Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Venance Methusalah Mwamoto (25 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nianze kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia. Nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kweli kwa kunifanya niwe mzima mpaka leo lakini niwashukuru sana Wananchi wa Kilolo ambao wamenirudisha baada ya miaka kumi kutoka hapa ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Mheshimiwa Rais iko vizuri na jana wenzetu walipotoka nje, bahati nzuri mimi nilipata bahati ya kuwa wa kwanza kutoka lakini kikubwa kilichofanya watoke ni kwamba hawana sehemu ya kuchangia. Sasa kwenye ile hotuba kama hauna sehemu ya kuchangia itakuwa siyo rahisi ubaki humu ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili wenzetu wanataka kuonekana Live. Mimi nilikuwa Mkuu wa Wilaya ya Kibondo, kuna watu walikuwa wanajua kuzungumza humu ndani mnawajua sitaki kuwataja na ilikuwa wakati anachanga unakuta vikundi vimeshajikusanya ukiuliza kuna nini wanakwambia leo jamaa anaongea na anataka kumchana live Waziri Mkuu, sasa nafasi hiyo haipo tena.
Kwa hiyo, wenyewe wanataka kuendelea kucheza live humu ndani lakini ukiangalia maendeleo kwenye maeneo yao hakuna, na walio wengi ninyi wenyewe mnahakika kabisa hawakurudi waliokuwa wanazungumza sana humu ndani. Wananchi wanataka maendeleo. Wanataka live kwenye maendeleo siyo live kwenye TV.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi binafsi kwa kweli kwa muda ule ambao umependekezwa ni muda ambao wananchi wengi kweli watakuwa wanaweza kuona kinachofanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwenye suala la maji. Wilaya ya Kilolo, Tarafa ya Mazombe - Ilula kuna tatizo kubwa sana. Mimi nina hakika mwaka 2000/2005 nilipokuwa Mbunge, tulipewa ahadi na Mheshimiwa wakati huo Rais Mkapa suala la maji, bahati nzuri haikuwezekana, wananchi walinihukumu wakanipa likizo, na mwenzangu aliyechukua nafasi yangu aliingia akapewa ahadi nzuri na Rais aliyekuwepo, naye inawezekana ni sababu hiyo hiyo amepewa likizo, sasa juzi alipifika Mheshimiwa Rais kuja kuomba kura tukamwambia sehemu moja nzuri anayotakiwa kwenda ni sehemu ya Ilula ambayo ina tatizo la maji. Aliahidi kwamba suala hilo analichukua, na ana hakika kabisa asilimia 100, akawaambia wananchi kwamba nirudishieni Mwamoto na nipeni kura, suala la maji limekwisha. Nitawaletea Waziri ambaye anajua matatizo ya maji.
Mheshimiwa Lwenge naomba uandike vizuri hiyo, kwa sababu ili uende kwenu kwenye Jimbo lako ni lazima upite Ilula. Huwezi kunywa maji, huwezi kupita Ilula. Uhakikishe maji yanapatikana na ni ahadi ya Mheshimiwa Rais. Sasa hivi ukienda pale ukimsalimia mtu wa Ilula, maana yake sisi huwa tunasalimiana kule kilugha kamwene, anakwambia maji, ukimwambia kamwene anakwambia maji, ukimwambia kitu chochote anakwambia maji, hapa kazi tu, maji. Sasa dawa yake ni kutoa maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, na ukikaa Ilula ukitaka kupanga chumba unapanga vyumba viwili kama unaanza maisha, unapanga chumba kimoja kwa ajili ya madumu ya maji na chumba kimoja kwa ajili ya kulala wewe. Sasa mimi nawaomba, kwa sababu ni ahadi ya Rais na Mheshimia Lukuvi naomba unisaidie, mimi mdogo wako nipo nisiondoke tena unisaidie maji na maji mengine kwako kule tutakuletea.
Mheshimiwa Naibu Spika, Ilula hakuna tatizo la maji, tatizo lake ni mgawanyo wa maji, maji yapo mengi, kuna mito mingi pale lakini unaifikishaje kwa wananchi ndiyo tatizo. Kwa hiyo, mimi naomba, Mheshimiwa Lwenge tuende pamoja.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni suala la barabara. Kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, iko wazi kabisa kwamba kila Wilaya barabara itaunganishwa kwa lami mpaka Makao Makuu ya Mkoa, lakini pia na kufanya uwezekano mkubwa na kuunganishwa na Wilaya nyingine.
Wilaya ya Kilolo toka mwaka 2002 mpaka sasa katika kilomita 35, kilomita zilizojengwa kwa lami ni kilomita saba, sasa sielewi ni kwa nini. Kwa hiyo kwa kuwa Profesa Mbarawa nilishazungumza naye, tutaona jinsi ya kutusaidia, lakini ni pamoja na kutuunganisha ile barabara ya TANROAD inaishia Idete, tulishaipitisha kwenye mpango wa barabara ya TANROAD kwamba iishie sasa Muhanga ili tuunganike na watu wa Morogoro, kwamba itoke Kilolo - Dabaga - Idete - Itonya ifike mpaka Muhanga ili tuende mpaka Mbingu kule Kilombero, Morogoro tuweze kuunganisha nao ili tuweze kufungua uchumi wetu kwa sababu uchumi wa Kilolo unategemea sana Kilimo na ili wananchi wale wapate fedha inabidi wauze mazao yao yale lakini kama barabara zitakuwa ni shida watanyanyaswa, watauza mazao yao kwa bei ambayo haifai.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni suala la pembejeo za kilimo. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo alifika Iringa na tukamwambia matatizo ya pembejeo. Lakini tatizo la Pembejeo Mheshimiwa Waziri wa Kilimo naona unanisikia, naomba hebu washikirishe Wakuu wa Wilaya kwenye suala hili la usambazaji wa pembejeo na ikiwezekana Wakuu wa Wilaya wasiwe Wenyeviti wa pembejeo kwa sababu wao ndiyo wanatakiwa wasimamie, kwa hiyo linapotokea tatizo hakuna wa kumuuliza! Mkurugenzi yupo mle, Mkuu wa Wilaya yupo mle, wao wasimamie tu mwenendo mzima wa pembejeo kwa sababu kuna ujanja mwingi sana kwenye pembejeo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi ndiyo wanapeleka mbegu Kilolo wakati sasa hivi ni wakati wa kupalilia, wanatakiwa wapeleke mbolea ya kukuzia, kwa hiyo kuna matatizo pale, tunaomba utusaide. Lakini pia na bei ya mbolea iko juu sana, tuangalie uwezekano wa kupunguza kama ni kodi, kama mambo mengine basi yapungue.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia suala la Mabaraza ya Kata. Mheshimiwa Waziri wa Sheria yupo, TAMISEMI yupo, Utawala Bora yupo, Wizara ya Mambo ya Ndani yupo. Mabaraza ya Kata kuna tatizo, tatizo ambalo lipo wanaoendesha hayo Mabaraza uwezo wao ni mdogo, hawapati mafunzo, lakini kazi ile ni kubwa sana na wamesaidia sana kutatua migogoro.
Kwa hiyo mimi nikuombeni tusaidiane kwenye hilo sambamba na madawati ya jinsia. Mheshimiwa Kitwanga, madawati ya jinsia yamesaidia sana kupunguza kero nyingi sana lakini matatizo ambalo lipo, yale Mabaraza ni vema ofisi zikawa kwa Mkuu wa Wilaya, kwa sababu watu walio wengi Mheshimiwa ukipigwa kibao na mke wako unaona aibu kwenda Polisi lakini ikiwa kwenye Baraza anahisi ni sehemu ya usuluhisho kwa hiyo inakuwa rahisi kwenda na kutoa elimu. Maana yake madawati ya jinsia siyo wanawake peke yake, hata wanaume. (Makofi)
Mimi naomba ikiwezekana tuma watu wako waende pale Kibondo wakaone lile Dawati linavyoendeshwa na kesi nyingi pale ni za wanaume kushtaki kwa kupigwa tena. Kwa hiyo unaona jinsi ambavyo elimu imefika kule. (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho ni suala la ujenzi wa ofisi, Wilaya ya Kilolo toka mwaka 2002 tumekuwa Wilaya lakini Mheshimiwa Kitwanga huna hata jengo moja ambalo limejengwa. Huna Makao Makuu ya Polisi ya Wilaya, huna nyumba ya Polisi Wilaya ya Kilolo. Kwa hiyo mimi naomba, baada ya Bunge hili mimi tutakwenda pamoja na nitachangia na mafuta maana haukuwa mpango wako ili tuende ukaone hali jinsi ilivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia na suala la hospitali hamna hospitali Wilaya ya Kilolo. Majengo yapo pale lakini mpaka leo hakuna hospitali ya Wilaya na kuna majengo ambayo wananchi wamejitolea wamejenga zahanati lakini hazijaisha, wamejenga vituo vya afya havijaisha, ukiwauliza wanakuambia bajeti tuliomba lakini tumeletewa bajeti finyu. Kwa hiyo nafikiri Mheshimiwa Kigwangalla tusimsumbue Mheshimiwa Waziri, tuende ukaone hali jinsi ilivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa muda bado ninao, kuna hili sula la uchangiaji wa elimu ambapo Mheshimiwa Rais amefuta...
Mheshimiwa Naibu Spika, basi naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza Waziri na Naibu Waziri wake. Ningependa kuchangia kuhusu suala la mbegu za mahindi zinazotumika kwa sasa, ningependekeza utafiti ufanyike ili tuweze kupata mbegu mpya. Kwani ni mbegu ambazo zinatumika sasa ni za muda mrefu zimechoka sana. Ukilima ekari moja unategemea kupata gunia siyo chini ya gunia 35, lakini mbegu hii iliyopo ukipata gunia nne ni bahati. Hivyo ni vema Serikali ikafanya utafiti kutumia vyuo vyetu ili tupate mbegu bora. „Kama ukitaka mali utaipata shambani’.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishauri suala la umwagiliaji litiliwe kipaumbele kwani tumeshuhudia mwaka huu mvua nyingi zimenyesha lakini sikuona jitihada za Serikali na hasa Wizara yako na Wizara ya Maji kuweza kuvuna maji ambayo tumeshuhudia maji mengi yakipotea bure.
Mheshimiwa Waziri hata suala la migogoro ya wakulima na wafugaji, tatizo siyo ardhi tatizo ni utengaji wa maeneo ya mifugo kupata sehemu ya kwenda kunywa maji. Hivyo endapo itatenga na kujenga mabwawa kwa ajili ya umwagiliaji na sehemu ya kunyweshea mifugo suala hili la migogoro ya wafugaji na wakulima litapungua sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho ningeomba sana Wizara ya Kilimo, iweze kumsaidia mkulima itabidi Wizara yake kushirikiana na wadau kuona jinsi ya kumaliza suala la Lumbesa, wakulima wanapata tabu sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuchangia kwa kupongeza hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Ningependa kujua sababu ambazo zimefanya kiwanda cha Chai-DABAGA kutofanya kazi sasa ni miaka zaidi ya 15 wakati wananchi wanalazimishwa kulima chai, nitaomba ufafanuzi.
Ningependa nijue hadi sasa Serikali imejipanga vipi kuwawezesha wazawa zaidi kupunguza ukiritimba ili waweze kujenga viwanda vya matunda na nyanya katika sehemu za Ilula ambako nyanya nyingi zinapatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Iringa kiwanda cha usagishaji cha N.M.C kilichopo Iringa Mjini kimekuwa kikifanya kazi kwa kusuasua. Ninaomba Mheshimiwa Waziri wewe mwenyewe ufike Iringa na utembelee Kiwanda cha Chai-DABAGA-Kilolo na Kiwanda cha usagishaji ili uone hali iliyopo pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba Waziri na Wizara yake wawasaidie wananchi, wakulima kuona uwezekano wa kuleta sheria ambayo itamsaidia mkulima kuweza kuuza mazao yao sokoni na kwa kutumia mizani na siyo lumbesa. Tumeshuhudia hata viwanda vimekuwa vikinunua mazao ya wakulima kwa bei ndogo tena bila kutumia mizani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba Mheshimiwa Waziri amtembelee Mtanzania Mzee Sallawa George aliyegundua jinsi ya kutengeneza Ulanzi na kuweka kwenye chupa bila kuharibika. Ninaomba Wizara yako imsaidie ili utaalamu wake usipotee. Wenzetu wa Kenya wanatengeneza juice ya Ulanzi, Bamboo Juice na mimi nitakuwa tayari kumuwezesha Mtanzania huyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nichangie hoja hii. Mimi ninatoka Wilaya ya Kilolo ambayo iko Mkoa wa Iringa, Hifadhi ya Udzungwa asilimia kubwa ipo katika Wilaya ya Kilolo japo Makao Makuu yapo Morogoro. Kuna vijiji ambavyo vinapakana na Udzungwa National Park. Vijiji vya Msosa, Ikula, Udekwa, Mahenge, Wotalisoli na kadhalika kuna tatizo kubwa la mamba, tembo hasa katika kijiji cha Msosa. Kwa sababu maji ya Mto Lukosi ndiyo yanayosababisha wananchi wengi kuliwa na mamba na pia kuuliwa na tembo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi:-
(1) Tunaomba Wizara iangalie utaratibu wa kujenga post (Kituo cha ulinzi wa vijiji vile pale Msosa), kujenga miundombinu ya maji yaani tanki la maji na kusambaza kijiji kile ili kupunguza ajali za mamba.
(2) Ujenzi wa barabara ya kutoka kijiji cha Mahenge kwenda Udekwa, kilometa 25 tu.
(3) Kuna mapango makubwa katika kijiji cha Udekwa ambayo ni kivutio kwa watalii wa ndani na nje, ningeomba wataalam wafike waone.
(4) Kutelekezwa kwa kivutio cha Kalenga, sehemu ambayo kichwa cha Mkwawa kimehifadhiwa, familia ya Mkwawa wanalalamika na kuna uwezekano mkubwa wa kuomba kukizika kichwa kile.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipongeza sana Wizara hii kwa kazi nzuri inayoendelea. Ilani ya CCM inaelekeza vizuri kuwa barabara zilizounganisha wilaya na mikoa zitajengwa kwa lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anaijua hii barabara ya Iringa – Kilolo – Dabaga – Idete. Mheshimiwa Waziri alifika Kilolo anaijua; ipo kama kilometa 27, lakini barabara hii kilometa tano ni za Jimbo la Iringa na kilometa 15 ni Jimbo la Kalenga na kilometa saba ni Kilolo. Hizi zote kwa pamoja ndiyo unapata barabara ya Iringa – Kilolo – Dabaga – Idete. Barabara hii ina mchango mkubwa kwa uchumi wa Taifa, ndiko ambako mbao nyingi zinatoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila nilipouliza swali kuhusu barabara hii jibu linakuwa la kutia matumaini lakini utekelezaji wake hakuna. Naomba sana barabara hii itengewe fedha ili ianze kujengwa kwa kiwango cha lami. Barabara ambayo inatakiwa ipandishwe daraja ni Dabaga
- Ng’ang’ange, Bomalang’ombe – Mwatasi – Mufindi. Vikao vyote vilipitisha ombi la barabara hii. Hivyo tunaomba barabara hii ipande daraja iwe ya mkoa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi hii ili niweze kuchangia leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nianze kwa kupongeza Wizara hii kwa jinsi ambavyo kwa kweli wameandika vizuri, kama tungelipata muda mrefu wa kuweza kusoma hiki kitabu, nafikiri michango yetu ingepungua kwa sababu kimeandikwa vizuri sana na maeneo yote yameguswa, na ukisoma unaona kweli Serikali imedhamilia kutuingiza kwenye uchumi wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo leo kazi yangu kubwa hasa ni kushauri, lakini kabla sijaanza kushauri pia niipongeze Serikali jana nilitoa taarifa hapa kwa Waziri wa Kilimo kwamba kuna paka ameingia kule Ilula, amejeruhi zaidi ya watu saba na alikuwa anajeruhi sehemu ambazo anazijua yeye, jana timu imetumwa na kazi imefanyika, kwa hiyo, naipongeza hii Serikali kweli hapa kazi tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema mimi nitaenda kwenye ushauri, ukiangalia dhana nzima ya Serikali yetu tumejikita kwenye uchumi wa viwanda, walioteuliwa wataalamu kwenda kwenye Wizara ile wote ni makini, lakini kitu ambacho ninaomba ni kimoja nitatoa mfano, Wahehe mimi natoka Iringa, Mhehe na Mgogo, Mhehe akiongea Kihehe, Mgogo anaelewa na Mgogo akiongea Kigogo, Mhehe anamuelewa, tatizo linakuwa Mhehe anapotaka kuongea Kigogo na Mgogo anataka kuongea Kihehe wanapotea njia. Maana yangu ni nini, mwanasiasa ninyi wataalam wa Wizara hii ongeeni kitaalam, msianze kwenda kwenye siasa mkiongea kitaalam sisi wanasiasa tutajua mnachozungumza na sisi wanasiasa hatuwezi kuingilia kwenye utaalam wenu tutaongea kisiasa mtatuelewa, lakini tatizo linakuja pamoja na mipango mizuri tukiingiza siasa mtataka kuwa wanasiasa, mkiashaingiza siasa mipango yote mizuri itaaribika.

Kwa hiyo, naomba mjikite Mheshimiwa Mwijage nakufahamu vizuri, ulipokuwa unasoma Tosamaganga ulikuwa unaitwa kijiko cha jikoni hakiogopi moto, sasa huo moto wako kweli upeleke. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajenga viwanda, mwanzo ni ujenzi wa viwanda, unapojenga viwanda kuna vitu ambavyo unatakiwa uwe navyo ni pamoja na malighafi. Watu wa Mchuchuma ndugu yangu pale amezungumza sana tunajenga viwanda tumejitayarisha? Sasa ilikuwa ni wakati muafaka kuhakikisha chuma chetu kile tunakiandaa ili tuweze kukitumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni wakati sasa wa kutumia malighafi nitatoa mfano mzuri, tupo kwenye ujenzi wa Makao Makuu ambapo kiasi kikubwa cha mbao zinatoka Wilaya ya Kilolo, mimi naomba Mheshimiwa Rais najua anasikiliza na anafuatilia, asilimia 75 zinatoka Kilolo na Mufindi, lakini miundombinu ya Wilaya ya Kilolo barabara siyo rafiki?

Sasa Wizara ya Viwanda naomba utoe ushauri kwa Wizara ya Miundombinu wahakikishe ile barabara inaweza kutengenezwa ili iwe rahisi kusafirisha mbao ambayo ni malighafi ya kujenga viwanda na itasaidia kupunguza gharama. Bila kufanya hivyo utakuwa hujatutendea haki. Mimi ninaomba tu Mheshimiwa Rais huko aliko anasikia siyo mbaya akiamua kuahirisha sikukuu moja zile fedha zikaenda zikajenga barabara ya kutoka Iringa mpaka Kilolo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine ambalo ningependa kulisemea ni Ilula Wilaya ya Kilolo tumejenga Kiwanda cha Nyanya, lakini kiwanda cha nyanya kile nyanya tunalima sehemu oevu ambayo maji yanatuama ili tuweze kupata mazao vizuri, leo hii imekuja tafsiri mbaya sana wanasema kwamba wananchi wasilime kwenye vyanzo vya maji. Sasa tafsiri ya vyanzo vya maji Mheshimiwa January Makamba upo mimi nakuomba Jumapili nipo tayari hata kukuchangia hata mafuta uende, tatizo ni kubwa, sivyo vile ambavyo unafikiria.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu sasa hivi wananyanyasika tunaita kilimo cha vinyungu, Mheshimiwa Chumi amepiga kelele, Waheshimiwa wa Wilaya ya Mufundi wamepiga kelele na mimi napiga kelele, tusaidie kwa sababu tukilima nyanya ndizo ambazo tutapeleka kwenye kiwanda. Sasa hatujatengeneza miundombinu mizuri ya kuwawezesha watu wa Kilolo na sehemu nyingine waweze kuzalisha ili wapeleke kwenye kiwanda sasa hatujatengeneza miundombinu mizuri ya kuwawezesha watu wa Kilolo na sehemu nyingine waweze kuzalisha ili wapeleke kwenye kiwanda, bila kufanya hivyo uchumi utatoka wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mwijage shirikiana Mheshimiwa January Makamba nami namuomba ikiwezekana kama haiwezekani toa kauli waache kuwasumbua wananchi tuweke mipango kwanza. Shirikiana na watu wa kilimo watengeneze miundombinu ya umwagiliaji lakini leo unavyosema chanzo cha maji Wilaya ya Kilolo au Mkoa wa Iringa ambao unasifika nchi hii kwa kutunza vyanzo vya maji, sasa leo unavyokwenda kuwabugudhi ni sawa sawa ukiwa na kuku anayetaga mayai ya dhahabu ukimsumbua utakosa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba utusaidie katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine ambalo ningependa kulizungumza Mheshimiwa ni mpango wa SIDO. Kwa kuwa tunakwenda kwenye viwanda, tujikite sasa kuhakikisha kwamba kila Wilaya angalau tunawatayarisha watu kwa kuwa na SIDO, kama usipowatayarisha watu ambao wanakwenda kwenye utekelezaji wa viwanda usitegemee kama tutapata chochote, lakini Mheshimiwa ninakusifu, ukiangalia na ukitaka kujua kazi nzuri ya Wizara yako ukienda ukurasa wa 107 kwenye malengo mambo yote mazuri yamezungumzwa humo kwa hiyo tujikite pake tusome na wengine wanabeza hapa wanasema viwanda havipo. Nenda kwenye ukurasa wa 167 utaona orodha ya viwanda, ukishaona orodha ya viwanda ambavyo viko kila mkoa nenda kwenye Mkoa wako kaulize.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu ambacho kinatusumbua Mheshimiwa Waziri ni tafsiri ya viwanda, unaposema viwanda una maana gani, ndipo hapo ambapo kuna kuwa na ukakasi kidogo. Pia Mheshimiwa Waziri Mwijage, hivi viwanda ambavyo tunanaza kuna vingiine ambayo wanaweza kuanzisha Watanzania, leo hii ukienda pale kuna Wachina wanauza juice, wanauza ice cream wewe kama Waziri unasemaje, maana yake ni viwanda watakuambiwa ni viwanda vile. Kwa hiyo, utusaidie Mheshimiwa Mwijage vile viwanda ambavyo vinaweza kuanzishwa na Watanzania basi vianzishwe na Watanzania wenyewe bila kujali mambo yanakwenda vipi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo ningependa kulizungumza ni suala la kilimo, Mheshimiwa Rais, anatuletea trekta nimesikia zaidi 2000 shirikiana na Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi kuna trekta zile ambazo zilitolewa mwanzo lakini leo hii wananchi wanaanza kunyang’anywa tena, hii haipendezi, tuweke tu mkakati mzuri kwamba wananchi wanazitumia zile trekta ili tuende kwenye kilimo.

Kiwanda cha ngozi mmezungumza vizuri, kwamba leo hii wafugaji nyama haina thamani, ngozi hazina thamani, ngozi ilikuwa inauzwa shilingi 4000 leo hii kwa kilo ngozi ni shilingi 2000 hazina thamani tena, sasa tusipoelekeza nguvu yetu kwenye viwanda kama hivyo matokeo yake tutaendeleza ugomvi wa wakulima na wafugaji wakati suluhu unazo wewe Mheshimiwa Mwijage.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumzie habari ya migogoro ya wakulima na wafugaji, mtu ambaye anaweza akatusaidia ni Waziri wa Viwanda kwenye jambo hili, ukishirikiana na Waziri husika, tukatenga maeneo haya ni ya viwanda, haya ni ya kilimo, haya ni ya mifugo ugomvi hautakuwepo na kutoa thamani kwenye mazao yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha Nyuzi, kwa mfano Kiwanda cha Pamba huwezi kujenga Iringa na ndiyo maana nilisema siasa, unaweza ukafanya siasa kikajengwa Iringa, leo hii pale sisi Ilula mmetujengea kiwanda cha nyanya lakini bado tunahitaji kiwanda kwa ajili ya vitunguu, tunahitaji kiwanda kwa ajili ya juice na mambo mengine ili wananchi wale wapate ajira, lakini ukisema tu viwanda vijengwe halafu havina muungozo itakuwa ni shida. Pia kuna athari za viwanda kwa sababu kuna mambo ya hali ya hewa lazima kuzingatia, kwa sababu unaweza kukuta baadae tumefika mwisho hali ya hewa, mazingira yanachafuka na watu wanaanza kupata athari mbaya, sasa hilo pia uzingatie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho ambalo ningependa kuzungumza ni kwamba tuangalie kwamba kiwanda hiki kinajegwa wapi na hiki kinajengwa wapi ili tuende sambamba na ukuaji wa uchumi kwa kutumia viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nianze kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia kidogo. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa mambo makubwa ambayo ameyafanya. Baada ya hapo nianze kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Naibu wake. Mimi niseme, imenitia moyo sana baada ya kuona upande mwingine unapigwa madongo. Ukiona upande mwingile ule unasifiwa ujue kazi huwezi. Sasa maana yake kazi yako ni nzuri, wewe endelea kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri ambayo amefanya katika kubadilisha baadhi ya Watendaji wa TRA ambako muda mrefu kumekuwa kukilalamikiwa. Sasa hivi mmeboresha, kuna mabadiliko makubwa ambayo tunayaona sisi ambao tuna macho, yanaendelea kufanyika. Kilio cha watu ambacho walikuwa wanalia cha jinsi ya style ya ukusanyaji bila kutumia mfumo imeanza kupungua na malalamiko ya watu yamepunguza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana utakuta fedha ambazo zitakusanywa mwezi huu zitakuwa zimeongezeka kiasi kikubwa sana. Hata ushauri aliompa Mheshimiwa Rais akutane na wafanyabishara, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, utamsaidia sana. Kwa sababu walikuwa wanakosa sehemu ya kwenda kuzungumza shida zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwamba, kuna Wizara ambazo zimefanya vizuri hasa tukienda kwenye nchi ya viwanda. Mimi nianze na Wizara ya Ardhi. Niseme Wizara ya Ardhi, wamefanya kazi kubwa sana, kwa sababu ukisema unataka maendeleo, unaanzia kwanza kwenye ardhi. Kesi, malalamiko kwenye Wizara ile sasa hivi yamepungua. Watu wamepewa hati na zimeonyesha thamani, wanaweza kukopa na kuzungusha fedha ambazo baadaye zinarudi kwenye mzunguko wa uchumi. Wizara ya Madini baada ya kukutana na Rais, kuna mabadiliko makubwa yameonekana na kodi sasa zinakwenda kukusanywa.

Mheshimiwa Naibu Spika, bila kuwa na nishati ya uhakika siyo rahisi pato la Taifa likaongezeka. Tumeona wenyewe, kama tunalalamika, basi ni vijiji vichache ambavyo havijafikiwa. Kikubwa zaidi naomba tu kwaMheshimiwa Waziri wa Fedha, ukizungumza nishati unazungumza habari ya usambazaji umeme vijijini na unazungumza habari ya nguzo; na ukizungumza habari ya nguzo ujue asilimia 45 zinatoka Wilaya ya Kilolo ambako barabara zake ni mbovu. Kwa hiyo, namwachia Mheshimiwa Waziri, tutaongea maana yake leo hatuji kuomba fedha, tutajua jinsi ya kuzungumza naye.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna vitu ambavyo inabidi tuzungumze, kama nilivyosema, ukiwa na ardhi, umeme, watumishi, maji na usafirishaji, unazungumza habari ya kuinua uchumi. Nimesema Wizara ya Ardhi inakwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa umeme, bwawa la maji tunajenga, litaongezea nguvu kule. Tutakuwa tunaongeza nguvu kwenye umeme, lakini kwenye umwagiliaji. Kwa upande wa maji, naishukuru Serikali na Bunge letu kwa kuamua kuunda Wakala. Tukipata Wakala wakawa na bodi yao wamejitegemea kama ilivyo TANROAD, tutafanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika usafirishaji, kama ambavyo tumeona standard gauge na ndege, kazi inaendelea. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali kwa kazi kubwa ambayo imefanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii, niwapongeze sana timu yetu ya Taifa ambao jana wamefungwa kule Misri. Ukiangalia tathmini, walicheza na timu ya Senegal. Timu ya Senegal, thamani ya timu ile kwa wachezaji ni pound milioni 380. Timu yetu thamani yake ni pound milioni 14. Sasa unaona tofauti yake. Maana yake timu ya Senegal thamani ukizipeleka kwenye fedha za Kitanzania ni trioni 1.1, wakati thamani ya timu yetu ni bilioni 44. Hii inakuja vipi?

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Cecil Mwambe.

TAARIFA

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu nimpe taarifa msemaji kwamba kama haya tuliyajua, sasa kwa nini tuliamua kupeleka timu yetu badala ya kujipanga na sisi tukafikia hapo walipotaka wengine? (Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwambe, ungemwacha amalize hoja yake ili uelewe. Sasa hajamaliza hata hoja, naamini hujamwelewa ndiyo maana unampa taarifa.

Mheshimiwa Mwamoto, endelea na mchango wako.

MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nitampa na nauli ili aende akaione kule. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilichokuwa nazungumza ni kwamba tusitake kufurahia kwenda Peponi wakati tunaogopa kufa. Maana yangu nini? Maandalizi, matayarisho ya timu yetu bado. Tunatakiwa sasa tukae tujipange, kwa sababu hawa wamewekeza; hawa wa-Senegal wamewekeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, timu nzima ile ya Taifa wachezaji wanacheza nje ya nchi yao, kwa hiyo kwa sababu wamewekeza, fedha zile ambazo zinapatikana sasa thamani yake inarudi kwenye uchumi wa nchi yao na kuongeza pato la nchi. Wachezaji wetu wanne tu ambao ndiyo wanacheza nje ya nchi na thamani yao ndiyo ile ambayo mmeiona. Kwa hiyo, ninachotaka kusema sisi ndiyo Wabunge wa kuishauri Serikali tufanyeje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu ni kwamba, kwa kuwa uwezekano wa kujenga academy kwa nchi yetu siyo rahisi, basi tuwatumie wachezaji aidha wa riadha, ngumi, mpira ambao walifika rank ya Kitaifa kuwasambaza kwenye Shule zote Tanzania hata kwa kuwalipa posho kufundisha michezo baada ya miaka mitatu tutaona nchi nzima itabadilika tutakuwa sawa na wenzetu wengine badala ya kuendelea kulalamika. Kwa hiyo niombe sana Mheshimiwa ulisikie hilo.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii pia niwaombe suala la kukuza michezo ya nchi yetu siyo la Serikali peke yake, wadau, TFF na Serikali kama vile ambavyo Mkoa wa Mwanza juzi wamezindua uwanja mzuri ambao Mwenyekiti alikuwa Mzee Kitwanga hapa. Kwa hiyo, haya ndiyo mambo ambayo yanatakiwa yafanyike badala ya kuendelea kulalamika, tusitake tufanye vizuri wakati hatuchangii pia TFF wajikite katika kupanga ratiba vizuri ili mambo yaende vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba awe ni Waziri Mkuu au Rais tena akutane na wadau wa maliasili na utalii. Utalii ni sehemu ambayo tunaweza tukapata fedha nyingi sana lakini tumepasahau kidogo. Kwa mfano, juzi kuna Wabunge wamekwenda kuangalia michezo kule, nilitegemea tungewapa hata vipeperushi (brochures), wakaenda navyo wakavisambaza kwa watu kule ili kutangaza utalii wetu, nami tarehe 26 nitakuwa mmojawapo ambae nitakwenda, niombe Waziri husika kama upo kama ni kilo 20 au 30 nibebeshe nitakwenda kufanyakazi hiyo ya kuvisambaza kwa niaba ya nchi yangu ya Tanzania kwa sababu naipenda.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ilikuwa ni nafasi pekee ya wawekezaji, dawati la wawekezaji wangekwenda kutumia fursa hiyo, zile ni fursa kwenda kutafuta wawekezaji kule, dawati likaenda kule lingeweza kutuletea watu kule wa kwenda kupanda Kilimanjaro, Serengeti, Manyara na sehemu nyingine ndiyo fursa zenyewe na sasa hivi ninavyozungumza kuna mechi zinaendelea hapa Tanzania, timu za walemavu za Afrika Mashariki zinapambana pale Dar es Salaam kwa kutumia nembo ya Tembo worriers sasa hizo ni fursa kwamba hata ukichukua wale walemavu ukawapeleka Kilimanjaro wakapanda Kimataifa tunaonekana na watu wanavutiwa kuja kuona mbuga zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nichukue nafasi hii niipongeze Serikali kwa kuwa wametujengea hospitali nzuri sana pale Wilaya ya Kilolo, hospitali ambayo ni ya mfano wa kuigwa ambayo Mheshimiwa Rais huenda akafungua kwa niaba ya nyingine zote. Kwa hiyo, niiombe Serikali muendelee kukusanya mapato kwa kutumia mfumo ambao utakuwa ni mzuri.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika suala la mwisho kabisa niombe kwenye zile mashine za EFD, zile mashine zinazofanyakazi ni chache sana. Ukifanya hesabu, kafanye hesabu ni ngapi unazo na ngapi mabao zinaingia kwenye mfumo wako, utashangaa ni fedha kiasi gani zinapotea nami niko tayari kukupa baadhi ya documents ukihitaji ili uone ambavyo fedha zinapotea. Kwa hiyo ninakuomba huu ni mfumo mzuri kwa sababu kwanza Watanzania sifa yetu kubwa ya Mtanzania ilikuwa ni kukwepa kulipa kodi lakini sasa hivi siyo ujanja. Ujanja mzuri ni kulipa kodi na kuokoka ndiyo ujanja ambao unafaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja.(Makofi)
Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi jioni ya leo. Nianze kwanza kwa kuwapongeza Wabunge wanne ambao wameingia safari hii baadaye, Mheshimiwa Shamsi Vuai Nahodha, Mheshimiwa Oliver Semuguruka, Mheshimiwa Lucy Owenya na Mheshimiwa Ritta Kabati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuishauri Serikali. Hakuna kitu ambacho kinanikera kama kuendelea kufanya vibaya kwa timu zetu za Taifa, juzi niliuliza swali Mheshimiwa alijibu, lakini nataka kumshauri leo. Bahati nzuri nimekuwa mchezaji kwa ngazi ya juu kabisa, nimekuwa kwenye Baraza la Michezo, Mjumbe kwenye TFF, nimekuwa Kapteni wa timu wa Bunge lililopita, na sasa hivi ndiye kocha wa timu ya Bunge hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu nashauri, kwa kuwa nilipokuwa kwenye Baraza na nina hakika kuwa Baraza letu linajiendesha katika mazingira magumu sana. Hakuna fedha ya kutosha ambayo inapelekwa pale, lipo pale kwa sababu lipo kisheria na sidhani kama linafanya kazi yake kama inavyotakikana. Nimekuwa TFF mzigo ni mzito nitatoa ushauri baadaye kwamba iweje kwa timu ya Taifa. Kwa kuwa Baraza la Michezo lina vitu vingi, michezo yote iko mle pamoja na wasanii wapo mle ndani. Ninapendekeza tuunde Shirika la Michezo. Ukienda Uingereza baada ya kugundua kwamba baadhi ya michezo haifanyi vizuri walianzisha Shirika la Michezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, umuhimu wa kuanzisha shirika la michezo badala ya baraza ni kwamba itakuwa rahisi kujitengemea, litakuwa linakaguliwa kama kawaida na Serikali/CAG, lakini litafanya kazi vizuri kuliko sasa kwa sababu sasa hivi halina fedha lakini tutakapounda shirika itakuwa rahisi wao kufanya mambo mengi. Kwa mfano, wanaweza wakatafuta kwenye harambee, wanaweza kuwa na vyanzo vingine vya mapato na hivyo itakuwa ni rahisi sana kuzihudumia hizi timu za Taifa. Leo kuna kuna mashindano ya olympiki, wakimbiaji wako Arusha, sijui wako camp, hawana fedha wanapata shida. Timu ya Taifa inaachiwa na TFF, TFF wanapata wapi pesa? Kwa sababu kiingilio kile nilitegemea makato ya ile kodi ingerudi baadaye ikasaidia kwenye timu ya Taifa. Lakini tunataka tu tuone timu ya Taifa inafanya vizuri bila kuipa support, hii ni pamoja na michezo mingine. Mheshimiwa Waziri ninashauri tuanzishe Shirika la Michezo, hapa ndipo utakapoona tofauti. Leo ni miaka mingapi hatujafanya vizuri?(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kushauri pia kuhusu timu ya Taifa. Ili timu ya Taifa ifanye vizuri ninashauri TFF najua wapo, idadi ya wachezaji ambao wanatoka nje, wanaoruhusiwa kuchezea vilabu vyetu vya ndani ni wengi mno kiasi kwamba leo ukienda timu ya Yanga wanaoongoza kufunga magoli ni wachezaji wa kutoka nje, ukienda timu ya Simba wanaoongoza kufunga magoli ni wachezaji wa nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lake ni nini, ukiangalia ligi ya Uingereza ndiyo ligi bora ninaamini kuliko ligi nyingine na ndiyo ligi yenye wachezaji wengi wa nje. Lakini timu ya Taifa ni mbovu sana kwa sababu wanaocheza ligi ile ni wageni, kwa hiyo na sisi tunanufaisha tu timu za Simba na Yanga lakini uwezo wa kunufaisha Taifa kwa kutumia wachezaji wengi wa nje itakuwa ni kizungumkuti, hatutafanya vizuri hata siku moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Waziri wa Kazi Mheshimiwa Mavunde yupo, hebu kapitie mikataba ya wachezaji wetu kwenye vilabu vyao, kwa sababu tofauti ya mshahara ya wachezaji wa nje na wachezaji wetu inakatisha tamaa. Ukienda pale wale watu unaweza ukafikiri labda wanafanya mgomo lakini wameshakata tamaa kiasi kwamba wanaona afadhali basi hawa wanaolipwa fedha nyingi ndiyo wacheze wenyewe. Sasa nafikiri Mheshimiwa Waziri pita pale kagua ile mikataba yao utaona kinachoendelea pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nigependa nishauri ni kwamba vilabu vyetu vinachukua muda mrefu sana kufanya uchaguzi na hii ni pamoja na mikoa. Mimi natoka mkoa wa Iringa, tunapokea malalamiko mengi sana kutoka kwenye klabu za Lipuli na klabu ya mkoa wa Iringa kwamba chaguzi hazijafanyika. Kwa hiyo, ningeomba taratibu zifuatwe kama ni Baraza la Michezo la Taifa au ni Mabaraza ya Mikoa yasimamiwe yahakikishe chaguzi zinafanyika kwa sababu hapo ndipo ambapo vurugu inaanzia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningependa kushauri ni jinsi ya kutenga siku maalum. Mheshimiwa Rais ametenga siku maalum ya usafi, sasa Mheshimiwa Waziri wa Michezo, kuna haja kabisa ya kuangalia kama nchi zingine, mfano ukienda Burundi, Congo na sehemu zingine wana siku maalum ya michezo na hii tungeanza Wabunge kwa sababu michezo ni afya, michezo ni dawa na michezo ni tiba. Tukifanya hivyo tutawafanya na watu wengine wakaona umuhimu wa michezo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni academy, lazima tuwe na academy. Sisi wakati tunacheza wakati huo tulikuwa tunatumia zaidi michezo ya shule za sekondari, vyuo na mashirika. Lakini ukiangalia hii michezo sasa hivi imekufa kabisa, zile ndizo zilikuwa academy. Leo ukianzisha academy unapata wapi vifaa, uwanja ule wa bandia ambao kodi yake na ununuzi huwezi ku-afford, vifaa vya michezo bei ziko juu, sasa bila kufanya hivyo matatizo yake yatakuwa ni makubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu wasanii ni vema kama nilivyosema tukiwa na shirika la michezo na wasanii waatakuwa ndani, itakuwa rahisi kuwasimamia haki zao. Wanadhulimika sana, wanafanya kazi kubwa lakini haki zao hazitambuliwi. Tumeshuhudia wacheza filamu, filamu zao zipo mitaani, wanachopata wao hakuna, ni shida tupu. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri naomba kabisa hebu kaa na watu wako muweze kuona mnawasaidiaje wasanii na wanamichezo wa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho kwa sababu muda bado ninao mimi nilikuwa Rais wa wacheza mpira Tanzania, chama kinaitwa Spurtanza (Chama cha Wachezaji Mpira). Mimi nigekushauri jaribu kuwatumia wale wachezaji tungeweza kuwatawanya kwenye shule za msingi hata kwa posho kidogo wangeweza kusaidia kufundisha michezo na ingekuwa ni academy tayari. Wapo wengi, anapomaliza kucheza mpira mchezaji wa Tanzania wengi maisha yao ni shida, lakini tayari wanakuwa wameshafikia level ya Taifa, kwa hiyo automatically wanakuwa kwenye level ya coaching ya mwanzo, ni kiasi cha kuwaendeleza tu. Kwa hiyo wangetumika kwenye shule zetu za misingi wangesaidia kubadili michezo kwenye nchi yetu kwa baadhi ya michezo kama mpira wa miguu, riadha,ngumi na kadhalika, badala ya kusubiri academy ambayo kwa kweli ni gharama kuziendesha na Serikali bado haijatia nguvu labda wakiamua kuweka ruzuku kwenye michezo hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba Mheshimiwa Waziri, pesa hizi ulizoomba ni ndogo hazitasaidia kitu chochote. Hizi ni za semina na mambo mengine, lakini kwenye mambo ya michezo sahau kama kutakuwana mabadiliko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia asubuhi ya leo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwashukuru wananchi wa Jimbo la Kilolo ambao kwa kweli wamenirudisha baada ya miaka 10 kukaa bench, nawashukuru sana. Pia nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais pamoja na Mawaziri, kwa mwanzo mzuri wa kazi nzuri ambazo tumeshuhudia Mawaziri wetu wakifanya na kufuatilia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuchangia kuhusu TASAF, kwanza naishukuru Serikali kwa mradi mzima huu wa TASAF, tulianza na TASAF I na II ambazo zenyewe zilijikita kwenye ujenzi wa barabara, ujenzi wa shule, ujenzi wa zahanati, vituo vya afya na kadhalika. Kazi ilifanyika vizuri na ilikuwa inafanyika kwa ushirikishi kati ya wananchi wa maeneo pamoja na mchango wa TASAF.
Mheshimiwa Naibu Spika, kinachosikitisha ni kwamba. baadhi ya maeneo na baadhi ya miradi ambayo ya awamu ya kwanza na ya pili mpaka leo haijamalizwa. Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI naomba nikushauri, jaribu kufuatilia ile miradi ya TASAF ambayo haikumalizwa kwenye awamu ya kwanza na ya pili ili iweze kumaliziwa, kwa sababu inavunja moyo sana kuona miradi ile bado ipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, TASAF III, napongeza uongozi mzima wa TASAF kutoka Makao Makuu mpaka Waziri husika. TASAF III ni TASAF ambayo imelenga kuondoa au kupunguza umaskini kwa wananchi, wamefanya kazi kubwa sana. Tumetembea baadhi ya maeneo tumeona jinsi ambavyo wananchi wameanza kubadilika. Kuna matatizo madogo madogo ambayo kama Serikali inabidi iangalie.
Moja ni kwamba wale wanaosimamia TASAF wakiwemo Wenyeviti wa Vijiji, wao wanasimamia kuwapa fedha wale watu maskini lakini wao hawalipwi, hawana posho Wenyeviti wa Vijiji, Wenyeviti wa Vitongoji anasimamiaje mtu kugawa nyama, wakati yeye mwenyewe hali, haiwezekani! Matokeo yake watu ambao wanaingizwa kwenye TASAF III wengine siyo wahusika, wanaingia baadhi ya ndugu wa viongozi, baadhi ya watu ambao wana nguvu zao, baadhi ya watoto wadogo, maana ya TASAF inaharibika.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa Mheshimiwa umesikia, muangalie na mfikirie jinsi gani ambavyo Wenyeviti wa Vijiji, iwepo sheria kabisa ya kutamka kwamba walipwe shilingi fulani, badala ya kusema Halmashauri zichangie asilimia hii itakuwa haiwezekani, kwa sababu kama Serikali wenyewe tumeshindwa kupeleka fedha kwa wakati, Halmashauri ambazo nazo zinategemea mapato ya ndani zitumie katika zile fedha ambazo Serikali ilikuwa ilete, kweli Mwenyekiti atapata hiyo fedha? Kwa hiyo tuiangalie, tuitungie sheria ili Wenyeviti walipwe, inawezekana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna jambo lingine naomba Waziri wa TAMISEMI uje utoe ufafanuzi, kwa sababu TASAF wanapeleka fedha kwa watu maskini ili kupunguza umaskini na yule mtu maskini ile fedha anaitumia kwa ajili ya kupika vitumbua, maandazi, anauza nyanya au mama lishe ili apunguze umaskini, lakini cha ajabu Halmashauri zetu zinakwenda kuwalazimisha kulipa ushuru wale watu maskini. Zinamwaga bidhaa zao, wanawekwa ndani kitu ambacho sasa hatujui tunawafanya nini.
Mheshimiwa Naibu Spika, TASAF inapeleka fedha kupunguza umaskini, Halmashauri inaongeza umaskini kwa kuwatoza kodi na kuwanyanyasa. Naomba Mheshimiwa Waziri utoe tamko kwamba hizi kodi ndogondogo za hawa watu, ambao ni watu wa chini, maskini, ambao kwa kweli anatafuta fedha kwa ajili ya kununua unga ili aweze kupika ugali ale na familia yake, siyo biashara. Halmashauri zijikite kutafuta biashara zingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha nyingi za Mfuko wa TASAF tunategemea kutoka nje, Serikali nafikiri imekuwa ikipanga fedha mara nyingi, lakini zile fedha hazijaenda kule. Nafikiri safari hii kwa kuwa tumeamua sasa kubadilika, kufanya kazi na kudhibiti mapato, basi Serikali ihakikishe inatenga fedha za kutosha na kuunga mkono kwenye Mfuko wa TASAF.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie kuhusu ukubwa wa Wilaya ya Kilolo. Wilaya ya Kilolo lilishaletwa ombi awamu iliyopita, ikakubalika kwamba igawanywe, eneo ni kubwa lina takribani ukubwa ambao ni sawa na Mkoa wa Kilimanjaro , lakini mpaka sasa hivi siyo rahisi kwa mwananchi wa Kilolo kuona ile impact ya fedha ambayo inapelekwa kwenye ile Wilaya na kugawanya kwenye Kata zote. Kwa kuwa tayari mmegawa Halmashauri, tumepata Halmashauri ndogo ya Ilula, Serikali iamue ile iwe Halmashauri ndogo, hii iwe Halmashauri kamili ili baadaye muangalie uwezekano wa kugawa Jimbo hilo na kupata Jimbo lingine kwenye Wilaya zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nijikite katika sehemu ya miundombinu. Wilaya ya Kilolo ni Wilaya ambayo ndiyo inayotegemewa kwa uzalishaji wa mazao mbalimbali, tatizo lake kubwa ni miundombinu. Miundombinu ambayo ipo ni ile ile ya miaka 10 iliyopita. Hivyo, nafikiri kwamba, barabara zetu ambazo tumeziomba zipandishwe hadhi, ikiwepo barabara ya kutoka Idete kwenda Itonya, Muhanga kwenda kutokea Morogoro, ipandishwe hadhi iwe barabara ya mkoa, ili iwe rahisi zaidi kufungua maendeleo kwa wananchi wa Wilaya ya Kilolo.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho ni suala la Wazee. Wazee pamoja na kuwa tumetamka kwamba wanatakiwa wapewe huduma bure pamoja na matibabu, lakini bado hatujawawekea utaratibu mzuri. Nashauri kwamba katika zahanati, dispensary na hospitali zetu litengwe eneo maalum kwa ajili ya huduma za Wazee, ili Mzee akifika pale hana sababu ya kukaa foleni kwa sababu sisi sote ni wazee watarajiwa, yale ambayo tunayafanya leo yatakuja kuturudia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa nina muda bado kidogo, zingumzie habari ya Wakuu wa Wilaya. Na-declare interest nilikuwa Mkuu wa Wilaya. Kazi ya Mkuu wa Wilaya ni kubwa, kwa sababu kinapotokea kipindupindu anayeulizwa ni Mkuu wa Wilaya, wanapotokea wafanyakazi hewa anayebanwa ni Mkuu wa Wilaya, unapotokea ujenzi wa maabara anayebanwa ni Mkuu wa Wilaya, yanapotakiwa madawati anayeulizwa ni Mkuu wa Wilaya, zinapoongezeka mimba mashuleni anayeulizwa ni Mkuu wa Wilaya, lakini uwezeshwaji wa Mkuu wa Wilaya bado haujakaa sawa.
Mheshimiwa Naibu Spika, OC ambazo wanapelekewa Wakuu wa Wilaya zinapita mikono mingi, nashauri kwamba isipunguzwe ile hela ya maendeleo ambayo imepangwa kwa ajili ya Mkuu wa Wilaya zipelekwe moja kwa moja kwake, kwa sababu haifurahishi kuona kwamba, Wakuu wa Wilaya wanakuwa ombaomba. Mtu ambaye anasimamia maendeleo na haki anatakiwa aombe hata mafuta, haipendezi!
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo basi, kama kifungu kipo kiende moja kwa moja bila kuguswa na RAS (Regional Administrative Secretary) au Mkuu wa Mkoa, kiende kwa Wakuu wa Wilaya moja kwa moja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amefanya leo nikapata nafasi hii. Lakini moja kwa moja niende kwenye mada. Kwanza nimpongeze sana Mkurugenzi Mkuu wa TANROADS, Engineer Patrick Mfugale, lakini pia nimpongeze sana na Meneja wetu wa TANROADS wa Mkoa kwa kazi nzuri ambayo amekuwa akiifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie habari ya barabara zetu za Kilolo. Wilaya ya Kilolo iko katika Mkoa wa Iringa, ukienda kwenye Ilani ya Chama chetu cha Mapinduzi inasema kwamba kila barabara inayounganishwa na Wilaya itawekwa lami. Barabara zote ambazo zinakwenda Wilaya za Mufindi na Iringa zina lami. Juzi kwenye swali langu niliuliza miaka saba imeanza kushughulikiwa, kati ya kilometa 35 ni kilometa saba tu ndizo ambazo zimewekwa lami, kwa miaka saba kilometa saba ndizo zimewekwa lami. Nilikuwa nauliza tu swali na hata juzi niliuliza kwamba kwa kilometa hizi zilizobaki ambazo ni karibu 28, je, ni kwa miaka 28 ndipo tutapata lami? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ningeomba Mheshimiwa Profesa wewe ni mtu makini na kilolo unaijua, umeshafika, hebu angalia uwezekano wa kuhakikisha kwamba, barabara ya kutoka Ipogolo kwenda Ndiwili - Ihimbo - Luganga - Kilolo inawekwa lami; walau tupate kilometa saba tu kwa mwaka huu wa fedha na mwakani ukitupa saba basi tutakuwa tumesogea, ili watu wawe na imani. Kwa sababu ukiangalia katika Mkoa wa Iringa maeneo ambayo yanategemewa kwa kilimo ni pamoja na Wilaya ya Kilolo. Sasa tusiposafirisha yale mazao yakafika kwenye Wilaya nyingine na baadhi ya Mikoa ambayo ina matatizo itakuwa ni tatizo. Kwa hiyo, nakuomba kabisa uhakikishe kwamba angalau mwaka huu tunapata lami. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, nikushukuru kwa kuwa barabara hii ya Mkoa ilikuwa inashia Idete na juzi nilipokuwa nauliza swali langu na tulishaomba kwamba barabara hii kwa kuwa inakwenda kutokea Mkoa wa Morogoro kupitia Idete - Itonya - Muhanga mpaka Mngeta kwa Mheshimiwa Susan Kiwanga, ningeomba hizo kilometa 26 ambazo zimebaki pale, wala pale hatuhitaji lami tunahitaji tu pesa kidogo tuweze kuunganisha ili iwe rahisi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, na nilisema kwamba leo hii ikitokea barabara ile pale Kitonga, aidha, pakaziba au pakabomoka uwezekano wa kwenda Morogoro unapotoka Zambia, Malawi, Afrika Kusini, Mbeya na Iringa yenyewe inabidi uje Dodoma, karibu zaidi ya kilometa 400 za ziada. Kwa hiyo, ningeomba Mheshimiwa kwa kuwa ulituahidi juzi hebu angalia uwezekano wa kutusaidia hizo kilometa 26 za kwenda kutokea Mngeta. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, ningependa kuzungumzia barabara nyingine ambayo inaanzia Ilula - Mlafu - Wotalisoli - Mkalanga - Kising‟a mpaka Kilolo, barabara hiyo ni ya Mkoa na ninashukuru Mungu kwamba imeanza kufanyiwa kazi. Ningeomba tu kwa kuwa barabara ile ni ya mkoa ina vipimo maalum ambavyo inabidi vizingatiwe. Na sisi Kilolo tumeweka msimamo kwamba tusingependa kwa wafanyakazi ambao hawatumii utaalam wakatoka nje ya mikoa yetu. Kama barabara ya Kilolo inatengenezwa basi vibarua watoke Kilolo badala ya kutoka maeneo mengine ili iwe rahisi wao kulinda zile barabara zao, kuona kama kuna udanganyifu kutoa taarifa kwa viongozi kwamba hapa tunaingizwa mjini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pi kuna madaraja pale. Nashukuru mmetaja habari ya madaraja kwamba mtatusaidia…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi kubwa na nzuri inayofanywa na Wizara hii, ninaomba vitu viwili:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Kilolo ni kati ya Wilaya kubwa Tanzania, ilianzishwa mwaka 2002 lakini hatuna Hospitali ya Wilaya na kituo cha afya ni kimoja tu. Ili mwananchi apate matibabu inabidi asafiri kilometa 100 hadi Ilula. Changamoto kubwa ni gari la wagonjwa, yaani gari langu sasa limekuwa gari la wagonjwa; Mheshimiwa Naibu Waziri anajua sana tatizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ninaomba sana nipate gari Wilaya ya Kilolo. Bado tuna ikama kubwa ya watumishi wa afya. Tunaomba sana uwasiliane na Wizara ya Utumishi ili tuongezewe watumishi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Wizara hii kufanya kazi kubwa, naomba nichangie kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Kilolo haina tatizo la maji, bali ina tatizo kubwa la usambazaji wa maji. Wilaya ina Tarafa tatu; Kilolo: tatizo lipo Kata za Udekwa, Ukwega, Ng’uluwe na Idete. Mazombe: tatizo kubwa liko Ilula na Irole tatizo ni kubwa. Mahenge: hawa wanategemea sana kilimo cha umwagiliaji hivyo naomba Mheshimiwa Waziri atume timu toka Wizarani kwenda kuangalia tatizo kubwa ambalo lipo kwenye eneo hili. Mfano, Kata ya Mahenge kuna mabwawa ya umwagiliaji lakini changamoto ni idadi ya watu kwamba imeongezeka lakini intake zipo vile vile. Hivyo, ni bora timu yako ipite huko hasa katika vijiji vya Ilindi na Magana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Nyanzwa, hapa pia changamoto ni ongezeko la watu. Sasa bwawa leo linahitaji kupanuliwa na ahadi za viongozi, kama aliyekuwa Waziri Mkuu Mheshimiwa Pinda alitoa ahadi ya kuboresha bwawa hilo. Eneo hili pia hawana kabisa maji salama na safi ya kunywa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Ruaha Mbuyuni, pamoja na tatizo la udogo wa mabwawa lakini pia kuna matanki ya maji yamejengwa, lakini fedha za kuyasambaza maji hayo hakuna. Ombi langu kubwa ni kuomba Wizara hii itume timu kwenda katika eneo hili na kubaini malalamiko haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais wetu alitoa ahadi ya kumaliza tatizo la maji Ilula, wakati wa kampeni. Sasa Mheshimiwa Rais anatarajia kwenda kuwashukuru wananchi hao, sasa wananchi lazima watampokea Mheshimiwa Rais kwa mabango, kwani bado tatizo lipo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue nafasi hii nikushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia. Nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake yote kwa kutenga bajeti kubwa ambayo haijawahi kutokea, asilimia alizotenga tuna uhakika kwamba umeme sasa utakuwa umefika sehemu zote.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaambie Waheshimiwa Wabunge kwamba leo mnachozungumzia hapa ni suala la umeme. Mheshimiwa Waziri wa Viwanda yuko pale bila ya umeme hatofanya chochote, lakini hamuelewi huo umeme mnaozungumza ni umeme gani. Umeme tunaozungumza sasa hivi ni ule ambao unatokana na nguvu za kule Kidatu, Kihansi na ule mwingine unaotoka kwenye bwawa la Mtera, yale maji yanatoka katika Wilaya ya Kilolo. Vyanzo vitano vya maji ambavyo vinajaza Kihansi vinaanza kwenye vyanzo ambavyo vinatoka kwenye Wilaya ya Kilolo, sehemu ya Muhu na Mkasi. Maji yanayojaza bwawa la Mtera yanatoka kwenye vyanzo vikuu ambavyo ni Mto wa Lukosi na Mto Mtitu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tulishaongea na Mheshimiwa Waziri nikamwomba kwamba ni vema sasa tukaenda kule akatembea aone uhalisia. Kwamba wale wanaopika chakula kizuri wenyewe hawali. Mpaka hivi ninavyomwambia kuna Kata ya Kimala, Idete, Ukwega, Udekwa, Kising‟a, Nyanzwa na Mahenge wanausikia tu umeme kwenye bomba, wakati wakijua kabisa kwamba chanzo kikuu ni Wilaya ya Kilolo. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, kwa kuwa alishaniahidi kufika kule, naomba afike ili aangalie ni jinsi gani atanifikiria tuweze kupata umeme vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nishauri tu, kwamba kwa kuwa mwaka wa juzi, mwaka wa jana tulikuwa kwenye kujenga maabara, maabara zile hazitakuwa maabara kama hakutakuwa na umeme, kwa kuwa sasa wananchi wenyewe hali zao si nzuri sana niiombe Serikali, Wizara ya Elimu ikishirikiana na Wizara hii tuweze kuhakikisha kwamba kwenye shule zote za sekondari ambako tumejenga maabara waweze kuingiziwa umeme, hilo atakuwa ametatua na ametusaidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine na-declare interest, nilikuwa Mkuu wa Wilaya, nikiwa Mkuu wa Wilaya nililetewa kesi hizi zinazohusiana na vinasaba, bahati nzuri nitazungumza yale ambayo ni ya ukweli na Mungu ananiona. Mfanyabiashara yule baada ya kukamatwa alikuja ofisini kwangu, baada ya kuja ofisini kwangu nikaomba watu wa EWURA waje, walipokuja walituelimisha jinsi gani watu wanavyotorosha mafuta. Baadaye alikubali kweli mafuta yale yalikuwa ni ya transit na alikuwa anakwepa kodi.
Baada ya kufanya utafiti ikaonekana kwamba zaidi ya wafanyabiashara 316,000 walikuwa wanakwepa kodi. Wafanyabiashara wa mafuta siyo mchezo ni ma-giant. Kwa hiyo, unaweza ukakuta kelele yote hii ambayo inapigwa hapa ni kwa sababu wale nao wana uwezo wao. Hivi jiulize, kama EWURA wasingeweza kudhibiti mafuta bei hii ambayo ipo sasa hivi ingekuwepo? Tulishafikia mpaka shilingi 3,000 kwa lita, leo tunanunua mpaka Shilingi 1,200 yanashuka, ni kwa sababu ya udhibiti mzuri wa EWURA.
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi EWURA wasikatishwe tamaa. Kwa sababu juzi nilisikia hapa kwamba hata tenda za kupata mtu wa kutoa vinasaba hazikutangazwa, kitu ambacho siyo kweli, zilitangazwa kwenye magazeti na kwenye tovuti na ushahidi upo, kwa nini tuseme uwongo? Naomba, badala ya kuwakatisha tamaa tuwape nguvu kitu gani tufanye ili mafuta yadhibitiwe, wananchi wetu bei zikipungua waweze kusafirisha mazao yao, waweze kusafiri, kwa sababu bila kudhibiti hiyo nawahakikishieni mifumuko ya bei haitapungua, itaongezeka. Nawaomba wasikate tamaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza sana watu wa EWURA, endeleeni na kazi hiyo, ongezeeni nguvu. Hawa ambao wanapambana nao wapo wengi wameshawakamata. Mtu anayekamatwa siku zote anakuwa na ugomvi na Polisi, akishaona Polisi anaona huyu mtu hafai. Tumuongezee. Mimi najua watu wameshaambiwa maneno hapa kama alivyosema yule bwana mdogo, siwezi kuwavunja, wana interest zao. Kama mtu ana interest a-declare interest hapa. Mheshimiwa Waziri asikate tamaa, moto ni ule ule, hapa kazi tu, kanyaga twende. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho ni kuhusu viwanda. Kama tunakwenda kwenye viwanda, tumeamua Serikali yetu kuwekeza kwenye viwanda, umeme lazima uwe wa uhakika. Kuna sehemu ambazo tumeweka maeneo kwa ajili ya EPZA, ziangaliwe zile ili Processing Zone zile tuweze ku-process mazao na kuyapa thamani ili kuweza kuuza na kupata bei zinazofaa. Mheshimiwa Waziri wa viwanda apige kelele atakavyoweza, kama umeme hautafika itakuwa haina maana yoyote. Washirikiane vizuri na Waziri wa Kilimo kwa sababu viwanda vyake pia kama hakutakuwa na mageuzi ya kilimo hatafanya chochote! Kama wasambazaji wa pembejeo wataendelea kuwa wababaishaji hatafanya chochote, ubora wake utabakia kwenye vitabu na maandishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ulanzi unatengenezwa pale Iringa, tunashindwa kwa sababu ya umeme, hebu Mheshimiwa Waziri aje atembelee, wenzetu Kenya wanasema ni bamboo juicy, lakini ndiyo ulanzi huo huo. Ulanzi siku ya kwanza unakuwa ni togwa, togwa ni juicy, siku ya pili unakuwa mkangafu, mkangafu ndiyo unaanza kuwa pombe, siku ya tatu unakuwa mdindifu, mdindifu ndiyo unalewa, yeye alisoma Tosamaganga najua alikuwa anapiga ule! (Kicheko/ Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri wa Mambo ya Ndani alisoma shule ya Tosamaganga na Naibu Waziri wa Maliasili alisoma Tosamaganga na wenyewe wanatoka Tosamaganga, kwa hiyo asiposaidia wakajenga viwanda atakuwa hajafanya kitu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nafikiri ni kengele yangu ya mwisho au bado?
NAIBU SPIKA: Bado Mheshimiwa.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ningeomba kwa kweli tufanye hivyo na kuna mambo mengi, kuna sehemu nyingi, kuna viwanda kwa mfano hata kule Busega hawana umeme, wangepata umeme wangeweza pia angalau wakachinja hata wale ng‟ombe badala ya kuleta ng‟ombe Dar es Salaam kwenye malori wangeleta nyama.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hawawezi kuleta nyama kama hamna umeme, Eeh! hakuna mabarafu yale zitaoza zile. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri atusaidie ili tupate umeme wa uhakika.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja!
Azimio la Bunge Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Udhibiti wa Matumizi ya Dawa na Mbinu za Kuongeza Nguvu Michezoni
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nichukue nafasi hii niweze kukushukuru kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuleta Azimio hili ili tuweze kulipitisha. Umechelewa kwa sababu mimi ni mmojawapo wa wachezaji ambao wamecheza miaka ya nyuma, baadhi ya kizazi kimeathirika kwa kiasi kikubwa kutokana na matumizi mabaya ya madawa haya. Kwenye timu zetu ni kitu cha kawaida, wachezaji walio wengi wamekuwa wakitumia bangi, lakini kabla ya kuendelea kuchangia tupeane pole kwa timu yetu ya Taifa kwa jinsi ambavyo tumefanya vibaya juzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili tumechelewa, niungane na wenzangu na wewe jinsi ambavyo umewasilisha hapa, kwamba sasa twende mbele, lakini kazi kubwa ambayo ipo ni kwamba tunafanyaje? Ni nani watahusika katika kulisimamia jambo hili?
Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyojua ni kwamba vikundi vingi vya michezo nchini kwetu vimesajiliwa. Ningependekeza kwamba, ukienda nchi nyingine zilizoendelea hamuwezi kuanza ligi mpaka wachezaji wamepimwa afya zao. Kwa hiyo aina ya Madaktari ambao wanakuwa kwenye vile vilabu wanakuwa waliosajiliwa, ni Madaktari wa kweli, ili pale linapotokea tatizo kwenye timu yake, amegundulika mtu ambaye anatumia zile dawa basi wa kwanza kuadhibiwa ni yule Daktari ambaye alimpima afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati nachangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri nilipendekeza kwamba sasa hivi umefikia wakati ikiwezekana lile Baraza la Michezo tulivunje, tuanzishe Shirika la Michezo. Kwenye Shirika la Michezo itakuwa rahisi zaidi lenyewe kutafuta fedha au kupata kwa wahisani au kuchangia au hata katika harambee ili liweze kuendesha, kusimamia timu za Taifa kwa udhibiti na kudhibiti dawa za kulevya, ni kazi yao. Leo inawezekana tunapitisha hapa sina hakika kama tulikumbuka kuweka bajeti hii ambayo inakwenda kutusaidia kufanya kazi hii ya udhibiti huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine, nilizungumza pia, hatuwezi kuendelea kufanya vibaya kwenye timu yetu ya Taifa. Ukiangalia, kama tungewapima wale wachezaji baadhi ungewakuta wanatumia, aidha kwa kujua au kwa kutojua. Kwa sababu dawa hizi zinaweza kutumika hata kwa kula vyakula tu. Kuna baadhi ya vyakula ambavyo vinaweza vikawa vinasababisha mtu kupata nguvu, yaani vikasababisha kupatikana na viashiria vya dawa za kulevya, vyakula ambavyo tunatumia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilipendekeza kwamba ili sasa timu zetu zifanye vizuri ni pamoja na kudhibiti matumizi mabaya ya madawa ya kulevya, sambamba na kuhakikisha kwamba wachezaji wanaotoka nje wanapunguzwa kwenye timu zetu. Kwa sababu wao wanakuwa bora tu pale vilabu vya Simba, Yanga, Azam vinapofanya vizuri na ukiangalia ndiyo wanaoongoza katika kufunga mabao, lakini unapokuja kutaka kuwatumia haiwezekani kwa sababu wao ni wa nje. Wachezaji wetu wa ndani tayari wanakuwa wamekata tamaa. Badala ya sasa kuitunza miili yao wanakwenda kwenye kuanza kutumia madawa ya kulevya ili wapate nguvu wafanane na wale wa nje, ambapo wenzetu lishe ndiyo bora kuliko kitu kingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Hafidh Ali amekuwa ni referee wa Kimataifa, amechezesha African Cup of Nations, amechezesha World Cup ya Vijana. Mchezaji kama Filbert Bayo mwanariadha, amekimbia Gidamis Shahanga na wengine wengi tu wamefanya vizuri kwa sababu walikuwa wanafuata zile ethics za michezo yenyewe. Leo hii itakuwa ni kazi kubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu kiundwe chombo kizuri cha jopo la Madaktari kuweza kutusaidia kutupa ushauri na kuweza kuangalia jinsi gani tunaweza tukawa tunawapima wachezaji wetu wote kabla ya kushiriki kwenye michezo. Kabla ya kuanza ligi daraja la kwanza, la pili wanakuwa wamepimwa aki-qualify ndipo anaingia, asipo-qualify basi tunam-disqualify, anakuwa hayupo tena kwenye mashindano.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, nakutakia kila la kheri katika utekelezaji.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2017/2018
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kuchangia hoja hii kwanza kwa kuunga mkono hoja kwa ujumla. Nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi nzuri ambayo anaifanya, lakini bila kusahau kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu ambaye kwa kweli ameonesha ujasiri mkubwa katika kupambana na gurudumu hili la maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu leo itakuwa moja tu kubwa. Tanzania wakati tunawasaidia wenzetu wapigania uhuru wa Nchi za Kusini mwa Afrika tulikuwa na makambi, kuna maeneo ambayo yalikaliwa na wakimbizi kwa nchi yetu zaidi ya maeneo 163, Mheshimiwa
Mwenyekiti, ilikuwa Dar es Salam, Mwanza, Mbeya, Mtwara, Lindi, Ruvuma, Pwani, Iringa, Dodoma, Tabora, Kigoma, Morogoro, Mara, Arusha, Zanzibar na Kagera. Kwa kutunza muda siwezi kuyataja makambi yao yote lakini lengo langu ni moja kwamba Dar es Saalam katika zile Ofisi Ndogo za CCM pale Lumumba baaada ya kuzaliwa Chama cha TANU ilifanywa Ofisi ya wapigania uhuru ambapo Chama cha SWAPO, FRELIMO, ANC, ZANU na POLISARIO walifanya kama makazi pale, kama ofisi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi za Kamati ya Uongozi ya Afrika (Special Unity) sasa hivi ni ofisi ambazo zinatumiwa na Tume ya Maadili ya Uongozi, makazi ya Hayati Eduardo Mondlane Osterbay, sasa hivi inatumika kama Ubalozi wa Msumbiji; Shule ya Sekondari Makongo na Lugalo walisoma watoto wa wapigania uhuru kwa sasa ni sekondari na Uwanja wa Magunia kule Tandale bado unatumika, ilikuwa ni sehemu ya mkutano pale, walifanyia mikutano pale. Morogoro kambi za wakimbizi zilikuwepo pale, kulikuwa na Mazimbu ambako sasa hivi ni Chuo cha Sokoine, kambi za Dakawa ambako sasa hivi kuna VETA na sehemu nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nia yangu ni kwamba kule Kilolo, Kihesa Mgagao walikaa wakimbizi, naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu tujaribu kubadilisha matumizi, wamefanya magereza ambayo haina tija kwa sababu wafungwa wako 40. Juzi Mheshimiwa Waziri wa Michezo tulipata ugeni kutoka Afrika Kusini kwenda kutembea kwenye kambi ile, alivyosikia kwamba ni magereza alikataa kwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale kuna sehemu ambapo Mheshimiwa Mandela na Sisulu walilala. Tulitegemea sasa kingekuwa ni kivutio kikubwa cha watalii. Kuna watoto pale wameachwa na wenzetu wa South Africa wengi tu. Kuna mambo ya kimsingi kabisa tungeweza kufanya sehemu hii kuwa kivutio kikubwa cha utali tungeweza kuingiza fedha kwenye nchi yetu bila matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali yetu, Mheshimiwa Rais anasikia, Mheshimiwa Waziri Mkuu na timu yake wanasikia wabadilishe matumizi kwa eneo lile ili tufanye aidha shule, chuo au VETA. Sasa hivi tunaenda kwenye nchi ya viwanda tunahitaji kutayarisha vijana wengi ili waweze kufanya shughuli hizo za viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili linawezekana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kukushukuru wewe na kukupongeza kwa kufika huu mwaka salama kwa sababu kuna wakati kidogo afya iliyumba, Mungu akubariki kwa sababu tunakuhitaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nianze kuwapongeza Mawaziri wote, Mheshimiwa dada yangu Kairuki pamoja na Mheshimiwa George Simbachawene na Mheshimiwa Waziri wa Sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuchangia katika Utawala Bora. Kabla sijaanza kuchangia nitoe pole sana kwa wananchi wa Jimbo la Kilolo kwa accident ya bus ya Vitu Laini ambayo ilitokea hivi karibuni na kuua watu wengi na jana pia ndege moja ndogo ilianguka katika Jimbo la Kilolo, nawapa pole sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuchangia; jana Mheshimiwa Rais alipokuwa kwenye shughuli ile ya haki kuna kitendo ambacho kilitokea pale, kitendo cha yule mama ambaye alipiga kelele alihakikisha kwamba anapata nafasi ya kuongea na Mheshimiwa Rais, lakini ukifuatilia malalamiko ambayo yule mama alikuwa anayalalamikia ni utawala bora. Kwamba ameingia kila mlango lakini alikosa kusikilizwa na kupewa haki zake. Ameingia Mahakama zote yule mama ameshindwa kusikilizwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilichokuwa najiuliza hivi ni akinamama wangapi hasa wajane ambao wanakosa haki zao? Je, watakuwa na ujasiri kama ule? Hii ni changamoto kwetu viongozi kwamba kama hatuwasikilizi watasubiri mpaka Mheshimiwa Rais atakapokuja kwenye mikoa yetu na wilaya zetu ndipo wasimame haki zao zipatikane. Naomba Mheshimiwa Waziri ajaribu kuangalia tunafanyaje jambo hili. Kuna watu wale wa Haki za Binadamu nafikiri wapo, kile kitengo nafikiri kikiimarishwa kikapewa nguvu kingeweza kusaidia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ukienda Mahakamani kesi zinachukua muda mrefu, ukienda mahabusu na magereza zetu zimejaa, lakini ukienda pale kesi ambazo mimi nikiri nilishawahi kuwa Mkuu wa Wilaya, nilikuwa naingia mara kwa mara kwenye magereza, unaweza ukashangaa kesi nyingine siyo za mtu kukaa mahabusu, ukikaa pale utashangaa. Nafikiria sasa ni wakati muafaka Jeshi la Polisi na Mahakama wakashirikiana, sio lazima mtuhumiwa akituhumiwa leo lazima akamatwe leo, upelelezi unaweza ukafanyika akiwa hata bado hajakamatwa, wakati anakamatwa basi moja kwa moja upelelezi unakuwa umekamilika na haki inatendeka, aidha, kuachiwa au kufungwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wengi wamelalamika kuhusu utendaji wa Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya. Kwanza nianze kwa kuwapongeza kwa sababu wenyewe wamekiri kwamba hawajapata semina. Mimi niwape tu semina kidogo ndugu zangu hasa Wakuu wa Wilaya kwa sababu na mimi nilikuwa Mkuu wa Wilaya, kwamba maamuzi yao yazingatie taratibu na haswa washirikishe Kamati zao za ulinzi na usalama, siyo kuanza tu kutoa maamuzi bila kushirikisha ile Kamati ya ulinzi na usalama. Naamini wakishirikisha Kamati ile basi busara zitatendeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia washirikishe vyombo na taasisi za dini, kuna wazee maarufu, linapotokea jambo haina haja ya kukurupuka, lazima usikilize pande zote mbili ndipo utoe maamuzi. Kwa sababu kuna baadhi ya watu ambao ni watendaji wazuri tunaweza tukawapoteza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia awamu hii imesaidia sana kutia nidhamu kwenye kazi. Leo hii ukienda Ofisi yoyote ukikaa pale kwenye benchi huwezi kukosa mtu wa kuja kukuuliza kwamba bwana una shida gani, umesikilizwa? Kwa hiyo, nikupongeze Mheshimiwa Kairuki kwamba sasa watumishi wanaanza kurudi kwenye line isipokuwa tu Wakuu wa Wilaya, Wakuu wa Mikoa na Watendaji wengine wapunguze, wawasiliane.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili linasikika sana kwa sababu nao kwa kiherehere wanataka kila jambo litoke kwenye vyombo vya habari, mambo mengine yanakuwa kimya kimya, ukitaka kila kitu kitoke madhara yake ndiyo hayo. Hiyo nidhamu ni nidhamu ya uwoga, waache uwoga wafanye kazi wataonekana tu. Mheshimiwa ameshajua nani atabaki na nani ataondoka, wasiwe na wasiwasi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la TASAF. Niseme wazi kwamba suala la TASAF ni kitu kizuri, niwapongeze sana TASAF kwa kazi nzuri ambayo wanafanya. Mimi ni Mjumbe wa TAMISEMI tumezunguka mikoa mingi, tumeangalia kazi ambazo zinafanyika na nyingine ukienda kama Pemba kule unaweza kushangaa mambo ambayo wanayafanya, wameenda mbali zaidi na sasa hivi wanafanya na mambo ya uchumi kwa kutumia fedha zile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nafikiri kwa kuwa baadhi ya sehemu kumeonekana kuna matatizo turekebishe yale matatizo, tatizo kubwa lipo kwa Watendaji wa Halmashauri zetu, kwa sababu hawa Watendaji ndiyo wanapelekewa pesa, kwa hiyo, wao kwa sababu ya mazoea ya miaka ya nyuma walishindwa kubadilika. Sasa hivi nafikiri tukae tuone tunafanyaje ili TASAF iweze kusonga mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikiri wazi hata Waheshimiwa Wabunge mmeona msongamano wa wale watu ambao walikuwa wanahitaji msaada kwetu umepungua, umepungua kwa sababu ya TASAF; wengi wanakuwa wamemaliziwa matatizo yao huko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho kabisa ni ajira. Tunashukuru sana kwa kazi ambayo mmeifanya, mmefanya uhakiki vizuri sana tena tunakuombea na Mungu akubariki. Sasa kazi iliyobaki ni ajira maana vijana ambao tumewasomesha sasa wasije wakaingia kwenye mambo mengine mabaya, juzi Dangote alitangaza kazi za udereva walioomba wengi ni kutoka Vyuo Vikuu kwa sababu hakuna kazi. Kwa hiyo, nafikiri wewe tangaza ajira na hivi umeshaanza basi wengi watapata na mimi niombe kwa kupitia nafasi hii vijana watulize munkari kwamba ajira sasa zitamwagwa na Serikali yetu hii itatujali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa kwa sababu muda ninao nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu. Kwa kweli kazi aliyoifanya ni kubwa, mabadiliko tunayaona na mwenye macho haambiwi tazama anaona mwenyewe, kazi iliyobakia ni sisi kuwasaidia. Tuwasaidie tufanye kazi tuwe kitu kimoja ili tusonge mbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania kanyaga twende, ahsante kwa kunisikiliza.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa
Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii jioni hii ya leo. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe kwa kazi nzuri ambayo anaifanya na ameonyesha kwamba yeye ni mwanamichezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nachukua nafasi hii kumpongeza sana Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Ndugai kwa kutupa ushirikiano mkubwa, hasa timu yetu ya Bunge Sports Club. Pia nimpe pongezi nyingi Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu yeye siyo tu kutupa ushirikiano, amekuwa ni mchezaji mahiri ambaye anapokosekana, basi inatupa shida. Kwa nafasi hii pia, nawapongeza sana timu yetu ya Lipuli Sports Club ya Iringa ambayo imepanda daraja. Naomba Mungu awajalie ili wahakikishe kwamba tunaendelea na tuweze kuchukua ubingwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kuchangia sana sana leo nitajikita kwenye kutoa ushauri zaidi, kwa sababu tumekuwa tukichangia mara nyingi kwenye Wizara hii ambayo kwa kweli ina wapenzi wengi kuliko Wizara nyingine. Kwa sababu wanamichezo wapo wengi kuliko wanachama wa vyama vyetu vya kisiasa, lakini bado haijatendewa haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ambayo Wizara hii imepitishiwa ni shilingi bilioni kama 28. Fedha hii haitoshi kwa sababu Wizara hii imebeba mambo mengi. Wizara hii mwaka 2016 tofauti na mwaka 2015 ambapo walipata fedha nyingi kuliko mwaka huu; sasa mimi sina hakika kama tuna dhamira ya kutaka kweli kupambana na mambo ya michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba tutawalaumu TFF kwamba hatufiki mbali, tutawalaumu michezo mingine lakini Serikali bado haijaamua kwa dhati kwamba tumeamua sasa michezo iwe kazi. Sasa hivi bado michezo ni baada ya kazi, lakini ingekuwa ni kazi, basi ingetengewa bajeti ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku moja niliuliza swali hapa Bungeni kwamba kwa nini michezo isifutwe? Wengi hawakunielewa, wengi walifikiria kwamba huyu jamaa vipi, amechanganyikiwa? Wengine wakafikiria labda sijui nafikiria kitu gani, lakini nilikuwa na maana tu kwamba kama kweli tunataka kuendeleza michezo kwa bajeti hii, hatutafika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe ushauri kwamba kama kweli tumedhamiria kuisaidia Wizara hii na Mheshimiwa Mwakyembe na Naibu wake waonekane wamefanya kazi, basi tuhakikishe Bodi ile ya Michezo ya Kubahatisha inahamia kwenye Wizara hiyo. Mheshimiwa Waziri wa Fedha bila kufanya hivyo Mheshimiwa Mwakyembe hutafanya lolote, utaondoka hutafanya chochote ambacho unaweza ukajivunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nafikiri kwa sababu sheria inasema, fedha ambayo inatoka kwenye Bodi hiyo ni ile ya mchezo wa Bahati Nasibu ya Taifa, lakini kwenye Bodi ile kuna michezo mingi kama betting, kuna casino ambazo zinaingiza fedha nyingi. Zile zinakwenda Wizara ya Fedha, inayokwenda pale ni kutoka kwenye mchezo wa Bahati Nasibu ya Taifa ambao unachezwa mara moja au mara nyingine hauchezwi kabisa kwa mwaka. Kwa hiyo, nafikiri tuhamishe Bodi hiyo iende iwe chini ya Wizara ya Michezo, kutakuwa kuna fedha ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, tuvunje Baraza la Michezo la Taifa (BMT) ma tuanzishe kitu kinaitwa Shirikisho la Michezo la Taifa. Ukishaweka shirikisho, maana yake itakuwa ni rahisi kutafuta vyanzo vya pesa; lakini leo Baraza la Michezo wako hoi, hawana kitu chochote. Na mimi nilikuwa Mjumbe wa Baraza na najua yaani hapo unawasukuma tu, lakini hatuna dhamira ya kweli ya kuinua michezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nafikiri tutoke. Mwaka 2016 nilishauri nikasema niko tayari mkitaka niwasaidie kuandika kitu hicho kizuri, kwa sababu nilishafanya utafiti, ninazo nondo za kutosha, hamtakwama. Msiogope kupata ushauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye TFF. TFF nawaomba pamoja na kuwa fedha ambazo mnapata ni kidogo, lakini hebu wekeni mambo vizuri, kwa sababu malalamiko kwa TFF sasa hivi yamekuwa ni makubwa, vilabu havifanyi chaguzi, Mabaraza ya TFF mikoani imekufa, ni migogoro. Kwa hiyo, tusitegemee kama tutakuwa na timu nzuri. Kwa hiyo, nashauri hebu jikiteni kwa wanachama wenu, wapeni uelewa waweze kuelewa wapi tunatoka na wapi tunakwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, tumekuwa tunafanya vibaya na timu yetu ya Taifa. Ukiangalia ligi ya Tanzania kwa Afrika Mashariki ndiyo ligi bora sawa sawa na Uingereza. Ligi bora kwa sababu gani? Kanuni za mchezo wa miguu kwa nchi yetu zinaruhusu kuwa na wachezaji wengi kwenye vilabu. Kwa hiyo, unakuta timu ya Taifa ligi ni nzuri, lakini unapokwenda kuchangua timu ya Taifa huwezi kupata wachezaji wazuri, kwa sababu wachezaji wale wengi ni wa nje ya nchi yetu kama ambavyo ligi ya Uingereza ilivyo. Ligi ya Uingereza ni nzuri, lakini hawana timu ya Taifa nzuri. Kwa hiyo, naomba warekebishe hizo kanuni ili tuweze kupata timu nzuri ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusu academy. Tunasisitiza kwamba kila timu iwe na academy na watu binafsi waanzishe academy, lakini kuanzisha ni gharama kubwa. Kwa hiyo, nafikiria tujikite zaidi kwenye mashindano ya UMISHUMTA, UMISETA, SHIMIWI na michezo mingine, zile ndiyo academy zetu ambazo sisi wengine tumetokea huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, njia ni ndogo tu, wachezaji wa mpira wa Tanzania wana chama chao, nami bahati nzuri ndio nilikuwa Rais wa kile chama kinaitwa SPUTANZA. Kupitia SPUTANZA wangeweza kupata wachezaji wale ambao wamestaafu wakagawanywa kwenye mashule yote.

Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI anasikia pale, mkashirikiana wale wachezaji wakagawanywa shule zote Tanzania, hata kwa posho ndogo, ungeona mabadiliko ambayo yangetokea kwenye michezo, lakini leo hii ni taabu kwa sababu huwezi kuwaajiri na fedha hazipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Chuo cha Michezo kiko Malya. Chuo kile kinapata kila mwaka bajeti ndogo. Sasa kuna haja ya kuanzisha Chuo kingine hasa Mikoa ya Nyanda za Juu ya Iringa, Mbeya, Rukwa tukawa na chuo kingine kule. Kile chuo watu hata hawakitambui, hata Makete tungeweza kuanzisha kwa sababu ya hali ya hewa nzuri, lakini sehemu inayofaa kabisa ni Kilolo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii niwapongeze sana wachezaji wa zamani. Leo Kitwana Manara amewawakilisha wote hapa. Hebu niseme, tuweke utaratibu wa kuwaenzi hawa watu. Leo hii kuna mtu kama Jela Mtagwa, amewekwa mpaka kwenye stamp ya nchi hii, lakini leo ukimwona unaweza ukatoa machozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mtu kama Athuman Chama, anaugua pale anakosa hata pesa, hivi kwa nini sasa Serikali, Mheshimiwa Mwakyembe usifanye mpango wakapata hata bima ya afya tu? Tutakuwa tumewaenzi wachezaji wote wa zamani, kitu ambacho kiko ndani ya uwezo wako. Kwa sababu haiwezekani ukawa unashangilia wakati anafanya vizuri, wakati akishachoka na yeye tunashindwa kumsaidia, kwa hiyo tuwasaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo yuko Sambu ametufanyia vitu vizuri, tumtunuku hata Bima ya Afya. Inawezekana hata Bima ya Afya yule hana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, kwa kweli nisingependa kuchukua muda mrefu, niseme tu Mheshimiwa Mwakyembe na Mheshimiwa Naibu wako, hebu zungumzeni na wadau wa michezo kwenye mikoa, wanawahitaji. Piteni pale mzungumze nao, wanaweza wakashauri kitu kizuri. Tuko wapi? Tumetoka wapi? Tunatakiwa kwenda wapi? Kwa sababu wameachwa, hawana watu wa kuwasikiliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mweyekiti, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuweza leo kupata nafasi hii ili niweze kuchangia. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa sababu tulipokuwa tunakwenda kwenye uchaguzi tuliomba atuletee Rais wa namna gani. Kwa hiyo nimshukuru, tusiposhukuru kwa kidogo huwezi kupata zaidi. Mwenyezi Mungu amesikia kilio chetu tumepata Rais ambaye tulikuwa tumemwomba kwa hiyo, ahsante sana Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais, alivyoingia wakati anagombea kuna vitu aliahidi; aliahidi kusimamia rasiliamli za Taifa, ameanza kazi na mmeona. Aliahidi kununua ndege, aliahidi kujenga reli, aliahidi kuendeleza ujenzi wa barabara, aliahidi kuboresha huduma za afya, aliahidi kurudisha heshima na nidhamu kazini, aliahidi kubana safari za nje, aliahidi kuendelea kuboresha ukusanyaji wa kodi, aliahidi kuleta amani kwa watu kufanya kazi kupunguza kuandamana. Kwa sababu unakuta maandamano mengi yalikuwa ni kwa sababu watu hawana kazi za kufanya, lakini leo watu wanafanya kazi, muda wa kuandamana haupo, kwa hiyo nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia aliahidi kuendelea kupunguza kodi, hasa za wakulima, mmeona kwenye bajeti yetu kodi zimepunguzwa, niseme sasa wengi wameona, yaliyopita si ndwele tugange yajayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepata bahati kubwa tusameheane, kwa sababu jana Mheshimiwa Dkt. Rwakatare na mimi niseme wazi Mheshimiwa Dkt. Rwakatare yupo hapa tunawapa kazi, Mchungaji ya kuombea Bunge hili ili watu tubadilike ukishirikiana na Mchungaji, Mheshimiwa Bilakwate yupo na Sheikh Ulega. Fanyeni kazi kubwa ya kuombea Bunge letu ili tubadilike tutetee maslahi ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii ni kweli kwa muda mrefu tumeibiwa, sasa tumesema basi na bahati nzuri tumepata bahati ya kupata Rais wa Wanasheria ambaye yuko humu ndani, tunakuomba Mheshimiwa , kwa sababu tumesema yaliyopita si ndwele utusaidie sasa tupambane tupate haki zetu kutoka kwa hao wazungu, kweli wewe ni rafiki yangu, tafadhali tuungane kwenye hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ustadh Ulega na Mheshimiwa Ustadh Lissu yupo pia. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo sasa nizungumzie habari ya hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango; niseme ningekuwa niko kule Kigoma ningesema Mheshimiwa ushimwe chane yaani ubarikiwe. Umetendea haki Taifa, umetendea haki Bunge, umewatendea haki Watanzania wote na Wanakigoma. Niseme kazi ni kwetu wenyewe sasa kusimamia, suala la kusimamia rasilimali za nchi sio la Serikali peke yake, ni suala letu sote kuhakikisha tunasimamia rasilimali zetu kwa umakini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye Jimbo langu sasa la Kilolo kidogo. Kwenye Jimbo la Kilolo Mheshimiwa Rais aliahidi kwamba atahakikisha tunapata maji safi na sasa hivi kazi imeanza, tumeanza kupata maji pale Ilula na sehemu nyingine mambo yanakwenda vizuri. Lakini pia kuna suala la kilimo cha umwagiliaji, kilimo hiki Iringa Wilaya ya Kilolo na Mkoa wa Iringa tuko milimani, kwa hiyo tunategemea sana kilimo cha mabondeni, wanasema vinyungu. Sasa ni suala la Serikali kutoa fedha kuboresha mifereji ili kile kilimo badala ya kuendelea kuzuia waache watu walime, waweke mpango mzuri, mifereji ya umwagiliaji ijengwe ili watu waendelee kulima badala ya kuendelea kuwazuia watu kulima kwa sababu tukifanya hivyo kuna hatari ya kupata njaa kwa Mikoa ya Iringa, Mbeya na mikoa mingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule Kigoma kilimo cha mabondeni wanaita masebura, ni kilekile kwamba mnalima mabondeni, nikisema hivi Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango amenielewa, kwamba masebura ni kilimo cha mabondeni sio cha kwenye vyanzo vya maji, vyanzo vya maji ni mbali lakini cha mabondeni wananchi waachwe waendelee kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokutafsiri vizuri sheria kutatufanya tulete njaa kwenye nchi hii. Kwa hiyo, nikuombe kabisa Mheshimiwa uniombee kwa Mheshimiwa Waziri wa Mazingira na Waziri wa Maji waweze kutafsiri vizuri zile sheria, kwamba kwenye vyanzo vya maji wazuie mita 60 lakini kwenye mabonde hawawezi kulima mita 60, hawaharibu vyanzo vya maji kule, wataalam wetu wasiwe wavivu wa kufikiria, ili washauri vizuri Serikali waende eneo husika wakaone kinachoendelea ndipo washauri Serikali, kwa sababu sasa hivi baada ya kutoa tangazo hilo Wakuu wa Wilaya kwa sababu wako kazini wanatetea vibarua vyao, Wakuu wa Mikoa, Watendaji wa Vijiji wameanza kuwanyanyasa wananchi. Sasa hata ile maana yote ya kupunguza kodi itakuwa haina maana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu REA nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete aliyepita kwa kuanzisha REA na Mheshimiwa huyu kuendelea kwa sababu leo nchi nzima inaenda kuwa nchi yenye nuru, taa zitawaka. Nishukuru kwamba katika Wilaya ya Kilolo vijiji vingi Mheshimiwa amenihakikishia tutapata na tutapata kwa sababu vyanzo vingi vya maji, vyanzo karibu vitano vya maji vinatoka Wilaya Kilolo, ndivyo vinavyojaza Bwawa la Kihansi, kwa hiyo lazima na mimi nipate ile ndiyo royalty au niseme ni privilege kwangu kwamba lazima tupate ili tuendelee kutunza vyanzo vya maji. Sasa ili tusiwakorofishe hilo, naomba Mheshimiwa tushirikiane waendelee kulima vile vinyungu vyao kwa kufuata taratibu ambazo zipo kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningependa kulizungumza vizuri kabisa ni suala la barabara; Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, Mheshimiwa Rais amehamia Dodoma, Wizara zimehamia Dodoma lakini asilimia 70 ya mbao zinazojenga hapa Dodoma zinatoka Wilaya ya Kilolo, lakini barabara ya Wilaya ya Kilolo iko dhooful-hali, Waarabu wanasema dhooful-hali yaani iko katika hali mbaya. Kwa hiyo, ningeomba utusaidie tuweze kupata lami, ni kilometa kidogo ziko kilometa takribani 17 na Serikali sasa hivi ilikuwa na mpango wa kila mwaka inajenga kilometa moja, lakini…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwamoto, nimekuongezea dakika moja.

MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Kwahiyo naomba Mheshimiwa utufikirie ili tuweze kupata barabara ya lami lakini pia yale maboma ambayo yamebakia hayajamalizika, wananchi wamejitolea waweze kumalizia, Mheshimiwa tenga hizo fedha, uwezo huo unao. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia hotuba ya Wizara hii. Kwanza kabisa, nianze kwa kuwapongeza Mheshimiwa Profesa Mbarawa, Mheshimiwa Injinia Nditiye pamoja na Mheshimiwa Kwandikwa pamoja na wataalam wa Wizara. Nimshukuru Mheshimiwa Profesa Mbarawa kwa kazi nzuri aliyoifanya alipokuja kule jimboni kwangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli mustakabali wa nchi hii unategemea sana miundombinu ya barabara. Tunakwenda kwenye nchi ya viwanda, tusipozungumza habari ya barabara, hakuna mafanikio tena kuhusu viwanda. Kwa hiyo, niwaombe sana hizi kelele ambazo tunapiga siyo kwa manufaa yetu bali ni kwa manufaa ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitakuwa na maneno mengi sana, nitakuwa na maneno kidogo sana. Kwanza nianze na barabara ya mkoa ya Kilolo ambayo inaanzia Iringa – Kilolo - Idete. Barabara hii si ngeni kwa sababu Marais wote waliopita walitoa ahadi, ni barabara ambayo iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri Mheshimiwa Profesa Mbarawa alifika na alituahidi alichotuahidi, wananchi wanaendelea kusubiri. Mheshimiwa Makamu wa Rais amefika, ameahidi na wananchi wanaendelea kusubiri.

Barabara hii siyo inaunganisha Kilolo tu, barabara ya Kilolo yenyewe sasa, tuliomba lami kutoka wilayani ni kilometa nane lakini inaunganika na kilometa tatu za Iringa Mjini, kilometa kumi za Kalenga, zote zinapita kwenye barabara hiyo zinafikia takribani kilometa 21.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahadi ambayo tunayo ni ya kujenga kilometa mojamoja. Nilishawahi kuuliza hapa Bungeni, barabara hii kwa ahadi hiyo itajengwa kwa miaka 21, Mheshimiwa Profesa Mbarawa hatakuwepo kwenye nafasi hiyo, mimi sitakuwepo tena, miaka 21 mingi, ndugu yangu Mheshimiwa Injinia Nditiye na yeye hatakuwepo na Mheshimiwa Kwandikwa hatakuwepo. Sasa tunaomba waitendee haki, unaposikia ujenzi wa Makao Makuu Dodoma mbao asilimia 60 zinatoka Kilolo. Kama kweli zinatoka Kilolo inakuwaje unamwacha mtu ambaye analeta maendeleo kwenye makao makuu ya nchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali kubwa, nzuri ya halmashauri ya wilaya imejengwa Kilolo, ndiyo hospitali ya mfano, lakini hospitali ile itawasaidia hata watu wa kutoka Iringa Mjini, Mufindi na sehemu nyingine, unawasafirishaje? Sidhani kama kuna mgonjwa ambaye atapona akiwa anapelekwa kwenye ile hospitali. Ili waendelee kuwaombea vizuri, Mheshimiwa Profesa Mbarawa afanye lile Mungu atakalomjalia kuhakikisha kwamba hizo kilometa tunazipata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Mfugale ambaye kwa kweli ametusaidia sana nchi hii pamoja na Mkoa wa Iringa kwa ujumla kwa kujua umuhimu wake. Mwenyezi Mungu aendelee kumpa afya njema, aendelee kumlinda ili aendelee kutusaidia pale atakapoweza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ya mkoa inakwenda mpaka Idete, nimeshawahi kusema hapa Bungeni kwamba barabara pekee inayounganisha Mkoa wa Iringa na Mkoa wa Morogoro inapita kwenye Milima ya Kitonga. Siku milima ile mawe yakadondokea barabarani
au kukatokea tafrani yoyote, uwezekano wa magari ya kutoka South Africa, Zambia, Malawi kwenda Dar es Salaam au Morogoro itakuwa hakuna. Kwa hiyo, barabara pekee ni kuunganisha Idete – Itonya – Muhanga - Morogoro (Mbingu) kwa Mheshimiwa Susan Kiwanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ile siyo ndefu, ni kilometa takribani 25, wananchi wameshaifungua na ahadi ya mwanzo ilikuwa kwamba barabara ile mkoa iichukue kwa sababu ni barabara ambayo ilikuwa ya mkoa. Sasa baada ya TARURA kuanza bado TANROADS wanaweza kuweka mkono wao hata kwa wataalam ili barabara ile sasa ipitike. Leo tunazungumza hapa kama mzaha lakini kuna siku watakuja kukumbuka maneno yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sitaki sana kusema kwa sababu nimeshasema sana kuhusu suala hili niende kwenye mawasiliano. Ndugu yangu Mheshimiwa Injinia Nditiye anajua tumetoka wote Kibondo kule, sasa akija akinitupa leo kwa kukosa mawasiliano nikienda Kibondo nitazungumza kule kwamba ndugu yangu ameshindwa kunisaidia, itakuwa siyo kitu kizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sehemu, kwa mfano, Ifua, Udekwa, Irambo, Ibumu, Magana, Ilindi ambako ni Mahenge, Imalutwa, Lugalo, hivyo ni Vijiji, Mbawi, Masisiwe, Isere, Ukwega, Ikula, Ruaha, Mbuyuni na Isagwa hakuna kabisa mawasiliano. Bado narudi palepale, tunakwenda kwenye nchi ya viwanda, unaendaje kwenye nchi ya viwanda wakati mawasiliano hakuna, barabara hakuna. Kwa hiyo, mimi nimwombe ndugu yangu, aliniahidi kufanya ziara, hebu afanye ziara. Kama atakuwa hana mafuta niko tayari kumwekea ili tuweze kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kwandikwa na yeye kwa sababu Mheshimiwa Profesa Mbarawa alishafika, kazi sasa ni yeye, wao ndiyo wasaidizi wake, aje Kilolo sio mbali, kilometa zile sio nyingi, ziko kwenye ilani. Nikileta Hansard hapa toka mwaka 2000 nikiwa Mbunge nimekuwa nikiambiwa habari zilezile. Sasa tusimuangushe Mheshimiwa Profesa Mbarawa, kama kweli wanampenda twende sote pale, sio mbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Rais, Mheshimiwa Dkt. Magufuli katutengenezea barabara, kutoka Iringa mpaka Dodoma ni saa mbili na nusu, hata kama Bunge limeahirishwa, twende tunarudi tunakuja kutoa maoni hapa. Mnajua hasira za watu wa Iringa, kuna mambo mengi ambayo hayaendi vizuri, sasa hivi hatujinyongi tena, tunapanda juu ya mti unajitupa kwenye lami unakufa vizuri. Kwa hiyo, tutengenezeeni lami tu ili tuache kujitundika kwenye miti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndege, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, amefanya kazi kubwa, ametuletea ndege za uhakika na kelele hizi zilikuwa zinapigwa nchi gani haina hata ndege, lakini leo tuna ndege. Mheshimiwa aendelee kuongeza kwa sababu siku zote vita ya kiuchumi lazima akubali na kelele lazima zipigwe. Wako ambao watasema huyo, huyo, yeye asigeuke nyuma, aende, pale alipo na sisi tupo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, standard gauge, hata kama haipiti Kilolo, Iringa huko ni kwa ajili ya nchi hii. Barabara zetu zinakufa kwa sababu hatuna reli, kila mtu anajua hilo. Kwa hiyo, reli ile itakwenda mpaka Moshi kwa Mheshimiwa Mdee kule itafika na tunaomba waifungue ile. Mheshimiwa Injinia Nditiye wajitahidi waifungue ili Mheshimiwa Mdee naye aone manufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema pia suala la kuimarisha barabara nyingine hasa hapa Dodoma. Mji huu umeshakuwa mkubwa na tumeshaanza kupata shida kwenye hizi barabara. Leo hii kama wanafikiria mambo ya mabasi yaendayo kasi hiyo mipango ianze sasa, siyo ifikie wakati tuanze kubomoa nyumba za watu, itakuwa ni aibu. Tufanye sasa, kama kuna madaraja wa-plan sasa hivi ili baadaye isije ikatokea bomoabomoa. (Makofi)


Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sipendi kuzungumza maneno mengi kwa sababu siasa ya Kilolo ni barabara. Waheshimiwa Wabunge wanashindwa hata kufanya ziara sehemu nyingine kwa sababu barabara zimeharibika. Unapokwenda kule unaulizwa habari ya barabara na uliahidi kutengeneza barabara unajisikia aibu. Kwa hiyo, tutengenezeeni barabara twende majimboni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nami nianze kwa kuwapongeza vijana wana Paluhengo Lipuli Sports Club kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. Bila kuwasahau Dar Young Africans. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaenda zaidi kwenye ushauri na mchango wangu utakuwa kwenye ushauri zaidi. Kwanza kabisa nianze kuishauri Serikali kwamba chombo kikuu ambacho kinasimamia michezo ni Baraza la Michezo la Taifa (BMT). Kwa mujibu wa sheria na taratibu, Sheria Na. 12 ya Mwaka 1967 ndiyo ilianzishia chombo hiki cha michezo maana yake Baraza na ikafanyiwa marekebisho mwaka 1971.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chombo hiki ndicho ambacho kinapaswa kusimamia, kuendeleza, kustawisha, kuratibu aina zote za michezo kwa kushirikiana na wadau. Ukiangalia chombo hiki kinategemea fedha kutoka Serikalini, sasa ukiuliza wanazo shilingi ngapi utashangaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nafikiria, either tuletewe hapa tubadilishe sheria au ikiwezekana Baraza la Michezo livunjwe kwa maana ya kuanzisha kitu kingine ambacho kinaweza kikajitegema, tukaanzisha labda Shirika la Michezo la Taifa badala ya Baraza kwa sababu ukileta likawa Shirika la Michezo la Taifa na kuna neno wadau pale wanaweza wakafanya biashara. Fedha zile ambazo tunasema ziende kwenye michezo ambazo ni za gaming za mambo ya michezo ya kubahatisha zingeweza kwenda kule wakawa na uwezo wa kujiendesha wenyewe kwa vyanzo mbalimbali ili sasa tukienda kwenye kutayarisha timu zetu tuwe na fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ambayo Mheshimiwa Mwakyembe amepata, kwanza nimpongeze sana kwanza kwa kazi nzuri ni fedha ambayo tungeweza tu kuiweka timu ya Taifa kwenye matayarisho ya michezo siyo ya Wizara. Kwa hiyo, akisema kwamba ataweza kufanya vizuri ni kujidanganya na ndiyo maana niliwahi kuuliza hapa siku moja kwa nini tusiifute michezo Tanzania? Hata hivyo, swali hili lilikuwa gumu kujibiwa. Maana yangu ni kwamba unataka kukamua maziwa wakati hujamlisha ng’ombe majani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, naomba tukae chini, tufikirie kitu gani tukifanye ili Baraza liwe na meno, uwezo kama tunataka kuendelea na Baraza, lakini kama haiwezekani tulivunje kwa sababu leo kazi kubwa ya Baraza la Michezo ni kusajili vyama vipya na kuvifunga na kuvifungia vile ambavyo vimefanya makosa, kazi ambayo siyo nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa michezo ya AFCON wa vijana chini ya miaka 17 itafanyika hapa, maandalizi sina hakika kama yameanza na hayawezi kuanza kwa sababu hamna fedha, kama yapo ni yale ya mechi hizi ambazo zinaendelea. Wasiwasi wangu ni kwamba inawezekana tukatumia fedha nyingi sana na gharama kwenye vikao kuliko maandalizi ya timu, matokeo yake tutakuja kutoa visingizio vingi, ningeomba Serikali iangalie uwezekano wa hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, medali nyingi Tanzania tulianza kuzipata kwenye michezo mbalimbali, mwaka 2003 tulipata medali 12 za wanariadha kwenye Special Olympic Ireland. Bahati nzuri fedha zilikuwa hamna tukatayarisha mechi kati ya Mabalozi na Wabunge, fedha iliyopatikana tuliwasafirisha wale watoto kwenda Ireland na walileta medali 13. Baada ya hapo hakuna medali ambayo imeletwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wanapokwenda kwenye riadha bahati nzuri Filbert Bayi yupo nimemwona, wanapokwenda kuwakilisha nchi, hawaendi watatu au wanne. Sisi tumepeleka wanariadha timu nzima nafikiri hawazidi 50, wanariadha waliotoka Kenya walikwenda 200 hawawezi kukosa medali, lakini sisi utapeleka wote hao kwa maandalizi gani? Kwa hiyo, naomba kama kweli tunataka michezo ya nchi iendelee basi tujipange. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri ajaribu kwa sababu Mabaraza hayapo yamekufa kama yapo hayana uwezo, akae na wadau tena aanzie hapa Bungeni, akae na wadau wa michezo tuko wengi tu halafu tuone tunatokea wapi ili tusimwache peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine Mheshimiwa Cosato Chumi amelizungumza na mimi niliwahi kuzungumza hapa, kwamba sisi tunataka timu ya Taifa ifanye vizuri. Timu zetu zimesajili wachezaji wengi wa kigeni kutoka nje ambao hawana uwezo. Kwa hiyo kinachofanyika wachezaji wetu wanakosa nafasi. Unasajili wachezaji ambao hata kwenye nchi zao hawana nafasi, unakuja inakuwa dampo. Kwa hiyo, ningeomba Ndugu yangu Karia yupo, hebu waangalie uwezekano wa kupunguza idadi ya wachezaji, ikishindikana basi angalau wale watakaokuja kucheza wawe ni watu ambao wana uwezo kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Timu ya Taifa inapocheza, jezi zile inazotumia hazina hadhi ya nchi yetu kwa sababu hazina bendera, rangi zetu zinafahamika za bendera yetu lakini leo tunavaa jezi nyeupe wapi na wapi, tumekosa rangi.

Kwa hiyo, niombe Karia yupo hapo, Kiganja nimemwona, ndugu yangu Tandau nimemwona, hebu wakae wafikirie, tusitie aibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia najua sana kwamba Wizara kwa kushirikiana na TFF watapita kuangalia viwanja vyenye hadhi vitakavyotumika Kimataifa ili viweze kutambulika na FIFA. Uwanja wa Samora Iringa hebu wapite pale waone umetengenezwa kisasa, uko vizuri na watu wako radhi wana uwezo wa kwenda kuangalia mpira na wameona timu ya Lipuli mambo ambayo inafanya, unaweza ukawauliza watu wa Singida wanaweza kueleza.(Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, ningependa kumpongeza sana Mwenyekiti wa Bunge Sports Club ndugu yangu William Ngeleja. Baada ya Wabunge kushiriki michezo tumepata faida kubwa sana; moja, ukiangalia idadi ya watu wanaokwenda hospitali kutibiwa imepungua. Idadi ya watu wanaokwenda kwenye sehemu za starehe kunywa pombe imepungua, ndiyo maana umeona hata walioitwa kwa Mheshimiwa Paul Makonda walikuwa wachache kwa sababu wamekuwa na shughuli sasa nyingine mbadala ya kufanya ambayo ni mazoezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Spika amwangalie Mheshimiwa William Ngeleja amwongeze fungu kwenye fedha zile ili wanamichezo wengine washiriki, lakini sitaacha pia kumshukuru Mwenyekiti pamoja na Majimarefu ambaye kwa kweli wanasaidia kwenye yale mambo mengine na kufanya timu yetu iweze kufanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchangiaji aliyemaliza amechangia vizuri sana, niombe badala ya kulalamikia viwanja vile ambavyo vina wenyewe, tuangalie uwezekano wa kuomba vingine kuna nafasi, ombeni CHADEMA muweze kupata viwanja vingine vya michezo waje waombe, Iringa tuna maeneo, Kilolo tuna maeneo, waje waombe ili nao wamiliki badala ya kugombea hivi ambavyo vipo, kwa sababu hivi tumerithi zamani Chama kilikuwa kimoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kukushukuru wewe kunipa nafasi hii jioni ya leo. Kwanza kabisa, nianze kumpongeza ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla pamoja na Naibu wake rafiki yangu Mheshimiwa Hasunga. Niseme Wizara hii ni nzito na usitegemee hata siku moja kupongezwa sana kwa sababu, inagusa watu wengi na mambo mengi. Kwa hiyo, niwapongeze kwa hapo mlipofikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuzungumza habari ya vivutio vilivyopo katika Wilaya ya Kilolo. Wilaya ya Kilolo ni moja ya wilaya ambayo ina vivutio vingi sana vya maliasili ambavyo naweza kusema vimesahaulika. Moja ya vivutio ni ile sehemu ambayo Wajerumani na Wahehe walipigania pale, ni sehemu ambayo ina sifa kubwa na mpaka kusababisha jeshi letu barracks yao kuitwa jina lile, Lugalo, lile jina linatoka pale. Ile sehemu kuna makaburi ya mtu anaitwa Zelewsky au Nyundo, ambaye aliuwawa pale na Wahehe lakini kivutio kile kimesahaulika kabisa na sidhani kama kuna Waziri yeyote ambaye alishafika pale. Ushauri wangu ni kwamba, hebu tuanze kufufua vivutio hivyo kwa sababu wenzetu wa Ujerumani wanapita kila mwaka pale wanaangalia na wanapiga picha wanaondoka, hatupati kitu. Kwa hiyo, naomba tu Mheshimiwa hebu tupite pale tuangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine nashukuru ndugu yangu Mheshimiwa Chumi amejaribu kuligusia, ni suala la Gereza ambalo liko kule Kilolo linaitwa Kihesa Mgagao. Ile sehemu ni nyeti sana, ni sehemu ambayo walikaa Wapigania Uhuru. Chumba alicholala Mzee Mandela kipo mpaka leo, Sisulu kuna chumba alicholala kiko pale mpaka leo, lakini cha ajabu sijui nani aliyetoa ushauri, tumeenda kufungua magereza. Leo wenzetu wa South Africa wamekuja, kuna makaburi pale, kuna familia wameacha, kuna watoto mpaka leo wameachwa pale, wanataka kuja kuangalia sehemu ile lakini hawaruhusiwi kuingia na wako tayari hata kutoa misaada mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu gereza liko chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani, ningeshauri mshisirikiane Wizara ya Mambo ya Ndani na Maliasili, ili kugeuza kile kiwe kivutio. Bahati nzuri na Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje yupo leo, tufanye kivutio na wewe unatoka Iringa, ambacho tutaingiza pesa nyingi tu kama mali ya kale. Kwa hiyo, niombe hilo lifanyike na ningeomba Mheshimiwa Waziri aweze kufika pale. Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla bahati nzuri tunalima jirani kule Kilolo na yeye ni mkulima wa Kilolo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la fuvu la kichwa cha Mkwawa. Ni sehemu ambayo kwa kweli sasa hivi mnaleta migogoro tu kwenye familia ile kwa sababu hakitunzwi vile kinavyotakiwa. Mmeleta mgogoro kati ya ma- chief na wananchi na Serikali yenu ambayo ni Wizara ya Maliasili. Kwa hiyo, ningeomba vitu kama vile ni vitu ambavyo havitokei kihistoria na identity ya sisi watu wa Iringa ni pamoja na vitu kama vile. Kwa hiyo, naomba mtutendee haki, tuangalie jinsi gani tunaweza tukafanya kikawa kivutio na Serikali ikaingiza fedha lakini kwa sasa hivi mmekitelekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabila langu ni Mzungwa, natoka kwenye Milima ya Udzungwa ambayo ni Kilolo, Iringa, lakini leo hii unaposema Udzungwa mtu yeyote anayejua anajua ni Morogoro kiasi kwamba sisi watu wa Kilolo au Udzungwa tunapopata miradi inaonekana kama ni hisani siyo haki yetu. Bahati nzuri Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla bado alikuwa yuko masomoni, lakini wanaojua Udzungwa ilipokuwa inaanza waliweka makao makuu Morogoro kwa sababu ilikuwa hamna njia ya kupita kwa kupitia njia ya Iringa lakini leo hii inaonekana beneficiary ni watu wa Morogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ningeomba aidha, sisi watu wa Iringa mtuhamishie Morogoro au tunufaike na mbuga hizo ikiwa ni pamoja na kutengenezewe barabara na miundombinu mingine. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla, wewe ni msikivu sana hebu lifanyie kazi hilo. Itakuwa siyo vizuri tutakapokuja kwenye bajeti ijayo, tukazungumzia kitu kilekile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye Mbuga za Udzungwa kuna Vijiji vya Ruaha Mbuyuni, Mahenge na Mgowelo, kuna shida kubwa sana ya wanyamapori. Tembo wamekuwa wakiuwa sana binadamu lakini kile kifuta jasho kimepitwa na wakati. Mimi ningefikiria hebu tushauriane kwanza tuongeze kifuta jasho lakini ulinzi ule shirikishi kati ya wananchi na Afisa Wanyamapori uwe karibu. Nimshukuru sana Mhifadhi Mkuu wa Kikosi cha Ujangili cha Mkoa wa Iringa jinsi ambavyo amekuwa akitupa ushirikiano. Kwa hiyo, niombe tubadilike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna suala la Ruaha National Park, niishukuru sana Serikali kwa kuamua kuboresha mbuga ile kwa kupeleka barabara ya lami na pia kwa Serikali kuamua kununua ndege. Kwa kawaida huwezi kuona faida ya ndege zile usipochanganya na utalii. Sasa hivi utalii utapanda kwa sababu watalii wengi watafika kwa sababu wanaweza kufika na ndege zipo na uwanja wetu wa Nduli Airport utakuwa umeboreshwa, kwa hiyo, tutapata wageni wengi. Kwa hiyo, nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa uamuzi wa kununua ndege zile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro kati ya wafugaji na hifadhi. Watu wengi wamelalamika, bahati nzuri nilishawahi kuwa Mkuu wa Wilaya, migogoro hiyo ipo siyo ya kuibeza. Changamoto ninayoiona mgogoro ule anaachiwa Maliasili peke yake wakati ukiangalia ni mgogoro mtambuka Wizara zinatakiwa zishirikiane, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Maliasili, Wizara ya Ardhi na Wizara ya TAMISEMI. Kwa sababu wanyama ni wa Maliasili, ardhi iko chini ya Wizara ya Ardhi na wale binadamu pale wako chini ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wangeshirikiana, wakajiuliza ni kwa nini wafugaji wanaingia kwenye hifadhi, ukiweza kujiuliza hilo swali mgogoro wote utakwisha. Kama mnataka kujua tatizo hili likoje, nafikiri mkakae pamoja na ikiwezekana tuunde mfuko wa pamoja wa hizi Wizara nne tuweze kutenga fedha na kufanya utafiti wa kina na kutoa elimu ya kutosha. Ni kweli wafugaji wanapata shida lakini kuna mambo ambayo yanasababisha mojawapo ni upimaji wa ardhi, watu wameshalalamika kwamba tuangalie, je, ni kweli Wizara ya Maliasili imeingia ndani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisingependa kulaumu Wizara wala Waziri ni vijana wenyewe wana matatizo, hasa hawa ambao wako kwenye hifadhi wa kikosi maalum kile cha kuzuia ujangili. Wanafanya kazi yao vizuri lakini inafikia mahali wanapitiliza, wanaweza wakaenda nje ya mipaka yao ya kazi. Kwa hiyo, nafikiri tukiunda tume ya pamoja au mfuko wa pamoja wa hizi Wizara nne tunaweza tukatatua tatizo hili ambalo linawasumbua wenzetu wafugaji, wamekuwa wakilia kwa muda mrefu bila suluhisho. Kwa hiyo, tuwasikilize kwa sababu ni wenzetu na mifugo ni yetu, wanyama ni wetu, hatutaki kuona wanyama wale wanapata matatizo kwa sababu tunahitaji hifadhi na fedha za kigeni, lakini hatupendi pia kuona wafugaji na mifugo yao wanapata shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wale ambao wamelalamika kwamba mifugo yao imeuzwa, tuwasikilize. Kwa kupitia tume hiyo, tutakuwa tumetatua. Niiombe tu Serikali iwasikilize ili tuweze kutatua tatizo hili. Kwa sababu mimi najua Rais wetu ambaye yupo sasa hivi ni Rais wa wanyonge…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuchangia hayo, niunge mkono hoja hii.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kuwapongeza Wenyeviti wa Kamati zote waliowasilisha taarifa zao na hasa Mheshimiwa Jasson Rweikiza ambaye ni Mwenyekiti wangu wa Kamati. Pia niipongeze Serikali kwa ujumla wake kwa kazi kubwa ambayo imefanyika kwa kipindi hiki cha miaka mitatu. Najua kuna changamoto ambazo sisi inabidi tuzifanyie kazi.

Mheshimiwa Spika, kwanza tulikuwa na upungufu mkubwa sana wa madarasa na vituo vya afya, zahanati pamoja na hospitali lakini Serikali kwa kujua hilo ilianza kupambana na changamoto hiyo. Changamoto kubwa ilikuwa ni majengo na sehemu kubwa majengo yamejengwa. Kwa hiyo, changamoto kubwa sasa ni upungufu wa wauguzi, walimu na kadhalika ambayo inaweza kutibika.

Mheshimiwa Spika, kwa huwa Serikali imesomesha kwenye vyuo vyetu vijana wengi kabisa na hawana shughuli na Serikali imewakopesha, kitu ambacho naishauri Serikali wapo ambao wapo tayari kujitolea, kwa nini Serikali isikubali vijana wale badala ya kukaa wakajitolea wakafanya kazi zile kupunguza upungufu wa wauguzi na walimu kwa miaka angalau miwili na shule zetu zote zingekuwa hamna upungufu sijui kuna kigugumizi gani? Pia wale ambao watafanya vizuri maana wanadaiwa na Serikali baadhi ya fedha zikapunguzwa kwenye mikopo yao ili waweze kufanya kazi kwa kujitolea na wengi wapo tayari. Naomba hilo Serikali ilichukue na ilifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ni hili la TARURA. Tulipitisha wenyewe hapa Bungeni Muswada wa TARURA lakini leo tumeshaanza kugeuka kwa kuanza kusema Meneja wale waende wakaripoti kwenye Baraza la Madiwani. Nafikiri kikubwa tungeangalia changamoto lakini kazi inayofanyika ni kubwa, kama sisi Wabunge tutapitisha fedha kwa maana ya mgao, maana mgao uliopo sasa hivi ni 70 kwa 30, tukawaongozea TARURA kelele zitakuwa hazipo. Kama ilivyo TANROADS wanafanya kazi vizuri, ukiwaingiza kwa Madiwani au Wabunge inakuwa ni mfumo wa kisiasa, kila mmoja atataka barabara yake ijengwe hata kama ni kilomita 2 lakini unapowaachia huru, wanatoa tu taarifa kazi zitakwenda. Nafikiri tujikite zaidi kuona tunawaongezea ngapi ili kazi ifanyike kwa sababu sisi wenyewe tulipitisha kwa kuangalia changamoto nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, asubuhi niliuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu na alinijibu vizuri sana. Nafikiri kuna haja Waziri wa Fedha mkawaongezea fedha wenzetu wa Wizara ya Michezo ili suala hili lipewe umuhimu. Kama nilivyosema asubuhi, sidhani hata baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hapa wana ulewa mzuri, michezo ya AFCON ni michezo ya Afrika nzima under 17 inafanyika Tanzania na hakuna matangazo ya kutosha ambayo yameshatolewa kuwapa watu uelewa waweze kuchangia pato la nchi ili fedha hizo siende kufanya kazi mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumenunua ndege ndiyo ulikuwa wakati wa kutangaza wa ndege zile hata ikiwezekana Meneja wa Shirika la Ndege akasema kwamba kwa wale wataokwenda kuangalia michezo kutoka Iringa na sehemu nyingine watapata punguzo wakati wa mechi wakikata tiketi mapema, fedha zile zingeongezwa kwenye uchumi wetu. Rais wa FIFA atakuwepo hapa na kundi kubwa kabisa la watu kutoka nje ilikuwa ndiyo wakati mzuri wa kutangaza utalii wa nchi yetu na wao wakitoka hapa wangeweza kuwa Mabalozi wazuri wakatutangazia nchi yetu huko nje ili tuingize pato kwenye utalii. Nafikiri hili ni suala na Mheshimiwa Waziri wa Michezo na Waziri wa Maliasili kuangalia wanafanyaje ili kuhakikisha tunatangaza vizuri mashindano haya na kutuingizia pato kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho kabisa ni suala ambalo pia limezungumzwa na watu wengi. Mwaka jana tulikuwa na tatizo kubwa sana la mlundikano wa wanafunzi waliofaulu, ikabidi tuanze mchakamchaka kwa ajili ya kujenga madarasa, mwaka huu tatizo liko palepale. Nafikiri kuna tatizo labda kwenye takwimu au la wataalam wengine. Kwa sababu hivi leo watakaomaliza mwaka huu mwishoni idadi tunayo, kwa nini tunangoja kuja kuanza kufanya mchakamchaka wakati tunaweza tukatatua jambo hilo mapema? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niishauri Serikali kwamba kama ni kwenye bajeti liingizwe ama lishughulikiwe kwa njia yoyote lakini mapema siyo kama sasa hivi kuna wanafunzi ambao hawatakwenda shule wanasubiri mpaka mwezi wa pili, tatu, madarasa yajengwe ndipo waende, nafikiri hapo kuna tatizo. Niombe Mawaziri wafanye kazi kwa nguvu zote na kushirikiana badala ya kufanya kazi ya zimamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nisingependa kusema mambo mengi, niunge mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii niweze kukushukuru kwa niaba ya Bunge Sports Club, nami mwenyewe. Kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa kazi nzuri ambayo wamekuwa wakiifanya na kutusaidia kupelekea timu zetu nyingi kufanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nianze kuchangia, nitajielekeza zaidi kwenye ushauri kuhusu michezo. Tulikuwa na mfumo mzuri sana wa kuwapata wachezaji kwenye timu zetu za Taifa toka zamani. Tulikuwa tuna michezo ya UMISETA, UMISHUMTA, SHIMUTA, michezo ya majeshi na michezo mingine. Huko ndiko ambako timu zetu za Taifa zilikuwa zinapatikana na ndizo academy zetu zilikuwa, lakini leo hivi vyote havipo, tumeua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ule uwezekano wa kupata timu nzuri umeanza kuwa shida. Kwa sababu ukiangalia pamoja na kuwa tumefanya vizuri kwenye Timu ya Taifa ambayo bahati mbaya jana na juzi imefungwa, jinsi walivyopatikana wachezaji inaonesha kabisa bado mfumo siyo mzuri, kwa sababu wale wachezaji wamepatikana kwenye academy.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika wachezaji ambao wako kwenye timu ya Taifa ile ya vijana; ni vijana wanane wanatoka kwenye Shule ya Alliance, Mwanza. Kwa hiyo, tungekuwa na academy au tungekuwa na michezo mingine mingi, maana yake tungepata wachezaji kutoka nchi nzima, lakini leo wanatoka sehemu moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naweza kusema kwamba hatuwezi kuwa na timu nzuri ya Taifa. Kwa hiyo, naomba, tuangalie ni mfumo gani sasa Serikali itaingia nao ili kushirikisha vijana wetu toka wadogo na wa kati mpaka kupata wanamichezo wazuri. Michezo yote; ukiangalia kwenye riadha sasa hivi the way jinsi ambavyo wanapatikana ni kubahatisha, lakini zamani ilikuwa unawapata kirahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Serikali itoke iangalie ni mfumo gani ambao tunaweza tukatoka nao. Kwa sababu ukisema academy ni gharama na siyo rahisi ukawa na academy nchi nzima, lakini kuna vitu ambavyo tukikaa na kubuni vinaweza vikatusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda nichangie tena kitu kingine ambacho nimekuwa nikisema siku zote, TFF bahati nzuri wapo. Niliwahi kusema kwamba Uingereza naweza kusema ndiyo nchi yenye ligi bora, lakini Timu ya Taifa ya Uingereza siku zote siyo nzuri kwa sababu ya utitiri wa wageni. Kwa hiyo, Tanzania, sipingi sana, mwanzo nilipendekeza kwamba tupunguze idadi ya wageni kwenye timu zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kinachosikitisha zaidi ni kwamba bidhaa zinapoletwa Tanzania zinakaguliwa, kuna chombo kabisa kimeundwa kwa ajili ya kukagua zile bidhaa ambazo zinaingia nchini, zile ambazo zinakuwa siyo bora zinateketezwa. Wachezaji wanaotoka nje kuja kucheza Tanzania leo hawana ubora. Kwa hiyo, Watanzania hakuna wanachojifunza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, bado narudi kusema hivi, tuweke sheria kama nchi nyingine wanavyofanya, kwamba mchezaji anapokuja kuchezea kwenye nchi yetu, lazima angalau awe anachezea Timu ya Taifa kwenye nchi yao. Leo wachezaji wanaokuja kuletwa hapa ni wachezaji ambao kule wameshindikana, hawachezi; wakija hapa ni majeruhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia upande wa Simba, kuna wachezaji wawili au watatu; Kagere, Okwi labda na Chama. Ukija upande wetu wa Yanga, unamkuta yuko mmoja tu pale, sasa wengine hata benchi hawakai.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nafikiri hebu TFF mtusaidie ili tuweze kuboresha timu zetu za Taifa. Bila kufanya hivyo, hatutakuwa na Timu ya Taifa nzuri hata siku moja. Tutakuwa tunaendelea tu kuzifurahisha Simba na Yanga, Azam lakini Watanzania watakuwa wanaendelea kukasirika kwa timu yao ya Taifa. Kwa hiyo, naomba tulifanyie kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia wenzetu juzi kwenye benchi la ufundi la Timu ya Taifa ya Nigeria, pale kwenye benchi la ufundi kulikuwa kuna wachezaji ambao walicheza Olympic mwaka 1996 alikuwepo mtu anaitwa Mateo Atepigu na Peter Lufly walikuwa kwenye benchi la ufundi, lakini ukiangalia Timu yetu ya Taifa kocha umri wake analingana karibu sawa na wale vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu huwa kwenye timu ya vijana wanaweka mtu ambaye ana umri mkubwa kwa ajili ya kuwalea kama watoto wake, watamwelewa. Sasa unaweka kijana ambaye ana umri unafanana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni ahadi. Wale watoto ni wadogo unapomwahidi gari, unaahidi fedha nyingi, wale watoto wanachanganyikiwa. Afadhali tungewaahidi basi kwamba utasomeshwa, nakadhalika. Ukiangalia kwenye Timu ya Nigeria wachezaji wanane wanacheza nje professional, lakini wa kwetu wale kama unavyoona. Kwa hiyo, hatulaumu, lakini tulipofikia siyo pabaya isipokuwa tujirekebishe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mashindano mengine yanakuja. Kuna Mashindano ya Walemavu ya Afrika Mashariki, tunapata heshima tena kama ambayo tumeipata hii. Kwa hiyo, kwa sababu tunapata hiyo heshima, haya ambayo yanaendelea siyo rahisi tena kushinda, tukishinda basi Mungu atakuwa ametusaidia, lakini yanakuja ya walemavu. Afrika Mashariki tumepata heshima hiyo tena na wanatupa heshima hiyo kwa sababu ya amani na usalama wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naiomba Serikali, Mheshimiwa Mwakyembe, tusiende kama tulivyokwenda ile, kwa sababu ile timu ndogo Taifa maandalizi ya AFCON yalikuwa siyo mazuri. Wenzetu walianza miaka mitatu kuziandaa hizi timu, sisi tumefanya miezi sita au mitatu tu. Kwa hiyo, hii timu ya walemavu angalia, inaitwa Tembo Warriors, tuangalie jinsi ya kuwasaidia sasa angalau tutoke na hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna vijana wenye mtindio wa ubongo hapa, wamechukua dhahabu kadhaa. Wale wazima wanashindwa kutuletea chochote; tuendelee basi tuwasaidie hawa wenzetu ambao wana uwezo. Kama hawa wenye mtindio wa ubongo na walemavu wengine ambao tuna uhakika wanaweza kufanya vizuri, michezo mingine imetushinda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, TBC, namwomba ndugu yangu, Mkurugenzi, rafiki yangu, kuna hawa wenzetu wenye ulemavu wa usikivu, kuna mtu ambaye anatakiwa apewe kazi pale kwa ajili ya kutafsiri alama zile ili wapate haki ya habari na wenyewe. Ni muda mrefu toka tumeomba, lakini bado hajaajiriwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hebu tuwatendee haki ili tuweze…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, lakini usikivu pia TBC kule Nkasi na Kibondo bado siyo mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba niunge mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa niunge mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, ndoto ya uchumi na viwanda haitawezekana bila kuwa na barabara, reli, mawasiliano, bandari na viwanja vya ndege na ndege zenyewe. Kwa hiyo mimi nishukuru, Mheshimiwa Waziri ujue kwamba unadhamana kubwa ya kututoa tulipo ya kutupeleka kwenye nchi ya uchumi ya viwanda, kama hutofanya vizuri kwenye Wizara hii/hamtofanya vizuri mjue kwenye hiyo ndoto ya kwenda kwenye uchumi wa viwanda itakuwa haiwezekani, kwahiyo mnatakiwa mfanye kazi kwa nguvu zote.

Mheshimiwa Spika, mimi niwapongeze baadhi ya sekta ambazo zimekuwa zikifanya vizuri, lakini sitaki kuchukuwa muda mwingi kuchanganua hii kwa sababu muda niliopewa ni mdogo.

Mheshimiwa Spika, nirudi jimboni kwangu, ninapozungumza sasa hivi mvua zinanyesha, barabara zote zote zinakufa. Kwa hiyo, mimi niombe kitu kimoja kwamba kwa kuwa tunakubali na tumepitisha Sheria ya TAKUKURU wenyewe, sasa basi tuangalie uwezekano wa kutusaidia, kuna maeneo, kuna Wilaya na Mikoa ambayo ni ya kiuchumi, mikoa ambayo inachangia pato la Taifa kwenye nchi mojawapo ikiwa ni Kilolo.

Mimi nishukuru sana Mheshimiwa Rais alifika Kilolo mwaka jana, akaahidi kutujengea barabara na ninashukuru Mheshimiwa Kamwelwe tumekuwa tukiongea kila siku na umenihakikishia kwamba barabara hiyo itajengwa ya kuanzia Iringa Mjini kwenda Kilolo na bahati nzuri kwa heshima ya pekee tumeipa jina la Engineer Mfugale kama vile ambavyo Mheshimiwa Rais ametoa daraja na sisi tumempa heshima ndugu yetu Mfugale kwanza anatoka Kilolo, lakini pia huwezi kuwa daraja bila kuwa na barabara, kwa hiyo, tumempa na barabara, kwa hiyo najua itajengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo na Mheshimiwa Kamwelwe pia kuna barabara tunategemea kukupa, kwa hiyo na wewe umeolea kule Iringa, kwa hiyo kwa heshima ya pekee lazima uhakikishe kwamba barabara ya Kilolo zinapatikana.

Mheshimiwa Spika, barabara za kiuchumi ni pamoja na Kongwa. Kongwa ni sehemu ambayo tumesema tutaweka maazimisho yote kule, kwa hiyo lazima ijengwe kama vile itajengwa Kilolo, kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa ile ahadi ya Rais usimwangushe na barabara ambazo ni barabara ya Mkoa kutoka Iringa - Dabaga - Edete inaunganika na barabara ya kwenda Mlimba; kwa kuwa barabara ile mmeipeleka TARURA, lakini TARURA awana fedha naomba hiyo barabara muikamilishe wenyewe kwa sababu Wilaya ya Kilolo kama nilivyosema safari hii kitaifa kuchangia pato tumekuwa watu wanne na kutokana na kuchangia vizuri tumeinua Mkoa wa Iringa umekuwa Mkoa wa kwanza kuchangia pato la Taifa na Mkoa wa pili umekuwa Geita, kwa hiyo niombe msituangushe.

Mheshimiwa Spika, kuna barabara ya kuanzia Kitoo - Pomerini - Kihesa - Mgagao - Mwatasi sasa hivi haipitika, mimi nikuombe Mheshimiwa jungu kuu halikosi ukoko, toa fedha hizo za tahadhari au za emergence ziweze kwenda kuwasaidia wananchi kule wanapata taabu. Wilaya ya Kilolo ndiko ambako nguzo za barabarani za umeme zinatoka, Wilaya ya Kilolo ndiko mbao nyingi zinatoka sasa hivi zinazojenga Makao Makuu, Wilaya ya Kilolo ndiko ambako tunazalisha pareto kwa wingi, inakuwaje mnaisahau?

Mheshimiwa Spika, mimi niombe mfanye kila jitihada ili zile barabara zijengwe na niombe pia barabara ile ambayo inaunganisha kama nilivyosema mkoa kwa mkoa na iko kwenye ilani ijengwe, na nimshukuru sana Engineer wa Mkoa Bwana Kindole ni mtu ambaye anatupa ushirikiano mzuri, kwa hiyo nishukuru sana.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna barabara ya Busega - Nyasuga - Ngasamo kwa ndugu yangu Chegeni, mimi naomba mumsaidie kwa sababu huyu ni mkongwe mwenzangu, tulitoka kwa ajili ya kukosa hizo barabara, sasa mmetupa matumaini tumerudi, sasa msituondoe tena kwa sababu bado tunapenda kuwatumikia Watanzania na wananchi wa majimbo yetu, ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kidogo, nafikiri mchango wangu utakuwa siyo mrefu sana. Kwanza kabisa kama ambavyo wenzangu wametangulia, tupongeze kwa jitihada kubwa ambazo zimefanywa katika Awamu hii, mambo mengi yamefanyika tukianza kwenye majimbo yetu, mambo makubwa yamefanyika ambayo kwa kweli kwa muda mfupi Serikali imeonesha jinsi ambavyo fedha zimetumika vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kujikita kwenye viwanda, niipongeze Serikali yetu kwa jinsi ambavyo iliamua kujikita kwenye suala zima la viwanda, kazi imefanyika na niseme wazi kwamba jitihada zimefanyika na viwanda vingi vimeanzishwa. Kikubwa ambacho ningependa kujua, mpaka sasa ni viwanda vingapi tayari vimeshaanzishwa? Kwa maana ya viwanda vikubwa ambavyo vinaenda kusaidia kuuinua uchumi wetu; viwanda vya kati na vidogo na je, sheria tumeshatunga za kulinda viwanda vyetu, kwa mfano, malighafi na upatikanaji wake? Nasema hivi kwa sababu ukiangalia viwanda vingi vitakuwa vikitegemea malighafi aidha kutoka ndani au nje, tumejipangaje kubadili sheria kwa sababu kwenye sheria, nyingi zimebaki kama zilivyokuwa kwa mfano sheria za kusafirisha malighafi nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano kuna Kiwanda kama cha Pareto pale Mafinga. Kiwanda kile kinategemea malighafi ya Tanzania, lakini sheria zamani hazikatazi malighafi hiyo pareto maua yale kusafirishwa nje, kuuzwa nchi zingine na tumeshuhudia sasa kiwanda kama hicho kinakosa malighafi na hivyo kushindwa kujiendesha kama ambavyo inatakiwa. Kwa hiyo, niombe tu tuangalie upya sheria zetu, lakini pia tuangalie hata bei za umeme kwa viwanda vyetu ambavyo vinakuja pamoja na kuwa tuna mategemeo makubwa baada ya kumaliza ujengaji wa bwawa, lakini tunatakiwa tuangalie mapema kwamba tutavilinda vipi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kodi; tuangalie sasa kama tutakuwa tumejenga viwanda na kuna malighafi ambazo zinatoka nje, tuangalie jinsi ambavyo tunaweza tukasaidia viwanda vyetu kupunguza kodi ili waweze kuingiza malighafi ili viwanda vyetu vijiendeshe, bila kufanya hivyo itakuwa hakuna tulichokifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nataka tu kujua kwa sababu tuko kwenye Mpango huu, nijue hali ya ushiriki wa watu akinamama na watu wenye ulemavu kwenye viwanda vyetu jinsi ambavyo watalindwa, kwa sababu ukiangalia unaweza ukakuta watu wenye ulemavu hawajawekewa mpango maalum na wao ni binadamu na wengine wana akili zaidi ya watu ambao wazima. Kwa hiyo Serikali iwe na mpango mkakati kabisa kwamba kiasi gani na asilimia ngapi wataajiriwa kwa sababu walio wengi siyo kwamba hawana uwezo kabisa, wana uwezo wa kushiriki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningependa tuangalie vilevile ni kuhusu unyanyaswaji wa wanawake na watoto katika Mpango wetu, kwa sababu ukiangalia wanawake na watoto ni watu ambao wamekuwa wakinyanyaswa kila pande na wao ukiangalia ndiyo ambao wanasaidia kwenye uchumi wetu, hasa huu wa viwanda. Ajira nyingi sana zinategemea akinamama wengi wataajiriwa, lakini tusipowawekea mkakati madhubuti wa kuhakikisha tunalinda usalama wao inawezekana uchumi wetu ukawa na shida. Nasema hivi kwa sababu tumeangalia Jeshi la Polisi ambavyo limekuwa likifanya kuanzisha Dawati la Jinsia jinsi ambavyo limeweza kusaidia kuinua maisha ya mwanamke hasa vijijini na kuongeza pato la watu. Kwa hiyo tuangalie hata katika Viwanda vyetu si mbaya kukawa na kuna Madawati ya Jinsia ili kulinda wafanyakazi na akinamama ambao wapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wa China mwaka 1978, uchumi wao ulikuwa sawa na sisi sasa, miaka 41 iliyopita, lakini leo wameshakwenda mbali kama ulivyosema na hii siyo kwamba lelemama, kuna vitu vya msingi vimefanyika. Ukiangalia China suala la rushwa hakuna ukikamatwa na rushwa unachinjwa, ukifanya kosa unapata adhabu ambayo inaonekana. Kwa hiyo na sisi lazima tujifunge mkanda, tunaweza tukapata tabu sasa, kwa sababu hata wale waliojenga reli walikuwa wamekuja wanavaa suruali ambazo zilikuwa zina viraka zinazofanana, lakini leo hii waliumia wale kwa ajili ya watu wengine ambao wanakula bata sasa. Kwa hiyo na sisi haya ambayo yanapita sasa tukubali, kuna maumivu yake kwa sababu ni mambo mapya. Kwa hiyo tukiumia, tukubali kuumia kwa ajili ya vizazi vyetu ambavyo baadaye vitakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia Mheshimiwa Rais juzi alivyokuwa ziarani kule mpakani mwa Zambia, alitoa msaada pale, kwa hiyo haya tusishangae, baada ya miaka mitano, kumi ijayo na sisi tutakuwa tunatoa misaada kwenye nchi nyingine badala ya kuendelea kuomba misaada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningependa kuliongelea ni kwa mujibu wa Sheria za Usajili wa Makampuni, Na. 12 ya mwaka 2002; Kampuni iliyosajiliwa inatakiwa katika kipindi cha kuanzia mwaka mmoja ifanye marejesho kwa Msajili maana yake BRELA yapo makampuni mengi yanayotaka kulipa marejesho ya Serikali kwa awamu kama ilivyo katika Mamlaka za TRA na Ardhi. Sasa kwa nini Serikali isikubali makampuni hayo yakalipa kwa awamu, kwa sababu ukiangalia kuna utoroshwaji mwingi wa fedha na yanashindwa kulipa, sasa matokeo yake kuna makampuni yanadaiwa mpaka miaka kumi hayajarejesha. Kwa hiyo nafikiri ni vizuri sasa sheria hii ikaangaliwa upya ili wao pia walipe kama vile ambavyo TRA inayatoza makampuni yale kulipa kwa awamu kwa sababu mzigo unapungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nimpongeze Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana pamoja na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango kwa kazi kubwa ambayo wanafanya, kama wanavyosema wengine ni kwamba mwanzo tulikuwa hatuwaelewi, tulikuwa tunawachukia sana, lakini sasa hivi tunawapongeza, endeleeni kukaza uzi ili nchi hii iende. Ahsante. (Makofi)