Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Jaku Hashim Ayoub (3 total)

MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Spika ahsante sana. Nami nikushukuru na vilevile nikutakie afya njema na kila zito Mwenyezi Mungu afanye jepesi kwa upande wako.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali hii isingekuweko madarakani bila kuwepo wananchi na wananchi ndiyo Serikali na Serikali ni wananchi, hata Mheshimiwa Waziri Mkuu wewe mwenyewe bila kuweko wananchi usingepata Uwaziri Mkuu hata Mheshimiwa Rais pamoja na sisi Waheshimiwa Wabunge wote humu ndani.
Mheshimiwa Spika, swali, afya huwezi kupata bila kupata chakula, mwanzo upate chakula ili upate afya. Hivi sasa kumekuwa na harufu inaweza ikawa nzuri au ni mbaya.
Mheshimiwa Spika, kumekuwa na upungufu wa chakula ikiwemo bidhaa muhimu ya sukari, na sijui kama Serikali mmefanya utafiti gani kuliangalia suala hili. Msemo wa Waswahili husema, usipojenga ufa, hutajenga ukuta. Mmechukua jitihada gani kama Serikali kuangalia hali ya sukari na mchele ilivyo sasa? Na wanaoumia ni wananchi na ukizingatia kesho kutwa tuna sikukuu na inahitaji sukari kwa kiasi kikubwa. (Makofi)
Je, kuna harufu Serikali imeagiza sukari. Ni kweli suala hilo kwa ajili ya kuwajali wananchi wake?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jaku, Mbunge kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ameeleza maneno mengi lakini muhimu ni kwamba kuna harufu ya upungufu wa bidhaa ya sukari nchini. Ni kweli huko nyuma tulikuwa na tatizo la sukari nchini kote na Serikali ikafanya jitihada ya kutambua mahitaji ya nchi, na yale mapungufu tuliyafanyia kazi kwa kuagiza sukari nje ya nchi na kuleta ndani kwa kiwango ambacho hakitaathiri uzalishaji wa ndani ili tuweze kuendelea kutoa huduma hiyo. Tumeendelea kufanya hilo mpaka pale ambapo tumeridhika kwamba viwanda vyetu vya ndani vimeanza kuzalisha na kuona uzalishaji ule na sukari ambayo tumeingiza vinaweza kutufikisha tena msimu ujao wa uzalishaji.
Mheshimiwa Spika, suala la sukari hatujaishia tu kuwa na maazimio ya kuagiza toka nje. Mkakati mkubwa tuliofanya ni kuhakikisha tunaimarisha viwanda vya ndani viweze kuzalisha. Tumekutana na wazalishaji wote wa sukari, TPC, Kilombero, Kagera pamoja na Mtibwa kupata picha ya uzalishaji kwenye viwanda vyao na mkakati walionao kuendeleza uzalishaji. Lakini bado tumegundua kwamba viwanda vyetu havitakuwa na uwezo kwa kipindi cha miaka minne ijayo kuzalisha sukari ikatosheleza nchini. Lakini pia kumekuwa na wasiwasi wa takwimu za mahitaji ya sukari nchini kwa sababu nchi jirani ya Kenya yenye watu milioni 45 mahitaji ya sukari ni tani 800,000, lakini tathmini ya Idara yetu ya Kilimo nchini kwa Tanzania yenye watu zaidi ya milioni 45 ile ile wanatuambia takwimu zile zinahitaji tani 420,000; kwa hiyo utaona tuna upungufu mkubwa.
Mheshimiwa Spika, tulichokifanya; kwanza tumeagiza Wizara ya Kilimo ifanye utafiti wa kina kuona mahitaji ya sukari nchini, lakini pili kutokana na maelezo tuliyopata kutoka kwa viwanda tumewapa maelekezo ya kuzalisha zaidi ili tuongeze sukari, na tumekubaliana hilo. Tatu, tumeamua kuwekeza kwenye ujenzi wa viwanda na uhamasishaji wa kilimo cha miwa ili tuweze kuzalisha sukari inayoweza kutosheleza mahitaji ya nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tayari tumeshapata wawekezaji walioonesha nia ya kuwekeza kwenye ulimaji wa miwa pamoja na uzalishaji wa sukari nchini ili na sisi tufikie kiwango ambacho kitakwenda kutambulika baada ya Wizara ya Kilimo kufanya sensa yake. Lakini wakati wote huu Serikali itahakikisha kwamba nchi haikosi sukari na wananchi wanaweza kupata kinywaji ambacho kinahitaji sukari, uendeshaji wa sukari kwenye viwanda kwa ajili ya kuzalisha mazao yanayohitaji sukari ili tuweze kuhakikisha kwamba biashara hii na zao hili linatosheleza kwa matumizi ya ndani ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini pia Mheshimiwa Jaku ametaka kuzungumzia upungufu wa chakula na jana Mheshimiwa Keissy aliomba Mwongozo wa kutaka maelezo ya hali ya chakula nchini na bado Serikali tumeahidi kutoa taarifa hapa Bungeni kabla ya mwisho wa wiki hii ya hali ya chakula nchini na mkakati wa taifa kama kuna upungufu huo wa kiasi hicho ili sasa kila mmoja wetu nchini aelewe nafasi tuliyonayo ili tuweze kushirikiana kwa pamoja kuondoa tatizo hilo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo taarifa ambayo itatolewa na Wizara ya Kilimo juu ya hali ya chakula ikiwemo na zao la sukari inaweza kusheheneza mahitaji ya uelewa kwenye eneo hili ahsante sana. (Makofi)
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa umakini na utendaji wake na kilichonivutia zaidi anapotoka hapa akienda ofisini kwake haifiki hata dakika, watu anaokutana nao njiani anasalimiana nao ni jambo la kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri bila kujali itikadi ya chama. Ninakupongeza sana, mara nyingi huwa nikikaa nje pale na nikienda kunywa chai ninakuona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu tunakaribiwa na Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kama wiki mbili tu panapo majaaliwa tukifika, hali ya kusikitisha ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, sukari inahitajika kwa wingi matumizi yake. Hata wananchi wa Ruangwa na Peramiho wanahitaji sukari. Mwenyezi Mungu alitupa mtihani wa mvua, viwanda vyetu vya ndani havikuweza kuzalisha sukari ya kutosha na uchunguzi au harufu niliyoipata tunahitaji kama tani laki moja na ushee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kusikitisha kwa taarifa niliyo nayo ni kuwa mmetoa vibali vya tani 30,000 na baya zaidi kuna msemo Waislamu husema nguo ya Ijumaa hufuliwa Alhamisi na mvua hii pengine isikauke. Sasa hawa mliowapa vibali, sukari yao navyotegemea hata ikifika Ramadhani itakwisha, itawasaidia nini wananchi? Mnatumia utaratibu gani kuwapa vibali hawa watu, wanarudia ndiyo wale wale au na wengine? Kuna formula gani ili kuokoa hatua hii.

Mheshimiwa Waziri Mkuu uko tayari kuleta watu angalau mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani wakaingiza sukari kwa kipindi hiki ili kuokoa hii hali na janga hili lilivyo? Hii sukari mliyowapa vibali hata ikifika Ramadhani itakwisha, itasaidia nini kwa wananchi?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jaku, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, najua amezungumza mengi na yaliyotengeneza maswali mengi sana. jambo la msingi alilotaka kuzungumza hapa ni kupungua kwa sukari na mahitaji ya sukari nchini kwa sasa. Napenda niwathibitishie Watanzania kwamba Serikali iko macho na inajua maeneo gani yanahitaji kuboreshwa kulingana na mahitaji ambayo yanahitajika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa suala la sukari ni kweli nchi yetu hatuna uzalishaji wa kutosha wa sukari kutosheleza mahitaji ya Watanzania. Katika mwaka wa kilimo, mahitaji ya sukari nchini ni zaidi ya tani 420,000, lakini uzalishaji tulionao hapa nchini ni tani 320,000; kwa hiyo tunakuwa na mapungufu ya sukari inayohitajika ya tani laki moja na ikiwezekana zaidi kwa sababu ya ongezeko la watumiaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kila mwaka tunao utaratibu wa kuagiza sukari na mwaka huu pia tumesahafanya hilo, tumeshaagiza sukari na mwaka huu tumeagiza sukari tunataka tuagize sukari ya tani 131,000 kwa mujibu wa takwimu zilizofanyiwa utafiti na Bodi ya Sukari, kati ya hizo tayari tumeshaagiza tani 80, kati ya tani 80 tayari zimeshaingia tani 35 na nyingine ziko bandarini. Hizi tani 35 tumeshaanza kuzigawa kwenye maeneo yote ya nchi ili ziweze kufika kwa wananchi ziweze kusaidia kupunguza gharama na bei.

Mheshimwa Naibu Spika, pia kwa kuwa, tunakabiliwa na Mwezi Mtukufu wa Ramadhani ambapo watumiaji ni wengi, utaratibu wa kuagiza sukari zaidi kufikia malengo umeshaandaliwa. Watanzania tushirikiane kuwasihi wafanyabiashara ambao sasa hivi wamepandisha bei bila sababu na hii inaumiza sana Watanzania kwa sababu bei zilizopandishwa hazina umuhimu wowote kwa sababu uzalishaji tulionao na hii sukari pengo tunavyoleta nchini inataka tu bei zile ziendelee kuwa ambazo zinaweza kuhimilika na Watanzania wenzetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, iko mikakati ya kuongeza uzalishaji kufikia malengo. Natambua tuna viwanda vinne, Kagera Sugar, Kilombero, TPC na Mtibwa, tuna kiwanda cha tano kilichoko Tanzania Visiwani, Mahonda navyo pia vinasaidia uzalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuondoa tatizo la kuagiza sukari nje ya nchi, tumejiwekea utaratibu wa kukutana na wafanyabiashara wenye viwanda na kuwasihi kuongeza uzalishaji na tumeona jitihada kadhaa ambazo zinafanywa na wazalishaji. Bahati nzuri sana wiki moja iliyopita nilikuwa Mkoani Kilimanjaro, nimepata nafasi ya kutembelea kiwanda cha TPC ambacho kimeonesha mafanikio makubwa ya uzalishaji zaidi. Mwaka jana walizalisha tani 100,000 na sasa wameongeza tani 20,000, kwa hiyo, sasa hivi wamefikia uwezo wa kuzalisha tani 120,000 na msimu huu wa kilimo wataongeza tani nyingi zaidi, hivyo hivyo na viwanda vingine kama Kilombero na Mtibwa Sugar.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nilipofanya ziara Mkoani Manyara, nilitembelea Manyara Sugar, kwa hiyo viwanda vingi vinaendelea kujengwa na sasa tunakamilisha taratibu za kuanza ujenzi wa kiwanda cha sukari Mkoani Morogoro kuna eneo la Mbigiri kwa ushirikiano na Magereza pia na eneo la Mkulazi ambalo linaandaliwa na Taasisi ya NSSF na PPF kwa pamoja na wawekezaji ambao pia wako tayari kutuunga mkono katika uzalishaji wa sukari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwaondoe mashaka Watanzania kwamba sukari ipo na wakati wa Ramadhani sukari ya kutosha itakuwepo wala hakuna sababu ya kuongeza bei, tutafanya hivyo na pia ufuatiliaji kuona bei haziongezeki ili kuwakera Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB:Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, na vilevile nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa ziara yake aliyoifanya Tanzania nzima bila kujali mvua, jua wala kula, nami ni shahidi upande wa kula; hasa kwa upande wa pili wa Muungano; Mheshimiwa nikupongeze kwa dhati kabisa, ni Waziri Mkuu wa Tanzania ikiwemo Zanzibar na kama kuna kitu kilichonivutia Mheshimiwa Waziri Mkuu ziara uliyoifanya katika …

SPIKA: Swali lako Mheshimiwa Jaku.

MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Spika, ahsante ziara uliyoifanya katika Kiwanda cha Sukari cha Mahonda, umeiona hali ile na ukatoa maagizo. Yale maagizo uliyotoa Mheshimiwa Waziri Mkuu ni sawasawa na maagizo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kuwa sukari ile inunuliwe pale, ikiisha ndipo waruhusiwe watu kuagiza nje yaani ni maagizo sawasawa uliyoyatoa wewe. Lakini kelele za mlango hazimkeri mwenye nyumba, wewe ndiyo mwenye nyumba zile kelele ulizozikuta pale zisikushughulishe soko kubwa la walaji liko Tanzania Bara.

Je, ni lini mtafikiria angalau ile bidhaa kama zinavyotoka hapa ni saruji ikiwemo Tanga cement, Twiga, Dangote, kiboko na mabati yanakwenda katika soko dogo la Zanzibar angalau nusu yake likaja katika soko lile…?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jaku, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru kwa kutambua jitihada kubwa tunazozifanya. Si mimi bali ni Serikali yetu; imeweka huo mpango na utaratibu wa kuwafikia wananchi popote walipo. Kwa hiyo ziara zangu ni utekelezaji wa mkakati wa Serikali wa kuwafikia wananchi kule waliko.

Mheshimiwa Spika,ni kweli nimefanya ziara kwenye Kiwanda cha Mahonda Mkoa wa Kaskazini Unguja; na nimepita ndani ya kiwanda nimeona, nimeenda mpaka Bohari tumekuta sukari nyingi bado imebaki. Kiwanda kile kinao uwezo wa kuzalisha tani 24,000 na sasa hivi kinazalisha tani 6,000. Mahitaji ya Unguja na Pemba ni tani 36,000. Hata hivyo nimeikuta sukari ghalani na bado mwekezaji wetu analalamika kwamba hana soko. Kwa kweli nililazimika kuwa mkali kidogo.

Mheshimiwa Spika, wakati Serikali inahamasisha wawekezaji kuja kuwekeza hapa na tumewahakikishia kuwa na masoko na kuwalinda, lakini bado hatumpi masoko; na hatumpi masoko kwa sababu tunakaribisha sukari nyingi ya nje kuingia halafu ya ndani inabaki. Kwa kufanya hilo tutakuwa hatumtendei haki yule mwekezaji.

Mheshimiwa Spika, ni vyema; umesema kwamba unahitaji soko pia na Bara, lakini palepale ilipo inapozalishwa sukari mahitaji ni tani 36,000, lakini hizo tani 6,000 hazijanunuliwa zimebaki bohari, mwekezaji anahangaika, anatafuta masoko, haiwezekani!

Mheshimiwa Spika, na mimi nilitumia lugha ile kwamba mpango huu si sahihi, mbovu kwa sababu kwanza tungehakikisha hizi tani 6,000 za ndani zinanunuliwa halafu uagize nyingine. Kama tani ni 36,000 ndiyo mahitaji ya eneo, kwanza tani 6,000 zingetoka; na wale waagizaji basi wangepewa masharti ya kwanza kuinunua sukari ya ndani halafu unawapa kibali cha kuweka top up.Sasa kuagiza sukari yote ya nje iwe inakuja ndani haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi kama Waziri Mkuu mwenye wajibu pia hata kwa chama changu kufuatilia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi; mimi kwa pamoja na Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar ndio wenye jukumu la kufuatilia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Suala la viwanda liko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na ninapaswa kwenda popote Tanzania kufuatilia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi, sina mipaka. Sasa leo ninapokuta mahali Ilani haitekelezeki lazima niwe mchungu na nitaendelea kuwa mchungu kwa kiasi hicho.(Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, lazima tuweke mpango wa kuwalinda wawekezaji wa ndani na kuwahakikishia masoko, na masoko tunayo. Pale naambiwa waagizaji wako watatu, kwa nini usiwape masharti angalau rahisi, ndio mpango mzuri. Waambie kwanza nunua tani 20,000 chukua tani 10,000 lete na mwingine, na mwingine, 6,000 tumezimaliza. Lakini unaagiza zote kutoka nje halafu huyu atauza wapi? Haiwezekani, haiwezekani. Halafu mtu anasema nimewachefua Wazanzibar; nimewachefua Wazanzibar au nimewachefua wanunuzi? (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, kwenye hili naomba nilieleze zaidi kile Kiwanda pale Mahonda kinawanufaisha wale wananchi wa Kaskazini Unguja kwa sababu wenyewe wanalima miwa, na soko lao ni kile kiwanda. Ukichukua sukari ya nje kama hainunuliwi wale wananchi miwa wanayolima haiwezi kupata soko unawaumiza Wazanzibar. Kile kiwanda kiko pale kinaajiri watumishi 400, wanufaika ni wale walioko Kaskazini Unguja; lakini leo usipouza huyu hawezi kuajiri, hawezi kulipa mishahara kwa sababu sukari iko bohari, haiwezekani! Leo kile kiwanda kiko pale kinalipa kodi, kodi ndiyo ile ambayo imeniwezesha kwenda kuona Kituo cha Afya kule Bambi, kituo cha afya kule Kizimkazi nimeona maabara nzuri imejengwa yenye viwango pale Bwejuu, nimeenda pia Unguja, Kaskazini Pemba nimekuta VETA inajengwa nzuri kwa sababu ya fedha ya kodi ya viwanda!Haiwezekani! (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, mimi naamini Watanzania walinielewa na Watanzania hawa hata wenzangu wa Zanzibar nilichosema ni sahihi. Hao wanaotamka kwamba wamechefuliwa ni wanunuzi, na wala wasio wazanzibari. Sera yetu ni moja ya kuwalinda Watanzania, na tutaendelea kufanya hilo; tutakuwa wakali pale ambapo mambo hayaendi. Ahsante sana. (Makofi)