Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niweze kusema yangu machache kwenye mpango huu wa Mheshimiwa Dkt. Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikiliza hotuba ya Waziri anayehusika lakini pia hotuba ya Kamati ya Bajeti, lakini pia hotuba ya Kambi ya Upinzani. Hotuba zote hizi zimekiri mapungufu ya kibajeti, ndio maana katika mipango yote iliyopita hatukufikia malengo. Sasa sielewi awamu hii katika mpango huu wa nne ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mpango anakuja na miujiza gani ili aweze kutekeleza yale yote ambayo ameyaweka kwenye mpango huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia takwimu katika mipango iliyopita hasa kile kipengele cha bajeti ya maendeleo, utekelezaji umekwenda kwa asilimia kati ya 50 na 60, mimi ninatafsiri matokeo haya kama sio yenye afya sana kwa sababu kama ni kule shuleni hiyo bado ni B wala sio B+; kwa hiyo tuko chini ya wastani. Kwa hiyo nilikuwa nataka niliseme kwamba hapa kinachotakiwa ni pesa ili mipango hii iweze kufanikiwa kinachohitajika ni pesa, lakini pia kingine kinachohitajika ni dhamira ya dhati ya kutekeleza yale yote ambayo tumekusudia kuyafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri maeneo machache, Mheshimiwa Waziri naomba nikushauri umwezeshe Msajili wa Hazina afanye kazi yake vizuri, Msajili wa Hazina ana makampuni au mashirika yasiyopungua 250 ambayo yanapaswa kuchangia kwenye Mfuko Mkuu wa Hazina, lakini mengi ya mashirika haya, yamekuwa yakitenda kwa kusuasua, mengine hayajui kabisa kutoa gawio kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali, mashirika mengine hata kama yanatoa gawio, yanatoa gawio kwa kile kiasi ambacho wao wanajisikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia yako mashirika ambayo kwa kweli yanahitaji kuondolewa kwa sababu yanachukua ruzuku Serikalini lakini mwisho wa siku hayazalishi kitu chochote, kwa hiyo nilikuwa nafikiri msaidie Msajili wa Hazina na huyu bwana ukimsaidia naye atakusaidia sana kupata pesa. Msaidie kupata watumishi, lakini pia mpatie vitendea kazi ili aweze kufanya kazi yake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, ni ukusanyaji wa kodi. Mheshimiwa Waziri, wewe ndio mkusanyaji mkuu wa kodi nchi hii, na nchi hasa awamu hii ya tano, imedhamiria kujiendesha kwa kukusanya kodi na kutumia kodi kwenye maendeleo, kwa hiyo unapokutana na wakwepaji wa kodi hawa watu naomba usiangalie sura yao, usiangalie dini yao, usiangalie na kabila yao, na usiangalie na vyeo vyao. Miezi michache iliyopita kulikuwa na lile sakata la makontena ya Makonda, ambayo yalikuwa na sura ya ukwepaji wa kodi, ulijaribu, ulijaribu kutoka hadharani na Watanzania tukakusifu na Watanzania tukasema tunaungana na wewe, sijui mwisho wa siku lile jambo limeishaje, umeshinda au ulishindwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba uje utuambie baadae, jambo lile liliisha namna gani, lakini kama tumekubaliana kuendesha nchi kwa kodi basi wale wote wanaostahiki kulipa kodi halali walipe na kusiwe na mianya ya watu kukwepa kodi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye eneo la kilimo, wengi wameongelea eneo hili na mimi naomba nipite pia huko huko. Nchi hii karibu asilimia 60/70 ya watu wake ni wakulima, na kwa hiyo kama tunahitaji mipango yetu ifanikiwe ni lazima tujielekeze kwenye namna ya kusaidia kundi hili kubwa liweze nayo kufanya kazi yake vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo, chetu bado ni duni, wakulima wetu wengi wanatumia jembe la mkono wachache wanatumia majembe ya kukokotwa na mifugo, wachache sana wanatumia matrekta, tunahitaji kufanya mapinduzi makubwa kwenye kilimo chetu, ili kilimo kiwe na tija.

Sasa ninajua uko mradi wa Matrekta na mengi yameanikwa pale Kibaha, takwimu zinasema nchi hii, nchi hii ya Tanzania inazo kilometa za mraba karibu laki nne zinazofaa kwa kilimo na kwa kilometa hizo unahitaji walau kiasi cha matrekta milioni mbili ili ulime vizuri, lakini Tanzania ya leo, ina matrekta yasiyozidi 30,000 yakiwemo yale ya pale Kibaha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sasa wewe utaona jinsi ambavyo kwa kweli, tunahitaji mapinduzi makubwa ili kilimo kiwe na tija, lakini pia suala mbegu, wakulima wetu wengi wanapanda zile mbegu ambazo sio zile zilizoboreshwa na matokeo yake wanavuna kiasi kidogo. Miaka ya nyuma tulikuwa na Kampuni inaitwa Tanseed iliyokuwa inazalisha mbegu ya mahindi, kampuni hii imetoweka, mbegu nyingi tunazopanda sasa hivi kwenye zao la mahindi ama zimezalishwa Kenya au Msumbiji au Malawi au Zambia zinazalishwa katika mazingira tofauti kabisa na haya ya kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini zinapokuja nyumbani zinauzwa kwa bei ghali mno, ni wakulima wachache wanaweza kupanda hizi mbegu ambazo zimaboreshwa.

Turudishe mashirika yetu ya Kitanzania yaweze kuzalisha mbegu hapa nyumbani ili wakulima wetu wapate mbegu kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye mbolea, maeneo mengi ya nchi hii kama hujaweka mbolea huvuni kitu, lakini tunayo Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) ambayo mimi naweza kusema ni kama kampuni inayoelea kuzimuni, kampuni hii inashindwa hata kujiendesha, zamani kampuni hii ilikuwa inazalisha mbolea pale Tanga, kiwanda kimekufa, sasa hivi wanaagiza, wanasambaza na wanauza mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kampuni hii, inaonekana haina uwezo kabisa wa kufanya kazi hii, kimsingi kampuni hii ya TFC inakosa mtaji wa uendeshaji yaani working capital. Mheshimiwa Dkt. Mpango, shirikiana na Waziri mwenzako wa Kilimo na Waziri mwenzako wa Viwanda, ili kuisadia Kampuni ya TFC iweze kufanya kazi yake vizuri, vinginevyo nchi hii suala la mbolea tutalisahau.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye eneo la Mchuchuma, Mchuchuma na Liganga imekuwa ni wimbo ambao hauna mwisho, hapa ndio nataka kusema kama kweli kama nchi tuna dhamira ya dhati hebu mradi huu ukamilike, miaka 25 ndani ya Bunge hili watu wanaongea habari ya Mchuchuma na Liganga, lakini miradi hii haikamiliki, kuna tatizo gani? Mimi nadhani kama tuna dhamira ya dhati jambo hili linawezekana, tuifanye Mchuchuma kama tulivyofanya kwenye reli, kama tulivyofanya kwenye ATC na kama tulivyofanya kwenye hiyo Striglers Gorge...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)