Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi ya kuchangia. Napongeza mapendekezo ya mpango kwa kweli ni mazuri isipokuwa naomba nijikite katika eneo moja au mawili hasa kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu umuhimu wa kilimo. Pamoja na kuwa tunasema kilimo ni uti wa mgongo ndiyo sekta itakayoleta ajira nyingi sana kwa vijana na itaondoa umaskini kwa kiasi kikubwa sana. Pamoja na kuwa na mikakati na miradi mingi ya kuendeleza kilimo katika nchi yetu mingi naiona bado iko katika mipango, utekelezaji bado haujaonekana kwa maana ya uboreshwaji wa kilimo ambacho kwa kiasi kikubwa takribani asilimia 65 mpaka 70 kinafanywa na wanawake vijijini ambayo ni nguvu kazi kubwa lakini wanafanya kazi kwa mazingira magumu sana. Changamoto zinafahamika na tungependa kuona kwenye mpango sasa jinsi gani hii mikakati na miradi mikubwa iliyoletwa akina ASDP II, SAGCOT na mikakati mingine yote katika sekta za uvuvi na ufugaji zinatiririka sasa kwenda kwa wale ambao ndiyo hasa wazalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko njia nyingi za kuendeleza kilimo kwa kukiboresha. Muda mrefu sana tumekuwa tukizungumzia mnyororo wa thamani, hiyo ilikuwa ni njia moja nzuri sana ya kuhakikisha kwanza kilimo chetu kinakuwa na tija lakini kinaleta ajira, kinaongeza thamani ya mazao yetu na kuwezesha soko la ndani kujihimili katika kujitosheleza kwa mahitaji yake na hata kuuza nje ya nchi. Hali ilivyo sasa hivi Serikali na wakulima wanagonganisha vichwa, kila tunakoenda wakulima wanalalamika sana na wana haki ya kulalamika kwa sababu wanatumia nguvu yao wenyewe nyingi, wanapoteza fedha nyingi lakini wanachokuja kupata baada ya kulima ni kitu ambacho kwa kweli hakiwatoshelezi wao hata Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema kuwa wakulima wengi ni wanawake lakini vilevile ajira nyingi zinaweza zikazalishwa kwa vijana kwa kutumia kilimo, ufugaji na uvuvi. Nini kifanyike, ni kuhakikisha kuwa zile changamoto zilizoainishwa ndiyo ambazo Serikali inaziwekea mkakati wa kuhakikisha kuwa wanazitatua. Upatikanaji wa mitaji kwa wakulima bado ni mdogo na unasuasua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hiyo Benki ya Wakulima iliyoanzishwa bado ina-deal na watu wa ngazi za juu, inataka vikundi vilivyosajiliwa na watu ambao wako kwenye mfumo rasmi, wakulima wetu wengi na vijana wetu wengi hawako kwenye mifumo hiyo. Kwa sababu hawako kwenye mifumo hiyo tulikuwa tunategemea benki ingeji-restructure iwakute hawa. Tanzania siyo peke yake inayofanya hivi, ziko nchi nyingi na zimefanikiwa kwa kuhakikisha kuwa mifumo yao ya kutoa mitaji kwa ajili ya kilimo inakwenda sambamba na aina ya wakulima tulionao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia suala la kuongeza thamani. Mnyororo wa thamani ndiyo utakaotuhakikishia kuwa kwanza tunaunganisha kilimo na sekta binafsi. Kwa sababu kwa upande mmoja sekta binafsi ndiyo inaingia katika mambo ya value addition na masoko na kwa kutumia weledi na nyenzo bora wanazotumia wao wanaweza kusaidia hata wakulima katika ngazi za chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu ambao wameendelea kwenye kilimo, kwa mfano Vietnam, South Korea, Thailand, wakulima wao wote bado ni wadogo lakini wametafuta hizo linkages na private sector, wakatumia outgrower schemes, irrigation schemes na ku-link na wanunuzi wakubwa wa nchi za nje kwa kutumia Serikali na wakafanikiwa sana. Sasa hivi wanatumia kilimo katika kuhakikisha kuwa wana export kwa wingi zaidi kutokana na hao wakulima wadogo wadogo. Naomba sana Mheshimiwa Dkt. Mpango angalieni jinsi gani mtaboresha mikopo na huduma za muhimu za ugani kwa wakulima wadogo ambao ni wengi na hapo ndiyo mtakapoona tija ya kilimo itakavyokuwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la kuhakikisha kuwa nyenzo bora zinapatikana. Wakulima wengi ni wanawake, tuna TEMDO, CAMARTEC, TIRDO na SIDO, wanafanya nini kuhakikisha kuwa akina mama hawa wanatengenezewa nyezo zitakazofaa kutumia wao kufuatana na nguvu zao na uwezo wao na jinsi ambavyo wanajikita kwenye mashamba yao. Tuna taasisi, makampuni na mabenki tunachotakiwa sasa kama Serikali ni kuwaunganisha hawa sasa na wakulima, vijana kwa wanawake ili sasa tija ipate kuongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalalamikia masoko, lakini hata soko la ndani lenyewe hatujalitosheleza kwa bidhaa hasa zile muhimu zinazohitajika. Tunaagizaje tomato paste, tomato sauce na chill sauce, wakati nyanya zinaoza mashambani. Vijana wamekaa hawana kitu cha kufanya wakati teknolojia ya kufanya hivyo ni ya nyumbani kwa mtu, unajifungia store unatengeneza tomato paste, tomato sauce na concentrate za tomato ambazo unaweza kuuza mpaka nchi nyingine au unaweka wakati ambao siyo msimu unatumia, kwa nini bado hatujalifikiria hili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna suala la umwagiliaji. Tanzania nafikiri ni nchi ya pili kama siyo ya tatu kwa wingi vya vyanzo vya maji lakini mpaka leo kilimo chetu kinategemea mvua. Napenda sana kuona zile scheme ambazo zimeshatengenezwa tayari lakini hazifanyi kazi zirekebishwe, zikarabatiwe ili wananchi walime kilimo cha umwagiliaji. Kila wilaya utakuta kuna scheme za umwagiliaji zimekufa au zina vitu vidogo tu vinavyohitaji matengenezo lakini havifanyiwi kazi tunafikiria mambo makubwa. Mambo makubwa ni mazuri lakini haya madogo ni mazuri zaidi kwetu sisi tunaotaka kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuuzungumzia SAGCOT pamoja na ASDP II. Hii yote ni miradi mizuri sana na inalenga kutukwamua lakini kwa kiasi kikubwa sana inategemea fedha ya nje. SAGCOT hundred percent I think ni hela ya nje. Sasa ikikosekana na wakati tunaona kabisa SAGCOT ndiyo ambayo inaelekeza sasa kilimo cha kisasa kwa kutumia mfumo wa sekta binafsi lakini tunawategemea watu wa nje. Napenda kuona Serikali na yenyewe inaingiza mkono wake kwa kuweka fedha ya kutosha kwenye SAGCOT ili sasa tuwe na uhakika kuwa huu mkakati utaendelea na kuwavuta watu wengi zaidi kuingia katika mfumo rasmi wa kuendesha kilimo na kukiendeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nirudi kwenye suala la vijana wetu, ajira nyingi sana za vijana zitatoka kupitia kilimo, ufugaji na uvuvi. Tujiulize kwa nini vijana hawapendi kuingia kwenye kilimo, ufugaji au uvuvi wa kisasa? Changamoto zao zinajulikana, vijana siyo watu wanaotaka kushinda shambani kutwa nzima na jembe. Ndiyo maana mpaka sasa hivi wengi wanaolima ni watu wazima na vijana wanawake lakini vijana wanaume wengi hawalimi kwa mtindo huu tunaoendelea nao sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sana kuona Serikali inakuja na mkakati wa ku-involve vijana kwenye kilimo specifically. Wale vijana wachache walioweza kulima wameona faida zake na huwaondoi huko. Kulikuwa na mradi wa MUVI ambao umekuwa ukisaidia vijana, wengi sasa hivi wamejikita kwenye kilimo na wanafurahia sana lakini bahati mbaya sasa na wenyewe wanakosa masoko kwa sababu hakuna ule mnyororo wa thamani ambao umeunganishwa katika hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kabla kengele haijalia Wizara haziongei, Wizara hazizungumzi, hakuna interconnection kama alivyosema Mheshimiwa Lucy asubuhi. Wizara ya Kilimo wana mikakati yao wanaendelea nayo huku na Wizara ya Viwanda wana mikakati yao wanaendelea huku wakati hawa ndiyo wanaotakiwa kuungana. Mpango utakapokuja sasa tuone kabisa ile link ya moja kwa moja kati ya kilimo na viwanda, uvuvi na viwanda, ufugaji na viwanda pamoja na ajira zao. Hii itaweza sasa kuona ile integration nzuri ya uchumi kuelekea uchumi wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la jinsi gani nguvu kazi watu inatayarishwa. Tuna miradi mikubwa mingi sana ambayo inaendelea sasa hivi, je, tunao wafanyakazi, vijana au watumishi wenye taaluma watakaokuja kufanya kazi kwenye miradi hii? Kwa hiyo, haya yote ni mambo ambayo ukiangalia lazima yawe linked…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naunga mkono lakini napenda sana kuona integration ya sekta zote muhimu au Wizara zote muhimu ku-converge kwenye uchumi wa viwanda. Hiyo ndiyo itakuwa njia peke yake ya kuhakikisha kuwa uchumi wetu na huu mpango unaenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.