Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Gibson Blasius Meiseyeki (7 total)

MHE. GIBSON B. MEISEYEKI aliuliza:-
Kwa nini Serikali isifanye jitihada za makusudi za kuwatafutia wafugaji mbegu bora za mifugo aina mbalimbali na kuwasambazia wafugaji kwa bei nafuu ili kuondokana na aina za mifugo ambayo haina tija kwa wafugaji?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gibson Ole-Meiseyeki, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inafanya jitihada za makusudi kuhakikisha wafugaji wanapata mbegu bora za mifugo kwa kutumia njia mbalimbali ikiwemo uhimilishaji kwa kutumia mbegu bora za mifugo zinazozalishwa katika Kituo cha Taifa cha Uhimilishaji cha Usa River (NAIC). Katika kipindi cha mwaka 2007/2008 hadi 2015/2016 kituo kilizalisha jumla ya dozi 951,789 za mbegu bora za ng‟ombe na kusambazwa nchini ambapo jumla ya ng‟ombe 871,183 wa maziwa na ng,ombe 80,606 wa nyama walihimilishwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, katika jitihada za kuwezesha wafugaji kupata huduma hii kwa urahisi, Serikali imeanzisha vituo sita vya Kanda vilivyopo, Kibaha (Pwani), Lindi (Lindi), Kizota (Dodoma), Uyole (Mbeya), Kituo cha Uchunguzi wa Magonjwa ya Mifugo cha Mwanza (Mwanza) na Mpanda (Katavi). Pia Serikali inaendelea na ujenzi wa kituo kingine cha Taifa cha Uhimilishaji cha Sao Hill kilichopo kwenye shamba la kuzalisha mitamba la Sao Hill (Mafinga-Iringa) kwa lengo la kusambaza huduma hii ya uhimilishaji katika Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia Serikali inazalisha na kuwasambazia wafugaji mifugo bora (majike na madume) kwa bei ya ruzuku kutoka katika mashamba yake. Mashamba haya yanazalisha mitamba ya ng‟ombe wa maziwa, mitamba na madume ya ng‟ombe wa nyama, mbuzi wa maziwa na nyama, kondoo na nguruwe. Kwa mfano, mtamba wa ng‟ombe wa maziwa unauzwa kati ya shilingi 800,000 – 1,000,000/= ikilinganishwa na bei ya soko iliyopo ya kati ya shilingi 1,200,000/= na 2,300,000/=. Aidha, katika kipindi cha mwaka 2009/2010 hadi 2015/2016, jumla ya mitamba 4,520 ilizalishwa na kusambazwa katika mikoa yote nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuhamasisha sekta binafsi kuona fursa ya kibiashara katika kuzalisha mbegu bora za mifugo ili kukidhi mahitaji. Aidha, nawashauri Waheshimiwa Wabunge waendelee kuwahamasisha wafugaji wakiwemo wa Jimbo la Arumeru Magharibi kutumia huduma za kuboresha mifugo zinazopatikana kwenye vituo vyetu ili kujipatia mifugo yenye tija.
MHE. ZAYNAB M. VULU – (K.n.y. MHE. GIBSON B. MEISEYEKI) aliuliza:-
Mkoa wa Arusha na Wilaya ya Simanjiro ni maeneo yanayotegemeana sana kiuchumi lakini hayana barabara ya kuwaunganisha kiuchumi:-
Je, ni lini Serikali itayaunganisha maeneo haya ya Arusha, Simanjiro, Naberera, Kibaya – Kongwa kwa barabara ili kuimarisha maendeleo ya kiuchumi katika maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Gibson Ole Meiseyeki, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa barabara ya Arusha – Simanjiro – Kibaya hadi Kongwa yenye urefu wa Kilomita 434 ni muhimu kwa shughuli za kiuchumi, kwani inapita katika maeneo muhimu ya uzalishaji wa kilimo, madini, ufugaji na utalii na pia inaunganisha mikoa mitatu ya Arusha, Manyara na Dodoma.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua umuhimu wa barabara hiyo, Serikali imepanga kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara ya Arusha – Simajiro – Kibaya hadi Kongwa yenye urefu wa Kilomita 434 ili hatimaye iweze kujengwa kwa kiwango cha lami.
Aidha, shilingi milioni 521.3 tayari zimetengwa na kiasi cha shilingi milioni 350 zimeombwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017 kwa ajili ya kuanza taratibu za manunuzi kwa ajili ya kumpata mhandisi mshauri wa kufanya kazi hiyo ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Mara baada ya kukamilika kwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, Serikali itatenga fedha za kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami kulingana na upatikanaji wa fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mipango hiyo na kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, Serikali imekuwa ikitenga fedha za matengenezo kila mwaka ili kuhakikisha inapitika majira yote ya mwaka. Kuanzia mwaka wa fedha 2013/2014 hadi 2015/2016, jumla ya shilingi 4,383,895,000/= zilitengwa kwa ajili ya matengenezo mbalimbali ya barabara hii ili iendelee kupitika majira yote ya mwaka.
MHE. GIBSON B. MEISEYEKI aliuliza:-
Wakulima na wafugaji wa Tanzania hawajawahi kuwa na uhakika wa bei ya mazao yao hasa katika msimu wa mavuno ya kutosha badala yake wanageuka watumwa wa mazao yao wenyewe kwa kukosa masoko, maghala na bei zuri ya mazao.
Je, ni lini tatizo hili litaisha ili kuwezesha Watanzania wengi zaidi kujiingiza kwenye kilimo na ufugaji?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Gibson Ole-Meiseyeki, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kama alivyoeleza Mheshimiwa Gibson, uhakika wa bei na masoko ya mazao ya kilimo umekuwa ni changamoto kwa wakulima na wafugaji wetu. Kwa kutambua hilo Serikali ilibuni Sera ya Masoko ya Mazao ya Kilimo mwaka 2008 mahususi kwa kuimarisha mifumo ya masoko ya mazao nchini. Aidha, mkakati unganishi wa maendeleo ya viwanda wa mwaka 2020 (intergrated industrial development strategy 2020 – IIDS) na Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Miaka Mitano wenye lengo la kujenga uchumi wa viwanda umezingatia kwa dhati uongezaji thamani wa malighafi za kilimo ili wakulima wapate masoko ya uhakika.
Mheshimiwa Spika, viwanda vya kipaumbele vinavyolengwa katika mkakati na mpango huo ni pamoja na viwanda vya kusindika mbegu za mafuta, kutengeneza nguo na mavazi, kubangua korosho, kutengeneza ngozi na bidhaa zitokanazo na ngozi, viwanda vya nyama, viwanda vya maziwa, uzalishaji wa sukari na usindikaji wa matunda na mboga mboga.
Mheshimiwa Spika, aidha, ili kufanikisha uhakika wa ubora, wingi wa malighafi na bei nzuri kwa wakulima, Serikali inaendelea kuimarisha Mfuko wa Stakabadhi za Ghala ambao unawezesha mazao kutunzwa na kupunguza uharibifu wa mazao baada ya kuvuna (post harvest loss).
Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa mipango iliyotajwa hapo juu itatuwezesha kutengeneza masoko ya uhakika na bei nzuri kwa wakulima na wafugaji. Kama ambavyo tumekuwa tukihimiza mara kwa mara tutashirikiana na kuiwezesha sekta binafsi kujenga viwanda.
Mheshimiwa Spika, Maeneo mengine ya ushirikiano ni pamoja na ujenzi wa miundombinu ya masoko kama vile maghala ya kuhafadhia mazao, barabara za vijijini na utoaji wa elimu kwa umma juu ya umuhimu wa uzalishaji wa tija.
MHE. GIBSON B. OLE-MEISEYEKI aliuliza:-
PPRA na TEMESA vimekuwa vyombo vinavyoisababishia Halmashauri zetu hasara kubwa katika utekelezaji wa miradi katika utengenezaji magari na mitambo badala ya kusaidia Serikali katika kutimiza majukumu yake kwa bei nafuu:-
Je, Serikali haioni umefika wakati wa kuvifuta vyombo hivyo au kuvibadilishia utaratibu wake wa kufanya kazi ili viweze kuwa na tija kwa Taifa letu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI (K.n.y. WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gibson Blasius Ole-Meiseyeki, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) umeanzishwa chini ya Sheria Na. 30 ya mwaka 1997 ya Wakala. TEMESA ina majukumu ya kusimamia matengenezo ya magari, pikipiki na mitambo ya Serikali, matengenezo ya mifumo ya umeme, elektroniki na viyoyozi kwenye majengo ya Serikali pamoja na kutoa huduma ya uendeshaji vivuko vya Serikali na ukodishaji wa mitambo. Aidha, TEMESA hutoa huduma za ushauri wa kitaalam kwa Serikali kwenye maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Ununuzi wa Umma ya mwaka 2011 na Kanuni zake za mwaka 2013, TEMESA ina jukumu la kutoa huduma zake kwa Serikali. Katika kuboresha utendaji wa TEMESA, Serikali kila mwaka imekuwa ikiwekeza katika kuboresha karakana za TEMESA, ikiwemo kuongeza vitendea kazi vya kisiasa na kuajiri wataalam wenye ujuzi wa magari na mitambo ya kisasa. Kwa sasa TEMESA ina jumla ya Wahandisi 78 na mafundi 344. Serikali pia imebadilisha Menejimenti ya TEMESA kwa lengo la kuongeza ufanisi.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali itahakikisha kuwa huduma za TEMESA zinaboreshwa na kutolewa kwa ufanisi bila urasimu wowote kwa kufuata Mkataba wa Huduma kwa Wateja na Mwongozo wa Matengenezo ya Magari ya Serikali. Vilevile, Serikali itaendelea kusimamia TEMESA ili kuhakikisha kuwa kuna usimamizi wa karibu wa ubora wa matengenezo ya magari na karakana zake zinatumia vipuri halisi katika matengenezo ya magari.
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa inayoikabili TEMESA ni madeni makubwa ambayo wakala unadai Wizara, Taasisi za Serikali na Halmashauri. Mpaka sasa TEMESA inazidai taasisi hizo zaidi ya shilingi bilioni 11. Kuchelewa kulipwa madeni haya kunaipunguzia TEMESA uwezo wa kutoa huduma. Napenda kutumia fursa hii kuzitaka Wizara, Taasisi za Serikali pamoja na Halmashauri zote zinazodaiwa na TEMESA kulipa madeni yao haraka kabla Serikali haijachukua hatua stahiki.
MHE. GIBSON B. MEISEYEKI aliuliza:-
Uhaba wa maji ni moja kati ya matatizo sugu katika Jimbo la Arumeru Magharibi ingawa maji yote yanayotumika katika Jiji la Arusha yanatokea kwenye Jimbo la Arumeru Magharibi:-
Je, ni nini mkakati wa haraka wa Serikali wa kutatua tatizo hilo la maji katika kata takribani 20 kati ya kata 27 za jimbo hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gibson Blasius Meiseyeki, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli zaidi ya asilimia 65 ya maji yanayotumika Jiji la Arusha yanatoka katika vyanzo vilivyopo katika Halmshauri ya Arusha lilipo Jimbo la Arumeru Magharibi. Mkakati wa Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP) ni kuboresha huduma ya maji vijijini na mijini kwa kujenga miradi mipya, kupanua na kukarabati miundombinu ya maji.
Mheshimiwa Spika, hadi sasa Serikali imekamilisha miradi mitatu katika Vijiji vya Ilkirevi, Oleigeruno na Nduruma na miradi mingine sita katika Vijiji vya Bwawani, Likamba, Ngaramtoni, Oloitushula, Nengun’gu na Loovilukuny ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji. Miradi yote hiyo ipo katika Halmashauri ya Wilaya ya Arusha.
Mheshimiwa Spika, Vijiji vya Kata za Moivo, Sokon II, Kiranyi, Bangata na Kiutu ambazo zipo katika Halmashauri ya Wilaya ya Arusha vinanufaika na huduma ya maji safi na salama yanayotumika katika Jiji la Arusha. Aidha, Kata tatu za Olturumet, Olmotony na Kimnyak ambazo pia zipo katika Halmashauri hiyo zitanufaika na mradi mkubwa wa maji unaotekelezwa hivi sasa katika Jiji la Arusha.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2017/ 2018, Serikali imetenga shilingi bilioni tatu kwa ajili ya Halmashauri ya Wilaya ya Arusha za kukamilisha miradi inayoendelea. Aidha, hivi sasa Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Uingereza kupitia Shirika la Kimataifa la Maendeleo (DFID) imetoa shilingi bilioni 3.5 kwa ajili ya usanifu wa mradi wa kuboresha huduma ya maji utakaohudumia Vijiji vya Lengijave, Olkokola, Ekenywa, Ngaramtoni na Seuri ambavyo pia vipo katika Halmashauri ya Wilaya ya Arusha. Usanifu wa mradi huo unatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2018.
MHE. GIBSON B. OLE MEISEYEKI aliuliza:-
Hivi karibuni Serikali ilianza zoezi la kubomoa nyumba kwenye vyanzo vya maji na waathirika wa operesheni hiyo sheria imewakuta na wengi wao walikuwa kwenye maeneo hayo tangu enzi za ukoloni hususani wananchi wa Kata ya Kiranyi:-
Je, Serikali inawafikiriaje wananchi hawa ambao sheria imewakuta kwenye maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gibson Blasius Ole-Meiseyeki, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kata ya Kiranyi na Olorien hutegemea kupata maji katika chanzo cha Sailoja katika Halamshauri ya Wilaya ya Arusha. Chanzo hiki kinahudumia sehemu ya Mamlaka ya Mji mdogo wa Ngaramtoni kwa ajili ya matumizi ya maji ya wakazi wa Mji huo na viunga vyake katika Jimbo la Arumeru Magharibi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Arusha imefanya utambuzi wa nyumba na mali zilizopo ndani ya chanzo cha maji cha Sailoja katika Kata ya Karanyi. Halmashauri inakusudia kukaa na watu ambao wamo ndani ya chanzo. Aidha, utambuzi wa awali umebainisha jumla ya Kaya 120 zimetambuliwa kwenye eneo la chanzo hicho cha maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Halmashauri ina mpango wa kukutana na wananchi ambao wamebainika kuwa katika chanzo hicho cha maji ili kufanya mazungumzo ya pamoja ya namna ambavyo utaratibu utakavyokuwa kwa kuzingatia sheria na miongozo iliyopo. Ofisi yangu itasimamia zoezi hili ili kuhakikisha kwamba sheria, kanuni na taratibu zinazingatiwa wakati wa kunusuru chanzo hiki.
MHE. GIBSON B. MEISEYEKI aliuliza:-

Mheshimiwa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete aliahidi ujenzi wa barabara yenye urefu kwa kilomita 12 katika Jimbo la Arumeru Magharibi na sasa imepita miaka 10 bila kutekelezwa ahadi hiyo:-

Je, ni lini sasa Serikali itatekeleza ahadi hiyo hasa ikitiliwa maanani kuwa katika Jimbo la Arumeru Magharibi hakuna barabara ya lami hata nusu kilomita?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gibson Blasius Ole Meiseyeki, Mbunge wa Arumeru Maghari kama ifuatayo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alitoa ahadi ya ujenzi wa barabara ya lami kilomita 12 Arumeru Magharibi mwezi Novemba, 2012 kwenye uzinduzi wa Hospital ya Wilaya ya Oltrumeti.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilikwishaanza utekelezaji wa ahadi hiyo ya Mheshimiwa Rais Msaafu ambapo kati ya mwaka wa fedha 2014/2015 hadi 2017/2018 barabara zenye urefu wa kilomita 3.55 kwa kiwango cha lami zimejengwa Arumeru Magharibi kwa gharama ya shilingi bilioni mbili. Barabara zilizojengwa ni kama ifuatavyo: Mianzini-Timbolo kilomita 0.8; Sarawani-Oldonyosapuk kilomita 0.7; Tribunal Road kilomita 2.5; na Sekei-Olglai kilomita nne (4). Serikali itaendelea kutenga fedha za ujenzi wa barabara hizo kwa kiwango cha lami kwa kadiri fedha zinavyopatikana.