Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Usimamizi wa Matumizi ya Fedha za Umma katika Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2017

Hon. Tunza Issa Malapo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Usimamizi wa Matumizi ya Fedha za Umma katika Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2017

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimwia Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Awali ya yote, nataka kusema kitu kimoja kieleweke, Halmashauri zote Afisa Masuuli ni Mkurugenzi ambaye anateuliwa na Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo, tukiona Halmashauri ya Kigoma Ujiji inapata hati chafu, tatizo sio Zitto tatizo ni Mkurugenzi na watendaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia suala la barabara ya Tubuyu – Nanenane na Maelewano ya kilometa 4.6...

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waitara.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tunza Malapo unaipokea taarifa hiyo?

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, asitafute umaarufu kupitia mimi, kwa hiyo, niache niendelee na hoja zangu za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nasema barabara hii ya kutoka Tubuyu kwenda Nanenane mpaka Maelewano katika Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro kilometa 4.6 imejengwa kwa shilingi bilioni 12.6 maana yake ni kwamba kila kilometa moja imejengwa kwa shilingi bilioni 2.74. Sio highway tuelewane, ni barabara ya mtaa. (Makofi)

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mlinga.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tunza Malapo, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee, taarifa yake sipokei.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii barabara ni ya mtaa na tumeitembelea sehemu nyingi haina hata vituo vya daladala, unajengaje kilometa moja kwa shilingi bilioni 2.74 na ni mkopo kutoka Benki ya Dunia, sisi Watanzania maskini tutakuja kulipa. Kitu chochote unapofanya lazima uangalie value for money. Hii barabara ni ya mtaani sio highway kwamba labda itapitisha malori, unaenda kujenga barabara ya mtaani ya kwenda nyumbani kwako kwa shilingi bilioni 2.7 halafu ni pesa ya mkopo ambayo tunakuja kulipa mtu anasema kama tuko Ulaya! That is the shame. Mimi sikubaliani nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niingie kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua kuhusu Ukaguzi Maalum. Wakati naongelea hii naomba yaeleweke mambo yafuatayo; Mkuu wa Mkoa wa kipindi hicho Bi. Fatma Mwassa alikuwa na uhusiano wa karibu, mtu na mume wake na mkandarasi ambaye alipewa tender hizo. Wakati huo huo, kwa sababu ukaguzi unaozungumziwa hapa ulifanyika kuangalia mambo ya fedha ya mwaka 2012/2013 mpaka 2016/2017; wakati huo huo miongoni mwa Wakurugenzi ambao walihudumu katika Halmashauri hiyo, ni Dkt. Athumani Kihamia ambaye sasa hivi ni Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wakati naongea hapa, naomba nieleweke hivi…

MHE. AMINA S. MOLLEL: Kuhusu Utaratibu.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tunza Malapo, kuna kanuni inavunjwa, Mheshimiwa Amina Mollel, kanuni.

KUHUSU UTARATIBU

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Mimi naomba twende taratibu, Hansard naomba ichukuliwe, mimi nilichosema, kwanza mimi ni Mjumbe wa LAAC mnielewe, nimesema hivi Ukaguzi Maalum wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua umefanyika kwa kipindi cha mwaka 2012/2013 mpaka 2016/2017. Nikasema miongoni mwa Wakurugenzi waliohudumu kipindi hicho ni pamoja na Mheshimiwa Dkt. Athumani Kihamia, nimesema lipi la uongo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba niendelee.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tunza cha kuelewa ni kwamba ulivyotaja kuanzia 2012 mpaka 2017 Wakurugenzi wengine wote hukuwataja ikiwa ni pamoja na aliyekuwepo 2014 aliyeingia mkataba, ni jambo rahisi tu. Kwa hiyo, maana yake ni hivi…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, tuelewane, maana yake ni hivi, kama lengo ilikuwa ni kuonesha Wakurugenzi waliopita basi ungemtaja aliyekuwepo wakati wa mkataba ndiyo hoja iliyopo hapa.

Kwa hiyo, naomba twende vizuri, hiyo ndiyo hoja, usiseme miongoni mwao halafu unamtaja mmoja kwa kuwa yeye anahusika sana. Kwa hiyo, inakuwa kana kwamba yeye ndiyo aliingia huo mkataba wakati wewe unajua wazi hakuingia yeye aliingia mwingine lakini wewe umemchagua yeye. Kwa hiyo Mheshimiwa Tunza Malapo endelea na mchango wako. (Kicheko/Makofi)

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi bwana naomba mniache nichangie, mbona hiyo mmeonesha sana interest, nimemtaja hapa Mkuu wa Mkoa, nimemtaja hapa mkandarasi, lakini ngoja niache sasa niendelee na hoja yangu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilichokuwa nataka kusema ni kwamba kumekuwa na ubadhirifu mkubwa katika Halmashauri hiyo ya Kaliua wa shilingi bilioni 3.5. Sasa ukiangalia mambo yenyewe, nasoma ukurasa wa 41 kwenye Ripoti ya Kamati ili twende sawa, ukiangalia ile namba (xii) inasema, malipo mbalimbali yenye viashirio vya ubadhirifu na kugushi nyaraka yenye kiasi cha zaidi ya shilingi bilioni 1.2. Mpaka sasa hivi hatujui hatua zilizochukuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, namba (xi), usimamizi dhaifu katika ukusanyaji wa ushuru wa tumbaku uliopelekea kutokukusanya mapato zaidi ya shilingi bilioni 1.35. Sasa hapa kwenye ushuru kuna mambo mawili, mimi ni Mjumbe wa Kamati. La kwanza, hawakutoza ushuru kwa maana hawakuchukua tu lakini la pili ilikuwa wametoza ushuru siku wanaenda kulipa ushuru wao, kwenye exchange rate wakaenda kwenye Bureau De Change ambazo zinabadilisha kwa kiwango kidogo kuliko ya Benki Kuu. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Duh.

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine, ukiangalia namba (viii), malipo kwa mkandarasi kwa fedha za Mfuko wa Barabara kwa kazi ambazo hazikufanyika, hakufanya kazi lakini alilipwa. Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua hiyo. (Makofi)

Mheshimwa Naibu Spika, ukienda namba (i), malipo ya awali ya shilingi milioni 121.7 yalifanyika kwa kutumia nyaraka za dhamana toka Benki ya Equity, nyaraka hizo ziligushiwa. Kugushi maana yake ni jinai lakini mpaka sasa hivi bado wanatanua mtaani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, malipo ukienda ile namba (iv) malipo yalifanyika kwa mkandarasi bila kuonyesha vipimo vya kazi na mchanganuo wa kazi zilizofanyika kiasi cha shilingi milioni 197, bado wanatanua mtaani. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)