Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Eng. Atashasta Justus Nditiye (63 total)

MHE. ALFREDINA A. KAHIGI aliuliza:-
Wananchi wa Mkoa wa Kagera wanakabiliwa na tatizo kubwa la ukosefu wa usafiri wa meli, jambo ambalo linawasababishia usumbufu mkubwa na usafiri wa mabasi umekuwa na gharama na hatari zaidi.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia usafiri wa meli wananchi hao ili kuwapunguzia gharama pamoja na ajali za mara kwa mara?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, ahsante sana, vilevile nichukue nafasi hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu. Nimshukuru na Rais wangu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniamini na kuniteua kuweza kumsaidia. Lakini vilevile nikushukuru kwa ushirikiano pamoja na Wabunge wote, ambao mmeendelea kunipa katika kipindi ambacho nilitumika kama Mwenyekiti wa Kamati na Mbunge.
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mheshimiwa Alfredina Apolinary Kahigi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, huduma za usafiri katika Ziwa Victoria kati ya Mwanza na Bukoba zilisimama mwezi Machi, 2017 baada ya meli ya MV Serengeti kupata hitilafu katika engine na mfumo wa shafti. Serikali imeipatia Kampuni ya Huduma za Meli (MSCL) kiasi cha shilingi milioni 300 kwa ajili ya ukarabati wa meli nne za Ziwa Victoria ikiwemo meli ya MV Serengeti. Matengenezo ya meli hii yamekwishaaza baada ya vifaa vyake kupatikana na yanatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Januari, 2018.
Mheshimiwa Spika, mbali na ukarabati wa MV Serengeti, Serikali kupitia MSCL inatekeleza mradi wa ukarabati mkubwa wa Meli ya MV Victoria. Mzabuni kwa ajili ya kutekeleza kazi hii amekwishapatikana ambaye ni KTMI Company Limited kutoka nchini Korea Kusini. Taratibu za uhakiki (due diligence) wa kampuni hii zinaendelea na mkataba unatarajiwa kusainiwa mwishoni mwa mwezi Novemba, 2017. Matengenezo haya yanatarajiwa kutumia muda wa miezi kumi tangu kusainiwa kwa mkataba.
Mheshimiwa Spika, Serikali pia imekamilisha utaratibu wa kumpata mkandarasi atakayetekeleza mradi wa ujenzi wa meli mpya katika Ziwa Victoria yenye uwezo wa kubeba abiria 1,200 na tani 400 za mizigo. Mkandarasi aliyepatikana ni Kampuni ya STX Shipbuilding and Chipyard Company Limited kutoka nchini Korea Kusini. Utaratibu wa uhakiki wa kampuni hii unaendelea na mkataba wa utekelezaji wa kazi unatarajiwa kusainiwa mwishoni mwa mwezi Novemba, 2017. Utekelezaji wa ujenzi huu utachukua takribani miezi 24 tangu kusainiwa kwa mkataba.
Mheshimiwa Spika, ni matumaini ya Serikali kuwa kukamilika kwa miradi hii mitatu itasaidia kuwaondolea adha ya usafiri wananchi wote watakaokuwa wanasafiri kwa njia ya maji katika Kanda ya Ziwa Victoria wakiwemo wakazi wa Mkoa wa Kagera. Ahsante.
MHE. RHODA E. KUNCHELA aliuliza:-
Ujenzi wa reli ya kati ni hatua inayochukuliwa kuboresha miundombinu katika nchi hii.
Je, Serikali inawasaidiaje wananchi wanaokumbwa na bomoabomoa kupata fidia zao kwa wakati hasa ukizingatia kuwa wananchi wengi ni maskini na hawawezi kumudu gharama za kujenga makazi upya?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kuendeleza mtandao mzima wa reli kwa kiwango cha kimataifa (standard gauge) ukiwa na jumla ya urefu wa kilometa 4,886. Mtandao huu wa reli unajumuisha Ukanda wa Kati ambao una kilometa 2,561 amabao unajumuisha reli ya kutoka Dar es Salam - Isaka – Mwanza (kilometa 1,219), Tabora – Uvinza – Kigoma (kilometa 411), Kaliua – Mpanda – Karema (kilometa 321), Isaka – Rusumo (kilometa 371), Keza – Ruvubu (kilometa 36) na Uvinza – Kalelema kuelekea Msongati (kilometa 203). Ukanda wa Kusini ambao unajumuisha reli ya kutoka Mtwara hadi Mbamba Bay na matawi yake ya kuelekea Liganga kwa ajili ya chuma na Mchuchuma kwa ajili ya makaa ya mawe yenye jumla ya urefu wa (kilometa 1,092) na Ukanda wa Kaskazini ambao unajumuisha reli kutoka Tanga – Arusha – Musoma yenye jumla ya urefu wa kilometa 1,233.
Mheshimiwa Spika, inakadiriwa kuwa asilimia 75 ya njia ya reli mpya itapita katika hifadhi ya reli iliyopo. Wananchi waliopo katika hifadhi ya reli wanapaswa kuondolewa bila kulipwa fidia kwani wamevamia maeneo ya reli. Aidha, zoezi la ubomoaji linaloendelea sasa linalenga kuwaondoa wavamizi wa hifadhi ya reli na maeneo ya uendeshaji yaliyotengwa tangu reli ya kwanza ilipoanza kujengwa kati ya mwaka 1904 na kuendelea.
Mheshimiwa Spika, mpaka sasa hakuna mgogoro wala athari zilizojitokeza katika utwaaji ardhi mpya ili kupisha mradi wa reli ya kisasa kwa sababu usanifu utakaoonyesha wananchi watakaopitiwa unakamilishwa.
Aidha, Kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli (RAHCO) imeajiri Mshauri Mwelekezi kutoka Chuo Kikuu cha Ardhi kwa ajili ya kufanya kazi ya utwaaji wa ardhi na tathmini kwa wananchi watakaolazimika kupisha reli hiyo. Ushirikishwaji wananchi, sheria na taratibu zote za nchi zitafuatwa ipasavyo katika kutekeleza zoezi la fidia, ahsante.
MHE. KAPT. ABBAS ALI MWINYI aliuliza:-
Ndege za Serikali aina ya Fokker 50 iliyoletwa nchini mwaka 1992 na Fokker 28 iliyoletwa nchini mwaka 1978 ni chakavu na teknolojia zake zimepitwa na wakati. Aidha, Kampuni iliyotengeneza aina hizo za ndege imeshafungwa hivyo upatikanaji wa vipuri vya ndege hizo kuwa mgumu na gharama kuwa kubwa.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuzibadilisha ndege hizo na kuleta mpya?
Je, ni lini Serikali itarekebisha hali ya hanger la kuegeshea ndege za Serikali?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimwa Kepteni Abbas Ali Mwinyi, Mbunge wa Fuoni lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli ndege aina ya Fokker 28 na Fokker 50 zina umri mkubwa. Hata hivyo kiutaalamu usalama wa ndege huwa haupimwi kwa miaka iliyonayo bali hupimwa kwa masaa iliyoruka. Hivyo, kwa hali ya kawaida muda wa masaa ya ndege kuwa chakavu (beyond economic benefit) ni masaa 90,000 na kati ya ndege hizi mbili hakuna hata ndege moja yenye masaa zaidi ya 15,000. Aidha, ndege hizo zimekuwa zikifanyiwa matengenezo kwa kuzingatia ratiba.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa ndege ya Fokker 50 ipo kwenye ubora wa kutumika na inaendelea kuhudumia viongozi wetu. Ndege ambayo haitumiki ni Fokker 28 kwa sababu ina matatizo ya breki na engine ya kulia. Serikali imewasiliana na mtengenezaji ili kuweza kutatua matatizo hayo. Ndege hizi mbili bado zina teknolojia ya kisasa na zimekuwa zikipelekwa kwenye matengenezo ya lazima kwa mujibu wa matakwa ya Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Anga (ICAO) na Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA). Kimsingi vipuli vya ndege hizo bado vinapatikana.
Mheshimiwa Spika, Kampuni ya kutengeneza ndege hizi haijafungwa bali wamesimamisha utengenezaji wa ndege mpya na wanaendelea kutoa huduma ya matengenezo (maintenance support) kwa zile ndege ambazo zimekwishawahi kutengenezwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili, Serikali inatambua changamoto za karakana ya kutengeneza ndege za (TGFA) kutokana na uchakavu. Tayari nimeshawaagiza Wakala wa ndege za Serikali TGFA kufanya tathimini ya gharama halisi zitazotumika kwa ajili ya kukarabati Karakana hiyo. Gharama halisi zitakapopatikana, Serikali itafanyia kazi marekebosho ya hanger hilo. Ahsante. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI (K.n.y. MHE. DKT. DAVID M.
DAVID) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itapeleka mawasiliano ya simu za mkononi katika kata za Jimbo la Same Magharibi hususani Kata za Msindo, Mshewa, Mhuzi, Vumari, Vuudee, Tae, Suji, Gavao, Saweni na Ruvu Jiungeni?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. David Mathayo David, Mbunge wa Same Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Vijiji vya Kata za Vumari, Suji na Ruvu Jiungeni vitafikishiwa huduma ya mawasiliano kupitia utekelezaji wa mradi wa Kampuni ya Simu ya Viettel. Utekelezaji wa mradi chini ya Kampuni ya Viettel unapaswa kukamilika mwezi huu wa Novemba, 2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Vijiji vya Kata za Mhezi, Msindo, Mshewa, Vuudee, Tae, Gavao na Saweni vinafanyiwa tathmini na Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote na vitaingizwa katika orodha ya miradi ya mfuko itakayotekelezwa kulingana na upatikanaji wa pesa.
MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza:-
Katika Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro, ipo karakana ya kutengeneza ndege (hangar) ambayo ilijengwa na Serikali ya Uholanzi, lakini sasa hivi haitumiki.
(a) Je, ni lini Serikali itafufua karakana hiyo ili ndege zetu za Bombardier na nyingine ziweze kufanyiwa matengenezo hapo?
(b) Je, ni nani mmiliki wa uwanja huo wa ndege?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE): alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo, Mbunge wa Viti Maalum, lenye Sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, karakana ya kutengeneza ndege ya KIMAFA iliyopo Kiwanja cha Ndege cha Kilimanjaro kwa sasa inaendeshwa na kusimamiwa na Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL).
Mheshimiwa Naibu Spika, Karakana hiyo ilijengwa mwaka 1980 na kukabidhiwa rasmi kwa Serikali mwaka 1985 na ina uwezo wa kuhudumia ndege kubwa aina ya B747’S au ndege tano aina ya B737’S kwa wakati mmoja. ATCL inaendelea kuifanyia matengenezo karakana hiyo ili iweze kurudi kwenye ubora wake na kutoa huduma za matengenezo ya ndege.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KIA) ni kati ya viwanja 59 vinavyomilikiwa na Serikali chini ya usimamizi wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Kiwanja hiki kinaendeshwa na Kampuni ya Uendeshaji wa Viwanja vya Ndege ya Kilimanjaro (Kilimanjaro Airports Development Company – KADCO) ambayo inamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100. Aidha, taratibu za kuunganisha KADCO na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA) ili kuwa na taasisi moja inayosimamiwa na viwanja vya ndege nchini zinaendelea na zinatarajiwa kukamilika kabla ya mwisho wa mwaka huu 2018.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB aliuliza:-
Utaratibu wa kuingiza mafuta nchini unaosimamiwa na Petroleum Bulk Procurement Agent (PBPA) kwa mfumo wa Bulk Procurement System, wakala hukusanya mahitaji kutoka kwa makampuni ya ndani na nje ya nchi lakini kampuni zote zikiweko zile zinazopeleka mafuta nje ya nchi zinalipa Dola za Marekani tatu hadi nne kwa tani kwa mafuta yanayopitia transit ya Dar es Salaam isipokuwa mafuta yanayopelekwa Zanzibar ambayo hutozwa Dola za Marekani 10 kwa tani.
(a) Je, ni utaratibu gani unaotumika kutoa nafuu ya malipo ya Wharfage kwa kampuni za nje zinazopitisha mafuta Dar es Salaam na kuitoza Zanzibar malipo makubwa?
(b) Mafuta yanayopitishwa transit ya Dar es Salaam kwenda Zanzibar yanalipiwa aina zote za ushuru, je, Serikali haioni kuwa inawabebesha wananchi gharama kubwa ya ununuzi wa mafuta kuliko nchi nyingine?
(c) Je, ni hatua gani Serikali inachukua katika kuhakikisha mafuta yanayopita transit ya Dar es Salaam yanalipwa kama mafuta mengine yanayopita transit ya bandari hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jaku Hashimu Ayoub, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu unaotumika kupanga tozo za bandari hautoi upendeleo kwa upande wowote. Tozo hizo zimewekwa kwa kuzingatia gharama za kutoa huduma, hali ya soko na umuhimu wa kuvutia shehena ya nchi jirani ili kutekeleza sera ya uchumi wa kijiografia na kufanya bandari ya Dar es Salaam kuwa kitovu yaani hub ya usafirishaji. Ushindani wa shehena ya mafuta ni mkali sana (cut throat competition) kwa bandari za TPA hususani Dar es Salaam na bandari za nchi jirani za Kenya, Msumbiji, Afrika Kusini, Namibia na Angola.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kutokana na hali ya soko (market place exigencies), tozo za bandari kwa shehena ya nchi ya jirani hutofautishwa na shehena ya ndani ya nchi ili kuvutia shehena nyingi kuhudumiwa na bandari ya Dar es Salaam. Kwa hivi sasa gharama ya Wharfage kwa shehena ya Tanzania ya kupakuliwa (imports) ni asilimia 1.6 ya thamani ya mzigo ulioidhinishwa na TRA na kwa kiwango cha chini kilichowekwa cha Dola za Marekani 10 kwa tani moja.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania Bara na Zanzibar ni nchi moja na kwa hiyo shehena yoyote iendayo Zanzibar ikiwa ni pamoja na shehena ya mafuta hutambuliwa kama ni shehena ya nchini (local cargo) na sio shehena ya nchi jirani yaani transit. Kwa mantiki hii, tozo zinazotumika ni tozo za shehena ya ndani (local cargo) ambayo ni sawa kwa Bara na Zanzibar.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia majibu ya (a) na (b) hapo juu ni dhahiri kwamba matumizi ya tozo ni miongoni mwa mikakati maalum ya kibiashara na masoko kwa ajili ya kuvutia shehena za nchi jirani ambazo huleta faida ya uchumi na kijamii hapa nchini (multiplier effect) siyo tu kwa bandari bali kwa wadau wote wa bandari na wananchi kwa ujumla.
MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH aliuliza:-
Baadhi ya maeneo katika Kisiwa cha Pemba yamekuwa na tatizo la kukosa mawasiliano ya simu kwa mitandao ya Tigo, Airtel na Zantel hali ambayo imekuwa ikisabbisha usumbufu.
Je, Serikali inatoa kauli gani kwa vile tatizo hili ni la muda mrefu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maida Hamad Abdallah, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jukumu la Serikali kupitia Mamlaka ya Mawasiliano, Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote na watoa huduma za mawasiliano kuhakikisha kuwa huduma bora za mawasilino nchini zinawafikia wananchi wote kwa kuhakikisha inatatua changamoto mbalimbali za kiufundi na kiutendaji. Kwa mujibu wa takwimu za Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote, Kisiwani Pemba kuna jumla ya minara saba ya Airtel, minara tisa ya Tigo, minara tisa ya Vodacom, minara 24 ya Halotel na minara 47 ya Zantel.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, minara hiyo imejengwa katika Kata zifuatazo: Kata za Kisiwa Panza, Muambe, Kangani, Stahabu, Kengeja, Jombwe, Kendwa, Mtambile, Ng’ombeni, Uweleni, Mtangani, Chambani, Ukutini, Ngwachani, Chumbageni, Mizingani, Kilindi, Pujini, Mvumoni, Kibokoni, Mgogoni, Kichungwani, Wara, Tibirinzi, Mkoroshoni, Ndagoni, Michungwani, Ngw’ambwa, Ziwani, Ole, Kiuyu Minungwini, Mtambwe Kusini, Piki, Mtambwe Kaskazini, Pandani, Limbani, Jadida, Utaani, Selem, Finya, Wingwi, Kinyasini, Junguni, Gando, Chimba, Kojani, Chwale, Konde, Makangale, Tumbe Magharibi, Kiuyu Mbuyuni na Kata ya Majenzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa takwimu hizi, tunaamini kuwa Kisiwa cha Pemba kinapata huduma nzuri ya mawasiliano kutoka kwa watoa huduma. Hata hivyo, kulingana na jiografia ya Pemba, baadhi ya maeneo yanaweza kupata shida ya kupata huduma kwa uhakika na mfuko utawasiliana na watoa huduma wakiwemo Zantel, Airtel, Tigo, Halotel na Vodacom ili kuona ni jinsi gani maeneo yote yenye changamoto hizi yanapata huduma nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, namwomba Mheshimiwa Mbunge kama ana majina ya vijiji hivyo vyenye shida ya mawasiliano, anikabidhi ili tuvifanyie kazi mara moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kutupatia taarifa hizi na pia naomba nimhakikishie kwamba Wizara yangu itaendelea kufanyia kazi changamoto za Mawasiliano katika maeneo mbalimbali ikiwemo Pemba.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-
Serikali imefanya kazi kubwa kujenga mtandao wa barabara za kiwango cha lami nchini, kipindi cha nyuma
barabara kuu zilikuwa zinawekwa matuta ili kudhibiti ajali, lakini hivi karibuni Serikali imefuta utaratibu wa kuweka matuta kwenye barabara hizo na hivyo kuwa chanzo kikubwa cha ajali zinazosababisha majeruhi, ulemavu na vifo. Kwa mfano, eneo la Buigiri, Wilaya Chamwino lina ajali nyingi kutokana na barabara kukosa matuta.
(a) Je, Serikali haioni kuwa kuna umuhimu wa kurejesha utaratibu wa kuweka matuta kwenye barabara?
(b) Kama utaratibu wa matuta hauwezekani, je, Serikali haioni kuwa kuna haja ya kuyaondoa matuta yote kwenye barabara kuu ili kuondoa malalamiko ya wananchi kwa viongozi wao kwenye maeneo ambayo hayana matuta?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Mwakanyaga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijatoa majibu ya swali namba 61 la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga Mbunge wa Chilonwa, lenye sehemu (a) na (b) napenda kutoa maelezo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kuboresha usalama barabara na kurekebisha sehemu hatarishi kwenye barabara kuu na barabara za mikoa nchi nzima ikiwemo barabara ya Morogoro - Dodoma eneo la Buigiri ili kupunguza ajali za barabarani. Hatua zilizochukuliwa na Serikali kupunguza ajali za barabarani ni pamoja na kuweka au kurudisha alama zote muhimu za barabarani ikiwemo za kudhibiti mwendo, kuweka michoro ya barabarani na kurekebisha kingo za madaraja zilizoharibika, uwekaji wa matuta na kadhalika kama ilivyokuwa ikifanya kipindi kilichopita.
Katika mwaka wa fedha 2017/2018 TANROADS itaendelea kuweka vivuko vya watembea kwa miguu (zebra crossing) na alama zote muhimu nchini pale tutakapohitaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kutoa maelezo ya awali napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga Mbunge wa Chilonwa, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli ajali za barabarani zina sababisha majeruhi, ulemavu na vifo kwa watu wetu ikiwa ni pamoja na kusababisha hasara kubwa kiuchumi kwa Taifa letu. Moja ya njia ambayo Serikali imekuwa ikitumia kupunguza ajali kwenye baadhi ya sehemu ni kuweka matuta ya barabarani. Hata hivyo, napenda kulieleza Bunge lako Tukufu kuwa, kiutaalam hairuhusiwi kuweka matuta kwenye barabara kuu. Aidha, matuta yaliyowekwa katika barabara kuu yaliwekwa kwa lengo la kupunguza ajali za barabarani kama njia ya mpito. Wizara inafanya utafiti kupata njia mbadala ya kupunguza ajali kabla ya uondoshaji wa matuta hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa mpito, Serikali inaendelea kurekebisha matuta ambayo yalijengwa bila kuzingatia viwango vilivyomo kwenye Mwongozo wa Wizara wa Usanifu wa Barabara (Road Geomentric Manual ya 2011) kulingana na upatikanaji wa fedha.
Aidha, inapobainika kuwa kuna haja ya kuweka matuta kwenye barabara, matuta hayo yatawekwa kulingana na viwango vilivyoainishwa kwenye mwongozo huu.
MHE. MUSSA B. MBAROUK aliuliza:-
Tanga kuna uwekezaji wa bomba la mafuta toka Hoima - Chongoleani, viwanda mbalimbali vya saruji, vivutio vya utalii vya Amboni Caves, Magofu ya Tongoni na Saadani National Park:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga kiwanja cha ndege kikubwa na cha kisasa katika Jiji la Tanga?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Bakari Mbarouk, Mbunge wa Tanga Mjini ambaye anapendwa sana na wapiga kura wake kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kiwaja cha ndege cha Tanga ni miongoni mwa viwanja 11 nchini vilivyofanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa kugharamiwa na Benki ya Dunia kupitia mradi wa Transport Sector Support Project. Viwanja vingine vilivyofanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ni Lake Manyara, Musoma, Iringa, Songea, Kilwa Masoko, Lindi, Moshi, Njombe, Simiyu na Singida.
Mheshimiwa Naibu Spika, usanifu huu ulikamilika mwezi Juni, 2017 na ulihusisha usanifu wa miundombinu ya viwanja hivi kwa ajili ya upanuzi na ukarabati ili kukidhi mahitaji ya sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeanza majadiliano na Benki ya Dunia ili kupata mkopo wa kugharamia ukarabati na upanuzi wa baadhi ya viwanja hivi kwa kuzingatia mapendekezo ya report ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ambao ulizingaia mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na ukuaji wa shughuli za uchumi, utalii na mahitaji ya usafiri wa anga. Katika upembuzi yakinifu na usanifu wa kina huo, kiwanja cha ndege cha Tanga ni miongoni mwa viwanja vilivyopewa kipaumbele kwa mahitaji ya ukarabati hivyo katika majadiliano ya awali, Benki ya Dunia imeonesha nia ya kugharamia ukaratabi wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi unaopendekezwa utahusisha mradi wa barabara ya kuruka na kutua ndege pamoja na barabara ya kiungio kwa kiwango cha lami. Ukarabati wa maeneo ya maegesho ya ndege, ujenzi wa jengo kubwa la kisasa la abiria pamoja na miundombinu yake, usimikaji wa taa pamoja na mitambo ya kuongozea ndege. Baada ya ukarabati unaopendekezwa kiwanja kitakuwa na uwezo wa kuhudumia ndege aina ya ATR 72 yenye uwezo wa kubeba abiria 70 au ndege za kufanana na hiyo na kitaweza kutumika kwa saa 24.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa majadiliano kati ya Serikali na Benki ya Dunia yanaendelea yakiwemo mapitio ya awali ya report za miradi inayopendekezwa pamoja na maandalizi ya taarifa mbalimbali zinazohitajika kabla ya mkataba wa mkopo kusainiwa na baadae kutangazwa zabuni.
MHE. MATTAR ALI SALUM aliuliza:-
Usafiri wa kutumia bandari ni usafiri muhimu sana na ni wa lazima kwa watu wanaotoka Tanzania Bara kwenda Unguja na Pemba; na zipo kampuni zinazotoa huduma ya usafirishaji lakini hazitoshelezi katika kutoa huduma hiyo muhimu.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kununua meli ili kukidhi mahitaji ya usafirishaji wa watu wetu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mattar Ali Salum, Mbunge wa Shaurimoyo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba usafiri wa kutumia bandari ni usafiri muhimu sana na hutumiwa na watu wengi wanaoishi maeneo ya mwambao wa Bahari ya Hindi hususan wanaotoka Tanzania Bara kwenda Unguja na Pemba. Ni kweli pia kampuni zinazotoa huduma ya usafirishaji katika maeneo hayo hazitoshelezi katika kutoa huduma hiyo muhimu kulingana na uhitaji wa abiria.
Mheshimiwa Naibu Spika, uwepo wa mahitaji ya huduma za usafiri wa majini katika maeneo hayo kwetu ni fursa kwa sekta binafsi nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kulitambua hilo Serikali imekuwa ikijenga mazingira wezeshi na kuihamasisha sekta binafsi kutoa huduma za usafiri kwa kutumia meli za kisasa kati ya wasafiri wanaotoka Tanzania Bara au kwingineko kwenda visiwa vya Unguja na Pemba.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ujumla juhudi za Serikali zimekuwa zikilenga katika kuhakikisha kuwa wakazi wa maeneo ya mwambao na visiwa vya Unguja na Pemba wanapata huduma za usafiri kwa njia ya maji zilizo salama na hivyo kuwaepusha kutumia vyombo vya usafiri huo visivyokidhi matakwa katika kubeba abiria na mizigo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na uhamasishaji huo, kwa sasa kampuni ya meli ya Azam ilianza kutoa huduma ya usafiri baina ya Tanga, Unguja na Pemba kuanzia tarehe 29 Januari, 2017 kwa kutumia meli ya kisasa iitwayo Azam Sealink 2. Meli hii inatoa huduma kutokea Tanga kuelekea visiwa vya Unguja na Pemba mara moja kwa wiki. Aidha, kampuni hiyo iko tayari kuongeza safari baina ya Tanga, Unguja na Pemba kwa wiki mara itakapobainika kuwa abiria wanaosafiri katika maeneo hayo wameogezeka.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaipongeza Kampuni ya Meli ya Azam kwa kuitikia wito wa kuanzisha huduma ya usafiri kwa njia ya maji baina ya Tanga, Unguja na Pemba na kuwataka wananchi kuepuka kutumia vyombo vya usafiri wa maji visivyokidhi matakwa katika kubeba abiria na mizigo.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kutumia nafasi hii kuendelea kutoa wito kwa wawekezaji wengine kama ilivyo kwa Kampuni ya Meli ya Azam kuwekeza katika vyombo vya kisasa vya usafiri kwa njia ya maji ili kutoa huduma ya usafiri katika maeneo ya mwambao ya Tanzania ikiwamo na Visiwa vya Unguja na Pemba. (Makofi)
MHE. ANTHONY C. KOMU (K.n.y. MHE. ZITTO Z. R. KABWE) aliuliza:-
Mnamo tarehe 26 Julai, 2017, Mawaziri wa Uchukuzi wa Uganda, Burundi, Congo DRC na Tanzania walifanya mkutano katika Manispaa ya Ujiji-Kigoma na kuazimia kuwa kuanzia Januari, 2018, Bandari ya Kigoma itakuwa bandari ya mwisho kwa bidhaa ya Burundi na Mashariki ya DRC (Kigoma Port of Destination CIF Kigoma). Pamoja na Azimio hilo, mradi wa Bandari ndogo za Ujiji na Kibirizi zilipaswa kujengwa na kuiwezesha miradi kama ya Ujiji City-Great Lakes Trade and Logistics Centre:-
Je, Serikali mpaka sasa imefikia hatua gani ya kiforodha na kibandari kuiwezesha CIF-Kigoma?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kabwe Ruyagwa Zitto, Mbunge wa Kigoma Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba katika Mkutano wa Mawaziri wa Uchukuzi wa Uganda, Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Tanzania waliazimia kuwa kuanzia Januari, 2018 Bandari ya Kigoma itakuwa Bandari ya mwisho kwa bidhaa za Burundi na Mashariki ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo yaani Kigoma Port of Destination.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kuwa bandari hii pia ni muhimu sana kwa uchumi na ustawi wa Mkoa wa Kigoma na ndiyo inategemewa na wananchi wa Mkoa wa Kigoma na Mikoa ya jirani katika utaoji wa huduma ya usafirishaji wa bidhaa zinazopitia reli ya kati kutoka bandari ya Dar es Salaam kwenda nchi jirani za Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo tena kwa gharama nafuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kulitambua hili, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari - Tanzania katika mwaka wa fedha 2017/2018 imetenga fedha kwa ajili ya kuendeleza Bandari ndogo za Ujiji na Kibirizi ili zikikamilika ziwezeshe miradi kama vile Ujiji City –Great Lakes Trade and Logistics Centre. Zabuni za kumpata mkandarasi wa ujenzi wa bandari hizi zilitangazwa. Hata hivyo, kwa bahati mbaya hakuna mzabuni hata mmoja aliyejitokeza kuomba kazi hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Machi, 2018, TPA imetangaza upya zabuni hizo Kimataifa ili kumpata mzabuni atakayefanya kazi za upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na athari za kimazingira. Zabuni hizo zimefunguliwa tarehe 3 Aprili, yaani juzi na jumla ya makampuni 21 yameonyesha nia ya kufanya kazi hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa kazi inayoendelea ni kufanya tathmini ya wazabuni ili kumpata mzabuni anayefaa kufanya kazi hiyo. Ni matarajio yetu kuwa kazi itaanza mara baada ya kumalizika kazi ya tathmini na kumpata mkandarasi wa kufanya kazi hiyo na hivyo kunyanyua kiwango cha utendaji wa Bandari ya Kigoma.
MHE. JUSTIN J. MONKO aliuliza:-
Barabara ya Singida - Ilongero - Mintiko hadi Haydom inayounganisha Mikoa ya Singida na Manyara ni kiungo muhimu katika kusafirisha mazao ya wakulima na bidhaa za wafanyabiashara na inapita katika Hospitali ya Rufaa ya Haydom ambayo wananchi hufuata huduma kwa kukosa Hospitali ya Serikali katika Halmashauri.
Je, ni lini barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami ili kunusuru maisha ya wananchi wa Singida Kaskazini?
NAIBU WAZIRI UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Justin Joseph Monko, Mbunge wa Singida Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Singida – Ilongero – Mtinko - Nkugi na Kidarafa hadi Haydom ni barabara ya mkoa yenye urefu wa kilometa 93.4 ambapo kilometa 84.36 zipo mkoani Singida na kilometa 9.04 zipo katika mkoa wa Manyara. Barabara hii inahudumiwa na Wakala wa Barabara nchini (TANROADS).
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa barabara hii kwa wananchi wa Mikoa ya Singida na Manyara kwa ajili ya usafirishaji wa abiria, mazao, bidhaa za biashara na pia wananchi wanaokwenda kupata huduma ya matibabu katika hospitali ya Haydom. Hivyo kwa umuhimu huo Serikali imekuwa ikiifanyia matengenezo ya aina mbalimbali barabara hii kila mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2017/2018 barabara hii ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni 2.246 kwa ajili ya matengenezo mbalimbali. Aidha, Serikali imejenga jumla ya kilometa 8 kwa awamu kwa kiwango cha lami kuanzia Singida Mjini kuelekea Ilongero na jumla ya kilometa tano za barabara hii zimepangwa kujengwa kwa kiwango cha lami katika mwaka wa fedha 2018/2019.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa kipaumbele cha Serikali ni kuunganisha kwa barabara za kiwango cha lami makao makuu ya mikoa na nchi jirani na baadae barabara za mikoa zitafuata.
MHE. DKT. DAMAS D. NDUMBARO aliuliza:-
Serikali ya Awamu ya Tano imeusaidia sana Mji wa Songea kwa kuleta ndege za Bombadier ambazo zinatoa huduma zake katika Uwanja wa Ndege wa Songea.
• Je, kwa nini uwanja huo hauongezwi urefu na kufanyiwa ukarabati ili kutoa huduma zaidi na kuruhusu ndege ziweze kutua kwa saa 24?
• Je, kwa nini Serikali haiweki mashine za ukaguzi wa abiria (scanning machine) ili kuondoa adha kwa abiria kukaguliwa mizigo yao kwa kupekuliwa ambapo inadhalilisha na kupoteza muda?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Damas Daniel Ndumbaro, Mbunge wa Songea Mjini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kiwanja cha Ndege cha Songea ni miongoni mwa viwanja 11 nchini vilivyofanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa ufadhili wa Benki ya Dunia kupitia mradi wa Transport Sector Support Project. Usanifu huu ulikamilika mwezi Juni, 2017 na ulihusisha usanifu wa miundombinu ya viwanja hivi kwa ajili ya upanuzi na ukarabati ili kukidhi mahitaji ya viwanja hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi sasa Wizara yangu, kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), inaendelea na taratibu za kumpata Mkandarasi pamoja na Mhandisi Mshauri kwa ajili ya kazi za awamu ya kwanza za upanuzi na ukarabati wa kiwanja cha ndege cha Songea, ambazo zitahusisha ukarabati wa barabara ya kutua na kuruka ndege, barabara za viungio, maegesho ya ndege, kusimika taa pamoja na mitambo ya kuongozea ndege, hivyo kuruhusu ndege kuruka na kutua kwa saa 24.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Wizara kwa kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), imenunua mashine za ukaguzi wa abiria na mizigo kwa ajili ya viwanja vya ndege vya Dar es Salaam, Mwanza, Dodoma na Songea na tayari mashine hizo zimepelekwa katika viwanja husika, kikiwemo kiwanja cha ndege cha Songea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa mafundi wanaendelea na zoezi la kufunga mashine hizo ambapo tunatarajia ifikapo katikati ya mwezi huu wa Aprili, 2018, kazi ya kufunga mashine hizo itakuwa imekamilika na hivyo mashine hizo kuanza kutumika katika viwanja hivyo, kikiwemo Kiwanja cha Songea.
MHE. FREDY A. MWAKIBETE aliuliza:-
Hapa nchini kumekuwepo na ukuaji na utumiaji wa mifumo mingi mipya ya teknolojia kwa ukusanyaji wa kodi na malipo mengine kwa njia ya mtandao (electronic):-
(a) Je, Serikali imejipangaje kukabiliana na wizi wa kimtandao kwa wananchi?
(b) Je, Serikali haioni umuhimu wa kuundwa kwa Bodi ya wana TEHAMA nchini ili kuwa na udhibiti na ufanisi wa watumiaji wa mitandao nchini wanataaluma wa TEHAMA waweze kuwa na Bodi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fredy Atupele Mwakibete, Mbunge wa Busokelo, lenye sehemu
(a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Serikali imechukua hatua kadhaa kwa ajili ya kuweka mazingira salama kwa wananchi hususani kwenye mitandao kama ifuatavyo:-
(i) Mwaka 2015 ilitungwa Sheria ya Makosa ya Mtandao na Sheria ya Miamala ya kielektroniki kwa lengo la kutambua miamala inayofanyika kimtandao pia kutambua makosa yanayofanyika kwenye mtandao ili kuweza kuchukua hatua stahiki yanapobainika makosa hayo.
(ii) Kimeanzishwa kitengo cha uhalifu wa mitandao chini ya Jeshi la Polisi kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa makosa ya mitandao ikiwemo wizi kwenye mitandao na kuandaa majalada ya kufungulia mashtaka kwa kusaidiana na Kurugenzi ya Mwendesha Mashtaka wa Serikali.
(iii) Kupitia Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta kimeanzishwa kitengo cha uratibu, ufuatiliaji na usimamizi wa matukio yanayotokea kwenye anga ya mtandao TzCERT. Kitengo cha TzCERT kinashirikiana kwa ukaribu na taasisi mbalimbali kama vile sekta ya fedha, mawasiliano, nishati , uchukuzi na jamii. Pia kinashirikiana na taasisi za kiintelijensia na kuhakikisha anga ya mtandao inakuwa salama.
(iv) Imeandaliwa mikakati ya Taifa ya usalama wa mitandao ambao unaweka bayana muundo wa Serikali kukabiliana na uhalifu wa mitandao.
(v) Mwisho elimu kwa umma imeendelea kutolewa.
(b) Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kuwa matumizi ya TEHAMA nchini yemeongezeka ikiwa ni sambasamba na ukuaji wa sekta ya TEHAMA kama mojawapo ya sekta zinazokuwa kwa kasi. Kwa kutambua changamoto ya kutotambuliwa kwa wataalam wa TEHAMA nchini Serikali imefanya yafuatayo:-
(i) Sera ya Taifa ya TEHAMA ya mwaka 2016 ambayo inaatamka kuwepo kwa mfumo wa kuwatambua na kuwaendeleza wataalam wa TEHAMA ili kuwa na rasilimali watu ya kutosha nchini ambayo inazingatia maadili na yenye uwezo wa kufanikisha jitihada za TEHAMA katika kujenga jamii maarifa na;
(ii) Kwa tamko la Rais la mwezi Novemba 2015 imeanzishwa Taasisi ya Tume ya TEHAMA (ICT Commission) ikiwa na lengo kuu la kukuza TEHAMA ambapo moja ya majukumu yake ni kusajili, kusimamia na kuendeleza utaalam wa wataalam wa TEHAMA nchini.
MHE. JOHN P. KADUTU aliuliza:-
Jimbo la Ulyankulu linakabiliwa na tatizo la mawasiliano ya simu hasa katika Vijiji vya Ibambo, Mwongozo, Ichemba, Kanoge, Ilege, Busanda, Bulela, Ikonongo, Igombemkulu na maeneo mengine mengi:-
Je, ni lini kampuni za simu zitamaliza tatizo la mawasiliano katika Jimbo la Ulyankulu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John Peter Kadutu, Mbunge wa Ulyankulu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iliingia Makubaliano na Kampuni ya Mawasiliano ya Vietel ya Vietnam (Halotel) kufikisha huduma ya mawasiliano katika maeneo mbalimbali nchini Tanzania yasiyokuwa na mvuto wa kibiashara ikiwa ni pamoja na maeneo ya Vijiji vya Ibambo, Mwongozo, Ilege, Bulela na Ikonongo. Utekelezaji wa kuleta mawasiliano ya simu kwa miradi hiyo umekamilika ambapo minara imejengwa katika Vijiji vya Ibambo, Keza na King’wangoko. Hata hivyo, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote itahakikisha maeneo yote yanapata huduma hiyo muhimu kama inavyotakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Vijiji vya Lihemba, Kanoge, Busanda na Igombemkulu vitaainishwa na kuingizwa katika orodha ya miradi ya kuwapatia mawasiliano inayosimamiwa na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote itakayotekelezwa siku za usoni kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA aliuliza:-
Kumekuwa na kero kubwa kwa wananchi wanaotumia huduma za Cable TV hasa Dodoma Cables; wananchi wanalipia lakini hawapati huduma ipasavyo:-
Je, ni lini Serikali itawadhibiti na kwa namna gani baadhi ya Service Providers kama hawa ambao wamekuwa wakiwadhulumu wananchi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asha Abdullah Juma, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imetoa leseni ya kutoa huduma za Cable kwa kituo cha Dodoma Cables ambapo kinatakiwa kiendeshwe kwa kufuata sheria na kanuni zinazohusu masuala ya utangazaji. Ili kukidhi ubora wa huduma za cable, TCRA imekuwa ikifuatilia maudhui na inafanya ukaguzi wa mara kwa mara kwenye vituo hivi kuangalia kama mitambo inakidhi vigezo vya utoaji wa huduma bora na ya uhakika kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyeki, kwa kuwa suala la Cable TV linahusu kuwepo kwa mtandao wa waya kutoka kwa mtoa huduma (cable operator) kwenda kwa wananchi, kuna wakati kumekuwa na changamoto za kukatika kwa nyaya ambapo wananchi wanapaswa kutoa taarifa kwa mtoa huduma ili apate msaada wa kiufundi pindi anapokuwa hapati huduma za matangazo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, TCRA imeweka mfumo wa kupokea malalamiko ambapo kama mwananchi atakuwa hapati huduma bora na stahiki anatakiwa kutoa taarifa kwa mtoa huduma na pindi asipopatiwa huduma kama alivyoahidiwa na mtoa huduma, mwananchi anatakiwa kupeleka malalamiko yake katika Ofisi za Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania ambayo kawaida huyapokea na kuyafanyia kazi ili kulinda maslahi ya wananchi na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na stahiki kwa malipo waliyotoa kwa mtoa huduma.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA aliuliza:-
Maeneo mengi ya Wilaya ya Kaliua hayana mawasiliano ya simu ya uhakika:-
Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kupeleka mawasiliano ya simu katika Jimbo la Kaliua kwenye Vijiji vya Mpanda Mlohoka, Usimba, Mwamashimba, Usinga, Kakoko, Ibumba, Kombe, Shela, Mkuuyuni n.k.?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Magdalena Hamis Sakaya, Mbunge wa Kaliua, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli maeneo mengi ya Wilaya ya Kaliua hayana mawasiliano ya simu ya uhakika na Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote imekwishaviainisha vijiji vya Mpanda Mlohoka, Kakoko, Usinga, Kombe, Shela na Ushimba kwa kuangalia mahitaji halisi ya kufikisha huduma ya mawasiliano ikiwemo idadi ya wakazi, ukubwa wa eneo pamoja na jiografia ya vijiji husika. Baada ya kuviainisha vijiji hivyo, Mfuko wa Mawasiliano umeingiza mahitaji ya vijiji husika katika orodha ya vijiji vinavyotarajiwa kupatiwa huduma ya mawasiliano katika zabuni itakayotangazwa mwezi Juni, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Vijiji vya Mwamashimba, Ibumba na Mkuyuni vitaingizwa katika miradi kwa kadri ya upatikanaji wa fedha hususani kwa mwaka wa fedha 2018/2019.
MHE. WILFRED M. LWAKATARE aliuliza:-
Kufuatia kuzama kwa Meli ya MV Bukoba, kuharibika kwa Meli za MV Victoria na MV Serengeti ambazo zilikuwa zikitoa huduma ya usafirishaji abiria na mizigo kati ya Mwanza na Bukoba kwa gharama nafuu katika Mkoa wa Kagera:-
(a) Je, ni lini Meli za MV Victoria na MV Serengeti zitamalizika kufanyiwa matengenezo yenye viwango vya uhakika ili zianze kutoa huduma?
(b) Je, ni lini ahadi ambazo zilianza kutolewa na Serikali ya Awamu ya Tatu tangu kuzama kwa MV Bukoba za kununuliwa kwa meli mpya zitatelekezwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. Eng.ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Wilfred Muganyizi Lwakatare, Mbunge wa Bukoba Mjini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua adha ya usafiri kwa njia ya maji wanayoipata wananchi wa Mwambao wa Ziwa Victoria, hususani wakazi wa Mwanza na Bukoba kutokana na Meli za MV Victoria na MV Serengeti kusitisha kutoa huduma kwa maeneo hayo kutokana na sababu mbalimbali, ikiwemo uchakavu hasa kwa Meli ya MV Victoria na hitilafu ya mitambo kwa MV Serengeti ilivyovipata vyombo hivyo vya usafiri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kulitambua hilo, Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ilitenga fedha katika Bajeti ya Mwaka 2017/2018 ya shilingi bilioni 24.496 kwa ajili ya ununuzi wa meli mpya mbili na ukarabati wa meli tano za Kampuni ya Huduma za Meli (MSCL) ikiwemo Meli za MV Victoria na MV Serengeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukarabati wa Meli za MV Victoria na MV Butiama, unatarajiwa kutekelezwa na Kampuni ya KTMI kutoka nchini Korea ikishirikiana na Yuko’s Enterprises Company Limited wakati wowote kuanzia sasa baada ya kusainiwa kwa mkataba wa utekelezaji wa mradi huo. Matengenezo haya yanatarajiwa kuchukua miezi kumi tangu kusainiwa kwa mkataba.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, zabuni ya ukarabati wa MV Serengeti ilitangazwa tarehe 25 Aprili, 2018 na inatarajiwa kufunguliwa tarehe 24 Mei, 2018. Uchambuzi wa kina utafuata mara baada ya ufunguzi wa zabuni hiyo ili tuweze kumpata mzabuni sahihi mapema iwezekanavyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa meli moja mpya katika Ziwa Victoria, zabuni za kumpata Mkandarasi wa kujenga meli hiyo ziligawanywa kwa makampuni makubwa mbalimbali ya ujenzi wa meli duniani ambapo kampuni zenye uwezo zilionesha nia ya kujenga meli katika Ziwa Victoria kwa vigezo vya Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mchakato wa kumpata mzabuni, tarehe 10 Aprili, 2018, Kampuni ya STX Engine Company Limited na STX Offshore & Shipbuilding Company Limited Joint Venture zilishinda zabuni ya ujenzi wa meli hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, kutokana na sababu mbalimbali, Serikali na kampuni hizi hazikufikia makubaliano ya mwisho na hivyo kushindwa kutia saini mkataba wa utekelezaji wa mradi na hivyo kulazimika kusitisha zabuni hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilitangaza tena zabuni hiyo tarehe 24 Aprili, 2018 na inatarajiwa kufunguliwa tarehe 24 Mei, 2018.
MHE. OTHMAN OMAR HAJI aliuliza:-
Pamoja na Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kuwa na uchakavu wa mitambo ya kuongezea ndege na miundombinu duni ya usafiri wa anga nchini, TCAA imechaguliwa kuwa Mjumbe wa Baraza la Shirika la Usafiri wa Anga Duniani kuanzia mwaka 2016 hadi 2019 na hivyo kuwa mwakilishi wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC).
Je, kupitia nafasi hii ya kipekee, Serikali kupitia TCAA ina mkakati gani wa kuboresha miundombinu ya usafiri wa Anga hapa nchini, ili iweze kulingana na ile ya nchi nyingine za SADC?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Othman Omar Haji, Mbunge wa Gando kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Usafiri wa Anga (TCAA) inaendelea kuboresha mitambo ya kuongozea ndege hapa nchini. Tayari mchakato wa usimikaji wa rada nne za kuongozea ndege katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro, Uwanja wa Ndege wa Mwanza na Songwe unaendelea. Aidha, utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi 18 kuanzia tarehe 9 Novemba, 2017.
Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo TCAA imekamilisha mradi wa usimikaji wa mtambo Mashariki upande wa nchi yetu unaofanya kazi ya kutambua na kuongoza ndege zinazopita katika anga la juu (Automatic Dependent Surveillance Broadcast) na mtambo wa mawasiliano ya sauti katika kituo chetu cha kuongozea ndege cha Julius Kambarage Nyerere International Airport na nchi nzima kwa ujumla na hivyo kuboresha usalama katika anga la Tanzania. Aidha, TCAA wamekamilisha usimikaji wa mitambo ya mawasiliano kwa njia ya redio baina ya waongoza ndege na marubani (VHF Radios) and area cover relays na hivyo kuwa na uhakika wa mawasiliano.
Mheshimiwa Spika, miradi mingine inayoendelea kutekelezwa na TCAA kupitia Serikali katika kuboresha miundombinu ya usafiri wa anga nchini ni pamoja na kukarabati mnara wa kuongozea ndege katika kiwanja cha Pemba na kuendelea na mchakato wa ununuzi na usimikaji wa mtambo wa kuwezesha ndege kutua kwa usalama katika kituo cha Zanzibar.
Mheshimiwa Spika, hatua hizi zote zinazochukuliwa na Serikali zinalenga katika kulifanya anga la Tanzania kuwa salama zaidi na hivyo kuvutia mashirika mengi ya ndege ya kigeni kuja hapa nchini kwetu. Aidha, Tanzania kupitia nafasi hii ya ujumbe wa Baraza la Washirika la Usafiri wa Anga Duniani kwa kuziwakilisha nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) itaendelea kuhamasisha mashirika ya ndege ya kigeni kuja nchini kwa kupitia mikutano mbalimbali ya kimataifa ambayo mamlaka uhudhuria na hivyo kuongeza mapato ya mamlaka na kwa nchi kwa ujumla kutokana na miundombinu ya usafiri wa anga nchini kuendelea kuboreshwa.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-
Katika nchi yetu kuna kampuni za simu zenye ushindani mkubwa lakini katika Jimbo la Kilolo, hasa maeneo ya Kimala, Kidabaga, hayana mawasiliano ya simu:-
Je, ni lini Serikali itazishawishi kampuni za simu kusimika minara yao kwenye maeneo ambayo hayana mtandao wa mawasiliano ya simu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASIALIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa, Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote iliainisha Kata ya Kimala na Kidabaga kwa ajili ya kupelekewa huduma za mawasiliano kupitia Kampuni ya Mawasiliano ya Halotel. Tayari Halotel imejenga mnara eneo la Kimala na mnara huo umeanza kutoa huduma tangu tarehe 17 Septemba, 2016. Halotel ni kampuni pekee inayotoa huduma za mawasiliano katika eneo hilo la Kimala. Vilevile Halotel imejenga mnara katika eneo la Kidabaga ambao pia, umeanza kutoa huduma tangu tarehe 9 Mei, 2016.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana wakati swali hili linaletwa na Mheshimiwa Mbunge, labda siku hiyo kulikuwa hakuna mawasiliano eneo hilo, lakini kuna barua ambayo nimeletewa na Mbunge wa Jimbo la Kilolo, Mheshimiwa Venance Mwamoto, ambayo inaeleza maeneo tofauti kabisa ambayo hayana mawasiliano tofauti na aliyoyataja Mheshimiwa Mbunge. Hata hivyo, Wizara itawatuma wataalam wake kwenda kuangalia maeneo hayo kama kuna changamoto yoyote ili tuangalie uwezekano wa kuongeza coverage katika maeneo hayo.
MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga minara ya Simu katika Kata za Yayeda, Ampa Arr, Tumati, Gidilim Gorati, Endaagichan na Haydere katika Jimbo la Mbulu Vijijini ili wananchi waweze kuwasiliana?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. Eng. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) iliyaainisha maeneo mbalimbali ya Jimbo la Mbulu vijijini yakiwemo maeneo ya Yaeda, Tumati, Gidilim Gorati, Masieda, Endaagichan, na Hyadere na kuyaingiza katika zabuni ya awamu ya tatu iliyotangazwa tarehe 5 Juni, 2018. Zabuni hii inategemewa kufunguliwa tarehe 23 Julai, 2018. Endapo mzabuni atapatikana, mkataba kwa ajili ya kazi husika unatarajiwa kusainiwa tarehe 29 Agosti, 2018 na ujenzi wa minara unatarajiwa kuchukua miezi tisa tangu kusainiwa kwa mkataba.
MHE. KIZA H. MAYEYE (k. n. y MHE. ZITTO KABWE) aliuliza:-
Kigoma Ujiji ni Mji wa kibiashara kwa kuwa ni Lango la Magharibi la nchi yetu kuelekea nchi jirani za Maziwa Makuu. Kutokana na hali hiyo Serikali ya Japan kupitia JICA imekuwa ikiandaa mradi wa kuboresha Bandari ya Kigoma kwa miaka kadhaa sasa:-
(a) Je, Mchakato wa mradi huo umefikia hatua gani hadi sasa?
(b) Je, mradi huo utagharimu kiasi gani cha fedha na utaboresha maeneo gani ya Bandari ya Kigoma?
(c) Je, mradi huo utaanza kutekelezwa lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zitto Ruyagwa Kabwe, Mbunge wa Kigoma Mjini, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali ya Japan kupitia Shirika lake la Maendeleo la Kimataifa JICA imekuwa ikiandaa mradi wa kuboresha bandari ya Kigoma ambapo tarehe 29 Juni, 2018 Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano na Wizara ya Fedha na Mipango na Serikali ya Japan kupitia JICA zilisaini makubaliano ya kitaalam ya utekelezaji ya ujenzi wa gati la abiria, jengo la kusubiria abiria, ghala la kutunzia mizigo na barabara itakayoelekea kwenye gati jipya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa JICA inasubiri kibali cha ufadhili huo kutoka Serikali ya Japan. Mchakato wa kumpata mkandarasi umepangwa kuanza Novemba, 2018 kulingana na makubaliano yaliyofikiwa kati ya Serikali yetu na JICA.
(b) Gharama halisi ya mradi zitajulikana baada ya kusaini makubaliano ya ufadhili na kumpata mkandarasi wa ujenzi.
(c) Mradi huo unatarajiwa kuanza kutekelezwa mwezi Juni, 2019 kulingana na makubaliano yaliyofikiwa kati ya Serikali yetu na JICA.
MHE.SHALLY J. RAYMOND (K.n.y. ANNE K. MALECELA) aliuliza:
Tarafa ya Ndungu iliyoko Wilaya ya Same imesheheni uchumi mkubwa sana wa mazao ya chakula na biashara, Serikali ya Awamu ya Nne ya Chama cha Mapinduzi ililiona hilo na ikakubali kujenga barabara ya lami kutoka Mkomazi kupita Ndungu, Kisiwani hadi Same; barabara hiyo iliwekwa lami vipara vipara kwa kilomita tatu Kihurio, tano Kisiwani, tano Ndungu na tano Maore.
Je, Serikali haioni kuwa kuna umuhimu wa kuunganisha vipande hivi ili kukamilisha barabara hii ya Mkomazi, Kisiwani hadi Same kwa kiwango cha Lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, Mbunge wa Kuteuliwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Same – Kisiwani – Mkomazi yenye urefu wa kilomita 100.5 ni barabara ya Mkoa inayojumuisha kilomita 96.46 zinazohudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Kilimanjaro na kilomita 4.04 Mkoa wa Tanga. Kama alivyoeleza vizuri Mheshimiwa Mbunge sehemu tano za barabara hii, zenye jumla ya kilomita 21 zimejengwa kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukamilisha ujenzi kwa kiwango cha lami barabara hii Serikali kwa mwaka wa fedha 2017/2018 ilisaini Mkataba wenye thamani ya shilingi milioni 890.221 na Kampuni ya Kihandisi ya Advanced Engineering Solutions Limited ya hapa nchini, ikishirikiana na Kampuni ya Advanced Construction Centre ya Misri ili kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa kilomita zote 100.5 za barabara hii. Kazi hiyo ilianza tarehe 28 Juni, 2018 na inatarajiwa kukamilika tarehe 25 Machi, 2019. Kwa sasa taarifa ya awali ya mradi (Inception Report) imewasilishwa kwa ajili ya mapitio.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kukamilika kwa utekelezaji wa Mkataba huu kutawezesha kujulikana kwa gharama za ujenzi hivyo kuwezesha Serikali kuanza hatua za kutafuta fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami barabara hiyo, kwa awamu kadri fedha zitakavyopatikana. Wakati usanifu unaendelea Serikali katika mwaka wa fedha wa 2018/ 2019 imetenga jumla ya shilingi milioni 1,113.595 kwa ajili ya kuifanyia matengenezo mbalimbali barabara hii ili iendelee kupitika majira yote ya mwaka.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE aliuliza:-
Stesheni ya treni ya Kidete - Godegode - Gulwe na Msagali treni hukwama mara kwa mara kutokana na mafuriko wakati wa mvua na Serikali ina mpango wa kujenga reli ya standard gauge kutoka Dar es Salaam mpaka Kigoma.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhamisha reli hiyo kuanzia Stesheni ya Kidete - Godegode - Gulwe mpaka Msagali na kupitisha eneo lingine ambalo hakuna mafuriko ili kuondoa usumbufu wa abiria ambao hukaa maeneo hayo treni inapokwama au reli inapochukuliwa na mafuriko?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Seneta George Malima Lubeleje, Mbunge wa Mpwapwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la mafuriko katika eneo hili ni la muda mrefu na Serikali kupitia Shirika la Reli Tanzania imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za muda mfupi za kukabiliana na changamoto hii zikiwemo ujenzi wa mabwawa pamoja na kuendelea kutafuta fedha kutoka taasisi mbalimbali za kifedha kwa ajili ya ujenzi wa suluhisho la kudumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Japan kupitia Shirika lake la Maendeleo la JICA tayari limekwishakamilisha upembuzi yakinifu kuhusu upatikanaji wa suluhisho la kudumu katika eneo hilo. Aidha, mazungumzo baina ya Serikali yetu na Serikali ya Japan yanaendelea ili kupata fedha kwa ajili ya kutatua tatizo hili la mafuriko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, ili kuepukana na uharibifu unaojirudia kila mwaka kutokana na mafuriko, yafuatayo yanafanyika katika ujenzi wa reli mpya ya standard gauge:-
(a) Reli mpya haitokuwa karibu na mito na kuipitisha vilimani zaidi ya kingo za Mito ya Mkondoa na Chinyasungwi na kuna maeneo korofi ambapo reli itakuwa zaidi ya kilometa mbili kutoka reli ya sasa ilipo.
(b) Reli itajengwa ndani ya mahandaki yaani tunnels na madaraja yenye mihimili iliyoinuliwa juu zaidi. Kwa kuzingatia utatuzi huu, kutajengwa mahandaki manne yatakayokuwa na umbali wa jumla ya kilometa 2.75 pamoja na madaraja yenye uwazi yaani span ya mita 400.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kutoa wito kwa wnanachi wanaoishi jirani na reli zetu wazingatie na kuheshimu eneo la njia za reli kuepuka uharibifu wa reli zetu ambazo zinagharimu pesa nyingi kuzirekebisha.
CONCHESTA L. RWAMLAZA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya Kanazi - Kyaka kwa lami na kuimarisha Daraja la Kalebe linalopitisha magari yenye mizigo tani kumi ili iweze kupitisha mizigo hadi tani 40?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Conchesta Leonce Rwamlaza, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Kanazi hadi Kyaka yenye kilometa 55.86 ni sehemu ya barabara ya Mkoa ya Kietama - Kanazi hadi Kyaka yenye urefu wa kilometa 60.65.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipaumbele cha Serikali kwa sasa ni kukamilisha utekelezaji wa sera yake ya kuunganisha makao makuu ya mikoa na nchi jirani kwa barabara za lami. Baada ya hapo ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara nyingine za mikoa ikiwemo ya Kanazi hadi Kyaka utafuata kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia umuhimu wa barabara hiyo Wizara ya Ujenzi na uchukuzi na Mawasiliano kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) imeendelea kuifanyia matengenezo ya aina mbalimbali barabara hiyo ili iendelee kupitika majira yote ya mwaka ambapo mwaka 2018/2019 jumla ya shilingi milioni 411.688 zimetengwa kwa ajili ya barabara hiyo.
MHE. JUMA KOMBO HAMAD (K.n.y MHE. MGENI JADI KADIKA) aliuliza:-
Minara mingi ya simu imejengwa katika makazi ya watu na minara hiyo inatumia mionzi hatari kwa maisha ya binadamu. Je, Serikali inaliangaliaje suala hilo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASIALIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mgeni Jadi Kadika, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa baadhi ya minara ya simu hujengwa karibu na makazi ya watu kwa lengo la kutoa mawasiliano bora. Ili kuhakikisha usalama kwa binadamu kuhusiana na madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na huduma za mawasiliano hususani mionzi inayotumika katika mawasiliano, Tanzania huzingatia viwango na miongozo ya udhibiti wa mionzi inayotolewa na Tume ya Kimataifa ya Kudhibiti Mionzi ijulikanayo kama International Commission on Non-Ionizing Radiation Protection (ICNIRP). Tume hii ilianzishwa na Umoja wa Mawasialiano ya Kimataifa International Telecommunication Union (ITU) ili kutafiti juu ya madhara yatokanayo na mionzi inayotokana na vifaa vya redio hususani simu za mkononi.
Mheshimiwa Mwenyekiti,kwa kuzingatia tafiti mbalimbali za kisayansi hakuna madhara yatokanayo na mionzi ya mawasiliano hata watu wanaoishi karibu na minara ya simu. Kulingana na tafiti za Tume (ICNIRP) imebainishwa kwamba hakuna athari zinazoweza kusababishwa na mionzi au masafa ya redio, kwa vile nguvu iliyomo katika masafa au mionzi inayosafirishwa hupungua kwa kiwango kikubwa sana kutoka kwenye antena (mara 1000 katika umbali wa mita moja kutoka kwenye antena) na kwa vile antenna hufungwa mita kadhaa juu ya minara, nguvu ya mionzi hiyo huwa ni ndogo sana ifikapo chini kiasi cha kuweza kuleta athari yoyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya Taifa ya TEHAMA ya mwaka 2016 inaelekeza kukuza usalama katika matumizi ya bidhaa na huduma za TEHAMA. Sawasawa na maelekezo haya ya kisera, katika kuhakikisha kuwa viwango vya mionzi vinavyotokana na minara ya mawasiliano havizidi kiwango kilichoelekezwa kimataifa. TCRA kwa kushirikiana na Tume ya Nguvu za Atomiki (Atomic Energy Commission) imekuwa ikifanya ukaguzi mara kwa mara na kubaini kwamba hadi sasa hakuna mionzi yeyote inayotokana na minara hii inayoweza kuathiri watu.
MHE. PULINE P. GEKUL aliuliza:-
Vijiji vya Imbilili, Hitimi na Managha katika Jimbo la Babati Mjini havina mawasiliano ya simu. Je, ni lini Serikali itavipa vijiji hivyo minara ya mitandao ya simu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Pauline Gekul, Mbunge wa Babati mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote ilifanya tathmini katika Kijiji cha Imbilili kata ya Singino, Himiti Kata ya Bonga pamoja na Kijiji cha Managha Kata ya Singena kwa kuangalia hali halisi ya mawasiliano pamoja na idadi ya wakazi. Vijiji hivyo viliingizwa katika orodha ya vijiji vinavyohitaji huduma ya mawasiliano. Vijiji hivyo vyote viliweza kupelekewa mawasiliano kupitia Kampuni ya Viettel ambayo inamilikiwa kampuni ya Halotel kwa ajili ya mawasiliano. Hata hivyo ninazo taarifa kwamba minara hiyo haifanyi kazi vizuri sana na nimetuma timu ya wataalamu kwenda kuhakikisha kwamba kuna tatizo gani katika minara hiyo kwa ajili ya kuhakikisha wanapata mawasilino wananchi wa eneo hilo.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA aliuliza:-
Barabara ya kutoka Ifakara mpaka Mahenge Mjini ni muhimu sana kwa usafirishaji wa mazao kama mpunga, mahindi, ufuta, ndizi na maharage. Je, ni lini Serikali itajenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano naomba kujibu swali la Mheshimiwa Goodluck A. Mlinga Mbunge wa Ulanga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Ifakara, Mahenge yenye urefu wa kilometa 70 ni sehemu ya barabara ya Mikumi - Ifakara - Mahenge - Lupiro - Malinyi - Londo, Lumecha ambayo ina kilometa 587.8 inayounganisha Mikoa ya Morogoro na Ruvuma. Ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara hii unatekelezwa kwa awamu kulingana upatikanaji wa fedha ambapo kwa sasa tayari Serikali imekamilisha ujenzi wa kiwango cha lami kwa sehemu ya Mikumi mpaka Kidatu ambayo ina kilometa 35 pamoja na ujenzi wa daraja la Magufuli katika mto Kilombelo na barabara unganishi yenye urefu wa kilometa 9.142.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwasasa ujenzi wa kiwango cha lami kwa sehemu ya Kidatu - Ifakara yenye kilometa 66.9 unayojumuisha Daraja la Mto Ruaha Mkuu (Great Ruaha) umeanza. Kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina pamoja na kuandaa nyaraka za zabuni kwa barabara ya Ifakara mpaka Mahenge, Lupiro - Malinyi - Londo hadi Lumecha umekamilika toka mwezi huu mwanzoni. Hivyo ujenzi wa kiwango cha lami kwa sehemu iliyobaki ikiwemo na sehemu ya Ifakara mpaka Mahenge yaani kilometa 70 utatekelezwa kwa awamu kutegemeana na upatikanaji wa fedha.
MHE. ALLY S. UNGANDO aliuliza:-
Kwa muda mrefu sasa wananchi wa Nyamisati wamekuwa wakipata adha kubwa sana katika eneo la kivuko. Je, ni lini Serikali itajenga Gati la Nyamisati?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Seif Ungando, Mbunge wa Kibiti, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa Gati la Nyamisati umeanza tangu tarehe 16 Machi, 2018 baada ya mkandarasi M/s Alpha Logistics Tanzania Ltd. na M/s Southern Engineering Company Ltd. kukabidhiwa na Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) eneo la mradi toka tarehe 2 Machi, 2018. Kazi ya ujenzi wa gati hili zinatarajiwa kukamilika katikati ya mwezi Machi, 2019 kwa gharama ya jumla ya shilingi bilioni 14.435.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua zilizofikiwa mpaka sasa hivi ni kufanya upimaji wa bahari (bathymetric survey), uchunguzi wa udongo (geotechnical investigation) katika sehemu ya kujenga gati na usafishaji wa eneo (site clearance). Pia mkandarasi anaendelea na maandalizi (mobilization) kwa ajili ya kuanza kazi rasmi baada ya kazi hizi za awali za upimaji kukamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufanya kazi hii kumekuwa na changamoto kadhaa kama vile mwingiliano wa vyombo vinavyotumia kivuko na vile vya mkandarasi. Mfano, vessel inayofanya kazi ya uchunguzi wa udongo inaingiliana na vyombo vya usafiri, changamoto hii inatatuliwa kwa kujenga gati la muda (temporary berth) kwa ajili ya kuhudumia wasafiri.
Aidha, wananchi waliokuwa wanatumia gati la zamani ambalo sasa linajengwa jipya katika eneo hilohilo walikuwa hawataki kuhama, hata hivyo, uongozi wa Wilaya umefanikisha wananchi hao kuhama lakini wanahitaji wajengewe choo katika eneo jipya la kufanyia biashara walilohamia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, TPA tayari wanaendelea na taratibu za kujenga choo hicho cha umma ambapo mpaka sasa wapo kwenye hatua za kumpata mkandarasi wa kujenga choo hicho.
MHE. OMARY T. MGUMBA aliuliza:-
Barabara ya Ubena, Ngerengere hadi Mvuha ina urefu wa zaidi ya kilometa 70 na inaunganisha Wilaya ya Bagamoyo na Halmashauri ya Morogoro ambako Makao Makuu ya Wilaya mpya ya Mvuha yanatarajiwa kujengwa. Aidha, barabara hii inaunganisha Mkoa wa Pwani na Morogoro. Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro haina uwezo wa kuhudumia barabara hiyo:-
(a) Je, ni lini Serikali itakubali ombi la kupandisha barabara hiyo kuwa ya Mkoa?
(b) Je, ni lini Serikali itatengeneza barabara hiyo ya Ubena – Mvuha kwa kiwango cha changarawe ili ipitike mwaka mzima?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Omary Tebweta Mgumba, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Ubena Zomozi kwenda Ngerengere hadi Mvuha yenye urefu wa kilomita 105.4 ilipandishwa hadhi na Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano tangu Januari, mwaka 2017 kutoka barabara ya Wilaya na kuwa barabara ya Mkoa baada ya kukidhi vigezo vya Sheria ya Barabara ya mwaka 2007 na Kanuni zake za mwaka 2009. Kwa sasa barabara hii inahudumiwa na Wakala wa Barabara (TANROADS) Mkoa wa Morogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu kubwa ya barabara hii inapitika kwa shida hasa wakati wa masika hususani kati ya kipande cha Ngerengere na Mvuha ambacho kina urefu wa kilomita 95.4. Sehemu iliyobaki kati ya Ubena Zomozi na Ngerengere inapitika vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS), Mkoa wa Morogoro, inaendelea kuifanyia matengenezo mbalimbali katika maeneo korofi ili iweze kupitika majira yote ya mwaka. Aidha, kutokana na umuhimu wa barabara hii ya Ubena Zomozi – Ngerengere – Mvuha – Kisaki – Stiegler’s Gorge inayoelekea katika mradi wa kufua umeme kwa kutumia maporomoko ya Mto Rufiji katika mwaka wa fedha 2018/2019 wizara yangu imetenga jumla ya shilingi bilioni tano kwa ajili ya ukarabati mkubwa.
MHE. ENG. RAMO M. MAKANI aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya kujenga uwanja wa ndege mbadala katika Mji wa Tunduru baada ya uwanja uliokuwepo awali kuhamishwa kutoka katikati ya mji?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Ramo Matala Makani, Mbunge wa Tunduru Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa mpaka sasa hivi Kiwanja cha Ndege cha Tunduru hakijahamishiwa rasmi kutoka katikati ya Mji wa Tunduru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu ilituma timu ya wataalam wake kutembelea viwanja vya ndege vya mikoa ya kusini ili kujionea na kutathmini hali halisi ilivyo katika viwanja hivyo ikiwa ni pamoja na changamoto za kuzungukwa na makazi ya watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kiwanja cha Ndege cha Tunduru ni miongoni mwa viwanja sita vya ndege vilivyotembelewa na timu hii mnamo mwezi Aprili, 2017. Viwanja vingine vilikuwa ni Kiwanja cha Newala, Masasi, Songea na Iringa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru imetenga eneo mbadala kwa ajili ya ujenzi wa kiwanja kipya cha Ndege cha Tunduru katika eno la Chingulungulu, Kata ya Muhesi, Tarafa ya Nakapanya, takriban umbali wa kilometa 17 kutoka Mjini Tunduru. Aidha, kiwanja cha sasa cha ndege cha Tunduru bado kinafaa kwa matumizi ya ndege na abiria isipokuwa kinahitaji kujengewa uzio ili kuimarisha usalama kiwanjani hapo wakati taratibu za kuhamia eneo jipya zikiwa zinaendelea.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU aliuliza:-
Moja ya sababu zinazochelewesha kuanza kwa Mgodi wa Kabanga Nickel ni umeme na reli:-
Je, ni lini reli ya Isaka – Keza kuelekea Burundi na Rwanda itajengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Constatine Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia ushirikiano baina ya nchi za Afrika Mashariki inatambua umuhimu wa ujenzi wa reli ya Isaka – Keza kuelekea Burundi na Rwanda, siyo kwa sababu tu ya kuanza kwa mgodi wa Kabanga Nickel, bali pia kuchochea kasi ya usafirishaji wa mizigo na shughuli za kibiashara na hivyo kuinua uchumi wa nchi yetu na nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali pia inatambua kuwa kila nchi ina wajibu wa kutekeleza mradi wa kujenga reli hii kwa sehemu yake. Hivyo, ni wajibu wa kila nchi kukamilisha mradi huo ili kuchochea maendeleo yanayotokana na ujenzi wa reli hiyo kwa kukidhi mahitaji makubwa ya ubebaji mizigo kwenda nchi jirani za Rwanda, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC). Aidha, hali hii itasaidia pia usafirishaji wa wananchi kwenda mikoani na nchi hizo za jirani kwa wingi na kwa kasi zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Tanzania, tayari imeshaanza kujenga kwa kipande cha kuanzia Dar es Salaam – Morogoro kilometa 202 na Morogoro – Makutupora kilometa 336, ikipitia Makutupora – Tabora kilometa 294, Tabora – Isaka kilometa 133 na Isaka – Mwanza kilometa 254 ikikamilika kwa urefu wa kilometa 1,219; na sehemu nyingine ni kutoka Tabora hadi Kigoma kupitia Mpanda – Kalemela – Tabora na Uvinza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kujenga reli kutoka Isaka kupitia Kabanga hadi Rusumo na kuingia Kigali nchini Rwanda, Serikali inakamilisha maandalizi ya kujenga reli hiyo. Mkataba wa usanifu na matayarisho ya zabuni umesainiwa mwezi huu wa Mei, 2018 na Kazi itaanza mwezi Juni, 2018 na zabuni itatangazwa ndani ya mwaka huu wa 2018.
MHE. KHADIJA HASSAN ABOUD (K.n.y. MHE. MAHMOUD H. MGIMWA) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itapeleka huduma ya mawasiliano katika Kata za Mpanda, Mpangatuzara, Ihanu na Ikweha?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mahmoud Hassan Mgimwa, Mbunge wa Mufindi Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua umuhimu wa huduma ya mawasiliano nchini, Serikali kwa kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote, uliyaainisha maeneo ya Kata za Mapanda na Ikweha na kuyaingiza katika zabuni ya awamu ya pili ‘A’ kwa ajili ya kuwekewa huduma za mawasiliano. Kata hizo mbili zilipata mzabuni wa kufikisha huduma ambaye ni Vodacom. Kazi ya kufikisha huduma ya mawasiliano ilishakamilika ambapo vijiji vya Ugenza, Ukelemi na Uyela katika Kata ya Ikweha vinapata huduma hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, baadhi ya maeneo ya Kata hiyo hususan Kijiji cha Ikweha hakina mawasiliano. Kwa upande wa Kata ya Mapanda, huduma inapatikana katika baadhi ya maeneo ya Kata hii lakini mengi ya Vijiji vya Mapanda, Chogo, Ukami, Uhafiwa na Ihimbo havina huduma hii muhimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote itayaainisha maeneo ya Kata za Ihanu zenye Vijiji vya Isipii, Lulanda, Ibwanzi na Kilosa; Kata ya Mpanga yenye Vijiji vya Mpanga, Tazara; Kata ya Ikweha, Kijiji cha Ikweha; na Kata ya Mapanda yenye Vijiji vya Mapanda, Chogo, Ukami, Uhafiwa na Ihimbo na kuyaingiza katika miradi ya mfuko ambayo itakayotekelezwa siku za usoni kwa kadri ya upatikanaji wa fedha hususani kuanzia mwaka huu wa fedha 2018/2019.
MHE. MUSSA B. MBAROUK aliuliza:-
Je, kwa nini Serikali isianzishe utaratibu wa kupima mizigo na usajili wa abiria katika vyombo vyote vya majini kama inavyofanyika Airport ili kuepusha ajali za mara kwa mara?
NAIBU WAZIRI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Bakari Mbarouk, Mbunge wa Tanga Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inao utaratibu wa kupima mizigo na usajili wa abiria katika vyombo vya usafiri kwa njia ya maji na utaratibu huo hutekelezwa kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa na Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) ambapo kwa hivi sasa utekelezaji wake unadhibitiwa na Wakala wa Meli Tanzania (TASAC).
Mheshimiwa Spika, vyombo vyote vya majini husajiliwa na kupewa vyeti vya ubora (Sea Worthiness Certificate) ambayo huonesha uwezo wa chombo husika kubeba mizigo au abiria. Aidha, Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) imeipa dhamana Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) kutoa kibali cha kuondoa chombo bandarini (Clearance Certificate) kutoka bandari moja kwenda nyingine baada ya kujiridhisha kuwa chombo husika kimebeba abiria au shehena kulingana na viwango vya usalama vilivyokusudiwa kwa shughuli ambazo chombo husika kimesajiliwa kufanya.
Mheshimiwa Spika, kwenye kibali cha kuondoa chombo bandarini hujazwa takwimu kama vile; idadi ya wafanyakazi wa chombo (crews), idadi ya abiria (passengers) idadi ya mizigo (cargo) na huambatanishwa na majina ya abiria (passenger manifest) na idadi ya mizigo (cargo manifest) kwa ajili ya ukaguzi, ukamilishaji wa miamala ya kibiashara, ufuatiliaji pindi ajali inapotokea na kumbukumbu za ofisi. Hivyo, vyombo vyote hubeba shehena au kupakia abiria kulingana na uwezo wake na hivyo kuepusha ajali zisizo za lazima.
Mheshimiwa Spika, napenda nitoe wito kwa Watanzania wenzangu hususani wanaoishi katika mwambao wa Bahari ya Hindi, Ziwa Victoria, Tanganyika na Ziwa Nyasa kuacha kutumia vyombo vya usafiri visivyosajiliwa na SUMATRA au TASAC, hususan vinavyotoa huduma katika bandari zisizo rasmi (bandari bubu) kwa upande wa Bahari Kuu na mialo kwa upande wa maziwa makuu ili kuepusha ajali za mara kwa mara na hivyo kunusuru maisha ya watu na mali zao.
MHE. CONSTATINE J. KANYASU aliuliza:-
Watanzania tuliaminishwa kwamba iwapo Tanzania ikiunganishwa na Mkongo wa Mawasiliano wa Taifa, tutaimarisha mawasiliano na kupunguza gharama za mawasiliano:-
Je, taarifa hizo zilikuwa sahihi kwa kiwango gani?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Constatine John Kanyasu, Mbunge mahiri wa Geita Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni sahihi kabisa kuwa kujengwa kwa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano kumeimarisha mawasiliano na kuleta faida ya kushuka kwa gharama za mawasiliano nchini, pamoja na faida nyinginezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkongo umewezesha kushuka kwa gharama za kusafirisha masafa kwa umbali unaozidi kilomita 1,000 kwa kiwango cha 2Mbps kutoka Dola za Kimarekani 20,300 mwaka 2009 hadi Dola za Kimarekani 160 kwa mwaka 2015. Hilo ni sawa na punguzo la zaidi ya asilimia 99. Hii imewezesha gharama za huduma za kupiga simu kwa mtumiaji wa mwisho kushuka kutoka Sh.147 kwa dakika mwaka 2009 hadi wastani wa Sh.56 kwa dakika mwaka 2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kumekuwa na ongezeko kubwa la matumizi ya simu na internet kutoka watumiaji 17,642,408 mwaka 2009 hadi kufikia watumiaji 40,080,954 mwaka 2017 kwa watumaiji wa simu; na kutoka watumiaji 520,000 mwaka 2009 hadi kufikia watumiaji 22,995,109 mwaka 2017 kwa watumiaji wa internet. Vilevile gharama za maunganisho baina ya mtandao mmoja na mwingine (interconnection fee) zimeshuka kutoka Sh.115 kwa dakika mwaka 2009 hadi Sh.15.6 kwa dakika mwaka 2018, ambapo imesababisha watoa huduma kuwa na huduma za vifurushi vinavyoruhusu mtumiaji kununua kifurushi kinachomwezesha kupiga simu katika mitandao yote na kutumia internet kwa bei nafuu kuliko ilivyokuwa hapo awali.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA aliuliza:-
Stesheni Kuu, vituo vidogo vidogo na maeneo yanayozunguka Stesheni za reli ya kati vimechakaa sana:-
Je, Serikali haioni haja ya kukarabati majengo ya Stesheni za reli ya kati na kuweka miundombinu ya maji safi na maji taka katika majengo hayo na maeneo yanayozunguka stesheni hizo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASHTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Asha Abdullah Juma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Reli Tanzania (TRC) lina jumla ya stesheni 124 katika mtandao wake wa reli hapa nchini. Aidha, shirika lilishaanza ukarabati wa stesheni za treni ambao pamoja na mambo mengine umezingatia uboreshaji wa mifumo ya maji safi na maji taka pamoja na sehemu za kukaa abiria wakati wa mvua kwa kutumia vyanzo vyake vya ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, stesheni zilizokwisha kukarabatiwa ni pamoja na Kigoma, Kaliua, Pugu, Malindi na Mwanza ambapo ukarabati bado unaendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, shirika linatambua changamoto ya ukosefu wa baadhi ya huduma katika stesheni zilizobakia za reli kutokana na kuwa na miundombinu chakavu na hivyo kuweka mpango mkakati wa kukarabati na kuboresha stesheni hizo hatua kwa hatua kadri hali ya kifedha itakavyokuwa inaruhusu.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-
Bandari zilizopo Ziwa Nyasa upande wa Wilaya ya Ludewa zipo mbalimbali kutoka moja hadi nyingine hivyo kusababisha wasafiri kutembea umbali mrefu kupata huduma ya usafiri:-
• Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza bandari katika maeneo ya Nkanda, Nsele na Makonde katika Tarafa ya Mwambao?
• Je, ni lini zitajengwa gati katika bandari zilizopo Ziwa Nyasa hususani eneo la Wilaya ya Ludewa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa Mngwali, Mbunge wa Ludewa, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imepanga kuboresha na kujenga miundombinu ya bandari na gati mbalimbali katika Ziwa Nyasa. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali kupitia TPA imetenga fedha kwa ajili ya kuendeleza Bandari za Mbamba Bay, Itungi, Kiwira, Ndumbi, Manda, Matema, Liuli na Lupingu-Wilayani Ludewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zabuni za kumpata Mshauri Mwelekezi wa kufanya kazi ya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na kuandaa nyaraka za zabuni na kumpata mkandarasi atakayejenga bandari na gati hizo ilitangazwa Februari, 2018. Kazi ya Mshauri Mwelekezi tunategemea itakamilika kabla ya mwisho ya mwaka huu 2018 na kazi ya ujenzi tunategemea itaanza mapema mwaka 2019. Ni matumaini yangu kwamba baada ya kuboresha na kujenga bandari na gati hizo, wananchi wa vijiji vya Nkanda, Nsele, Makonde, Yigha katika Tarafa ya Mwambao watakuwa wamesogezwa huduma karibu na vijiji vyao.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB aliuza:-

ATCL Corporation ni Shirika la Ndege la Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na limekuwa likifanya vizuri chini ya Uongozi wa Mkurugenzi Mkuu Engineer Matida:-

(a) Je, kwa nini ATCL kila Jumatatu inapoondoka Dar es Salaam kwenda Dodoma isipitie Zanzibar ili viongozi pamoja na wananchi wanaotaka kwenda Dodoma wapate huduma hiyo?

(b) Je, Serikali haioni kuwa sasa ni wakati muafaka wa safari za ATCL kutoka Dar es Salaam zipitie Zanzibar kwa Jumatatu zote kupunguza tatizo la usafiri kwa wananchi wa Zanzibar wanaotaka kwenda Dodoma kwa shughuli mbalimbali?

(c) Je, ni lini safari hizo zitaanza ili viongozi, wananchi wa watalii kutoka Zanzibar waone kuwa Serikali yao inawajali na inadumisha Muungano wetu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jaku Hashim Ayoub, Mbunge wa Konde, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, dhumuni la Serikali kupitia Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) ni kuhakikisha wananchi wote wa Tanzania Bara na Visiwani wanapata huduma ya usafiri wa anga kwenye kituo (destination) chochote chenye maslahi ya kibiashara. Aidha, ATCL inatumia kituo cha Dar es Salaam kama kitovu ili kuwa na muunganiko wa kupeleka abiria sehemu nyingi na kukidhi mizania ya kibiashara kwani bila kufanya hivyo inaweza kukosa abiria wa kutosha kutoka kituo kimoja kwenda kingine.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia hilo, Serikali kupitia ATCL imebaini kuwa Zanzibar ni moja ya vituo ambavyo kuna maslahi kibiashara. Hivyo, imesharekebisha ratiba zake ili kuhakikisha wasafiri kutoka Zanzibar wanakuwa na uwezo wa kusafiri kwenda Dodoma kupitia kitovu (hub) cha Dar es Salaam kwa kuwa na ndege ya siku ya Ijumaa kutoka Zanzibar kuja Dar es Salaam ambapo abiria hao wataweza kuunganisha safari kwenda Dodoma kwa ndege ya alasiri siku hiyo hiyo ya Ijumaa Aidha, ATCL ina ndege ya Jumapili inayotoka Zanzibar kuja Dar es Salaam asubuhi ambayo itaungaisha na ndege inayokwenda Dodoma.

(b) Kama nilivyoeleza kwenye jibu la kipengele (a) cha swali hili, hivi sasa siyo wakati muafaka kwa kila Jumatatu ndege ya ATCL inapoondoka Dar es Salaam kwenda Dodoma ipitie Zanzibar. Aidha, utaratibu huo wa safari za ATCL kutoka Dar es Salaam kupitia Zanzibar kwa kila Jumatatu utaanza pindi muunganiko wa kupeleka abiria Zanzibar kutoka Dar es Salaam na sehemu zingine kwa siku ya Jumatatu utakidhi mizania ya kibiashara.

(c) Safari za ATCL kila Jumatatu kutokea Dar es Salaam kwenda Dodoma kupitia Zanzibar kama nilivyoeleza kwenye majibu ya swali (b) zitaanza pindi muunganiko wa kupeleka abiria sehemu zingine kupitia Zanzibar utakapokidhi mizani ya kibiashara.

Aidha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inawajali viongozi, wananchi na Watalii kutoka Zanzibar na ndio maana inajitahidi kwa kila hali kuhakikisha kuwa Viongozi, Wananchi na Watalii kutoka Zanzibar wanapata usafiri wa kuunganisha kutoka kituo cha Dar es Salaam kama kitovu kwenda Dodoma kwa kadiri inavyowezakana.
MHE. SEIF K. S. GULAMALI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa vibali kwa Kampuni za Halotel na Vodacom ili kuweza kuweka minara yao katika Kata ya Igoweko, Uswaya, Tambarale, Mwashiku, Ngulu, Ntobo na Mwamala?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kulipatia vizuri kabisa jina langu la kwanza.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Seif Khamis Gulamali, Mbunge wa Manonga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali haina kizuizi kwa kampuni yoyote inayotoa huduma za mawasiliano kama itazingatia utaratibu wa kuomba vibali vya ujenzi wa minara yao kwa mujibu wa sheria pamoja na kupata cheti cha tathmini ya mazingira kutoka Baraza la Taifa la Usimamizi wa Hifadhi ya Mazingira (NEMC).

Mheshimiwa Spika, Kata ya Igoweko, Ngulu na Sungwizi zimeainishwa na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote na kuingizwa katika orodha ya miradi itakayotekelezwa na Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) ambapo TTCL wako katika hatua za mwisho za taratibu za manunuzi ili kuanza kutekeleza miradi hiyo. Miradi hiyo yote inategemewa kukamilika ifikapo mwezi Aprili, 2019.

Mheshimiwa Spika, maeneo ya Kata za Uswa, Tambarale, Mwashiku, Ntobo na Mwamala zitaingizwa katika orodha ya miradi inayofadhiliwa na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote kwa mwaka wa fedha 2018/2019 na kutekelezwa kutokana na upatikanaji wa fedha. Hata hivyo, tunatoa wito kwa makampuni mbalimbali kuendelea kuwekeza minara ya mawasiliano katika Jimbo la Manonga na maeneo mengine nchini yale hasa yenye uhitaji kwa kuzingatia taratibu.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA aliuliza:-

Maeneo mengi katika Jimbo la Tabora Mjini na Iramba Mashariki hayana mawasiliano ya simu:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga minara ya simu katika maeneo hayo ili wananchi wa maeneo hayo wapate mawasiliano?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Emanuel Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa wote inasimamia utekelezaji wa Sera ya Taifa ya TEHAMA ya mwaka 2016 inayoelekeza kufikisha huduma ya mawasiliano katika maeneo yote, yakiwemo maeneo yasiyo na mvuto wa kibiashara. Mpaka sasa hivi jumla ya kata 703 katika mikoa yote Tanzania zimefikiwa na huduma za mawasiliano kwa jitihada za Mfuko, ambapo Watanzania zaidi ya milioni nne wanapata huduma za mawasiliano. Tabora Mjini zaidi ya wakazi 12,992 wamefikishiwa huduma za mawasiliano katika Kata za Kabila na Kampuni ya Halotel, Kalunde na Kampuni ya Vodacom na Uyui na Kampuni ya Vodacom vilevile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada za Serikali zinazoleta mafanikio hayo bado kuna maeneo nchini yakiwemo baadhi ya maeneo ya Jimbo la Tabora Mjini ambayo hayajafikiwa na huduma za mawasiliano. Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote itafanya tathmini kamili ya upatikanaji wa huduma za mawasiliano katika vijiji vyote vya kata za majimbo ya Tabora Mjini na vijiji vitakavyobainika kukosa mawasiliano au kuwa na mawasiliano hafifu vitaingizwa katika orodha ya vijiji vitakavyojumuishwa katika zabuni zitakazotangazwa hivi karibuni.
MHE. SELEMAN J. ZEDI aliuliza:-

Je, ni lini ujenzi wa barabara ya Tabora – Mambali – Itobo - Kagongwa yenye urefu wa Kilometa 149 utaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? Kwani ni ahadi ya Mheshimiwa Rais na pia imo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2015 - 2020.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi Uchukuzu na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Selemani Jumanne Zedi, Mbunge wa Bukene, kama ifuatavyo:-



Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeanza kutekeleza mpango wa ujenzi wa barabara ya Tabora – Mambali – Itobo–Kagongwa yenye urefu Kilometa 149 kwa kuanzia na hatua ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) wameingia mkataba na Mhandisi Mshauri NIMETA Consult Ltd. kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara ya Tabora – Mambali – Itobo – Kagongwa kwa gharama ya shilingi milioni 789. Hadi sasa Mhandisi Mshauri amekamilisha kazi ya upembuzi yakinifu na kazi ya usanifu wa kina itakuwa imekamilika kufikia Juni, 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara baada ya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, gharama za ujenzi pamoja na maandalizi ya nyaraka za zabuni kukamilika, Serikali itatafuta fedha za kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara hii. Aidha, wakati kazi ya usanifu ikiendelea, Wizara kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) itaendelea kutenga fedha za matengenezo mbalimbali kwa barabara hii ili iweze kupitika majira yote ya mwaka. Jumla ya shilingi 345 zimetengwa katika mwaka wa fedha 2018/ 2019 kwa ajili ya kazi hiyo. Ahsante.
MHE. JEROME D. BWANAUSI aliuliza:-

Serikali iliahidi kujenga minara ya simu katika Kata za Sindano, Lipumburu, Namtona, Mcharu, Chikolopola na Mkundi.

Je, ni lini ahadi hiyo itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jerome Dismas Bwanausi, Mbunge wa Lulindi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa wote iliviainisha Vijiji vya Kata za Sindano, Lipumburu, Namtona, Mchauru, Chikolopola na Mkundi kwa ajili ya tathmini kuangalia mahitaji halisi ya Mawasiliano kwenye eneo hilo. Baada ya tathmini husika kukamilika, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa wote iliviingiza Vijiji vya Kata za Mchauru katika mradi wa mpakani na kanda maalum unaotekelezwa na Kampuni ya Simu ya Tigo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari vibali vya ujenzi kutoka NEMC vimeshapatikana, hivyo Kampuni ya simu ya Tigo inategemea kuanza ujenzi wa mnara sambasamba na kufunga vifaa vya mawasiliano mara moja. Aidha, ujenzi wa mnara huu unatarajiwa kukamilika mwezi Januari, 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za Sindano na Lipumburu ziliingizwa katika mradi wa awamu ya tatu ambao ulitiwa saini tarehe 13 Desemba, mwaka 2018 na utekelezaji wake unategemewa kukamilika mnamo mwezi Septemba, 2019. Kata ya Sindano itafikishiwa huduma ya mawasiliano na Kampuni ya Vodacom na Kata ya Lipumburu itafikishiwa huduma ya mawasiliano na Kampuni ya TTCL.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vijiji vya Kata za Namtona, Chikolopola na Mkundi vitaingizwa katika orodha ya miradi ya zabuni zinazotangazwa katika siku za usoni kulingana na upatikanaji wa fedha hususan katika mwaka huu wa fedha 2019/2020.
MHE. ALLY K. MOHAMED (K.n.y. MHE. MOSHI S. KAKOSO) aliuliza:-

Vijijini vya Kapanga, Katuma, Simbwesa, Kasekese, Kungwi na Kabage havina mawasiliano ya simu:-

Je, ni lini Serikali itapeleka huduma ya mawasiliano ya simu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Moshi Selemani Kakoso, Mbunge wa Mpanda Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Vijiji vya Kapanga, Katuma Mpembe na Simbwesa vilipatiwa huduma ya mawasiliano mwaka 2016. Mradi huu ulitekelezwa na Kampuni ya Mawasiliano ya Simu ya Vodacom kwa ufadhili wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote. Vijiji vya Kasekese, Kungwa na Kabage vya Kata ya Sibwesa vilifikishiwa huduma ya mawasiliano kupitia mradi wa Halotel wa kufikisha huduma ya mawasiliano katika vijiji 4,000 nchini mwezi Septemba, 2018. Hata hivyo, baada ya kukamilika vifaa vya mawasiliano vilivyofungwa vilipata tatizo la kiufundi na kupelekea wananchi wa vijiji hivyo kutopata huduma ya mawasiliano.

Mheshimiwa Spika, vifaa vya mawasiliano vilivyopata matatizo vimeshaagizwa na vinategemewa kuwasili hivi karibuni na vitafungwa kabla ya mwisho wa mwezi Juni, 2019 ili wananchi wapate huduma ya mawasiliano itakayowasaidia kujiletea maendeleo.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. ANNA J. GIDARYA aliuliza:-

Jimbo la Babati Vijijini linakabiliwa na changamoto ya muda mrefu ya huduma ya mawasiliano ya simu hasa katika Vijiji vya Yorotonik, Endagwe, Hoshan na Endakiso ambako hakuna kabisa mnara wa mawasiliano ya simu:-

Je, ni lini Serikali itapeleka huduma hiyo katika maeneo ya vijiji husika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anna Joram Gidarya, Mbunge wa Viti Maalumu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuratibu utekelezaji wa jitihada muhimu za kuwezesha maeneo yote nchini kufikiwa na huduma za mawasiliano sawasawa na maelekezo ya Sera ya Taifa ya TEHAMA ya mwaka 2016. Kupitia Mfuko wa Mawasiano kwa Wote Serikali itaviainisha Vijiji vya Yorotonik, Endagwe, Hoshan na Endakiso kwa kuangalia ukubwa wa eneo, idadi ya wakazi wake pamoja na kufanya tathmini ya mahitaji halisi ya ruzuku kwa ajili ya kufikisha huduma ya mawasiliano maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, baada ya tathmini kukamilika, vijiji hivyo vitajumuishwa katika orodha ya miradi itakayoingia katika zabuni zinazotarajiwa kuingizwa katika mwaka wa fedha 2019/2020.
MHE. HALIMA A. BULEMBO (K.n.y. MHE. KHADIJA NASSIR ALI) aliuliza:-

Kwa kuwa, Serikali ya Awamu ya Tano inaendelea na zoezi la kununua ndege:-

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kuhakikisha kuwa ndege hizo zinakwenda kila mkoa wenye kiwanja cha ndege pamoja na nchi jirani ili kusaidia kushusha gharama za usafiri?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Khadija Nassir Ali, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nia ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kuhakikisha kuwa Kampuni ya Ndege Tanzania (Air Tanzania Company Limited) inakuwa na ndege za kutosha ili kuweza kutoa huduma za usafiri wa anga ndani na nje ya nchi kwa ufanisi na tija. Uwepo wa ndege mpya na za kutosha kutaiwezesha ATCL kuweza kuhimili ushindani katika utoaji wa huduma za usafiri wa anga katika masoko ya ndani, kikanda na kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upanuzi wa mtandao wa huduma za usafiri wa anga katika kila mkoa wenye kiwanja cha ndege na nchi jirani, unatekelezwa kwa kufuata Mpango Mkakati (Corporate Strategic Plan) wa ATCL wa miaka mitano unaoishia mwaka wa fedha 2021/2022 pamoja na Mpango wa Biashara unaoandaliwa kila mwaka. Hadi sasa, ATCL inasafirisha abiria katika mikoa tisa (9) na katika nchi tano (5) kama ifuatayo: Kwa Tanzania tunasafirisha Mkoa wa Dodoma, Mwanza, Bukoba, Kigoma, Mbeya, Kilimanjaro, Zanzibar, Tabora na Mtwara. Pia ATCL inatoa huduma za usafiri wa anga kwa safari za Kikanda kama ifuatavyo: Hahaya (Comoro), Harare (Zimbabwe), Bujumbura (Burundi), Entebe (Uganda) na Lusaka (Zambia). Hivyo, huduma za usafiri wa anga katika kila mkoa wenye kiwanja cha ndege na nchi jirani unatekelezwa kwa kufuata mpango wa upanuzi wa mtandao wa safari za ATCL pamoja na uwepo wa abiria wa kutosha ili kuifanya kampuni yetu ijiendeshe kwa ufanisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ATCL inatarajia kupokea ndege mbili mpya, Bombadier moja na Boeing moja mwishoni mwa mwaka huu, matarajio yetu ni kuwa ATCL itakuwa na uwezo wa kuongeza mtandao wa safari katika mikoa mingine pamoja na safari za kikanda na kimataifa.
MHE. MUSA R. NTIMIZI alliuliza:-

Kata ya Mmale haina mawasiliano kabisa ya simu:-

Je ni lini Serikali itawapatia wananchi hao mawasiliano kwa kuweka minara ya mawasiliano katika kata hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Musa Rashid Ntimizi, Mbunge wa Igalula, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ya Uyui, zaidi ya wakazi 66,056 wamefikishiwa huduma za mawasiliano katika Kata za Kizengi, Loya, Lutende, Mabama na Miswaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mafanikio hayo, bado kuna changamoto za upatikanaji wa huduma za mawasiliano katika Kata ya Mmale. Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote itaviainisha vijiji vya Kata ya Mmale iliyopo katika Jimbo la Igalula kwa kufanya tathmini ya mahitaji kwa ajili ya kuvifikishia huduma ya mawasiliano na kuvijumuisha katika orodha ya miradi itakayoingia katika zabuni zinazotarajiwa kutangazwa ifikapo mwezi ujao wa tano.
MHE. IGNAS A. MALOCHA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya maandalizi ya awali ya upembuzi yakinifu kwa ajili ya kuweka lami barabara muhimu ya Kibaoni-Kasansa-Muze- Kilyamatundu-Kamsamba kutokea Mlowo; ambayo inaunganisha mikoa mitatu ya Katavi, Rukwa na Songwe?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibiwa swali la Mheshimiwa Ignas Aloyce Malocha, Mbunge wa Kwela, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeanza kutekeleza mipango ya ujenzi wa barabara ya Kibaoni- Majimoto- Kisansa-Muze-Kilyamatundu- Kamsamba hadi Mlowo yenye urefu wa kilometa 149 kwa kuanza na ujenzi wa daraja la Momba ambalo limekamilika hivi karibuni. Daraja hili limekuwa kikwazo kikubwa cha mawasiliano kati ya wananchi wa Mikoa ya Katavi, Rukwa na Songwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii katika mwaka wa fedha 2018/2019, jumla ya shilingi milioni 200 zilitengwa kwa ajili ya upembuzi yakinifu wa barabara ya Kibaoni-Majimoto-Inyonga ikiwa ni sehemu ya barabara ya Kibaoni-Kasansa-Muze-Kilyamatundu- Kamsamba hadi Mlowo. Aidha, katika mwaka wa fedha 2019/2020, fedha zimeombwa kwa ajili ya kuanza upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara ya Ntendo-Muze- Kilyamatundu ikiwa pia ni sehemu ya barabara ya Kibaoni –Kasansa-Muze-Kilyamatundu-Kamsamba hadi Mlowo. Mara baada ya kukamilika upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na maandalizi ya nyaraka za zabuni za gharama ya ujenzi kujulikana Serikali itatafuta fedha za kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami kwa barabara hii.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza:-

Meli ya MV Chato inafanya safari zake kati ya Chato, Senga, Mshalamba, Izumacheli na Nkome. Inapofika Izumacheli huegesha kwenye jiwe kutokana na kukosekana kwa gati:-

Je, ni lini Serikali itajenga Gati katika Kijiji cha Izumacheli?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHATA J. NDITIYE): alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, Mbunge wa Geita Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Awamu ya Tano ina mkakati wa kuhakikisha kuwa huduma za usafiri zimeboreshwa katika maeneo yote nchini, huku kipaumbele kikiwekwa kwenye maeneo yenye mahitaji maalum na pia maeneo yenye kuchochea kwa haraka shughuli za kiuchumi. Kwa kutambua hilo Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA) pamoja na TEMESA imeandaa programu ya namna bora ya uboreshaji wa huduma za usafiri katika Ziwa Viktoria (Lake Victoria Modernisation Programme) kwa lengo la kubaini maeneo yote yanyohitaji ujenzi wa ama bandari au gati.

Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa mpango huu unaendelea ambapo ujenzi wa gati, maghala ya kuhifadhia mizigo na majengo ya abiria katika Bandari za Magarini ambayo iko Muleba na Nyamirembe ambayo iko Chato, Mwigobero ambayo iko Musoma na Lushamba ambayo iko Geita unaendelea. Naomba nimtaarifu Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Izumacheli Mkoani Geita kuwa, Serikali inatekeleza mpango wake kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha hivyo, Serikali itatoa kipaumbele kwa eneo hili awamu zinazofuata, ili kuruhusu kukamilika kwanza kwa miradi iliyokwishaanza katika Ziwa Victoria.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA (K.n.y. MHE. HAWA A. GHASIA) aliuliza:-

Je, ni lini ujenzi wa reli kutoka Mtwara – Mbambabay na matawi yake ya Liganga na Mchuchuma utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHATA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Abdulrahman Ghasia, Mbunge wa Mtwara Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa awali (feasibility and preliminary design) wa ujenzi wa reli kutoka Mtwara – Mbambabay kupitia matawi ya Mchuchuma-Liganga zenye urefu wa kilometa 1,092. Mshauri Mwelekezi wa kifedha na uwekezaji (transaction advisor) tayari amepatikana, mkataba na mshauri wa uwekezaji unatarajiwa kusainiwa ifikapo Juni, 2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mshauri wa Uwekezaji atakuwa na jukumu la kuunadi mradi huu kwa wawekezaji mbalimbali, ikizingatiwa kuwa mradi huu unatekelezwa kwa utaratibu wa ubia kati ya Sekta ya Umma na Binafsi (PPP). Hii ni katika kuhamasisha ushiriki wa sekta binafsi katika ujenzi wa reli nchini kwetu. Hivyo, baada ya kukamilika kwa utaratibu wa kumpata mwekezaji kwa njia ya PPP, ujenzi wa reli hii utaanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimtaarifu Mheshimiwa Mbunge kuwa hata sasa tumekuwa tukipokea wawekezaji wanaotaka kuwekeza katika reli hii ambapo tumekuwa tukiwaelekeza kufuata sheria na taratibu za ununuzi kwa miradi inayotekelezwa kwa mfumo wa PPP. Taratibu hizo zinawaelekeza kuandaa na kuwasilisha wazo lao (proposal) la kufanya uwekezaji kwa Shirika la Reli Tanzania (TRC) ambalo litawasilishwa katika Wizara yetu baada ya kuwa wamejiridhisha. Aidha, baada ya kuchambuliwa kwa kina na Wizara, litawasilishwa katika kitengo cha PPP kilichopo Wizara ya Fedha na Mipango kwa ajili ya uchambuzi wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Fedha na Mipango kupitia kitengo hicho, wakimaliza uchambuzi na kuridhia, mwekezaji atatakiwa naye kufanya upembuzi yakinifu wake ambao baadaye utalinganishwa na upembuzi yakinifu uliofanywa na Serikali kabla ya kukamilisha taratibu za uwekezaji.
MHE. RASHID A. SHANGAZI (K.n.y. MHE. STANSLAUS S. MABULA) aliuliza:-

Serikali kupitia Mamlaka ya TCRA wamefungia Local Channels kuonekana kwenye baadhi ya ving’amuzi hapa nchini, mfano Azam Tv, DSTV na vinginevyo.

(a) Je, Serikali haioni kwa kufanya hivyo imewanyima wananchi fursa ya kujua mambo yanayoendelea kwenye Taifa lao?

(b) Je, ni lini Serikali itatoa muafaka wa jambo hili?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Stanslaus Shing’oma Mabula, Mbunge wa Nyamagana, lenye Sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa wananchi kupata fursa ya kujua mambo yanayoendelea kwenye Taifa. Kwa misingi hiyo, imetoa leseni zenye masharti tofauti ikiwemo leseni ya public, yaani utangazaji wa umma ambapo matangazo huruhusiwa kurushwa kwa watoa huduma wenye must carry. Hivi sasa matangazo ya umma ni TBC 1 na TBC 3 maarufu kama Safari Channel.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha makampuni yanayomiliki visimbusi au ving’amuzi vya DSTV, Zuku na Azam hayakustahili kutoa huduma ya kubeba channel za ndani zisizolipiwa, yaani free to air local channels, kutokana na masharti ya leseni zao. Utoaji wa huduma za maudhui kupitia visimbusi vyao uko kwenye mfumo wa kukidhi soko la kimataifa na maudhui yake kuwa ya kulipia. Masharti ya leseni hizo na mfumo mzima wa miundombinu ya utangazaji husika yamelenga soko la kimataifa na hutofautiana na masharti ya leseni za watoa huduma za maudhui ya ndani ya nchi. Kuruhusu channels za ndani kuoneshwa kwa kutumia leseni za matangazo ya kimataifa kutazifanya free to air local channels kuwa za kulipia badala ya kuonekana bure.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TCRA imefanya jitihada ikiwa ni pamoja na kukaribisha maombi ya leseni ya kubeba maudhui ya channels za ndani, yaani multiplex operator, kutoka kwa wanaohitaji kutoa huduma yakiwemo makampuni ya Azam, DSTV na Zuku ili yaweze kupata leseni stahiki na kuweza kutoa huduma za kubeba au kuonesha maudhui ya ndani kupitia visimbusi vyao. Kwa sasa TCRA inashughulikia maombi yaliyopokelewa ili iweze kushauri kuhusu utoaji wa leseni stahiki.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Gati katika Kijiji cha Bukondo Halmashauri ya Wilaya ya Geita?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lolesia Jeremiah Bukwimba, Mbunge wa Busanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ina mpango wa kufanya upembuzi yakinifu kwenye Maziwa yote Makuu ya Victoria, Tanganyika na Nyasa ili kutambua maeneo yanayofaa kujenga magati. Zabuni kwa ajili ya kumpata mtaalam mwelekezi wa kufanya kazi ya upembuzi yakinifu ilitangazwa na kupata kampuni ya RINA kutoka nchini Italia mwezi Desemba, 2018 kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumpata mshauri mwelekezi huyo kumekuwa na mazungumzo ya maridhiano ya bei ya kufanya kazi ambayo yalikamilika mwezi Desemba, 2019. Kazi ya Upembuzi Yakinifu inatarajiwa kuanza mwezi Februari, 2020 na kukamilika ndani ya miezi
18. Hivyo, ujenzi wa gati katika eneo la Bukondo utategemea mapendekezo ya taarifa ya mshauri mwelekezi.
MHE. ESTER A. MAHAWE aliuliza:-

Kata za Naberera, Kitwai, Lorbene, Loibosroit, Norakauwo na Komolo katika Wilaya ya Simanjiro hazina huduma ya mawasiliano ya simu:-

Je,ni lini sasa Serikali itapeleka minara ya simu ili wananchi hao waweze kupata huduma ya mawasiliano ya simu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa, Ester Alexander Mahawe, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Manyara, kama Ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya kufikisha huduma za mawasiliano nchi nzima. Kata ya Naberera, ilijumuishwa kwenye zabuni ya mwezi Agosti, 2017 na vijiji vitano vilipata mtoa huduma kampuni ya Vodacom ambayo tayari imefikisha huduma ya mawasiliano katika vijiji hivyo. Aidha, vijiji vingine vitatu katika Kata hiyo ya Naberera vilijumuishwa katika zabuni ya awamu ya tatu mwezi Disemba, 2018 na kupata mtoa huduma kampuni ya mawasiliano Tanzania TTCL ambayo inaendelea na utekelezaji wa mradi wa kufikisha mawasiliano katika vijiji hivyo. Hadi hapo ifikapo tarehe 30 Juni, 2020 tunategemea mradi utakuwa umekamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Kata za Kitwai na Loibosroit zilijumuishwa kwenye zabuni ya awamu ya tatu na kupata watoa huduma kampuni ya Halotel kwa Kata ya Loibosroit na kampuni ya mawasiliano Tanzania kwa Kata ya Kitwai. Zoezi la kusaini mkataba lilifanyika tarehe 13 Desemba, 2018 na fedha za awali tayari zilikwishatolewa kwa watoa huduma ambapo kwa sasa wanaendelea na taratibu za ujenzi wa mnara ili kukamilisha mradi ifikapo Juni, 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Kata ya Komolo iliingizwa kwenye zabuni ya awamu ya nne ya Julai, 2019, japokuwa haikufanikiwa kupata mtoa huduma hivyo tunategema itajumuishwa tena katika zabuni ya awamu ya tano. Aidha, Vijiji vya Kata za Lorbene na Norakauwo vyote kwa pamoja vitajumuishwa kwenye zabuni ya awamu ya tano ambayo itatangazwa katika mwaka wa fedha 2019/2020.
MHE. SALUM MWINYI REHANI aliuliza:-

(a) Je, ni lini Mamlaka ya Hali ya Hewa itakuwa inatoa taarifa sahihi na za wakati kuhusiana na mabadiliko ya hali ya hewa nchini?

(b) Je, ni lini Mamlaka ya Hali ya Hewa kwa kushirikiana na Idara ya Earthy Warming watakuwa wanatoa taarifa za hali ya upatikanaji wa mvua na ukame ili kuwaepusha wakulima wengi kulima na kupata hasara kwa kukosa mvua wakati wao wanajua hali itakavyokuwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Salum Mwinyi Rehani, Mbunge wa Uzini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Hali ya Hewa (TMA) imeendelea kuboresha usahihi wa taarifa za hali ya hewa kwa kuhakikisha uwepo wa vifaa muhimu katika vituo vya utabiri wa hali ya hewa nchini. Kwa sasa usahihi wa taarifa zinazotolewa umefikia asilimia 87.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, TMA imeanzisha Jarida la Klimatolojia ambalo hutolewa kila mwaka kuhusu tathmini ya viashiria vya mabadiliko ya hali ya hewa nchini. Pia, mwaka 2015, Mamlaka iliandaa taarifa inayoonesha mwelekeo wa mabadiliko ya hali ya hewa ikiwa ni pamoja na mwelekeo wa unyeshaji mvua na joto kwa miaka 30 ijayo. Kimsingi tangu mwaka 2015, kiwango cha usahihi katika tabiri za hali ya hewa kimekuwa zaidi ya 80% ambacho ni kiwango cha chini kinachokubalika na Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO).

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, TMA hutoa taarifa mbalimbali za hali ya hewa kwa umma ikijumuisha zile za utabiri wa kila siku, misimu ya mvua na tahadhari ya hali mbaya ya hewa nchini. Taarifa zinazotolewa zinajumuisha ushauri na tahadhari pale inapoona dalili za kuwepo kwa matukio ya mafuriko au ukame wakati wa misimu ya mvua. Aidha, TMA inashirikiana na vyombo mbalimbali vya habari na Serikali ikiwemo Wizara ya Kilimo (Idara ya Usalama wa Chakula, Kitengo cha Early Warning) ili kuhakikisha kwamba taarifa za hali ya hewa zinawafikia Maafisa Ugani na watumiaji kwa wakati. Taarifa hizi pia husambazwa kupitia ofisi zote za hali ya hewa nchini.

Mheshimiwa Spika, katika taarifa zinazotolewa, wakulima hushauriwa kupata ushauri kutoka kwa wataalam mbalimbali wakiwemo Maafisa Ugani. Mamlaka ya Hali ya Hewa pia imeanzisha mfumo wa kusambaza Taarifa za Hali ya Hewa kwa wakulima kupitia njia ya ujumbe katika simu za viganjani (farm sms).
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza:-

Maeneo ya mipakani katika Wilaya za Kakonko, Kibondo, Kigoma Vijijini, Buhigwe na Kasulu yanakabiliwa na tatizo la mawasiliano ya simu kutokana na kukosekana kwa minara ya simu:-

Je, ni lini Serikali itajenga minara ya simu katika maeneo ambayo hayana minara Mkoani Kigoma ili kuondoa tatizo la mawasiliano kwa Wananchi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Gezabuke, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote mwezi Julai 2019, ilitangaza zabuni kwa ajili ya kufikisha huduma za mawasiliano katika kata 521 zenye vijiji 1,222 nchini. Zabuni hii ilifunguliwa Oktoba, 2019 na baada ya tathmini yake maeneo yaliyopata wazabuni nchi nzima na maeneo mbalimbali ni kama yafuatavyo:-

(i) Kwa upande Wilaya ya Kakonko, nikizungumzia Mkoa wa Kigoma kata zilizopata miradi ni Kata za Nyamtukuza na Rugenge, Kijiji cha Kasongati;

(ii) Katika Wilaya ya Kigoma Vijijini, ilikuwa ni Kata ya Ziwani ikijumuisha Vijiji vya Kalalangabo na Kigalye;

(iii) Katika Wilaya ya Buhigwe, tulikuwa na Kata ya Mugera, Kijiji cha Katundu; na

(iv) Katika Wilaya ya Kasulu, ilikuwa Kata ya Kitanga na Kijiji cha Kitanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maeneo yaliyopata wazabuni, utekelezaji utaanza mapema mwezi wa Desemba, 2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Upande wa Wilaya ya Kibondo, Kampuni ya Simu ya Viettel (Halotel) itajenga mnara ili kufikisha huduma za mawasiliano katika Kijiji cha Kibuye ambapo wanatarajiwa kuanza mwisho wa mwezi Desemba, 2019.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA aliuliza:-

Kumekuwa na usikivu hafifu wa mawasiliano katika baadhi ya visiwa vidogo hapa nchini kama vile Kisiwa kidogo cha Tumbatu:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua tatizo hili?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) atajibu:

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Othman Hija, Mbunge wa Tumbatu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya kufikisha huduma za mawasiliano kote nchini vikiwemo visiwa vidogo. Kwa upande wa Kisiwa cha Tumbatu, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote itafanya tathmini ya kitaalamu kwa kuangalia ukubwa wa eneo, idadi ya wakazi wake pamoja na mahitaji halisi ya ruzuku kwa ajili ya kufikisha huduma ya mawasiliano. Baada ya tathmini hiyo Kisiwa hicho kitaingizwa katika orodha ya miradi ya Mfuko inayosubiri kutekelezwa kulingana na upatikanaji wa fedha za ruzuku hususan kuanzia mwaka huu wa fedha 2019/2020.
MHE. MUSA R. NTIMIZI aliuliza:-

Wananchi wa Kata ya Tura katika Vijiji vya Mwamlela, Mmunyu na Nkongwa hawana kabisa mawasiliano ya simu licha ya umuhimu wa mawasiliano kiusalama na kiuchumi:-

Je, Serikali inatoa ahadi gani ya kupatikana kwa mawasiliano katika vijiji hivyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Musa Ntimizi, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba uniruhusu nitoe ufafanuzi wa Serikali kuhusu hoja iliyojadiliwa jana na baadhi ya wajumbe kuhusu sifa za mtu kuajiriwa kufanya kazi katika Shirika letu la Ndege la ATCL. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika letu la Ndege la ATCL na Serikali kwa ujumla limeainisha sifa mbalimbali zinazomruhusu Mtanzania kuweza kuajiriwa na Shirika hilo la Ndege. Sifa yetu ya kwanza kabisa ni Mtanzania yeyote mwenye umri wa miaka 18 na kuendelea ambaye anafahamu kwa ufasaha lugha mbili za Kiingereza na Kiswahili. Pia Mtanzania huyo anatakiwa awe na Cheti cha Kuongoza Ndege au Cheti cha Kufanya Kazi ndani ya Ndege (cabin crew) ambacho kitakuwa kina mafunzo maalum ya usalama ndani ya ndege lakini na huduma kwa abiria ambao wanatumia ndege ile. Sifa nyingine ya tatu na muhimu kabisa ni lazima awe na leseni ya kuruka inayotolewa na Mamlaka ya Anga au TCAA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sifa ya ziada ni lazima awe na uelewa mkubwa wa masuala ya kitaifa, kidunia, utalii hasa nchini kwetu lakini awe ni mtu awe na hekima, ana discipline na very ethical na tutamchunguza katika hayo kuhakikisha kwamba anaweza kuajiriwa ndani ya Shirika letu la Ndege. Sifa nyingine zote zilizozungumzwa siyo ambazo zinazingatiwa na ATCL wala zinazingatiwa na Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, nijibu swali la Mheshimiwa Musa Ntimizi, Mbunge wa Igalula kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya kufikisha huduma za mawasiliano kote nchini. Mwezi Julai, 2019, Mfuko ulitangaza zabuni ya awamu ya nne kwa ajili ya kufikisha huduma za mawasiliano katika Kata 521 zenye vijiji 1,222. Kata ya Tura ilijumuishwa kwenye zabuni hiyo ikiwa na vijiji vya Karangasi, Mmunyu na Mwamlela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zabuni hiyo ilifunguliwa na baada ya tathmini, tulipata wazabuni katika maeneo hayo. Utekelezaji utaanza baada ya mkataba kusainiwa mwezi Desemba, 2019.
MHE. MUSSA B. MBAROUK aliuliza:-

Katika Vijiji vya Kigombe Wilayani Muheza na Kipumbwi Wilayani Pangani kuna bandari bubu zinazotumika kwa uvuvi na kusafirisha abiria na bidhaa:-

Je, ni lini Serikali itarasimisha bandari hizo kwa kujenga gati pamoja na kituo cha forodha?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Bakari Mbarouk, Mbunge wa Tanga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali ina taarifa ya uwepo wa bandari bubu yaani bandari zisizo rasmi katika Mwambao wa Pwani pamoja na changamoto za kiusalama, kiulinzi na kiuchumi zinazoletwa na bandari hizo.

Mheshimiwa Spika, ili kudhibiti matumizi ya bandari hizo, mamlaka zinazohusika zimeelekezwa kushirikiana na kuweka mikakati ya pamoja ya kudhibiti matumizi ya bandari hizo. Miongoni mwa mikakati hiyo ni pamoja na kutambua bandari zenye umuhimu kwa wananchi kiuchumi na kijamii ili kuzirasimisha kwa kuziweka chini ya uangalizi wa vijiji vilivyo kwenye maeneo husika.

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza maelekezo hayo, Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) ilikamilisha zoezi la kukusanya taarifa za bandari Tanzania Bara na kubaini kuwa kuna bandari zisizo rasmi 208 katika Mwambao wa Bahari ya Hindi. Baada ya zoezi hilo, TPA iliainisha bandari ambazo zinafaa kurasimishwa.

Mheshimiwa Spika, napenda kulitaarifa Bunge lako Tukufu kuwa Bandari za Kigombe na Kipumbwi Wilayani Muheza na Pangani ni miongini mwa bandari 24 zenye umuhimu kwa wananchi kiuchumi na kijamii na zimeorodheshwa kwa ajili ya kurasimishwa.

Mheshimiwa Spika, hatua inayoendelea hivi sasa kuhusu bandari hizo ni kuzipanga katika madaraja (classification) ili kubaini zile ambazo zitachukuliwa na TPA moja kwa moja kwa kuziendesha baada ya kuboreshwa na kuendelezwa kwa miundombinu yake ikiwemo kujenga gati pamoja na kuweka kituo cha forodha, zile ambazo zitaendeshwa kwa mkataba na zile ambazo zitawekwa chini uangalizi wa halmashauri kwa maeneo husika. Kazi hii inatarajiwa kukamilika kabla ya kumalizika kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020.

Mheshimiwa Spika, baada ya urasimishaji huo, usimamizi wa sheria na udhibiti wa maeneo hayo utafuata.
MHE. MATTAR ALI SALUM aliuliza:-

Kampuni ya Azam Marine ambayo inafanya biashara ya kusafirisha abiria kwa kutumia boti kupitia baharini, huuza tiketi kwa abiria kwa ajili ya safari lakini abiria anapochelewa safari tiketi hiyo huwa haitumiki na hivyo kusababisha hasara kwa abiria pamoja na usumbufu;-

(a) Je, Serikali inalijua hilo?

(b) Je, Serikali ina mkakati gani wa kutatua tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mattar, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali ina taarifa ya jambo hili kwa kuwa limekuwa likijitokeza mara kwa mara. Ufuatiliaji uliofanywa na Wizara yangu kupitia TASAC umebaini kuwa Kampuni iliyotajwa ina utaratibu wa namna abiria anavyoweza kuahirisha safari na namna nauli itakavyorejeshwa. Aidha, Kampuni hiyo imekuwa kuahirisha safari na namna nauli itakavyorejeshwa. Aidha, Kampuni imekuwa ikiruhusu abiria kutoa taarifa na kubadili muda wa safari bila gharama ya ziada ikiwa msafiri atatoa taarifa kabla ya chombo kuondoka. Utaratibu huu unatoa fursa kwa kampuni kuuza nafasi iliyoachwa wazi kwa wasafiri wengine ili kuepuka hasara.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa vyombo vya kampuni hii vimesajiliwa katika daftari la usajili linalosimamiwa na Mamlaka ya Bandari Zanzibar (ZMA), Wizara yangu kupitia TASAC itaendelea kufanya ufuatiliaji kwa kushirikiana na Wizara husika Zanzibar kupitia ZMA ili kusimamia utekelezaji wa utaratibu huu wa Kampuni ili uwasaidie abiria wanapoahirisha safari na kutoa taarifa kwa wakati.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA (K.n.y. MHE. EZEKIEL M. MAIGE) aliuliza:-

Ilani ya CCM 2015 – 2020 imeielekeza Serikali ya CCM kujenga upya reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge na Mheshimiwa Rais tayari ameshapata fedha za mkopo kutoka Serikali ya China kwa ajili ya kutekeleza mradi huo.

(a) Je, utekelezaji wa ahadi hiyo ya CCM na Mheshimiwa Rais Magufuli kwa mradi huu umefikia hatua gani?

(b) Kwa kuwa Isaka ni eneo la makutano ya reli ya Tabora – Mwanza na reli mpya (itakayojengwa) kati ya Isaka hadi Keza (Ngara) na hatimaye Kigali – Rwanda; je, Serikali iko tayari kuifanya Isaka kuwa ndiyo karakana kuu ya ujenzi na baadaye ukarabati wa reli hiyo?

(c) Je, Serikali imejipangaje kuwasaidia wananchi waishio jirani na mradi huo ili wanufaike kiuchumi wakati wa ujenzi huo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ezekiel Magolyo Maige, Mbunge wa Msalala kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 – 2020 kwa upande wa uendelezaji wa miundombinu ya uchukuzi, Serikali kupitia Shirika la Reli Tanzania (TRC) inaendelea na ujenzi wa reli ya kisasa yaani standard gauge railway kwa awamu, ambapo awamu ya kwanza ni kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza kilometa 1219; ujenzi wa reli kutoka Tabora hadi Kigoma kilometa 411; Kaliua - Mpanda hadi Karema kilometa 320; Isaka hadi Lusumo - Kabanga kilometa 393 na Uvinza - Kalelema kuelekea Msongati kilometa 150.

Mheshimiwa Spika, hivi sasa ujenzi wa reli awamu ya kwanza umeanza kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro kilometa 300 na utekelezaji wake umefikia asilimia 47.87 kwa mujibu wa taarifa ya mwezi Machi, 2019. Aidha, ujenzi wa kipande cha pili kutoka Morogoro hadi Makutupora ambacho kina urefu wa kilometa 422 ambao umefikia asilimia 7.96 kwa mujibu wa taarifa ya mwezi Machi, 2019.

(b) Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuendelea kuifanya Isaka kuwa bandari kavu yaani dry port kwa ajili ya kuhudumia shehena itakayobebwa na reli ya sasa meter gauge na pia ile ya kisasa ya SGR. Aidha, kwenye mradi wa ukarabati wa reli iliyopo yaani meter gauge kupitia mkopo wa Benki ya Dunia Tanzania Intermodal Railway Project itahusisha ujenzi wa Kituo kikubwa cha kuhudumia shehena.

Mheshimiwa Spika, uamuzi wa kujenga au kutojenga karakana kuu Isaka utafanywa wakati wa kufanya usanifu wa msingi, yaani baseline design kutoka Makutupora hadi Mwanza, kwa sasa reli mpya inayojengwa kutoka Dar es Salaam hadi Makutupora itakuwa na karakana kuu katika eneo la Kwala lililopo Mkoa wa Pwani eneo la Ruvu.

(c) Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwasaidia wananchi waishio jirani na mradi huu kwa kupata manufaa wakati wa ujenzi unaoendelea kwa kuhakikisha kuwa kukamilika kwa mradi huo kutachochea shughuli za ukuaji wa uchumi kwa wananchi waishio jirani na mradi huu na Watanzania wote kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, mradi huu unatarajiwa kutoa ajira kwa wazawa, kutumia malighali za ndani kwa zile zinazopatikana nchini na pia kutoa fursa na kuwajengea uwezo wazawa.
MHE. ZAYNABU M. VULU aliuliza:-

Serikali inajenga reli ya standard gauge na itapitia baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Pwani?

Je, Serikali imeweka mkakati gani wa kuboresha vituo vya zamani na hasa vituo vidogo vidogo ili kuimarisha njia ya usafiri na vituo hivyo vidogo ni vipi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zaynabu Matitu Vulu, Mbunge wa Viti Maalum - Pwani kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuhakikisha kuwa reli iliyopo meter gauge inaendelea kukarabatiwa ili kuhakikisha inatoa huduma za uchukuzi hasa kwa mizigo ya ndani ya nchi, hivi sasa Serikali inaendelea na ukarabati wa reli hii kutoka Dar es Salaam hadi Isaka kupitia mkopo wa Benki ya Dunia wa dola za Kimarekani milioni 300.

Mheshimiwa Spika, kwa ukarabati huo, wakati ukarabati huo unaendelea katika mwaka wa fedha 2019/ 2020 Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kupitia Shirika la Reli Tanzania (TRC) imetenga fedha kupitia kifungu namba 4216 kwa ajili ya kuendelea na ukarabati ikiwemo stesheni ya Soga, Ruvu na Kwala zilizopo katika Mkoa wa Pwani.

Mheshimiwa Spika, pamoja na ukarabati huu, mpango wa Serikali ni kuunganisha stesheni za zamani na mpya zinazoendelea kujengwa kupitia mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa yaani SGR. Yapo maeneo yatakayounganishwa kwa barabara na pia kwa madaraja ya juu kwa baadhi ya maeneo yanayokaribiana na vituo hivyo, kwa mfano, Stesheni ya Soga ya zamani ya Mkoa wa Pwani itaunganishwa na daraja la juu la Stesheni mpya ya SGR.
MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y. MHE. CECILIA D. PARESSO) aliuliza:-

Mfumo wa Vehicle Tracking System umefungwa katika mabasi yote nchini ili kudhibiti mwendokasi kwa lengo la kupunguza ajali za barabarani:-

(a) Je, mfumo umegharimu fedha kiasi gani?

(b) Je, mzabuni wa kazi hii kwa nini hakupatikana kwa ushindani kwa kufuata Sheria ya Manunuzi?

(c) Je, mfumo huu unaendeshwa na kusimamiwa na nani?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Cecilia Daniel Paresso, Mbunge wa Viti Maalum kuhusiana na mfumo wa Kuratibu Mwenendo wa Mabasi (Vehicle Tracking System), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo wa VTS ni mfumo unaowezesha upatikanaji wa taarifa mbalimbali za basi likiwa safarini. Taarifa hizo ni pamoja na mwendokasi, mahali basi lilipo, matukio ya ajali, jina la dereva na kadhalika. Taarifa hizi hupatikana baada ya basi kufungwa kifaa maalum cha mawasiliano kinachochukua matukio na kuyarusha kupitia mfumo wa satelaiti na teknolojia ya Global Postioning System
- GPS pia kupitia mitandao ya simu yenye teknolojia za Global Pocket Radio System - GPRS na hivyo kutoa taarifa za basi husika kwa wakati (real time). Lengo la kuweka mfumo huo pamoja na mambo mengine ni kudhibiti matukio ya ajali.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo ya utangulizi, sasa naomba nijibu swali la Mheshimiwa Cecilia Daniel Paresso, kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Mfumo wa VTS uligharimu kiasi cha shilingi bilioni 2.4 ambazo zilitokana na mapato ya Serikali kupitia SUMATRA.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, mzabuni aliyefanya kazi hii ni Kampuni ya BSMART Technologies ya Malaysia akishirikiana na Kampuni ya Computer Center ya hapa nchini na alipatikana kwa njia ya ushindani kwa mujibu wa kifungu cha 150 cha Kanuni ya Sheria ya Manunuzi, Tangazo la Serikali No.446 la mwaka 2013. Zabuni hiyo ilitangazwa kupitia zabuni ya kimataifa Na.AE/025/2015-2016/HQ/G/22 katika gazeti la Daily News la tarehe 14 Januari, 2016 pia kupitia PPRA Tender Portal, Tanzania Procurement Journal Toleo No. ISS:1821 VOL IX-No.3 pia zabuni ilitangazwa kwenye tovuti ya SUMATRA.

(c) Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo huu unasimamiwa na kuendeshwa na SUMATRA kupitia kituo maalum kilichoko Mikocheni Jijini Dar es Salaam. Hata hivyo, SUMATRA imeingia mkataba na Kampuni ya TERA Technologies and Engineering Company kwa ajili ya kufunga vifaa hivyo kwenye magari. Kampuni hiyo ilipatikana kwa ushindani kupitia zabuni (Invitation for Tenders Na.AE/025/2016- 2017/HQ/G/39 ya tarehe 25 Oktoba, 2017 ambayo pia ilitangazwa kupitia PPRA Tender Portal, Tanzania Procurement Journal na kwenye tovuti ya SUMATRA.
MHE. ALEX R. GASHAZA aliuliza:-

Wakati wa Mkutano wa Bunge wa Bajeti niliwasilisha Orodha ya Vijiji 11 vinavyohitaji kujengewa minara ambavyo ni Chivu, Runzenze, Kigina na Ntoboye Kata ya Ntoboye, Murubanga, Kititiza, Kumubuga Kata ya Nyamagoma, Kijiji cha Mukalinzi Kata ya Muganza na Kijiji cha Ruhuba Kata ya Mbuba:-

Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa minara hiyo ili kurahisisha mawasiliano kwa wananchi wa vijiji hivyo hasa ikizingatiwa kuwa vijiji hivyo viko pembeni mwa Jimbo na hali ya usalama katika maeneo hayo siyo nzuri?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Alex Raphael Gashaza, Mbunge wa Ngara, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Kata za Ntoboye, Nyamagoma, Muganza na Mbuba zipo pembezoni mwa Jimbo la Ngara. Katika Kata ya Mbuba, vijiji vya Kumwendo, Mbuba na Kanyinya tayari vimepata mawasiliano. Pia Kata ya Muganza Kijiji cha Mukabu kimepata huduma ya mawasiliano pia. Aidha, Kijiji cha Mukalinzi utekelezaji wa upelekaji mawasiliano utakamilika mwezi Septemba mwaka huu 2019 ambapo ruzuku ilitolewa kwa Kampuni ya Viettel au Halotel.

Mheshimiwa Naibu Spika, Vijiji vya Chivu, Runzenze, Kigina na Ntoboye Kata ya Ntoboye, Murubanga, Kititiza, Kumubuga Kata ya Nyamagoma na Kijiji cha Ruhuba Kata ya Mbuba vitafanyiwa tathmini kwa kuangalia mahitaji halisi na kisha kuingizwa katika orodha ya miradi itakayotekelezwa katika mwaka wa fedha 2019/2020.
MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:-

Katika kukabiliana na ushindani na Bandari za nchi jirani, Mamkala za Usimamizi wa Bandari Tanzania ina mpango wa kuanzisha bandari kavu katika eneo la kimkakati la Inyala lililopo Wilaya ya Mbeya:-

(a) Je, ni lini tathmini ya fidia kwa wananchi itakamilika?

(b) Je, ni lini ujenzi wa Bandari Kavu ya Inyala utaanza;

(c) Je, kuna mkakati wa ujenzi wa reli kuunganisha Bandari Kavu ya Inyala na Bandari ya Itungi (Kyela)?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

(a) Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA) ina mpango wa kujenga Bandari Kavu katika eneo la kimkakati la Inyara, Mbeya ili kuhudumia wateja wa Zambia, Malawi, DRC na wafanyabiashara wa Tanzania kutoka Nyanda za Juu Kusini ili kukabiliana na ushindani na bandari za nchi jirani. Katika bajeti ya mwaka 2019/2020 TPA imepanga kufanya upembuzi yakinifu katika eneo lenye ukubwa wa ekari 100 ili kubaini mahitaji halisi na eneo linalofaa kwa ajili ya kujenga Bandari Kavu. Baada ya kukamilisha zoezi hilo, uthamini utafanyika na baada ya kukamilika taratibu za kulipa fidia kwa wananchi watakaopisha mradi huo zitaanza.

(b) Ili Bandari Kavu itakayojengwa ilete tija, mpango wa Serikali kupitia TAZARA ni kufanya upembuzi yakinifu kwa lengo la kutandika reli kuelekea kwenye eneo itakapojengwa Bandari Kavu ya Inyala. Mpango huu unatarajiwa kuanza katika mwaka wa fedha 2020/21.

(c) Mkakati uliopo ni kuunganisha Bandari Kavu ya Inyala na Itungi iliyoko Kyela kwa reli ya TAZARA ili kuweza kuhudumia nchi jirani za DRC, Zimbabwe, Malawi na Zambia.

Hata hivyo, mkakati huu utaanza kutekelezwa baada ya kukamilika kwa ujenzi wa kipande cha reli ya TAZARA.