Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba kusini

Primary Question

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO aliuliza:- Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwapa posho ya mazingira magumu wafanyakazi hasa walimu wanaopangiwa kazi mikoa ya pembezoni?

Supplementary Question 1

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, hata hivyo ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa Wilaya ya Muleba ina kata tano ambazo ziko katikati ya Ziwa Victoria ambako huduma nyingi za Serikali hazijafika. Je, Serikali ina mkakati gani wa kutupatia angalau ambulance kwa ajili ya kuharakisha usafiri hasa walimu na wafanyakazi wengine wanapopata matatizo ya afya? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa kuna taasisi za Serikali ambazo zinatoa motisha kwa wafanyakazi wake; je, Serikali haioni haja ya kuharakisha huo mwongozo ambao imeusema hapa kwa ajili ya kuwaboreshea maisha wafanyakazi hasa walimu na manesi ambao wako pembezoni kabisa mwa nchi ambako hakuna umeme na nyumba za kuishi ili waweze kutumikia Serikali kwa moyo wao wote? Ninashukuru sana. (Makofi)

Name

Deus Clement Sangu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwela

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Kikoyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; nimpongeze kwa namna anavyowasemea wananchi wake wa Jimbo la Muleba Kusini. Suala la kwanza, ameongelea juu ya ambulance. Nimhakikishie Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuboresha huduma za afya katika maeneo yote nchini na hivi karibuni Mheshimiwa Rais alitoa ambulance nchi nzima, na anaendelea kufanya hivyo kutokana na mazingira mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Dkt. Kikoyo jambo la kupeleka ambulance katika kata hiyo yenye changamoto tutawasiliana na wenzetu wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuona namna ya kupeleka ambulance katika eneo hilo na hiyo ndiyo nia ya Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la motisha kwa watumishi hili ni jambo la jumla. Mheshimiwa Rais alionesha nia ya dhati na hata juzi alipokuwa anazindua Sera ya Elimu ya 2014, Toleo la Mwaka 2023 amesema wazi tunaenda kupitia upya maslahi hasa maslahi ya walimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nikuhakikishie pia, suala hili la motisha ni kati ya mambo ambayo tunayapa kipaumbele kama Serikali na kutokana na hali ya uchumi na upatikanaji wa fedha nikuhakikishie jambo hili tutalitekeleza na hasa kwa watumishi wako wa Jimbo la Muleba Kusini. Ninakushukuru sana.