni nchi ya mwanzo inayokandamiza washirika wa Muungano wa Zanzibar na watu wake. Hili halikubaliki, lakini tunakokwenda siyo kuzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mnajifariji hapa kwa kuona kwamba sisi hatuna uwezo wa silaha lakini tuna silaha kubwa kuliko zenu ninyi na silaha yetu ni umoja wetu na Wanzazibari kwa umoja wetu tumekubali kufanya mabadiliko ili kuviondoa visiwa hivi pale vilipo viende mbele pamoja na wale wasakatonge wenu mliowaweka Zanzibar ambao wanakuja hapa wakitetea matumbo yao na siyo kutetea maslahi ya Wazanzibari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ni aibu gani wakati Marekani wanafikiria kuondoa gereza la Guantanamo bay kule Cuba, leo Watanganyika mmeligeuza gereza la Seregea kuwa Guantanamo bay ya Wazanzibari. Mmewachukua Masheikh wa Zanzibar ndani ya miaka mitatu wako hapa kesi zao hata ushahidi tembe moja hamjapeleka wa kuthibitisha ugaidi wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Brussels pametokea ugaidi juzi, wamekufa watu within one week, yule mwanamme mmoja ameachiwa huru kwa kusema hakuna ushahidi unaoonesha alihusika vipi na ugaidi wa pale. Leo ninyi hata aibu wala haya hamna, wanazuoni wa Zanzibar three years mnawanyima kukaa na watoto wao na wake zao, mmewaweka wake wajane ilhali waume zao wako, mmewaweka watoto mayatima ilhali baba zao wako. Haki gani, Muungano gani? Alaysa-Allah biahkami lhakimina hakika Mwenyezi Mungu atalipa juu ya udhalimu wote mnaowafanyia watu wa Zanzibar. Hatuna nguvu za vifaru, lakini nguvu zetu ni umoja wetu na iko siku Mwenyezi Mungu atatusikia kilio chetu cha kuona haki iko wapi mtaifuata mtake msitake! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niseme wazi msimamo wetu wa kutoitambua Serikali ya Zanzibar. Wako wengine wanasema hapa kwamba, kama hamuitambui Zanzibar mbona mmekuja hapa? Katika busara ya kawaida unapokwenda porini ukakutana mbwa mwitu utafanya vyovyote ujinasue na mbwa mwitu, lakini ukitembea mtaani ukakutana na mbwa anakubwekea na mwenye mbwa unamuona yaani mfugaji wake, huna haja ya kuparuana naye, mtafute mwenye mbwa u-deal naye.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Utaweza kumwambia mwenye mbwa, kwa hivyo tunajua kwamba Zanzibar mpiga filimbi wake yuko hapa na tunajitahidi kusema….
MWENYEKITI: Muda wako kwanza umekwisha;
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuwa mchangiaji wa mwanzo jioni yetu ya leo hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uhai wake nikaweza kusimama hapa na mimi kutoa mawazo yangu haya ambayo nitayatoa. Kabla ya yote nielezee tu kuridhika kwangu kwa jinsi unavyolisimamia vizuri Bunge hili. Kwa kweli shukrani sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanza kabisa mimi leo nataka nianze na jambo moja ambalo ni kuhusu maswali tunayoleta Wabunge hapa Bungeni. Leo nataka nitumie fursa yangu hii ili kupitia Waziri husika anijibu maswali ambayo kuanzia Bunge la Kumi nikiwa Mbunge niliyapeleka kwenye Ofisi ya Maswali Bungeni sikupata majibu na katika Bunge hili tumekuwa na miaka miwili na nusu maswali hayo pia hayajajibiwa na mpaka sasa tamaa inakuwa ni ndogo. Hivyo naona ni bora nitumie fursa ya muda wangu huu wa kuchangia ili ikimpendeza na nimuombe Mheshimiwa Waziri wakati wa winding up ili anipe majibu ya mambo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimewahi kuuliza swali hili na najua liko katika meza ya maswali, Serikali yetu inatumia vigezo gani kuitambua BAKWATA kuwa ndiyo chombo kikuu cha kuwasemea na chenye mamlaka ya uislamu wa Tanzania. Niliuliza hili swali, Serikali inatumia sheria ipi ili kuitambua BAKWATA kwamba ndiyo Baraza Kuu la Waislamu Tanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliuliza hili kwa kutambua kwamba Tanzania haina dini na waasisi wa Taifa letu waliweka hilo wazi ili kuepuka mambo makubwa yanayohusu kuingiliana mambo ya dini na kiutendaji wa Serikali. Niliuliza hili kwa sababu waislamu tuna taasisi nyingi kama zilivyo dini zingine. Kuna taasisi nyingi ambazo kwa mujibu wa sheria yetu ya kiislamu ambayo Serikali si juu yake kuingilia utendaji wetu waislamu, kila muislamu ana maamuzi kwa taasisi na Jumuiya anayoiona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kusikitisha sana, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kuitambua BAKWATA na kuipa mamlaka makubwa ikiwemo kusimamia hija za waislamu jambo ambalo si haki! Ikiendelea kusimamia mashtaka ya waislamu jambo ambalo pia si haki! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu madhehebu haya yanatofautiana na ni jukumu la Waislamu kujiamulia madhehebu wanayoyataka niliuliza hili ili Serikali ituweke wazi, kwanini mmetambua BAKWATA pekee kama ndiyo chombo kikuu cha waislamu Tanzania jambo ambalo haliko kwenye kitabu chetu kitukufu cha Qurani, Qurani haitambui BAKWATA, Qurani haitambui uamsho, Qurani inatambua waislamu na imani yao ya kiislamu. Haya maamuzi tumeyafanya wenyewe waislamu. Kama ambavyo wakristo wana taasisi zao wanazozitambua, haifai kwa Serikali kujiingiza kuitambua BAKWATA. BAKWATA iwaachie waislamu wafanye maamuzi kwa jumuiya. Kwa hivyo natoa wito kwa Serikali kuanzia sasa iache kuitambua BAKWATA kama ndiyo Baraza Kuu la Waislamu Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema hilo sikujua kama siku moja hata Bunge letu litaingia kwenye mtego. Leo Bunge limewakaribisha BAKWATA kuweka mkutano wa mambo ya kiislamu ndani ya ukumbi wa Bunge hili, jambo ambalo leo hii kila taasisi ikitaka kupewa nafasi hiyo kwa sababu mmeanza kwa BAKWATA itakuwa tatizo, wengine hamtawapa. Kuna Wapentekoste watataka waje mle, Walokole, Walutheri, ndiyo kwa sababu mmeanza njia mbaya! Kuna Uamsho, ni jumuiya halali na mpaka leo nadhani ina usajili watataka kuja humu, kuna mabaniani wanaabudu ng’ombe wataingia na ng’ombe humu ndani waabudi baa baa! Mko tayari? Haya ni mambo ya kuyaangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili niliuliza, Serikali wakati walipomtaka Komandoo Salmin Amour ajitoe katika uhusiano wa Jumuiya ya Kiislamu (OIC) ilitoa ahadi kwa Watanzania Serikali ya Jamhuri itaangalia namna bora ya kujiunga ili jambo hili liwe la Kimuungano, Jumuiya ya Kiislamu OIC. Ahadi hiyo watu wanaitambua na wawakilishi wao wanatukumbusha tuijulishe Serikali. Kama limewashinda bado Zanzibar kwa maslahi ya kiuchumi, sio ya kidini tunaomba Serikali ya Jamhuri ya Muungano iachie Zanzibar ijiunge na Jumuiya hii kwa maslahi ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la tatu nililouliza ambalo sikupatiwa jibu. Niliuliza hivi; kulikuwa na utaratibu ambao sio wa kisheria lakini ulikuwa ni utamaduni mzuri. Viongozi wa Mataifa ya nje wanapokuja Tanzania wanapewa nafasi ya kuzuru Zanzibar na sisi Zanzibar tulikuwa tunapata nafasi ya viongozi wetu kuwaambia baadhi ya mambo yetu. Utamaduni huu umeondoka, mtuambie ni kwa nini. Hayo matatu ni maswali ambayo sikupata majibu 2010, naomba leo Mheshimiwa Waziri unijibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia suala la vikao vya Makamu wa Rais vinavyohusu kero ya Muungano. Nasikitika sana, kama kuna mambo ambayo nadhani kwa maoni yangu ni mambo ya aibu ni Wanamuungano wa Tanganyika na Zanzibar kukaa Makamu wa Rais na baadhi ya Mawaziri kujadili kero ambazo siku zote hazipatiwi muafaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hapa tumeshuhudia, Mheshimiwa Yussuf akizungumzia kuhusu sukari ya Zanzibar kuzuiwa kuingia Tanzania Bara. Suala hili limezungumzwa kwenye Baraza la Wawakilishi Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili wamekuja Mawaziri wamekaa na Mawaziri wenzao wa Bara na suala hili wawakilishi wa wananchi tumepewa tulisemee humu. Kwa hivyo, inapoonekana tunaposemea mambo ya Zanzibar wenzetu inawauma inabidi mvumilie sana kwa sababu kila kitu kina gharama zake. Leo nisingejibu hili lakini nimesikitishwa sana na Naibu Waziri wa Muungano kusimama na akajibu kwamba sukari ya Zanzibar haiwatoshi wenyewe Wanzanzibari, ni kidogo, iweje iletwe huku, jamani! Ni vingi vidogo Zanzibar lakini wananchi wa Bara mwavitumia! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, viko vingi vidogo, hata humu Bungeni vimo vidogo vingi, lakini tunavitumia na wala hakuna ubaya ndugu zetu wa damu, wajomba kuvitumia vya Zanzibar kama sisi ambavyo hakuna ubaya kuvitumia vya Bara. Leo ajabu kubwa eti sukari ya Zanzibar inakuwa ni aibu kuingia Bara. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, leo hii Mheshimiwa Yussuf amesema pamba ya Tanzania haitoshi kutengeneza nguo lakini wazalishaji wa pamba wanaruhusiwa kuuza nje wakati tunaaagizia mitumba kuingia Tanzania, aibu iko wapi? Hapa linaloangaliwa na Mheshimiwa Yussuf amemuambia Naibu Waziri, tunazungumza biashara! Leo kiwanda kile kwa udogo wake na idadi ndogo inayozalisha mkikipa fursa ya kufaidi soko la Tanzania Bara kitajipanua na kuongeza ajira kwa Zanzibar. Ninyi kosa lenu mkiiona Zanzibar inaendelea, tatizo lenu nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali jana kupitia Waziri Mahiga alisema Zanzibar inafaidika na Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa kufaidika kuuza mazao yao katika Soko la Afrika Mashariki. Afrika Mashariki ipi tutaifikia ikiwa daraja la mwanzo ni Tanganyika hamtaki tuguse? Hebu niambieni, tutafika vipi Afrika Mashariki wakati ndugu zetu wa damu mnakataza bidhaa ya Zanzibar kuingia ndani ya Tanganyika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zetu wa damu ikitokea Tanzania ina vita, juzi tumepokea majeneza ya askari waliokufa kuiteteta heshima ya Taifa letu. Kati yao ilikuwa nusu kwa nusu tumepokea Zanzibar. Mimi binafsi akiwemo mmoja ndugu yangu wa damu. Tumepokea kwa kutetea maslahi ya Tanganyika na Zanzibar. Tanzania tunakuwa pamoja katika maumivu lakini katika kula mnatutupa, huu ni Muungano wa aina gani? Leo tukienda kutetea maslahi na heshima ya Taifa hili Wanzanzibari tunakufa pamoja na ninyi, lakini tukirudi hapa Mzanzibari kuchukua packet za sukari kuleta hapa mnasema tunatafuta njia ya kuleta magendo. Mnaidhalilisha Serikali ya Zanzibar kwamba Serikali nzima ya Zanzibar ni Serikali haramu inayofanya magendo. Hili jambo hatuwezi kukubali, binafsi kwa imani yangu simtambui Rais wa Zanzibar kama ni Rais halali, lakini natambua maslahi yanayokwenda Zanzibar kwa sababu yanasaidia wananchi wote wa Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani maziwa ya Zanzibar mmeyawekea vikwazo, maji ya Drop kutoka Zanzibar mmeyawekea vikwazo, kila kitu. Tulikuwa na Kiwanda cha Sigara Zanzibar mmekiua kwa vikwazo, leo mnaitakia nini Zanzibar? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwenyezi Mungu katika Qurani tukufu kuna sura inaitwa Suratul-Falaq amezungumzia namna ya uhasidi. Husda mbaya, kisiwa cha Zanzibar mnakiangalia kwa husda, haifai sisi ni ndugu wa damu. Leo hii hasidi huhusudi hata yule maiti kwa sanda aliyozikwa nayo. Hukaa akamwangalia; “hee, sanda yote nyeupe anazikwa nayo huyu” hasidi itamfaa nini sanda maiti na anazikwa? Inamfidia nini ndugu yangu? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu rekebisheni, tafadhalini, Muungano huu ni tunu ya Taifa letu, lakini niwaambieni tena kwamba kile kidogo cha Zanzibar mkiruhusu kifaidi soko la Afrika Mashariki, kifaidi soko la Tanzania Bara, vilindeni mna vyombo vya dola mna Polisi, mna TRA zote zilizoko Zanzibar ni za Muungano, msituambie sababu kwamba italetwa kwa magendo wakati mnajua mna vyombo vyote vinavyosimamia ni vyombo vya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kama Kiwanda cha Zanzibar kinazalisha packet 10,000 waacheni wafaidi soko la huku hata wanywaji wa Zanzibar hawafiki 1,000 lakini bia ya Tanganyika inawalewesha Wazanzibari. Wazanzibari hawana Kiwanda cha Bia, wakianguka kwa ulevi ni bia mliyotengeneza ninyi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo soko la nyanya limekuwa kubwa. Mwaka jana nyanya zilikuwa zinaliwa na ng’ombe. Mwaka huu sasa hivi kilo ya nyanya Zanzibar inafika shilingi 4,000. Mkulima wa Dumila hamuwezi kumzuia asipeleke Zanzibar kwa sababu hapa kwetu hazijatosha. Kwa nini iwe Zanzibar? Tunasema haya yanayofanyika siyo halali na sisi Wapinzani ndiyo tunaimarisha Muungano na ninyi wa Chama cha Mapinduzi kwa matendo yenu haya, uhasidi huu, hamuusaidii Muungano wetu. Tafadhalini sana msimchore Makamu wa Rais.

Mheshimiwa Naibu Waziri wewe unafaa kuadhibiwa leo, kwa sababu kumbe ulijua haliwezekani kwanini unamuacha Makamu wa Rais anakaa vikao kujadili jambo ambalo wewe jibu unalo? Why? It’s a shame for you Mheshimiwa Naibu Waziri, ungemuambia Makamu wa Rais kwenye vikao vyenu vya cabinet kwamba hili unalotaka kulisimamia Makamu wa Rais ni jambo lisilowezekana, akaacha kuhangaika Mama wa watu tunamheshimu sana Mheshimiwa Samia, kwa nini? It’s a shame for all CCM. Kwaherini.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi kuwa mchangiaji wa mwanzo jioni ya leo. Naomba Mwenyezi Mungu aniongoze niseme yale yenye busara kwa nia njema ya kuimarisha amani na usalama wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nataka nizungumzie kwenye ukurasa 46 wa hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri inayozungumzia usajili wa vyama vya kijamii na vyama vya kidini. Tunajua kwamba vyama na taasisi zote vinavyosajiliwa kwa mujibu wa sheria ya nchi hii vinakuwa ni vyama ambavyo vinatakiwa kufuata sheria ambazo zinawekwa chini ya usajili wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kidogo hapa niseme kwamba Serikali iwe makini sana hususan na taasisi za kidini, nimeona Mheshimiwa Waziri ameeleza kama kuna baadhi ya taasisi ambazo hawakuzipa usajili na naamini kwamba waliangalia sababu na wakajiridhisha kwamba hazifai kupewa usajili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu hapa ni kwamba, usajili wa taasisi za kidini lazima uendane na masharti kwa sababu nchi yetu haina dini; lakini Watanzania wana dini zao. Nasema hili nikirejea hoja yangu wakati wa hotuba ya Waziri Mkuu Mheshimiwa maneno ya mwanzo ambalo ni suala linanipa shida sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge ni wawakilishi wa wananchi. Si kwamba Mbunge anaposimama hapa anakuwa na yake tu, sometime anakuwa na mawazo yake lakini wakati mwingine anawakilisha. Mimi ni Muislam na naelewa tatizo lililopo sasa hivi. Tatizo ambalo nataka kulisemea ni kwamba taasisi za kidini zote zinapopata usajili wa aina moja lazima isiwepo taasisi ikajiona leo taasisi hiyo ni kubwa kuliko nyingine. Hilo kosa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hili kwa kutambua, kwa mfano sisi Waislam tuna taasisi nyingi na narudia kusema hivyo. Siku ya mwanzo niliyosema nashukuru Mheshimiwa Waziri alinijibu moja kati ya mawili la kusema kwamba hakuna tatizo kwa taasisi zozote kutumia ukumbi wa Bunge. Limeondoa masuala katika jamii kwa sababu lile jambo lililotendeka baadhi ya wananchi wengi walidhani ni jambo geni sana kwa Bakwata kufanya mkutano humu ndani, lakini baada ya ufafanuzi ule wananchi wametulia na wameridhika kwamba taasisi yoyote inaweza kuja na kufuata masharti na ikafanya vikao ndani ya Bunge, hakuna tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hili la kuifanya BAKWATA kuendelea kuwa ni wasemaji wakuu wa Waislam Tanzania, hili kosa! Kwa sababu Bakwata haina usajili wa aina yake. Leo tumemsikia, niliuliza swali kwa Serikali, nilitegemea majibu nipate kwa Serikali, lakini bahati mbaya sana nasema kwamba wametokea Masheikh huko wamenijibu na mimi sijaisema BAKWATA kwa ubaya. Nataka sheria na haki iwepo sawa kwa taasisi zote isitokee moja ikajiona kwamba wao ni juu ya wengine, hilo ni kosa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna hivi leo usajili wa vilabu hivi vya michezo hata Simba akiwa bingwa mara 10 hana mamlaka juu ya vilabu vingine. Hiyo ni club iliyosajiliwa kwa sheria sawa na vilabu vingine hali kadhalika NGO’s na vitu vingine. Kwa hiyo, naiomba Serikali bado itoe majibu ni sheria gani wanayoitumia kuitambua BAKWATA kama ndiyo chombo kikuu cha Waislam Tanzania? Nitashukuru nikipata hilo majibu na sitarudia tena kulizungumza hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ninalotaka kuzungumzia ni hali ya usalama ndani ya nchi. Kwa masikitiko makubwa sana, Taifa hili ndiyo lililokuwa nchi ya mstari wa mbele katika ukombozi wa Bara la Afrika. Kitovu na ndiyo tuliowapa makambi wapigania uhuru wa nchi mbalimbali kupigania amani za nchi zao, kwa sababu hawakuridhika na mateso.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, Mwalimu Nyerere hakuridhika na unyama wa Makaburu uliokuwa unafanyika Afrika Kusini. Alikuwa anaumia sana kwa matendo wanayotendewa Waafrika ndani ya Afrika Kusini. Leo tuliwapigania sisi tunarudi kule ambako tulikuwa tukiwapigania wenzetu. Mauaji ya kiholela, utesaji usio na tija, utekaji wa hovyo hovyo ndani ya nchi, tayari umeshamiri na unashika kasi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vitu vya kusikitisha sana. Ukisikia leo tumelala tumeamka salama hatujasikia sehemu kumetokea tukio ni jambo la kumwomba Mungu. Juzi wiki tatu zilizopita Pemba wameenda kuchukuliwa vijana sita na watu na magari yao na taarifa imetolewa kwa Kamanda wa Polisi kwamba gari zilizokuja kuchukua watu hawa ni namba hizi na zikafuatiliwa mpaka mamlaka wa usajili wa vyombo vya moto na kuonekana gari zile ni za watu fulani. Sasa hebu niambieni mpaka leo hakuna hata gari moja wala mtu mmoja aliyekamatwa kuhusishwa na tukio lile, tunakwenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hilo tu! Pale Dar es Salaam lipo tukio lilitokea, mtu mmoja alienda akatekwa nyara, bahati wananchi pale Buguruni wakavamia gari wakalikamata, wakalipeleka kituo cha Polisi Buguruni na washtakiwa, lakini mpaka leo kesi hiyo haikwenda mahakamani na gari lile hatimaye liliachiwa, kwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayalea matukio haya, lakini madhara yake yatakuwa makubwa sana baadaye. Kwa sababu uvumilivu wa watu unaweza ukawaishia. Leo kuna watu wanao majina wakipatwa na tatizo nchi nzima inaelewa, lakini kuna watu hawana majina. Mfano, miezi miwili iliyopita pale Zanzibar ameenda kuchukuliwa Mzee wa watu anaitwa Ali Juma Suleiman. Mzee wa watu amechukuliwa na vyombo, magari yanayojulika na watu wanaojulika, wakaenda wakamchukua nyumbani kwake mbele ya watoto wake, wameenda kumpiga siku ya pili kufa hospitali, hakuna anayezungumza, hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taifa limekaa kimya kwa sababu aliyekufa pale ni mtu hana jina. Hapa akifa mwanasiasa au watu mwingine ndiyo kidogo unasikia. Sasa matukio kama yale yanaleta hasira ndani ya jamii, taasisi iliyopewa dhamana ya kusimamia usalama wetu, badala ya jeshi la polisi kuwa usalama wa raia leo unajeuka kuwa uhasama wa raia? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana suala la utekekaji wa kiholela unaoendelea, suala la matukito haya ya kuumiza watu kwa kweli sio masuala ya kibinadamu hayo ni masuala wanayofanya wanyama tena wale wanyama wanapokuwa na njaa ndio wanapokula mnyama mwenziwe. Sio katika hali ya kawaida, hawezi kufanya tukio kama hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi suala lingine niongelee suala la waendesha mashtaka. Juzi tumepata taarifa kama ndugu yetu Aquilina faili lake limefungwa kwamba limeishia limefungwa, kwa nini hatujui! Hata hivyo, upelelezi huu uliotumika haraka kufikia kufunga shauri la Aquilina kwa nini hauendi upelelezi huo katika mashtaka mengine mengi yaliyomo ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama wametumia si zaidi ya miezi miwili kujiridhisha kama ushahidi haupo na wameamua kufunga lile jalada, hebu waniambie ni kwa nini leo miaka mitano, Masheikh wa Uamsho kutoka Zanzibar wameshindwa kufunga faili hilo wakati wameshindwa kupata ushahidi. Hebu watuambie lililoko nyuma ya pazia. Kwa sababu ubinadamu hisia za utu lazima zitujie sana, sote ni wazazi, sote tuna baba tuna mama, tuna watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna yeyote kati yetu humu kama ni baba yake wala ni mama yake au ni ndugu yake angeridhika kuona watu wale miaka mitano wameshikiliwa pasipo mashtaka yao kufafanuliwa wakahukumiwa kwa ajili ya kesi zao, hakuna! Kati yetu mmojawapo angekuwa mtu yule anamhusu hakuna, hisia za ubinadamu na utanzania ziturudie. Tuangalieni mateso wanayopata familia za wale, wake wawili wa Wazee wale waliko gerezani tayari wameshafariki. Hawakuonana tena na wapendwa zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaswali kila asubuhi kumwomba Mungu atupe baraka, sisi tuliopewa madaraka kuongoza Watanzania je, tunatenda haki kwa tunaowaongoza ili tupate baraka ya Mwenyezi Mungu? Huwezi kumwomba Mungu akujalie baraka wakati wewe umepewa mamlaka lakini hutendi kwa baraka kwa watu unaowaongoza. Vipi Mwenyezi Mungu atalihurumia Taifa hili. Tuongoze kwa dhahabu Afrika, kwa mifugo, kwa makinikia na mengine lakini kama hatutendi haki kwa tunaowaongoza Mungu hatatujalia baraka katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, suala la kesi ya Masheikh ya Uamsho ni suala ambalo linatukera sana Watanzania na wapenda haki wote na naamini kwa ukimya huu hata Bunge hili hawafurahii tena kuona suala hili la Masheikh wale wanaendelea kushikiliwa katika kipindi kirefu namna hii haiwezekani. Leo ikiwa tukio la kufa mtu Aquilina limechukua miezi miwili, tukio la Masheikh wale waliodaiwa magaidi hajakufa hata kuku ndugu zangu Wabunge. Hata kuku hakuuliwa katika tukio lile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko mifano ya nchi zinazotokewa na matukio haya. Ubelgiji pale palitokea tukio la kutisha airport na wapo watu walishikwa ndani ya miezi mitatu vyombo vya upelelezi vilijiridhisha kama watu wale hawakuhusika na waliachiwa huru mara moja. Leo tumefikwa na nini Watanzania?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nataka kuwasemea ndugu zangu hawa wa Jeshi la Polisi, jambo la kuwapandisha vyeo hawa na wakashindwa kuwalipa stahili zao zinazolingana na vyeo vyao ni jambo linaloumiza sana. Leo askari anapanda miaka minne lakini bado marekebisho ya mishahara yake hayatekelezwi kwa nini? Miaka minne kwa nini? Wengine mpaka wafikia kustaafu na nyota begani lakini mshahara hauongezeki, what is this?
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuwa mchangiaji wa mwanzo katika hotuba hii Bajeti ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya njema na kuweza kusimama hapa. Napenda ni-declare interest mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naanza kwa masikitiko, hotuba ya Mheshimiwa Waziri ambayo naamini maneno yale mengi kama yatatekelezwa ni mwendelezo mzuri na ningependa na ningetamani sana Watanzania waisikie na pia wasikie maoni ya Kambi ya Upinzani ili kuonesha mwelekeo sahihi wa ile kauli ya Rais ya Tanzania ya Viwanda, nilitamani sana. Kwa bahati mbaya sana Bunge hili bado tumeendelea kukaa gizani, tutaambiana sisi kwa sisi, tunaendelea kuambiana haya tuliyoambiana kwenye Kamati, mengi tunayajua.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nifarijike jana tu kwa Wabunge wawili wa CCM, niwapongeze sana kwa kitendo chao kizuri sana walichoionesha jamii ya Watanzania kwamba sisi siyo wapinzani tu tunaopenda haya tunayoyasema hapa kwamba Bunge hili lionekane live. Wao walitumia jitihada ya kupigana picha za video, Mheshimiwa Abuu na Mheshimiwa Aeshi na gazeti la Nipashe likaonesha Watanzania kumbe letu ni moja, lakini tunatofautiana tu kimtazamo.
Mwimbaji mmoja kule Zanzibar aliimba nyimbo akasema kisebusebu na kiroho kiko papo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, haya tuendelee kuambiana katika njia za upole nadhani tutaelewana tu, hakuna haja, muone tu umuhimu wa haya mambo. Mheshimiwa Mwijage leo katika majibu yako ya maswali hapa, kuna raia wangu alinipigia akasema nilitamani nimwone Mwijage kila muda lakini wapi umeyatupa ndugu yangu hulitetei hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kusema kwamba Msemaji wa Kamati, Makamu Mwenyekiti alizungumzia jambo moja zuri. Alizungumzia umuhimu wa biashara na namna Serikali inavyowa-treat watu wanaoingiza bidhaa kutoka nje kutokana na ukadiriaji wa kodi ambazo wakati mwingine tunasema hazina mashiko. Kwa mfano, hivi sasa Watanzania wengi wanafilisiwa magari yao katika Bandari ya Dar es Salaam kwa tatizo moja tu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wewe hukuwepo Bunge la Kumi, nilisimama hapa wakati Waziri wa Fedha akiwa Mheshimiwa Saada Mkuya nikasema ikiwa Serikali mmeweza kuweka Maafisa wa TBS katika nchi tunazochukua bidhaa kwa ajili ya kufanya ukaguzi wa ubora wa bidhaa, ni kipi kinachowashinda katika suala hili la bei? Kwa sababu nchi ambazo Watanzania tunachukua magari kubwa ni tatu tu hapa duniani, ni Uingereza, Japan na Dubai, wakaweka usahihi wa ile bei ya gari Mtanzania analonunua ili akifika hapa atozwe kodi kulingana na thamani halisi ya gari. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa sababu kauli ile ilitoka left hand ikaonekana haifai. Leo Wabunge wenyewe wameonja bakora hii, wameagiza magari, thamani ya gari anavyolinunua akija hapa TRA tayari wameweka bei yao ambayo hiyo ni bei astaghfirullah wameifanya kama bei ya Msahafu maana Msahafu na Bibilia ndiyo ambayo haipingiki. Hii inapelekea watu kuona ugumu kiasi fulani wa kufanya biashara na watu wengi kufilisiwa gari zao zinapofika pale bandarini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naweka msisitizo wa hili, gari aina ya Suzuki Carry inauzwa si zaidi ya dola 500 Japan na ukiingia kwenye mitandao utaziona hizo bei, leo inachukuliwa hata carry ni gari ya anasa? Tungeondoa kutumia wanyama huko vijijini, mkulima mdogo mdogo analima mazao yake badala ya kutumia wanyama na kuokoa muda na kufikisha bidhaa zake katika soko angeweza kununua carry kwa dola 500 akija hapa akalipishwa kwa thamani ya ununuzi na usafirishaji ambayo haizidi dola 800, dola 1500 ikapigwa thamani lakini ukifikisha hicho kigari TRA wanakuambia thamani yake ni dola 2,500. Hii si haki, ni dhuluma na ni aibu sana kwa Serikali kuwadhulumu raia wake, tuliangalieni hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kumekuwa na wigo na maneno mengi juu ya biashara ya magendo baina ya Tanzania Bara na Zanzibar. Yamekuwa yakisemwa njia za panya zimekithiri katika ukanda wa bahari, lakini sababu ni moja. Sababu inayochangia hili ni vikwazo vya wafanyabiashara wa Zanzibar wanapoingiza bidhaa katika soko la Tanzania Bara. Kumekuwa na vikwazo na ugumu mkubwa sana ambao unasababishwa na Mamlaka ya Bandari na TRA Dar es Salaam kuwafanya wafanyabiashara wa Zanzibar watafute njia mbadala.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata katika hali ya kawaida ukimziba mdomo lazima atatoa pumzi kwenye pua. Wafanyabiashara wale wa Zanzibar cha kushangaza TRA ni moja, maafisa wa TRA wanateuliwa na Kamishna Mkuu wanafanya kazi kule Zanzibar, hakuna TRA mbili. Leo hii bidhaa kutoka Zanzibar zinapofika Dar es Salaam zinatazamwa kwa mtazamo hasi na kuonekana ni bidhaa ambazo hazifai kuingia ndani ya nchi yaani zinaangaliwa kwa ukakasi mkubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na Tume za Pamoja toka miaka ishirini ya Bunge hili kujadili kuondoa vikwazo vya wafanyabiashara wa Tanzania Bara na Zanzibar lakini hili nalo linaonekana ni jipu. Ninukuu usemi wa Mheshimiwa Nahodha, Waziri Kiongozi Mstaafu wa Zanzibar namheshimu sana kwamba ni jukumu la uchumi mkubwa kusaidia uchumi mdogo. Kwa hiyo, badala ya kuitazama Zanzibar kwa jicho hasi na wafanyabiashara wake lazima sasa muwatazame kwa mtazamo wa huruma na kuwaongoza katika njia stahiki ili biashara ifanyike pasipo na vikwazo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hapo hapo, nilisema na ninarudia raia wa nchi yoyote jirani ana haki ya kutoka na gari lake akaingia Tanzania, akitumia ruhusa ya kibali maalum kwa kukaa ndani ya nchi karibu miezi mitatu. Hilo kwa Zanzibar limeondoka na halipo, hawezi Mzanzibar kutamani kwenda Mikumi na gari yake na watoto wake ku-enjoy akaingiza gari lile na akapewa permit ya kwamba utakaa miezi mitatu gari kwa sababu labda kodi ya Zanzibar na hapa ina tofauti ukimaliza miezi mitatu urudi Zanzibar, hilo halipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii raia wa Burundi ambaye hayupo kwenye Muungano ataingia na gari lake na ata-enjoy kukaa nchi hii anavyotaka Wakongo halikadhalika. Kwa hiyo, hili nalo ni jambo linalotakiwa liwekewe utaratibu. Wapo wanaoleta magari yao kwa biashara wapitie ule utaratibu wote wa kiforodha na kama kuna makusanyo ya kodi ni sawa lakini anayekusudia kuja kukaa na gari lake katika kipindi kifupi kuna tatizo gani kupewa temporary document ya kukaa hapa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mbona mkitoka na gari zenu hapa mkiingia kule hakuna kikwazo hiki, kwa nini? Leo hii ukitoka na gari lako Tanzania Bara ukiingia nalo Zanzibar njoo Konde uta-enjoy utaenda kulala under water room kule Jimboni kwangu hakuna tatizo lakini hapa kwa nini? Tatizo ni kwamba …
MHE. KHATIB SAID HAJI: Hatujipambi wakati wa kuolewa twajipamba wakati wa kuachwa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nami namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kusimama hapa kuchangia katika hoja hii iliyo mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nilimsikia Waziri wa Mambo ya Nje, Mheshimiwa Profesa Kabudi akiisifia nchi yetu juu ya mafanikio na sifa waliyoipata duniani kutokana na uhuru wa vyombo vya habari. Juzi alikuwa akizungumza hapa na aliisema nchi yetu kwamba imepokea sifa kwa uhuru wa vyombo vya habari. Moja kati ya eneo alilolizungumzia ni kwamba Tanzania imesifiwa kwa kuwa na idadi kubwa sana ya magazeti. Kwa hiyo, hiyo ilikuwa ni sifa moja kubwa sana kwa Taifa letu, nadhani alikuwa akieleza aliyokutana nayo huko nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, siku mbili baadaye tumemsikia Msemaji Mkuu wa Serikali na Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo akiyataka magazeti yaliyoripoti taarifa aliyoitoa Kiongozi wa Chama cha ACT cha majirani, kwamba waende wajieleza kwa namna walivyochambua taarifa ile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili jambo kwa kweli limetupa mashaka. Anakwenda duniani anapata sifa juu ya uhuru wa vyombo vya habari, lakini nyumba yake Serikali, vyombo vya habari kuripoti taarifa ambayo ilitolewa siyo taarifa ya msituni, ni taarifa iliyokuwa public na ya wazi ambayo vyombo vya habari wana haki na ni moja katika kutimiza majukumu yao katika kuwaelimisha Watanzania ni nini kimezungumzwa na kiongozi yule wa chama cha siasa. Hilo limekuwa ni kosa; na wenzetu wahariri wa wahabari wanakiwa wajieleze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunaposifiwa, ni kwa lipi? Tunaporudi, tunafanya nini? Maana inakuwa hatueleweki. Leo vyombo vya habari vinatakiwa vijieleze kwa kosa lao, lipi? Watu wa habari, wanalipwa mishahara, wanafanya kazi kwa kutengemea habari zinazotoka wawaelimishe Watanzania ni kipi kinachoendelea katika nchi. Inatokea sasa tayari Msemaji Mkuu na Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo, Dkt. Hassan anavitaka vyombo vya habari vileze hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, cha kusikitisha zaidi; na Mheshimiwa Waziri naomba unisikilize; yapo mambo ambayo kama Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo na wewe Waziri, mngevitaka baadhi ya vyombo vya habari vijieleze, ni muhimu zaidi. Kwa mfano, kuna vigazeti fulani hapa, kimoja kinaitwa Jamvi la Habari na kingine kinaitwa Fahari yetu na kingine kinaitwa Tanzanite. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi vigazeti kazi yake kubwa kuchafua watu, kufitinisha watu, kuleta ugomvi baina ya watu. Mheshimiwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari hajawahi kuviita, hajawahi kuwaita Wahariri wa Magazeti haya akawaambia njooni mjieleze kwa namna namvyowachafua watu. Wamewachafua watu wengine tunaowaheshimu sana ndani ya nchi hii. Mfano, Comrade Kinana, huyu mtu muhimu kwenye nchi hii, lakini amechafuliwa na watu hawa, lakini hakuna Mkurugenzi wa la Waziri ambaye amemwita Mhariri wa Gazeti hili, Mkurugenzi wake Musiba mkamwambia ajieleze kwa namna ambavyo anawachafua watu. Kwa nini haitwi? Yuko nyuma ya nani anayejiamini mpaka aweze kumchafua yeyote? Yeyote kwenye nchi hii Musiba akiamua kumchafua anachafua na hakuna lolote linakuwa. Yupo nyuma ya nani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilidhani watu kama huyu ndio wangeitwa wakajieleza, wakaelekezwa, TCRA wakamwelekeza kama anachofanya sicho, lakini yeye yupo huru. Watu wengine wakitoa kwenye mtandao maoni tofauti kidogo na Serikali, wao wataishia kupelekwa sehemu kushitakiwa na wengine kwenda kufungwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Mheshimiwa tunafanya nini? Mimi nataka hili lizingatiwe.

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. KHATIB S. HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatibu kuna taarifa. Mheshimiwa Mlinga.

T A A R I F A

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Anayoongea Mheshimiwa Khatib ni kweli, ila amesahau kuna kijigazeti kimoja kinaitwa Tanzania Daima na chenyewe kazi yake ni kuchafua Serikali pamoja na watu. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatibu Haji, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. KHATIB S. HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wapemba tuna mila moja, yule kijana Bunge lililopita tuliishi na mama yake, kwa hiyo, mimi namchukulia kama mwanangu, siwezi kumjibu. (Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatib, mama yake alikuwa ameshafariki wakati huo, nadhani una hiyo taarifa. Sasa sijajua umekuwa umeishi naye wakati gani.

Waheshimiwa Wabunge, kuna mambo ambayo mnaweza mkafanya utani na kuna mambo ambayo siyo ya utani. Kwa hekima kabisa na heshima ambayo mnaitwa Waheshimiwa, Mheshimiwa Khatib tafadhali, huyo mama amefariki na ninaamini wewe ni sehemu ya watu ambao umefanya naye kazi.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, tuwe tunasikilizana. Hata wewe angekuwa ni mama yako anayezungumziwa hapa ningesema vivyo hivyo ninavyozungumza sasa hivi. Mheshimiwa Khatib, tafadhali mtunzie Marehemu heshima yake.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, sikuwa na nia mbaya, lakini kama limekwaza, naomba nifute hilo neno. Naomba kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niendelee na fungu kuhusu mgao wa fungu na fedha zinazotoka FIFA kwa Tanzania. Kuna siku nimewahi kuuliza swali; na katika hili Naibu Waziri alinijibu sijui kwa makosa au kwa bahati mbaya; akasema ZFA ipo chini ya TFF, jambo ambalo siyo kweli. TFF ni chombo mbali, Wizara ya Habari na Michezo Zanzibar, ni kitu mbali; na Wizara ya Michezo Bara na TFF ni kitu mbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ZFA ipo Zanzibar chini ya Wizara ya Habari na Michezo Zanzibar na TFF ipo hapa chini ya Wizara ya Michezo. Ni vyombo ambavyo havina mwuingiliana wa kisheria wala kikatiba. Hapa linalojitokeza ni kwamba mara nyingi sana tunapolilia juu ya haki ya Zanzabar katika vitu vinavyopatikana ambavyo ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wakati mwingine tunahisiwa kama sisi ni walalamishi sana, lakini hayo tuliyoyapata na faida zilizotokana na mengine tuliyoyalalamikia, bila shaka kulikuwa na haki ambayo labda ilikuwa imejificha sehemu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kazi yetu moja iliyotuleta hapa Wabunge wa Zanzabar ni kutetea maslahi ya Zanzibar kwenye Muungano. Kama wapo Wabunge wametoka Zanzibar wamekuja hapa, mfano ndungu yangu Ally King, kama yeye amekuja kucheza taarab, atacheza taarab; lakini sisi tuliokuja kutetea maslahi ya Zanzibar, tutatetea maslahi ya Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hakuna mgao halali kutoa fungu la FIFA. Mheshimiwa Mwakyembe hili naliomba leo anapohitimisha aliweke wazi, kwa sababu Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inajumisha nchi mbili; Zanzibar na Tanganyika.

MHE. MATTAR ALI SALUM: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mattar.

MHE. MATTAR ALI SALUM: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpe taarifa kaka yangu Mheshimiwa Khatib, Mheshimiwa Ali King hakuja Bungeni kucheza taarab, Mheshimiwa Ali King ni Mbunge ambaye kachanguliwa na wananchi wake wa Jimbo la Jang’ombe kuja kuwatetea. Namwomba sana Mheshimiwa Khatib aweze kurekebisha maneno yake ambayo ameyasema na afute kauli yake ahsante.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatib.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, najua Mheshimiwa Ali King aliletwa hapa kama nilivyoletwa mimi, lakini pia nami nimeletwa hapa kuwakilisha, lakini navuta Mchezo wa Kamba na tunachukua kombe kule Burundi na nchi nyingine tofauti. Kwa hiyo, hii ni michezo na hii michezo imo humu, unakataa nini? Kwa hiyo, kama yeye nyanja yake ni taarab, mimi nipo kwenye kuvuta kamba, timu simika. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hili jambo namwomba Mheshimiwa Waziri, hebu akutane na wenzie wa Zanzibar tuone kile kidogo kinachopatikana kutoka FIFA na sisi Wazanzibar tunafaidika nacho vipi? Ile ni haki ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa hiyo, Watanzania wote wanapaswa kufaidika na mgao ule wa FIFA kwa Zanzibar. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. KHATIB SAID HAJI: Leo hamtanipa nafasi, Pasaka hii. Naomba nimalizie muda wangu.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge hii itakuwa taarifa ya mwisho kwa Mheshimiwa Khatib, Mheshimwa Nyongo.

NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Khatib kwamba ZFA ni mwanachama wa TFF (Tanzania Football Federation) kama mikoa mingine ya Tanzania ilivyokuwa wanachama. Kila Chama cha Mpira ni mwanachama wa Tanzania Football Federation; na vilevile, kwa mfano, naomba nitoe mfano…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Mpeni nafasi amalize, Mheshimiwa Zitto naomba ukae, unazifahamu kanuni. Mpeni nafasi amalize, naomba mkae anazungumza. Kaa chini Mheshimiwa Juma tafadhali. Mheshimiwa Khatib, wewe unapewa taarifa, kwa hiyo, kaa utapewa fursa. Wewe kaa, amalize. Mheshimiwa Nyongo…

NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mfano mzuri ni kwa United States of America. California wana Chama cha Mpira, ukienda Majimbo mengine yote yana Chama cha Mpira; na wote ni Wanachama wa Football Federation of United of States America. Kwenda World Cup haiendi California, haiendi nchi nyingine, inakwenda United States of America na kuna more than 50 sets of United State of America. Wasipotoshe wananchi, ZFA ni Mwanachama wa TFF.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatib, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshangaa sana. Hayo maandishi umetoa wapi, hata unakuja kusimama hapa unasema ZFA ni mwanachama wa TFF? Kwanza…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatib zungumza name. Nimeuliza swali, unaipokea ama huipokei? Zungumza na Kiti, usizungumze naye. Zungumza nami, atakusikia ukizungumza nami.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nipokee nini hapo utumbo huo anaozungumza yule! Mheshimiwa TFF, TFF…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatib, una uwezo wa kukataa hiyo taarifa bila kuiita majina ambayo unataka kutuaminisha hapa kwamba ndiyo hayo aliyoyasema. Wewe ikatae taarifa yake, endelea na mchango wako, ndiyo kanuni zetu zinavyosema. Sasa hii habari ya nyama, ya utumbo umefanyaje, hebu ondoa hiyo habari ya utumbo hapo. Siyo lugha ya kibunge, ondoa maneno “utumbo” uendelee kuchangia kama umeikata taarifa yake.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakuheshimu sana, mimi nakataa hiyo taarifa yake ni rubbish kabisa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Utaratibu.

KUHUSU UTARATIBU

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, kuna kanuni inavunjwa. Mheshimiwa Jenista, kanuni iliyofunjwa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu
Spika, kuhusu utaratibu, nakwenda kwenye kanuni ya 64 (1) (b) ambayo inakataza Mbunge ama Wabunge kutokuzungumzia jambo ambalo halipo kwenye mjadala.

Mheshimiwa Naibu Spika ninaanza kuona sprit ya majadiliano yetu leo inahama kutoka kwenye hoja iliyopo mezani, sasa watu wanataka kuwachanganya Wabunge na kulichanga Taifa kuhusu Muungano wetu katika maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana, wakati tukiendelea na mjadala huu, Wizara iiliyokuwa inashughulika na masuala Muungano tulishaifunga jana. Watu wajikite kwenye maudhui ambayo yanaenda sambamba na Wizara ambayo hoja yale iko mezani, lakini masuala nyeti yanayohusu Muungano naomba...

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Zitto, Mheshimiwa Zitto! Mheshimiwa Jenista.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, masuala yanayohusu tafsiri za Kikatiba kuhusu Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Serikali ya Muungano yasiwe ni part ya mjadala huu katika siku ya leo.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nisisitize jambo hili ili kuondoa mkanganyiko wa mtazamo wa Kimuungano katika mjadala unaondelea hapa Bungeni.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, amesimama Mheshimiwa Jenista akitukumbusha kwamba kanuni ya 64(1)(a) na (b) na ameweka mazungumzo yake kwa kirefu na sikusudii kuyarudia; ametupeleaka kwenye fasili ya (b) kwamba Mbunge hatazungumzia jambo ambalo halipo kwenye mjadala.

Waheshimiwa Wabunge, nadhani hii kanuni ya 64 sote tunaifahamu, kwa hiyo, Mheshimiwa Jenista ametukumbusha. Mheshimiwa Khatib na Waheshimiwa Wabunge wengine waliotoa taarifa na waliochangia tuendelee na mjadala wa Wizara hii kwa yale mambo ambayo yanahusika. Wapo wengine hawajapewa fursa ya kuzungumza, lakini namna wanavyoyazungumza kwa kuwa yale wanayoyasema mengine yanasikika, basi yanaleta upotoshaji kwenye hoja nzima, hata ambayo alikuwa anazungumza Mheshimiwa Khatib. Wakati hoja yenyewe ni ya wazi na imenyooka.

Kwa hiyo, nawaomba Waheshiwa Wabunge tufuate kanuni zetu, mambo yasiyoruhusiwa tusiyafanye. Kwa sasa mjadala ulioko mbele yetu tunaufahamu, ni hoja ya Mheshimiwa Waziri; na yale aliyoyasoma Mheshimiwa Waziri na yaliyosomwa na Kamati ndiyo ambayo tunapaswa kujikita katika hayo ili tutoe maoni katika kuhakikisha tunaboresha ama tunataka Wizara kwenye yale mambo ambayo imeyaleta irekebishe wapi. Ndiyo maana Kamati imetuletea kwenye yale maoni yake.

Kwa hiyo, nawaomba tufuate hiyo kanuni ya 64 tujikite kwenye mjadala hasa kwa kuzingatia maoni….

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: …ya Kamati ili tutakapokuwa tunasonga mbele tuone wenzetu wametuongoza mambo gani ambayo tunapaswa kuishauri Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Khatib.

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Mheshimiwa Naibu Spika, Kuhusu Utaratibu.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Eeeh, hee!

KUHUSU UTARATIBU

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Najma ukisimama sasa hivi, maana yake mimi ndio nimekosea tena.

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Mheshimiwa Naibu Spika, hapana siyo hiyo.

NAIBU SPIKA: Kama hilo siyo lengo lako, inabidi nimpe fursa Mheshimiwa Khatib.

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Haya ahsante.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatib.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nitaendelea kwa lugha ya upole kabisa.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Eeeh!

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba unipe muda nimalize.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa, alinitaja.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ali King, kwa kuwa nilikuwa nimeshasema taarifa ya Mheshimiwa Nyongo itakuwa ni ya mwisho kwa Mheshimiwa Khatib, utapewa fursa wakati wa kuchangia. Mheshimiwa Khatib. (Makofi)

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nadhani nitakuwa sijatoka nje ya mada na sitaki kutoka nje ya mada. Hapa nilichokieleza ni kwamba tulikuwa tunalilia lile fungu la mgao unaotoka FIFA kwa Zanzibar. Ni ukweli ambao nitaendelea kuuamini kwamba Zanzibar sio Mwanachama wa TFF na Zanzibar ni chombo huru, kipo kiko chini ya Wizara ya Habari kwa Zanzibar.

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utaratibu.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatib, kuna kanuni inavunjwa, Mheshimiwa Najma.

KUHUSU UTARATIBU

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie Kanuni ya 64(1)(a) ambayo hairuhusu humu ndani mtu kuzungumza jambo ambalo si la kweli.

Mheshimia Naibu Spika, Mheshimiwa Nyongo wakati anatoa taarifa alizungumza kauli ambayo inasema kwamba Zanzibar ni sawasawa kama mikoa mingine. (Makofi)

Kwa hiyo, naomba tu Mwongozo wako kwamba hili suala aliweke sawa au aondoe kauli yake kwa sababu Zanzibar ndani ya Tanzania ni nchi, nje ya Tanzania ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, nimetoka kuzungumza hapa na kama kuna mtu mwingine hakumsikia sawasawa Mheshimiwa Nyongo anaweza akapewa fursa ya kuangalia Hansard. Amezungumzia chama cha michezo sio Zanzibar kama mkoa.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, kila mtu ana masikio na amesikia na kwa kawaida walimu wapo wengi sana humu ndani. Kuna watu ambao huwa wana kitu kile ambacho kwa kiingereza kinaitwa selective listening, yeye anasikiliza anachotaka kusikia yeye. Kwa hiyo, tuelewane vizuri kwenye hili Mheshimiwa Nyongo hajasema Zanzibar ni mkoa, amesema chama cha mpira cha Zanzibar ni mwanachama wa TFF kama ambavyo vyama vingine. Kwa hiyo...

Mheshimiwa Zitto naomba utupe fursa tafadhali tuendelee na shughuli nyingine.

Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge mimi nampa fursa Mheshimiwa Khatib amalizie mchango wake, mtu yeyote mwenye taabu na mchango wa Mheshimiwa Nyongo ataenda akaisome Hansard yale aliyoyasema Mheshimiwa Nyongo. Kwa hiyo, hajaasema Zanzibar ni mkoa, tuelewane vizuri.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatib nimeshamjibu Mheshimiwa Najma naomba tusirudi pale, malizia mchango wako.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kosa alilolifanya Nyongo ni kubwa sana, hawezi kuifananisha Zanzibar na mkoa hata siku moja na kama ni mchango bora niishie hapa, haina haja ya kuchangia tena. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kusimama hapa. Kwanza, nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kunijalia uzima wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile leo ni mara ya mwanzo kusimama katika Bunge lako hili, napenda nitoe shukrani kidogo kwa wanaostahiki. Kwanza, nawashukuru kwa dhati kabisa wananchi wa Jimbo la Konde kwa kunipa kura za kunirudisha tena hapa Bungeni. Naamini kabisa maamuzi yao yalikuwa ni sahihi na nataka kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu anijalie niwawakilishe kwa usahihi kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka nitoe shukrani za dhati kwa chama changu cha ACT Wazalendo kwa kuniamini kunipa fursa na wanajimbo wakanichagua kuja hapa. Pia napenda kwa dhati kabisa kutoka ndani ya moyo wangu nimshukuru kiongozi wa chama chetu Mheshimiwa Zitto Kabwe, Mwenyekiti wa Chama, Maalim Seif Shariff Hamad, niwaombee kwa Mungu awape afya njema wazidi kusimamia mpaka pale haki itakaposimama ndani ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuchangia, nataka niongee kwanza katika hotuba ya Mheshimiwa Rais aligusia habari ya viwanda,nataka hapa kidogo niongelee suala hili, dakika ni chache lakini tutagusa maeneo kidogo kidogo hivyo hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kuita wawekezaji tuanzishe viwanda ndani ya nchi ni maono yenye lengo la kuleta manufaa kwa nchi yetu na watu wetu, naunga mkono juhudi zote zinazofanywa na Serikali katika kuhimiza wawekezaji kuingia ndani ya nchi yetu. Niseme kwamba tunapoomba wawekezaji waingie ndani ya nchi yetu tunawajibu wawekezaji kuwalinda ili wafanye kazi zao ili kuleta tija tunayodhamiria kuipata. Umezuka mtindo ambao naomba Mheshimiwa Waziri wa Viwanda awe makini sana, tunakuwa mahodari wa kutaka wawekezaji waingie, wanakuja na viwanda vinaanzishwa, lakini matokeo yake baada ya muda inatokea migogoro au sintofahamu inayoifanya viwanda hivyo vishindwe kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa karibuni mtakumbuka palikuwa na mgogoro mzito wa Kiwanda cha Dangote, uwekezaji ule mkubwa lakini ulikuwa utendaji wake ni wa kusuasua. Kwasababu zozote zile nashukuru nimepata taarifa kwamba sasa kiwanda kile tayari kinafanyakazi, hilo ni jambo zuri na napongeza jitihada zote zilizofanyika kupelekea kiwanda kile kurudi katika uzalishaji. Hongera sana kwa wote waliohusika kufanikisha hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo pale Tanga tuna kiwanda kikubwa sana cha kuzalisha ngano, Pembe Mills, hiki kiwanda sasa kina takriban mwaka wa nne kimesimama na ni uwekezaji mkubwa, ni miongoni mwa viwanda vichache vikubwa vya unga ambavyo vipo katika nchi yetu. Nataka Mheshimiwa Waziri afuatilie na jitihada zilizofanyika kufanya Dangote irudi kufanyakazi na watu wa Tanga wanahitaji Kiwanda cha Pembe Millskirejee katika uzalishaji ili wananchi wa Tanga wafaidike na ajira na mapato yao. Katika suala la viwanda naomba niishie hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudi katika suala la katiba mpya, nilibahatika kuwa Mjumbe wa Bunge la Katiba na wewe ulikuwa shahidi, Mheshimiwa Spika alikuwa ni Mwenyekiti wangu wa Kamati. Maamuzi yale yaliyofanyika ninahakika yalipata Baraka ya Chama Cha Mapinduzi kwa 100% kwasababu Chama Cha Mapinduzi na ndiyo chama tawala na ndiyo chama chenye Serikali, kama jambo lile walikuwa hawakulikubali lisingefikia kuingia kwenye Bunge la Katiba, ninahakika walikubali na walikuwa na dhati ya nafsi zao kulifanya jambo lile lifanikiwe. Kubwa zaidi tulikwenda kwa wananchi Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilikwenda kwa wananchi ikazunguka nchi nzima kuchukua maoni ya Watanzania na Watanzania walijibu walichokitaka. Bahati nzuri Bunge la Katiba lilifanyakazi Watanzania waliyoitaka na bahati nzuri zaidi ni kwamba wako viongozi ambao wamepewa nishani kwa kufanikisha kazi ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunachokizungumza hapa si jambo geni wala jipya, ni jambo ambalo liko katika ahadi kwa wananchi wa Tanzania wakupatiwa katiba mpya. Kwahivyo tunapolizungumza hili katika hotuba ya Mheshimiwa Rais lipo, 2015 na kuna ahadi yake mwenyewe, kwahivyo tunapokumbushana ni kwa lengo jema la kujenga. Naomba Serikali ilete majibu Watanzania...

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatib kuna taarifa.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST:Nashukuru naomba nimpe taarifa muongeaji kwamba suala la katiba mpya lipo katika hotuba ya Rais ukurasa wanane, akiahidi kwamba atahakikisha analitimiza.

NAIBU SPIKA: Ngoja ngoja tuelewane vizurikwasababu wewe tulikuwepo wote hapa, yeye kashasema ipo kwenye hotuba ya Rais, wewe unampa taarifa kwamba ipo kwenye hotuba ya Rais, ni taarifa gani unayompa maana kashasema…

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Nasaidia kumweleza.

NAIBU SPIKA: Hebu soma kanuni yako inazungumza nini kuhusutaarifa,ni taarifa gani unayoweza kutoa, siyo taarifa ambayo yeye anaijua hapana, taarifa ambayo yeye hajaisema, sasa yeye kashasema, ni taarifa gani unampa.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: kwenye floor kuna mtu alitaka kujua ipo wapi ina maana kuna mtu wa...

NAIBU SPIKA: Nani aliyekuuliza Mheshimiwa siyo wewe unayechangia? Yeye kashasema ipo, sasa wewe unasema taarifa, lazima umpe kitu ambacho yeye pengine amepitiwa ama hakifahamu. Mheshimiwa Khatib endelea na mchango wako.

MBUNGE FULANI: Hicho ni kiherehere.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme kwamba imani ya Watanzania ni kwamba itakapopatikana Katiba mpya pia katika katiba mpya moja ya tunda muhimu la katiba mpya itakuwa ni Tume huru ya Uchaguzi. Ndani ya nchi hii tunaamini, ni imani yetu sisi na imani yetu hailazimishi imani yangu mimi kuikubali mtu mwingine, tunaimani na tunaamini hivyo kama katika nchi yetu ya Tanzania hatuna Tume huru ya Uchaguzi, whatever wengine tumerudi, lakini kurudi kwetu kama mnavyotuona hili benchi loote lilikuwa letu enzi zile za CUF na hili loote lilikuwa la CHADEMA, Tume ya Uchaguzi imetufanya tumekuwa maskini, tumekuwa mayatima, tumerudi kajipande hiki tu, Wabunge wa Majimbo tuko watano wanaume tuliobakia wote tuna wanawake humu jamani haki hii? (Kicheko)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatibu kuna taarifa nyingine kutoka kwa Mheshimiwa David Ernest Silinde.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza kabisa nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Khatib wakati wa mchakato wa Katiba mpya na mimi wakati huo nilikuwa upande wa pili. Kwahiyo mimi nilikuwa sehemu ya ule mchakato na bahati nzuri sana tangu wakati tume inaundwa ilikuwa bado ni Serikali ya Chama Cha Mapinduzi ndiyo ilitengeneza ile tume na tume ikakusanya maoni. Serikali ya Chama Cha Mapinduzi wakati huo niko upinzani, ilipounda tume ikaleta mchakato ule wa maoni yote ukaletwa ndani ya Bunge na mimi niko ndani ya Bunge, mchakato ukaanza tukaushiriki, sasa baada ya kuona kwamba ile ngoma ngumu, wakati huo na mimi niko upande wa pili, sisi tukaingia mitini umenielewa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwahiyo wakati ule wa mchakato siyo CCM waliokwamisha, wakati ule ni sisi tuliokimbia ndani ya Bunge na uzuri ni nini? Jambo hili Tanzania nzima inajua siyo kwamba lilikuwa la kificho, Bunge lilikuwa liko wazi, lilikuwa linarushwa, sisi ndiyo tukagoma, tukakaa kule ndani kwa mashinikizo na shinikizo kubwa lilikuwa kwamba tunataka Serikali tatu, ndiyo sababu iliyotuondoa ndani ya Bunge.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwahiyo nilikuwa nataka nimpe tu taarifa kwamba malengo ya Serikali ya Chama Cha Mapinduzi yataendelea kubaki kuwa sahihi, isipokuwa mwisho wa siku sisi na ilitakiwa wakati Mheshimiwa Khatib anachangia hapa ilitakiwa aseme kwa kweli sisi tulikimbia, kwahiyo tunaomba kwa kukimbia kwetu kule Mheshimiwa Rais atusamehe. Ahsante sana.(Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatib unapokea taarifa hiyo?

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme hivi nimesikiliza taarifa yake, lakini nataka nimfahamishe ndugu yangu Silinde kwamba tuliokimbia ni sisi Wabunge wa CHADEMA na CUF…

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Hawakukimbia Watanzania maana yake nini?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti uwe na utulivu kidogo kwasababu taarifa anayoijibia ni hii aliyopewa sasa unataka kuweka taarifa juu ya taarifa utulie kidogo eee mama.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Kama kutoka kwetu sisihakukuondoa majority ya Bunge la Katiba kufikia maamuzi na ndiyo maana ninyi mliendelea kubakia, kama kutoka kwetu sisi kulikuwa na maana kwamba katiba isipatikane? Ninyi mlikaa mkasubiri kufanya nini?Na kwanini mlimalizia? Na ninyi ilikuwa mtoke kuonekana kwamba sisi tulichokataa hakina maana kwaWatanzania, lakini kutoka kwetu sisi na mlichokiamua tumeona bado kama kuna kosa tulilifanya lakini kulikuwa na maana kwa Watanzania. Kwa hiyo ina maana kwa Watanzania madai yao, hayakufa kwasababu ya kutoka sisi. Mheshimiwa Silinde usijisahau leo kwa kuwa uko kwenye kiti kikubwa zaidi, kwasababu una V8, ndugu yangu ni mapito tu hata sisi V8 tutapanda. (Kicheko).

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee nataka nizungumzie habari ya mikopo ya elimu ya juu. Kimekuwa ni kilio cha wanufaika wa mikopo hii na hili ndugu zangu wana CCM wanabunge la kijani, naomba sana tuangalie athari ya makato yaliyoongezwa ya wanufaika wa mikopo, yanawaumiza. Inaanza kujengeka dhana sasa kuona kwamba utajiri ni muhimu kuliko elimu tuondokane na hilo, yaani inaanza kujengeka dhana matajiri wengi siyo wasomi…

NAIBU SPIKA: Endelea Mheshimiwa Khatib.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Kwamba matajiri wengi siyo wasomi umuhimu wa elimu utabaki kuwa muhimu kuliko chochote katika maisha ya mwanadamu, lazima tukubaliane hilo. Kwahiyo tuangalie namna ambavyo wamepandishiwa marejesho yale ya 15% na Serikali badala ya 8% ikiwezekana naunga mkono Mbunge mmoja wa CCM aliotoa hoja jana kwamba ikiwezekana ishushwe mpaka 5% kwa wanufaika wa mikopo ya elimu ya juu naomba sana hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nataka nizungumzie habari ya utawala bora. Kuna watu wenye mamlaka vyombo vyetu Jeshi la Polisi limekuwa likifanya mambo ambayo siyo utawala bora, juzi iko taarifa inasambaa kwenye vyombo vya habari askari polisi kule Mbeya wamemshusha raia driver kwenye gari na wakamuua, matendo yaliyokuwa yalifanyika Afrika Kusini enzi za Makaburu, ndiyo matukio ambayo vyombo vyetu vya ulinzi baada ya kusimamia usalama wa raia, sasa vinajenga uhasama wa raia. Naomba Serikali itoe tamko kali na zito kuhusiana na kadhia ya raia Yule,driverYule, aliyetolewa kwenye gari, akapigwa akauliwa na askari wa Jeshi la Polisi. [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Namshukuru Mwenyezi Mungu pekee kwanza dakika zenyewe ni tano.
MWENYEKITI: Mheshimiwa khatib dakika tano.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Ahsante.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa haya yanayotukuta hapa Bungeni, nimshukuru Mungu kwa kila linalotukuta. Leo nimesikitishwa sana na kilichotokea kwa njia yote ile iliyosababisha hotuba yetu ya Kambi ya Upinzani kufanya isisomwe hapa ndani ya Bunge imenisikitisha sana. Lakini nataka nikuambie tu kwamba, mmejaribu kufunga banda farasi ameshatoka. Watanzania wanaelewa kila kilichomo kwenye hotuba ile, taarifa ziko na wote wanajua ni nini, ujumbe gani umekusudia kuwafika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili niwashukuru wananchi wa Pemba hususani wa Jimbo langu la Konde kwa mapokezi makubwa waliompa kipenzi chao, Maalim Seif Sharif Hamad, jana katika ziara yake aliyofanya kule Pemba. Sasa mapokezi yale ni ishara tosha kwamba, hakika Wazanzibari nyoyo zao ziko na Maalim Seif. Kilicho chema ni chema hakibadili tabia, ni bure mngekisema na mengi kukizulia, Mungu hukipa baraka na amani kukitia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo baada ya tukio la kuzuiliwa hotuba, nilimuuliza, ninaye mtabiri wangu wa nyota na mtabiri wa ndoto, nikamuuliza hatua ya mwanzo ndani ya Bunge yamezuiliwa matangazo live ya TV, wananchi wasione tunachokisema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea, leo tayari tumezuiliwa hotuba yetu isisomwe ndani ya Bunge nikamuuliza what is next? Jibu aliloniletea muda mfupi ananiambia kinachoendelea baada ya kuweka dole mtawekewa vibakuli vya gundi wapinzani tutatia gundi ndi! Tukiingia hapa kimya. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni wajibu wetu kuona tunakoelekezwa kwenda, tuna hiari sasa kuamua kukubali kila tunalofanyiwa na wenzetu kwa sababu ya wingi wao au kuangalia ni hatua gani madhubuti tunachukua tukatae dhuluma yote ndani ya Bunge hili. Tukatae kunyamazishwa kwa namna yoyote sauti yetu hata humu ndani pia zisisikike, tukatae kabisa na tukatae. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka kuzungumzia suala moja ambalo linaendelea. Jeshi la Polisi, nimekereka sana na kitendo chao cha kuwashikilia watu zaidi ya muda wa kisheria ambao wanatakiwa kuwa-hold katika vituo vya polisi. Hili limesemewa na mimi nalisemea na linaniuma sana, kwa sababu ukiacha hilo kule Zanzibar, Jeshi la Polisi linatumika sana kisiasa, anaweza kutokea tu Mkuu wa Mkoa akasema wakamate hao weka ndani na wanafanya hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siku kumi hili linaniumiza sana, nalisema sana. Siku kumi kabla ya uchaguzi haramu wa marudio Zanzibar, wananchi wangu wa Jimbo la Konde wasiopungua 30 walizuiliwa katika vituo vya polisi katika muda usiozidi siku 14, wakapelekwa mahakamani, mahakama wakasema hatuoni kesi hawa ya kuwafungulia tulichotegemea kirudishwe vituo vya polisi watapewa dhamana, matokeo yake imetoka amri kutoka hatujui wapi, wanaambiwa endeleeni kuwashikilia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumuuliza Waziri wa Mambo ya Ndani, ni yeye, ni Naibu wake au ni nani anayesimamia amri hii haramu ifanyike kwa wananchi wangu. Leo akija hapa Mheshimiwa Waziri mimi na yeye na mshahara wake mpaka tujue nani anayetoa amri haramu ya kuwazuia wananchi zaidi ya muda wa kisheria unaotakiwa uwe nao au uwe umewapeleka mahakamani kwa hatua za mbele zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashindwa sana, hapa alinyanyuka, katika moja ya maneno mabaya aliyowahi kusema kiongozi mmoja mwandamizi wa CCM ambaye sasa hivi ni Waziri, ni pale alipotamka katika mmoja wa mkutano wake akiwa ndani ya kanisa kwamba, tatizo la Zanzibar ni Uislamu, Mheshimiwa Lukuvi, alisema hayo maneno, nataka niseme tatizo la Zanzibar sio Uislamu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkutano wa Bunge la Kumi kwenye taarifa ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Serikali ilianzisha kauli mbiu isemeyo; “Utalii Uanze kwa Mtanzania.” Pamoja na kauli hii kuonesha msisitizo kwa Watanzania kuweza kujivunia na kunufaika na sekta hii, bado zaidi ya robo tatu ya Watanzania hawanufaiki hata kidogo na sekta hii ya utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli hii iliyotolewa na Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii wa wakati huo, ni hadaa kubwa kwa Watanzania. Inajulikana bayana kwamba kima cha chini cha mshahara wa Mtanzania hakizidi shilingi 300,000. Kutembelea mbuga zetu ni lazima kila Mtanzania kuchangia kiasi cha shilingi 5,000 mpaka shilingi 15,000, lakini pamoja na mchango huu, kama Mtanzania atalazimika kulala mbugani katika hoteli kwa usiku mmoja itamlazimu kulipa gharama mara mbili zaidi ya mshahara huo kwa kima cha chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vyema Watanzania wakafahamu kuwa Mtanzania anapotaka kwenda mbugani kwa siku mmoja tu inagharimu dola za Kimarekani takribani 145 sawa na fedha za Kitanzania shilingi 316,825 kwa exchange rate ya shilingi 2,185. Hii ni kwa hoteli yenye gharama nafuu zaidi mfano Rhino Lodge. Gharama hii haijahusisha chakula wala huduma nyingine yoyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Chama cha Mapinduzi inayojipambanua na kauli ya Hapa Kazi Tu kwa nini isingeona umuhimu wa kuvaa viatu vya wananchi hawa wa kipato cha chini na kuona ilivyo kazi kuweza kuishi kwa kiasi hicho cha fedha kitakachomfanya Mtanzania huyu aweze na yeye kujisikia sehemu ya kulinda na kuzifahamu mbuga zetu? Ni kwa nini Serikali isifike mahali ikaona umuhimu wa dhati kuweza kumsaidia Mtanzania huyu kuweza kujisikia kuwa sehemu ya rasilimali zilizo ndani ya nchi yake kwa kuweka mazingira nafuu zaidi kwa bei ambayo Watanzania wengi wataweza kulipia na kufurahia mandhari mazuri ya mbuga zetu? Ni vyema sasa tukaaza kujivunia vya kwetu kwa vitendo ili basi Watanzania wasiwe ni watu wa kusimuliwa au kuona mandhari ya mbuga zetu kwenye runinga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini Serikali inafumbia macho malipo yanayofanywa kwa fedha za kigeni hasa kwenye sekta ya utalii? Mara nyingi tumekuwa tukilizungumzia suala la matumizi ya dola katika mzunguko wa fedha hapa nchini, lakini ni kwa nini Serikali haichukui hatua?
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, Mtanzania anayeamua kufanya utalii wa ndani na kuamua kulala kwenye hoteli zilizopo ndani ya mbuga, hasa zile zilizoko kwenye Hifadhi ya Ngorongoro, Serengeti na hata hoteli kubwa za Zanzibar, ni lazima afanye malipo kwa dola. Katika hali ya kawaida, ni Watanzania wangapi wanamiliki dola katika uchumi wao? Hii ina maana kwamba ni lazima wabadili fedha zao katika maduka ya kuuza fedha ili waweze kufanya malipo. Ifike mahali hasa Serikali ijitathimini. Ukienda nchi za wenzetu walioendelea, mfano, Norway, Switzerland, German na nyingine, huwezi kununua kitu kwa fedha ya kigeni. Wanathamini fedha yao zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni aibu na ni fedheha kubwa kwa Serikali kuendelea kushiriki katika michezo ya kuua thamani ya shilingi yetu kwa kuruhusu makampuni haya kuendelea kufanya tozo mbalimbali ndani ya nchi kwa fedha za kigeni. Serikali ije na sera lazimishi ya kuhakikisha kuwa fedha yetu inatumika. Wageni waweze kununua fedha yetu ili tuwe na akiba ya dola. Tunawezaje kufikia ndoto ya kuwa na uchumi na kati wakati sisi wenyewe ndiyo tunadidimiza thamani ya shilingi yetu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, inashangaza sana kuwa booking za hoteli za kitalii kwenye hifadhi za nchi hii zinazofanywa kupitia kwa mawakala walio nje ya nchi yaani ukitaka kupata nafasi ya hoteli unapiga simu Afrika Kusini au Nairobi kwa Wakala ambaye yeye ndio atakupa nafasi au laa. Tunataka kujua ni kwa nini jambo hili linafanywa kwa namna hii? Ni kwa nini booking zote za hoteli zilizopo hapa nchini zisifanyike kupitia mawakala waliopo ndani ya nchi yetu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wakati sasa Tanzania kuweza kuthamini vitu alivyotupa Mwenyezi Mungu. Inasikitisha sana kuona vyura wa kipekee kabisa duniani hawapewi nafasi ya kutosha kuweza kufahamika kwa wananchi wetu. Vitu hivi vya kipekee kabisa ambavyo duniani kote hakuna, mfano wa vyura hawa wa Kihansi wanaozaa na kunyonyesha, ni dhahiri kabisa tunakuwa hatuwatendei haki wananchi wetu na hata watoto wetu ambao watakuwa watu wazima na hawaifahamu nchi yetu na vivutio vyetu vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ije na mpango mkakati wa kuhakikisha vyura kama hawa ambao ni amphibia, pamoja na malikale nyingine zinaingizwa katika mitaala mbalimbali ili watoto wetu waweze kuvifahamu vizuri.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nikuelezee tu kwamba moyo wangu unasikia burudani sana unapokaa kwenye Kiti hicho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu sana kunijalia na mimi leo kusema hapa. Pia nataka nimwombee dua zaidi kiongozi wetu wa Chama cha Wananchi CUF, Katibu Mkuu, Seif Sharif Hamad kwa majaribu anayokumbana nayo Wazanzibari na Watanzania wapenda haki wako sambamba na yeye. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema kila aliaye anashika kichwa chake, hashiki kichwa cha mwenzie. Tarehe 25 Julai, kama sikosei, mwaka 2011, nilisimama kwenye Bunge hili wakati huo ikiwa Wizara ya Afrika Mashariki nikilalamikia kitendo cha Jamhuri ya Kenya wanachowafanyia wananchi wetu wa Zanzibar wanaokuwepo Kenya wakishiriki katika shughuli za kujitafutia rizki kupitia njia ya uvuvi. Nililalamika hilo na Waziri aliyekuwepo wakati ule alifuatilia kiasi chake mambo yale yalitulia kwa kiasi lakini katika miaka ya karibuni masuala ya askari wa Kenya kuwakamata wavuvi kutoka Kisiwani Pemba kule Kenya ni suala ambalo linaonekana ni jambo la kawaida. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yamekuwa yakitokea, hivi karibuni tu, nadhani miezi mitatu iliyopita, wananchi karibu 100 kutoka Visiwa vya Pemba, wengi wao wakitoka katika majimbo yetu ya Kaskazini, Wilaya ya Micheweni, Wete walishikiliwa pale na sababu za msingi za kuwashikilia watu wale hawana, tumekuwa tukilalamika sana. Balozi wetu wa Kenya, Balozi mdogo aliyeko Mombasa amekuwa akifuatilia mambo haya na wakati mwingine amekuwa akiambiwa hakuna hasa shtaka la kuwashtaki watu wale badala yake wanapigwa faini ambazo kwa bahati mbaya sana tunalazimika Wabunge sisi kutoka Zanzibar hasa kutoka Pemba, tuchangishane mifukoni mwetu kwenda kuwagomboa watu wale kwa kuwalipia faini kubwa sana, haya mambo hayafai. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar tuko kwenye Muungano, hatuna Wizara wala hatuna utetezi wa moja kwa moja, lazima tupitie kwenu. Mliyafanya, mnayaweza lazima muyaweze. Kule Zanzibar asilimia 90 ya watandika vitanda kwenye hoteli za kitalii ni Wakenya, wala hawanyanyaswi. Kwa nini Wapemba wanapata tabu katika Jamhuri ya Kenya? Naomba sana, Mheshimiwa Waziri akija atuambie tumekosea nini, wavuvi wetu wanapokuwa katika Jamhuri ya Kenya wanapata matatizo makubwa na yanajirudia kila mwaka. Hili haliwezekani na hatutakubali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tufike mahali tuseme kunyanyasiwa watu wetu imetosha, raia wa Tanzania ana thamani sana. Kwa hiyo, kuwaacha Wazanzibari ambao sasa ni Watanzania wakiendelea kuteseka na Balozi yupo, Mheshimiwa Waziri afuatilie jambo hili, linatukera sana. Kama wameshindwa wafikirie upya Zanzibar kuwa mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki waone tutakavyotetea haki zetu kule. Hilo la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nataka nizungumzie suala lingine la mahusiano. Tanzania imezuka aibu sana hasa kwa viongozi na watu wanaosimamia usalama wa nchi hii. Jambo dogo ugaidi, kuna ugaidi, kuna magaidi Amboni, kuna ugaidi Zanzibar, hii hatujengi! Neno ugaidi ukilitaja kwa watu wengine huko macho yao yanakaa hivi. Leo pale Zanzibar imetajwa ni kisiwa ambapo kuna magaidi yako mahakamani wakati hakuna tendo la ugaidi ambalo limewahi kufanyika Zanzibar, kama lipo litajeni!
MHE. KHATIB SAID HAJI: Sio sifa kutaja ugaidi wakati hakuna ugaidi.
Mkataba wa Ubia wa Uchumi baina ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Ulaya.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nianze kwa kusema kwamba, wakati tuna msiba mkubwa uliolipata Taifa kwa kuondokewa na kipenzi chetu, nasikitika kwamba tunaletewa tena msiba mwingine ambao ni mkataba usiofaa hata kuujadili. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hili jambo leo nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge wenzangu, nimesimama hapa kama mzalendo wa Tanzania. Katika mambo ya kinchi, katika mambo ambayo yataleta tija au hasara kwa nchi hii, na mimi nakubaliana, lazima tuwe wamoja. Naupongeza sana uongozi wa juu wa chama changu kwa kuliona hili na kutuletea mawazo ambayo siyo lazima, lakini kutuelekeza katika njia ya kwenda katika mjadala huu ambao ni hasara kwa Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nimejaribu kutafuta nondo zangu hapa, kila nilivyoangalia sizioni, lakini nina wasiwasi ndugu yangu Mheshimiwa Zitto Kabwe kazichukua. Kwa sababu yale niliyopanga kuyasema hasa, ndiyo yale ambayo ameyawakilisha. Hongera sana Mheshimiwa Zitto Kabwe. Ametupa somo na funzo zuri ambalo tunafika mahali kama Taifa lazima tukubaliane katika mambo ya msingi kama hili ambalo tunalo sasa hivi mbele ya meza yetu. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Spika, binafsi kuna kipengele katika mkataba huu kinachosema kwamba tutakaposaini mkataba huu hatutakuwa tena na uwezo kama nchi kuwa na ushirikiano na nchi nyingine, hii ni aibu! Hii ni aibu kwa sababu Tanzania ni Taifa huru. Hautakuja mkataba wowote ambao utatuzuia kuwa na ushirikiano wa kibiashara, ya kiuchumi au ya kisiasa na nchi nyingine, mkataba huo ukawa na una manufaa kwa nchi hii, haiwezekani. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuna kifungu kingine kinasema kwamba tukishaingia katika mkataba huu, suala la kupandisha kodi kwa bidhaa itakuwa halina tena nafasi.
Mheshimiwa Spika, nchi yetu hii kila mwaka unaona kodi zetu ni hizo za sigara, bia, vilevi na kadhalika. Hizo ndiyo kodi; revenue kubwa inatokana na hayo. Leo tukisaini mkataba huu, hayo mambo yatakuwa hayapo. Kuingiliwa uhuru wa nchi yetu kwa namna yoyote ni janga ambalo mzalendo wa ukweli haifai kulishabikia.
Mheshimiwa Spika, isionekane kwamba wapinzani ni watu wa kukataa kila kitu. Niwahakikishie, likija jambo lenye maslahi tutakuwa pamoja na hatutaangalia chama, lakini niwatahadharishe wenzangu, hasa upande huo, likija jambo la ovyo ovyo kama vile ulivyokuwa Muswada wa Habari, tutaukataa mpaka mwisho wa kiama. Tuambiane ukweli, mkileta lenye manufaa ni kama mnavyotuona, lakini mkija na mambo ya ovyo hatutakuwa pamoja, lazima muone mawazo yetu na muelewe kwamba sisi tupo kwa ajili ya Tanzania yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nina mashaka sana. Jamhuri ya Kenya ni watu ambao wakati mwingine sijui wanatuona sisi Watanzania tukoje. Wamekuwa ni watu wa ku-beep, beep tu. Hii Afrika Mashariki haikuja kwa lengo la kunufaisha nchi moja katika Afrika Mashariki na nchi nyingine ziwe mashahidi, haiwezekani. Leo wenzetu Kenya kwa sababu katika mauzo ya nje wana karibu asilimia 90 na kitu, kwa hiyo, wao ni haraka sana kusaini katika hili; na wamekimbilia sana katika hilo, lakini hawatuangalii sisi. Nao ni miongoni mwa zile nchi zilizojifanya wako tayari katika kila jambo. Kwa hiyo, kama hili wako tayari, watakwenda peke yao, sisi bado. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Spika; Mheshimiwa Spika, umekuwa mtoro sana siku hizi mpaka tunakusahau. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Spika, Kenya hao hao tuliokaa nao katika makubaliano ya single custom territory, ndio hao wametuacha kwenye junction. Sisi tumekwenda, wao wamechomoa. VAT on transit goods, hao hao Wakenya tulikubaliana, wakati wa kusaini, sisi tumeingia kichwa kichwa, wao wamechomoa. Mpaka lini Kenya watatuona sisi ni watu ambao ni kama wa kututumia rubber stamp ya kuendeleza mambo yao na sisi kutuacha nyuma. Haiwezekani, lazima tujiangalie. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hii inatupa funzo moja kubwa sana. Waheshimiwa, Serikali hii ya CCM hebu sasa fikirieni, dira na sera zetu za kiuchumi zinatuelekeza vipi? Haya ndiyo matatizo makubwa tunayoyapata; kuna mjuvi wa maneno mmoja au mjuaji wa kusema mmoja, alisema kwamba nahodha bora ni yule anayejua bahari anayokwenda. Kwa nahodha asiyejua bahari anayokwenda, hakuna upepo utakaokuwa muafaka katika safari yake, hakuna. Kwamba nahodha ni yule anayejua nchi yangu hii Tanzania, Serikali yetu; sera zetu za kiuchumi zinapelekea sasa wenzetu kuweka mikataba hii na kutuletea kuona kwamba sisi kwa sababu ya dhiki zetu, kwa sababu ya njaa zetu, wao watuletee lolote na tutakubali.
Mheshimiwa Spika, sasa tunasema kwamba ni afadhali tufe na dhiki zetu kuliko kukubali mikataba ya ovyo ovyo kama hii. Hatutakuwa tayari kufungiwa ngulai na kwa sababu eti ni nchi maskini tuendelee kukubali. Sasa umaskini huu ni lazima tuwaulize watawala wa miaka 50 mlioitawala nchi hii, kwa nini nchi yetu inaendelea kuwa maskini wakati sera nzuri na mambo mazuri mnayataja kwenye mikutano, lakini kwenye utekelezaji tunakuwa zero? Why? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lazima sasa mtimize wajibu wenu. Nakiomba sana chama kizee cha CCM, wengine wanaposema chama kizee wanaona kama ni kejeli; uzee ni busara.
Mimi ninapokiita chama kizee, naamini kuna busara. Niliwaambia bahati nzuri sana Bunge hili asilimia karibu 60 ni vijana na wengi ni ninyi, tusifike mahali tukaona wale wazee waliokuwemo kwenye Bunge hili ni bora kuliko vijana ninyi mlio na mawazo ya kizee kupita kiasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi kuwa mchangiaji wa mwanzo katika siku ya leo. Awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uhai wake na leo tuko hapa tunaendelea kuwakilisha wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nianze kuchangia kuhusu mpango huu kwanza nikigusa suala la uwekezaji wa ndani ya nchi. Tumekuwa tukitarajiA mengi kutokana na utajiri wetu wa rasilimali nyingi zilizomo ndani ya nchi. Mipango na maneno, wenzetu Chama Cha Mapinduzi mnaongea sana, mnapanga sana, mipango hii ukichukua toka ilivyoanza mpaka leo kwa hakika tungekuwa hatupo hapa tulipo lakini tunapanga hatutimizi mipango yetu, sijui kwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, toka sijaingia katika Bunge hili tumekuwa tukisikia suala la Liganga na Mchuchuma. Nilipoingia ndani ya Bunge hili nilibahatika kuwepo kwenye Kamati ya Uchumi, Viwanda, Biashara na Uwekezaji, ni kati ya mmoja wa mwanakamati tuliokwenda kutembelea maeneo yale. Kwa kweli katika kutembelea maeneo yale tuliiona shani ya Mungu ilivyo kubwa ya utajiri mkubwa wa chuma ambacho Mwenyezi Mungu ametujalia katika nchi yetu. Yamepangwa, yamepangwa lakini hadi leo tumeshindwa kutumia Mradi ule wa Chuma cha Liganga na Mchuchuma katika kuwaletea wananchi maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nchi yetu iko katika ujenzi wa miundombinu ya nguvu kweli kweli, nimshukuru Rais wetu kwa kusimamia ujenzi wa miundombinu katika nchi hii. Laiti mipango tuliyoipanga, Chuma cha Liganga na Mchuchuma kingeanza kuzalishwa leo hii ingekuwa hatuagizi chuma kutoka nje katika kujenga reli ambayo tunaijenga ndani ya nchi yetu. Waheshimiwa pigeni makofi kwa maneno haya mazuri. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imebaki ni story lakini hatutashiba maneno, Watanzania wanataka vitendo, tuliyoyapanga tuyaoneshe kuyatenda kwa vitendo. Mradi ule wenzetu nchi jirani wanaulilia na kutuona sisi Watanzania ni watu wa ajabu sana kwamba tunajaliwa rasilimali ambayo ni mali kubwa kweli kweli duniani, ilitegemewa leo Tanzania tunaiuzia Afrika nzima chuma kutoka Liganga lakini matokeo yake imekuwa tunaletewa story kila mwaka. Nataka nimuombe Rais wangu, viongozi wa Chama cha Mapinduzi na Wabunge wa Chama cha Mapinduzi, isimamieni Serikali yetu itekeleze mradi huu muhimu kwa uchumi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu mnyonge mnyongeni haki yake mpeni na anayetenda jema msifu mchukie kwa sura yake na mengine lakini katika suala la kuchukua maamuzi magumu kwa maendeleo ya nchi Mheshimiwa Rais amefanya vema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Rais ni Waziri wa Ujenzi alitamani kupanua barabara kutoka Ubungo mpaka Kibaha, lakini bahati mbaya hakufanikiwa. Alipoingia madarakani ametekeleza mradi ule mpaka nikajiuliza laiti leo ingekuwa wazo lile hakulifanyia kazi, basi kutoka Chalinze mpaka Dar es Salaam tungetumia saa ngapi? Bila shaka tungekesha, tungelala Kibaha lakini limetekelezwa. Sasa nimuombe Mheshimiwa Rais maamuzi magumu aliyoyachukua kwa kutekeleza mradi ule wa Kibaha mpaka Ubungo achukue maamuzi magumu pia kutekeleza Mradi huu wa Liganga na Mchuchuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwa wafanyabiashara. Kama tunataka nchi yetu tuendelee lazima wafanyabiashara wetu wasaidiwe. Tatizo kubwa linalowakwaza wafanyabishara hasa wadogo wadogo ni utitiri wa kodi zinazowekwa na TRA katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunasema wafanyabiashara wakubwa wanaondoka lakini hata hawa wadogo nao watapotea kwa sababu kodi zimezidi ukubwa wa biashara zao. Ukiacha kodi, makadirio yasiyo na ukweli ni mengi. Wafanyabiashara wengi wanaofunga biashara ni mfanyabishara amefanya biashara yake anapelekewa makadirio anaambiwa wewe unadaiwa milioni 500, ukiangalia biashara haifiki milioni 300, mfanyabiashara huyo kweli atakaa? Lazima atatafuta namna ya kuacha biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuunge mkono sana Mheshimiwa Musukuma jana kwa jinsi alivyoyaona haya na akayaweka wazi. Kwa yale aliyoyazungumza na Kanuni zetu zinatukataza kurudia, nitaishia hapo lakini tuangalie utitiri wa kodi uliopo kwa wafanyabiashara wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano hai tu, toka hapo nje, utaona hao wajasiriamali wanaouza nguo, vitenge na mashuka, wanakwamba mashuka kutoka Uganda, why not kutoka Kariakoo Dar es Salaam? Yameshuka bandari ya Dar es Salaam, yamesafiri yamekwenda Uganda, wafanyabiashara wetu imekuwa ni nafuu kwao kwenda kuchukua Uganda wakarudisha hapa kuliko kuchukua Kariakoo wakaleta hapa Dodoma, why? Bado hatukai tukajiuliza kuna tatizo gani? Tatizo nchi zilizotuzunguka wameweka kodi zinazolipika, sisi tunataka utajiri kwa wafanyabiashara hao kumi waliojikusanya, haitawezekana, tupanue wigo wafanyabiashara walipe kodi inayolipika ili wawe wengi nchi yetu ipate kodi nyingi na tuweze kuendelea. Nadhani hiyo imeingia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala utawala bora, katika ukurasa wa 40, kifungu 2.6.3.3, naomba ninukuu kidogo: “Utawala bora, uwajibikaji na utoaji wa haki. Katika kipindi cha utekelezaji wa Mpango wa Pili, Serikali iliendelea kupambana na rushwa, kuongeza uwajibikaji kwa watumishi wa umma na kujenga miundombinu ya utoaji wa haki kudumisha utawala bora”. Naishia hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nataka nimsifu Rais kuwashinda nyie CCM. Nampongeza Mheshimiwa Rais kwa uamuzi wake kwa kuiheshimu Katiba ya nchi hii. Kabla yetu alitangulia kuapa kuilinda na… malizia. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais ameendelea kuwa ni mlinzi wa Katiba. Uamuzi wake wa kumtuma Mheshimiwa Humphrey Polepole (Mwenezi) awaambie wana CCM kwamba hataongeza kipindi cha utawala, ni ishara ya Rais wetu ya kuilinda na kuienzi Katiba. Atakuwa ni Rais wa kwanza katika ukanda wetu wa nchi za Afrika ambaye baadhi ya Wabunge wake wanamwomba aongeze muda lakini tayari ameweka msimamo wa wazi na alimtuma Mheshimiwa Polepole.

Mheshimiwa Polepole waambie CCM Mheshimiwa Rais hana shida ya kuongeza muda. Alikutuma na video zinatembea tunaziona kwa nini unawaacha kina Mheshimiwa Sanga hapa wanaendelea kupotosha, kwa nini hamheshimu mawazo ya Mheshimiwa Rais? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge lililopita nilimwambia Mheshimiwa Ally Keissy, alinyanyuka na kujipendekeza hivi hivi, nyi nyi nyi nyi! Nikamwambia nchi hii ni ya kidemokrasia na Rais anaheshimu Katiba na Rais wetu ameshasema hataongeza muda. Kama mna wasiwasi hamna mtu wa kuwa Rais sisi wapinzani tunao. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, why Mheshimiwa Dkt. Magufuli ni mzuri sana…

MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Haya Mheshimiwa Khatib, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Humphrey Polepole.

MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutumia nafasi hii kumpa taarifa Mheshimiwa Mbunge ambaye alikuwa anaendelea kuzungumza kwamba masuala ya Chama cha Mapinduzi yanazungumziwa kwenye vikao vya Chama cha Mapinduzi. Hapa Bungeni Wabunge wana uhuru wa kutumia uhuru wa Bunge kuzungumza lakini kinachozungumzwa huku ndani hakiathiri msimamo wa Chama cha Mapinduzi ambao tumekwishakuutoa. Msemaji wa Chama ni Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli na kama si yeye mimi husema kwa niaba yake, Mheshimiwa Rais hataongeza muda lakini isizuie watu kuzungumza huku Bungeni. Ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Khatib, nadhani umeipokea taarifa hiyo?

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepokea si ni nzuri! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wale wenzangu ambao wanadhani kuja hapa wakasema Rais atake asitake, hataki sasa, mwamtafutia nini? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee na utawala bora, Mahakama imejenga majengo mengi lakini kujenga majengo ya mahakama, shule na hospitali lengo ni kutoa huduma kwa wananchi. Ili huduma zipatikane, ni lazima iambatane na mambo mengine, watendaji na vifaa ni muhimu katika kukamilisha majukumu ya Mahakama. Mahakama ni industry na ili iweze kuwa productive ni lazima ipate material. Material ya Mahakama ni Waendesha Mashtaka kupeleka ushahidi kwa wakati ili kuzifanya Mahakama ziweze kutenda kazi zake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mlundikano wa mahabusu si utawala bora, nchi yenye utawala bora…

Mheshimiwa Mwenyekiti, unanipa dakika tatu za nyongeza?

MWENYEKITI: Hapana. (Kicheko)

MHE. KHATIB SAID HAJI: Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Na mimi kwa sababu ya muda mfupi nikubaliane na kumuunga mkono dada yangu Mheshimiwa Halima kwa hapo alipofika. Nikuhakikishie kwamba na sisi tunajua kama kuna utapeli umefanyika wa kulisadikisha Bunge hili kwamba Lugumi walichokuja nacho mara ya pili ni cha ukweli wakati ukweli halisi unajulikana. Kama alivyosema ni maajabu katika muda wa mwezi mmoja kutoka vituo 14 vikaja 153. Huo ni uongo, ni uongo, ni uongo kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nataka nianze kuchangia kwa kusema kwamba nasikitika sana kwa taarifa hizi nzuri ambazo tumeletewa hapa na wenzetu wa PAC na LAAC lakini kuna upungufu na nataka nianze na hii ripoti ya LAAC.
Kamati hizi ni za Bunge na ni Kamati za mahesabu. Umuhimu wa Kamati hizi hakuna ambaye hawezi kuuona kwa vyovyote vile iwe kwa jicho la karibu au kwa mbali. Hata hivyo, malalamiko makubwa yaliyopo hapa, nataka nisome katika ukurasa wa nne wa taarifa hii ya LAAC, anasema, nanukuu:-
“Zipo namna kuu tatu za kutekeleza majukumu ya Kamati ambazo ni:-
3. Kamati kuzuru na kufanya ukaguzi wa matumizi ya fedha katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika baadhi ya Halmashauri ili kujiridhisha na thamani ya fedha katika miradi hiyo (value for money).”
Mheshimiwa Naibu Spika, cha kusikitisha sana ni kwamba tunaletewa taarifa hizi, siyo LAAC wala PAC, wote wanasema hakuna aliyepata fungu la kwenda kujiridhisha na taarifa hizi tulizoletewa hapa. Kwa maana nyingine ni kwamba wao wamepelekewa taarifa kwenye meza na wametuletea sisi hapa bila kuthibitisha chochote, hili ni kosa moja kubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ni mambo ya kimahakama kosa hili linafanana na utakatishaji fedha, uhaini, ugaidi, makosa ambayo hayana dhamana, ndiyo! Kwa sababu tunakotoka tunajua mambo yaliyokuwa yanaletwa kwenye makaratasi na wanapokwenda field kwenye ukaguzi kulikuwa kunakuja manyago makubwa sana. Kulikuwa kunakuja mambo ya hatari, mtu anaoneshwa hapa imejengwa shule wakifika hata kiwanja hakuna. Leo Bunge mmeridhia tuletewe haya kwenye makaratasi badala yake tunakuja kulishwa humu na tunapiga makofi tunakubaliana nayo. Hili ni kosa moja kubwa sana ambalo Serikali haihitaji kupewa dhamana juu ya kosa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa najua tunabana na kubana mimi najua kuna utamu wake, lakini na kubanua kuna raha zake. Huwezi kubana moja kwa moja ukadhani mambo yataenda, haiwezekani. Lazima sehemu nyingine ubanue kidogo ndiyo raha ipatikane. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka ninukuu usemi…
Mheshimiwa Naibu Spika, hicho ni Kiswahili cha mwambao. (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka ninukuu usemi wa hekima aliosema Rais Mstaafu kipenzi cha nyoyo, Jakaya Mrisho Kikwete. Hivi karibuni alisema hivi, unapokuwa mpya watu wanataka mambo mapya, lakini yawe mapya ya kimaendeleo siyo mapya ya kuharibu kule tulikotoka. Huu ni usemi mmoja wenye hekima sana kwa Rais wetu yule mpendwa mstaafu, Mungu amjalie akae kwa amani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hizi taarifa za CAG ndizo zilizosaidia kuonesha madudu makubwa sana yaliyofanyika ndani ya nchi hii lakini leo hata CAG amelalamika kushindwa kwenda kufanya verification kwa sababu hakupewa bajeti ya kutosha. Mnataka kuficha nini ikiwa CAG sasa hapewi uwezo wa kwenda field kuangalia uhalisia wa mambo yanayofanyika? Mmeanza kubana Bunge lisionekane live, mmeanza kubana mikutano ya vyama vya siasa, mmeanza kumbana mpaka CAG asiende kwenye kazi zake? Tunawatendeaje haki Watanzania? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni hatari na kama huko tunakokwenda mwendo wenyewe ndiyo huu jiangalieni upya. Mliwaambia Watanzania mnaleta ajira, mnaleta maisha mazuri, mnaleta afya, Watanzania wakawaamini na kuwapa kura zao sasa fanyeni yale mliyowaahidi Watanzania msiende kinyume chake. Siku ya hukumu inakuja na haiko mbali, siku zinakwenda kweli kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeshangazwa na jambo lingine na mimi nataka niliseme kwamba Kamati ya PAC wamelalamika hapa na mchangiaji mmoja amelalamika anasema wametaka taarifa ya madeni ya TIB wamenyimwa. Hili ni kosa lingine la uhaini kabisa kwa Kamati ya Bunge kunyimwa taarifa ili wafanye kazi zao. Hili Bunge linaonekanaje sasa? Hili siyo Bunge tulilotokanalo sasa tunataka kuchezewa na sisi tumekubali kuweka videvu vichezewe, haiwezekani! Ni lazima tuoneshe wajibu wetu kama wawakilishi wa wananchi ni vipi tumeisimamia Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Kamati yangu hatukukubaliana na hili na TIB walileta orodha yote ya waliokopa Community Import Support tukawa nayo. Kwa hiyo, haiwezekani ni lazima wakubaliane na matakwa ya Kamati za Bunge, hakuna namna nyingine, ahsante sana.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nimshukuru Mwenyezi Mungu kunijaalia kupata nafasi na mimi kuchangia kidogo na nikushukuru na wewe kwa kunipa nafasi hii na shukrani kwa pekee zizidi kwako na nikuhakikishie tu kwamba uwepo wako katika kiti hicho unatupa raha ndani ya roho zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka nizungumzie nikiwa nimejieleza wazi kwamba ni Mjumbe wa Kamati hii ya Viwanda na Biashara na nimpongeze kwa dhati Mwenyekiti wetu. Kati ya Wenyeviti makini wa Kamati hizi za Bunge, Mheshimiwa Dalaly Peter Kafumu naweza kusema ni nambari moja.
Sasa katika Kamati zetu siku moja, alikuja mchumi fulani akatuambia kwamba wawekezaji ni kama ndege, kule wanapokuwa wanaruka angani wanaangalia ni nchi gani inafaa kuwekeza ndipo wanaleta uwekezaji wao. Na kati ya vigezo muhimu sana vinavyowavuta wawekezaji na vivutio muhimu sana, kimojawapo ni amani na usalama katika nchi. Wawekezaji wanaangalia mazingira ya usalama ndani ya nchi, hayo yanawafanya wawe na umuhimu wa kukaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwenendo tunaokwenda nao sasa hauashirii kuwakaribisha wawekezaji katika nchi yetu. Juzi tu hapa wakati nauliza swali nilimshukuru Mwenyezi Mungu sana kwa kuijaalia nchi yetu kuwa ni miongoni mwa nchi ambazo haziko katika janga, tishio la ugaidi, hili ni jambo la kushukuru sana na tumuombe Mungu azidishe hilo. Lakini jambo la kusikitisha, Mheshimiwa Waziri, ninaemuheshimu sana alikuja akalipinga hilo na akaona kwake yeye ni bora kusema kama nchi yetu ni miongoni mwa nchi zilizo katika tishio hilo, ni kitu cha ajabu sana. Mimi namheshimu sana Mheshimiwa Mwakyembe, lakini ningeweza nikadhani labda sijui kuna kitu kimemvuruga au vipi lakini tuyaache hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hilo dogo, leo hii tunashuhudia vitu vya aibu ambavyo vinafanyika ndani ya nchi. Leo hii mtu mmoja anayejipa madaraka ambae aliwahi kujiita Mungu wa Dar es Salaam anafikia hadi ya kutaja majina ya wawekezaji na wafanyabiashara wakubwa kwamba hao ni drug dealers wakubwa sana, kitu ambacho wale wawekezaji tayari wanatafakari upya na kuendelea kuwekeza kwao, je, hawa walioko nje watajifikiriaje kuja kuwekeza katika nchi yetu? Upande mmoja tunahimiza wawekezaji waje kuweka viwanda, upande wa pili tunawa-harass wawekezaji juu ya uwekezaji wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii ina mfumo kamili wa ulinzi wala sidhani kama umetetereka. Kuna Jeshi la Polisi, kuna Waziri wa Mambo ya Ndani makini sana tunayemuamini, mchapa kazi, kuna vyombo vya ulinzi wa usalama makini sana, kuna Usalama wa Taifa tunaamini ni makini sana, kuna Jeshi la Ulinzi ni makini sana. Leo vyombo vyote hivi vimeonekana havina maana, father god wa Dar es Salaam aliyejiita Mungu wa Dar es Salaam ndiye amejipa jukumu la kusema kila kitu katika nchi hii? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mungu wa Dar es Salaam leo anaweza kumtaja yoyote na isiwe lolote siku ya pili anatoa amri aje central police, ni nani huyu katika nchi hii?
Waheshimiwa Wabunge, vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vilipopewa jukumu la kusimamia mambo haya muhimu ya ulinzi na usalama, dawa za kulevya na everything vimelala wapi? Vinamuachia Makonda aliyejibatiza kujiita Mungu leo anafanya kila kitu, ni nini, what for, tunakwenda wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi leo nataka niliseme hili kwa sababu azma ya kuwekeza kwenye viwanda haiwezi kwenda kwa matamshi ya ajabu ajabu na maamuzi yanayotolewa na mtu mmoja kwa sababu yeye kauli yake inaonekana inasikilizwa sana na Mheshimiwa Mtukufu Rais, haiwezekani. Mimi nadhani sasa kila mmoja atajua wajibu wake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa la mwisho mimi nataka kumwambia ndugu yangu Waziri, Mheshimiwa Waziri nia yako nzuri ya kuimarisha viwanda na mimi nakubaliana na wewe lakini Mheshimiwa Waziri kila mchezo una sheria zake. Kwenye riadha ile kuna mbio za vijiti. Huwezi kukimbia tu ukafika…..
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante,
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia leo kuwepo hapa katika hali ya uzima. Pili, nakushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi hii kuweza kuchangia hotuba hii muhimu iliyopo mbele yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kuchangia naomba kwa heshima kubwa tu nimwombe Mheshimiwa Waziri Mkuu na nimwombe Mufti Bulembo kidogo ampe nafasi Mheshimiwa Waziri Mkuu ili atusikilize. Naomba tu Mufti Bulembo, tafadhali!
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nachukua nafasi hii kwa dhati ya nafsi yangu kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kumteua Profesa Kabudi kuwa Waziri wa Sheria na Katiba. Hii inatoka ndani ya moyo wangu. Sambamba na hilo, nampongeza kwa kumwondoa Mheshimiwa Mwakyembe katika nafasi hiyo na kumpeleka katika Wizara ile ya kucheza; atacheza, sasa tunamwona anapiga makofi uwanja wa Taifa. Huu ni ujumbe tosha kwamba akufukuzaye hakwambii toka, waona nyendoze zimebadilika; waweza ukae, huwezi ondoka. (Kicheko/ Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuipongeza sana Kamati ya Katiba na Sheria. Naipongeza kwa dhati sana kwa kuacha mapenzi ya vyama na kueleza lile lililo sahihi na la ukweli kwa mustakabali wa nchi yetu. Nawapongeza kwa dhati kwa kuona umuhimu wa kumwambia na kumweleza Msajili wa Vyama vya Siasa kama yeye wajibu wake ni kuvisajili na kuvilea vyama vya siasa na siyo kuvifarakanisha vyama vya siasa. Atekeleze wajibu wake na siyo kufanya mambo kwa mapenzi yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba sana utusikilize. Mheshimiwa vyama hivi, mpaka chama kinaposimama kuna mambo mengi kinayopitia. Siyo jambo rahisi; vimeundwa vyama zaidi ya 20 ndani ya nchi hii, lakini hadi leo vyama vilivyosimama ni vyama visivyozidi vinne. Leo kwa sababu tu ya ulevi wa madaraka wa mtu mmoja, anatumia nafasi yake kufanya hujuma za waziwazi kwa ajili ya kukiteketeza Chama cha Wananchi - CUF, hilo jambo siyo sahihi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunasikitika sana kwamba amani ya nchi yetu ni miongoni mwa sekta muhimu ambayo vyama vya siasa wanabidi kuvisimamia inavyopasa. Leo hii tunaona yanayofanyika, tunaona jitihada zinazofanywa hata kumbeba yule kibaraka anayetumiwa na wanaomjua; baada ya kufanikiwa kuingia Buguruni, leo wanaandaa njama za kuvamia katika Makao Makuu ya Chama Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, haya yanafanywa chini ya usimamizi wa watu wanaojulikana na kuna Waziri mmoja wa Zanzibar anaitwa Hamad Rashid ndiye plan master wa kuandaa mambo haya kwa kushirikiana na Makamu wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ally Iddi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunasema wazi haya ili dunia ijue na Watanzania waelewe. Haya yanayotokea kwetu siyo ya bure, ni mambo yamefanywa. Haiwezekani mtu anaacha chama mwenyewe zaidi ya mwaka mmoja anaenda kukaa huko, anarudi anajishauri. Hata kama ni mke, unakuta ameshaolewa na watoto ameshazaa na mume mwingine. Haiwezekani! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, haya yanayofanyika kwetu, leo hii nitashangaa nisikie Sofia Simba leo karudi kajitangaza tayari ni Mwenyekiti tena UWT. Hamtakubali! Kwa hiyo, kuchochea hayo katika vyama vyetu vya upinzani ni jambo la athari mbaya, jambo ambalo halitaipeleka Tanzania
katika neema ambayo tunatarajia kuipata kwa Mwenyezi Mungu.
Mheshimiwa Naibu Spika, neema ya Mwenyezi Mungu inakuja kwenye masikilizano. Msituchochee ndani ya Vyama vya Upinzani ili mkidhi haja zenu. Haiwezekani! Mlipoomba kura kwa Watanzania, mlisema Watanzania mtawaletea maendeleo, mtaleta elimu, maji; hamkusema kama
mtafitinisha vyama vya siasa ili mambo hayo muweze kuyapata. Haiwezekani! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tukae tufikirie, tunapoandaa uwanja; tunapopanda nyasi tucheze vizuri, msitupandie michongoma ili tuumie miguu yetu. Haiwezekani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani ujumbe huo umeupokea, naomba tufanye kila linalowezekana lililo ndani ya uwezo wenu, Serikali isaidie kutatua migogoro hii na isiwe wao ndio sababu ya kuimarisha migogoro hii. Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, hivi karibuni katika vyombo mbalimbali vya habari ilitangazwa kwamba Watanzania tuko nafasi ya 153 kwa kukosa furaha duniani. Kwa kweli hili jambo lilinisikitisha, lakini halikunipa homa sana, lakini sasa baada ya kukosa furaha, inakuja Tanzania tunajengewa hofu ya lazima. Hili la furaha tungeliacha mbali,
lakini hofu ambayo Tanzania tunajengewa sasa ndiyo jambo ambalo linanitisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, matokeo haya yanayotokea ndani ya nchi sasa hivi katika tawala zote zilizopita hatukuzoea kuyaona. Wamepita Marais kadhaa na Mawaziri Wakuu kadhaa, hatukuona matukio yanayotokea ndani ya Tanzania yetu ya leo. Leo hivyo vikosi vinavyokwenda
vinachukua watu na kuwapeleka ambako hakujulikani na bado sisi Watanzania, sisi Wawakilishi wa wananchi wa Tanzania tuliomo humu, kama hatukusemea hili na Serikali ikawajibika katika hili, itakuwa hatutendi haki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kundi la swala, anaweza akanyakuliwa mmoja, wawili na swala wakaendelea na safari, lakini siyo kundi la binadamu, kundi la Watanzania. Iwezekane yafanyike hayo na bado sisi tuendelee kufanya mambo mengine; hili jambo ni la hatari. Leo Mheshimiwa Bashe amesema, kama kuna orodha ya Wabunge kumi ambao wako listed haijulikani ni nini kitakachowapata wakati wowote. Mimi nimeingiwa na homa, sijui kama na mimi nimo! Eeh, Mungu wangu, tulinde waja wako na hizi hujuma ambazo hatujui nani anayeziandaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kitu cha hatari! Mheshimiwa Bashe anasema amepata taarifa kutoka kwa baadhi ya Mawaziri wa Serikali; hili siyo jambo dogo. Nadhani leo sisi Wabunge tusingekuwa na lingine la kujadili zaidi ya kufikiria hili. Kama kuna list ya Waheshimiwa Wabunge, hao raia wadogo wao wakoje?
Mheshimiwa Waziri Mkuu, tunajadili bajeti ya maendeleo, maendeleo yapi yatakayopatikana wakati tayari tumejengewa hofu ya namna hiyo? Maendeleo yanaletwa pale watu wanapokuwa na amani, wanapojadili mambo kwa uwazi, wanaposema kwa uwazi; na mambo yale wakakaa wakapata muda wa kuyafikiri. Leo ikiwa Wabunge kumi hatujui, Mheshimiwa Selasini sijui yuko, sijui nani yupo, tunakaa sasa kila mmoja ana maswali ndani ya moyo; haijulikani ni nani yumo kwenye hiyo list, hebu Serikali tutoleeni hofu juu ya haya mambo. Tutoleeni hofu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo Wafanyabiashara hawana furaha, Wamachinga hawana furaha, Wanasiasa hawana furaha, bodaboda hawana furaha; sasa jamani ikiwa kila mtu hana furaha na kila mtu anaiishi kwa hofu, ni Tanzania ipi tunaipeleka na ni wapi tunaipeleka? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo anayeapa nambari moja Tanzania ni Mheshimiwa Rais, anaapishwa mbele ya Watanzania wote wanaona. Leo Mheshimiwa Rais baada ya kula kiapo kulinda na kuitetea Katiba, ni wa mwanzo anayetangaza vyama vya siasa ni marufuku kufanya mikutano ya kisiasa katika nchi hii. Hebu niambieni, ni nini kinachofanyika? Vyama vya siasa mnavipa ruzuku; sasa mnavipa ruzuku waende wakale na wake zao? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mnawapa ruzuku wajitangaze watoe elimu ya siasa, elimu ya uraia, wajipanue wapate wanachama ili siasa za ushindani zitendeke ndani ya nchi. Leo mnawaambia tunawapa ruzuku, lakini ni marufuku kufanya mikutano ya vyama vya siasa. Maana yake
nini? Sasa wataenda kuvizuia vyama vya siasa kupewa ruzuku, mnamchukua kibaraka Lipumba, mnamchotea mahela ya Serikali, anaenda kutumia anavyotaka yeye. Hiyo siyo sawa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana, haya mambo anayefikiria kwamba kufa kwa CUF ndiyo neema yenu Zanzibar, anajidanganya. Ziko roho zilizotangulia kwa ajili ya CUF na ziko tayari roho nyingine kuzifuata kama mtafikiria kukifuta Chama cha Wananchi – CUF. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsanteni sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mungu pekee kwa sababu ni dakika tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, muongeaji anasema mwanadamu uvumilivu unapomuishia anakuwa ni afadhali mnyama kuliko mwanadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatukumuacha Lipumba na vibaraka wake na wanaomtumia kwa sababu

tunamuogopa, hapana. Tulimuacha kwa sababu Watanzania na dunia ijue ujinga wao na hao wanaomtumia kufanya ujinga ule. Watanzania waelewe ujinga wa Lipumba na hao wanaomtumia kudhihirisha ujinga wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyama vya siasa vipo kwa mujibu wa sheria. Vyama vya siasa waasisi wa kuleta vyama hivi vya siasa mmojawapo ni Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, mnamuita Baba wa Taifa na sisi tunakubali ni Baba wa Taifa, hawezi kutokea mjanja akamuona Baba wa Taifa aliyekubali vyama vingi vije nchi hii ni mjinga yeye ndiyo mwerevu, huyo ni zumbukuku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme wazi kwamba mgogoro unaoendelea ndani ya Chama cha Wananchi (CUF)kwa kupandikizwa na watu tunaowajua, akiwemo Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani wa Tanzania, Mheshimiwa Hamad Yussuf Masauni. Mheshimiwa Waziri umesema maneno makubwa sana nakuheshimu na katika Mawaziri kwenye Bunge hili ninaowaheshimu ni Mheshimiwa Mwigulu, lakini msaidizi wako hafai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umesema Mheshimiwa Waziri hakuna ushirika wowote wa waovu utakaoweza kuishinda haki, nakubaliana na wewe sana. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri Masauni umekuwa ukifanya mambo kadhaa kwa kushirikiana na hao mnaoona wanaweza kuiuwa CUF, lakini nikuambie hukuijua ilivyozaliwa na hutoishuhudia ikifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kuna matukio 13 ya utekwaji wanayofanyiwa watu wa CUF na bado watu wa CUF tumeendelea kudumisha amani na kuvumilia. Hivi niambieni yule mwendawazimu aliyetumwa na hawa akina Maftaha juzi, akapigwa pale, kama siyo uvumilivu na ukomavu wa watu wetu, angekuwa hai leo? Angekuwa hai leo kama si ustaarabu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wetu, chama chetu, viongozi wetu wameendelea kuilinda amani na kuhakikisha damu haimwagiki kama anavyotaka Mheshimiwa Masauni imwagike ili apate sababu ya kufuta chama chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Hamad Masauni juzi uliratibu kikao cha kuhakikisha Tanga Mwenyekiti wetu hafanyi kikao, wewe kwa kushirikiana na Mheshimiwa Maftaha pamoja na mungiki wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumevumilia vyakutosha, hatumuogopi Lipumbana ninakuambieni sasa tunamnyoosha Lipumba na watu wake…

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwezo wa kumnyoosha tunao, nia ya kumnyosha tunayo na sababu ya kumnyosha tunayo.(Makofi)

Uvumilivu umetuishia, na ninakuambia hawa mungiki kwetu hawajai kwenye mkono mmoja.

Hawa ni wadogo sana, Chama cha Wananchi ni kikubwa sana ndani ya nchi hii, tunawaambia ifike mwisho na wakome, tupo tayari kwa lolote, lakini tutamnyoosha Lipumba na watu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie suala la mrundikano wa mahabusu mahakamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imezungumzwa sana kuhusu mrundikano wa mahabusu ndani ya magereza yetu. Hivi karibuni tunakwenda kwenye mfungo wa Ramadhani ilhali Masheikh wa Uamsho bado wakiwa gerezani wanaendelea kukaa bila kufikishwa mahakamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, mungiki tutawanyoosha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nichukue fursa hii adhimu kuwatakia kheri na baraka Waislamu wenzangu katika Mfungo huu Mtukufu wa Mwezi wa Ramadhani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nianze na utangulizi ufuatao. Tarehe 25 Oktoba, 2015, Watanzania walifanya maamuzi ya kumchangua Rais, John Pombe Magufuli kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tunakubaliana hilo halina hoja wala dawa, ni jambo lilitokea na sisi tunakubali.

Hata hivyo, Watanzania hao hao sambamba na kumchagua Rais waliwachagua Wabunge hawa kuwa ndiyo kioo cha kuisimamia, kuielekeza na kuishauri Serikali yetu. Kwa hivyo, tulichaguliwa pamoja naye Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo, ana wajibu mkubwa sana kutusikiliza vizuri sana na kupitia Waziri Mkuu mimi ningependa tu mpelekee salamu moja Mheshimiwa Rais ya upendo, kwamba tulichaguliwa pamoja naye kwa hivyo ayape uzito sana tunayoyasema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa uchaguzi ule kuna wenzetu wengine walitukimbia hapa, waliondoka wakati mbaya sana, kuna wengine walikwenda Rwanda kuona dada wenye shingo refu kule, lakini leo wamerudi hapa Mheshimiwa Rais ndiyo anawafanya watu wa karibu sana kuwaalika Ikulu kila linapotokea jambo, hawafai hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati ule wa mapambano ilikuwa tukae pamoja kuivusha nchi yetu katika uchaguzi ule wapo tuliokuwa naye na hatutamuacha, aendelee kushirikiana na sisi, aachane na wale wengine wababaishaji, hawatamsaidia. Mheshimiwa mpe hiyo salamu, ahsante sana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie habari ya wafanyabiashara, inaonekana Waziri Mkuu hukunifahamu lakini nitakuja kwenye meza yako nikupe vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafanyabiashara si maadui, wafanyabiashara wa Tanzania ni watu tunaowategemea sana katika kuleta pato la nchi hii. Katika nyendo tunazokwenda nazo hivi sasa kauli zetu, kauli za viongozi haziashirii wema kujenga ukaribu na wafanyabiashara badala yake tunajenga uhasama na chuki na wafanyabiashara jambo ambalo halitatuletea tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapotaka kuvuna maziwa mengi katika ng’ombe lazima tumlishe vizuri, usitegemee ng’ombe usiyemlisha utapata mavuno mazuri, hutapata maziwa yanayostahiki. Kwa hiyo, tunatakiwa tuangalie, hivi sasa tunakuwa na tabia hasa Mawaziri wetu mnakuwa na ile kitu kuona mseme yale yanayompendeza Mheshimiwa lakini hamtaki kumwambia hali halisi tuliyonayo katika nchi. Sasa hivi Kariakoo mlango wa biashara ulikuwa unatoa kilemba mpaka shilingi milioni 30 kuupata kabla ya kulipa kodi lakini sasa hivi wafanyabiashara wenye majumba wamekosa kabisa wafanyabiashara wa kukodisha fremu za milango. Hiyo ni ashirio moja kwamba biashara inakokwenda sio kuzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuna wajibu wa kukaa nao wafanyabiashara tukaona ni kipi kinachowakwaza. Jana alisema mwenzangu mmoja hapa hamtangazi tena mapato ya kila mwezi lakini iko sababu kwa nini hamtangazi. Tuliwaambia mwanzo mnachokusanya ni arrears zinazotokana na malimbikizo ya nyuma zikimalizika hizi makusanyo hayo tunayojidai nayo yatakuwa hayapo tena na ndicho kinachotokea sasa. Likija suala la mapato Taifa linakuangalia wewe Waziri nakushauri hebu tukae na wafanyabiashara tuangalie yanayowakwaza ili tupate njia ya kutokea. Sasa hivi tumekwama na tunapoelekea ni kubaya zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo nataka niseme habari ya kodi wanayotozwa watu wenye magari mabovu, jana mwenzangu mmoja alizungumzia na mimi nataka kulirudia. Elimu ni kitu muhimu, Watanzania unapokuja mfumo mpya wa kodi au jambo jipya ni lazima kwanza waelekezwe. Mfano mtu alikuwa na gari amenunua limekufa miaka 10 nyuma lakini leo akinunua kigari chake kingine akienda TRA anaambiwa gari hii uilipie kodi zote za miaka 10, hii kweli ni haki? Haya mambo yapo na sasa hivi imekuwa ni shida kubwa sana kwa watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi napendekeza Mheshimiwa Waziri, ili gari litembee lazima lipate mafuta, tuhamishie hayo mengine hata kama ni percent ndogo iwekwe kwenye mafuta kwa sababu gari linalotembea litakuwa linatozwa pale gari linapotumika, gari likifa itakuwa hakuna tena kesi baina ya raia na Serikali. Sasa inakuwa tunajenga uadui, wananchi wanaona TRA kama maadui wakubwa na siyo hivyo, nchi za wenzetu wafanyabiashara ni marafiki wakubwa na vyombo vinavyokusanya kodi, kwa nini sisi tunakuwa mahasimu wakubwa? Ni kwa sababu nakuwa na sheria za mwendo kasi, halichachi, ni pale mnapoamka mkaamua kufanya mnafanya, haiwezekani. Lazima tuwaandae watu wetu linapotokea badiliko la kisheria ili watu wajiandae na hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie misaada ya nje ya nchi ya wahisani. Hakuna asiyejua kwamba nchi yetu misaada tuliyokuwa tukipata toka Millennium Challenge Account imekatika na haikukatika kwa bahati mbaya wameacha kutusaidia kwa sababu walizoziainisha mapema. Waliainisha mambo mawili wakisema wao hawatakuwa tayari kuendelea na ufadhili kwamba mambo haya ndani ya nchi hayakushughulikiwa nayo ni suala la uchaguzi wa Zanzibar na suala la Sheria ya Mitandao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mambo mawili wahisani walitueleza wazi na bahati nzuri sana Waziri wa Mambo ya Nje nilimsikia kwa masikio yangu akisema kwamba; “haya ni mambo madogo, tutayashughulikia haraka na ufumbuzi utapatikana” yaah, ndiyo alivyozungumza. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea kwa kauli ile murua, mwanana, burudaa wal asilia, jambo hili litapatiwa kweli ufumbuzi. Niwaulize wenzangu mmeshindwa nini? Utawala wa JK tulikuwa na changamoto za kiuchaguzi lakini watu walizungumza wakafikia makubaliano na nchi ikaenda, nchi haikuzuiliwa misaada, tatizo nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwetu sisi lililokuwa kubwa lipi ambalo halizungumziki. Watanzania ni wamoja, linakuja jambo, msaada ule wa Millennium Challenge ulikuwa ukisaidia sana umeme vijijini, leo sababu ya Wazanzibar milioni moja na nusu na Watanzania milioni 50 wanakosa msaada ule muhimu kwa upande wa Tanzania Bara, kwa jambo ambalo tungeweza kukaa kuzungumza kwani kubwa lipi sisi tunatoa moto kwenye midomo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, maneno asali tunatoa midomoni mwetu, kwa nini nyie msitoe maziwa tukawa karibu, tatizo nini? Msaada ule bado ni muhimu, kweli kuomba ni aibu, lakini ukiwa huna omba kuliko kuiba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nasema bado tuna haja na Waheshimiwa Wabunge nawasikia kila siku hapa likija suala la umeme vijijini kila mmoja ananyanyuka REA, REA, hakuna REA ile pesa haiko, mimi nawaambia, tusidanganyane. Ile pesa kubwa iliyokuwa ikitupa kiburi kuendeleza miradi ya REA ya umeme vijijini imekatika kwa sababu ya mambo mawili tu, Sheria ya Mtandao na Uchaguzi wa Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukizungumza uchaguzi wa Zanzibar wengine mnakasirika na huu Mwezi wa Ramadhani sipaswi kumkwaza mtu, nasema kwa lugha nyepesi sana kwa lugha ya maziwa na asali tukaeni tujadili tuone umuhimu wa kuzishawishi nchi za European Union kurudisha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. HAJI KHATIB KAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu, muumba wa mbingu na dunia kwa kuniamsha salama siku ya leo nikiwa na afya na kuweza kufunga funga ya mwezi Mtukufu wa Ramadhani. Vilevile niwatakie Ramadhan Mubarak waislamu wote duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kutoa mchango wangu kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na Wizara kwa ujumla baada ya kuhoji kwa muda mrefu na kutaka wananchi wa Kisiwa cha Pemba waweze kufikishiwa elimu ya Mtangamano wa Soko la Afrika Mashariki. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kumshukuru Mheshimiwa Waziri, niseme kwamba elimu ya mtangamano ya Afrika Mashariki haikuwafikia walengwa. Hii ni kutokana na kwamba wakati wa maandalizi Wabunge wa Pemba hawakushirikishwa, hasa mimi ambaye muda wote wakati nikiwa kwenye Kamati nimekuwa nikihoji ni lini wananchi wa Kisiwa cha Pemba hasa kule Kaskazini watafikishiwa elimu hii ambayo itaweza kuwasaidia na kuweza kujua wajibu wao na haki katika Soko la Afrika Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kisiwa cha Pemba, hasa Kaskazini Pemba, wananchi asilimia kubwa ni wavuvi. Wavuvi hawa kila mwaka, inapofika mwezi wa kumi hadi mwezi wa tatu wamekuwa wakisafiri kwenda nchini Kenya kufanya dago. Ni wazi kwamba wanakuwa wakipata matatizo na wananchi wangu wamewahi kufungwa nchini Kenya miezi sita na faini ya shilingi 20,000 juu. Kwa hiyo, hii ni kutokana na kwamba wananchi hawa hawajui wajibu na haki zao katika soko hili la Afrika Mashariki. Ndiyo maana nikasema kwamba wananchi wa Kisiwa cha Pemba hasa wale walengwa hawakufikiwa na elimu hii ya mtangamano wa soko la Afrika Mashariki ambayo ni muhimu kwa wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema Desemba, 2015/2016 wapiga kura wa Jimbo langu wapatao 130 walifungwa kwa kuonewa. Hii yote ni kutokana na kwamba hawajui wajibu wao na ndiyo maana nikasema walengwa hawakufikiwa na elimu hii. Naomba nishauri kwa Mheshimiwa Waziri kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, endapo mara nyingine Wizara itaandaa utaratibu wa kwenda kutoa elimu ya mtangamano wa soko la Afrika Mashariki, basi ibadilishe maneno, badala ya kusema Wizara inaenda kufanya semina, basi maneno yasemwe kwamba tunaenda kutoa mafunzo. Hii itasaidia wale walengwa hasa kuweza kufikiwa na elimu iliyokusudiwa. Kwa kuwa Pemba ina sehemu kuu mbili, naomba na ninamshauri Mheshimiwa Waziri kwamba elimu hii igawanywe katika sehemu kuu mbili; katika Kisiwa cha Pemba kuna sehemu ya Kaskazini na Kusini, kwa hiyo, ni vyema katika taaluma hii au uelewa huu ugawanywe katika sehemu mbili ili taaluma hii iweze kuwafikia kama ilivyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, niseme kwamba katika taaluma hiyo hiyo ya Soko la Afrika Mashariki, yaani mtangamano ni vyema Wizara itapanga utaratibu na kuhakikisha kwamba Wabunge kutoka Pemba wote wanashirikishwa wakati wa maandalizi katika hoja hiyo ambayo itakuwa imepangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, ili kuondoa matatizo ambayo wavuvi wetu ambao wamekuwa wakiyapata hadi kufugwa jela nchini Kenya, ni vyema Serikali hizi mbili…

MWENYEKITI: Ahsante.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. KHATIB S. HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia name kusimama hapa mchana wa leo siku tukufu ya Ijumaa ili name niweze kusema machache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nianze kuwapongza kwanza Waheshimiwa Wabunge wenzetu wote walionekana na Mheshimiwa Rais wanafaa kuwa Mawaziri na wamepata uteuzi ule, nawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee napenda nimpongeze kwa dhati kabisa Mheshimiwa Mbunge mwenzetu Lazaro Nyalandu kwa uamuzi wake mtukufu kabisa wa kuamua kuhama Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza kwa dhati na niwaombe wenzetu pale wenzetu wanapofanya maamuzi wa huku kuja huko au wa huko kuja huku isichukuliwe ni uadui tunabadilishana tu kila jambo na wakati wake, msianze kuwapa majina mabaya mukasema wanarembua macho, ni mafisadi hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna orodha ya wote mnaowadhania huku hawafai kuweko huko hawa hawatafaa kuweko huku, kwa hivyo mnabidi muwaeleze mapema kama ninyi hana sifa kuwepo. Msingoje akitoka huko akija huku ndio mnaanza kufichua mabaya yake kichokuwa shinda kukila msikitie hila. Ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye Mpango, kwa mara ya kwanza baada ya Mheshimiwa Spika juzi kuwataka Wabunge wafunguke kuishauri Serikali kuhusiana na Mpango huu nimefurahi kuona kwamba hakukuwa na utofauti bali walikuwa ni Wabunge wote wa Bunge hili kutoa mawazo ya kuionesha Serikali pale inapokosea na inapotakiwa kujirekebisha. Kwa dhati kabisa niwapongeze Mheshimiwa Bashe, Mheshimiwa Serukamba, Mheshimiwa Msigwa, Mheshimiwa Sugu na wenzao wote ambao haionekani tofauti ya kiitikadi ya kivyama bali wote tunalenga katika kuilekeza Serikali maana na uhalisia wapi tunataka kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika yote kwa dhati, nimwambie Mheshimiwa Mpango, katika mambo yaliyotusikitisha hapa wengine ni pale Wajumbe wa Kamati ya Bajeti wanaposimama hapa na wakasema kwamba unakaidi kupokea mashauri na maelekezo yao. Sasa kama Kamati ndiyo wawakilishi wa Bunge zima katika sekta wanayoisimamia kwa hivyo unapoanza kuidharau Kamati katika mashauri wanayokupa maana yake ni kwamba hata sisi humu utatupuuza lakini na sisi tunatimiza wajibu wa kusema yale tunayoona yanafaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo dhamira ya Rais wetu na mpango mkuu wa kufufua viwanda hatuoni mafanikio yanayopatikana kama wenzetu walivyosema kwamba kuiachia Serikali kila kitu itekeleze kwa pesa yake hilo jambo haliwezekani. Hayo ni mashauri ya kutaka private sector iingie katika kuendesha biashara ili tukwamuke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikupe mfano mdogo, leo ni mwaka wa 10 Mheshimiwa Mpango tumekuwa tukiimba nyimbo ya kukifufua Kiwanda cha General Tyre cha Arusha lakini hebu niambie leo tumefikia wapi?

Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Viwanda na Biashara, tumefanya ziara mara kadhaa, tumependekeza mara kadhaa, kama kuna umuhimu wa viwanda vya sukari pia katika kiwanda muhimu katika nchi ni kiwanda cha matairi.

Leo hebu niambieni ni Mbunge gani anayefika hapa bila kutumia gari? Gari linakwendaje bila tairi? Mahitaji ya tairi ni makubwa sana. Kama tunashindwa kufufua kiwanda muhimu kama kile ambacho ukiangalia kwa umakini soko la matairi yatakayozalishwa pale ukienda kwenye Taasisi za Serikali na Mashirika ya Umma pekee hawawezi kulibeba soko la matairi yatakayozalishwa pale General Tyre, tunataka nini?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante nakushukuru, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kusimama hapa kutoa mchango wangu katika Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, lakini nataka nianze kwa salamu moja ya pongezi kwa dhati kabisa kwa Mheshimiwa Waziri na Wizara yake kwa jambo moja kubwa la udugu walilolifanya, kwa sababu tunaelewa kama Serikali Tanzania tunazo Serikali mbili na zote Serikali mbili ni za Chama cha Mapinduzi. Kwa hiyo, udugu wa Serikali hizi mbili umedhihirika mara hii kwa udhati pale walipoweza kulitamka gawio halisi la Zanzibar la shilingi bilioni 200 kwa kweli tunawashukuru. Huu ni udugu na hii imeonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nilifuatilia Baraza la Wawakilishi, wawakilishi wakihoji hela zile zimefikia wapi na Waziri alikosa jibu, Waziri wa Zanzibar alikosa jibu. Kwa hivyo namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kutueleza hapa atuambie pesa hizi zimekwenda wapi au zimekwama wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili, kidogo nitakuwa tofauti kabisa na wenzangu leo na ninaomba mnisamehe sana kwa sababu katika mwezi ambao huu tunapaswa kusema ukweli ni huu. Kwa hiyo leo nataka niwe tofauti kidogo na wenzangu wa upinzani, katika jambo la kuikosoa Serikali kupita kiasi hasa kwenye masuala haya ya hela. Nasikia na nawaona wenzangu mnavyosimama sana kuhoja shilingi trilioni 1.5, mimi sikuihoji mimi nimetaka zile bilioni 200 Zanzibar ziende. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na nasema hivi kwa sababu mbora wa mkosoaji ni yule anayeanza kujikosoa mwenyewe. Na kuna mwana mashairi mmoja alisema; “mtu akitaka sema kwanza hutazama lake, akajigeuza nyuma kutizama aibu zake, ni aibu kusimama kuyasema ya mwenzake.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema haya kwa nini? Mheshimiwa imetolewa ripoti wote tumeng’anga’nia kwenye shilingi trilioni 1.5. Lakini kwenye ripoti hiyo hiyo kuna maelezo yaliyotolewa kuhusu utumiaji mbaya wa fedha za rukuzu zinazotolewa na Serikali. Jambo hilo naomba tusikilizane, leo sihitaji makofi nahitaji mnisikilize.

Mheshimiwa Spika, Chama cha Mapinduzi kimeguswa kwamba kuna maeneo hayako sawa, CHADEMA kimeguswa, ACT kimeguswa chama changu mwenyewe kimeguswa. Sasa mimi nitaacha vyote vilivyoguswa. Na wengine wameguswa wamepeleka hesabu lakini, zina makando kando. Bahati mbaya sana chama changu ambacho nimesimama hata taarifa hakikupeleka. Hata taarifa kwa Mkaguzi hazikupelekwa, hivi mimi napata wapi ujasiri wa kukosoa shilingi trilioni 1.5 wakati chama changu kinachopokea 120 million per month kimeshindwa kupeleka hesabu kwa Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali, inanipa shida sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nayasema haya nikijua kwamba Katibu Mkuu cha Chama ndiye Accounting Officer na ndiye Masuhuli wa kujibu mambo yote yanayohusiana na pesa za chama. Naelewa na ninajua na nitaka nikufahamishe kama ni mtu ninaye mheshimu sana Katibu Mkuu wangu Maalim Seif Sharrif Hamad, lakini katika hili naomba nieleze ukweli, kwamba kwa kweli hajakitendea haki chama hiki kuacha kupeleka hesabu zinazotakiwa kwa Msimamizi Mkuu wa Hesabu za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, whatever tuna vyombo vinavyopaswa kufanya kazi ya kulinda fedha za chama. Naomba mnisikilize vizuri, sitamtaja yeyote kuhusiana na kutokushindwa kupeleka hesabu, nitamtaja Katibu Mkuu wa chama changu. Sasa kama kuna mengine yanayojificha naomba sasa TAKUKURU, Waziri wa Mambo ya Ndani, ahojiwe Katibu Mkuu aeleze ni kwa nini hakupeleka hesabu kwa Msimamizi wa Hesabu za Serikali. Tuanze hapo ndio nasema Mbora wa mkosoaji huangalia aibu zake kabla ya kusema za wenzake. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, haya mambo yanataka ujasiri sana. Itakapokuja tokea kwa bahati mbaya yakaja yakatoa ya kutokea naomba Kanuni ile inayomlinda Mbunge kwa anayozungumza humu itumike kikamilifu. Yasije yakaenda ya mwendo wa kasi kama yaliyowakumba wenzangu. Nakuomba sana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naamini niliowataja wanaohusika na vyombo vya upelelezi watalifanya hili kwa sababu Mheshimiwa Spika ameliunga mkono kwa hiyo sitaki longo longo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nizungumzie suala la pili, kwa muda mrefu tumekuwa na kilio. Zanzibar hapa tunapozungumza siku zote mafuta ya petroli yanakuwa na tofauti kati ya 200 au 300 zaidi juu kulinganisha na Tanzania Bara. Sababu ni nini? Sababu ni moja tu, Mheshimiwa Waziri mafuta yanayokwenda Zanzibar yanakuwa-charged dola 10 per tone, ikiacha mbali tofauti na dola tatu/nne isiyozidi tano kwa nchi nyingine tunazopakana nazo. Kwa nini jambo hili linatokea kwa Zanzibar?

Mheshimiwa Spika, sisi kama ni kuhurumiana, huruma kwanza inaanza kwa ndugu na jirani. Hivi sadaka gani inayoanza Zambia, Malawi na Kongo ikaacha Zanzibar ambao sisi ni ndugu? Ni jambo la kusikitisha sana, kwa nini mpaka leo suala hili tumekuwa tukiliuliza Mheshimiwa Waziri bado mmelitafutia kona ya kuliweka ni kero ya Muungano. Tusiishi kwa mazoea ya kero, kero hupatiwa utatuzi suala hata hili la mafuta Zanzibar kutozwa dola 10 kwa tani ikiacha nchi nyingine wakienda na dola tatu/nne na isiyozidi tano, ni suala ambalo naomba mliondoe kwenye kero za Muungano na mlifanye ni suala maalum na mlipatie ufumbuzi wa haraka ili angalau Wazanzibar waweze kununua mafuta kwa bei inayofanana na wenzao wa Tanzania Bara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumekwenda mbali zaidi sasa hata ng’ombe wakipelekwa Zanzibar baada wanavyolipa mnadani wale Wazanzibari au wafanyabiashara wanaopeleka ng’ombe Zanzibar wakifika bandarini wanakuwa-charged tena kama wanaoenda Comoro. Hasa inachukuliwaji Zanzibar? Ni foreigner’s au ni nchi ya Tanzania? Haliko sawa hata kidogo.

Mheshimiwa Spika, naomba mliangalie sana, nawaomba sana, hata ng’ombe kwa hivyo hayo masuala mengine tusirundike tu kero za Muungano. Mambo ambayo yanaweza kutatuliwa kwa uharaka yatatuliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuje na suala la usajili wa vyombo vya moto, mwaka wa 20 leo ukitoa gari Zanzibar ukija hapa bado limewekwa kwenye kero za Muungano. Yanasemwa maneno tunalifuatilia, hadi lini? Vitu vingine vinasababisha manung’uniko yasiyo na msingi. Basi kama inashindikana, wenzetu wanaingiaje? Kongo wanapofika pale border wana-surrender document wanapewa permit ya kuishi na gari yao hapa ndani ya nchi yetu miezi mitatu. Akimaliza anarudi tena anaweza kukaa nayo hivyo. Basi kama Zanzibar inawezekana ikiingia gari pale bandari zizuiwe kadi Mzanzibari au yeyote anaingia na gari yake ikiwa document zimezuiwa pale, tutumie utaratibu huo. Naelewa huo hauwezekani kwa sababu sisi ni nchi moja, hilo linakuwa shida maana yake mkianzisha hilo tufungue ubalozi Zanzibar wa Tanzania. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, maana yake sasa tuna-treat kama nchi nyingine wakati sisi ni ndugu na ni nchi moja. Kwa hiyo, hebu na hili Mheshimiwa Waziri lifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nataka kuzungumzia hapa ni suala la ushuru bambikizi, ushuru mkubwa. Jana alisema Mheshimiwa Mbunge mmoja hapa akasema kwamba tatizo moja kubwa ambalo tunalo ni kuweka kodi kubwa kwa kutegemea tutapata pesa nyingi. Matokeo yake watu wanatafuta mbinu za kukwepa tunakosa hata hicho kidogo. Nakushuru.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kupata nafasi ya kuchangia hoja iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Waziri, nitaunga mkono hoja yake kwa mara ya mwanzo iwapo ataturidhisha kwa majibu ya maswali yetu tunayoyatoa hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na suala la TRA. Wafanyabiashara wa Tanzania wanateseka sana kwa matatizo yanayosababishwa na Maafisa wa TRA. Kilio cha Waheshimiwa Wabunge ni matokeo halisi ya kinachofanyika huko nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi Jiji Kuu la kibiashara la Dar es Salaam, maeneo ya Kariakoo, fremu nyingi zimefungwa na wafanyabiashara wameamua kuacha kufanya biashara kutokana na manyanyaso yanayotokana na TRA. Maafisa wa TRA wanajipa uwezo mkubwa wa kuandaa mazingira, Mheshimiwa Hawa amezungumza vizuri, nami namuunga mkono sana kwa alichokizungumza. Bahati nzuri kafikia mpaka kuwa shahidi wa matendo ya udhalilishaji wanayoyafanya baadhi ya Maafisa wa TRA wasio waaminifu kwa wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wafanyabiashara hususan wadogo wadogo wa nchi hii ni watu ambao wanajiandalia mazingira; maana mitaji yao kuanzia mwanzo wa biashara zao ni watu ambao hawana msaada wowote unaotokana na chanzo chochote cha Serikali, ni jitihada zao binafsi zinazowafikisha mpaka kupata mitaji wakaanzisha biashara zao ndogo ndogo. Bahati mbaya sana mfanyabiashara huyo mdogo wa Tanzania, anapopata wazo tu la kufanya biashara, anapoenda TRA kutaka kuanza hiyo biashara yenyewe, kwanza anaambiwa lipa kodi ya mapato. Hata biashara hajaifanya anatakiwa kulipa kodi. Kuna kitu kinaitwa clearance, hiyo huwezi kuipata kama hujalipa kodi ya mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niwaulize TRA, kodi ya mapato iliyotokana na nini? Hebu mtuambie, hiyo kodi ya mapato inatokana na nini? Ana wazo la kufanya biashara, anaenda kutafuta certificate zinakazomruhusu kufanya biashara lakini anaambiwa kwanza lazima ulipe clearance, ulipe nini, umepata nini na kutoka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, matokeo ya kufungwa fremu za Kariakoo siyo tija kwa TRA wala kwa Taifa. Matokeo ya wafanyabiashara kuhama nchi wakaenda kufanya biashara nchi za jirani siyo tija kwa Taifa hili. Mnapofanya jitihada za kuongeza mapato, lazima mzingatie mambo haya muhimu sana. Busara itumike katika kukusanya kodi, pia lazima kodi zetu ziendane na uhalisia wa kipato cha anayelipishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna vitu vya ajabu sana. Nataka kutoa mfano mdogo. Leo hii ukileta kontena la vitenge kutoka nje, kodi inayotozwa na TRA kwa takwimu zao na hesabu zao, ni karibia shilingi milioni 80, kontena moja. Matokeo yake wafanyabiashara wanaingiza vitenge lakini kinachofanyika inakuwa ni transit goods, zinaishia nchi jirani ya Zambia. Kontena zinaenda Zambia na Uganda. Wanafungua kule na wanazirejesha ndani ya nchi yetu kwa njia za vichochoroni, njia zisizo rasmi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda leo Kariakoo utakuta vitenge vya nje vingi vinauzwa lakini nenda kwenye taarifa za TRA uone ni kontena ngapi za vitenge zimelipiwa, mtakuta hamna lakini kwenye soko la vitenge Kariakoo vimejaa tele. Kwa sababu ukienda Zambia kontena la vitenge haliwezi kuzidi shilingi milioni 20, lakini ninyi mmejiwekea kodi ya shilingi milioni 80, mmetaka yote, mmekosa yote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, bidhaa ya magari yaliyotumika. Sheria za Kodi zilizoweka viwango, sina tatizo, asilimia 25 ni import duty, excise duty zote siyo tatizo. Tatizo linakuja kwenye valuation ya gari iliyotumika kutoka nje. Hivi tokea lini kitu cha kununuliwa mnadani TRA wanakiwekea valuation, yaani hiyo ni bei ambayo haitikisiki. Umeona wapi? Kitu cha mnada maana yake inategemeana na bei ya soko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Suzuki Carry hata uki-google hapo utaikuta Japan inauzwa dola 500, 700 mpaka 1,000. Rudi kwenye tariff za TRA, utaikuta imewekewa valuation ya dola 3,000. Maana yake akileta gari lile maana yake analipia kodi ambayo siyo halali kwa sababu sheria inataka valuation itozwe kulingana na viwango vya kodi ya TRA. Sasa vitu vya mnada toka lini vikawekewa indicative price ambayo inatumiwa na TRA? Hii inasababisha watu watafute njia nyingine za vichochoroni kupitisha magari yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii gari aina ya Land Cruiser V8 ushuru wake unafikia shilingi milioni 80. Tembea, Land Cruiser zote zilizopo nchini, asilimia 90 ni ya msamaha wa kodi, ni la Msikiti, Kanisa hata kama wanaoendesha siyo wenyewe. Hii ni kwa sababu ya kodi ya shilingi milioni 80 laiti kodi ingewekwa shilingi milioni 25, 30 au 40 watu wangelipa, lakini mnataka nyingi, mnakosa vyote. Tuliache hilo, lakini nawaambieni tena, rudini muangalie, Maafisa wa TRA wanachowafanyia wafanyabiashara kinawaudhi na tena kinakera na sisi wawakilishi wao tunasema na naomba mchukue hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumzie kilio ambacho wenzetu wa Kusini wanalia sana. Tunaapa hapa kila asubuhi, tunamwomba Mungu kwa dua kwamba tuwatendee Watanzania haki na tunamwombea sana Rais wetu Mungu amwongezee hekima ili yeye na sisi tunaoshauri tutimize haki kwa Watanzania. Watu wa Mtwara au watu wa Kusini wanalia kilio hiki kwamba pesa zao wenyewe mnazizuia, humtaki kuzipeleka wakaendeleza maisha yao, nia ya Waziri ni nini kwa wananchi wa Kusini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamdhihaki Mungu kwa sababu tunapomlilia Mungu kwa kiapo na tunapoanza harakati zetu kwa kiapo cha kuwatendea haki Watanzania, tunakuwa tunamshtakia mambo yetu Mungu leo tunamdhihaki Mungu. Mheshimiwa Jenista ni hodari sana kusimama anapodhihakiwa Mheshimiwa Rais hapa lakini sio hodari wa kusimama anapodhihakiwa Mungu kwa kutowatendea haki Watanzania, hata kidogo. Akiguswa Mheshimiwa Rais, najua anatimiza wajibu wake lakini tutimize wajibu, asidhihakiwe Mungu kwa kutokuwatendea haki Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanacholilia watu wa Kusini ni haki yao, siyo kwamba wanaomba, ni chao wenyewe. Serikali inayosema imeongeza makusanyo, uchumi umekua, mko vizuri lakini nawaambieni, kama uchumi kukua ni hivi, maisha ya Watanzania yalivyo, ni afadhali ule utawala wa Mheshimiwa Kikwete uliopita ambao ulionekana unawapigaji, una wanaosafiri nje sana, kuna hewa nyingi lakini bado tija kwa Watanzania ilionekana. Serikali iliyodhibiti leo watumbuaji wanatumbua mpaka pesa za wakulima wa korosho wa Kusini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana awali ya yote nachukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia leo kuweza kusimama hapa na kUweza kutoa mchango katika hoja iliyo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kuanza kuchangia naanza na utangulizi ambao ni muhimu kwa ninavyoona. Katika siku za karibuni kwenye nchi yetu umezuka mjadala mpana kuhusiana na juu ya ndoa za jinsia moja. Tumesikia sauti/kauli za baadhi ya Mawaziri akiwemo Mheshimiwa Kangi Lugola na Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Nje. Katika kauli zao inaonekana kuna kamtego wa juu ya kuonekana kwamba kukubaliana na jambo hili na kukinzana na jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba niwaambie Waheshimiwa iwe ni mtego au ni bahati mbaya, lakini sisi Watanzania hatutoingia katika mtego wa ushoga, Watanzania hatutaki ushoga hiyo ni mtego. Narudia kama alivyosema Mheshimiwa Kabudi iwe mmetumwa au ni bahati mbaya Watanzania hatutoingia kwenye mtego wa kukubali ndoa za jinsia moja na nawaambia m-take note please, u- take note Mheshimiwa Lugola, Tanzania ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ni muungano wa nchi mbili Zanzibar na Tanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar asilimia 99 ni waislamu na waislamu kwa vyovyote suala la ushoga hawalikubali, tunawaambia nyoosheni maneno sawa, nchi yetu haikubali ushoga na huo ndio msimamo wa Tanzania nadhani mmenielewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naumia sana moyoni mwangu kuona nchi iliyostaharabika, nchi yenye utamaduni wetu wa asili, leo kuna baadhi ya watu wanasingizia misaada iwe ni ajenda ya kututoa sisi kutupeleka kwenye ubaradhuli, haiwezekani, hili jambo ni baya na Watanzania hawataki kusikia kabisa. Nawaomba viongozi wetu kama hili jambo likae kimya kama hamuwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hapa tumezungumza kuna mawe yale ya chuma kule Liganga, hivi kwa nini tusitumie akili zetu kwa rasilimali alizotupa Mwenyezi Mungu mpaka tunafikiria kulainisha maneno ooh, hatutawanyanyasa, hatutawafanya hivi. Watanyanyaswa kwa sababu sheria ya nchi yetu haikubali ushoga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kuchangia sasa, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, Rais aliyepita Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete aliwahi kusema…

T A A R I F A . . .

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Taarifa bora zilizowahi kutolewa kwenye Bunge hili, hii itakuwa inaongoza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea majibu ya kiuanaume kama hilo lililotolewa na Mheshimiwa Kangi. Ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu matamu kwa wote. Nilitumia dakika moja sasa naanza upya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete wakati alipoazimia na akaweka nia ndani ya moyo wake kwamba Tanzania ipate Katiba Mpya alikuwa na maono mapana juu ya kuipeleka nchi hii katika mema tunayoyatarajia. Nataka ninukuu baadhi ya maneno machache aliyoyasema Mheshimiwa Rais Mstaafu wakati wa maazimio ya kutunga Katiba Mpya. Mheshimiwa Rais Mstaafu Kikwete alisema, nanukuu;

(i) “Tutatunga Katiba Mpya itakayoainisha Muungano wetu kwa kuondoa changamoto zilizopo sasa.

(ii) Tutatunga Katiba mpya itakayoipa nchi yetu mfumo bora wa kuongoza na kuendesha mambo yetu.

(iii) Katiba itakayoimarisha upendo, ushirikiano na mshikamano miongoni mwa wananchi wa Tanzania licha ya tofauti zao za asili kwa upande wa Muungano na maeneo wanakotoka na tofauti za jinsia, rangi, kabila, dini, ufuasi wa vyama vya siasa.

(iv) Katiba itakayodumisha amani na usalama wa nchi yetu.

(v) Katiba itakayostawisha zaidi demokrasia, kuheshimu haki za binadamu, utawala wa sheria, utawala bora na kudhibiti maovu.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli hii na maneno haya hakuna yeyote ambaye anaweza kuyapinga kwamba ni kauli iliyo hai na ni kauli ambayo haitakufa milele na milele na milele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais John Pombe Magufuli wakati wa kulifungua Bunge hili aliwahi kutamka uzuri wa juu ya kazi aliyorahisishwa na Rais aliyepita wa kuandaa Katiba Mpya na akawaeleza Watanzania kwamba yeye ataendeleza pale palipobakia. Hiyo ni ahadi aliitoa ndani ya Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tumemsikia tena Mheshimiwa Mtukufu Rais akisema kwamba hayuko tayari kutoa pesa watu waje wale bure kwa ajili ya Katiba Mpya. Mimi nataka kutoa ujumbe kwa Watanzania, Mheshimiwa Rais alipozungumza na akasema kwamba ataiendeleza Katiba ile alisema akiwa ndani ya Bunge hili, Bunge la wananchi na hii ndiyo nchi ya Tanzania. Yeye Mheshimiwa Rais ni sehemu ya Bunge na Bunge hili aliliaminisha hivyo, kwa hiyo nawaomba Watanzania bado waichukue kauli ya Rais kwamba ile iliyotoka kweney Bunge ndiyo kauli official ya umuhimu wa kuendeleza Katiba Mpya mpaka pale itakapopatikana.

KUHUSU UTARATIBU . . .

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mimi mpango uliopita Mheshimiwa Mpango hapa nilishauri nikamwambia hivi, kodi zetu si rafiki kwa wafanyabiashara na nilikutolea mfano wa kontena moja la vitenge katika tariff zenu ninyi TRA hapa Tanzania mnai- charge karibu milioni 80; lakini kontena hilo hilo likifika Zambia wana-charge kama milioni 20. Matokeo yake mzigo unapita kwenye Bandari ya Dar es Salaam, unaenda kupelekwa Zambia na wafanyabiashara wetu wanalipia Zambia mzigo ule unakuja kidogo kidogo unauzwa katika soko la nchi yetu. Hilo nililishauri nikakwambia angalieni kodi rafiki, wafanyabiashara waweze kulipa, hamkulizingatia. Sasa ndiyo maana tukaona hata tukishauri hamfanyi kitu, turudi huku kwenye Katiba Mpya ndiyo itakayotuongoza ili tufikie mafanikio. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii mipango tumekuwa tukishauri mambo mengi sana. Wewe unaelewa Mheshimiwa Mpango kama biashara Tanzania imeanguka, wafanyabiashara wanakimbia nchi, tumeshauri njia. Mheshimiwa Zungu jana alisema gharama za Bandari ya Mombasa na Dar es Salaam ni tofauti kama ardhi na mbingu. Yanashauriwa hayo hamna mnachokifanya, turudi kwenye Katiba, Katiba ikituongoza tukipata uongozi bora, yote haya yataondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapolilia Katiba iwe bora, tunapolilia uongozi bora matokeo yake ziko nchi walizoweka miundombinu yao ya reli iwe na kila kitu. Ziko nchi ambazo zilifanikiwa katika mambo yote, walichokosa, ni uongozi bora dakika tano iligharimu mazuri yote yaliyotokana na waliotekeleza, Syria iko wapi leo, Libya iko wapi, Misri iko wapi leo? Ilikuwa hawana shida ya pesa wala miundombinu. Walichokosa ni uongozi mzuri, ushirikisho wa wananchi katika nchi zao ilisababisha kila kitu. Hii leo tunajenga hizo reil, Stieglers Gorge na vitu vingi tunafanya, tutakapokosa ushirikiano, amani, uongozi bora, siasa safi matokeo yake itakuwa tunafanya kitu cha hovyo. Dakika tano nyingi inaweza kuja kutokea watu wabaya wakamaliza jitihada zote kubwa mnazozifanya zikaonekana hazikuwa na msingi wala maana yoyote.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. KHATIB S. HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uhai wake nikaweza kusimama hapa jioni hii ya leo.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuongelea suala la ugonjwa wa UKIMWI. Asubuhi hapa nilimsikia Mheshimiwa mmoja akiongea kwamba ishara za wafadhili zinazoonesha kusita kutoa misaada ambayo kwa kiasi kikubwa inatusaidia katika sekta hii ya kuwahudumia wenzetu wenye maradhi haya ni kiwango ambacho ni kikubwa sana, jambo ambalo mazingatio tunayopaswa kuwa nayo kwa sasa ni kuona umuhimu kama Taifa kuanza kuona jinsi gani ya kufanya kuweza kukabiliana na hali hii.

Mheshimiwa Spika, kila siku zinavyokwenda mbele masharti ya wahisani wetu yanazidi kuwa makubwa. Masharti yanapozidi kuwa mengi na makubwa na mengine yanakuwa hayatekelezeki, ni fundisho tosha la kutufundisha sisi kuona sasa kidogo tunachokipata kuangalia maeneo muhimu. Kati ya maeneo muhimu ni maeneo yanayogusa uhai wa watu moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo hili la wagonjwa wa UKIMWI ni eneo ambalo kwa kiasi fulani tumepata mafanikio ya kupunguza maambukizi mapya kutokana na msaada mkubwa wa kifedha ambao wahisani wetu walikuwa wanatusaidia. Kutokana na hii hali ambayo imeanza kuonekana, masharti kila yanavyozidi kuongezeka yanatishia juu ya fungu hili la kusaidia wenzetu ambapo hakuna anayejijua lini litamkuta hili.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama kuna maeneo ambayo tunapaswa kuyazingatia sana ni kuangalia namna gani tutaweza kukabiliana na tishio la wafadhili wetu kuacha kutusaidia katika mambo mazito na muhimu ya uhai ya wananchi wetu na sisi wenyewe kwa ujumla. Kwa hiyo, angalizo langu ni kwamba aomba Serikali kupitia Wizara ya Afya, katika mipango yake, sasa ijielekeze zaidi kutathimini maeneo haya ambayo kwa kweli yanasononesha na yanatishia sana.

Mheshimiwa Spika, nataka niongelee suala la pili ambalo ni kuhusu Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo. Asubuhi ya leo niliuliza swali kuhusiana na namna Zanzibar tunavyonufaika na misaada kutoka FIFA.

Mheshimiwa Spika, kama unavyofahamu na wote tunafahamu kwamba Tanzania ni Taifa moja na masharti ya Taasisi zile, Shirikisho la Mpira Duniani, FIFA na CAF yote kati ya masharti yao ni kwamba hawatambui, hawawezi kupokea nchi mbili kuwa wanachama wa taasisi zile.

Mheshimiwa Spika, hili lilitokea mwanzoni mwa miaka miwili iliyopita pale Zanzibar ilipobahatika kujiunga na wanachama wa CAF kwa jitihada kubwa zilizofanywa na mapenzi ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano kwa kusaidiana na washirika wa kimichezo hadi kuifanikisha Zanzibar kuingia katika wananchanma wa CAF, lakini kwa bahati mbaya haikuchukua zaidi ya miezi minne Zanzibar ikaondolewa katika Uanachama ule kwa masharti yale kwamba haiwezekani Taifa moja likawa na wanachama wawili. Kwa hiyo, hayo ni masharti ya Katiba zao na sisi hatukuwa na la kufanya.

Mheshimiwa Spika, hapa ninaongelea ni kwamba, asubuhi jibu nililolipata ni kwamba ZFA ni sehemu ya TFF, siyo sahihi. Kama ni sahihi, naomba Mheshimiwa Waziri tafadhali aje aliweke sawa jambo hili nione uhalali wa jambo hili. Kwa sababu kama nilivyosema na narudia kusema, Wizara ya Habari na Michezo ya Tanzania ni Wizara inayohusika na upande mmoja wa Muungano, kama ilivyo Zanzibar, Wizara ya Habari na Michezo Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, TFF ni chombo cha mpira wa Tanzania Bara na Zanzibar iko ZFA. Kwa hiyo, linapokuja suala la misaada kutoka nje ya kimichezo kupitia FIFA, inapoingia TFF, kama kuna kilichowahi kwenda, basi ilikuwa ni huruma TFF. Hakuna mfumo maalum wa kuona upande wa Zanzibar ambaye siyo mwanachama wa FIFA wala CAF anafaidika vipi na fungu la mgao kutoka FIFA?

Mheshimiwa Spika, hili ni suala ambalo naiomba sana Serikali iliangalie kwa umakini tusije tukazalisha kero ya ovyo katika Muungano, kwa sababu masuala ya michezo ni sekta inayogusa vijana wengi; na kama tunaavyojua, vijana wana mihemuko mingi. Leo kuliacha jambo hili ambalo taarifa zipo; kwa mfano, sasa hivi tunatarajia kama hazijaingia, zitaingia muda wowote, 1.25 billion Dollar msaada wa FIFA kwa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, katika hili, kabla haujafika huo mgao, napenda kutoa mapendekezo yangu kwa Mheshimiwa Waziri, waangalie kupitia Wizara yake na Wizara ya Michezo ya Zanzibar, ni namna gani kale kasungura ka michezo ambako kanatolewa na FIFA kwa nchi ya Tanzania? Tanzania ikijijua ni nchi yenye Muungano wa mchi mbili vilevile, kwa hiyo, hili jambo liwekewe mfumo maalum ili Zanzibar tuone tunanufaika vipi kupitia FIFA.

Mheshimiwa Spika, hili ni jambo na ambalo limekuwa na malalamiko makubwa kwa upande wa Zanzibar. Kwa hiyo, ni vizuri sana kuzingatia moja kwa moja isiwe ni kwa bahati mbaya; leo ukiongelea habari ya msaada wa FIFA kwa Zanzibar siku zote jibu linakuja, “tulisaidia Uwanja wa Gombani kuweka nyasi.” Hilo tu! Kuweka nyasi Uwanja wa Gombani imekuwa ni slogan ya kuonesha kwamba ilitosha kwa Zanzibar kufaidika na misaada ya FIFA. Hiyo siyo sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tungeweka mfumo ambao hautakuwa na mgongano wa kujua katika kinachopatikana kutoka FIFA wao Zanzibar moja kwa moja kifungu chao at list kitakuwa ni hiki na tuondoe huu mgongano ambao sioni umuhimu wowote wa kuweza kufikia hali ya kuwekwa nayo kama ni kero ya Muungano. Nadhani hilo limeeleweka.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho na la muhimu sana, hapa kuna jambo linazungumzwa, lakini mara nyingi Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakilizungumza kana kwamba ni jambo la utani na ni jambo ambalo linachukuliwa kwa utani.

Mheshimiwa Spika, suala hili la tohara kwa wanaume, nilivyomsikia mchangiaji leo akisema madhara yanayopatikana kufikia kansa, siyo jambo la kulichukulia utani tena, ni jambo serious kwamba kwa sababu hilo jambo linagusa kila maisha ya mwanadamu, siyo jambo la kusema hapa tukawa tunacheka. Kama leo kuna ugonjwa, nilidhani labda ni kupunguza chachu ya mambo fulani, lakini sasa kuna gonjwa la hatari la kansa ambalo linapatikana kutokana na wanaume ambao hawajafanyiwa tohara. Hilo siyo jambo la utani tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ingekuwa ushauri wangu, akina mama wa Tanzania wananisikiliza, ningewaambia wawagomee wanaume wowote ambao bado hawajakubali kufanyiwa tohara. Wawagomee kabisa, wawaambie bila tohara hilo jambo haiwezekani, no! Kwa sababu leo unaenda kumwoa mke...

SPIKA: Mheshimiwa Khatib siyo fitina hiyo! (Kicheko)

MHE. KHATIB S. HAJI: Mheshimiwa Spika, hapana. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, siyo fitina kwa sababu leo mtu anaenda kuoa mke, kesho amegombana, anamuacha; wewe unaenda kuoa tena; kumbe yeye alikuwa na tatizo hilo kutokana na maradhi ya kujitakia.

Mheshimiwa Spika, mara nyingi nimewaambia wanaume ambao bado na tatizo hilo, tuulizeni tunafaidika vipi sisi ambao tulibahatika mwanzo kujaliwa kuwa na tohara? Leo nimekuja siyo faida pekee, bali ni madhara makubwa ambayo yanatokea kiasi cha kuwapatia ndugu zetu kansa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tusichukulie utani. Kama kuna ugonjwa mkubwa ambao dada yangu asubuhi ameutaja pale, hili jambo lazima tuwe serious kuona kwamba hili suala ni muhimu kwa tohara ya wanaume wote.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nasema ahsante sana, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Namshukuru Mungu kwa kunijalia kusimama hapa nami niweze kutoa mchango wangu. Kwa kuanza, kwa masikitiko makubwa sana nami naungana na Wabunge wenzangu wote kwa lile suala wanalolilia la vyanzo vya mapato vya Halmashauri vyote kuchukuliwa na Serikali Kuu, jambo ambalo litapeleka Halmashauri zetu kuendelea kudorora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa umekuja mpango huu wa vitambulisho vya wajasiriamali, ile ni sehemu moja muhimu ambapo Halmashauri zilikuwa zinajikusanyia mapato yake. Yalianza mabango, yakaja majengo na sasa wamemalizia kwenye wafanyabiashara au wajasiriamali wadogo wadogo. Nami naungana na wenzangu kulitaka jambo hili liangaliwe upya kwa sababu Halmashauri zina majukumu makubwa na lazima zijiendeshe kwa kuwa na vyanzo hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, mimi leo nashukuru sana, kwanza nilisahau hapo mwanzo nilitaka kusema kwamba nilishukuru Bunge letu kwa kukubali kuipokea ile ripoti ya CAG. Nashukuru sana kwa sababu jambo hili tayari lilikuwa limeleta mjadala mkubwa huko lakini kwa umahiri imepokelewa na nashukuru ina sign ya mwenyewe Profesa Assad, kwa hiyo, ni jambo la kufurahisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yaliyopita, iko methali ya Kiswahili inasema: “Funika kombe mwanaharamu apite. Hata hivyo, katika hili la CAG tutafunika kombe lakini mwanaharamu hapiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie utawala bora. Hii dhana ya utawala bora ni pana sana na Mzee wangu Mheshimiwa Mkuchika amepewa Wizara hii kwa umahiri wake, nampongeza sana. Hata hivyo, mambo yanayotendeka ndani ya hchi hii yanakwenda kinyume kabisa na utawala bora. Nataka niseme wazi, Mheshimiwa Waziri umepewa jukumu la kuhakikisha utawala bora unaendelea ndani ya nchi lakini kuna mambo yanayofanyika hayaendani kabisa na dhana ya utawala bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupiga marufuku mikutano ya vyama vya siasa ni moja kati ya jambo ambalo mnakiuka masharti ya utawala bora. Tanzania imesaini mikataba mbalimbali ya dunia kusimamia haki za raia wake lakini leo sheria, Katiba na vitu vyote vinasema wazi haki ya vyama vya siasa ya kufanya mikutano ya hadhara lakini mmezuia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnajua kuna vyama zaidi ya 20 ndani ya nchi hii na mnajua kuna Wenyeviti wa vyama vingine hawana Mbunge hata mmoja, vyama hivyo vitawezaje kujitangaza kwa wananchi kama mmewazuia wasifanye mikutano ya hadhara? Lengo lenu ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Jeshi la Polisi limejipa mamlaka hata vikao vya ndani ya vyama vya siasa wanazuia, kitu ambacho hakihitaji kibali wala ruhusa ya mtu yeyote vyama vya siasa kufanya vikao vya ndani. Hebu hili liangalieni kwa umakini sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili linaumiza watu, tunakwenda kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa hivi karibuni tu leo vyama ambavyo vinatikiwa kushiriki katika chaguzi hizo haviruhusiwi kufanya siasa ndani ya nchi hii lakini mshindani wetu mkuu Chama cha Mapinduzi mnapiga jaramba mtakavyo. Ndugu Humphrey Polepole anafanya mikutano anavyojisikia yeye lakini Makatibu Wenezi na Makatibu Wakuu wa vyama vingine hilo ni haramu, mnatenda dhambi Mungu anawaona, si haki. Zuio hili linahusu opposition lakini ninyi kwenu hakuna marufuku yoyote (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe tahadhari yangu, tunapokwenda mbele, ziko lugha zinasemwa na wenzangu wametangulia kusema kwamba kwenye Uchaguzi Mkuu Wapinzani hawatarudi. Sawa, hakuna tatizo. Tusiporudi kwa maamuzi ya wananchi, hiyo hakuna kesi; lakini msitarajie ule upuuzi uliofanyika Korogwe na uliofanyika Majimbo mengine; Msimamizi wa Uchaguzi anachukua fomu anakwenda kujificha halafu anatangaza kwamba Mgombea wa Upinzani katika eneo hili hakurudisha fomu. Huo ni upuuzi, hatutakubali, lazima tutahadharishane mapema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako huku Waheshimiwa Wabunge wameingia kwa njia hizo, wamejificha na ushahidi uko, kwamba Wagombea wa Upinzani wanarejesha fomu, Wakurugenzi wa Halmashauri wanajificha kukataa kupokea fomu za Wapinzani. Haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale wanaotegemea kurudi kwa njia ya mkato ya aina hiyo, wale wanaotegemea mteremko wa aina ile, mwaka 2020 tutapeana tahadhari kabisa. Tanzania ni yetu sote, Vyama vya Siasa vipo kwa mujibu wa sheria na tutasimamia sheria mpaka tone la mwisho la damu yetu. Hatutakubali Mkurugenzi yeyote au msimamizi wa uchaguzi apokee amri haramu kusimamia uharamu wa kuwabatilisha Wagombea wa Upinzani. Hilo never, never never. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea tena kwenye Utawala Bora. Kwenye Magereza wamejaa watu wengi sana. Wamejaa watu ambao hawastahili kuwepo kwenye Magereza kwa sasa. Kuna watu kesi zao zimechukua zaidi ya miaka sita. Kosa moja tu, upelelezi haujakamilika. Jamani, wale walioko kule ndani ni wazee wetu, ni ndugu zetu, ni watoto zetu. Hatupiganii makosa yao wasamehewe, tunataka kesi zao siendeshwe, ushahidi utolewe, wahukumiwe kwa mujibu wa sheria. Siyo uhodari wa kuwachukua watu mkawalundika ndani halafu mkasema upelelezi haukamiliki. Lini upelelezi utakamilika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema especially kesi ya Mashehe wa Uhamsho wa Zanzibar, hili suala linatukera sana. Wazanzibar wanakereka na hakuna Mtanzania yeyote aliye radhi kuona kesi ile inaendelea kukaa ukiambiwa tu kwa sababu ushahidi haujakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama yuko aliye radhi, mfano kwenye Bunge hili, aseme mimi niko radhi watu wale waendelee kukaa kwa kisingizio tu ushahidi haujakamilika. Leo ni miaka sita wazee wa watu wanasota ndani ya Magereza. Aliye radhi asimamie Mbunge mmoja aseme mimi niko radhi dhuluma ile iendelee. Asimame humu ndani ya Bunge!

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii ina sheria. Kama kesi zinaonekana hazina ushahidi, ziko sheria za kuyaahirisha mashauri ili ushahidi mwaka wowote ukipatikana mashauri yale yarudi tena Mahakamani. Kwa nini hazitumiki hizo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wananyimwa fursa. Wako wale walioshitakiwa kwa kesi za ubakaji, wakahukumiwa jela wakafungwa. Wamefaidika na fursa ya Mheshimiwa Rais ya kutoa msamaha kwa wafungwa. Leo wazee wale yalaiti wangekuwa wamehukumiwa kwa makosa yao, nina hakika Mheshimiwa Rais hawezi kusamehe wabakaji akaacha kuwasamehe Mashehe Wana wa Zuoni. Nina hakika wangehurumiwa na leo wangekuwa huru wakaendelea kulea familia zao. (Makofi)

Mheshimiwa Menyekiti, tuna hasira sana na tunajisikia uchungu sana kwa Mashehe wa Uhamsho na Watanzania wengine wowote wanaoendelea kulundikwa Magerezani kwa kisingizio tu cha ushahidi haujakamilika. Ushahidi utapatikana lini? Mheshimiwa Waziri wa Utawala Bora, nakuomba sana, wewe ni mzazi, wewe ni mzee, yafikirieni tena haya, Serikali liangalieni, viambieni vyombo vyenu vya upelelezi; suala la Mashehe wa Uamsho wa Zanzibar lifikie mwisho. (Makofi)

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Taarifa.

Hiki kidonda kinachotutonesha, naomba sana suala hili lifikie mwisho.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Namshukuru Mwenyezi Mungu kunijalia kuweza kusimama hapa, na niwatakie heri na baraka katika mfungo wa mwezi wa Ramadhani wananchi wote wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kutoa shukrani na pongezi za dhati kabisa kwa namna Mheshimiwa Waziri, Naibu wake na Watendaji wake wanavyoisimamia Wizara hii, Wizara ambayo ni uhai wa Taifa la Tanzania, ni uhai wetu sote. Mimi binafsi hata kama sitasema hadhara, lakini kwa kusema kweli naikubali sana Wizara hii na Watendaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nianze kuhusu suala la wagonjwa wa figo, Mheshimiwa Waziri, binafsi anafahamu, mimi nimewahi kuugua ugonjwa huo, nimepitia mazito ambayo kwa kweli kati ya magonjwa mazito na magumu sana ni ugonjwa wa figo. Kwa hivyo ninapozungumza hapa nazungumza kitu ambacho nimekipitia, nakijua na naendelea nacho.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka Mheshimiwa Waziri, kuna jambo moja linatatiza sana wagonjwa wa figo, jambo hili ni upatikanaji wa dawa za wagonjwa wa figo, wagonjwa wa figo ambao wako kwenye bima, Watanzania wengi hali zao za kiuchumi ni za chini sana, wale walioko kwenye bima, hizo bima hata ukikata lakini kuna masharti ya kufikia kupata dawa za figo, yako masharti, mtu kawaida ukikata ile bima unaambiwa lazima ikae muda fulani iwe ndiyo inakuwa matured ya kuweza kupatiwa dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna binadamu yeyote anayejiombea ugonjwa kumfika, kama imewezekana kwa wagonjwa wa UKIMWI kupewa dawa hizi pasipo na masharti na wagonjwa wa figo waangaliwe urahisi wa kuzipata dawa hizi. Kwa kweli, hili jambo ni la kuliangalia sana, pamoja na hilo Mheshimiwa Waziri anajua mgonjwa wa figo anapopata tu ugonjwa huu, akithibitika kuna hatua za kupitia wakati anasubiri upasuaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, huduma ya uchujaji wa damu, huduma za uchuchaji wa damu, kwa mtu asiye na bima ya afya sasa hivi ni 180,000. Watanzania wa hali ya chini kwenda kupatiwa huduma hii kwa 180,000 kila siku anayokwenda kwenye huduma hii ni jambo zito na ambalo Watanzania wengi hawawezi kulimudu. Hili linapelekea vifo vyao kabla hata hawajafikia kwenye kufanyiwa transplant. Kwa hiyo namwomba Mheshimiwa Waziri, aliangalie hili sana, kwa sababu Watanzania wengi wasio na uwezo wanafikia, hawafikii hatua ya kutafuta ndugu kuwasaidia upandikizaji tayari wamekuwa wamekufa katika hatua ya kufanyiwa uchujaji wa damu dialysis, kwa hivyo naomba suala hili liangaliwe nalo kwa umakini sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo mimi ni mmoja wa wanachama wa Chama cha Wagonjwa wa Figo na wanachama wenzangu wamenituma hapa nilisemee hilo, kwa hivyo Mheshimiwa Waziri, naomba alichukue kwa uzito stahiki. Naongea kama Khatib na naongea kama mwakilishi wa wagonjwa wenzangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ninalotaka kulizungumzia, Mheshimiwa Ummy katika Hospitali ya Rufaa ya Bombo lipo tatizo, lipo tatizo ambalo sasa ni karibu miaka mitano, tatizo la lift katika wodi ya Galanosi ambayo wazazi wanakaa kwenye ghorofa ya tatu, theatre room iko chini. Kinachotokea sasa hivi anapofanyiwa operation, akipelekwa kule juu lazima abebwe mzega mzega. Tanzania ya leo mgonjwa kubebwa kwenye machela akapandishwa kwenye ngazi hilo ni jambo ambalo halikubaliki. Akinamama hao, ambao wanajifungua kwa operation wako chini, akinamama hao Mheshimiwa Waziri ajue ndiyo wengine wanajifungua Marais, wengine watajifungua Mawaziri Wakuu, wengine watajifungua Waziri wa Afya kama yeye, wengine watajifungua wachungaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni vizuri sana Mheshimiwa Waziri jambo hili aliangalie na nataka nimpe rai, kwa sababu mimi ni mdau wa Tanga, mimi ni mpiga kura ambaye natokea Zanzibar lakini mimi ni mkazi wa Tanga na familia yangu yote. Namwomba sasa, kama hili jambo limekuwa zito na mwaka wa tano limeshindikana, tuna bahati sana Mkoa wa Tanga na Jimbo la Tanga Mheshimiwa Waziri wa Afya ni mtu wa Tanga; Katibu Mkuu wa Wizara hii ni mtu wa Tanga, Dkt. Chaula; yupo Mbunge wa Jimbo la Tanga Mheshimiwa Mussa Mbarouk na nipo Mbunge mimi kutoka Zanzibar, lakini ni mdau mkubwa wa Tanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri ahitishe harambee mimi na wenzangu niliowataja tuwashirikishe matajiri wa Tanga wapo pale wa kina RATCO, yupo pale Raha Leo, yupo Simba Mtoto, tuitishe na harambee kubwa ambayo itasaidia kuitengeneza lift ile ili wagonjwa wetu, akinamama wetu wa Tanga waepukane na adhabu ile. Namwomba sana Mheshimiwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza, nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kusimama hapa dakika za mwisho mwisho, dakika za majeruhi.

Mheshimiwa Spika, nitoe shukrani za dhati na pongezi kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano, Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mheshimiwa Waziri wa Afya, kwa jinsi wanavyochukua juhudi katika kushughulikia janga hili la dunia maana hili siyo janga la Taifa ni janga la Dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nataka niseme kitu kimoja. Mheshimiwa Waziri Mkuu ni Waziri Mkuu wa Tanzania na juhudi anazozichukua ni kwa ajili ya Taifa zima la Tanzania. La kusikitisha na jambo ambalo limenifanya leo nimuombe Mheshimiwa Spika kwa bidii zote angalau kunipa hizi dakika tano ili nikupe ujumbe huu ni kwamba kuna mchezo na mzaha mkubwa juu ya maisha ya watu Zanzibar kuhusu ugonjwa huu wa Corona. Upo mchezo, mzaha na dharau.

Mheshimiwa Spika, kuna Waziri mmoja alikuwa safari nje ya nchi aliporudi Zanzibar akiwa katika hali ya kuumwa alikataa kukaa kwenye karantini. Waziri huyu Salama Aboud Talib alienda kukaa nyumbani kwake ugonjwa ulipomzidia alirudi hospitali ya umma ya Mnazi Mmoja. Taarifa na uamuzi wa Serikali ni kwamba wagonjwa wote wanaohisiwa kuwa na ugonjwa wakae karantini, alikataa, ndani ya muda wa siku tatu ameng’ang’ana kukaa Hospitali ya Mnazi Mmoja. Baada ya kuonekana hili jambo limekuwa kubwa na minong’ono na malalamiko kuwa mengi ndiyo alikubali kuwekwa karantini kwa nguvu. Athari yake tayari nyumbani kwake wapo wawili aliowaambukiza na pale hospitali haijulikani ni nini kilichoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, alifanya hivi kwa sababu ya kiburi cha madaraka yake. Nachukua fursa hii kumpongeza sana Makamu wa Rais wa Zanzibar alipotoka safari alikwenda kukaa kwenye karantini yeye mwenyewe bila kulazimishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huu ndiyo utu na uongozi. Leo Waziri huyu aliyekiuka amri ya Serikali, amri yako wewe Waziri Mkuu na hata amri ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nani yeye na kiburi hiki kakitoa wapi?

Mheshimiwa Spika, jana tumeona kwenye taarifa za habari za Kenya, Naibu Gavana ametoka pale hospitali na pingu anaenda kusulubiwa. Kwa sasa hatuwezi kumchekea mtu kwa sababu ni Waziri au ni nani, lazima Mheshimiwa Waziri Mkuu hili alichukulie hatua haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, isitoshe baada ya kiburi hiki, kuna mpumbavu mwingine anaitwa Hafidh, ni daktari, hadi ninavyoongea ameng’ang’ana hospitali hali ya kuwa ameathiriwa na ugonjwa huu wa Corona. Yuko pale Hospitali ya Mnazi Mmoja. Kwa nini anafanya hivi? Ni kwa sababu ana nasaba au ukoo wa wakubwa. Hii ni hatari inayofanyika Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siwezi kusema wakubwa wa Zanzibar wanawaogopa watu hawa lakini nachosema ni mchezo unaofanywa kwa kuhofia watu na madaraka yao. Leo Uheshimiwa wake ni kwa sababu ana uhai wa Mwenyezi Mungu, anapumua, dakika moja akifumba jicho anageuka anakuwa marehemu, sasa na awe marehemu yeye asiue wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, taharuki iliyopo katika Hospitali ya Mnazi Mmoja baada ya matukio hayo ni kubwa. Hivi ninavyoongea nataka Mheshimiwa Waziri Mkuu afuatilie huyu Daktari anayeitwa Hafidh kama bado yupo pale Mnazi Mmoja au amekubali kwenda karantini? Kwa sababu kauli anazotoa kwenye mitandao ya Facebook anasema hakuna yeyote anayeweza kumfanya lolote, anazitoa yeye mwenyewe. Pia matusi anayotukana, hayawezi kusemeka kwenye hadhara ya watu wastaarabu.

Mheshimiwa Spika, napenda kumtaarifu Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba mambo haya yanafanyika Zanzibar. Sasa tufanye nini? Kuna msemo wa Kiswahili unasema: “Zumari ikipigwa Chopocho Pemba anacheza wa Mtwara”. Haya maradhi yakianza popote ndani ya nchi ujue ni athari kwa Taifa zima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, anaogopewa vipi mtu huyu? Hivi vitu vinasikitisha sana. Tukiangalia juhudi za Serikali, Taifa na dunia imekaa katika tension lakini kuna watu kwa sababu tu eti naitwa Waziri anaamua kuhatarisha maisha ya watu. Huyu mtu wa namna hii anatakiwa akiua mtu na yeye auliwe. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana. (Makofi)

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kutujaalia uhai wake ambao leo umewezesha kukutana hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu imepita katika mtihani mkubwa sana katika kipindi hiki. Umauti uliowakuta viongozi wetu wakuu wawili katika nchi hii, kwakweli ni pigo kubwa sana. Kuondokewa na Dkt. John Pombe Magufuli na Mheshimiwa Seif Sharif Hamad, Makamu wa Rais wa Zanzibar. Kwa kweli ni msiba mkubwa ambao katika historia ya nchi hii haujawahi kutokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kusema kwamba naungana na Watanzania wote na Wabunge wenzangu kuyasifu, kuyaadhimisha na kuyapongeza mema yote waliyoyatenda viongozi wetu. Nataka niseme kwamba kwa imani yangu tunapaswa kumsema Marehemu kwa mema yake na sisi tunatimiza ibada kwa kuyasema mema ya Dkt. Pombe Magufuli kwa yale aliyoyafanya katika uhai wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najua Dkt. Pombe Magufuli ni binadamu na hakuwa mkamilifu lakini hatupaswi kuyasema sasa kwani nafasi ya kujitetea hana tena. Kwa hivyo, nijielekeze katika kumpongeza kwa yale mema ambayo ametuachia na sisi tuko tayari kushirikiana na uongozi mpya uliopo kuyatekeleza kwa vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepata Rais wetu mpya mama Samia Suluhu Hassan. Binafsi niseme nina imani na mama Samia Suluhu Hassan kama walivyo na Imani Watanzania wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mola wetu Mtukufu alipoiumba dunia alimuumba Adam, kwa mujibu wa vitabu vitakatifu vinavyosema lakini akaiona dunia siyo mpaka alipomtoa mama Hawa ubavuni kwa Adam. Kwa hivyo, Hawa ana nafasi kubwa sana na ndiyo maana leo akina mama tunawapa nafasi kubwa hata kama sisi tumewatangulia katika uumbaji wake Mola wetu Mtukufu. Hebu leo tujiulize bila akina mama hii dunia ingekalikaje? Ingekuwa ni mtihani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati mama Samia ameshika madaraka ya nchi hii ilianza kuonesha jinsi ambavyo atayadumisha yale mema ya mtangulizi wake. Pia tunaridhika na alivyotuonesha kwamba ni mama anayejiamini kweli kweli. Kwa hiyo, hatuna shaka hata kidogo na uongozi wa mama Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka niseme kwamba tumepata pia Makamu wa Rais miongoni mwetu kwa maana ametoka hapa ndani. Nimevutiwa sana na aliyoyaongea hapa, ameongea mambo mengi jinsi watakavyosimamia yale maendeleo waliyoyaanzisha pamoja na mtangulizi aliyekuwepo. Amezungumzia habari ya kuimarisha barabara, reli, maji, elimu na afya. Hayo ni mambo mema ambayo kila Mtanzania anatakiwa ayapongeze yalivyofanyika na walivyopanga kuendelea kuyatekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, nataka nimuombe Mheshimiwa Makamu wa Rais huko aliko kama ananisikia, katika hotuba yake amegusia maendeleo ambayo wanatarajia kuyafanya. Nataka aweke highlight katika dondoo chache ambazo nitampa sasa hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu imeingia katika uchumi wa kati kwa jitihada zao na zetu. Sasa nataka kuiona Tanzania chini ya uongozi wao ikiingia katika demokrasia ya kati. Tutoke demokrasia tuliyonayo twende demokrasia ya kati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namaanisha nini? Tunataka kuona uhuru wa vyama vya siasa unatekelezwa kwa vitendo. Tunataka kuona vyama vya siasa vinafanya kazi zake pasipo kubughudhiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka Makamu wa Rais aweke highlight Katiba mpya ni mahitaji ya Watanzania, sisi na wenzetu wa CCM. Siyo mahitaji ya wapinzani kama inavyodhaniwa na baadhi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ada ya mja kunena, muungwana ni vitendo, sisi waja tunapozungumza, waungwana onesheni vitendo. Katiba mpya haikuwa mahitaji ya Upinzani, Katiba mpya kwa mujibu wa ilipofikia tayari ilipitishwa, kilichobakia ni umaliziaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naona fedheha sana kama mimi nilikuwa Mjumbe wa Bunge la Katiba na tulipiga kura kuipitisha leo akitokea mwingine akisema kwamba si kipaumbele cha nchi hii, ni ahadi na zilitumika pesa za Watanzania ili ipatikane Katiba mpya kwenye nchi hii. Kwa hivyo namuomba Mheshimiwa Makamu wa Rais aweke highlight juu ya jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana uhuru wa vyombo vya habari. Najua upo na tunaposema haya si kwamba hayakuwepo unapodai leo barabara nzuri, siyo kwamba tulikuwa tukipita kwenye mapori, barabara zilikuwepo lakini tunataka barabara zilizoimarika Zaidi. Tunapozungumza tunataka uhuru wa vyombo vya habari siyo kwamba haukuwepo kabisa lakini tunataka uhuru uliomarika kweli kweli. Hatutaki uhuru ambao mwandishi akiandika jambo anafikiria usiku mzima…

T A A R I F A

MHE. MUNDE A. TAMBWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatibu, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Munde Tambwe Abdallah.

MHE. MUNDE A. TAMBWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba nimpe Taarifa kaka yangu Mheshimiwa Khatib kwamba wakati tunapitisha Katiba Mpya Wabunge wa Upinzani waliikataa na wakatoka nje. Nashangaa leo wanavyong’ang’ania Katiba Mpya. Hawa watu wakoje, wanataka nini? Tulikuwa tunaipitisha wakaikataa, leo tumekubaliana, wanaitaka tena. Yote hiyo wanataka kutuvuruga, hatutoki kwenye reli ya maendeleo. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khatib unaipokea Taarifa hiyo?

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimjibu dada yangu Munde. Mahitaji ya Katiba Mpya hayakuwa mahitaji ya Wabunge wa Upinzani, yalikuwa ni mahitaji ya Watanzania. Ninyi Wabunge wa Chama cha Mapinduzi kwa kuona yale ni mahitaji ya Watanzania ndiyo maana mliipigia kura ikapita kwa kishondo na mkacheza ngoma zote ndani ya Bunge hili. Kwa hivyo, kila tunalolikataa sisi kama na ninyi mnalikataa tuambiane kuanzia leo tujue hayo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuendelea. Katiba Mpya ni ahadi na tayari imepitishwa. Namuomba Mheshimiwa Rais ambaye naye alikuwa Makamu Mwenyekiti wa Bunge la Katiba aliangalie kwa jicho pana jambo hili kwa manufaa ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niligusia kuhusu uhuru wa vyombo vya habari siyo kwamba haukuwepo, tunapoomba mambo kuboreka ni kwamba tunataka twende mbele. Uhuru wa vyama vya siasa sio kwamba haukuwepo, lakini tunataka zaidi uimarike. Leo tunakuwa marafiki wakati tunazungumza hapa ukifika wakati wa uchaguzi mnabadilika, mnakuwa sura nyingine, tunakwenda wapi? Tunataka mambo haya yaondoke kama alivyosema mama Samia na sasa twende kwenye nchi ya kistaarabu, tufanye siasa kistaarabu, anayeshinda ashinde, anayeshindwa ampe mkono, Tanzania iende mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili natoa wito kwa wale wenzetu wote wanaoisema vibaya nchi hii sasa warudi nyumbani mambo yamenoga. Wasikae huko kuipaka matope, mama Samia yuko. Gwajima amesimama hapa amesema Konki Fire, sasa nasema rudini tujenge nchi yetu, tunaambizana hapa, tunasikilizana hapa, tufanye mambo yetu kama Watanzania. Tuache kubaguana kwa vyama, leo tumepiga kura hapa haijapungua hata moja, kwa nini? Tunapowapa mkono wa aalan wasaalan, mtoe mkono wa aalan marhaba, sawa? Tusiwape mkono mbele mkashika panga nyuma, hatutafika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuweze kuchangia hoja hii iliyopo mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya yote nipende kuwatakia Watanzania wote heri na baraka ya Mfungo wa Mwezi wa Ramadhani ambao tumeuanza leo, Mwenyezi Mungu atujalie tuifunge kwa heri na tumalize kwa heri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru wenzetu ambao si Waislamu lakini wameonesha kutuunga mkono kwa njia zote. Nikiangalia leo Bunge lako hijabu zimeongezeka, si kwa Waislamu peke yake, na mavazi ya staha yameongezeka sana. Na hii ni kutuunga mkono na kutusaidia kutupunguzia majaribu; ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuchangia hotuba hii kwa kusema yafuatayo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, sisi wote ni Watanzania na tunajenga Tanzania moja. Tuna wajibu wa kuyaenzi yale mema yote ambayo… katika nchi yetu. Binafsi toka imeanza hotuba ya mpango na mpaka tunakwenda hotuba ya bajeti, nimesikiliza sana, nimekaa kimya sana kuyazingatia sana yanayosemwa na naomba niseme tu, hoja hujibiwa kwa hoja, hoja haipigwi rungu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapotoa hoja ikaonekana hoja zetu wakati mwingine zinakinzana na yale mawazo waliyonayo wenzetu, wajaribu kutujibu kwa hoja zile zile ili mwisho wa siku tufikie mwafaka katika kujenga Taifa letu hili moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitamke bayana, sioni aibu, hata kama ni mpinzani, kusifia lolote jema linalofanywa na Serikali hii. Lakini hali kadhalika, msione soo! Pale tunapolisema lolote baya linalofanywa na Serikali hii kwasababu lengo linarudi palepale, kwamba lengo letu ni kujenga nchi moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia kuhusu miradi ambayo ilianza katika utawala wa Awamu ya Tano. Niseme wazi, wako wasomi, wachumi, walioongelea sana kuhusu miradi lakini nitamke bayana, miradi ambayo imetumia fedha nyingi za Watanzania kwa malengo ya kuliletea tija Taifa hili, hata kama kuna kasoro zinazoonekana katika utekelezaji wa miradi ile, hatuwezi kui-dump miradi ile kwasababu ya kasoro hizo. Na kufikiria kui-dump miradi hii na kuitelekeza kwasababu ya kasoro zilizopo ni kosa moja ambalo kizazi kijacho kitatuhukumu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesikia baadhi wakisema kwamba mradi wa bwawa la umeme hauna tija na utupiliwe mbali, nimesikitika sana. Mama mwerevu anapopika chumvi ikazidi kwenye nyungu, watoto wanasubiri chakula, haendi kulitupa lile sufuria watoto wakafa njaa, ataongeza maji ukali wa chumvi upungue na watoto waweze kula; huyo ndio mama mwerevu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Watanzania, Wabunge sisi, tuna wajibu wa kuyaona makosa yaliyomo kwenye miradi ile, tusiwe wanafiki wa kusifia kila kitu wakati tunajua yako mapungufu ambayo yanatakiwa kurekebishwa ili kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono mradi wa bwawa uendelee (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hali kadhalika, naomba kasoro zilizopo katika Mradi wa Bandari ya Bagamoyo tuangalie tena upya, mahitaji ya Bandari mpya ya Bagamoyo bado ni muhimu kwa uchumi wa Taifa letu, ni muhimu kwa ustawi wa viwanda vilivyotarajiwa kujengwa maeneo ya Bagamoyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi wasafiri wa kwenda Zanzibar tunapopanda boti mara kwa mara, hakuna siku utakuta hapana meli chini ya 50 ambazo zinasubiri kufunga geti katika Bandari ya Dar es Salaam, hakuna. Inaaishiria bado kuna mapungufu katika Bandari ya Dar es Salaam. Kupata Bandari ya Bagamoyo ni ukombozi wa eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulipofikiria kujenga Bandari ya Bagamoyo wenzetu wa Kenya hawakuwa hata na wazo la kujenga Bandari ya Lamu, walipotusikia tu wao walianza, na tayari Bandari ya Lamu imekamilika. Sisi bado tunakaa tunabishana tukidhani kwamba kuna kasoro; kasoro zirekebishwe na kazi iendelee, hayo ndiyo mawazo yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na katika hili, kipekee sana nampongeza kiongozi wangu wa chama, Mheshimiwa Zitto Kabwe. Katika maoni yake yote ameonesha kukubaliana na mapungufu lakini akitaka kazi nzuri iliyoanza tufikirie namna ya kuifanya, kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumzie katika ukurasa wa 22 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, ameongelea suala la uendeshaji mashtaka na utoaji wa haki. Nipende kusema kwamba huu ni Mwezi Mtukufu wa Ramadhani; tarehe 03 Novemba, 2014, nilisimama hapa kuongelea ucheleweshwaji wa kesi na niligusia sana kuhusu kesi ya Mashekhe wa Uamsho kutoka Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilisema – wakati huo kesi ile nadhani ikiwa kama na miaka minne – leo tena ni Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, nasimama hapa kusema, tayari umefika mwaka wa nane, tunakwenda mwaka wa tisa. Kesi ile imechelewa sana na wanasiasa wanapenda kusema justice delayed, justice denied, lakini wanazungumza mdomoni, hawaitafsiri kwa vitendo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kila mshtakiwa anapokwenda mahakamani anachokisubiri ni hukumu ya makosa yake. Haki ya mtuhumiwa ni kuhukumiwa, siyo kukaa gerezani katika kipindi kirefu. Kunyongwa ni hukumu, kufungwa maisha ni hukumu, kufungwa miaka kadhaa ni hukumu; ni haki ya mshtakiwa kulingana na makosa yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unapomnyima hizo hukumu wakati ilikuwa ni haki yake tayari unamyima haki yake ya msingi. Matokeo yake ni nini; kwa mujibu wa sheria zetu Mheshimiwa Rais wa Jamhuri anayo mamlaka ya kumsamehe mfungwa yeyote aliyeko gerezani. Lakini Mheshimiwa Rais hana mamlaka ya kumsamehe mtuhumiwa aliye na makosa. Kuchelewesha kumpa hukumu mtuhumiwa aliyeko gerezani ni kumnyima Rais wa Jamhuri haki yake ya kuwahurumia baadhi ya wafungwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano tulionao leo, akina Babu Seya leo wasingekuwa huru kama wasingekuwa wamehukumiwa. Kama wangekuwa wanaendelea kushutumiwa na kukaa pale mahabusu, bado wangekuwa wako mahabusu. Lakini kwasababu walihukumiwa, Mheshimiwa Rais alitumia nafasi yake ya kikatiba kuwasamehe watuhumiwa wale, na leo wako huru na familia zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunakwenda mwaka wa tisa, sheria zetu Waheshimiwa Wabunge, tuna dhima kwa Mwenyezi Mungu tunapopitisha sheria ya kwamba anayehukumiwa kwa kosa la ugaidi, utakatishaji fedha, uhujumu uchumi, akishtakiwa kwa makosa hayo hapewi dhamana. Tuangalie upya namna gani ambavyo tunakiuka haki za msingi za binadamu. Kwasababu laiti ingekuwa anayeshtakiwa kwa makosa haya ana hukumu ya kukaa katika hali ya kuwa mahabusu, ingekuwa bado tumetenda haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwendesha mashataka anapoamua tu kwamba shtaka hili linaangukia katika maeneo haya matatu basi huyo haki yake ni kukaa rumande katika muda usiojulikana. Waheshimiwa Wabunge, kama tunalamikia kupanda kwa bei za bundles na tukapiga makelele ikasimama, kikokotoo kikasimama; kwa nini tusilalamikie haki za wananchi wetu ambao wakishtakiwa kwa makosa hayo wanasota magerezani kwa muda wa miaka kadhaa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Walahi juzi kuna mama mmoja alikwenda kumuangalia mtoto wake katika washtakiwa wale wa uamsho, alipotoka mahakamani tu umauti ukamchukua. Alipotoka Segerea hajarudi kwao Zanzibar, umauti ukamchukua kwa uchungu aliopata kwa watoto wake kukaa gerezani muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaapa kwa Mungu kila siku atuongoze kufanya mema na tumshauri Rais katika mambo ili nchi hii ipate tija kwa Mwenyezi Mungu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari za Mwaka 2016
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Tuko hapa kujadili Muswada wa Habari. Kabla ya yote nimkumbushe dada yangu aliyemalizia kuchangia hapa kwamba kuna methali ya Kiswahili inasema: “Ukienda kwa wenye chongo fumba lako jicho” ili ufanane nao hata kama wewe macho yako yanaona sawasawa, lakini jaribu kufumba yako ufanane nao, kwa hivyo jiangalie.
Waheshimiwa Wabunge wenzangu leo katika kituko cha karne kinachotokea ni anaponyanyuka Mbunge wa CCM ndani ya Bunge akatulaumu kwa sababu eti tunampenda Lowasa, hiki ni kituko cha karne. Waheshimiwa rudini kwenye kumbukumbu kidogo tu. Mkutano Mkuu wa CCM, jinsi kale kawimbo katamu “kweeli”...
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuhakikishie tu kati ya watu ninaowaheshimu katika Bunge hili ni Mwenyekiti wewe kwa busara zako na hekima zako, lakini Mheshimiwa inapokuja hoja kutoka upande ule na tunaijibu kwa uzito unaofanana ule, naomba utupe nafasi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, utawala uliopita ulikuwa una nyenzo zote; una dola, una vitu vyote, Ikulu ilikuwa kwao, vyombo vya mashtaka vilikuwa kwao, kila kitu uwezo, power ya dola yote ilikuwa kwao. Katika kipindi chote walishindwa nini kumshtaki na kumshughulikia Lowassa mpaka yanakuja leo? Kwa hivyo, ninachosema ni kwamba ukienda kwa wenye chongo fumba lako jicho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuchangia kwa hadithi moja ndogo pia. Mheshimiwa Rais wa kwanza wa Zanzibar baada ya uhuru, marehemu Abeid Amani Karume, Mungu amuweke anapostahiki, alipokuwa na Maswahiba zake wa karibu baada ya nchi ile kupata uhuru, baada ya mapinduzi yale matukufu, moja kati ya sheria alizoweka, Zanzibar akiwa na maswahiba wake wa karibu kabisa, aliidhinisha chakula cha gerezani, Zanzibar kule kwetu tunaita Chuo cha Mafunzo kiwe ni dona, sembe na maharage, hiyo ndiyo kanuni aliyoipitisha. Hicho ndiyo chakula cha gerezani na kwa wakati ule Zanzibar kumlisha mtu dona na maharage ilikuwa kweli ni adhabu, ilikuwa ni adhabu kweli kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haukupita muda mrefu alikosana na baadhi ya maswahiba zake waliotunga pamoja hiyo sheria. Matokeo yake wale mabwana wakaenda gerezani, watu wawili hao sipendi niwataje ni marehemu. Walipofika gerezani walikutana na chakula dona na maharage. Wale Mabwana mmojawapo alianza kula mmoja kilimshinda hakuweza kula. Siku ya mwanzo, siku ya pili, ilipofika siku ya tatu yule mwenzake amwambia “Shekhe inabidi ule kwa sababu hii sheria tuliipitisha wenyewe, tulikuwa pamoja wakati wa kupitisha hili na hivyo leo tumekuja hapa lazima tule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo sheria hizi, Muswada huu unaoletwa leo hapa, madhumuni makubwa ikiwa kwamba wanakomolewa watu fulani na kukiwa na lengo mahususi la kulenga uchaguzi wa 2020, Mungu ni mkubwa sana hapo katikati bado kuna safari ndefu sana. Linaweza likatokea lolote la kutokea, wanaotuletea huu leo wakawa waathirika wa mwanzo na Inshallah kwa Mwenyezi Mungu awajaalie wawe waathirika wa mwanzo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo binafsi sitaki niseme sana, lakini wakati mwingine tunapotoa hoja huku zinaangaliwa wanaotoa ni Wapinzani. Tunapotoa mawazo huku yanaangaliwa wanaotoa ni Wapinzani hata mazuri yanabezwa, matokeo yake leo hii tunaathirika kwa Sheria ya Ugaidi iliyopitishwa na Bunge hili. Sheria za ugaidi za kuwakamata watu na kuwaweka makorokoroni katika muda ambao hata haupatikani ushahidi ni moja kati ya sheria ambazo zilipitishwa na Bunge hili ambazo zinawaathiri, zinawanyanyasa, zinawanyima haki watu wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uko ushahidi kadhaa, leo katika magereza Tanzania, kuna wafungwa wanaohusishwa na kesi za ugaidi walioko mahabusu wasiopungua 85, Masheikh wa dini ya Kiislam, ni miongoni wa zile sheria zinazopitishwa kwa uharaka ili kukidhi mahitaji ambayo wenzetu mnaona yana maana sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge hili hili lilikaa Bunge la Katiba, yakapitishwa maamuzi tukashauri vizuri, Katiba hii siyo, rasimu inayofaa kufuatwa ni hii, mkafanya mliyoyafanya, mkaona yale mawazo yetu hayana maana, matokeo yake jana mmesikia Mtukufu Rais alivyosema. Yote hayo ni kutokana na kupuuza maneno yetu ambayo wakati mwingine msipokubali leo, kesho mtakubali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kusikitisha zaidi katika hili, Waheshimiwa tunakaa hapa tunajadili hili jambo, kabla ya kujadili hili jambo ni nini kilitokea? Sote tunajua. Hawezi kutumikia mtu mabwana wawili kwa wakati mmoja. Uchague kutumikia wananchi au uchague kutumikia nguvu ya pesa. Waswahili wanasema penye udhia penyeza rupia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Mtukufu Rais anasema ukiingia kesho anausaini na anao uwezo wa kusema hivyo kwa sababu anajua nini kilichotangulia, anajua, anajua nini kilichotangulia. Sasa ninachosema ni kwamba tunapoteza muda bure, leo Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi Mwenyekiti wa Kamati hii ambayo ameutetea Muswada huu na amekataa wadau wasitoe maoni yao katika muda muafaka ni sawa na mchawi aliyepewa mtoto alee. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vyovyote asingekwenda vingine kwa sababu anajulikana ni mtu wa upande gani au ni mtu ana mwelekeo gani. Kwa hivyo, haya yanayotokea tunafanya kazi bure lakini kwangu mimi Muswada huu na mtayarishaji mkuu, Waziri huyu ambaye mwelekeo wake toka alfajiri alipoingia hapa tulianza kuuona, toka akiwa huko nje tulianza kumwona, mtu maarufu wa goli la mkono. Msitegemee katika maisha yake ataleta kitu cha heri katika Bunge hili hata siku moja. Msitegemee hata siku moja kama ataleta jambo lenye heri kwa Watanzania, huyu ni mchafuzi, ni mchafuzi tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naseme kwamba haya mnayoyafanya jiangalieni vizuri. Bunge lililopita tulikuwa tumeishia mstari huu hapa, Bunge hili tumebakisha ka-quarter kadogo. Mwaka ujao he! He! 2020 na matendo haya na kwa Mawaziri hawa akina Nape Nnauye, Watanzania wahukumuni Musha-Allah. (Makofi)
Waheshimiwa msihuzunike sana. Muswada huu naufananisha na utunzi wa mtunzi mmoja anaitwa Suleiman Rashid…
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi wa Mwaka 2018
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo si dhana sahihi, haiwezi kuletwa bajeti inamkamua mtu. Mfano katika bajeti tulichangia tukasema umeme ZECO tunaonewa Wazanzibar lakini ikapitishwa hivyo hivyo, sasa unaletewa bajeti unasema ndiyooo maana yake nini ulichokitetea? Ulichokitetea ni nini, kwa hiyo, hili lieleweke kwamba, tunaungia mkono suala hili la hii sekta ya ubia wa sekta ya Serikali na sekta binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka kusema hivi, kwamba katika kukubaliana na hili Serikali iwe makini katika kuingia mikataba na hawa wawekezaji ambao tutaingia nao ubia katika suala hili. Makosa mengi yaliyofanyika ni wakati wa kuingia kwenye mikataba, tunakuwa hatuko makini kiasi ambacho baada ya muda mfupi nchi yetu inaingia katika majanga makubwa kama ambayo yako sasa hivi huko duniani yanatokea. Kila kesi zinazokwenda katika mahakama za kimataifa tunapigwa, tunapigwa na makosa hayo mliyafanya ninyi wakati wa kuingia kwenye mikataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sasa tunapofikia katika hali hii na kutaka kujinasua, naomba sana uwepo umakini wa hali ya juu sana. Naishukuru Serikali yetu kwa kuona sasa iko haja ya kujiondoa na ile dhana ya kujifanya Serikali ya Mungu wa Kibaniani. Mungu wa kibaniani ana mikono nane lakini hakuna hata mmoja unaoshika, yote ipo tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wameona haja ya kuiweka sekta ya binafsi ili kusaidia uchumi wetu, kwa hiyo, naomba tuondokane na hiyo dhana ya mikono nane lakini ambayo haishiki. Lakini katika hoja hii hii tulipitisha sheria hapa katika Bunge ya kwamba kesi zote zinazohusu wawekezaji zitaendeshwa ndani ya nchi yetu. Hili jambo litawapa wakati mgumu sana wawekezaji wenye mitaji mikubwa kuingia katika sekta hii kwa kuhofia mahakama zetu na uendeshaji wa kesi zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hili suala liangaliwe sana, haitatoa fursa nzuri ya kufanya wawekezaji wa nje waone hadhi kwa sababu watakuwa wana wasiwasi wa kuona kwamba hawatapata haki katika masuala ya kisheria na izingatiwe kwamba nchi yetu imeingia mikataba mbalimbali ya kuridhia ya kuendesha mambo yetu inapofikia mashtaka katika Mahakama za Kimataifa. Kwa hivyo suala hili halitawapa nafasi nzuri ya kuona kwamba iko haja ya kuwekeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa nilichangie ni hili sharti mliloliweka katika muswada huu wa kuona kwamba wawekezaji lazima fedha zao waziwekeze katika Benki Kuu ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia hili mliangalie tena na kwa umakini kwa sababu mwekezaji, hili maana yake labda mngetupa uzoefu mmeli-quote wapi? Au ni nchi gani ambazo zimeingia katika sekta kama hizi mmeona wao wamewawekea masharti haya na yamekuwa ni muafaka kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo liangalieni, tunapoweka masharti makubwa na wao ndipo wanapoona vikwazo vya kufikia lengo la kuwekeza katika nchi yetu. Sioni umuhimu wa hoja hii ya kuwataka wawekezaji lazima waweke fedha zao katika Benki Kuu yetu. Muwape uhuru wa kuamua na mabenki ya kibiashara yako mengi wao waamue na wawe huru wa kuamua ni wapi watawekeza fedha zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili nadhani ni jambo jema na binafsi naunga mkono, kama nilivyosema hoja hii kwa sababu ni matumaini yetu kwamba sasa tunafikia mahali ambapo tunapalenga, na tutaondokana na hii kuwa miongoni mwa nchi za Kiafrika ambazo kila siku tunaenda kubembeleza mikopo kutoka China. Mikopo kutoka China tunaiona athari zake. Kwa hiyo, tutumie fursa hizi zilizopo katika nchi yetu ili kuwekeza na kuwavuta wawekezaji ili wawekeze katika sekta hizi na tuondokane. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mfano ambalo naona ni nzuri sana, mfano barabara kutoka Chalinze mpaka Dar es Salaam. Ingawa sasa tayari Mbunge mmoja aliongea kwamba tayari Serikali imeshajitokeza kuanza kujenga barabara sita mpaka Kibaha, sehemu ambayo ni muhimu sana kutoka Dar es Salaam mpaka Chalinze ingepata kuanzia na hii private sector ikaanzia Chalinze mpaka Dar es Salaam baada ya kuanza kuichokonoa kidogo kidogo kiasi ambacho mwekezaji ataona pale patamu pameshaliwa amebakishiwa pale pachungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni vema muangalie kwa makini fedha zetu zitasaidia katika mambo mengine mengi sana na haya mambo ambayo yanaweza kutekelezwa na sekta binafsi kwa kuingia ubia ni mambo ambayo yataifanya Serikali iwe stable katika pesa ndogo tunayoikusanya twende kwenye mambo mengine. Nchi nyingi zilizofanya katika mfumo huu zimeendelea na zimepata manufaa makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho nirudie kusema nampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na nakuambia uzi ni huo huo, mbane Makonda mpaka mwisho ili haki ipatikane, ahsante sana.