Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SUBIRA K. MGALU (K.n.y. MHE. AZZA H. HAMAD) aliuliza:- Je ni lini Serikali itakamilisha ahadi ya kuchimba Bwawa la Mradi wa Umwagiliaji Masengwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga?

Supplementary Question 1

MHE. SUBIRA K. MGALU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza na namshukuru Naibu Waziri kwa majibu yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa suala la upembuzi yakinifu limekuwa likijibiwa hata Bunge la Kumi kwenye swali hili la msingi na kwa kuwa hata majibu ya msingi ya swali hili yameonesha hakuna hata kiwango cha fedha kilichotajwa waziwazi kutengwa kwa mwaka wa fedha 2017/2018, hali inayopelekea wasiwasi wa utekelezaji wa kazi hii. Je, Mheshimiwa Waziri yupo tayari kuambatana na Mbunge Mheshimiwa Azza kutembelea eneo hili la Masengwa ili asikie kilio cha wananchi hawa na ikizingatiwa Mkoa huu wa Shinyanga umekuwa ukiendelea kunyemelewa na janga la ukame?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa matatizo ya maji ya Halmashauri ya Shinyanga yanafanana kabisa na matatizo ya maji ya Halmashauri ya Chalinze yanayotokana na kusuasua kwa mradi wa Chalinze Wami Awamu ya Tatu na kwa kuwa mradi huu pia ulitembelewa na Mheshimiwa Waziri Mkuu miezi miwili iliyopita na kutoa maelekezo kwa mkandarasi kukamilisha kazi hii kwa siku 100. Je, mpaka sasa Wizara imefikia hatua gani katika ufuatiliaji wa maelekezo ya Waziri Mkuu ili tatizo la maji linaloikumba Halmashauri ya Chalinze hususani Mji wa Chalinze, Ubena na maeneo mengine lipate majibu? Ahsante sana.

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Subira kwamba utaratibu wa utekelezaji wa miradi huwa unaanza na hatua ya awali ambao kwa lugha ya kigeni tunaita basic concept baada ya hapo tunakwenda kwenye feasibility study. Kumekuwa na lugha ya kiujumla ambayo inafahamika kwa wengi (usanifu wa awali). Kwa hiyo, hiyo iliyokuwa inatajwa mwanzoni ilikuwa ni kwa ajili ya basic concept sasa ni kweli tunaenda kwenye feasibility study ambao ni usanifu wa awali.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia amesema hajaona fedha iliyotengwa Mheshimiwa Mbunge leo ndiyo tunaanza kusoma bajeti ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa mwaka 2017/2018. Asingeweza kuiona kabla ya hapo lakini kwa leo baada ya kuanza kusoma bajeti nina uhakika ataona tunaelekea wapi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa ameomba pia tuambatane na Mheshimiwa Azza, ni kazi ya mimi Naibu Waziri kuhakikisha kwamba natembelea Majimbo na Halmashauri zote kujionea utekelezaji wa miradi ya maji safi na salama pamoja na miradi ya umwagiliaji. Kwa hiyo, asiwe na wasiwasi hata huko Shinyanga nitafika.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Mheshimiwa amezungumzia utekelezaji wa mradi wa Chalinze, kwanza nimwambie kwamba sasa hivi mkandarasi ana kasi kubwa ya utekelezaji wa mradi wa Chalinze. Mheshimiwa Waziri pamoja na mimi tunapata taarifa kila siku na taarifa ya jana ni kwamba mkandarasi amefikisha asilimia 44.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ni kweli Mheshimiwa Waziri Mkuu alitembelea pale na wakati ule tulitamka siku 100 za kumpima mkandarasi, tunakupa siku 100 ili tuone kama utaongeza speed basi tutaendelea na wewe. Sasa anaendelea kuthibitisha kabla ya hizo siku 100 kwamba ameongeza kasi. Kama ataendelea hivyo, tutaendelea naye kuhakikisha kwamba mradi ule unakamilika.

Name

Aysharose Ndogholi Mattembe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SUBIRA K. MGALU (K.n.y. MHE. AZZA H. HAMAD) aliuliza:- Je ni lini Serikali itakamilisha ahadi ya kuchimba Bwawa la Mradi wa Umwagiliaji Masengwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga?

Supplementary Question 2

MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa wanannchi wa Jimbo la Manyoni Mashariki wanategemea maji ya mabwawa na visima na kwa muda murefu sana wamekuwa wakitaabika na kero kubwa ya ukosefu ya maji safi na salama. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha Jimbo la Manyoni Mashariki linapata maji safi na salama kwa uhakika? Ahsante. (Makofi)

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, tumekamilisha awamu ya kwanza ya utekelezaji wa program ya maji hapa nchini na tumeanza awamu ya pili Julai mwaka huu 2017. Tumeweka utaratibu wa kutenga fedha kwa kila Halmashauri ili zenyewe zihakikishe kwamba zinabuni na kutekeleza miradi ya maji. Zaidi ya hapo, kuna bwawa kubwa tumejenga katika Halmashauri ya Manyoni Mashariki ambalo lile litafanya kazi mbili, moja ni umwagiliaji kwa ajili ya kilimo cha mboga mboga, lakini pili litasaidia katika maji ya matumizi ya majumbani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge wala asiwe na wasiwasi, tunaendelea na utelekezaji kuhakikisha kwamba wananchi wa Manyoni Mashariki wanapata maji. Nimshukuru kwa sababu yeye ni mama wananchi wake wa Singida anawapenda ndiyo maana anawatetea. (Makofi)

Name

Salome Wycliffe Makamba

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SUBIRA K. MGALU (K.n.y. MHE. AZZA H. HAMAD) aliuliza:- Je ni lini Serikali itakamilisha ahadi ya kuchimba Bwawa la Mradi wa Umwagiliaji Masengwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga?

Supplementary Question 3

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali la nyongeza kwa Waziri Maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi takribani wiki mbili inakwenda ya tatu sasa Shinyanga, Kahama maji hayatoki. Wale watu wanatumia maji ya kununua hakuna maji kabisa. Tatizo inasemekana kwamba hamjalipa bili ya umeme kama Mheshimiwa Rais alivyoagiza. Mheshimiwa Waziri wale watu wanapata shida, hivi ni lini mtarudisha yale maji ili watu waendelee ku-enjoy tunu za Taifa hili? Ahsante.

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli wiki mbili zilizopita Mamlaka nyingi za maji zimekumbwa na tatizo la kukatiwa umeme hivyo kufanya mitambo ya kuzalisha maji isifanye kazi, hii ni kwa Shinyanga pamoja na maeneo mengine pia. Kutokana na tatizo hilo, tarehe 8 Wizara ya Maji, Hazina na Mkurugenzi wa TANESCO walikaa kikao na kuna makubaliano ambayo yamefikiwa. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya muda mfupi suala hili litatuliwa ili liwe na ufumbuzi wa kudumu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini napenda Mheshimiwa Mbunge ajue kwamba ni kweli kabisa kwamba Mamlaka zimekuwa hazilipi bili za umeme na kama Mamlaka hazilipi bili za umeme TANESCO itakufa. Kwa hiyo, tumeweka utaratibu kwamba tuhakikishe tunalipa umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wamekuwa na nia nzuri kabisa ya kuwatetea wananchi wao, wengine wanasema kwamba bili ni kubwa na kadhalika lakini bila kuweka bili ya kiwango ambacho kitawezesha hizi Mamlaka ziweze kujiendesha wenyewe tatizo hili tutaendelea kuwa nalo. Kwa hiyo, naomba sana EWURA wanapopita kufanya hesabu za maji tuwe waangalifu tunapojaribu kuziingilia zile kwa sababu zinatusababisha tufike kwenye hii hali ambayo tumefika.

Name

Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Primary Question

MHE. SUBIRA K. MGALU (K.n.y. MHE. AZZA H. HAMAD) aliuliza:- Je ni lini Serikali itakamilisha ahadi ya kuchimba Bwawa la Mradi wa Umwagiliaji Masengwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga?

Supplementary Question 4

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa suala la lililopo kule Masengwa linafafanana kabisa na bwawa ambalo Serikali imetuahidi katika Kata ya Mnazi na Kivingo kule Lushoto. Je, ni lini sasa Serikali itatenga fedha kuanza mradi huo wa uchimbaji mabwawa?

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza eneo la Lushoto ni zuri sana, ni green, lina mvua za kutosha na linafaa kwa kilimo cha umwagiliaji. Sasa hivi Wizara yetu imepata fedha kutoka Serikali ya Japan na inashirikiana na wataalam wa Serikali ya Japan kupitia mpango kabambe wa kuhakikisha kwamba unaainisha maeneo yote yaliyotambuliwa kwa kilimo cha umwagiliaji ili uweze kuweka mkakati na kuweka mbinu kama nilivyozungumza kwenye swali moja la msingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, katika huo mpango ambao tunatarajia ukamilike mwaka 2018 maeneo yote yataainishwa na matatizo mengi ambayo yamejitokeza yataangaliwa ili tuhakikishe tunajenga miundombinu ambayo itawezesha kilimo cha umwagiliaji. Nimhakikishie Mheshimiwa Shangazi kwamba katika kazi hii inayoendelea tutahakikisha kwamba tunafika mpaka Lushoto.