Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018

Hon. Nuru Awadh Bafadhili

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Na mimi namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama hapa na kuweza kuchangia kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kuipongeza Kamati yangu ya miundombinu kwa taarifa nzuri iliyotolewa. Mimi ntazungumzia suala zima la Barabara yetu hii ya Dodoma – Dar es Salaam; kwa kweli Wizara imejitahidi sana kutengeneza barabara nzuri hii ya Dodoma – Dar es Salaam, lakini kuna tatizo linalojitokeza; Dodoma kama Jiji tukifika pale Ihumwa karibu kilometa sijui 10 mpaka kufika hapa katikati ya jiji kunakuwa na giza mno, kwa hiyo naiomba Serikali ijitahidi angalau kutuwekea taa za barabarani ili unapoingia katika sehemu zile za kukaribia jiji ujihisi kweli naingia katika jiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii sio tu Barabara ya Dodoma – Dar es Salaam, ile barabara ya Iringa, ile barabara ya kwenda Kondoa na barabara ya kwenda Singida, barabara zote hizi unapokaribia karibu na jiji ziwe zimewekwa taa kwa usalama wa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna tatizo linalojitokeza katika hizo barabara. Katika barabara zile kuna zile zebra crossing, naiomba Serikali iwape wananchi elimu ya kuzitumia zile zebra, kwa sababu mwananchi anajua kuwa ukifika kwenye zebra pale gari inasimama anapishwa yeye, basi unakuta mtu anachezea simu, eti anavuka kwenye barabara anachezea simu. Sasa kuna madereva wengine wanakuwa na uvumilivu lakini dereva mwingine anapita tu. Hiyo inaweza ikasababisha vifo vya watu kutokana na uzembe wao ambao wameona kuwa Serikali imetengeneza sheria kuwa zile zebra crossing gari inasimama na wao wanavuka, sasa badala ya kuvuka straight yeye anachezea simu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia sasa barabara yetu ya kutoka Dar es Salaam – Tanga, Dar es Salaam – Tanga tunaunganishwa na Daraja ambalo liko katika Mkoa wa Pwani na Mkoa wa Tanga, Daraja la Wami. Kwa kweli daraja lile tunaambiwa na Serikali kuwa litatengenezwa na lipo katika mkakati wa kutengenezwa, lakini ninachoomba, Serikali ilipe kipaumbele lile daraja kwa sababu mwaka jana mwezi Desemba tu kwa siku mfululizo magari yalitumbukia mara mbili kwenye lile daraja. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali itakapojenga lile daraja ihakikishe inajenga daraja pana ambalo litaruhusu magari kupishana kwa sababu pale magari wakati mwingine inabidi gari moja lisimame lipishe lingine na wakati mwingine gari inafeli breki, kwa hiyo yanaweza yakaingiliana na kuweza kusababisha ajali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu viwanja vyetu vya ndege; Uwanja wa Ndege wa Tanga una mgogoro na wakazi wa maeneo ya karibu ya ule uwanja. Kwa hiyo tunaiomba Serikali ihakikishe ule mgogoro unamalizika ili uwanja uweze kupanuliwa. Uwanja wetu ni mkubwa, hatuna sababu yoyote ya kuhamishwa uwanja mwingine, lakini tatizo linakuja kuna mgogoro uliopo kati ya wananchi pamoja na shirika la ndege, kwa hiyo tunaomba hilo Serikali ilifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuomba Serikali ihakikishe kama inavyosema kuwa itahakikisha kuwa inaunganisha barabara kati ya wilaya na wilaya. Katika barabara ya Tanga kuelekea Jimbo la Mkinga lakini kwenye Tarafa ya Maramba, kwa kweli mpaka leo barabara ile haina lami na wakati wa mvua kunakuwa na matatizo magari yanateleza na wakati mwingine wananchi pia wanashindwa kupitia. Kwa hiyo tunaiomba Serikali ihakikishe barabara ile ya Tanga – Maramba iwekwe lami ambayo itafika mpaka Daluni itaunganisha mpaka Korogwe, kwa sababu biashara nyingi zinafanyika kule lakini unakuta barabara haina lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho lakini sio kwa umuhimu, kuna mabango yale yanayowekwa ya alama mbalimbali za barabarani na watu wetu ambao sio waangalifu wala hawana uchungu na pesa za Serikali wanang’oa yale mabango kwa ajili ya kwenda kuuza vyuma chakavu. Naiomba Serikali ihakikishe katika zile alama za barabarani badala ya kuweka mabango yanayotumia mabati ihakikishe inaweka mabango yanayowekwa kwa kutumia zege kwa sababu mtu mpaka akaja akavunja zege itakuwa ni kazi kubwa, lakini yale mabati wanayang’oa na kwenda kuuza vyuma chakavu. Vilevile wito kwa wananchi, Watanzania wenzangu; tulinde miundombinu yetu ili tuweze kupata maendeleo katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuishukuru Serikali kutuletea ndege; ni kweli watu wanabeza lakini vitu vingine jamani, Waswahili wana methali wanasema: “Mengine ehee, mengine mmh”. Kwa hiyo, tunasema kuletewa ndege pia kumetusaidia tumerahisisha kazi ya kusafiri kwa muda mrefu. Mwezi uliopita nilitoka hapa Dodoma asubuhi nikaenda Dar es Salaam, tulikwenda kwenye kikao cha Kamati na tukaweza kuwahi na tumefika Dar es Salaam kutokana na kurekebishwa miundombinu ya Daraja la Mfugale tuliweza kutoka Airport mpaka tukafika jengo la bandari kule mjini haikuzidi nusu saa, tumefika pale na tukaweza kuwahi kikao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa vitu vingine sio tubeze, tunashukuru tumerahisishiwa kuliko tungepanda Noah, ingebidi tuondoke siku moja kabla kuelekea Dar es Salaam na kwenda kuhudhuria hivyo vikao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru. (Makofi)