Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Juma Ali Juma (3 total)

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. JUMA ALI JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kupata ufafanuzi wa Ibara ya 48 ya kitabu cha Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mfuko wa Mazingira wa Dunia (Global Environment); je, sifa zipi zinazotakiwa kwa vikundi vya kijamii vinavyotarajiwa kuandika miradi midogo midogo ili viweze kunufaika na ufadhili wa G.E.F katika mwaka wa fedha. Je, katika vikundi 53 vya kijamii vilivyoshauriwa na Ofisi ya Makamu wa Rais ni vikundi vingapi kutoka Zanzibar vilifaidika na ushauri huo.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. JUMA ALI JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa uwasilishaji wake Mungu ampe nguvu ili aweze kutimiza majukumu yake katika kulitumikia Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha nimpongeze Naibu Waziri, kwa msaada mkubwa anaompa Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naunga mkono hoja asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JUMA ALI JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kutoa mchango wangu.

Kwanza kabisa naunga mkono hoja na mimi ni Mjumbe wa Kamati hiyo. Pili, nimpongeze Mheshimiwa Waziri na watendaji wake wote kwa kazi nzuri wanayoifanya katika Wizara hiyo licha ya hali ngumu ya bajeti waliyonayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina machache tu, moja nilitaka kujua na kupata maelezo juu ya Chuo cha Utafiti wa Sayansi Baharini kilichopo Zanzibar. Chuo hiki kinafanya kazi nzuri na kikiendelezwa vizuri kinaweza kikatoa matumaini ama kufufua uchumi wa nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale kuna jengo Mheshimiwa Waziri la Chuo hicho, jengo hili toka lianzishwe huu ni mwaka wa 13 bado limesimama, jengo limekuwa chaka la uhalifu na vibaka wanajificha pale. Hivyo nakuomba Mheshimiwa Waziri hebu litembelee lile jengo ulione. Tafiti za Chuo hiki zinatumiwa sana na kina mama, akina mama ndiyo wakombozi wa nchi yetu, wamesemaji waliopita hapa, kikiweza kuboreshwa hiki chuo basi tutaweza kuwakomboa akina mama. Kwa mfano, tafiti zilizofanyika kwenye chuo hiki wameweza kugundua mazao yanayopatikana yatokanayo na bahari imegundulika lulu, tunajua lulu thamani yake na faida yake kwenye nchi yetu, pia mwani wameweza kuugundua na mazao mengine mengi kabisa yatokanayo na bahari.

Mheshimiwa Waziri, tukiweza kutumia tafiti hizi vizuri tunaweza tukaendelea vizuri. Bahari ni mkombozi mkubwa kweli, kwenye bahari hakuna mafuriko Mheshimiwa Waziri, kwenye bahari hakuna ukame, sasa hivi wakulima wengi waliolima mazao mengi yamekwenda na mafuriko, lakini tukiwekeza vizuri kwenye tafiti hizi basi tunaweza tukawaomboa wananchi wetu wengi.

Kwa hiyo, mimi naomba ufanye ziara Mheshimiwa Waziri kwenye hicki chuo, pana wataalam wazuri pale, pana maprofesa, lakini ukienda unawaonea huruma ni wanyonge wamejikunja kwa sababu hawana kazi ya kufanya. Nakuomba sana Mheshimiwa Waziri tuelekee huko ili tuweze kuwasaidia wananchi wetu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine Mheshimiwa Waziri, nakuomba ukae na Wizara ya Elimu Zanzibar ili muangalie mfumo wa elimu yetu. Kwa sababu mfumo wa elimu ya Zanzibar na Bara hasa ngazi ya msingi uko tofauti, lakini tunapokuja kwenye elimu ya juu tunakutana kwa
pamoja. Kwa hiyo, hebu kaeni na Wizara ya Elimu Zanzibar mpange mkakati ambao utaweza kwenda sambamba kusudi tunapokutana huku juu kwenye elimu ya juu basi wanafunzi wetu wote waendelee kufanya vizuri. Maana kule Zanzibar sasa hivi watoto wanamaliza darasa la sita wadogo mno, lakini ukija huku wanamaliza darasa la saba, pia mitaala haiendani ya msingi wa kule na msingi wa huku mwisho wanakuja kuungana huku juu, wanafanya mitihani ya Taifa, hivyo, naomba mkae ili muweze kuliangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninarudia tena kuunga mkono hoja mia juu ya mia.