Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Usimamizi wa Matumizi ya Fedha za Umma katika Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2017

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Usimamizi wa Matumizi ya Fedha za Umma katika Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2017

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhitimisha majadiliano ya Taarifa ya Kamati yako tukufu ya Hesabu za Serikali za Mitaa mbele ya Bunge lako tukufu, naomba kuhitimisha kwa kulieleza Bunge lako tukufu kwamba Kamati ya LAAC ilihoji Halmashauri 58. Kamati iliainisha maeneo yenye matatizo makubwa kwenye Halmashauri zote nchini, kutokana na muda kuwa mfupi wa ufuatiliaji, utendaji na kuhoji kuwa mfupi Taarifa ya Kamati ilibaini mapungufu katika maeneo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ilikuwa ni ubadhirifu wa fedha za miradi ya maendeleo ya Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua kiasi cha shilingi bilioni 3.5 kilichofanyika katika kipindi cha mwaka wa fedha 2012/2013 hadi 2016/2017.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili ilikuwa ni kutotekelezwa kikamilifu kwa mapendekezo ya Kamati na tatu, kucheleweshwa kwa mchakato wa kukamilisha Kanuni za Uendeshaji wa Mfuko wa Wanawake, Vijana na Watu Wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa ya Kamati hii imechangiwa na jumla ya Wabunge watano, hakukuwa na michango ya maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijatoa ufafanuzi wa michango ya Waheshimiwa Wabunge naomba nilieleze na kulisisitiza Bunge lako tukufu kuhusiana na mapendekezo ya Kamati ya LAAC katika Ukaguzi Maalum katika Halmashauri ya Kaliua, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa imebainika kuwa kuna ubadhirifu wa fedha za miradi katika Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua kiasi cha shilingi bilioni 3.5 kilichofanyika katika kipindi cha mwaka wa fedha 2012/2013 hadi 2016/ 2017;

Na kwa kuwa hadi sasa Ofisi ya Rais, TAMISEMI imepokea taarifa hizo lakini haijachukua hatua stahiki dhidi ya watu wote walioshiriki katika ubadhirifu huo;

Kwa Hiyo Basi Kamati inaliomba Bunge lako Tukufu liazimie:-

(a) Ofisi ya Rais, TAMISEMI ichukue hatua stahiki dhidi ya wahusika wote walioshiriki katika ubadhirifu huo mara moja kwani suala hili lina sura ya kijinai.

(b) Watumishi wanaohusika moja kwa moja na ubadhirifu huu warejeshwe kwenye kituo hicho ili waweze kujibu tuhuma hizo za jinai.

(c) Taarifa hii ya ukaguzi maalum ikabidhiwe kwenye vyombo vya dola kwa ajili ya kuendelea na taratibu za kisheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Kamati ya LAAC inafanya kazi kwa kupitia Taarifa Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali, ikiwemo pamoja na Ukaguzi Maalum wa Halmashauri ya Kaliua;

Na kwa kuwa Ukaguzi Maalum ni conclusive;

Kwa hiyo basi, watumishi wote waliotajwa na ripoti ya ukaguzi huo kama ilivyoelezwa na kusisitizwa na Mheshimiwa Juma Hamad, Mheshimiwa Tunza Malapo pamoja na Mheshimiwa Felister Bura ikiwemo aliyekuwa Mkurugenzi Dkt. Athumani Kihamia na Wakurugenzi wengine wote waliohudumu katika Halmashauri hiyo kuanzia mwaka 2012 hadi 2017 pamoja na Mkuu wa Mkoa, Ndugu Fatma Mwassa, watawajibika kulingana na mapendekezo ya taarifa ya Kamati hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Tunza Malapo na Mheshimiwa Abdallah Chikota walieleza pia kuhusiana na matumizi mabaya ya shilingi bilioni 12.6 kwa ajili ya ujenzi wa kilometa 4.6 tu katika miradi ya ujenzi wa barabara pale Morogoro ambayo ingeweza kutumika kujenga zaidi ya kilometa kumi. Kamati inasubiri Taarifa ya Ukaguzi Maalum (Comprehensive Specific Audit) katika miradi yote ambayo inatekelezwa chini ya mradi huu wa Urban Local Government Strengthening Program (ULGSP) ili kuweza kuishauri Serikali vizuri juu ya hatua zaidi zinazopaswa kuchukuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Selemani Zedi alieleza kuhusiana na suala zima la kufutwa kwa malimbikizo ya madeni ya Mfuko wa Wanawake na Vijana na Watu Wenye Ulemavu yanayofikia kiasi cha shilingi bilioni 13.9; Kamati inakubaliana naye. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia alieleza kuhusu suala zima la kutopelekwa kwa fedha za maendeleo zilizopidhinishwa katika bajeti; pia Kamati inakubaliana naye. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini alieleza suala zima la udhaifu wa mifumo ya udhibiti wa ndani; Kamati inakubaliana naye pia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Spika kwa kutuwezesha Kamati kufanya kazi ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuchukua nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota - Makamu Mwenyekiti wangu ambaye tunashirikiana bega kwa bega katika kuiongoza Kamati hii. Vilevile nichukue nafasi hii kumshukuru Ndugu Dismas Muyanja Katibu wa Kamati, Ndugu Victor Mhagama - Katibu Msaidizi wa Kamati, Ndugu Waziri Kizingiti - Msaidizi wa Kamati, pamoja na Wajumbe wote wa Kamati ambao tumekuwa tukishirikiana bega kwa bega kuhakikisha Taarifa ya Kamati hii inakuwa imekamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni matumaini ya Kamati kuwa Serikali itazingatia mapendekezo ya Kamati hii ambayo yatakuwa ni Maazimio ya Bunge lako tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja kwamba Bunge likubali Mapendekezo ya Kamati hii ya LAAC ili yawe Maazimio ya Bunge lako tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, Naafiki.