Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Term | Session | Sitting | Sector | Ministry | Qn No | Date |
---|---|---|---|---|---|---|
2015-2020 | Session 18 | Sitting 9 | Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives | Wizara ya Mifugo na Uvuvi | 109 | 2020-02-07 |
Name
Joseph Michael Mkundi
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Ukerewe
Primary Question
MHE. JOSEPH M. MKUNDI aliuliza:-
Je, ni vikundi au wavuvi wangapi katika Kisiwa cha Ukerewe wamepewa elimu na mitaji ili waweze kufanya uvuvi wenye tija?
Name
Abdallah Hamis Ulega
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Mkuranga
Answer
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mkundi, Mbunge wa Ukerewe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikitoa elimu kwa wavuvi wa Kisiwa cha Ukerewe juu ya uvuvi endelevu, matumizi ya zana na mbinu bora za uvuvi zinazokubalika kwa mujibu wa Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya mwaka 2003 na madhara yatokanayo na uvuvi haramu. Lengo la elimu hiyo ni kuwawezesha wavuvi wadogo wa kisiwa cha Ukerewe kufanya uvuvi endelevu na hivyo kunufaika na rasilimali za uvuvi zilizopo katika maeneo yao. Zaidi ya wavuvi wadogo na wadau wengine wa uvuvi wapatao 520 kutoka visiwa vya Ghana, Kunene, Lyegoba na Hamukoko katika Halmashauri ya Kisiwa cha Ukerewe walipatiwa elimu hiyo kwa njia ya mikutano.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeanzisha Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) ili kuwezesha wavuvi kupata mikopo yenye riba nafuu kwa ajili ya kununua zana bora za uvuvi wakiwemo wavuvi wa Kisiwa cha Ukerewe. Ili kuwezesha wavuvi kunufaika na fursa hiyo, Serikali imeendelea kuwahamasisha wavuvi wadogo nchini wakiwemo wa Kisiwa cha Ukerewe, kuunda na kujiunga katika Vikundi vya Ushirika vya Wavuvi na Vyama vya Akiba na Mikopo ili kuwasaidia wavuvi kupata mikopo kutoka taasisi za kifedha.
Aidha, hadi sasa jumla ya shilingi million 250 zipo katika hatua ya mwisho ya kutolewa kwa wavuvi wa Kisiwa cha Ukerewe kama mkopo kupitia Chama cha Ushirika cha Bugasiga kupitia Benki ya Maendeleo ya Kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, uhamasishaji huo umewezesha kuanzishwa kwa Chama cha Ushirika cha Wavuvi katika Kisiwa cha Ukerewe, visiwa vidogo vya Ghana, Kunene, Lyegoba na Hamukoko ambacho kipo katika hatua za usajili. Uanzishwaji wa chama hiki utawezesha wavuvi kutoka Kisiwa cha Ukerewe kupata mikopo kwa urahisi kutoka Taasisi za Kifedha na hivyo kufanya uvuvi wenye tija.
Copyright © Bunge Polis 2021. All Rights Reserved