Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:- Je, ni lini Serikali itapitia upya Sera ya Elimu kwa lengo la kuongeza tija na kuendana na mahitaji ya sasa?

Supplementary Question 1

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu ya Serikali ninayo maswali mawili ya madogo ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa Sera ya elimu ya mwaka 2014 imetamka wazi kwamba elimu ya msingi itaishia darasa la sita na hadi hivi tunavyozungumza Serikali bado haijatekeleza katika eneo hilo. Je, Serikali inatuambiaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni kwa kiasi gani Sera hii ya Elimu inazingatia ubora wa elimu, hasa ukizingatia kwamba miongoni mwa mikoa ambayo huwa haifanyi vizuri katika mitihani mbalimbali ni Mkoa wa Tanga. Sasa nataka kujua ni kwa kiasi gani Sera hii ya elimu inazingatia suala zima la ubora wa elimu kwa maana ya quality assurance? Ahsante.

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Rashid Shangaz, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kujibu, naomba nitumie nafasi hii kusema kwamba Mheshimiwa Shangazi amekuwa akifuatilia suala hili na masuala yote yanayohusiana na elimu na kwa kweli kwa nafasi yake hakuna ubishi kwamba ni moja kati ya Wabunge bora kabisa ambao wamewahi kutokea katika Bunge hili. Swali lake la kwanza ni hilo kwamba kwa nini hatujatekeleza wazo lile la Sera la kuishia darasa la sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jibu letu ni kwamba Sera siyo Msahafu, kwa hiyo Serikali inabadilisha Sera kadiri inavyoona kwamba inafaa kulingana na mahitaji ya wakati huo. Kwa sasa busara imetujia upya kwamba elimu kuanzia darasa la kwanza mpaka la saba siyo kitu kibaya, kwa hiyo hatuna haja ya kubadilisha na ndiyo maana tumebakia na mfumo wa zamani na hatujavunja sheria, Sera siyo lazima itekelezwe, Sera unatekeleza na unabadilisha kadiri unavyoona inafaa. Kwa sasa tuko kwenye mapitio na ni moja ya mambo ambayo tuliona kwamba hatutatekeleza na tutaendelea na utaratibu wa zamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuhusiana na ubora wa elimu ni kweli kwamba Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, imeweka msisitizo mkubwa katika masuala ya udhibiti ubora wa elimu na ndiyo maana kumetokea mabadiliko makubwa sana katika mfumo wetu wa udhibiti ubora. Zamani tulikuwa tunasema ni ukaguzi wa elimu lakini siku hizi tunadhibiti ubora, lakini vile vile mtindo mpya wa kudhibiti ubora ni wa kiushirikishwaji zaidi unawaleta wadau wote kushiriki katika kudhibiti ubora wa elimu, lakini vilevile kama wote mnavyojua sasa tuko katika mikakati mikubwa ya kuhakikisha kwamba Wadhibiti Ubora wanawezeshwa kwa kupata vifaa na ofisi. Kimsingi tumeweka mikakati mikubwa sana ya kuhakikisha kwamba elimu yetu inakuwa bora. Moja kati ya masuala ambayo tunayafanyia kazi katika mapitio ya Sera ni kuendelea kuweka mifumo ambayo itawezesha kudhibiti ubora wa elimu.

Name

Masoud Abdalla Salim

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtambile

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:- Je, ni lini Serikali itapitia upya Sera ya Elimu kwa lengo la kuongeza tija na kuendana na mahitaji ya sasa?

Supplementary Question 2

MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja dogo la nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mapitio ya Sera ya Elimu na kuweka mikakati ya ubora wa elimu, ni mara kadhaa hapa Bungeni Serikali imekuwa ikiahidi kuboresha maslahi ya walimu ikiwemo posho ya kufundishia (teaching allowance). Vilevile kwenye sherehe mbalimbali za walimu katika maeneo kadhaa Serikali wamekuwa wakiahidi kuboresha posho ya kufundishia (teaching allowance) lakini hadi sasa waliopata fedha hizo ni Wakuu wa Shule na Waratibu wa Elimu. Naomba kujua kama Serikali iliwadanganya walimu na lini fedha hizo zitatolewa?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali na Mheshimiwa Masoud, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli katika azma ya kuboresha elimu maslahi ya walimu na wafanyakazi wengine katika sekta ya elimu ni kitu muhimu. Ndiyo maana kwa sasa Serikali inajaribu kupitia upya utaratibu mzima wa maslahi ya watumishi wa umma kwa jumla wakiwemo na walimu ili baada ya hapo tuweze kuwa na maslahi ya walimu ambayo yataenda na wakati wa sasa lakini vilevile ili waweze kufanya kazi yao vizuri katika sekta ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu swali la madeni, naomba nimtaarifu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ilijikita kwanza katika zoezi la kufanya uhakiki ili kubaini madeni ya kweli. Baada ya hapo tayari baadhi ya malipo yalishafinyika na mengine yataendelea kulipwa.

Name

Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:- Je, ni lini Serikali itapitia upya Sera ya Elimu kwa lengo la kuongeza tija na kuendana na mahitaji ya sasa?

Supplementary Question 3

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mwezi Januari, 2019, Wizara ya Elimu ilitoa Mwongozo juu ya Muundo wa Bodi za Shule kuanzia shule za msingi mpaka Serikali. Katika muundo ule, Wizara imeelekeza katika shule ya sekondari na shule za msingi muundo utoe nafasi kubwa sana kwa walimu ambapo watakuwa watano lakini pia wazazi au nje ya walimu wanakuwa watatu. Je, katika maana nzima ya makusudio ya Bodi kwenda kuangalia ufanisi wa taaluma na majengo na mambo yanayoendelea shuleni, Wizara haioni kwamba jambo hili limekosewa na kwamba linahitaji lirekebishwe haraka sana kabla hapajaharibika?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba hivi karibu tumetoa Mwongozo mpya wa Bodi za Shule na lazima niseme kwamba baada ya kuutoa tumegundua kuna maeneo ambayo yangeweza kuwa bora zaidi na mojawapo ni hilo alilosema Mheshimiwa Kikwete. Naomba nimhakikishe kwamba tayari Wizara inaupita upya tena Mwongozo ule kwa kushirikiana na wadau ili tuwe na Mwongozo ambao utakotupeleka mbali zaidi.