Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

MHE. AMINA S. MOLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia mawili matatu katika hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa John Joseph Pombe Magufuli.
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba nimshukuru Mwenyenzi Mungu kwa kunijalia afya njema lakini pia familia yangu, pamoja na wote wa UWT walioniwezesha kufika hapa.
Baada ya kusema hayo naomba nianze kwa kuchangia kwanza kabisa kwa kumpongeza Rais, kwa kuteuliwa kwake, lakini nimpongeze sana kwa kazi nzuri aliyoifanya kwa sababu katika kipindi cha miezi mitatu siku 100 ndizo hizo ambazo hivi sasa zinaelekea kutimia, tumeona mengi ambayo ameweza kuyafanya kwa kipindi kufupi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kubwa kabisa kwa niaba ya watu wenye ulemavu kwa kweli nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa jitihada za kutambua kundi hili kuliwezesha katika sekta mbalimbali. Tumeshuhudia kwa mara ya kwanza katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tunaye mwakilishi na vilevile masuala ya watu wenye ulemavu kuyahamishia katika Ofisi ya Waziri Mkuu. Hiki kilikuwa ni kilio cha watu wenye ulemavu kwa kweli tunamshukuru sana kwa hili. Vilevile tunamshukuru sana kwa kutupa Mawaziri hawa na nina imani kabisa kama waswahili asemavyo uchungu wa mwana aujuae mzazi, ninaamini kabisa Mheshimiwa Jenista Mhagama atakuwa msaada mkubwa kwa kweli, kwetu sisi katika kundi hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, moja kwa moja nianze kuchangia baada ya shukrani hizi kwa sababu ningekuwa mchoyo wa fadhila. Mheshimiwa Rais katika hotuba yake aligusia masuala ya watu wenye ulemavu na kama nilivyosema awali ameanza kuonyesha kwa vitendo. Tunafahamu tunapozungumzia umasikini katika nchi hii watu wenye ulemavu ndilo kundi linaloongoza kwa umaskini, na hata unapokutana na watoto wenye ulemavu wengi wao pia wametoka katika familia maskini. Kwa hiyo, suala la elimu ni muhimu sana, kwa kundi hili, ukimuwezesha kupata elimu kwanza mtu huyu anaweza kujitegemea yeye mwenyewe, lakini pia hata unapomwezesha katika nyenzo mbalimbali inakuwa ni msaada mkubwa kwake yeye ili kuweza kujitafutia riziki kwake yeye, lakini pia katika familia yake kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa nchini Tanzania ni 4% tu ya watoto wenye ulemavu ndiyo wanaopata elimu, na tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwamba amefanya elimu kuwa bure, tunaamini kabisa mojawapo ya vikwazo ambavyo wazazi wengi walikuwa wanaona taabu kuwapeleka watoto wao shule, kama ana watoto wawili mwenye ulemavu na asiye na ulemavu anaona ni afadhali ampeleke asiye na ulemavu na huyo mwenye ulemavu abaki nyumbani. Kwa hiyo tunaamini kabisa kwamba hivi sasa wazazi wengi watawapeleka watoto wao shule ili waweze kupata elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naiomba Serikali ichukue hatua kali, sheria ifuate mkondo kwa wale wazazi ambao mpaka hivi sasa bado wanawaficha watoto wenye ulemavu nyumbani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii mzazi wangu angenificha mimi tusingekuwa na Amina hapa Bungeni, tusingekuwa na akina Mheshimiwa Ikupa, tusingekuwa na Waheshimiwa wengine wote kama wazazi wetu wangetuficha. Lakini walitambua thamani ya sisi ndiyo maana leo hii tuko hapa. Kwa hivyo, ninaamini kabisa kukiwepo na sheria ambayo itawabana wazazi wote wanaowaficha watoto wao majumbani na kuwakosesha haki yao ya msingi ya kupata elimu ninaamini kabisa watoto hawa wataweza kufika mbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala hili la elimu, hivi sasa elimu katika shule za msingi na sekondari ni bure, lakini tunafahamu kwamba wanafunzi wanaokwenda Vyuo Vikuu kuna mikopo. Hivi kuna utaratibu gani mzuri ambao unaandaliwa kwa wanafunzi hao wenye ulemavu ili waweze kupata elimu? Kwa sababu wengine hawapati hizo asilimia za mikopo. Kwa hiyo, niishauri Serikali yangu na ninaamini kabisa mwanzo mzuri tumekwisha uona, ianze kutoa ruzuku kwa wanafunzi wenye ulemavu, wanaokwenda Vyuo Vikuu, sekondari na hata form five na six, ili basi waweze kujikimu, lakini pia ule mzingo ambao wengine ni walemavu na familia zao ni masikini zaidi wataweza kwenda shule. Ombi langu ni hilo kwa Serikali.
Mheshimwia Naibu Spika, lakini pia mimi ni mwanataaluma, nimetoka katika taaluma ya habari. Hawa waandishi huko wanakotoka wengi wao mishahara yao ni midogo na mimi nimuombe sana kaka yangu Mheshimiwa Nape, nakuomba sana kuhakikisha kwamba waajiri wengi kunakuwepo na utaratibu mzuri ambao utawawezesha Waandishi wa Habari waweze kuifurahia kazi yao. Wananchi wanafaidika kwa sababu ya hawa Waandishi wa Habari. Tukiwa katika misafara, wakiwa katika shughuli zozote za kitaifa muda wote wako busy kufanya kazi zao, lakini waajiri wengi hawatambui thamani ya Waandishi wa Habari.
Mheshimiwa Naibu Spika, nina ombi kwa Serikali, tuwaangalie sasa ili waandishi hawa waweze kufurahia taaluma yao, waweze kuifanya kazi yao ipasavyo kwa kuboresha maslahi yao, lakini vilevile kwa sababu wanakumbana na changamoto nyingi wanapofanya kazi, tuangalie utaratibu pia wa kuwaandalia bima, kwa sababu waandishi wengi na hata katika matukio mengi wao ndiyo wanaokuwa waathirika wa kwanza. Kukiwa na matukio ya milipuko mabomu, tukio lolote lile wao ndiyo wa kwanza kwa sababu mwajiri ili aweze kupata taarifa lazima huyu mwandishi awepo pale.
Kwa hiyo, kaka yangu Mheshimiwa Nape, ninakuomba sana uangalie ni kwa jinsi gani tutaweza kuboresha maisha mazuri kwa hawa Waandishi wa Habari.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Molel muda umekwisha.
MHE. AMINA S. MOLEL: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante, naunga mkono hoja