Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018

MHE. MOSHI S. KAKOSO - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MIUNDOMBINU: Mheshimiwa
Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuwasilisha na kupokea maoni ambayo wameyatoa Waheshimiwa Wabunge juu ya Kamati ya Miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo anaifanya hasa kwenye Sekta hii ya Miundombinu. Ametekeleza miradi mikubwa sana ambayo Serikali imeanza kuitekeleza na imeonekana kwenye jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ya usimamizi wa Serikali, nawapongeza Mawaziri, na Waziri mwenye dhamana ambaye anasimamia hii sekta, kwa kazi kubwa sana aliyoifanya kwa Kamati. Ushirikiano ambao ameuonyesha umetekeleza miradi ambayo ni mingi na ushauri wa Kamati umefanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kazi kubwa aliyoifanya ya kusukuma fedha kupeleka kwenye Sekta ya Miundombinu ambako kumeonekana miradi mingi ambayo imeanza kutekelezwa na zaidi kulipa fedha nyingi za Makandarasi waliokuwa wanadai, karibu ya zaidi shilingi trilioni tatu zimelipwa kwa kipindi cha miaka hii mitatu iliyokuwa na malimbikizo ya madeni huko nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge waliochangia ni 12. Kati ya hao, 11 wamechangia kwa kuzungumza na Mbunge mmoja amechangia kwa maandishi. Nawapongeza sana na kuwashukuru kwa kazi kubwa ambayo wameitoa na ushauri wao karibu asilimia kubwa umepitia mapendekezo ya Kamati. Mjumbe wa kwanza alikuwa ndugu yetu Mheshimiwa Musukuma, ametoa mapendekezo yake na kuishauri Kamati juu ya magari ambayo yanatumia super single.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo ambayo ametoa Mheshimiwa Mbunge, Kamati ilishatoa mapendekezo na yalishaanza kufanyiwa kazi na Serikali. Kwa bahati nzuri, Waziri mwenye dhamana, Mheshimiwa Isaack Kamwelwe, amezungumza nia ya Serikali kuangalia upya sheria ambayo ipo, nasi kama Kamati tunasisitiza kwamba, ni vyema Serikali ikaliangalia hilo, kwani nchi yetu siyo kisiwa, tumekaa katika maeneo ambayo ni ya mzunguko, ambapo tunahitaji kuwa na mawasiliano na nchi za jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo ambayo ameyatoa Mbunge Kamati ilishatoa mapendekezo na yalishaanza kufanyiwa kazi na Serikali kwa bahati nzuri, Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana Isack Kamwelwe amezungumza nia ya Serikali kuangalia upya sheria ambayo ipo na sisi kama Kamati tunasisitiza ni vyema Serikali ikaliangalia hilo kwani nchi yetu sisi sio kisiwa, tumekaa katika maeneo ambayo ni ya mzunguko ambayo tunahitaji kuwa na mawasiliano na nchi za jirani, kwani maeneo mengine ambapo tulitunga sheria hii hii, wapo wanaoitekeleza na wapo ambao hawaitekelezi. Kwa hiyo, ni vyema Serikali ikaliangalia upya na waweze kuliangalia kwa manufaa mapana ili liweze kufanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mjumbe mwingine aliyechangia Mheshimiwa Ally Saleh alizungumzia sana juu ya Shirika la Ndege ambalo mawazo yake makubwa alikuwa anashauri kwamba Shirika la Ndege lisiwe la kutoa huduma tu bali liwe la kibiashara na watendaji wajue shughuli ya kuliendesha hili shirika linahitaji ufanisi mkubwa. Kamati ilishatoa mapendekezo katika ukurasa wa 33 hadi 34, tumetoa mapendekezo juu ya kuliboresha shirika hili, lakini bado yapo mambo ya msingi ambayo ni vyema akayafahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shirika lina mpango wa kuweka business plan ambayo shirika linalo. Plan yao ni ya kuanzia mwaka 2016 hadi 2017 na sasa wanayo plan ya 2017 hadi 2022 ambapo wamejipanga kuwa na Bombardier nne, Airbus tatu, Boeing mbili na pia wamepanga safari za nje na walishaanzisha Entebbe na sasa wanajipanga kwenda Harare, Lusaka, Guangzhou na baadaye wana mpango wa kwenda Kigali, Nairobi, Lubumbashi na London ili kuweza kushiriki kwa karibu sana kwenye biashara ya nje ambayo itatusaidia sana kukuza sekta ya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Hawa Mchafu ameipongeza Serikali kwa jitihada ambazo zimefanywa. Naamini kwa ambaye anaona, anaona juhudi kubwa sana za Serikali ambazo zimefanywa, miradi mingi imetekelezwa, lakini ushauri alioutoa ni juu ya kuzingatia umuhimu wa kutoa fedha kwa wakati. Kwa bahati nzuri sana Mheshimiwa Waziri amelitolea ufafanuzi na bado Waziri mwenye dhamana, Waziri wa Fedha kaeleza jinsi ya mikakati ambayo anaendelea kulipa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia amepongeza Serikali kwa ununuzi wa ndege na kuanzisha safari za nje. Vile vile amezungumzia masuala ya GN inayosababisha kuchelewa kwa miradi, kwa nini vifaa visipelekwe site mapema. Hili tumelishauri kama Kamati na tunaomba Serikali ilizingatie kwani linachelewesha sana miradi ya maendeleo hasa pale ambapo panahitajika kutoa msamaha wa kodi kwa vifaa vinavyohitaji kwenda kufanya kazi. Tunaomba Serikali ilifanyie kazi kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la Mheshimiwa Daniel Nsanzugwanko, amezungumzia sana juu ya umuhimu wa ujenzi wa reli. Kama mnavyofahamu Serikali imeanza kutekeleza miradi ya reli kwa ujenzi wa kiwango cha standard gauge. Reli hiyo imeanza kujengwa Dar es Salaam mpaka Morogoro lakini kipo kipande cha kutoka Morogoro kuja Dodoma. Mipango ya baadaye ya Serikali ni kuhakikisha reli inajengwa kufika Tabora, Tawi la Mwanza na Tawi la Kigoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishauri Serikali kwamba mapendekezo yaliyopendekezwa na Kamati ni vyema yakaangaliwa upya kwani sisi tunaamini kwamba eneo la ukanda wa maziwa ndilo ambalo litakuwa na mzigo mkubwa sana. Kwa hiyo tunaamini Serikali wataangalia na karibu mapendekezo waliyoyatoa yapo kwenye ukurasa wa 31 na Kamati ilishatoa mapendekezo yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kazungumzia juu ya ujenzi wa kuimarisha TAZARA. Reli ya TAZARA ni muhimu na kielelezo pekee cha cha urafiki kati ya nchi ya Tanzania na China na ndugu zetu wa Zambia. Tunaomba Serikali ilifanyie kazi kwa haraka sana ili kulinusuru shirika hili kwani bado lina nafasi ya kuweza kufanya kazi kwa ufanisi unaotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Amon Saul amepongeza Serikali kwa ununuzi wa ndege na imesaidia sana kupunguza ajali za viongozi; tunashukuru na tunapokea pongezi zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa James Mbatia amezungumzia suala la bandari, umuhimu wa watu wetu kupata elimu, weledi katika mataifa mengine; bandari na reli lazima viende sambamba; suala la mizigo mikubwa reli ielekezwe huko ndiko msingi wa kiuchumi. Nami nimepitia na nimeeleza mapendekezo yaliyokuwa yameelezwa na Kamati. Karibu asilimia kubwa ya mapendekezo yaliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge mengi ni yaleyale ambayo tumeyatoa kwenye Kamati husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Nuru Bafadhil amezungumzia juu ya kuimarisha barabara ya Chalinze kwenda Tanga hadi Kilimanjaro, hasa lile daraja la Mto Wami. Naamini Serikali ilishaanza kulifanyia kazi na tayari sio muda mrefu mkandarasi ataanza kulifanyia kazi eneo lile husika. Pia kashauri juu ya umuhimu wa kuweka taa kwenye Jiji la Dodoma; mapendekezo hayo tunayapokea na tutawaambia Serikali waweze kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Genzabuke amezungumzia reli ya standard gauge, pia amezungumzia juu ya ujenzi wa barabara ya Kibondo mpaka Kakonko. Barabara hizi zipo kwenye mpango na tayari Serikali ilishaanza kuzifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Amina Mollel ametoa pongezi kwa Serikali kufufua TTCL, shirika lijiendeshe kwa faida na wizara na taasisi zilipe madeni; viwanja vya ndege hasa Terminal III itasaidia kuleta wageni wengi toka nje, miundombinu kwa watu wenye ulemavu ni muhimu kuzingatiwa . Naamini Serikali kila inapojenga viwanja huwa inazingatia yale ambayo Mheshimiwa Amina Mollel ameyapendekeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maoni ya ujumla; nitoe pongezi za dhati kwa Serikali kwa kuweza kukubali ushauri wa Wabunge kwa kiwango kikubwa sana. Ndio maana asilimia kubwa, Kamati yangu imepokea pongezi nyingi kwa sababu miradi mingi imetekelezwa. Tunaomba sana Serikali iweze kuzingatia kwenye maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni eneo la bandari. Ili bandari iweze kufanya kazi vizuri na ili bandari iweze kutoa msaada kwenye bandari zingine hasa za maziwa makubwa; Ziwa Victoria, Ziwa Tanganyika na Ziwa Nyasa ni vyema tukaijengea uwezo. Tunapendekeza Serikali izingatie na kiasi cha asilimia 40 ya mapato yake kiweze kupelekwa bandarini ili iweze kusimamia miradi ambayo ina nafasi kubwa ya kusukuma shughuli za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Serikali iangalie upya sheria hasa hii inayokataza magari ya single custom/ super single. Eneo hili ni vyema Serikali ikalitazama upya kwani tusipoliangalia tutawafanya wafanyabiashara wa nchi za nje wakashindwa kutumia barabara zetu na kukwepa kwenda kufanya shughuli sehemu zingine. Tunaomba hili Serikali tunajua ni sikivu, wataliangalia kwa makini ili waweze kulichunguza na kuufanyia kazi ushauri ambao Wabunge wameutoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza sana Serikali kwa jitihada ambazo wamezifanya na kupokea ushauri wa Wabunge. Mheshimiwa Waziri Mpango amezungumzia mambo ambayo kimsingi yalikuwa yanaleta tabu kidogo hasa kwenye utekelezaji wa miradi. Tunawahimiza ile misamaha ya kodi ambayo kimsingi inaweza ikachelewesha miradi, tunaomba sana waiangalie kwa kina wasipende kuchelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lijualikali amechangia kukwama kwa ujenzi wa barabara ya Kidatu – Ifakara. Kubwa zaidi ni kuchelewa kwa msamaha wa kodi; tunaomba wahusika wakae pamoja waweze kutekeleza kwa haraka kwani miradi inapochelewa inalifanya Taifa liingie gharama kubwa zisizokuwa stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuishukuru tena Serikali na tunaahidi sisi kama Kamati kuendelea kuipa support na mawazo ya Waheshimiwa Wabunge waliochangia kwa Kamati tutayafanyia kazi na tutaendelea kuishauri Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naomba kutoa hoja.

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.