Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Kiswaga Boniventura Destery

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Magu

Primary Question

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA aliuliza:- Serikali kwa sasa ina Sera ya Elimu Bure kuanzia chekechea hadi kidato cha nne:- Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa elimu bure kwa kidato cha tano na sita?

Supplementary Question 1

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali pamoja na mikakati mizuri ambayo Serikali inaiweka lakini ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa nina imani kwamba Waziri na Maprofesa wote mlioko ndani humu mmesoma bure A-Level na kwa sababu watoto hawa wanachaguliwa, wengine wanashindwa kuendelea na masomo haya kwa kukosa fedha, kwa sababu bado ni watoto wa maskini na wengine wamefaulu vizuri masomo ya sayansi pamoja na hesabu, je, Serikali haioni kwamba inapoteza vijana wazuri ambao wanaweza kusaidia Taifa?(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa hawa watoto wanaochaguliwa kuendelea na A-level ni wachache kuliko wale ambao wanahudumiwa na Serikali kwa maana ya O-Level, je, Serikali haioni kwamba ni wakati muafaka sasa wa kuleta bajeti ili tuweze kuwasaidia watoto hawa wa maskini ili waweze nao kusoma bure wafaidi matunda ya Serikali hii? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi Serikali ingependa kusomesha wanafunzi katika ngazi zote za elimu bure endapo uwezo ungekuwa wa aina hiyo. Kama nilivyosema ni kwamba awamu ya mwanzo tuliongeza shule za msingi lakini tukaja tukaongeza shule za sekondari kila kata na sasa hivi tunaendelea kuongeza shule za kidato cha tano na sita (A-level) kwa sababu ni chache ukilinganisha na wanafunzi wanaofaulu na hasa baada ya Serikali kuchukua jitihada za makusudi za kuongeza ubora wa elimu, imekuwa sasa wanafunzi wanaofaulu ni wengi na hivyo hatuwezi kuwaacha bila kupata elimu hiyo. Kwa hiyo, kabla hatujaweza kutoa fedha kwa kuwalipia hiyo ada, ina maana kama hawana sehemu ya kusomea itakuwa bado hatujafanya jambo la msingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili la kuongeza bajeti, hilo ni suala letu sote kama Wabunge. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais lakini pia Mheshimiwa Waziri Mkuu ambaye tukonaye humu, Wizara yetu ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ni kati ya Wizara ambazo zinapewa kipaumbele cha hali ya juu kwa kupewa bajeti kubwa kuliko Wizara nyingine. Kwa hiyo, naamini Serikali itaendelea kufanya hivyo.