Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Godfrey William Mgimwa (12 total)

Kuwawezesha Wananchi Kupata Umeme wa Bei Nafuu
MHE. GODFREY W. MGIMWA aliuliza:-
Licha ya Serikali kupeleka umeme vijijini kwa kasi kupitia mradi wa REA, bado kuna changamoto za kuunganisha umeme kwa wananchi.
(a) Je, Serikali ina mpango gani kuwawezesha wananchi kupata umeme kwa bei nafuu?
(b) Nguzo za umeme zinasimikwa kwenye njia kuu tu; je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha nguzo hizi zinapelekwa kwenye vitongoji?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Kalenga, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuwezesha wananchi kupata umeme kwa gharama nafuu, Serikali kupitia mradi kabambe wa kusambaza umeme vijijini (REA) inaunganisha umeme kwa gharama ya shilingi 27,000 tu na hii ikiwa ni Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT).
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) imepunguza gharama za umeme kwa kuondoa gharama za malipo ya maombi ya kufungiwa umeme yaani shilingi 5,000 pamoja na malipo ya huduma ya kila mwezi (service charge) ambayo ni shilingi 5,520 kwa wateja wote wa majumbani; hatua hii imeanza tangu tarehe 1 Aprili, 2016.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kuwekeza zaidi katika uzalishaji wa umeme kwa kutumia vyanzo vya gesi asilia, joto-ardhi, jua, maji na makaa ya mawe pamoja na tungamotaka, ili kupunguza gharama za umeme zaidi.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli, nguzo nyingi zimesimikwa kwenye njia kuu, hata hivyo katika Mpango wa REA Awamu ya Tatu utakaoanza bada ya bajeti yetu kupita mwezi Julai mwaka huu, maeneo mengi ya vitongoji yatafikiwa kwa kupewa huduma ya umeme, ili kurahisisha shughuli za uchumi za wananchi wa maeneo ya Kalenga.
MHE. GODFREY W. MGIMWA aliuliza:-
Tatizo la mawasiliano ya simu katika Jimbo la Kalenga bado ni kubwa.
Je, ni lini Serikali itapeleka minara ya simu kwenye vijiji vya Kaning‟ombe, Ikungwe, Lyamgungwe, Igunda na Ikuvilo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Kalenga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua ukubwa wa tatizo la mawasiliano ya simu katika Jimbo la Kalenga. Kwa kulitambua hilo Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote iliainisha vijiiji vya Kata ya Wasa kikiwemo kijiji cha Ikungwe na kuviingiza katika Mradi wa Awamu ya Kwanza (A). Mradi huu unatekelezwa na Kampuni ya Simu ya TTCL kwa ruzuku ya dola za Kimarekani 107,968 ambapo mpaka sasa mnara tayari umeshajengwa. TTCL itaanza kutoa huduma za mawasiliano huko Kalenga mwishoni mwa mwezi Juni, 2016 baada ya kukamilisha ufungaji wa vifaa vya mawasiliano katika mnara uliojengwa.
Aidha, vijiji vya Igunda na Lyamgungwe kutoka katika Kata ya Lyamgungwe vimeingizwa katika utekelezaji wa miradi ya mawasialiano ya Viettel katika awamu ya pili na awamu ya tatu iliyoanza Novemba, 2015 na kutarajiwa kukamilika Novemba, 2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, kijiji cha Kaning‟ombe katika kata ya Mseke na kijiji cha Ikuvilo katika kata ya Luhota vitaingizwa katika miradi ya mwaka wa fedha 2016/2017 kupitia mfuko wa mawasiliano kwa wote UCSAF kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. GODFREY W. MGIMWA Aliuliza:-
Tatizo la mawasiliano ya simu katika Jimbo la Kalenga bado ni kubwa:-
Je, ni lini Serikali itapeleka minara ya simu kwenye vijiji vya Kaning’ombe, Ikungwe, Lyamgungwe, Igunda na Ikuvilo.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO Alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Kalenga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa wote iliainisha maeneo mbalimbali katika Jimbo la Kalenga na kuyaingiza katika miradi mbalimbali ya utekelezaji. Vijiji vya Igunda na Lyamgungwe kutoka katika Kata ya Lyamgungwe vimo katika utekelezaji wa mradi wa Viettel. Utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kukamilika ifikapo Novemba 2017. Aidha, Vijiji vya Ikungwe na Kaning’ombe vimeingizwa katika orodha ya miradi inayosubiri fedha ili kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2017/2018.
MHE. EDWARD F. MWALONGO (K.n.y. MHE. GODFREY MGIMWA) aliuliza:-
Tatizo la umeme bado ni kubwa licha ya jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali.
Je, ni lini Serikali itatatua tatizo hili na hatimaye kuvipatia umeme Vijiji vya Kipera, Lupalama, Itagutwa na Lyamgungwe?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Kalenga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatarajia kuvipatia umeme Vijiji vya Kipela, Lupalama, Itagutwa, Ikongwe na Lyamgungwe katika Awamu ya Tatu ya uetekelezaji wa Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini (REA III) inayoendelea kwa sasa. Aidha, kwa Mkoa wa Iringa miradi hiyo inatekelezwa na mkandarasi Kampuni ya Sengerema Engineering Group na tayari yupo katika eneo (site) akifanya upimaji wa awali kwenye vijiji tajwa pamoja na vijiji vingine 145 vya Mkoa wa Iringa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivyo tajwa inajumuisha ujenzi wa njia za umeme wa msongo wa kilovolti 33 na 11 zenye urefu wa kilometa 22; msongo wa kilovolti 0.4 yenye urefu wa kilometa 18; na uwekaji wa transfoma tisa pamoja na kuwaunganisha umeme wateja 215. Gharama ya kutekeleza miradi hiyo ni jumla ya shilingi bilioni 2.3.
MHE. GODFREY W. MGIMWA aliuliza:-
Miradi mbalimbali ya maji katika Jimbo la Kalenga imesimama kutokana na wakandarasi kutolipwa licha ya wananchi kukabiliwa na tatizo la maji.
Je, ni lini Wakandarasi hao watalipwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Jimbo la Kalenga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Iringa kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji imeendelea kutekeleza miradi mitano ya maji katika Vijiji vya Igangidung’u, Kikombwe, Weru, Mfyome, Magunga - Isupilo
- Itengulinyi - Lumuli kuanzia mwezi Juni, 2012. Gharama ya miradi yote ni shilingi 4,060,691,054 ambapo hadi mwezi Machi, 2017 kiasi cha fedha zilizokuwa zimelipwa kwa wakandarasi waliofanya kazi ni shilingi 3,027,831,071 sawa na asilimia 74.56. Hadi sasa miradi minne ya Vijiji vya Igangidung’u, Weru, Mfyome na Kikombwe imekamilika na inatoa huduma ya maji. Miradi hii ilikuwa na gharama ya shilingi 1,862,549,397 na kiasi cha shilingi 1,716,002,352 kimelipwa na kilichobaki kitalipwa baada ya kipindi cha matazamio (defects liability period) kukamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa Magunga - Isupilo
– Itengulinyi – Lumuli wenye mkataba wa gharama ya shilingi 2,198,141,657 ulisimama mwezi Julai mwaka 2015 wakati mkandarasi akiwa amelipwa shilingi 1,311,828,719 na utekelezaji wa mradi ulikuwa umefikia asilimia 45. Kutokana na kuchelewa kwa malipo, mkandarasi alifungua kesi ya madai (Adjudication na Arbitration NCC) ya kulipwa riba kwa kucheleweshewa malipo ya interest pamoja na standby cost zinazofikia shilingi 939,276,170. Halmashauri haikukubaliana na madai hayo, hivyo, mkandarasi (RJR Construction Co. Ltd) akafungua shauri la madai (arbitration NCC) na shauri limeshasikilizwa tunasubiri uamuzi wa arbitrator ili tujue hatma ya madai hayo. Ni azma ya Serikali kuendelea na ujenzi wa mradi ili ukamilike na kuanza kutoa huduma kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuleta fedha ili kuwalipa Wakandarasi kulingana na kazi zilizofanyika na kuhakikiwa. (Makofi)
MHE. GODFREY W. MGIMWA aliuliza:-
Je, ni nini tamko la Serikali juu ya idadi kubwa ya Benki za Biashara kufunguliwa kwenye miji mikubwa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Kalenga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kufuatia mabadiliko ya mfumo wa kiuchumi nchini unaotekelezwa tangu mwanzoni mwa miaka ya 1990, shughuli nyingi za kiuchumi hususan benki zinaendeshwa na sekta binafsi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa sekta binafsi lengo lake ni kufanya biashara na kupata faida, uanzishaji wa huduma za Kibenki hutegemea upembuzi yakinifu ambao unazingatia zaidi fursa za kiuchumi zilizopo katika maeneo husika, uwepo wa miundombinu wezeshi na usalama. Kiuhalisia miji mikubwa inakidhi vigezo muhimu vya uwekezaji kwa sekta ya fedha kama vile uwepo wa fursa nyingi za kuchumi, miundombinu ya kisasa na usalama ikilinganishwa na maeneo ya vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na miji mikubwa kuvutia zaidi wawekezaji wa sekta ya fedha, Serikali inajitahidi kuboresha miundombinu katika maeneo ya vijijini ili kuweka mazingira bora na salama yatakayovutia wawekezaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, sote ni mashahidi kuwa Serikali inaboresha kwa kasi miundombinu ya mawasiliano, umeme, maji na taasisi za usalama za umma ili kuhakikisha kuwa wawekezaji wanavutiwa kusogeza huduma mbalimbali zikiwemo huduma za kibenki karibu na wananchi. (Makofi)
MHE. GODFREY W. MGIMWA aliuliza:-
Mradi wa Maji wa Kalenga – Tanangozi ni wa muda mrefu na miundombinu yake imechakaa kabisa na hivyo kushindwa kukidhi mahitaji ya wananchi:-
Je, ni lini Serikali itaanza kurekebisha mradi huu ili wananchi wapate maji ya uhakika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Jimbo la Kalenga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Maji wa Kalenga
– Tanangozi ni mradi uliojengwa kwa ushirikiano wa Serikali ya Tanzania na Shirika la Kimataifa la Denmark (DANIDA) na kukamilika mwaka 1982. Mradi huo ni wa maji ya mtiririko ambao ulikuwa unahudumia vijiji 10 vyenye wakazi 12,000 kwa wakati huo. Aidha, kutokana na ongezeko la watu, taasisi mbalimbali na uchakavu wa miundombinu, maji ya mradi huo kwa sasa hayatoshelezi mahitaji ya wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua adha ya maji ambayo wananchi wanaipata kutokana na kutotosheleza kwa maji katika mradi wa Kalenga – Tanangozi, Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Iringa katika mwaka wa fedha 2017 imeweka mradi huo katika mpango wa ukarabati kwa kutumia fedha za Payment By Result (PBR). Ukarabati utahusisha sehemu zote korofi za mradi huo na hivyo kuwapunguzia adha ya maji wananchi wa Kalenga – Tanangozi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango wa muda mrefu, Serikali inaendelea kutafuta raslimali fedha za kutosha ili kukarabati mradi huo kwa kuwasilisha andiko la mradi kwa wadau wa maendeleo.
MHE. GODFREY W. MGIMWA aliuliza:-
Wananchi wa Jimbo la Kalenga katika kata na vijiji mbalimbali wamejitolea kujenga miundombinu mbalimbali ikiwemo ujenzi wa zahanati na vituo vya afya lakini hakuna wauguzi na baadhi ya vifaa tiba. Je, Serikali inaisaidiaje Halmashauri kuhusu tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey Mgimwa, Mbunge wa Kalenga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti,ili kutatua changamoto ya watumishi wa umma katika sekta ya afya, Serikali imeendelea kuajiri watumishi wa kada za afya kadri wanavyohitimu katika vyuo vya afya pamoja na hali ya bajeti inavyoruhusu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia Julai 2018/2019 Serikali imeajiri watumishi 8,447 wa kada mbalimbali za afya. Kati ya hao Halmashauri ya Wilaya ya Iringa ilipangiwa watumishi 68 ambapo vituo vya kutolea huduma za afya vilivyoko katika Jimbo la Kalenga vilipata watumishi 40. Serikali inaendelea kutoa kipaumbele cha ajira kwa watumishi wa kada za afya ili kukabiliana na upungufu uliopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la vifaatiba, Halmashauri ya Wilaya ya Iringa inapokea fedha za Mfuko wa Pamoja wa Afya ambapo sehemu ya fedha hizo zinatumika kununulia vifaa tiba. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 Halmashauri ya Wilaya ya Iringa ilitumia shilingi 21,554,700 kwa ajili ya kununulia vifaa tiba ambavyo vilipelekwa katika vituo vya kutolea huduma za afya vilivyoko katika Jimbo la Kalenga. Vilevile Halmashauri inakusanya fedha za Mfuko wa Afya wa Jamii (CHF) ambazo kipaumbele cha matumizi kinapaswa kuwa ununuzi wa dawa na vifaa tiba.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO (K.n.y. MHE. GODFREY W. MGIMWA) aliuliza:-

Taarifa mbalimbali za kitafiti zinaonesha kwamba Mkoa wa Iringa unaongoza kwa tatizo la utapiamlo:-

(a) Je, ni vigezo gani vinatumika kufikia kwenye takwimu hizo?

(b) Je, jitihada gani zinachukuliwa na Serikali kunusuru tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Kalenga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kulifahamisha Bunge lako Tukufu kuwa ni kweli kabisa Mkoa wa Iringa ni miongoni mwa mikoa inayoongoza kwa tatizo la udumavu kwa asilimia 42. Wastani wa Kitaifa ni asilimia 34, kwa mujibu wa takwimu za utafiti wa demografia na afya wa mwaka 2015/2016 uliofanywa na Ofisi ya Takwimu ya Taifa kwa kushirikiana na Wizara ya Afya Tanzania Bara na Zanzibar pamoja na Wadau wa Maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vigezo vilivyotumika kufikia takwimu hizo ni pamoja na kuchukua sampuli za kaya zilizochaguliwa kushiriki kupitia utaratibu maalum wa kitaalaam ili kuziwakilisha kaya nyingine katika Wilaya. Kwa kaya zilizochaguliwa watoto chini ya miaka mitano walipimwa urefu au kimo, uzito, kupimwa wekundu wa damu pamoja na kuhoji maswali kwa Mkuu wa Kaya au mlezi kwa kutumia dodoso maalum.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imechukua hatua mbalimbali katika kunusuru tatizo hilo ikiwa ni pamoja na kuandaa na kutekeleza Mpango Mkakati Jumuishi wa Kitaifa wa Utekelezaji wa Afua za Lishe (National Multisectoral Nutrition Action Plan) wa mwaka 2016/2017 ambayo itaisha mwaka 2021/2022 ambao una vipaumbele vinavyolenga kupunguza utapiamlo ifikapo mwaka 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kushirikiana na wadau wa lishe inaendelea kutekeleza afua za lishe zenye matokeo makubwa ambayo ni pamoja na:-

(i) Utoaji wa vidonge vya madini chuma na asidi ya foliki kwa wajawazito;

(ii) Utoaji wa matone ya vitamin A na dawa za minyoo;

(iii) Uongezaji wa virutubishi vya madini na vitamin kwenye vyakula hususani unga wa ngano, mahindi, mafuta ya Kula pamoja na urutubishaji wa kibiolojia wa mazao katika viazi vitamu, mahindi, maharage na mihogo;

(iv) Kutoa matibabu ya utapiamlo mkali kwa watoto chini ya miaka mitano;

(v) Utoaji wa elimu na huduma ya lishe kwa wanawake, wasichana na watoto wachanga na wadogo, elimu ya ulaji wa vyakula mchanganyiko na mtindo bora wa maisha; na

(vi) Utoaji wa Ajira Maafisa Lishe katika ngazi za mikoa na halmashauri.
MHE. GODFREY W. MGIMWA aliuliza:-

Jimbo la Kalenga lina vivutio vya utalii vinavyoweza kuingiza nchi yetu pesa za kigeni kama vile Isimila Stone Age na Makumbusho na Mtwa Mkwawa Mkwavinyika:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kushirikiana na Halmashauri ya Iringa Vijijini kuimarisha na kujenga mazingira na kuvitumia vivutio hivyo ili kuongeza Pato la Taifa?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Jimbo la Kalenga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Isimila Stone Age na Makumbusho ya Mtwa Mkwawa yanasimamiwa na Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) ambapo Shirika lina jukumu la kuhifadhi na kuendeleza vituo hivi. Aidha, kwa kuzingatia changamoto zilizopo katika vituo tajwa, Wizara kupitia Mradi wa Kusimamia Maliasili na Kuendeleza Utalii, Nyanda za Juu Kusini yaani (Resilient Natural Resources for Tourism and Growth - REGROW) na kwa kushirikiana na Halmashauri za Mkoa wa Iringa, itaimarisha miundombinu hiyo. Kwa kupitia mradi wa REGROW maeneo haya yataboreshwa ikiwa ni pamoja na kujenga ituo cha Kumbukumbu na Taarifa ili uhifadhi Kumbukumbu ya Mtwa Mkwawa na utamaduni wa Wahehe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sanjari na hatua hiyo, Wizara kwa kushirikiana na Mkoa wa Iringa pamoja na Chuo Kikuu cha Iringa imekarabati boma la Mjerumani na kulifanya kuwa Makumbusho ya Mkoa. Aidha, Wizara ilitoa wataalam wa ujenzi kuandaa na kupanga vioneshwa ndani ya makumbusho ya jengo hilo, duka la zawadi, mgahawa na studio ya kurekodi nyimbo za asili. Mapato yatokanayo na jengo hilo yanaingia katika Mkoa wa Iringa.
MHE. PAULINE P. GEKUL (K.n.y. MHE. GODFREY W. MGIMWA) aliuliza:-

Tatizo la ukosefu wa nyumba za Walimu kwenye maeneo mengi ya Jimbo la Kalenga kumesababisha Walimu kuhama na hivyo kudhoofisha ukuaji wa elimu kwa ujumla: -

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuisaidia Halmashauri ya Iringa Vijijini ili kuhakikisha inajenga nyumba za kutosha kwa Walimu?

(b) Mapato ya ndani ya Halmashauri hii hayatoshi kujenga nyumba za Walimu. Je, nini mkakati wa Serikali juu ya tatizo hili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Kalenga lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali tayari imetoa Shilingi milioni 50 kwa ajili ya ukamilishaji wa ujenzi wa nyumba 2 za walimu katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa. Serikali inaendelea kutafuta fedha kupitia vyanzo mbalimbali kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya shule zikiwemo nyumba za walimu.

(b) Mheshimiwa Spika, Mkakati wa Serikali ni kuziwezesha halmashauri kuandaa maandiko ya miradi ya Kimkakati itakayoongeza mapato ya halmashauri ili kukidhi mahitaji yaliyopo ikiwemo ujenzi wa nyumba za walimu. Aidha, Halmashauri zimeelekezwa kubuni vyanzo vipya vya mapato na kuimarisha makusanyo ya mapato ya ndani na usimamizi wa vyanzo vilivyopo ahsante.
MHE. GODFREY W. MGIMWA aliuliza:-

Barabara ya Kalenga kuelekea Ruaha National Park ni ya muhimu sana kwa uchumi wa Jimbo la Kalenga, Iringa na Tanzania kwa ujumla:-

Je, Serikali ina mpango gani juu ya kuitengeneza barabara hiyo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Kalenga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Kalenga kuelekea Ruaha National Park ambayo inajulikana kama barabara ya Iringa – Msembe ni barabara ya mkoa inayosimamiwa na Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Iringa. Barabara hii ina urefu wa kilometa 104, kati ya hizo, kilometa 18.4 zimejengwa kwa kiwango cha lami na kilometa 85.6 zimejengwa kwa kiwango cha changarawe.

Mheshimiwa Spika, barabara hii inaunganisha Makao Makuu ya Mkoa wa Iringa na Mbuga ya Wanyama ya Ruaha na inapita katika maeneo muhimu ya Makumbusho ya Mkwawa na maeneo mengine yenye kilimo cha mpunga na mahindi.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), imekamilisha kazi ya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na kuandaa makabrasha ya zabuni kwa ajili ya kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami na kazi hii imefanywa na Kampuni ya ENV Consult (T) Ltd ya hapa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2019/ 2020, jumla ya shilingi billioni 4.221 zimetengwa kwa ajili ya maandalizi ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara hii kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.