Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. George Mcheche Masaju (36 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa fursa hii, lakini zaidi nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kuendelea kuishi na kuweza kuchangia katika Bunge hili Tukufu.
Kwanza kabisa niseme naunga mkono hoja, nawashukuru Wizara ya Fedha kwa kuja na Mapendekezo haya ya Mpango. Pia nawashukuru Wabunge wote kwa kuhudhuria na kushiriki kikao hiki, lakini pia na kupata fursa ya kuchangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kuzungumza hoja chache zile ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezisema. Moja, nimalizie pale alipoishia Mheshimiwa Mwakyembe kwamba haya ni mapendekezo katika kipindi hiki hatuhitaji Sheria; ile Kanuni ya 94 ipo wazi kabisa, lakini baadaye Mpango ukisoma sasa Kifungu cha 20 cha Sheria ya Bajeti ya Mwaka 2015 na Kifungu cha 26 cha Sheria ya Bajeti, Mpango huu utakapoletwa mahususi wenyewe ndiyo msingi wa kutengenezea Bajeti. Halafu baadae Bajeti inapokuja kutengenezwa ndiyo inatengenezewa Sheria ya Appropriation Act, Sheria ya…
Kwa hiyo, nafikiri niiweke hii wazi kwa baadhi ya Wabunge ambao walikuwa wamefikiri kwamba Serikali imekosea kutokuja hata na Sheria.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Niliona nilitolee ufafanuzi hili kwa sababu baadhi ya Wabunge walikuwa wanajiuliza kwa sababu hawaoni hata Muswada wa Sheria! Nimeona niliweke wazi hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ambalo naomba kuliongelea ni suala la Zanzibar. Suala hili ni suala nyeti kwa mustakabali wa Taifa. Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatambua uwepo wa Serikali mbili na hizi Serikali uwepo wake ni Katiba; kuna Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Katiba ya Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma Ibara ya (4) ya Katiba hiyo siyo tu inaweka mgawanyo wa madaraka katika mihimili mitatu ya dola, lakini pia, inaweka mgawanyo wa madaraka kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na imeelezwa vizuri na kuna mambo ya Muungano na ambayo siyo ya Muungano. Kwa hiyo, Katiba ya Zanzibar sio ya Muungano, ila Katiba ya Jamhuri ni ya Muungano na Katiba ile ya Zanzibar ndiyo inazaa Tume ya Uchaguzi ambayo inasimamia uchaguzi Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kile ambacho baadhi ya Wabunge wamekisema hapa, ni kama kuitaka Serikali ya Jamhuri ya Muungano iingilie mamlaka ya Zanzibar! Tafsiri yake ni kwamba kama unataka kuleta hoja ya kujengwa Serikali moja, lakini kwa mujibu wa Katiba ni Serikali mbili. Sasa tukienda kwa namna hiyo tutakuwa tunavunja siyo tu Katiba ya Jamhuri ya Muungano, lakini pia Katiba ya Zanzibar. Serikali haiwezi ikakifanya hicho na kuwepo kwa Serikali yoyote ni Katiba!
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hoja ya kusema kwamba, Serikali ya Jamhuri ya Muungano iingilie kule, Rais Magufuli aingilie, ana mamlaka tu yeye kuingilia mambo ya ulinzi na usalama ndiyo ya Muungano na mpaka sasa kule Zanzibar kuna amani, Rais anafanya kazi yake vizuri, utengamano ni mkubwa kabisa na usalama upo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo nishauri Waheshimiwa Wabunge kwamba tunapochangia suala la Zanzibar lazima tuheshimu mamlaka ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na tuchangie kwa namna ambayo si ya kuhamasisha uvunjifu wa amani, uhaini au kuvunja umoja na mshikamano! Ikitokea uvunjifu wa amani hapa hakuna yeyote atakayefaidi, wala hatafaidi siasa wala kitu gani! Niliona nilishauri hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, kwa mara nyingine tena nikushukuru na niwashukuru Wabunge wote. Naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipatia fursa hii ili niweze kuchangia lakini zaidi nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kuchangia hoja hii. Naunga mkono taarifa ya Kamati na ushauri uliotolewa na Kamati ni mzuri sana na moja; wameshauri juu ya umuhimu wa kulipa deni. Ni hoja na ushauri mzuri sana kwa sababu usipolipa deni madhara yake ni makubwa sana mbali ya haya yanayoweza kujitokeza kwa hawa ambao wameikopesha Serikali, lakini pia gharama zinaongezeka pale ambapo wanaotudai wanaweza wakatupeleka hata Mahakamani, kwa hiyo gharama zinaongezeka kwa hiyo ushauri ule ni mzuri, sisi tunaupokea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nililotaka kuchangia ni suala tu la namna ambavyo Waheshimiwa Wabunge tunajenga hoja hapa. Kanuni zinatukataza wakati wa mijadala kutumia jina la Rais kwa dhihaka katika mijadala au kwa madhumuni ya kushawishi kufikiwa maamuzi fulani. Kwa hiyo, naomba tu nikumbushe Wabunge wanapokuwa wanashiriki kutekeleza jukumu lao la Kikatiba la kuishauri na kuisimamia Serikali wanapojenga hoja, wajenge hoja kwa namna ambavyo pia haikiuki kanuni tulizojiwekea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia tu kusema kwamba kauli za Rais na Viongozi wengine tuzitazame katika muktadha wa yale anayozungumza katika contextual meaning kuliko una-peak tu sehemu fulani halafu unalipotosha kabisa lile kusudi lililokusudiwa. Kwa hiyo, nishauri hivi; tunatambua Katiba imeweka uhuru, haki ya kila mtu kuwa na uhuru wa mawazo na fikra zake, ni jambo la msingi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na haki hiyo lakini tuitumie vizuri kwa kuangalia muktadha wenyewe wa ile kauli yenyewe, tusipotoshe. Kwa mfano, Mheshimiwa Lwakatare amezumgumza aliyozungumza Rais kuhusu ngono au katerero, amekiri kabisa kwamba yale mambo yapo Bukoba na watu wanaweza kwenda kujifunza kule na kiko Kijiji mahususi kwa ajili hiyo, lakini ukweli ni kwamba Rais alikuwa anazungumzia ngono na katerero? Hapana.
Kwa hiyo, ushauri wangu ni kwamba Waheshimiwa Wabunge tunapotumia haki yetu ya Kikatiba ya kuwa na uhuru wa mawazo na fikra, basi tutoe tafsiri sahihi kwa kauli zinazotolewa na viongozi wa Serikali kwa kuzingatia muktadha wa kauli hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipatia fursa hii na mimi niweze kuchangia. Nikushukuru wewe mwenyewe Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti wote wa Bunge kwa namna ambavyo mnasimamia
uendeshaji wa shughuli za Bunge hili kwa ufanisi mkubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii baada ya kuwa nimesikiliza mjadala huu na mimi nichangie kwa kushauri mambo ambayo yamejitokeza, mambo ya kikatiba na kisheria. Bunge ni taasisi muhimu sana kwa mustakabali wa Taifa lolote lile, ndiyo maana wanapewa jukumu la kutunga sheria. Kwa sababu ya umuhimu huo mimi nitambue umuhimu wenu ninyi Waheshimiwa Wabunge ni watu muhimu, your so much very important person, ndiyo maana mnaitwa Waheshimiwa, lakini Bunge hili nalo lina utaratibu wake wa kufanya kazi; na majukumu ya Bunge yametajwa katika Katiba Ibara ya 63 inaeleza vizuri majukumu ya Bunge.
Mheshimiwa Spika, Ibara ya 63(2) inasema; “ Sehemu ya pili ya Bunge itakuwa ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya Muungano ambacho kitakuwa na madaraka kwa niaba ya wananchi, kusimamia na kuishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa Katiba hii.
(3) Kwa madhumuni ya utekelezaji wa madaraka yake Bunge laweza-
(a) kumuuliza Waziri yeyote swali lolote kuhusu mambo ya umma katika Jamhuri ya Muungano ambayo yapo katika wajibu wake;
(b) kujadili utekelezaji wa kila Wizara wakati wa Mkutano wa Bunge wa kila mwaka wa bajeti;
(c) kujadili na kuidhinisha mpango wowote wa muda
mrefu au muda mfupi unaokusudiwa kutekelezwa katika Jamhuri ya Muungano na kutunga sheria ya kusimamia utekelezaji wa mpango huo; (d) kutunga sheria pale ambapo utekelezaji unahitaji kuwapo sheria; na
(e) kujadili na kuridhia mikataba yoyote inayohusu Jamhuri ya Muungano ambayo kwa masharti yake inahitaji kuridhiwa.
Mheshimiwa Spika, pia Bunge limepewa uhuru wa mijadala humu ndani, Ibara ya 100. Lakini Ibara ya 100(2) imeweka masharti kuna mipaka, Ibara ya 100(2) ya Katiba inasema hivi; “Bila kuathiri Katiba hii, au masharti ya sheria nyingine yoyote inayohusika, Mbunge yeyote hatashtakiwa au kufunguliwa sharti la madai mahakamani kutokana na jambo na lolote alilolisema au kulifanya ndani ya Bunge, au alileta Bunge kwa njia ya maombi, muswada, hoja au vinginevyo.” Katiba hii pia imegawa madaraka katika mihimili mitatu ya dola ambayo ni Bunge lenyewe, Mahakama na Utendaji.
Mheshimiwa Spika, Bunge linatunga sheria na kuismamia Serikali utekelezaji wake, Mahakama inatafsiri sheria inatoa haki na Serikali kwa maana ya utendaji, inasimamia utekelezaji wa sheria zilizotungwa na Bunge.
Katiba hii inaposema kwamba bila kuathiri masharti haya ina maana kwamba Bunge lazima ifanye kazi zake kwa mujibu wa sheria. Ndiyo maana sasa Ibara ya 26 ya Katiba inaeleza kila mtu ana wajibu wa kuifuata na kuitii Katiba hii na sheria za Jamhuri ya Muungano na kwamba kila mtu ana haki ya kufuata utaratibu uliowekwa na sheria kuchukua hatua za kisheria kuhakikisha hifadhi ya Katiba na sheria za nchi.
Mheshimiwa Spika, moja ya sheria zilizotungwa ni Sheria ya Kinga, Haki na Madaraka ya Bunge, ambayo inaeleza kitu gani Bunge linaweza kufanya na ambacho hawawezi kufanya na imeweka makosa ya jinai mle ndani. Niwakumbushe tu Waheshimiwa Wabunge kwamba tunazo
Kanuni za Bunge ambazo zinatungwa chini ya Ibara ya 89 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano kwa ajili ya kuendesha shughuli za Bunge hili.
Ibara hii ya 64 inasema hivi; “ Bila ya kuathiri masharti ya Ibara ya 100 ya Katiba yanayolinda au kuhifadhi uhuru wa mawazo na majadiliano katika Bunge, Mbunge:
(a) Hatatoa ndani ya Bunge taarifa ambazo hazina ukweli;
(b) hatazungumzia jambo ambalo haliko kwenye mjadala;
(c) hatazungumzia jambo lolote ambalo linahusu uamuzi wa Mahakama au jambo lolote ambalo lilijadiliwa na kutolewa uamuzi kwenye Mkutano uliopo au uliotangulia na ambalo halikuletwa rasmi kwa njia ya hoja mahsusi.
Vilevile hatapinga uamuzi wowote uliofanywa na Bunge isipokuwa kwa kutoa hoja mahususi inayopendekeza kuwa uamuzi huo uangaliwe upya;
(d) Hatatumia jina la Rais kwa dhihaka katika mjadala au kwa madhumuni ya kutaka kulishawishi Bunge kuamua jambo lolote kwa namna fulani;
(e) Hatazungumzia mwenendo wa Rais, Spika, Mbunge, Jaji, Hakimu au mtu mwingine yeyote anayeshughulikia utoaji wa haki, isipokuwa tu kama kumetolewa hoja mahsusi inayohusu jambo husika.
(f) Hatamsema vibaya au kutoa lugha ya matusi kwa Mbunge au mtu mwingine yeyote, hatatumia lugha ya kuudhi au inayodhalilisha watu wengine.
Mheshimiwa Spika, nimeona niliseme hili ili kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge wajibu wetu kwamba shughuli zetu humu ndani zinaongozwa na masharti ya Katiba, zinaongozwa na masharti ya Kanuni tulizozitunga wenyewe, zinaongozwa na sheria. Tukifanya vile ndipo
tutaweza kutekeleza jukumu letu kwa ufanisi ipasavyo la kuisimamia na kuishauri Serikali katika utekelezaji wa majukumu yake.
Mheshimiwa Spika, wakati mjadala unaendelea hapa yamejitokeza mambo. Moja yamezungumzwa mambo ambayo yapo Mahakamani, naomba kushauri mambo yote ambayo yako Mahakamani, Katiba imekataza Ibara ya 30(2) ya Katiba imekataza, mambo yaliyopo Mahakamani, inalinda uhuru wa Mahakama na heshima ya watu walioko Mahakamani.
Mheshimiwa Spika, kesi ya mgogoro wa Chama cha CUF yapo Mahakamani. CUF wamepeleka Msajili wa Vyama vya Siasa Mahakamani na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Kwa hiyo ushauri kwamba mambo haya tusiyazungumze tena na mambo mengine. Pia mambo ya kutaja jina la Rais hovyo hovyo mambo hayo yote yamekatazwa hapa, kuwaudhi na yamewekewa utaratibu.
Waheshimiwa Wabunge wote tuna mamlaka lakini mamlaka haya yana mipaka. Ibara ya 100 ya Katiba imeshatafsiriwa na Mahakama Kuu ya Tanzania kwenye katika kesi ya Mheshimiwa Pinda na mimi ndiye niliyeendesha kesi ile, kwa hiyo tuna mipaka yetu. Tunapotekeleza wajibu
wetu tuzingatie mipaka hii, hakuna mtu ambaye yuko juu ya sheria na Mheshimiwa Mbowe amesema kwenye taarifa yake. Kwa hiyo, kama hivyo tunavyotambua hivi tufanye hivyo na naomba kushauri.
Mheshimiwa Spika, Kanuni hizi na sheria hizi, zimempa mamlaka Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuwapeleka watu Mahakamani, sitaki kufika huko mimi, kwanza nawapenda sana, nawathamini sana. Hata Waziri Mkuu amesifu utendaji wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali uliohakikisha kwamba hizi kesi zilizokuwa zinawakabili zimekamilika mapema ili mrudi muwawakilishe wananchi wa majimbo yenu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hilo lazima mlielewe. Kipindi cha bajeti hii Wabunge nawashauri m-concentrate sana kwenye mambo yanayohusu wananchi wenu. Kule kuna shida nyingi watu wanataka maji, watu wanataka elimu, watu wanataka umeme, you would wish to concentrate on those important issues. Haya mambo mengine yaachieni Serikali itayashughulikia tu yenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mawaziri wote wanaohusika na Ofisi yake na timu yake kwa kazi nzuri wanayofanya, wameleta hapa hotuba nzuri sana inayoonyesha mambo makubwa ambayo Serikali hii imefanya mpaka sasa katika kipindi cha mwaka mmoja.Mungu aibariki Serikali hii, Mungu akubariki Waziri Mkuu,
Wabunge na wananchi wote. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuna mambo ambayo kimsingi hayapaswi kuletwa hapa, yamezungumzwa hapa mambo yanayohusu Usalama wa Taifa na mustakabali wa Taifa hili. Wabunge, tumetunga sheria sisi wenyewe hapa, tunayo Sheria ya Usalama wa Taifa ya mwaka 1970 na tunayo Sheria ya Idara ya Usalama wa Taifa ya mwaka 1996. Juzi tumetunga sheria ya Whistleblower and Witness Protection, tumeweka masharti ni yapi ambayo yanaweza kuzungumzwa na yapi hayawezi kuzungumzwa na ni makosa ya jinai haya.
Ninawashauri Waheshimiwa Wabunge muda hautoshi, ningekuwa na muda ningesema yote haya, wazisome vizuri hizi sheria ni mambo gani ambayo hayapaswi kuzungumzwa kwa mustakabali wa Taifa hili.
Mheshimiwa Spika, haya mambo ya ulinzi na usalama yamewekewa utaratibu wake, hata Kamati yako, unayo Kamati ya Kudumu ya Ulinzi na Usalama, mnaona mambo yake yanazungumzwazungumzwa hapa hovyo hovyo? Halafu hatujajua kwamba hapa ni watu wa Usalama tu
kama alivyosema Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, hivi kila mtu anayebeba bunduki ni mtu wa mambo ya usalama, hatuwezi kufika kule.
Mheshimiwa Spika, kwanza kuna suala hapa nilitegemea Waheshimiwa Wabunge kwenye issue ya usalama watajikita sana kwenye mauaji ya viongozi wa Serikali kule Rufiji, watu wameuawa kule, and then tujiulize hii habari ya kutekateka hivi wameshatekwa watu wangapi? Katika
Serikali hii wametekwa wangapi? Hakuna hata watu wawili, ni mmoja. Kwa sababu aliyekwisha kutekwa mimi ninayemfahamu ni huyu mwanamuziki anayeitwa Mkatoliki. Huyu wa kwanza anayeitwa Ben Sanane so far haijulikani, ameondoka nchini, amejificha, yuko wapi, sasa
huwezi kusema ametekwa huyu. Halafu tutofautishe kuteka na kukamatwa na vyombo vya dola kwa ajili ya kuhojiwa.
Ukikamatwa na polisi ukaenda kuhojiwa huwezi kusema umetekwa.
Mheshimiwa Spika, naomba kulishauri Bunge lako Tukufu, kwenye suala hili we need to be so much serious and strict on enforcement of our rules. Hatuwezi tukafikia hatua, hivi kwanza mimi nashangaa, hili suala mtu mmoja na muda mfupi tu amepatikana na Waziri ameenda kuangalia pale mna-challenge, mlitaka achelewe kupatikana na huyo aliyesema Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, kazi zake zimetajwa kwenye sheria ya Baraza la Usalama wa Taifa. Vyombo vyote vya upelelezi viko pale, kama wamemwambia kwamba mwenendo wetu wa uchunguzi unaelekea tutampata hivi karibuni,
mnamhusishaje na utekaji nyara wa watu? Hili suala naomba lisikuzwe, linakuzwa nadhani lina sababu tatu za msingi.
Moja, inawezekana matukio haya wanataka kuyatumia watu wasio na nia njema na Taifa hili kufanya uhalifu, waseme kwamba kulikuwa na hii mipango, if you have any serious information about the crime… taarifa zote za uhalifu pelekeni kwenye vyombo vya dola. Hatuwezi
kufanya hivi. Huyu Ben Sanane hamuwezi kusema kwamba amekufa, Sheria yetu ya Ushahidi inasema ili uweze kuthibitisha kama mtu amekufa baada ya miaka mitano imepita na yule anayedai amekufa ndio ana jukumu la kwenda kuthibitisha hayo. Someni kifungu cha 117 cha Sheria ya Ushahidi, hatuwezi kufanya hapo.
Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni kwamba watu wana vitendo vya uhalifu, labda wanahisi kwamba wakati wote watakamatwa na kuhojiwa inakuwa ni pre-emptive method.
Mheshimiwa Spika, yamezungumzwa hapa mambo ya uchaguzi Zanzibar, uchaguzi Zanzibar umeshapita. Uchaguzi wa Zanzibar
unatawaliwa na Katiba ya Zanzibar.
Mheshimiwa Spika, uchaguzi wa Novemba ulifutwa Kikatiba wakasema wanarudia mwezi wa tatu, 2016 ukarudiwa na sasa kuna Serikali kule haya yasizungumzwe hapa.
Mheshimiwa Spika, kuna mambo yanayozungumwa hapa ya mchakato wa Katiba Mpya. Mchakato wa Katiba Mpya tulitunga sheria, ipo Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, ipo Sheria ya Kura ya Maoni, hatua zote zimeshakamilika sasa kimebaki ni kiporo kwa mujibu wa ile sheria, muda muafaka utakaofika ambao mimi siujui mtaenda huko kwenye kupiga kura kama mtaamua hivyo. Kwa sababu kwanza ninyi wenyewe mlikuwa ni divided mara mlikuwa hamuitaki wengine mkasusia, eeh! Hata mimi nilivyosema tutunge sheria mkakataa wengine! Kwa hiyo, wakati muafaka hiyo mtapiga Kura ya Maoni we can not go back to the Constitution whatever.
Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Katiba na Sheria
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipatia fursa hii ili nami niweze kuchangia. Kubwa nakushukuru kwa jinsi ulivyoliongoza Bunge lako Tukufu asubuhi kwenye sala ama dua. Wabunge tuna tabia tunapofika hapa asubuhi shughuli zetu kabla hazijaanza tunaanza na sala au dua. Unapotafakari maneno mazuri yaliyopo kwenye ile sala hakika huwezi kuamini kwamba baada ya muda mfupi tu ule tunaweza kusahau commitment yetu kwa Mungu tukaanza ku-behave kama watu ambao hatukutambua mamlaka ya Mungu tunayemwomba kila siku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa ya kuchangia hapa na aendelee kutukuzwa sana. Pia nimshukuru Waziri na kumpongeza Mheshimiwa Profesa Kabudi kwa hotoba hii nzuri ya bajeti yake ambayo naiunga mkono. Kusema kweli imezungumza mambo ya msingi ambayo yanalihusu Taifa hili. Kwa sababu hiyo, naungana nawe Mwenyekiti kwa ushauri wako ulioutoa mbele ya Bunge lako Tukufu muda mfupi uliopita kwamba hotuba hii imesheheneza mambo ya msingi kwa mustakabali wa Taifa hili. Laiti Wabunge tungeelekeza michango yetu kwenye mambo mazuri yanayosimamiwa na Wizara ya Katiba basi tungeweza kuishauri Serikali vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kitu ambacho napenda kusema hapa kwamba Bunge kama Bunge tunapaswa tutambue wajibu wetu. Wakati fulani huwa nakaa hapa nasikiliza sana kwa makini, lakini hatuwezi kuligeuza Bunge hili kuwa sehemu ya burudani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mambo ya msingi yanazungumzwa kwa mustakabali wa Taifa hili halafu baadhi yetu tunageuza Bunge hili kuwa sehemu ya burudani na watu wengine wanaleta sauti za wanyama kama ulivyosema fisi, wakati fulani najiuliza mimi kama Mshauri wa Sheria wa Serikali hii hivi tutumie Sheria ya Afya ya Akili? Maana tunayo Sheria ya Afya ya Akili ambayo tunaweza kuitumia kuangalia kama baadhi yetu akili zetu ziko sawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mtu ambaye akili yake iko sawa na anashiriki mjadala kuna namna ya kushughulika na mjadala, mjadala ama ni kwa kuzungumza au kwa maandishi lakini siyo kwa kuzomea au kwa kupiga kelele. Unapofika hatua hiyo katika mjadala sisi ambao tumeshiriki sana kwenye mjadala, mimi nilikuwa Mwenyekiti debating club shuleni, ujue huyu mtu ameishiwa hoja za msingi na kwenye hotuba kama hii hamkupaswa kuishiwa hoja za msingi yapo mambo mengi ambayo yalipaswa yazingatiwe.
Mheshimishiwa Mwenyekiti, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na mambo mengine inataja mihimili mitatu ya dola na mgawanyo wake katika Ibara ya 4; Bunge linatunga sheria, Mahakama inatafsiri sheria na kutoa haki na Serikali inasimamia utekelezaji wa sheria. Sasa humu ndani yamezungumzwa mambo ambayo mengine yameingilia kwenye mihimili mingine kwa mfano yale mambo ambayo yako Mahakamani, hayo hayapaswi kuletwa hapa Bungeni. Moja, yamezungumzwa hapa mambo ya kesi ambazo ziko Mahakamani.
Huyu Msemaji wa Kambi ya Upinzani yeye mwenyewe ana kesi nne Mahakamani analeta hoja hapa kuhusu mambo ya Mahakamani.
Godbless Lema ana kesi mbili Mahakamani. Hawa ambao wanashtakiwa kwa sababu ya kukiuka Sheria ya Makosa ya Mitandao wana kesi Mahakamani. Kwa hiyo, mambo yote haya ambayo yako Mahakamani tuyaachie mhimili wa Mahakama iyashughulikie. Bunge haliwezi kugeuka kuwa ndiyo mtunga sheria, Jaji na Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna tuhuma, Bunge linapotunga sheria hapa maana yake zifanyiwe kazi. Bunge hili lilitunga Sheria ya Cyber Crimes Act, Electronic Transactions Act na sheria chungu nzima, kama wapo watu ambao wamekiuka zile sheria, Serikali iliyopewa jukumu la kusimamia utekelezaji wa sheria lazima ichukue hatua ipasavyo. Watu hawa wanaposhtakiwa Serikali isichukuliwe kwamba ni dikteta au inanyanyasa, ndiyo wajibu wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kushauri, katika hotuba hizi zote na michango yote hii yale mambo ambayo yako Mahakamani Kiti chako kisiyatilie maanani na wananchi wayapuuze kwa sababu upo mhimili mahsusi kwa ajili hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Subira Sungura amezungumza juu ya utata wa umri wa mtoto wa kike kuolewa. Hili pia limezungumzwa na Mheshimiwa Kiteto Koshuma, ni hoja za msingi sana lakini Serikali imekuwa ikichukua hatua. Jana Waziri wa Katiba na Sheria alizungumza na atazungumza lakini suala hili jinsi lilivyo Serikali imeshachukua hatua. Moja, kuna kesi Mahakamani. Kwa hiyo, kwa vile kuna kesi iko Mahakamani Kanuni zetu na Katiba vinakataza tusiyazungumze haya humu ndani jamani. Tuna prejudice Mahakama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba hii Ibara ya 30(2)(d) inasema kwamba:-
“Kulinda sifa, haki na uhuru wa watu wengine au maisha binafsi ya watu wanaohusika katika mashauri mahakamani; kuzuia kutoa habari za siri; kutunza heshima, mamlaka na uhuru wa mahakama”.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pamoja na michango yao mizuri kuhusu huu utata wa umri wa kuolewa kwa sababu kuna kesi Mahakamani, naomba kulishauri Bunge lako Tukufu Wabunge wavute subira, tuiachie fursa Mahakama, Mahakama itaamua, tuishie tu pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mimba za utotoni pia Serikali imeshachukua hatua. Kwanza, kuna Sheria ya Kanuni ya Adhabu ambayo inapiga marufuku mtu kujamiana na mtoto wa kike ambaye yuko chini ya umri wa miaka 18. Ukifanya kitendo hicho basi unakuwa umetenda kosa la kubaka na adhabu yake ni miaka 30 na kama yuko chini ya miaka 12 ni kifungo cha maisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumerekebisha Sheria ya Elimu kama alivyosema Mheshimiwa Koshuma, mwaka 2016 hapa, tukaweka kwenye kifungu cha 60A kwamba ikawa ni marufuku mtu kuoa au kuolewa na mwanafunzi au kuozesha au kwa namna yoyote kumfanya mwanafunzi aache kusoma, ni kosa la jinai.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hapo, tuliwapa jukumu wakuu wa shule kwamba kila robo wawe wanatoa taarifa za incidences case za ndoa, za utoro kwa Afisa Elimu wa Wilaya. Kwa hiyo, Serikali kama Serikali imechukua hatua za kisheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya hilo, Serikali pia imechukua hatua za kisera, moja, imejenga sekondari za Kata kila sehemu; sekondari nyingine zipo mpaka vijijini. Pia ikaifanya elimu hii ya msingi mpaka sekondari kuwa bure.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukingo ule uliowekwa unamwezesha huyu mtoto asome. Ni wakati gani anapata umri wa kuolewa? Polisi hawezi kuwa kila wakati, lakini Sheria ya Mtoto (The Law of the Child, 2009) kifungu cha (8) na (9) kinatoa jukumu kwa mzazi kuhakikisha kwamba mtoto wake anapata elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa kuwa Serikali imeweka sera hizi za elimu bure, imejenga shule, imetunga sheria, ombi langu kwa wazazi sisi, tuipe Serikali ushirikiano ili tuisimamie hii sheria na watoto wetu wapate elimu. Kwa hiyo, wazazi tuna jukumu hilo la msingi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Sabreena Sungura amezungumzia juu ya Serikali… (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza masuala ya kidini, Waheshimiwa Wabunge hatuwezi kutumia Bunge hili kuleta mtafaruku wa kijamii kwa kutumia Bunge hili kuwafanya watu ambao ni ndugu wasielewane. Unapozungumza, unailaumu BAKWATA hapa, sasa unatambua taasisi gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba yetu Ibara ya 19 inasema, masuala ya kidini na ya imani hayawezi kuingiliwa na Serikali. Eeh, hatuwezi kwenda huko. Katiba iko wazi, kama kuna mgogoro uende kwa Kabidhi Wasii Mkuu, ndivyo sheria zinavyosema. Hamwezi kutumia Bunge hili kupanda mbegu za chuki kwa wananchi wa Tanzania. We cannot allow this. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninashangaa hata mnayoyaleta humu ndani, nawe Mheshimiwa Kubenea, unajua vitu vinazungumzwa hapa, ngoja nianze kuwashauri. Hili la Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam lazima tuheshimu Sheria na Katiba tulizozitunga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo sheria hapa, inaitwa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma. Sheria hii inatoa fursa kwa sisi viongozi wa umma tunaokiuka kushitakiwa kule. Meya wa Ubungo amefungua kesi dhidi ya huyo RC, iko pale. Kwa hiyo, tusiwe na haraka. Mnavyoiharakisha, mnaiharibu.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mnataka Mheshimiwa Rais achukue hatua gani dhidi ya huyu mtu wakati tayari iko kwenye mamlaka nyingine inashughulikiwa? Ile Tume ikiona kuna mambo ya jinai, itapendekeza, kwa sababu ina mamlaka mle ya kupeleka PCCB, kupeleka polisi. Eeh, msiwahishe hivi vitu. Mnajua mkiingilia hizi kesi Mahakamani, mnaziharibu. Sisi tunaoendesha kesi, kuna kitu kinaitwa mis-trial; na mimi naende kule tunasema bwana umeshahukumiwa, hiyo kesi unaiharibu. Kwa hiyo, isije ikawa ni mikakati ya kuharibu hizi kesi. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, vuteni subira. Utawala wa Sheria mnaoutaka ni lazima mzingatie hamwezi kuwa mnaisema Serikali tu, na ninyi hamtaki kuizingatia hiyo kitu. Kwa hiyo, RC anayo mamlaka yake ya uteuzi na sasa hivi sijui ametuhumiwa amevunja, amepelekwa kwenye hiyo Sekretariati. Let us be patient, hatuwezi kuwa tunahukumu tu hivi hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, aaah, Mheshimiwa Shahari amezungumza hili la mashehe. Hili suala liko mahakamani na ni ushauri wangu tu ni kwamba tuliache Mahakama ichukue hatua. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wetu sisi tutajitahidi kuharakisha uendeshaji wa kesi hii, ama upelelezi ukamilike mapema hatima yake ijulikane, lakini hili siyo jambo la kuzungumzia humu ndani, unajua masuala ya kuzungumzia kesi zilizopo Mahakamani, mnaziharibu halafu mnaingilia uhuru wa Mahakama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ya Mheshimiwa Maige na Muswada binafsi tuliupokea ule Muswada unashughulikiwa na Serikali. Kwa wakati muafaka atashirikishwa, kwa hiyo naomba Mheshimiwa Maige uwe na subira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ester Mmasi ametushauri vizuri sana Serikali. Ushauri wa Mheshimiwa Mmasi ni mzuri sana, kuna kila sababu ya sisi Serikali kuchukua mambo mazuri anayoyatoa pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ambacho naweza kuahidi, moja, tunachoweza kufanya, Mheshimiwa Waziri wa Nishati na Madini atazungumza wakati wa Bajeti yake, kuna umuhimu wa kuirekebisha ile sheria ili nako tuweke fursa local content kwa maana ambayo itazingatia ajira, fursa nyingine, goods and services na kadhalika; na hapa Watanzania anaowazungumza watapata hizo fursa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siwezi kwenda kwa undani, lakini ninachoweza kusema ni kwamba ni ushauri mzuri, Serikali itautafakari na muda muafaka Waheshimiwa Wabunge mtaona matokeo yake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli niseme tu kwamba Mheshimiwa Mchengerwa ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba na Sheria amelisaidia sana Bunge hili. Kwa hiyo, sisi kwa upande wetu tumeunga mkono mchango wake katika hili na tuseme tu kwamba kama Wabunge wote mkiwa mnatoa michango ya aina hii ingetusaidia sana. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba, haya mambo ya kuzungumza viongozi wa mahakama yakome. Kambi yenu ya Upinzani na hasa Msemaji wenu wa Upinzani ana tabia sana ya kuwasema Majaji Wakuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tumekuwa hapa kwenye Bunge, kila akiwemo Jaji Mkuu, alikuwa anamshambulia sana Jaji Mohamed Chande amekuja huyu, naye anamshambulia tu. Sasa uliwahi kuona anaingia humu ndani? Kwa hiyo, acheni. Wananchi, muwapuuze hawa watu. Huyo anayekaimu ana mamlaka sawa na Jaji mwenyewe in full. Ndivyo tafsiri ya sheria inavyosema na wananchi waendelee kuwa na imani na mahakama yao. Hakuna kitu chochote kinachovurugwa. Kama ni mashauri waende mahakamani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine la ushauri, tuzingatie sana sheria. Haiwezekani Serikali ambayo imepewa jukumu la kusimamia utekelezaji wa Sheria, inapochukua hatua za kusimamia zile sheria mliozitunga ninyi wenyewe, mnasema hii ni Serikali ya kidikiteta, haiwezekani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unavunja sheria, unashitakiwa. Huwezi kushitakiwa halafu ukasema ni dikiteta. Mwalimu Nyerere alisema hivi, Serikali ni sheria. Hakuna kitu kinaitwa Serikali bila sheria na sheria zikishatungwa ni lazima zifuatwe. Ndiyo msingi wa utawala wa sheria mnaousema Mheshimiwa Shahari na ndiyo msingi wa Ibara ya 26 ya Katiba ya nchi yetu inayotaka kila mtu kuzingatia Katiba na sheria za nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hapa hakuna cha dikteta. Nchi hii inaongozwa kwa demokrasia na taasisi zake zote za kidola likiwemo Bunge, Mahakama na Executive, vinafanya kazi kwa ufanisi; na Ma-Rais walioko madarakani, wameingia madarakani kidemokrasia kwa Uchaguzi Mkuu. Eeh, Mheshimiwa Rais Magufuli na Mheshimiwa Rais Shein, wala hapa hakuna cha Udikteta. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ile ya kubadilisha Mawaziri na yenyewe ni kitu cha kawaida. Mheshimiwa Rais amepewa mamlaka ya kuteua Mawaziri wake na hatukuweka sheria ya ukomo kwamba huyu ata-serve kwa muda fulani na akimbadilisha anampeleka Wizara fulani. Msianze kuwatisha viongozi. (Makofi)
Mazingira hayo mnayojenga kwenye jamii ya watu kwamba kuna hofu imetanda, mwache. Kwa sababu huko nyuma mliwahi kusema kwamba mtaifanya Serikali isitawalike, haiwezekani. Mliwahi kusema mtafanya nchi isitawalike, haiwezekani. Wakati ule mlichukua vitendo, sasa mnaleta hoja kwamba hofu hofu, wakati mambo yanaendelea hapa. Shughuli zote za kijamii, kiuchumi, kisiasa zinaendelea kama kawaida, halafu mnasema eti kwamba kuna hofu. Haya lazima tuyapuuze. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia kushauri, haya mambo yote ambayo yametajwa hapa kwamba kesi sijui na vitu gani, haiwezekani ninyi mnashabikia wengine washitakiwe, ninyi mkishtakiwa mnasema sijui tunaonewa. That cannot be the case. Kesi nyingine mnayosema walifikishwa mahakamani wakaachiwa…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii.
The Written Laws (Miscellaneous Amendment) Bill, 2016
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mara nyingine tena nikushukuru kwa kunipa fursa hii niweze kujibu hoja mbalimbali na michango mizuri iliyotoka kwa Waheshimiwa Wabunge na kwa dhati kabisa nawapongeza Wabunge hawa waliopata fursa ya kuchangia na wengi hawakuchangia pia kwa sababu kama alivyosema Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria, walipata fursa ya kushiriki kwenye Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala wakati Kamati hiyo ilipokuwa ikijadili Muswada huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu uliotumika kwenye Kamati ya Katiba ya Sheria na Utawala ilikuwa ni kwamba, waliwaita kwenye Miswada hii ya marekebisho ya sheria mbalimbali. Waliamua kuwaita hata Wenyeviti wa Kamati mbalimbali ambazo zinaguswa na marekebisho ya sheria hii katika Miswada yote miwili. Pia waliwakaribisha hata Wajumbe wengine Wabunge wakaenda kutoa mawazo yao kwa vile kanuni zinaruhusu ndiyo maana umeona hali ni hii. Kwa hiyo, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao mizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Naomba kuwatambua Mheshimiwa Peter Serukamba, Mheshimiwa Adadi Rajabu, Mheshimiwa Janeth Mbene, Mheshimiwa Hussein Bashe, Mheshimiwa Shangazi, Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Harrison Mwakyembe na Wabunge wengine wengi na wengine wameniandikia vikaratasi hapo. Kwa hiyo niwashukuruni sana Waheshimiwa, bila kumsahau Mheshimiwa Andrew Chenge, Mtemi ambaye yeye pia alishiriki sana kwenye Kamati hii na hapa tumeendelea kusaidiana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, Waheshimiwa Wabunge, mchango wa Mheshimiwa Serukamba, Serikali tunaupokea kwa sababu ni ushauri mzuri, aliyoyasema yote kwamba ofisi hii, iyape kipaumbele sana mashauri haya ya ufisadi, lakini pia Serikali itenge fedha za kutosha kuifanya hii Division Maalum ya Mahakama Kuu iweze kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi ipasavyo, lakini bila kuzisahau pia Divisions na Mahakama nyingine na zenyewe ziweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme pia kwamba yeye ameunga mkono hoja hii iliyoko mbele yetu ya Serikali na Waheshimiwa wameizungumzia, Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria ameizungumzia, Mheshimiwa Shangazi amelizungumzia na tumelizungumzia sisi pia hata katika hotuba yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, unajua unapoanzisha division kuna mambo mengi sana, moja ni hili suala la kisera, lakini la pili ni haya masuala tu ya fedha kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wamezungumza na sisi, tumesema Jaji Mkuu ataanzisha kwa Subsidiary Registration yaani sheria ndogo, wakati fulani sasa ili hiyo division aende kuianzisha unaweza kuhitaji marekebisho katika sheria nyingine ili iwe na maana. Kwa hiyo ukiacha tu lile suala la kisera na gharama zitakazotumika katika mahakama hiyo wakati fulani akifanya consultation na Serikali inaona sawa, lakini ngoja pia sasa hii Mahakama yako unayotaka kuja kuianzisha iwe na maana, tu-harmonize na sheria hizi nyingine kwa sababu hii sheria ndogo haiwezi kufanya marekebisho katika sheria nyingine, ndiyo msingi huu wa kumtaka tu Mheshimiwa Jaji Mkuu anapotaka kuanzisha division hii apate kuweza kum- consult au kushauriana na Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili suala lenyewe kwanza halihusiani hata na utoaji wa haki kama tulivyofafanua ingekuwa ni kwamba akitaa kuhukumu kesi ndiyo sasa ashauriane na Mheshimiwa Rais unasema hapa anaingilia muhimili wa Mahakama na huu uhuru wa Mahakama umewekwa kwenye Katiba yetu na nchi ya Tanzania ni moja wapo ya nchi zinazosifika sana duniani kwa uhuru wa Mahakama.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba kushauri Waheshimiwa Wabunge wamechangia kwa nia njema sana, ni mashauriano tu ambayo hayaendi kabisa katika masuala ya kiutendaji waikubali hoja ya Mheshimiwa Jaji Mkuu kushauriana na Rais anapotaka kuanzisha hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hili ambalo baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wameshauri kwamba kila Jaji Mkuu; kuna sheria nyingi siyo hii tu, kuna sheria nyingi zinazosimamiwa na Waziri wa Katiba na Sheria ambazo zinamtaka pia Jaji Mkuu wakati fulani akitaka kutunga Kanuni fulani ashauriane na Waziri wa Katiba na Sheria au Waziri mwenye dhamana ya mausala ya Katiba na Sheria kwa nini? Kwa sababu yapo mambo mengine ya kisera, kama alivyosema Mheshimiwa Shangazi mambo mengine yanaibuka kule, ni hawa Mawaziri au Serikali wanakuwa katika mazingira mazuri ya kujua hasa mahitaji ya wananchi ni nini kwa wakati fulani. Wana nafasi kubwa ya ku- interact yaani kukutana na wananchi katika mikutano ya hadhara labda pengine wakati wa kampeni au wanaposhughulika na malalamiko mengine ambayo hayahusiani na mahakama.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kushauriana ni sawa tu, zaidi pia inaboresha hata hatua hiyo unayotaka kuja kufanya baadae. Kwa hiyo, huu ushauriano kati ya Mheshimiwa Jaji Mkuu na Waziri katika zile sheria ambazo zinataja kwamba kabla hajatengeneza Kanuni basi ashauriane na Waziri mwenye dhamana ya masuala ya sheria haiwezi kuchukuliwa kwamba inavunja muhimili na kwa sababu pia inaingilia mamlaka ya muhimili huu mwingine, kwa sababu Mahakama hii ipo kwa ajili ya kuwahudumia wananchi kama ambavyo Serikali ipo kwa ajili ya kuwahudumia wananchi kama ambavyo pia Bunge lipo kwa ajili ya kuhudumia wananchi.
Tofauti na wanasiasa labda kama tuseme Wabunge na Mawaziri huwezi kumkuta Jaji yeye anaitisha mkutano wa hadhara kule kwamba jamani ninyi mna kero gani hapo, ni vitu gani vinawasibu hayo anayapata kupitia kwa Waziri, Mbunge, Diwani, Viongozi wa Vitongoji na Mitaa au kwa Rais, Waziri Mkuu na Mawaziri wengine ndiyo msingi huu. Kwa hiyo, Kanuni zinazokuja kutungwa sasa na Mheshimiwa Jaji Mkuu ziakisi matakwa hasa na matarajio ya wananchi katika jamii ile, ndiyo msingi wa hilo Mheshimiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii hoja ya Mheshimiwa Janet Mbene, kwanza kila mtu anapaswa aitii na kuifuata Katiba ya nchi na sheria za nchi, kwa hiyo hata hawa ambao watafanya kazi au watahusika tu na utumishi kwa namna yoyote ile katika Mahakama hii awe ni Jaji, Mwanasheria wa Serikali, Wakili wa Kujitegemea au Mtumishi mwingine yoyote awe Polisi au Mtumishi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Ruswa, Law enforcement agencies wao pia wanapaswa kutekeleza wajibu wao kwa kuzingatia Katiba na Sheria za nchi. Kwa hiyo wakifanya makosa watawajibishwa kama wengine provided that, ili mradi ni kosa ambalo halikufanywa kwa sababu sheria inachosema kwa makosa haya sisi watumishi karibu wote tumelindwa hivyo na sheria mbalimbali ambayo yanafanywa na kitendo ambacho umekifanya in good phase inapimwa mahakamani. Kwa hiyo sio kwamba ni lazima uanzishe chombo kinginge cha hawa ma-ombudsman wa kukuchunguza na kuna check and balances na mfumo wa kufanya na maadili kwamba watu wazingatie hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala hili la bilioni moja, limezungumzwa wapo Waheshimiwa Wabunge wanaunga mkono bilioni moja na wengine wanasema ni kidogo sana, lakini mapendekezo haya yameletwa kwetu kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa na hawa ndiyo wapo kwenye industries yenyewe, wanajua hiki kitu ambacho tangu miaka mingi tumekuwa tukisema those grand corruptions, rushwa kubwa kubwa kama alivyosema Mheshimiwa Hussein Bashe ndiyo wakati wake, hawa watu wana uwezo huo. Kwa hizi kesi ya kufikia bilioni moja na kuendelea zipo za kutosha vinginevyo wasingetuletea hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiacha hiyo katika Muswada huu kwenye ile Ibara ya 8 tumezungumza, tunaporekebisha kile kifungu kidogo cha 3(c) mbali na makosa hayo yaliyoorodheshwa pale ya bilioni moja, kinatoa fursa pia kwa Mahakama ile kusikiliza kosa lolote ambalo kwa mujibu wa ile sheria, utaona makosa mengine wala hata kwa asili yake huwezi ukayaweka na thamani ya kifedha yapo mule ndani. Pia kifungu cha 12(4) cha Sheria hii ya Uhujumu Uchumi kinampa mamlaka Mkurugenzi wa Mashtaka au Mwanasheria yeyote aliyepewa mamlaka na yeye, kwenye masuala ambayo yana maslahi ya umma hata kama haifikii kile kiwango wala hata siyo lazima iwe kosa la uhujumu uchumi kuipeleka hilo suala mahakamani ili likasikilizwe na hiyo Mahakama.
Waheshimiwa Wabunge, naomba kuwatoa wasiwasi kwa ambao mnadhani kwamba makosa yale mengine hayatofika kule, labda yanayofikia milioni 800, au milioni 500 au milioni 300, kukiwepo na maslahi tu yatashughulikiwa. Siyo kwamba sasa haya hayatafikishwa mahakamani, tumezungumza kwamba haya yatashughulikiwa na Mahakama nyinginezo, iwe ni Mahakama ya Wilaya, Mahakama ya Hakimu Mkazi au hata Mahakama Kuu. Kwa hiyo, naomba kuwatoa wasiwasi Waheshimiwa Wabunge kuhusu hili ambalo mmekuwa mkitushauri hapa kwamba hiki kiwango cha bilioni moja kipunguzwe.
Mheshimiwa Rajab Adadi pia ametushauri kwamba pengine sasa hivi tuangalie badala ya kuweka kwenye thamani ya kifedha kwa makosa kama ya kukutwa na nyara za Serikali au madawa ya kulevya tuanze kutumia uzito badala ya thamani. Lakini hata thamani na yenyewe ina maana yake, ukiweka tu uzito itakuwa shida lakini uzuri ni kwamba makosa yote haya yatashughulikiwa naomba kushauri tu kwamba hata kama huu ushauri tungeukubali pengine pia tuipatie Serikali fursa tushauriane na wadau wengine tuone je, tukija na utaratibu huu tutafika wapi, itatusaidia au namna gani. Kwa hiyo ni ushauri mzuri cha msingi tu kwamba tushirikiane kupambana na vitendo vya ufisadi na hasa haya madawa ya kulevya, ujangili na makosa yote ambayo yameorodheshwa humu ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, ametoa ushauri muhimu sana kwamba tutakaohusika na utendaji katika Mahakama hii, awe ni Jaji, Mwanasheria wa Serikali, Taasisi yale yanayohusikana na makosa, kupata mafunzo ni muhimu kweli na tumekuwa tukifanya hivi ni ushauri mzuri huu tunauzingatia, ili sasa kuifanya hii Mahakama iwe na maana ambayo ilikusudiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama kuna jambo nimelisahau basi Waheshimiwa Wabunge waniwie radhi, kwa mara nyingine tena nikushukuru wewe mwenyewe kwa kunipa fursa hii, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge, naomba kutoa hoja.
The Written Laws (Miscellaneous Amendment) (No.2) Bill, 2016
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuweza kutujalia tena kupata fursa hii kutimiza wajibu wetu kama Wabunge ambao moja ya jukumu letu kubwa la msingi ni kutunga sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru pia kwa kunipatia fursa hii na pia kwa mwongozo ambao umeutoa siyo muda mrefu uliopita.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kabla sijaendelea, niseme tu kwamba kwa kuzingatia hayo uliyoyasema mwishoni, pia Serikali imeandaa jedwali la ziada la marekebisho, the further schedule of amendment ambayo pia imezingatia hili ambalo umelisema kuhusu adhabu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia niseme kwamba, hizi sheria unazoziona ni sheria mbalimbali na kila sheria ina scheme yake ndiyo maana unaona kwenye sheria fulani adhabu yake ni hii, halafu kwenye sheria fulani adhabu yake inakuwa ni tofauti na nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kwanza niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao pia mmepata fursa ya kuchangia kuanzia juzi na mpaka leo asubuhi hii tunapoenda kuhitimisha hoja hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kuwataja Waheshimiwa ambao wamepata fursa pia ya kuchangia kwenye hoja hii, Mheshimiwa Sophia Simba, Mheshimiwa Taska Mbogo, Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mheshimiwa Salum Rehani, Mheshimiwa Kanyasu, Mheshimiwa Subira Mgalu, Mheshimiwa Janet Zebedayo Mbene, Mheshimiwa Mwalongo, Mheshimiwa Martha Moses Mlata, Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma na Mheshimiwa Ester Michael Mmasi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wao umekuwa mzuri sana kuhusu Muswada huu na mengine yalikuwa ni mapendekezo na mengine yalikuwa ushauri. Kwa ujumla ushauri tunauzingatia.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala ambayo ilipitia fursa kubwa fursa kubwa ya kuangalia Muswada huu kwa undani sana. Mapendekezo na ushauri walioutoa, tumeuzingatia na mtaona tumeyazingatia haya mapendekezo ya Kamati kwenye jedwali letu la marekebisho ambayo tumewagawia Waheshimiwa Wabunge.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, nisingependa sana kuchukua muda wako kwenye eneo hili. Hili nikiri tu kwamba Waheshimiwa Wabunge wenyewe wakishaona jedwali letu la marekebisho, ushauri wote wa Kamati ya Katiba, Utawala na Sheria umezingatiwa kama ambavyo inaonekana hapo na sisi tunawashukuru sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niseme kwamba kitu ambacho kimewagusa sana Waheshimiwa; kwanza, nawapongeza wote kwa kuunga mkono hoja hii, Waheshimiwa Wabunge wote mliopata fursa ya kuchangia, lakini pia sasa kuna kitu ambacho naomba nikizungumze hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, moja ni hili suala ambalo la matumizi ya vipimo ya DNA kusudi kuthibitisha kosa. Huu ni ushauri mzuri sana kwa sababu moja, kanuni ya msingi katika mashauri ya jinai ni kwamba shitaka linathibitishwa tu pale kunakuwa hakuna shaka yoyote. Proof beyond reasonable doubts, yaani wanaoendesha kesi wana jukumu la kuthibitisha shitaka dhidi ya mshtakiwa bila kuacha shaka yoyote ya msingi.
Kwa hiyo, sasa hapo ndipo unapoona umuhimu wa hoja za Waheshimiwa Wabunge, kwamba aah, sasa kama suala lenyewe ni hili, halafu linabeba adhabu kubwa ya miaka 30; kuna umuhimu sasa kabla ya huyu mtu hajatiwa hatiani, basi kuwe na uthibitisho kabisa na moja ya uthibitisho huu kama Waheshimiwa Wabunge walivyoshauri angalau ikiwa imepata vipimo ya DNA, maana vile kwa kawaida ni mara chache kusema uongo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwaambia Waheshimiwa Wabunge kwamba, licha ya hivi vipimo vya DNA, Mahakama iko makini sana kwa sababu wakati wote upande wa mashitaka una jukumu la kuthibitisha kesi yao bila kuacha shaka yoyote ya msingi. Kwa utaratibu tulionao sasa hivi, maabara yetu, uwezo wake ni kupima vile vinasaba vya DNA wakati mtoto ameshazaliwa, siyo wakati bado yuko tumboni. kwa hiyo, kwa muda tutaendelea kutumia hii ya ushahidi wa kawaida wa kuthibitisha bila kuacha shaka yoyote ya msingi. Wakati fulani labda mtu mwenyewe amekiri hadi hapo itakapofika huko.
Mheshimiwa Naibu Spika, furaha yangu mimi Waheshimiwa Wabunge mtaona kwenye Bunge lako hili Tukufu, tumesoma kwa mara ya kwanza Muswada wa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa sasa katika sheria hii, moja ya mambo ambayo yatafanyika ni kuimarisha hii Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali ili aweze kuwa na uwezo mkubwa zaidi wa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi ipasavyo. Mtapata fursa sasa maana umesoma kwa mara ya kwanza Bunge linalokuja mnaweza mkapata fursa ya kuisoma na mara ya pili na ya tatu na kutunga, lakini tunatambua umuhimu wa hoja hii ambayo imetolewa na Waheshimiwa Wabunge.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ameshauri Mheshimiwa Mwalongo kwamba miezi tisa nayo siyo mingi sana. Tutaangalia utaratibu unakuwaje, lakini ni ushauri mzuri sana kwamba kabla mtu hajatiwa hatiani, si asuburi tu mtoto azaliwe kwanza?
Mheshimiwa Naibu Spika, tunawashukuru pia Waheshimiwa Wabunge kwa mchango wao kuhusu adhabu. Hii adhabu ya miaka 30 sisi tulichokifanya kwa mtu anayempa mimba mtoto wa shule au ambaye yuko chini ya miaka 18, tumeoanisha na Ile sheria iliyopo ya kanuni ya adhabu. Ukisoma ile Sheria ya Kanuni ya Adhabu, kifungu cha 31, ndiyo adhabu inavyosema.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, siyo adhabu mpya, tumefanya kuoanisha tu ile adhabu. Siyo kwmaba hii adhabu ni mpya, hapana. Tumeoanisha tu pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, wamezungumza Waheshimiwa Wabunge kwamba sasa sheria hii inagusa tu wale ambao wako shuleni na wale ambao hawako shuleni je?
Mheshimiwa Naibu Spika, ile Sheria ya Kanuni ya Adhabu inawagusa hata ambao hawako shuleni ambao wako chini ya miaka 18 kwa sababu ukifanya tendo la kujamiiana na mtoto huyu ambae yuko chini ya umri wa miaka 18 hata kama mlikubaliana kwa mujibu sheria tunasema hiyo ni kubaka yaani ile ridhaa ya yule mtoto haichukuliwi kwamba kweli ni ridhaa. Kwa hiyo hiyo hata hawa ambao hawako shuleni ni marufuku kupewa ujauzito ilimradi wako chini ya miaka 18.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo tunaloliona hapa ni kwamba upande wetu Serikali kwa kiasi fulani hatukusimamia vizuri utekelezaji wa sheria zile, lakini Serikali haiko kila mahala, tuwaombe Waheshimiwa Wabunge mtusaidie ninyi ndiyo mnaishi vizuri na Wananchi kule. Mya-report matukio haya halafu Serikali iyachukulie hatua. Huo ndiyo ushauri ambao ningependa kuusema kwa ujumla.
Mheshimiwa Rehani alichangia akitushauri juu ya mwaka mmoja wa mafunzo ya vitendo kazini, internship training program kwa veteran medical officers, alisema kwamba huu hautoshi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi upande wetu tunaomba kushauri Wabunge wakubali mapendekezo ya Serikali kwamba utaratibu katika hizi fani zote hizi iwe ni medicine, iwe ni legal, internship imekuwa inachukuliwa ni mwaka mmoja. Mafunzo haya ndiyo sasa huyu mtu amesoma degree yake amemaliza sasa ili atambuliwe kwamba ni Veterinary Medical Officer (Daktari wa Mifugo) ndiyo anapaswa pia aende mafunzo ya vitendo na uzuri ni kwamba kwa madaktari wa binadamu na hawa Veterinary Medical Officer wakati wako shuleni mafunzo yao kimsingi huwa yanahusisha vitendo sana.
Kwa hiyo, tunaomba kwamba huu mwaka mmoja huu unatosha ni kwa mtu ambaye sasa ana shahada ya kwanza ya veterinary medicine sasa ili atambuliwe na kusajiliwa kwamba huyu ni Veterinary Medical Officer basi awe amepitia mafunzo kuliko ilivyo sasa hivi tu kwamba anamaliza shahada ya Chuo Kikuu labda pale Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine halafu anatambuliwa bila hata kwenda ile practical training, kwa hiyo huo ndiyo ulikuwa msingi wa mapendekezo yetu hayo tunaomba Waheshimiwa Wabunge waunge mkono.
Mheshimiwa Naibu Spika Mheshimiwa Rehani alishauri pia kwamba viboko tu havitoshi, tuongeze vingine mbadala, lakini spirit ya sheria hii ni kwamba watoto wote hawapaswi kuchapwa viboko na ndiyo tumeshauriwa na Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala kwamba turekebishe hiyo na tumerekebisha kwahiyo Watoto hawa wanapofanya makosa au mtu yoyote ambae ana miaka chini ya 18 hata akimpa mtu mzima ujauzito au akampa ujauzito mtoto mwenzake yaani under 18, adhabu yake siyo kifungo, adhabu yake ataadhibiwa huyu kwa mujibu wa chini ya sheria hii ya watoto ambayo hairuhusu hata hivyo viboko. Kwa hiyo Waheshimiwa naomba kushauri hili tulizingatie.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wakati pia ambapo tunapendekeza sana watoto hawa wasichapwe viboko, ushauri wangu pia ni kwamba sisi wazazi tuimarishe usimamizi wa watoto wetu kuwalea katika maadili yanayopasa vinginevyo tutabaki na Taifa la watu wa ajabu sana who are not much responsible yaani mtu ambaye yeye kila kitu kwake ni ruhusa. Haheshimu wazazi, haheshimu cha mtu mzima yaani kila kitu yeye ni halali, tusije tukatengeneza Taifa la wahalifu. Tutakuja kutengeneza Taifa la watu wahalifu tu, watu wanaokuwa wanapiga watu hovyo hovyo, watu watakaoanza kuoana wenyewe kwa wenyewe wanaume kwa wanaume, wanawake kwa wanawake kama ambayo yanatokea huko kwahiyo mimi naomba sana Waheshimiwa wakati tunashauri Serikali kuondoa viboko kwa watoto ni kweli sawa, lakini tusimamie malezi ya watoto wetu, ndiyo ushauri wangu mimi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunaupokea ushauri wa Mheshimiwa Subira Mgalu ambaye amesema kwamba drop out zimekuwa nyingi sana, yaani utoro na yeye amesema unaitwa mdondoko na utoro huu hausababishwi na ujauzito na kuolewa tu, kwa hiyo ni kweli lakini naomba kulijulisha Bunge lako tukufu kwamba zipo kanuni za elimu ambazo pia zinawataka Maafisa Elimu wa Wilaya kila robo mwaka watoe taarifa za ujauziuto, za ndoa na za utoro zilizotokea katika maeneo yao na kufanyiwa kazi. Katika hali hii ambayo sasa Serikali imekuja na mpango huu mahususi wa kuhakiksha kwamba watoto wote wanapata elimu kuanzia elimu ya msingi mpaka elimu ya sekondari na ukiona mapendekezo ya Serikali kwenye kifungu cha 60 cha Sheria ya Elimu inaweka mkazo zaidi sasa hawa watu sasa waweze kwenda kusoma wamalize shule, wasioe wala wasiolewe. Kuna umuhimu sana sisi upande wa Serikali kusimamia suala hili kusudi kwanza tupunguze hawa ambao hawako chini ya miaka 18, hawajafikisha miaka 18 lakini hawakupata fursa ya kwenda shule, fursa hii ya kutoa elimu bure itatuwezesha na kama sisi Serikali tukilisimamia vizuri sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunauunga mkono na tunaukubali ushauri wa Mheshimiwa Janet Zebedayo Mbene kuhusu Serikali kutoa elimu kuhusu hii Sheria ya Trafficking in Persons na kweli waathirika wakubwa ni watoto na wakina mama. Elimu inatakiwa itolewe ya kutosha na mimi naomba Waheshimiwa Wabunge hili mtusaidie kulifanya na sisi Serikali tutachukua hatua kwa kweli alichokisema Mheshimiwa Mbene ni kweli, tatizo ni kubwa na mimi nasikitika sana, haya ni mojawapo ya mambo ya msingi ambayo Waheshimiwa Wabunge tunapaswa tuyapigie kelele sana kwasababu kwanza wanadhalilisha sana wanawake na watoto. Mimi ninachoshangaa ni kwamba kila tunapoenda kwenye kusisitiza haki za watoto na wanawake, lakini wakati huo huo haki za watoto na wanawake ndiyo zinazidi kuingiliwa zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo lazima tuje na Mkakati mpya zaidi tunaposhugulika na mambo kama haya kwa hiyo nakubali kabisa ushauri wa Mheshimiwa Mbene juu ya elimu hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ametushauri kuhusu watoto wanapotoa ushahidi wao. Kwa mujibu wa sheria ile, ushahidi wa watoto na hasa kwenye mambo ya kubakwa hapa hiyo sheria ya kanuni ya adhabu. Kesi yoyote ile ambayo inamhusu mtoto hasa hawa waliobakwa huwa zinasikilizwa kwa siri kwa lugha ile ya kiingereza wanaita incamera, haisikilizwi kwenye mahakama ya hadharani, kwa hiyo hii kesi itasikilizwa kwenye chamber siyo kwenye open court na mle ndani hata waandishi wa habari hawaruhusiwi na ile mahakama ina-regulate proceedings zake ili kumlinda huyu mtoto, moja apate fursa ya kutoa ushahidi akiwa huru lakini cha pili kuondoa ile kadhia ya mnyanyasiko ule.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunakubali pia ushauri wa Mheshimiwa Mwalongo kuhusu kuimarisha usimamizi wa Sheria ya Misitu lakini pia ametushauri Mheshimiwa Mwalongo juu ya kutaifisha zile mali za mazao ya misitu. Ni kwei sheria ya sasa inaruhusu hivyo lakini comfort ambayo Waheshimiwa Wabunge wameomba kuwapatia ni kwamba kama hii sheria tuliyopitisha juzi hapa ya Economic and Organized Crimes Control Act ile ya mafisadi ile, kufanya makosa chini ya Sheria hii ya Misitu pia ni kosa la uhujumu uchumi na ambalo hilo kosa la uhujumu uchumi kwa mujibu wa sheria ile pia adhabu zinazotolewa ni pamoja na kutaifisha zile mali lakini hata sheria yenyewe ya misitu sasa hivi kama alivyosema Mheshimiwa Mwalongo imetoa hiyo fursa, tatizo liko kwetu sisi watendaji tumekuwa hatuisimamii hii.
Kwa hiyo, niwaombe tena Waheshimiwa Wabunge kwamba katika maeneo yenu mliko mtusaidie ku-report vitendo vya aina hiyo kusudi moja, tuzuie deforestation yaani tuzuie mambo ya kuharibika kwa misitu yetu lakini cha pili tupate mazao stahili na cha tatu tuwafanye hawa watu wanaofanya uhalifu hawa wasiweze kunufaika na huo uhalifu wao, kwa hiyo, nishukuru sana.
Mheshimiwa Martha Mlata tumesema sehemu fulani nimejibu swali lako na sasa sheria haiwezi kumlazimisha mtoto huyu wa kike atoe ushirikiano yaani tukaweka nayo ni adhabu. Tukimuwekea naye huyu adhabu tunaweza tukajikuta tunakosa kabisa hata ushirikiano. Kwanza ameshapewa ujauzito akiwa under 18 nayo ni adhabu ya kutosha, sasa sisi tutumie mbinu za kawaida za medani kumfanya huyu mtoto atoe ushirikiano. Lakini ushirikiano pia nao aseme tu Mheshimiwa Kanyasu ametusaidia hapa amesema unaweza ukakuta binti mmoja amekuwa ana watu wengi anafanya nao mambo haya kabla hata ya umri wake. Sasa anaweza akatoa ushirikiano kwamba akamtaja mtu fulani lakini kumbe yule siyo huyo, mhusika mwingine ni yule pale na hapo ndipo unapokuja kuona ushauri mzuri tunaupewa na Waheshimiwa Wabunge kwamba kuna umuhimu mkubwa sana wa kutumia vipimo vya DNA.
Kwa hiyo mimi naomba sana huyu mtoto wa kike tumuache tu kwanza. Kwanza anakuwa na umri mdogo na yeye tukianza kumuwekea adhabu itatupatia shida.
Mheshimiwa Naibu Spika, ametushauri tu kwamba yule anayetiwa hatiani Mheshimiwa Mlata ametushauri basi alipe fidia kabla hajaenda kutumikia adhabu. Naomba kushauri kwamba sheria yenyewe ile ya kanuni ya adhabu inayohusu haya makosa ya kubaka pia imetoa fursa ya kutoa ile fidia, sasa ni wakati gani, kama anazo atazilipa kabla hajakwenda huko gerezani vinginevyo atatoka, akitoka ndipo atakuja kulipa.
Kuna Mheshimiwa amezungumza nadhani ni Mheshimiwa Mlata, alizungumza juu ya matunzo madogo yanayotolewa kwa ajili ya mtoto. Haya matunzo yalikuwa chini ya Sheria inaitwa Affiliation Act. Sheria ile ilifutwa na Sheria ya Mtoto na chini ya Sheria ya Mtoto sasa kila mtoto lazima awe na mzazi haijalishi kama amezaliwa ndani ya ndoa au nje ya ndoa ndizo sheria tunazozitunga hapa na imetoa jukumu la msingi ni lazima kwamba wazazi wanajukumu la kuwatunza watoto wao kuhakikisha kwamba wanapata chakula, wanapata elimu na matunzo mengine. Kwa hiyo, hiyo ndiyo hali halisi na kwahiyo viwango vile siyo kama ilivyokuwa wakati ule kwenye ile Sheria ya Affiliation Act ambayo ilishafutwa, watoto wote sasa wanatambulika na wazazi tumepewa jukumu la kuhakikisha kwamba wanapata elimu, wanapata chakula na matunzo mengine yoyote stahili na sisi tunaokiuka tunawajibishwa chini ya hiyo sheria.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mchafukoga, Mheshimiwa Hawa Chakoma, naomba samahani kwa Mheshimiwa kwa kulitamka hilo jina vibaya.
Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma, moja ameipongeza Serikali kwa kuja na kifungu kipya cha Ibara 45A ya Sheria hii ya Taasisi za kazi na tunashukuru sana. Lakini pia tumepata fursa ya kuliangalia jedwali lake la marekebisho na sisi tumekubali yale mapendekezo yake na tumeandaa further schedule of amendements (marekebisho ya ziada ya Serikali).
Moja, ambacho tumekifanya, pendekezo lake lile la kufanya adhabu isiwe chini ya kuanzia 100,000 hilo tunashauri kwamba avute subira kwanza kwa sababu tulichokifanya pale hii ni adhabu ya chini ya kuanzia. Ukisoma kile kifungu tumesema not less than yaani yule anayetiwa hatiani adhabu yake hatujaweka ukomo. Sasa labour officer ambaye atakuwa ni mtu wa ajabu sana atakuwa anatumia vibaya madaraka yake akaona pale huyu hastahili kupigwa 500,000 halafu akampiga 100,000 kuna matatizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha pili Waheshimiwa Wabunge, spirit ya hizi compounding offences haya makosa ya papo kwa papo huwa kwa kawaida ni makosa madogo madogo, huwa hatu-deal na makosa makubwa na kwa hiyo ukisoma ile Sheria ya Labour Institutions Waheshimiwa wabunge someni kifungu cha 63 na 64 kimeorodhesha sasa yale makosa makubwa makubwa na adhabu yake, kwa hiyo ndiyo msingi huo kwamba hii tungeshauri kwamba ibaki hii akitiwa hatiani anapewa adhabu isiyopungua shilingi 100,000 lakini anaweza akampiga shilingi 1,000,000.
Mheshimiwa Naibu Spika Waziri amepewa Mamlaka sana chini ya kifungu cha 195 cha sheria hiyo ya kwenda kutengeneza kanuni. Kwahiyo kwenye kanuni zile, Waziri mwenye dhamana ya masuala ya kazi atatengeneza kanuni na viwango kwamba huyu akifanya kosa hili atoe kiwango gani cha adhabu hii ambayo huyu mtu anaruhusiwa kumpa adhabu pale pale. Na niseme pia kwamba adhabu hii huwa haitumiki kama huyo anayepewa adhabu hakuridhia, kwa hiyo huyu mtu anayepewa adhabu ndiyo anaridhia la sivyo hilo suala sasa linabidi liende mahakamani. Hilo la kwanza niliomba nilifafanue.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili Mheshimiwa mapendekezo yake, tumechukua ile sehemu ya mwisho katika mapendekezo yake yale sub-section 6 anayoipendekeza. Sisi badala ya kwamba haya yaende kwenye Social Security Regulatory Authority tumesema kama Labour Officer wakati anakagua, moja akagundua kwamba huyu Bwana ame-under declare au ametoa taarifa ambazo siyo za kweli, a-report huyu Labour Officer kwa mfuko stahili wa ile social security. Kwa mfano, kama hawa watu ni watu wa NSSF basi huyu a-report NSSF kwamba hapa Bwana kuna tatizo hili, watu wako hawatoi contribution yaani mtu ambae hapeleki ile michango ya watumishi. Badala ya ku-report kwa Social Security Regulatory Authority sasa social security yeye ha-deal na waajiri yeye ana-deal na hii mifuko. Yeye anaikagua hii mifuko kwa hiyo anapoikagua ile mifuko ndiyo anajua kwamba ninyi kwanza contribution kwa nini ziko chini? You don’t enforce the law, hamsimamii vizuri wajibu wenu.
Kwa hiyo, sisi tunaomba Mheshimiwa Chakoma ukubali mapendekezo haya ya Serikali kama yanavyooneka kwenye jedwali la ziada la marekebisho ya Serikali, lakini pia tumekubali tunarekebisha tulifanya makosa pale, tuliruka kifungu cha nne kwahiyo pia katika marekebisho hayo kama yanavyoonekana kwenye jedwali lile tume-renumber, tumeviandika vifungu vile upya na hiyo Mheshimiwa ndiyo tulikuwa tunaomba ushauri kuhusu hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba kumshauri Mheshimiwa Mmasi kwamba hawa watoto wa shule ikiwa wako chini ya miaka 18 hawawezi kwenda gerezani, ni wale ambao tu wamezidi miaka 18. Kwa hiyo asiwe na wasiwasi kwamba magereza yetu yatajaa vijana, nguvu kazi lakini na wao wajifunze kuishi basi kwa kuzingatia Katiba na sheria za nchi na maadili wanayopewa na wazazi na kwenye taasisi za dini kama makanisani na misikitini ili wawe watoto wazuri.
Kwa hiyo, mimi ndicho ambacho ninachoweza kusema kwamba…na ndiyo maana unaona katika sheria hii tunasema inapotokea mhalifu ni mtoto aliye chini ya miaka 18 yeye atahukumiwa kwa mujibu wa Sheria ya Watoto ambayo haitoi adhabu ya kwenda gerezani.
Mheshimiwa Mmasi ametushauri pia kwamba Serikali ipitie tena upya sheria ya ndoa na sheria ya vileo ili kuioanisha na haya mapendekezo ya sheria hizi zinazoletwa sasa na sisi tunakubali ni ushauri mzuri, hili ni suala linalohitaji ushirikishi mpana wa kijamii, si suala ambalo tunaweza tukaliamulia hapa lakini ushauri wa Mheshimiwa Mmasi ni ushauri mzuri na sisi Serikali tunaunga mkono, tunakubaliana na ushauri huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sikumbuki pia kama kuna kitu nimeakiacha hapa lakini niseme tu kwamba nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii na nawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa mara nyingine naomba kutoa hoja.
Muswada wa Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi, wa Mwaka 2016
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kupata nafasi hii ya kuchangia kwenye Miswada hii miwili muhimu. Nikushukuru kwa kunipa fursa hii na naomba kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, Uvuvi na Mifugo kwa kuleta Miswada hii miwili ambayo ni muhimu sana kwa maslahi ya Taifa hili kwenye masuala haya ya kilimo na uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Wabunge wote waliopata fursa ya kuchangia Miswada hii na sisi tunawashukuru tumeyafanyia kazi yale mapendekezo yao. Wajibu wangu asubuhi hii ni kujibu tu hizi hoja chache za kikatiba na za kisheria pengine zitatusaidia wale ambao hatuelewi masuala ya Katiba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni Muswada wa Kilimo kutotaja matumizi ya sheria hii katika pande mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa mujibu wa Katiba siyo lazima utaje kwenye Muswada kwamba sheria hii itatumika upande upi kwa sababu masharti yenyewe yamewekwa kwenye Katiba. Ukisoma Ibara ya 64(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzani, inasema:-
“Mamlaka yote ya kutunga sheria juu ya mambo mengine yote yahusuyo Tanzania Bara, yatakuwa mikononi mwa Bunge”.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kama yanakuwa mikononi mwa Bunge, Bunge linalozungumzwa hili ni Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania siyo lazima utaje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inaendelea kusema kwenye ibara ndogo ya (2) kwamba:-
“Mamlaka yote ya kutunga sheria katika Tanzania Zanzibar juu ya mambo yote yasiyo mambo ya muungano yatakuwa mikononi mwa Baraza la Wawakilishi”.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli sheria inapotungwa ina maana itatumika pale pale na Ibara hii ya 64 imeendelea kufafanua mambo mengine mengi. Ibara ndogo ya (4) inasema hivi:-
“Sheria yoyote iliyotungwa na Bunge kuhusu jambo lolote haitatumika Tanzania Zanzibar ila kwa mujibu wa masharti yafuatayo:-
(a) Sheria hiyo iwe imetamka wazi kwamba itatumika Tanzania Bara na vilevile Tanzania Zanzibar au iwe inabadilisha, kurekebisha au kufuta sheria inayotumika Tanzania Zanzibar”.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sharti lililopo pale ni kwamba kama hiyo sheria tunayoitunga itatumika pande zote mbili za Muungano ndiyo lazima utaje. Kwa sababu hiyo tuna sheria nyingi sana ambazo zimetungwa bila kulazimika kutaja hivyo, nitawatolea mifano. Sheria hizo ni kama zifuatazo:-
(i) The Marine Parks and Reserve Act, No. 29 of 19994;
(ii) The Plant Protection Act, Cap.132, No. 13 of 1997;
(iii) The Plant Breeders‟ Right, Cap.344, Na. 9 of 2012;
(iv) The Merchant Shipping Act, Cap.165, Na.21 of 2003;
(v) The Tanzania Fisheries Research Institute Act, Cap.280, No. 6 of 1980;
(vi) The Tanzania Industrial Research and Development Organization Act, Cap.159, No. 5 of 1979; na
(vii) The Public Service Act, Cap.298, No. 8 of 2002.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, siyo lazima sheria itaje, lakini tumekuwa tukipokea haya kwa masharti ya Katiba yenyewe. Katika tu kufanya ufafanuzi tumekuwa na tabia sheria nyingine tunaandika kwamba sheria hii itatumika Tanzania Bara peke yake lakini hata usipotaja siyo kosa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge hili lina mamlaka mawili; moja linatunga sheria za kutumika pande zote mbili kwa mambo ya Muungano lakini pili linatunga sheria kwa ajili ya Watanzania Bara kama ambavyo tumeshasoma katika Ibara ya 64. Kwa hiyo, kama haikutaja ujue tu kwamba hiyo sheria itatumika Tanzania Bara peke yake. Waheshimwa Wabunge, mkisoma Ibara yote ya 64 mtaona tunachokifanya kwenye hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tulikubali tu ushauri wa Kamati ili kuleta clarity kwenye uandishi. Kwa hiyo, hata jana tulipowasilisha Muswada huu Waziri aliwasilisha pia na Schedule of Amendment na Wabunge walipokuwa wanachangia tayari ile Schedule of Amendment walikuwa nayo ambayo inataja kwamba hii sheria itatumika Tanzania Bara peke yake. Kwa hiyo, niliona nitoe ufafanuzi wa suala hili ili litusaidie tunapokwenda mbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nimeona nilitolee ufafanuzi hapa ni kwamba masuala ya utafiti yako kwenye mambo ya Muungano, ni kweli unaipata kwenye Ibara ya 4(3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jedwali la Kwanza linalotaja mambo ya Muungano pale ndiyo unaona utafiti. Hata hivyo, suala la msingi hapa ina maana kila ukishakuwa utafiti unakuwa wa Muungano? Tafsiri ya sheria ni kwamba huo utafiti unaoutungia sheria ni ule unaohusu Muuungano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma hiyo Nyongeza ya Kwanza ya Katiba utakachokiona ni kwamba suala la kilimo na mazao ya kilimo siyo masuala ya Muungano na suala la samaki na uvuvi siyo suala la Muungano. Kwa hiyo, huwezi kutunga sheria na kuifanya kuwa ya Muungano eti kwa sababu tu imetajwa kwenye utafiti. Kama unataka kufanya utafiti kwenye mambo ya ulinzi na usalama hilo ni la Muungano utatunga sheria ambayo ni ya Muungano na mambo mengine yaliyowekwa pale. Kwa hiyo, hili siyo lazima na nilifikiri nilitolee ufafanuzi ili litusaidie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Deep Sea Fishing Act, kule uvuvi umefanywa kuwa wa Muungano kwa sababu ya United Nation Convention on the Law of the Sea. Katika international community pale hakuna Tanzania Bara wala hakuna Zanzibar and this should be so much clear and understood by whole Members of the House. Katika Jumuiya ya Kimataifa tunajulikana kama Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ndiyo maana tumetunga sheria kwa makubaliano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwamba uvuvi katika kina cha chini cha bahari huo utakuwa ni suala la Muungano na hapo hakuna dhambi madam Serikali za nchi mbili hizi zilikubaliana, kwa hiyo, niwatoe wasiwasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria iliyokuwepo ya Tanzania Fisheries Research Act ya mwaka 1980 ambayo ndiyo tunakusudia kuifuta kama mtaridhia ilikuwa inatumika upande mmoja tu. Kwa hiyo, hili nalo nilifikiri nilitolee ufafanuzi ili kuwaondoa wasiwasi Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kulitolea ufafanuzi na ambalo linajirudia mara kwa mara na nashindwa kuelewa ni kwa nini nalo ni jukumu la Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Mwanasheria Mkuu wa Serikali anazaliwa na Ibara ya 59 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na pale anatajwa kwamba pale na katika sheria nyingine ataitwa tu Mwanasheria Mkuu haisemi ni Attorney General of the Executive.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kuchanganya katika matumizi ya neno Serikali kwa sababu ya umaskini wa msamiati kwenye Kiswahili tu. Tunaitumia Dola/State kwa kusema Serikali, tunatumia Executive pia kwa kusema Serikali but kinachozungumzwa kwenye Ibara ya 59 pale ni State/Dola ambayo inagusa mihimili yote na maana yake kwa Kingereza ni Government, someni The Interpretations of Laws Act.
Mheshimiwa Mwenyekiti, unaposema Government it includes all the three department of the state that is the Executive, the Legislature and the Judiciary. Kwa hiyo, pale unaipata Mahakama, Bunge na Utawala. Hata katika kuandika hapo, mimi naandika hizi sheria unaona pale nimeandika Attorney General sisemi Attorney General of the Executive. Ndiyo maana Mawakili wa Serikali wote kama mimi hapa naitwa State Attorney/Wakili wa Dola na hapa ni Dola ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hatuiti Mawakili wa Executive ni State Attorneys, State ni Dola, kule Uingereza wanaitwa Crown Counsel. Kwa hiyo, nilifikiri niliseme hili litusaidie kwa sababu linajirudiarudia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mlinzi wa maslahi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika international community na ndani ya nchi ni Attorney General. Ndiyo maana kifungu cha 17 cha Sheria ya Utekelezaji wa Majukumu ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mwanasheria Mkuu wa Serikali anaweza kuingilia shauri lolote lile ili mradi lina maslahi ya umma na imetajwa pale Waheshimiwa Wabunge someni kifungu cha 17 mtaona. Kinasema Mwanasheria Mkuu wa Serikali anaweza kuingilia masuala yanayohusu Bunge, Mahakama na maslahi ya taasisi yoyote ya Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 59(4) nafikiri niisome labda itatumalizia mambo haya yasiwe yanarudiarudia, haki hii imewekwa Kikatiba, hamuwezi mkataka Attorney General asiingilie kwenye mambo yanayohusu maslahi ya nchi hii, ni mpaka mfute hii Ibara ya 54 ndiyo mtake Attorney General asiwepo pale. Inasema hivi:-
“Katika kutekeleza kazi na shughuli zake kwa mujibu wa ibara hii, Mwanasheria Mkuu atakuwa na haki ya kuhudhuria na kusikilizwa katika Mahakama zote katika Jamhuri ya Muungano.” (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, so go and amend this Article of the Constitution and then you are done with the Attorney General, sijui kama itawezekana. Mkiunda Serikali ambayo haiheshimu mamlaka ya Attorney General, itakufa siku hiyohiyo. Kwa hiyo, nilifikiri niliseme hili litusaidie tumalize haya mambo. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mifano mingi sana ya sheria ambazo zimetungwa tangu nyuma ambazo zinataja umuhimu wa Attorney General kuingilia kati siyo tu kwenye hizi sheria tunazozitunga leo. Sheria hizo ni:-
(i) The Ports Act ya mwaka 2004 yaani Sheria ya Mamlaka ya Bandari ya mwaka 2004, section 4(2);
(ii) The Surface and Marine Transport Regulatory Authority, hii Sheria ya SUMATRA ya mwaka 2001;
(iii) The Energy and Water Regulatory Authority ya mwaka 2001, hii ni Sheria ya EWURA; na
(iv) The Tanzania Communication Regulatory Authority ya mwaka 2003.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, siyo sheria za kwanza hizi. Ukielewa lengo la Katiba kama lilivyo kwenye Ibara ya 59 then hutakuwa na shida. Kwanza siyo lazima aingie, anaingia pale ambapo inalazimika. Kwa hiyo, nilifikiri niyatolee ufafanuzi masuala haya kwa faida yetu sisi wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari za Mwaka 2016
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipatia fursa hii ili kuweza kupata nafasi ya kuchangia na kutoa ufafanuzi kwenye masuala ya kisheria na ya kikatiba ambayo yamejiri hapa. Lakini nikupongeze pia wewe kwa kuongoza mkutano huu vizuri na wakati huo huo nampongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutimiza mwaka mmoja ofisini akiwa mkuu wa nchi hii, kiongozi wa Serikali na Amiri Jeshi Mkuu wa nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia fursa ya kumpongeza kwa umuhimu anaounesha kwa waandishi wa habari. Moja imedhihirika hata anapotimiza mwaka mmoja ofisini waandishi wa habari ndio watu aliochagua kuongea nao ili ku-communicate na wananchi wote. Kusema ukweli Serikalini na kwenye hizi taasisi za umma tunawasiliana kwa madokezo, kwa maandishi lakini ni Serikali kwa ajili ya wananchi. Huwezi kuwasiliana na wananchi kwa barua, kwa simu wala kwa dokezo; ndipo hapo unapokuja umuhimu wa vyombo vya habari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili; ni kwa kuridhia tu kwamba Muswada ambao uliandaliwa na Serikali ya Awamu ya Nne na yeye aliposhika madaraka akaona umuhimu wa kuendeleza mwenzake alipoishia na akauleta Muswada huu ambao umeboreshwa kwa kiwango kikubwa na unaoenda ku-regulate taaluma hii ya waandishi wa habari kwa maslahi ya Taifa hili na kwa maslahi ya waandishi wenyewe, kwa hiyo, leo tuna kila sababu ya kumpongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri waliyoifanya kuleta Muswada huu, lakini niipongeze sana Kamati ya Huduma za Jamii chini ya Mheshimiwa Peter Serukamba ambayo imefanya kazi kubwa sana. Sisi Serikalini tumeshirikiana nao sana kuboresha Muswada huu na nawapongeza sana. Kama tungeufanya utaratibu wa aina hii ukawa utaratibu wetu wa kudumu, tungekuwa tunafanya vizuri zaidi katika sheria tunazozitunga. Kwa hiyo niwashukuru sana Wabunge wote kwa kupata fursa ya kuchangia kwenye Muswada huu na Mwenyezi Mungu apate kuwabariki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kusema tu kwamba mambo yote ambayo Waheshimiwa Wabunge waliyasema na ambayo wameyasema humu ndani Serikali imechukua hatua imeyaboresha kwenye jalada la kwanza la marekebisho ya Serikali na jalada la pili lile ambalo tumeyaleta, yote yamezingatiwa. Muda ni mdogo lakini Waheshimiwa Wabunge wamepata kuyaona haya kweli tumeyazingatia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili ninalotaka kushauri Bunge hili Tukufu; Katiba imetoa mamlaka ya kutunga sheria, ukisoma Ibara ya nne na Ibara ya 64 kwa Bunge, yaani Wabunge ndio mna jukumu la kutunga sheria. Jukumu la kutunga sheria halikuwekwa kwa wadau wala hata waandishi wa habari; kwa hiyo ninyi ndio mnatunga sheria. Kwa hiyo, hata kama wadau hawakuwa tayari kutoa ushauri, lakini nimemsikiliza Mheshimiwa Waziri jana alitoa hata na taarifa mezani za jinsi wadau walivyoshiriki. Kwa hiyo, jukumu letu sisi Wabunge ni kutunga sheria si jukumu la wadau, hivyo ndivyo Katiba inavyosema, wadau tu wanaweza kutusaidia kuboresha. Kwa hiyo, hili nafikiri niliweke wazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, imezungumzwa juu ya haki za waandishi wa habari kwamba zimekiukwa. Tumeshafanya mabadiliko kwenye schedule of amendment kwenye ibara ya saba ile ya Muswada, hizi haki zingine zimezingatiwa na Serikali isingeweza kwa sababu haki hizi zipo kwenye Katiba, Ibara ya 18 na ndiyo msingi huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mengine ambayo ningeenda kutolea ufafanuzi ni suala kwamba masharti yaliyokuwepo kwenye sheria tangu ilivyotungwa wakati wa ukoloni baada ya uhuru, Sheria ya Magazeti ile yameendelezwa hata katika Muswada huu. Kwanza hakuna sharti la kikatiba wala la kisheria linalosema kwamba sheria inapotungwa mpya baada ya kufutwa sheria iliyopita mambo mazuri yaliyokuwepo katika sheria inayofutwa hayataletwa kwenye sheria hii. Ndivyo tunavyotunga na ndiyo maana pia hata tunakuwa na clause ya serving pale; sasa mambo haya kama yalikuwa mazuri lazima yaendelezwe tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niseme tu kwamba, mambo yote yaliyopo kwenye ibara ya saba yale hakuna hata sehemu moja ambayo yamekiuka Katiba ya nchi hii na yamewekwa pale kwa kuzingatia sheria nyingine zozote zile. Sheria hii haikusudii kuwabana Watanzania kuwashughulikia watu wanaokiuka maadili katika utumishi wa umma au awe anafanya ufisadi kwa sababu unaisoma sheria hii pamoja na sheria nyingine; kwa sababu tuna Sheria ya Tanzania Extractive Industry Transparency And Accountability, tulitunga kwenye Bunge la mwaka jana. Kwa hiyo, hatukufichi kitu chochote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetunga sheria ya Whistle Blowers Protection Act haiwezi kuficha watu sijui wanafanya kwenye mikataba, kwa hiyo lawful interest ambazo zimekuwa protected pale wamesema lawful interest, commercial interest including intellectual properties, huu ni utaratibu wa kawaida katika utungaji wa sheria kwa sababu kwenye mikataba hii kuna vitu vinaitwa confidentiality clauses zinazolinda maslahi haya, lakini ni yale ambayo ni lawful. Kuna sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu kile jinsi kilivyo kinachosema kuhakikisha kwamba haiathiri hiyo hakikusudii kumlinda mtu yeyote mhalifu, waandishi watakuwa na haki ya kuripoti tu, lakini wana mipaka yao pia. Kwa hiyo, niliona hili nilisemee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumerejesha baada ya kushauriwa na Wabunge hapa kwa sababu makosa haya ni sensitive. Sheria iliyopo ilikuwa ili umpeleke mahakamani kwa kosa la uchochezi, seditious offence kupata kibali cha Mkurugenzi wa Mashtaka, essentially kibali cha Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa sababu ilikuwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tumeshauriwa hapa na Wabunge tumekirejesha kile kifungu na inaendelea pia hata ambaye mitambo yake imechapisha seditious content naye huwezi kumpeleka mahakamani mpaka upate kibali cha Mkurugenzi wa Mashtaka ili kufanya sasa polisi akikaa pale hamtaki Zitto, anaye-print anaenda anakamatwa. Kwa hiyo, tumeangalia yote hayo Waheshimiwa Wabunge na tumeyazingatia. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nafikiri nichangie hapa ni hili suala la kufungia magazeti. Limezungumzwa hapa kwamba Waziri anabaki na madaraka ya kufungia magazeti. Suala hili lilishasikilizwa na kuamuliwa mbele ya mahakama kwenye kesi ya kikatiba iliyofunguliwa hapa Dodoma na Mchungaji Mtikila dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na malalamiko kwamba vifungu vile jinsi vilivyo kwenye Sheria ya Magazeti vinakiuka Katiba, sijui Jaji alikataa na ilikuwa ni kesi ya kikatiba na alienda hata Mahakama ya Rufaa wakakataa.
Kwa hiyo, mlioona vitabu hivi nendeni msome Tanzania Law Report of 1995 page 31, go and read page 55 and page 56, muda hauturuhusu ningewasomea hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mahakama ilisema hivi vifungu hivi havikiuki Katiba na as per role ni administrative and implementation, ni kwa ajili ya utawala na kusimamia utekelezaji tu. Hata hivyo, katika Muswada huu ambaye haridhiki na maamuzi ya Waziri amepewa fursa ya kwenda mahakamani. Kwa hiyo, hiyo hoja na yenyewe niliona niitolee ufafanuzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ambalo ningetolea ufafanuzi ni issue ya accreditation. Accreditation ilizungumzwa hapa kama ni kuwadhibiti waandishi. Wazungumzaji waliopita wamelifafanua vizuri. Taasisi nyingi zina hizi hivi vitu, sana sana ni kuwasaidia wao wafanye kazi yao tu kwa mujibu wa taaluma. Sasa hii habari ya haki na hapa ndipo tunapo-miss point; katika scheme ya katiba yetu haki zinaenda na wajibu na hakuna haki isiyokuwa na wajibu, someni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yale yote yaliyopo kwenye ibara ya sabae yamekuwa saved yanalindwa na ibara ya 30(2) ya katiba someni yote yaliyopo pale. Hata ibara ya 29(5) na hii ningependa nisome, ibara ndogo ya tano inasema:-
“Ili watu wote waweze kufaidi haki na uhuru vilivyotajwa katika Katiba hii kila mtu ana wajibu wa kutenda na kuendesha shughuli zake kwa namna ambayo hataingilia haki na uhuru wa watu wengine au maslahi ya umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi wananchi mnataka tufungue kwamba hata mwanamke aliyebakwa kesi yake isikilizwe in the open court? Hata mtoto mdogo aliyekuwa defied au kubakwa kesi yake isikilizwe in the open court na haya yamelindwa hata kwenye Katiba na haki za watu ambao wana mashauri yao mahakamani imezungumzwa kwenye ibara ya 30, masuala ya ulinzi na usalama haya (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi kwa mara nyingine tena nikushukuru kwa kunipatia nafasi hii na kuongoza mkutano huu vizuri. Naunga mkono hoja basi na Mwenyezi Mungu atubariki hii ni siku takatifu. Amina.
Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu anayetuwezesha Wabunge kutekeleza majukumu yetu hapa kama ambavyo tunamuomba kila siku wakati wa dua. Baada ya kusema hayo pia niseme moja kwa moja kwamba niwapongeze Waheshimiwa Wabunge ambao kwa kutumia haki zao za Kikatiba wameamua kuchangia uboreshaji wa Mpango huu wa Taifa wa Maendeleo wa miaka mitano ambao ni Mpango halali Kikatiba na kisheria.
Ninaunga mkono moja kwa moja hoja hii ya Mpango huu wa Taifa wa Maendeleo wa miaka mitano.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kutoa ufafanuzi na kushauri baadhi ya maeneo ya Kikatiba na kisheria ambayo yameguswa wakati Waheshimiwa Wabunge wakichangia hapa Bungeni. Moja ni hoja ya kwamba ilipaswa Mpango huu uletwe pamoja na Muswada wa sheria. Naomba kushauri kweli kwamba Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 63(3)(c), inaeleza kwamba Bunge hili litajadili mpango wa muda mrefu au wa muda mfupi na kutunga sheria, lakini pia Ibara hiyo 63(3)(d) inaelekeza juu ya kutunga sheria pale ambapo utekelezaji unahitaji kutungwa kwa sheria. Kwa hiyo Ibara hizi lazima zisomwe zote pamoja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niseme hivi, tayari ipo sheria mahsusi ya kusimamia utekelezaji wa mpango, uwe wa muda mrefu au wa muda mfupi, na hii ni Sheria ya Tume ya Mipango ya mwaka 1989. Ukisoma ile Sheria Kifungu cha 5 kinachoelezea ile kazi ndiyo unaona sasa kazi ya Tume ya kusimamia utekelezaji, vipimo, ile monitoring and evaluation hiyo ni sheria ya jumla inayosimamia utekelezaji wa mpango wowote ule, uwe wa muda mrefu au wa muda mfupi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia Sheria ya Bajeti ya mwaka 2015 tuliyoipitisha Waheshimiwa Wabunge hapa, ukisoma vifungu, kuanzia kifungu cha 7, kifungu cha 8, 9, 11, 13, 15, 19, 21, 20 na 26 na 32 vinaeleza vizuri. Lakini zaidi ya hizi sheria Bunge lenyewe kwa mujibu wa Katiba limepewa mamlaka ya kusimamia utekelezaji wa Mpango wowote ule ni wakati huo linapojadili bajeti kwa kipindi kama hiki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hakukuwa na sababu ya kuja na Muswada wa sheria mahsusi wakati unapoleta mpango hapa, kwa sababu hata Mpango wenyewe haujapitishwa sasa utauleteaje na Muswada wa sheria? zaidi ya hizi Sheria zipo sheria hii ya bajeti imetaja vizuri katika vifungu nilivyovisema.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango huu wa miaka mitanp una nyumbuliwa katika Mpango wa mwaka mmoja mmoja na Mpango wa mwaka mmoja mmoja huu ndiyo unatengenezewa bajeti na ili Mpango huu upitishwe, ili utekelezwe ndiyo unatungiwa sheria ya Finance Act. Lakini pia unatungiwa Sheria ya Appropriation Act na Sheria nyinginezo. Zaidi ya hapo Mpango huu unatekelezwa kwa kusimamiwa na sheria mbalimbali za kisekta.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango wenyewe maana yake ni nini? Mpango ni mkakati wa Kikatiba na kisheria wa kukuza uchumi na mapato ya Serikali kwa ajili ya kuleta Maendeleo ya Wananchi. Kwa sababu hiyo, zipo na sheria mbalimbali nyingine za kisekta ambazo zinasimamia utekelezaji wa Mpango. Kwa hiyo hakukuwa na sababu ya kuleta muswada mahususi kwa ajili hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nizungumze juu ya Zanzibar, Uchaguzi wa Zanzibar ulifanyika kwa amani na kuwepo kwa majeshi Zanzibar, suala la ulinzi na usalama ni la Muungano. Kwa hiyo, Majeshi yaliyopo Zanzibar yalisimamia amani na utengemano Zanzibar, kwa sababu ni suala la Muungano siyo kwamba watu wamepelekwa tu kule na ndiyo maana uchaguzi ukafanyika kwa amani na utengamano. Mkuu wa Mkoa wa Pemba aliyetoa maagizo yale aliyatoa kihalali pia chini ya Sheria ya National Security Council. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Waheshimiwa Wabunge, wamezungumza juu ya kufanyiwa ukaguzi juu ya Deni la Taifa, hii ni mamlaka ya wazi kabisa ya Control And Auditor General iko pale hawezi kuzuiliwa hiyo haikupaswa kuletwa hata kuzungumziwa humu ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nizungumzie kuhusu Mheshimiwa Rais. Ukisoma Ibara ya 35 wamezungumza juu ya Good Governance ya utendaji wa Rais. Ibara ya 35 ya Katiba inasema hivi shughuli zote za utendaji katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zitatekelezwa na watumishi wa Serikali kwa niaba ya Rais. Ibara ya 36 inampa Rais kuteua viongozi hawa wote na kusimamia hata nidhamu yao hata kama kuna mamlaka nyingine imesema nidhamu yao itasimamiwa na mamlaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma Ibara 36(4) haimnyimi Rais kuchukua hatua za kinidhamu kwa watumishi wanaokiuka maadili yao. Kwa hiyo, haya ndiyo ambayo wananchi wanataka. Kama sisi watumishi wa umma wajibu wetu ndiyo tunatekeleza majukumu yetu kwa niaba ya Rais, Rais hayuko tayari kuangushwa na watumishi ambao hawafanyikazi kwa kuzingatia sheria. anachokifanya Rais anamsimamisha hata kukiwa na tuhuma ya hadharani kama ya juzi hakumfukuza moja kwa moja, alisema asimamishwe akachunguzwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa kuchunguzwa mtu anaweza akajitetea hajachukua nafasi ya mtu kwamba labda anaingilia nafasi ya mtu yeyote, vyovyote vile mtu anaweza akaenda Mahakamani. Kwa hiyo, niliona niyaseme hayo kwa sababu ya muda mfupi ulionipatia lakini pia ningechukua nafasi hii…
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, basi naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara nyingine tena nachukua fursa hii ninapopata nafasi hii ya kuchangia, kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye kwa rehema zake anatuwezesha kushiriki kwa ufanisi mkubwa katika vikao hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naendelea kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri ambayo imesheheni taarifa katika nyanja zote, kiuchumi, kisiasa na kijamii kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wa Taifa hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hakika Mheshimiwa Waziri Mkuu unaweza, unaweza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo, pia nawashukuru Waheshimiwa Wabunge ambao wamepata fursa ya kuchangia kuboresha hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ambao wameitumia haki yao ya Kikatiba kwa ufanisi ipasavyo. Niseme kwamba Katiba katika Ibara ya 63 inatoa haki kwa Bunge na mojawapo ya haki ya Bunge na majukumu yake ni kuisimamia Serikali inapokuwa inatekeleza majukumu yake ya Kikatiba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majukumu haya yametajwa, ni pamoja na kuuliza maswali yoyote; swali lolote kuhusu mambo ya umma katika Jamhuri ya Muungano ambayo yako katika wajibu wake, kujadili utekelezaji wa kila Wizara wakati wa Mkutano wa Bunge wa kila mwaka wa Bajeti, kujadili na kuidhinisha mpango wowote wa muda mrefu na wa muda mfupi unaokusudiwa kutekelezwa katika Jamhuri ya Muungano na kutunga Sheria ya Kusimamia Utekelezaji wa Mpango huo. Kutunga sheria pale ambapo utekelezaji unahitaji kutunga sheria na kujadili na kuridhia mikataba yote inayohusu Jamhuri ya Muungano ambayo kwa masharti yake inahitaji kuridhiwa. Haya ni mamlaka ya Bunge ambayo yamewekwa Kikatiba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ambavyo Serikali imeleta bajeti yake katika Bunge hili, Serikali kwa namna yeyote haijapoka mamlaka ya Bunge ya kuisimamia na kuishauri Serikali katika utekelezaji wa majukumu yake ya kikatiba. La sivyo, isingeleta hapa hii bajeti, lakini inajua kabisa kwamba bajeti ni lazima iende iidhinishwe na Bunge. Kwa hiyo, hoja au madai kwamba Serikali imepoka madaraka ya Bunge, siyo sahihi, ni hoja ambayo haipaswi kuzingatiwa na Waheshimiwa Wabunge
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme pia kwamba Bunge hili limepewa uhuru na haki ya kujadili, haki ambayo haiwezi hata kupingwa au kuhojiwa katika Mahakama yoyote. Hivi ndivyo Ibara ya 100 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inavyosema. Haki hii pia imewekwa katika Sheria ya Mamlaka na Kinga na Haki za Wabunge kwenye kifungu cha (3) na kwenye Kanuni, Kanuni ambazo zinatungwa chini ya Ibara ya 89 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, haki hii haipaswi kuzuiliwa na mtu yeyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi, kifungu cha 29 cha Sheria ya Mamlaka, Kinga na Haki za Wabunge, inafanya kosa la jinai mtu yeyote kumzuia Mbunge asichangie, asitekeleze haki yake ya msingi ya kusimamia Serikali. Hilo ni la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ambalo napenda kushauri au kulitolea ufafanuzi ni suala la instrument inayotolewa na Mheshimiwa Rais baada ya kuunda Baraza lake la Mawaziri. Hati hiyo inatungwa chini ya Sheria ya Utekelezaji wa Majukumu ya Mawaziri au kwa Kiingereza inaitwa The Ministers (Discharge of Ministerial Functions Act). Hii ni sheria ambayo inaeleza majukumu ambayo Rais anabaki nayo na hayo mengine anaamua kuwagawia Mawaziri wengine.
Baada ya Mheshimiwa Rais kuunda Baraza lake la Mawaziri, Mawaziri wameendelea kutekeleza wajibu wao, bila hata migongano kwa sababu zile Wizara jinsi zilivyotajwa, kwa mfano Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Kwa hiyo, Waziri anatekeleza hayo hayo. Cha msingi tofauti na ambavyo imezungumzwa; na hili ni jambo ambalo siyo zuri sana kwa Waheshimiwa Wabunge; Kifungu kile cha (5) ambacho kimetajwa, hakimlazimishi Mheshimiwa Rais kutoa hiyo hati, kwa sababu kile kifungu kinatumia neno “may” na tafsiri za sheria kwenye Kifungu cha 43 imeeleza vizuri kwamba neno “may” ni hiari (discretion).
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana kwa mujibu wa sheria hiyo, kama kuna jambo lolote Kifungu cha 5(2) mtu anataka kujua kwamba hivi suala hili liko mamlaka ya Wizara ipi? Kule Mahakamini ataambiwa nenda kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Atakapoenda kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali atakachokisema Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwamba suala hili liko chini ya dhamana ya Wizara fulani, ndiyo mwisho wa hilo suala. (Makofi)
Kwa hiyo, moja, kitu chenyewe siyo cha lazima, hata kama hapa ameandika “shall,” kilichosemwa kwenye sheria ni “may.” Cha pili Mheshimiwa Rais hakupewa timeline, hakupewa masharti ndani ya muda fulani awe ameitangaza; na cha tatu, Serikali tofauti na kilichozungumzwa hapa kwamba Serikali inafanya kazi bila mwongozo, hapana. Serikali inafanya kazi kwanza kwa kuzingatia Katiba na Sheria, kwanza Katiba, Sheria na Sera za Chama ambacho kimeunda hiyo Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa sababu ni hiari, tumwachie Rais. Kwa sababu Sheria yenyewe inasema from time to time; inawezekana sisi tukawa tunazungumza hapa, huko ameshatoa, sisi hata hatujui. Kama ameshatoa, well and good kama hajatoa, tumwachie wakati wowote atakapoona inafaa kutoa atatoa. Afterall, hajavunja sheria yoyote kwa sababu sheria yenyewe hiyo, hiyo instrument anaitoa yeye mwenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, hili suala ambalo amelisema Dkt. Mpango, Waziri wa Fedha kuhusu madai ya kuvunjwa kwa Katiba, amelifafanua vizuri ila naomba kuongeza Waheshimiwa Wabunge kwamba kifungu kilichotajwa cha 41 cha Sheria ya Bajeti, hicho kifungu hakina yale maneno yaliyowekwa pale. Muisome ile sheria, hayapo hayo maneno Waheshimiwa Wabunge, isomeni hiyo sheria. Hayo maneno yaliyosemwa, hayapo na kifungu hiki cha 68 cha sheria hii ndicho kinasema sheria hii ya bajeti yenyewe ina mamlaka ya utawala dhidi ya sheria nyingine zote zinazohusu masuala ya bajeti.
Kwa hiyo, tunatambua kwamba masuala ya matumizi ya fedha pia yanaongozwa na kutawaliwa na Katiba, Sheria ya Public Finance, Appropriation Act na Budget Act na imeweka masharti. Pale ambapo ni lazima kwa masharti yale ya kutekelezwa, Serikali italeta Bungeni, lakini kwa namna ambayo Mheshimiwa Waziri wa Fedha amesema mpaka sasa. Mambo yenyewe haya Waheshimiwa Wabunge, ni ya ndani mno ya kiutendaji. Kwa Mbunge asingeweza akayajua haya. Mkitaka kuyajua haya, mtumieni Controller and Auditor General ambaye anafanya ile kazi, anasema hapa Serikali imefanya hivi. Sisi wenyewe hatuwezi kujifanya tunao watu wa ndani kuyajua yale mambo. Kama mna watu wanawajulisha yale mambo, basi wanawa-mislead. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, naomba kusema suala la uhuru wa vyombo vya habari. Hivi vinazungumzwa juu ya Kifungu cha 18 cha hii Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Naomba nishauri hivi, labda nikisome kifungu hiki: “(a) kila mtu anao uhuru wa kuwa na maoni na kueleza fikra zake; (b) anayo haki ya kutafuta kupokea na kutoa habari bila kujali mipaka ya nchi; (c) anao uhuru wa kufanya mawasiliano na haki ya kutokuingiliwa katika mawasiliano yake; (d) anayo haki ya kupewa taarifa wakati wote kuhusu matukio mbalimbali muhimu kwa maisha na shughuli za wananchi na pia kuhusu masuala muhimu kwa jamii.”
Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge, unapoyasoma haya, niwarejeshe kwenye haki zenu za majukumu yenu kwenye Ibara ya 63 kama nilivyosema. Sasa (d) kwanza ibara hii inachosema ni haki ya kupewa taarifa wakati wowote kuhusu matukio mbalimbali. Haki ya kupewa taarifa, siyo haki ya kutangazwa wakati wote. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana huwezi ukaenda Mahakamani popote ukaanza kusema mimi sijatangazwa. Ndiyo maana pia kuna Waandishi wa Habari na sisi tunasoma magazeti kila siku, hata juzi waliniandika Citizen na Mwananchi. Taarifa hiyo ni mambo ambayo yameshafanyika na ndiyo maana kuna taarifa za habari katika Television na katika Redio na ndiyo vipindi ambavyo vinapendwa sana duniani. Hapa kungekuwa na tatizo, kama Waandishi wa Habari wangekuwa wanazuiliwa hata kuandika chochote kinachoendelea humu ndani, naona Waandishi wa Habari wako pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siku Mheshimiwa Waziri Mkuu alipowasilisha hoja yake, Mwandishi wa Citizen aliniandikia ki-note hapa, akasema Mheshimiwa AG tunaomba maoni yako kuhusiana na maoni ya Kambi ya Upinzani. Nikamwambia kwamba subiri majibu ya Serikali tutakapokuwa tunahitimisha na akaandika hivyo hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hapa hakuna haki ya msingi na niseme tu; moja, itakuwa siyo vyema sana ni matumizi mabaya ya haki zetu sisi Wabunge kuacha kuchangia kutetea Jimbo lako, eti kwa sababu haki iliyoko hapa siyo haki ya mwonekano; haki iliyopo kwenye Bunge ni haki ya kujadiliana na kufanya maamuzi. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maamuzi ya Bunge hayafanywi kwa mwonekano, yanafanywa kwa kujadiliana, kwa kuzungumza au kuandika au kwa kupiga makofi kama unaunga mkono hoja. That is how decision are made. Kwa hiyo, itakuwa siyo jambo jema, nami nimewatetea sana kwenye kesi zinazowakabili kule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na kesi 52 za uchaguzi, tayari kesi 29 tumeshashinda, unatetea Wabunge waje wawakilishe wananchi wao hapa, halafu wana-abdicate majukumu yao, that is not fair. (Makofi)
Wananchi wanachotaka ni what is there kwenye Jimbo; ni kitu gani? Ni aibu sana kwa Waheshimiwa Wabunge. Nawashauri Waheshimiwa Wabunge wote, tutumie vizuri Bunge la Bajeti kwa sababu ndilo Bunge ambalo tunasimama kutetea kipato cha Taifa kwa ajili ya maslahi ya watu wetu kule Majimboni. Ni aibu kuacha kuchangia eti unadai kwamba unataka uonekane kwenye television and that is not very fair.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niseme tu kwa mara nyingine kwamba, naunga mkono hoja hii. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii kwa mara nyingine niweze kuchangia hoja hii muhimu sana ya Waziri wa Katiba na Sheria. Nikushukuru wewe Mheshimiwa Naibu Spika kwa kunipa fursa hii na nichukue fursa hii pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri na niseme moja kwa moja kwamba naiunga mkono hoja hii.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema haya, naomba sasa nijielekeze kutoa ufafanuzi na ushauri kwenye hoja mbalimbali ambazo zimeelezwa na Waheshimiwa Wabunge ndani ya Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nianze na yale ambayo nimeyasikia kutoka kwa Wabunge hapa. Waheshimiwa Wabunge wameleta mapendekezo, kwa mfano Mheshimiwa Kakunda na Mheshimiwa Maige wameleta mapendekezo ya kufanya mabadiliko kwenye Sheria hii ya Manunuzi ya mwaka 2011.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kulifahamisha Bunge lako Tukufu kwamba katika Mkutano huu wa Bunge Serikali italeta Muswada wa Marekebisho ya Sheria hii ya Manunuzi. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge mjiandae wakati utakapofika mchangie kukosoa ubovu wa ile sheria iliyopo sasa hivi ili tuwe na sheria nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nichukue fursa hii kujibu hoja ambayo imezungumzwa na Mheshimiwa Makamba ambapo alikuwa anasisitiza juu ya umuhimu wa wanafunzi wanaosoma Shule ya Sheria kwa Vitendo ya Tanzania kupata mikopo. Niwafahamishe Waheshimiwa Wabunge kwamba katika Bunge hili mlishapitisha sheria, katika Bunge la mwezi wa kumi mpaka wa kumi na moja mwaka 2014 ambayo inawapa haki sasa wanafunzi wanaosoma Shule hii ya Sheria ya Tanzania kupata mikopo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia Mheshimiwa Mtolea amezungumza akishauri kwamba pengine ingekuwa vizuri kwamba wakati wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria basi Kamati ya Sheria Ndogo nayo ingekuwa inatoa taarifa. Naomba kushauri tu kwamba ile Kamati haiwezi kutoa taarifa kwa sababu sio Kamati ya Kisekta. Kwa hiyo, hii Kamati ina muda wake huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho ambalo ningependa kulitolea ufafanuzi katika hoja ambazo nimesikia kwa Waheshimiwa hapa ni kuhusu mapendekezo ambayo yameletwa na Mheshimiwa Holle kuhusu umuhimu wa kufanya mabadiliko kwenye Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia kuchukua fursa hii kulijulisha Bunge lako Tukufu kwamba katika Mkutano huu wa Bunge hili pia Serikali italeta Muswada kwa ajili ya marekebisho ya sheria mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba nichukue fursa hii kuzungumza mambo ya msingi sana ambayo yamejitokeza ndani ya Bunge hili Tukufu.
Kwanza nianze kwa kuwatahadharisha na kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge kwamba Ibara ya 12 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na hasa ile Ibara ndogo ya (2) inasema; ―Kila mtu anastahili heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake.‖
Mheshimiwa Naibu Spika, huu ndiyo msingi ambao pia umewekwa kwenye Kanuni ya 64 ya Kanuni za Kudumu za Bunge. Kanuni ya 64(1)(f) na (g) zinasema, Mbunge; ―(f) hatamsema vibaya au kutoa lugha ya matusi kwa Mbunge au mtu mwingine yeyote na (g) hatatumia lugha ya kuudhi au inayodhalilisha watu wengine.‖
Mheshimiwa Naibu Spika, huu ndiyo msingi ambao unapaswa utawale. Kwa sababu hizi Kanuni ambazo zina msingi wake kwenye Katiba, Ibara ya 12, zikitawala Bunge litaendeshwa kwa amani na Waheshimiwa Wabunge mtajikita tu kwenye hoja, mtawasaidia wananachi wenu ambao wanawasikiliza na ambao wamewatuma ili mje muwatete.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba hizi nimeona mambo haya ya kudhalilishana yakijitokeza na mambo yameanzia kwenye hotuba rasmi ya Kambi ya Upinzani. Naomba kushauri kwamba hatupaswi kufikia hatua hiyo. Nianze na hili la kuwaita Majaji kama majipu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, Katiba hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 30(2)(d) inalinda hadhi na uhuru wa mahakama na heshima yao. Ibara hii inasema hivi, naomba kunukuu yaani; ―ni wajibu wa kila mtu na kila raia kulinda sifa, haki na uhuru wa watu wengine au maisha binafsi ya watu wanaohusika katika mashauru mahakamani; kuzuia kutoa habari za siri; kutunza heshima, mamlaka na uhuru wa mahakama.‖
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona imezungumzwa vibaya hapa, Waheshimiwa Majaji wakiitwa majipu, hiyo ni kuwavunjia heshima yao. Pia ni kuudhalilisha mhimili wa Mahakama ambao tunapaswa tulinde heshima yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu fulani kwenye hotuba hii imezungumzwa kwamba sasa hivi Majaji hawa siyo watakatifu na kweli hakuna mtu ambaye ni mtakatifu lakini wanaishi kwa kuzingatia Katiba na sheria. Wao katika Ibara ya 107 Katiba inasema watakuwa huru wanapotekeleza majukumu yao isipokuwa tu watapaswa kuzingatia masharti ya Katiba hii na sheria za nchi. Kwa hiyo, nilikuwa naomba kushauri kwamba tunapokuwa tunazungumzia ama mtu au mihimili tutumie lugha fasaha ili kulinda hadhi na sifa za mihimili mingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna hii haikuwa sahihi pia kumzungumzia Mheshimiwa Jaji Mkuu kwa namna ambayo imezungumzwa, ni kinyume cha Ibara ya 12 ya Katiba na Kanuni kwa sababu Kanuni yenyewe ya 64(1)(c) inakataza hata unapojadili kutolitumia vibaya jina la Jaji, Rais na kumuongelea mtu ambaye hayupo.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Kwa hiyo, mimi nilikuwa nashauri kwamba mambo haya tuyazingatie sana tunapotekeleza majukumu yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa sababu ya kulinda hadhi na thamani ya utu ambao umewekwa katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania sharti tuheshimu mamlaka ya viongozi wa Serikali walioko.
Sehemu fulani katika hotuba hii imezungumzwa kwamba Rais Shein ni kibaraka. Rais Shein kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar huyu ni Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, utamwitaje Rais wa nchi kwamba ni kibaraka. (Makofi)
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Huku ni kumdhalilisha kitu ambacho kimekatazwa na Kanuni zetu za Bunge, ni kumvunjia hadhi, ni kuidharau mamlaka ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Hili halipaswi kusemwa na Wazanzibari wako hapa halafu wanashangilia that is too much odd to me. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niwakumbushe tu kwamba sisi Wabunge tunapokuja hapa tunakula kiapo. Kwa mujibu wa Ibara 68 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatupasa tule Kiapo cha Uaminifu. Kanuni ya 24 ya Kanuni za Kudumu pale kuna kiapo cha utii na ambacho kinasisitiza kulinda na kuhifadhi Katiba, wote tumeapa hapa. Muungano huu upo kwenye Katiba na ni kwa sababu ya Muungano huu ndiyo maana leo tuko hapa na ndiyo maana tunapata fursa ya kuzungumzia wananchi wetu na kutoa hoja mbalimbali za kuisaidia Serikali. Kwa hiyo, mimi naomba tuheshimu viapo vyetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Zanzibar haiwezi kuwa koloni. Ukisoma Ibara ya 1 ya Katiba ya Zanzibar inasema hiyo ni nchi ambayo kabla ya Muungano ilikuwa ikiitwa Jamhuri ya watu wa Zanzibar. Ibara ya 2 inasema, Zanzibar ni mojawapo ya nchi mbili zinazounda Jamhuri ya Muungano Tanzania. Sasa leo Zanzibar itakuwaje tena koloni? Lazima muelewe haya mambo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, si kweli kwamba Zanzibar imekuwa koloni la Tanzania, Zanzibar ni mamlaka halali. Ibara hii ya 1 na ya 2, ukiacha tu makubaliano ya 1964 (Articles of Union) zimepitishwa baada ya kupigiwa kura ya maoni na Wazanzibari wote wakakubali ule Muungano. Kwa hiyo, si vizuri kutumia fursa hii kuwavuruga wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Ibara ya 28(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inataka kila raia pamoja na mambo mengine alinde, adumishe na kuhifadhi umoja wa Taifa letu. Ibara ya 23(4) ya Katiba ya Zanzibar nayo inawataka Wazanzibar kudumisha umoja wa Wazanzibar. Mimi naona kama tunakuwa salama sana tunapokuwa tunadumisha umoja kuliko kuja kutofautiana hapa kwa sababu ambazo wala hazina sababu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge kwamba Ibara ya 20(2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inakataza vyama vya siasa kupigania kuvunjwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Huwezi kuwa umekula kiapo cha kuitii Katiba ambayo ina masharti ya kutokusajili vyama vinavyopigania kuvunjwa kwa Muungano wa Tanzania halafu ukabaki Bungeni. Mimi nafikiri umefika wakati sasa mamlaka zinazohusika zichukue hatua. (Makofi)
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nizungumzie hili la hati ya mgawanyo wa madaraka ya Rais. Nimesema sana hapa na naomba nirudie tena kwa sababu ni kazi yangu. Baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hawakuwepo na nalazimika kuirudia hii ili niweke record sawa.
Moja, Mawaziri hawa wanateuliwa na Rais kwa mujibu wa Ibara ya 55 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wanakabidhiwa majukumu yao chini ya Sheria ya Utekelezaji wa Majukumu ya Mawaziri, Sura ya 299 halafu kuna hiyo hati inaweza ikatolewa na Rais.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mchengerwa amelifafanua vizuri hili, nilimuona Mheshimiwa Tundu akimpigia makofi na mimi nimeshalisema siku nyingi sana yaani hata kulisema naona kama nachoka. Kwa sababu neno linalozungumzwa pale katika ile kifungu cha 5 linasema, the president „may‟ from time to time na matumizi ya neno ‗may‟ limetafsiriwa vizuri kabisa katika Sheria ya Tasfiri ya Sheria, kifungu cha 53 kinaeleza nini maana ya maneno ‗may‟ na ‗shall‟ yanapotumika katika sheria. Neno ‗may‟ linaashiria hiari na ‗shall‟ inaashiria lazima, kwa hiyo, hili lisingekuwa ni tatizo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika hali ya kawaida hata Waheshimiwa wasomi wanafahamu kwamba sheria ndogo (subsidiary legislation) haiwezi ika-supersede sheria kuu, ile sheria yenyewe ya Utekelezaji wa Majukumu au Katiba. Rais alipokuwa anatangaza zile Wizara alisema kabisa, kwa mfano Wizara inaitwa Wizara ya Maliasili na Utalii…
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Kwa hiyo, unajua kwamba haya ni majukumu yao. Kwa hiyo, kutoitoa ile hati hakuwa amevunja Katiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, nieleze pia kwamba Sheria hii ya Utekelezaji wa Majukumu ya Mawaziri inasema ikiwa kuna jambo lolote labda linachunguzwa Mahakamani au is likely to be inquired in the court, basi hawa watu wataenda kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mwanasheria Mkuu wa Serikali atakachosema ni kwamba suala hili linaangukia dhamana ya mtu fulani au Wizara fulani ndiyo mwisho wa hilo suala, kwa hiyo, sheria yenyewe haimlazimishi Rais. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niwaambieni Kanuni zinatukataza kusema uongo. Jana niliwaambia na wiki iliyopita nilisema mpaka nikawapa waandishi habari, gazeti la Sauti ya Watu Daima liliandika kwamba Rais alishatoa hiyo hati tangu tarehe 22/04/2016…
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Kupitia government notice ambayo ni public notice.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hili halipaswi kutusumbua sana. Ni suala ambalo linaletwa labda kwa namna ya kupotosha tu. Haiwezekani kwamba subsidiary legislation ika supersede sheria kuu na hata Katiba yenyewe.
MBUNGE FULANI: GN namba ngapi?
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Ni GN namba 144…
MBUNGE FULANI: Iko wapi?
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Ya tarehe 22 Aprili, 2016.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa AG naomba uongee na Kiti.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kutakuwepo kwa hiyo, haisaidii kwa sababu Mawaziri na Serikali yote inafanya kazi kwa mujibu wa Katiba, sheria, sera na Ilani ya Uchaguzi ya chama kinachotawala. Mpaka sasa hivi hakuna mtu yeyote aliyekwenda mahakamani au aliyekuja kuniuliza mimi kwamba hivi suala hili linaangukia kwenye dhamana ya nani? Rais hakupewa muda kwamba ndani ya muda fulani awe ametekeleza suala hili. Kwa hiyo, mimi naomba kushauri hili suala labda sasa kama Kiti chako kinaweza kuamua kiamue kwa sababu tumelisemea mno halina tija kwa Watanzania. (Makofi)
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba Mheshimiwa Rais huyu ambaye amezungumzwa hapa kwamba anatawala kiimla Rais huyu hatawali kiimla. Ibara ya 33 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema Rais ni Mkuu wa Nchi, Kiongozi wa Serikali na Amiri Jeshi Mkuu. Kama kiongozi wa Serikali katika mgawanyo wa madaraka, Serikali ina mamlaka ya kusimamia utekelezaji wa sheria, anachokifanya sasa Rais ni kutukumbusha turejee kutekeleza sheria kwa ufanisi. Hata haya mambo yanayofanyika ya uwajibishaji ni katika kuturejesha katika uzingatiaji wa sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Rais mwenyewe ana mamlaka chini ya Ibara ya 36 ya Katiba kuwawajibisha hata wale ambao hakuwateua, lakini pia Mawaziri wana mamlaka ya kuwawajibisha wale ambao wanawateua, Makatibu Wakuu na Bodi zina mamlaka ya kuwawajibisha wale ambao wanawateua. Mtu ambaye anadhani ameonewa Mahakama iko pale aende akatafute haki yake. Watanzania wengi sana ambao walidai wameonewa wameenda mahakamani wamepata haki zao. Kinachofanyika hawafukuzwi, wanachoambiwa ni kwamba wanawekwa pembeni ili wakachunguzwe na wakati wa kuchunguzwa wanapewa fursa ya kujitetea.
MBUNGE FULANI: Naam!
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Kama wana hatia basi wanawajibishwa, kama wengine wana makosa ya jinai wanashtakiwa. Kwa hiyo, hili sasa halipaswi kurudiwarudiwa hapa kila siku kana kwamba ni jambo la msingi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo naomba kulizungumzia ni suala la kudai kwamba Bunge linaongozwa na Ikulu hii si kweli.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma Ibara ya 62 ya Katiba inamtaja Rais kuwa sehemu ya Bunge hili na Ibara ya 63 ndiyo inasema Bunge ndicho chombo kwa niaba ya wananchi kina jukumu la kuisimamia na kuishauri Serikali. Rais huyu huyu ambaye ni sehemu ya Bunge hili ndiye anayelipa hata hizo posho kwa masharti yenu yale. Masharti ya posho zile mpaka ziidhinishwe na Rais.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, haya mambo ya matangazo ni mambo ambayo iliamuliwa na ikapitishwa humu kwamba matangazo sasa yafanywe na studio ya Bunge na Bunge likapitisha hapa Sheria ya Matumizi ya Fedha. Kwa hiyo, siyo sahihi kudai madai hayo. Halafu mnawachonganisha viongozi wa Bunge, Bunge ni mhimili ambao hauwezi kuingiliwa tu na Serikali itauingiliaje?
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, suala hili mimi nashauri Kiti chako kilichukulie hatua.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 3) wa Mwaka 2016
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara nyingine tena nikushukuru kwa kunipatia fursa ili niweze kuichangia hoja hii nikitoa ufafanuzi kwa hoja ambazo zimetolewa na Waheshimiwa wabunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao mizuri. Labda kwa sababu tumekuwa na mambo mengi bado tuna majonzi tangu jana na asubuhi tumekuwa na mambo mengi lakini nilipokuwa nawasilisha hoja asubuhi, hotuba yangu ile ilikuwa very comprehensive na baadhi ya hoja ambazo zimezungumzwa na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hapa zinajibiwa na hotuba ile. Hata hivyo, napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru Waheshimiwa Mawaziri ambao wamepata pia fursa ya kufafanua baadhi ya hoja ambazo zimeulizwa na Waheshimiwa Wabunge.
Mhshimiwa Mwenyekiti, moja ambalo napenda kulisemea hapa, kwa sababu limezungumzwa kwa namna ya kupotoshwa ni hili suala la role ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma ya kuwa na jukumu la kuridhia mapendekezo ya mishahara na marupurupu mengine au posho yanayotoka kwenye taasisi nyingine za Serikali. Limezungumzwa kana kwamba hapa tunarudi nyuma na kwamba tunataka watu waishi maisha ya kishetani, hiyo siyo kweli kabisa. (Makofi)
Mheshimikwa Mwenyekiti, lakini wakati haya yanazungumzwa pia kuna mifano imetolewa hapa namna gani ambavyo baadhi ya wenzetu kwenye taasisi hizi za umma walivyokuwa wanaishi maisha so much lavishly lakini pia kwa namna ambayo ilikuwa na ufujaji mkubwa sana wa matumizi ya fedha za umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mmesikia hoja ikizungumzwa hapa na mzungumzaji mmoja akieleza namna jinsi ambavyo hata mikutano mingine ya Bodi ilikuwa inafanyika nje ya nchi, sasa tunafurahia hili? Wote sera yetu si ni kupambana na ufisadi na kuhakikisha kwamba fedha za umma zinatumika vizuri? Kwa hiyo, mapendekezo haya yanakuja kwa nia nzuri kabisa ili kushughulikia kasoro hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati haya yanazungumzwa, Bunge hili lilishajitungia Sheria ya The National Assembly Administration Act ya mwaka 2009, inatambua na inaweka utaratibu kwamba hata wakati ambapo Bunge lina utaratibu wa kujipangia mishahara yake na ya watumishi wake na marupurupu na kadhalika lakini inapeleka kwa Rais.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia imeweka masharti, msome kifungu cha 20 na 21 ya sheria hii, kwamba pamoja na Tume ile kuwa na mamlaka hayo lakini itazingatia National economy, uchumi wa Taifa unaruhusu, the wage bill na kuangalia sera nyingine katika utumishi wa umma zinazotawala masuala ya maslahi. Sheria ya Mahakama ambayo ilitungwa mwaka 2011 nayo inasema hivyo hivyo kwenye vifungu vya 30 na 31.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni mihimili muhimu sana katika nchi hii, lakini ninyi wenyewe mliona pamoja na kujiwekea mamlaka hayo mkasema muweke utaratibu mapendekezo yetu tunayojiwekea ya mishahara, posho na marupurupu pia yaendane na uwezo ambao Taifa linaweza likauhimili kiuchumi. Sasa kama ninyi Waheshimiwa Wabunge ambao ni mhimili na Waheshimiwa Majaji na Mahakama zao ambao nao ni mhimili waliona hilo ni muhimu sembuse hizi taasisi za umma ambazo ni za Serikali? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili limeletwa kwa nia njema kabisa na siyo kila wakati ambapo Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma inapopata fursa ya ku-regulate au kuidhinisha maslahi haya ni lazima ipunguze. Nimeeleza vizuri, tunataka kuoanisha tu maana baadhi ya watu wamelalamika wanasema kuna tofauti kubwa sana ya kipato kati ya mtu wa chini na wa juu. Kwa hiyo, niliona nilifafanue hili lakini moja, hakuna Katiba ilipokiukwa na pia hakuna sehemu yoyote ambapo sheria imekiukwa, ni kwa nia njema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninyi mlio na sheria maana sheria hizi natembea nazo, The Judiciary Administration Act ninayo hapa, nendeni msome kifungu cha 30 na 31. Mamlaka ya kupendekeza maslahi ya Judiciary yamewekwa kwenye Judicial Service Commission ya Mahakama (Tume ya Utumishi wa Mahakama). Vilevile kwenye National Assembly Administration Act, 2009, kifungu cha 20 na 21, mamlaka haya yamewekwa kwenye Tume ya Utumishi wa Bunge, lakini bado wanazingatia haya. Hizi sheria zinazozungumzwa sasa za mashirika ya umma, regulatory authorities, bodies hazikuwa na masharti hayo kama yalivyo kwenye hizi sheria za Mahakama na ya Bunge. Ndiyo maana Serikali inakuja hapa sasa na Muswada huu ili tuoanishe vitu hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu mwaka 2009, Sheria hii ya Utumishi wa Umma ilifanyiwa mabadiliko kwenye kifungu cha 31. Kifungu kile kilikuwa kinasema kwamba taasisi hizi zitaendeshwa na sheria zilizozianzisha lakini ikawekwa kifungu kidogo cha (2) kinachosema pia Sheria ya Utumishi wa Umma itatumika. Mwaka jana kwenye Sheria Na.17 ya mwaka 2015 kupitia kifungu cha 22, Bunge hili lilifanya mabadiliko pia kwenye kifungu cha 34 kikaongezwa kifungu kipya cha 34(A). Kifungu hiki kilisema hivi:-
“Where there is an inconsistency between the provision of this Act and any other written law governing executive agencies, public institutions or such as public service offices, the provision of this Act shall prevail”. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, that is the essence kwamba tumeondoa yale mapendekezo yaliyokuwa kwenye kifungu cha 26 cha Muswada huu. Msingi wake ni kuwa na vitu vya aina hii, una-harmonize. Si kwamba Katibu Mkuu Utumishi wa Umma yeye anakaa anaanza kupanga, mapendekezo yanatoka kwenye taasisi husika, wanajenga hoja. Kama ni mashirika ya umma labda yamezalisha sana, lazima akubali tu kwamba hawa jamaa wamezalisha au wamebana matumizi lazima tuwape incentives hapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka niseme hili wazi kusudi twende na uelewa wa pamoja, ni kitu ambacho kilinigusa sana. Kwa hiyo, baada ya kulisema hilo nadhani Waheshimiwa Wabunge watakuwa wamelielewa hili. Mengine yamezungumzwa lakini nadhani Wabunge hawakupata nafasi ya kusoma, Serikali imeshaleta majedwali mawili, kwa hiyo, mengine yote haya yameshakuwa taken care of. Naomba Waheshimiwa Wabunge muikubalie hoja hii nzuri ipite tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yameulizwa maswali hapa, maana nikiwa nimekaa hapa Waheshimiwa Wabunge wameendelea kuleta michango, hivi msingi wa mabadiliko kwenye ile sheria inayozungumzia mita 60 kwa ajili ya ulinzi wa mazingira ulikuwa ni nini? Hii imekuwepo hata kwenye Sheria ya Mazingira lakini shida ilikuwa ni kwamba unaanzaje kuzihesabu hizi na nimesema kwenye hotuba yangu, how to calculate this one, where do you begin and where do you end?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuondoa mgogoro huo ndiyo tukasema sasa tunaleta hiyo tafsiri na kuweka clarity. Kwa mfano, wewe una shughuli zako kwenye eneo la mita 60 au umejenga mle, mimi naweza kusema aah, aah mimi niko nje. Sasa kunapokuwa na migogoro kama hii labda anashtakiwa, ndiyo tunataka kuondoa huo utata. Huo ndiyo msingi wa mabadiliko yale, kwa hiyo, naona muunge mkono hoja hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo naomba kulisemea hapa limezungumzwa na Mheshimiwa Bashe kuhusu ile Bodi ya Mfuko wa Mazingira. Tulikuwa na proposal kutoka Serikalini tuongeze watu watatu ili wafike kumi na moja na watu hawa ilidaiwa kwamba walitakiwa wawe na ujuzi na utaalam kwenye mambo ya uendeshaji wa Mifuko. Nadhani ilikuwa ni oversight, Serikali yenyewe tumeshajiwekea mwongozo kwamba katika hizi hatua za kubana matumizi yasiyokuwa ya lazima kwa kuwa na Bodi nyingi, nyingine ndiyo mnasema zinafanyia mikutano Dubai na kadhalika, basi tu-streamline ili Bodi moja wawe aidha wajumbe saba wasizidi tisa. Ndiyo maana Waheshimiwa Wabunge mnaona kwenye ile Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu walikuwa wajumbe 15 tumewapunguza, lakini pia kwenye Muswada huu tumeweka fursa ya kualika mtu mwingine ili ku-co-opt watu wengine wanaotaka kuwasikiliza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tungeenda hivi Serikali ingekuwa inajikanyaga yenyewe. Hapa unaleta watu wengine eti kwa sababu wana utaalam wa uendeshaji wa Mifuko unaongeza gharama kule halafu Bodi ya muhimu sana kama hii ya Mikopo ya Elimu ya Juu unawapunguza wale watu. Kwa hiyo, ndiyo maana tukaondoa pale ili warudi tisa lakini tumefanya mabadiliko kwenye Schedule of Amendment Waheshimiwa Wabunge ambapo sasa huu Mfuko unapata fursa ya kumwalika mtu mwingine yeyote siyo kutoka kwenye mifuko ya uendeshaji bali mtu yeyote kwa maana kama anaweza kuja kuwasaidia namna ya ku-combat na kuimarisha vita dhidi ya uharibifu wa mazingira awasaidie siyo utaalam wa kuendesha Mifuko tu. Kwa hiyo, naomba hili Waheshimiwa Wabunge mlikubali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huu pia ndiyo ulikuwa ushauri wa Kamati. Ndiyo msingi wake lakini mtu yeyote kama ana utaalam, anaweza akatusaidia ku-mobilize availability ya funds kwa ajili ya running of the activity of this fund, anakaribishwa. Kwa kweli siamini kabisa kwamba kwa kuweka wale watu mle ndani ndiyo fedha zinaweza kupatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeshauri sana on this one with a serious note, hali ya uharibifu wa mazingira ni mbaya sana, if this does not going to be checked accordingly then we are in a mess. Kwenye suala hili Serikali na Wabunge lazima tuungane tuwe kitu kimoja tupambane na vita kali ya uharibifu wa mazingira, mimi hii naiona ni vita kubwa second to ufisadi. Unajua hiyo ndiyo survival ya nchi yenyewe. Kwa hiyo, hilo nilifikiri nilifafanue namna hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeulizwa swali hapa wakati Waheshimiwa Wabunge wakichangia wakitaka nieleze msingi wa Mkurugenzi wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga ikiwa amekamata ndege. Msingi wake nimesema ni pale ambapo hiyo ndege inakuwa kwa namna yoyote wamefanya makosa ya sheria hiyo, lakini makosa ambayo ni kinyume na utaratibu wa Mkataba wa Chicago wa Usafiri wa Anga (Chicago Convention on International Civil Aviation).
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu huu siyo mpya, upo kwenye sheria hii ambayo leo tunaibadilisha. Kwa hiyo, huo ndiyo msingi wake tu, tunataka sasa kukidhi zaidi masharti ya mkataba ule na ni kwa nia njema kwa ajili ya usalama wenyewe, ndiyo msingi wake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mtu ambaye labda hakuridhika na uamuzi ule anafanyaje? Ukienda Sehemu ya XI ya Civil Aviation Act unaona kuna utaratibu pale wa review and appeals procedures, haya ni mambo technical, hayawezi kwenda moja kwa moja kwa Waziri. Kwa hiyo, wameweka utaratibu pale kuna Internal Review Committee na mambo mengine kwa sababu ndege zenyewe nazo hazipaswi kukaa sana. Kwa hiyo, utaratibu ule upo kwa mtu ambaye amekuwa aggrieved na maamuzi yaliyotolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ilitushauri kwamba tuweke utaratibu huo kwenye Kanuni na Mheshimiwa Waziri anasema anaboresha zile Kanuni zake vizuri kufuatia kuingizwa kwa mabadiliko haya katika sheria. Kwa hiyo, Kanuni ita-take care hakuna mtu atakayeweza kudhulumiwa. At any given point in time kama mtu hakuridhika na uamuzi wa review panel au wa Waziri au wa Mkurugenzi anaweza akaenda Mahakamani. Hilo nalo pia niliona nilifafanue ili liweze kutusaidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo niseme mambo kadhaa. Kuna hoja hapa imejengwa kwamba siyo vizuri kuleta Muswada wa Sheria Mbalimbali. Ukweli ni kwamba Bunge linaruhusu Miswada yote ya aina mbili, Muswada wa Mabadiliko ya Sheria Mbalimbali na Muswada unaojitegemea wenyewe. Kanuni wala Katiba haikatai na ni utaratibu mzuri tu na tumesema kwa nini. Kwa mfano, hapa tunabadilisha sheria tisa yaani hapa sasa leo tungekuwa na Miswada tisa inayojitegemea inawasilishwa na Mawaziri na wakati sheria nyingine labda unabadilisha kifungu kimoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii hoja kwamba haya ni mambo ya kisera, mambo ya kisera siyo ya Bunge ni ya Serikali. Kama Muswada unakuja hapa Serikali tayari huko imeshafanya maamuzi ya kisera. Wajibu wa Bunge sasa ni kutunga sheria ama unaikubali au unaikataa tu.
Kwa hiyo, kuletwa kwa Muswada huu eti kwa sababu ni wa kisera na hakuna sheria au kanuni inayosema kwamba kwenye mambo ya kisera na Miswada yote anyway ni ya kisera tu. Kwa sababu Miswada ya sheria si inatokana na sera? Unaanza na sera ndiyo unakuja kuitungia sheria. Hakuna panaposema kwamba ikiwa ni suala la kisera you bring a stand-alone kind of a Bill. Niliona hilo na lenyewe nilifafanue ili lieleweke vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala mengine ya uwakilishi kwenye Bodi na kadhalika tumeyazingatia kama unavyoona kwenye Schedule of Amendment. Nataka kulizungumza moja ambalo Mheshimiwa Kairuki amelizungumzia. Imesemwa hapa kwamba hatua hii ya Rais kuteua Wakurugenzi na watendaji wengine ni kuvunja Katiba, hapana. Mimi ni mtaalam wa Katiba na mimi siyo mtaalam pekee ninayejua Katiba, kuna wanasheria wengi tu waliopo hapa na wasiokuwepo hapa. Ukweli ni kwamba kwa hatua hiyo hakuna sehemu yoyote ambayo Rais anavunja Katiba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza amepewa mamlaka chini ya Ibara ya 36, lakini pia Sheria ya Utumishi wa Umma imesema kuwa hawa Wakurugenzi watateuliwa na Waziri mwenye dhamana ya Local Authorities.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa The Ministers (Discharge of Ministerial Functions) Act, Rais na yeye mwenyewe ni Wizara anaweza akapanga akajiachia madaraka yake. Hata hivyo, kwa mujibu wa mwongozo ule mliokuwa mnaudai wakati ule, haya ni mojawapo ya mambo ambayo ameyaacha Wizarani kwake, yeye ndiye mwenye dhamana. Kwa hiyo, hakuna ambapo sheria imevunjwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, kwa mara nyingine tena nikushukuru na naomba kutoa hoja.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.4) wa Mwaka 2016
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara nyingine tena ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa na kuniwezesha na mimi kuhitimisha hoja hii na kujibu baadhi ya hoja mbalimbali ambazo zimechangiwa katika Bunge lake Tukufu na Wabunge.
Kwanza niwatambue Wabunge ambao wamepata fursa ya kuchangia muswada huu nawapongeza sana. Kwanza nitambue mchango wa Kamati ya Kudumu ya Katiba na Sheria ambayo ilichambua muswada huu na kuujadili na ikatoa taarifa yake kwa mujibu wa ukurasa wa 23 wa taarifa ya Kamati hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maoni yaliyotolewa na Kamati katika muswada huu yamezingatia kwa kina maoni ya wadau, uchambuzi wa kitaalam uliofanywa na Sekretariati ya Bunge na majadiliano mapana kati ya Serikali na Kamati. Hivyo, Kamati inaamini kwamba sheria hii itakuwa bora na yenye manufaa kwa Watanzania wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na Kamati nitambue pia mchango wa taarifa ya Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani na ambaye yeye pia amekiri kwamba anakubaliana na taarifa ya Kamati na niwatambue pia Mheshimiwa Juma Kombo Hamad, Mheshimiwa Japhet Hasunga, Mheshimiwa Innocent Bashungwa, Tundu Lissu, Andrew Chenge, Hawa Ghasia, Ali Hassan Omar King na hatimaye Waziri wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wapo Wabunge ambao wamechangia hoja hii kwa maandishi nao naomba niwatambue. Mheshimiwa Lucia Mlowe, Mheshimiwa Mary Deo Muro na Mheshimiwa Juma Othman Hija. Kwa hiyo, hawa wote pamoja na Wabunge wote naomba kuwapongeza kwa kuweza kuchangia katika muswada huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo sasa niende moja kwa moja kujibu hoja ambazo zimeletwa mbele ya Bunge lako Tukufu na Waheshimiwa wakati wakichangia hoja hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kumekuwa na dhana potofu ambayo imekuwa ikijirudia katika Bunge hili Tukufu kwamba pengine hii Miswada ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali siyo miswada mizuri. Ukweli ni kwamba miswada hii inafaa na miswada ni halali inayotambulika na mpaka sasa hakuna katazo lolote la Kikatiba au la kisheria au la kikanuni linalopiga marufuku uwasilishaji wa Miswada ya mabadiliko ya sheria mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili niseme kwamba Miswada hii ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali ni muhimu kwa sababu siyo wakati wote inalazimika sasa Waziri alete muswada hapa unaojitegemea kwa sababu mabadiliko yenyewe hata katika sheria yanaweza yakawa ni madogo madogo; lakini mengine pia tunayoyaleta Serikali ndani ya Bunge lako Tukufu yanatokana na michango na ushauri na mapendekezo ya Wabunge, badala ya kusubiri utaratibu mrefu wa kuandaa miswada inayojitegemea basi huwa tunaona kwamba tulete kwa utaratibu huu wa Miswada ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia imezungumzwa juu ya tafsiri katika sheria hii. Tunavyojua ni utaratibu wa kawaida kwamba katika sheria yoyote inayotungwa kwa kawaida huwa ina kifungu au ibara ya tafsiri ni jambo jema na hili linaletwa ili kurahisisha matumizi mazuri ya sheria hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba sisi tunayo sheria, Sheria ya Tafsiri ya Sheria, ndiyo Sura ya Kwanza ya Sheria za Tanzania, ni kuonesha umuhimu wa kutafsiri maneno ambayo yanatumika na hasa maneno mahsusi yanayotumika katika sheria mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo maneno ambayo yameletwa kama kutafsiri kwenye sheria hii ambayo tunaifanyia mabadiliko Sehemu ya Pili ya Muswada ya Government Loans Guarantees and Grants Act ni muhimu sana yakawepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa wameshajibu baadhi ya hoja na mimi nawapongeza. Kulikuwa na hoja kwamba Zanzibar sasa inawekwa kwenye wigo sawa na Local Government Authorities na mashirika mengine ya umma. Waheshimiwa Wabunge kama mnavyoona katika Jedwali la Marekebisho kifungu kile kimeandikwa upya sasa Zanzibar inasimama peke yake na masharti yake na tumeondoa katika sehemu vifungu vile vilivyokuwa vinatajwa pamoja na hizi taasisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jedwali letu la Marekebisho limeeleza vizuri na Mheshimiwa Chenge amefafanua vizuri juu ya hoja hii inayosema kwamba Zanzibar sasa itakuwa pamoja sawa hadhi na hayo mashirika, hapana. Kwenye Jedwali la Marekebisho tumeiandika upya ile Ibara ya 12 ambapo wala hata siyo lazima, tumetumia neno “may” isipokuwa Zanzibar pale ambapo tu huyo mkopeshaji anataka tuwe na utaratibu wa aina hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar kuwa na mamlaka ya kukopa hili nalo nimeshalitolea ufafanuzi humu, bado suala la mikopo ya nje ni la Kikatiba, muda utakapofika basi Zanzibar itakuwa na mamlaka yake ya kukopa ikiwa imejitegemea yenyewe. Mheshimiwa Chenge ametoa ufafanuzi mzuri kuhusu suala hili, Mheshimiwa Ali Hassan Omar King ametoa ufafanuzi kuhusu suala hili. Kwa hiyo, Waheshimiwa naomba muunge mkono hoja hii ya Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, isipokuwa Mheshimiwa Juma Othman Hija akiunga mkono hoja hii, yeye ameshauri kwamba kutokana na uchumi wa Zanzibar kutokua imara sana basi wakati Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wanapokuwa na utaratibu huu waaangalie uwezekano wa kuiwekea Zanzibar masharti yenye wepesi na hiyo ni hoja nzuri, itategemea labda masharti pia kutoka kwa huyo anaetukopesha anasema nini. Lakini ni mchango mzuri na sisi Serikali tunaupokea ushauri huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Bashungwa kwa mchango wake mzuri, kiujumla tunakubaliana na ushauri wake na tunakubaliana na mchango wake, isipokuwa tu tuseme kwamba kwenye hili suala la elimu kwa ajili ya mikopo ya juu, kupanua wigo; lengo la muswada huu katika sehemu ya tatu inaporekebisha hiyo Sheria ya Mikopo ya Elimu ya Juu ni kuongeza huo wigo kwa sababu sheria jinsi ilivyo sasa hivi imefunga kwenye hayo maeneo yanayotajwa kwenye hicho kifungu, lakini kwa kumpa Waziri sasa mamlaka kwa kuangalia vipaumbele vya Taifa; wigo kwa watu wanaostahili kupata mikopo utaongezeka, ni ushauri mzuri kwa Serikali na sisi tunaupokea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, isipokuwa hili la kwamba taasisi za kidini kupata msamaha wa kodi pengine hili naomba kushauri kwamba hili ameliwahisha sana labda tutalifikiria wakati wa Muswada wa Sheria ya Fedha, linapaswa ombi kama hilo lije labda wakati wa Muswada wa Finance Act wakati wa kutunga Sheria ile ya Bajeti, lakini haliwezi likaingizwa kwenye muswada huu wa sasa na hiyo pia itakuwa kama Wizara yenye dhamana na kusimamia hii sheria itakubaliana na hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango mwingine ulitoka kwa Mheshimiwa Tundu Lissu ambaye alitumia muda wake mrefu kuzungumza juu ya Sheria hii ya Mikopo ya Serikali, Dhamana na Misaada. Lakini pia ndani ya Bunge hili tumepata ufafanuzi kutoka kwa Mheshimiwa Chenge, Mheshimiwa Ali King na Wabunge wengine waliochangia kwamba, moja, Zanzibar haifanywi sasa kuwa mdeni wa kudumu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa sababu kwanza tulishakubaliana tangu mwanzo kwamba suala la mikopo ya nje ni suala la Muungano, hiyo ni sababu ya kwanza kwamba inaifanya Zanzibar isiwe mdeni wa kudumu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, siyo wakati wote Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itakuwa inakopa na utaratibu huo uliowekwa kama ambao tumekwisha ufafanua ni pale ambapo hata hao wanaotukopesha watakapokuwa wameweka kwamba hili nalo ni sharti la mikopo na Zanzibar kwa maana ya kifungu kilichoandikwa pale inao utashi wa kukataa au kukubali. Lakini Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hizi ni Serikali ndugu. Kama kuna jambo lolote la maslahi ya Zanzibar hizi pande mbili huwa zinakaa na kuelewana. Mheshimiwa Chenge amelifafanua vizuri sana hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hii ya kusema kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ikishindwa kulipa itakuwaje, hata jinsi muswada ulivyoandikwa pale hakuna sehemu yoyote ambayo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema ikishindwa kulipa inawajibika, uwajibikaji umewekwa kwenye taasisi za Serikali. Kwa hiyo, Wabunge naomba tuelewane kwenye hili, hakuna sehemu katika muswada huu pale ambapo inatolewa adhabu, ambapo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeshirikishwa. Zilizoshirikishwa hapa ambazo zimehusishwa ni taasisi za umma ambazo kwa mujibu wa sheria hii ni Mashirika ya Umma na Local Government Authorities.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba kuwatoa wasiwasi Waheshimiwa Wabunge kwamba sasa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaenda kuwajibishwa, utaiwajibishaje? Hawa ni ndugu na nchi moja, hakuna namna ya kuiwajibisha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa na mchango hapa kuhusu Joint Finance Commission. Katika muswada huu hakuna hata sehemu yoyote tunayozungumzia hili suala. Kwa hiyo, ni mchango ambao pia umeletwa pengine mapema zaidi haukuwa sehemu yake na wala hapa pia hatuzungumzii General Basket Fund, haiingii kwenye sehemu yoyote ya muswada.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hii hoja Mheshimiwa Tundu Lissu pia kulikuwa na mchango kuhusu hoja ya Sheria ya Hifadhi ya Wanyamapori ambapo ilidaiwa kwamba sasa ushahidi ukishakuwa tendered tu pale mahakamani, mtuhumiwa anapatikana na hatia na kufungwa, hiyo siyo kweli. Lakini msingi wa sheria yenyewe hii nini? Ni kwamba kuna vitu vinaharibika haraka kwa mfano nyara za Serikali, sasa hizi nyara za Serikali zinazoharibika haraka, mpaka usikilize kesi ianze kuisha yule mnyama atakuwa ameshaharibika na hajulikani, kesi itamalizika lini?
Kwa hiyo, tumeweka utaratibu hata pale ambapo kesi haijaanza badala ya hayo mambo kufanywa na Mkurugenzi wa Wanyamapori kama ilivyokuwa na Mahakama ya Rufaa ikakataa, iende Mahakamani sisi tutoe pale huyo mnyama kama ni mnyama hiki kitu ambacho kinaweza kikaharibika haraka, Mahakama iamue ikione itoe maamuzi kwamba hiki sasa jinsi kilivyo kikikaa hivi kitaharibika, kiharibiwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, itatumika kama ushahidi wa kuwepo kitu hicho siyo ushahidi wa kwamba huyo anayekwenda kushtakiwa kama atashtakiwa itakuwa ni ushahidi wa kuthibitisha dhidi yake kwamba ametenda lile kosa. Kwa sababu kama ni masuala ya wanyamapori, kwanza kosa hapa ni suala la kukutwa na umiliki, kukutwa na vile vitu isivyo halali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, huo ni ushahidi ambao utakuja kutolewa Mahakamani baadae kwamba je, huyu mnyama alieletwa hapa Mahakamani wewe Bwana ndiyo ulikutwa naye huyu? Kwa hiyo, ni kitu kingine tofauti na huo ushahidi kama atashtakiwa utakuja kutolewa huko baadae.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waheshimiwa Wabunge wayakubali mapendekezo ya muswada huu kama yalivyowekwa. Kusema ukweli kwenye Kamati namshukuru Mheshimiwa Tundu Lissu walitusaidia sana walipokuwa anahoji jinsi muswada huu ulivyokuwa umeandikwa na mimi nikawaahidi kwamba naenda kuuboresha, nimeuboresha muswada huu vizuri kabisa na Kamati imeridhika na Mheshimiwa Tundu Lissu naye amekubaliana na Taarifa ya Kamati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jinsi ilivyo sasa hivi na sisi tunaleta uwazi, Mheshimiwa Tundu Lissu angeweza kuona ile sheria ya Kenya angeogopa, maana hata wakati natafuta kuboresha muswada huu nilipata hiyo sheria ya Kenya wenzetu wanafanyaje, ila Waheshimiwa Wabunge siyo vema kusema kusema sheria za nchi nyingine lakini ile isingetusaidia. Sisi tunataka transparency and accountability.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukasema hapana, hii scheme ya Kenya tuiache tutumie hii ya leo ya sasa na ndiyo maana tunaenda hata mahakamani, ni lazima Waheshimiwa Wabunge tuiheshimu mahakama. Sasa Mahakama nae ataenda kumbambikiza huyo mtu? Kwa sababu kwanza pale mbele wakati huo hakuna hata ushahidi, lakini pia utaratibu huu kwenye kifungu cha 2(d) ndiyo utaratibu ambao upo kwenye Sheria yetu ya Mashauri ya Mwenendo wa Jinai, kwenye kifungu cha 353 kinaweka utaratibu wa aina hiyo.
Waheshimiwa Wabunge, naomba kukubaliana na hoja ya Serikali kwamba haya nayo jinsi yalivyoletwa Muswada huu na kama unavyoonekana kwenye Jedwali pale tukubaliane. Pia Serikali imewasilisha Jedwali la ziada kwenye hiki kipengele maana kilikuwa kiko wazi tu hivi; sasa tumesema hapana, mahakama iseme atakayekwenda kuharibu hiyo basi awe ni Mkurugenzi wa Wanyamapori na siyo mtu mwingine yeyote yule na ndiyo utaratibu na scheme ya sheria hiyo. Waheshimiwa Wabunge naomba mkubaliane na hoja hii ya Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Hawa Ghasia kwa ujumla ameunga mkono hoja hii na ametoa ushauri na haya mambo mengine ni ya msingi sana tutayazingatia ndani ya Serikali. Pia Mheshimiwa Ali Hassan Omar King ameunga mkono hoja hii na akafafanua vizuri sana ninamshukuru.
Mheshimiwa Chenge pamoja na kuunga mkono ametushauri vizuri matumizi ya maneno “secured” popote pale yanapoonekana kwenye Muswada huu yaondolewe “secured or contracted” na badala yake yaingizwe maneno “raised” na sisi tunakubaliana na ushauri huu wa mchango wa Mheshimiwa Andrew Chenge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nifafanue kwamba Mheshimiwa Chenge hakuwa na uhakika tulipokuwa tunasema kwamba tunafuta yale maneno stock, ukweli ni kwamba kwenye Muswada ulivyoandikwa mara ya kwanza tulikuwa tunaondoa lakini tulipoenda kwenye Kamati tukashauriwa, hivyo kwenye Jedwali la Marekebisho hayo maneno stock yaani tunayafuta hayapo tena, yaani hatuyaondoi kwenye sheria, yanabaki yalivyo. Inaonekana vizuri zaidi kwenye hili Jedwali la Marekebisho, tunaondoa kwenye ule Muswada ndiyo maana ya kwamba tunayafuta pale, kwa hiyo Mheshimiwa Chenge kwenye hili tupo pamoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mary Muro, Mbunge wa Viti Maalum, ameishauri Serikali kutafuta fedha za kutosha kwa ajili ya kukopesha wanafunzi wote. Serikali inaupokea ushauri huu ni ushauri mzuri, kama mnavyoona wakati fulani Serikali inakuwa na mambo mengi, lakini pale ambapo uwezo unaruhusu haya ni mambo mazuri ya kutekelezeka. Nia ya Serikali ni kwamba watu wake wote wapate elimu, kwa hiyo, ushauri huu wa Mheshimiwa Mary Deo Muro, tunaukubali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunakubali ushauri wake kuhusiana na marekebisho ya Sheria ya Sukari, ameshauri kwamba wakulima wadogo wadogo wa miwa washirikishwe kikamilifu katika kuandaa sheria zinazowahusu. Hili ni jambo jema na tumeambiwa na Kamati asubuhi umuhimu wa kuwashirikisha wadau wote wakati tunapotunga sheria, ushauri huu nao ni mzuri Mheshimiwa Muro tunaukubali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lucia Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, amependekeza kifungu cha 7A kinachoweka masharti ya wakulima kupata kibali cha bodi kabla ya kujiunga katika Vyama vya Ushirika kirekebishwe ili kuondoa masharti hayo, na sisi tumekubali, hili limezingatiwa kwenye Jedwali la Marekebisho. Alishauri pia kuhusu Ibara ya 41 ambayo inapendekezwa kifungu cha 11A kinachoweka masharti ya kushauriana kabla ya kupanga bei elekezi kifanyiwe marekebisho ili kuwahusisha wadau wote. Huu ni ushauri mzuri tumeuzingatia uko kama unavyoonekana kwenye Jedwali la Marekebisho. Pia alishauri Ibara ya 42 inayopendekeza kifungu cha 17A kirekebishwe ili kuweka hatua mbalimbali za ukataji wa rufaa kutoka kwa Bodi kwenda kwa Waziri na kutoka kwa Waziri kwenda kwa Mahakama Kuu. Ushauri huu pia tumeuzingatia kama unavyoonekana kwenye Jedwali la Marekebisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepata ushauri pia kupitia hayo Majedwali ya Marekebisho na haya yanamhusisha Mheshimiwa Dkt. Immaculate Sware Semesi, Mbunge wa Viti Maalum, amependekeza Ibara ya 40, kifungu cha 7A kirekebishwe kwa kuondoa neno may na kuweka neno shall ili Bodi ilazimike kuongeza muda wa kusajili wakulima wa miwa. Marekebisho haya ni mazuri lakini kuna shida moja. Moja, tukikubali hili pendekezo maana yake ni kwamba itakuwa ni lazima tu Bodi iwe inaongeza hata pale ambapo hakuna sababu, ndiyo msingi wa kutumia neno may. Kwa hiyo, mamlaka ya Bodi ya kuongeza muda wa usajili yatategemea mazingira yaliyopo, hivyo ni sahihi kuacha neno may kama ilivyo kwenye kifungu hicho cha 7A(3) ili huu muda uongezwe pale ambapo mazingira yataruhusu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Dkt. Sware pia alikuwa na mapendekezo kwenye Ibara ya 42 ambapo inapendekezwa kifungu cha 17A(1) kifanyiwe marekebisho kuongeza muda wa miezi isiyozidi 12 kwa ajili ya kuwasilisha mpango wa maendeleo. Mapendekezo haya japokuwa yalikuwa na nia njema, kwa kuwa tayari kifungu cha 17A kinaipa Bodi mamlaka ya kupanga muda wa kuwasilisha mpango wa maendeleo kwa kadri Bodi itakavyoona inafaa, hivyo basi, Bodi inaweza kupanga miezi hiyo inayopendekezwa au vinginevyo kutegemea na hali itakavyokuwa kwa sababu hili ni suala linalohusisha wadau wengi na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaona kwamba Bodi imepewa mamlaka pia ya kuwa inasimamia utekelezaji wa mpango huu, pendekezo hili japokuwa lilikuwa zuri, lakini sheria jinsi ilivyoandikwa sasa hivi inakidhi matokeo ambayo Mheshimiwa anayapendekeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Dkt. Sware pia amependekeza kwamba Ibara ya 17A inapendekeza aya ya (b), (c) na (d) zifutwe. Mapendekezo hayo tunasita kuyakubali kwa kuwa aya hizo zinaainisha mambo muhimu ambayo yanatakiwa kuzingatiwa katika mpango wa maendeleo ili kuweka muundo wa andiko la mpango huo kufaa. Pia Mheshimiwa Dkt. Sware alikuwa na mapendekezo kuhusu Ibara ya 45, inapendekezwa kifungu cha 45(1)kifanyiwe marekebisho kuondoa neno Director na badala yake kuweka Kituo cha Polisi (Police Station). Tunakubali kwamba haya ni mapendekezo muhimu lakini kwa sababu mtekelezaji wa sheria hii ni Mkurugenzi wa Wanyamapori, badala ya kuweka Polisi tumuweke Mkurugenzi wa Wanyamapori na ndicho ambacho tumefanya Serikali kupitia hili jedwali la marekebisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Halima Mdee naye alipata fursa ya kuchangia kwa kuboresha alipoleta Jedwali la Marekebisho ambapo yeye alipendekeza kwamba Ibara ya 19(3) kifanyiwe marekebisho kinachoweka masharti ya mtu mwingine kuhudhuria kikao cha Kamati ya Taifa kwa niaba ya Mjumbe aondolewe ili Mjumbe mhusika ahudhurie mwenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo haya yalikuwa muhimu kwa kutaka kuwawajibisha watu wa-take this matter seriously, lakini ukiweka utaratibu huo itafikia hatua tutakwama kwenda na utaratibu wa uwakilishi ni utaratibu wa kawaida isipokuwa tumeweka masharti kwamba huyo anayeenda kumwakilisha huyu Mjumbe wa Kamati tumeweka zile sababu za msingi pale, basi awe ni Afisa Mwandamizi, kwa mfano kama Attorney General hivi ni Mjumbe wa ile Kamati, kama hayupo basi aende Deputy Attorney General ndiyo msingi.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Mdee tunashauri ukubali tu ushauri wa Serikali Muswada jinsi ulivyo sasa hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, alikuwa na mapendekezo pia kuhusu Ibara za 35 na 36, kwamba marekebisho yafanyike katika vifungu hivi ili kuondoa tozo inayopendekezwa. Kama utakavyoona mapendekezo haya hayahitajiki tena kwa sababu Serikali tayari imeshaondoa sehemu hii katika muswada ule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 41 pia alipendekeza kwamba kifungu cha 11A kiongezwe masharti ya kuitaka Bodi izingatie mazingira ya uzalishaji kabla ya kupanga bei ya sukari. Nia yake ilikuwa njema lakini mapendekezo haya yanaweza kuleta athari kama yatakubalika kwa sababu masharti yanaweza kuzingatia wakati wa mashauriano baada ya Waziri, Bodi na wadau kama ilivyo katika Jedwali la Marekebisho. Pia jambo la pili hapo, hatuangalii tu masharti ya production, kuna vitu vingi vinatazamwa pale, siyo uzalishaji tu kwa hiyo tuiache sheria jinsi ilivyo ibaki hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 42 alikuwa na mapendekezo kwamba kifungu cha 17A kirekebishwe ili kuweka hatua mbalimbali za ukataji wa rufaa kutoka kwa Bodi kwenda kwa Waziri na kutoka kwa Waziri kwenda kwa Mahakama Kuu. Pendekezo hili limeridhiwa na Serikali kama inavyoonekana katika Jedwali hili la Marekebisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo kwa mara nyingine tena nikushukuru wewe mwenyewe binafsi kwa kusimamia Mkutano huu vizuri na kwa hekima na ninawashukuru tena Waheshimiwa Wabunge wote waliopata fursa ya kuchangia na Mwenyezi Mungu aendelee kuwajalia amani na kuwabariki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kutoa hoja.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Na. 3 wa Mwaka 2017
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa fursa ya kuweza kuchangia. Nichukue nafasi hii pia kuwashukuru na kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge ambao wametenga muda wao na kuchangia. Kwa ujumla Wabunge waliochangia ni Wabunge Nane na Waheshimiwa Mawaziri wawili.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Mwita Mwikabe Waitara Mbunge wa Ukonga; Mheshimiwa Zuberi Kuchauka, Mbunge wa Liwale; Mheshimwa Hamidu Bobali; Mbunge wa Mchinga; Mheshimiwa Joseph G. Kakunda, Mbunge wa Sikonge; Mheshimiwa Dkt. Diodorus B. Kamala, Mbunge wa Nkenge; Mheshimiwa Omary T. Mgumba, Mbunge wa Morogoro Vijijini; Mheshimiwa Mary D. Muro, Viti Maalum; na Mheshimiwa Lucia Mlowe Mbunge wa Viti Maalum. Pamoja na Waheshimiwa Injinia Kamwelwe, Naibu Waziri wa Maji na Profesa Ndalichako Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, michango yao ni mizuri na sisi tunaizingatia.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimshukuru Msemaji wa Kambi ya Upinzani kwa hotuba yake bila kumsahau Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kwa hotuba zao nzuri. Waheshimiwa Wabunge, baada ya kusema hayo naomba tu kutoa ufafanuzi wa mambo machache ambayo yamejitokeza wakati wa michango hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja la kwanza na ambalo linajirudia ni hili suala la Hati ya Dharura. Naomba kushauri Waheshimiwa kwamba suala hili la Miswada ya Sheria kuletwa hapa kwa Hati ya Dharura ni suala la Kikatiba. Ibara ya 89 ya Katiba ndiyo inatambua kutungwa kwa Kanuni za Kudumu za Bunge ambazo zitasimamia uendeshaji wa
shughuli za Bunge. Kwa hiyo hili ni suala la Kikatiba, ni halali Kikatiba na limewekwa kwenye Kanuni zetu za Kudumu kwenye Kanuni ya 80.

Mheshimiwa Naibu Spika, tusichanganye hati ya dharura kwa maana ya emergency sijui certificate of emergency, hii siyo cerficiface of emergency, it’s a certificate of urgency na Bunge kama alivyosema Mheshimiwa Mgumba, Bunge kazi yake kubwa ni kutunga Sheria. Kwa hiyo sharti hili liliwekwa kwa makusudi kwamba kama kuna mambo ya msingi, ya muhimu yanayogusa jamii ya wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Bunge lisisubiri. Hivi kuna dharura hapo mtasubiri mpaka Muswada uende sijui mpaka miaka mingapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hii ipo kwa faida ya wananchi. Hivi kwa mfano; mimi nimesikiliza hapa Wabunge wamepongeza kwa mfano juu ya kufutwa kwa RUBADA, imekuwa ni kero. Wabunge wamepongeza hapa juu ya VAT, Wabunge wamepongeza hapa karibu kila kitu. Kwa hiyo, haya nayo yangesubiri sijuii lini, hamuoni kwamba ni mambo ya maana sana? Kwa hiyo, naomba kushauri kwamba hii Miswada kuletwa hapa kwa hati ya dharura ni halali Kikatiba, ni halali kwa mujibu wa Kanuni zetu lakini pia ni kwa maslahi ya wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya pili ambayo naomba kuitolea ufafanuzi ni suala hili la mikataba tunayoingia kama Taifa na Mataifa mengine. Naomba kushauri kwamba Taifa nalo lina legal personality katika Jumuiya ya Kimataifa, lina haki, lina wajibu, linapohusiana na Mataifa mengine. Mataifa hayo nayo ni sovereign, yana mamlaka huru, mfano mkiwa na mgogoro na Malawi kwenye matumizi ya Mto Songwe, utamleta Mahakama ya hapa Kinondoni? It’s not possible, lazima muende kwa mtu mwingine na ndiyo maana hii mikataba ambayo moja tumeiridhia jana hii ya bomba la mafuta na hii ya matumizi ya Mto Songwe inaenda kwenye usuluhisi kwa mtu mwingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukimwambia Uganda kwamba aje hapa kwenye Mahakama ya kwetu hatakubali. Ndiyo hivyo tu. Ndiyo maana Waheshimiwa Wabunge mkizisoma zile Sheria tuliacha kwa makusudi kutumia maneno convention, protocols, statutes ambazo ndizo sheria na mikataba zinazo-govern mahusiano ya Mataifa na Mataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ni halali hiyo mikataba pamoja na kuwepo kwa sheria hizi ambazo tumezitaja hapa na tulizozipitisha hizi, hiyo mikataba inayohusu uhusiano wa Taifa hili na Taifa lingine iwe kwenye Regional yaani Kikanda, iwe Continental, halafu iwe International iende kwenye hayo Mabaraza mengine ya Usuluhishi na vyombo vingine. Hilo niliomba nilitoe.

Mheshimiwa Naibu Spika, na zaidi ya hapo, hii mikataba yenyewe mnayozungumza ya mto Songwe na hii ya bomba la mafuta imeingiwa mwezi wa Mei mwaka huu, sheria hizi zimepitishwa mwezi wa saba. Kwa hiyo hata katika hali ya kawaida bado huwezi kulaumu kwamba hivi ilikuwaje? Kwa hiyo, ni halali hizo sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo naomba kulitolea ufafanuzi hapa ni suala la sheria kutungwa Mkutano uliopita halafu inakuja kurekebishwa hapa Mkutano unaofuata. Ni kama tulivyoshauri hapa, hayo mambo ya msingi yale kama kuna kasoro haziwezi kusubiri mpaka muda fulani upite, lakini ukweli ni kwamba tunayo sheria inayotuongoza kwenye tafsiri ya sheria. Kwa hiyo, tunayo Sheria ya Tafsiri ya Sheria ambayo ndio sheria ya kwanza kabisa katika sheria inayoitwa The Interpretation of Laws Act (Sheria ya Tafsiri ya Sheria).

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria hii Kifungu cha 24 kimesema sheria inaweza ikatungwa katika Mkutano mmoja wa Bunge ikarekebishwa na kufutwa katika Mkutano huo huo wa Bunge, hicho ni Kifungu cha 24 cha Sheria ya Tafsiri ya Sheria. Kwa hiyo, hii ya kuja baada ya Mkutano mwingine unaofuatia it is not even a matter of contention. Naomba kushauri kwamba Waheshimiwa Wabunge walielewe hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo kwenye zile Sheria ya Natural Wealth and Resources, (Permanent Sovereignty) Act, of 2017 and Natural Wealth and Resources Contract (Review and Renegotiation) of Unconscionable Terms Act. Tulizungumza pale kwamba Bunge haliwezi likawa na mamlaka ya kuwa tena sasa linakuja kuidhinisha mikataba humu, ikatu-skip kwenye hii Sheria ya Petrol tulipokuwa tunarekebisha ile Sheria ya Petroli it was just an oversight.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, Bunge jukumu lake sasa katika mgawanyo wa madaraka katika Mihimili mitatu ya dola kwa mujibu wa Ibara ya 63(2) ni kuisimamia na kuishauri Serikali inapotekeleza majukumu yake. Majukumu ya kuingia mikataba na mataifa na taasisi nyingine yale yako kwa Serikali kama Mhimili (Executive). Bunge likianza na lenyewe kuidhinisha mikataba tutajifunga, sasa nani atamkosoa mwingine? Hiyo kasoro tumeiona, tukasema tuoanishe hii Sheria ya Petroli na sheria hizi nyingine ambazo zinazosimamia rasilimali hizi za nchi. Halafu mnasema ni shida, shida gani jamani?

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani wakati fulani ni kutokuelewa. Kwa hiyo Mwanasheria Mkuu wa Serikali yuko hapa Bungeni kwa ajili ya kuwasaidia watu kwenye masuala haya ya sheria, naamini wataendelea kuelewa tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna suala limezungumzwa juu ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, katika maelezo yale nimeeleza kwa nini. Kwa mujibu wa Ibara ya 59(4) Mwanasheria Mkuu wa Serikali amepewa mamlaka, ana haki za kuingia katika Mahakama zote hapa nchini katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Sasa turekebishe basi Katiba kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya hapo tunazo sheria kwa mfano Sheria ya the Office of Attorney General Discharge of Dispute Act, ya mwaka 2005, kwenye Kifungu cha 17 imetaja Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuingilia kwenye shauri lolote linalohusu Bunge, linalohusu Mahakama, linalohusu mali na taasisi au maslahi yoyote ya umma. Kwa mfano, mashirika ya umma yale yanamilikiwa na Serikali asilimia 100, Serikali haiwezi kufanya biashara inasema wewe utakuwepo hapa TANESCO kwa mfano, utafanya hiyo biashara. Sasa TANESCO ni mtoto wa Serikali akishtakiwa uache kwenda kumsaidia mtoto wako? That is simple logic. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano hii Tume ya Madini inayozungumzwa kwenye Kifungu cha 21 cha Sheria ya Madini, unaona ina mamlaka makubwa sana na inahodhi maliasili na rasilimali za nchi hii. Usipowalinda itakuwa shida sana, ndiyo tukasema basi kama ni lazima inapolazimika Attorney General aende kuwatetea, hakuna ubaya. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, naomba mlikubali hili nalo ni jema tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mambo yamezungumzwa hapa na hili la, Mheshimiwa Spika alikuwa amelizungumzia hapa lakini inajitokeza. Naomba kushauri hii habari ya migogoro kwenye Vyama vya Siasa, tuna Mhimili wa tatu wa dola ambao ni Mahakama. Hata katika uchaguzi watu wanapofanya Uchaguzi Mkuu kwenye
Majimbo yule anayeshindwa, ambaye haridhiki anaenda Mahakamani, si ndivyo tunavyofanya?

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kazi kubwa ni kuwatetea Wabunge wote wanaoshinda, haijalishi kwamba anatoka kambi ipi, ndivyo hali halisi ilivyo. Sasa kwenye hili kama kuna mgogoro, kuna Wabunge wa Chama cha Wananchi waende Mahakamani, Bunge hili haliwezi kuamua nani awe Mbunge, nani asiwe Mbunge. Nafahamu hivi ninavyozungumza kuna kesi Mahakamani, kwa hiyo hili ni kuleta tu purukushani isiyokuwa na sababu za msingi kwenye chombo hiki, tukitumie chombo hiki kutekeleza majukumu yake ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuweza kuhitimisha na nawashukuru tena kwa mara nyingine Wabunge wote mliopata fursa ya kuchangia kwenye hoja hizi, Mwenyezi Mungu aendelee kuwabariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.
Muswada wa Sheria ya Wakala wa Meli Tanzania wa Mwaka 2017
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia fursa hii ili niweze kuchangia kwa baadhi ya masuala ambayo mengi yamejitokeza mbele ya Bunge lako Tukufu. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii pia na nimeshangia sana kwenye Kamati. Kwa kweli katika Kamati kulikuwa na ushirikiano mkubwa sana, Serikali ilishauriwa sana. Nikushukuru sana kwa hekima yako kubwa sana kwenye masuala haya ya msingi unavyokuwa na msimamo katika kuwakilisha maslahi ya wananchi wote imetufikisha hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli kama sio uzalendo wa Kamati ile ya Miundombinu leo tusingekuwa na Muswada huu. Kwa hiyo, nakushukuru sana na nalishukuru sana Bunge lako hili. Inaonekana tunaposhirikiana kama alivyosema Mheshimiwa Kabati basi mambo haya tunayosimamia umma yanaenda vizuri sana. Mwenyezi Mungu aendelee kulibariki hili Bunge lako Tukufu liendelee kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo ni kwamba, Kamati kwa kweli ilikuwa na hoja kama ambazo baadhi ya wajumbe sasa wanazizungumza hapa kwamba inawezaje ukawa regulator halafu tena wewe mwenyewe ukawa wakala. Walikuwa na haki ya kusema vile kwa sababu mwanzo Muswada ulivyokuwa umeandikwa kwenye kifungu cha sita na cha saba ilikuwa kana kwamba huyu wakala atafanya kazi zote za uwakala.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tukakubaliana na Kamati kwamba hapana hilo halikuwa kusudi isipokuwa ni uandishi tu hatukuandika vizuri. Huyu yeye japokuwa atafanya kazi ya uwakala lakini amejikita kwenye masuala mahsusi tu ambayo yametajwa kwenye Ibara ya saba (7) ya Muswada huu ambayo Wabunge wote wanakubaliana kama ambavyo tumewasikiliza wote wakizungumza.

Mheshimiwa Spika, tumefanya mabadiliko kwenye hili jedwali la mabadiliko haya, yeye pale sasa anaweza akafanya shughuli nyingine tu ambayo haimhusu (yaani hizi za kawaida) kama kuna mambo matatu labda yamejitokeza; moja, labda kama mmiliki wa meli amemtaka yeye ndiyo afanye, pili; labda huyu wakala ameshindwa kutekeleza wajibu wake na tatu; kama labda wakala amekosa sifa za uwakala. Sasa bandari lazima iwe na sifa zake. Moja; ile reliability and efficiency na hii ni Taasisi ya Umma, ukisema tumwache tu hivi basi sifa za bandari zitaporomoka.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tukasema huyu afanye tu hizo kazi nyingine. Kama hayo mengine yakijitokeza na akimalizana na hiyo ameacha hiyo kazi. Kwa hiyo tumembana kabisa, lakini pia tumemwekea masharti. Ukisoma, tumefanya mabadiliko kwenye Kifungu cha 10 cha Muswada ukisoma hili jedwali la marekebisho. Waheshimiwa wengi wakati Mheshimiwa Waziri anasoma hotuba yake na wakati hata wengine wanachangia pengine Waheshimiwa Wabunge walikuwa hawajapata fursa ya kulisoma hili jedwali lakini tumeweka haya.

Mheshimiwa Spika, kwanza, moja la msingi yeye anapotekeleza jukumu lake lile la u-regulator, asi-assume intentionally kutaka kuwa na status ya predominancy yaani sasa anaweza akawa anawaonea wenzake tu kusudi yeye apore yale madaraka. Tumesema hapana! Halafu asi- discriminate watu na pia mu-encourage competition kwenye hiyo sekta, asiwe biased, tumemfunga kabisa pale na kama anatumia vibaya mamlaka yake tumesema aggrieved party alalamike kwa Waziri na kama haridhiki na maamuzi ya Waziri basi aende Mahakamani, kwa hiyo tumembana!

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuhakikisha kwamba hatatumia madaraka yake vibaya tumeweka utaratibu kwamba kutoa leseni maana hapa ndipo kunapoweza kuwa na shida akimwangalia huyu anasema huyu anaweza akanipiku, anasema wewe sikupi leseni, tumemuundia Kamati ya kumshauri ambayo ina evaluate zile application za leseni zile. Kwa hiyo, utaona kwamba kile ambacho Waheshimiwa Wabunge walikuwa wanahofia, hiyo sasa tumeifanyia kazi. Kwa hiyo nafikiri nishauri hili na Kamati yenyewe iliridhika vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeshauriwa sana kwenye Kamati, moja hatukuwa pia tumezingatia masharti ya bajeti yale. Tumeenda tumefanya mabadiliko. Utaona kwenye jedwali la marekebisho. Masuala la kuzingatia Sheria ya Bajeti kuhusu Mamlaka ya Treasury Registrar nayo tumeweka mle ndani. Kwa hiyo kwa ujumla, kama Waheshimiwa Wabunge tungekuwa na muda mrefu sana kwa mfano, kama tungekuwa na muda mrefu baada ya mabadiliko yote yale tungetengeza Muswada mpya, lakini muda haukuturuhusu kusudi kufanya iwe user friendly.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, karibu kila ambacho Kamati ilitushauri tumezingatia ukiacha jambo moja tu ambalo Mheshimiwa Waziri atalitolea maelezo na ziko sababu za kisheria na za kiufundi kwa nini Serikali ingependa kubakiza hilo jina, Waziri atalisema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kuna masuala haya kwa mfano mamlaka ya huyu Mkurugenzi. Ile ya kuwaonea wenzake anapotoa leseni tumeshamwekea stop order, lakini tumesema lazima yeye kama ana license pia awe na mamlaka ya kufuta hizo leseni. Haya ni masharti ya msingi kwenye tafsiri ya sheria.

Mheshimiwa Spika, ukisoma kifungu cha 47 kinasema aliye na mamlaka ya kutoa leseni pia na mamlaka ya ku- cancel au kui-suspend. Kinasema pia mtu yeyote ambaye anakuwa aggrieved na huyo, atachukua hatua zake kama anaona haki yake imekiukwa. Kwa hiyo, kama tukiisoma hii sheria sambamba na sheria nyingine utaona kwamba kwa kweli ule wasiwasi wao na hoja zao zimezingatiwa kwenye jedwali la marekebisho. Tumeona baadaye hapa majedwali ya marekebisho, lakini karibu yote yale yalikuwa yamezingatiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya ambayo tumepata mchango asubuhi na yenyewe tumeandaa further schedule of amendment, tumeyazingatia yale pale. Kwa hiyo, naomba kwa kauli hii ya umoja ambayo Wabunge wote wanaionesha hapa, huu Muswada tuuruhusu uendelee. Kazi ya kutunga hii sheria ni endelevu. Kimsingi tafsiri ya sheria inasema kwamba sheria inaweza ikatungwa Bunge hilo hilo na ikarekebishwa au ikafutwa kwenye Bunge hilo hilo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunalo Bunge lingine linakuja, kama kuna upungufu kadri tunavyoendelea kuitekeleza ile sheria tunaweza tukafikiria tu kwamba; bahati nzuri ninyi Waheshimiwa Wabunge wenyewe mnaangalia sana, mnasema hii imekaa vibaya, wenyewe mtashauri. Hata hivyo, bila hata ninyi kutushauri, Serikali kwa sababu inataka kunufaika na hii industry, itachukua hatua kuyarekebisha yale. Kwa hiyo, kazi hii ya kufanya mabadiliko ya sheria ni endelevu, kazi ya kutunga sheria ni endelevu. Kwa hiyo, tunaomba tu Waheshimiwa Wabunge huu moyo wa kuunga mkono juhudi za Serikali kudhibiti hizi rasilimali mnaouonesha hapa uendelee.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa na mchango kwamba, hapa Attorney General anakuja kushirikishwa kwenye kuendesha kesi tu mwanzoni hakuwepo, mbona katika mikataba hashirikishwi? Naomba kulishauri Bunge lako Tukufu kwamba ukisoma Ibara ya 59 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano inamhusisha Attorney General hata kwenye hayo mambo ya mikataba.

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Manunuzi ya Umma inasema mkataba lazima uwe umehakikiwa na Attorney General. Hauwezi kuingiwa, haijalishi kwamba ni ya taasisi ya Central Government au Shirika la Umma au Taasisi yoyote,
lazima mikataba yote iende kwa Attorney General. Pia Sheria ya Ubia, The Public Private Partnership Act hakuna mkataba utakaoingiwa kama Mwanasheria Mkuu wa Serikali pia hajashirikishwa na sheria mbalimbali. Kwa hiyo, hii japokuwa haikutajwa hapa naomba kushauri kwamba Waheshimiwa Wabunge wasiwe na wasiwasi hayo yatazingatiwa.

Kwa hiyo mengine haya labda niyaache, lakini niseme tu hivi, kulikuwa na hoja hapa kwamba kwa mfano kwa nini sasa kuna tofauti ya adhabu iliyoko Ibara ya saba (7) na Ibara ya 46. Ninachotaka kusema hapa ni kwamba, hii tofauti lazima iwepo. Moja, Ibara ya 46 inatoa adhabu ya jumla, (general penalty), lakini kwenye Ibara ya saba (7) hapa sasa hii ni mahsusi na kwa nature ya mambo haya yaliyoko pale ambayo Waheshimiwa Wabunge mnasema wote kwa kauli moja kwamba haya lazima yadhibitiwe na Serikali, ndiyo, maana unaona tumefanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, Ibara ya (7) kwanza tumeshaifanyia mabadiliko, kwa hiyo tuisome sambamba na jinsi ambavyo inaonekana kwenye jedwali la marekebisho. Kwa hiyo hii adhabu kwamba akipatikana na hatia apate adhabu isiyopungua kiwango cha dola 20 za Marekani, tumeacha tu hivyo huko kusudi hayo mengine Jaji aamue kutegemea na extent/gravity of the loss yaani kiwango labda cha hasara na uharibu sijui tuseme kwa Kiswahili gani hiki, ambacho kinaweza kuwa kimesababishwa na huyu bwana kujitwalia majukumu ambayo kimsingi yangekuwa ya Serikali. Huo ndiyo msingi wa kutokui-cap, tumwachie tu hiyo. Kwa hiyo, Mahakama i-assess.

Mheshimiwa Spika, nilifikiri nichangie hayo na kwa mara nyingine tena nakushukuru sana kwa hekima yako kubwa ya kuwezesha Muswada huu kufikia hatua hii. Pia nalishukuru sana Bunge na naishukuru Kamati. Mwenyezi Mungu aendeee kuwabariki. Naunga mkono hoja. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Waheshimiwa Wabunge kusema ukweli tusingekuwa hapa wala katika hatua hii kama sio ushirikiano mkubwa sana aliouonesha Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa Kamati ya Miundombinu kabisa, kabisa. (Makofi)

Pia tunampa ushauri kwamba wale Wanasheria wake wanaokwenda kwenye Kamati mbalimbali ni vizuri wapewe ushauri wakiwa wanakuja hapa wasije, kuna mmoja alifafanua vizuri nadhani Mary Muro; yaani wanakuja wanafikiri wao Wanasheria wa Serikali ndiyo wanaotunga sheria, hawajui kwamba Bunge ndilo linalotunga sheria. Wanakuja wanagomea Kamati, wanagomea kila kitu, hata wakiambiwa vipi wanakuwa na… lakini alipokuja Mwanasheria Mkuu wa Serikali akaweka maneno vizuri ndiyo maana leo tuko hapa. Spirit hiyo ndiyo tungependa tuwe nayo, kwa sababu mwisho wa siku ni ninyi Waheshimiwa Wabunge mnaotunga.

Kwa hiyo kupitia Kamati zenu msiwe wanyonge kwa chochote. Mkiwa wanyonge ni unyonge wenu wenyewe tu. Katika kutunga sheria lazima mwelewe kila kitu, mtuletee mambo yakiwa mazuri hapa. Kwa hiyo, Kamati you are empowered kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri sasa karibu sana. Una dakika 30, Mheshimiwa Profesa Mbarawa tafadhali.
Muswada wa Sheria ya Shirika la Mawasiliano Tanzania wa Mwaka 2017
MWANASHERIA MKUU A SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru ka kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha na mimi nipate fursa ya kushiriki nanyi nikishauri mambo kadhaa ambayo yamejitokeza humu ndani na hasa masuala ya katiba na sheria. Nianze kwa kusema tu kwamba naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli Serikali imechelewa sana kuleta Muswada huu. Sababu za kuwa na shirika linalosimamia mawasiliano yake nchini ni muhimu sana. Ngoja Waheshimiwa Wabunge niwaambie, yule mtu anayemiliki miundombinu ya mawasiliano anakutawala. Anayemiliki miundombinu ya uzalishaji wa umeme anakutawala. Kwa hiyo haishangazi mifano inayotolewa kuhusu China unaona wanamiliki miundombinu ya mawasiliano na mnaona ni the giant, one of the super powers, hata wakubwa wanalazimika kusafiri kutoka huko kwenda China. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Tambwe; labda niseme tu hivi unajua sisi tunaosoma ujamaa kila wakati, ujamaa ndio unaotawala sasa hivi. Kwa sababu hata katika hii corporate world kuna corporate social responsibility kwamba wewe ulienacho hakikisha kwamba unashirikiana na wengine. Kuna suala la kulipa kodi, kuna suala la floating shares kwenye stock exchanges watu wananunua shares. Kwa hiyo, unakuta mwananchi au mtu yeyote na miliki ile. Kwa hiyo tusiseme ujamaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilifikiri niliseme hili wazi kabla hatujaenda kusema. Kwa hiyo mimi nasema naunga mkono hoja muswada huu kama walivyoshauri Waheshimiwa Wabunge na kama ulivyoletwa na Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza ambalo ningeanza kulisemea ni suala kutunga sheria zinazotumika pande mbili za Muungano. Utaratibu umewekwa kwenye Katiba, Ibara ya 98(1) (b) imeeleza vizuri sana, sidhani kama nahitaji kuisoma kwa sababu nina muda mfupi sana. Lakini hayo mambo yanayohitaji theluthi mbili ya Wabunge kutoka Bara na theluthi mbili ya Wabunge kutoka Zanzibar ni yale mambo ambayo yameongezwa katika nyongeza ya pili, jedwali la pili.

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo yenyewe ukiyasoma; na ni lazima niyaseme sasa hapa; essentially ni mambo ya Katiba. Yaani katiba haijiandiki yenyewe inaletwa na Muswada. Kwa mfano kuwepo kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni suala la katiba hilo, ukishakwenda kwenye Katiba lazima uwe na theluthi mbili kutoka Bara na theluthi mbili kutoka Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuwepo kwa Ofisi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano, madaraka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano, kuwepo kwa Bunge la Jamhuri ya Muungano na madaraka ya Serikali ya Zanzibar ni masuala ya katiba yapo kwenye Katiba hii. Mahakama Kuu ya Zanzibar, orodha ya mambo ya Muungano na idadi ya Wabunge kutoka Zanzibar ni suala la Katiba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ukitaka kubadilisha haya unaleta Muswada wa Mabadiliko ya Katiba, ni lazima sasa hizi nchi mbili zinarudi katika position zake, wakubaliane. Kwa hiyo, Waheshimiwa na hii si sheria ya kwanza ambayo tumetunga kwa njia hii, tumetunga sheria nyingi tu hapa ambazo zinaenda kutumika Zanzibar kwa sababu hapa hatubadilishi katiba. Kwa hiyo ni suala tu la uelewa wa katiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliona nilifafanue hili lakini nadhani Waheshimiwa watanielewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni hili ambalo limezungumzwa na Mheshimiwa Bashe. Unajua ibara ya 36 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano, imeweka utaratibu wa namna ya kupata watendaji wakuu wa vyombo hivi. Kabla sijasema pale niseme hivi, Msajili wa Hazina (Treasury Registrar) ana sheria yake mahususi na chini ya sheria ile ndiye
anayesimamia utendaji wa haya mashirika kwenye level ya utendaji. Kwamba wanafanya kwa kadri inavyotakiwa lakini Waziri yeye msingi wake anahangaika na masuala ya kisera na msingi wake anahangaika na masuala ya kisera na msingi wake…

T A A R I F A . . .

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, siipokei, unajua sio wote wataalam wa Constitutional Law, hili nimelishalitafsiri. Nasema haya masuala yamewekwa mahususi tena mbele pale wamesema kwamba haya ndiyo yanayohusika na ibara ya 98(1)(b) ya kupigia kura. Waliokuwa ndani ya Bunge hili mwaka 2015 ilikuja hoja kama hii, Waziri Mkuya alikuwa na Miswada mitatu, Saada Mkuya akiwa Waziri yuko hapa; wakasema ni lazima twende Zanzibar tukatoa ufafanuzi hapa tukaelewana.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata kama tusingekuwa tumeliamua hapa, 2015 mbona hiki kifungu kinajieleza? Unasemaje haya yaliyopo pale, sheria za Utumishi, Immigration ambazo ndilo hasa Taifa lenyewe hilo kwa nini hazipigiwi kura mara mbili? Kwa hiyo, naomba kusema hivi kwenye masuala haya technical muachie Attorney General awasaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba uniongezee muda ili niyamalize haya. Hoja ya kusema kwamba mashirika haya ndiyo yaachwe kwa Treasury Registrar; ukweli ni kwamba Treasury Registrar ana mamlaka yake chini ya Sheria ya Treasury Registrar Act. Yeye ana mamlaka sasa ya kusimamia utendaji wa mashirika haya. Mamlaka haya ya Waziri yanayozungumzwa humu ni ya usimamizi wa masuala ya kisera na mamlaka hayo anapewa tangu kwenye kifungu cha sita (6) cha Sheria ya Mashirika ya Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo masuala ya kisera, someni sheria mama ya mashirika ya umma kifungu cha sita
(6) pale. Kwenye mambo ya utendaji sasa kuhakikisha kwamba yanafanya kazi kwa mujibu uliokusudiwa na yanajiendesha kibiashara, hakuna ufisadi, hakuna vitu gani hiyo ni kazi ya Treasury Registrar iko kwenye sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu hiyo pia, huyu Msajili wa Hazina hawezi kuteua viongozi hawa na yeye mwenyewe anateuliwa na Rais atateua nani? Kwa hiyo ibara ya 36, ibara ndogo ya Katiba inasema hivi:-

“Rais atakuwa na madaraka ya kuteua watu wa kushika nafasi za madaraka ya viongozi wanaowajibika kuweka sera za idara na taasisi za Serikali, na watendaji wakuu wanaowajibika kusimamia utekelezaji wa sera za idara na taasisi hizo katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano, nafasi ambazo zitatajwa katika Katiba hii au katika sheria mbalimbali zilizotungwa na Bunge kwamba zitatajwa kwa uteuzi unaofanywa na Rais.”

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, hawa lazima moja wateuliwe na Rais, kwamba Mtendaji Mkuu ateuliwe na Rais kama ambavyo Muswada unavyosema. Hawezi huyu akaachiwa akateuliwa na Waziri wala na Treasury Registrar. Treasury Registrar madaraka yake ni madogo sana, ni kwenye kusimamia utendaji bora wa mashirika haya ya umma ambayo Serikali ina hisa na ambayo Serikali haina hisa. Kwa mfano kuna mashirika mengine Serikali ina hisa kidogo sana, sasa unafanyaje, kule nako atateua Treasury Registrar? Kwa hiyo nilifikiri haya mawili ya kikatiba niyafafanue.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ningependa kushauri ni hili ambalo amelisema Mheshimiwa Saada Mkuya. Unajua ukija na scheme ya aina ile mnaanzisha ubaguzi usiokuwa na sababu, si tu kwamba ni kuvunja Katiba ibara ya 13(2), (4) na (5) pia sio utaratibu mzuri na hata ibara ya 17
(1) ya Katiba. Mimi nawafahamu Watanzania wenye asili ya Zanzibar ambao wengi wanaishi na kufanya kazi Bara. Kupata ajira katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania au taasisi yoyote ya umma wala haiangalii Uzanzibari wala Utanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sifa tu ni kwamba ukishakuwa raia wa Tanzania una nafasi ya kufanya kazi kila sehemu. Kwa hiyo kwa utaratibu huu unaopendekezwa kwamba kama ni Mkurugenzi tu sijui Zanzibar anakaa pale pale wengine Wapemba wanakaa pale pale mnataka kulivunja Taifa hili. Ni utaratibu ambao Wabunge msiuruhusu, ni kinyume cha Katiba na naomba kuwashauri muachane na mapendekezo ya aina hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine linazungumzwa…

T A A R I F A . . .

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa hiyo siipokei na naomba uniruhusu niendelee. Ushauri huo ndio tunaoujibu sasa hadharani kama ulivyotolewa hadharani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo nimeombwa nichangie ni hili ambalo limezungumzwa na Mheshimiwa Richard Mbogo ambaye pamoja na kuunga mkono ameona kwamba kile kifungu cha 22(1) (a) kwenye Muswada kiondolewe ili shirika liweze kujiendesha. Pia nimesikia michango mingi ya Waheshimiwa Wabunge ambao wanataka sasa shirika hili liwezeshwe kimtaji ili liweze kwenda kufika sehemu ambazo huduma hizi hazifikiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu hiki kimewekwa hapo makusudi ili kulisaidia sasa shirika hili liwe na mtaji wa kutosha kuja kutekeleza majukumu ambayo sasa linapewa ikiwa ni pamoja na kupeleka huduma za miundombinu katika sehemu mbalimbali ambako huduma hizi hazipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nafikiri kwamba kuna umuhimu sana kifungu hiki kikabaki, kisipobaki na wengine wamesema hapa sehemu nyingine hakuna, sasa watapata wapi pesa za kujiendeshea lazima waendeshwe pale. Ila kazi ya Wabunge sasa itakuwa ni kuishauri Serikali mbona hamjatenga fedha za kuwezesha miundombinu ili Shirika hili la simu lifike huko tunakokwenda?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme tu kwamba Serikali kwa kweli ilisikiliza sana Kamati ya Miundombinu ikafanya jedwali la marekebisho. Kwa hiyo, yale ambaye umeyazungumza tulishawasilisha ndani ya Bunge lako Tukufu jedwali la marekebisho ambalo limeyafikiria yote haya. Yale ambayo pia mmechangia asubuhi tayari tumeshaweka kwenye jedwali la marekebisho na tumewagawia Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nashukuru kwa kunipa fursa hii niweze kuchangia katika hizi hoja mbili na niseme tu kwamba naunga mkono hoja zote mbili. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii pia kushiriki katika kuchangia hoja hizi mbili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nitoe ufafanuzi katika baadhi ya masuala ya kikatiba na kisheria ambayo yamezungumzwa hapa. Niseme tu kumekuwa na hoja zinazojirudia sijui kama ni mkakati wa makusudi au ni kutokuelewa kwamba mambo yanatolewa ushauri hapa wa kisheria na Kikatiba lakini yanarejewa wakati fulani kwa namna ya kupotosha. Kwa sababu mimi wajibu wangu ni kutoa ufafanuzi wa eneo hilo, sitachoka kulisaidia Bunge liweze kuelewa wajibu wake vizuri linapotekeleza majukumu yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, moja, kumekuwa na hoja inayodai kwamba Serikali inapoka madaraka ya Serikali za Mitaa. Hii si kweli kwa sababu Serikali za Mitaa ziko kwa mujibu wa Katiba. Ukisoma Ibara ya 145 na 146 ya Katiba zimeeleza vizuri Serikali za Mitaa. Katiba hiyo imesema pia kwamba hizi Serikali za Mitaa zitafanya kazi mbali ya Katiba pia kuzingatia sheria zilizotungwa na Bunge hili. Kwa sababu hiyo, zimetungwa Sheria kwa mfano The Local Government District Authorities, The Local Government Urban Authorities, The Local Government Finance Act na sheria nyinginezo. Kwa mujibu wa Ibara ya 146(2), majukumu ya hizi Serikali za Mitaa ni kutekeleza kazi za Serikali za Mitaa katika eneo lake, kuhakikisha utekelezaji wa sheria na ulinzi wa wananchi, kuimarisha demokrasia katika eneo lake na kuitumia demokrasia kuharakisha maendeleo ya wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mambo haya yote ndiyo msingi wa Katiba na hata sheria hizo zinazoongoza Serikali za Mitaa katika kutekeleza majukumu yake zimeweka Mabaraza ambayo wajumbe wake wanateuliwa na wananchi wenyewe. Kwa mfano, Sehemu ya Tano ya Sheria ya The Local Government District Authorities, inaeleza majukumu ya Serikali za Mitaa kuwa ni:-
(a) To maintain and facilitate the maintainance of peace, order and good governance within its area of jurisdiction.
(b) To promote the social welfare and economic well-being of all persons within its jurisdiction.
Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hiyo imeeleza mambo mengine mengi. Pia Sheria ya Tawala za Mikoa imeweka mamlaka ya Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya. Hawa ni wawakilishi wa Serikali Kuu katika hizi Serikali za Mitaa kuhakikisha kwamba haya mambo yanatekelezeka. Sheria hizi za Serikali za Mitaa zote mbili pia zinaeleza mamlaka ya Wakuu wa Mikoa na mamlaka ya Wakuu wa Wilaya katika hizo Serikali za Mitaa. Wakuu wa Mikoa wametajwa katika Ibara ya 61 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano na kazi zao zimetajwa pale. Kwa hiyo, Wakuu wa Mikoa au Wakuu wa Wilaya wanapokuwa wanatekeleza majukumu yao ambayo wamepewa kwa mujibu wa Katiba na kwa mujibu wa Sheria za Serikali hizi Mitaa na Sheria ya Tawala za Mikoa wasichukuliwe kwamba wanaingilia mamlaka ya Serikali za Mitaa, hilo la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba vyeo hivi viko kihalali. Ukisoma Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya kwanza imeeleza eneo la Jamhuri ya Muungano, baadaye ibara ndogo inaeleza kwamba hili eneo la Jamhuri ya Muungano litagawanywa katika maeneo mbalimbali ya kiutawala ambayo ni pamoja na mikoa na wilaya na wanawekwa huko viongozi wa kusimamia. Kama ilivyo kwenye Bunge ambapo unakuwa na Spika, unakuwa na Wabunge, unakuwa na Madiwani ndivyo ilivyo pia kwenye executive ambapo unakuwa na Rais, Mawaziri, Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya. Kwa hiyo, huwezi ukavunja ile sasa ukasema kwamba hivi vyeo vifutwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo napenda kulitolea ufafanuzi ni suala la kwamba Serikali ilete Muswada wa Sheria ili kumpatia mamlaka Mkurugenzi wa TAKUKURU kufungua kesi mahakamani bila hata kupata kibali cha Mkurugenzi wa Mashtaka. Naomba kulishauri Bunge lako Tukufu kwamba sheria iliyopo inatoa mamlaka kwa Mkurugenzi wa TAKUKURU kufungua mashtaka mahakamani kwa baadhi yake bila kulazimika kupata kibali cha Mkurugenzi wa Mashtaka. Ukisoma kifungu cha 57 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa kinaeleza hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la msingi zaidi ni kwamba Ibara ya 59B ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inampa mamlaka Mkurugenzi wa Mashtaka kuwa na uwezo wa kufungua, kuendesha na kusimamia mashtaka yote nchini. Kwa mfano, katika kifungu cha 15 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, makosa ya kudai, kushawishi, kupokea au kutoa ahadi za kupokea au kutoa rushwa haya yanafunguliwa na Mkurugenzi wa TAKUKURU bila kulazimika kupata kibali cha Mkurugenzi wa Mashtaka. Huyu Mkurugenzi wa Mashtaka, kwa mujibu wa sheria yao yeye ni huru, haingiliwi. Isipokuwa anatekeleza majukumu yake kwa kuzingatia mambo yafuatayo, Ibara ya 59B(4) inasema;
“Katika kutekeleza mamlaka yake, Mkurugenzi wa Mashtaka atakuwa huru, hataingiliwa na mtu yeyote au mamlaka yoyote na atazingatia mambo yafuatayo:-
(a) nia ya kutenda haki;
(b) kuzuia matumizi mabaya ya taratibu za utoaji haki; na (c) maslahi ya umma.”
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kama kuna watu hawafikishwi mahakamani amezingatia tu haya. Vilevile kama kuna watu wanafikishwa mahakamani amezingatia tu haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kulishauri Bunge lako Tukufu, Waheshimiwa Wabunge tujiepushe kuzungumzia mambo yaliyoko mahakamani. Hatua hiyo inakuwa na nia ya kuvuruga mwenendo wa mashauri yaliyoko mahakamani. Hakuwezi kukawa na parallel processes, Bunge lishiriki halafu Mahakama iendelee, sijui ufungue kesi nyingine Uingereza, how can we? Hii ni kuharibu tu mashauri haya yanayoendelea. Lazima Wabunge sisi tutambue mipaka ya madaraka yetu. Hizi hoja nyingine Waheshimiwa Wabunge tutumie hekima tunapokuwa tunazifikiria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme moja, uchaguzi wa Zanzibar ni uchaguzi huru, ulifanyika kwa haki kwa sababu ulisimamiwa na Tume Huru ya Uchaguzi. Tume ambayo ilitekeleza jukumu lake la Kikatiba kwa ufanisi ipasavyo.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hakuna chombo kilichosema kwamba uchaguzi ule haukuwa huru na wa haki.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilisisitize hili kwa sababu Katiba yenyewe ya Zanzibar katika Ibara ya 21(1) inasema; “Kila Mzanzibari anayo haki ya kushiriki katika shughuli za utawala wa nchi, ama moja kwa moja…”
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa walipewa nafasi hiyo, wakakataa wao wenyewe kushiriki. Hawawezi kudai kwamba uchaguzi ule ulikuwa sio huru wala wa haki. (Makofi)
NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa AG, muda wako umekwisha.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nikushukuru kwa kunipatia fursa hii niweze kuchangia hoja hii muhimu. Nimshukuru Mwenyezi Mungu lakini pia nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, mwenye dhamana ya Muungano kwa hotuba yake nzuri ambayo naiunga mkono. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kutoa ufafanuzi kwenye masuala machache ya kikatiba. Moja, ni lile linalodaiwa kwamba Tanganyika imejivika koti la Muungano na inafanya ukoloni na unyonyaji Zanzibar.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hii si kweli kwa sababu Muungano huu unatokana na ridhaa ya mataifa mawili yaliyoungana mwaka 1964. Kupitia Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2010, Ibara ya 1 inatamka hivi; “Zanzibar ni nchi ambayo eneo la mipaka yake ni eneo lote la Visiwa vya Unguja na Pemba pamoja na Visiwa vidogo vilivyoizunguka na bahari yake ambayo kabla ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ikiitwa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 2 inasema hivi; “Zanzibar ni miongoni mwa nchi mbili zinazounda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, mabadiliko haya yalipigiwa kura ya maoni na Wazanzibari wote wakaridhia. Kwa hiyo, si kweli kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano imejivika koti la Muungano na inafanya ukoloni na unyonyaji kule Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Serikali hizi mbili zimegawana majukumu. Ukisoma Ibara ya 4 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeeleza wazi majukumu ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano, majukumu ya Serikali ya Zanzibar, majukumu ya Bunge la Jamhuri, majukumu ya Baraza la Wawakilishi, majukumu ya Mahakama ya Jamhuri ya Muungano na majukumu ya Mahakama ya Zanzibar. Moja ya mambo hayo ni mambo ya ulinzi na usalama na Mheshimiwa Dkt. Mwinyi ameyatolea ufafanuzi. Kwa hiyo, si kweli kabisa kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano imejivika koti la Muungano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu ni hili ambalo linazungumzwa kwamba Muungano huu ni wa kulazimishwa.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimekwishasema mabadiliko haya ya Katiba ya mwaka 2010 yamepigiwa kura ya maoni na vyama vyote na wananchi wote wa Zanzibar walishirikishwa wakasema Muungano huu wanaukubali. Katiba hii ya Zanzibar yenyewe inasema Zanzibar ni mojawapo ya nchi mbili zinazounda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la nne ambalo ningeomba kulizungumzia ni suala hiari ya mtu kushiriki uchaguzi. Hii iko kwenye Ibara ya 21 ya Katiba ya Zanzibar, naomba kusoma; “(1) Kila Mzanzibari anayo haki ya kushiriki katika shughuli za utawala wa nchi, ama moja kwa moja au kwa kupitia Wawakilishi waliochaguliwa kwa hiari.
(2) Kila Mzanzibari anayo haki na uhuru wa kushiriki kwa ukamilifu katika kufikia uamuzi juu ya mambo yanayomhusu yeye maisha yake au yanayolihusu Taifa.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ushiriki ni wa hiari na kule Zanzibar kuna vyama vingi, vyama vingine vilishiriki, chama kingine kikaamua kutoshiriki ni hiari yao. Kwa hiyo, walitumia haki yao ya hiari kuamua ama washiriki au wasishiriki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hii ni haki yao ambayo iko kwenye Katiba kwamba ni hiari huwezi kuwalazimisha watu waende kwenye uchaguzi na wao walioamua kutoshiriki hawawezi kudai kwamba hawakushiriki. If any thing wanaweza kwenda mahakamani kwa Ibara ya 72 ya Katiba ya Zanzibar inayosema kwamba mtu yeyote anayepinga matokeo ya uchaguzi wa Zanzibar ataenda mahakamani. Mpaka leo napozunguza hakuna raia yeyote aliyeenda kufungua kesi kwenye Mahakama ya Zanzibar kupinga matokeo ya Baraza la Wawakilishi katika Jimbo lolote lile. Bunge hili haliwezi kutumika tena kupoka mamlaka ya Zanzibar na Katiba ya Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, naomba kushauri kwamba Waheshimiwa tuna wajibu kwanza wa kudumisha umoja wa Kitaifa. Hivi ndivyo tunavyoelekezwa na Katiba ya Jamhuri kwenye Ibara ya 28(1) na ndivyo pia tunavyoelekezwa na Katiba ya Zanzibar Ibara ya 23(4). Ni wajibu kabisa wa Kikatiba na Mungu anawapenda sana watu wanaodumisha amani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanaosoma Biblia imeandikwa sehemu fulani kwamba heri mpatanishi kwa kuwa ataitwa mwana wa Mungu. Kwa hiyo, tunapozungumza mambo ya umoja wa Kitaifa, naomba kushauri kwamba tuwe waaminifu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2017.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nikushukuru kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia. Pia nikupongeze kwa jinsi ambavyo umeendelea kuliongoza Bunge hili kwa ufanisi ipasavyo. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kuchangia na nawashukuru sana watumishi wote na Wanasheria wa Serikali wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa jinsi ambavyo wameendelea kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi ipasavyo kwa maslahi ya Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa hotuba nzuri sana ambayo naiunga mkono. Niipongeze Kamati ya Bajeti kwa kazi kubwa waliyoifanya kui-engage Serikali ambayo ilisababisha Serikali ikaja na mapandekezo haya ambayo sasa inayajadili na Wabunge wanaunga mkono kwa maslahi ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kufafanua mambo machache kwa sababu ya muda mfupi nilionao:-

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza kwa ufupi na kwa harakaharaka sana, baadhi ya Wabunge wamechangia juu ya kuleta mabadiliko kwenye ile Urban Authorities Rating Act, kwamba wale wazee wenye umri wa miaka 60 na kuendelea wasitozwe kodi ya majengo. Uamuzi huu tayari ulishafanyika kupitia Sheria ya Fedha ya Mwaka 2016. Ukisoma Kifungu cha 69 kimeeleza na pale tumeweka vizuri, pale wazee miaka 60 na kwenda mbele, lakini na watu watu wengine wote wenye ulemavu ambao hawana namna ya mapato, hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ambalo naomba kuliweka wazi ni hili; kumekuwa na michango hapa kwamba msamaha wa tozo ya usajili wa magari kwamba, ni kiini macho kwa sababu hatukuleta Mabadiliko hapa ya Sheria ya Traffic (Road Traffic Act). Ukweli ni kwamba hizi kodi ziko kwenye Kanuni, kwa hiyo, hatuhitaji kuleta hapa Muswada. Someni hizi Kanuni, Government Notes Number 177 ya Mwaka 2001 ambayo ilirekebishwa tena na Kanuni Namba 235 ya Mwaka 2013, kwa hiyo hatuhitaji kuleta Muswada hapa, kila kitu kiko sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho ambalo naomba kushauri ni hili la uhalali wa Muswada huu. Kwa ufupi naomba kusema hivi; Muswada huu haukuvunja Kanuni yoyote zinazo- cover utungaji wa sheria, sehemu ya nane yote imezingatiwa. Waheshimiwa Wabunge wameshirikishwa ipasavyo kupitia kwenye Kamati, hawa wadau wameshirikishwa na wadau wale pamoja na Wabunge ndio tukaboresha ule Muswada kwa yale waliyopendekeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Muswada wa awali ulikuwa na sheria tisa, kwa waliyopendekeza tumeongeza sehemu ya sheria sita. Sasa Kanuni zetu zinazotuongoza kwenye Bunge linapokaa, linaturuhusu kufanya mabadiliko kuboresha kwenye vifungu vya Sheria zilizoko kwenye Muswada, haikuwepo! Kwa hiyo, hekima ikasema tuuchapishe huu Muswada upya, na kuuchapisha Muswada upya imeruhusiwa kwenye Kanuni zetu, someni Kanuni ya 86(10), Muswada ulichapishwa upya.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya mambo kwa sababu ni ya msingi sana, naomba muishukuru Serikali kwa kuyakubali haya na naishukuru sana Kamati ya Bunge na Wabunge wote ambao wameunga mkono suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumalizia kwa kuendelea kuwaunga mkono ndugu zangu Waislamu ambao wanashiriki toba hii, Mungu aendelee kuwabariki. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii nami niweze kuchangia. Nianze kwa kusema tu kwamba naunga mkono hoja. Naomba nitoe ufafanuzi wa masuala matatu ya kisheria ambayo yamejitokeza hapa. La kwanza ni hili ambalo limekuwa likijirudia, nadhani na lenyewe linahitaji kutolewa ufafanuzi kila linapojirudia.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la ile Hati ya Rais ya mgawanyo wa madaraka kwa Mawaziri anaowateua; tumewahi kutoa ufafanuzi kwenye Bunge hili Tukufu na kwa sababu pengine Waheshimiwa Wabunge wanapenda kujua zaidi, nami nitaendelea kutoa ufafanuzi huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba hata kama ile hati ingechelewa kutolewa, kwa sababu Rais alipokuwa alikuwa anakamilisha Serikali yake, kutokuwepo kwa ile hati isingekuwa ni sababu kwamba Mawaziri na Serikali washindwe kuwa na Mwongozo wa kufanya kazi zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwongozo wa Serikali na kama ilivyo kwa raia yeyote wa Tanzania, ni Katiba ya nchi, sheria zenyewe, sera zilizopo na Ilani ya Chama kinachotawala. Ndiyo maana hata Mawaziri walipokuwa wanafanya kazi yao kabla ya hiyo Hati ya Mgawanyo wa Madaraka yao haijatoka, hakuwahi kutokea mgongano wowote. Kama nilivyosema, kukitokea mgangano kwa mujibu wa ile sheria, Mahakama itasema tu kwamba hili liende kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Mwanasheria Mkuu wa Serikali atakachokifafanua ndiyo itakuwa mwisho wa hilo suala.
Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa hii kulifahamisha Bunge lako Tukufu kwamba, Mheshimiwa Rais tayari ameshatoa hii Hati ya Mgawanyo wa Madaraka ya Mawaziri, kupitia tangazo la Serikali Namba 144, lililochapishwa tarehe 22 Aprili, 2016 na mwongozo huu siyo kama labda ndiyo unawaelekeza kwamba wafanye hiki, wasifanye hiki; siyo mpango kazi wala siyo strategic plan au plan yenyewe. Wenyewe unachokifanya, unatoa tu mgawanyo kwamba Wizara fulani itashughulika na hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, nitoe mfano Wizara hii ya leo ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, wao watashughulikia yafuatavyo, nitasoma kwa Kiingereza:-
(a) Policies on agriculture, livestock, fisheries, food security and cooperative and their implementation;
(b) Agriculture, livestock and fisheries land use planning;
(c) Agricultural research and extention services on agriculture, livestock and fisheries;
(d) Food security management;
(e) Crop warehouse licensing;
(f) Strategic food reserve management;
(g) Commodit exchange;
(h) Development of Societies and Cooperatives;
(i) Cooperative Savings and Credit Societies;
(j) Agriculture live stock and fisheries infrastructure development;
(k) Marketing and value addition for agriculture, livestock and fisheries products;
(l) Livestock and fisheries product development;
(m) Veterinary services;
(n) Fish farming;
(o) Perfomance, improvement and development of human resources under this Ministry; and
(p) Extra Ministerial Department, Parastatal Organization, Agencies, Programme and Projects under this Ministry.
Kwa hiyo, wenyewe huu haukuongozi kwamba kafanye hiki; ni mwongozo tu. Hilo la kwanza ambalo naomba Waheshimiwa Wabunge walifahamu, kwamba siyo kitu ambacho kinapaswa kiwe kinawasumbua sana.
La pili ambalo naomba kulitolea ufafanuzi ni hili suala la ripoti ya Tume iliyoundwa na Mheshimiwa Rais kuchunguza jinsi Operesheni Tokomeza ilivyoendeshwa. Tume hii iliundwa chini ya sheria inayoitwa Commission of Enquiry Act na Mheshimiwa Rais, hii Tume anapaswa aiunde pia kwa kutumia Government Notice. Kupitia Government Notice Namba 131 ya tarehe 2 Mei, 2014, aliunda hii Tume na Tume ikishaundwa kwa mujibu wa sheria hii, haileti ripoti yake Bungeni, inaundwa na Rais na ripoti yake inaenda kwa Rais.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii Tume ilishamaliza kazi yake, iliripoti kwa Mheshimiwa Rais, naye akaelekeza na ana mamlaka chini ya sheria hiyo ya Commission of Enquiry Act kuamua kwamba hiki kitu kiwe public, yaani kiwe cha wazi au kibaki jinsi ilivyo. Alichokifanya, ameelekeza; kutokana na mapendekezo yalitolewa na ile Tume, zile Taasisi zinazohusika zishughulikie. Kwa mfano, Maliasili wana maelekezo yao; Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Idara ya Mashtaka ina maelekezo yao; Wizara ya Mambo ya Ndani, Jeshi la Polisi wana maelekezo yao na wanachukua hatua. Kwa hiyo, hakuna sababu ya kulileta humu, muiachie Serikali itekeleze hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho ninalotaka kutoa ufafanuzi ni hili suala la kesi ya Tawariq1. Baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wamesema kwamba ilikuwa ni maamuzi yasiyozingatia sheria. Tusiilaumu Mahakama jamani. Mahakama haiwezi kufanya maamuzi halafu tukasema ni maamuzi yasiyozingatia sheria. Hata Mkurugenzi wa Mashtaka alipoamua kulitoa lile shitaka Mahakamani, alikuwa amezingatia mamlaka yake aliyonayo chini ya Ibara ya 59(b)(4) inayosema kwamba katika kutekeleza mamlaka yake, Mkurugenzi wa Mashtaka atakuwa huru, hataingiliwa na mtu yeyote au mamlaka yoyote na atazingatia mambo yafuatayo:-
Nia ya kutenda haki, kuzuia matumizi mabaya ya taratibu za utoaji haki na maslahi ya umma. Kwa hiyo, tuna kila sababu ya kuamini kwamba Mkurugenzi wa Mashtaka alipoondoa lile shauri Mahakamani, haya yamezingatiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, mpaka sasa hakuna amri yoyote ya Mahakama iliyosema kwamba tulipe fidia ya shilingi bilioni mbili.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri ambayo imejaa mipango na mikakati na hatua ambazo Serikali inachukua katika sekta hii ya afya na nichukue fursa hii pia kumshukuru Waziri Kivuli wa Afya kwa hotuba yake nzuri ambayo imeeleza ushauri mzuri kuhusiana na mikakati ambayo Serikali inachukua katika kutekeleza wajibu wake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze tu kwa kufafanua mambo machache ya Kisheria na Kikatiba. Nikianza na hili linalozungumzwa juu ya Ibara ya 46(1)(g) ya Katiba inayodaiwa kueleza kwamba, wanawake wana haki ya kupata huduma za afya (women with right to health).
Mheshimiwa Mwenyekiti, nisme tu kwamba, Serikali inatambua kuwa, wanawake wanastahili na wana haki ya kupata huduma za afya na imekuwa ikichukua hatua mbalimbali kuhakikisha kuwa huduma hii inapatikana kama ilivyoelezwa na Waziri katika hotuba yake. Hata hivyo, ni vizuri kuweka kumbukumbu sahihi kuwa Ibara ya 46(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haiweki masharti kuhusu haki ya wanawake kupata huduma za afya kama ilivyoelezwa na Mheshimiwa Mbunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 46 ya Katiba inaweka masharti kuhusu kinga aliyonayo Rais dhidi ya mashtaka ya madai au jinai. Masharti kuhusu haki ya wanawake kupata huduma ya afya yalivyotajwa na Mheshimiwa Mbunge yako katika Ibara ya 57(1) ya rasimu ya Katiba iliyoandaliwa na iliyokuwa Tume ya Marekebisho ya Katiba. Hata hivyo, haki hiyo iliboreshwa na Bunge Maalum la Katiba na kuwekwa katika Ibara ya 57(f) ya Katiba inayopendekezwa ambayo inaelezwa kwamba, kila mwanamke ana haki ya kupata huduma bora ya afya ikiwemo afya ya uzazi salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba hii inayopendekezwa inatoa haki mbalimbali ikiwemo haki ya kupata maji salama na safi. Hata hivyo, Katiba hii inayopendekezwa sasa haina nguvu za kisheria kwa sababu haijapigiwa kura na kuanza kutumika. Hilo niliona nilitoe kama ufafanuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya pili ambayo naomba kuifafanua ni kwamba, imedaiwa kuwa, kuna manyanyaso, ukatili na hakuna haki ya watoto walioko magerezani au wenye kesi za kwamba, wananyimwa haki kuanzia kwenye usikilizwaji wa kesi mpaka kwenye mazingira wanayoishi ndani ya gereza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kushauri kwamba pamoja na changamoto zilizoelezwa na Waheshimiwa Wabunge kuhusu usikilizwaji na uendeshwaji wa kesi za jinai dhidi ya mtoto. Napenda kulifahamisha Bunge hili kuwa Serikali imeweka mfumo wa kitaasisi na kisheria kuhusu namna ya kushughulikia masuala yanayohusu watoto ikiwemo kesi za jinai.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali pamoja na kuridhia mikataba inayohusu haki za watoto (The United Nation Conventions for the Rights of the Child and African Charter on the Rights and Welfare of the Child), imetunga Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 ambayo imeweka masharti yaliyomo katika mikataba hiyo. Hii sheria inaweka masharti kuhusu haki ya mtoto ambayo anakabiliwa na kosa la jinai na kuweka masharti kuhusu kukamatwa kwake, kuwekwa mahabusu, uendeshaji wa kesi yake na adhabu na baadhi ya masharti hayo ni kama ifuatavyo:-
Moja, imeweka Mahakama ya Watoto, ambayo itafahamika kama Mahakama ya Watoto kwa madhumuni ya kusikiliza na kuamua masuala yanayohusiana na watoto.
Pia, Mahakama ya Watoto itakuwa na uwezo wa kusikiliza na kuamua mashauri yote ya jinai dhidi ya mtoto na kwenye Kifungu cha 99 inawekwa utaratibu wa kuendesha mashauri katika Mahakama ya Mtoto katika masuala yote kulingana na Kanuni zitakazokuwa zimetungwa na Jaji Mkuu, kwa namna yoyote zitakuwa ni kulingana na masharti yafutayo:-
(i) Kwanza, Mahakama ya Watoto itakaa mara nyingi kama itakavyolazimu;
(ii) Mashauri yataendeshwa kwa faragha;
(iii) Kadri inavyowezekana mashauri yataendeshwa kwa njia isiyo rasmi na yataendeshwa kwa kuulizwa maswali bila kuwekwa mtoto katika utaratibu wa advisory, atahudhuria pia Afisa wa Ustawi wa Jamii;
(iv) Mzazi, mlezi au mtu anayemwakilisha mtoto atakuwa na haki ya kuhudhuria;
(v) Mtoto atakuwa na haki ya kuwa na nguvu na kuwakilishwa na Wakili, kuwa na ndugu;
(vi) Haki ya kukata rufaa itawekwa bayana kwa mtoto; na
(vii) Mtoto atakuwa na haki ya kujieleza na kutoa maoni yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wakati wa…..
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Mheshimiwa AG, ahsante.
Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kupata fursa ya kuchangia kwenye hoja hii muhimu na nakushukuru wewe kwa kunipa fursa hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa hotuba yake nzuri na mipango mizuri kwa ajili ya Jeshi hili la Ulinzi wa Wananchi wa Tanzania. Pia niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango yao ya kuboresha hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kutoa ufafanuzi wa masuala mawili, matatu hivi ya kikatiba na kisheria ambayo yamejitokeza hapa. Moja, linahusu utumishi wa Jeshi la Ulinzi wa Wananchi wa Tanzania katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetajwa na Ibara ya 1 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano kwamba ni nchi moja nayo ni Jamhuri ya Muungano. Ibara ya 2 ya Katiba inasema:-
“Eneo la Jamhuri ya Muungano ni eneo lote la Tanzania Bara na eneo lote la Tanzania Zanzibar, na ni pamoja na sehemu yake ya bahari ambayo Tanzania inapakana nayo”.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kupata fursa ya kuchangia kwenye hoja hii muhimu na nakushukuru wewe kwa kunipa fursa hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa hotuba yake nzuri na mipango mizuri kwa ajili ya Jeshi hili la Ulinzi wa Wananchi wa Tanzania. Pia niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango yao ya kuboresha hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kutoa ufafanuzi wa masuala mawili, matatu hivi ya kikatiba na kisheria ambayo yamejitokeza hapa. Moja, linahusu utumishi wa Jeshi la Ulinzi wa Wananchi wa Tanzania katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetajwa na Ibara ya 1 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano kwamba ni nchi moja nayo ni Jamhuri ya Muungano. Ibara ya 2 ya Katiba inasema:-
“Eneo la Jamhuri ya Muungano ni eneo lote la Tanzania Bara na eneo lote la Tanzania Zanzibar, na ni pamoja na sehemu yake ya bahari ambayo Tanzania inapakana nayo”.
Mikoa, kifungu cha tano (5) kinataja majukumu ya Wakuu wa Mikoa, naomba kunukuu:-
“(1) Mkuu wa Mkoa atakuwa mwakilishi mkuu wa Serikali katika eneo la mkoa ambalo ameteuliwa na kwa madhumuni hayo majukumu yote ya kiserikali yanayohusu mkoa huo yatatekelezwa na/au kupitia Mkuu wa Mkoa.
(2) Katika kuendeleza madhumuni na masharti ya kifungu kidogo cha (1) Mkuu wa Mkoa atakuwa na wajibu wa kusimamia utekelezaji wa sheria na uwepo wa amani katika mkoa huo, kutoa mwelekeo mahsusi wa sera za jumla za Serikali katika mkoa na kutekeleza kazi na majukumu mengine kama yanavyotekelezwa au kutolewa kwake na/au chini ya sheria hii au sheria nyingine yoyote”.
Mheshimiwa Naibu Spika, utaona kwamba hawa hawahusiki kabisa na shughuli za vyama vya siasa. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge waamini kama Serikali ilivyokwisha kufafanua hapa kwamba, hawa ambao Katiba imewapiga marufuku kuwa wanachama wa vyama vya siasa kama Wanajeshi, hata wanapoteuliwa kuwa Wakuu wa Wilaya au Mikoa, hawawezi kuwa Wajumbe wa Kamati za Siasa za Kamati za Halmashauri Kuu za CCM.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hivi hakuna sheria yoyote katika hizi ambazo zimeshatungwa zinazotoa majukumu kwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya kujihusisha na vyama vya siasa. Kimsingi wanapoteuliwa, mara ya mwisho nilishuhudia pale Ikulu Mheshimiwa Rais alipowateua hawa Wakuu wa Mikoa wa mwisho wakiwemo na Wanajeshi, aliwakabidhi katiba na sheria. Hata Wakuu wa Wilaya wanapoapishwa kule na Wakuu wa Mikoa wanakabidhiwa katiba ya nchi na sheria, hawakabidhiwi hizi katiba za vyama vya siasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kushauri tu kwamba, hili ambalo linaleta wasiwasi humu ndani Waheshimiwa Wabunge hawana sababu ya kuwanalo. Jeshi letu lina watu wanaheshimika sana, wana nidhamu kubwa sana, wana utii mkubwa sana, hawawezi wakakiuka masharti ya Amiri Jeshi Mkuu. Mkiangalia sehemu yao kubwa wanapelekwa katika maeneo ambayo yana matatizo ya ulinzi na usalama. Hawa Maafisa wa Jeshi walioteuliwa wamekwenda kwenye maeneo yale ambayo yana matatizo makubwa ya usalama. Ukiisoma ile Sheria ya Tawala za Mikoa unaona kabisa mojawapo ya majukumu yao ni kusimamia ulinzi na usalama katika maeneo yao ya utawala.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 – Wizara ya Fedha na Mipango
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kupata fursa hii ya kuchangia, nikushukuru wewe Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia na nianze kusema tu kwamba naunga mkono hoja hii kwa sababu mbili kubwa zifuatazo; kwanza hoja yenyewe iliyoletwa mbele yetu ya bajeti imeandaliwa vizuri kukidhi matarajio na matakwa ya wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili ni kwamba bajeti ndiyo interface kwa kiingereza, wanaita interface yaani kiunganishi kati ya wananchi na Serikali yao. Kwa hiyo, mkutano wa bajeti ni mkutano muhimu sana na wananchi wanaufuatilia wanataka kuona kile ambacho Serikali iliahidi kinatekelezwa na kwa sababu hiyo mimi naunga mkono hoja hii na ni kwa sababu ya bajeti hakuna mkutano ambao ni mrefu kuliko mikutano yote isipokuwa mkutano wa bajeti. Katiba ambayo imetoa jukumu kwa Wabunge la kuisimamia na kuishauri Serikali inapokuwa inatekeleza wajibu wake pia imetoa jukumu kwa Wabunge kujadili utekelezaji wa kila Wizara wakati wa bajeti na ninawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge, mmefanya kazi kubwa sana ya kuisimamia Serikali yenu na kuishauri ili matarajio ya wananchi mnaowawakilisha yaweze kutekelezwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, muda mfupi uliopita tumewasikiliza Mawaziri wakitoa mchango wao namna gani watatekeleza zile hoja ambazo zimezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge. Kwa hiyo, nichukue fursa hii kuwapongeza sana Waheshimiwa Wabunge.
Mheshimiwa Naibu Spika, imezungumzwa hoja hapa kwamba, kwamba sasa hivi hakuna mgawanyo wa Serikali. Hii siyo kweli kwa sababu sisi wote tuna katiba Ibara ya 4 imeweka mgawanyo wa dola, kuna Serikali, inaitwa vyombo vya utendaji, kuna Bunge na mahakama, halafu Katiba hiyo imeendelea kutoa ufafanuzi wa kazi wa kila mhimili na ndiyo maana leo tuko hapa Bungeni, sisi leo hapa tunajadili bajeti ya Serikali na ndiyo jukumu la Bunge, yes hapa atuhumu kwa sababu hukumu ni mambo ya mahakama.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia Bunge hili unaweza kujiuliza, kama Katiba imeweka utaratibu katika Ibara ya 26 kwamba kila mmoja lazima aifuate na kutii Katiba hii na sheria za nchi na kwamba imetoa fursa mtu yeyote kwenda mahakamani kulinda hifadhi ya Katiba na sheria hiyo iweje leo iseme kwamba kama kungekuwa na hiyo fursa yenyewe au mwanya au viashiria tu kwamba sasa mgawanyo wa madaraka katika hii mihimili mitatu imevunjwa mpaka sasa hivi hakuna kesi yoyote iliyokwishakufunguliwa mahakamani na kwa hiyo, kama kungekuwa na viashiria hivyo mtu yeyote ana haki ya kwenda mahakamani. Kwa hiyo, hii ni hoja ambayo haina msingi na haiwezi ikawa na maana tu kwa sababu kwamba hakuna matangazo ya hadharani.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshasema ndani ya Bunge hili kwamba Ibara ya 100 imetoa huru na haki kwa Wabunge huru wa kujadili bila hata mipaka yoyote, siyo uhuru wa kutangazwa, haiwezekani yasipokuwa matangazo ya moja kwa moja ukasema kwamba madaraka ya Bunge yanapokwa au Wabunge wanazuiliwa kujadili, Wabunge wangeweza kuwa wanazuiliwa kujadili leo wasingeweza kujadili wakaishauri Serikali mpaka Serikali ikatoa maelezo kiasi hiki. Ninaloweza kusema pia kwamba kumekuwepo na hoja hapa kwamba Bunge limegeuzwa kuwa rubber stamp haiwezekaniki, kwa sababu kwanza mfumo wenyewe Bunge ambalo limepewa mamlaka kwa niaba ya wananchi kuisimamia Katiba litawezaje kuwa rubber stamp haiwezekaniki kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha pili kwa hiyo Serikali haiwezi ikapitisha bajeti yake bila Bunge kushiriki na kuamua kwa hiari yao. Lakini mfumo wenyewe wa maandalizi ya bajeti na utendaji wa Serikali ni kwamba ni shirikishi kwanza unaona katika Katiba yenyewe Ibara ya 63(2)(3) lakini pia sheria kwa sababu hiyo ikatungwa sheria ya bajeti na Sheria ya Bajeti ni shirikishi na kanuni zenyewe unaweka ushirikishi kati ya Serikali na Wabunge kuhusu bajeti. Kwa hiyo, kifungu cha tano na cha sita kinatoa mamlaka kwa mfano kifungu cha tano fiscal policy object, halafu cha sita microeconomic policies na kifungu cha saba kinasema kutakuwa na uanishaji wa mpango mfupi na mpango mrefu na bajeti sasa inaandaliwa kwa ajili ya mpango wa mwaka mmoja, mmoja. Kwa hiyo, bajeti katika mpango ambao umegawanyika katika kipindi cha mpango mrefu wa miaka mitano inakuja kutekelezwa kupitia mpango wa mwaka mmoja ambao ndiyo unaandaliwa bajeti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana nahoja za Wabunge wana kiu kwa ajili ya maendeleo ya majimbo yao kwa sababu ndiyo hasa, lakini pia kuwakumbusha tu ni kwamba kiu itatimizwa au itakidhiwa haja pale ambapo kila mwaka tunaleta mapendekezo kwa ajili ya utekelezaji huo. Kwa hiyo, yale ambayo hayakutekelezwa mwaka huu yatatekelezwa mwaka mwingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo niseme tu kwamba kanuni zenyewe zinaweka ushirikishi na Bunge lenyewe limepewa mamlaka chini ya kifungu cha nane na Kamati ya Bajeti imepewa mamlaka chini ya kifungu cha tisa namna ya kuangalia hivyo. Kwa hiyo, hoja ya kwamba Bunge limebaki rubber stamp haiwezekani ikawa ni ya kweli. Kwa hiyo, mimi nimeshiriki mle kwenye Kamati ya Bajeti, nimeshiriki humu Bungeni mnajua mimi siyo Mbunge mtoro, nakuwepo karibu muda wote humu ndani nimeona jinsi ambavyo Wabunge wamechangia sana, wameshauri Serikali yao na Serikali imeitikia vizuri, tumempigia makofi mengi sana hapa Mheshimiwa Mwijage muda mfupi uliopita kuonyesha kwamba Wabunge wametekeleza sana jukumu lao la Kikatiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na nikushukuru Mheshimiwa Naibu Spika na hili ni la msingi sana, kwenye jambo la msingi sana kama la bajeti linalowaunganisha wananchi na Serikali yao ambayo ndiyo interface yao, Bunge hili linahitaji kwa kweli kuendeshwa kwa namna ambayo italiwezesha Bunge lifanikishe utekelezaji wa majukumu yake. (Makofi)
Kwa hiyo, tunapofanya maamuzi haya chombo kinachoendeshwa kwa majadiliano kinahitaji kizingatie Katiba, sheria na kanuni zilizojiwekea. Kwenye hili mimi nakuomba na umefanya vizuri sana kuendelea kulisimamia hivi vizuri kusudi matarajio ya wananchi yaweze kutekelezwa, tunafanya reform ambazo lazima ziendane na kuzingatia Katiba na sheria za nchi. Mwanasheria Mkuu wa Serikali wakati hoja ya kumthibitisha Waziri Mkuu alisema juu ya umuhimu wa kuzingatia Katiba na sheria tunapotekeleza majukumu yetu hapa. Kwa hiyo, mimi naomba sana usikatishwe tamaa, umefanya vizuri na ndio maana Bunge hili linakuja na mapendekezo mazuri sasa. Bunge kama hili la bajeti ambalo ndiyo kiungo cha wananchi na Serikali yao likianza kuvurugwa matarajio ya wananchi yanaenda wapi? Kwa hiyo, usikate tamaa, uwezo unao, nia ya kufanya vizuri unayo na sababu za kuongoza Bunge hili unalo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru nami niweze kuchangia, kwa mara nyingine tena nimshukuru Mwenyezi Mungu. Kwanza naunga mkono hoja iliyoko katika meza yako. Naomba nitoe ufafanuzi wa mambo mawili matatu ambayo yamezungumzwa hapa. Hoja ya kwanza ni iliyoletwa na Mheshimiwa Esther Matiko kuhusu uhifadhi na utunzaji wa watoto walioko magerezani.
Sheria ya Mtoto, The law of the Child ya Mwaka 2009, katika kifungu cha 144 inaeleza namna gani mtoto aliyeko gerezani kwa sababu amekwenda kule na mama yake au na mzazi, anavyopaswa kutunzwa. Naomba niisome sheria yenyewe na ambacho tumefanya katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, kwa sababu ya umuhimu wa sheria hii, tuliamua kuitafsiri, kwa hiyo, iko kwa Kiswahili. Ni sheria muhimu sana na naomba Waheshimiwa Wabunge mtafute hii sheria muisome, itatusaidia sana kwenye maeneo yetu kule tunapokuwa tunaongelea haki za watoto, haki za Watoto wanaoshtakiwa Mahakamani, walioko mbele za Polisi na hawa ambao sasa wanakwenda magerezani wakiwa na mama zao au wamezaliwa kule magerezani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kifungu cha 144 cha sheria hii kinasema hivi:-
(i) Pale ambapo mama atakuwa gerezani na mtoto wake katika mazingira yoyote yale, hatua zote zitachukuliwa na uongozi wa magereza kuhakikisha kuwa mtoto anapata matunzo yanayohitajika kutoka kwa mama inavyostahili, mlo kamili, virutubisho na huduma ya afya pamoja na chanjo.
(ii) Uongozi wa Magereza utamfahamisha Afisa Ustawi wa Jamii wa Wilaya kuhusu mtoto aliye gerezani na mama yake na ambaye ameacha kunyonya.
(iii) Endapo Afisa Ustawi wa Jamii amepokea taarifa kutoka katika uongozi wa gerezani, ataamua sehemu stahili ya kumweka mtoto huyo ambayo inaweza kuwa;
(a) Mzazi ambaye hayuko gerezani;
(b) Ndugu;
(c) Mlezi; na
(d) Mtu anayefaa kumlea huyo Mtoto.
(iv) Iwapo watu waliotajwa chini ya Kifungu kidogo cha (3) wanakosekana, Afisa ustawi wa Jamii ataagiza mtoto huyo apelekwe katika makao yaliyothibitishwa hadi hapo mama yake atakapoachiliwa kutoka gerezani
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, utakuta sheria imeweka utaratibu na mwongozo mzuri. Inawezekana kukawa na changamoto Waheshimiwa Wabunge mnapokwenda kule mnazipata, haya basi mzijulishe mamlaka zinazohusika ili hatua zile zirekebishwe. Magereza wenyewe wana utaratibu mzuri sana wa kuwaangalia hawa watoto wadogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ambalo ningeomba kushauri, hili ni wajibu wa kikatiba wa kila mwananchi. Ibara ya 26 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania naomba kuisoma tu hii inasema hivi: “Kila mtu ana wajibu wa kuifuata na kuitii katiba hii na sheria za Jamhuri ya Muungano.” Sasa Bunge hili na lenyewe linaongozwa na katiba, sheria na kanuni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika chombo kama hiki ambacho kinafikia maamuzi yake kwa majadiliano, maana maamuzi hapa yanafikiwa baada ya kujadiliana, inafaa sana zile sheria ambazo tumejiwekea za kuongoza majadiliano humu ndani ili tufikie Maamuzi ziheshimiwe sana na sheria zenyewe kwanza ni Katiba yenyewe; pili, sheria ya haki na kinga za Bunge, tatu na kanuni hizi ambazo zinatungwa kwa mujibu wa ibara ya 89, tukifanya hivi, Waheshimiwa Wabunge shughuli zetu hapa zitafanyika kwa amani, kwa hekima kubwa, kwa ufanisi mkubwa, kila tunachotaka kuishauri Serikali kitafika kwa wakati maana hakutakuwa na kuingiliana na Serikali itachukua hatua kukifanyia kazi. Huo ndiyo ushauri wangu, vinginevyo hakuna mtu ambaye yuko juu ya sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili naona niliomba nilifafanue kusudi turudi katika utamaduni wa Bunge hili wa kufanya shughuli zetu kwa amani, kwa ufanisi, kwa kuzingatia katiba na sheria na kanuni ambazo tumejiwekea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu na la mwisho ambalo ningeomba kushauri hapa, Jeshi la Polisi mimi nafanya nalo kazi, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali inafanya kazi kwa karibu sana na Jeshi la Polisi. Ni jeshi ambalo linafanya kazi kwa ufanisi mkubwa sana kuhakikisha kwamba amani na usalama katika nchi hii vinaendelea kuwepo. Unaweza ukawepo upungufu kwa baadhi ya askari, lakini haiwezi ikachukuliwa kwamba ni jeshi lote na haiwezi kuwa kwamba, kama wote hawa wangekuwa ni wala rushwa, kama wote hawa wangekuwa wameshiriki ku-league uchaguzi, basi baadhi ya Wabunge leo wasingekuwa humu ndani ya Bunge hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilifahamishe Bunge lako Tukufu, baada ya Uchaguzi Mkuu kulikuwa na mashauri 52 ya uchaguzi ambayo yamefunguliwa lakini katika mashauri yote hayo wako wa Chama cha Mapinduzi, wako wa Vyama vya Upinzani CHADEMA, CUF na NCCR, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imewatetea na sasa mashauri 39 yameshamalizika Mahakamani. Kwa hiyo, kama kuna kasoro zimetokea hoja siyo kuleta humu Bungeni, kwa mfano, aliyosema Mheshimiwa Lwakatare kama kungekuwa na shida pale hoja ingekwenda mahakamani pale, lakini hakuna hata election petition kutoka kwenye lile Jimbo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba kushauri kwamba, Waheshimiwa Wabunge tujizuie sana kutoa majumuisho ya jumla jumla ya kulaumu jeshi kwamba linafanya hivi, linafanya hivi, lazima tuishi tu kwa kuzingatia sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga hoja mkono. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi ninashukuru kwa kunipatia fursa hii niweze kuchangia. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kuchangia hoja hii na nianze kwa kusema kwamba naunga mkono hoja hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hoja hii ina- cut across kwenye Wizara nyingi ndani ya Serikali naomba kuwashauri Wabunge wote wakubali kuliko kumbana Waziri tu, kwa sababu hapo yapo ya Wizara ya Katiba na Sheria, yapo ya Ardhi, yapo ya Nishati na Madini, yako ya Kilimo na Mifugo. Leo Waziri anaonekana hapa anaongelea haya lakini peke yake hayawezi akayatatua. Kwa hiyo, kwa sababu Waheshimiwa Wabunge wamezungumza kwa uchungu na wametoa ushauri mzuri sana kwa Serikali naomba tumuunge mkono Mheshimiwa Waziri ili aweze kuyatekeleza haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kushauri juu ya mambo matatu hivi ambayo yamezungumzwa hapa ya kisheria. Kwanza baadhi ya Wabunge wamezungumza mambo ambayo yanagusa utendaji wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa maamuzi yanayofanywa na Mawakili wa Serikali walioko kwenye Mikoa. Naomba kushauri mambo mengine muwe mnanishirikisha tu kule tunayamaliza, nawaomba Wabunge hawa waniletee hizo taarifa ili tuchukue hatua, inarahisisha zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni hili ambalo limezungumzwa juu ya huu mkataba mbovu wa Kiwanda cha Mgololo (Mgololo Paper Mills), hili naomba kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba nimeagiza waniletee ule mkataba kwenye Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ili tushirikiane ndani ya Serikali kuangalia kama kweli kuna maeneo ambayo ni mabovu yanaweza kuboreshwa tuyafanyie kazi. Kwa sababu mikataba hii yote kwa kawaida huwa ina vipengele vya marekebisho ya mikataba ile kila wakati inapotokea. Ninawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa kuleta taarifa hiyo humu ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ninaomba kulitolea ufafanuzi ni jambo ambalo limezungumzwa kwa hisia nzuri na kwa ushauri kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge. Hili suala ni la taarifa ya Tume ya Uchunguzi na asili ya taarifa hii ni kwamba kulikuwa na Kamati Teule ya Bunge, Kamati Teule ya Bunge iliundwa kuchunguza juu ya Operesheni Tokomeza na moja wapo ya maazimio ya Bunge ilikuwa ni kwamba Serikali iunde Tume ya Uchunguzi ili kulichunguza hili suala. Kwa mujibu wa sheria ya Tume za Uchunguzi Sura ya 32 ya Sheria za Tanzania, anaeunda Tume hii kwa mujibu wa kifungu cha tatu ni Rais wa Jamhuri ya Muungano na ndiyo anaipatia Tume hii hadidu za rejea. Rais wa Jamhuri ya Muungano aliunda Tume hii kupitia Government Notice Na. 132 ya tarehe 2 Mei, 2014 akaipa hadidu za rejea na ika-report kwake mwezi wa nane, pia akatoa maamuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maamuzi kwa mujibu wa Kifungu cha 21 cha Sheria hii kinaeleza hivi;
“Baada ya kupokea ripoti ya Kamishna wa Uchunguzi Rais anaweza;
(a) Endapo Rais atajiridhisha kuwa upelelezi zaidi unaweza kufanyika au mashtaka kufunguliwa atamuelekeza Mkurugenzi wa Mashtaka kulishauri Jeshi la Polisi kuhusu utaratibu unaopaswa kufanyika au kuelekeza yafunguliwe mashitaka yanayostahili;
(b) Endapo Rais atakuwa na maoni kwamba hatua nyingine stahili zinapaswa kuchukuliwa dhidi ya mtu au watu ataamuru kwamba hatua hizo zichukuliwe.
(2) Pale ambapo itagundulika kuwa kulikuwa na hasara baada ya uchunguzi uliotokana na mwenendo wa mtu yeyote Rais anaweza kuamuru mtu anayehusika kulipa fidia kwa kiasi ambacho Waziri atathibitisha kuwa ni kiasi hicho kinachostahili.
(3) Rais anaweza kuelekeza kwamba taarifa yoyote ya Kamishna izuiliwe kutangazwa au izuiliwe kwa muda ambao Rais ataelekeza.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala hili Rais ameelekeza kwa taasisi zote ambazo watendaji wake wamethibitika kutenda makosa au kukiuka sheria au utaratibu zote za utelekezaji wa Operesheni Tokomeza kuwachukulia hatua kwa mujibu wa sheria. Aidha, kuzifanyia marekebisho sheria na kanuni zilizopendekezwa kufanyiwa marekebisho. Sasa kwa kuwa hatua ambazo zimechukuliwa na Rais kwa kuelekeza taasisi mbalimbali za Serikali zinahusisha uchunguzi, siyo vyema suala hili likatolewa taarifa hadharani katika kipindi hiki na sheria inamruhusu Rais nimewasomea hiki kifungu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo siyo vyema na kwanza hii sio Taarifa ya Bunge ni Taarifa ya Rais, tuipe Serikali fursa aifanyie kazi haya mambo haya la sivyo tutaharibu hata uchunguzi na kile ambacho Waheshimiwa Wabunge wanataka kukifikia hawatakifikia. Huo ndiyo ushauri wangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo naomba kulitolea ushauri ni hili ambalo limezungumzwa juu ya kesi ya Kamran. Kamran na wenzake watumishi wa Serikali walishitakiwa kwenye Kesi ya Uhujumu Uchumi Na. 4 ya mwaka 2011 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi. Tarehe 5 Disemba, 2014 Kamran alitiwa hatiani akiwa hayupo kwa sababu yeye alipopewa dhamana alitoroka, lakini wale wenzake watatu waliachiwa hawakuonekana na hatia. Serikali imekata rufaa katika shauri la rufaa namba moja la 2016 Mahakama Kuu Moshi, kesi hiyo ya rufaa inasikilizwa kesho Moshi.
Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge naomba kuwaambia kwamba Serikali imechukua hatua lakini cha pili suala hili lipo Mahakamani nawapa hizo taarifa kesi hii ya rufaa ya Serikali dhidi ya hawa watu inasikilizwa kesho Moshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine sambamba na hili ni kwamba hatukukaa tu hivi pale, kulikuwa pia na watumishi wengine halafu pamoja na huyu Kamran Ahmed. Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imechukua hatua, imeomba Serikali ya Pakstan katika utaratibu unaoitwa mutual legal assistance watuasaidie mambo fulani kuhusiana na tukio husika ili tuchukue hatua zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii pia Serikali inachukua hatua naomba kuwatoa wasiwasi Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali hii iko makini inajali maslahi ya wananchi kama ambavyo mnaishauri hapa, mtupe fursa tutekeleze yale ambayo tunaweza kuyatekeleza mambo mengine hayana shortcut, hatuwezi kuchukua bunduki tukailazimisha Serikali ya Pakstani itupatie vitu fulani ambavyo walikusudia kutupatia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoa ushauri huo naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kupata fursa ya kuchangia jioni hii kwenye hoja hii muhimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nikushukuru kwa kunipa fursa hii nami niweze kuchangia. Nichukue fursa hii pia kukupongeza kwa kazi nzuri unayofanya ndani ya Bunge hili, ili kuwezesha chombo hiki muhimu ambacho kimepewa jukumu kwa niaba ya wananchi, kuisimamia na kuishauri Serikali kitekeleze majukumu yake ya Kikatiba ipasavyo, kiweze kufanya majukumu yake kwa kuzingatia Sheria, Katiba na Kanuni kilichojiwekea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, siku moja niliwahi kushauri hapa kwamba, chombo kama hiki, ambacho kinafikia maamuzi yake kwa majadiliano ni lazima kiheshimu Katiba, Kanuni na Sheria zinazotawala katika uendeshaji wa shughuli za chombo hicho. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja iliyoko mbele ya meza yako Tukufu na nampongeza Mheshimiwa Waziri na Wizara nzima kwa kuleta hoja hii mbele ya Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeombwa kuchangia ili kueleza mambo machache ya Kikatiba na Kisheria, ambayo yamejili katika michango ya Waheshimiwa Wabunge, ambao nao nawapongeza kwa michango yao ya kuboresha Hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza ni hili linalohusu Sheria za Mifuko ya Hifadhi za Jamii, kuhusu mapendekezo ya kurejesha au kuwa na fao la kujitoa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kusema tu kwamba, mafao ya wafanyakazi yanasimamiwa na Sheria za Mifuko ya Jamii na Sheria hizo ni Sheria ya Mfuko wa Mafao ya Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Sheria ya Mfuko wa Mafao ya Serikali za Mitaa (LAPF), Sheria ya Mfuko wa Mafao ya Mashirika ya Umma (PPF), Sheria ya Mfuko wa Mafao ya Utumishi wa Umma (PSPF) na Sheria ya Mfuko wa Mafao wa GEPF.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa msingi wa mafao haya ya watumishi wa umma ni katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ibara ya 11 ya Katiba hii, Mheshimiwa naomba uniruhusu niisome, hii ndiyo inaweka msingi wa mafao hayo ya watumishi wa umma na yenyewe inasema hivi:-
Mamlaka ya Nchi itaweka utaratibu unaofaa kwa ajili ya kufanikisha utekelezaji wa haki ya mtu kufanya kazi, haki ya kujipatia elimu na haki ya kupata msaada kutoka kwa jamii wakati wa uzee, maradhi au hali ya ulemavu na katika hali nyinginezo ambazo mtu huwa hajiwezi.
Mheshimiwa Naibu Spika, huo ndio msingi wa mafao haya ya wafanyakazi hawa. Sasa sheria tulizonazo zimegawanyika kwenye makundi mawili; Sheria ya LAPF na Sheria ya PSPF, zenyewe bado zinalo fao la kujitoa, lakini Sheria ya NSSF, Sheria ya PPF na Sheria ya GEPF haina fao la kujitoa. Sasa kumekuwa na hoja kwamba, labda kama kuondolewa kwa fao hilo la kujitoa kunavunja Katiba ya nchi?
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kusema kwamba, kwanza hizi Sheria, ambazo hazina fao la kujitoa ndizo zinazozingatia matakwa ya Katiba ya nchi, lakini pia suala hili liliwahi kufikishwa mahakamani. Mahakama ya Rufaa katika shauri la rufaa namba 105 (consolidated civil appeal) namba 105 na 81 za mwaka 2006, kati ya Nassoro Athuman Gogo na James William Lugiana, wakiwakilisha wenzao 2,487 liliamua kwamba, Sheria ya PPF iliyokuwa haina fao hilo la kujitoa ilikuwa haivunji Katiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, huu ndiyo ushauri wangu, ndiyo msimamo wa Katiba, ndiyo msimamo wa Sheria kwenye masuala haya. Lakini Bunge linaweza kufanya maamuzi, maamuzi ambayo lakini pia linapoyafanya lazima lizingatie Katiba na maamuzi ya Mahakama ya Rufaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni hili ambalo limezungumzwa kuhusu suala la kampuni moja inaitwa Quality Plaza, kwa sababu nimeliona hapa, halikuzungumzwa hadharani. Mashauri yako mahakamani yanayohusu masuala haya na yameshasikilizwa na inasubiriwa tu sasa kutolewa hukumu. Kulikuwa na mashauri mengi na vyema niyataje tu mashauri haya, lakini sitaenda ndani kwa sababu suala liko mahakamani.
Mheshimiwa Naibu Spika, moja, kulikuwa na shauri namba 33 la mwaka 2009 Mahakama Kuu, shauri namba 40 la mwaka 2011 Mahakama Kuu, shauri namba 59 la mwaka 2012 Mahakama Kuu, shauri namba 77 la mwaka 2012 Mahakama Kuu. Hata hivyo, baadaye mashauri yote haya yaliunganishwa kwa pamoja yakawa consolidated kwamba ni shauri namba 33 la mwaka 2009 kwa sababu yote ni ya migogoro ya upangaji. Shauri hili limesikilizwa, linasubiriwa tu kutolewa hukumu na kwa sababu hiyo hatuwezi kulijadili hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hata hivyo, Quality Plaza walifungua shauri namba 97 la mwaka 2015 walipotakiwa kuhama na liko mahakamani, hatuwezi kuyaongelea hapa. Kwa hiyo, ndiyo niliona kwamba, niyaseme hivi, lakini ukweli ni kwamba, PSPF imekuwa ikichukua hatua za kuhakikisha kwamba, inalinda maslahi kwenye pango hili isipokuwa kama tu kwa sababu ya technicalities za mahakama.
Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu, ambalo naomba kuliongea ni hili suala la chombo kinachoitwa Financial Intelligence Unit. Naomba kulifahamisha Bunge lako Tukufu kwamba, mwaka 2014 ndugu George Mcheche Masaju, wakati huo akiwa Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali aliiwakilisha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Taasisi moja ya masuala ya kifedha duniani inaitwa Financial Action Task Force. Tanzania ilikuwa imekuwa blacklisted for almost five years, kwamba tuna mifumo dhaifu ya kupambana na utakatishaji wa fedha haramu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi Januari, mwaka 2014, nikatumwa Paris kwenye Financial Action Tax Force, nikaitetea wale wakubwa wakaridhika. Mwezi wa Nne wakaja kufanya On site visit Inspection, wajiridhishe na mifumo yetu ya Sheria, wakaridhika. Mwezi wa Saba, 2014, Tanzania ikaondolewa katika lile kundi la nchi ambazo zina mifumo dhaifu ya udhibiti wa fedha haramu na vitendo vya ugaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Tanzania ina mifumo imara ya kisheria ya kudhibiti vitendo vya utakatishaji wa fedha na ugaidi. Na ni kwa sababu hiyo pia, imejiunga na Egmont Group, ambayo ni jumuiya ya Taasisi hizi za Financial Intelligence Unit, hilo la kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kumekuwa na hoja kwamba, Financial Intellegence Unit ya Tanzania ilipaswa iwe na mamlaka ya kuchunguza kama zilivyo mamlaka nyingine. Haiwezekani! Yenyewe hii, kuna makundi matatu ya hizi Financial Intelligence Unit.
Mheshimiwa Naibu Spika, moja ni Administrative kama ya kwetu hii, ya kiutawala. Yenyewe inapata taarifa hizi, inazipeleka kwenye vyombo vya uchunguzi kama Polisi, PCCB na Taasisi nyingine halafu na Vyombo vya mashtaka. Pia, kuna kundi la pili linaitwa Investigative Financial Intelligence Unit, hii inakuwa na mamlaka yenyewe ya kuchunguza, inachunguza tu, lakini inapeleka kwenye vyombo vingine vya mashtaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kundi la tatu ambalo ni Hybrid lenyewe linachunguza na kushtaki. Mifumo yote hii mitatu imekubaliwa katika kundi hili la Egmont Group na ndiyo maana sisi tulijiunga mwaka jana kwenye hii Egmont Group kwamba tuna sifa zote za kutekeleza hayo. Kinachozingatiwa zaidi kwenye hizi financial intelligence ni kwamba; je, hizi Taasisi ni huru? Hilo la kwanza. La pili, zina uwezo wa kuchunguza na kujiridhisha kufanya focused investigation ikiwa ni pamoja na kushirikiana na Taasisi nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba kushauri tu kwamba, hii Taasisi ya Financial Intelligence Unit iliyopo hapa kwetu, kwa sababu tu yenyewe haichunguzi au kwamba, haipeleki mashtaka mahakamani kwamba, basi ni dhaifu, hapana. Ndivyo ilivyo na ni utaratibu katika dunia kwa haya makundi matatu na sisi tunaingia kwenye kundi hilo, hakuna matatizo mengine yoyote.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niseme tu kwamba, naunga mkono hoja kama ambavyo nilishaongea tokea mwanzo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kupata fursa hii ya kuchangia, nikushukuru wewe Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia na nianze kusema tu kwamba naunga mkono hoja hii kwa sababu mbili kubwa zifuatazo; kwanza hoja yenyewe iliyoletwa mbele yetu ya bajeti imeandaliwa vizuri kukidhi matarajio na matakwa ya wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili ni kwamba bajeti ndiyo interface kwa kiingereza, wanaita interface yaani kiunganishi kati ya wananchi na Serikali yao. Kwa hiyo, mkutano wa bajeti ni mkutano muhimu sana na wananchi wanaufuatilia wanataka kuona kile ambacho Serikali iliahidi kinatekelezwa na kwa sababu hiyo mimi naunga mkono hoja hii na ni kwa sababu ya bajeti hakuna mkutano ambao ni mrefu kuliko mikutano yote isipokuwa mkutano wa bajeti. Katiba ambayo imetoa jukumu kwa Wabunge la kuisimamia na kuishauri Serikali inapokuwa inatekeleza wajibu wake pia imetoa jukumu kwa Wabunge kujadili utekelezaji wa kila Wizara wakati wa bajeti na ninawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge, mmefanya kazi kubwa sana ya kuisimamia Serikali yenu na kuishauri ili matarajio ya wananchi mnaowawakilisha yaweze kutekelezwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, muda mfupi uliopita tumewasikiliza Mawaziri wakitoa mchango wao namna gani watatekeleza zile hoja ambazo zimezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge. Kwa hiyo, nichukue fursa hii kuwapongeza sana Waheshimiwa Wabunge.
Mheshimiwa Naibu Spika, imezungumzwa hoja hapa kwamba, kwamba sasa hivi hakuna mgawanyo wa Serikali. Hii siyo kweli kwa sababu sisi wote tuna katiba Ibara ya 4 imeweka mgawanyo wa dola, kuna Serikali, inaitwa vyombo vya utendaji, kuna Bunge na mahakama, halafu Katiba hiyo imeendelea kutoa ufafanuzi wa kazi wa kila mhimili na ndiyo maana leo tuko hapa Bungeni, sisi leo hapa tunajadili bajeti ya Serikali na ndiyo jukumu la Bunge, yes hapa atuhumu kwa sababu hukumu ni mambo ya mahakama.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia Bunge hili unaweza kujiuliza, kama Katiba imeweka utaratibu katika Ibara ya 26 kwamba kila mmoja lazima aifuate na kutii Katiba hii na sheria za nchi na kwamba imetoa fursa mtu yeyote kwenda mahakamani kulinda hifadhi ya Katiba na sheria hiyo iweje leo iseme kwamba kama kungekuwa na hiyo fursa yenyewe au mwanya au viashiria tu kwamba sasa mgawanyo wa madaraka katika hii mihimili mitatu imevunjwa mpaka sasa hivi hakuna kesi yoyote iliyokwishakufunguliwa mahakamani na kwa hiyo, kama kungekuwa na viashiria hivyo mtu yeyote ana haki ya kwenda mahakamani. Kwa hiyo, hii ni hoja ambayo haina msingi na haiwezi ikawa na maana tu kwa sababu kwamba hakuna matangazo ya hadharani.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshasema ndani ya Bunge hili kwamba Ibara ya 100 imetoa huru na haki kwa Wabunge huru wa kujadili bila hata mipaka yoyote, siyo uhuru wa kutangazwa, haiwezekani yasipokuwa matangazo ya moja kwa moja ukasema kwamba madaraka ya Bunge yanapokwa au Wabunge wanazuiliwa kujadili, Wabunge wangeweza kuwa wanazuiliwa kujadili leo wasingeweza kujadili wakaishauri Serikali mpaka Serikali ikatoa maelezo kiasi hiki. Ninaloweza kusema pia kwamba kumekuwepo na hoja hapa kwamba Bunge limegeuzwa kuwa rubber stamp haiwezekaniki, kwa sababu kwanza mfumo wenyewe Bunge ambalo limepewa mamlaka kwa niaba ya wananchi kuisimamia Katiba litawezaje kuwa rubber stamp haiwezekaniki kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha pili kwa hiyo Serikali haiwezi ikapitisha bajeti yake bila Bunge kushiriki na kuamua kwa hiari yao. Lakini mfumo wenyewe wa maandalizi ya bajeti na utendaji wa Serikali ni kwamba ni shirikishi kwanza unaona katika Katiba yenyewe Ibara ya 63(2)(3) lakini pia sheria kwa sababu hiyo ikatungwa sheria ya bajeti na Sheria ya Bajeti ni shirikishi na kanuni zenyewe unaweka ushirikishi kati ya Serikali na Wabunge kuhusu bajeti. Kwa hiyo, kifungu cha tano na cha sita kinatoa mamlaka kwa mfano kifungu cha tano fiscal policy object, halafu cha sita microeconomic policies na kifungu cha saba kinasema kutakuwa na uanishaji wa mpango mfupi na mpango mrefu na bajeti sasa inaandaliwa kwa ajili ya mpango wa mwaka mmoja, mmoja. Kwa hiyo, bajeti katika mpango ambao umegawanyika katika kipindi cha mpango mrefu wa miaka mitano inakuja kutekelezwa kupitia mpango wa mwaka mmoja ambao ndiyo unaandaliwa bajeti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana nahoja za Wabunge wana kiu kwa ajili ya maendeleo ya majimbo yao kwa sababu ndiyo hasa, lakini pia kuwakumbusha tu ni kwamba kiu itatimizwa au itakidhiwa haja pale ambapo kila mwaka tunaleta mapendekezo kwa ajili ya utekelezaji huo. Kwa hiyo, yale ambayo hayakutekelezwa mwaka huu yatatekelezwa mwaka mwingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo niseme tu kwamba kanuni zenyewe zinaweka ushirikishi na Bunge lenyewe limepewa mamlaka chini ya kifungu cha nane na Kamati ya Bajeti imepewa mamlaka chini ya kifungu cha tisa namna ya kuangalia hivyo. Kwa hiyo, hoja ya kwamba Bunge limebaki rubber stamp haiwezekani ikawa ni ya kweli. Kwa hiyo, mimi nimeshiriki mle kwenye Kamati ya Bajeti, nimeshiriki humu Bungeni mnajua mimi siyo Mbunge mtoro, nakuwepo karibu muda wote humu ndani nimeona jinsi ambavyo Wabunge wamechangia sana, wameshauri Serikali yao na Serikali imeitikia vizuri, tumempigia makofi mengi sana hapa Mheshimiwa Mwijage muda mfupi uliopita kuonyesha kwamba Wabunge wametekeleza sana jukumu lao la Kikatiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na nikushukuru Mheshimiwa Naibu Spika na hili ni la msingi sana, kwenye jambo la msingi sana kama la bajeti linalowaunganisha wananchi na Serikali yao ambayo ndiyo interface yao, Bunge hili linahitaji kwa kweli kuendeshwa kwa namna ambayo italiwezesha Bunge lifanikishe utekelezaji wa majukumu yake. (Makofi)
Kwa hiyo, tunapofanya maamuzi haya chombo kinachoendeshwa kwa majadiliano kinahitaji kizingatie Katiba, sheria na kanuni zilizojiwekea. Kwenye hili mimi nakuomba na umefanya vizuri sana kuendelea kulisimamia hivi vizuri kusudi matarajio ya wananchi yaweze kutekelezwa, tunafanya reform ambazo lazima ziendane na kuzingatia Katiba na sheria za nchi. Mwanasheria Mkuu wa Serikali wakati hoja ya kumthibitisha Waziri Mkuu alisema juu ya umuhimu wa kuzingatia Katiba na sheria tunapotekeleza majukumu yetu hapa. Kwa hiyo, mimi naomba sana usikatishwe tamaa, umefanya vizuri na ndio maana Bunge hili linakuja na mapendekezo mazuri sasa. Bunge kama hili la bajeti ambalo ndiyo kiungo cha wananchi na Serikali yao likianza kuvurugwa matarajio ya wananchi yanaenda wapi? Kwa hiyo, usikate tamaa, uwezo unao, nia ya kufanya vizuri unayo na sababu za kuongoza Bunge hili unalo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kupata fursa hii ya kuchangia kwenye hoja hizi mbili muhimu. Nikushukuru wewe kwa kunipa fursa na pia niwashukuru Wenyeviti wa Kamati hizi mbili kwa taarifa zao muhimu sana wakati Bunge linapotekeleza jukumu lake la kikatiba la kuishauri na kuisimamia Serikali. Mimi kwa moyo mmoja niseme kwamba naunga mkono hoja za Kamati hizi mbili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilichosemwa katika taarifa hizi zote mbili ni cha kweli. Nilikuwepo wakati Mheshimiwa Shangazi anachangia kilichojiri juu ya hadhi na mazingira ya kazi katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali alipokuwa anazungumza kuhusu Mbunge mmoja aliyezimia alisema ni Wizara ya Katiba lakini ukweli ilikuwa ni Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Kwa hiyo, hii inaonesha ni kwa kiasi gani hizi taarifa zimezungumza ukweli. Nami niungane na Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamepata fursa ya kuchangia hapa kuisaidia Serikali iweze kutekeleza majukumu yake ya Kikatiba kwa ufanisi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kushauri, imetolewa hoja kwa mfano juu ya wafungwa wa kunyongwa, wanaitwa condemned kwamba labda wanakaa sana pale na hawanyongwi labda tubadilishe sheria, hapana. Mamlaka haya yapo kwenye Katiba, Ibara ya 45 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ndiyo imempa Rais mamlaka ya kusamehe kosa lolote lile hata hilo la kunyongwa au kuwashushia adhabu. Inategemea kwamba hawa waliotumia fursa yao kutokuwanyonga wametumia mamlaka yao ya Kikatiba halali kabisa. Pia hatuwezi tukafuta hili kwa sababu anaweza akaja Rais mwingine akasema aah aah, hawa wawe wananyongwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie Waheshimiwa Wabunge Law Reform Commission, ile Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania ilishafanya utafiti hii miaka ya karibuni tu kwamba hii adhabu tuiondoe au tusiiondoe? Wananchi walisema hii adhabu ibaki pale. Mahakama ya Rufaa ya Tanzania iliwahi kusema kwamba hii ni adhabu halali kwa hiyo, iko pale. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge wale watu kuwepo pale isitufanye tukawa na nia ya kutaka kurekebisha ile sheria. Hilo la kwanza niliomba nichangie kwenye hilo.Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, imezungumzwa juu ya ukiukwaji wa taratibu na Sheria za Uchaguzi wakati wa uchaguzi wa Madiwani. Wote tunajua utaratibu, kama sheria au utaratibu umekiukwa, ushauri wangu tu ni kwamba yule ambaye anaona taratibu zimekiukwa basi anaweza akaenda Mahakamani akafungua shauri la kupinga matokeo ya uchaguzi. Ndivyo tulivyofanya hata katika uchaguzi mkuu, huo ndiyo utaratibu. Ndiyo ushauri wangu kwenye suala hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo limezungumzwa pia na Mheshimiwa Mussa na amelizungumza kwa hisia, hata mimi linanihusu, linaumiza. Wakati fulani unaenda gerezani unamwona mama ana mtoto mdogo na mimi nimeenda sana magerezani. Nimemsikia Mheshimiwa Mwamoto akizungumzia lile Gereza la Kahama pale, mimi nilienda pale kwa mara ya kwanza Desemba, 2003 nikiwa na Waziri Mwapachu, wakati huo mimi ni msaidizi wake, Mzee Mwapachu alilia machozi kutokana na hali iliyopo pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Serikali imechukua hatua imeboresha hali hii. Kifungu cha 144 cha Sheria ya Mtoto sasa kinaweka utaratibu wa namna gani mama aliye na mtoto gerezani anapaswa atendewe. Siwezi kutafsiri kwa Kiswahili hapa, lakini nisome, kinasema hivi:-
“(1) Where a mother is in prison with her child under any circumstances, all measures shall be taken by the prison authorities to ensure that the child receives the required child care in the form of adequate diet, nutrition and child health care including immunization”.
(2) The prison authorities shall inform the District Social Welfare Officer about the child who is in prison with his mother and who is no longer breastfeeding.
(3) Where the social welfare officer has received information from the prisons authority, he shall determine the most suitable place for the child, which may be –
(a) the parent who is not in prison;
(b) a relative;
(c) a guardian; or
(d) a fit person;
(4) In the absence of persons referred to under subsection (3), the Social Welfare Officer shall cause the child to be admitted in an approved residential home until such times when the mother is discharged from prison.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sheria ya Serikali tayari imeshaweka utaratibu wa aina hiyo. Hata hivyo, tunakubali ushauri ambao umetoka kwa Mheshimiwa Mussa kwenye suala hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo imezungumzwa hapa ni hii hoja ya msongamano wa mahabusu magerezani na ni kweli Wabunge wamesema kwa hisia. Sisi jana tulikuwa pale Dar-es-Salaam kwenye Law Day na ndicho ambacho pia Rais amesisitiza sana. Taasisi za umma ambazo zimepewa majukumu ya kusimamia administration ya justice tutekeleze majukumu yetu kwa ufanisi. Kama ni Mahakama hivyohivyo, kama ni Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ni hivyohivyo, kama ni Jeshi la Polisi hivyohivyo, kama ni Jeshi la Magereza hivyohivyo, kila mmoja awajibike. Kwa hiyo, nakubaliana na Waheshimiwa Wabunge ambao wamesema kuhusiana na suala hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ambalo pengine ningeomba kulichangia, limezungumzwa hapa suala kuhusu kauli za Rais. Kwanza niseme hivi, kwa kuwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano Ibara ya 18(a) inatamka kwamba kila mtu anao uhuru wa kuwa na maoni na kueleza fikra zake; inawezekana kwamba baadhi ya wananchi mara nyingi labda wanatafsiri hizo kauli za Rais kwa sababu ya kutumia haki hii. Nilivyokuwa nasoma Lake Secondary, Mwalimu mmoja alitufanyia zoezi akasema hivi, kadri habari inavyotoka kwa mtu mwingine kwenda kwa mtu mwingine ndivyo inavyobadilika. Akatufanyia zoezi, akamnong‟oneza kitu mwanafunzi wa kwanza kwenye dawati pale, yule wa mwisho kabisa alikuja na taarifa tofauti kabisa na alichoambiwa na Mwalimu na mengine haya huwa tunayasikia wakati hata sisi hatukupata kusikiliza kitu kama hicho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme kwanza Mheshimiwa Rais anatambua na anazingatia mgawanyo wa madaraka kati ya mihimili mitatu ya dola. Pili, anatambua na kuzingatia utawala wa sheria…
Anachokifanya Mheshimiwa Rais ni kuhimiza utawala wa sheria na uwajibikaji wa taasisi na vyombo vya umma na Serikali katika utekelezaji wa majukumu yao na hili ni sharti la msingi.
Kwa sababu hata Ibara ya 26 ya Katiba ndiyo inayoweka utawala wa sheria na ndicho Rais anachosisitiza na hata jana amesisitiza sana na hili lilikuwa liko wazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa hiyo, anachokisisitiza Mheshimiwa Rais ni utawala wa sheria na hata jana amesisitiza sana Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali tekelezeni majukumu yenu kwa ufanisi, Mahakama hivyohivyo, Magereza hivyohivyo, Polisi hivyohivyo, TAKUKURU hivyohivyo. Sasa huyu ndiyo ana mandate, ndiyo Mkuu wa Nchi ana wajibu wa kutusisitizia. Anaposisitiza kauli zake wakati fulani kwa sababu ya uhuru huu wa Kikatiba ya kuwa mtu na fikra na mawazo yake anaweza kuwa ameelewa vibaya akamtafsiri vibaya lakini ukweli ni kwamba Rais bado yuko kwenye Katiba anatekeleza tu wajibu wake kwa ufanisi. Ibara ya tisa inatukumbusha kwamba mamlaka ya nchi na vyombo vyake vyote vinawajibika kuelekeza sera ya shughuli zake zote katika lengo la kuhakikisha kwamba sheria za nchi zinalindwa na kutekelezwa ipasavyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, kwa mara nyingine tena nikushukuru na naunga mkono hoja. Ahsanteni sana.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha na mimi kupata fursa ya kuchangia. Nikushukuru wewe mwenyewe, lakini pia niwashukuru Wenyeviti wa Kamati wa kuwasilisha hizi taarifa zote mbili ambazo ni taarifa muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na niseme tu kwamba na mimi naunga mkono hoja za taarifa zote hizi mbili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, tumepokea ushauri wa Waheshimiwa Wabunge kupitia Kamati yao kuhusu uwepo wa mikataba mibovu na mingine inayodaiwa kuwa mibovu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niliambie Bunge lako Tukufu kwamba tayari Serikali imechukua hatua, inaipitia na inaendelea kupitia mikataba hii na inaendelea kuipitia. Ushauri wangu ni kwa Wabunge, popote pale walipo, wanapopata taarifa za uwepo wa mikataba mibovu basi wawasiliane na Wizara za kisekta ili walete kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali tuzipitie wote kwa pamoja ndani ya Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mikataba yote kwa kawaida huwa na vipengele vya marekebisho (amendment clauses) ndiyo inayotoa fursa kwa wahusika wa mikataba hiyo kuirekebisaha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ambalo naomba kushauri ni hiki ambacho mmeshauri kuhusu Sheria kama ya EWURA na TCRA kutokuwa na utaratibu wa succession plan. Ukweli ni kwamba ziko succession plan, ukisoma jedwali la kwanza la hizi sheria zote mbili, jedwali la pili limeweka muundo wa ile bodi na namna gani ambavyo hawa Wajumbe wanapatikana. Kwa mfano hii ya EWURA, imeweka kwenye Ibara ndogo ya kwanza Chairman anakaa miaka minne, Director General miaka minne, Mjumbe mmoja anakaa miaka mitatu, Wajumbe wawili wanakaa miaka mitano. Halafu ana fursa ya reappointment, na vivyo hivyo hata ya TCRA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia Sheria zote za bodi zinatoa fursa ya reappointment for one more other term, hii yote imewekwa mahsusi kwa ajili ya kuendeleza ile succession plan na institutional memory ya wale wajumbe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ambayo nilikuwa naomba kushauri ni hili suala la Msajili wa Hazina. Ukisoma ile Sheria ya Msajili wa Hazina, kifungu cha 8 na kifungu cha 10 kilifanyiwa marekebisho mwaka 2010 na kupitia Bunge lako Tukufu kupitia Sheria Namba 15 ya mwaka 2015 tumefanya mabadiliko pia kifungu cha 10 tukaongeza 10(a), vifungu vyote hivi vinampa mamlaka Msajili wa Hazina hata kusimamia hii Mifuko ya Hazina kwasababu inataja juu public corporation na statutory corporation havikuiondoa hiyo mifuko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunatambua pia kwamba mifuko hii kuna wasimamizi wengine kama SSRA na Benki Kuu. Tutakachofanya ndani ya Serikali ni kukaa namna gani sasa tumuwekee mipaka huyu Msajili wa Hazina kusudi tusije baadae tukaleta mgongano, lakini kwa ukweli ni kwamba anayo mamlaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nikushukuru tena. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa
Mwenyekiti, kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kunipa fursa na mimi niweze kuchangia hapa. Nakushukuru wewe pia kwa kunipa nafasi hii.

Pia nachukua nafasi hii kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa utendaji wake wa ufanisi uliotukuka sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza na Mawaziri wawili wanaomsaidia na timu nzima ya ofisi yake na watendaji wote kwa hotuba nzuri ambayo imeonesha mambo ambayo Serikali imeyafanya katika mwaka huu na inayokusudia kuyafanya mwaka ujao wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kushauri mambo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili suala la utekaji nyara na mambo ya hofu, yanajitokeza sana hapa na sijui ni kwa nini? Naomba kushauri kwamba polisi waendelee kushirikana na watu walio karibu sana na huyu mtu anayedaiwa amepotea. Waisaidie polisi ili tupate ukweli; kwanza familia yake, watu ambao amekuwa akifanya nao kazi kwa karibu, watoe ushirikiano kama ambavyo Bunge wameshauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala hili hatuwezi kuwa na double standard. Kwa mujibu wa Katiba Ibara ya 26, kila mmoja anawajibika kutii Katiba na sheria ya nchi. Mheshimiwa Mbowe ametusaidia, kwenye hotuba yake amesema hakuna aliye juu ya sheria. Moja, akatueleza tangu huyu mtu anayedaiwa kupotea au kufariki. Alipopotea, ilichukua muda gani kutoa taarifa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu familia au watu waliokuwa karibu na huyu mtu, kwa mfano, wameshapeleka taarifa kwenye vyombo vya habari kwamba huyu mtu labda amepotea, hebu mtu yeyote aliyopo kwenye public atusaidie, then tu-take action accordingly. Mimi ninavyojua polisi ilivyokuwa inafanya kazi, siku hizi wanafanyaje kazi? Sasa hivi tungekuwa na watu wanaisaidia polisi kwa karibu mno! Sasa this is how we can handle this matter so much successful. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabla hatujaenda huko Scotland Yard, watu waliokuwa wanafanya kazi kwa karibu na familia y ake, watoe taarifa, vyombo vyetu vifanyie kazi kwa karibu mno, hilo ni la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, hili siyo suala la uhuru wa mijadala humu Bungeni. Ibara ile ya 100 uisome ina vifungu viwili vidogo; kifungu cha kwanza na cha pili, hata uhuru wa mijadala, haukuwekwa uhuru wa haki ya kuvunja sheria. Ukisoma Ibara ndogo ya (1) na ya (2), unayo hiyo haki tu kama katika mjadala wa kutekeleza majukumu yako ya Kibunge unazingatia Katiba na Sheria za nchi, la sivyo, basi wewe ungekuwa tu unaua mtu, unapiga mtu, unasema mimi nina haki sijui ya nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kushauri tusitumie vibaya uhuru wa mijadala. Hata huku kutangazwa, wanaita matangazo mubashara, someni Ibara ya 100 kama ipo hiyo haki. Someni Sheria ya Haki, Kinga na Mamlaka za Bunge kama ipo hiyo haki ya kutangaza mubashara. Someni Kanuni 143, haki tuliyonayo ni ya Taarifa za Bunge. Ibara ya 18 ya Katiba inatoa haki ya watu kupewa taarifa na mpaka sasa hivi Serikali haijakataza vyombo vya habari kuripoti mambo yanayoendelea humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ngoja niwashauri Waheshimiwa Wabunge, kama mnataka kurudi katika Bunge hili, tetedni mambo yanayowanufaisha wapigakura wenu. Bunge la mwaka 2015 lilikuwa na hiyo live broadcasting, lakini Wabunge wengi hawakurudi. Kitakachowafanya watu wenu wawakubali ni yale mnayotekeleza. Matangazo mubashara hayasaidii chochote, eeh! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu kuna hoja imezungumzwa jana hapa, ni aibu! Unasema Serikali hii inaongozwa na watu wasio competent; how can this be? Serikali ni nini? Huyo Rais mwenyewe amekuwemo Bungeni humu tangu mwaka 1995. Mawaziri wanaomsaidia wengi walikuwepo hapa; sisi watumishi wa umma tumekuwemo humu. Mimi nimeanza kazi mwaka 1994. Kinachobadilika ni wanasiasa; nanyi wenyewe mlienda kwenye kura. Mkashindwanishwa walio na uzoefu na wasio na uzoefu. Walio na uzoefu wakashinda, ndiyo wameunda Serikali, mnasema they are not competent. How can this be? This is not seriously at all, we need to be serious! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyo Rais mnayemsema, mimi nilikuwepo pale Ubungo mwezi jana, siku linawekwa jiwe kwenye ujenzi wa barabara sijui mnaita ya magorofa, yule Rais wa Benki ya Dunia alisema hivi; “mimi nimekuja Tanzania kwa sababu huko duniani viongozi wanasema
nenda Tanzania kwanza.” Hatujisifu! Leo udhaifu wa aina gani? Naweza kusema hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoweza kushauri Bunge lako Tukufu ni kwamba Serikali hii inaongozwa na watu wanaomudu majukumu yao kwa ufanisi ipasavyo na ndiyo maana imeweza kutekeleza mambo hayo katika muda ambao haujafiakia hata miaka miwili na Serikali imeripoti kupita hizi Wizara mbili na Ofisi ya Waziri Mkuu so far na mwenye macho haambiwi tazama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba nimemsikia Mheshimwia amesema huu ushirikiano mnaoutaka Serikali ni lazima uanzie humu Bungeni, uta-extend mpaka kwenye majimbo yenu. Hamwezi mkawatukana Mawaziri hapa, Attorney General mnamtukana, Waziri mnamtukana halafu kesho mnasema aje Jimboni kwako, aje kufanya nini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuwe courtesy. Ni naomba kushauri, Serikali kwa maana ya mihimili yote ya dola, I am talking about the government now.
Executive, Judiciary and Legislation.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba kushauri jambo hili, Serikali kwa maana ya government haiwezi kuruhusu watu wachache wakaharibu mustakabali wa Taifa hili ama kwa vitendo au kwa kauli zao au kwa mienendo zao, ni lazima turudishe nidhamu ndani ya Bunge hili. Ni lazima amani na usalama vitawale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia. Nakushukuru wewe, lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Makamu wa Rais chini ya uongozi mahiri wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Waziri Mkuu na wanavyoshirikiana na Rais Dkt. Mohamed Shein wa Zanzibar kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze sana Waheshimiwa Mawaziri kwa hotuba yao nzuri, ambayo imetoa taarifa ya mambo ambayo yamefanyika mwaka huu na ambayo yanategemewa kufanyika mwaka ujao. Niseme tu kwamba kwa sababu muda ni mdogo, naunga mkono hoja kabla ya muda wangu haujakwisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilifafanue tu kwamba Mheshimiwa Ngwali amezungumza hapa juu ya Sheria ya Mafuta na hili suala la Muungano. Naomba kuwaambieni hapa kwamba moja, Katiba haikuvunjwa wakati tunatunga sheria hii mwaka 2015 na bahati nzuri tulikuwa wote humu wengine wakaamua kuondoka tukabaki na Wabunge wawili wa Opposition. Sheria hii iliyotungwa inazingatia maslahi ya Muungano wa pande zote Zanzibar kama alivyosema Mheshimiwa Nahodha, kwavhiyo tuiunge mkono.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kifungu cha 2 cha Sheria ya Mapato ya Gesi na Petroli hayatoi maelekezo kwamba Bunge la Zanzibar litunge sheria, inasema masuala ya mapato yanayotokana na gesi na petroli yatashughulikiwa kwa mujibu wa sheria zinazotungwa na Zanzibar, ndivyo hali halisi ilivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge naomba kuwatoa wasiwasi tuunge mkono suala hili. Tulichokifanya katika Sheria hii ya Petroli Kifungu cha 4, tulisema kwa sababu hili suala bado liko kwenye Katiba, tuliwekee utaratibu kwamba hili linabaki bado kuwa Jamhuri, lakini tukasema litasimamiwa na Serikali zote hizi mbili. Ukisoma hiki Kifungu ndivyo kilivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kikishasimamiwa na Serikali zote mbili, Katiba ya Zanzibar Ibara 88 inatoa mamlaka kwa Baraza la Wawakilishi kutunga sheria ku-regulate hiki kitu. Kwa hiyo, suala liko kwenye Katiba sawa la Muungano lakini utaratibu wa kushughulikia hayo mapato umewekwa kwenye sheria. Kwa hiyo hizi sheria hizi mbili ndicho nilichokuwa nazungumza hapa lisituchanganye sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni hili ambalo Mheshimiwa Ngwali amependekeza kwamba, tulete mabadiliko ya Katiba hapa ili tuondoe suala hili kwenye Muungano. Hili anataka tu kuharakisha hoja, kwa sababu bado tuna kiporo cha Katiba Mpya na Katiba yenyewe kilichobaki ni kupigiwa kura. Muda muafaka tutapiga kura kwa Katiba Mpya, kama wananchi watairidhia ikapita ndiyo itakuwa Katiba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la msingi hapo Waheshimiwa Wabunge ni kwamba, unajua Zanzibar tayari imepata hii fursa, tusiwafanyie hiyana mbaya hapa, kwa sababu uliondoe kwenye Katiba sijui vitu gani, tayari wamepata hii fursa ya kusimamia hii rasilimali kule Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sitaki kwenda kwenye siasa ninachoweza kusema tu ni kwamba hakuna Katiba yoyote ambayo tumevunja kwenye hili. Hilo naomba kushauri hivyo.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo naomba kusema ni hili la Mheshimiwa Aeshi amelizungumzia na akaungwa mkono na Mheshimiwa Kangi Lugola. Unajua haya mambo mengine, haya masuala hoja zao hizi, haya masuala yako Mahakamani. Serikali ilipoanza zoezi hilo, watu walifungua kesi Mahakamani. Kama anachosema tumefanya maamuzi yanayovunja Katiba, Mahakama itaamua. Katiba hii msiisome upande mmoja tu isome holistically. Hatuwezi kuacha watu wanaumia, watu wanakuwa wahalifu, kwanza pia wanavunja sheria zile halafu tukasema eti sijui tunafanya vitu gani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa huko vijijini huko Kahama, nimeenda kule wanasema wanaishukuru Serikali kwa hatua iliyochukuliwa. Wanasema watoto wetu walikuwa wanaenda kufa, halafu walikuwa wanashiriki uhalifu. Leo Serikali inachukua hatua hizi mnasema tuache, that cannot be entertained. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia, lakini pia namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii. Yapo mambo kadhaa yamezungumzwa hapa ya Kikatiba na Kisheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwanza niseme hivi; Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inatoa haki za msingi, lakini na wajibu. Hivi vitu vinakwenda pamoja; haki na wajibu.

Katiba hiyo hiyo ndiyo inayoipa Bunge mamlaka ya kusimamia na kuishauri Serikali. Ibara ya 100 ina vifungu viwili; cha kwanza na cha pili. Kimoja kinatoa uhuru wa majadiliano, lakini kifungu kidogo cha pili kinasema, bila kuathiri masharti ya Katiba hii na Sheria na huo ndiyo msingi wa kanuni ya 64.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge Ibara ya 29(5) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano inasema hivi;

“Ili watu wote waweze kufaidi haki na uhuru vilivyotajwa katika Katiba hii, kila mtu ana wajibu wa kutenda na kuendesha shughuli zake kwa namna ambayo hataingilia haki na uhuru wa watu wengine au maslahi ya Umma.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, yamezungumzwa mambo hapa ambayo kimsingi yanawadhalilisha Wanajeshi na Jeshi la Wananchi wa Tanzania. Bunge lisiruhusu hiki kitu. Bunge limetunga Sheria; tunayo Sheria ya Usalama wa Taifa (The National Security Act) na sheria hii, Kifungu cha (4) inataja “Public officer” ikiwajumuisha na Wabunge. Yako mambo ambayo huwezi ukayasema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kifungu cha (4) cha Sheria ya The National Security Act; na hata kama umeambiwa hizo habari, ndiyo maana tuna fursa hapa za kuchangia hata kwa maneno na kwa maandishi kwa sababu haya mambo yapo protected. Someni Kifungu cha (4) cha Sheria ya Usalama wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais Kikwete enzi zake aliwahi kutuambia; “akili za kuambiwa, changanya na ya kwako.” Hamwezi mkazungumza mambo ambayo hata yanadhalilisha wanawake wa Wanajeshi; Hao Wanajeshi wenyewe wako humu halafu tunakaa kimya!

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nilikuwa nataka kusema hivi…

T A A R I F A . . .

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hii taarifa naikataa. Yeye alikusudia kueleza tu mamlaka. Nimesema hapa, Ibara ya 100(2) inasema:

“Bila kuathiri Katiba hii au masharti ya Sheria nyingine yoyote inayohusika.”

Nimesema hivi, Katiba yetu inatoa haki na wajibu. Kwa mfano, huwezi ukapiga mtu au ukatukana mtu, ukasema nina uhuru wa hapa. Haiwezekani! Tunatambua Katiba inatoa mamlaka hayo na tumetunga sheria hizi hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami ngoja niwashauri hapa. Najua hapa wakati fulani mnapotoshwa. Uhuru huo mnaotafsiri Katiba vibaya, kuna siku nyingine mtajikuta pabaya, that is it! Eeh! (Kicheko/Makofi)

Hamuwezi, kwa sababu Katiba iko wazi, nakupeleka tu Mahakamani. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, aliyasema; lakini ninachotaka kusema ni hivi, Waheshimiwa Wabunge watumie uhuru wao kuishauri na kuisimamia Serikali kwa hekima. Eeh! Haya mambo yapo hapa. Siku hizi wameanzisha utaratibu yale unayoyakataa, wanaweka kwenye mitandao. Wakiweka kwenye mitandao, nitawachukulia hatua za kisheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawawezi kuwa protected.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nasimamia ununuzi hata Mikataba yote inapita hapa, vifaa vya kisasa wananunua; unaweka maneno hayo, una-expose Taifa hili kwa watu wengine kwamba Jeshi la Tanzania lina vifaa duni, kwa hiyo tunaweza tukaenda tukawavamia kule. Haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa hapa na kukubali kwamba Katiba Ibara 147 imepiga marufuku Wanajeshi kujiunga na Vyama vya Siasa. Hiyo ni kweli kwa sababu ni sharti kabisa la Kikatiba lakini, Ibara ya 45, Kifungu cha 25 cha Sheria ya Ulinzi wa Taifa (The National Defence Act) kimetoa Mamlaka kwa Rais ku-second mtu yoyote.

Kipindi chote hicho, huyo mtu anaendelea kuwa Mwenyekiti. Sasa kwa mfano, kama ameteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya au Mkuu wa Mkoa, tunajua yuko Mwenyekiti wa Chama wa Mkoa; Mwenyekiti wa Chama wa Wilaya ana majukumu yake, hawezi kuchukuliwa na Mkuu wa Mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Katiba yenyewe ya Chama cha Mapinduzi imesema kwenye Ibara ya 94 na Ibara ya 80; “Mkuu wa Mkoa atakuwa Mjumbe wa hizo Kamati kama anatokana na Chama cha Siasa.” Eeh, na wote tunafahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa sababu huyu anakwenda kufanya mambo ya Serikali kule siyo ya Chama. Katiba iko wazi. Huyu anatokana na Chama cha Siasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru kwa kunipatia hii fursa na mimi nichangie. Nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa mimi kupata fursa kipindi hiki lakini niwapongeze sana Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa hotuba yao nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kuwatakia heri ya Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani Waislamu wote wa Tanzania wanaofunga. Mwenyezi Mungu atubariki, mnapokuwa mnashiriki toba hii mshiriki na sisi waovu wengi mtuombee pia. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Magufuli kwa hatua aliyochukua kuhusiana na mchanga. Unajua Katiba yetu, Ibara ya 27 imeeleza vizuri wajibu wetu kama Serikali kuhusu matumizi ya maliasili tulizonazo na hii ni maliasili. Naomba Waheshimiwa Wabunge wote kwenye hili tushirikiane na Serikali kuhakikisha kwamba tunalinda maslahi ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili hakuna sababu ya kulaumiana, ni mapema sana kuilaumu Serikali kwa hatua ilizochukua. Zimeundwa Kamati mbili, hii ya kwanza na Kamati nyingine ya sheria ambayo inaangalia pia na mikataba. Kati yetu hakuna hata aliyewahi kuona mikataba hii au aliye na hii mikataba. Kwa hiyo, naomba tutambue kwamba sisi ni familia moja, tunayoyasema leo yatakuja kuturudia, hatuwezi tukaanza kuilaumu Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kuwashauri Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwamba tunapochangia tuchangie kwa hekima, kwa heshima na kwa nidhamu kubwa kwa maslahi ya Taifa letu na kwa viongozi wa Taifa hili na kwa lugha ya Kibunge. Tunazo kanuni
zinazotuongoza, mimi sioni hii ina maslahi gani kwa watu, kwa sababu tusichangie kana kwamba tunachochea watu wengine watuchukulie hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Waheshimiwa Wabunge waiunge mkono Serikali kwenye suala hili. Ni suala ambalo lilipaswa lituunganishe sisi kama watu wamoja kwa ajili ya maslahi ya Taifa letu. Hii baadhi yetu mnayoshabikia kwamba tukishtakiwa, hakitashtakiwa Chama cha Mapinduzi kama ni liability itakuwa ni ya Serikali nzima. Hapa hawachagui kwamba ni huyu au ni yule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia, naomba tuendelee kuipatia Serikali ushirikiano, Wizara inafanya vizuri, wawekezaji kwa kweli wataendelea kuja. Nimerudi asubuhi hii kutoka Uganda kusaini mkataba ule wa bomba la mafuta na ninyi wenyewe mmeona Waziri wa Viwanda na Biashara amewasilisha hapa bajeti yake wiki moja iliyopita na mwitikio umekuwa mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge tunapochangia, tusichangie kwa kuogopesha watu kwamba mambo ni mabaya sana. Kila kilichofanyika kwenye hatua hii ya michanga ni halali kisheria na kimikataba. Kwa hiyo, tutakapokamilisha ile ripoti ya Kamati ya Sheria tutaona tufanye nini kwa sababu Sheria ya Madini inatoa fursa ya ku-review mikataba ile kila baada ya miaka mitano. Sasa mnawezaje ku-review kama hamko well informed? Yaliyotokea sasa kwenye taarifa hii yanatusaidia sisi kuwafuata wenzetu na kuwaambia jamani hiki ndicho tulichoona, turekebishe hapa, sasa kosa lake ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naunga mkono hoja asilimia mia moja.
Muswada wa Sheria ya Upatikanaji wa Habari wa Mwaka 2016
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa mara nyingine tena kuniwezesha na mimi niweze kushiriki katika mjadala huu. Pia nakushukuru kwa kuniruhusu na vilevile namshukuru sana Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe kwa kuleta muswada huu ikiwa ni kukidhi hitaji la Katiba kwenye Ibara ya 18(d) ambayo inatoa haki ya watu kupewa taarifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hakika muswada huu umeletwa na mtu ambaye hasa ndio anayestahili kuleta, kwa sababu kwa background yake, yeye ni mwanataaluma wa uandishi wa habari, lakini pia mwanasheria aliyebobea kwa kuleta muswada huu, ameangalia mambo yote. Ameangalia haki ya kupata hizo taarifa, lakini pia na wajibu wa huyo mtu anayetaka kutoa taarifa au kuzisambaza hizo taarifa. Ni kwa maana hii sasa unaona mantiki ile ya Ibara ya 6 katika muswada huu.
Mhehimiwa Mwenyekiti, ni kwamba katika scheme ya Katiba yetu ni haki na wajibu. Ukisoma Ibara ya 12 mpaka 28 ya Katiba, inaeleza juu ya haki na wajibu. Inaeleza juu ya haki na wajibu, Ibara ya 29 na ya 30. Kwa hiyo, hakuna kitu ambacho kimekiuka Katiba katika yale yaliyoorodheshwa katika Ibara ya 6 ya muswada. Mambo yote yale Usalama wa Taifa, siri, faragha, mambo yote yaliyowekwa pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kusema kweli, mambo haya tayari yako katika sheria mbalimbali za nchi yetu. Utakuta katika Sheria ya National Security Act, utakuta katika Sheria ya Whistle Blowers and Witness Protection Act, utakuta katika sheria nyingi. Kitu ambacho tumefanya katika muswada huu, ni kuyaleta pamoja haya ambayo yamekwishatamkwa katika sheria hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitashangaa kama miongoni mwetu kwa kweli tukaanza kutilia mashaka mambo ambayo yameorodheshwa katika Ibara ya 6 ya muswada huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambieni pia kwamba muswada huu pia haukusudii kuua upatikanaji wa habari kwa sababu Ibara ya 5(3) imeeleza vizuri kwamba muswada huu hauzuii kutungwa kwa sheria nyingine ile ambayo inaruhusu utoaji wa habari. Kwa hiyo, muswada huu haukusudii wala hata kuficha sijui mnaita ufusadi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, tayari tumetunga sheria ya Whistleblowers and Witness Protection Act ambayo inatoa fursa kwamba hata vitendo vya uhalifu vitajwe, mambo ya ufisadi yatajwe; lakini tunayo sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa imeeleza hayo mambo. Tumetunga Sheria ya Tanzania Extractive Industry (Transparency and Accountability). Kwa hiyo, kusema kwamba tunatunga sheria hii kwamba hiyo itakuwa ni namna ya kuzuia upatikanaji wa habari, hapana. Ni namna ya ku-enhance zaidi upatikanaji wa habari lakini kwa namna ambayo tutafanya kwa kuzingatia maslahi ya Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikia baadhi yetu tumezungumza Ibara ya 16, maslahi ya umma. Moja ya mambo mnayoweza kuyasema, haiwezekani kila kitu tuna-define kwamba ni maslahi ya umma, lakini ukieleza yale mambo yaliyotajwa yote katika Ibara ya 6 hayo ni sehemu ya maslahi ya umma na kipimo chake ni public. Ndiyo maana sasa mtu anayeona kwamba hakuna maslahi ya umma hapa, anaweza akaenda mahakamani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kusema kwamba siyo vyema kulaumu sana hapa kwamba kumekuwa na ukiukwaji wa Katiba. Ni nani amekiuka hii Katiba? Katiba yenyewe inamtaka Rais kusimamia na kutekeleza sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 36 ya Katiba hii inatutaka kila mmoja azingatie Katiba na Sheria ya nchi; na mtu ambaye anaona kwamba hiyo Sheria inavunjwa au Katiba aende mahakamani. Haiwezekani kwamba sasa mtu anayesimamia utekelezaji wa sheria aonekane kwamba yeye ndio anayevunja Katiba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana wakati fulani nikiongea na umma niliuliza ni kifungu gani cha Katiba? Ni kifungu gani cha sheria kimekiukwa? Maana yake hapa wamezungumza, nimewasikia wanasema anavunja Katiba, anavunja Katiba. Waseme ni kifungu kipi cha Katiba so far kimekiukwa? Kwa hiyo, tuwe responsible tunapochangia ndani ya Bunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilifikiri kwamba ni vizuri tukawa makini tunapochangia kwenye masuala haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata fursa hapa, nimewasikiliza Waheshimiwa Wabunge wakizungumza kwamba muswada huu ambao utatumika Bara peke yake lakini umechangiwa na watu kutoka Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Katiba yetu, uraia ni jambo la Muungano. Bunge hili linatoa haki kwa kila Mbunge, haijalishi anatoka Rombo au anatoka Musoma au anatoka Unguja au anatoka Pemba. Kwa hiyo, hii tabia ya kuanza kubaguana humu ndani nayo siyo nzuri. Haiwezekani ninyi mkawa wamoja halafu mkaanza kubaguana baguana humu ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo vizuri kuunganisha na maslahi ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hivi vitendo lazima tuvikemee, hivi ndivyo vinavyovunja Katiba. Kwa sababu Ibara ya 100 ya Katiba ya nchi inayosema haki ya kujadili ya Mbunge yoyote aliyoko hapa bila kujalisha kwamba ni wa Viti Maalum, anatoka Pemba, anatoka Musoma au ni wapi. Kwa hiyo, mambo haya tunachezea lakini ni ya gharama kubwa sana. Ndiyo maana namuunga mkono sana Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe kuja na muswada huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa naomba kushauri tu kwamba Waheshimiwa Wabunge tuupokee huu muswada, ni mzuri kwa mtu ambaye anataka kuishi vizuri kwa kuzingatia sheria na Katiba za nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nimepata fursa hapa, namshukuru sana Mheshimiwa Halima Mdee ameleta mapendekezo ya kuboresha muswada huu na katika Ibara ya 6 hii ame-single out kifungu kidogo…
Iko kwenye amendment, hiki ndicho tunachokitaka. Kwa sababu nina muda mdogo tu hapa, kama ningekuwa na muda nikayasoma yale mambo yote yaliyoorodheshwa kwenye Ibara ya 6 yale, nani anaruhusu, kama yeye angekuwa kiongozi? Hivi ninyi mnazungumza mambo ya faragha; mambo ya faragha yale yako protected Ibara ya 16.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo yanayoendelea mahakamani, tumetunga sheria hapa, tunayo Sheria ya Mtoto inayozungumza kwamba hata zile proceedings zinazomhusu mtoto zisikilizwe kwa usiri (in camera). Wanawake waliobakwa, mashauri yao yanasikilizwa kwa siri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii ni sheria tu, nadhani Waheshimiwa Wabunge hawakupata fursa ya kuisoma. Wale ambao wamepata fursa wameisoma, wameelewa. Mimi naomba kushauri Waheshimiwa Wabunge tuunge mkono hoja hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali, 2017
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kwa mara nyingine tena kuwapongeza na kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamepata fursa ya kuchangia kwenye hoja hii muhimu sana. Natambua uwezo mkubwa na umakini wa Wabunge hawa, ambao ni wawakilishi wa wananchi wa kuisimamia na kuishauri Serikali inapotekeleza majukumu yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa namna ya pekee leo pia naomba kutambua sana uwezo mkubwa walionao Wabunge, muda hautoshi, nitawataja hawa waliopata fursa ya kuchangia ambao kwa elimu yao kubwa sana wamenisaidia hata mimi kuelewa mambo mengi na bila shaka Wabunge ambao walikuwa hawaelewi wameelewa mambo mengi ya msingi wa mabadiliko haya ya sheria. Naomba niwataje; Mheshimiwa Mhagama, Mbunge wa Madaba; Mheshimiwa Zedi, Mbunge wa Bukene; Mheshimiwa Joram Hongoli, Mheshimiwa Richard Mbogo na Mheshimiwa Rashid Shangazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge hawa wametoea elimu kubwa sana katika Bunge hili kuhusu umuhimu na maudhui ya Muswada huu. Naamini Waheshimiwa ambao walikuwa hawaelewi nao wamenufaika sana na elimu hii. Waheshimiwa hao ni pamoja na Mheshimiwa Waitara, Mbunge wa Ukonga; Mheshimiwa Riziki Shahari, Mbunge wa Viti Maalum; Mheshimiwa Dkt. Sware, nadhani ni hao. Kwa hiyo nichukue fursa hii kuwapongeza sana Wabunge hawa… (Makofi)

KUHUSU UTARATIBU...

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, na pia namshukuru Mheshimiwa Waitara kwamba sasa ameelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo mazuri ya mchango wa Wabunge hawa ndani ya Bunge hili sitakuwa na mengi ya kusema. Isipokuwa kwa sababu nina wajibu wa Kikatiba wa kufafanua hoja hizi za kisheria; niseme tu kwamba, moja, Waheshimiwa Wabunge naomba kuwahakikishia, kama ambavyo baadhi ya Wabunge
wamechangia, mabadiliko haya ya sheria hayakusudii kwa namna yoyote kupora au kupoka mamlaka ya Kikatiba na kisheria na Kikanuni ya Bunge hili kuisimamia na kuishauri Serikali kwa ufanisi ipasavyo, inapokuwa inatekeleza majukumu yake ya Kikatiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, majukumu haya ya Kikatiba bila kurejea Katiba yameelezwa vizuri Ibara ya 63(2) na (3) kuwa Mbunge anaweza akamuuliza Waziri na Serikali jambo lolote lile linalohusu mambo ya Muungano, lakini ni vizuri niliseme kwa sababu nadhani muda utaweza kutosha ili wananchi nao wapate kulielewa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, Katiba hii inasema hivi, 63(2): “Sehemu ya pili ya Bunge itakuwa ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya Muungano ambacho kitakuwa na madaraka, kwa niaba ya wananchi, kuisimamia na kuishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa Katiba hii.”

Mheshimiwa Naibu Spika, 63(3); “Kwa madhumuni ya utekelezaji wa madaraka yake Bunge laweza–

(a) kumuuliza Waziri yeyote swali lolote kuhusu mambo ya Umma katika Jamhuri ya Muungano ambayo yako katika wajibu wake;”

Mheshimwa Naibu Spika, haya hayategemei hizi ripoti za robo mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika 63(3);

(b) kujadili utekelezaji wa kila Wizara wakati wa Mkutano wa Bunge wa kila mwaka wa bajeti;”

Mheshimiwa Naibu Spika, Muswada huu wala sio Muswada wa kubadilisha Sheria ya Kinga, Madaraka na Haki ya Bunge, wala sio Muswada unaobadilisha Kanuni za Bunge na Muswada huu haukubadilisha kabisa kifungu cha tisa (9) cha Sheria ya Bajeti ambayo bado mamlaka yake yamebaki pale pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu cha tisa (9) cha Sheria ya Bajeti kinahusu madaraka ya Kamati ya Bajeti. Naomba niyasome madaraka haya ya Kamati ya Bajeti tuone kama yameguswa kwa mabadiliko haya. Kifungu cha 9(1) kinasema:

“The Parliamentary Budget Committee shall, in addition to functions provided under the Parliamentary Standing Orders, carry out the following functions:

(a) discuss and review the Plan and Budget Guidelines, budget estimates and make recommendations to the National Assembly;

(b) consider the Budget and make recommendations to the the National Assembly;

(c) scrutinize the budget estimates of the National Audit Office, Judiciary and National Assembly;

(d) provide general recommendations to the National Assembly and Parliamentary Standing Committees on budgetary matters;

(e) monitor all budgetary matters falling within the powers of the National Assembly under this Act or any other law and report on those matters to the National Assembly;

(f) monitor adherence by the Government and public entities to the principles of public finance set out in the Constitution, other laws in force, and to the fiscal responsibility principles set out in the Public Finance Act and this Act;

(g) examine quarterly financial statements and other documents submitted to the National Assembly and make recommendations for improving the management and accountability in respect of public finances;

(h) conduct periodical study on the performance trend of the Budget and make recommendations to the National Assembly for improvements;

(i) do any other act or activities relating to budgetary matters as may be assigned to it by the National Assembly under this Act or any other written law; and

(j) in relation to oversight responsibility, discharge or perform any function as spelt out under the Parliamentary Standing Orders.

(2) For the purpose of subsection (1), the Parliamentary Budget Office shall provide the Parliamentary Budget Committee with professional services in respect of budget, finance and economic matters.”

Mheshimiwa Naibu Spika, mnaona kabisa Waheshimiwa Wabunge mamlaka ya Kamati ya Bajeti hayakuguswa kabisa hata katika mapendekezo haya, wala hata mamlaka yake hayazungumzi hata quarterly ya ripoti ukiisoma hii, it does not mention about quarterly reports. Hata hivyo, wamepewa mamlaka, tena kwa wakati wote wapo pale. Yaani wao mamlaka yao pale wanaendelea kuangalia wakati wote performance ya bajeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba kushauri kwamba Waheshimiwa Wabunge mridhie mapendekezo haya ambayo yameletwa na Serikali. Kwa namna yoyote hayataathiri Mikutano ya Bunge, mikutano hiyo ni ya Kikatiba, ni ya kikanuni na mamlaka yenu ya kuisimamia Serikali hayapokonywi na haya. Kwa hiyo, kwa mara nyingine tena niseme tu kwamba nimeridhika na kufarijika sana na mchango mzuri na elimu iliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge hawa ambao nimeshawataja na ufafanuzi huu unatosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kushauri Bunge lako Tukufu liunge mkono hoja hii, naomba kuwasilisha.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 5) wa Mwaka 2017
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara nyingine tena nichukue fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuungana kwenye suala la msingi sana kwa maslahi ya nchi; kama hili suala la Muswada huu ambao tunaona hoja zote ambazo zimeletwa kwenye muswada huu; mabadiliko ya Sheria ya Ardhi, mabadiliko ya Sheria ya Utumishi wa Umma, mabadliko ya Sheria ya Ufilisi, Sheria ya Bajeti na sheria zote ambazo zimeletwa mbele yako. Kwa kweli kwangu nimepata faraja sana ninapoona Waheshimiwa Wabunge wanaungana na kuwa kitu kimoja. Kwa sababu Wabunge wote wameunga mkono hoja hii na Waheshimiwa Wabunge wamechangia vizuri; kwanza naanza kwa kuwashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua mchango mzuri wa Kamati ya Kudumu ya Katiba na Sheria. Mchango mzuri wa Kambi ya Upinzani, mchango mzuri wa Waheshimiwa Wabunge wote na naomba niwataje Wabunge hawa kwa heshima yao kabisa. Kwanza Mheshimiwa Mhagama, Mbunge wa Madaba; Mheshimiwa Najma Murtaza Giga, Mbunge wa Viti Maalum; Mheshimiwa Tasika Mbogo, Mbunge wa Viti Maalum, Mheshimiwa Salome Makamba, Mbunge Viti Maalum; Mheshimiwa Joram Hongoli, Mbunge wa Lupembe; Mheshimiwa Ally Salehe, Mbunge wa Malindi; Mheshimiwa Magdalena Sakaya, Mbunge wa Kaliua; Mheshimiwa Joyce Sokombi, Mbunge wa Viti Maalum; na mwisho Mawaziri wawili, Profesa Ndalichako Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia na Mheshimiwa William Lukuvi Waziri wa Ardhi na Makazi. Samahani nimemsahau Mheshimiwa Lucy Mollel, Mbunge wa Viti Maalum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwa ujumla, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge na michango yao kwa kweli ilikuwa mizuri, sijui hata kama nitakuwa na ya kuongeza hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme tu moja, suala la kuoanisha umri huu wa kustaafu; Waheshimiwa Wabunge pamoja na kuunga mkono wamesema kwamba labda tungeenda kama miaka 70 hivi. Ni suala ambalo pia hata ukiangalia bado kuna kubishana kama twende miaka 65 na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ninachoweza kusema tu ni kwamba mpaka sasa umri wa kustaafu katika makundi mbalimbali ya watumishi wa Umma tulionayo yana miaka
60. Miaka 65 ni Majaji wa Mahakama ya Rufaa akiwemo na Jaji Mkuu. Miaka 65 wengine ni Controller and Auditor General (Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali) ambaye naye anastaafu kwa miaka 65. Watumishi wengine tunaobaki tunastaafu kwa miaka 60 kwa lazima, japokuwa kwa hiari ni miaka 55. Kwa hiyo naomba tuendelee na standard hii ya kiwango hiki; nashukuru lakini kwamba mmeunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali ya maelezo mazuri aliyoyatoa Mheshimiwa Waziri kuhusu hili la watu wa hati za Kimila kuachwa, ukweli ni kwamba tumeweka kile kifungu pale makusudi ili kutokuleta mkanganyiko; kwamba je, Sheria hii pia itatumika na kwa hati za kimila? Hati za kimila zina sheria yake mahususi, Sheria ya Ardhi ya Vijiji. Ukisoma ile Sheria ya Ardhi ya Vijiji ya Mwaka 1999 inaweka utaratibu wote wa matumizi ya hati hizo za kimila; na Sheria ile inatambua kwamba hati ile ina hadhi sawa na hati ya Kiserikali ya kumiliki ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili la watakaowajibishwa namna gani ya kuwawajibisha hawa waliochukua mikopo kwa kutumia hati hizi lakini ardhi haikuendelezwa. Mheshimiwa Waziri wa Ardhi ameshasema, kuna kitu kimoja hiki nadhani hakikueleweka vizuri. Kipindi cha ndani ya miezi sita, huyu anayechukua mkopo anatakiwa tu kuwasilisha kwa Kamishna utaratibu na namna gani atakavyoutumia huo mkopo wake, si kwamba sasa ndiyo anatakiwa aeleze jinsi ambavyo ameendeleza hiyo ardhi. Miezi sita haiwezekani, ni muda mdogo sana na utaratibu wa namna gani na kusimamia utawekwa kwenye kanuni na Mheshimiwa Waziri. Kwa hiyo hilo nalo niliona nilitolee ufafanuzi kwa sababu lingeweza kuleta mkanganyiko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani kama kuna kitu nimekisahau hapa madam Waheshimiwa Wabunge wote wameunga mkono, kwa mara nyingine namshukuru Mwenyezi Mungu, niwashukuru sana Wabunge Mwenyezi Mungu aendelee kuwabariki na wewe mwenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.