Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Shally Josepha Raymond

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza:- Ushirika hususani wa mazao hauna maendeleo mazuri na umekuwa ukisuasua kwa sababu mbalimbali. (a) Je, ni vigezo gani vinatumika kupima na kutathmini maendeleo ya ushirika? (b) Je, ni hatua zipi zinachukuliwa na Serikali kuboresha mazingira ya ushirika kukua?

Supplementary Question 1

MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ili wananchi waupende ushirika ni pamoja na kuona kuwa mali zao ziko salama na wananufaika.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuuliza Serikali, kwa Vyama vya Ushirika ambavyo mali zake zimetapanywa yakiwemo mashamba, viwanja, nyumba, hususani KNCU, Serikali inasaidiaje ili kurejesha mali hizo ili wananchi wanufaike? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Serikali inasaidiaje mikataba mibovu iliyoingiwa na Vyama vya Ushirika na wale ambao wamechukua mali za vyama hivyo iletwe ili irekebishwe wananchi hao waweze kuona sasa ushirika wao unaendelea vizuri?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa kwamba baadhi ya mali za Vyama vya Ushirika zimetapanywa na hazitumiki kwa utaratibu unaotakiwa na ndiyo maana Wizara yangu kwa kushirikiana na Maafisa Ushirika nchini kote kwa sasa wanafanya tathmini kuhusiana na mali zote za Vyama vya Ushirika ili kujua ni zipi ambazo hazitumiki, zipi ambazo zimeingia mikononi mwa watu binafsi kinyume na taratibu, kwa lengo la kuhakikisha kwamba zile ambazo zimechukuliwa kinyemela ziweze kurudi, lakini vilevile ili mali hizo za ushirika ikiwa pamoja na ardhi ziweze kutumika katika mazingira ambayo yanaleta tija zaidi na kwa manufaa ya ushirika na wana ushirika wenyewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile Mheshimiwa Mbunge ameuliza swali la pili kwamba tunafanyaje kurejesha mali ambazo zilichukuliwa kinyume na taratibu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa sasa tokeo Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani, tumechukua hatua kadhaa za kuhakikisha kwamba uovu uliokuwa ukifanyika katika Vyama vya Ushirika hautokei tena. Kwa hiyo, wale wote ambao wamehusika katika kufanya ubadhirifu na upotevu wa mali za ushirika wanachukuliwa hatua za kisheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile hata viongozi wa Vyama vya Ushirika ambao nao wanakuwa ni sehemu ya ubadhirifu huo tumeendelea kuwachukulia hatua. Ni hivi karibuni tu tumevunja Bodi za Vyama vya Ushirika zaidi ya 200 Mtwara na Lindi. Vilevile mmesikia yaliyotokea Nyanza, jitihada zinaendelea kurudisha mali za Ushirika wa Nyanza. Pia tunajitahidi kuendelea kusaidia vyama vingine ambavyo siku za nyuma kimsingi taratibu zilikiukwa na mali zao kwenda nje kwa watu binafsi bila kufuata utaratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na maswali haya na jitihada za Serikali, naomba niendelee kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wahamasishe wanaushirika wawaeleze kwamba ushirika ni wa kwao, Serikali yenyewe inasaidia. Kwa hiyo, inatakiwa wenyewe wawajibike kuhakikisha kwamba mali za ushirika zinalindwa na pale kasoro zinavyotokea basi watoe taarifa kwa Serikali ili tuweze kuchukua hatua.

Name

Kiteto Zawadi Koshuma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza:- Ushirika hususani wa mazao hauna maendeleo mazuri na umekuwa ukisuasua kwa sababu mbalimbali. (a) Je, ni vigezo gani vinatumika kupima na kutathmini maendeleo ya ushirika? (b) Je, ni hatua zipi zinachukuliwa na Serikali kuboresha mazingira ya ushirika kukua?

Supplementary Question 2

MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Naomba nianzie pale ambapo Naibu Waziri wa Kilimo ameishia, kwamba Bodi ya Nyanza (Nyanza Cooperative Union) na yenyewe pia imekuwa ikilegalega. Je, ni kwa namna gani Serikali inaweka mikakati ya kuhakikisha wakulima wa pamba Mkoani Mwanza wanafaidika na Nyanza Cooperative Union na kushirikishwa katika vikao vinavyoendelea katika Bodi hiyo?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, jitihada zinazoendelea kushughulikia changamoto ambazo zimekikumba Chama cha Ushirika wa Nyanza ni kwa ajili ya kuwanufaisha wakulima wa pamba ambapo kimsingi chama kile kilianzishwa kwa ajili ya kuwasaidia. Kwa hiyo, tunavyojaribu kurudisha mali zile ambazo zilichukuliwa kinyume na taratibu, tunaamini baadaye zitaendelea kuwaongezea wakulima wa pamba wanachama wa Nyanza katika kuendeleza zao la pamba. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba maboresho ambayo tunayafanya na ufuatiliaji ambao tunaufanya yote lengo lake kubwa ni kuwasaidia wakulima wa pamba.

Name

Mary Deo Muro

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza:- Ushirika hususani wa mazao hauna maendeleo mazuri na umekuwa ukisuasua kwa sababu mbalimbali. (a) Je, ni vigezo gani vinatumika kupima na kutathmini maendeleo ya ushirika? (b) Je, ni hatua zipi zinachukuliwa na Serikali kuboresha mazingira ya ushirika kukua?

Supplementary Question 3

MHE. MARY D. MURO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa matatizo yaliyoko sehemu nyingine ya Vyama vya Ushirika ni sawa na tatizo lililoko kwenye Mkoa wa Pwani kwa Coastal Region Cooperative Union - CORECU, majengo yake kutaka kuuzwa na kununuliwa na wajanja wachache. Je, Serikali ina kauli gani juu ya ku-rescue hali hiyo?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa kwamba Chama Kikuu cha Ushirika cha Pwani - CORECU kimekuwa kikipita katika wakati mgumu pamoja na mambo mengine kwa sababu ya madeni makubwa ambayo yameendelea kutishia uhai wa chama hicho. Hivi tunapozungumza CRDB ambao wamekuwa wakikidai chama hicho fedha nyingi, tayari walishaenda mahakamani na taratibu zilianza za kutaka kuuza mali za CORECU. Ni suala ambalo limetokana na mchakato wa kimahakama lakini pamoja na hayo, Serikali na Wizara inaendelea kufanya majadiliano kuangalia namna gani ya kunusuru mali zile zisiuzwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kurejea kusema kwamba naomba Waheshimiwa Wabunge tutoe elimu kwa wanaushirika kwamba wao ndiyo hasa inatakiwa wawe watu wa kwanza kulinda mali za ushirika. Kwa sasabu wanapoingia kwenye mikataba ambayo inahatarisha mali zile, baadaye ni vigumu sana Serikali kusaidia kwa sababu inakuwa ni suala la kisheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Serikali ilisaidia sana kujaribu kuondoa changamoto ya CORECU kwa sababu hata kwenye mkopo ambao wanadaiwa Serikali ilishasaidia kulipa baadhi ya fedha, nafikiri imelipwa zaidi ya shilingi bilioni moja. Hata hivyo, nimueleze Mheshimiwa Mbunge kwamba jitihada zinaendelea kuangalia ni namna gani ya kunusuru mali za CORECU zisiuzwe.

Name

Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Primary Question

MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza:- Ushirika hususani wa mazao hauna maendeleo mazuri na umekuwa ukisuasua kwa sababu mbalimbali. (a) Je, ni vigezo gani vinatumika kupima na kutathmini maendeleo ya ushirika? (b) Je, ni hatua zipi zinachukuliwa na Serikali kuboresha mazingira ya ushirika kukua?

Supplementary Question 4

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Zaidi ya nusu ya Vyama vya Ushirika nchini havijafanyiwa ukaguzi kazi ambayo ilipaswa kufanywa na Tume ya Maendeleo ya Ushirika. Kutokana na uwezo mdogo wa Tume yetu wa kifedha na watendaji tumeshindwa kufanya hivyo. Serikali ina mkakati gani wa kuiwezesha Tume ya Ushirika iweze kufanya kazi yake kikamilfu? (Makofi)

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge kwamba kumekuwepo na changamoto ya kufanya ukaguzi kwenye Vyama vyote vya Ushirika. Kwa sasa Wizara na Tume ya Ushirika imejipanga kuhakikisha kwamba katika mwaka unaokuja wa fedha Vyama vyote vya Ushirika vinakaguliwa, lakini zaidi kuweka mfumo ambapo utaratibu wa ukaguzi utakuwa unafanyika mara kwa mara bila kukosa.