Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Venance Methusalah Mwamoto (10 total)

MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:-
Kwa nini Serikali isifute michezo Tanzania?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Methuselah Mwamoto, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza nimtambue Mheshimiwa Venance Mwamoto kama mwanamichezo ambaye amewahi kucheza mpira wa miguu katika timu ya ligi daraja la kwanza wakati huo, sawa na ligi kuu Tanzania kwa sasa, yaani timu ya Majimaji ya Songea na RTC ya Kagera lakini pia timu ya Taifa.
Mheshimiwa Spika, hapa Bungeni Mheshimiwa Venance Mwamoto ndiye Kocha Mkuu wa timu ya mpira wa miguu ya Bunge. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kufuatia sifa hizo za Mheshimiwa Venance Methuselah Mwamoto, binafsi naamini kuwa swali lake limelenga kupata maelezo ya kwa nini michezo haiendelei kwa kasi wanayotamani wapenda michezo wengi hapa Tanzania na wala siamini kuwa anayo nia ya kutaka Serikali ifute michezo kwa kuwa anafahamu fika umuhimu wa michezo kwa Taifa paoja na wananchi kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Serikali ya Tanzania haiwezi na wala haina nia ya kufuta michezo nchini kwa sababu yoyote ile, badala yake nia ya Serikali ni kuiendeleza sekta hiyo muhimu kwa maendeleo ya Taifa hili kwa kuwekeza katika miundombinu ya michezo, elimu ya michezo ya kushirikiana na wadau wengine kuhakikisha kuwa sekta ya michezo inaendelezwa ipasavyo.
Mheshimiwa Spika, nimuombe Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote wa Bunge lako Tukufu kushirikiana na Serikali kuhimiza maendeleo ya michezo katika majimbo yetu. Aidha, tunashauri na kuhimiza wadau wote wa michezo ikiwemo Serikali za Mitaa, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Waheshimiwa Wabunge, sekta binafsi na wadau wengine kuibua vipaji vya michezo kwa watoto kuanzia umri mdogo na kuviendeleza.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara na Taasisi zake itaendelea kutenga fedha kupitia bajeti yake na vyanzo vingine kadri inavyowezekana kila wakati ili kuendeleza michezo katika ngazi mbalimbali.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:- Mkoa wa Iringa ulitenga eneo la EPZ katika Wilaya ya Kilolo. Je, ni lini eneo hilo litaanza kuendelezwa na ni nini faida ya EPZ?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI alijibu:- Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Venance Methusalah Mwamoto, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni maagizo ya Serikali kwa mikoa yote nchini kutenga maeneo kwa ajili ya uwekezaji kwa mfumo wa EPZ na SEZ. Baada ya Serikali katika ngazi ya Mikoa na Wilaya kutenga maeneo hayo inatoa taarifa kwa Mamlaka ya EPZ, ili maeneo hayo yaweze kutangazwa kama maeneo huru ya uwekezaji nchini chini ya Mamlaka ya EPZ. Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi Mamlaka ya EPZ haijakabidhiwa eneo lililotengwa kwa ajili ya uzalishaji katika Wilaya ya Kilolo kama ilivyobainishwa. Hii inazingatia kuwa tangu kufutwa kwa umiliki wa kwanza wa shamba hilo, kupitia Tangazo la Serikali Namba 130 la tarehe 17 Februari, 2012 taratibu za kulitangaza kama EPZ zilikuwa hazijakamilika. Hata hivyo, Halmashauri imeanza hatua ya awali ili iweze kukamilisha taratibu za kukabidhi eneo la Ruhundamatwe lililotengwa kwa ajili ya uendelezaji wa viwanda. Michoro (master plan) ya eneo husika imekamilika na kazi inayoendelea sasa ni kupima eneo husika. Kazi hiyo ikikamilika Halmashauri hiyo itakabidhi rasmi eneo husika kwa Mamlaka ya EPZ kwa ajili ya uwekezaji. Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekezaji chini ya Mamlaka ya EPZ una faida zifuatazo:- Mheshimiwa Spika, kwanza, kukuza mauzo nje ya nchi hivyo, kuongeza mapato ya fedha za kigeni; pili, kukuza sekta ya viwanda; tatu, kuongeza ajira na kufundisha stadi za uzalishaji viwandani; nne, kuendeleza uhawilishaji wa teknolojia ya viwanda; tano, kuhamasisha isindikaji wa mazao yetu na uchakataji wa malighafi ili kuongeza thamani; na ksita, uchangia katika kuongeza kipato kwa wananchi, hivyo kupunguza umaskini.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:-
Vyanzo vingi vya maji vinavyojaza Bwawa la Kihansi vinatoka Wilaya ya Kilolo.
Je, Wilaya hii inanufaika vipi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Methusalah Mwamoto, Mbunge wa Jimbo la Kilolo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli vyanzo vingi vya maji vinavyojaza Bwawa la Kihansi vinatoka katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo.
Mheshimiwa Naibu Spika, uwepo wa Bwawa la Kihansi unategemea sana vyanzo hivyo muhimu ambapo Taifa linanufaika kutokana na shughuli kubwa inayofanyika katika bwawa hilo ya kufua umeme. Uhifadhi wa Bwawa la Kihansi unatokana na vijiji 22; kutoka Wilaya za Mufindi vijiji nane, Wilaya ya Kilolo vijiji nane na Kilombero vijiji nane ambapo kwa sasa kuna mradi maalum unaosimamiwa na Baraza la Mazingira la Taifa kwa ajili ya uhifadhi mzima wa Bonde la Mto Kihansi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo inanufaika na bwawa hilo kwa kupata umeme ambao umesambazwa na Wakala wa Umeme Vijijini (REA) katika maeneo mengi ya vijijini ambapo katika Wilaya ya Kilolo vijiji vilivyonufaika ni pamoja na Masisiwe, Boma la Ng’ombe, Mwatasi, Ng’ingula na Wangama. Pia uwepo wa Bwawa la Kihansi umesababisha mashirika mbalimbali kuanzishwa kwa lengo la kusaidia jamii katika mambo mbalimbali kama vile upandaji wa miti kwa lengo la kuhifadhi mazingira, ufugaji wa nguruwe, mbuzi pamoja na ufugaji wa samaki.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile wananchi wa Halmashauri ya Kilolo wameendelea kupata huduma ya maji kupitia miradi mbalimbali iliyotekelezwa chini ya mpango wa miradi ya vijiji kumi, ambapo jumla ya miradi saba ya Irindi, Ihimbo, Mwatasi, Kipaduka, Vitono, Ikuka na Ilamba imekamilika na miradi mingine ipo katika hatua mbalimabli za utekelezaji.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:-
Timu yetu ya Taifa imeendelea kufanya vibaya katika michezo ya kimataifa. Je, Serikali imeliona hilo na imechukua hatua gani?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Methusalah Mwamoto, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikifanya juhudi katika kuendeleza michezo ili kuwa na timu bora za michezo katika ngazi mbalimbali hasa ngazo za timu za Taifa na baadhi ya juhudi hizo ni pamoja na:-
(i) Kuboresha mazingira ili wadau wa michezo wawekeze kisayansi katika michezo kuanzia umri mdogo kwa lengo la kugundua na kukuza vipaji na hatimaye kupata wachezaji mahiri wa timu za Taifa.
(ii) Kuendesha mafunzo mbalimbali ya michezo kwa wataalam wa michezo nchini katika Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya.
(iii) Kutoa mafunzo ya michezo mbalimbali ya muda mfupi kwa Wilaya na Mikoa kupitia Baraza la Michezo la Taifa.
(iv) Kutoa ushauri elekezi kwa vyama vya michezo wakati wa maandalizi ya timu za Taifa zinazoshiriki kwenye michezo ya Kimataifa mfano Olympiki, Michezo ya Afrika (All African Games) na michezo ya Jumuiya ya Madola.
(v) Serikali imetenga shule mbili kila Mkoa kama shule maalum za michezo na pia inaendelea kuhamasisha wadau kuanzisha shue za aina hiyo (sports academy).
(vi) Kuelekeza vilabu na vyama vya michezo kuwa na timu za umri wa chini na kuanzisha ligi zao kwa michezo hiyo.
(vii) Kushirikiana na Wizara nyingine kuendesha na kuratibu mashindano ya michezo kwa ajili ya wanafunzi wa shule za msingi (UMITASHUMTA) na ile ya shule za sekondari (UMISETA).
Mheshimiwa Spika, ili tufanikiwe katika hilo, Wizara inatoa rai kwa Waheshimiwa Wabunge kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya michezo katika maeneo yao ikiwa ni pamoja na zile za uibuaji wa vipaji na ujenzi wa miundombinu kwa kuhamasisha wadau mbalimbali. Aidha, Wizara inatoa wito kwa Halmashauri zote nchini kuendelea kuyalinda maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya shughuli za michezo na burudani pamoja na kuhakikisha mipango ya matumizi ya ardhi katika maeneo yao inazingatia utengwaji wa maeneo ya michezo na burudani.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:-
Je, ni kiasi gani cha fedha kinatolewa kwa Wilaya ambazo zinapakana au zilizo na Hifadhi za Taifa ikiwamo Wilaya ya Kilolo katika Hifadhi ya Udzungwa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Mwamoto, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maliasili na Utalii, kupitia Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA), inatekeleza Mpango wa Ujiarni Mwema (Support for Community Initiated Projects) ulioanzishwa mapema miaka ya 1990. Lengo la mpango huu ni kuishirikisha jamii katika kupunguza changamoto za uhifadhi na kuwanufaisha wananchi waishio jirani na hifadhi. Utekelezaji wa Mpango wa Ujirani Mwema unahusisha vijiji katika Wilaya zinazopakana na Hifadhi za Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa, vijiji vinaibua miradi ya maendeleo na kuchangia asilimia 30 ya gharama za miradi na shirika kuchangia asilimia 70 ya gharama hizo. Kupitia mpango huu kila mwaka TANAPA inatenga kati ya 5% hadi 7% ya bajeti yake kwa shughuli za miradi hiyo. Vilevile mpango huu unahusisha utoaji wa elimu ya uhifadhi na kuwashirikisha wananchi katika uhifadhi wa maliasili na mazingira kama vile upandaji wa miti na kadhalika.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha kuanzia mwaka 2000/2001 hadi mwaka 2017/2018 Hifadhi ya Taifa ya Udzungwa imefanikiwa kutekeleza miradi ya ujirani mwema katika Wilaya ya Kilolo yenye thamani ya jumla ya shilingi 435,962,656. Baadhi ya miradi iliyotekelezwa na inayoendelea kutekelezwa Wilaya ya Kilolo inahusu uwekaji wa umeme, ujenzi wa barabara, ununuzi wa samani na ununuzi wa vifaa vya maabara vya Sekondari ya Lukosi katika Kijiji cha Mtandika ambapo jumla ya shilingi 49,460,937 zimetumika.
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa nyumba wa awamu za walimu katika Kijiji cha Ikura umegharimu shilingi 60,000,000; ukarabati barabara ya Ilula – Udekwa, ujenzi na ununuzi wa samani Kituo cha Polisi, nyumba ya walimu, shule ya msingi katika Kijiji cha Udekwa umegharimu shilingi 227,501,719 na mpango wa matumizi bora ya ardhi na nyumba ya walimu shule ya msingi Msosa katika Kijiji cha Msosa shilingi 81,000,000 na ununuzi wa madawati kwa ajili ya Wilaya ya Kilolo umegharimu shilingi 18,000,000. Jumla ya fedha zote zilizotolewa na Shirika ni shilingi 435,962,656.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza
(a) Je, kuna wachezaji wangapi wa nje wanaoruhusiwa kucheza kwenye Ligi Kuu Tanzania?
(b) Je, tulianza na wachezaji wangapi miaka ya nyuma na sasa wako wangapi?
(c) Je, ni zipi sababu za kuongeza au kupunguza wachezaji na ni nini manufaa yake?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Methusalah Mwamoto, Mbunge wa Kilolo, lenye vipengele (a), (b) na (c), kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa taratibu za usajili za TTF wachezaji wa nje wanaoruhusiwa kucheza kwenye Ligi Kuu Tanzania ni saba kwa kila klabu. Tulianza na wachezaji watano kati ya mwaka 2010 hadi 2015 na baadaye kuanzia msimu wa 2015/2016 idadi imeongezeka na kufikia wachezaji saba.
Mheshimiwa Naibu Spika, sababu ya kuongeza wachezaji wa nje kwenye Ligi Kuu hii ya Tanzania ni maombi ya wadau wenyewe wa mpira wa miguu, vikiwemo vilabu vya mpira wa miguu na mazingira mazuri ya mpira wa kulipwa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, uwepo wa wachezaji wa nje kwenye ligi kuu ya Tanzania umeongeza ushindani miongoni mwa wachezaji wetu kiweledi na kinidhamu na kuwa chachu ya vilabu kupanua wigo wao wa mapato kwa ajili ya usajili. Aidha, kuchanganya wachezaji wazawa na wageni ni fursa kwa wachezaji wetu kujifunza kutoka kwa wenzao na kunatangaza ligi yetu nje ya nchi ambako wachezaji wa kigeni wanatoka na maendeleo yao yanafuatiliwa kwa karibu na timu zao za Taifa.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:-
Je, ni nini faida ya hati miliki za kimila?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Mwamoto kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa fungu la 18, 28 hadi 47 la Sheria ya Ardhi ya Vijiji namba tano ya mwaka 1999 hati ya hakimiliki za hati ya kumiliki ardhi kwa kuzingatia mila na desturi kwa raia wa Tanzania na ina hadhi sawa na hakimiliki nyingine inayotolewa kisheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna faida nyingi za hati za hakimiliki ya kimila, miongoni mwa faida hizo ni pamoja na kuwa na usalama wa miliki, kupunguza migogoro baina ya watumiaji ardhi, kutumika kama dhamana katika taasisi za fedha na vyombo vya kisheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia Machi, 2018 jumla ya hatimiliki za kimila 56,506 zimeandaliwa katika maeneo mbalimbali nchini. Wananchi katika maeneo hayo wamenufaika kiuchumi kutokana na mikopo waliyoipata katika taasisi za kifedha kwa kutumia hati za hatimiliki za kimila kama dhamana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia Juni, 2017 kiasi cha shilingi bilioni 59.2 zimekopeshwa kwa wananchi kwa kutumia hati za hakimiliki za kimila kama dhamana kutoka mabenki na taasisi za kifedha. Miongoni mwa taasisi hizo ni pamoja NMB PLC, CRDB PLC, Stanbic Bank, SIDO, PSPF, Agriculture Trust Fund, Meru Community na Mfuko wa Pembejeo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai kwa wananchi wote kutoa ushirikiano katika miradi ya utoaji hati za hakimiliki za kimila inayoendelezwa katika maeneo yao ili ziweze kuwanufaisha kwa ustawi wa kiuchumi na kijamii.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:-
Je, Serikali inajua tatizo la ukosefu wa maji Kilolo linasababishwa na nini na nini suluhisho lake?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Mwamoto, Mbunge wa Jimbo la Kilolo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara ya Maji na Umwagiliaji, imeandaa mipango madhubuti katika kuhakikisha inaboresha huduma ya maji kwa wananchi wa Mji wa Kilolo. Katika lengo hilo Wizara inatekeleza mpango wa muda mfupi na muda mrefu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa muda mfupi, Serikali kwa kushirikiana na Shirika la USAID kupitia programu ya WARIDI, inatekeleza kazi za uboreshaji wa huduma ya maji kwa Mji wa Kilolo. Kazi zinazotekelezwa katika mradi huo ni ukarabati wa kitekeo cha maji (chanzo cha maji), ujenzi wa bomba kuu lenye urefu wa kilometa 12.8, ujenzi wa mtandao wa usambazaji maji wenye urefu kwa kilometa sita, ujenzi wa vituo sita vya kuchotea maji, ujenzi wa tanki lenye ujazo wa mita za ujazo 100 na ukarabati wa matanki matatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia mwezi Machi 2018, utekelezaji wa mradi huo umekamilika kwa wastani wa asilimia 90. Kukamilika kwa mradi huo kutawanufaisha wakazi 6,200 wa Mji wa Kilolo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mpango wa muda mrefu, Serikali imakamilisha usanifu wa mradi wa maji katika Mji wa Kilolo. Kazi zitakazotekelezwa ni ujenzi wa chanzo cha maji katika Mto Mtitu, ujenzi wa mtambo wa kuchuja maji, ujenzi wa bomba kuu, ujenzi wa mtandao wa usambazaji maji na ujenzi wa mfumo wa umeme wa kuendesha mitambo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi huo utakapokamilika utaongeza uzalishaji wa maji kutoka lita 380,000 kwa siku hadi lita milioni 4.4 kwa siku ifikapo mwaka 2025, ambapo mahitaji ya maji kwa sasa ni lita milioni 2.7 kwa siku. Gharama za utekelezaji wa mradi huo ni dola za Marekani milioni 4.3. Serikali inaendelea na jitihada za kutafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:-

Je, Serikali imetenga fedha kiasi gani ya ujenzi wa mabwawa ya maji ili kupunguza matatizo ya maji katika Wilaya ya Kilolo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Mwamoto, Mbunge wa Jimbo la Kilolo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, hali ya upatikanaji wa huduma ya maji katika Halmashauri ya Kilolo kw aupande wa Vijijini ni asilimia 71. Kilolo Mjini ni asilimia 80 na Ilula ni asilimia 47.5. Aidha, halmashauri ya Wilaya ya Kilolo imekamilisha ujen zi wa miradi ya vijiji 10 kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji pamoja na Ujenzi wa vijiji vitano kupitia ufadhili wa Taasisi isiyo ya Kiserikali ya WARIDI.

Mheshimiwa Spika, kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019, Halm ashauri ya Wilaya ya kilolo inatekeleza miradi ya maji katika vijiji vitatu vya Lundamatwe, Kitelewasi na Ilambo. Pia miradi miwili katika miji midogo ya Kilolo na Ilula. Aidha, Halmashauri ya Kilolo kwa kutumia fedha za ndani inakarabati mabwawa matatu yaliyopo katika vijiji vya Uhambingeto, Image na Mgowelo kwa ajili ya binadamu na mifugo.

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na channgamoto ya uhaba wa maji kwa mwaka huu wa fedha 2018/2019 Halmashauri ya Kilolo imepokea jumla ya shilingi bilioni 1.7 ili kuhakikisha miradi ya maji inatekelezwa na kukamilika na kuwapunguzia keri ya maji wananchi wa wilaya hiyo.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:-

(a) Je, ni nini sifa au vigezo vya kupata Halmashauri?

(b) Inachukua miaka mingapi kuendelea kuitwa Halmashauri ya Mji Mdogo hadi kuwa Halmashauri kamili?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la kaka yangu Mheshimiwa Venance Mwamoto, Mbunge wa Kilolo, Mkoani Iringa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya), Sura 287 na (Mamlaka za Miji) na Sheria ya Serikali za Mitaa Sura 288 zimeweka utaratibu wakuzingatiwa katika kupandisha hadhi maeneo ya utawala. Vigezo vya kuanzisha Mamlaka za Miji Midogo vimeainishwa kwenye Mwongozo wa Uanzishaji wa Mamlaka za Serikali za Mitaa wa mwaka 2014, Kipengele Na.4.2.5 (a-q) na miongoni mwa vigezo muhimu ni pamoja eneo linalopendekezwa kuwa na idadi ya watu isiopungua 50,000, kata zisizopungua 3, vitongoji visivyopungua 30 na ukubwa usiopungua kilometa za mraba 150.

Mheshimiwa Spika, vigezo vya kuanzisha Halmashauri ya Wilaya au kuipandisha hadhi Mamlaka ya Mji Mdogo kuwa Halmashauri ya Wilaya vimeanishwa kwenye Kipengele Na. 4.2.4 (a-q) kama nilivyosema awali na miongoni mwa vigezo muhimu ni pamoja na uwezo wa kujitegemea kibajeti kwa walau 20% kutokana na mapato ya ndani, eneo lenye ukubwa usiopungua kilometa za mraba 5,000, kata zisizopungua 20, vijiji visivyopungua 75 na idadi ya watu wasiopungua 250,000. Hivyo, upandishaji wa hadhi wa Mamlaka za Mji Mdogo kuwa Halmashauri unategemea vigezo vilivyoainishwa na sio muda wa Halmashauri.