Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Mendard Lutengano Kigola (17 total)

MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Serikali iliahidi kupeleka gari la wagonjwa katika Kituo cha Afya Mgololo lakini hadi sasa gari hilo halijapelekwa:-
Je, ni lini gari hilo litapelekwa ili liweze kusaidia Vijiji vya Idete, Itika, Holo, Isaula, Rugema, Makungu, Rugolofu na Kitasengwa?
NAIBU WAZIRI WA TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, UTUMISHI NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi ina gari moja linalotumika kuhudumia wagonjwa. Hata hivyo, gari hilo ni chakavu kiasi cha kuhitaji matengenezo ya mara kwa mara.
Mheshimiwa Naibu Spika, kila Halmashauri inapaswa kuweka kipaumbele na kutenga bajeti kwa ajili ya ununuzi wa magari ya kubebea wagonjwa kwa kuzingatia mahitaji yaliyopo. Katika bajeti ya mwaka 2016/2017, Halmashauri imeomba shilingi milioni 543.0 kwa ajili ya kununua magari matatu (ambulance) ambapo kati ya hayo gari moja litapelekwa katika Kituo cha Afya Mgololo na mengine katika Vituo vya Afya vya Sadani na Kasanga ili yasaidie kuwafikisha wagonjwa wenye dharura kwenye vituo vya kutolea huduma kwa haraka.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Jimbo la Mufindi Kusini linazungukwa na msitu wa Serikali na vijana wanaishi humo hawana ajira.
(a) Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwapa vibali vya kupasua mbao ili kwa kazi hiyo wajiajiri?
(b) Je, Serikali haioni haja ya kuwapa vijana hao mtaji ili waanzishe viwanda vidogo vya mbao?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Mufindi Kusini linapakana na msitu wa shamba la miti la Sao Hill ambalo ni miongoni mwa mashamba ya misitu ya kupandwa 18 nchini. Upasuaji wa mbao ni sehemu moja tu ya mchakato mzima wa uvunaji wa mazao ya misitu unaotekelezwa na Wizara yangu kwa mujibu wa mwongozo wa uvunaji endelevu na biashara ya mazao ya misitu yanayovunwa katika mashamba ya miti na misitu ya mikoko kwa mwaka 2014, chini ya Sheria ya Misitu namba 14 ya mwaka 2002 na Sera ya Taifa ya Misitu ya mwaka 1998. Mwongozo huo umeweka vipaumbele mbali mbali katika uvunaji wa mazao ya misitu ikiwemo vikundi vya vijana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua changamoto za kiuchumi na kijamii kwa vijana katika maeneo husika Serikali imekuwa ikishirikiana na umoja wa vikundi vya kijamii Wilayani Mufindi kwa kuwapatia vibali kwa ajili ya kuwezesha kupata mitaji ili kuwekeza katika miradi mingine ya kiuchumi. Kwa miaka mitatu mfululizo 2013/2014 hadi 2015/2016 vijana kupitia umoja huo wamekuwa wakigawiwa mita za ujazo 200 kila mwaka. Fedha inayotokana na vibali hivi huratibiwa na umoja wao, na imewawezesha kuanzisha shughuli mbalimbali ikiwemo kununua mizinga ya ufugaji nyuki, ufugaji wa ng’ombe wa maziwa, ufugaji wa kukuna hata mitaji kwa ajili ya biashara ndogo ndogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha uwezeshaji wa vijana wanaoishi jirani na msitu kwa namna endelevu, shamba la miti Sao Hill hutoa miche ya miti kwa ajili ya kupanda kwenye mashamba wanayomiliki wenyewe ili waweze kuvuna na kuuza mbao na kujipatia mfanikio ya kiuchumi na kijamii ikiwemo upatikanaji wa ajira. Kwa mfano katika mwaka 2015/2016 shamba lilitoa bure miche 600,000 yenye thamani isiyopungua shilingi 120,000,000 kwa ajili ya kuwawezeshavijana hao.
Aidha, ili kuhakikisha kuwa jamii inanufaika na uwepo wa shamba hilo na kuwapunguzia adha ya michango kwa shughuli za maendeleo vijiji vinavyozunguka shamba hilo vinapatiwa vibali vya kuvuna miti kwa ajili ya shughuli za kimaendeleo ikiwemo kutengeneza madawati, kazi ambayo pia hupewa mafundi ambao ni vijana wanaishi katika vijiji vinayozunguka shamba hilo. Kwa mfano, katika kipindi cha mwaka 2011/2012 hadi 2014/2015 jumla ya meta za ujazo 40,000 zilitolewa kwa vijiji vya jirani na kwa mwaka 2013/2014 pekee baadhi ya vijiji vilitumia mgao huo kutengeneza jumla ya madawati 2,469.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu inatoa ushauri kwa vijana kuungana pamoja na kuunda ushirika ambao utawezesha kupata mikopo kutoka taasisi mbalimbali za fedha na hatimaye kujenga uwezo wa kuendesha shughuli zao za kila siku ikiwa ni pamoja na kuwekeza katika viwanda vya mbao yaani saw mills ili waweze kuomba vibali vya uvunaji kajadiliwa kama wateja wengine wenye viwanda.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Upembuzi yakinifu wa barabara ya kutoka Nyololo hadi Mtwango yenye urefu wa kilomita 40 umefanyika mwaka 2013/2014:-
Je, ni lini barabara hiyo itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina pamoja na uandaaji wa nyaraka za zabuni kwa barabara ya Nyololo - Igowole hadi Kibao ilikamilika mwaka 2014 yakiwa ni maandalizi ya ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami. Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali kupitia Wakala wa Barabara TANROADS, itaendelea kuifanyia matengenezo ya aina mbalimbali barabara hii kwa kiwango cha changarawe ili iendelee kupitika majira yote ya mwaka wakati taratibu za kutafuta fedha za kuijenga kwa kiwango cha lami zinaendelea na ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ambayo imeelekeza hii barabara katika ukurasa wake wa 61.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA (K.n.y. MHE. MENDRAD L. KIGOLA) aliuliza:-
Mradi wa maji katika Kata ya Mtwango umechukua muda mrefu bila kukamilika na wananchi wanaendelea kupata shida ya maji:-
Je, ni lini mradi huo utakamilika na kukabidhiwa kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa mradi wa maji katika Kata ya Mtwango ulianza rasmi mwezi Juni, 2015. Mradi huo katika bajeti ya mwaka 2015/2016 ulitengewa shilingi milioni 488.8 ambapo utekelezaji wa mradi huo umefikia 60%.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kukamilisha mradi huo katika Bajeti ya mwaka 2016/2017 Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi imetengewa shilingi milioni 643.5 kwa ajili ya kazi zilizobaki, ili mradi huo uanze kutoa huduma ya maji kwa wananchi.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika Kata za Mtambula, Idunda, Maduma, Kiyowela na Idete ili wananchi waweze kufaidika na huduma hiyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ridhaa ya kiti chako, niombe dakika moja niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kabla sijajielekeza kwenye kujibu maswali yaliyoulizwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu nawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge jinsi ambavyo walijitoa kwenye msiba mzito wa mama yangu uliotokea wiki tatu zilizopita, nawashukuru sana na ningependa kwa ruhusa yako kwa uwakilishi wa Waheshimiwa Wabunge niwatambue wachache walioweza kufanikiwa kufika Chato kwa ajili ya msiba, lakini nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa ridhaa hiyo. Baada ya kusema hayo Mungu awabariki sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na madini, napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kutekeleza miradi ya kufikisha umeme nchi nzima ikiwa ni pamoja na maeneo ya vijiji vya Mufindi Kusini. Vijiji vya Kata ya Idete, Idunda, Kiyowela, Maduma pamoja na Mtambula vitapatiwa umeme kupitia mradi kabambe wa REA Awamu ya Tatu unaoanza Disemba mwaka huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kupeleka umeme kwenye vijiji hivyo nilivyovitaja vya Wilaya ya Mufindi itahusisha itahusisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovolt 33 yenye urefu wa kilometa 242, ujenzi wa njia ya msongo wa kilovolt 0.4 yanye urefu wa kilometa 81, ufungaji wa transfomer 24 pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 3,533. Kazi inatarajiwa kuanza mwezi huu wa Disemba, 2016 na kukamilika katika kipindi cha mwaka wa fedha 2019/2020. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 11.92.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itamaliza kujenga mradi wa maji wa Sawala, Mtwango, Rufuna na Kibao?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa maji wa Sawala - Kibao ambao utahudumia vijiji vya Sawala, Mtwango, Rufuna na Kibao vilivyopo katika Kata ya Mtwango ulianza kutekelezwa tarehe 01/06/2015 na ulitarajiwa kukamilika tarehe 01/06/2016 kwa gharama ya shilingi bilioni 2.55.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa mradi huo ulipangwa kufanyika kwa awamu tatu ambazo ni kujenga intake na kupeleka maji kijiji cha Sawala, kujenga mfumo wa bomba kuu kutoka kijiji cha Sawala hadi Kibao na kujenga mtandao wa kusambaza maji katika vijiji vya Mtwango, Rufuna na Kibao. Awamu ya kwanza utekelezaji umefanyika katika kijiji cha Sawala kwa mkataba wa gharama ya shilingi milioni 644.21.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi sasa, jumla ya shilingi milioni 261.64 zimetumika kwenye mradi. Kazi zilizotekelezwa hadi sasa ni pamoja na ujenzi wa intake, sump well, pump house, ulazaji wa bomba kuu, ujenzi wa tenki la mita za ujazo 200, ujenzi wa vituo vya kuchotea maji 16 na sehemu ya mabomba ya usambazaji kilometa 3.4; kwa wastani kazi iliyofanyika imefikia asilimia 50 kwa kijiji cha Sawala tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huo haukuweza kukamilika kwa wakati kutokana na mkandarasi kushindwa kukamilisha kazi kwa mujibu wa mkataba. Mwezi Novemba, 2016 Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi ilivunja mkataba na mkandarasi huyo, na kuamua kuutangaza upya tarehe 07/02/2017 ili kuweza kupata mkandarasii mwingine wa kumalizia kazi zilizobaki. Mkandarasi anatarajiwa kupatikana mwezi Juni, 2017 na kazi itakamilika katika mwaka wa fedha 2017/2018.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara ya kilometa 40 ya kutoka Nyololo - Igowole - Mtwango kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Nyololo- Igowole hadi Mtwango au hadi Kibao yenye urefu wa kilometa 40.4 ni barabara ya Mkoa inayohudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS). Maandalizi kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami yanaendelea ambapo upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na uandaaji wa nyaraka za zabuni kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara hii yamekamilika. Kwa sasa Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuifanyia matengenezo ya aina mbalimbali barabara hii ili iweze kupitika katika majira yote ya mwaka wakati ikiendelea kutafuta fedha kwa ajilii ya ujenzi wa kiwango cha lami. Aidha, katika mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali imetenga jumla ya shilingi milioni 450.077 na katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali imetenga jumla ya shilingi milioni 160.511 kwa ajili ya kuifanyia matengenezo ya aina mbalimbali barabara hii.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itamaliza kujenga Mradi wa Maji kwa Kata ya Mtwango katika Vijiji vya Sawala, Mtwango, Rufuna na Kibao?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Vijiji vya Sawala, Mtwango, Rufana na Kibao katika Kata ya Mtwango ni miongoni mwa vijiji 12 vilivyopendekezwa na Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi kupatiwa huduma ya maji kupitia Programu Ndogo ya Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini. Utelekezaji wa mradi ulipangwa kufanyika kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Ujenzi wa mradi huo ulianza tarehe 01 Juni, 2015 na ulitakiwa kukamilika tarehe 01 Juni, 2016 kwa gharama ya shilingi bilioni 2.36. Awamu ya kwanza ilikuwa ni ujenzi wa miundombinu ya maji katika Kijii cha Sawala pekee ambapo hadi sasa ujenzi umefikia asilimia 50.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi mwezi Novemba 2016 mkandarasi alikuwa hajakamilisha kazi na hivyo Halmashauri kuamua kuvunja mkataba. Halmashauri ilitangaza upya zabuni kwa ajili ya ukamilishaji wa kazi zilizobaki. Mkandarasi mwingine amepatikana na utekelezaji wa mradi huo unatarajiwa kuanza mwezi Desemba, 2017 kwa muda wa miezi 12 kwa gharama ya shilingi bilioni 1.81. Serikali katika mwaka wa 2017/2018 imetenga kiasi cha shilingi bilioni 2.56 kwa ajili ya Halmashauri ya Mufindi ili kukamilisha mradi huo katika Vijiji vyote vya Sawala, Mtwango, Rufuna na Kibao na kuendelea na utekelezaji wa miradi mingine ya vijijini.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Ujenzi wa Vituo vya Afya Kata za Mninga na Mtwango bado haujakamilika, hivyo wananchi wa Kata hizo wanaendelea kupata shida ya matibabu:-
Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa vituo hivyo ili wananchi waweze kupata huduma za matibabu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa Kituo cha Afya Kata ya Mtwango ulianza mwaka 2012, ambapo umeshagharimu Sh.22,500,000/=. Aidha, Kituo cha Afya Mninga kilianza kujengwa mwaka 2008 ambapo umegharimu Sh.41,000,000/=. Vituo hivyo vipo katika hatua ya umaliziaji wa majengo ya OPD na nyumba za watumishi ili huduma zianze kutolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka wa fedha wa 2016/2017, Serikali ilitenga Sh.32,500,000 kwa ajili ya kuendelea kuchangia ukamilishaji wa Vituo vya Afya Kata ya Mninga na Mtwango. Fedha zilizopokelewa mpaka sasa ni Sh.8,000,000/=. Aidha, katika mwaka wa fedha 2017/2018, zimetengwa Sh.65,000,000/= kwa ajili ya kuimarisha Vituo vya Kasanga na Kituo cha Afya Mbalamaziwa katika Jimbo la Mufindi Kusini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mpango wa Serikali kuunga mkono juhudi za wananchi katika miradi ya maendeleo kwa kutenga fedha kupitia LGDG kila mwaka ili kumalizia miradi mbalimbali.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika Kata za Mtambula, Idunda, Itandula, Kiyowela, Idete, Maduma na Nyololo Shuleni?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI (K.n.y. WAZIRI WA NISHATI NA MADINI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa mradi kabambe wa usambazaji umeme vijijini awamu ya tatu umeanza kwa nchi nzima tangu mwezi Machi, 2017. Mradi huu utajumuisha vipengele-mradi vitatu vya Densification, Grid Extension na Off-Grid Renewable ambayo inalenga kuongeza wigo wa usambazaji umeme katika vijiji na vitongoji ambavyo havikufikiwa na miundombinu ya umeme. Kata za Idete, Idunda, Itandula, Kiyowela, Mtambula, Maduma pamoja na Kata nyingine za Wilaya ya Mufindi zimejumuishwa katika utekelezaji wa mradi wa REA awamu ya tatu wa Grid Extension utakaokamilika mwaka wa fedha 2020/2021.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme katika vijiji vya kata hizo itahusisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 153.65; ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 0.4, yenye urefu wa kilometa 233; ufungaji wa transfoma 92, pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 3,225. Gharama ya kazi hii ni shilingi bilioni 14.1. (Makofi)
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itamalizia ujenzi wa Vituo vya Afya Kata za Mtwango, Mninga na Makungu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na ujenzi wa vituo vya afya awamu kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 kipaumbele kimewekwa katika ujenzi wa Kituo cha Afya Malangali kilichoko katika Jimbo la Mufindi Kusini ambao unahusisha ujenzi wa jengo la upasuaji, nyumba ya watumishi, maabara na jengo la wazazi kwa gharama ya shilingi milioni 400 ili kukiwezesha kutoa huduma za dharura za upasuaji.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi imetenga jumla ya shilingi milioni 40 kwa ajili ya umaliziaji wa Kituo cha Afya cha Mninga. Fedha hizo zinatarajiwa kufanya umaliziaji wa jengo la wagonjwa wa nje (OPD) ambapo itatumika kiasi cha shilingi milioni 30 na shilingi milioni 10 za kuanzia ujenzi wa nyumba ya mganga.
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa Vituo vya Afya Mtwango na Mninga umefikia hatua mbalimbali ambapo majengo ya maabara na nyumba ya mtumishi imefika hatua ya umaliziaji na vifaa vyote vya umaliziaji vimekwishafika site. Majengo ya upasuaji na akina mama yamefikia hatua ya kunyanyua kuta na vifaa vyote vya ukamilishaji vipo site, tunategemea kukamilisha kabla ya tarehe 31 Mei, kwa mujibu wa mkataba.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Kata ya Makungu hakuna ujenzi unaoendelea isipokuwa kuna kituo cha afya kinachomilikiwa na Kiwanda cha Karatasi cha Mgololo. Katika kituo hicho Serikali imepeleka Watumishi ambao wanalipwa mishahara na stahili zote kutoka Serikalini na kuchangia dawa pamoja na vifaa.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itamaliza ujenzi wa miundombinu ya maji katika Kata za Igowele, Nyololo, Mninga, Mtambula, Nyigo na Idunda?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za Igowele, Nyololo, Mninga, Mtambula na Idunda zina jumla ya vijiji 23 vyenye wakazi takribani 69,119. Katika Mwaka wa Fedha 2017/2018, Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi imetenga shilingi bilioni 2.67 kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji vijijini zikiwemo kata hizo. Hadi kufikia sasa usanifu wa kina umekamilika na kwa sasa uandaaji wa makabrasha ya zabuni unaendelea na unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Mei, 2018. Kazi hizo zinatekelezwa na Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Iringa (IRUWASA) kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi na Sekretarieti ya Mkoa wa Iringa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa miundombinu ya miradi hiyo ya maji unatarajiwa kuanza katika Mwaka wa Fedha 2018/2019, ambapo Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 2.29 kwa ajili ya miradi ya maji vijijini katika Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi zikiwemo Kata za Igowele, Nyololo, Mninga, Mtambula, Nyigo na Idunda. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Serikali imekuwa na mpango kabambe wa kupeleka umeme vijijini:-
Je, ni lini Serikali itawapelekea umeme wananchi wa Kata Itandula, Nyololo Shuleni, Maduma, Udumka, Kilolo, Kiyowole na Idete?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatekeleza Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza kuanzia Julai, 2017 hadi Juni 2019. Katika Wilaya ya Mufindi jumla ya vijiji 53 vitapatiwa umeme kupitia mradi huu unaotekelezwa na mkandarasi Kampuni ya Sengerema Engineering Group Limited aliyepewa kazi za mradi huo kwa Mkoa wa Iringa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Mufindi Kusini, mradi utapeleka umeme katika Kata za Makungu, Igowole, Mninga, Nyololo, Isalavanu, Mbalamaziwa na Kasanga ambapo Vijiji vya Lugolofu, Mukungu, Lugema, Ibatu, Kisasa, Makalala, Ikwega, Itulituli, Lwing’ulo, Njojo, Nyololo Shuleni, Mjimwema, Idetero, Kimandwete, Ukemele, Udumuka, Lyang’a, Kilolo, Ihomasa pamoja na Maduma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi za mradi katika Wilaya ya Mufindi zinahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 139.63, njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 170, ufungaji wa transfoma 85 za kVA 50 na 100, pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 2,596. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 11.92. Kwa sasa mkandarasi ameshasimika nguzo za umeme wa line kubwa za HT kwa asilimia 90 na nguzo za umeme wa line ndogo LV kwa asilimia 95 kwa jimbo la Mufindi Kusini. Kazi ya ufungaji transfoma na kuunganisha wateja itaanza mwishoni mwa Septemba, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji vingine vya Kata ya Itandula, Kiyowole na Idete vitapatiwa umeme katika mzunguko wa pili wa mradi wa REA III unaotarajia kuanza Julai, 2019 na kukamilika Juni, 2021. Ahsante.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itapeleka gari ya kuwahudumia wagonjwa katika kituo cha Afya cha Magunguli –Mgololo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Menrald Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, gari la wagonjwa kwa ajili ya Kituo cha Afya Magungulu - Mgololo kilichopo kata ya Magungulu imekwishapatikana. Gari hili lilitolewa na Mheshimiwa Rais wakati anatoa msaada wa magari ya wagonjwa kwa halmashauri mbalimbali hapa nchini mnamo mwezi Machi, 2018 na taratibu za usajili zinaendelea.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kwa kutambua uhitaji wa gari katika kituo hiki, gari hili limepelekwa kituoni moja kwa moja na kuanza kutumika huku taratibu za usajili wake zikiwa zinaendelea. Ni matumaini yetu kuwa gari hili, litasaidia kuleta wepesi kwa wananchi kufikia huduma za afya pale mahitaji yatakapo yanajitokeza.
MHE. OMARI M. KIGUA (K.n.y. MHE. MENDRAD L. KIGOLA) aliuliza:-

Sekondari za Jimbo la Mufindi Kusini zinakabiliwa na tatizo la hosteli kwa ajili ya wanafunzi wanaotoka mbali:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kujenga hosteli kwa kila sekondari katika Jimbo la Mufindi Kusini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa
Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi ina shule za sekondari 43 ambapo kati ya hizo shule 21 zina daharia (hostel). Katika mwaka wa fedha 2018/2019, shule nyingine mbili za sekondari za Ihowanza na Mninga zinaendelea na ukamilishaji wa ujenzi wa hosteli ili kufanya idadi ya shule zenye hosteli kufikia 23.

Aidha, kwa mwaka wa fedha 2019/2020, Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi imetenga kiasi cha shilingi milioni 60 kupitia mapato ya ndani ili kusaidia ukamilishaji wa daharia zilizopo katika hatua ya ukamilishaji. Vilevile Lyara in Africa wamepanga kusaidia ujenzi wa hosteli katika Shule za Sekondari za Kiyowela na Idunda na CAMFED wamesaidia ujenzi wa hosteil ya Ihowanza.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-

Mradi wa maji katika Kata ya Mtwango bado haujakamilika:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha mradi huo ambao umechukua muda mrefu bila kukamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako kwanza naomba nitoe pole kwa wananchi wa Jimbo langu la Pangani pamoja na wananchi wa Mkoa wa Tanga kwa mafuriko ambayo yalikuwa yametokea, tumepoteza ndugu zetu lakini pia kuharibika kwa miundombinu. Tunamshukuru Mkuu wa Mkoa kwa hatua ya haraka ya kuweza kurejesha miundombinu ile.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli Mradi wa Maji wa Kata ya Mtwango umechukua muda mrefu kutokana na changamoto iliyokuwepo ya wakandarasi kutokamilisha kazi kwa wakati hali ambayo ililazimu kuwaondoa.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2019/ 2020, Serikali imetenga shilingi milioni 300 kwa lengo la kukamilisha mradi huo. Kazi zitakazofanyika ni ujenzi wa matenki, ununuzi wa pampu na ununuzi wa mabomba ya kusambaza maji kwa wananchi. Kazi hizo zitafanywa na wataalam na Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini yaani RUWASA katika ngazi ya wilaya na mkoa. Taratibu za kukamilisha kazi zilizobaki katika Kijiji cha Sawala zinaendelea. Mradi huo unategemewa kukamilika katika mwaka wa fedha 2019/2020.
MHE. RITTA E. KABATI (K.n.y. MHE. MENDRAD L. KIGOLA) aliuliza:-

Miundombinu ya shule nyingi za msingi katika Jimbo la Mufindi Kusini ni chakavu:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kukarabati miundombinu ya shule hizo?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, moja ya changamoto kubwa zinazoikabili Sekta ya Elimu hapa Nchini ni uhaba na uchakavu wa miundombinu ya shule ikiwemo nyumba za walimu, vyumba vya madarasa pamoja na vyoo. Serikali kupitia Programu ya Lipa Kulingana na Matokeo katika Sekta ya Elimu (Education for Results – EP4R) inaweka kipaumbelea na kutenga bajeti kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu hiyo ya elimu.

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2018/ 2019, Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi imepokea jumla ya shilingi milioni 223.2 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu katika Shule za Msingi Kilolo na Makalala. Shule ya Msingi Kilolo ilipokea jumla ya shilingi milioni 136.6 kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu, ujenzi wa madarasa manne na ujenzi wa matundu sita ya vyoo na Shule ya Msingi Makalala imepokea jumla ya shilingi miloni 86.6 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vinne vya madarasa na matundu sita ya vyoo. Serikali itaendelea kutoa fedha kwa kadri ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya elimu ya msingi kulingana na upatikanaji wa fedha.