Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Sophia Mattayo Simba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SOPHIA M. SIMBA aliuliza:- Lugha ya Kiingereza ina umuhimu mkubwa katika majadiliano na wenzetu wa nchi nyingine na pia hutumika kufundishia katika shule zetu kuanzia sekondari hadi vyuo vikuu, lakini lugha hii imekuwa changamoto kubwa kwa wanafunzi katika masomo yao. (a) Je, Serikali haioni umuhimu wa kufundisha lugha ya kiingereza kuanzia shule za awali na kuendelea ili Watanzania wawe na lugha ya pili inayotumiwa na watu wote? (b) Je, Serikali haioni kuwa wananchi wengi wanapenda kuongea kiingereza hivyo ione namna ya kuwawezesha?

Supplementary Question 1

MHE. SOPHIA M. SIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jinsi alivyojibu kwa umakini sana na hususani pale alipozungumzia kwamba walimu wanapata mafunzo zaidi, refresher course ambazo kwa kweli wengi wanazihitaji. Lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuiuliza Serikali je, haioni kwamba kuanza kutumia kiingereza kama lugha ya kufundishia kuanzia masomo ya sekondari inasababisha kuleta ugumu sana kwa wanafunzi na matokeo yake wanakuwa wanakariri hasa katika masomo ya sayansi na teknolojia, kitu ambacho kinapelekea wasifanye vizuri sana katika masomo hayo wakati wa mitihani yao, na wale ambao wapo kwenye shule za private wanafanya vizuri zaidi? Sisemi shule zote, lakini hii ni sababu mojawapo ya shule za sekondari za private kufanya vizuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, Serikali haioni kwamba upo umuhimu wa kipekee kabisa kuhakikisha kiingereza kinatiliwa mkazo kwa sababu kwenye soko la ajira mara nyingi unaona inatokea kwamba interview zinafanywa kwa kiingereza. Hata mashirika mengine ya umma wakienda vijana interview unawauliza mmefanyiwaje anasema ni kwa kiingereza. Isitoshe sisi tunawakaribisha wawekezaji lakini wale wawekezaji wanahitaji wale ambao wana lugha ya pili ambayo ni kiingereza ili ku-communicate. Je, Serikali haioni kwamba tunapoteza ajira nyingi kutokana na ukosefu wa kujiamini wa kuongea lugha ya kiingereza na matokeo yake uakuta hata kwenye EPZ wako Wakenya, Waganda na Wazimbabwe wameajiriwa na mashirika haya ya uwekezaji. Naomba anijibu hilo tunafanya nini, ajira zinapotea. Ahsante sana

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda ifahamike lugha ya kiswahili ni lugha ambayo ni lugha ya taifa, na ni lugha ambayo inafahamika na wananchi wengi toka wakiwa wadogo. Mwanafunzi anapofundishwa lugha ambayo ameiozoea na amezaliwa nayo ni rahisi zaidi kupokea mitaala anayowekewa kuliko pale ambapo unamfundishia lugha mpya kabisa. Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa misingi hiyo tunasema kwamba, sisi kwa kuzingatia kwamba kiswahili ndiyo lugha yetu ya msingi tunasema kwamba mtoto aanze kufundishwa kwa lugha hiyo, lakini mara anapofika darasa la tatu dozi ya kiingereza inaanza kuongezeka kama nilivyosema mpaka kufikia vyuo vikuu. Kwa siku za nyuma kulikuwa na upungufu zaidi kwa sababu unakuta kwamba walimu walikuwa wanaweza kufundisha somo la Kiingereza hata kama alikuwa hana ufaulu wa kutosha. Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile unakuta mwalimu mmoja alikuwa anafundisha masomo mengi. Kadiri tunavyoenda na kuimarisha sifa za walimu na kuongeza idadi ya walimu kutakuwa na specialization kiasi kwamba sasa mwalimu atakuwa anafundisha somo husika na somo alilofaulu na hivyo kiingereza kitazidi kuimarika. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwa upande wa suala la kukosa ajira nipende tu kusema ukweli kwamba kiingereza kimekuwa kikiendelea kuzingatiwa; na niseme tu kwamba kwetu Watanzania yawezekana pengine unyanyapaaji wetu nao unachangia katika kuwafanya watoto waogope somo la kiingereza; na kila wakati kutokujiamini na kutokuzungumza kiingereza kwa hofu kwamba nitaambiwa sijui kiingereza. Mimi nasema kwamba kiingereza ni lugha sawa na lugha nyingine, mtu zungumza bila uoga sawa na ambavyo wengine wanaweza kujaribu kuzungumza kiswahili bila uoga na watu tunaelewana. Mheshimiwa Mwenyekiti, serikali itaendelea kuweka mikakati ya kuboresha somo la kiingereza katika shule na kuongeza mijadala katika shule au midahalo, lakini vilevile kupata hata wataalam mbalimbali wanaopenda kuja kujitolea katika nchi yetu kutoka nchi mbalimbali. Kwa hiyo, niwaombe wote tushikamane kuona kwamba lugha hii ya pili ambayo itatusaidia zaidi katika masuala ya mawasiliano hasa ya kibiashara ili nayo iweze kupata nguvu sawa na ambavyo tunasisitiza katika lugha yetu nzuri lugha ya kiswahili, lugha ambayo ni ya upendo na upole. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hali kadhalika tunasema kwamba bado lazima tuongeze jitihada hata katika lugha za alama kwa sababu huyu mwanafunzi si kiingereza peke yake, ni pamoja na lugha ya alama…