Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Daniel Nicodemus Nsanzugwako (17 total)

MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-
Mkoa wa Kigoma unaongoza kwa kuwa na vijana wengi wanamichezo na wasanii mfano Shaaban Robert, Diamond, Ali Kiba, Banana Zoro, Linex, Mrisho Mpoto na kadhalika:-
(a) Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika Mkoa wa Kigoma kwa kujenga Jumba la Sanaa (Theater Centre) ili vijana wa aina hii wawe na sehemu nzuri ya kuendesha shughuli zao?
(b) Kama Serikali inakubaliana na hoja hiyo, kituo hicho kitaanza kujengwa lini?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inatambua mchango mkubwa wa wasanii mashuhuri wenye asili ya Mkoa wa Kigoma kama vile Diamond, Ali Kiba, Banana Zoro, Mrisho Mpoto japokuwa nimepata taarifa kwamba huyu Mrisho Mpoto origin yake ni Mkoa wa Ruvuma na wengine ambao wameiletea sifa na kuitambulisha nchi yetu katika fani ya muziki na sanaa.
Mheshimiwa Spika, katika Sera ya Utamaduni ya mwaka 1999, Sura ya 4, kipengele Na.4.1.9 inasema, Serikali itahakikisha kuwa panakuwa na jengo la kisasa la sanaa za maonesho katika ngazi ya Taifa. Aidha, wananchi watahamasishwa kuhakikisha kwamba wanatenga maeneo ya maonesho.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inaendelea kuhimiza Halmashauri na Manispaa zote nchini kutenga maeneo ya kujenga vivutio vya sanaa. Kuhusu Mkoa wa Kigoma, tunashauri Serikali ya Mkoa kwa kushirikisha Halmashauri zote za Mkoa huo ione umuhimu na namna bora ya kupanga na kutekeleza ujenzi wa Jumba la Sanaa. Aidha, tunatoa wito kwa Halmashauri zote nchini zione umuhimu wa kujenga majengo hayo.
(b) Mheshimiwa Spika, kazi ya kujenga miundombinu katika Halmashauri mbalimbali nchini ni jukumu la Halmashauri husika. Hivyo kila Halmashauri inashauriwa kutenga fedha katika bajeti zao kwa ajili ya Maendeleo ya Sanaa.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-
Mkoa wa Kigoma ni kati ya Mikoa mitatu inayopata mvua nyingi katika nchi yetu kwa wastani na takribani milimita 1,300 kwa mwaka ikifuatiwa na Mkoa wa Katavi.
(a) Je, ni kwanini Serikali haifanyi jitihada ya kuwekeza katika kilimo ili kunufaika na uwepo mzuri wa hali ya hewa?
(b) Je, ni kwanini Mkoa wa Kigoma uliondolewa katika Mikoa na yenye uzalishaji mkubwa na kupata mgao mdogo wa pembejeo?
(c) Je, ni kwanini kituo cha Mbegu cha Bugaga kilichopo Wilaya ya Kasulu kimetekelezwa.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi ningependa kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa kwa siku za nyuma Mikoa ya pembezoni ukiwepo Mkoa wa Kigoma imekuwa na changamoto nyingi za kimaendeleo kutokana na kukosekana kwa miundombinu muhimu kwa maendeleo. Serikali imefanya jitihada kubwa kuwezesha uwekezaji katika Mikoa hii ikiwa ni pamoja na kukamilisha ujenzi wa miundombinu muhimu kama barabara.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa katika Mkoa wa Kigoma, zinaendelea tafiti mbalimbali za kilimo kwa kushirikiana na wadau wengine kama vile kampuni ya Kigoma Sugar kwa zao la Miwa, na Belgium Technical Cooperation kwa zao la chai kabla ya kuanza kuhamasisha sekta binafsi kwa uzalishaji mkubwa. Aidha, Mkoa wa Kigoma uko katika mpango wa BRN katika kilimo cha miwa (Sugarcane Cluster) ambapo katika mpango huo, mashamba makubwa mawili yameshatambuliwa na wawekezaji kama vile Kigoma Sugar wameshaonyesha nia ya kuzalisha sukari kwa kushirikiana na wakulima wadogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kigoma umepewa kipaumbele kwa upande wa ruzuku ya pembejeo ambapo ni kati ya Mikoa mitano iliyopewa ruzuku kubwa ya pembejeo kwa msimu wa 2015/2016 kati ya Mikoa 24 Nchini. Hii ni kutokana na umuhimu wake katika uzalishaji mkubwa wa chakula hasa mahindi hapa Nchini. Idadi ya kaya zilizopata ruzuku ya pembejeo za kilimo katika Mkoa wa Kigoma imeongezeka kutoka kaya 60,239 msimu wa 2013/2014 na kufikia kaya 74,000 msimu wa 2015/2016. Aidha, mgao mdogo wa ruzuku ya pembejeo za kilimo kwa wakulima kila Mkoa ikilinganishwa na mahitaji hutokana na ufinyu wa bajeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, shamba la kuzalisha mbegu la Bugaga lenye ukubwa wa hekta 336.906 limekaa muda mrefu bila kuzalisha mbegu kutokana na ufinyu wa fedha. Wizara imeweka mkakati wa kulifufua shamba hilo katika msimu wa 2016/2017 ili liweze kuzalisha mbegu kwa wingi kwa ajili ya wakulima wa Kanda ya Magharibi ikiwemo Wilaya ya Kasulu. Aidha, Serikali inahimiza makampuni na vikundi mbalimbali Mkoani Kigoma kushirikiana na ASA katika shughuli za uzalishaji mbegu za mazao mbalimbali ili kuchangia maendeleo ya kilimo katika Mkoa wa Kigoma.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-
Mji wa Kasulu ni Mji wa siku nyingi sana tangu enzi za Wajerumani lakini hauna mtandao wa maji unaokidhi mahitaji ya wakazi wa mji huo:-
(a) Je, ni lini Serikali itakarabati vyanzo vya maji vilivyopo ili maji yafike katika mitaa ya Kata za Mrusi, Mwilavya na Kidyama?
(b) Je, ni kwanini Serikali haitoi fedha ili kujenga tenki la kusafisha maji kwa sababu maji yaliyopo ni machafu?
(c) Je, ni kwanini Serikali haitoi pesa ili chanzo kingine kilichoainishwa kijengwe?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini, lenye sehemu(a) (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto ya mtandao wa maji inayoukabili Mji wa Kasulu. Katika mwaka wa fedha 2016/2017 imetenga shilingi milioni 200 kwa ajili ya kupanua mfumo wa usambazaji maji katika Mji huo. Fedha hizi zitatumika kwa ajili ya kuboresha hali ya huduma ya maji ikiwemo kuongeza mtandao wa maji Mjini Kasulu ambapo pia Kata za Mrusi, Mwilavya na Kidyama zitapata huduma ya maji safi na salama.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali pia imekamilisha usanifu na uandaaji wa makabrasha ya zabuni kwa ajili ya mradi wa maji safi Mjini Kasulu. Usanifu huo pia umehusisha chujio la kutibu maji katika Mji wa Kasulu. Kwa sasa andiko la mradi limewasilishwa Tume ya Mipango kwa ajili ya kuombea ufadhili kutoka Serikali ya India. Gharama za mradi huo ni kiasi cha Dola za Marekani shilingi milioni 9.89.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu katika kipengele (b) hapo juu, Serikali inaendelea kutafuta fedha za ujenzi wa mradi huo kupitia ufadhili au mkopo nafuu kutoka Serikali ya India. Fedha hizi zikipatikana, ujenzi wa chanzo kingine utafanyika.
MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITILE (K.n.y MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO) aliuliza:-
Miji mingi nchini inakabiliwa sana na uhaba wa Maafisa Ardhi na Maafisa Mipango Miji.
(a) Je, ni kwa nini Serikali isianzishe utaratibu wa kuajiri Maafisa hawa moja kwa moja wanapohitimu Vyuo Vikuu?
(b) Je, ni kwa nini Serikali isichukue jukumu la kununua vifaa vya kupimia ardhi kama vile darubini, GPS na kadhalika na kuvisambaza kwenye Miji yetu ikiwemo Mji wa Kasulu?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna upungufu mkubwa wa wataalam katika sekta ya ardhi na tafiti zinaonesha kwamba hadi kufikia Machi, 2016 idadi ya wataalam wa sekta ya ardhi kwa maana ya Maafisa Ardhi, Mipango Miji na Wapima Ardhi, Wathamini na Mafundi Sanifu katika Halmashauri 161 ilikuwa ni 1,087 ukilinganisha na mahitaji ya wataalam 3,040. Idadi hii ni sawa na asilimia 36 ya mahitaji kamili ya watumishi hao. Tafsiri ya mapungufu haya imekuwa ikionekana katika kiwango kidogo cha upangaji, upimaji na umilikishwaji wa ardhi iliyopimwa mijini na vijijini.
(a) Mheshimiwa Spika, kuhusu utaratibu wa kuajiri maafisa moja kwa moja wanapohitimu Vyuo Vikuu, Serikali imekuwa ikichukua jitihada mbalimbali ili kukabiliana na tatizo hilo. Mathalani katika kipindi cha mwaka huu wa fedha 2016/2017 Wizara yangu imeomba kibali cha kuajiri watumishi wapya 252 katika sekta ya ardhi. Kama kibali hicho cha kuajiri kitapatikana basi nina uhakika pengo litapungua ingawa ni kwa kiasi kidogo.
Hata hivyo nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kuliona hili na nimwahidi kuwa Serikali imechukua wazo lake na pia itaendelea kulifanyia kazi.
(b) Mheshimiwa Spika, kuhusu ununuzi wa vifaa vya upimaji, Wizara yangu tayari imetenga kiasi cha shilingi bilioni nane katika bajeti ya mwaka 2016/2017 kwa ajili ya kununua vifaa vya upimaji ambavyo vitasambazwa katika ofisi zetu za Kanda na hata hivyo Halmashauri za Wilaya, Miji na Majiji ndizo zenye dhamana ya kusimamia upimaji wa ardhi kwenye maeneo yao, hivyo zinapaswa kutenga fedha kwa ajili ya kununua vifaa vya upimaji. Aidha, katika kukabiliana na upungufu wa vifaa vya upimaji, Wizara imekuwa ikinunua vifaa vya kupimia ardhi na kuvisambaza kwenye Halmashauri kila fedha zinapopatikana.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-
Katika Mto Malagarasi iko miradi mikubwa mitatu ambayo ni mradi wa kutoa maji Mto Malagarasi kwenda katika vijiji 69 vilivyopo Wilaya ya Urambo, uwekezaji katika kilimo cha umwagiliaji wa miwa na mradi wa uzalishaji wa umeme wa megawati 44.5.
(a) Je, Mto Malagarasi una ujazo gani wakati wa masika na kiangazi?
(b) Je, maji ya mto huo yanatosheleza mahitaji ya miradi hiyo mitatu?
(c) Je, Serikali imefanya utafiti wa kiufundi kujua bajeti ya maji katika mto huo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imepanga kutekeleza miradi mbalimbali kwa kutumia Mto Malagarasi, ikiwemo mradi wa maji kwa ajili ya Miji ya Urambo na Kaliua, kilimo cha umwagiliaji na uzalishaji umeme wa megawati 44.5. Wakati wa masika mto huu unakuwa na maji yanayotiririka kwa mita za ujazo 55 kwa sekunde; na wakati wa kiangazi unakuwa na mita za ujazo 40 kwa sekunde.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji Awamu ya Kwanza imekamilisha mipango ya pamoja ya uendelezaji na usimamizi wa rasilimali za maji katika Bonde la Ziwa Tanganyika ambako Mto Malagarasi unapatikana. Hii ni sehemu ya utafiti wa kiufundi wa kujua wingi na ubora wa maji pamoja na mgawanyo sawia wa matumizi ya maji katika Bonde dogo la Mto Malagarasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika utafiti huo, umeonesha ya kuwa Mto Malagarasi una maji ya kutosha kwa miradi mbalimbali itakayoibuliwa ikiwemo miradi mitatu iliyotajwa na bado yatabaki kuelekea yakitiririka kwenda Ziwa Tanganyika.
MHE. KABWE Z. R. ZITTO (K.n.y MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO) aliuliza:-
Hivi sasa yapata miaka 11 utafiti wa mafuta na gesi katika mwambao wa Ziwa Tanganyika kwenye maeneo ya Kigoma, Rukwa na Katavi umefanyika au unaendelea kufanyika.
(a) Je, ni nini hali ya utafiti huo?
(b) Bonde la Mto Malagarasi nalo limefanyiwa utafiti
wa mafuta na gesi; je, hali ya utafiti huo ikoje?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodem Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini, lililoulizwa kwa niaba yake na Mheshimiwa Kabwe Zuberi Zitto, Mbunge wa Kigoma, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni ya Beach Petroleum
ya nchini Australia ilianza kufanya utafiti wa mafuta na gesi Kusini mwa Ziwa Tanzanyika tangu mwaka, 2010. Kampuni hiyo ilifanya utafiti na kukusanya data ambazo kimsingi ziliwezesha kupatikana taarifa za uchunguzi pamoja na utafiti. Kampuni hiyo imeshindwa kuanza kuchimba gesi kwa sababu zifuatazo:-
Kwanza kabisa ni kwa sababu ya kupanda kwa gharama za uwekezaji, lakini pia kupanda na kushuka kwa bei za mafuta duniani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 10 Oktoba, 2016, Serikali za Tanzania na DRC ziliingia makubaliano ya (MoU) ya kufanya utafiti wa mafuta na gesi pamoja katika Ziwa Tanganyika. Maeneo makubwa ambayo yamekubalika kufanyiwa kazi ni pamoja na kutathmini kwa pamoja data za kijiolojia pamoja na kijiofizikia ili kutambua ukubwa wa mashapo ambayo yatavuka mpaka, vilevile kuandaa jinsi zitakavyofanya kazi kwa ushirikiano. Nchi za Burundi na Zambia nazo zimeomba kuingizwa katika makubaliano hayo ili kufanya utafiti katika ziwa lote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kampuni ya Motherland Industries ya nchini India iliingia ubia na Serikali kupitia TPDC kufanya utafiti wa mafuta na gesi asilia katika eneo la Bonde la Mto Malagarasi mwaka 2012. Kufuatia kushuka kwa bei ya mafuta duniani tangu wakati huo, kampuni imeshindwa kukamilisha majukumu yake ya kazi kama ilivyokubalika kwenye mkataba wa Production Sharing Agreement, kutokana na hatua hiyo, Serikali inakusudia sasa kurudisha eneo hilo kwa ajili ya utangazaji na wawekezaji wengine wapya.
MHE. PETER J. SERUKAMBA (K.n.y. MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO) aliuliza:-
Athari za mazingira ni kubwa na vyanzo vingi vya mito (water sources) vimeathirika sana (mfano Mto Makere):-
Je, Serikali ina mpango gani wa muda mfupi na mrefu wa kukabili hali hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ruhusa yako, napenda nichukue fursa hii ya mwanzo kabisa kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuniamini na kuniteua kwenye Baraza lake. Nishukuru pia Wabunge wenzangu ambao wamenipa ushirikiano na wewe mwenyewe Mwenyekiti ulikuwa mjumbe mwenzangu wa Tume kwenye Utumishi wa Bunge, nakushukuru sana kwa ushirikiano ulionipa. Niwashukuru wananchi wa Mwibara pia kwa kunifanya Mbunge wao na Rais akaniona. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), sasa naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwako, Mbunge wa Kasulu Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukabiliana na uharibifu wa mazingira ya ardhi na vyanzo vya maji, Serikali ilipitisha Mkakati wa Kuhifadhi Mazingira ya Ardhi na Vyanzo vya Maji wa mwaka 2006. Mkakati huu umeainisha hatua za muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu za kukabiliana na uharibifu wa mazingira ya ardhi na vyanzo vya maji. Aidha, mwaka 2008, Serikali iliandaa Mkakati wa Hatua za Haraka za Kuhifadhi Mazingira ya Bahari, Maziwa, Mabwawa na Mito ili kuhifadhi maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2012, Serikali ilipitisha kwa ajili utekelezaji Mkakati wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi. Aidha, mwaka 2016, Serikali ilielekeza utekelezaji wa Programu ya Kupambana na Kuenea kwa Hali ya Jangwa na pia Serikali inakusudia kuzuia matumizi ya kuni kwenye taasisi za umma ili zianze kutumia nishati mbadala. Mikakati yote hii inalenga kukabiliana na athari za uharibifu wa mazingira na vyanzo vya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua za muda mfupi zilizoainishwa na mkakati wa mwaka 2006 ni pamoja na kuwaondoa wafugaji waliovamia mabonde na maeneo ya vyanzo vya maji; kusimamisha shughuli zote za kilimo na kuwaondoa wavamizi kwenye maeneo yaliyoharibika sana; kuzitaka taasisi na watumiaji wengine wakubwa wa miti, kuni na mkaa kuwa na mshamba yao ya miti; kudhibiti shughuli za umwagiliaji usio endelevu na kuzitaka wilaya zote kubainisha vyanzo vya maji na kufanya tathmini ya hali ya mazingira yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua zingine ni kudhibiti matukio ya uchomaji moto wa misitu; kupiga marufuku upandaji wa miti isiyofaa katika maeneo ya vyanzo vya maji; kuendeleza Kampeni ya Taifa na Kupanda na Kutunza Miti; Kuendeleza Program ya Kitaifa ya Elimu ya Mazingira kwa Umma; kuwa na programu za hifadhi ya mazingira na mipango shirikishi ya matumizi bora ya ardhi kwa kila wilaya na kutekeleza na kupiga marufuku uchimbaji holela wa madini kwenye vyanzo vya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua za muda wa kati ni pamoja na kujenga na kuendeleza malambo, visima na mabwawa katika maeneo ya wafugaji na wakulima; kuhuisha na kusambaza kwa mpango kabambe wa matumizi ya ardhi ili uanze kutumika mara moja na kuianisha na kuondoa miti isiyofaa kwenye vyanzo vya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua za muda mrefu ni pamoja na kuendeleza teknolojia sahihi za kuvuna, kuhifadhi na kusambaza maji ya mvua na ya ardhini, kuharakisha matumizi ya njia mbadala za kuzalisha umeme ili kupunguza gharama za umeme kwa watumiaji na hatimaye kupunguza mahitaji ya kuni na mkaa. Aidha, Serikali imeanzisha Tuzo ya Rais ya Kuhifadhi Vyanzo vya Maji, Kupanda na Kutunza Miti. Lengo la tuzo hii ni kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika kuhifadhi mazingira ya ardhi na vyanzo vya maji. Tuzo hii hutolewa kila baada ya miaka miwili.
MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA (K.n.y. MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO) aliuliza:-
Ibara ya 89 hadi 101 ya Mkataba ulioanzisha Jumuiya ya Afrika Mashariki inazitaka nchi wanachama wa Afrika Mashariki kubadilishana uzoefu (exchange of information on technological development and research findings).
(a) Je, ni taarifa zipi kiutafiti ambazo nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki zimeshirikiana?
(b) Je, ni taarifa zipi za sekta ya kilimo na mifugo ambazo nchi zimeshirikiana?
(c) Je, ni watumishi wangapi waandamizi kutoka Tanzania ambao wamepata ajira katika Jumuiya ya Afrika Mashariki?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ruhusa yako na kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzungwanko, Mbunge wa Kasulu, lenye vipengele (a), (b) na (c), naomba kutoa maelezo mafupi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 89 hadi ya 101 ya Mkataba ulioanzisha Jumuiya ya Afrika Mashariki inazitaka nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kubadilishana uzoefu na kushirikiana katika uendelezaji wa sekta ya uchukuzi kwa maana ya barabara, reli, bandari, usafiri wa anga na majini, taratibu za usafirishaji wa shehena, huduma za posta na simu, mawasiliano, hali ya hewa na nishati. Aidha, Ibara ya 103 ya Mkataba huo imeweka misingi ya ushirikiano kwenye sayansi na teknolojia ikiwemo kubadilishana taarifa za utafiti wa kisayansi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo haya mafupi, naomba kujibu swali sasa la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsazungwanko, Mbunge wa Kasulu, lenye vipengele (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zinashirikiana katika kuandaa taarifa za kitafiti hususani katika hatua za upembuzi yakinifu na usanifu wa miradi ya kikanda inayotekelezwa kwa pamoja miongoni mwao kama vile Mpango wa Uendelezaji wa Mtandao wa Barabara na Reli wa Afrika Mashariki.
Aidha, nchi wanachama zinashirikiana kwenye tafiti za kuandaa sera, mikakati, sheria za Jumuiya ili kupata matokeo tarajiwa. Vilevile nchi wanachama zimeanzisha Kamisheni ya Pamoja ijulikanayo kama Kamisheni ya Afrika Mashariki ya Sayansi na Teknolojia ambapo makao yake makuu yapo Jijini Kigali, Rwanda. Uwepo wa Kamisheni hii utaiwezesha nchi wanachama kufanya utafiti kwa pamoja, kubadilishana uzoefu na hata kunufaika pamoja kutokana na matokeo ya tafiti hizo.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 105 ya Mkataba ya Jumuiya ya Afrika Mashariki inazitaka nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kushirikiana katika sekta ya kilimo na mifugo. Katika eneo hili nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zimeendelea kushirikiana katika masuala yanayohusu mbegu, madawa ya mimea na mifugo, usalama wa chakula na udhibiti wa magonjwa ya wanyama na mimea.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na muundo wa utumishi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, Jumuiya ina nafasi tano za Maafisa Waandamizi Wateule ambapo Tanzania inashikilia nafasi mbili ambazo ni Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Masuala ya Mipango na Miundombinu na Mwakilishi wa Majeshi. Kwa upande wa nafasi zinazojazwa kupitia ushindani ambazo ni Wakuu wa Taasisi za Jumuiya katika nafasi saba Tanzania ina nafasi mbili ambazo ni Mtendaji Mkuu wa Kamisheni ya Utafiti wa Afya na Naibu Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uvuvi wa Ziwa Victoria. Kwa upande wa nafasi za Wakurugenzi, kati ya nafasi 12 katika Jumuiya Tanzania ina nafasi nne.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maelezo hayo tuna jumla ya Watanzania nane wanaoshikilia nafasi ya watumishi waandamizi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na taasisi zake.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-
Mahakama ya Wilaya ya Kasulu ni ya zamani sana, ni chakavu sana na wakati mwingine huduma hazitolewi kabisa.
• Je, ni kwa nini Serikali imeitelekeza Wilaya ya Kasulu?
• Je, mahakama hiyo itajengwa lini?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzungwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa jengo la Mahakama ya Wilaya ya Kasulu ni chakavu. Hata hivyo, mpango wa Serikali kwa mwaka wa fedha 2016/2017 ilikuwa ni kujenga upya jengo la Mahakama ya Wilaya ya Kasulu ambapo hadi sasa mkandarasi wa ujenzi huo ameshapatikana na anategemea kuingia makubaliano ya ujenzi huo mwishoni mwa mwezi huu wa Juni, 2017. Hivyo napenda kumuhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa kwa mwaka wa fedha 2017/2018 Mahakama itaanza utetelezaji wa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Kasulu.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-
Katika nchi yetu suala la usawa na haki kwa wananchi wetu ni jambo linalozingatiwa sana na utawala wa Serikali ya Awamu ya Tano; taarifa ya hali ya umaskini nchini imebainisha kwamba ipo mikoa minne ambayo kiwango cha umaskini kipo juu sana na mojawapo ya mikoa hiyo ni Kigoma.
Je, ni hatua zipi za makusudi (kibajeti) zinazochukuliwa ili Mkoa wa Kigoma ujinasue na hali ya umaskini ambayo kwa kiasi cha asilimia 80 umesababishwa na madhila ya kihistoria (historical injustices) na Serikali kuacha au kushindwa kujenga miundombinu ya maendeleo kama barabara, vituo vya afya na kadhalika?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 Wizara ya Fedha na Mipango, Idara ya Kuondoa Umaskini kwa kushirikiana na REPOA ilifanya uchambuzi wa kina wa hali ya umaskini kwa lengo la kupata takwimu za hali ya umaskini katika ngazi ya Mikoa na Wilaya (poverty mapping). Kwa mujibu wa takwimu zilizopatikana, Mkoa wa Kigoma ulikuwa na kiwango kikubwa cha watu wanaoishi chini ya mstari wa umaskini cha asilimia 48.9.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kulitaarifu Bunge lako tukufu na Watanzania kwa ujumla kwamba siyo kweli kwamba Serikali iliacha au kushindwa kujenga miundombinu ya maendeleo kama barabara, vituo vya afya na kadhalika katika Mkoa wa Kigoma na hivyo kusababisha watu wa Kigoma kuwa maskini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ya maendeleo iliyotekelezwa na Serikali katika Mkoa wa Kigoma ni pamoja na Daraja la Jakaya Kikwete katika Mto Malagarasi, Kivuko cha MV Malagarasi, barabara ya Kidahwe hadi Uvinza, Kigoma – Kidahwe na Mwandiga – Manyovu. Aidha, miradi ya barabara inayoendelea ni pamoja na Kidahwe – Kasulu, Kibondo – Nyakanazi na Kibondo – Mabamba mpaka mpakani mwa Burundi. Miradi mingine ni kukamilika kwa ujenzi wa majengo ya kitega uchumi ya NSSF na NHC, miradi ya umeme vijijini na uwanja wa ndege Kigoma awamu ya kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii yote imelenga kufungua fursa za kiuchumi kwa Mkoa wa Kigoma na hivyo kuongeza kasi ya kupunguza umasikini wa kipato kwa wananchi wa Kigoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa miaka mitano (2016/2017 hadi 2020/2021), Serikali imepanga kuendeleza eneo maalum la uwekezaji Kigoma, upanuzi na uboreshaji wa bandari ya Kigoma, ujenzi na upanuzi wa uwanja wa ndege wa Kigoma, ujenzi wa mradi wa kuzalisha megawati 44.7 za umeme wa maji kutoka mto Malagarasi na kuunganishwa na Gridi ya Taifa ifikapo mwaka 2020.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia imepanga kujenga reli ya Kisasa na kuimarisha reli ya zamani na kununua vichwa 63 vya treni na mabehewa ya mizigo 1,960 kwa ajili ya kuimarisha shughuli za usafiri na usafirishaji kwa watu, bidhaa na huduma ifikapo mwaka 2020. Ni matarajio yetu kuwa kukamilika kwa miradi niliyoitaja kutafungua fursa za kiuchumi, kuongeza ajira na kupunguza umaskini kwa kiwango kikubwa katika Mkoa wa Kigoma.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-
Takwimu za Mpango wa Maendeleo 2016/2017 zimeonesha kuwa Mkoa wa Kigoma ni miongoni mwa Mikoa mitano (5) iliyo maskini zaidi nchini:-
• Je, Serikali inafanya nini kuhakikisha Mikoa hiyo inapata rasilimali fedha na watu ili iweze kuondokana na hali hiyo ya umaskini?
• Je, nini kifanyike kwa Mkoa wa Kigoma ili kujenga ulinganifu katika maendeleo?
• Je, kwa nini Serikali isitenge shilingi bilioni 5 kwa kila mwaka kwa kila Mkoa ili kuondoa kitisho cha Mikoa hiyo kuachwa nyuma kimaendeleo?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel N. Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasuli Mjini, lenye vipengele (a), (b), (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Serikali yetu huzingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo, Ilani ya Uchaguzi ya Chama Tawala, Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano na mwaka mmoja mmoja pamoja na Mwongozo wa Bajeti kugawa rasilimali fedha na watu ili kukabiliana na changamoto za umaskini. Aidha, mgawanyo wa rasilimali fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo huenda sambamba na mgawanyo wa rasilimali watu kwa ajili ya utekelezaji, usimamizi, uperembaji na kutoa huduma kulingana na aina ya miradi.
(b) Mheshimiwa Spika, katika kujenga ulinganifu wa maendeleo katika Mkoa wa Kigoma, Serikali imebainisha maeneo na miradi ya kimkakati kwa ajili ya utekelezaji ili kufungua fursa za kiuchumi. Miongoni mwa maeneo ya kimkakati yaliyobainishwa na kuanza kutekelezwa kwenye Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2016/ 2017 – 2020/2021 ni Mradi wa Upanuzi wa Ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kigoma; Mradi wa Uzalishaji wa Umeme wa Maji katika maporomoko ya Mto Malagarasi MW 44.7; kuanzisha na kuendeleza Eneo la Uwekezaji Kigoma (Special Economic Zone); Mradi wa Gridi ya Kaskazini Magharibi KV400; na ujenzi wa Reli ya Kati kwa Kiwango cha Kimataifa.
(c) Mheshimiwa Spika, mgawanyo wa rasilimali fedha huainishwa kwenye Mwongozo wa Bajeti ya Serikali kwa kila mwaka ambao huandaliwa kwa kuzingatia vipaumbele vilivyoainishwa kwenye Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano; Dira ya Taifa; na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Tawala. Hoja ya kutenga shilingi bilioni 5 kwa kila Mkoa, kila mwaka ni lazima ifungamanishwe na Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Tawala. Hivyo basi, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa, kwa sasa Serikali haina Sera wala Mwongozo wa kutenga shilingi bilioni 5 kwa kila mwaka, kwa kila Mkoa ili kukabiliana na changamoto za umaskini.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE (K.n.y. MHE. DANIEL NSANZUGWANKO) aliuliza:-
Mkoa wa Kigoma hususan Wilaya za Kasulu na Kibondo zimekuwa makazi ya wakimbizi kwa muda mrefu sana.
Je, ni lini Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na UNHCR itakuja na mpango kabambe wa kusaidia maeneo yaliyoathiriwa na ujio wa wakimbizi hao (a comprehensive plan and support for refugee affected areas)?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli baadhi ya maeneo ambayo hupokea wakimbizi nchini hupata athari mbalimbali ikiwemo uharibifu wa mazingira. Hata hivyo, Serikali kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Kuhudumia Wakimbizi Duniani (UNHCR) inatekeleza mipango mbalimbali inayolenga kuboresha huduma kwenye jamii katika Wilaya zinazohifadhi wakimbizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Wilaya za Kibondo na Kasulu huduma ambazo zimekuwa zikiboreshwa ni pamoja na afya, elimu, kilimo, masoko, ujasiriamali pamoja na hifadhi ya mazingira.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-

Wafungwa wakimbizi toka nchi za Burundi na DRC wamekuwa wakijaza mahabusu na magereza yetu:-

(a) Je, kwa nini Serikali isikubaliane na nchi za Burundi na DRC kubadilishana wafungwa ili wakimbizi hao wafungwe katika nchi zao?

(b) Je, wafungwa wa aina hiyo wanapokuwa mahabusu na magereza, Shirika la UNHCR linachangia gharama kwa kiasi gani?

(c) Je, UNHCR imechangia fedha kiasi gani kwa wafungwa wakimbizi waliofungwa au kuwekwa mahabusu nchini kuanzia mwaka 2017/2018?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nichodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimwa Mwenyekiti, suala la kubadilishana wafungwa baina ya nchi moja na nyingine huongozwa na mkataba wa makubaliano ulioingiwa baina ya nchi moja na nyingine. Lengo la mkataba huo ni kumpa fursa mfungwa anayetumikia kifungo chake gerezani kutumikia sehemu ya kifungo chake kilichobaki katika nchi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ieleweke kuwa ni utamaduni wa kisheria duniani kwamba mahabusu na mfungwa bila kujali kama ana hadhi ya ukimbizi, wanapopokelewa na kuhifadhiwa katika magereza, jukumu la kuwatunza hufanywa na Serikali ya nchi husika. Serikali yetu imekuwa ikifanya hivyo kwa kufuata Sheria na Kanuni za Magereza zilizopo ambazo kimsingi zimeipa Serikali jukumu hilo. Aidha, ifahamike kuwa kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Magereza hakuna mahabusu au mfungwa mkimbizi kwani wahalifu wote hupokelewa kwa hati kutoka Mahakama zetu zenye utambulisho wa hadhi ya mahabusu au mfungwa tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, kwa misingi hiyo suala la Shirika la UNHCR kuchangia gharama za kuwatunza wafungwa na mahabusu wanaodaiwa kuwa ni wakimbizi huwa halipo na halifanyiki kwa sababu kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Magereza zilizopo hazijaainisha kumtambua mahabusu au mfungwa mkimbizi katika magereza yetu.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-

Tatizo la ufisadi na wizi nchini limeachwa likaendelea kwa muda mrefu sana:-

(a) Je, ni kwa nini TAKUKURU wasiachiwe kuendesha mashauri makubwa ya ufisadi na wizi Mahakamani moja kwa moja bila ya kuomba kibali cha DPP?

(b) Je, DPP amezuia majalada mangapi ya uchunguzi kufikishwa Mahakamani na ni kwa nini?

(c) Je, Serikali haioni kwamba DPP anaweza kutumika kulinda maslahi ya viongozi ambao kwa kiwango kikubwa wanajihusisha na vitendo vya wizi na ufisadi pamoja na matumizi mabaya ya madaraka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS (MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora), napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini, lenye sehemu (a),(b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa kifungu cha 57(1) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na.11 ya mwaka 2007, TAKUKURU wanayo mamlaka ya kufikisha watuhumiwa waliotenda makosa ya hongo kinyume na kifungu cha 15 cha Sheria Na.11 ya mwaka 2007 moja kwa moja Mahakamani bila kupitia kwa Mkurugenzi wa Mastaka (DPP). Makosa mengine yaliyosalia yanapaswa kupata kibali cha DPP kabla ya kupelekwa Mahakamani kama ilivyoelekezwa kwenye kifungu cha 57(1) cha Sheria Na.11 ya mwaka 2007.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa kifungu cha 57(2) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na.11 ya mwaka 2007, DPP anapaswa kutoa au kutotoa kibali kuwafikisha watuhumiwa Mahakamani ndani ya siku 60 tangu Jalada la Uchunguzi kumfikia. Hata hivyo, DPP anapokea majalada ya uchunguzi kutoka vyombo mbalimbali vya uchunguzi vikiwemo TAKUKURU, Polisi, na Uhamiaji. Kwa siku DPP hupokea takribani majalada 10 kutoka TAKUKURU. Hivyo, kuna kila sababu DPP akaongezewa rasilimali watu na fedha ili aweze kutekeleza majukumu yake kwa wakati. Dhana ya kuwa DPP anazuia Majalada ya Uchunguzi yasifikishwe Mahakamani siyo sahihi.

(c) Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba DPP ni Ofisi inayojitegemea na mamlaka yake yako kwa mujibu wa Katiba. Hata hivyo, sote tumeshuhudia kwamba viongozi mbalimbali wa Serikali wakiwemo Mawaziri wakifikishwa Mahakamani na kuhukumiwa kwenda jela. Naomba nitumie fursa hii kuwaasa watumishi na viongozi wote wa umma mkiwemo ninyi Waheshimiwa Wabunge kutojihusisha na vitendo vyovyote vile vya rushwa. Ahsante.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWAKO aliuliza:-

Katika nchi yetu na hasa Mkoa wa Kigoma kuna vyanzo vingi vya maji (Water sources) Jimbo la Kasulu peke yake kuna vyanzo vya uhakika zaidi ya 150.

(a) Je, kwa nini Serikali haiji na Mkakati wa kina wa uhifadhi wa vyanzo vya maji katika Wilaya ya Kasulu:-

(b) ambo hili haliwezi kuachiwa Halmashauri zetu peke yake. Je, ni lini Serikali itakuja na mpango "A Comprehensive Water Sources Protection Program‟ ili vyanzo vya maji vilindwe na vitunzwe ili kukabiliana na uharibifu wa mazingira na kukabiliana na madhara ya tabianchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwako, Mbunge wa Kasulu Mjini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inayo mikakati mbalimbali ya kuhifadhi vyanzo vya maji nchini ikiwemo Wilaya ya Kasulu. Mikakati hiyo ni pamoja na:-

(i) Mkakati wa hatua za haraka za kuhifadhi mazingira ya ardhi, vyanzo vya maji nchini ulioandaliwa mwaka 2006 wenye hatua za muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu; na

(ii) Mkakati wa hatua za haraka za kuhifadhi mazingira ya bahari, maziwa, mabwawa na mito uliandaliwa mwaka 2008 kwa lengo la kuboresha mazingira ya bahari, maziwa, mabwawa na mito ili kuongeza kasi ya kulinda vyanzo vya maji kama vile mito ikiwa ni pamoja na kulinda na kuhifadhi bioanuai na rasilimali zake.

Aidha, Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na UNEP inaandaa Mradi wa urejeshaji wa mifumo ya ikolojia pamoja na hifadhi ya bioanuai katika Bonde la Mto Malagarasi, Ruaha na Ziwa Rukwa. Mradi huu utatekelezwa katika ngazi za Mgazi, Uvinza, Buhoro, Msambala na Basunzu zilizopo katika Wilaya ya Uvinza, Kasulu na Kibondo Mkoani Kigoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iko kazini na inashirikiana na wadau wengine katika suala la kulinda vyanzo vya maji, hii ikiwa ni pamoja na kuvitambua vyanzo vya maji na kuweka mipaka na kulinda eneo hilo kwa mujibu wa Sheria. Kazi hii inafanywa na Wizara ya Maji na Umwagiliaji. Aidha, hatua mbalimbali za kisheria zinaendelea kuchukuliwa kwa waharibifu wa mazingira. (Makofi)
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-

Nchi yetu kwa muda sasa imekumbwa na uhaba mkubwa wa mbegu hasa za mahindi na maharage ambayo ni mazao ya chakula, kwa taarifa zilizopo Wizara ya Kilimo 2018 nchi yetu inazalisha mbegu hizo kwa asilimia zisizozidi 35 tu:-

(a) Je, kuna mkakati gani wa kutatua tatizo hilo ili angalau nchi itosheleze kwa asilimia 70?

(b) Je, ni kwa nini shamba la mbegu la Bugaga lililopo Wilaya ya Kasulu lisiwe kitovu cha kuzalisha mbegu za mahindi na maharage?

(c) Je, ni kwa nini Serikali haiwekezi katika uzalishaji wa mbegu hizo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nsanzugwanko Mbunge wa Kasulu Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, upatikanaji na uzalishaji wa mbegu bora ikiwemo za mahindi ngano, maharage, mpunga, soya, alizeti, mtama, ufuta na mbegu za mazao ya bustani kwa msimu 2018/2019 ulifikia tani 49,000, kati ya hizo tani 38,000 sawa na asilimia 78 zilizalishwa nchini, tani 8,361 sawa na asilimia 17 ziliagizwa nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, mikakati ya Serikali ya kuongeza uzalishaji wa mbegu ni pamoja na kuwezesha Wakala wa Mbegu za Kilimo (ASA) kuongeza uzalishaji wa mbegu bora katika mashamba ya Mwele, Dabaga, Mbozi, Msimba, Bugaga na Arusha, kutumia Taasisi za Utafiti wa Kilimo kuzalisha mbegu mama, msingi na zilizodhibitiwa ubora na kukodisha maeneo kwa mashamba ya ASA kwa kampuni binafsi za mbegu ili kuongeza uzalishaji wa mbegu bora za mazao mbalimbali ikiwemo mahindi na maharage.

Mheshimiwa Spika, aidha, mkakati mwingine ni kuongeza eneo la umwagiliaji katika mashamba ya mbegu ya Msimba, Arusha, Dabaga na mashamba ya vituo vya utafiti kutoka hekta 200 hadi 600, kushirikisha taasisi za umma kama Jeshi la Magereza na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kuzalisha mbegu bora pamoja na vikundi vya wakulima wadogo kuzalisha mbegu za daraja la kuazimiwa ubora.

Mheshimiwa Spika, shamba la mbegu la Bugaga lililopo katika Wilaya ya Kasulu lina ukubwa wa hekta 200. Shamba hilo linamilikiwa na ASA na kwa sasa linatumika kuzalisha mbegu bora za mahindi, maharage na alizeti. Aidha, shamba hilo linatumika kuzalisha miche bora ya mchikichi, miche ya matunda ya machungwa na maembe. Pia Serikali imeanza kuchimba kisima cha maji katika shamba hilo ili kuwezesha uzalishaji wa mbegu kwa kipindi chote cha mwaka. ASA imejenga kitalu nyumba cha kukuzia miche ya michikichi pamoja na kuandaa bustani ya kukuzia miche hiyo ya michikichi na miche ya matunda.

Mheshimiwa Spika, mkakati wa Serikali ni kuongeza uzalishaji wa mbegu ambapo Serikali katika Mwaka wa Fedha 2019/2020 imetenga takribani shilingi bilioni 1.3 kwa ajili ya utafiti wa mbegu kupitia Taasisi ya Utafiti wa Mbegu – TARI na uzalishaji wa mbegu kupitia Wakala wa Mbegu za Kilimo – ASA kwa ajili ya kuzalisha mbegu kwa njia ya umwagiliaji ili kuongeza uzalishaji mara tatu hadi nne zaidi ya sasa.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuzisihi Halmashauri kutotumia maeneo yaliyotengwa kwa tafiti za kilimo kwa shughuli zingine ikiwemo kujenga stendi za mabasi. Aidha, Wizara ya Kilimo itaamua kuyaachia maeneo haya kwa shughuli zingine baada ya kujiridhisha kwamba maeneo haya hayana tija kwa shughuli za kilimo.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-

Suala la kupima na kupanga Miji ni jukumu la Serikali:-

(a) Je, Kwanini Serikali isije na mkakati endelevu wa kupanga Miji yote ambayo imetangazwa kwenye gazeti la Serikali?

(b) Je, kwanini Serikali inatoa hoja nyepesi kwamba kazi ya kupima na kupanga Miji ni kazi ya halmashauri wakati inajua kwamba halmashauri nyingi nchini hazina nguvu ya kifedha kufanya kazi hiyo?

(c) Mji wa Kasulu ni mkongwe; je, ni lini Serikali itasaidiana na Halmashauri ya Mji wa Kasulu kupanga Mji huo?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, heshima yako.

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali imeanza utekelezaji wa mkakati wa kupanga Miji yote ambayo imetengazwa kwenye gazeti la Serikali kwa kuandaa mipango kabambe ya Majiji, Manispaa na Miji. Aidha, Serikali imeainisha upya maeneo yote ambayo yameiva kuendelezwa kimji kwa ajili ya kuyatangaza katika gazeti la Serikali kuwa maeneo ya mipango yaani planning areas na hivi sasa maeneo ambayo tumeshayatangaza kwamba yameiva kimji mtayaona kila Mbunge ataona kwenye bajeti yangu vijiji na maeneo ambayo yametangazwa kuiva kimji yanayofika 455.

(b) Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kifungu namba 7(1) na (5) cha Sheria ya Mipango Miji namba nanne ya Mwaka 2007, jukumu la kupanga na kupima Miji ni la mamlaka za upangaji ambazo ni Halmashauri za Majiji, Manispaa na Miji na mamlaka ya Miji midogo. Hata hivyo Serikali imeendelea kuzisaidia halmashauri kupanga na kupima Miji yao kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo. Kwa mfano, katika Mwaka wa Fedha 2018/2019 Serikali kupitia Wizara imetoa jumla ya shilingi bilioni 6.4 kwa halmashauri 29 kwa ajili ya upangaji, upimaji na umilikishaji wa ardhi. Aidha, inawezesha uandaaji wa mipango kabambe Miji 18 hivi sasa kupitia program ya kuzijengea uwezo mamlaka za Miji ambayo iko chini ya Ofis ya Rais, TAMISEMI.

(c) Mheshimiwa Spika, mwaka 2008 Serikali iliandaa mpango wa muda wa kati wa matumizi ya ardhi wa Mji wa Kasulu wa miaka 10 (2008 - 2018) ambao ulikuwa unatumika kuongoza na kusimamia uendelezaji wa mji huo wa Kasulu ambako ndiko Mheshimiwa Nsanzugwanko ni Mbunge wake. Mpango huo uliisha muda wake mwaka 2018 hivyo ni jukumu la Halmashauri ya Mji wa Kasulu kuanza mchakato wa kuandaa mpango mwingine kabambe wa kuongoza na kusimamia uendelezaji wa Mji wa Kasulu.