Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Deogratias Francis Ngalawa (16 total)

MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-
Wananchi wa Ludewa wamekuwa wakisikiliza mipango ya Serikali juu ya miradi mikubwa ya Makaa ya Mawe, Mchuchuma na Liganga ambapo kumekuwa na mipango mingi ambayo kwa sasa inaonekana kutekelezwa:-
(a) Je, ni lini wananchi walioachia ardhi yao kupisha miradi hiyo watalipwa fidia?
(b) Je, ni lini miradi hiyo inatarajiwa kuanza?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, miradi ya makaa ya mawe ya Mchuchuma na Liganga inasimamiwa na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji lakini inafanywa hivyo kwa kupita Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC). Miradi hii inaendelezwa kwa pamoja kwa maana ya (Intergrated Projects) kati ya Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) lenye asilimia 20 ya hisa na Kampuni ya Sichuan Hongda (Group) Company Limited ya China yenye hisa asilimia 80 kupitia kampuni ya ubia Tanzania China International Mineral Resources Limited (TCIMRL).
Mheshimiwa Spika, Serikali ilitoa leseni za uchimbaji mkubwa SML namba 533/2014 ya tarehe 09/10/2014 katika eneo la Liganga lenye ukubwa wa kilomita za mraba 30.41. Lakini SML ya pili namba 534/2014 ya tarehe 9/10/2014 katika eneo la Mchuchuma lenye ukubwa wa kilomita za mraba 25.46. Leseni hizi zilitolewa kwa kipindi cha miaka 25 na zitaisha muda wake tarehe 08/10/2039.
Mheshimiwa Spika, Kampuni ilifanya uthamini wa mali za wananchi walioko ndani ya maeneo ya miradi ambao walitakiwa kupisha shughuli za utekelezaji wa miradi mwezi Agosti, 2015 na kuridhiwa na Mthamini Mkuu wa Serikali mwezi Agosti, mwaka huo huo. Mpango wa kulipa fidia unatarajiwa kuanza mwezi Juni, mwaka huu chini ya usimamizi wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.
(b) Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa mradi unatarajiwa kuanza Machi, 2017 na kukamilika mwezi Julai, 2020 na utafanywa hivyo chini ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-
Bonde la Mto Ruhuhu lililopo katika Kata ya Ruhuhu Wilaya ya Ludewa ni eneo muhimu sana, linaweza kuzalisha mazao mengi na kupunguza uhaba wa chakula Tanzania:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuliendeleza bonde hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deo Francis Ngalawa, Mbunge wa Jimbo la Ludewa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa Bonde la Mto Ruhuhu linalojumuisha Kata ya Manda, Wilayani Ludewa Mkoa wa Njombe na Kata ya Lituhi Wilayani Nyasa katika Mkoa wa Ruvuma kwa kilimo cha mazao ya aina mbalimbali yakiwemo mpunga, mahindi, mihugo na mboga mboga.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika maandalizi ya uendelezaji wa bonde hilo, upembuzi wa awali ulifanyika kati ya mwaka 2013 na 2014 na kubaini uwezekano wa kujenga bwawa kubwa katika eneo la Kikonge kwa ajili ya matumizi mbalimbali ikiwemo kudhibiti mafuriko katika Bonde la Mto Ruhuhu, kuendesha kilimo cha umwagiliaji kwa eneo la takriban hekta 4,000 na kufua umeme mkubwa utakaounganishwa kwenye Gridi ya Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Afrika ipo katika hatua ya kutafuta fedha kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa eneo hili pamoja na kuweka miundombinu ya umwagiliaji.
MHE. DEOGATIAS F. NGALAWA aliuliza:-
Serikali ilitoa ahadi ya kutengeneza barabara ya lami toka Itoni – Njombe – Manda na upembuzi yakinifu tayari umeshafanyika.
Je, ni lini ujenzi huo utaanza hasa ikizingatiwa kuwa barabara hiyo imekuwa kero kubwa hasa kipindi cha masika lakini pia ni muhimu kwa sababu ya ujiio wa miradi ya makaa ya mawe Mchuchuma na chuma cha Liganga?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa barabara ya Itoni – Ludewa hadi Manda yenye urefu wa kilometa 211.4 kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Maandalizi kwa ajili ya ujenzi wa barabara yameshaanza ambapo kwa sasa barabara inafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, usanifu wa kina kwa sehemu ya barabara yenye urefu wa kilometa 50 kuanzia Kijiji cha Lusitu hadi Kijiji cha Mawengi umekamilika na taratibu za kumpata mkandarasi wa kujenga sehemu hii ya barabara zipo katika hatua za mwisho. Ujenzi wa kiwango cha zege wa sehemu ya Lusitu hadi Mawengi umepangwa kuanza katika mwaka wa fedha 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, usanifu wa kina wa sehemu ya barabara iliyobaki, unatarajiwa kukamilika Julai, 2016. Serikali itaendelea na ujenzi wa barabara hii kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. DEOGRATIUS F. NGALAWA aliuliza:-
Pamoja na kwamba Jimbo la Ludewa lina vyanzo vingi vya maji, lakini kuna matatizo makubwa sana ya maji na wadau mbalimbali wamekuwa wakijitokeza kusaidia tatizo hili lakini Serikali na Halmashauri zimekuwa hazitoi ushirikiano kwa kurudi nyuma katika kuchangia sehemu yao kwa kigezo cha kutokuwa na fedha. Mfano vijiji vya Maholongwa, Mlangali, Mavanga, Manda, Nkomang’ombe na Lwela.
(a) Je, Serikali iko tayari kuweka kipaumbele katika kusaidia pale inapohitajika kuchangia?
(b) Je, nini kauli ya Serikali katika kushughulikia tatizo la maji Jimboni Ludewa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deogratius Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa miradi ya maendeleo unafanyika kwa njia shirikishi yaani Serikali, wadau wa maendeleo na wananchi kupitia mpango wa fursa na vikwazo kwa maendeleo. Kwa utaratibu huo mafanikio makubwa yamepatikana katika kuboresha huduma kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya mwaka 2016/2017, Serikali imeweka kipaumbele na kutenga shilingi milioni 861 kwa ajili ya kukamilisha mradi wa maji katika Kijiji cha Lugarawa, ukarabati wa miradi ya maji Lifua/Manda na Kijiji cha Ludewa K. Vilevile Serikali inashirikiana na taasisi isiyo ya Kiserikali ya Lusala Development Association kwa ajili ya kukamilisha mradi wa maji katika vijiji vya Mlangali, Mavanga na Nkomang’ombe utakaogharimu shilingi milioni 250 ambapo mchango wa Serikali ni shilingi milioni 50.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inapongeza mchango mkubwa wa wadau mbalimbali kushirikiana na wadau wa maendeleo katika sekta za maji zikiwemo taasisi za dini. Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo na kuhakikisha bajeti inatengwa kila mwaka kwa ajili ya kutatua tatizo la maji kwa wananchi wa Ludewa na maeneo mengine hapa nchi.
MHE. DEO F. NGALAWA Aliuliza:-
Shirika la Posta Tanzania lilitumia fedha zake kuwalipa Wastaafu wa lililokuwa Shirika la Posta na Simu la Afrika Mashariki:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kulirejeshea Shirika hilo fedha hizo ili kulinusuru?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO Alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deo Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli Shirika la Posta Tanzania lilitumia fedha zake kuwalipa wastaafu wa lililokuwa Shirika la Posta na Simu la Afrika Mashariki na kuwasilisha madai Serikalini ili lipate kurejeshewa fedha zake. Hadi sasa Shirika limelipa shilingi bilioni 5.9 na Serikali imesharejesha shilingi bilioni 2.7 kama ifuatavyo:
Mheshimiwa Spika, Novemba, 2016 Serikali ilirejesha Shilingi milioni 700; Desemba, 2016 Shilingi 1,000,000,000; na Januari, 2017, Serikali ilirejesha Shilingi 1,000,000,000. Aidha, Serikali itaendelea kurejesha kiasi kilichobaki cha Shilingi 3,200,000,000 kwa kadri fedha zitakavyopatikana.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Msajili wa Hazina inaendelea na jukumu la kuwalipa pensheni ya kila mwezi wastaafu wa lililokuwa Shirika la Posta na Simu la Afrika Mashariki wapatao 292.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-
Miradi ya Makaa ya Mawe ya Mchuchuma na Liganga imekuwa ikiwekwa katika mipango ya Serikali katika Awamu karibu zote nne zilizopita, hata Awamu hii ya Tano bado miradi hii imewekwa.
(a) Je, ni lini wananchi walioachia maeneo yao ili kupisha miradi hii watalipwa fidia yao?
(b) Je, ni lini miradi hii itaanza kazi?
(c) Je, ni kweli Serikali imejipanga kuhakikisha miradi hii inaanza?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa, lenye sehemu (a), (b) na (c), kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Mchuchuma na Liganga umeainishwa katika Dira ya Taifa 2025; Mkakati wa Fungamanisho la Maendeleo ya Viwanda 2015; Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2016-2021) na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya 2015 - 2020. Ni majukumu na wajibu wa Serikali kutekeleza maamuzi na maelekezo yaliyorejewa hapo juu. Ni kweli, Serikali imejipanga kuhakikisha miradi hii inaanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naelewa tatizo la Mheshimiwa Mbunge ni kuchelewa kuanza kwa mradi na hasa malipo ya fidia kwa wananchi waliopisha mradi. Kuchelewa kuanza kwa mradi kumetokana na nia nzuri ya Serikali ya kutaka kuhakikisha miradi inatekelezwa na wakati huo huo Taifa linapata manufaa stahiki kutokana na uwekezaji huo. Timu ya wataalamu imekamilisha kazi ya kupitia vipengele vyote vya vivutio na kuwasilisha taarifa yao Kamati ya Kitaifa ya Uwekezaji (NISC). Kamati hiyo imetoa maelekezo kwa timu ya wataalam kujadiliana na mwekezaji maeneo yenye mvutano. Ni imani yangu kuwa baada ya makubaliano kwenye maeneo hayo machache yaliyobaki, vikao husika vitatoa baraka za mwisho na mradi utaanza mara moja ikiwemo kulipa fidia kwa watu waliopisha mradi.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-
Wafanyakazi wa TTCL wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki waliolipwa pesheni ni wale waliofungua kesi mahakamani na kushinda. Aidha, wapo ambao wanastahili malipo lakini hawakuwa na uwezo wa kumlipa Wakili katika kuendesha kesi hiyo.
Je, ni lini Serikali itawalipa wafanyakazi wa TTCL wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki madai ya pesheni zao?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Wiziri ya Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, siyo kweli kwamba wafanyakazi wa TTCL wa iliyokuwa Jumuiya ya Mashariki waliolipwa pesheni ni wale tu waliofungua kesi mahakamani. Kumbukumbu zinaonyesha kwamba tarehe 31 Disemba, 1990 Serikali ilisitisha mfuko wa ujulikanao kama East Africa Non Countributory Pension Scheme baada ya kushauriana na kukubaliana na Menejimenti pamoja na Chama cha Wafanyakazi wa TTCL wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Baada ya kusitishwa kwa mfuko huo kila mfanyakazi alilipwa asilimia 50 ya michango yake na asilimia 50 iliyobaki ilipelekwa NSSF kwa ajili ya pesheni ya kila mwezi pindi watakapostaafu. Ni vema ikafahamika kwamba, wafanyakazi wote wa TTCL wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki wanalipwa pesheni zao na NSSF baada ya kustaafu.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, baada ya malipo ya asilimia 50 kwa 50 kukamilika, wafanyakazi 254 hawakuridhika na maamuzi ya Serikali ya kusitisha mfuko wa East African Non Countributory Pension Scheme na kufungua kesi Na. 69/ 2005 Mahakama Kuu kupinga maamuzi ya Serikali. Katika shauri hilo, Mahakama Kuu iliamua kuwa uamuzi wa Serikali kusitisha mfuko huo haukuwa sahihi kisheria na hivyo wafanyakazi 254 waliokuwa katika shauri hilo walipwe madai yao ambayo yalijumuisha malipo ya mkupuo, riba pamoja na pensheni ya kila mwezi ya wafanyakazi hao.
Mheshimiwa Spika, baada ya uamuzi huo wa Mahakama Kuu, Hati ya Makubaliano (Deed of Settlement) yenye tuzo ya shilingi 13,685,450,397.82 ilisainiwa mnamo tarehe 27 Agosti, 2013 na kusajiliwa Mahakama Kuu ya Tanzania, Dar es Salaam mnamo tarehe 2 Agosti, 2013 ikiwa ni tuzo kwa wafanyakazi wote waliofungua shauri husika. Aidha, mahakama ilielekeza kuwa wadai katika kesi hiyo ambao bado wako kazini malipo yao yatafanyika mara baada ya kustaafu. Kwa mujibu wa Hati ya Makubaliano malipo yaligawanywa katika awamu tatu ambapo hadi kufikia Julai 2017 awamu zote tatu zimelipwa jumla ya shilingi 12,665,994,447.92.
Mheshimiwa Spika, hadi sasa wastaafu 245 wameshalipwa madai yao yote ya fedha za mkupuo ambapo kati yao wastaafu 54 wamefariki dunia na fedha zao walilipwa warithi na wastaafu 198 wanaendelea kulipwa malipo ya nyongeza ya pensheni ya kila mwezi. Kwa upande wa wadai ambao bado wapo kazini amebaki mmoja na wengine wawili wamestaafu hivi karibuni na tunatarajia kuwaombea fedha zao mwezi huu wa Novemba, 2017.
Mheshimiwa Spika, baada ya Mahakama Kuu kutoa uamuzi huo, lilijitokeza kundi lingine la wastaafu wa TTCL waliokuwa chini ya Jumuiya ya Afrika Mashariki likiongozwa na Bwana L. Mwayela na wenzake 324 na kuomba kuunganishwa katika Deed of Settlement ya kesi Na 69/2005 kati ya Bwana Berekia G. Mkwama na wenzake 254 dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Kwa kuwa Mahakama Kuu iliamua pamoja na mambo mengine kuwa wafanyakazi waliofungua kesi hiyo ndiyo walipwe madai yao na kwamba Deed of Settlement iliyosajiliwa Mahakamani ilihusisha wafanyakazi waliofungua kesi hiyo tu, wafanyakazi wengine ambao hawakuwa sehemu ya kesi hiyo hawawezi kulipwa kwa kutumia hukumu na tuzo ya kesi ambayo hawakuwa sehemu yake. Kwa msingi huo, Serikali haiwezi kulipa madai mengine ambayo hayajathibitika kisheria.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-
Miradi ya Makaa ya Mawe ya Mchuchuma na Chuma Liganga imekuwa ikizungumzwa na Serikali kwa Awamu hii ya Tano na imewekwa katika Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2016-2021).
(a) Je, ni lini miradi hii itaanza?
(b) Je, ni lini Serikali italipa fidia kwa wananchi wa Mundindi na Mkomang’ombe waliotoa maeneo yao kupisha miradi hii?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kuwa miradi unganishi ya Mchuchuma na Liganga inazungumziwa sana na Serikali na imeainishwa katika Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano kama moja ya miradi ya kipaumbele. Kutokana na umuhimu wa miradi katika uchumi wa Taifa, Serikali imejipanga kuhakikisha miradi hii inaanza kwa kufuata utaratibu sahihi na kwa kuzingatia manufaa mapana ya Taifa wakiwemo wananchi wa Mkoa wa Njombe, hususan Wilaya ya Ludewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, utakumbuka kuwa mwezi Mei, 2017 wakati nikijibu swali la Mheshimiwa Ngalawa kuhusu miradi hii, nililieleza Bunge lako Tukufu kuwa Kamati ya Wataalam ilikuwa imekamilisha kupitia vivutio alivyoomba mwekezaji ili viwasilishwe Serikalini kwa lengo la kuhakikisha Taifa linapata faida zaidi.
Hata hivyo, mwezi Julai, 2017 Bunge lako Tukufu lilifanya marekebisho ya Sheria ya Madini ya mwaka 2010 pamoja na kutunga sheria mbili mpya za The Natural Wealth and Resources Permanent Sovereignty Act, 2017 na The Natural Wealth and Resources Contract (Review & Re-Negotiation of Unconscionable Terms) Act, 2017. Maelekezo ya sheria rejewa hapo juu yanakinzana na baadhi ya vifungu vya mikataba ya ubia (joint venture agreement) na mgawanyo wa hisa (Shareholding Subscription Agreement-SSA) iliyokuwa imeingiwa kati ya mwekezaji na NDC mwaka 2011.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na ukinzani wa kisheria uliojitokeza, Serikali imeunda timu ya wataalam ya kufanya majadiliano na mwekezaji ili kutafuta ufumbuzi. Timu hiyo iliyokwishaanza kazi imepewa jukumu la kufanya mapitio ya mikataba yote na vivutio alivyoomba mwekezaji ili kuainisha maeneo yenye ukinzani na kujadiliana na wabia wenza ili kuepuka kutekeleza miradi kinyume na maelekezo ya sheria za nchi. Ni imani yangu kuwa baada ya makubaliano ya mwekezaji mwenza kwenye maeneo kinzani, Serikali itatoa baraka za mwisho na mradi utaanza mara moja ikiwemo kulipa fidia kwa wananchi.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-
Tarafa ya Mwambao katika Wilaya ya Ludewa yenye Kata za Lupingu, Lifuma, Makonde, Kilindo na Lumbila hazina mtandao wa mawasiliano ya simu:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapelekea wananchi wa maeneo hayo mtandao wa mawasiliano ya simu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote inatambua tatizo la huduma ya mawasiliano katika maeneo ya Tarafa ya Mwambao. Kwa kulitambua hilo, Serikali kupitia Mfuko huo wa Mawasiliano kwa Wote imeainisha maeneo ya Vijiji vya Kata za Lumbila, Kilindo, Makonde na Lupingu na kuyaingiza katika zabuni iliyotangazwa tarehe 20 Februari, 2017. Zabuni hiyo ilifunguliwa tarehe 27 Aprili, 2017. Aidha, baada ya tathmini ya zabuni kukamilika Kata za Lumbila, Kilindo, Makonde na Lupingu zimepata mtoa huduma wa kufikisha huduma ya mawasiliano.
MHE. DEO F. NGALAWA aliuliza:-
Serikali iliamua pamoja na mambo mengine ya kulinusuru Shirika la Posta kuhakikisha jukumu la kulipa pensheni za wastaafu lililokuwa Shirika la Posta na Simu la Afrika Mashariki kwenye mojawapo ya Mifuko ya Pensheni:-
Je, Serikali itakuwa tayari kuhamisha jukumu hili kwenye mojawapo ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deo Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na jukumu la kuwalipa pensheni ya kila mwezi wastaafu wa lililokuwa Shirika la Posta na Simu la iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Kwa sasa wastaafu hao wanalipwa pensheni ya kila mwezi na Shirika la Posta na kwamba Serikali hurejesha fedha hizo baada ya shirika kuwasilisha madai yake hazina kupitia kwa Msajili wa Hazina.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Serikali haiwezi kuhamisha jukumu la kulipa pensheni wastaafu wa Shirika la Posta na Simu wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki kwenda kwenye mojawapo ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kwa kuwa zoezi la kuunganisha Mifuko ya Pensheni halijakamilika. Ni rai ya Serikali kwamba, uamuzi wa kuhamisha au kuendelea kwa sasa utaratibu wa sasa utatolewa baada ya zoezi la kuunganisha Mifuko ya Pensheni kukamilika.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-
Kumekuwa na tatizo kubwa la ukosefu wa barabara pembezoni mwa Ziwa Nyasa, hususan Wilaya ya Ludewa na Mkoa wa Njombe; eneo hilo lenye urefu wa kilomita 150 hutegemea usafiri wa meli ambao hauna tija kwa wananchi walio wengi:-
(a) Je, Serikali itawasaidia vipi wananchi wa maeneo hayo yenye vijiji 22 kupata barabara ya uhakika?
maeneo hayo yenye vijiji 22 kupata barabara ya uhakika?
(b) Kwa kuwa wananchi wameanza kutengeneza wenyewe barabara kwa nguvu zao. Je, Serikali inatoa tamko gani la kuunga mkono juhudi hizo za wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2017/2018, TARURA imetoa shilingi milioni 500 kwa ajili ya kufungua kipande cha barabara ya Mwambahesa - Makonde chenye urefu wa kilomita 3.67 na ujenzi wa daraja moja na box culvert mbili katika milima ya Mwambahesa. Tayari mkandarasi G.S. Contractor ameanza kupeleka vifaa katika eneo la mradi ili kuanza ujenzi ambao utakamilika Novemba, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, TARURA Mkoa wa Njombe inaendelea na upembuzi yakinifu katika barabara yote yenye urefu wa jumla ya kilomita 115.51 ili kuifanyia matengenezo makubwa pamoja na ujenzi wa madaraja. Kazi hiyo ikikamilika itawezesha TARURA katika Mkoa wa Njombe kupata gharama halisi na kutenga fedha kwa ajili ya kufungua na kujenga barabara hizo pembezoni mwa Ziwa Nyasa.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-
Bandari katika mwambao wa Ziwa Nyasa kutoka moja kwenda nyingine zipo kwa umbali mrefu sana hususan upande wa Wilaya ya Ludewa; hii imekuwa ni kero kubwa kwa sababu hakuna miundombinu ya barabara ambayo ingerahisisha huduma ya usafiri:-
(a) Je, ni lini Serikali itatupatia bandari katika Vijiji vya Nkanda, Nsele, Kyaghomi, Makonde na Yigha?
(b) Je, ni lini huduma za usafiri wa meli zitaanza tena ili kupunguza kero ya usafiri kwa wananchi waishio kandokando ya Ziwa Nyasa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) ina mkakati wa kuboresha na kujenga miundombinu ya bandari na gati mbalimbali katika Ziwa Nyasa. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali kupitia TPA ilitenga fedha kwa ajili ya kuendeleza Bandari za Mbambabay, Itungi, Kiwira, Ndumbi, Manda, Matema, Liuli na Lupingu Wilayani Ludewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mipango hiyo, bado kuna timu toka Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania inafanya usanifu wa awali katika vijiji alivyotaja Mheshimiwa Mbunge vya Nkanda, Nsele, Kyaghomi, Makonde, Yigha na maeneo jirani. Baada ya usanifu wa awali, Serikali itatambua maeneo gani yanafaa kuweka vituo vya kushusha na kupakia abiria na mizigo ili kuwaondolea adha abiria katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali bado inaendelea kumalizia ujenzi wa meli ya abiria itakayotoa huduma katika eneo la Ziwa Nyasa, hivyo tunatumaini wananchi watapata huduma ya usafiri wa meli kabla ya mwaka huu 2018 kwisha.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-
Bandari zilizopo Ziwa Nyasa upande wa Wilaya ya Ludewa zipo mbalimbali kutoka moja hadi nyingine hivyo kusababisha wasafiri kutembea umbali mrefu kupata huduma ya usafiri:-
• Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza bandari katika maeneo ya Nkanda, Nsele na Makonde katika Tarafa ya Mwambao?
• Je, ni lini zitajengwa gati katika bandari zilizopo Ziwa Nyasa hususani eneo la Wilaya ya Ludewa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa Mngwali, Mbunge wa Ludewa, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imepanga kuboresha na kujenga miundombinu ya bandari na gati mbalimbali katika Ziwa Nyasa. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali kupitia TPA imetenga fedha kwa ajili ya kuendeleza Bandari za Mbamba Bay, Itungi, Kiwira, Ndumbi, Manda, Matema, Liuli na Lupingu-Wilayani Ludewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zabuni za kumpata Mshauri Mwelekezi wa kufanya kazi ya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na kuandaa nyaraka za zabuni na kumpata mkandarasi atakayejenga bandari na gati hizo ilitangazwa Februari, 2018. Kazi ya Mshauri Mwelekezi tunategemea itakamilika kabla ya mwisho ya mwaka huu 2018 na kazi ya ujenzi tunategemea itaanza mapema mwaka 2019. Ni matumaini yangu kwamba baada ya kuboresha na kujenga bandari na gati hizo, wananchi wa vijiji vya Nkanda, Nsele, Makonde, Yigha katika Tarafa ya Mwambao watakuwa wamesogezwa huduma karibu na vijiji vyao.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanzisha Kituo cha Forodha katika Bandari ya Manda, Ludewa ili kurahisisha huduma kwa wananchi wanaoenda nchi jirani hasa kwa shughuli za biashara?
NAIBU WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogatias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa kufungua Kituo kipya cha Forodha unatakiwa kuzingatia Sheria ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, 2004 ambayo inaitaka nchi mwanachama kuwasilisha kwenye Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki maombi ya idhini ya kuanzisha Kituo kipya cha Forodha na hatimaye kutangazwa kwenye Gazeti la Jumuiya ya Afrika Mashariki ili kupata nguvu ya kisheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchakato wa ndani wa kuwasilisha maombi ya kufungua kituo kipya cha forodha unaanza katika ngazi ya mkoa ambapo mkoa husika unatakiwa kuwasilisha maombi ya kufungua kituo kipya cha forodha Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Baada ya Wizara ya Mambo ya nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kujiridhisha, itamfahamisha Kamishna Mkuu wa mamlaka ya Mapato Tanzania ili kufanyia kazi maombi husika kwa kuzingatia Sheria ya Forodha ya Afrika Mashariki na hatimaye kuwasilisha maombi hayo kwenye Sekretaieti ya Jumuiya ya Afika Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia taratibu za kufungua kituo kipya cha forodha hapa nchini, tunamshauri Mheshimiwa Mbunge kushirikiana na uongozi wa mkoa ili kuandaa andiko na kuwasilisha Serikalini kwa hatua stahiki.
MHE. EDWIN M. SANNDA (K.n.y. MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA) aliuliza:-

Serikali iliahidi kulipa fidia wananchi walioachia maeneo yao kupisha miradi ya makaa ya mawe, Mchuchuma na Liganga lakini mpaka sasa hawajalipwa:-

(a) Je, ni lini Serikali italipa fidia hizo ili wananchi husika waendelee na shughuli nyingine za kiuchumi?

(b) Je, kwa nini Serikali haitoi mrejesho pindi panapotokea mkwamo?

(c) Je, Serikali inaweza kuthibitisha kuwa miradi hiyo itaanza kutekelezwa kama ilivyoahidi Bungeni?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya uthamanishaji mali ya wananchi watakaopisha mradi unganishi wa Mchuchuma na Liganga awamu ya kwanza ilikamilika tarehe 18 Agosti, 2015, lakini ulipaji fidia kwa wakati huo haukuweza kufanywa. Kwa vile muda mrefu ulikuwa umepita, Serikali ilifanya uhakiki na uthaminishaji mwingine mwezi Desemba, 2018 ambapo imebainisha malipo stahiki yatakayopaswa kulipwa. Taratibu hizo zimekuwa shirikishi na zikifanywa kwa kuwahusisha Mamlaka husika ikiwemo Mamlaka za Serikali za Mitaa katika maeneo ya miradi. Malipo ya fidia kwa mujibu wa uthaminishaji wa sasa utafanywa pindi taratibu za msingi za kimaandalizi zikikamilishwa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi huo umeanza kutekelezwa kwa kufanya maandalizi ya awali ambapo pamoja na mambo mengine yanajumuisha upembuzi yakinifu wa mradi, uthaminishaji wa mali na maeneo ya wananchi watakaopisha mradi na kujenga barabara ya kiwango cha changarawe kuunganisha eneo la mradi na barabara kuu ya lami li kuwezesha kufikisha mitambo na huduma nyingine katika eneo la mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizo kasi ya utekelezaji imekuwa ndogo kutokana na changamoto mbalimbali zilizojitokeza hususan majadiliano na mwekezaji kuchukua muda mrefu zaidi kuliko tulivyotegemea. Hata hivyo, Serikali inaendelea kuangalia njia bora zaidi ya kuwezesha mradi huo kuendelea kutekelezwa kwa tija na kuleta manufaa mapana zaidi kwa wananchi wa eneo hilo na Taifa letu kwa ujumla.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-

Kumekuwa na uhakiki wa mara kwa mara wa maeneo ya watu waliopisha miradi ya Mchuchuma na Liganga:-

Je, ni lini wananchi hao waliopisha na kutoa maeneo yao watalipwa fidia?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikiri na kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa jinsi alivyo makini katika kuwakilisha wananchi wake katika mradi huu muhimu hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo tumekuwa tukijibu mara kwa mara, Serikali imeendelea kujipanga kutekeleza miradi ya kimkakati awamu kwa awamu sambamba na kuandaa wataalam wenye ujuzi wa kutosha katika kuendeleza miradi hiyo kwa tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutekeleza mradi huu muhimu wa Chuma cha Liganga chenye ujazo wa takribani tani milioni 126 na makaa ya mawe tani milioni 428 ikiwa ni pamoja na kulipa fidia kwa wananchi wanaopisha eneo la mradi, Serikali imeendelea kutafuta fedha ili kukamilisha ulipaji huo wa fidia. Nikuahidi Mheshimiwa Mbunge, Serikali itatekeleza ahadi hiyo mara pale hali ya kifedha itakaporuhusu ikizingatiwa kuwa kwa sasa iko katika majukumu mengine muhimu yanayofanana na hayo yakiwemo ujenzi wa Bwawa la Umeme la Mwl. Nyerere, ujenzi wa Vituo vya Afya pamoja na kuweka mazingira wezeshi kwa uwekezaji wenye tija unaohusisha kufanya tafiti stahiki.