Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Asha Abdullah Juma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA aliuliza:- Je, Serikali ina mkakati gani wa kukabiliana na ongezeko la wasichana wanaokatishwa shule kwa sababu ya mimba?

Supplementary Question 1

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nashukuru kwa majibu niliyopatiwa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ongezeko la watoto wetu wanaoendelea kupata mimba bado limeshika kasi. Ni juzi tu tumepata habari kwamba kuna mwalimu amewafanya wake zake watoto wa primary karibu 10. Wako wanaopata mimba kwa kubakwa, wako wanaopata mimba kwa kushawishiwa na wako wanaopata mimba kwa bahati mbaya yoyote ambayo inatokezea lakini huwa siyo dhamira, dhamira hasa ni watu hawa wapate haki ya kielimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni zito sana…

MWENYEKITI: Swali sasa.

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Sheria Na. 5 imetoa adhabu ya miaka 30 kwa yule mharibifu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Abdullah, nipe maswali.

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la kwanza, nataka niiulize Serikali ni lini hasa itakaa chini itizame upya kadhia hii inayowakuta watoto wa wanyonge, wafanyakazi na wakulima, wasichana ambao wanakosa haki yao kielimu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, lini Serikali itatafuta mbinu mbadala ya kuwasaidia watoto hawa ambao wanakosa haki yao ya kimsingi? Hili jambo linauma sana, lazima Serikali itazame upya.

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema katika jibu langu kwenye swali la msingi, Serikali inachukua hatua kadhaa kuhakikisha inadhibiti tatizo hili. Kubwa ambalo limezungumziwa ni mabadiliko ya sheria ambapo imekuwa ni kosa la jinai kwa mtu yeyote kumpa mimba mwanafunzi wa shule ya msingi au sekondari. Tunachoomba na Waheshimiwa Wabunge ni mabalozi wazuri katika hili, Serikali ina dhamira ya kuhakikisha kwamba wale wote wanaokutwa na makosa haya wanachukuliwa hatua kwa mujibu wa sharia na kama tulivyosema tumeweka kifungo cha miaka 30.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi kinachotokea ni kwamba ushirikiano kutoka kwa wazazi wa wanafunzi ambao wameathirika unakuwa siyo mkubwa. Pindi tutakapopata ushirikiano na ushahidi ukiwepo, Serikali itaendelea kuchukua hatua kuhakikisha kwamba wale wahusika wote wanachukuliwa hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili tunachukua hatua zipi kuhakikisha kwamba wale wanafunzi wanaoathirika wanaendelea na safari ya masomo? Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba mwanafunzi kupata mimba haimaanishi kwamba ndiyo mwisho wa safari yake ya masomo. Serikali imeweka taratibu kadha wa kadha ili kuhakikisha wanafunzi wale bado wanapata fursa nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fursa hiyo ipo katika maeneo matatu makubwa; moja Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima ina utaratibu wa kutoa elimu nje ya mfumo rasmi. Napenda kutoa taarifa kwamba kwa mwaka jana kuna wanafunzi 10,000 ambao wamehitimu kidato cha nne kupitia utaratibu wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima na 6,000 ni wasichana. Tunaamini kwamba baadhi yao ni wanafunzi wale ambao walikatisha masomo kwa sababu ya mimba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia Wizara ya Elimu kwa kushirikiana na UNICEF tunaendesha Mradi wa Elimu Changamani kwa wanafunzi ambao wameshindwa kuendelea na shule kwa sababu ya kupata ujauzito. Pia, Serikali imeendelea kuimarisha elimu ya ufundi, kwa hiyo, wanafunzi ambao hawajaweza kwenda sekondari au ambao wameshindwa kuendelea kwa sababu ya kupata ujauzito kuna fursa vilevile ya kupata elimu ya ufundi na tumeendelea kuimarisha na elimu hiyo sasa hivi ni bora.

Kwa hiyo, tunachosema kimsingi, hata kama mwanafunzi amepata ujauzito sio mwisho wa safari yake ya masomo kuna fursa nyingine na kuna wengi ambao wamenufaika. Nina hakika hata baadhi ya Wabunge kwenye Bunge hili wamenufaika na mipango hii ya Serikali.

Name

Fatma Hassan Toufiq

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA aliuliza:- Je, Serikali ina mkakati gani wa kukabiliana na ongezeko la wasichana wanaokatishwa shule kwa sababu ya mimba?

Supplementary Question 2

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tatozo la mimba utotoni pia linawahusu sana watoto wenye ulemavu walio nje ya shule na ambao wako ndani ya shule. Je, Serikali inawanusuru vipi hawa watoto wenye ulemavu na mimba za utotoni?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Toufiq, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu niliyotoa kuhusu watoto wa kike wanaokatishwa safari ya masomo kutokana na mimba, vilevile yanaweza yakatumika kwa ajili ya watoto walemavu kwa sababu tunachosema Wizara yetu na Serikali kwa ujumla inahakikisha kwamba hakuna mtoto yoyote wa Kitanzania atakayekosa elimu kwa sababu yoyote ile. Sisi tunachotaka ni ushirikiano kutoka kwa wazazi kwa sababu tayari Serikali ina mipango ya kuhakikisha kwamba yeyote yule anapata elimu bila kujali changamoto yoyote imempata katika safari yake.

Name

Masoud Abdalla Salim

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtambile

Primary Question

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA aliuliza:- Je, Serikali ina mkakati gani wa kukabiliana na ongezeko la wasichana wanaokatishwa shule kwa sababu ya mimba?

Supplementary Question 3

MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nina swali moja dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mikakati ya Serikali ya kuweza kutoa adhabu kali na sheria ya kifungo cha miaka 30 kwa wale ambao wanawapa mimba wanafunzi lakini inaonekana bado wanafunzi wanapata mimba na idadi inaongezeka. Je, Serikali ina mkakati gani wa ziada kwa baadhi ya madereva wa bodaboda wanaowachukua wanafunzi wetu ambapo wamekuwa wakilalamika kwamba wanatendewa vitendo visivyo za kutoa elimu ya kutosha kwa madereva hao wanaowachukua wanafunzi kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Masoud, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, jibu langu nilitoa katika majibu yangu ya swali la msingi kwamba Serikali inachukua hatua kadha wa kadha. Moja ni kuzuia na tunazuia kwa njia mbili na kubwa kupitia kitu tunachoita deterrence; kwa kuwaadhibu wale wanaofanya makosa ili wengine wasije wakafanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu changamoto ambayo watoto wanapata wakiwa wanaelekea shuleni, Serikali imeendelea kujenga shule karibu na wananchi lakini vilevile kwenye maeneo ambayo shule ziko mbali tumejenga mabweni. Vilevile tunatoa elimu kwa umma na wanafunzi kwa kupitia huduma za unasihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nachotaka tu kusema ni kwamba Serikali inajua hili ni tatizo kubwa lakini hatujakaa kimya tumeendelea kufanya kila linalowezekana kuhakikisha kwamba hayatokei. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kutokana na takwimu tulizonazo tatizo haliongezeki limepungua.