Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Mendard Lutengano Kigola (26 total)

MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri, lakini pamoja na majibu yake Naibu Waziri kwamba hili gari kwenye bajeti ya mwaka 2013/2014 na swali la msingi niliuliza mwezi wa Tisa na kwenye bajeti walisema kwamba wametenga milioni 150 kwa ajili ya ununuzi wa hili gari la wagonjwa wa kule Mgololo, mpaka leo hili gari halijapelekwa. Niliwahi kumuuliza Waziri wa Afya akaniambia kwamba kuna magari matano yamenunuliwa mojawapo litapelekwa kule, lakini mpaka leo halijakwenda. Je, bajeti ya mwaka uliopita ambayo ilitengwa kwa ajili ya hilo gari, hiyo fedha ya shilingi milioni 150 ilikwenda wapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, hii gari ni ya msingi sana, kwa sababu itahudumia Kata tatu, kuna ya Kiyowela, Kata ya Idete na Kata ya Makungu. Kule kuna watu wanakaribia karibu 120,000 hivi, akinamama wanapata taabu sana kuna milima, jiografia ya kule ni ngumu sana. Sasa naomba Mheshimiwa Naibu Waziri anithibitishie kwa sababu hii pesa ya Halmashauri haina uhakika, ni lini hii gari hili la wagonjwa litapelekwa Mufindi?
NAIBU WAZIRI WA TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikiri wazi kwamba nilifika Mufindi katika Jimbo la Mheshimiwa Mbunge mpaka Mgogolo. Hili ni miongoni mwa Jimbo ambalo lina changamoto kubwa kutokana na jiografia yake ilivyo. Hata hivyo, nipende kumshukuru pia kwa juhudi kubwa anayofanya katika kuhakikisha mambo yanakwenda katika Jimbo lake kwa sababu katika miaka mitano iliyopita alikuwa akipigania mambo mbalimbali katika maeneo yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala la msingi la kwanza aliposema bajeti ya mwaka ilitengwa lakini haikupatikana ni kweli, na nyinyi mnafahamu sio bajeti ya ambulance peke yake, isipokuwa miradi mingi sana ya maendeleo katika kipindi kilichopita, imekumbwa na changamoto kubwa sana hasa ya upelekaji wa fedha. Maombi haya yalikuwa ni katika maombi maalum, hivyo ni imani yangu kwamba katika bajeti ya mwaka huu sasa kwa vile jiografia yake inajulikana, Ofisi ya Rais - TAMISEMI tutaweka kipaumbele kuhakikisha gari hilo linapatikana. Kikubwa zaidi katika hayo yote maana yake maombi maalum wakati mwingine yana changamoto kubwa sana na sana sana zinalenga katika collection ya mapato.
Mheshimiwa Naibu Spika, basi niwaombe Waheshimiwa Wabunge wote tushikamane kwa pamoja kuisaidia nchi yetu ili tupate mapato ya kutosha, yale maombi maalum yote tuliyoyapeleka, Serikali iweze kuona ni jinsi gani yatayafanyiwa kazi.
Sehemu ya pili, ni kwamba ni lini gari litapatikana, nimesema kwamba, Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa sababu tunaguswa na hili, katika uongozi wetu wa sasa tutapambana kwa kadri iwezekanavyo. Ndugu yangu wa Mufindi tujitahidi kwa pamoja Mungu akijalia tutapata gari, naomba amini Ofisi yako.
kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Katika Mpango wa REA kwamba itapeleka umeme vijijini, kuna vijiji vya Jimbo la Mufindi Kusini vyapata karibu 30 havijapata umeme, kuna nguzo zilipelekwa kule na baadaye zile nguzo zikaenda kuhamishwa na wananchi wana wasiwasi. Mheshimiwa Waziri naomba uwathibitishie wananchi kwamba kwenye mpango huu wa tatu wanaweza kupata huo umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa katika maeneo ya Mufindi kuna nguzo zilipelekwa na mashimo yakachimbwa, lakini kutokana na scope ya kazi ile ilionekana kwamba mashimo yalikuwa yamechimbwa maeneo ambayo siyo yenyewe. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tu, tumeshakaa na Mheshimiwa Mbunge, tumetathmini vijiji vyake vyote vya Mufindi Kusini na vyote alivyoviorodhesha vitaingia kwenye REA III na vitapatiwa umeme kwenye REA III inayoanza mwezi Julai mwaka huu.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Kwanza, hii barabara ni ya muhimu sana na ni ya miaka mingi sana na bahati nzuri sana hata Naibu Waziri wa Ujenzi mwaka 2015 alifika kule Mufindi na alifanya mikutano miwili na aliwaambia wananchi kwamba, baada ya kumaliza uchaguzi hii barabara itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami kufuatana na umuhimu wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoongelea viwanda, viwanda kule tayari viko, kuna kiwanda cha Kibwele pale, kuna kiwanda cha Kilima Factory, kuna kiwanda cha Lugoda factory, hivi ni Viwanda vya Chai na vinategemea hii barabara. Mheshimiwa Waziri aniambie kwa sababu upembuzi yakinifu walishamaliza na Serikali iliahidi na Chama cha Mapinduzi kimeahidi kwamba kitaweka kiwango cha lami. Ni lini hizi fedha zitapatikana na wataanza kujenga kwa kiwango cha lami?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wananchi walishaambiwa tayari kuna nyumba zao zilishawekewa alama ya X na wanatarajia kuhama! Je, Serikali ni lini itaenda kutoa fidia kwa wale ambao walijenga nyumba jirani na barabara na Serikali ilisema itawalipa fidia kwa mfano, wananchi wa Kijiji cha Nzivi, Igowole, Kibao, Mtwango na pale Lufuna, kuna nyumba ziliwekewa X, Serikali itaenda kuwalipa lini ili waanze kuhama?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii. Tunapoongelea ujenzi ni pamoja na fedha za fidia pamoja na fedha za ujenzi wenyewe. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kama ambavyo barabara hii ipo katika ahadi ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015/2020, namhakikishia ahadi hiyo itatekelezwa, asiwe na wasiwasi!
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kujibu maswali vizuri, lakini tunajua kabisa kwamba kuna tatizo kubwa sana la walimu wa sayansi katika Wilaya zote. Sasa je, Serikali ina mkakati gani wa kuchagua chuo kimoja kuweza kusomesha walimu wa sayansi tu? Kwa mfano, Chuo Kikuu cha Mkwawa pale, tungeamua kitoe masomo ya sayansi ili tuweze kupata walimu wengi?
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kwa nini Serikali sasa isitoe mkopo kwa asilimia mia moja kwa wale wanafunzi ambao wanasomea masomo ya sayansi ili kuwavutia wanafunzi waweze kujiunga na ualimu wa sayansi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala la mkakati wa kuwapata walimu wa sayansi, kama unavyofahamu kwamba tayari Serikali ilishachukua hatua na kama mnavyokumbuka kwamba tulikuwa na wanafunzi zaidi ya 7,800 ambao walikuwa katika Chuo cha UDOM ambao kwa sasa tumewatawanya katika vyuo mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wale ambao wana vigezo sasa hivi kwa kufundisha shule za sekondari ni zaidi ya walimu 6,305 wakishamaliza masomo yao wataweza kwenda kwenye hizo shule. Kwa hiyo, Serikali inaendelea kuweka mikakati ya kufundisha walimu wa sayansi na wakati huo huo kuhakikisha kwamba maabara kwa ajili ya shule za sekondari ili kupata wanafunzi wengi zaidi katika maeneo ya sayansi yaweze pia kukamilika na kupewa vifaa vinavyostahili.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Suala la umeme vijijini pamoja na ahadi nzuri za Serikali na kwenye bajeti hii ya 2016/2017, Serikali imeahidi vizuri sana na tunasema vijiji vyote vitapewa umeme. Kwenye shule za sekondari, shule za misingi, zahanati na sehemu nyingine za hospitali. Tunaomba Serikali itoe commitment kwamba katika mwaka huu wa fedha tuta-specialize hasa kwenye vituo vya afya na zahanati ili tusi-generalise kwamba tutapeleka kila sehemu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo tumekuwa tukieleza, labda niwaombe Waheshimiwa Wabunge watupe ushirikiano kuhusu jambo hili. Wananchi na Waheshimiwa Wabunge wengi wamekuwa wakiomba sana kupelekewa umeme kwenye vijiji vyao badala ya huduma za afya na taasisi nyingine. Namshukuru sana Mheshimiwa Kigola lakini niseme tu mpango wa Serikali wa awamu ya tatu ya REA, unazingatia sana vipaumbele vya kuwapelekea umeme taasisi za jamii pamoja na kwamba tunawapelekea pia kwenye matumizi ya nyumbani. Kwa hiyo, mpango wetu unatekelezwa hivyo. Nimwombe Mheshimiwa Mbunge ikibidi anilitee taasisi zake za umma kabla hatujatoka kwenye Bunge hili ili nimhakikishie kwamba tutaanza na hizo kabla ya kuwapelekea umeme kwenye nyumba zao.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri lakini nina maswali mawili tu ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; katika upelekaji wa umeme vijijini, REA wanapeleka kwa kufuata barabara na kwenye centres, lakini unaweza ukaona kwamba kwenye shule za msingi, sekondari, vituo vya afya na zahanati kule umeme haupelekwi. Sasa Naibu Waziri naomba anihakikishie wananchi wa Jimbo la Mufindi Kusini kwenye maeneo haya niliyotaja kama watapewa umeme?
Mheshimiwa Mwenyekiti la pili, namuomba Naibu Waziri, kwa majibu haya aliyoeleza vizuri, kwa programu ya awamu ya tatu ambayo inaanza, je, utakuja lini Mufindi ukafanya mkutano angalau hata mmoja kuongea na wale wananchi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwajulisha Waheshimiwa Wabunge na wananchi kwa ujumla kwamba mradi kabambe wa REA Awamu ya Tatu utapeleka umeme katika maeneo yote ya taasisi ikiwemo shule za msingi, sekondari, hospitali na katika taasisi nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Kigola, jimbo lako la Mufindi Kusini, maeneo yote niliyoyataja ikiwemo pia katika vijiji vyako vya Mbaramaziwa, Tambarang‟ombe kwenda mpaka Tengereo mpaka kule Kilowelo vitapelekewa umeme kwenye taasisi nilizozitaja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu suala lake la pili, kwamba ni lini sasa tutatembelea katika maeneo yale? Nimhakikishie Mheshimiwa Kigola; kwanza kabisa nikupongeze umeshaanza kuchimba visima kwa ajili ya kuhitaji umeme. Napongeza sana kwenye Kitongoji chako cha Msumbiji umeshaanza kujenga, lakini pale Idambaravumo pia umeshaanza kujenga na pia unatarajia kupeleka umeme pale Kilowelo centre, na pia kwenye vijiji vyako vingi sana ikiwemo kama nilivyosema pale Kisaula tutakupelekea mashine ya umeme, lakini pia kwenye vijiji vyako vingine mbali na vijiji na Kitongoji cha Msumbiji na pale Changarawe kwa Mheshimiwa Kigola kwa vijiji vyako 47 vilivyobaki vyote vitapata umeme wa uhakika.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Spika,
nashukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza. Kwa vile viwanda vya chai vipo Mufindi na katika majibu ya Waziri ameeleza vizuri sana viwanda vya Unilever na Mufindi Tea Company na ni kweli kabisa kwamba wakulima wa Mufindi wanapata shida sana kuhusiana na
bei ya chai na makampuni makubwa yanakopesha wakulima mbolea halafu wanakatwa kwenye bei ile ya chai mwisho wa siku wale wakulima hawapati kitu chochote.
Je, Serikali haioni kwamba kuna umuhimu wa
wakulima wadogowadogo wale wa Mufindi Serikali ikasimamia wakajenga kiwanda chao, badala ya kuuza majani mabichi waweze kuuza majani makavu?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa kwamba kuuza majani ghafi husababisha bei kuwa ndogo na ndiyo maana Serikali ya Awamu ya Tano inaweka jitihada katika uchumi wa viwanda. Tunaamini kwamba tutakapojenga viwanda vingi
maana yake wakulima wetu watakuwa na faida zaidi. Kwa hiyo, Wizara iko tayari kushirikiana na wakulima wa Mufindi na wakulima wa chai wa maeneo mengine ili kuendelea kuongeza viwanda vya chai tuweze kufanya uchakataji badala ya wakulima kuendelea kuuza chai ghafi. Nakubaliana nae kwamba ni kitu na Wizara itafuatilia.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Naibu WazirI ninaomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza kutangaza na kutafuta mkandarasi sasa hivi imeanza muda mrefu toka mwezi wa pili na imechukua karibu miezi sita sasa, ukisema mpaka Juni itachukua miezi sita. Swali langu, je, kutafuta
mkandarasi kisheria inatakiwa miezi mingapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Jimbo langu la Mufindi Kusini tuna tatizo kubwa sana la maji, ukizingatia Serikali ilijenga matenki ya maji katika kijiji cha Igowole, Nyororo, Idunda, Itandula, Kiyowela matenki haya yote yameharibika sasa hivi yana miaka karibu sita, je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha watu wa Igowole na Nyororo na
vijiji nilivyotaja vinaweza kupata maji na kukarabati mitandao ambayo imeharibika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja anasema muda au mchakato wa kumpata Mkandarasi unakuwa mrefu sana unatumia muda gani; upo kwa mujibu wa sheria. Muda wa manunuzi upo kwa mujibu wa sheria ambayo ilipitishwa katika Bunge hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni kuna matenki 11 yaliyojengwa na sasa hayana maji, ni kweli tatizo hili nilikuta pia Nanyamba, kuna matenki zaidi ya saba ambayo yalijengwa na AMREF na yalikuwa hayana maji. Matenki yale
yalikuwa yamejengwa pamoja na visima. Sasa jumuiya za watumiaji maji ambazo tuliziunda tumekuta changamoto ziko nyingi unakuta kulikuwa na pump, pump imekufa, kuna jenereta, jeneretaimekufa. Wakati mwingine kisima kinakuwa kimekosa maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa sasa nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunachokifanya sasa hivi tumefanya uchunguzi tukakuta kwamba hzi jumuiya zinaelekea kushindwa kufanya hii kazi; lakini sio kwamba ni
kwa sababu yao tu, hapana; ila ni kwa sababu ya
miundombinu iliyowekwa hawana uwezo wa kuiendesha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tumechukua
utaratibu wa kuweka solar na visima vilivyopo tutavisafisha maeneo yaliyokuwa na mtiririko tutayaweka vizuri kuhakikisha kwamba wananchi wanapata huduma na yele matanki yanafanya kazi iliyotarajiwa.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti…
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize kwali la nyongeza. Kuna barabara ya kutoka Nyororo – Igohole mpaka Mtwango ina kilometa 40 na upembuzi yakinifu ulishafanyika miaka miwili iliyopita. Je, Serikali ni lini itaanza ujenzi wa kiwango cha lami ile barabara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba Mheshimiwa Mbunge tuwasiliane tupate takwimu sahihi ya barabara unayoongelea inaanzia wapi, inafikia wapi, ina kilometa kiasi gani na kama imeshajadiliwa kwenye Road Board ya Mkoa ili hatimaye tutende haki ya kile kinachotakiwa katika barabara hiyo.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, lakini hii barabara ina miaka minne sasa tangu upembuzi yakinifu kukamilika. Naibu Waziri wa Ujenzi aliyepita aliwahi kuja kule akaongea na wananchi akasema kwamba ujenzi wa kiwango cha lami utaanza mara moja. Naibu Waziri naomba awaambie wananchi ni lini barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami kwa sababu upembuzi yakinifu ulishakamilika? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wananchi wa kijiji cha Nyololo, Nziwi, Igowole, Mninga, Kibao, Lufuna na Mtwango waliwekewa alama ya ‘X’ kwenye nyumba zao na Serikali iliahidi kwamba alama ya ‘X’ ambayo ni ya kijani watapewa fidia. Wananchi wameshindwa kuendeleza nyumba za biashara kwa sababu zimewekewa alama ya ‘X’. Ni lini Serikali italipa fidia wananchi wale ambao wanasubiria mpaka leo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA
MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi barabara hii tutaanza kuijenga mara tutakapoanza kupata fedha. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Kigola kwamba Serikali itatumia kila aina ya nguvu zake kuhakikisha kwamba inapata fedha na kutekeleza ahadi au dhamira ambayo Naibu Waziri aliyepita aliionyesha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ni kwamba ni kweli wote waliowekewa alama ya ‘X’ za kijani watalipwa fidia na zitalipwa tutakapopata hizi fedha za ujenzi. Ulipaji wa fidia unaenda sambasamba na ujenzi wa barabara husika. Kwa hiyo, fedha hizi tunazozitafuta tunazitafuta zote, za ujenzi na za kulipa fidia.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kuna barabara ambazo upembuzi yakinifu ulishakamilika toka mwaka 2015/2016. Kwa mfano, barabara ya kutoka Nyororo - Igohole mpaka Mtwango upembuzi yakinifu ulishafanyika. Ni lini sasa Serikali itaanza utekelezaji wa kujenga barabara ile kwa kiwango cha lami?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kigola anafahamu tulipokuwa Wilayani kwake tulizunguka maeneo mbalimbali na barabara anayoizungumzia ilikuwa ni barabara ya TANROADS na kulikuwa na barabara zingine za Halmashauri ambazo TARURA itashughulikia na zile barabara za Kimkoa ambazo TANROADS itashughulikia. Najua wazi kwamba mazoezi ya upembuzi yakinifu katika maeneo mbalimbali yanafanyika na kwa vile ile ilikuwa katika ahadi na Ilani ya Chama cha Mapinduzi, naomba nimhakikishie kwamba Serikali ni moja, tutahakikisha jukumu la Serikali tunalifanya ili barabara ile ya Nyororo iweze kujengwa kwa kadri iwezekanavyo.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa vile mradi huu ni wa siku nyingi unaenda miaka saba sasa na Serikali imetoa commitment kwamba mwezi Desemba, 2017 itaanza utekelezaji. Sasa kwa sababu ni wa muda mrefu mwezi Desemba isipoanza utekelezaji nini kifanyike?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Waziri wa Maji tuliwasiliana naye kuhusiana na maji Kata za Igohole, Nyololo na Mninga na niliagizwa kwamba tupeleke andiko linaloonyesha gharama za utekelezaji wa maji katika vijiji hivi nilivyotaja na andiko lile nimeshapeleka na gharama zote, liko kwa Katibu Mkuu. Sasa lini utekelezaji wa maji katika Vijiji vya Igohole na Nyololo utafanyika kwa sababu hawana maji kabisa na hivi ninavyoongea hawana maji. Ni lini Serikali itatekeleza? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe kwamba nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba wananchi wanapata maji na kwa kuwa maji ni uhai na pasipo maji hakuna uhai, labda nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama ilivyoahidiwa kwamba mwezi Desemba mradi ule unatekelezwa na mimi kama Mheshimiwa Waziri nitasimamia na kusukuma kuhakikisha kwamba mradi ule unatekelezwa ili wananchi wa eneo lile waweze kupata maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili kuhusu andiko na umuhimu wa suala la maji labda nimwombe sana Mheshimiwa Mbunge kama anavyowapigania wananchi wake baada ya kikao cha Bunge tukutane na mimi nipate nafasi ya kupitia andiko lile tuangalie namna ya kuweza kuwasaidia wananchi wa Igohole na Nyololo. Ahsante sana.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Naibu Waziri lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, Mheshimiwa Naibu Waziri alipokuja kule Mufindi hakufika kwenye Jimbo la Mufindi Kusini kuzungumza na wananchi na ukizingatia Jimbo la Mufindi ndilo lililozungukwa na misitu sasa wananchi wanakuuliza, je, utaenda lini ili uweze kuongea na wale wadau wanaozunguka msitu ule? (Makofi)
Swali la pili, kuna makundi ya vijana wameshajiunda tayari ambao wazazi wao waliacha maeneo makubwa sana ambayo yalichukuliwa na watu wa Maliasili na vikundi hivyo Igowole kuna vijana 60, Mninga 60, Kihanga 60, Nzigi 60, Mtwango 60, Sawala 60, Kasanga 60, Mabaoni 60, Kitasengwa 60, Kiyowela 60, Nyororo 60, Kibao 60, Mkalala 60, Mbala Maziwa 60, Malangali 60, Mtambula 60, Ihowanza 60, Logolofu 60 na Luhunga 60. Hawa ni vijana waliojiunga kwenye vikundi tayari na ukitokea moto wanakimbia mbio na bodaboda kwenda kuzima moto katika msitu ule. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa viko vikundi 20 tu na wanaomba kila kikundi kipewe kibali kimoja, Mheshimiwa Naibu Waziri upo tayari mgao huu kuwapatia vibali vyao vijana?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza kuhusu ziara ile niliyoifanya na maelezo kwamba baadhi ya maeneo ambayo yanapakana na shamba la Sao Hill sikuweza kufika. Kwanza ni kweli kutokana na ratiba niliweza kufika tu kwenye baadhi ya maeneo lakini nataka nimthibitishie kwamba bado umuhimu wa kutembelea kwenye maeneo yaliyobaki uko pale pale. Jitihada za Serikali za kuweza kutekeleza Ilani ya CCM, ya kuhakikisha kwamba Hifadhi za Taifa zikiwemo hifadhi za misitu zinawanufaisha wananchi wanaoishi jiraniau wanaopakana nazo iko pale pale na kwa hiyo, napenda tu nimhakikishie na nimpe ahadi tu kwamba nitafika kwenye maeneo hayo na safari hi sitafanya kikao pale Mufindi Mjini nitakwenda kufanya kikao kule kule mashambani porini niweze kuzungumza na wanavijiji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusu vikundi alivyovitaja na idadi ya vijana ambao wako kwenye vikundi hivyo. Kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, nani vyema tukaenda kwa pamoja na Mheshimiwa Mbunge kwanza nikupe pongezi kwa kuwatetea na kuwazungumzia vijana hao na wananchi kwa ujumla katika maeneo hayo. Lakini vilevile niseme kwamba ni nia ya Serikali sasa kwamba hatutasubiri vijana wasubiri tu kunufaika na uvunaji wa mazao ya misitu kutoka kwenye misitu ya Taifa. Lakini sasa mwelekeo ni kuweza kuwafanya vijana na wenyewe waweze kumiliki mashamba yao ndio maana tunagawa mbegu kama vile ambavyo nimesema kwenye jibu la msingi miche karibu laki sita iligawiwa kwenye matukio ya pale awali.
Mheshimiwa Naibu Spika, tutaendeleza utaratibu wa kuwezesha vikundi hivyo ili baadae viweze kusimama vyenyewe kwa kuwa na mashamba ya kwao ya miti. Nitoe wito na ushauri kwa Halmashauri inayohusika kuweza kuwagawia maeneo vijana hao ili waweze kupata miti, wachukue miche kutoka kwenye Wizara yangu na waweze kupanda katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu maombi yake kwamba katika maombi ya mwaka huu kuweza kuzingatia maombi ya vijana wake kwenye eneo lile ninalichukua nitalifikisha kwa wataalam. Lakini litaenda kutazamwa sambamba na maombi mengine ambayo yamekwishapokelewa kwa mujibu wa muongozo ambayo nimeutaja hapo awali.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri. Hivi vituo vilianza miaka mingi sana, sasa hivi ni miaka tisa bado havijakamilika na mimi swali langu nimesema ni lini sasa Serikali itamaliza ujenzi huu kwa sababu umechukua muda mrefu sana? Hilo ni swali la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imesema itapeleka Sh.35,500,000 na imeshapeleka Sh.8,000,000 tu, bado Sh.24,000,000 bado. Je, ni lini Serikali sasa itapeleka hii fedha Sh.24,000,000 ili ujenzi ule ukamilike? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge, tulipokuwa kule site; miongoni mwa maeneo tuliyotembelea ni Sekta ya Afya katika Jimbo lake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kweli hivi sasa imepelekwa shilingi milioni nane, bado takriban shilingi milioni 24. Hata hivyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge; hivi leo asubuhi nilikuwa naongea na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi, Bwana Shemdoe. Katika mambo ambayo tumekubaliana ni kwamba atenge fedha kwa kadri inavyowezekana kuhakikisha vituo hivi vinakamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, najua wazi kwamba Jimbo la Mufindi Kusini ni miongoni mwa Halmashauri tajiri ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Rasilimali walizonazo zikisimamiwa vizuri tutaweza kufanya vitu vingi zaidi. Kwa hili Mkurugenzi amenipa commitment leo hii asubuhi wakati naingia getini, amesema kwamba atashirikiana na Waheshimiwa Wabunge ahakikishe miradi yote ambayo bado haijakamilika watumie fedha, own source, wakamilishe miradi yote wasiwe na viporo tena vinavyoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itasimamia vizuri, lakini kwa sababu na wao wamejipanga vizuri, yeye na Mheshimiwa Mgimwa, nadhani hakuna kitu kitakachoharibika katika Halmashauri yao kwa sababu ni miongoni mwa Halmashauri tajiri, own source yao ni kubwa kuliko jambo lingine lolote.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; katika awamu ya pili ya REA ambayo imekwisha kuna vijiji ambavyo havijapitiwa na katika upelekaji wa umeme ule ulienda kwenye makao makuu ya kata. Kwa mfano, pale Malangali Vijiji vya Isinikini, Kingege, Ibangi na Ikaning’ombe pale bado havijapata umeme. Je, Serikali itarudi kwenye kutekeleza ile ambayo ilikuwa ni awamu ya pili?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Serikali ilisema kwamba itapeleka umeme kwenye vituo vya afya, zahanati, pamoja na shule za sekondari na shule za msingi, lakini mpaka sasa hivi shule za msingi bado hatujaona programu kwamba, Serikali inapeleka. Je, katika awamu hii ya tatu mnatuhakikishia kwamba, katika maeneo haya niliyoyataja watapewa umeme?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niseme utekelezaji wa miradi ya umeme unafanana sana na miradi ya maji. Katika utekelezaji wa miradi ya umeme Wilaya zote kwa sasa wanafungua Ofisi za TANESCO. Awamu ya pili amesema kwamba, kuna vijiji ambavyo vimeachwa, kama tayari Ofisi ya TANESCO iko pale, basi wale ambao hawajapata wapeleke maombi kwenye zile ofisi ambazo zitaendelea kufanya extension ikiwa ni pamoja na kuingiza umeme kwenye majumba ya wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, vivyo hivyo, Taasisi za Serikali naomba sana Mheshimiwa Mbunge kwamba, kukishakuwa na ofisi ni vema hizo taasisi za Serikali kama zina mahitaji ya umeme na ni lazima zina mahitaji ya umeme, basi ni kuwasiliana na ofisi zilizopo jirani kupeleka maombi, ili waweze kufikiriwa kupelekewa umeme kwenye hizo taasisi. Kama bajeti itakuwa haitoshelezi kwenye ofisi za Wilaya au Mkoa wao basi wata-forward moja kwa moja hayo mahitaji Makao Makuu ya TANESCO ili waweze kupatiwa pesa au waweze kuingiza hizo shule na taasisi za Serikali ziweze kuingizwa katika mradi mkubwa. (Makofi)
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, kwa vile kwenye Jimbo la Mufindi Kusini Wilaya ya Mufindi, tuna ujenzi wa hospitali ambayo ni kubwa sana.
Je, Wizara ya TAMISEMI mnaweza mkatusaidia kupata ramani ambayo ni standard kwa ajili ya kujenga hospitali pale Jimbo la Mufindi Kusini?
Swali langu la pili, kama alivyoeleza kwenye majibu yako kwamba tuna ujenzi mkubwa sana pale Malangali Kituo cha Afya. Kwanza naishukuru Serikali kwa kutupatia zile milioni 400; lakini kile kituo cha afya tunategemea kifunguliwe na mtu mkubwa sana. Je, Naibu Waziri uko tayari kutuunganisha na Waziri Mkuu aweze kufika pale Malangali kufungua kile kituo cha afya ili kianze kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nichukue nafasi hii kuipongeza Halmashauri kwa kazi nzuri waliyofanya kuhakikisha kwamba kituo cha afya kile kinakamilika na ni miongoni mwa vituo vya afya ambavyo vimejengwa kwa ustadi mkubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, juu ya suala la ujenzi wa hospitali ya Wilaya hitaji lake kubwa ni upatikanaji wa ramani, naomba nimhakikishie kwamba Wataalam wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI pamoja na Wataalam Wizara ya Afya, wako mbioni kukamilisha ramani ambazo zitatumika katika ujenzi wa Hospitali za Wilaya hizo 67 ikiwemo ya kwake ya Mufindi. (Makofi)
Swali lake la pili anaomba Ofisi ya Rais, TAMISEMI imuunganishe uwezekano wa Mheshimiwa Waziri Mkuu kuwa miongoni mwa watu watakaoenda kuzindua kituo chake cha afya. Naomba nimhakikishie utaratibu unaandaliwa chini ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutaanza vituo 44 vyote vile ambavyo vimejengwa na kukamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatarajia pale Mheshimiwa Rais kwa nafasi yake na jinsi atakavyoridhia kutakuwa na uzinduzi ambao utafanyika nchi nzima tukianzia na hivyo vituo 44; sina uhakika sasa kwa nafasi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kama ataweza kwenda kuzindua kwake. (Makofi)
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Naibu Waziri. Mheshimiwa Waziri alikuja Mufindi na alikuja kwenye Kata ile ya Mtwango. Mradi wa Kata ya Mtwango una miaka karibu sita na mkandarasi yupo site, Serikali haijapeleka fedha mpaka leo. Hebu awaambie wananchi wa Kata ya Mtwango, ni lini Serikali itapeleka fedha kwenye kata ile?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, naishukuru Serikali kwa kutenga bilioni 2.67 kwa ajili ya Miradi ya Igowole, Mtambula, Nyololo, Idunda na Itandula. Sasa, je, Naibu Waziri, ni lini atakuja katika Jimbo la Mufindi Kusini awaeleze haya aliyoeleza leo Bungeni? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana kwa kazi kubwa anayoifanya na amekuwa na usumbufu mkubwa sana kuhusu suala zima la maji katika Jimbo lake. Naendelea kusema sisi Wizara ya Maji na kwa kuwa siyo Wizara ya Ukame, nataka nimwambie Katibu wangu Mkuu ndani ya mwezi huu tutapeleka fedha wananchi wako waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuhusu mimi kwenda Mufindi, nipo tayari, baada ya Bunge tuongozane na Mheshimiwa Mbunge twende tukazungumze na wananchi wake. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali na nitoe pongezi kwa mkandarasi ambaye amepangwa kwenye Jimbo langu la Mufindi Kusini kwa kazi nzuri anayoifanya. Tulikuwa tuna tatizo la transfoma pale Ihowanza baada ya kumpa taarifa nimepata taarifa kwamba ameshaipeleka na pale Mbalamaziwa tulikuwa tuna tatizo la transfoma ameshaipeleka na sasa hivi mkandarasi yupo site. Kwa kazi hiyo nzuri, naipongeza sana Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali langu la kwanza kuna vitongoji vingi sana kwenye Jimbo langu la Mufindi Kusini ambavyo havikufanyiwa survey na tulikuwa tumeandika hata majina tukapeleka pale TANESCO, je, vile vitongoji ambavyo vilikuwa vimerukwa mara ya kwanza na vyenyewe vitapewa umeme?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ningemuomba Waziri kama atapata nafasi kwa sababu kwenye Jimbo langu la Mufindi Kusini hawajaja, je, atakuja sasa kufanya mkutano akielezea vizuri matumizi haya ya umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tumepokea pongezi za Mheshimiwa Mbunge kwa namna ambavyo miradi ya REA III inavyoendelea katika Wilaya ya Mufindi hususani katika jimbo lake. Namshukuru kwa kulithibitishia Bunge lako kama mkandarasi yupo anaendelea vizuri na kweli mkandarasi Sengerema ni miongoni wa wakandarasi ambao wanafanya kazi zao vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimpongeze yeye mwenyewe Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia masuala ya nishati katika jimbo lake, anafanya kazi vizuri. Ndiyo maana katika maswali yake ya nyongeza amekiri kwamba kulikuwa na tatizo la transfoma kwenye kata alizozitaja na kutokana na maelekezo ya Mheshimiwa Waziri transfoma hizo zimeshafika katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake moja ameuliza ni lini vitongoji ambavyo havijafikiwa na umeme vitapata? Nataka nilitaarifu Bunge lako Tukufu na Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inaendelea kufanya upembuzi yakinifu kwenye Mradi wa densification II baada ya kufanikiwa kwa densification I, ambayo itahusisha mikoa 17 pamoja na Mkoa wa Iringa na katika vitongoji ambavyo vitasalia vitapatiwa umeme katika mradi wa ujazilizi awamu ya pili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili kuhusu kutembelea katika Jimbo lake la Mufindi Kusini na hususan Wilaya ya Mufindi, nataka nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya Bunge hili kwa kweli tutatembelea Mkoa wa Iringa kwa sababu mpaka sasa hivi tuna vijiji takribani 20 vinatakiwa kuwashwa umeme lakini pia kuna mradi ambao unaendelea wa BTIP ambao kwa kweli umefanya vizuri. Hivyo, nataka nilitaarifu Bunge ipo kazi ya kufanya katika huo Mkoa wa Iringa na Jimbo lake la Mufindi Kusini, kwa hiyo, tutakuja. Ahsante sana.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Kuna barabara ya kutoka Nyororo mpaka Mtwango kilimeta 40, barabara ya kutoka Mafinga mpaka Mgololo kilometa 84 na upembuzi yakinifu Serikali ilishafanya miaka miwili iliyopita. Sasa ni lini itaanza kujenga ile barabara kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kigola kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina nia na lengo la kuunganisha kwanza mikoa kwa kiwango cha lami. Hatua zitakazofuata baada ya kuunganisha mikoa yote kwa kiwango cha lami, tutaunganisha wilaya zote kwa kiwango cha lami. Namwomba sana Mheshimiwa Mbunge awe na subira, tunafahamu suala lake na siyo la kwake peke yake, wilaya nyingi sana Tanzania hazijaunganishwa kwa kiwango cha lami. Tutakapofikia mahali pa kuunganisha kwa kiwango cha lami wilaya zote tutafahamishana na tutaanza taratibu hizo mara moja. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi hii kwa kumshukuru sana Makamu wa Rais alipokuwa amekuja kwenye jimbo langu na mimi nilimwomba Ambulance siku ile na utekelezaji umefanyika nashukuru sana. Swali langu la kwanza kule jimboni kwangu nina vituo vya afya kama vitatu ambavyo viko vijijini sana hakuna magari kwa mfano pale Mninga na Mtwango ni vituo vikubwa sasa. Je, Serikali itanisaidia tena kuniletea (Ambulance katika hivyo vijiji viwili ambao wananchi wanapata shida sana?
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, nina tatizo kubwa sana la watumishi wa Afya kwenye vituo vyangu vya afya na zahanati kwenye jimbo langu. Je, Wizara ya Afya ina utaratibu gani wa kuhakikisha kwamba watumishi wa Afya tunaweza kuwapata?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kwanza kwa niaba ya Serikali naomba nipokee shukrani ambazo zimetolewa na Mheshimiwa Mbunge. Katika suala lake la kwanza, anaongelea vituo vya afya vingine viwili ambavyo viko mbali sana na vina uhitaji mkubwa wa magari ya Ambulance.
Mheshimiwa Spika, naomba nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni azma ya Serikali pale ambapo gari zinapatikana tutazisambaza na hasa tutazingatia maeneo yenye uhitaji mkubwa sana. Sasa kama na eneo la kwake litakuwa miongoni mwa hayo maeneo ambayo yana uhitaji mkubwa hakika sisi tutatekeleza hilo, lakini ni vizuri pia akatambua kwamba kuna baadhi ya maeneo ambayo hawakupata hata hiyo gari ambayo yeye amepata kwa hiyo kwa kadri gari zitakapopatika tutafuata uwiano unaotakiwa ili haki iweze kutendeka.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili, anaongelea juu ya vituo vyake vya afya kutokuwa na watumishi wa kutosha, naomba nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge sasa hivi Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumeshatangaza nafasi 6,180,000 na naamini pale ambapo watakuwa wameajiriwa na eneo la kwake litaweza kufikiriwa kupelekewa.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kweli Wilaya ya Mufindi tuna tatizo kubwa sana la mawasiliano na Mheshimiwa Naibu Waziri amesema ni kutokana na jiografia ilivyo. Vijiji vya Idete, Kasanga, Ihowanza, ni sehemu kubwa sana hawana mawasiliano kabisa na amesema kwamba atakuja na timu yake, je, yuko tayari sasa timu hiyo iende ikafanye survey kwenye vijiji hivi ili wananchi wale waweze kupewa mawasiliano?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE):
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Kigola, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kifupi, niko tayari kwenda naye kuangalia maeneo hayo. Ahsante.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Mpaka sasa hivi Mkoa wa Njombe kuna tatizo kubwa sana la kuuawa watoto wadogo. Sasa Serikali inasemaje kuhusiana na hili, maana wananchi wa Njombe sasa hivi wana wasiwasi mkubwa na wazazi wanawapeleka watoto wao shuleni. Je, Serikali inasemaje kuhusiana na mauaji haya yanayoendelea katika Mkoa wa Njombe?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kumekuwa na sintofahamu na kuzuka kwa taharuki katika Mkoa wa Njombe kutokana na vitendo vya baadhi ya Watanzania wenzetu ambao wamekuwa wakiwachukua watoto wadogo na kuwaua. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kuanzia juzi Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Injinia Hamad Masauni yuko kule Mkoa wa Njombe anafanya vikao na Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya pamoja na Mkoa kuhakikisha kwamba vitendo hivi vinakomeshwa, lakini taarifa za awali zinaonesha ni imani za kishirikina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Wabunge watupe ushirikiano
kwa sababu Waheshimiwa Wabunge maeneo yale wanayafahamu vizuri. Nitoe onyo siyo kwa Njombe peke yake bali kwa Watanzania wote kwamba wasitingishe kiberiti cha Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, wasipoacha vitendo hivyo watakipata cha mtema kuni na tunaanza na kule Njombe ambako tumeshabaini majina kwa ajili ya kuwachukulia hatua za kisheria.
MHE. MENDRARD L. KIGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kuna Vituo vya Afya vya Mtwango, Nunga na Iramba tushaezeka na kila kitu tayari. Je, Serikali itamalizia lini yale majengo ili wananchi waanze kuvitumia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Mufindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Mufindi kuna kituo cha afya kimekamilishwa na wananchi lakini vituo vingi vya afya vimejengwa nchini kama nilivyosema katika jibu langu la msingi. Tunawapongeza wananchi kwa kushirikiana na Serikali kuiunga mkono katika hatua hii muhimu ya kuboresha huduma za afya. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutawasiliana tuone wamefikia hatua gani kwa kushirikiana na Halmashauri na kama kuna mpango wao basi tuone namna ya kumaliza kituo hiki ili kuunga mkono nguvu za wananchi ili zisipotee bure.
MHE. MENDARD L. KIGOLA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, huu mradi wa maji wa Sawala umechukua muda mrefu sana zaidi ya miaka 6 na Serikali mara ya kwanza ilitoa fedha zaidi ya milioni 200 lakini hakuna kitu ambacho kimefanyika. Mara ya pili imetoa milioni 230, hakuna kitu kilichofanyika na wananchi pale sasa wanakata tamaa. Swali langu, ni lini mradi huu utakamilika ili wananchi waanze kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna wakandarasi wawili wameshatolewa, sasa hivi Serikali inatumia mbinu gani ili kuhakikisha kwamba ile kazi inafanyika kikamilifu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuweza kufuatilia miradi yake ya maji. Kikubwa utekelezaji wa miradi ya maji katika ubora unategemeana na upatikanaji mzuri wa wakandarasi.

Mheshimiwa Spika, nilifika pale Mufindi Kusini eneo lile la Mtwango, moja ya changamoto kubwa mkandarasi ambaye amepewa kazi ile alikuwa wa kibabaishaji (kanjanja) kwa hiyo tulimuondoa mkandarasi yule lakini tumeiagiza TAKUKURU kuhakikisha fedha zile za wananchi walipakodi azitapike mkandarasi yule. Sisi kama wizara tumehukua jukumu sasa la kuwapatia ndugu zetu wa Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA) kwa maana ya kufanya kazi ile kwa force account mradi ule ukamilike na wananchi wake waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kumuhakikishia Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Wizara ya Maji tunatumia forced account katika kuhakikisha mradi ule tunautekeleza kwa wakati na wananchi wako waweze kupata huduma hii muhimu. (Makofi)
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Jimbo la Mufindi Kusini tuka kata 16, tuna vijiji 80, tuna vitongoji 365, lakini hatuna Ofisi Za TANESCO, na bahati nzuri tumeanza kujenga Hospitali kubwa sana pale Igohole na Halamshauri ya Mufindi itajengwa pale, Makao Mkuu. Je, Serikali ina mkakati gani sasa kujenga ofisi ya TANESCO kubwa kwa ajili ya kuhudumia vijiji nilivyotaja?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Umeme TANESCO limekuwa likiweka ofisi kulingana na mahitaji na uhalisia wa upatikanaji wa fedha. Kwa sasa taratibu zinazotumika ni kwamba, sehemu ambayo ina wateja zaidi ya 10,000 na laini ya umeme kutoka inapochukuliwa mpaka kufikia huko, umbali wa kilomita 500, mara nyingi imekuwa ikiwekwa ofisi. Lakini vilevile tumekuwa tukiangalia mazingira halisi ya umbali kutoka katika makao makuu ya Serikali kwa maana ya mkoa au wilaya na vilevile pale ambapo inaonekana kwamba mazingira yake ni magumu kiasi kwamba upatikanaji wa huduma ni mgumu zaidi, tumekuwa tukiweka ofisi za TANESCO na kwa kuanzia tunaweka hata zile ofisi ndogo za kuhudumia wananchi.

Kwa hiyo, niseme tu kwamba, eneo hilo litapewa umuhimu baada ya kutathmini hayo ambayo nimeyazungumza.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Tuna Zahanati iko katika Kata ya Luhunga Kijiji cha Igoda, ile zahanati tulishamaliza kujenga kila kitu na vitanda tulishaweka, na sasa ina miaka miwili haijafunguliwa. Je, ni lini Serikali sasa itaenda kufungua ile zahanati ambayo imejengwa na wananchi ili iweze kuanza kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie fursa hii kutoa maelekezo kwa Waganga wote wa wilaya nchini, kwamba maeneo ambayo wananchi wamejenga zahanati na zimekamilika hakuna sababu ya kuendelea kusubiria zisianze kutoa huduma; na hasa pale anaposema Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari vifaa vyote vipo. Kwa hiyo ni vizuri ndani ya Wilaya wahakikishe kwamba wanapeleka watumishi; kazi ambayo inawezekana kabisa; ili zahanati hiyo ianze kufanya kazi na wananchi wafaidi matunda ya jasho lao.