Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii ili kutoa mchango kwenye hoja iliyokuwepo mbele yetu. Kwanza nichukue nafasi hii kuwashukuru Wabunge wote waliopata nafasi ambao wametoa mchango wao na sisi kwa niaba ya Wizara ya Kilimo kuna hoja chache zimetugusa, mawazo yote waliyoyatoa tunayachukua na tunaendelea kuyafanyia kazi ili kuboresha biashara hii, sekta ya kilimo iende vizuri. Kuna hoja ziko kama tatu au nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya kwanza ni hoja ya kurasimisha mfumo wa kangomba kwenye korosho. Kuna wengine Waheshimiwa Wabunge wamefananisha kilimo cha mkataba na biashara ya kangomba. Biashara ya kangomba imekataliwa kisheria kwa mujibu wa Sheria ya Stakabadhi Ghalani, Sheria Na. 10 ya mwaka 2005; Sheria Tasnia ya Korosho Na.18 ya Mwaka 2009 na kanuni zake za Mwaka 2010, mwongozo Na. 13 wa Mfumo wa Stakabadhi Ghalani wa mwaka 2018, lakini pia na Sheria ya Ushirika Na. 6 ya Mwaka 2013, zote hizo zimevipa mamlaka Vyama vya Msingi vya Ushirika na vyama vya Vikuu ndio wenye jukumu la kukusanya korosho kutoka kwa wakulima na kuzifikisha kwenye maghala ya masoko yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa sheria hizo nilizozitaja, hayupo yeyote mwingine anayeruhusiwa kununua au kukusanya korosho kutoka kwa wakulima isipokuwa wakulima wenyewe kupitia vyama vyao vya msingi na ushirika, hivi ni kwa mujibu wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama Mheshimiwa Mbunge au Wabunge wanaona sasa sheria hizi zimepitwa na wakati hazina manufaa labda kwa Taifa au kwa wakulima, basi kwa mujibu wa kanuni zetu, Kanuni ya 81 ya Toleo la Januari, 2016, inaruhusu Mbunge kuleta hapa hoja binafsi, ailete hapa, basi itachakatwa, ikionekana inafaa itapitishwa, lakini sisi kama Serikali kazi yetu kubwa ni kusimamia utekelezaji wa sheria kwa sababu sheria hii ilipitishwa na Bunge lako Tukufu hapa, tutaendelea kuisimamia ili sheria hii iendelee kutekelezwa. Mpaka sasa mfumo unaotambulika kisheria na kikanuni na kimwongozo ni mfumo wa stakabadhi ghalani na korosho zote zitaendelea kukusanywa na vyama vyetu vya ushirika na si vinginevyo.

Mheshimiwa Mwenyekti, pia kuna hoja nyingine imetolewa kuhusu kuna kesi ngapi ambazo zipo mahakamani au polisi. Labda niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kesi zipo za kutosha na ushahidi upo na zipo ngazi mbalimbali, kuna kesi zipo ngazi ya polisi zingine ziko mahakamani. Kwa mfano, wiki moja iliyopita nimetoka Newala na nichukue nafasi hii kuwapongeza sana Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Newala, walikuwa na kesi zaidi ya 47 na mojawapo ni korosho, mtu walipomkamata na tani 10 anasema korosho zile zimetoka Malinyi Morogoro, unaona namna gani kwamba udanganyifu upo na maana yake ametoka Morogoro amepita Pwani, amepita Lindi mpaka Mtwara na kufika Newala na Newala kwenyewe sio mjini kule vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hizo kesi zipo na kama Mheshimiwa Mbunge bado ana nia ya kutaka takwimu sahihi kwa sababu ni suala la kitakwimu, tutampatia baada ya Bunge hili atuone afike pale Wizara tutampatia takwimu kesi ngapi na ziko mahali gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna hoja imetolewa hapa kusema turuhusu uagizaji wa korosho kutoka Mozambique. Hilo haliwezekani kwa mujibu wa sheria kwa sababu korosho za Mozambique grade yao iko chini…

MWENYEKITI: Malizia.

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA):… zikija hapa zitatuharibia ubora wa korosho zetu na soko bei yake itapungua, hatuwezi kufanya hilo lazima tuwalinde wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi.