Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami nichangie mapendekezo ya mpango yaliyo mbele yetu. Pia nami niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wa Wizara hii kwa kuteletea mpango ambao unaonekana kabisa kwamba ni mwendelezo wa utekelezaji wa mpango wetu wa miaka mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita sehemu mbili, ya kwanza itakuwa ni kilimo. Kuna watu ambao wanabeza kwamba hatuwekezi vya kutosha katika kilimo lakini ukiangalia ukurasa wa 29 wa kitabu cha Waziri tunaona kabisa kwamba sekta hii mwaka jana ilipanda kwa asilimia 7.1, hongera sana. Kuna uwekezaji ambao unafanya kwenye sekta hii ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimpongeze Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa kwa kazi kubwa anayoifanya kwenye mazao ya kimkakati. Tumeona anahangaika na kawaha, chai, mchikichi vile vile amehangaika na tumbaku na pamba kwa kiasi kikubwa sana. Nampongeza kwa sababu jitihada zake kwa kiasi kikubwa zimechangia ongezeko hili la sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma sasa takwimu utakuta zao la korosho ndilo lililochangia zaidi kwenye mafanikio hayo. Kwenye zao la korosho kwa miaka mitatu mfululizo kuna ongezeko la uzalishaji. Mwaka 2015/2016 tulikuwa na tani 155; mwaka 2016/2017 tani 265; na mwaka 2017/2018 kuna tani 315,000. Hili ni ongezeko kubwa na linatokana na uwekezaji mkubwa ambao ulifanywa kwenye zao hili la korosho. Rai yangu kwa Serikali, korosho bado inahitaji uwekezaji mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, bado Serikali ina mambo ya kufanya ili kuhakikisha uzalishaji wa korosho unaendelea kuongezeka kama takwimu zinavyoonesha. Kwanza lazima tuwe na mipango sahihi ya kupatikana kwa pembejeo. Tusiachie wafanyabiashara binafsi walete pembejeo ambazo hatuna uhakika na ubora wake na wanawauzia wakulima wetu kwa bei ya juu. Kwa hiyo, Serikali bado kuna kitu inahitajika kufanya ili kuhakikisha zao letu la korosho halishuki kwa uzalishaji kama tunavyoona kwenye takwimu za miaka hiyo mitatu iliyopita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye korosho kuna changamoto mwaka huu. Takwimu zinaonesha hadi sasa kwa Mkoa wa Mtwara tu Chama Kikuu cha Ushirika cha Tandahimba na Newala (TANECU) wana tani 30,000 na Chama cha Ushirika cha Mtwara, Nanyumbu na Masasi (MAMCU) kuna tani takribani 30,000 zimekusanywa lakini hadi sasa ni tani 2,200 zimenunuliwa. Hapa kuna changamoto ya soko la Dunia lakini vilevile mwaka huu kuna syndicate ya wanunuzi wa korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali yangu, hawa wanunuzi wamewasilisha barua kuhusu punguzo la kile ambacho Mheshimiwa Rais na nimpongeze anavyosimamia ununuzi wa korosho mwaka huu, kwa sababu amekuwa akifuatilia siku hadi siku nini kinaendelea kwenye soko la korosho. Kwa hiyo, naishaiuri Serikali yangu ifanye mashauriano na hawa wafanyabiashara, kama kweli madai yao ni ya msingi basi itafutwe mbinu ya kufidia ile Sh.200 ambayo wanaomba wapunguziwe ili waende sokoni wakanunue korosho. Kama madai yao si sahihi basi lile pendekezo au wazo la Mheshimiwa Rais, kwamba korosho zitanunuliwa na Serikali yetu, muda umefika sasa Serikali itoe tamko ili korosho zikanunuliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu tuna wiki tatu tu ambazo sisi tuna nafasi ya kuuza korosho ikishafika mwezi Desemba korosho za nchi nyingine zinakuwa tayari na wanunuzi wataenda maeneo mengine. Kwa kuwa Serikali yangu ni sikivu haya watayafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuondoke hapa nini kifanyike? Tuwekeze kwenye ubanguaji. Siku za nyuma tulifanya kazi kubwa sana ya kuwekeza kwenye viwanda, tuna viwanda 12 vya ubanguaji wa korosho. Viwanda hivi umefika wakati sasa tufanye maamuzi magumu. Wale wanunuzi walionunua viwanda hivyo ambao hawafanyi kazi ya ubanguaji wanyang’anywe viwanda hivyo. Kuna Kiwanda Mtwara, Newala, Masasi, Nachingwea, Mtama, Likombe, Lindi, Kibaha, Tanita I, Tanita II, Newala II na Tunduru. Viwanda hivi havifanyi kazi ya kubangua korosho, kuna viwanda vingine sasa hivi vinatumika ma-go-down.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali ifanye maamuzi magumu. Wale ambao wamevichukua viwanda hivi na kuvifanya ma-go-down, hawabangui korosho wanyang’anywe ili wapewe wawekezaji wapya ambao wameonyesha nia ya kubangua korosho yetu hapa hapa nchini. Kwa kufanya hivyo, tutaondokana na tatizo la kupeleka korosho ghafi India ambako kwa njia moja au nyingine wafanyabiashara wa nchi hii huwa wana kawaida ya kupanga bei na hivyo kumdhoofisha mkulima wa zao la korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mpango huu vilevile naomba nichangie kuhusu eneo maalum la uwekezaji na hasa eneo la Mtwara. Nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa inayofanya katika upanuzi wa Bandari wa Mtwara. Tumeona kuna uwekezaji mkubwa sasa hivi umefanyika kwenye Bandari ya Mtwara na sasa hivi meli za mafuta zimeshaanza kutia nanga na hivyo kurahisisha upatikanaji wa mafuta Kanda ya Kusini Mikoa ya Mtwara, Lindi na Ruvuma na hata nchi za jirani Malawi na Msumbiji. Vilevile tunaona kuna ukarabati mkubwa ambao umeanza kwa uwanja wa ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili eneo hili la Mtwara liwe rahisi kuwekeza kuna kazi mbili zimebaki sasa hivi. Kwanza kuna suala la barabara yetu ya uchumi, barabara ya Mtwara- Nanyamba-Tandahimba-Newala-Masasi, km 210. Barabara ile matengenezo yameanza kwa km.50. Tunaomba sasa mpango ujao zitengwe fedha za ujenzi wa barabara kuanzia Mnivata-Newala-Masasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna barabara nyingine muhimu sana, barabara ya ulinzi ambayo ipo Kusini mwa Tanzania na inaunganisha Wilaya zote na pembeni mwa Mto Ruvuma. Barabara hii haitengewi fedha za kutosha. Tunaomba katika mpango ujao zitengwe fedha za kutosha kwa ajili ya matengenezo makubwa ya barabara yetu ya ulinzi kwa ajili kuimarisha ulinzi wa nchi yetu. Kama mnavyofahamu kwamba kule wenzetu Msumbiji kuna nyakati kunakuwa na changamoto za ulinzi, kwa hiyo, barabara yetu iwe inapitika muda wote na vijana wetu wa ulinzi na usalama waweze kuitumia kwa ajili ya kulinda nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu mwingine utajikita kwenye suala la kufungamanisha uchumi na maendeleo ya watu. Kuhusu elimu na ujuzi, hapa lazima tuwekeze vya kutosha. Mpango ujao unatakiwa utenge fedha za kutosha kwa ajili ya sekta ya elimu. Mpango wa Maendeleo wa Elimu ya Msingi ambao ulitekelezwa kuanzia mwaka 2002 kulikuwa na ujenzi mkubwa wa madarasa pamoja na nyumba za walimu, lakini madarasa yale yanahitaji ukarabati mkubwa sana. Wote mtakuwa mashahidi zilitengwa fedha takribani shilingi milioni tatu na laki moja kwa ajili ya ujenzi wa chumba cha darasa kwa miaka hiyo. Ujenzi uliofanyika kwa wakati ule muda wa kukarabati majengo hayo sasa umeshafika. Naomba mpango ujao utakaowasilishwa zitengwe fedha za kutosha kwa ajili ya kukarabati miundombinu ya elimu ya msingi kama vile vyumba vya madarasa, nyumba za walimu na ujenzi wa matundu ya vyoo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini si hivyo tu, bado kuna suala la motisha kwa walimu. Walimu wetu wanahitaji motisha na kupata mafunzo kazini. Ni mwaka wa tatu sasa mishahara ya walimu na watumishi wengine bado haijaongezwa.

Mimi ninawasemea walimu kwa sababu ni kundi kubwa na ni asilimia 60 ya watumishi wa umma wa nchi hii. Watumishi hawa wakikata tamaa basi kazi zote ambazo tunawekeza katika maeneo mengine hazitakuwa na maana. Kwa hiyo, naomba katika bajeti ijayo tutenge fedha za kuongeza mishahara ya walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja.