Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Primary Question

MHE. HUSSEIN M. BASHE (K.n.y. MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU) aliuliza:- Mji wa Igunga unakabiliwa na tatizo kubwa la maji kutokana na kupanuka kwa kasi wakati miundombinu ya maji ni ile ile na pia imechakaa sana na haitoshelezi mahitaji ya maji kwa wakazi wake:- Je, ni lini Serikali itawapatia wananchi wa Mji wa Igunga maji ya kutosha?

Supplementary Question 1

MHE. HUSSEIN M. BASHE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Igunga pamoja na upatikanaji wa maji kitakwimu wa asilimia 60, lakini kutokuwepo kwa umeme wa uhakika kunapelekea upatikanaji wa maji katika Mji wa Igunga kuwa angalau kwa wiki mara mbili. Je, Waziri ama Serikali wakati tunasubiri mradi wa maji wa Ziwa Viktoria, inaweza kutusaidia katika Mji wa Igunga kuwapatia angalau generator ili liwe pale ambapo umeme haupo, basi waweze kupata maji ya uhakika?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, tatizo la Igunga linafanana sana na tatizo la Mji wa Nzega; na upatikanaji wa maji katika Mji wa Nzega kwa sasa ni asilimia 30 tu ya maji na maji haya yanapatikana kwa wiki mara tatu: Je, Serikali ni lini itatekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais ya ujenzi wa matenki matano na kuweka chujio la maji katika bwawa la Kilime na pampu ili wananchi wa Mji wa Nzega wasiendelee kupata shida wakati tunasubiri mradi wa maji wa Ziwa Viktoria?

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza nashukuru amekiri kwamba asilimia 60 ya maji inapatikana katika Mji wa Igunga, lakini tatizo lililopo ni tatizo la umeme. Ameuliza kwa Wizara ya Maji na Umwagiliaji, lakini pamoja na Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, tukiwa katika Bunge hili Mheshimiwa Waziri anayehusika na umeme na nishati ameshatupa majibu kwamba sasa hivi kunajengwa umeme wa msongo wa Kilowatt 400 ambapo tatizo la umeme sasa litakwisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia, amependekeza kwamba, katika kipindi hiki kwa sababu ya tatizo la umeme, maji yanapatikana mara mbili kwa wiki, ni vyema tukafanya utaratibu wa kununua generator. Kupitia Bunge lako Tukufu, namwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Igunga, aweze kuleta andiko ili tuweze kuangalia uwezekano wa kununua generator iweze kusaidia katika kipindi hiki tunaposubiri kuwa na mradi mkubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, amezungumzia Mji wa Nzega kwamba unapata 30% na maji yanapatikana mara tatu kwa wiki. Je, Serikali ni lini itajenga matenki matano yaliyoahidiwa na Mheshimiwa Rais?
Mheshimiwa Naibu Spika, nimjibu kwamba, matenki matano makubwa yanajengwa kupitia huu mradi wa kutoa maji Ziwa Viktoria na kupeleka Miji ya Tabora, Nzega na Igunga. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa kwamba matenki hayo yatajengwa kupitia mradi huu, lakini pia, mradi utahusisha ujenzi au upanuzi wa mtambo wa kusafisha na kutibu maji. Kwa hiyo, mradi huu ukikamilika, hoja zote ulizonazo Mheshimiwa Mbunge, zitakuwa zimeshapitiwa.

Name

Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Primary Question

MHE. HUSSEIN M. BASHE (K.n.y. MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU) aliuliza:- Mji wa Igunga unakabiliwa na tatizo kubwa la maji kutokana na kupanuka kwa kasi wakati miundombinu ya maji ni ile ile na pia imechakaa sana na haitoshelezi mahitaji ya maji kwa wakazi wake:- Je, ni lini Serikali itawapatia wananchi wa Mji wa Igunga maji ya kutosha?

Supplementary Question 2

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Miradi mingi sana ya maji imeanzishwa nchini na katika Jimbo langu kuna mradi umeanzishwa katika Kijiji cha Shimbi Mashariki, mwingine umeanzishwa katika Kijiji cha Rea, visima vile 10 na vinahitaji kujengewa miundombinu. Sasa kinachosumbua ni fedha zinasuasua kwenda ili kukamilisha umaliziaji wa miundombinu ili wananchi wapate maji. Nauliza je, ni lini fedha zitakwenda ili miradi hiyo ipate kukamilika?

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikuhakikishie kwamba tumeanza Program ya Pili ya Maendeleo ya Sekta ya Maji. Pili, fedha zimeanza kutolewa. Natoa wito kwa Wakurugenzi wote kwamba kama wana hati ziko mezani, basi waziwasilishe kwa Katibu Mkuu Wizara ya Maji. Fedha tunazo na tayari maeneo mengi fedha tumeshapeleka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kama kazi imeshafanyika, hati zipo, hata kesho alete tutampatia fedha.