Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza kabisa, naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu siku ya leo kunipa fursa ya kuchangia hapa.

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kwa niaba ya Wabunge wote ambao wanatokana na maeneo ya ufugaji lakini pia wafugaji Tanzania nzima kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa maamuzi ya busara na makubwa aliyofanya hivi karibuni. Katika maeneo mbalimbali nchini, ni furaha kubwa sasa watu wamekuwa na matumaini makubwa na tunaamini kabisa kwamba suala hili sasa litafika mwisho na hii migogoro baina ya hifadhi mbalimbali, baina ya wakulima, wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi yote sasa itafika kilele. Tunampongeza Mheshimiwa Rais na tunaomba sasa watendaji wote ambao watafuatilia wafanye kazi kwa umakini ili patokee matokeo mazuri na pande zote ziwe na mafanikio makubwa. (Makofi)

Mhesheshimiwa Spika, naomba pia nikumbushe kuwa haya maeneo mengi ambapo wafugaji wapo watu wengi sasa hivi hata humu ndani baadhi ya Wabunge wamechangia kwamba ni waharibifu wa mazingira, kama sio wafugaji wa asili hizi hifadhi zote zisingekuwepo. Kwa mfanom Kanda ya Kaskazini kama siyo wafugaji wale wametunza hayo mazingira na yamekaa vizuri na wanyamapori, hizo hifadhi zote zisingekuwepo.

Mheshimiwa Spika, tunapongeza na tunajua kabisa sasa katika maeneo ya Ayamango, Gedamag, Gidejebong ambayo tumeyasemea kwa muda mrefu lakini pia kwa maeneo ya WMA ya Burunge katika Wilaya ya Babati, changamoto zote hizi sasa zitapata ufumbuzi. Nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Ulega, kwa kufika pale, alitolea ufafanuzi mzuri na kila upande ulifurahi na sasa wanasubiri utekelezaji lakini naamini kwamba na wengine wote watafuata nyayo za Mheshimiwa Ulega. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikijikita kwa upande wa kilimo, nipongeze Kamati zote kwa kazi na ripoti nzuri na nikiwa mmojawapo katika Kamati ya Kilimo. Nimpongeze Waziri wa Kilimo na Naibu wake wote wawili, Waziri wa Maliasili na Utalii lakini pia Waziri wa Ardhi kwa kazi kubwa na nzuri wanayofanya, changamoto zitaendelea kuwepo, ni kawaida lakini naona mafanikio ni mengi ziadi kuliko changamoto. Kwa hiyo, tuendelee kushirikiana, tuendelee kufanya kazi ili changamoto zote ziishe.

Mheshimiwa Spika, ombi langu kubwa kwa upande wa kilimo, ili tuwe na usalama wa chakula ambao tunaimba kila siku, jambo la kwanza kabisa naomba tuwe tunazalisha mbegu zetu. Asilimia 75 ya mbegu zetu zinatoka nje ya nchi hasa mbegu ambayo ni ya chakula chetu kikubwa yaani mahindi lakini pia mbegu za mbogamboga zote asilimia zaidi ya 90 zinatoka nje ya nchi. Nashauri tuiwezeshe ASA ambao ni Wakala wa Mbegu nchini pamoja na mashamba yao waweze kuzalisha mbegu ya msingi (foundation seed) ili tuwe na uhakika wa mbegu ndani ya nchi ambazo zitakuwa zinafanya vizuri badala ya kuagiza mbegu kutoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, tunaagiza bidhaa kutoka nje ambazo zinaweza kuzalishwa hapa nchini kwa mfano sukari, mafuta ya kula, mchele, ngano, mbogamboga, matunda, maziwa pia nyama na samaki. Hizi zote tuziwekee muda kwamba ndani ya muda fulani, ndani ya miaka mitatu au mitano itakuwa hatuagizi tena kutoka nje badala yake tutakuwa tunazalisha ndani ya nchi, fursa zipo na tuwekeze katika hayo maeneo ili tuweze kuzalisha vya kutosha lakini pia ziada tuwe tunatuma nje na uwezo huo upo kabisa.

Mheshimiwa Spika, lingine naomba tuwekeze kwenye utafiti hasa katika masuala ya bioteknolojia na vituo hivi 17 vya utafiti hapa nchini. TARI ambayo inafanya kazi kubwa isipowezeshwa, haya mambo ya mbegu lakini pia utafiti mbalimbali wa udongo na mambo mbalimbali, hatutaweza kufikia malengo ambayo tunatarajia. Jambo la muhimu ni kwamba ile bajeti ambayo tumetenga kwenda kule TARI iende. Lengo ilikuwa tutenge asilimia 1 ya bajeti yetu nzima iweze kwenda katika masuala mbalimbali ya utafiti kwa ujumla, siyo kilimo peke yake.

Mheshimiwa Spika, pia kwenye kilimo, mbali na kuchanganya bajeti zile nyingine ambazo zinaingiliana ambazo ni mtambuka, bajeti ya kilimo peke yake tu kama kilimo iwe ni asilimia 10.

Mheshimiwa Spika, lingine ni uzalishaji wa mbolea, tunaagiza mbolea nyingi sana kutoka nje ya nchi. Tunacho kiwanda kimoja ambacho mbolea yake hatuitumii hapa nchini inavyotakiwa badala yake mbolea nyingi ya Kiwanda cha Minjingu inapelekwa nchi za jirani. Serikali za huko zinanunua kama Bodi ya Mazao Mchanganyiko Kenya ndiyo wananunua tani zaidi ya 20,000. Mheshimiwa Rais alishatolea maelekezo kwamba mbolea hiyo inunuliwe katika maeneo ambayo inafaa itumike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbolea ni sawa na binadamu, unapoumwa ndiyo unaenda unapimwa, ukipimwa ndiyo unapewa dawa, tusichukulie tu kwamba mbolea ya Minjingu kila mahali itafanya kazi. Mahali mbolea ya Minjingu isipofanya kazi hata hiyo DAP inayotoka nje ya nchi haitafanya kazi kwa sababu haitakiwi hiyo DAP. Kwa hiyo, tuendelee na utafiti na masuala ya kitaalam, kwa hiyo, tutumie viwanda vya ndani.

Mheshimiwa Spika, tuliambiwa kwamba kuna suala hili la kujenga kiwanda kule Lindi ili tuzalishe urea nchini. Tukiwa na urea na phosphate, NPK itapatikana hapa nchini. Baada ya hapo ni kuchanganya ratio kwamba unahitaji asilimia ngapi ya aina moja ya N, P au K unapata mbolea za aina mbalimbali, hakuna zaidi ya hapo, hiyo ni baseline nyingine zote ni nutrients za ziada ambazo zinatakiwa zinatokana na upimaji wa udongo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la maji, nipongeze Wizara inafanya kazi nzuri sana, wamekuwa na mpango mzuri na niwapongeze kwa kupitisha sheria hii mpya juzi ambayo italeta mabadiliko makubwa kwa upande wa maji. Nikirudia kwa upande wa maji vijijini, napongeza na naomba suala hili la uanzishwaji wa RUWASA, uwe wa haraka lakini pia kwenye jambo hilo kanuni zake zitoke mapema.

Mheshimiwa Spika, ombi langu lilikuwa ile shilingi 50 ambayo tulikuwa tunasema iende kwenye Mfuko wa Maji, narudia tena kwamba iende kwenye RUWASA yaani maji vijijini. Ikienda huko ambapo kuna changamoto kubwa huu Mfuko mwingine wa Maji mkubwa utaendelea kupata kutoka kwenye vyanzo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado naendelea kuomba tuongeze na shilingi 50 nyingine ili iwe 100. Hata ukiangalia kwenye mtiririko, fedha nyingi ambazo zimekwenda huko vijijini ndiyo hiyo shilingi 50 ambayo tulitenga kwenda huko na bajeti ya kawaida pesa iliyoenda ni kidogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia Serikali iangalie tutakapofika kwenye bajeti iendelee kuondoa kodi na tozo mbalimbali katika kuagiza mitambo ya uchimbaji maji, mitambo ambayo inaweza kutengeneza mabwawa na malambo mbalimbali ili tuwe na uvunaji wa maji. Tukivuna maji katika maeneo mbalimbali kwanza tutaondoa uharibifu unaotokea kwenye miundombinu ya barabara, reli, lakini yale maji yatatumika kwenye kunywa binadamu na mifugo, ufugaji wa samaki na kwa matumizi mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kama walivyosema pia watu wa Maliasili, ni muhimu sana tuhakikishe kwamba Mto Ruaha Mkuu unaendelea kutiririka. Njia pekee sisi kwenye umwagiliaji lazima twende na mambo ya kisasa, mambo ya teknolojia mpya, tukitumia teknolojia ile ya zamani ya kumwagilia kwa kujaza ardhi yote ijae maji iwe kama bwawa ndiyo upande mpunga au mazao mengine, tuondokane na huko tutumie drip irrigation.

Mheshimiwa Spika, tukitumia drip irrigation, mahali ambapo una maji ya eka tano kwa kumwaga kwenye shamba zima kwa drip irrigation utamwagia eka 20. Kwa hiyo ukiwa na eka moja ya kawaida utafanya eka tano. Kwa hiyo, tunaweza kutumia maji kidogo lakini kwa kutumia teknolojia tukapata mashamba makubwa mengi zaidi ambapo kutakuwa na ufanisi mkubwa na ule mto ukiendelea kutiririka, Stiegler’s Gorge pia itaweza kufanikiwa kwa sababu lazima tuhakikisha maji yanatembea ili Stiegler’s Gorge iweze kupata maji ya uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbali na hiyo, kwa upande wa utalii, naipongeza Serikali kwa kazi kubwa na naomba hizi ndege ambazo tumenunua sasa ziendelee kufanya kazi na ziweze kutangaza nchi yetu ili kuleta mafanikio. Ombi moja tuangalie charges mbalimbali ambazo zipo katika viwanja vyetu, kwa nini bado gharama zetu za usafirishaji, hasa kwenye mazao ya kilimo, maua zinakuwa juu na badala yake kupelekea kupitia Kenya. Kwa hiyo, Wizara zote zikishirikiana naamini tutapata mafanikio. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi lingine kwa ujumla kwenye kilimo, mifugo na maji huko kote tuangalie. Blue print ile tuliyoileta hapa Bungeni na Serikali iliahidi itaifanyia kazi bado uzalishaji wetu gharama yetu iko juu sana; regulatory bodies zina-charge gharama nyingi sana na ndiyo maana inafanya biashara zetu zote hazikui, haswa viwanda ambavyo vinachakata mambo mbalimbali ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye utalii bado wamekuwa na changamoto kubwa, wameendelea kupigwa faini za ajabu. Mtu akikutwa na nyama ambayo haina label ambapo sisi tunahamasisha wafugaji wadogo wadogo wafuge kuku, samaki wakiuzwa kwenye zile hotel wanapigwa faini ya shilingi milioni moja, milioni tano, milioni 20, hilo jambo naomba lifike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juzi tu, halina siku mbili jirani na Jimbo la Babati Vijijini hoteli moja imepigwa faini ya shilingi milioni moja kwa ajili ya kutoa nyama kwenye fridge ili iyayuke (defrost). Wamekata tamaa wanauliza wawe wanaagiza kutoka sokoni au buchani mtalii akija ndiyo tuweze kuwapikia watu? Naomba tusifike huko, naamini Serikali hii itaweza kuleta mabadiliko. Juzi kwenye briefing tuliambiwa kwamba suala hili limesitishwa lakini naweza kuleta ushahidi kwamba bado linaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipongeze kwamba sasa tuna Waziri wa Uwekezaji. Naamini Waziri huyu akikaa pamoja na Mawaziri wote wa Kilimo, Mifugo, Uvuvi tutaweza kufanya kazi kubwa na kuleta mabadiliko.

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo naunga mkono hoja, ahsanteni sana. (Makofi)